Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2017-11-09

Name

Pauline Philipo Gekul

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali imekuwa ikitoa kauli na matamko mbalimbali kwa wakulima wa mbaazi kote nchini kwamba Serikali inafanya mazungumzo na Serikali ya India ili wakulima hawa wapatiwe soko. Hata hivyo hadi sasa mazungumzo hayo hayajakamilika na wakulima wamebaki na mazao yao.

Mheshimiwa Spika, ninaomba nifahamu, kwa nini Serikali isione ni busara kuwatangazia wakulima wa mbaazi kote nchini kwamba wameshindwa kuwapatia soko na wasiende kulima katika msimu huu wa kilimo ambao unakwenda kuanza sasa?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Gekul, Mbunge wa Babati Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hata juzi wakati tunapeana maelekezo ya msingi jambo hili la matatizo ya masoko ya mazao yetu lilijitokeza, mbaazi ikiwemo. Ninachoweza kusema hatuwezi kuwaambia wakulima msimu huu wasijiandae kulima kwa sababu suala la masoko, awali zao la mbaazi tulikuwa na soko la uhakika la nchi ya India na ndio wanunuzi wakuu wa zao hili. Huku kwetu sisi mikoa yote inayolima imeendelea kulima kila mwaka na tumeendelea kufanya biashara na nchi ya India bila tatizo lolote lile.

Mheshimiwa Spika, lakini pia hata hivi karibuni Waziri Mkuu wa India alipokuja nchini, aliweza kusisitiza pia tulime mbaazi nyingi na wao pia wanalima na sisi tumelima. Sasa tulipofikia hatua ya kuuza kwa bahati mbaya au nzuri kwao nchi ya India imeweza kuzalisha mbaazi kwa asilimia 30 zaidi na kwa maana hiyo wana mbaazi ziada na kwa hiyo, walisitisha utaratibu wa kununua mbaazi kutoka nchi za nje kuingiza kwao mpaka hapo akiba yao watakapoifikiria vinginevyo. Kwa kufanya hilo wametuathiri kwa sababu soko pekee la mbaazi kwetu sisi ilikuwa ni nchi ya India.

Mheshimiwa Spika, sasa nini jukumu la Serikali kwa sasa; tunaendelea kutafuta masoko na ndiyo sababu tumewasihi wakulima wa mbaazi nchini kote, na ni mikoa mingi inayolima sana mbaazi, tumeendelea kuwasihi kwamba waendelee kutusubiri kwa sababu Bodi ya Mazao Mchanganyiko ambayo inashughulikia mbaazi pia sasa inaendelea kutafuta masoko, likiwemo na lile zao la tumbaku ambalo nimelieleza muda mfupi uliopita.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, jitihada hizi zitakapofikia hatua nzuri, tutauza. Kwa sasa hatuwezi kuwaambia kwamba tutauza kwa sababu bado negotiations zinaendelea na mataifa ambayo yatataka kununua zao hili la mbaazi ikiwemo na India yenyewe kwa sababu ya ile commitment ambayo ilikuwa imeshatolewa kati yetu na wao; na ndiyo utaratibu wa kawaida kwa nchi ambazo tunafanya nao biashara za mazao. Pale ambapo kunatokea tatizo lazima na sisi tupate taarifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hii ni taarifa kwa wakulima wote wa mbaazi kwamba kwa sasa wawe watulivu, tunaendelea na utaratibu huu wakati wowote tutawapa taarifa. Ni kweli tunajua wanaathirika sana lakini ni muhimu pia taarifa hii kuwa nayo na uvumilivu ni muhimu pia kuwa nao.

Additional Question(s) to Prime Minister