Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 16 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2019-04-25

Name

Zainab Athuman Katimba

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kumekuwa na matukio ya uhalifu katika maeneo ya mipakani na ni kutokana na mwingiliano wa wageni kutoka nchi jirani. Je, nini kauli ya Serikali kuhusiana na kuimarishwa na kudhibiti hali ya usalama katika mipaka yote nchini hususan katika maeneo ya Mkoa wa Kigoma ambako kumekuwa na matukio ya mara kwa mara ya uhalifu ambayo yanahusisha matumizi ya silaha za moto?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Katimba, Mbunge wa vijana, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, suala la ulinzi na usalama nchini ni jukumu letu sote, suala la ulinzi na usalama nchini napenda kuwahakikishia Watanzania na wote ambao wanakuja nchini Tanzania kwamba, ulinzi na hali ya amani na utulivu nchini inaendelea vizuri kwa sababu vyombo vyetu vya ulinzi vinaendelea kufanya kazi katika maeneo yote na kuhakikisha kwamba Tanzania inabaki kuwa salama.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Mbunge amezungumzia wasiwasi wake wa hali ya ulinzi na usalama kwenye mipaka na ameeleza hasa Mkoani Kigoma ambako natambua yeye pia anatoka Mkoani Kigoma. Nimefanya ziara Mkoani Kigoma, yako matukio kadhaa yameripotiwa, lakini hasa matukio haya ni kutokana na mchanganyiko tulionao na hasa kwenye mikoa yote iliyoko pembezoni.

Mheshimiwa Spika, nimeenda Kigoma, Kagera na Mkoani Kilimanjaro nimeona dalili hizo na taarifa za Jeshi la Polisi, lakini sehemu kubwa ni salama. Nini tahadhari ya maeneo haya, ni kutokana na mwingiliano wa nafasi ambazo tunazo na nchi jirani ambazo zinazunguka kwenye maeneo haya, tahadhari kubwa imechukuliwa. Nataka pia nitumie nafasi hii kuwasihi Watanzania hasa wale tulioko mipakani kushiriki kikamilifu katika kulinda mipaka yetu na kubaini vyanzo vyote vinavyoashiria kuleta uvunjifu wa amani nchini tukishirikiana na vyombo vya dola ambavyo vyenyewe vina nafasi ya moja kwa moja kwenye ulinzi wa usalama hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, tunachokifanya ni nini kwenye mipaka? Kwanza, tumeimarisha mipaka hiyo kwa kuweka maeneo maalum ya wanaoingia nchini ili kuweza kuwatambua wote wanaoingia na kukagua wamengia na zana gani kwa lengo la kudhibiti uingiaji wa silaha ambazo haziruhusiwi kuingia hapa nchini. Pia vyombo vyetu vya ulinzi vimeweka tahadhari kubwa sana na nchi jirani ambazo sasa tunashuhudia huko kuwa na migogoro mingi ya ndani, kwamba migogoro hiyo kwenye nchi hizo jirani isihamie kwenye nchi yetu.

Kwa hiyo, Majeshi yetu na vyombo vyote vya dola vinaendelea na umakini huo ikiwemo na Mkoa wa Kigoma ambako tunapakana na nchi jirani zisizopungua mbili, tatu, nne ambazo na zenyewe pia tunaendelea kujenga mahusiano ya kiulinzi kuhakikisha kwamba hakuna mwananchi kutoka nchi moja kwenda nchi nyingine anaweza kuhamishia migogoro nchi nyingine ili kufanya nchi hizi kuendelea kuishi kwa umoja, mshikamano pia kuwa na ulinzi wa pamoja.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na nataka niwahakikishie wananchi wote wanaoishi maeneo ya pembezoni matukio yote madogo yanayoripotiwa yanachukuliwa hatua lakini udhibiti wa mipaka hiyo unaendelea kuimarishwa lakini nitoe wito sasa kwa Watanzania wenyewe tushirikiane, tushikamane katika kubaini viashiria vyote vinavyoleta uvunjifu wa amani nchini kwa lengo ya kuifanya Tanzania kuendelea kuwa salama, kwa lengo la kuifanya Tanzania kuwa ni kimbilio la wale wote wanaopenda amani, kwa lengo la kuwafanya Watanzania wenyewe kufanya shughuli zao za maendeleo wakiwa na uhakika wa maisha yao, wakiwa na uhakika wa shughuli zao.

Kwa hiyo, tutaendelea kushirikiana kuhakikisha kwamba vyombo vya usalama vinalinda maeneo yote ili kuhakikisha kwamba nchi inabaki salama. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister