Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Dr. Florence George Samizi (10 total)

MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Hayati Dkt. John Magufuli, Makamu wa Rais wa sasa na Waziri Mkuu ya kujenga Kituo cha Afya Kata ya Murungu katika Wilaya ya Kibondo ili kusogeza huduma na kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kibondo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi Mbunge wa Jimbo la Muhambwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kujenga na kukarabati Vituo vya Kutolea huduma za Afya kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuboresha utoaji wa Huduma za Afya ya Msingi kwa wananchi ikiwemo upatikanaji wa huduma za upasuaji. Ujenzi na ukarabati wa huo unahusisha pia utekelezaji wa ahadi za Viongozi Wakuu wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, Katika kutekeleza mkakati huu, Serikali imepeleka fedha shilingi bilioni 25.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Vituo vya Afya kwenye Tarafa 90 zisizo na Vituo vya Afya ikiwemo Tarafa ya Kibondo Mjini inayoundwa na Kata tisa za Murungu, Bunyambo, Kibondo Mjini, Biturana, Kumwambu, Kitahana, Rusohoko, Misezero na Bitare ambapo kiasi cha shilingi milioni 250 kimepelekwa kwa jili ya ujenzi wa Kituo cha Afya kwenye Kata ya Bunyambo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na utekelezaji wa mkakati huu, Serikali, itaendelea kutoa fedha kwenye halmashauri kwa ajili ya utekelezaji wa ahadi zote za Viongozi.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamalizia ujenzi wa soko la ujirani mwema katika Kijiji cha Mukarazi ikiwemo miundombinu na ujenzi wa Kituo cha Forodha cha Pamoja katika Jimbo la Muhambwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Folrence George Samizi, Mbunge wa Jimbo la Muhambwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Soko la Mukarazi ulianza kutekelezwa Juni, 2018 na kukamilika Oktoba, 2020. Ujenzi wa Soko hilo umegharimu kiasi cha shilingi milioni 442.61 na kwa sasa soko limekamilika kwa asilimia 100 na linatumika mara mbili kwa wiki.

Mheshimiwa Spika, ili kufanya soko hilo kutumika kikamilifu Halmashauri imetoa kiasi cha Shilingi milioni 5.6 kwa ajili ya kupima viwanja 145 katika eneo la soko kwa ajili ya matumizi mbalimbali ikiwemo biashara, huduma za polisi na forodha. Ahsante.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza: -

Je, ni lini Ofisi ya TRA itajengwa katika Halmashauri ya Kibondo ili kuzuia biashara holela katika masoko ya ujirani mwema kati ya Tanzania na Burundi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Muhambwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, TRA ilifanya utafiti katika maeneo yote nchini yenye uhitaji wa ofisi za kudumu za usimamizi wa kodi ikiwemo Halmashauri ya Kibondo na kubaini kuwa gharama za usimamizi wa kodi katika Wilaya ya Kibondo zitakuwa kubwa ikilinganishwa na kiwango cha kodi kinachotarajiwa kukusanywa. Kwa muktadha huo, TRA itaendelea kufuatilia kwa karibu mwenendo wa ukuaji wa shughuli za kiuchumi na ukusanyaji wa kodi katika wilaya hiyo ili mara tu itakapokidhi vigezo, TRA itafungua ofisi za kudumu. Aidha, TRA itaendelea kuimarisha mfumo wa sasa wa kuhudumia walipakodi wa Wilaya ya Kibondo ili kuwawezesha kulipa kodi bila usumbufu wowote. Ahsante.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga minara ya simu na TBC Redio katika Jimbo la Muhambwe?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Muhambwe, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Kuhusu Ujenzi wa Minara ya simu, Serikali itajenga minara ya mawasiliano katika Kata za Bunyambo, Murungu na Nyaruyoba ambazo zimebainika kuwa na changamoto ya upatikanaji wa huduma za mawasiliano katika Jimbo la Muhambwe. Zabuni ya minara hiyo itatangazwa kabla ya mwaka wa fedha wa 2021/2022 kukamilika.

(b) Kuhusu TBC Redio, mtambo wa masafa ya FM katika Jimbo la Muhambwe, Mwezi Machi, 2022 mtambo huo ulipigwa na radi iliyoharibu vipuri vyake. Vipuri hivyo vimeshaagizwa na tayari vimeshawasili nchini. Kazi ya kufunga vipuri hivyo itakapokamilika, na kuwashwa na kufanyiwa majaribio ya kiufundi kabla ya tarehe 30 Mei 2022 hivyo kurejesha usikivu wa TBC katika Jimbo la Muhambwe na maeneo ya jirani. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Daraja la Mto Lumpungu katika Jimbo la Muhambwe?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Muhambwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mto Lumpungu unatenganisha nchi ya Burundi na Tanzania katika Wilaya ya Kibondo Mkoa wa Kigoma kwenye Kijiji cha Kibuye, Kata ya Kumsenga. Kwa kuwa ujenzi wa daraja hili utahusisha nchi mbili Burundi na Tanzania, Serikali itaanzisha mazungumzo na nchi ya Burundi ili ziweze kukubaliana kuhusu ujenzi wa daraja hili, ahsante.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza: -

Je, ni lini Wakulima wa Tumbaku watalipwa fedha zao kutoka Kampuni ya JESPAN ya msimu wa mauzo 2021 Jimboni Muhambwe?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi Mbunge wa Muhambwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika msimu wa mwaka 2020/2021, kampuni ya JESPAN Company Limited ilinunua jumla ya kilo 512,426 za tumbaku zenye thamani ya Dola za Marekani 662,651. Kampuni hiyo iliweza kulipa wakulima wa Kibondo, Kakonko na Kasulu kiasi cha Dola za Marekani 471,500 na kubaki deni la kiasi cha Dola za Marekani 191,151.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ucheleweshwaji wa malipo, Serikali imeanza kuchukua hatua za kisheria kwa kampuni zilizonunua tumbaku kwa wakulima na kushindwa kufanya malipo. Hivyo basi, malipo ya wakulima yatafanywa kwa mujibu wa maamuzi ya vyombo vya haki ikiwemo Mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni hiyo iliyoshindwa kulipa wakulima baada ya soko la kuuza tumbaku iliyonunua kuyumba na kutouza kutokana na athari za UVIKO – 19. Aidha, Wizara kupitia Bodi ya Tumbaku na Chama Kikuu cha Wakulima wa Tumbaku Mkoa wa Kigoma (KTCU) na Ofisi ya Mashtaka ya Mkoa wa Kigoma inakamilisha taarifa za kuifungulia kesi ya madai kampuni ya JESPAN Company Limited ili kukamilisha malipo ya wakulima.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati kwenye Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Kibondo pamoja na nyumba za Askari Polisi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Muhambwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Kibondo pamoja na nyumba za makazi ya Maofisa na Askari ni chakavu. Tathmini ya uchakavu kwa ajili ya kufanya ukarabati imefanyika na kiasi cha Sh.28,914,250/= kinahitajika kwa ajili ya kukarabati Kituo cha Polisi na Sh.109,288,000/= zinahitajika kwa ajili ya ukarabati wa nyumba nane za makazi ya Maofisa na Askari Polisi. Kulingana na hali ya upatikanaji wa fedha, Serikali imepanga kutekeleza ukarabati huo katika mwaka wa fedha 2024/2025, nakushukuru.
MHE.SYLIVIA F. SIGULA K.n.y. MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kumalizia ujenzi wa Kituo cha Afya Kata ya Kizazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Jimbo la Muhambwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika mwaka wa fedha wa 2023/2024, Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Kata ya Kizazi.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA K.n.y. MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa Vitambulisho vya NIDA kwa wananchi wa Mkoa wa Kigoma hususan Jimbo la Muhambwe?

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Muhambwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imesajili jumla ya wananchi 975,844 katika Mkoa wa Kigoma wakiwemo wananchi wa Jimbo la Muhambwe na jumla ya vitambulisho 123,962 vimezalishwa kwa ajili ya wananchi wa mkoa huo. Katika Jimbo la Muhambwe ambalo liko katika Wilaya ya Kibondo, wananchi 139,588 walitambuliwa na vitambulisho 5,126 vilitolewa na kugaiwa kwa wananchi. Serikali inatarajia kukamilisha utoaji wa vitambulisho kwa wananchi wote wenye sifa katika mwaka wa fedha 2022/2023. Nashukuru.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza: -

Je, lini Serikali itakarabati Kituo cha Afya cha Kifura – Muhambwe?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Jimbo la Muhambwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Kifura kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo ni moja ya vituo vya afya 199 chakavu ambavyo Ofisi ya Rais TAMISEMI imeviainisha. Serikali inaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ukarabati na kuongeza majengo kwenye vituo vya afya chakavu vyote nchini kikiwemo Kituo hiki cha Afya cha Kifura, ahsante.