Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 56 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2017-06-29

Name

Omary Tebweta Mgumba

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Primary Question

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali la kwanza.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, wewe ndiye Kiongozi wa Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi ndani ya Bunge, lakini pia ndiye kiranja mkuu wa Serikali hii ya Awamu ya Tano. Mheshimiwa Waziri Mkuu, kama unavyofahamu kuna wazabuni wengi katika Halmashauri zetu tunakotoka ambao sisi ni wawakilishi wao pamoja na Serikali Kuu, walifanya kazi ya kutoa huduma katika taasisi za Serikali na Serikali yenyewe kwa muda mrefu, wengine wana miaka miwili, mitatu, wengine mpaka mitano, lakini mpaka sasa hawajalipwa stahiki zao.

Mheshimiwa Waziri Mkuu ukizingatia mnamo tarehe 01 Juni ndani ya Bunge hili, uliliambia Bunge hili kwamba malipo yanachelewa ni kwa sababu wanafanya uhakiki, ambalo ni jambo zuri, kuwagundua wale ambao wanastahili kulipwa…

SPIKA: Swali Mheshimiwa Mgumba, moja kwa moja!

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nataka kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu, watu hawa wamesubiri kwa muda mrefu na ukaguzi umeshafanyika zaidi ya mara tano, nini kauli ya Serikali, watawalipa lini wazabuni wote waliotoa huduma ndani ya Serikali?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mgumba, Mbunge wa Morogoro Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba, Serikali inadaiwa na wazabuni wetu waliokuwa wanatoa huduma kwenye maeneo mbalimbali. Wako ambao wametoa huduma kwenye Halmashauri za wilaya kwa maana ya huduma kwenye shule, kwenye magereza, lakini pia wako ambao wamefanya kazi za kutoa huduma kwenye Wizara mbalimbali. Na kwa mara ya mwisho nilikuwa hapa nilipata swali la aina hii linalowahusu wadai/wazabuni wa pembejeo, wote hawa ni watoa huduma ndani ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumeweza kugundua kwamba baadhi ya madeni na baadhi ya wadai wachache miongoni mwao wametuletea taarifa za madai ambayo si sahihi sana. Na kweli, tulichokifanya tulitoa maagizo kwenye maeneo yote, ili kuhofu kupoteza fedha, kulipa fedha ambayo haikufanyiwa kazi kwa madai yale.

Kwa hiyo, tumeendesha zoezi la uhakiki chini ya Wizara ya Fedha na taasisi yetu kupitia CAG, hasa kule kwenye madeni makubwa ili kujiridhisha viwango vinavyotakiwa kulipwa kwa wazabuni hawa.

Mheshimiwa Spika, tuliweka utaratibu kwamba angalao kufikia mwishoni mwa mwezi huu tuwe tumemaliza hilo zoezi la uhakiki halafu tuanze kulipa madeni haya. Kwa hiyo ni matarajio yangu kwamba Wizara ya Fedha watanipa taarifa, na Wizara zile zote ambazo zina madeni ya watoa huduma zitatoa taarifa ya viwango vya fedha, halafu sasa tusimamie Wizara ya Fedha kuweza kuwalipa hawa watoa huduma.

Mheshimiwa Spika, nataka nitumie nafasi hii, kwanza niwashukuru kwa uvumilivu wao wadeni wote wanaotudai, lakini pili tuwasihi waendelee kutuvumilia na taratibu hizi kwa lengo lilelile nililokuwa nimelieleza awali la kuokoa fedha ambazo zinalipwa kwa watu ambao hawakutoa huduma. Hata hivyo bado tutaendelea kuwatumia watoa huduma kutoa huduma ndani ya Serikali kwenye maeneo ambayo wameendelea kutoa huduma na tuwahakikishie tu kwamba tutawalipa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge kama wako watoa huduma kwenye eneo lako endelea kuwahakikishia kwamba Serikali tutlipa madeni. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Omary Tebweta Mgumba

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Question 1

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kuna swali dogo tu la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa majibu mazuri ambayo kutoka Serikalini.

Swali dogo la tu la nyongeza, kwa kuwa kama ulivyosema kwenye majibu yako ya msingi, kwamba mmegundua kuna watu ambao wameleta madai ambayo si sahihi, lakini naamini pia kuna watu ambao watakuwa madai yao ni sahihi. Sasa nini kauli ya Serikali kwa wale ambao madai yao ni sahihi ambao wamekaa muda mrefu kiasi kwamba imewaongezea gharama kwa maana ya riba sehemu walizokopa, nani atalipa gharama hizi kwa ajili ya usumbufu uliotokea na gharama zilizoongezeka kwenye madeni hayo?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mgumba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeeleza kwenye jibu la awali kwamba kwanza tunathamini sana kazi waliyoifanya katika kutoa huduma kwenye sekta zetu. Lakini mbili, tumewashukuru kwa uvumilivu kwa kipindi chote hiki ambacho sisi tunafanya uhakiki. Baadhi ya wadai nimepata nafasio ya kukutana nao hapa Dodoma wakati huu wa Bunge na kuzungumza nao na kuwaambia kwa nini tumechelewa kuwapa fedha zao, wale ambao kweli wana madai halali.

Mheshimiwa Spika, lakini bado nirudi tena kusema kwamba, hatuna namna nyingine ya kufanya zaidi ya uchelewaji huu wa kulipa kwa sababu tuko kwenye zoezi la kuhakiki, ili tujiridhishe. Kama ingekuwa tumechelewa tu, kwamba hatuna kazi yoyote, tumeacha tu hapo kungekuwa na swali ambalo naamini unacholenga kingeweza kupata maelezo. Lakini bado niwahakikishie kwamba taratibu zinakamilika na tulisema tunakamilisha tarehe 30 Juni, yaani kesho tu tarehe 30 Juni, tunatarajia Wizara ya Fedha itapewa taarifa kutoka kwenye Wizara mbalimbali, kwamba madai yetu halali ni haya kwa ajili ya watu hawa kwa huduma waliyoitoa, baada ya hapo tunalipa tu na tutaendelea kuwapa nafasi zaidi ya kutoa huduma.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niwahakikishie kwamba wataendelea kutoa huduma, hasa wale ambao ni waaminifu kwenye awamu ijayo hii ya mwaka wa fedha mpya wa mwaka 2017/2018.