Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 16 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2019-04-25

Name

Amina Saleh Athuman Mollel

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi. Swali langu ninapenda kufahamu, kwa kuwa takwimu za Taifa kwa sasa zinaonyesha kuwa kila mwaka watu 82,000 wanaambukizwa virusi vya UKIMWI hapa nchini na ni-declare interest kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati ya UKIMWI na Dawa za Kulevya.

Mheshimiwa Spika, kati ya hao wanaoambukizwa ni kuanzia miaka 15 mpaka 64 na asilimia kubwa inaonyesha kwamba vijana ndiyo wanaoongoza hivi sasa kwa asilimia 40 na kati ya hao vijana, watoto wa kike ndiyo ambao wanaoongoza kwa asilimia kubwa.

Mheshimiwa Spika, watu wanaoishi na virusi vya UKIMWI kwa sasa, takwimu za Taifa…

SPIKA: Sasa swali Mheshimiwa Mollel.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, swali langu; nilipenda kufahamu mkakati wa Serikali, tamko la Serikali juu ya hali hii kwa sababu hali ni mbaya. Nini tamko la Serikali katika kusaidia Taifa na hasa vijana ambao ndiyo tunawategemea katika nguvu kazi ya Taifa?

Mheshimiwa Spika, ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Amina Mollel, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tatizo la UKIMWI nchini limekuwa likiratibiwa vizuri sana na Serikali toka tulipoanza kampeni ya kupambana na maambukizi ya UKIMWI kwa kushirikisha Wizara zote ambazo zinahusika katika kulinda afya ya Mtanzania. Ofisi ya Waziri Mkuu ndiyo hasa inasimamia suala la mapambano dhidi ya UKIMWI kwa kuwa tumeshaunda Taasisi inayoitwa TACAIDS. Tunafanya kazi kwa pamoja na Wizara ya Afya ambayo ndiyo ina wajibu wa kusimamia afya ya Mtanzania.

Mheshimiwa Spika, pia Bunge letu la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Kamati ya Kudumu ya Bunge ambayo inashughulikia masuala ya UKIMWI nayo pia imekua ikishiriki kikamilifu. Kwa hiyo, mkakati huu wa pamoja ndiyo unaowezesha sasa kupambana na maambukizi ya UKIMWI ambayo sehemu kubwa yanaathiri sana maisha ya vijana kama ambavyo umeeleza na takwimu ambazo unazo mezani kwako.

Mheshimiwa Spika, muhimu zaidi ni kwamba mkakati wetu sasa ambao tunao ni kuhakikisha kwamba wale Watanzania wote kwanza tunatakiwa kupima ili kujitambua afya yetu na malengo yetu kufikia mwaka 2020 kila Mtanzania awe ameshapima. Ndiyo maana tumeweka kampeni ya upimaji karibu maeneo yote na kila mahali wanapokutana, wananchi zaidi ya 100 lazima pawe na eneo la kupimia ili kutoa fursa kwa Watanzania kwenda kupima. Kwa hili pia tuna kampeni kubwa, tumegundua wanaopima sana ni akina mama kuliko wanaume, nami ni Balozi wa wanaume wa upimaji. Kwa hiyo, tunahamasisha kwa ujumla wake watu wapime.

Mheshimiwa Spika, pili, wale wote waliopima na wamegundulika kuwa na maambukizi, kufikia mwaka 2020 tunataka wote wawe wameshaanza kutumia dawa za kufubaza hivyo virusi vya UKIMWI. Tunataka kufikia mwaka huo kila ambaye amepima, akishajitambua aanze kutumia dawa. Malengo yetu ni wale wote ambao wamepima na kukutwa na virusi wawe wameanza kutumia dawa, ifikapo mwaka 2020 tupate idadi kubwa ya watu ambao tayari wamefubaza virusi vya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, nini ujumbe hapa? Ujumbe ni kwamba Serikali inaendelea na mkakati wa kuhakikisha kwamba tunapunguza kwa kiasi kikubwa maambuki ya UKIMWI nchini kupitia Kampeni, Kupitia Programu zetu ambazo tunazo, pia tunaendelea kuwaelimisha Watanzania kuendelea kutambua afya zao pale ambako wanajikuta wana maambukizi waende wakapime moja kwa moja na hasa vijana ambao umewalenga wa kati ya miaka 18 mpaka 25 ambayo sehemu kubwa ndio waathirika wakubwa hao ndio tunafanya kampeni.

Mheshimiwa Spika, hiyo kama haitoshi, tumeendelea kutoa elimu hii kwenye shule za msingi na sekondari ya maambukizi ya UKIMWI na kuwataka watoto sasa, vijana wetu kwenye shule za msingi na sekondari wawe na tahadhari ya maambukizi, waaache kujiingiza katika maeneo ambayo yana maambukizi ili waendelee kuwa salama na wao ndio wawe Walimu wa Watanzania wengine katika kujikinga na maambuki ya UKIMWI.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo programu za kujikinga na UKIMWI zinaendelea na Serikali inaendelea na mpango wa kuwahamasisha Watanzania na niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kupitia Kamati kazi nzuri wanayoifanya kuisaidia Serikali ya kuhakikisha kwamba Watanzania wanatambua umuhimu wa kupima, kupata madawa na umuhimu wa kujilinda wakati wote hapa tunapoendelea na shughuli zetu. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister