Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Mohammed Said Issa (3 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii adhimu kuweza kusimama leo katika Bunge lako Tukufu hili, ikiwa ni mara ya kwanza kwangu mimi kuweza kusimama na kuzungumza na mimi kutoa mchango wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ningependa kuanza na kutoa shukurani kwa sababu, mimi ni mara yangu ya kwanza kuzungumza katika Bunge hili. Ningependa kuwashukuru kwanza wapiga kura wangu wa Jimbo la Konde kwa kunichagua kwa kura nyingi sana, walinipa ushindi wa asilimia 72 katika uchaguzi ambao ulifanyika wa marudio nawashukuru sana. Pia ningependa kushukuru chama changu, Chama cha ACT-Wazalendo kwa kuniamini na kuni- support mpaka kufikia ushindi huo ambao leo nimepata heshima kubwa ya kuwa Mbunge katika Jimbo la Konde, nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya yote mimi nimekaa hapa kwenye kiti baada ya msiba wa marehemu Kaka yangu Khatib Said Haji, Mwenyezi Mungu ailaze mahali pema roho yake peponi. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Amina.

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru wewe pia kwamba ulikuwa unawasiliana na familia kwa ajili ya kusimamia matibabu ya Mheshimiwa Marehemu Khatib Said Haji. Yale mawasiliano uliyokuwa unafanya ulikuwa unafanya na mimi na niliziona juhudi zako. Kwa niaba ya familia tunakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niishukuru Serikali mbali ya juhudi ulizozifanya wewe, tulikuwa tukipata mawasiliano kupitia Serikali. Kwa ajili ya kuhakikisha mpendwa wetu yule maisha yake yanaokoka lakini kwa mapenzi ya Mwenyezi Mungu ilikuwa bahati mbaya Mwenyezi Mungu alimuhitaji zaidi. Kwa hiyo, kwa hali hiyo nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa kuishukuru Serikali kwa kuendesha uchaguzi wa marudio wa Jimbo la Konde. Uchaguzi ambao ulikuwa ni mfano wa kuigwa, uchaguzi ambao ulionesha kwamba Tanzania tunaweza kufanya uchaguzi wa demokrasia, demokrasia ikashika nafasi yake na watu wote wakafurahia matunda ya demokrasia. Kwa kweli naipongeza sana Serikali kwa kufanya uchaguzi ule ambao hata kunguni hakuuliwa wala hakuguswa. Ahsanteni sana Serikali kwa kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependa kumshukuru pia Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan na kumpongeza sana, katika hotuba yake ambayo alionesha dhahiri ana nia ya kusimamisha demokrasia katika nchi yetu pale alipokuwa kwenye kumbukizi ya maisha ya Marehemu Maalim Seif Shariff Hamad. Namshukuru sana na ninamuomba, aendelee na nia hiyo hiyo ya kusimamisha demokrasia ili Tanzania tusiwe ni wahanga wa demokrasia tuwe tunafurahia matunda ya demokrasia. Kwa hiyo, ningependa kushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo nije kwenye mpango. Mimi natoka Visiwa vya Zanzibar ni Mbunge kutoka visiwani. Ukisikia Visiwa ni kwamba tumezungukwa na bahari. Bahari sasa hivi imekuwa ikimeza visiwa kila uchao, visiwa vimekuwa vikimegwa kupitia bahari. Hili lipo katika sehemu ya mazingira. Ukija kwenye Jimbo langu la Konde nimezungukwa na bahari kupitia sehemu zangu za Msuka, Makangale, Tondooni, Mnarani kote ni bahari tupu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahari imeshakula karibu nusu kilomita ya eneo la ardhi katika Jimbo langu. Sasa, nikija kwenye mapendekezo ya mpango napendekeza kwamba, katika Jimbo langu kuna kilimo kikubwa sana cha mwani, kilimo hiki mwenzangu Mheshimiwa Omar alikizungumzia jana lakini mimi nitakizungumzia katika eneo tofauti. Nitazungumzia katika maeneo mawili. Eneo la kwanza ni kwamba, kilimo cha mwani ni kilimo ambacho kinalimwa baharini na unapolima kilimo cha mwani maana yake bahari unaifanya ikimbie katika eneo la ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo hiki kilimo ni kilimo ambacho Serikali inatakiwa kukiangalia sana na kukipa nguvu kubwa ili kuokoa ardhi kuliwa na bahari. Lakini lingine katika kilimo hiki unapolima kilimo hiki maana yake kunapatikana mazalia ya samaki, pia ni faida kubwa sana nimeona katika mpango, tunategemea kupata meli nane za uvuvi pia kama tutakuwa tuna mazalia wengi sana ya samaki, maana yake hizo meli za uvuvi ndio zitaweza kupata kazi. Kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba Mheshimiwa Waziri katika mpango wako uweke kipaumbele katika kilimo cha mwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikihama katika sehemu hiyo nakuja katika kukuza mapato. Katika mpango umetueleza kwamba mapato yameendelea kukua kwa asilimia 7.2 ni kweli kwa data ulizonazo wewe ni hivyo, kama tunavyojua njia kuu ya mapato ya Serikali ni TRA, TRA ndiyo wanakusanya mapato kwa asilimia kubwa ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lililopita TRA walilalamikiwa sana kwa kufanya makadirio ambayo yalisababisha wafanyabiashara wengi kufunga biashara zao. Sasa hawa TRA wamekuwa kama vile sijui nisemeje mimi. Maana yake wakati ule walilalamikiwa kwa kutoa makadirio makubwa, kuwalazimisha wananchi kodi ambazo hazina msingi, sasa wamehama katika stage ile wamewachenga kidogo wafanyabiashara, sasa hivi wameleta e-filing. E-filing maana yake mfanyabiashara atapeleka ripoti zake kwa kutumia mfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini e-filing tuelewe kwamba wafanyabiashara wengi hawana uelewa wa mambo ya mitandao. Wafanyabiashara wetu ni wale ambao wameshindwa na maisha wakaamua kujiingiza katika biashara. Sasa basi e-filing walivyoileta wameweka mambo ambayo ni ya ajabu ambayo hayamsaidii mfanyabiashara. Kwa sababu, kama walikuwa na shida ya kukusanya mapato kwa kutumia system hii ni sawa, lakini kwanza wangetoa elimu kwa wafanyabiashara hili halikufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili wameingiza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimshukuru Allah Subhanahu wa Ta’ala kwa leo kupata nafasi na mimi kuweza kuchangia katika Bunge hili tukufu katika Hotuba ya Waziri Mkuu. Lakini pia nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii ambayo ni kwa ruksa yako ndiyo naweza kuzungumza hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mchango wangu kwanza utajikita katika biashara; na hii biashara ni katika nchi mbili hivi Zanzibar na Tanganyika, yaani Tanzania Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar na Tanzania Bara tumekuwa tukitegemeana katika mambo mengine ikiwemo biashara. Tunatumia bandari zetu ya Zanzibar na Dar es Salaam.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Waheshimiwa tumsikilize mchangiaji.

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatumia bandari zetu ambazo zipo katika Zanzibar na Tanzania Bara katika kupitisha mizigo yetu, lakini mara nyingi biashara huwa inatokea Zanzibar kuja Dar es Salaam ama Tanzania Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye biashara ambayo tunafanya sisi Wazanzibar au wananchi wa Zanzibar tumekuwa tukikutana na changamoto nyingi sana ambazo kwa kiasi kikubwa imeonekana inakuwa ni tatizo linalosababishwa makusudi lakini si mipango ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango hii mara nyingi iko vizuri, lakini watendaji ndio wanaoiharibu. Nitoe mfano kidogo. Katika suala la declaration ya mizigo ambayo inasafiri kutoka Zanzibar kuja Tanzania Bara, mizigo ile mara nyingi meli yetu inakuwa ni za hapo kwa hapo siyo zile Meli ambazo tayari zina shadow. Kwa maana hiyo wafanyabiashara ambao wanaleta mizigo wanakuwa na mizigo ambayo ni ya kushtukizwa. Kwa mfano kama kipindi hiki cha mwezi wa Ramadhan, mfanyabiashara ananunua mzigo leo anataka apakie mzigo kwenye meli lakini kwa bahati mbaya ni lazima awe ametuma ripoti mapema ili mzigo ule uweze kupakiwa na kufika kule, nje ya hapo mzigo ule ukifika meli inapigwa faini na mzigo unapigwa faini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hii ni changamoto ambayo wafanyabiashara wa Zanzibar wanakutana nalo. lakini si hilo tu, wafanyabiashara wa Zanzibar tumekuwa tukikutana na changamoto ya mizigo ambayo inafika pale Dar es Salaam. Tunakutana na bei kubwa ya wharfage ambayo inakuwa inachajiwa mizigo ambayo inatoka Zanzibar. Kwa hiyo tungeomba bei ile iendane na hali halisi, hasa ukizingatia ile sehemu ambayo inashushwa ni sehemu ambayo fedha zake za kujengea pale zilitoka kwa Rais wa Kwanza wa Zanzibar Mheshimiwa Abeid Aman Karume, kwa ajili ya kuwasaidia Wanzazibar lakini leo imekuwa inawakwaza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, baada ya kuyasema hayo, ningependa kwenda kwenye hilohilo la TRA. Mizigo inapotoka bandarini kwenda madukani imekuwa ikisumbuliwa na TRA haohao ilhali imeshafanyiwa inspection na kulipiwa kodi kama kawaida lakini ikifika njiani ikifika tu, ikitoka nje ya geti kuna TRA wengine wanajitokeza na kuwasumbua wafanyabiasha hawa na kushindwa kufanya kazi zao vizuri. Kwa hiyo hili naomba lifanyiwe kazi ili kuendeleza Muungano wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nizungumzie suala la Muungano. Katika ukurasa wa 72 Mheshimiwa Waziri Mkuu ameelezea kuudumisha, kuuenzi na kuulinda Muungano na mimi naipongeza Serikali yetu hilo ndiyo tunalolihitaji kwa sababu Muungano huu ni tunu ya taifa na sote tunaupenda. Lakini kubwa zaidi nilitaka nichangie hapa; hizi kero za Muungano ambazo zimekuwa zikifanyiwa kazi, mimi nakubaliana nazo, ni nzuri na zinasaidia kuondoa changamoto lakini bado tunatakiwa tufike kwa wananchi kujua ni changamoto gani hasa zinaweza kuulinda Muungano? Kwa sababu wananchi bado wanasema kwamba hizi changamoto ni zile zinazoikabili Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Tanzania, siyo zinazowakabili wananchi. Kwa hiyo, baada ya kutatua changamoto hizi 11 basi turudi kwa wananchi ili na wao waseme ni lipi hasa linaweza kuimarisha Muungano wetu huu na ukawa Muungano wa mfano kama ilivyosema Hotuba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hapo, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia katika Wizara hii ya Nishati. Awali ya yote, niwapongeze Mheshimiwa Waziri wa Nishati Mheshimiwa January Makamba pamoja na Naibu wake, lakini pamoja pia na watendaji wake katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli dira ambayo wameionesha ya kutuhakikishia Watanzania kupata umeme wa uhakika ni nzuri sana, mipango yao kwa kweli mimi binafsi naipongeza. Pia hii imeonesha, pale ambapo katika michango yetu ya leo Wabunge, baada ya kupata semina ambazo zimetupa uelewa mkubwa, nimeona pia Wabunge wengi sana wameelewa mipango ya Wizara. Kwa hiyo, hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu nitaanza kwa sehemu ya Umeme wa Joto Ardhi yaani geotherm. Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake hapa ameonesha kwamba tutapata umeme wa megawatt 195 ya Umeme wa joto ardhi, lakini mimi kama Mjumbe wa Kamati tulivyofuatilia tumeona kwamba bado Sheria ya JotoArdhi haijawa sawasawa, haijatekelezwa. Sasa najiuliza maswali, ni wapi hasa Waziri anaweza kuja kutekeleza kuzalisha umeme wa jotoardhi wakati bado haijatambulika kwamba bado ni sehemu ya madini ama ni sehemu ya nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waziri anapokuja ku-windup atueleze tayari amefikia wapi kwanza sheria haijaletwa, lakini la pili hakuna miundombinu na la tatu pia bado fidia kwa wanaomiliki maeneo haya yenye jotoardhi haijafanyika. Kwa hiyo, tunakujaje kuzalisha umeme huu wakati haya mambo ya msingi bado. Tunaomba anapokuja ku-windup atufahamishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa REA, tunawapongeza sana mpango wao ni mzuri kwa kuhakikisha kila kijiji, kila kitongoji kinapata umeme unaostahiki, lakini kuna tatizo kidogo ambalo limejitokeza. Tulivyofanya ziara Kamati tuliona kwamba REA imepeleka umeme kijijini lakini nyumba zilizounganishwa ni mbili. Ina maana hapa hakuna maandalizi mazuri, watu hawakuandaliwa na pale tayari kuna mkandarasi tayari ameshalipwa, waliopata umeme ni watu wawili ama watatu, lakini zipo nyumba za jirani hazipata kwa sababu hawakuandaliwa. Nashauri kabla ya kufika pale wananchi waandaliwe, wafanye fitting ili wote wa-enjoy ule umeme wa REA unaokwenda pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine pia ni hili suala la ujazilizi; naona REA kwanza tulianza mita moja, halafu tukaenda mita mbili, halafu tunaenda ujazili, yaani tunakwenda mwisho tutafika hata majina mengine hatuyafahamu. Kwa hiyo, nashauri kwamba sisi lengo letu si mita moja, si ujazili lengo letu ni kuwapa umeme wa uhakika wananchi. Kwa maana hiyo tuhakikishe ile sehemu ambayo tuna deal nayo, basi wapate umeme wote sio tunarudia, hili jambo linatutia hasara kama Taifa, kesho tunarudia, kesho mkandarasi huyu, kesho mkandarasi huyu, linatutia hasara. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri alichukue hili pamoja na timu yake waliangalie ili kuondoa hasara kwa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine niende kwenye suala la bei za umeme; hili suala la bei za umeme, nazungumzia umeme wa mijini, sizungumzii umeme wa vijijini ambao huo tumeshaujua ni Sh.27,000. Mheshimiwa Waziri watu wa mijini ambao tayari wana umeme, wale wenye uwezo tayari wameshaweka umeme kwa maana hiyo watu ambao hawajaweka umeme, hawana uwezo kwa nini sasa tumekwenda kuweka bei ya shilingi 320,000; shilingi 500,000 au shilingi 600,000 bila kuangalia hawa maskini ya Mungu, watu wanaishi mjini wanasaidiwa na watu wa vijijini. Kwa maana hiyo lazima hizi bei za umeme kwa sehemu za mijini bado tuziangalie, hii shilingi 320,000 ni kubwa mno, maskini ni wengi pale, tuna umaskini mkubwa katika nchi hii hata kama watu wanaishi mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba bei hii ya shilingi 320,000 ni kubwa sana, hata kama hawatalipa shilingi 27,000 lakini iangaliwe ilipwe ya nafuu ameshauri hapa Mbunge wa Manonga kwamba wao walikuwa wanalipa shilingi 170,000, hiyo kidogo ni affordable, lakini huwezi ukalipa 320,000 hata kazi huna na wewe unataka umeme, unataka kuuza ice-cream, unataka kuuza biashara ndogondogo, lakini hamna. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba aliangalie hili ili tupate bei nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia pale ambapo mwananchi ameshalipa kuunganishia umeme, kunakuwa na muda mrefu anafuatilia muda mrefu, tunaomba Waziri aje na commitment hapa baada ya kulipa atachukua muda gani kuunganishiwa umeme kwa sababu watu wanachukua mpaka miezi miwili, mitatu, tayari wameshalipa lakini hawapati umeme. Kwa hiyo, Waziri atuambie muda halisi hasa baada ya kulipa ni shilingi ngapi na baada ya hapo nini kitafuata kama mwananchi hakupata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri hapa sikuona sehemu ambayo kutakuwa na ukarabati wa mabwawa kama vile Hale, Kidatu, Nyumba ya Mungu, Rusumo ambayo haya ni mabwawa yetu ambayo sasa hivi yanatuzalishia umeme, hakuna ukarabati, kwa maana hiyo anapokuja ku-windup atueleze kwamba haya mabwawa ambayo sasa hivi ndiyo tunafaidi keki yake, kuna mpango gani wa kuyaendeleza kwa sababu sasa hivi unapokwenda pale ukiangalia ile mitambo imechakaa. Kwa nini tusiipangie mipango ili ikawa nayo ni mazuri iendelee kutupa umeme wa uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye suala la mafuta; kwa kweli suala la mafuta napongeza bei ambazo zimetangazwa kwa sababu zimekuja kuleta unafuu mkubwa kwa Mtanzania. Kwa mfano, Dar es Salaam imepata ruzuku ya kila lita ya petrol Sh.306 lakini diesel Sh.320. Hii ni nafuu kubwa Mheshimiwa Rais anapaswa kupongezwa, lakini pia Wizara imefanya kazi nzuri, tunategemea kwamba huu mpango utakuwa ni endelevu na wananchi wapate nafuu waweze kufaidika na hii hali nzuri ya mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nataka kuzungumzia hii TPDC. Hii TPDC ina mchango mkubwa kwa Taifa, tuliiunda wenyewe na kwa ajili ya kufanya biashara ya mafuta, lakini cha kushangaza mtaji wake wote umemegwa na TANESCO na sababu ni nini? TANESCO wanauziwa umeme kwa kutumia gesi, lakini hawalipi, sasa leo unakuja kutuambia unaanzisha vituo vya TANOIL, yaani unaandaa nguo za mtoto lakini mama unampiga viboko atazaaje huyu mama… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. MOHAMED SAID ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)