Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Emmanuel Lekishon Shangai (19 total)

Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na binafsi nikupongeze kwa sababu najua umechaguliwa siku ile nami nikaapishwa; kwa hiyo mimi ni Mbunge wako uliyemuapisha kati ya Wabunge wote waliopo kwenye Bunge hili.

Mheshimiwa Spika, pia niipongeze Kamati kwa taarifa yao nzuri. Hata hivyo nitoe taarifa kwenye Bunge lako Tukufu kwamba eneo la Ngorongoro haliwezi kufa, kwa sababu wananchi walioko katika Eneo la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ni wananchi ambao ni wahifadhi namba moja tofauti na wahifadhi wa vitabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi waliopo Tarafa ya Ngorongoro au Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ambayo inaongozwa kwa mfumo wa ardhi mseto ni wananchi ambao katika eneo hilo wameishi miaka 60 bila kula wanyama na bila kuwa wawindaji. Wananchi hao sasa hivi tukiona kwenye vyombo vya habari wako very victimized, wanaitwa ni majangili, ni watu maskini ndani ya Tanzania, as if kwamba kuna ombaomba katika eneo la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, kuna vyombo vya habari ambavyo sasa hivi kila siku ni kuandika kuhusiana na eneo la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, kwamba wananchi sasa hivi ni tatizo. Nadhani Serikali kwanza ingewatambua wale wananchi kama wahifadhi waliohifadhi kwa niaba ya wananchi wengine milioni 60 wa Tanzania, lakini si kuwaona kama tatizo.

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe taarifa kwamba, kwenye eneo la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro watoto wanakwenda shule, si kama inavyotangazwa kwenye vyombo vya habari vya akina Kitenge. Kule kwetu kuna shule za msingi 30 na watoto wanakwenda shule; kuna vituo vya afya, kuna zahanati, kuna maendeleo mengine ambayo Watanzania wengine wanayo. Kama imefika sehemu tunaona labda ni tatizo, mheshimiwa Rais tarehe 16 mwezi wa Kumi, akiwa Arusha alisema kwamba ni lazima tukae na wananchi ili tutafute suluhu ya changamoto zilizopo katika eneo la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niishauri Kamati pamoja na Wizara, kwamba ni lazima kukaa na wale wananchi. Kwa hali ilivyo kwa sasa, kumekuwa na enmity kubwa sana kati ya Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na wananchi waliopo ndani ya eneo la Hifadhi ya Ngorongoro; huku tukijua kwamba wananchi hao wako kisheria, hawajavamia. Wale wananchi walikuwepo na waliingia mkataba na mkoloni mwaka 1959 wakati walipofanya makubaliano kutoka Moru – Serengeti kutoka mwaka 1918 mpaka mwaka 1948, ndipo wananchi wale wakaamua kuhama kutoka Serengeti na kuja katika maeneo ya higher land ambayo ni Ngorongoro ya sasa (Makofi).

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tunawaona wale wananchi kama ni wananchi ambao ni wavamiaji. Hao waandishi wa habari wa mitaani, anatoka mtu anasema nimesafiri kilometa 400 kumtafuta tembo Ngorongoro, hiyo si kweli. Ngorongoro tembo wako njiani kwa wale waliokwenda na ni wapi katika eneo la Hifadhi ya Ngorongoro unaweza ukasafiri kilometa 400 katika eneo la square kilometer 8,100? Hakuna. Sehemu ya mbali ni Nayobi ambayo ni kilometa 80 na sehemu nyingine ni Kakensya ambayo ni kilometa 75, hakuna sehemu unayoweza ukatembea hivyo. Kwa hiyo, niombe, kwanza, Serikali iingilie kati utumiaji wa vyombo vya habari kwa ajili ya kuwaonesha wananchi wale kama hawafai.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ole-Sendeka amesoma lile gazeti. Ukisoma kama mwananchi uliye Ngorongoro, ukaona jinsi unavyoandikwa, unaishi na wanyama, unaishi na pofu, unaishi na wanyama wote na pundamilia, wanalala mpaka bomani, lakini unaonekana kama mtu ambaye hufai. That is totally haihitajiki katika maisha haya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi ni…

T A A R I F A

SPIKA: Mheshimiwa Olelekaita.

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge wa Ngorongoro kwamba sheria nchi hii hairuhusu kabisa aina ya reporting iliyofanyika na magazeti hayo na kwamba kuna regulation inaitwa The Electronic and Postal communication (online contempt regulation, 2018) inakataza aina ya publication inayo-cause public disorder, bad language, discouraging, abuse na calculated words to offend a particular group ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo sheria za nchi zinakataza na ni suala tu la Mheshimiwa Attorney General na Serikali kuliangalia hili ili haya yasitokee. Ahsante sana.

SPIKA: Mheshimiwa Emmanuel Shangai.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, kuhusiana na eneo la Pori Tengefu la Loliondo; najua pori hilo lilitangazwa pamoja na mapori mengine 49 mwaka 1974 kwa G/N 459, lakini ukijaribu kuangalia, baada ya kutangazwa mwaka 1974 Waziri alitakiwa kutangaza ndani ya miezi 12, lakini hayakufanyika hivyo.

Mheshimiwa Spika, eneo la pori tengefu tunaloliongelea watu wengine huku nje tunaona kama vile ni ardhi ambayo haina watu. Ardhi ile inakaliwa na wananchi zaidi ya 80,000, kuna vijiji zaidi ya 23, kuna kata nane. Sasa leo hii ukisema uchukue kilometa 1,500 wale wananchi hawana sehemu nyingine ya kwenda na wala hawana sehemu ya malisho kwa ajili ya mifugo yao na huku tukijua kwamba Wilaya yetu ya Ngorongoro asilimia 95 ni wafugaji, wanategemea mifugo.

Mheshimiwa Spika, bahati mbaya Mkuu wa Mkoa alikwenda Loliondo, amekwenda kutoa matamko ambayo yameleta taharuki ndani ya Wilaya ya Ngorongoro. Kwa sasa hivi wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro na niiombe Serikali kutafuta namna ya kutuliza hali ile ambayo inatumika na magazeti na baadhi ya watu ambao hawana nia na wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, niiombe tu Serikali, kama ina nia njema ya kutatua matatizo ya Wilaya ya Ngorongoro ni lazima ikae na wananchi meza moja na kutafuta njia ya kutatua changamoto zilizopo.

Mheshimiwa Spika, Kamati imeweka vizuri, kwamba tutafute namna bora ya kutatua matatizo yale. Kwa sababu wananchi wetu wanategemea kwamba Serikali yao itawasaidia, itawasikiliza na kuwaletea maendeleo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa nafasi na mimi kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, kwanza niwapongeze Serikali kwa kazi nzuri wanayofanya. Kule Ngorongoro kazi kubwa imefanywa sana na Serikali kwa kutupa miradi mikubwa ya maji, hasa mradi wa vijiji Nane ambao unaitwa ni mradi wa Mageri. Nimpongeze na Waziri wa Maji kwamba ameweza kufika na kufuatilia kwa kila hatua, amefika zaidi ya mara tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa sijawatendea wananchi haki nisipozungumzia suala la bei ya mafuta na vyakula. Kwa sasa hivi kule nje maisha ya wananchi ni magumu sana, kule Loliondo sasa hivi watu wananunua mafuta ya dumu la lita tano kwa Shilingi 40,000, sukari imeenda Shilingi 3,500 lakini tunakaa huku tunajifungia tunasema ni kwa sababu ya vita vya Ukraine, kuna tatizo kule nje.

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Serikali na ninaishauri Serikali ni wakati muafaka sasa Serikali kupita kwa wazalishaji wote na kuangalia kwamba bei ya vyakula na bei ya mafuta je, ni uhalisia au ni artificial? Ni muhimu sana Serikali kuliangalia hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala ambalo tunalizungumzia la barabara, Wilaya ya Ngorongoro haijaunganishwa na Mkoa wa Arusha haijaunganisha na nchi ya Jirani. Tunaishukuru Serikali kwamba imetupa barabara ya lami ya Kilomita 50 kutoka Loliondo mpaka Sale, lakini bado tunahitaji barabara ya lami kutoka Sale mpaka Mto wa Mbu au Kigongoni. Kwa hiyo, ninaiomba Serikali iweze kuiangalia Wilaya ya Ngorongoro kwa sababu maisha ya wananchi yanakuwa magumu kwa sababu hatujaunganishwa na Mkoa wetu wa Arusha na ndiyo maana hata bei ya vyakula inapanda kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kuna suala ambalo Ofisi ya Waziri Mkuu imefanya kule Ngorongoro, ninashukuru kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu amekubali kupokea maoni ya wananchi kuhusiana na eneo la pori tengefu na Ngorongoro. Hiyo ni nia njema ya Serikali na nimshukru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa sababu amekuwa tayari wakati wote tukizungumza na yupo tayari kuwapokea watu wangu, aliwapokea Maleigwanani, akazungumza nao na tukakubaliana kwamba tutamletea maoni ya wananchi. Kwa hiyo nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hilo. Hiyo ni nia njema ambayo itatusaidia kutatua matatizo yaliyopo Ngorongoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kulielezea Bunge lako na kuelezea masikitiko yangu kwa mbaadhi ya mambo yanayoendelea sasa hivi. Wananchi wa Ngorongoro hawana shida na mtu yeyote ambaye ana hiari ya kutoka Ngorongoro naomba niweke wazi hilo, hakuna mtu mwenye shida na mtu yeyote pale. Wale wote waliojiandikisha kwa ajili ya kuondoka kama Serikali ilivyosema hakuna mtu ambaye anawazuia, ninawashangaa waliojitokeza kusema kwamba wanaomba ulinzi wasipewe ulinzi hakuna shida wataondoka kwa amani.

Mheshimiwa Spika, kuna tatizo moja kwa sasa hivi wale wanaobaki ambao watakuwepo Ngorongoro inaonekana kwamba Serikali inawawekea vikwazo vya kimaendeleo, kuna fedha ambazo zilipelekwa kwa ajili ya vituo vya afya, kwa ajili ya maji, kwa ajili ya madarasa, inaonekana sasa Serikali inahamisha zile fedha kwenda Halmashauri ya Handeni.

Mheshimiwa Spika, Walimu wameandikiwa vituo vya afya wameandikiwa kwamba hizo fedha zihamishwe ziende Handeni. Ninachojiuliza sasa Serikali imeona watu wa muhimu pale Ngorongoro ni wale wanaohiari kuondoka? Wale wanaobaki maisha yao yatakuwaje kama tunawanyima vituo vya afya, kama tunawanyima maji, kama tunawanyima shule; Je, wale wananchi watakuwa sehemu ya Watanzania?

Mheshimiwa Spika, suala lingine kwenye zoezi ambalo linaendelea chini ya ofisi ya Mheshimiwa Nape la anuani ya makazi, kule Ngorongoro hakuna zoezi hilo, Tarafa ya Ngorongoro hakuna zoezi hilo kwanini tusiwahesabu wananchi tukaendelea na program zingine?

SPIKA: Mheshimiwa Ole Shangai kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Innocent Bashungwa.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa mchango wake mzuri, lakini ninapenda kumuondoa wasiwasi, wananchi wote ni wa kwetu kule Handeni tunapeleka miradi lakini hata Tarafa ya Ngorongoro kazi inaendelea. Kwa hiyo asubiri bajeti yangu tutamuonesha ni namna gani ambavyo tumejipanda kuhakiksiha hata Tarafa ya Ngorongoro miradi inaenda kama kawaida. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ole Shangai unaipokea taarifa hiyo?

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, hiyo taarifa siIpokei.

Mheshimiwa Spika, kwa nini sipokei taarifa hiyo, wananchi gani hawa ambao unawasubirisha bajeti nyingine, wakati fedha ambazo zipo kwenye akaunti unaondoa kupeleka Handeni. Leo fedha Shilingi Milioni 500 ambazo zilikuwa kituo cha afya Nainokanoka mnahamisha kupeleka Handeni, fedha Shilingi Milioni 600 kwa ajili ya maji Kata za Alaitolei, Masamburai, Oloirobi na maeneo mengine mnahamisha kwa ajili ya kuwawekea wananchi vikwazo vya kimaendeleo.

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, taarifa!

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, naomba ulinde muda wangu.

SPIKA: Mheshimiwa Ole Shangai kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Waziri wa Maji, Mheshimiwa Aweso.

T A A R I F A

WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza ninampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa anayoifanya katika Jimbo lake, lakini nataka nimhakikishie kwamba hakuna maelekezo yoyote ambayo Wizara ya Maji tumepewa tusiendelee na shughuli za maji pale.

Mheshimiwa Spika, tuna mitambo ambayo ipo inatekeleza uchimbaji pale katika Jimbo lake, nami kama Waziri wa Maji nimefika. Nataka nimhakikishie na shughuli zinaendelea na Mheshimiwa Waziri Mkuu ametupa maelekezo mahsusi ya kuhakikisha visima vile vinakamilika kwa wakati. Ahsante sana.

SPIKA: Mheshimiwa Ole Shangai unaipokea taarifa hiyo?

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Taarifa hiyo naipokea lakini anachozungumza Mheshimiwa Waziri yeye anazungumzia miradi ya maji inayoendelea Tarafa ya Sale na Loliondo siyo Tarafa ya Ngorongoro, hakuna mrdi wowote wa maji unaoendelea Tarafa ya Ngorongoro hakuna! Sasa hivi miradi yote imesitishwa na Serikali kwa sababu ya kuwawekea wananchi vikwazo vya kimaendeleo.

Mheshimiwa Spika, kwa nini tunawawekea vikwazo? Wananchi hawa wamekuwa pale kwa miaka 60, is it a nightmare tukawaondoa kwa siku moja? Kwa mfano, hospitali ya Enduleni ilikuwa inapata shilingi milioni 500 kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro kwa ajili ya kuwatibu wananchi imeondolewa pia.

Kwa hiyo, watoto wadogo akinamama wanakufa kwa kukosa huduma!

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali gani hii sasa ambayo inawawekea wananchi vikwazo? Kama tunataka kupunguza watuNgorongoro siyo kwa namna hiyo ya kuwawekea vikwazo vya kimaendeleo. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ole Shangai kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze mwenzangu kwa mchango wake mzuri, lakini nimhakikishie tu na nimuondoe wasiwasi kwamba hata jana Shilingi Milioni 321 zimetengwa kupitia Global Fund kuelekea kwenye eneo analolitaja la Enduleni. Kwa hiyo, asiwe na wasiwasi kimsingi inawezekana source za taarifa zimemtisha lakini nikuombe tu kwamba hilo jambo litasimamiwa na uamini ambacho Waziri wa TAMISEMI amekisema na wengine wanachokuambia, tuanze kushirikiana kuanzia sasa tuone tunaenda Pamoja. Kama ambavyo Waziri Mkuu amekuwa akishirikiana na ninyi basi na hayo mengine tushirikiane kwa pamoja tutakwenda vizuri.

SPIKA: Mheshimiwa Ole Shangai unapokea taarifa hiyo?

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, napokea taarifa hiyo kwa masharti, nendeni kwa wananchi mkawaambie mnachosema hapa. Kwa sababu, kinachosemekana hapa ni ili tu tumalize hapa, lakini kinachoendelea Ngorongoro kama walivyoshauri Wabunge wakati mwingine ni bora Bunge hili likajiridhisha kwamba yanayoendelea Ngorongoro siyo haki kwa wananchi wale!

Mheshimiwa Spika, wakinamama mpaka wasafiri Karatu wakapate huduma za afya sasa hivi, vituo havina dawa wananchi tunawawekea vikwazo vya kimaendeleo kwa ajili gani?

Mheshimiwa Spika, leo ukijaribu kwenda pale kupita kwenye geti la Ngorongoro wameweka vikwazo kibao, wananchi ili uingie ni lazima upekuliwe na wengine wanarudishwa hawajui pa kwenda kulala Karatu, unakuta ni mgonjwa alikuja Karatu anazuiliwa getini.

Mheshimiwa Spika, nadhani kwa Serikali inayojali utu, kwa Serikali inaowajali wananchi wake, ni muhimu sana tusifanye zoezi hili la watu kuhiari kutoka Ngorongoro kama ndiyo njia ya kuwaumiza wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro wanaobaki. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, hii itakuwa ni taarifa ya mwisho kwa mchangiaji Ole Shangai, Mheshimiwa Kundo. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Mbunge katika yale ambayo anatamani wananchi wake wafanyiwe. Bahati nzuri tulifika katika Jimbo lake na Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoa maelekezo kwa sababu ni Serikali kuhakikisha kwamba wananchi wake wanasogezewa huduma za msingi na kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, upande wa mawasiliano tunapeleka huduma ya mawasiliano kujenga minara zaidi ya 24 ndani ya Jimbo la Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge awe na amani kabisa kwamba ndani ya Jimbo lake la Ngorongoro tunakwenda kufanya kazi nzuri sana, asiwe na wasiwasi kuhusu anuani ya makazi na Postcode. Nashukuru. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ole Shangai unaipokea taarifa hiyo?

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, sasa taarifa iliyotolewa na Naibu Waziri, Ngorongoro kuna Tarafa tatu, Tarafa ya Loliondo, Tarafa ya Sale na Tarafa ya Ngorongoro ambayo ndiyo naizungumzia. Kama Naibu Waziri ana uhakika kwamba anazungumzia Tarafa ya Ngorongoro naomba list ya Kata ambazo utapeleka minara hiyo, ziwe kwenye Tarafa ya Ngorongoro na siyo Tarafa ya Sale na Loliondo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala ambalo lipo liliwasilishwa kwenye hotuba ya Waziri Mkuu kwamba, sasa hivi tunaanzisha mashamba darasa ya kulima nyasi kwa ajili ya mifugo. Wakasema kuna moja lipo Loliondo, mimi ninaamini kwamba Serikali inatakiwa kutatua matatizo ya wananchi wake na tunatakiwa kutatua matatizo kwa muda mfupi na muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, naamini kwamba kwa eneo letu la Loliondo, wananchi wataleta maoni yao chochote kile ambacho kinatakiwa kufanyika tuache mpaka maoni ya wananchi yafike kwanza, tuone wananchi wanavyofikiria kuhusiana na eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo mimi nashukuru lakini wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro wasiwekewe vikwazo vya kimaendeleo. Nashukuru sana (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Awali ya yote ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwamba ameendelea kunilinda na kwamba nipo hai sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Rais, kwa kuendelea kuwatumikia Watanzania kwa weledi mkubwa sana, ninamshukuru pia kwamba kwenye Jimbo letu la Ngorongoro tumeendelea kupata fedha nyingi sana kwa ajili ya maendeleo zikiwepo fedha za afya, elimu, maji pamoja na umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba pia nichangie hoja ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia katika Bunge lako, kuhusiana na masuala ya ufisadi kwenye nchi yetu. Nimesikia kwamba Wabunge wengi wanasema hao watu watupishe. Watupishe waende wapi? Wanatakiwa warudishe fedha za Watanzania ndiyo waweze kitupisha, hili linatakiwa kufanyika na wale wote waliopewa mamlaka na Mheshimiwa Rais, kwa sababu inaonekana Mheshimiwa Rais yeye amechukia ufisadi sana, lakini inaonekana kwamba baadhi ya watu ambao ni wateule wa Mhehsimiwa Rais, hawauchukii ufisadi ndiyo maana tunamuona Rais anachukia lakini watu wengine wamenyamaza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo langu la Ngorongoro tumepata fedha nyingi kwa ajili ya maendeleo lakini kunakuwepo na vikwazo vingi sana. Kwa mfano, leo Wizara ya TAMISEMI inaleta fedha kwa ajili ya ujenzi wa madarasa lakini unampa mtu wa Ngorongoro shilingi milioni 20 ajenge darasa sawa na mtu aliyeko Dar es Salaam! Kule ukitoa cement kutoka Arusha mpaka Ngorongoro cement inafika kwa shilingi 25,000. Mwananchi aliyeko Arusha Mjini ananunua cement kwa shilingi 16,000. Inatakiwa tunapotoa fedha kwa jaili ya miradi ya maendeleo tuangalie umbali na mazingira katika Majimbo yetu. Siyo unampa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro milioni 20 ajenge darasa na hivyo hivyo unampa mtu wa Dar es Salaam Milioni 20, Mkurugenzi wa Dar es Salaam ananunua cement kwa shilingi 14,000 mpaka 15,000 lakini Ngorongoro cement inafika kwa shilingi 25,000, yule Mkurugenzi utakuwa unamuonea! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunawaomba watu wa TAMISEMI wanapanga miradi ni lazima waangalie maeneo wanayopeleka hizo fedha. Unampa Mkurugenzi shilingi milioni 400 ajenge Sekondari akiwa Dar es Salaam, akiwa Morogoro unampa pia na wa Ngorongoro ajenge kwa shilingi milioni 400. Wakati kule hata lori ya mchanga ni zaidi ya shilingi 300,000 lakini kusafirisha kutoka Arusha mpaka Ngorongoro unatumia gari za shilingi 1,500,000 mpaka Ngorongoro wakati mtu wa Arusha anakodisha gari kwa shilingi labda 200,000 tu. Kwa hiyo, ukijaribu kuangalia ni lazima tutekeleze miradi, tutenge fedha za miradi kwa kuangalia maeneo. Majimbo yetu yaliyoko mbali ni lazima tu – consider cost tunazowapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo letu la Ngorongoro huduma zetu za afya bado ni duni sana. Ukijaribu kuangalia kwenye Kata zetu. Kati ya kata 28 unakuta kwamba ni zaidi ya Kata Sita tu ndiyo zenye vituo vya afya lakini Kata nyingine 22 hakuna vituo vya afya. Kwenye Vijiji pamoja na Kata hakuna zahanati, lakini mwaka jana Serikali ilisitisha huduma kwa ajili ya ndege ya Fly Medical Service iliyokuwa inatoa huduma ya chanjo kwenye vituo 18 ndani ya eneo la Ngorongoro. Kupitia Hospitali ya Wasso kulikuwa kuna vituo 10, kupitia Hospitali ya Kanisa ya Endulen walikuwa wana vituo Nane lakini Serikali imesitisha huduma hiyo. Kwa hiyo, wale wananchi waliokuwa wanahudumiwa kwenye vituo 18 kwenye Kata ambazo hazina zahanati na Serikali haijafikisha barabara katika yale maeneo wananchi wale hawapati huduma ya chanjo, watoto wadogo pamoja na wakina mama wajawazito.

Mhehsimiwa Naibu Spika, ninaishauri Serikali tuiangalie kwa sababu ndege ile imesajiliwa Marekani mwaka 1979 na imetoa huduma Tanzania kwa miaka yote 44 bila shida, lakini hatujui ni nini kimetokea mwaka 2022 ndege ile ikanyimwa kufanya kazi. Wale wananchi wakina mama wajawazito ambao hawana namna ya kufikia hospitali na watoto kupata chanjo ni wakati muafaka sasa Serikali kuwaruhusu wale wamisionari waweze kutoa huduma tena katika eneo la Ngorongoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaishauri Wizara ya Afya pamoja na Wizara ya Uchukuzi, Waziri wa Afya Mheshimiwa Ummy Mwalimu anajua nilishamwandikia, Waziri wa Uchukuzi anajua, pamoja na Waziri Mkuu anajua nilishamwambia suala hili kwa muda mrefu, toka mwaka jana mwezi wa Sita mpaka sasa hivi kuna watoto wadogo wanazaliwa na ambao wana miezi Tisa sasa hawapati huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Waziri Mkuu ilikuwa inaratibu suala lingine la kuhama kwa hiyari eneo la Ngorongoro. Suala lile hakuna mtu anayepingana na mtu anayehama kwa hiari, wananchi wamendelea kwenda wenyewe. Tumeona kwenye ripoti ya CAG kwamba wananchi waliohama ni 2.5 percent ambayo ni kaya 500 zenye watu zaidi ya 2,580, lakini wananchi wengine waliobaki kwa sensa ya juzi ni zaidi ya kaya 25 ambazo zina watu zaidi ya 100,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakaa, siku ile Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema hapa kwamba ni suala la hiyari, lakini wananchi waliobaki zaidi ya 100,000 ukienda kwenye eneo la Tarafa ya Ngorongoro kuna shule zaidi ya 26 za msingi zenye watoto zaidi ya 18,167. Watoto wa Sekondari zaidi ya 3,250 hakuna vyoo, watoto wanaenda chooni porini kwa sababu Serikali imekatalia kujenga vyoo, vyoo vimejaa, hawatoi ruhusa ya wananchi kujenga vyoo kwa ajili ya watoto wao, kwa nini hili linatokea kama suala lenyewe ni hiari kwa nini watu walazimishwe kuishi katika maisha ambayo hayafai kwa binadamu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninashauri kwamba ni lazima Serikali iweke wazi lengo lao kwenye eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, kama ni kuhama kwa hiari watu wanaondoka lakini mpaka leo watu waliojiandikisha ni kaya 1,500, lakini mpaka leo wamechukua kaya 500. Wale waliobaki kaya zaidi ya 1,000 hawana mbele wala nyuma hawajui wanafanya nini, wako stranded katika maisha yao hawawezi kuendelea tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ninaomba katika eneo letu la Tarafa ya Ngorongoro Wizara ya TAMISEMI inapanga fedha inapelekwa wananyimwa vibali kwa ajili ya kujenga na watoto wanakaa madarasani mpaka nje. Ni lazima Serikali iweke wazi wale wananchi wasiendelee kuishi kama watu ambao hawatambuliki kama watu ambao hawatambuliki katika nchi yao. Ni vizuri tujue kwamba wale wananchi wako pale lakini suala hili ni la hiari. Suala lenyewe limekuwa ni upigaji mtupu, angalia leo usafiri kutoka Ngorongoro mapaka Handeni gari ni sawa na kontena kutoka China kuja Tanzania ni ufisadi mtupu. Watu wanajitochotea fedha, watu wanawalipa watu ambao hawahusiki, unakuta nyumba zingine ni hewa. Nyumba unaandikiwa namba 59 hiyo nyumba haipo, mkatafute, au nyumba namba 57 na 58, 55 na 56, nyumba hazipo, watu wanajiandikia wanajichukulia fedha za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kilichoonekana kwenye ripoti ya CAG ninaishauri Serikali mkafuatilie ule mradi muone kwamba ni mradi wa watu ambao ulibuniwa kulikuwa kuna fedha ambazo zipo walitaka wale wakakosa njia. Eneo la Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro sasa hivi watu wanasema limejaa lakini eneo lenye watu ni five percent only, maeneo mengine yako wazi, bado inaweza kumudu model ya multiple land use model.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende tena kwenye suala la barabara yetu ya lami kutoka Wasso mpaka Sare. Tunaishukuru Serikali kwamba tumepata kilomita 49, lakini niiombe Serikali muendelee kutuangalia, Ngorongoro barabara iliyopo ni hiyo moja na ndiyo inashikilia uchumi wa Wilaya yetu ya Ngorongoro. Nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, kwamba aliahidi kilomita 50 tunaiomba kwenye bajeti hii iweze kututengea kwa ajili ya wananchi wa Jimbo la Ngorongoro nao kunufaika na matunda ya rasilimali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni suala la umeme. Tunazo Kata za Malambo, Samunge, Pinyinyi pamoja na Kata ya Kirangi eneo la Mageri pamoja na Bwero Kata ya Samunge na maeneo mengine ambayo hayana umeme kwenye Jimbo letu la Ngorongoro. Wameweka nguzo zaidi ya miaka 5 mpaka sasa hivi nguzo zingine zinaanguka, ninaishauri Serikali sasa iweze kumalizia miradi ya umeme kenye Wilaya yetu. Wananchi wanahitaji maenedeleo na umeme ni maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo ningetaka kulizungumzia ni suala la elimu. Wataalam wanasema ukitaka kuliua Taifa uharibu vitu viwili. Suala la kwanza ni afya pamoja na elimu. Kwenye shule zetu za msingi tunakuwa na mrundikano mkubwa wa wananfunzi ambao inapelekea wengi kuhitimu Darasa la Saba hawajui kusoma na kuandika, nimesikia pia Wizara ya Elimu wako katika utaratibu wa kuweza kubadilisha mitaala yetu. Nafikiri tusifanye elimu kama eneo la majaribio.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti ya Serikali. Mimi nimshukuru na kumpongeza Kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa bajeti nzuri pamoja na Serikali kwa ujumla.


Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeweka mikakati mingi sana lakini mwisho wa yote tunachokusanya ndicho kitakacho-determine kile ambacho tutaenda kufanya. Tusipokusanya vizuri hatuwezi kutekeleza mikakati yote ambayo tumeweka kama Serikali. Bajeti hii itaenda kutekelezwa vizuri kama tutaweka nguvu nyingi sana kwenye ukusanyaji wa fedha pamoja na kuamua kuondoa mianya yote ya rushwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Wilaya yangu ya Ngorongoro nilishamwambia Mheshimiwa Waziri kwamba tunahitaji tujengewe kituo cha forodha mpakani mwa Kenya na Tanzania. Wananchi wale wanataabika sana kufanya biashara. Kutoka Loliondo mpaka Namanga ni zaidi ya kilomita 120. Kwa hiyo, mpaka wetu bado ni mkubwa sana, tukijenga Serikali itakusanya mapato makubwa katika lile eneo pamoja na wananchi kufanya biashara kiurahisi katika lile eneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala lingine Mheshimiwa Waziri is not your classic kwenda kuchukua fedha za asilimia 10 ya Vijana pamoja na akina mama kwa ajili ya kuwapa machinga. Kwa hiyo, na mimi nishauri kama alivyosema Nusrat Hanje, kwamba tuache hilo, tusifikirie kabisa. Tunaweza kukusanya fedha katika maeneo mengine ambayo itaisaidia Serikali na wale akina mama pamoja na Vijana nao wanufaike na hiyo asilimia 10 katika ngazi ya halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoshauri katika halmashauri zetu kuna upotevu mkubwa wa mapato; nina uwezo wa kutoa ushuhuda. Nilipokuwa Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro niliamua siku moja kwenda kukusanya mapato mwenyewe kwenye mnada ambao wataalamu walikuwa wanakusanya shilingi 1,000,000, nilikusanya shilingi 5,000,000. Nikasimamia mnada huo consecutively for four months; kwa sababu tarehe 15 na tarehe 02 nikakusanya shilingi milioni 40. Lakini ukiangalia data za wataalam wetu wao kwa miezi minne wanakusanya shilingi 5,000,000. Sasa kule chini kuna upotevu mkubwa. Nikawapa Madiwani kwenye minada mingine. Nikawaambia hebu tusimamie tuone kwamba ni kwamba hakuna fedha au ni wataalam hawakusanyi. Kila mnada aliyesimamia Mheshimiwa Diwani ili-double na ku-triple kwa wakati mwingine. Mnada ambao wao wanakusanya 1,000,000 sisi tukawa tunakusanya zaidi ya 4,000,000 kwa mwezi, lakini wao wanakusanya 1,000,000. Fedha nyingi za Watanzania zinaenda kwenye mifuko ya watu wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwaombe TAMISEMI msimamie ukusanyaji wa mapato, kule Wakurugenzi hawakusanyi mapato. Tulitakiwa kukusanya zaidi ya bilioni 800, tumekusanya 700 na hamsini na kitu. Kwenye Halmashauri zetu tuna uwezo wa kukusanya mpaka trioni mbili tukiamua kuwapa watu waadilifu, lakini tukiendelea hivi tutaendelea na story zilezile kila siku. Hata hii asilimia 10 wananchi wetu wangekuwa wananufaika sana kama makusanyo yangefanyika. Lakini pia TRA tunapoteza fedha nyingi sana kwenye misamaha ya kodi ambayo haina maana. Ni lazima sasa Mheshimiwa Waziri usimamie hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala lingine ni suala la kuondoa ada kidato cha tano na sita; niipongeze Serikali, lakini iendane sambamba na kuondoa michango ambayo haina maana. Kwa mfano leo mwanafunzi anaenda kuripoti shule hiyo ina zaidi ya miaka 50 unamwambia aende na kiti na meza. Ina maana kwa miaka yote kila mwanafunzi anayemaliza anaondoka na meza na kiti chake? Kila mwaka tunachanga fedha kwa ajili ya viti na meza? Haiwezekani! Kwa hiyo, niipongeze Serikali kwa kuondoa ada hiyo kwa sababu itawasaidia Watanzania wengi, lakini iendane sambamba na kuondoa michango ambayo haina maana kwa Watanzania kama kweli tunataka kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza haya niende kwenye hoja ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia. Wengi hawajui kinachoendelea katika eneo la Pori Tengefu la Loliondo. Mimi ni Mbunge, ni wananchi wangu ndiyo wanaoteswa kule. Naomba niwaambie kitu kimoja, watu wengi hapa wanasema, akinyanyuka mtu anasema kwamba ardhi ya Tanzania ni ya Rais. Tusimchonganishe Rais na wananchi, ardhi ya Tanzania kwa mujibu wa Sheria ni ya Umma. Rais amepewa kama mdhamini tu. Kwa hiyo kwa mtu yoyote anayesimama ukitaka soma Land Policy ya Tanzania ya mwaka 1997. Naomba kunukuu kipengele “(a) All land in Tanzania is public land, versed in the President as a trustee on behalf of all Tanzanian.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wengine tunasimama wanaofanya kazi inayofanyika Loliondo siyo Rais ni watendaji wake ambao hawataki kujifunza kutoka kwa waliyowatangulia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ni lazima tujue, ardhi square kilometer 1,500 katika eneo la Loliondo ni ardhi ya vijiji; kata nane, vijiji 14. Na kwa nini ardhi ile inatwaaliwa, Sera yetu ya Ardhi inatuambia nini kuhusiana na unapotaka kuchukua ardhi ya wananchi, ardhi ya vijiji? Kipengele Na. 4 inasema; “Consultation and consent of all Village council will be required whenever alienation of Village land is necessary”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule Loliondo kinachofanyika ni unyakuaji wa ardhi, hakuna mwananchi, hakuna Serikali ya Kijiji ambayo imeridhia ardhi ile kutengwa, hakuna. Lakini watu wanasema ni ardhi, it’s not a bared land, is the land with people. Kwa hiyo, kinachofanyika pamoja na masuala mengine lakini ieleweke wananchi wa Loliondo…

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Ridhiwani.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa msemaji anayesema sasa asipotoshe. Kinachofanyika Loliondo ni uwekaji wa mawe kuonesha mipaka baina ya ardhi ya kijiji na ardhi ambayo inatumika kwa ajili ya kupita maeneo ya mifugo. Kwa hiyo asiseme kwamba hapa kuna ardhi inayochukuliwa, hakuna ardhi inayochukuliwa kinachowekwa ni mipaka kuonesha baina ya maeneo ambayo yanatumika na wananchi na maeneo ambayo kwa shughuli nyingine. Ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shangai, unaipokea hiyo taarifa.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ni watu wazima, unatenga ile ardhi kutoka ardhi ya nani? Unatenga kutoka kwenye ardhi ya nani.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa Mzungumzaji, kwamba eneo la Pori Tengefu la Loliondo kwa mara ya kwanza lilitangazwa na Serikali ya Kikoloni kupitia Fauna Conservation Ordinance ya Mwaka 1959. Na tangu wakati huo hatujafuta, tumekuwa tukifuta Sheria tuna-repeal na kutengeneza nyingine. Kinachofanyika ni kuweka alama kwenye eneo la square kilometer 1,500 kati ya square kilometer 4,000 za eneo la Pori Tengefu la Loliondo. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shangai, unaipokea hiyo taarifa.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba utunze muda wangu, hawa wana nia tu ya kumaliza muda wangu. Lakini ukweli ni kwamba mimi ninajua kinachoendelea. Ardhi ile ni ardhi ya vijiji kwa mujibu wa sheria zote za Tanzania.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa hajaanza hata kusema jambo jingine, msubiri aseme halafu utaomba taarifa.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, anaongopa, anavuruga, haongei ukweli.

MWENYEKITI: Hata akimaliza kusema nitakupa utoe taarifa. Mheshimiwa Shangai endelea.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapoongelea suala la ardhi tunaongelea maisha ya wananchi na uchumi wao. Naomba ni-quote maneno kwa ruhusa yako ya Bwana William Tenga ambaye ni Mtaalam wa masuala ya ardhi, ambaye amehusisha suala la migogoro ya ardhi kwamba ni sehemu ya maisha ya wananchi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, anasema hivi; “Nobody can live without land and most people have to share it, creating, competing right. This be about righting land the not be avoided. People relationship to land depend on many factors and have a strong cultural element”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapozungumzia ardhi ile ya Loliondo ninazungumzia maisha ya watu wanaoishi pale na Wilaya zote za wafugani kwa sababu…

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

Taarifa Mheshimiwa Shangai.

T A A R I F A

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hata huyo Mheshimiwa anayezungumza sasa hivi Mbunge wa Loliondo, hata kwenye hiyo definition aliyoitoa sasa hivi inasema hakuna mwananchi anaweza akaishi bila ardhi. Hata hawa wanaohama Loliondo kwa hiyari yao wameonyeshwa maeneo mengine ya kuishi, kwa hiyo wako within hiyo definition ambayo yeye ameisoma sasa hivi.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shangai, unaipokea hiyo taarifa.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei kwa sababu hajui anachozungumza. Mimi nazungumzia Loliondo hakuna mwananchi anayehama Loliondo, yeye akarejee Ngorongoro, ndicho anachotaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nirejee pia maneno ya Profesa wa Sheria Chris Maina Peter, anasema; “Land is an important resource in the world today, it is the main source of live loud and survivor. Therefore, whoever control land logically control the lives of others. This is because that person or persons control what guarantee survivor of human being. Due to the proximity of land to survivor it is frequently related to the right to live”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia suala la ardhi ile tunazungumzia maisha ya wananchi wetu. Mimi nadhani Serikali inatakiwa kufikiria upya. Pamoja na kwamba wameweka mipaka lakini ile ardhi bado ni muhimu kwa ajili ya wananchi wale. Wananchi wale ukijaribu kuangalia katika wilaya zetu za wafugaji, ukiangalia lile eneo la Loliondo kuna vijiji. Naibu Waziri juzi alisema kwamba hakuna vijiji, wapo wananchi. Ukienda Longido kwenye lile eneo ambalo wanataka kupandisha liwe pori la akiba kuna vijiji 22.

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Shangai.


T A A R I F A

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri sana wa Mbunge makini wa Ngorongoro; kumekuwepo na hoja zinazozunguka za kuzungumza habari ya maslahi ya taifa na urithi wa dunia. Tunazungumza urithi wa dunia ipi bila Ngorongoro? maslahi ya taifa lipi bila Ngorongoro? Wale ni binaadamu wenye haki sawasawa na binaadamu wengine ni sehemu ya urithi na ni sehemu ya Taifa hili. Hivyo, wana haki waachwe kwenye eneo lao kwa sababu eneo hilo ni lao ni ardhi ya wazazi wao walikowazika mababu zao. Waendelee kupata maisha yao na Sheria inawalinda na repealing clauses zote za Sheria ya Mwaka 1974 na Sheria ya mwaka 2009 Kifungu cha 120 na Kifungu cha 85 na 86 ya Wildlife Conservation Act ya 1974 zote zime repeal mambo hayo ambayo yanazungumzwa. Ni vizuri watu wakasoma Sheria kwa ukamilifu na hasa hawa waliyokuwa wanadai jana kama ni wanasheria waende kwenye repealing clause na transition clause. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shangai, unaipokea hiyo taarifa.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya napokea. (Makofi/Vicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiuhalisia ninajua kwamba wengi wanacheka kwa sababu siyo maisha ya watu wao. Lakini mimi ni maisha ya wananchi wangu, wazazi wangu, wadogo zangu na kaka zangu; lakini watu wanafanya michezo, tunapotosha; kwa sababu yaliyofanyika Loliondo kwa wale wananchi very inhuman. Wananchi wametoroka wameenda Kenya, wananchi wanakimbia kwenda kutibiwa Kenya kwa sababu wamenyimwa PF3, kwa sababu na Hospitali zenyewe zilizopo kilomita 70 na nyingine kilometa 30…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shangai, samahani hayo unayosema una uthibitisho nayo maana usije ukazungumza hapa Bungeni jambo ambalo huna uthibitisho nalo, halafu mwisho wa siku badala ya kusema wewe usahihi ikawa ndiyo wananchi wanapotoshwa.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosema ni kwamba wananchi wameenda kutibiwa Kenya. Naomba unilinde na watu waniheshimu.

MWENYEKITI: Malizia maana muda wako kengele ilikuwa imepiga kwa hiyo kutokana na muda huu nakuongezea dakika moja tu umalizie.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumaliza.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia Mapendekezo wa Mpango wa Maendeleo wa mwaka 2024/2025.

Naomba niwapongeze Mawaziri wote wawili kwa kazi nzuri ya uwasilishaji wa hotuba zao ambazo zimesheheni mambo mazuri kwa Watanzania. Napenda kusema kwamba Nchi yetu kwa miaka yote haijawahi kuwa na shida ya mipango. Tatizo letu kubwa ni namna tunavyotekeleza mipango tunayojiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapanga vizuri sana tunaandika kwenye makaratasi vizuri sana. Leo mwananchi akisikiliza huko nje anadhani kesho kutakuwa kuna mto unatoa maziwa, lakini kwa jinsi tunavyotekeleza inakuwa ni tatizo. Leo kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, Profesa Kitila ukurasa wa 13 amesema kwamba; “Ili kuhakikisha kuwa ukuaji wa uchumi unakuwa na athari chanya katika kuinua kiwango cha maisha ya watu wetu na kupunguza umaskini, mipango ya muda mrefu na mfupi ijayo itajikita katika kuhakikisha kuwa ukuaji wa uchumi wetu unakuwa jumuishi, unapunguza umaskini, unazalisha ajira nyingi, unatengeneza utajiri na unachochea mauzo ya bidhaa zilizoongezwa dhamana nje ya nchi…” Katika aya ya mwisho amesema: “…kazo wa kipekee utakuwa katika kuchochea maendeleo kijamii na kiuchumi or rural social – economic development.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite katika maeneo mawili, kwanza suala la elimu. Nataka baadaye Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo anapokuja atuambie ni namna gani tunaweza kuwajumuisha wananchi wa vijijini ili waweze kushindana na watoto wa mjini. Leo mtoto anayesoma Shule ya Msingi ya Samunge, Kata ya Samunge, Wilaya ya Ngorongoro anawezaje kushindana na mtoto aliyeko Dar es Salaam. Yule mtoto aliyeko Samunge yeye anategemea jua ili asome, lakini aliyeko Dar es Salaam yeye anategemea jua na wakati huo huo anategemea umeme. Nadhani ni vizuri tujikite kuangalia katika suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni namna gani tunaweza ku-balance au kuweka sawia Walimu; Waziri atuambie kwenye mpango wake ni namna gani tunaweza ku-balance uwepo wa Walimu katika shule zetu za vijijini kwa sababu, leo tukiangalia kuna kipindi fulani Mheshimiwa Jenista alisema, ukiangalia kwenye shule za mjini unaangalia somo moja lina Walimu zaidi ya saba, somo moja mjini, lakini kule kijijini Mwalimu mmoja anafundisha zaidi ya masomo 12. Kwenye mpango wa Waziri aje atuambie kwa sisi tuliopo kule vijijini, ni kwa namna gani tunaweza kupata watumishi ambao watawafundisha watoto wetu kule chini. Sambamba katika sekta zote kwenye afya pamoja na elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la mifugo. Sisi wafugaji tunategemea ardhi kwa kila kitu, lakini kumetokea tatizo kubwa sana hapa, coordination ya Wizara zetu. Kwa mfano, leo tunaweza tukawa na Wizara ya Maji, Wizara ya Maji anapeleka maji labda kwenye kata fulani, lakini pia mtu wa mifugo anataka ajenge josho, lakini wakati huo huo anaenda kujenga josho eneo ambalo hakuna maji na Waziri wa Maji ataenda kuweka mradi wa maji katika eneo fulani ambalo mifugo hawaogeshwi kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani Mpango wetu useme ni namna gani hizi Wizara ziongee, kwa sababu Wizara zikiongea itasaidia kutatua matatizo makubwa katika nchi yetu. Leo mtu wa Maji ni lazima aongee na mtu wa Mifugo, kwa sababu unaenda kutatua tatizo la maji ili kuogesha mifugo, tunahitaji maji, lakini mtu wa mifugo anaenda kujenga josho eneo ambalo hakuna maji, hiyo nayo ni misplacement ya resources, ni lazima tuzungumze. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine Mheshimiwa Profesa natamani atuambie Mpango huu ni namna gani unaenda kutatua migogoro ya ardhi katika nchi yetu. Suala la migogoro ya ardhi limekuwa ni tatizo kubwa kwa miaka mingi. Mpango wa Waziri utuambie ni namna gani wanaenda kutatua migogoro ya ardhi. Leo ukienda kwenye wilaya nyingi za wafugaji kuna migogoro ya ardhi. Ukienda Longido kuna migogoro ya ardhi, Simanjiro, Kiteto na maeneo yote yanayozunguka hifadhi zetu kuna migogoro ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tukiangalia kwenye Wilaya yangu ya Ngorongoro, toka mwaka jana Serikali imetenga eneo la kilometa 1,500 wananchi wangu wameendelea kuumia kwa sababu hawana ardhi. Nataka Profesa akija hapa atuambie, mpango huu utaenda kuwasaidia hawa wananchi waweze kupata ardhi ya malisho kwa sababu hawana ardhi ya malisho mpaka sasa hivi. Kwa mfano kila siku hata leo kuna mifugo imekamatwa zaidi ya 834, wapo na wananchi wanaenda kutozwa fedha, lakini mpaka sasa zaidi ya mifugo 2,082 wametaifishwa, ni kwa sababu wananchi hawana ardhi kwa ajili ya kulisha mifugo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wafugaji wa kule kijijini tunategemea mifugo kwa ajili ya chakula, kwa ajili ya kusomesha watoto wetu, kwa ajili ya afya. Ni lazima sasa mpango huu uje utuambie hawa wananchi ambao hawana ardhi, kuanzia Ngorongoro ukienda Lake Natron ukienda maeneo ya Mara, wananchi hawa wanalia kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaamini kwamba Mheshimiwa Rais wetu ana moyo wa dhati wa kuwasaidia wananchi na kuwaletea maendeleo, lakini tuangalie kwenye mipango yetu pamoja na Mawaziri wote, tuone namna ya kumsaidia kutatua changamoto zilizopo. Leo wananchi wa Ngorongoro wanasema angalau hata hao mifugo wakale tu kwa sababu hatuna namna, ni bora tufe polepole kuliko kufa kwa wakati mmoja, kwa sababu kama mwananchi unategemea mifugo kwa ajili ya chakula huna pa kulisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliambiwa hapa kwamba watu watachimbiwa maji, mpaka leo ni visima viwili na havitoi maji ambayo mifugo inatumia na ile mifugo ilikuwa inategemea maji kutoka eneo lile la kilometa 1,500 kwa ajili ya kupata maji. Walisema wataweka malisho hakuna, hakuna malisho ya aina yoyote sasa wale wananchi wataishije, mpango huu uje utuambie ni namna gani wanaweza kwenda kutatua changamoto za wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, kuna suala hapa wanazungumza, naomba mpango huu utuambie, je mpango huu unawahusu wananchi 100,000 wa Tarafa ya Ngorongoro ambao Serikali imewawekea vikwazo vya maendeleo kwa zaidi ya miaka miwili sasa. Hawapati maji, hawapati chochote. Mpango huu uje utuambie, Serikali ina mpango gani kwa ajili ya hawa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, …

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shangai Kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ole-Sendeka.

TAARIFA

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge Shangai wa Ngorongoro juu ya hali ya tarafa yake ya Ngorongoro aliyoieleza, kwamba kutokana na urasimu ulioko katika Hifadhi ya Mamlaka ya Ngorongoro, hivi sasa kuna baadhi ya shule ambazo vioo vyake vimevunjika, vimepasuka na hawaruhusiwi wala hawapewi kibali cha kujenga. Kwa miaka hii miwili wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro kwa miradi ya maendeleo waliyokuwa wamepangiwa, miradi hiyo yote fedha zake zimesimama. Mpango huu utuambie ni Mpango wa Tanzania nzima isipokuwa Tarafa ya Ngorongoro ili tujue wananchi wa Ngorongoro watapangiwa mpango wao lini na kuletwa katika Bunge hili Tukufu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shangai unaipokea hiyo taarifa?

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napokea taarifa ya Kaka yangu, Mheshimiwa Ole-Sendeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposema maendeleo jumuishi, maana yake tunalenga zaidi wale ambao wako nyuma kimaendeleo ambao ni watu wa vijijini ambao wanategemea kilimo. Kwa hiyo, niiombe Serikali kuhusiana na suala hili la Tarafa ya Ngorongoro pamoja na suala la Tarafa ya Loliondo na Sale, ni muhimu sana Serikali iangalie namna wale wananchi wanaangamia. Waziri aje na mpango mzuri wa kuwajali na wao kwa sababu ni Watanzania wanahitaji maendeleo. Tunaposema uchumi mzuri, ni lazima tunawaongelea na wao, lakini sasa tutakuwaje na maendeleo jumuishi kama kuna watu bado tunawauzia mifugo, haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala la infrastructure; coordination yetu katika Wizara zetu, Wizara ya Maliasili na Utalii Mheshimiwa Rais alitangaza Royal Tour, lakini sasa hivi ukienda kwenye hifadhi zetu, nitolee mfano, Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro pale getini. Wazungu hawataki silaha getini, kule ni hospitality industry, ni watu ambao wanaenda kwa starehe, lakini wanapoenda getini wanakutana na watu wenye silaha wanashangaa. Tutengeneze mifumo ya utalii ambayo itasaidia nchi yetu kupata mapato makubwa na Wazungu wanaokuja waende na kurudi tena. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa kengele ya pili hiyo.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kengele ya pili?

MWENYEKITI: Ndiyo.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia taarifa iliyowasilishwa mbele ya Bunge lako Tukufu kuhusiana na Kamati za PAC, PIC pamoja na LAAC.

Mheshimiwa Spika, nitajikita zaidi kwenye hoja ya KADCO. Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumzia suala la KADCO, lakini wengi hawajaingia kwa ndani sana. Binafsi naomba niweze kuelezea kwamba KADCO ni mtoto mmoja aliyezaliwa tarehe 11 Machi, 1998 akiwa na wazazi wawili ambao ni, Mott McDonald aliyekuwa na hisa asilimia 99 na mtu mwingine anaitwa Inter-Consult Tanzania Limited akiwa na hisa asilimia moja. Kampuni hii ilisajiliwa kwa mujibu wa Sheria ya Makampuni, Sura ya 212 kama shirika binafsi.

Mheshimiwa Spika, tarehe 17 Julai, 1998, KADCO waliingia makubaliano na Serikali pamoja na McDonald lakini alikuja kujiunga mtu mwingine anaitwa South African Infrastructure Fund wakagawana shareholders kati ya Serikali na wale wamiliki wengine. Serikali ikachukua asilimia 24 ya hisa, McDonald wakawa na asilimia 41.4 ya hisa. South African Infrastructure Fund wakawa na asilimia 30 ya hisa, Inter-consult wakawa na asilimia 4.6.

Mheshimiwa Spika, tarehe 10 Novemba, 1998, KADCO na Serikali wakaingia mkataba wa uendeshaji kwa ajili ya kuhakikisha kwamba miundombinu kwenye uwanja wa KIA inaendelezwa kwa miaka 25. Mwaka 2006 baada ya miaka hiyo yote, Serikali ilikuja ikafanya tathmni ya KADCO kama inafanya kazi ipasavyo kulingana na concession agreement lakini baada ya tathmini Serikali ikasema kwamba tuangalie masuala yafuatayo: -

Je, KADCO inafanya kazi kama ilivyokubaliwa? Serikali ikagundua kwamba wanahisa wenzake ambao ni Mott McDonald waliokuwa na asilimia 41.4, South Africa Infrastructure Fund waliokuwa na asilimia 30 ya hisa, Serikali ambayo ilikuwa na asilimia 24 na Inter-Consult Tanzania Limited waliokuwa na asilimia 4.6. Serikali ikaja kuona kwamba hao wenzake wanahisa hawafanyi kazi vizuri. Serikali ikaamua kwamba, sasa umefika wakati wa kuchukua KADCO moja kwa moja na kununua hisa zote kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, kinachotushangaza, kinachonishangaza mimi kama Mjumbe wa Kamati ya PAC, tumemwita Afisa Masuuli Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, tumemuuliza kuhusiana na hawa watu McDonald, South Africa Infrastructure Fund pamoja na Inter-Consult Limited hizo hisa zao zilikuwa na value kiasi gani? Hakuna jibu mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kinachoshangaza tena, baada ya Serikali kuchukua hisa zote kwa asilimia mia moja, Serikali kupitia TAA ikaenda kukopa fedha kutoka CRDB USD million 5.3 kwa ajili ya kuwalipa wanahisa wenzake ambao wameshindwa kazi. Hata hivyo, tunachojiuliza hizo fedha zimelipwa kwa kigezo gani? Tumechukua mkopo ambao utalipwa na Serikali kupitia fedha za walipakodi shilingi milioni 5.3 USD kwa ajili ya kuwalipa watu ambao hatukujua hizo hisa zao zina value kiasi gani.

Mheshimiwa Spika, kinachoshangaza vile vile, leo bado Serikali baada ya kununua hisa zote bado tuna concession agreement na KADCO. Huyu KADCO ni nani? Ni swali la kujiuliza huyu KADCO ni nani ambaye bado tuna concession agreement ya miaka 25 ambayo huuhishaji wake utaisha tarehe 16 Julai, 2025. Kama Serikali imesajili kwa mujibu wa mashirika ya umma huyu KADCO ni nani ambaye bado tuna concession agreement na yeye? fedha za walipakodi bado zinapotea kwa sababu hiyo.

Mheshimiwa Spika, ninachojiuliza, kama ni TAA ilichukua mkopo kutoka CRDB shilingi milioni 5.3 Dola za Marekani, maana yake wao ndio wangetakiwa kusimamia Uwanja wa KIA na siyo mtu mwingine tena. Kwa hiyo nitoe pendekezo kama kweli tupo tayari kwa ajili ya kuisaidia nchi hii hatuhitaji kumsikia mtu anaitwa KADCO, labda waje watupe jibu hapa ndani kwamba KADCO ni nani ambaye sisi Wabunge wengine hatumjui. Kwa hiyo Uwanja wa KIA ukabidhiwe kwa TAA ili waweze kuendesha kwa manufaa ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, suala lingine katika kupitia ripoti za CAG kuna mtu anaitwa DUWASA hapa Dodoma, ambao wanatusaidia kusimamia miradi ya maji, kwenye ripoti ya CAG tumeona kwamba DUWASA walichimba visima viwili Kongwa vyenye thamani ya Shilingi Billion1.5. Kitu cha kushangaza kisima kimoja baada ya Miezi Mitano hakitoi maji, kisima kingine hakijawahi kutumika kwa sababu maji yana chumvi, kuwauliza kwa nini? Wanasema tulikuja kuona kwamba yale maji yana chumvi. Kinachoshangaza kwani watalam wetu wanapochimba maji, tuna maabara ya maji, kabla ya maji kutumika ni lazima tupeleke kwenye maabara ya maji yakaangaliwe ubora wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tumepoteza Fedha za wananchi kwa kuchimba visima, kisima kingine baada ya miezi mitano hakifanyi kazi, tumeishapoteza fedha na naamini ni fedha za walipa kodi. Suala lingine la kusangaza kwenye mradi huohuo ulikabidhiwa mitambo na kibanda ambacho kilikuwa na pampu lakini haijawahi kutumika hata siku moja.

Mheshimiwa Spika, nishauri fedha hizi za walipa kodi zinalipwa na Watanzania nasi kama Wabunge tulipewa nafasi hii kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunazilinda hizo fedha ili zilete manufaa kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, naomba pia nigusie suala la TRA kwenye ripoti ya CAG kutoka Mwaka 2018/2019 mpaka 2020/2021, TRA imeshindwa kukusanya Shilingi Trilioni 6.78, lakini tunajua kwamba Mamlaka ya Mapato Tanzania tumewakabidhi jukumu la kuhakikisha kwamba wanatukusanyia fedha kwa ajili ya kufadhili miradi ya maendeleo. Kila Mbunge yupo kwenye Bunge hili na anataka maendeleo yaende kwenye Jimbo lake, lakini TRA Watumishi waliopo wamekuwa wanashindwa kukusanya mapato yaliyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, ninaomba nishauri Bunge lako Tukufu, kuna mianya mingi ya rushwa kwa sababu ya TRA, ukijaribu kuangalia kuna makadirio ya chini ya kodi nyingi in value inaweza ikafika zaidi ya Billion 30 lakini kuna maeneo mengine wanashindwa kukusanya kodi. Kwa mfano, kwa Mwaka wa Fedha wa 2020/2021 wameshindwa kukusanya Shilingi Billion 8.5 kwa mafuta yanayotumiwa ndani ya nchi. Kwa hiyo TRA wanatakiwa nao kusimamiwa kwa ajili ya kukusanya mapato.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja kwa Kamati zote. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora. Awali ya yote niwashukuru sana Wizara nzima kwa kazi nzuri wanayoifanya, wakiwepo watendaji wote, TAKUKURU Pamoja na Katibu Mkuu, mwalimu wangu Dkt. Laurean Ndumbaro na wote ambao wanafanya kazi hizo kwenye Wizara. Pia nipende kusema kwamba Wizara hii wanafanya kazi nzuri sana, na kuanzia Awamu hii ya Sita. Mimi nilikuwa Mwenyekiti wa Halmshauri nimeona kazi kubwa iliyofanywa watumishi kule wanaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi cha nyuma watumishi walikuwa wanafanya kazi ili mradi tu, watumishi walipopandishwa vyeo pamoja na kubadilishiwa madaraja naona sasa wanafanya kazi kwa morale. Kwa hiyo niiombe Wizara iendelee kufanya kazi hiyo. Nimeona kwamba mmepanga kuwapangisha watumishi wengine madaraja pamoja na kuwapandisha vyeo. Niombe kwamba tuendelee kutumia sheria zetu tulizonazo ili wasiwepo watumishi ambao wataachwa bila kupandishwa vyeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na pia niiombe Wizara, kwamba kuna watumishi wa kati tunafanya zoezi la kuwapandisha vyeo pamoja na madaraja, kuna watumishi ambao waliachwa niombe wizara mtoe nafasi tena kwa watumishi hao ili wapate nafasi kama watumishi wengine ndani ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kwenye ajira ambazo zimetangazwa kuna maeneo ambako watumishi wamekuwa wakiondoka. Kwa mfano halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro mwaka jana walipoajiriwa walimu waliajiriwa watumishi ambao ni walimu 10; walimu nane walikuwa wa shule za msingi na walimu wawili walikuwa ni shule za sekondari. Kwa bahati mbaya wale watumishi walishaajiriwa nyuma wakaacha ajira za Serikali. Kwa hiyo wakati wanaingizwa kwenye mfumo ilionekana kwamba wale watumishi hawawezi kuajiriwa tena. Kwa hiyo badala na halmashauri yetu kunufaika na watumishi 10 wale watumishi walirudishwa mpaka leo hawajulikani walipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niiombe wizara kwenye ajira hizi tunaomba replacement ya zile nafasi 10 pamoja na watumishi wengine kwa sababu kwenye halmashauri yetu ya Ngorongoro watumishi wengi wanaondoka kwa sababu ya mazingira.

Mheshimiwa Spika, na ili kutatua tatizo hili nishauri Wizara, kwamba tuangalie maeneo ya pembezoni. Nakumbuka siku moja Mbunge Mheshimiwa Kandege alizungumza kwa maeneo ya Nkasi na Rukwa na maeneo mengine; kwa miaka ya nyuma Serikali kupitia mradi wa Mkapa Foundation kuna maeneo kama haya ambayo walikuwa wanapewa motisha walikuwa wanaajiriwa na Mkapa Foundation ili watu kufanya kazi kwa mkataba wa Serikali. Jwa hiyo maeneo kama halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro na maeneo mengine ya pembezoni tuwape kipaumbele ili angalau maeneo yale wananchi nao wapate huduma.

Mheshimiwa Spika, Lakini kuna maeneo mengi sana mwaka 2017 Serikali iliwaondoa watumishi wa darasa la saba kwenye ajira. Wengine waliondolewa kwa haki na wengine waliondolewa kwa kuonewa. Nitoe mfano ya watumishi waliondolewa na mamlaka ya hifadhi ya Ngorongoro; watumishi wenyeji 63 wengi wao waliajiriwa miaka 1993 na wengine waliajiriwa kabla ya mwaka 2004 lakini wote waliondolewa kwenye ajira na inaonekana hilo kulikuwa na chuki kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi niombe Wizara ifanyie kazi malalamiko ya watumishi hao; na nimuombe Waziri, kwamba niwalete watumishi hao waje kuaonana na wewe pamoja na Katibu Mkuu ili mshughulikie matatizo yao, na wale wenye sifa warudishwe kazini.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna watumishi wengine wa Baraza la Wafugaji Ngorongoro, nao waliachishwa kazi. Kulikuwa na mkataba ambao Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro pamoja na Baraza la Wafugaji waliingia mabkubaliano kwamba wale watumishi wa Baraza la Wafugaji walitakiwa kuajiriwa na Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro; lakini baadaye waliomba kibali utumishi; kiuhalisia walikuwa na bajeti lakini baadaye wakasema utumishi wamenyimwa kibali. Kwa kuwa tayari Baraza la Wafugaji ni taasisi ya Serikali iliyoanzishwa na Sheria ya Bunge hapa hapa; kwahiyo mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri na watumishi hawa nao waangaliwe.

Mheshimiwa Spika, Serikali yoyote duniani ina kazi ya kuhakikisha kwamba huduma kwa wananchi zinatolewa. Na ili watumishi nao waweze kufanya kazi ni lazima wawe na maslai mazuri ili waweze kufanya kazi masaha yote yanayotakiwa. Kwa hiyo niendelee kuishauri Wizara, kwamba tuwaangalie watumishi, hasa kupokea malalamiko yao kwa wakati na kufanyia kazi kwa wakati. Unakuta kwamba kuna malalamiko yameletwa wizarani, mtu anasubiri miezi sita, sijui tunafanya nini mpaka miezi sita inapita bila kufanyiwa kazi? Tunatakiwa kwamba watumishi wanapoleta malalamiko yao yanatakiwa kufanyiwa kazi kwa specified time; siyo mtu anakuja Dodoma anatoka, Kikoma anatoka Arusha, kila wakati anakuja Dodma hapati majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona kwamba mmeanda mfumo wa kupokea malalamiko, lakini wakati mwingine watumishi hawapati majibu yao kwa wakati. Niombe Wizara kufanyia malalamiko kazi kwa wakati wale wahusika wapate majibu yao kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono kwa asilimia 100.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, nami nichangie hotuba ya Waziri wa Maji. Awali ya yote niwashukuru wananchi wa Jimbo la Ngorongoro kwa kunichagua kwa kura nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, nami niungane kuwapongeza timu nzima ya Wizara ya maji kuanzia Waziri Mwenyewe, Makatibu Wakuu, na Naibu Makatibu Wakuu, lakini pia nimpongeze Eng. Andrew ambaye ni meneja wa RUWASA Wilaya ya Ngorongoro. Pamoja na mazingira ya Wilaya yetu na kutokuwa na vitendea kazi kwasababu hawana gari kwa sasa kwasababu gari yao waliyokuwa wanaitumia ni mbovu; na unavyojua Wilaya yetu ya Ngorongoro ukitoka Kata moja kwenda Kata nyingine unatumia zaidi ya kilometa 70 hadi
100. Kwa hiyo ni lazima tuwatafutie vitendea kazi ili waweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti iliyopita mwaka 2021/2022 Wilaya yetu ya Ngorongoro tulitengewa bajeti ya Shilingi bilioni 7.1 lakini mpaka ninavyozungumza tumepokea Shilingi 1,200,000,000 tu kwa ajili ya miradi ya maji. Sasa tumebakiza mwezi mmoja kwa ajili ya kukamilisha mwaka wa fedha.

Mheshimiwa Spika, tushukuru kwamba tumepata kiasi hicho, lakini kiuhalisia tukijaribu kuangalia, kwasababu tuna miradi 13 inayoendelea mpaka sasa hivi; lakini fedha zilizotengwa pia kwa mwaka 2022/2023 zimetengwa Shilingi bilioni 1.9; na kabla hatujamaliza mwaka huu bado tunadai zaidi ya Shilingi bilioni sita na fedha ambazo hazijaenda kwa ajili ya miradi ya maji inayoendelea kule Wilaya ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, je, tunategemea nini? Kwasababu leo tunawadai Shilingi bilioni sita ya bajeti iliyopita maana yake sasa miradi inayoendelea pale kwenye Wilaya ya Ngorongoro ni miradi ambayo tutaenda kuiona kama ni White Elephant Projects. Kwasababu kama hatupeleki fedha kila siku labda tunapeleka kwa mradi wa Shilingi milioni 300 tunapeleka Shilingi milioni 50 itawezesha wananchi kupata maji? Na ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi inasema kwamba ifikapo mwaka 2025 vijijini tuwe na asilimia 85 ya watu wanaopata maji na mjini ni 95. Kwa mtindo huu wa kuweka bajeti halafu tunapeleka a little amount of money tutatekeleza kweli miradi hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini suala lingine, ukijaribu kuangalia miradi mingi ambayo imetekelezwa; Mheshimiwa Aweso nikukumbushe tu na nikupongeze pia, kwamba umeweza kufika kwenye mradi wa vijiji nane ambao ni mradi maarufu sasa hivi Ngorongoro. Mradi huo umeanza tangu mwaka 2018 lakini mpaka leo bado tunajenga chanzo tu. Niombe tu, kwamba tutenge fedha za kutosha ili tuweze kumaliza mradi huo wa vijiji nane ambao ni maarufu kwa jina la mradi wa Mageri.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali, kama kweli tunataka kuwasaidia wananchi, akina mama kwenye vijiji na kwenye vitongoji kwenye kata za Enguserosambu, Tinaga, Digodigo na kata nyingine zilizopo karibu kwa ajili ya mradi huo akina mama wanateseka kwenda kuchota maji mtoni kila siku, wanateseka kufuata maji usiku na mchana; kama kweli tunawapenda wananchi wetu na ni kweli kwamba tunataka nao waondokane na umaskini tuwaletee maji ili muda wanaotumia kwenda kuchota maji mtoni watumie kwa ajili ya shughuli nyingine za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini suala lingine ambalo linatokea, sisi wafugaji tunahitaji maji kwa ajili ya binadamu pamoja na mifugo. Kwenye Ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi inasema kwamba tutajenga mabwawa kwa kila Wilaya, lakini Wilaya yetu ya Ngorongoro hakuna hata bwawa moja, ukienda pia Longido hakuna hata bwawa moja. Tunahitaji kujenga mabwawa kwa ajili ya mifugo ambayo kwa sisi tunaweza kutumia yale mabwawa kwa ajili ya mifugo pamoja na binadamu. Sisi wakati wa mvua tunaweza tukapata maji, kuna maeneo mengi. Kwa mfano Kata za Malambo, Oloipiri pamoja na Maalon hawana maji; na kata nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi Wilaya yetu tuna vijiji 65 lakini vijiji ambavyo vinapata maji angalau ni 34, vijiji 28 vinapata maji ambayo si toshelezi na vijiji zaidi ya 13 havina maji kabisa. Kwa hiyo niiombe Wizara tuangalie namna ya kuwasaidia wale wananchi nao waweze kupata maji ya kunywa.

Mheshimiwa Spika, lakini suala lingine, kule Loliondo wananchi wanapata maji Unit moja kwa shilingi 2,500, hicho ni kiasi kikubwa sana. Mama zetu na watu wengine wameamua kurudi kwenda kuchota maji mtoni kwasababu hawawezi kumudu gharama ya maji. Wakati mwingine wanasema wasimamizi wanaweka bei ambazo wananchi hawajui. Kwa hiyo tuombe, kama ikiwezekana wizara ijipange zilete zile pre-paid meters ambazo zitawasaidia Watanzania kuibiwa.

Mheshimiwa Spika, lakini suala lingine mimi niombe na nisisitize sana. Fedha hizi ambazo zilitengwa kwa bajeti ya mwaka 2021/2022, nikuombe sana uweze kuangalia angalau hata tupate fedha kwaajili ya miradi inayoondelea. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha mchango wangu wa maandishi.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Waziri wa Afya na Naibu wake kwa kazi nzuri sana ambayo wamekuwa wakiifanya kwa niaba ya Watanzania wote.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu naomba niiombe Wizara iangalie kwa jicho la umakini zaidi katika maeneo yafuatayo; kwanza kumekuwepo na wizi mkubwa wa dawa katika vituo vya afya nchini, baadhi ya watumishi wasio waaminifu wanachukua dawa kutoka kwenye vituo vya afya na kwenda kuuza kwenye maduka ya watu binafsi. Wizara iweke nguvu kubwa kwenye udhibiti wa vifaa tiba na dawa.

Pili, afya kwa wanadamu ni muhimu sana, hivyo tuwekeze nguvu pia kwenye uzalishaji wa wahudumu wa afya wenye sifa na ujuzi usiotiliwa shaka. Hivyo, tupitie upya sifa zinazohitajika kwa ajili ya kuwadahili wanafunzi watarajali kwenye vyuo vya afya.

Mheshimiwa Spika, ombi, ninaomba vifaa tiba na dawa na vitendanishi kwenye Hospitali ya Wilaya ya Ngorongoro na Kituo cha Afya Samunge kilichojengwa kwa nguvu za wananchi.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kumpa hongera sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kwa kuendelea kuwatumikia Watanzania kwa weledi mkubwa. Pamoja na kwamba Serikali imeendelea kuboresha huduma mbalimbali kwenye Jimbo langu la Ngorongoro ikiwepo elimu na afya bado kuna changamoto kubwa sana katika nyanja mbalimbali za kijamii.

Mheshimiwa Spika, nianze na afya; kata nyingi hazina huduma za afya kwa maana ya kutokuwa na zahanati wala kituo cha afya, hivyo wanakosa huduma hizo na kupelekea kupoteza maisha wakiwa njiani kufuata huduma za afya sehemu za mbali ambayo ni wastani wa kilometa 60 hadi 100.

Mheshimiwa Spika, wananchi wameendelea kujitolea na kuanza ujenzi wa majengo mbalimbali kwa ajili ya uhitaji wa huduma za afya; ombi langu naomba Wizara itenge fedha kwa ajili ya umaliziaji wa vituo vya afya vifuatavyo ambavyo vimejengwa kwa nguvu wananchi: -

(i) Kituo cha Afya Arash - wananchi wamejenga majengo matano na yote yamepauliwa kwa nguvu zao wenyewe, Serikali ikitupatia shilingi 300,000,000 wananchi watapata huduma ukaribu sana.

(ii) Kituo cha Afya Samunge - wananchi wamejenga majengo saba na yote yamepauliwa, Serikali inatakiwa kutenga fedha kwa ajili kukamilisha ujenzi wa kituo hiki cha afya ili wananchi wapate huduma kwa ukaribu.

Mheshimiwa Spika, kata ambazo hazina vituo vya afya ni pamoja na Kata ya Kirangi, Kata ya Piyaya, Kata ya Maaloni, Kata ya Engusero Sambu, Kata ya Oldonyosambu, Kata ya Ololosokwan, Kata ya Ngaresero, Kata ya Pinyinyi, Kata ya Soitsambu na Kata ya Digodigo.

Mheshimiwa Spika, wananchi kutoka kwenye kata nilizozitaja hapo juu hufuata huduma za afya kwa wastani wa kilometa 60 hadi -100 jambo ambalo linahatarisha maisha yao. Hivyo, naomba Wizara itenge fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu elimu; bado suala la elimu kwa Wilaya yangu ya Ngorongoro ni duni sana, shule nyingi za msingi zimechakaa sana na zinahatarisha maisha ya wanafunzi wanaosoma kwenye madarasa chakavu. Hivyo, basi naiomba Serikali kutenga fedha za kutosha kwa ajili ya ukarabati wa majengo chakavu na ujenzi wa madarasa mapya pamoja shule mpya kwenye vijiji vya Kirtalo (Losirwa) Kijiji cha Soitsambu (Esilalei).

Kwa upande wa elimu ya sekondari; Wilaya ya Ngorongoro ina shule 11 tu Serikali kati ya kata 28. Hivyo, niiombe Serikali kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule za sekondari kwenye Kata za Pinyinyi, Arash, Soitsambu, Enguserosambu, Oloirien Magaiduru, Digodigo na Kata ya Maaloni.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ugawaji wa maeneo ya utawala, naomba Wizara itusaidie kuongeza maeneo ya utawala hasa kwenye kata ambazo zina kijiji kimoja badala ya vijiji zaidi ya kimoja ambapo Kata ya Ngaresero ina kijiji kimoja; Kata ya Sale ina kijiji kimoja; Kata ya Digodigo ina kijiji kimoja; Kata ya Pinyinyi na Kata ya Piyaya ina kijiji kimoja.

Mheshimiwa Spika, tunaomba Wizara itusaidie kugawa baadhi ya kata zifuatazo ambazo utoaji wa huduma kwa wananchi imekuwa ngumu sana; kata hizo ni Enguserosambu, Soitsambu, Ololosokwan, Malambo, Oldonyosambu na Oloirien Magaiduru.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa barabara, Wilaya ya Ngorongoro ina mtandao wa barabara wa kilometa 934, hivyo naomba tuongezewe fedha za kutosheleza kutengeneza barabara zote ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa pongezi kwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Naibu Mawaziri na watendaji wakuu wa Wizara kwa kazi nzuri ambayo wameendelea kuwafanyia Watanzania.

Napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa fedha ambazo zilifanikisha ujenzi wa barabara ya lami kutoka Loliondo_Sale (kilometa 50). Kwa kuwa barabara hii ni muhimu kwa uchumi wa Wilaya ya Ngorongoro kwa ajili ya kuunganisha Wilaya ya Ngorongoro na Mkoa wa Arusha.

Kwa kuwa Waziri alishaagiza TANROADS kutangaza kilometa 50 zingine, naiomba Wizara iharakishe mchakato huo wa kutekeleza mradi huo wa kilometa 50 kutoka Sale - Ngaresero na baadaye kutoka Ngaresero mpaka Mto wa Mbu. Barabara hii itasaidia kufungua uchumi ya Wilaya ya Ngorongoro huku tukifahamu kuwa Wilaya yetu ya Ngorongoro ina vivutio vingi vya utalii na ili kurahisisha ufanyaji wa biashara ya utalii na watalii kufika kwenye vivutio hivyo, ni muhimu sana barabara hii kutengenezwa.

Mheshimiwa Spika, Wizara pia itenegeneze fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi wa barabara ya lami Makao Makuu ya Wilaya ya Ngorongoro eneo la Wasso - Loliondo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na mimi niweze kuchangia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo. Kwanza nitangulize pongezi kwao Wizara nzima akiwemo Waziri mwenyewe, Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na Naibu Makatibu wawili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza ambalo ninapenda kusema ni kwamba kwa Tanzania tumekuwa na figures za mifugo kila mwaka tunaongeza. Lakini ukijaribu kuangalia takwimu zetu sijui kama tunazo takwimu ambazo ni sahihi. Tunasema leo tuna ng’ombe milioni 36.6, mbuzi milioni 26.6 na kondoo milioni 9.1.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukijaribu kuangalia kwa idadi ya mifugo tulionao na mchango kwenye Pato la Taifa kidogo inafikirisha. Ni lazima tujiulize kama Taifa kwamba tunajali mifugo kama kitega uchumi au tunaona mifugo kama tatizo kwenye Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu leo hii tukijaribu kuangalia Nchi kama Ethiopia ina mifugo zaidi ya milioni 70, lakini hatusikii Serikali yao ikisema kwamba mifugo wamekuwa ni tatizo. Lakini sisi Tanzania tumewatangulizia wafugaji tunawaona kama tatizo kwenye nchi hii. Ukishamtangulizia mtu ukamuona kama tatizo, huwezi ukamsaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tu-change mentality kama Serikali ili wafugaji tuwaone kama ni watu ambao nao kwenye nchi hii tunaweza kuwasaidia wakaongeza uchumi wetu na maisha yao yakaimarika. Lakini tukiwaona kama tatizo tutaendelea kuwalaumu kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la hereni, kaka yangu, Mheshimiwa Musukuma pale, alizungumza, lakini binafsi pia wananchi wangu kila siku wamekuwa wakilalamika kuhusiana na suala la hereni. Binafsi sioni kwamba ni kitu ambacho kitatusaidia kujua idadi ya mifugo Tanzania. Kinachotakiwa, kama tunataka kujua idadi ya mifugo tulionao tuendeshe sensa kwa kila wilaya; tuna wakuu wa wilaya, tuna ma-DAS, tuna wakurugenzi, tuna watendaji wa vijiji, tuna watendaji wa kata, wafanye hiyo kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo tunakwenda tena kuwatoza Watanzania wenzetu, wafugaji, fedha kwa ajili ya kuhesabu mifugo yao. Sisi kama Serikali tuwekeze ili tupate kujua idadi ya mifugo na ili tuweze ku-accrue economic bases kutoka kwa wafugaji. Siyo tunawaona wafugaji kama tatizo. (Makofi)

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Emmanuel, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Edward Kisau.

TAARIFA

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu nimpe taarifa kwamba idadi ya mifugo tayari inajulikana. Tumeambiwa hapa ni milioni 30. Kwa hiyo sasa sijui wanakwenda kufanya nini tena.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Emmanuel, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo taarifa inapokelewa kwa mikono yote miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama wafugaji ambao tumekuwa kwenye ufugaji kuanzia utotoni mpaka sasa hivi tunajua mifugo ni mali, ni dawa na ni kitanda kwetu. Kwa sababu mfugaji nalalia ngozi, nakula nyama, nakunywa maziwa. Nikiugua nachinja mifugo kwa ajili ya kuleta afya yangu ijirudie katika hali ya kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini watu wengine Tanzania tumewaona wafugaji kama ni watu ambao hawafai. Hata kwenye vyombo vya habari tunawaona wafugaji kama ni watu ambao ni wa kutoka hapa kwenda pale kila siku, kuzunguka. Kwa nini wafugaji wanazunguka Tanzania nzima; ni kwa sababu tumewanyang’anya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukijaribu kuangalia kwa Wilaya yangu ya Ngorongoro kabla ya eneo lile la Pori Tengefu kutengwa hatujawahi kuhamahama lakini mwaka huu itakuwa mara ya kwanza kwa wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro kuhama kwenda kutafuta malisho kwa sababu tumewanyang’anya ardhi yao. Na ili tuone ni tatizo baada ya lile eneo la pori tengefu kutengwa, mifugo zaidi, ng’ombe 5,780 wamekamatwa kwenye lile eneo, na Serikali kuwatoza zaidi ya shilingi milioni 578. Kwa sababu hawana malisho itabidi waende. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni lazima kama Wizara, sijui kama ndugu yangu, Mheshimiwa Ulega, wafugaji Tanzania hii – ukimuona Waziri wa Maliasili ana wivu na tembo wake, sasa sijui wewe utakuwa na wivu na mifugo? Kwa sababu Watanzania wafugaji wanaumia kwenye hii nchi. Hatujawahi kumsikia Waziri wa Mifugo akizungumza hadharani na kukemea tabia ya wafugaji kukamatwa na kutozwa shilingi 100,000; hatujawahi kumsikia. Kwa nini tusisikie, na wewe umepewa na Rais Wizara hii usimamia uweze kuwatendea haki wafugaji wa nchi hii. (Makofi)

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Sasa sijui kama kuna Wizara…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shangai, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Cherehani.

TAARIFA

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpe taarifa mzungumzaji kwamba kweli Waziri wa Mifugo anatakiwa awaonee wivu wafugaji wake; wanakamatwa, wanatozwa faini, na wengine, mfano Yohana Mahona aliuziwa ng’ombe wake 1,221 na alishinda kesi Waziri hajatoa tamko. Lakini kuna Shabani Roya wa Ngorongoro, ng’ombe 170, alishinda kesi lakini Waziri hajatoa tamko. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Emmanuel, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni taarifa inayopokelewa kwa mikono yote miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe taarifa kwamba Desemba mwaka jana familia 27 walitaifishiwa ng’ombe 1,922 Ngorongoro. Mpaka leo familia hizo zimekuwa maskini. Kwa hiyo, niombe pamoja na masuala mengine tuwatafutie wafugaji wetu maeneo ya malisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais hawezi kukunyima fedha ukiwa na big vision lakini ukiwa Waziri unayekaa kila siku, kama walivyosema wengine, ni lazima ufikirie namna ya kuwakamua hawa wafugaji wa nchi hii. Tumechoka kuonewa kwenye nchi hii. Tunahitaji na sisi tuthaminike na tuweze kuchangia uchumi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la chanjo; nashukuru umetuletea dozi 1,200 za PPR. Lakini toka mwezi Septemba mwaka jana mpaka sasa hivi hawajachanja mifugo kwa
sababu kwenye wilaya zetu wewe unapeleka chanjo lakini huna fedha za operesheni kwa ajili ya kufanikisha. Sasa sijui chanjo zitakwenda kwa mifugo yenyewe? Tunahitaji gari na fedha kwa ajili ya wataalamu kwenda kuchanja mifugo. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, muda wako umekwisha.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, wamechukua muda wangu kwa taarifa, naomba uniongezee.

MWENYEKITI: Hapana Mheshimiwa, taarifa ni sehemu ya mjadala.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia bajeti ya Wizara ya Maji. Nitangulize kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuwatumikia Watanzania kwa upendo mkubwa pamoja pia na kumpongeza Waziri wa Maji, Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu na Wasaidizi wote pamoja na watumishi wa RUWASA Wilaya ya Ngorongoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi binafsi nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri. Nimemfuata sana kuhusiana na suala la mradi wa maji wa vijiji nane, mradi wa Mageri. Mradi huo umeanza toka mwaka 2016, mradi huu ungetakiwa kuwasaidia zaidi ya wananchi 80,000 lakini mpaka leo bado una suasua. Nashukuru kwamba nilikuona toka wiki iliyopita umeweza kutusaidia tumepata zaidi ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya mradi huo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru pia kwenye mradi wa Lopolu umetupatia shilingi milioni 100 ambayo itaenda kumaliza tatizo la maji kwenye Kijiji cha Lopolu pamoja Oldonyouwas, nashukuru kwa hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Wilaya yetu ya Ngorongoro tuna miradi zaidi ya 14 ambayo inaendelea, miradi hiyo yote inahitaji zaidi ya shilingi bilioni 10 ili iweze kuwahudumia wananchi, lakini mpaka sasa kwenye bajeti ya mwaka jana tumepta fedha 40% tu kwa miradi yote inayoendelea. Kwa hali hiyo ni kwamba hatuwezi kwenda kutatua shida ya maji tunakuwa na miradi mingi inayoendelea lakini fedha hazitoki. Mimi nikusihi Mheshimiwa Waziri tunaomba tunapotenga fedha hasa katika maeneo ambayo yana shida ya maji kama Wilaya ya Ngorongoro tujitahidi kuwapa kipaumbele, tuwaletee fedha kwa wakati ili wananchi wanufaike na juhudi za Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna suala lingine, kwa mfano leo kati ya miradi inayoendelea kwenye Wilaya ya Ngorongoro kuna mradi wa maji Digodigo. Inahitaji shilingi milioni 42 na imefika 90%, tukipata hizo fedha mradi huu utaisha. Tuna mradi wa maji wa Oldonyosambu Masusu. Mradi huu umeanza toka mwaka 2018 lakini mpaka leo mradi huo umefikia 85%, mkandarasi hajalipwa, fedha zinadaiwa shilingi milioni 270 kwenye mradi huo.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni uchimbaji wa visima viwili katika Vijiji vya Loswas na Soitsambu. Inahitajika shilingi milioni 112 na mradi umefikia 100% lakini fedha hazijafika. Wananchi wanahitaji kutumia yale maji lakini bado fedha hazijalipwa, maana yake kuna vitu bado vinahitajika kwa ajili ya kumalizia. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri utupe kipaumbele kwenye miradi hii ili wananchi waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi mwingine ni mradi wa ukarabati Oldonyosambu, Kisangiro, Olaika imefikia 95% lakini fedha shilingi milioni 117 bado hamjapeleka. Nikuombe wewe binafsi Mheshimiwa Waziri unafanya kazi nzuri lakini tukichelewesha fedha maana yake wananchi hawatapata maji. Nikuombe mpeleke fedha huko.

Mheshimiwa Spika, mradi wa Olemishiri nashukuru kwamba hilo umeshatatua tumepata shilingi milioni 100 kwa ajili ya kumalizia mradi ule lakin mradi wa Mbuke awamu ya kwanza na awamu ya pili bado wanadai shilingi milioni 550 hamjapeleka mpaka leo. Wananchi wale wanafuata maji zaidi ya kilometa 40. Tunatakiwa kuwasaidia mradi wa Mbuke phase one and two. Kwa sababu baada ya wataalamu kuanza kufanyia marekebisho kwa sababu ni existing project sasa hivi wananchi hawapati maji. Niwapongeze wataalamu kwa sababu juzi wamefunga solar lakini bado haiwafikii wananchi imefika Shule ya Msingi Arash lakini haifiki kule ambako kuna wananchi kwenye DP zile tisa zingine.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri suala lingine ambalo nataka tuone ni kwamba kwenye Wilaya ya Ngorongoro kuna zile Kata ambazo zimefuatana na eneo la Pori Tengefu. Wananchi wale walikuwa wanategemea maji kutoka yale maeneo yaliyotengwa lakini sasa hivi hawana maji. Ukienda Kata ya Ololosokwan wananchi wanategemea kwenda kuchukua maji kule kwenye eneo la Pori Tengefu lakini hakuna na kule pia hakuna vyanzo vingine vya maji. Mlichimba visima lakini mpaka leo tunasikia tu procurement ya pump bado zinafanyika ngazi ya Wizara. Tunaomba mfanyie kazi hilo kwa sababu wananchi hawapati maji na ndiyo maana bado unasikia kwamba bado kuna vurugu kati ya wananchi na wahifadhi kwa sababu hawapati maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine kwenye Kata za Arash pamoja na Piaya inaonekana kwamba kuna uhaba wa vyanzo vya maji. Kwa hiyo, tunahitaji visima zaidi. Suala lingine ni suala la Kata ya Piaya. Mheshimiwa Waziri nikuombe ombi special kabisa. Kwenye Kata hiyo ya Piaya wananchi wanakunywa maji ya chumvi ambayo ina fluoride ambayo ukiwakuta watoto wadogo wanadhurika. Kwa hiyo, nikuombe ututafutie mtambo wa kusafisha maji kwenye Kata ya Piaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni suala la bei ya maji na hii nitaondoka na mshahara wako leo usipotuambia. Ukija kuhitimisha hapa, mwaka jana nilichangia kwenye Mji wa Waso na Loliondo bei ya maji ni kubwa sana ambayo wananchi wanashindwa kumudu. Nikuombe tena utakapokuja kuhitimisha utuambie kwamba kwa sababu ulishawatuma wataalam wa EWURA kuja kushughulikia jambo hilo tujue kwamba limefika wapi ili wananchi wapate ahueni. Wananchi wengine wameamua badala sasa ya kuchota maji kwenye bomba kama anavyodhamiria Mheshimiwa Rasi, kuna wakina mama wamerudi mtoni kwa sababu hawawezi kumudu bei ya maji kwenye Mji wa Waso na Loliondo. Kwa hiyo nikuombe sana uweze kushughulikia hilo.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni suala la vitendeakazi. Unajua jiografia ya Wilaya ya Ngorongoro Mheshimiwa Waziri kwa sababu wewe umefika. Ukitoka Makao Makuu uende mpaka Pinyinyi kwenye mradi uliopo ambao unatekelezwa ambao pia bado inahitaji fedha na gari lenyewe iliyopo kwenye Wilaya yetu ambayo RUWASA wanayo ni gari bovu. Wanaweza wakakaa zaidi ya wiki mbili hawawezi kwenda kwenye mradi kwa sababu ya tatizo la gari. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri kama nilivyowasilisha mwaka jana nikuombe tena uweze kutusaidia kupata gari kwa ajili ya wataalam wa RUWASA ili wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro wanufaike na matunda ya Serikali ya Awamu ya Sita. Kwa hiyo, nikuombe sana hayo uweze kufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo mimi nishauri, naomba nishauri urasimu mkubwa uliopo kwenye Wizara yako. Tujaribu kuangalia namna ya kuweza kutatua tatizo hilo kwenye utekelezaji wa miradi.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia hotuba ya Waziri wa Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninampongeza Mheshimiwa Rais kwa filamu yake ya Royal Tour tunaona watalii wanaendelea kuja nchini. Nimpongeze pia Makamu wa Rais kwamba amefanya ziara kwenye Wilaya yetu ya Ngorongoro. Kiuhalisia amefika na at least wananchi wanaona kwamba Serikali itaenda kutatua baadhi ya changamoto ambazo zipo kwenye Wilaya ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza pia Mheshimiwa Waziri Mkuu, najua kwamba wakati zoezi la uwekaji wa beacons kwenye eneo la Ngorongoro eneo la Pori Tengefu la Loliondo alishatoa road map Tarehe 08 mwezi wa Sita mwaka jana. Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema kwamba baada ya eneo lile kuwekwa beacons kwa sababu ilitakiwa kushirikisha wananchi na wananchi hawajashirikishwa katika zoezi la uwekaji wa beacons, kwa hiyo, ilitakiwa kwamba baada ya zoezi lile kukamilika kwa sababu wananchi hawajashiriki, ni vizuri sasa tukakaa na wale wananchi tuone yale maeneo ambayo yameumia zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Mheshimiwa Mchengerwa kwa nia ya dhati, wewe siyo wa kulaumiwa leo ni wa kushauriwa kwa sababu kila bajeti ikipita tunakuja na Mawaziri wapya kwa hiyo nikuombee usiwe Waziri wa bajeti moja nikuombee uwe Waziri mpaka mwisho. Ni kwa namna gani utaweza kuwa Waziri? Ni kuepukana na machozi ya wananchi. Wizara ya Maliasili imekuwa ni sehemu ya kusababisha machozi kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Ngorongoro tukiangalia eneo la Pori Tengefu la Loliondo baada ya kutengwa, Mheshimiwa Waziri baadhi ya maeneo, kwa mfano tukiangalia Kata ya Arash, Kata ya Piyaya, Kata ya Malambo na Kata Ololosokwan na Kata ya Soit Sambu ni Kata ambazo zimeathirika sana. Tukitolea mfano, Kata ya Arash toka eneo limetengwa Mwezi June mwaka jana mpaka Februari mwaka huu, mifugo zaidi ya 6,770 imekamatwa kwa sababu wananchi hawana eneo lingine la kulisha. Kama wananchi wangekuwa na eneo lingine la kulisha mifugo yao wasingeweza kupeleka tena katika lile eneo, mifugo zaidi ya 6,700. Ukienda Kata ya Soit Sambu vivyo hivyo, ukienda Kata Ololosokwan ni hivyo hivyo Kata Oloipiri hata jana, Kata ya Malambo Kijiji cha Sanjan mifugo zaidi ya 87 imekamatwa na kutozwa shilingi milioni nane na laki saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Waziri, mimi nadhani tuna uhitaji uhifadhi sana, lakini uhifadhi huu ni kwa ajili ya nani? Ni kwa ajili ya Watanzania. Kwa hiyo, uhifadhi unaowaumiza wananchi tusiendekeze. Niombe Wizara hii inayoongozwa na Mheshimiwa Mchengerwa, kwa nia ya dhati kabisa nikuombe tuende Ngorongoro, nitatenga muda wangu nitatembea na wewe, tuangalie maeneo yote ambayo yameathirika tuweze kuwasaidia wananchi, tuwasaidie kwa sababu haiwezekani leo, hivi Mheshimiwa Mchengerwa leo Kata ya Arash wametaifishwa mifugo 276, kaya zaidi ya 280 hawana mifugo tena, watoto wao wameacha shule waliokuwa kwenye vyuo, waliokuwa sekondari, wameacha shule. Sasa naamini kwamba uhifadhi huu siyo kwa ajili ya kuwaumiza wananchi hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikuombe wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro kwa ujumla ukienda Kata, nikuambie tu niliuliza swali Namba 343 alijibu Naibu Waziri hapa. Alisema Kijiji cha Ngaresero hakipo ndani ya eneo la Poloreti. Mheshimiwa Waziri nipo tayari tusindikizane nikupeleke pale kama Kijiji cha Ngaresero hakijaingia kwenye Pori la Poloreti mimi nitajiuzuru Ubunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, beacon Namba 31 mpaka beacon Na. 159 zipo kitongoji cha Leparagashi, Kijiji cha Ngaresero zaidi ya kilomita tisa. Kwa hiyo, niwaombe wakati pia wa kujibu maswali hapa consult Mbunge anayehusika akupe ukweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku ile wakati unajibu nilikuwa Ngorongoro tulikuwa na Makamu wa Rais, wananchi walikuwa wanacheka! Kijiji hicho mifugo zaidi ya mia tano wamekamatwa, hata ya Mwenyekiti wa Kijiji cha Ngaresero ng’ombe 400 wamekamatwa, wakatozwa shilingi milioni 40. Sasa leo tukikaa tusidanganyane, ni bora tutatue matatizo ya wananchi kiuhalisia, kwa sababu utalii tunaupenda, uhifadhi tunaupenda lakini leo isiwe ni sehemu ya kuwafanya wananchi wa Tanzania kuwa maskini, iwe ni sehemu ya kuwasaidia kutatua matatizo yao. Pale tatizo linapotokea ni muhimu kukaa na wananchi tuyamalize. Naomba upange ratiba yako na tutamwomba Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Rais akuwezeshe utatue migogoro ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwenye Kata ya Ololosokwan, Soit Sambu, Oloipiri wananchi hawana mahindi. Tembo wameingia kwenye mashamba wamemaliza. Kutoa fidia mnatoa elfu ishirini na tano kwa heka imsaidie nani. Ni wakati muafaka pia tufikirie mtu shamba lake tembo wakila shamba zima tunakadiria tunapata gunia ngapi kwenye shamba mtu asiibiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunafikiria nimeona kwenye mipango yenu. Mnafikiria tena kupandisha hadhi Pori Tengefu la Lake Natron. Lake Natron imebeba Kata ya Ngaresero na Pinyinyi pamoja imeingia kwenye Kijiji cha Jema Kata ya Oldonyo Sambu. Ukija huku Tarafa ya Ngorongoro, kwa hiyo Wilaya nzima ya Ngorongoro itakuwa uhifadhi kwa asilimia 85. Hawa wananchi sijui watakuwawapi tena kwa ajili ya kuendeleza maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuende kwenye suala la uhamaji wa hiari. Suala hili tulianza na Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Waziri Mkuu alisema wananchi washirikishwe kwa dhati. Kwa jinsi zoezi linavyokwenda, ushirikishwaji umekuwa hafifu. Kuna timu zimeundwa kwa ajili ya kuandikisha watu wanaoenda. Zoezi lenyewe siyo wazi, mwananchi unamfanyia tathmini halafu unakuja kuvunja nyumba yake, siku hiyo anaondoka ndiyo unaenda kumwonesha unachomlipa. Humuoneshi kabla, lakini baada ya kuvunja makazi yake yote ndiyo unaenda kumuonesha kwamba utalipwa hiki. Mwananchi hana namna lazima aende kwa sababu umeshamvunjia makazi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba pamoja na zoezi lote, wewe umeona kwamba sasa hivi waliondoka ni wananchi 3,010 tu, wananchi waliopo pale ni zaidi ya laki moja na kumi ambao wamebaki walioandikishwa ni watu 5,000 maana yake ukishaondoa hapo tutabaki na zaidi ya watu laki moja na elfu mbili. Halafu Mheshimiwa Mchengerwa choo ikijaa unawanyima hata, naomba kwa sababu wewe ndiyo umeingia tujaribu namna ya ku-consult jamii, tuzungumze kwa pamoja tuone namna ya kutatua matatizo, kwa sababu leo huwezi ukasema kwamba wanaondoka hao watu 7,000 halafu ndiyo zoezi limeisha. Pia, kinachotakiwa zoezi liwe wazi tusifichane. Wananchi wanahitaji kujua kwamba ni watu wangapi wanahitaji kuondoka? Leo hii tunasema kwa hiari uwazi uko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni bora tuanzishe tena vikao tuzungumze kwa pamoja jamii ishirikishwe, wewe binafsi kama Waziri, mimi niko tayari kama Mbunge tushirikiane pamoja kufanya suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri lakini naomba masula yote ya Ngorongoro pamoja na Pori Tengefu la Loliondo tushirikiane kwa pamoja ili wananchi waache kulia. Nashukuru sana niunge mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Bajeti Kuu ya Serikali. Nianze kwa kumpongeza kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu pamoja na Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara ya Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiona yote yanayofanyika kwenye nchi yetu ni kwa sababu ya uongozi imara wa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, lakini hawezi kufanya kazi mwenyewe lazima wawepo washauri. Kwa upande wa fedha Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba ameonekana kujipambanua na kumshauri Rais ipasavyo. Kwa hiyo nimpongeze sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kwenye bajeti yetu tumeweka vipaumbele vingi, lakini ili tuweze kutekeleza yale yote ambayo tumesema ni lazima tusimamie makusanyo na fedha na tuweke nguvu kwenye Mamlaka yetu ya Mapato (TRA). Kuna maeneo ambayo tunaona hatukusanyi vizuri na ili tuweze kutekeleza yote kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ni lazima tuwe na fedha ambazo zinatosheleza kutekeleza miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja nimwombe Mheshimiwa Waziri, kila siku tumekuwa tukizungumza he is a humble person. Nimemwambia kule Loliondo tunahitaji Kituo cha Forodha eneo la Olaika, Ololosokwani ambapo wananchi wanatoka kilometa 500 mpaka Namanga ndiyo wakapate huduma. Wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro na unavyojua sisi hatuna barabara ya lami ni Wilaya ya Ngorongoro tu ndiyo bado hatujaunganishwa na Mkoa wa Arusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa imagine mtu anatoka Waso – Loliondo mpaka Namanga kilometa 501.5 kwa ajili ya kufuata huduma. Kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu nimwombe TRA walishafanya upembuzi yakinifu mwaka 2016, wameweka mpaka miundombinu ya maji, lakini mpaka leo hawajajenga, nimwombe sana atafute fedha popote atejengee kituo cha forodha. Wananchi wa Ngorongoro watamshukuru na watamshukuru Mheshimiwa Rais kwa yote ambayo wanatenda pamoja na hicho kituo cha forodha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, Wilaya yetu ya Ngorongoro bado hatujaunganishwa na Mkoa wa Arusha. Ukijaribu kuangalia wilaya zingine zote saba zimeunganishwa kwa lami na mkoa, lakini sisi hatujaunganishwa. Tunahitaji na ukijaribu kwenda kule kwetu usafiri ni wa shida. Hata leo Mawaziri ukiwaambia njooni Ngorongoro, ukimwambia atatembea kilometa 300 rough road anaanza kufikiria hapo kweli nitarudi salama? Naomba basi na sisi watukumbuke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Makamu wa Rais aliagiza kwamba kilometa 39 kutoka Ngaresero mpaka Engaruka ziingizwe kwenye bajeti, zimeingizwa. Kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu akiona tu Barabara ya Loliondo kwa ajili ya lami naomba apitishe usiku hata asisubiri asubuhi kwa sababu wale wananchi wanateseka. Unaambiwa sisi tuna gari moja ya Loliondo Coach, ndiyo inatoka Arusha kila siku kwenda Loliondo, kwa sababu magari mengine yakija, kesho yake hayawezi kurudi kwa sababu ya miundombinu iliyopo. Kukodisha gari kutoka Arusha mpaka Loliondo kwa ajili ya huduma ya wananchi na biashara wananchi wanashindwa kufanya biashara na kuboresha maisha yao kwa sababu ya ughali wa maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukipata barabara hii itatusaidia na sisi kuongeza uchumi wa wilaya yetu na huku pia tukijua kwamba barabara ile kutoka Kigongoni kupita Oldonyo Lengai mpaka Loliondo ndiyo watapita watalii wataenda mpaka Serengeti. Kwa hiyo niwaombe sana Serikali, tujaribu kuangalia namna tuharakishe barabara ile, tuweke hata kwenye mpango wa EPC+F, itatusaidia kuboresha maisha ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, Wilaya ya Ngorongoro tuna kata 28, lakini mpaka leo tuna vituo vya afya sita tu, zahanati tunazo 31 kati ya vijiji 62. Tulikuwa na huduma na fly medical service, TCIAA wanasema kwamba ni lazima wasajiliwe nchini, SMS wameweza kufanya kazi kwa miaka 40. Leo Wilaya ya Ngorongoro vifo vya akinamama na watoto vimeongezeka ghafla kwa sababu ndege ile ndiyo ilikuwa inawasaidia. Kwa hiyo nimwombe sana Waziri, wanasema lazima tulipe kodi, niombe washirikiane na Wizara ya Uchukuzi na Wizara ya Afya, wale watu tuwape kibali cha kutoa huduma kwa wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu leo mtu amekuja, amefanya kazi miaka 40, halafu leo unakuja kumkatisha kwamba tunataka ujisajili, tunataka ulipe kodi na anatoa huduma ambayo Serikali imeshindwa kutoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa mchango wa maandishi kufuatia kuwasilishwa kwa bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, ifuatayo ni mchango kwa Wizara hii; kwanza ili kuboresha utalii na kuvutia watalii wengi nchini Wizara haina budi kushirikiana na Wizara nyingine kwa ajili ya kuboresha miundombinu mbalimbali ya barabara hasa barabara ya kutoka Loduare mpaka Nabi Gate kwani ni barabara muhimu sana kwa watalii wanaotembelea Hifadhi ya Ngorongoro na Serengeti na barabara ya lami kutoka Mto wa Mbu mpaka Loliondo kwani nayo ni muhimu kwa watalii kufika Oldonyo Lengai.

Mheshimiwa Spika, Wizara ipitie na kufanyia kazi maoni ya wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro, Sale na Loliondo kwani ndiyo mwarobaini wa changamoto za muda mrefu za maeneo hayo. Ni muhimu sana Serikali ione kuwa eneo la pori tengefu la Loliondo ni ardhi ya vijiji, hivyo vijiji husika ziruhusiwe kutumia ardhi yao bila usumbufu na wananchi waondokane na mgogoro wa ardhi iliyodumu kwa miaka 31 sasa, kimsingi mgogoro huu umewarudisha wananchi nyuma kiuchumi na wengine kupoteza maisha pamoja na mali zao.

Mheshimiwa Spika, Wizara itafakari upya namna ya kufanya kazi na Baraza la Wafugaji ili kurejesha mahusiano na wananchi wanaoishi kwenye eneo la Hifadhi ya Ngorongoro, pamoja na kutekeleza jukumu lake la kuwapatia wananchi wenyeji maendeleo kama ilivyo kwenye sheria ilyoanzisha eneo hilo bila kuwawekea vikwazo vya kimaendeleo kama ilivyo sasa.

Pia Wizara itekeleze MoU iliyoingiwa kati ya Wizara, Baraza la Wafugaji, NCAA na Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro na kuwaajiri watumishi wa Baraza la Wafugaji.

Mheshimiwa Spika, mwisho ni kuhusu kuboresha huduma za waongoza watalii na quality za magazine.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru pia kwa kunipa nafasi kuchangia kwenye Wizara hii ya Kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika na Mheshimiwa Waziri, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa upendo wake kwa Watanzania kwa kukubali kutenga fedha nyingi kwa ajili ya Wizara hii ya Kilimo. Kama tunavyojua, kilimo kimewaajiri Watanzania wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri na watendaji wote kwenye Wizara hii. Ni wasikivu sana. Jana tu nilikuwa na tatizo kwenye Jimbo langu lakini nimemplekea Mheshimiwa Waziri na watendaji wake, wameshafanyia kazi. Hawa ni watendaji, ni watumishi wa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana bajeti hii, kutoka Shilingi bilioni 294 mpaka Shilingi bilioni 751 ni ishara kwamba tumeamua sasa kuwakwamua wakulima wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kitu kimoja. Kwenye Wilaya ya Ngorongoro kuna maeneo mengine ambayo sasa hivi tunatafuta namna ya kupata maji, lakini sisi kwenye Kata za Pinyinyi, Oldonyosambu, Digodigo na maeneo mengine kama Engaresero, Enguserosambu kuna maji ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachotakiwa ni kuweka miundombinu kwa ajili ya wananchi wetu kuanza kunufaika na mfumo wa umwagiliaji. Tukijaribu kuangalia kwa mfumo wa sasa hivi wa dunia, watu wengi wamekwenda kwenye kilimo cha umwagiliaji. Kwa nini, na nchi nyingi, kwa nini wameamua kwenda? Ni kwa sababu kilimo cha umwagiliaji ndicho kilimo cha uhakika kuliko kilimo cha kutegemea mvua. Tukichukulia mfano mwaka huu, watu gani wana uhakika wa kuvuna ni watu wanaotegemea kilimo cha umwagiliaji. Kwa sababu kwa wale wanaotegemea kilimo cha mvua wengi wamepata hasara hakuna mvua za kutosha. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kuamua sasa kuangalia katika mfumo huu wa irrigation system ambao utakwenda kuwakwamua Watanzania wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri, kwenye Wilaya yetu ya Ngorongoro wananchi wanapata hasara sana kwa sababu hawana hata ghala moja kwa ajili ya kuhifadhi chakula kipindi cha mavuno. Inawabidi wauze mazao yao kwa bei ya hasara; kwa sababu hawana namna ya kuhifadhi. Kwa hiyo, nikuombe kwenye Wilaya yetu ya Ngorongoro kaangalie kwenye mifuko yako yote, chonde chonde utupe angalau ghala moja kwa ajili ya wananchi kuhifadhi chakula chao. Kila mwaka sisi tumekuwa tukiuza chakula, mahindi kwa Wakenya kwa sababu hatuna maeneo ya kuhifadhi, na wao wanatumia opportunity hiyo kuja kununua chakula mpaka mashambani; ni lazima tuwalinde wakulima wetu namna ya kunufaika na kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala lingine niombe tupeleke mbolea pia. Ukienda leo Kata ya Pinyinyi, ni eneo ambalo tukiamua kuwekeza tutazalisha mbegu nyingi sana. Sasa hivi Kampuni ya Kibo Seeds wanawapa wakulima mbegu za alizeti na bamia wanazalisha halafu wanawapa bei wanayotaka wao. Lakini Serikali pia tunaweza kuzalisha mbegu katika eneo lile, ukienda kwenye Kata ya Oldonyosambu tunaweza tukatumia maji yaliyopo kwaajili ya wananchi kunufaika. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri tuwasaidie wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niomba kitu kingine, kuna tatizo la emergence services kwenye Wizara ya Kilimo pia. Mwaka huu mwanzoni mwezi wa tatu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: …wananchi walipata shida sana. Nashukuru sana niunge mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuwa mchangiaji wa mwisho wa hotuba ya Waziri wa Maliasili na Utalii. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa filamu yake ya Royal Tour ambayo Mheshimiwa Naibu Spika alisema asubuhi kwamba, mama ameupiga mwingi na sisi tunaupiga wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mimi niwashauri Wizara kwamba Mheshimiwa Rais ametutangaza vya kutosha, sisi tunatakiwa kuweka miundombinu wezeshi kwa ajili ya kuwapata watalii. (Makofi)

Kwanza ukijaribu kuangalia barabara zetu zinazokwenda kwenye hifadhi zetu nikitolea mfano barabara kutoka Lodoare kwenda Nabi Gate ni barabara ambayo yanapita magari yanayokwenda Hifadhi ya Ngorongoro pamoja na Serengeti, kwa hiyo, tunatakiwa kuhakikisha kwamba, tunaboresha miundombinu yetu. Lakini pia barabara inayotoka Mto wa Mbu kuelekea Loliondo ni barabara muhimu pia ambayo Wizara hii inatakiwa kwa kushirikiana na Wizara ya Ujenzi kuangalia namna ya kuboresha ili watalii waweze kupita katika njia zile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kipengele cha idara ya wanyamapori, nimeona mapendekezo yao ya kuweza kupandisha baadhi ya mapori tengefu kuwa mapori ya akiba. Mapori hayo yaliyotajwa, kipengele namba 5.3.1.1 Lake Natron, Kilombero, Loliondo, Lolkisale, Longido, Mto wa Mbu na Simanjiro. Mimi naomba niwaambie kwa upande wa pori tengefu la Loliondo wananchi wa Loliondo wameleta mapendekezo yao na wameshakabidhi kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Niishauri Wizara mkapitie taarifa zile za Loliondo pamoja na Ngorongoro ili angalau zikafanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini leo huku tunalia Loliondo, mmeshaenda Lake Natron. Wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro pande zote mnapiga Mashariki, Kusini, Kaskazini, wananchi wanalia kote. Lake Natron ni Wilaya ya Ngorongoro pia, Loliondo ni Wilaya ya Ngorongoro, ukienda Ngorongoro tarafa ya Ngorongoro eneo la Ngorongoro Conservation Area ni Wilaya ya Ngorongoro. Sasa hao wananchi kwa nini hamtaki wapumue? Kila upande mnawapiga, kwa nini? Leo mnakuja kusema mnapandisha pori tengefu la Mto wa Mbu, hivi pori tengefu la Mto wa Mbu liko wapi? Liko wapi?

Mheshimiwa Spika, kote kumekuwa ni mji, sasa maana yake tunaendelea tena kwenda kuongeza taharuki kwa wananchi wa Wilaya ya Monduli. Bado hatujamaliza Monduli, Wamasai wa Longido watalia kwa sababu mmeandika hapa, bado hawajapumzika hao tunaenda Lolkisale watalia kule, bado hatujanyamaza tunaenda Simanjiro. Hao wananchi tunawatakia nini? Huu uhifadhi tunaouhifadhi ni kwa manufaa ya nani?

Mheshimiwa Spika, kama uhifadhi sasa imekuwa kilio kwa wananchi haina haja ya kuwa na uhifadhi huu. Ni lazima tuwe na uhifadhi ambao unawaletea wananchi maendeleo, lakini uhifadhi ambao unaleta kilio kila siku kwa Watanzania hauna manufaa kwa sababu leo wakilia wananchi wa Kilombero, watakimbia Loliondo, wakilia wa Loliondo wataenda Lake Natron, wataenda Simanjiro, wataenda Lolkisale, sasa sijui hawa wananchi tunawatakia nini?

Mheshimiwa Spika, mimi nadhani kinachotakiwa sasa ni lazima tuamue mgogoro wa eneo la Loliondo umedumu kwa zaidi ya miaka 31 sasa, Serikali ni lazima tufikirie namna wale wananchi waachwe waendelee na maisha yao, tumewarudisha nyuma kimaendeleo, kiuchumi na lile eneo ndipo wanapochungia mifugo yao.

Kwa hiyo, mimi nishauri Wizara kuna maeneo mengi tumeshahifadhi, square kilometer 307,800 za Tanzania nzima ambayo ni asilimia 32.5 mpaka 40 ya ardhi yote tuliyonayo Tanzania. Maeneo mengine tuwaache wananchi waendelee na maisha yao.

Mheshimiwa Spika, lakini suala lingine Wizara hii, kama alivyosema Mheshimiwa Mulugo, wanyamapori wanaingia kwenye mashamba ya wananchi, tunasema tunatoa fidia, lakini miaka yote tumeshindwa kutoa fidia kabisa. Kama alivyosema Mheshimiwa Kuchauka hata wananchi wangu wa Kata za Oloipiri, Soitisambu, Ololosokwan na kata nyingine mashamba yao yote yameliwa na tembo. Sasa tutafute namna ya kuwapelekea chakula kwa sababu tembo wanaingia kwenye mashamba wanamaliza moja kwa moja, lakini hakuna fidia yoyote inayotolewa na Wizara ya Maliasili, lakini pia kuna wananchi wanauawa na tembo na wanyama wengine wakali…

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Shangai, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Londo.

T A A R I F A

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, sio tembo tu, hivi tunavyozungumza kwa wiki nne ndege wanashambulia mashamba ya wakulima katika Kata ya Kilangali, Wilaya ya Kilosa, lakini ndege hawa wanahifadhi ndani ya Hifadhi ya Mikumi na tumeomba zaidi ya mara tatu/mara nne tupate kibali cha Wizara ya Kilimo kwenda kuuwa ndege hawa, hatujapata mpaka sasa. Kwa hiyo, sio tembo tu wanakula mazao ya wakulima, hata ndege pia. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Ole-Shangai.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, mimi nashukuru na ninapokea Taarifa ya Mheshimiwa Londo, lakini kikubwa…

SPIKA: Ngoja, subiri kidogo.

Waheshimiwa Wabunge, ili upokee au ukatae Taarifa, lazima Kiti kiwe kimekuuliza unaipokea au unaikataa? Kwa hiyo, mimi sijakuuliza swali hilo, nimekuita tu ili uendelee kuzungumza.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, niendelee kwa sababu, jamaa ameamua kula muda wangu, lakini mimi nishauri Wizara hii wananchi wa Tarafa ya Ngorongoro wameleta maoni yao, wamekabidhi kwa Waziri Mkuu, mkaisome, hayo ndio maoni ya wananchi na ndio msimamo wao.

Mheshimiwa Spika, naomba niende kukaa, ili badae Waziri atakapokuja atuambie fine kwa ajili ya mifugo wanaoingia hifadhini ni shilingi ngapi? Kwa sababu kumekuwa na varieties, leo unakuta ni 10,000; 50,000; mpaka laki moja; kwa hiyo, baadae Waziri atuambie ni kiasi gani kinatakiwa mifugo wanapoingia hifadhini? Ahsante nashukuru. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia taarifa ambazo zimewasilishwa na Kamati zetu za Kudumu za Bunge kuhusiana na Ripoti ya CAG.

Mheshimiwa Spika, ninaomba kutumia nafasi hii, kabla sijachangia naomba kuwapa pole wananchi wa Jimbo langu, kaya 30 ambao wametaifishiwa mifugo yao 900 na TANAPA wiki hii. Inafadhaisha, yanayotokea sasa hivi hapa, inaonesha kuna watu hawatekelezi majukumu yao vizuri. Kwa sababu, kwa suala hili la hawa wananchi kutaifishiwa mifugo ninaamini kwamba walipelekwa mahakamani wakasema hawana mwenyewe na wala hawana wenyewe.

Mheshimiwa Spika, kiuhalisia hili suala lilikuwa linajulikana. Kwa hiyo, tutoe tahadhari kwamba Serikali yetu isije ikawa ni sehemu ya kuwafanya wananchi wawe maskini. Kwa sababu, kutaifisha mifugo 900 kaya 30 maana yake wale wananchi wameshakuwa fukara. Sijui tutawaingiza kwenye mfumo wa TASAF au tutafanyaje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jana nilikuwa ninatafakari kuhusiana na Ripoti ya CAG…

SPIKA: Mheshimiwa Oleshangai ngoja hili Bunge tulielekeze vizuri kwenye kufanya maamuzi. Jambo hili unalolizungumza sasa ni sehemu ya Taarifa ya CAG au ni la kwako kama Mbunge kwa sababu linawagusa wananchi?

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, ni la kwangu kama Mbunge kwa sababu linawagusa wananchi wangu.

SPIKA: Sawa, sasa ngoja tuliweke vizuri. Kwa sasa, kwa sababu umesimama kuchangia hoja iliyoko mezani, ikiwa kuna jambo ambalo unataka kulifikisha ili Serikali ilifanyie kazi, inabidi utumie kanuni nyingine ili Taarifa zetu za Bunge zikae vizuri. Kwa sababu, kwenye hoja hii, hoja ni ya Kamati. Kwa hiyo, hata uhitimishaji watakuja kuhitimisha Wenyeviti ambao hawana uwezo wa kulizungumzia hilo. Ili likae vizuri, utakapomaliza mchango wako unaohusu Taarifa ya CAG baadaye tukishamaliza hayo tafuta kanuni ambayo itakufanya uliseme hilo jambo la wananchi wako.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, ninashukuru na ninaomba kuendelea kuchangia Ripoti ya CAG. Nilikuwa natafakari kuhusiana na yanayotokea. Kwenye taarifa zetu kuhusiana na Ripoti ya CAG. CAG amepewa majukumu, ukijaribu kusoma ni kwamba anaitwa ni Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Serikali. Ninaamini kwamba CAG amekuwa akitekeleza jukumu moja la ukaguzi lakini udhibiti imekuwa labda sio sehemu ya kazi zake.

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye Mfuko wa NHIF tumekuwa tukilalamika kwamba mfuko hauwezi kusaidia kuhudumia wananchi ambao wanaenda hospitali kwa ajili ya kutibiwa, cha kushangaza ni kwamba, kuna fedha ambazo watumishi wa NHIF wamekopeshana zaidi ya shilingi bilioni 41. Hizi fedha wamekopeshana wakati sheria inawaruhusu kukopeshana kutumia mfuko wa kuzungusha au revolving funds, lakini wao wamekuwa wakikopeshana fedha ambazo zinatokana na michango ya wanachama wa NHIF.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo ninataka kulichangia kuhusiana na NHIF, Waziri wa Afya kila siku hapa amekuwa akisema mfuko wa NHIF unakufa. Lazima ufe, kwa sababu, Serikali yenyewe inadaiwa zaidi ya shilingi bilioni 228 na hamtaki kulipa, Serikali haitaki kulipa fedha hizo kwa mfuko wa NHIF kwa ajili ya kuwahudumia wanachama wake na leo hii tumeondoa ile Toto Afya Card lakini Serikali ingeweza kulipa fedha nyingine ambazo zingeweza kuwahudumia watoto wa maskini ambao hawapati huduma.

Mheshimiwa Spika, suala lingine. Kuna ununuzi wa vifaa ambavyo vilifanyika kupitia bohari ya dawa. Kuna Kampuni ya Alhandasia ambayo walipewa kandarasi ya kununua vifaa aina 75 kwa shilingi bilioni 3 lakini mpaka kufikia tarehe 30 Oktoba, 2021 kampuni hiyo imeonekana kwamba ni kampuni hewa. Ukiwauliza watu wa bohari ya dawa wanasema tuliwatafuta online tukalipa fedha online na fedha zikapotea na yule mtu ajulikani alipo.

Mheshimiwa Spika, tunashangaa. Ni mtumishi gani wa Serikali ambaye unaweza ukalipa fedha online halafu ukasema huyo mtu hayupo na namba ya account baada ya kulipa ikatoweka. Are we serious? Kwa sababu, leo unalipa fedha halafu unasema baada ya kulipa, halafu mtu anatoweka. Anajitokeza mtu mwingine anaitwa EPICO anasema mimi nitaleta hivyo vifaa pamoja na zile za Alhandasia. Maana yake inawezekana kuna ushirika fulani ambao unatengenezwa halafu baadaye tunasema hatumjui mtu, kumbe huyo EPICO ndiyo huyo huyo tena amebadilika jina alikuwa anaitwa Alhandasia sasa hivi anaitwa EPICO. Kwa nini sasa yeye akubali kubeba gharama za yule mtu ambaye ametoweka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaamini kila mtu akiweza kutimiza wajibu wake tunaweza ku-control haya matatizo yanayotokea. Hivi kweli mtu anasema alitoweka, wewe ulimlipaje mtu kama haumjui. Bahati mbaya au nzuri walimwandikia Balozi wa Misri, Balozi wetu. Akawaambia huyu mtu sisi hatumfahamu, baadaye wao wakaamua kulipa. Halafu hawa watu bado wanatembea mitaani. Huku tunakimbizana na machinga kuwanyanganya shilingi elfu 20 wakati huku tunapoteza shilingi bilioni 5. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baadaye huyu mwingine anaitwa EPICO anajitokeza anasema ataleta hivyo vifaa aongezewe shilingi bilioni 10 ili alete zile za shilingi bilioni 3 lakini sharti lake alipwe shilingi bilioni 10. Imagine!

Mheshimiwa Spika, ninaamini kwamba, tuna tatizo ambalo tusipoamua kulitibu kama nchi tutaendelea kuwaumiza Watanzania. Leo tukifikiria shilingi bilioni 3 tutajenga vituo vya afya vingapi? Lakini zimepotea. Nimeangalia ripoti… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa dakika moja malizia. Kengele ya pili imeshagonga.

MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Spika, kuna suala lingine la halmashauri zetu, halmashauri zetu kuna tatizo moja kubwa la ukusanyaji wa mapato. Niishauri TAMISEMI, kule chini ukijaribu kuangalia ukusanyaji wa mapato kuna POS machine lakini zinapoletwa kwenye Taarifa ya CAG, kuna POS machine ambazo hazifanyi kazi moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, Mheshimwa Waziri itabidi uwaagize Wakurugenzi, zote zipitiwe zile ambazo hazifanyi kazi tuondoe hizo quarries. Mimi nimekuwa Mwenyekiti wa Halmashauri, unakuta kuna POS Machine, tumewapa wale watu wa mitaani waingize au wakusannye ushuru. Badala ya kuandika shilingi elfu nane unakuta ameandika shilingi milioni 8. Halafu ndiyo hizo CAG anaenda kusema ni fedha ambazo hazijakusanywa. Kuna POS errors ambazo watu wanaingiza fedha. Mfano, mbuzi mmoja ni shilingi 2500 lakini unakuta kwenye POS Machine mtu anaandika vibaya, anaandika elfu 25 kufuta hawezi mpaka atoke mtu makao makuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwenye halmashauri zetu kuna vitu vingine ambavyo vinahitaji hekima pamoja na ku-act haraka ili tuweze kuondoa hizi querries ambazo hazina maana. Kwenye halmashauri zetu, unakuta mtu anataka aandike shilingi elfu 80 anaandika shilingi laki 8. Hawezi kurekebisha mpaka atoke mtu makao makuu. Hiyo kama Serikali tunahitajika kuchukua hatua pamoja na kuwatafuta wataalamu wa kukusanya mapato wengine kule chini.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru. (Makofi)