Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 9 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2017-11-09

Name

Freeman Aikaeli Mbowe

Gender

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Hai

Primary Question

MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kumuuliza Waziri Mkuu swali la kwanza.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu nina imani utakubali kwamba usalama wa nchi na mahusiano mema miongoni mwa raia ni tunda la mahusiano mazuri kati ya vyama vya siasa, Serikali na vyombo vyote vya dola.

Mheshimiwa Spika, siku za karibuni kumekuwa kuna mwendelezo wa matukio mengi yanayovunja usalama huo, yanayovunja amani na yanayojenga chuki miongoni mwa vyama vya siasa na kuharibu utengamano wetu wa kitaifa.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, tukio la kushambuliwa kwa risasi kwa nia ya kuua kwa Mheshimiwa Tundu Anthipas Lissu, Mbunge na Mnadhimu wa Kambi ya Upinzani Bungeni limezua hofu kubwa sio tu kwa Taifa ila katika Bara zima la Afrika na Jumuiya ya Kimataifa. Nina hakika taharuki hiyo imeharibu sana sura ya Taifa, heshima tuliyokuwa nayo kama Taifa na hatujaona kama Serikali inachukua hatua zozote kujaribu kufanya jambo hili lisiendelee kuharibu image yetu kama Taifa.

Mheshimiwa Spika, aidha, Mheshimiwa Waziri Mkuu atakumbuka kwamba hapo nyuma vimetokea vifo vya kisiasa. Alifariki Mwenyekiti wetu wa Mkoa wa Geita, Bunge na Serikali tulilizungumza hapa na Serikali ikasema inafanya uchunguzi, hadi leo hakuna hatua iliyochukuliwa.

Mheshimiwa Spika, akapotea msaidizi wangu Ben Saanane, nikakuomba Waziri Mkuu na Serikali yako iruhusu uchunguzi wa kimataifa ili kutatua tatizo hili, ukasema vyombo vyetu vya ndani vina uwezo hadi leo hakuna lililopatikana. Tumeomba vilevile kushambuliwa kwa Mheshimiwa Tundu Lissu kuchunguzwe na vyombo vya uchunguzi vya kimataifa vilivyo huru, visivyofungamana na upande wowote, bado Serikali inaonekana ina kigugumizi katika jambo hili.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, unatupa kauli gani sisi kama chama, Wabunge na Taifa?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kwanza nataka nieleze kwamba amani yetu na utulivu ndani ya nchi ni jambo ambalo Watanzania wote lazima tushikamane na tushirikiane katika kulidumisha. Ndilo ambalo linaendelea kutupa heshima duniani kwa sababu Watanzania wote tunashirikiana katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yapo matukio yanajitokeza, Mheshimiwa Mbowe umezungumzia upande wa siasa lakini pia matukio haya yapo kwa ujumla wake nchini kwenye maeneo kadhaa kwa ngazi ya familia, lakini pia na maeneo mbalimbali ya mikusanyiko, na watu wengine pia. Wapo wenzetu ambao hawana nia njema nchini wanajitokeza katika kutenda matendo hayo.

Mheshimiwa Spika, na hata hili analolisema la Mheshimiwa Tundu Lissu si Mheshimiwa Tundu Lissu pekee ingawa hatupendi mambo kama hayo yatokee, lakini pia tumepoteza Watanzania wengi. Hata mnakumbuka Wilaya za Mkuranga, Kibiti na Rufiji tumepoteza watu wengi. Hata hivyo pia hata siku za karibuni Kamanda wetu wa Jeshi la Ulinzi nchini (JWTZ) naye alipigwa risasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuyazungumze haya kwa ujumla wake na tunapoyazungumza haya kwa ujumla wake, na kwa utamaduni ambao tumeujenga wa nchi hii katika kujilinda wenyewe na kuhakikisha kwamba nchi inaendelea kuwa salama, nataka nikuhakikishie kwamba vyombo vyetu vya dola vinaendelea kufanya uchunguzi wa haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na uchunguzi huu hauwezi kuwa wa leo leo ukapata ufumbuzi kwa sababu wanaotenda matendo haya wanatumia mbinu nyingi za kujificha. Kwa hiyo, na sisi lazima tutumie mbinu zetu za kutambua hao waliotenda matendo hayo katika kila eneo ili pia baadaye tuweze kutoa taarifa ya jumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niendelee kukuhakikishia pia kwamba vyombo vya dola haviko kimya, vinaendelea. Nataka nikuhakikishie vilevile kwamba vyombo vyetu vya dola vinao uwezo wa kusimamia usalama ndani ya nchi, ni suala la muda ni wakati gani wanakamilisha taratibu na hatua gani zichukuliwe. Sasa hilo linategemea na waliotenda matukio na namna ambavyo wamejificha na namna ambavyo na sisi tunatumia njia mbalimbali za kuweza kuyapata haya na kuweza kujua na kutoa taarifa kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nikusihi na familia zote ambazo zimepata athari na zimeripoti polisi na wameripoti kwa vyombo vya dola na vinaendelea kufanya kazi kwamba, pale ambapo tutakamilisha uchunguzi tutatoa taarifa kwa ngazi ya familia ambazo pia zimepata athari au ndugu au jamaa kupata athari hiyo na kuwaambia hata hatua ambayo sisi tunaichukua pia. Kwa hiyo, nataka niwasihi kwamba jambo hili tuendelee kujenga imani kwa vyombo vyetu vya dola vitakapokamilisha kazi zake vitatoa taarifa.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Freeman Aikaeli Mbowe

Gender

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Hai

Question 1

MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, nakubaliana na wewe kwamba maisha ya kila Mtanzania yana thamani kubwa, lakini swali langu lilikuwa specific, sikuzungumza suala la Watanzania wote wanaoathirika kwa matukio mbalimbali. Swali langu lilikuwa very specific ya jambo linaloitwa political persecution, na ningeomba nieleweke hapo.

Mheshimiwa Spika, matukio ya kushambuliwa Mheshimiwa Lissu, lile tukio si la kawaida na naomba tusijaribu kuli-dilute kwa kuchanganya na matukio mengine mengi. Nimeuliza swali specific ambalo ninaomba specific answers. Na uonevu dhidi ya viongozi na wanachama wa vyama vya upinzani nchini umekuwa ni utamaduni wa kawaida. Vyombo vya dola vinafanya, vinatesa watu na vinaumiza watu.

Mheshimiwa Spika, leo ninavyozungumza hivi ni siku ya tatu tangu Mbunge wangu wa Ndanda, Mheshimiwa Cecil Mwambe akamatwe na polisi Mtwara na yuko chini ya custody sasa hivi ni zaidi ya saa 48, kisa alikuwa anafanya mkutano wa kampeni ya uchaguzi katika kata mojawapo pale Mtwara Mjini, polisi wakamshika. Huyu ni Mbunge na Mwenyekiti wa Kanda ya Kusini yenye Mikoa ya Lindi, Mtwara na Ruvuma, yuko ndani siku ya tatu sasa. Sasa matendo haya ya uonevu yanaendelea na hivi tunavyokwenda kwenye uchaguzi wa marudio katika hizi kata chache, viongozi wetu kadhaa wanakamatwa, wanawekwa ndani, wanapigwa na wanateswa.

Mheshimiwa Spika, sasa Mheshimiwa Waziri Mkuu ninachouliza, mimi nilikuomba specific utuambie Serikali inaona shida gani? Kwa sababu si mara ya kwanza kwa Serikali hii kuomba msaada wa vyombo vya uchunguzi kutoka nchi za nje. Wakati Benki Kuu ilipoungua Scotland Yard walikuja hapa kufanya uchunguzi kuhusu jambo hili, ni mambo ya kawaida katika jamii ya kimataifa.

Mheshimiwa Spika, na kwa sababu vyombo vya dola tumevi-suspect kwamba either havikuchukua tahadhari ya kulinda viongozi au havikuchukua hatua ya mapema kuzuia uharifu ule aidha kwa kutaka ama kwa kushiriki. Lakini ambacho napenda nikuambie Mheshimiwa Waziri Mkuu, mimi nina imani kabisa vyombo vyetu vya ndani vina uwezo wala sidharau, ila hakuna dhamira ya kuchunguza jambo hili, hapo ndio kwenye tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kwa sababu hakuna dhamira na kwa sababu wanaoonekana wanaumia ni wa upande mmoja tunaitaka Serikali itoe hiyo clearance. Waje watu wafanye investigation kama ni ku-clear kila mtu anaehusika awe cleared ili jambo hili likomeshwe kwa sababu linaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nakuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu, ni kwa nini sasa usikubali kwa niaba ya Serikali turuhusu vyombo vya uchunguzi vya kimataifa vije vikamilishe jambo hili ili tukate huu mshipa wa fitina?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbowe, Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbowe unaposema jambo hili nilijibu umeliuliza specific, naweza kusema kwamba unapotaka specific basi inabidi sasa vyombo vya usalama vikamilishe kazi yao ndio vije viseme hasa kwa tukio ambao umetaka lizungumzwe. Hakuna mtu yeyote aliyefurahishwa na tendo alilofanyiwa Mbunge mwenzetu. Hakuna mtu yeyote anayefurahishwa na matukio yanayojitokeza huko iwe ya mauaji au ya mashambulio au migongano inayoendelea kwenye jamii yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vyombo vya dola tumevipa jukumu la kusimamia na kuhakikisha kwamba tunalinda usalama wa raia na mali zao kwa kiwango kinachotakiwa. Na pale ambapo kunatokea tatizo, vyombo vya dola vina majukumu ya kuhakikisha kwamba vinafanya uchunguzi na kuwakamata wale wote ambao wamehusika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nimeeleza hapa kwamba wakati wote watenda makosa ni watu ambao wanafanya matendo yale wakiwa wameshajiandaa pia kuweza uovu wao na kujificha dhidi ya vyombo vya dola. Wanapojificha sio kwamba vyombo vyetu vya dola havina uwezo wa kufanya kazi yake ya uchunguzi. Mimi nimekwambia haya matukio yote, wanayo matukio megi yamejitokeza katika kipindi kifupi, tumeanza hayo kama nilivyoeleza na huwa ninapozungumza Kibiti, Rufiji na Mkuranga sina maana ya kuficha au kulifanya jambo hili lisitambulike, hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunachukua mwenendo wa matukio, tunachukua uwezo wa vyombo vyetu na namna vinavyofanya kazi ili kuhakikisha kwamba tunabaini matukio haya na ndiyo sababu wakati wote Watanzania tumeendelea kuwaambia na kuwahamasisha kwamba ni lazima tushirikiane katika kuilinda nchi yetu na kila mmoja ashiriki katika kutoa taarifa. Sisi tunakaribisha mtu yeyote anayejua kama kuna mwelekeo wa jambo hili atusaidie ili
vyombo vya dola viweze kufanya kazi yake kwa urahisi zaidi.
(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, najua unazungumzia kwa upande wako kama Kiongozi wa Kambi ya Upinzani na yeye Mbunge mwenzetu ambaye ni Mheshimiwa Tundu Lissu anatoka kwenye upande wako, lakini utambue kwamba na sisi pia ni Mbunge mwenzetu na jambo hili ni letu pia, lazima tushirikiane kuhakikisha kwamba jambo hili linapata mwelekeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nikuhakikishie vyombo vyetu uwezo upo, lakini pale ambapo wataona kama kuna umuhimu huo, vyombo vyenyewe vitafikia hatua vinaweza vikalieleza, lakini mimi siwezi kuhakikishia Taifa kwamba tumekosa uwezo kwa sababu tunaamini vyombo vyetu vinao uwezo wa kufanya uchunguzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Kiongozi mwenzangu wa Kambi ya Upinzani naomba uamini kabisa kwamba Serikali yetu inayo nia njema, familia za wale wote walioathirika akiwemo Mbunge mwenzetu, Mheshimiwa Tundu Lissu waamini kwamba Serikali yetu inayo nia njema ya kukamata, lakini pia ya kulinda amani ya nchi hii ili kila mmoja, hata sisi pia tuwe na uhakika wa shughuli tunazozifanya za kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tutaendelea kufanya hilo na tutaendelea kuwasiliana nawe kama kiongozi mwenzetu ili uweze kuona haya na namna ambavyo tunaweza tukatatua matatizo haya ya ndani, juu ya matatizo ambayo yanajitokeza kwenye maeneo yetu, ahsante sana.