Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 16 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2019-04-25

Name

Venance Methusalah Mwamoto

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Primary Question

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Spika, hivi karibuni nchi yetu ilipata heshima kubwa ya kuandaa mashindano ya AFCON, lililotokea Watanzania wote wameshuhudia lakini tumejifunza mambo mengi. Sasa kwa kuwa tumepata heshima nyingine tena ya kuandaa mashindano ya watu wenye ulemavu ya Afrika Mashariki. Je, Serikali sasa inasemaje ili watuondoe kimasomaso?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Mwamoto, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba nchi yetu sasa tumeanza kushuhudia na kuona mwamko wa Watanzania kushiriki katika michezo mbalimbali. Pamoja na mwamko huu tuliokuwa nao tumeanza kuona pia hata mashirikisho mbalimbali duniani na Afrika wanaendelea kututambua Watanzania na kutupa heshima ya kuendesha mashindano mbalimbali. Leo hii nchini tunayo mashindano ya vijana wetu wa umri chini ya miaka 17 yanaendelea nchini na sisi tulipelekea timu yetu, hatujafanya vizuri lakini tumejifunza mambo mengi kupitia mashindano haya.

Mheshimiwa Spika, pia nafurahi kusikia kwamba nchi yetu pia imepata heshima ya kuendesha Mashindano ya Walemavu ya Afrika Mashariki. Jambo hili kwetu kama Tanzania ni tunu kwa sababu tunaanza kuona mashirikisho mbalimbali ya michezo duniani na Afrika yakitupa hadhi ya kusimamia mashindano hayo, maana yake ni nini? Maana yake nchi yetu inatambulika au kwa upande wa usalama au uwezo wa kusimamia pia inatutengenezea fursa kwa Watanzania kutumia mashindano hayo kuboresha pia masuala ya uchumi. Hili litatufanya pia na sisi sasa tuondoke hapa tulipo kimichezo katika michezo mbalimbali na tuweze kufikia hatua nzuri ya kuweza kushindana mpaka ngazi ya dunia.

Mheshimiwa Spika, mashindano ambayo yanaendelea na hayo ambayo yatakuja, tutaendelea kujifunza na kuandaa vizuri timu zetu za ndani zinapokwenda kushiriki zipate kombe lililotarajiwa na ambalo tumeletewa hapa nchini ili tuweze kuboresha. Vile vile Serikali sasa tumeanza kusimamia michezo hii ikichezwa kutoka umri mdogo kwenye shule za msingi na sekondari, kwenye vyuo ili kuweza kupata kuunda timu za Kitaifa ambazo sasa tunaanza kuona mwelekeo huo mkubwa. Hiyo ndiyo ilifanya hata mashindano haya ya vijana wa umri chini ya miaka 17 kuruhusu vijana wote wa shule za msingi, sekondari walioko likizo na Watanzania wote kuingia bure kwenda kushuhudia michezo inayochezwa kwa lengo la kujifunza zaidi kwenye michezo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hadhi na heshima ambayo tunaipata Serikali ni pamoja na kupata fursa za kuongeza uchumi, kutangaza nchi, kuboresha sekta ya utalii na kila mmoja hasa watoa huduma kupata fursa ya kuweza kutoa huduma. Nitoe wito kwa Watanzania, tuanze sasa kuona michezo kuwa ni fursa kwetu na tuendelee kuungana pamoja kuhakikisha kwamba michezo inachezwa katika maeneo yote na michezo yote, tuunde vilabu, tuvisimamie vizuri, viingie kwenye mashindano na kila shirikisho la kila mchezo lishawishi kwenye ngazi yake ya Afrika, ngazi ya Dunia michezo iweze kuchezwa hapa ili fursa zile sasa ziwewe kunufaisha Watanzania. Kwa hiyo kwa kupitia michezo sasa Serikali na Watanzania tunaweza kunufaika zaidi. Ahadi ya Serikali kwenye hili ni kusimamia michezo. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister