Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Florence George Samizi (14 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia bajeti ya wizara hii muhimu sana ya Nishati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ikiwa ni mara ya kwanza kusimama kuongea katika Bunge hili lako Tukufu, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu aliyenipa neema na kibali cha kuwa Mbunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nikishukuru Chama changu Cha Mapinduzi kikiongozwa na Mwenyekiti wetu wa Chama mama yetu mama Samia Suluhu Hassan ambaye pia ni rahisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na kuniteua kuweza kupeperusha Bendera ya Chama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee niwashukuru wananchi wa Jimbo la Mhambwe ambao wamenipa ridhaa kwa kunipatia kura za kutosha ili niweze kuwatumikia, ninawaahidi wananchi wa Mhambwe kwamba sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niishukuru familia yangu kipekee mume wangu mpenZi Sadoki Mgendi, Watoto wangu Naomi, George, Georgette na Noah kwa uvumilivu, lakini na ushirikiano wao walionipa kipindi chote cha harakati hizi, Mwenyezi Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda niwashukuru Wabunge wenzangu wa Chama Cha Mapinduzi, wakiongozwa na Wabunge wa Mkoa wa Kigoma kwa mchango wao wa hali na mali ulioniwezesha kuweza kufanikisha safari hii. Napenda niwashukuru ndugu jamaa na marafiki wote ambao walikuwa na mimi katika safari hii nzima, Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niungane na wenzangu waliokwisha kuongea kuendelea kumpongeza Waziri wa Nishati na Madini Mheshimiwa Dkt. Medard Kalemani, Naibu Waziri Stephen Byabato, lakini na Katibu Mkuu Mheshimiwa Leonard Masanja na viongozi wote wa Wizara hii, lakini na viongozi na wafanyakazi wote wa TANESCO kwa kazi kubwa, lakini kwa ripoti nzuri ambayo kwa ukweli imetujibu mambo mengi ambayo tulikuwa tukiyafikiria, mmetoa ripoti nzuri, mmefanya vizuri hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaanza kwa kuipongeza Serikali kwa jitihada kubwa sana inayofanya ya kutuunganishia umeme wananchi wake, umeme wa uhakika, lakini umeme wa bei rahisi, hii inajidhihirisha kwa miradi mbalimbali ambayo Waziri wetu wamewakilisha, lakini pia kwa miradi ile inayoendelea ule ukanda wangu wa Jimbo la Muhambwe ikiwemo ujenzi wa kituo cha kufua umeme katika maporomoko ya Rusumo megawatt 80.

Mheshimiwa Spika, lakini na ujenzi wa kituo cha kufua umeme katika Mto Malagarasi Megawatt 49.5. Hii ni dhahiri kwamba baada ya miradi hii kukamilika basi itatupunguzia mzigo wa kuendesha umeme kutumia generator ambayo ni gharama kubwa kutumia mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile itatusaidia tuweze kupata umeme wa uhakika, naipongeza sana Serikali kwa jitihada hizo tunaomba miradi hii isimamiwe vizuri ili iweze kuisha katika kipindi kilichopangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo bado pana changamoto hasa katika usambazaji wa umeme vijijini. Jimbo langu la Muhambwe lina vijiji 50, katika vijiji hivyo 50 umeme umeunganishwa katika vijiji 8 tu na uunganishaji huo ni ile tunaita katikati ya Kijiji tu. Haujafika kwenye nyumba nyingi za wananchi, lakini haujafika kwenye taasisi kama vile, shule, makanisa, misikiti na kadhalika, hospitalini na vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ilitokana na ucheleweshaji wa vifaa vya mkandarasi bandarini, ambavyo vifaa vile vilikaa zaidi ya miezi 12 vikidaiwa kodi. Nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali ambayo iliingilia kati na kutusaidia kuvitoa vile vifaa, vifaa hivyo vimetoka wiki iliyopita. (Makofi)

Mheshimiwa Spia, sasa basi, nimuombe Waziri wa Nishati kutokana na ucheleweshaji huu, naomba sasa Jimbo langu la Muhambwe lipewe kipaumbele. Maana vijiji ambavyo havijapata umeme ni vingi, ikiwemo Kigaga, Kichananga, Rukaya, Magalama, Kumkuyu, Kibuye, Kukinama, Nyakilenda, Malolegwa na kadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakuomba Mheshimiwa Waziri wa Nishati, kasi iongezeke, ili tuweze kusambaziwa umeme katika vijiji vyetu. Sambamba na hili, tunayo Kata ya Bitale, hii Kata iko takribani kilometa 2 kutoka Mji wa Kibondo kwa maana ni karibu sana. Lakini Kata hii bado imepata umeme katikati tu ya hiyo Kata, lakini vijiji vyake kama vile Kumuhama na Rubanga bado haijafikishiwa umeme.

Mheshimiwa Spika, naomba pia Kata hii ipewe kipaumbele, maana iko karibu mno kukosa umeme ni aibu kwa Jimbo langu la Muhambwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niishauri Serikali, kumekuwa na changamoto ya ucheleweshaji wa vifaa kufika eneo la utekelezaji kwa madai ya ucheleweshaji wa kodi au kwa ucheleweshaji wa kibali cha kusafirisha vifaa ambavyo vina uzito. Lakini naamini taasisi zote hizi ni za Serikali kwa maana kwamba, bandari, TANROADS zote ni mali ya Serikali na TANESCO ni Shirika la Serikali. Na TANESCO hii inatekeleza miradi ambayo ni mali ya Serikali, basi kuwepo na mazungumzo ndani ya taasisi hizi. Taasisi hizi ziweze kuongea kwa maana kwamba, ucheleweshaji huu usilete madhara kwa wananchi, wananchi wanahitaji kuona matokeo chanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo ikibidi basi kibali kitolewe cha kuruhusu vifaa hivi viweze kufika eneo la tukio huku kodi zikiendelea kulipwa. Hii itaharakisha mradi kutekelezeka, lakini pia, itatupunguzia gharama za kutekeleza mradi. Lakini pia, itatusaidia kwamba mradi uishe kwa wakati uliopangwa, ili Serikali iweze kulipa gharama ambazo ni sahihi kwa mlaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kusema hayo, naomba kuunga hoja mkono. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti hii ya kimkakati iliyowasilishwa mbele yetu. Kwanza kabisa nianze kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango kwa kazi nzuri na bajeti nzuri, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, nimpongeze Naibu wake Mheshimiwa Eng. Masauni, Katibu Mkuu wa Wizara Ndugu Emmanuel Tutuba na watumishi wote wa Wizara kwa kutuwasilishia bajeti nzuri ambayo kwa kweli ni bajeti ya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kumpongeza Mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye ametuletea bajeti ambayo inaonesha matumaini makubwa maana aimejielekeza katika huduma za jamii ambazo zinagusa maisha ya wananchi moja kwa moja. Ni bajeti nzuri ambayo kwa kweli, imeleta matumaini, wana-Muhambwe wameleta shukrani nyingi sana na mimi naziwakilisha kwa heshima na unyenyekevu mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini bado kuna maeneo ambayo naona yanaweza yakafanyiwa kazi zaidi ili tuweze kuongeza kipato maana ni ukweli usiopingika tunahitaji kodi kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. Nitachangia upande wa maliasili na utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo lango la Muhambwe linayo hofadhi ya Moyowosi, hifadhi hii ni hifadhi kubwa sana ambayo ina wanyama wote wakubwa watano, lakini pia ina wanyama ambao wanapotea kama vile statunga, lakini pia kuna ndege ambao ni adimu kama vile shubiri. Hifadhi hii inafanya utalii wa uwindaji tu, tunavyo vitalu sita, tumekodisha vitalu vinne, lakini viwili bado havijakodishwa. Hifadhi hii ina ardhi oevu, lakini pia ni ardhi yenye majimaji inachangia pato la Taifa sana kama tunavyojua maliasili inachangia takribani asilimia 17 ya pato la Taifa, lakini inachangia asilimia 25 ya pesa za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hifadhi hii haijatumika inavyotakiwa kwa sababu ya miundombinu. Kama nilivyosema hifadhi hii ina maji, barabara hazipitiki kabisa, hakuna vyombo vya usafiri katika hifadhi hii, hii inachangia kwamba, vile vitalu vingine visiweze kupata, lakini watu wasipende kwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali zile hifadhi zinazofanya vizuri ina maana kuna nguvu iliwekwa ndio zikafanya vizuri, ili ukamue maziwa vizuri kwa ng’ombe lazima huyu ng’ombe umtunze. Naomba Serikali iangalie vizuri Hifadhi ya Moyowosi, bado ina vivutio vikubwa ituwezeshe kutuletea magari, ilituahidi kutuletea trekta na boti, ituletee ili na sisi pato likipanda katika halmashauri automatically wananchi mmoja-mmoja watafaidika maana watapata ajira mahali pale, pato litaongezeka, lakini na nchi itafaidika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sio hivyo tu hifadhi il eina mito mingi ambayo ina samaki bado inaweza ikatumika kwa kufanya uvuvi wa hapohapo, spot fishing, lakini pia tunaweza tukaweka utalii wa picha. Hii yote ni kujitahidi kuitumia hii hifadhi kwa kiasi kikubwa, ili tuweze kujiongezea pato. Tuilee hii hifadhi, mtusaidie tupate vyombo hivi vya usafiri, tuitangaze maana vitalu viwili kukaa bila wawekezaji hii ni hasara kwa halmashauri yetu ya Kibondo, lakini pia kwa nchi nzima; tunaomba tuitangaze Wizara itenge bajeti kabisa rasmi kwa ajili ya kutangaza hivi vivutio ili tuweze kuongeza kipato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naishukuru Serikali kwa sababu, inaendelea kuonesha jinsi gani inawekeza katika kupanua biashara za ujirani mwema. Jimbo langu la Muhambwe limebahatika tuna ujirani mwema na Burundi. Tunaishukuru Serikali ilitujengea soko katika Kata ya Mkarazi hii ni kati ya Mabamba na Gisulu, Burundi, lakini bado hili soko halijatumika ipasavyo ndio yani kama kila siku kama linaanza, kwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna vitu muhimu. Hatuna TRA pale, hakuna polisi, hakuna mambo ya ndani, ina maana Warundi pia wanaona hofu kuja kufanya pale biashara. Soko hili likiwezeshwa tukaweka One Stop Centre pale ina maana biashara pale zitafanyika tutajiongezea pato la Taifa, wananchi watafanya biashara zao pale, mazao yetu yataenda pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kabisa Jimbo langu la Muhambwe tunalima sana mihogo na wanunuzi wakubwa ni Warundi. Kwa hiyo, tukiweka soko zuri pale tukaliboresha hili soko la Mkarazi ambalo Serikali imeshaweka pesa, lakini haikuwekwa kwa utimilifu kwa sababu, haikukamilisha kuweka mambo muhimu ili biashara iweze kufanyika. Basi tunaamini ikifanya vizuri katika lile soko basi tutakuwa na biashara nzuri ya ujirani mwema na hivyo, kipato kitaongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuboresha barabara maana mazao ili yaweze kufika pale Mkarazi lazima barabara ziwe nzuri. Barabara zile hazipitiki kabisa wakati wa mvua kwa hiyo, mazao yanaharibika shambani. Tuinaiomba Serikali itusaidie kwa sababu, halmashauri ikiongeza mapato basi pato la Taifa moja kwa moja litaongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee pia kuishukuru Serikali kwa jinsi inavyoona kuboresha miundombinu ya shule kwa ajili ya vijana hasa kwa kuongeza bajati kwenye vyuo vya ufundi stadi. Zipo VETA nchini, lakini kuna sehemu nyingine hatuna VETA ila tumebahatika kuwa na vyuo vya wananchi ambavyo vilianza miaka mingi sana, kama Jimbo langu la Muhambwe chuo kimeanza mwaka 1975 kwa hiyo, kwa picha ya kawaida unaweza ukaona hiki chuo kiko katika hali gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaishukuru Serikali ilituletea pesa milioni 500, tulifanya ukarabati kwa kiasi. Ili tuwasaidie vijana wa Jimbo la Muhambwe tunaomba chuo hiki kiangaliwe vizuri kwanza wakati tukijipanga kwenda kwenye VETA. Tuongezewe pesa ili tukiboreshe zaidi, tuongeze mabweni, tuongeze madarasa, tuongeze vifaa, ili vijana nao wa Muhambwe waweze kupata ujuzi mdogomdogo ili waweze kujiajiri kwa ajili ya kufanya biashara, ili tuweze kuongeza kipato kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaipongeza Serikali kwa tozo hizi ilizoleta tozo ya line za simu, tozo za miamala, tozo mbalimbali ambazo hizi zitatusaidia kupata kipato, tutaendelea kupata kipato kwa watu wengi kidogo kidogo kipato ambacho ni kodi ambayo si ya moja kwa moja kwa hiyo hii haimuumizi sana mwananchi, ombi langu kwa Serikali fedha hizi zikipatikana basi siende kule tulipozielekeza, hasa kwenye TARURA maana sisi wa vijijini hasa tunalilia kwanza barabara zipitike, barabara hazipitiki kabisa, vijiji haviunganishwi kama vijiji haviunganishwi Pato la Taifa litaongezeka vipi wakati watu hawawezi kuingiliana barabara ya kwenda kijiji kingine hakuna! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha kusikitisha bajeti ya sisi tunaotoka tunaitwa pembezoni kama Jimbo langu la Muhambwe bajeti ya TARURA inapingua kila mwaka tulianza na one billion 2017/2018, lakini 2021/2022 Milioni 800, nilidhani kwa kuwa ni pembezoni basi tutaongezewa ili na sisi tuwasiliane japo vijiji, lakini inaendelea kupungua kwa hiyo naishauri Serikali sisi wa pembezoni pia tuna uwezo wa kuchangia pato la Taifa kama mta- invest kwenye Wilaya zetu ili tuweze kufanya vizuri, tusitolee macho tu kule kulikofanya vizuri tuanzishe na huku ambako kunaweza kukafanya vizuri zaidi, japo ni pembezoni lakini bado kuna fursa nyingi ambazo hatujazitumia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kuipongeza Serikali kwa miradi ya maji ambayo tumeona kabisa fedha hizi tutakwenda kuzipata na zitaisaidia miradi ya maji. Ushauri wangu kwa Serikali miradi ya maji jamani ni mingi hata jimboni kwangu ipo lakini Jimbo la Muhambwe ni Jimbo ambalo Kibondo Mjini nikikuonyesha maji yake ni aibu ni tope, japo ukiuliza unaambiwa kuna mradi wa kwanza wa pili na wa tatu, miradi ya maji ambayo haizai matunda sielewi utafiti haufanyiki tunapoanzisha mradi, sielewi usimamizi haufai sijui vizuri naona wataalam wa maji watusaidie kwa nini tuna miradi lakini hii miradi tunaisoma kwenye makaratasi haitoi maji? kama Kata yangu ya Kibondo Mjini ni tatizo maji hakuna na yanayotoka ni tope. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, basi tunaishauri Serikali fedha hizi ambazo tutawakata walipa kodi kwenye lane zao za simu kwenye miamala zitumike inavyostahili miradi waione hii itawafanya wananchi waendelee kuwa na moyo na ari ya kutoa na hizi kodi hazitawaumiza.

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kuipongeza Serikali pia kwa posho ya Madiwani, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi nami niweze kuchangia hoja tulizokuwanazo mbele yetu. Nianze kwa kuunga mkono hoja zote mbili za Kamati ya Ardhi na Kamati ya Viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Rais wetu, mama yetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ameonesha kwa vitendo kwa kufanya The Royal Tour ambayo imeenda kuimarisha utalii katika nchi yetu. Takwimu zinaonesha kwamba watalii wameongezeka katika nchi yetu ambapo mwaka 2020/2021 tulikuwa na watalii 922,692 lakini mwaka 2022 tumekuwa na watalii 1,454,000. Hii ni takribani ongezeko la asilimia 57.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utalii wa ndani uliongezeka kwa asilimia 199.5 pale ambapo mwaka 2020/2021 tulikuwa na watalii 788,000 lakini mwaka 2022 tulikuwa na watalii wa ndani 2,363,000. Hii inatuambia nini sasa? Hii inatuambia kwamba, Serikali inapaswa kujipanga kuendelea kuwapokea hao wageni kwa sababu Mheshimiwa Rais ameshaonesha njia kwa kufanya The Royal Tour ili kuongeza utalii katika nchi yetu. Ndiyo maana tumeona watalii wameongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali inapaswa kuendeleza hizi jitihada kwa kuweka mikakati madhubuti ambayo itasababisha utalii uzidi kuendelea mbele. Iko mikakati ambayo Serikali inaweza kuendelea kuifanya ikiwemo kuimarisha na kuboresha mazingira ya watalii. Ukiangalia taarifa ya CAG inatuambia kwamba yapo maeneo makubwa ambayo Serikali inaweza kuyafanyia kazi, ikiwemo kuboresha hoteli na lodge katika nchi yetu, kwa sababu imeonekana kuna changamoto ya watalii kupata malazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili, ni kuongeza vivutio vya utalii. Kwa hiyo, Serikali inapaswa iyafanyie kazi hayo mambo mawili ili kuhakikisha kwamba mapato na utalii unakua katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza kwenye hoteli na lodge zilizokuwepo ambazo zilikuwa zinasimamiwa na Serikali. Ikumbukwe kwamba mwaka 1992 Serikali ilibinafsisha hizi hoteli kwa Sheria ya Mashirika ya Umma ya Mwaka 1969. Hapo Serikali ilikuwa na hoteli na lodge 23. Hizi hoteli 23, 17 zilikuwa zinasimamiwa na Shirika la Taifa na hoteli 6 zilikuwa zinasimamiwa na Shirika la Reli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilikuwa na lengo zuri kwamba sasa wawekezaji waweze kuja nchini kwetu wawekeze lakini tushirikiane katika kumiliki na uendelezaji. Hili halikutokea kwa sababu hapo mwanzo wakati hoteli hizi zinaandaliwa zilikuwa zinaendeshwa kwa hasara, na pia zilikuwa na madeni mengi. Lengo lilikuwa zuri lakini tija hiyo haijaweza kufikiwa kwa sababu mwaka 2022 mwezi wa Tano Serikali iliunda Tume Maalum ambayo ilikwenda kuzifanyia tathmini hizi hoteli. Ilionekana katika hizo hoteli 23, ni hoteli 10 ambazo zinafanya kazi. Katika hizo hoteli 10 zinazofanya kazi, hoteli nne ndiyo zimefanyiwa ukarabati ambao ni sahihi, lakini hoteli sita zimefanyiwa ukarabati ambao hauridhishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoteli sita hazifanyi kazi, kwa hiyo, hata taarifa zake za kujua uwekezaji wake ukoje, hazikuweza kupatikana. Hoteli nyingine sita hazijaweza kufanya kazi kabisa. Hii ikiwemo na Hoteli ya Embassy ambayo ipo Mjini kabisa Dar es Salaam. Hoteli ya Musoma, imeungua, ni pori, ni kichaka cha kulala popo. Hoteli ya Mbeya haifanyi kazi na nyingine nyingi katika hizi sita ambazo hazijafanya kazi na ni magofu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo hoteli nyingine ya Moshi Hotel ambapo hii mwekezaji alikopa na baada ya kushindwa kulipa, TID imeuza hoteli. Kwa hali tuliyokuwanayo nchini ya hili ongezeko la watalii linalojitokeza, lazima Serikali ije na mkakati madhubuti wa kuhakikisha kwamba hizi hoteli sasa zinaweza kufanya kazi. Ifanyaje sasa? Maana kwa hali ya kawaida, hata sisi wananchi tukinunua viwanja kama hujakiendeleza kwa muda Fulani, unapaswa kunyang’anywa, lakini Sheria yetu ya Mashirika ya Umma haina ukomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali ianze mchakato wa kuangalia sheria. Sheria ya Uwekezaji iwe na ukomo ili pale ambapo mtu ameshindwa kuendeleza, basi sheria iweze kuchukua mkondo wake. Hizi hoteli ambazo hazijafanyiwa ukarabati tangu mwaka 1992 mpaka leo hazijafanyiwa ukarabati, ukarabati sijui ni wa miaka mingapi, Serikali irejee upya mikataba kuhakikisha kwamba hizi hoteli zinarudi, zifanyiwe ukarabati, tutafute wawekezaji wenye uwezo. Kwa sababu wawekezaji ambao wamechukua hizo hoteli wamekaa nazo miaka yote hii ni dhahiri kwamba hawataweza kutatua hii shida ya malazi tuliyokuwanayo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipo kipengele kingine ambacho naomba Serikali ikiangalie pia kwa jicho la pili. Tume yetu imeshauri kwamba hizi hoteli zirudishwe kwa Shirika la Reli ambalo lililokuwa linamiliki hapo awali. Kwa mfano, Hoteli ya Musoma na Hoteli ya Mbeya wamekubaliana na sasa zimerudishwa Serikalini kwenye shirika hili. Hata hivyo Shirika letu la Reli bado lina majukumu makubwa ya kuboresha miundombinu yetu ya reli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba kwa kuwa Wizara ya Maliasili ni Wizara ambayo kwa sasa ina uhitaji mkubwa wa hizi hoteli; kwa hiyo, nina hakika wakipewa jukumu hili kuzisimamia wao, basi watazipa kipaumbele cha kuzitengeneza ili watalii wetu waweze kupata sehemu ya kulala. Kwa hiyo, Serikali iwarudishie Wizara ya Maliasili ili waweze kutafuta wawekezaji wenye uwezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo eneo jingine ambalo Wizara yetu inaweza kuboresha zaidi ambalo nimesema ni kuongeza vivutio. Tunazo hifadhi zetu ambazo zinafanya matumizi machache. Kwa mfano, nitatoa mfano wa Hifadhi yangu ya Muyoozi ambayo ni hifadhi ya uwindaji. Hifadhi hii ina wanyama wote wakubwa watano lakini pia ina wanyama ambao wanaenda kupotea kama vile statunga ambayo ni jamii ya swala lakini na ndege shubil ambao hawapo maeneo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Wizara ichukue umahususi wake kabisa kuanzisha utalii mwingine ikiwemo utalii wa picha kwenye hifadhi ile ili kuongeza kipato. Kuna utalii wa kuvua ambao unaweza ukafanyika ili kuongeza kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tofauti ya utalii wa uwindaji na utalii huu wa picha na wa uvuvi, huu unaruhusu jamii kupata faida ya moja kwa moja. Utalii wa uwindaji tuna faidika na CSR, sawa tunashukuru lakini hatupati faida ya moja kwa moja kwa sababu muwekezaji anakuja moja kwa moja hifadhini anawinda anaondoka. Tukipata utalii huu wa picha basi tunaamini watalii watafika katika jimbo letu katika ile Kata ya Busagara, Kijiji cha Kifura, wananchi pale watafaidika kwa sababu watakunywa maji, atanunua hiki basi watakiongezea kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana wetu wa maeneo ya pale basi watawasaidia hawa watalii kuhakikisha kwamba wanaweza kufika kule mbugani kwa hiyo tutaweza kupata mapato zaidi. Pia upo utalii wa fukwe ambao bado hatujafanya vizuri. Tukifanya vizuri kwenye utalii wa fukwe basi tutaongeza vivutio na ni dhahiri kwamba watalii wanapenda utalii wa fukwe ndiyo maana tunaona watalii wanapenda kwenda Zanzibar kwenye utalii wa fukwe kuliko huku kwetu. Basi tufanye, Wizara tunaiomba Serikali ijielekeze kwenye utalii wa fukwe ili tuweze kuongeza vivutio ambavyo vitatusaidia kuongeza pia mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna utalii wa malikale, malikale ziko maeneo mengi sana ambapo bado hazijafanyiwa kazi vizuri. Zikifanyiwa kazi vizuri hizi malikale basi zitaisaidia Serikali kuongeza mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema naishukuru sana Serikali kwa jinsi ambavyo inaendelea kufanya kazi vizuri katika Wizara yetu ya Maliasili, nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Wizara nzima kwa jinsi ambavyo wanaendelea kufanya kazi vizuri kuhakikisha kwamba Serikali inaendelea kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee tunaendelea kuomba Serikali iongezewe bajeti. Tumesema TANAPA ilikuwa na hifadhi 16, lakini sasa imeongezewa hifadhi sita nyingine lakini bajeti yake ni ile ile. Ni ukweli usiopingika kwamba huduma haziwezi kuwa vile vile na kama huduma siyo nzuri basi tunawapoteza watalii wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Afya. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa jinsi ambavyo amejipambanua kuendelea kuboresha huduma za afya. Wenzangu wameshasema, tumeona jinsi ambavyo amekwenda kuboresha huduma za afya kwa kuongeza vituo vya kutolea afya. Tumepata hospitali nyingi, tumepata vituo vya afya, zote hizi ni jitihada za Mheshimiwa Rais kuhakikisha kwamba afya za Watanzania zinakwenda kuimarika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata sisi kule Muhambwe tumepata vituo vya afya viwili ambavyo vimeshakwisha kabisa katika Kata ya Kibondo Mjini na Kata ya Kunyambo na sasa hivi tunaendelea na ujenzi wa Kituo cha Afya katika Kata ya Rugongwe, ili kuendelea kuboresha afya za wananchi wa Muhambwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Afya na Naibu Waziri kwa jinsi ambavyo wanafanya kazi. Wamejituma na wamejipambanua kuhakikisha kwamba, wanafikisha huduma na hasa huduma bora ambazo ndio wananchi wanazitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri amekuwa akisema kila siku kwamba, si bora huduma, hapana, anachotaka ni huduma bora. Tunampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kujua kwamba, wananchi sasa wanahitaji huduma bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali kwa jinsi ambavyo imepeleka vifaa kila mahali. Wenzangu wameshasema, sasa ni jukumu letu sisi kuendelea kuvisimamia vile vifaa kule ambako tumeletewa ili viweze kutoa huduma inayostahiki kwa kuvitunza, ili viweze kutoa huduma hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepitia lengo la Wizara na nikaona katika vipaumbele vyao wameweka kuimarisha huduma za afya ya mama na mtoto ya uzazi na mimi nitajielekeza hapo. Nimeona pia kwenye takwimu vifo vya mama na mtoto vimepungua kwa asilimia nne, niwapongeze sana Wizara kwa jitihada hizi za kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa sababu, wote tunafahamu kwamba, afya ya jamii yoyote inapimwa kwa kupunguza vifo vya mama na mtoto. Kama kuna vifo vingi vya mama na mtoto, basi jamii hiyo haina afya iliyo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee bado tuna mikoa ambayo haifanyi vizuri sana, ukiwemo Mkoa wangu wa Kigoma. Tumeona hapa kuna vifo 900. Katika hivi vifo 982 Mkoa wangu wa Kigoma una vifo 102, accumulative ni vifo vingi japo hatujazidi kwingine, lakini kwa vifo hivi bado akinamama wanakufa katika Mkoa wa Kigoma. Wilaya yangu ya Kibondo tumepata vifo 12 kwa mwaka huo 2023 kwa hiyo, ina maana tuna kifo cha mama mmoja kila mwezi. Bado hali hii haikubaliki kwa wananchi wa Muhambwe, bado tunahitaji jicho la pekee. Mheshimiwa Waziri Ummy anaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Mkoa wa Kigoma tumejipambanua na tumekuja na Kauli Mbiu inasema Kigoma Safi ya Kijani Bila Vifo vya Mama na Mtoto Inawezekana. Sisi peke yetu hatutaweza, tunamwomba Mheshimiwa Waziri, atuangalie kwa jicho la pekee hasa kwa watumishi. Tunafahamu ziko changamoto nyingi zinazosababisha haya, Mheshimiwa Rais ameshaleta vifaa, ameleta majengo, sasa watumishi bado ni tatizo. Tuna uhaba, upungufu wa watumishi kwa asilimia sabini na kitu, ni ukweli usiopingika kwamba, hawawezi kukabiliana na vizazi hivi ambavyo viko vingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa watu 12 wamekufa katika vizazi hai 17 elfu kwa hiyo, unaweza ukaona ile burden tuliyonayo. Tuna burden ya wazazi wanaojifungua wengi kwa hiyo, tunaomba Mkoa wa Kigoma kipekee tupewe kipaumbele hasa kwa hawa watumishi ambao wanategemea kuajiriwa, ili waje kutia nguvu katika haya mapambano ambayo kipekee sisi wenyewe tumeyaanza. Nichukue nafasi hii kumpongeza RMO Jesca, kwa kweli ni mwanamama anajituma anafanya kazi. Tunaamini kabisa wakituwezesha watumishi basi, tutatoka huko tuliko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopinga kwamba, bado tumeona kwenye taarifa ya Wizara ukurasa wa 66 wameonesha ni jinsi gani halmashauri na zahanati, kliniki zina burden kubwa ya wagonjwa wa OPD. Amesema wameongezeka kutoka asilimia 16 hadi 22 na tukiangalia katika lile jedwali hospitali za rufaa zinachangia asilimia 5.5 ya wagonjwa wa nje, tunaita OPD. Hospitali za rufaa asilimia 6.6, lakini hospitali za halmashauri asilimia 22.8 na zahanati zinachangia asilimia 39, hii ina maana gani sasa?

Mheshimiwa Naibu Spika, bado tunahitaji kuelekeza huduma nyingi sana kule kwenye Halmashauri zetu kwa sababu, ndiko ambako wale wagonjwa wataweza kupatikana na wakipata huduma nzuri, basi tutapunguza hata wale wagonjwa wa kuwapeleka kwenye referral. Maana Dkt. Mzuri wa kwanza au nesi mzuri wa kwanza ni yule anayemwona mgonjwa mara ya kwanza na akaweza kutoa diagnosis iliyo sahihi na akaweza kutoa matibabu yaliyo sahihi. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri kwamba, halmashauri zetu, zahanati zetu na hivi vituo vya afya bado vinahitaji wahudumu wa afya na huduma bora kwa sababu ndiko wagonjwa wengi ambako wanaanzia.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inawezekana kwa sababu, nimpongeze kwa hii program ya Samia Tuvushe Salama, ina maana wataalam hawa 100 wafike kule kwenye zahanati zetu, wafike kule kwenye kliniki zetu, wakafanye hizo mentorship na coaching ili tuweze kupata ujuzi ulio bora na weledi kwa watumishi wetu wa afya ili waweze kutoa huduma bora kwa wananchi wetu kule kwenye halmashauri zetu na kwenye zahanati zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimemwona Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake ameeleza vizuri jinsi gani ya kuboresha maslahi ya watumishi wa afya, motisha itaenda kuchangia kuleta huduma bora kwa watumishi. Ni ukweli usiopingika kwamba, bado hakuna ulinganifu wa mishahara na motisha kwa watumishi wa afya kwenye hospitali za referral na hospitali za halmashauri. Kama tunaenda kupeleka watumishi kwenye halmashauri zetu na kwenye zahanati, lakini bado maslahi yao yako chini, basi tutashindwa kuwashikilia kule kwenye zahanati zetu kwa sababu, wote tumeshuhudia ajira zikitangazwa Muhimbili watu wanaomba kutoka kwenye halmashauri zetu wanakwenda Muhimbili. Ajira zikitangazwa huku kwenye hizi taasisi watumishi wanahama, wanahama kwa sababu Daktari Bingwa wa akinamama aliyepo kwenye Hospitali ya Kibondo na Daktari Bingwa yuleyule aliyeko kwenye Hospitali ya Muhimbili mishahara ni tofauti, motisha ni tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hatutaleta ulinganifu wa hizi motisha za watumishi wa afya kwenye hospitali za referral na hospitali zetu za halmashauri, tutawapeleka hawa watumishi kwenye zahanati zetu na hawatakaa maana kila mtumishi anatafuta green pastures. Kama anatafuta green pastures, hawezi kukaa kusubiri mwongozo ambao kwa kweli mwongozo huu umeongelewa miaka mingi. Tuliambiwa unapitiwa ulinganifu, zile zahanati na dispensary na hospitali za referral, ni miaka mingi. Tunaiomba Serikali, sasa ni muda muafaka, kwa sababu Serikali imeshawekeza kwenye zahanati na vituo vya afya, basi na maslahi ya watumishi wa halmashauri yaboreshwe ili yaweze kulingana na hospitali nyingine humu nchini. Imewezekana kwenye taasisi nyingi, kilimo walikuwa na shida hiyo, I mean mifugo walikuwa na shida hiyo, lakini waliweza kuweka ulinganifu na watumishi wameweza kukaa mahali pale, kwa hiyo, hili linawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuishukuru Serikali kwa haya magari ya ambulance yaliyoletwa. Tumeona Serikali inavyopambana kupunguza vifo vya mama na mtoto na kwenye Taarifa ya Mheshimiwa Waziri amejipambanua kabisa akinamama sasa wameongezeka kwenda hospitalini. Tumeona akinamama walioenda hospitali mara moja asilimia 96, walioenda mara nne asilimia 86, ambao wameenda chini ya mimba ya wiki 12 ndio wchache asilimia 36. Hii ina maana gani?

Mheshimiwa Naibu Spika, ina maana akinamama wengi wanakwenda hospitali. Sasa akinamama tunawa-miss wapi? Tunawa-miss sana pale kwenye huduma ya kwenda kujifungua. Tumeona jinsi M-Mama imeanza juzi na inafanya vizuri sana. Sasa nimwombe Mheshimiwa Waziri, hawa watumishi wa afya ya jamii ambao tumeamua kuwasomesha na kuwawezesha tuwaweke kwenye mitaa yetu, hawa ndio waweze kujua mzazi yuko wapi na ambulance inaenda saa ngapi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshuhudia ambulance zikikaa hospitali kusubiri referral. Kama tuna ambulance nne kila halmashauri, kwa nini zipaki hospitali zisiwahudumie hawa akinamama wajawazito ili waweze kuwahi hospitali? Kwa nini zipaki kusubiri mgonjwa mahututi na wakati mwingine hayupo? Ndio maana unakuta hizi ambulance saa nyingine zinafanya kazi ambazo hazikukusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri hawa watumishi wa ngazi ya jamii tuwatumie vizuri kwenye jamii zetu kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa maana kwamba, waweze kuwa na coordination, huyu mama anapata uchungu saa ngapi, anategemea kujifungua saa ngapi, gari la ambulance liko wapi, ili limuwahishe hospitali ili aweze kupata huduma za afya. Hapa tutakwenda kupunguza vifo vya mama na mtoto kwa sababu, ambulance tunazo, ambulance haibebi mgonjwa kila wakati, tukifanya coordination nzuri hii inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee nimpongeze Waziri kwa jinsi alivyoona kwamba, sasa alete huduma ya ujuzi wa uongozi. Ni ukweli usiopingika kwamba, tunakuwa Madaktari hospitali na Manesi, tunajiongoza wenyewe hakuna kiongozi hospitalini. Kwa hiyo, naamini kabisa hii kozi ambayo ameamua kuileta ya leadership…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Dkt. Florence. Kengele ya pili.

MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, ninapongeza kwa juhudi zote zinazofanywa na Serikali katika kuimarisha afya nchini. Ombi langu tunaomba wale wataalamu waliohitimu katika Kituo cha Sekomu Lushoto, Tanga, kama Mental Health and Rehabilitation Officer, wapo kama 143 nchi nzima, watambuliwe kwenye Muundo wa Kazi au Work Scheme ili waweze kuajiriwa kwa utaalamu wao. Kwa sasa wanafanya kazi kwa taaluma au madaraja mengine kama Maafisa Tabibu ngazi za Wilaya ambayo sio yao kwa sababu ya kukosa muundo huu.

Mheshimiwa Spika, ahsante na naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii. Nami niungane na wenzangu kuwapongeza viongozi wote wa Maliasili kwa kazi nzuri wanayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kwenye hoja ya msingi. Jimboni kwangu tunao wafugaji wa nyuki. Tunao wafugaji wa nyuki takriban 2,400 ambao wameundwa na Kata mbalimbali ikiwemo Bitale, Murungu, Kitahana, Lusohoko, Kimodo Mjini pamoja na Misezero. Wafugaji hawa wanaweka mizinga yao katika msitu wa Myowosi. Tunaishukuru Serikali ilitenga shilingi milioni 507 kwa ajili ya kujenga kiwanda cha kuchakata mazao ya nyuki. Tumekwisha kupokea shilingi milioni 300 ambazo zimejenga jengo. Tunasubiri shilingi milioni 207 ambazo zinakwenda kununua vifaa kwa ajili ya kuchakata mazao ya nyuki. Tunaishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mazuri hayo, bado tuna changamoto. Changamoto ya kwanza ni tozo. Wafugaji hawa wa nyuki walikuwa wakitozwa shilingi 5,000/= kwa mwezi kwa kwenda kurina asali au kuweka mizinga. Ni wiki tu iliyopita wametangaziwa kwa kupewa tahadhari kwamba ifikapo mwezi wa Saba mwaka mpya wa fedha watakwenda kutoa shilingi 15,000/= kwa mwezi kwa ajili ya kuingia msituni. Ni kubwa sana kwa mwananchi wa kawaida tena mfugaji wa nyuki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile wameongezewa kodi ya baiskeli, shilingi 200/= kwa siku; hiyo inaleta shilingi 6,000/= kwa mwezi. Kwa hiyo, kwa mwezi mmoja huyu mrina asali atatoa shilingi 21,000/= ili aweze kufanya kazi zake kule msituni. Tunaiomba Wizara iangalie upya kabla haijaanza kutumika. Hii ni gharama kubwa sana kwa mfugaji wa nyuki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili, mfugaji yule wa nyuki haruhusiwi kuingia na pikipiki. Angalia mfugaji wa nyuki mwenye ndoo 200 za asali, asombe kwa pikipiki na ana kibali cha mwezi mmoja, haitekelezeki. Tunaomba Wizara iangalie vizuri upya kuona jinsi gani huyu mfugaji ataweza kuyachukua haya mazao yake ya nyuki; asali kuweza kutoa kule msituni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya tatu ni eneo la kuweka ile mizinga. Wafugaji wale wameweka mizinga kilometa tano mpaka kumi. Mwanzo walikuwa wakienda mpaka kilometa 25, imekuja sheria warudi nyuma zaidi. Ombi lao, wafugaji wa nyuki wamenituma, wanaomba waendelee kuachwa pale pale kilometa 20 mpaka 25 kwa sababu hawataki wale nyuki wale haya mazao ambayo yanawekwa kemikali. Maana Jimbo langu la Muhambwe linaongoza kwa asali nzuri organic, hivyo nyuki wale wakila hizi kemikali asali ile itakuwa haifai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa wakulima ambao wanalima karibu na hiyo hifadhi ya Myowosi. Wameshalima, wameshapalilia, umefika muda wa kuvuna, hawaruhusiwi kwenda kuvuna. Naomba hekima itumike, wakulima waweze kwenda kuvuna mazao yao, baadaye sheria itafuata mkondo wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo Kata ya Mrungu katika Kijiji cha Kumbanga. Hiki Kijiji kimeanza mwaka 1974 kikiwa na wakazi 800. Tukiwa tunafahamu kabisa growth rate ya 2.7 tunaweza tuka-imagine hiki Kijiji sasa hivi kina watu wangapi? Kijiji hiki kipo mpakani kabisa mwa Pori la Myowosi na mpaka uko chini ya kilometa moja. Wananchi hawa wamenituma, wanaomba wasogezewe mpaka kwa sababu ni dhahiri wameshaongezeka. Kama idadi ya watu imeongezeka, basi na shughuli za kijamii zimeongezeka ikiwemo kilimo, ufugaji na ziada. Naomba Mheshimiwa Waziri ikikupendeza twende wote Murungu, pale Kumbaga…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kuunga mkono hoja.
(Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana nami kunipatia nafasi niweze kuchangia Hotuba hii ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Rais wetu kwa jinsi ambavyo anaendelea kujali huduma za wananchi wetu. Kipekee niendelee kumpongeza kwa jinsi ambavyo nami nimefaidika sana katika Jimbo la Muhambwe. Tumepata miradi mbalimbali ambayo kwa kweli wananchi wa Muhambwe tunamshukuru sana kwa sababu tutaimarisha huduma za jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu imeendelea kuboresha huduma za afya kupitia sera ya mwaka 2007 kwa kuendelea kutoa huduma za afya kwa makundi maalum. Hii ikiwemo watoto chini ya miaka mitano, wajawazito na wazee wasiojiweza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hotuba ya Mheshimiwa Waziri mkuu kwenye ukurasa wa 13 na wa 53 imeendelea kujipambanua zaidi kuonyesha jinsi gani itaendelea kujali afya za makundi haya. Tumeendelea kufanya vizuri kwa sababu taifa lolote lenye ustawi wa afya ya jamii yake linapimwa kwa vifo vya mama na mtoto. Na kipekee nchi yetu kupitia takwimu za mwaka 2015/2016 Demographic survey inaonyesha kwamba tunapata vifo vya akina mama 556 katika kila vizazi 100,000 vya Watoto hai. Haya ni mafanikio makubwa sana katika jamii yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na mafanikio yote hayo tuliyokuwa nayo, sera hii ya mwaka 2007 ya kutoa huduma kwa makundi haya maalum bado inatoa mianya ya changamoto kwa makundi haya. Tumejitahidi katika hospitali zetu tumeweka madirisha ya kuyahudumia makundi haya, kama vile dirisha la kuhudumia wazee au dirisha la kuchukulia dawa kwa wazee au mabango yanayosema kwamba mzee atahudumiwa kwanza. Hata hivyo ni ukweli usiopingika kwamba madirisha haya mengi yamekuwa kama picha au anasa maana yanaandaliwa tu pale ambapo tunasikia kuna usimamizi shirikishi (supportive supervision), ili viongozi wetu wakija wayaone, lakini kiuhalisia yale madirisha hayafanyi kazi inavyotakikana ndio maana yale makundi bado yanapata tabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile sera hii ni ya muda mrefu tangu mwaka 2007 na Serikali yetu imejikita kuwa na malengo maalum yaliyozinduliwa mwezi wa sita mwaka jana, na kuonyesha jinsi gani inaendelea kuboresha huduma za afya na kipekee makundi maalum na jinsi ambayo taarifa ya Waziri Mkuu imeonyesha, basi ni muda muafaka sasa kuipitia ile sera ili iweze kuendana na hali ya sasa. Kwa maana kwamba makundi haya yaratibiwe vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ushauri wangu katika hili, kwa vile Serikali inatoa pesa nyingi kwa ajili ya kuyahudumia makundi haya basi ni muda muafaka twende kwenye bima ya afya kwa makundi haya. Ile pesa tunayotumia kama ruzuku katika manunuzi ya dawa basi tuwakatie bima za afya ili waweze kupata huduma hizi kwa uhakika. Hii itasaidia kwanza waweze kupata dawa, lakini pili itawaondolea unyanyapaa wanaoupata wanapoenda hospitalini na kuwaambia hawa ni wale wa bure. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile itawasaidia muda wote waweze kupata dawa, na pia itawapunguzia watumishi Maafisa Ustawi wa Jamii ambao wanafanya kazi ya kuratibu tu hawa wagonjwa kwa kugonga muhuri na kuwaorodhesha, ambapo hawa maafisa ustawi wa jamii wangeweza kufanya kazi zingine zenye maana zaidi kama vile kuratibu malezi ya watoto wetu, zero mpaka miaka nane, kudhibiti ukatili wa kijinsia ili kuboresha afya zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile naungana na wenzangu wote walioongea kuhusu ajira. Bado suala la ajira ni tatizo katika nchi yetu; na kipekee nitajikita kwa wale vijana wa Muhambwe ambao wanapitia changamoto kubwa ya kukosa ajira kwenye ile miradi ambayo tunayo katika Jimbo letu. Tunashukuru Mungu Jimbo letu lina mradi mkubwa wa barabara ya kutoka Kibingo mpaka Kasulu. Lakini ni ukweli usiopingika kwamba vijana wetu hawapati ajira katika miradi ile.

Mheshiimwa Mwenyekiti, Waziri Mkuu ana sera nzuri sana ya kusema vijana wapate ajira. Lakini ni nani ana ratibu hili zoezi mpaka kufika kule? Je, mkataba wa huyu mwekezaji unaonesha ni vijana wangapi watapata kazi? Ni wangapi wazawa, na ni wangapi watafanya kazi za kubeba vibendera? Inasikitisha sana pale ambapo hata mbeba kibendera ametoka kwingine. Hatumaanishi ubaguzi lakini tunaomba vijana wa Muhambwe wafikiriwe kwanza kwenye hii miradi inayotekelezeka katika Jimbo letu ili nao waweze kupata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo la mradi mkubwa wa barabara, naiomba Serikali; kwa vile ujenzi wa barabara unaendelea na unatia matumaini kwa kasi nzuri sana, lakini miradi hii inayo miradi shikizi ya jamii, ikiwemo vituo vya afya, shule, kituo cha zimamoto ambavyo kwenye Jimbo langu vinategemea kujengwa pale Nyankwi katika Kata ya Busunzu. Tunaona ujenzi wa barabara unaendela lakini hatuoni miradi hii ikianza kujengwa. Ninafahamu mingine iko Kasulu na mingine iko Buhigwe. Tunaiomba Serikali basi, miradi hii shikizi ya barabara iende sambamba na ujenzi wa barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache naomba kuunga hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na mimi kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumpongeza Rais wetu mama yetu mpenzi, kwa jinsi ambavyo anatekeleza ahadi yake ya kumtua mama ndoo kichwani kwa vitendo. Tumeshuhudia jinsi ambavyo ametoa fedha kwa asilimia 95 kwa Wizara hii. Ni pongezi kubwa sana tunamshukuru mama Mwenyezi Mungu aendelee kumbariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami niungane na wenzangu kuwapongeza Wizara, Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri lakini na Katibu Mkuu Engineer Sanga. Kwa kweli Wizara hii imekuwa faraja kwetu. Tunapokwenda pale hata kama hujapewa fedha lakini unaondoka umecheka ni wakarimu ni Rahim wanatujibu vizuri wanatusikiliza; kwa kweli endeleeni kupiga kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunampongeza sana Engineer Mwenda wa Mkoa wa Kigoma kwa ushirikiano anaotupa pamoja na watendaji wake wote; Engineer Aida, Engineer Almasi wanafanya vizuri sana pale katika Jimbo la Muhambwe kuhakikisha kwamba tunatatua changamoto za maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuishukuru Serikali kwa miradi ya maji vijijini ambayo imetekelezwa katika Jimbo la Muhambwe. Tumeupokea mradi wa maji katika Kijiji cha Mkarazi wenye thamani ya bilioni 1.2. Tumeupokea mradi wa maji katika Kijiji cha Mkabuye wenye thamani ya bilioni 1.4. Tumepata maji katika Kijiji cha Buyezi wenye thamani ya milioni 230. Isitoshe tumepata pesa kutokana na pesa za UVIKO, milioni 500 ambazo zimekwenda kutekeleza maji katika Kijiji cha Mshwagule. Tumepata pia milioni 500 ambazo zimetekeleza mradi wa maji katika Kijiji cha Samvura, Kata ya Mnyambo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio hayo bado nina vijiji 11 mbavyo havina maji. Hivi ni vijiji vya Kumkuyu, Rubunga, Kukinama, Magarama, Kigina, Nyaruranga pamoja na Kasana. Nimepitia bajeti hii tunayokwenda kuipitisha sasa na mimi nitakwenda kuipitisha kwa kiwango cha hali ya juu, nitaiunga mkono kwa sababu, nimeona nimetengewa maji katika vijiji vitatu, Mikonko, Magarama na Lukaya ambayo itagharimu takribani bilioni 1.7. Naishukuru sana Serikali kwa kuendelea kulijali Jimbo la Muhambwe. Naishukuru sana Serikali kwa kuendelea kumtua mama ndoo kichwani kwa vitendo katika Jimbo hili la Muhambwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo niishauri Serikali. Miradi hii ya vijijini scope yake imekuwa ndogo; kwa maana kwamba tunapata yale maji na tunapata yale magati, lakini watumiaji wale wa magati wanakuwa wengi na bado hatujawa na mtandao katika vijiji vyote. Hii inasababisha miradi hii kuharibika kwa haraka hasa uchakavu wa mabomba. Sasa, niiombe Serikali katika miradi hii ya vijijini tujitahidi kusambaza maji vijijini ili tufikie lengo la mwanamke asitembee zaidi ya mita 200 kufuata maji, ili kupunguza uharibifu wa haya mabomba, lakini pia kupunguza mwendo mrefu wa mama kwenda kwenye kituo cha kuchotea maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile niishukuru Serikali kwa kuona umuhimu wa kutuletea wataalam katika hivi vituo. Wote ni mashahidi, changamoto ya maji vijijini ni kuwa na jumuiya za watumia maji hazina wataalam. Kwa hiyo, kwa kitendo hiki cha kutuletea wataalam kwenye jumuiya za watumia maji inatupa uhakika kwamba maji yapatikana. Kwa mfano kule kwangu Kumuhasha tunakaribu miezi sita hatupati maji kwa sababu tu hatuna mtaalamu mahali pale. Kule Malolegwa hatupati maji kwa sababu hatuna mtaalamu. Kwa hiyo, kwa kuja na suluhisho la kuwa na wataalamu kwa jumuiya za watumia maji tutakuwa na uhakika wa kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunayo Mamlaka ya Maji Mjini; niendelee kuishukuru Serikali kwa jinsi ambavyo imetusaidia. Ni mwaka mmoja sasa tulikuwa na asilimia 27 ya huduma za maji. Unaweza ukaona jinsi gani ilikuwa ni changamoto maji Kibondo Mjini nah ii ilikuwa ndio fimbo ya kumchapia Mbunge, hatuna maji. Nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali kwa jinsi ambavyo imetusaidia, imetupatia milioni 595 tumejenga chujio pale mto wa Mgoboka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hiyo, imetupatia tena milioni 590 ambazo tumekwenda kununua pump na mabomba kwa ajili ya kuongeza mtandao wa maji Kibondo Mjini. Tunakwenda kuongeza mtandao wa maji kwa kilometa 11.9 ambazo zitatupa faida kwa watumiaji 550. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sio hivyo tu, tulukuwa na deni kubwa sana la umeme kwenye vyanzo vya maji, milioni 283. Serikali imetusaidia imetulipia deni na sasa tumebaki na milioni 104 ambazo tunaamini Serikali hii ni sikivu, Serikali yetu ya mama yetu Samia Suluhu Hassan, itakwenda kutusaidia kumalizia hizo milioni 104. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumeshapata yote. Tumepata chujio, tumepata mabomba, tumepata na pump za ku-pump, maji haya tutayapeleka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali itusaidie. Ombi letu tunaomba tupate tank la kuhifadhia haya maji ili tuweze kuyasambaza. Tumeshaleta maombi, tunaomba tank la lita milioni 100.5 ambalo litagharimu bilioni 1.1. Ombi langu, naomba mtusaidie ili tuweze kutoka kwenye asilimia hizo tulizokuwanazo, maana baada ya kutusaidia tumetoka 27 tuko 56 na tunalenga na sisi tufike huko 74 ambazo sinasemwa kwamba, ni za kitaifa. Sasa ili na sisi tufike kule tunaomba na sisi tupate tank la maji la thamani hiyo ya bilioni 1.1 ili tuweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, waswahili wanasema kushukuru sana ni kuomba tena. Niendelee kuiomba Serikali itusaidie wataalamu; mamlaka zetu hazina wataalam, hatuna technical staff pamoja na wahasibu. Ma-engineer hawa, Engineer Aidan na Almas wanakimbia sana. Mkiwaongezea hawa wataalamu basi kazi itafanyika vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niombe Serikali itusaidie miradi hii imetekelezwa kwenye maeneo ya watu ambao wanahitaji fidia. Katika Kituo kile cha Kumwai mradi huu umetekelezwa kwenye eneo la watu ambao wanadai fidia, milioni nane. Serikali haishindwi naomba mtusaidie. Familia hizi za akina Hamisi Omary na wenzake kila nikifika jimboni, mama tusaidie; na mimi nakuja leo kuiomba Serikali, naomba tuwalipe fidia wananchi hawa wa Kumwai ambao miradi hii ilitekelezwa kwenye maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niombe vitendeakazi. Jamani Jimbo la Muhambwe ni jimbo lililoko pembeni, tunaomba magari tupate japo gari moja liweze kutusaidia tuweze kutembelea hivi vijiji ili utendaji kazi wa ma-engineer hawa uweze kuboreka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imelea bajeti kwa ajili ya ujenzi wa mabwawa. Na mimi nichukue nafasi hii kuiomba, tuna ahadi ya Mheshimiwa Rais, hayati Magufuli, ya kujengewa bwawa katika Kata ya Busunzu. Naona sasa ni muda muafaka madam tumetenga bajeti basi na mimi naomba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Dkt. Florence Samizi kwa mchango wako.

MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi nami niweze kuchangia bajeti hii ya TAMISEMI. Nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayofanya katika nchi yetu, amejipambanua kwa jinsi ambavyo analeta pesa nyingi katika Majimbo yetu. Ninaapongeze wasaidizi wake Makamu wa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa jinsi ambavyo wanamsaidia na jinsi ambavyo wanakimbia kimbia huko kwenye Majimbo yetu kuhakikisha kwamba utekelezaji wa Ilani unakwenda kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Watendaji wa Wizara ya TAMISEMI nikianza na Mheshimiwa Waziri Angela Kairuki na Wasaidizi wake wote na timu yake nzima wanafanya kazi nzuri kuhakikisha kwamba kule Majimbani tunaweza kusimama kwa kujiamini kwa sababu miradi mingi inatekelezeka katika Majimbo yetu. Niwapongeze watumishi wetu wa Mkoa wa Kigoma wakiongoza na CP. Thobias Andengenye, hususani wale wa Halmashauri ya Kibondo kwa jinsi ambavyo wanapambana kutekeleza hii miradi inayokuja na kipekee kwa jinsi ambavyo wamekamilisha kwa wakati miradi iliyokuja ya madarasa na vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wananchi wa Muhambwe naomba nifikishe pongezi na shukrani nyingi kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa pesa nyingi alizoleta. Jimbo letu limepokea Bilioni 18 zikiwa ni pesa kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Hizi zimewezesha kutekeleza miradi mbalimbali katika Jimbo letu la Muhambwe. Tumetekeleza miradi mingi kwenye elimu afya na barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pesa hizi bado Jimbo la Muhambwe lina changamoto. Nitaanza na changamoto kubwa ya ajira hasa ajira ya Walimu na Watumishi wa Afya. Mkoa wetu wa Kigoma una watumishi 1,955 wa afya ikiwa mahitaji yetu Mkoa wa Kigoma wote tunahitaji watumishi 7,699 kwa hiyo tuna uhaba wa asilimia 74 kwa kiwango cha juu cha uhitaji, lakini kwa kiwango cha chini cha uhitaji tuna uhaba wa asilimia 64.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu la Muhambwe lina mahitaji ya juu ya watumishi 977 lakini tuna watumishi 311 tu ikiwa ni upungufu kwa asilimia 76, Jimbo hili la Muhambwe tunazalisha wakinamama 50 mpaka 55 kwa siku. Kwa hiyo, kwa mwaka mzima tuna vizazi hai 17,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba huu mzigo tuliokuwa nao jimbo la Muhambwe basi na Mkoa mzima wa Kigoma katika ajira hizi tunazotegemea kupata naomba Serikali ituangalie kwa jicho la huruma tukiwa ni Mkoa wa pembezoni, watumishi wengi wanakimbia, tupewe watumishi wa kutosha wakati huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uhaba wa walimu. Katika Jimbo la Muhambwe tuna shule ambazo zina walimu wanne kama ile ya Nyaruhaza na Ntoyoyo tuna walimu wanne tu shule ya msingi. Vilevile nimepata taarifa kwamba kwenye mgao huu wa walimu tumepata mgao wa Walimu 15 hawatoshi kabisa. Nimuombe Waziri, Jimbo la Muhambwe mtusaidie tupate walimu 60 ili angalau hizi shule ambazo zina digit moja moja basi angalau kutoka wanne wawe nane. Tuna shule zina walimu sita nyingi, naomba mtusaidie Jimbo la Muhambwe tupate walimu 60 wa msingi ili tuweze kupambana na uhaba wa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile shule za sekondari tuna uhaba mkubwa sana, kipekee nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu kwa mgao wa madarasa tuliyopata Jimbo la Muhambwe tumefanikiwa kusajili shule tatu za sekondari mwaka 2022 na mwaka 2023 tumesajili shule nne, hivyo tuna uhaba mkubwa wa walimu. Niiombe Serikali tupate mgao mkubwa kwa ajili ya walimu wa sekondari angalau walimu 70 ili tuweze kukabiliana na uhaba huu wa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya Shule 24 tulizonazo za sekondari tuna sekondari Tatu tu za Kidato cha Tano na cha Sita. Kati ya hizo, shule za sekondari moja ilikuwa ni Kambi ya Wakimbizi ya Mkugwa, ninamuomba Mheshimiwa Waziri siku moja aje tukaitembelee hii shule inatia aibu haina madarasa. Ninakuomba shule hii ipatiwe madarasa pia ninaomba tupatiwe na mabweni mawili ili tuongeze shule mbili za Kidato cha Tano ikiwa ni ile shule ya Busagara na Kumgogo ili angalau tuwe na Shule za Kidato chaTano Tano katika Jimbo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwa TARURA nami niwapongeze TARURA wanafanya kazi nzuri na Engineer Victor kwa kweli anastahili sifa zote tulizompa. Sisi tumepata utekelezaji wa madaraja ya mawe, tumepata madaraja ya mawe 19 katika Jimbo la Muhambwe. Kwa hiyo, baada ya kupata haya madaraja tunazo barabara ambazo zinahitajika kuunganishwa, hizi barabara zikiunganishwa basi wananchi wetu wataweza kupita. Tunahitaji kuunganisha Kitahara na Bunyambo, tunahitaji kuunganisha Luhunga na Bunyambo, tunahitaji kuunganisha Nengo na Mbizi, tunahitaji kuunganisha Nyakasanda na Mukarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji Milioni 591 tumeomba, ninawaomba TARURA, nimuomba Mheshimiwa Waziri anisaidie kupata hizo pesa ili hizi Kata na hizi barabara ziweze kuunganishwa kwa sababu tunayo tayari madaraja ya mawe ambayo yamejengwa na Shirika la Enabel, kwa hiyo, tunaomba tuunganishiwe hizi barabara ili wananchi waweze kupita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo bado pia tunauhitaji wa madaraja ya mawe ambayo pia tumeleta, tunahitaji madaraja ya mawe 20 ambayo tunategemea kujenga kule Kagoti na Nyaruranga ili kuwasaidia wananchi wanokwenda mashambani lakini na watoto wa shule wanaokwenda mashuleni wasipite kwenye maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali tuchukue teknolojia hii ya bei nafuu ya kutengeneza madaraja ya mawe ili tuweze kuwasaidia wananchi wa Muhambwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Muhambwe nalo lina maboma ambayo yanahitaji kumaliziwa ikiwemo lile boma la kituo cha afya cha Kizazi lakini madarasa ya karukambati, madarasa ya Kigina, niombe TAMISEMI waje na mpango mahsusi wa kumalizia haya maboma kwa sababu hizi ni nguvu za wananchi na wananchi wanapenda kuona utekelezaji ukifanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuomba utekelezaji wa ahadi za viongozi. Niombe ahadi ya kituo cha Afya cha Mulungo na ahadi ya Milioni 200 kituo cha afya cha Nyaruyoba iweze kutekelezeka. Wananchi wanasubiri kuona utekeleaji wa ahadi hizi kwa sababu ni ahadi za viongozi wakubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia hotuba hii ya Kilimo ambayo ndio uti wa mgongo kwa kuwa tumeona asilimia 65 ya wananchi wetu ni wakulima. Nami nianze kwa kuunga mkono hoja. Pia niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayofanya, lakini kumpongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake nzima kwa jinsi ambavyo wanaitendea haki Wizara hii ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona jinsi ambavyo utekelezaji wa mbolea katika majimbo yetu ulivyofanyika kwa ufanisi mkubwa sana. Ukisoma taarifa ya Mheshimiwa Waziri inaonyesha kabisa kwamba upatikanaji wa mbolea umepatikana kwa asilimia 126, zaidi ya lengo ambalo waliokuwa wamejiwekea la kuingiza mbolea tani 650,000. Hii imetokana na kwa sababu waliingiza tani 617,000 kutoka nje, lakini 75,000 zilitoka ndani ambayo ni takribani kama asilimia saba tu ilitoka ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na mwenzangu aliyepita kusema mbolea ni usalama wa nchi na mbolea ni usalama wa chakula. Tumejionea wenyewe jinsi tulivyopata magonjwa ya mlipuko wa Covid na tuliingia kwenye adha kubwa ya kukosa mbolea lakini vita ya Ukraine na Urusi ndio imekuwa wimbo wetu kwamba imesababisha tumekosa mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani ni muda muafaka sasa kuwekeza zaidi kwenye viwanda vya ndani ili kuepukana na changamoto hiyo. Hii ni pale tu ambapo tutaamua kupeleka ruzuku kwenye viwanda hivi, kwanza ili tuweze kuwapa motisha lakini kama mwenzangu alivyochangia tunaenda kupata hizi trickle down effect. Tutapata ajira, hela yetu itabaki humu humu ndani, pesa itazunguka ndani, tutapata ajira, watalipa kodi, lakini wananchi wetu watafaidika CSR ni hapa hapa ndani na wawekezaji wengine wa nje watafurahia kuja ili sasa tuwe na uhakika wa mbolea kutoka nchini mwetu ili hii asilimia 92 inayoagizwa kutoka nje, basi iwe ya viwanda vya ndani. Tunayo Minjingu, tunayo intercom, wawezeshwe kwa kuwapa motisha ili na wawekezaji wengine waweze kuvutiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, tutaweza kuuza malighafi maana yake samadi tunayo nchini, gesi tunayo, phosphate tunayo, chokaa tunayo, kwa hiyo tutafaidika pia kuweza kuuza haya material yetu katika viwanda vyetu vya ndani na Serikali sasa itafanya kazi zingine kwa sababu kwanza watumishi ni wachache, kwa hiyo uratibu wote tutawaachia wafanyabiashara kwa sababu Serikali basically haifanyi biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye hoja ya umwagiliaji. Ninapongeza Serikali kwa ajili ya umwagiliaji, taarifa imetuambia mabadiliko ya tabianchi yamechangia kuleta matatizo mengi. Ninaishukuru Serikali nimeona sasa hivi na mimi nimewekwa kwenye upembuzi yakinifu, niiombe Serikali kama kweli tunataka kupata kubadilisha kilimo hiki cha umwagiliaji basi tuende kwa vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri ameonesha kabisa yeye ameshaingia mikataba 48 katika mikataba 69 ambayo ni asilimia 70. Kama ameingia mikataba ya shilingi bilioni 234 ni ukweli usiopingika kwamba miradi hii haijatekelezeka, na hii inathibitika kwenye taarifa ya CAG ambayo inasema Serikali imepeleka shilingi bilioni 48 tu sawa na asilimia 18 kwenye miradi ya umwagiliaji. Ndiyo maana hapa kila mtu anasema sijaona skimu hata mimi sijaona skimu. Mheshimiwa Waziri Kaka yangu Mheshimiwa Bashe nakushukuru nimepangwa kwenye upembuzi yakinifu kwenye skimu za Kigina, Muhambwe, Kumbanga, Nyendara. Ninakuomba skimu ya Nyendara naomba ifanyiwe kazi mapema, kwa sababu ilijengwa ikafikia nusu na sasa imekuwa ni majanga. Tumeshapata matukio ya vifo vifo sita pale maana it’s incomplete work, watu wanatumbukia kwenye ile skimu, niombe kama haiwezekani kuisha tufunike wananchi wa Muhambwe wamesema bora tufunike iwe hamna ili watu wasife, kuliko wananchi kutumbukia kwa sababu skimu ile haijaisha. Skimu ile ili iishe inahitaji shilingi milioni 300 mpaka 500 tu. Imefikia asilimia 80, niwaombe katika mpango huu nami niwekwe kwenye mkakati ili wananchi wangu wa Nyendara, wananchi wangu wa Kata ya Misezelo waweze kuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuiombe Serikali sasa kwa hali hii hatuna sababu ya kuendelea kutumia nguvu nyingi sana kusema kwamba Serikali imeongeza bajeti. Tutumie nguvu nyingi sana kuwaambia wananchi mnaona skimu, mnaona hiki, mnaona hiki itakuwa kazi rahisi sana kuliko kutumia nguvu nyingi kuwaambia bajeti imeongezeka. Wananchi wetu wanataka kwenda kuona uhalisia wa hii bajeti kwenye maisha yao ya kila siku kwa maana waweze kuzalisha kwa sababu ndiyo kazi yao ya kila siku. Kwa hiyo, naamini Mheshimiwa Bashe katika hili mtakwenda kunisaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ninaipongeza Benki ya Kilimo nimeona imetoa mikopo kwa wananchi lakini wananchi wa Muhambwe hawajafaidika kwa sababu bado benki hii ina pesa kidogo. Naomba Serikali iiongezee mtaji ili na wananchi wa Muhambwe waweze kufaidika kupata vitendeakazi. Hatuna matrekta, hatuna magari, tunalima bado kwa jembe la mkono, ninaiomba benki hii iweze kuongezewa fedha ili sasa iwafikie wakulima wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona kwenye taarifa wakulima wadogo wadogo wamekopeshwa shilingi bilioni 60 tu ni ndogo sana kwa wananchi wetu. Kwa hiyo, niiombe Serikali iwasaidie wakulima wadogo wadogo kwa kuongeza mtaji kwa benki hii ili wananchi wetu waweze kujikwamua na waondokane na hiki kilimo ambacho wanaona kwamba ni shida kwa sababu hawana vitendeakazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba mradi wa BBT unakwenda kuleta mabadiliko kwa vijana wetu, lakini niungane na wenzangu, wale watu waliokuwa wanalima hiki kilimo ambao walikuwa wanahangaika wenyewe na wametulisha kwa miaka mingi waangaliwe pia kule kule waliko ili nao waweze kusaidiwa. Vijana wasaidiwe lakini na wale watu waliotutunza miaka yote wasaidiwe. Changamoto zao tunazifahamu nao tuwalenge kule kule waliko ili waweze kusaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu liko mpakani, ninaiomba Serikali kwa sababu mazao yetu mengi na hasa muhogo tunawauzia nchi jirani, niombe kusaidiwa maghala ili tuweze kutunza kwa sababu wale wa nchi jirani wananunua mashambani kwa hiyo wanawaibia wakulima. Niombe maghala ili wananchi wangu waweze kutunza mazao na tuwe na masoko ya ujirani mwema kwa sababu tutawauzia ile mihogo nchi jirani kwenye soko la pamoja. Nikipata maghala, nikipata soko, nikapata na vitendeakazi basi wananchi wangu wa Jimbo la Muhambwe watakwenda kufaidika na watakwenda kuzalisha kwa kiwango cha hali ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi naamini kwa haya machache, naunga mkono hoja kwa sababu kilimo ni uti wa mgongo wa Jimbo la Muhambwe. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuiongoza nchi yetu lakini kipekee kwa nia yake ya dhati kabisa ya kuifungua nchi yetu kwa miradi mikubwa ya barabara, reli, ndege wote tunaona jinsi gani nchi yetu inakwenda kufunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Waziri Profesa Mbarawa na Naibu Mawaziri, Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa mashirika yote, Bandari, TASAC, Shirika la Ndege wote vijana wanachapa kazi, wanafanya vizuri tunaona jinsi gani wanaweza kuyaendesha hayo mashirika na tunaona jinsi gani Tanzania inakwenda kubadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisiwe mchoyo wa fadhila, nimshukuru Kaka yetu Engineer Choma, Engineer wa TANROADS Mkoa wa Kigoma anachapa kazi vizuri katika Mkoa wetu wa Kigoma, anatupatia ushirikiano wa kutosha, tunaona jinsi miradi ya Mkoa wa Kigoma inavyofanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wananchi wa Muhambwe nasimama hapa leo kutoa shukurani nyingi kubwa sana kwa Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo miradi ya barabara inaendelea katika Jimbo la Muhambwe. Tunao mradi wa Barabara wa Mvugwe – Nduta Junction kilometa 59 ambao mwaka huu umefikia asilimia 66, mwaka jana ulikuwa asilimia 25, tunaipongeza Serikali inafanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunayo barabara ya Nduta Junction - Kibondo Mjini kilometa 25.9 mwaka jana ilikuwa asilimia 44 na mwaka huu sasa hivi wako asilimia 58. Tumesaini mkataba wa ujenzi wa barabara kutoka Kibondo Mjini kwenda Mabamba kilometa 47.9 kwa gharama ya takribani shilingi bilioni 69. Hizi ni jitihada za dhati kabisa za Serikali za kuendelea kuwaunganisha wananchi wake kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee tunaenda kufaidika kabisa maana barabara hii inakwenda kuboresha soko la ujirani mwema pale katika Kijiji cha Mkarazi ambacho tunafanya biashara na ujirani mwema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio hayo ya miradi hii inayoendelea katika Jimbo la Muhambwe, bado ziko changamoto ndogondogo. Kwanza kabisa barabara hizi zitategemewa kuisha mwaka huu Desemba na kama tuko kwenye asilimia 66 ni ukweli usiopingika kwamba tunatakiwa kuongeza kasi. Wananchi wa Muhambwe wamenituma wanaomba kasi ya ujenzi wa hizi barabara ili tuweze ku-meet target. Ziishe kwa wakati kwa sababu hili ni Jimbo ambalo lilikuwa halijaunganishwa kwa lami bado. Kwa hiyo, nawaomba watendaji kwa nia ya dhati kabisa Mheshimiwa Rais ya kutuunganisha na lami basi kazi ifanyike kweli kweli ili barabara hizi ziweze kuisha kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hizi pia zina miradi ya CSR ambayo miradi hii ilitegemewa kujengwa Kibondo, Kasulu na Buhigwe. Barabara zimefikia asilimia 66 lakini miradi hii bado haijaanza. Ninajua michakato inaendelea, niiombe Serikali miradi hii ya CSR ambayo inategemewa kujengwa katika Majimbo haya matatu Kibondo, Kasulu na Buhigwe basi nayo iende kwa kasi ili barabara zitatakapoisha na miradi hii pia iwe imekwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipo kipande cha barabara ambacho Wabunge wa Mkoa wa Kigoma tumekuwa tukikisemea sana, Uvinza – Malagarasi kilometa 51. Ukipita kwenye ile barabara ni changamoto yaani ukimaliza pale lazima upeleke gari yako service. Kipande kile ni kibaya sana na kwa taarifa ya Mheshimiwa Waziri kipo asilimia 26 kwa hiyo ni ukweli usiopingika kwamba bado kiko nyuma sana. Tunaomba Serikali itusaidie sisi Wabunge wa Mkoa wa Kigoma barabara hiyo inatupa changamoto siyo nzuri, haipitiki tunaomba kasi iongezeke. Kama kuna changamoto kwenye kile kipande basi zifanyiwe kazi ili kipande kile nacho kiweze kuisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na miradi hii ya lami bado ziko barabara za TANROADS ambazo tunahitaji ziwe kwenye kiwango cha lami ambapo kwa sababu ya mvua hizi zinazonyesha barabara hizi hazipitiki. Hii ni barabara ya Kitaha na Nyange ni mbaya sana haipitiki, iko chini ya TANROADS, hii ni Barabara ya Kifura – Nyange haipitiki, Barabara ya Bunyambwe – Nyange haipitiki. Nimuombe Engineer Kaka yangu Engineer Choma ninamuamini sana anaweza. Tunamuomba kule Kibondo atusaidie kutengeneza hizi barabara kwa kiwango cha changarawe na kipekee niombe kusisitiza kwamba barabara hizi zinavyotengenezwa basi ziwekwe mifereji kwa sababu mvua imekuwa chanzo kubwa cha kufanya ziharibike sana. Naamini zitatekelezeka kwa sababu TANROADS wanafanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wote wamesema Wabunge wa Mkoa wa Kigoma, Rukwa na Katavi kwa kweli tunaipongeza Serikali kwa jinsi ambavyo wamejenga MT Sangara na tumeona ipo asilimia 90 meli ambayo itaenda kubeba mafuta. Hii Serikali imelenga kufanya biashara lakini Serikali kama Serikali mbali na biashara lengo kuu la Serikali kwanza ni kuwahudumia wananchi, ustawi wa wananchi wake. Jamani wananchi wa Mkoa wa Kigoma, Wananchi wa Rukwa na Katavi tunaomba meli ya abiria na mizigo midogo midogo ili wananchi wetu waweze kusafiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona imepita bajeti hapa ya kutengeneza MV Liemba, MV Mwongozo, tunaomba kama ambavyo Mheshimiwa Waziri ameweka commitment kwamba itaanza mwezi wa sita na mwezi wa nane itakuwa imeisha. Tunaomba mchakato huu uende haraka sana. Kwa nini? Mwenzangu amesema tumejenga bandari, Kigoma tumejenga, tumejenga Karema, tumejenga Kabwe, Kipili, Kasanga. Kama hatuna meli tulitaka ku-achieve nini kwa ajili ya hizi bandari? Tunajenga SGR inakwenda kupeleka watu kule, bila kuwa na meli tunaenda ku-achieve nini? Tunaiomba Serikali ituangalie Wananchi wa Mkoa wa Kigoma, Katavi na Rukwa ili tuweze kufunguka kibiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamesema sana kuhusu Shirika la Ndege. Ni ukweli usiopingika kwamba shirika hili linafanya kazi sana. Tumeona lilikotoka na lilipo sasa, ninampongeza sana Mkurugenzi na watumishi wote. CAG amesema pamoja na jinsi ambavyo shirika linafanya, bado hili shirika ukisema mashirika ambayo yanajiendesha kwa hasara kwa miaka mitano mfululizo basi unataja shirika hili. Ukisema shirika ambalo lina mitaji hasi unataja shirika hili na tumeona kinachochangia kikubwa ni uendeshaji wa hili shirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Kamati imeshauri, CAG ameshauri. Nafikiri ni muda muafaka sasa Serikali kurudi nyuma na kuangalia jinsi gani ya uendeshaji na kipekee kuwapunguzia hii gharama ya kukodi ndege, kwa sababu tumeona CAG amesema mikataba mibovu katika kukodi ndege imesababishia shilingi bilioni 19.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya ndege ya Tanzania, wakala wa ndege wa Tanzania mikataba inakuwaje mibovu kiasi kwamba shirika linapata hasara? Basi tuwape nafasi tuwapatie hizi ndege ili waweze kuendesha wenyewe. CAG anasema, Serikali ilitoa ruzuku, shilingi bilioni 30, lakini shirika likapata hasara ya shilingi bilioni 35. Ina maana bila ruzuku, shirika lingepata hasara ya shilingi bilioni 65. Sasa kama tunapeleka ruzuku na tunataka wafanye vizuri, tuwasaidie kwa sababu wanafanya vizuri ili waweze kujiendesha. Wapewe ndege na pia walipiwe madeni yao ili waweze kuendelea kujiendesha kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Serikali kwa jinsi ambavyo inaendelea kutuangalia Mkoa wa Kigoma na inaendelea kutaka kutufungua kwa uhakika. Bajeti ya Uwanja wa Ndege wa Kigoma ilitengwa mwaka 2021, hakikufanyika kitu; 2022 imetengwa, hakikufanyika kitu; 2023 imetengwa tena shilingi bilioni tisa. Wananchi wa Kigoma wamechoka kuambiwa kwamba bajeti imetengwa, wanataka kuona utekelezaji. Running way tumesaini mkataba pale, tunaamini mkandarasi atafika site kwa wakati.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Dkt. Florence, muda wako umeisha.

MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Kufutwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi ili Kuruhusu Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Msitu wa Kigosi na Azimio la Bunge la Kuridhia Kurekebisha Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi.

Mheshimiwa Spika, niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa jinsi ambavyo amejionesha kwa vitendo kwamba anapenda amani kwa sababu anakwenda kutatua migogoro. Na naunga mkono maazimio yote mawili kwa sababu yana faida kubwa na tija kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yoyote yenye migogoro haitawaliki, kwa hiyo Mheshimiwa Rais anataka kuondoa migogoro. Nitaanza na mgogoro wa Mbarali; mgogoro huu umekuwepo tangu 2008 pale ilipowekwa GN 28. Baada ya GN 28 kuwekwa wananchi hawakuridhika kwa sababu kuna maeneo ya uzalishaji ambayo yalikwenda kwao.

Mheshimiwa Spika, kwa bahati mbaya au nzuri kuna eneo la mwekezaji ambalo lenyewe lilibaki, eneo la Kapunga. Kwa hiyo, hili eneo lilisababisha wananchi waone kama wao hawakutendewa haki. Kiukweli eneo hili lilibaki kwa sababu lina miundombinu mazuri ya maji, kwa hiyo, maji hayapotei.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Kamati tumekwenda pale tumejionea na tumeridhika na yale maamuzi. Lakini ili kuondoa mgogoro wa Mbarali, Kamati tunashauri lile eneo ambalo liko sambamba na mwekezaji ambalo ni Mpunga Mmoja ambapo maeneo yote haya mawili awali yalikuwa ya wananchi, wananchi waliyatoa yale maeneo bure kwa ajili ya mwekezaji, basi nalo liwekewe miundombinu ambayo itasababisha maji yasipotee, na eneo hili wananchi walitumie kwa kilimo. Hili likifanyika wananchi wa Mbarali wameelewa kabisa na wanaunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais kwa sababu wanaona kabisa uharibifu unaotokea.

Mheshimiwa Spika, tumejionea jinsi gani uharibifu unatokea katika hili Bonde la Ihefu. Hili beseni ambalo tunasema ni la maji, maji hakuna, yamekauka, maji yapo kidogo sana. Kwa hiyo, hii inakwenda kuathiri uzalishaji wa umeme Kidatu na Bwawa la Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hatua hizi ambazo Serikali imechukua ni mahususi, tunaunga mkono asilimia 100 kwa sababu miradi hii imetumia pesa nyingi, Rais Dkt. Samia ameweka pesa nyingi kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere. Bila kufanya hivi basi bwawa hili halitazalisha.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mbarali wanatambua kwamba wanahitaji umeme. Tunachotakiwa kufanya tusimamie yale tuliyoyaamua sasa. Tunayasimamia vipi, basi hivi vigingi viwekwe mahali pote ili mipaka iimarishwe. Kwa sababu bila mipaka kuimarishwa siku ya siku wananchi watarudi.

Mheshimiwa Spika, tumeona mpaka ng’ombe wameanza kwenda kule. Kwa hiyo, hii mipaka isipoimarishwa uharibifu utaendelea kufanyika katika Bonde hili la Ihefu. Kwa hiyo, miradi yetu ya umeme itaharibika. Tutaharibu mazingira yote, maji hayatapatikana ambayo yanatiririka kwa ajili ya kwenda kwenye Mto Ruaha.

Mheshimiwa Spika, tunaiomba Serikali pia iweke mkuza kuzunguka yale maeneo muhimu, na siyo huko tu, nchi nzima, ili haya maeneo yetu tuweze kuyadhibiti kwa sababu tunavyokuwa tumelegalega ndiyo wananchi wanaingia, kuwatoa tunawatoa kwa gharama kubwa sana. Kwa hiyo, tuhakikishe kwamba tumejikinga kabla ya hatari ili wananchi wasiweze kuingia.

Mheshimiwa Spika, ushirikishwaji ni kitu ambacho wananchi wametuambia, wanaomba kushirikishwa. Washirikishwe kuanzia awali, waelimishwe ili wasione kama Serikali inawaonea, ili wasione kama Serikali inapendelea wawekezaji, ili wasione kwamba Serikali inawanyanyasa; waelimishwe na wapate elimu ya kutosha wao na wawakilishi wao.

Mheshimiwa Spika, sisi tulipata bahati ya kukutana na Madiwani na hili waliliongelea, kwamba sisi ni Madiwani, tukielewa tutawafahamisha wananchi wetu. Kwa hiyo, wawakilishi na wananchi wafahamishwe ili wananchi wetu waweze kuelewa.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tumesikia, kuna vijiji vitano vitaondoka kabisa. Hawa watu wapewe fidia kwa wakati kwa sababu sasa baada ya kuambiwa kwamba wao wanaingia kwenye hifadhi hawawezi kuendelea kufanya chochote, hawawezi kuendelea kulima wala kuendeleza maisha yao. Kwa hiyo, watakuwa wamesimama, kama ikichukua muda mrefu basi wananchi hawa wataingia hasira na Serikali na kusababisha migogoro.

Mheshimiwa Spika, kwa juhudi hizi alizozifanya Mheshimiwa Rais, na hayo niliyoyasema yakizingatiwa, basi tuna uhakika kwamba bonde letu litaendelea kuwa salama, umeme utapatikana na migogoro itaisha.

Mheshimiwa Spika, niongelee Kigosi, Kigosi pia tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa jinsi ambavyo anajali wananchi wake. Haya matatizo ya wafugaji nyuki kukosa mahali pa kuweka mizinga yapo katika mapori mengi, ikiwemo Kigosi, hata Moyowosi kule ambako ni hifadhi ya wanyamapori, hii shida ipo.

Mheshimiwa Spika, ikishakuwa hifadhi, wananchi wetu ambao walikuwa wanafuga nyuki hapo awali kwenye hiyo misitu wanakosa pa kuweka mizinga. Kwa hiyo, kwa hatua hii ya Mheshimiwa Rais kuruhusu kwamba hii ishushwe hadhi ina maana wananchi wanaruhusiwa kufanya shughuli zao. Watafanya shughuli hizo za ufugaji nyuki, watafanya shughuli za uvuvi na za matambiko.

Mheshimiwa Spika, tunaomba sasa Serikali kufanya uratibu mzuri kwa sababu bado ni hifadhi ya misitu, bado tunahitaji kulinda misitu yetu, haimaanishi misitu ikatwe sasa, hapana, ametoka TAWA lakini sasa TFS anachukua charge.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaomba Serikali iweke uratibu mzuri na hasa wa zile tozo. Tozo zieleweke; anayekwenda na baiskeli anakwendaje, na pikipiki anakwendaje, kwa sababu hizi tozo pia ni moja ya sehemu ambazo zinapigiwa kelele.

Mheshimiwa Spika, tunamuunga mkono Mheshimiwa Rais, anawajali wananchi wake ndiyo maana anaachia maeneo, maeneo yote anayoachia anasema wapelekewe wananchi kwa sababu anataka waweze kuendelea na uzalishaji. Amerudisha maeneo hifadhi hii iwe na misitu ili viwanda viweze kufanya kazi ili sasa wananchi waweze kuweka mizinga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunasema sisi sasa hivi ondoa shoka uweke mzinga. Kwa hiyo tunaamini miti yetu sasa badala ya kukatwa, mtu hawezi kukata kwa sababu yeye mwenyewe anataka kuweka mzinga, kwa hiyo, kwa kuwashirikisha wananchi wao wenyewe watakuwa ni wahifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa haya machache, naunga mkono hoja. Naipongeza Serikali, nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii kwa ushirikiano mkubwa aliotupa; Naibu Waziri, Katibu Mkuu na timu nzima. Wao ndio wamesababisha tuweze kuratibu jambo hili na tuweze kufika hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayofanya ya kuwaletea maendeleo wananchi wa Tanzania. Wenzangu wamesema apewe maua yake, nami nasema Mheshimiwa Rais apewe maua yake, anafanya vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Naibu Waziri na timu nzima ya wizara, mnafanya kazi nzuri, taarifa nzuri sana, kila unapoisoma unaona raha, kwa kweli package ni nzuri kwa ajili ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, ninayo machache ya kuchangia katika bajeti hii. Mheshimiwa Waziri katika hotuba yako umesema kabisa kwamba wastani wa watu waliochangia kodi ni asilimia 20 tu ndio waliochanga vizuri. Umesema kwamba walipa kodi waliosajiliwa ni 4,455, wenye TIN halali ni 4,400,000; wenye TIN halali ni milioni moja, hawa milioni moja wamechangia trilioni 16.7 kwa maana ya asilimia 80 ya mapato yetu, ambayo mwenyewe umesema kabisa mapato hayo yamepatikana na idadi ya wachangiaji wadogo sana, asilimia 20. Palepale ukasema kwamba katika maneno muhimu ya kuzingatia ni ukweli kabisa kwamba wastani wa walipa kodi siyo mzuri sana kwa sababu wanaolipa kodi ni wachache kwa hiyo wachache ndio wanachangia kodi ya nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema nini; nataka kusema kwamba bado kuna kazi kubwa tunatakiwa kufanya ili tuweze kuongeza mapato, ili tuweze kuongeza hawa wachangiaji wa hii kodi yetu. Na hii inaweza kusaidiwa kwa kuendelea kuongeza vyanzo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichangia hapa mwaka jana, na leo nasema; bado tu sisi tunaotoka majimbo ya mpakani; Kakonko, Kibondo, bado tuna fursa ambayo haijatumika vizuri, fursa ya mipaka yetu. Bado masoko ya ujirani mwema yanafanyika kiholela, masoko ya ujirani mwema ni shamba la bibi kwa sababu uratibu haupo. Kila mtu pale ni afisa mkusanyaji mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliomba hapa kujengewa forodha ya pamoja ili tuwe na TRA pale, tuwe na polisi na migration ili biashara iweze kufanyika vizuri kwenye Soko langu la Mkarazi na Soko langu la Kibuye. Haya yote yameshindikana. Haya ni mapato ambayo yanapotea. Tungeweza kudhibiti haya mapato tusingeendea kukandamiza wananchi kwa kung’ang’ania vyanzo vichache, lakini walipa kodi wachache ndio wanatuchangia Pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, nakuomba uje kwenye masoko yetu ya ujirani mwema. Kule Muhange, Mkarazi na Kibuye, tunaomba uje, kuna pesa kule, turatibu zile biashara za kwenye mipaka ili tuongeze walipa kodi na ili tuweze kuratibu hizi biashara za mipakani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, tukiongeza walipa kodi hatutakuwa tunaongeza kodi kwenye vile vyanzo tunaona kwetu ni rahisi. Nimeona hapa tumeongeza tena kwenye mafuta na cement, ina maana tunatafuta urahisi wa kupata hii pesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi leo ninavyoongea Jimbo la Muhambwe cement inauzwa 23,000 kwa mfuko mmoja wa kilo 50. Sasa ninajiuliza hii kodi ikiongezeka kwenye cement wananchi wa Muhambwe tutajenga kweli? Mtu wa Dar es Salaam ananunua 14,000, tunaambiwa usafiri ndiyo unasababisha cement iwe 23,000 Kibondo. Sasa mafuta nayo yameongezeka, wananchi wa Muhambwe hii cement hawataweza kuinunua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, ninawaomba, hebu tutoke nje ya boksi na wataalamu watusaidie, akili ichangamke kidogo, basi turatibu hii bei, bei iliyoko Dar es Salaam na bei iliyoko Kibondo iwe ileile ndiyo tuongeze hizi kodi. Lakini kama tunasema usafirishaji unasababisha cement iwe ghali basi tunaomba hii kodi ya cement itolewe. Maana yake mpaka sasa ni 23,000, kwa hiyo, itakuwa changamoto kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, mafuta yatakwenda kuleta matatizo mengi; nauli itapanda, mazao yatapanda, kila kitu kitapanda. Kwa hiyo, ninaomba wataalamu wetu nao akili zao zijiongeze tunasema watoto wa mjini watafute vyanzo vingine ili tusiendelee kumkamua ng’ombe wa maziwa mmoja huyohuyo, atakufa maana yake atakamuliwa mno Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, vilevile niombe; ni hakika tunahitaji hizi pesa, hata natamani tuzipate kwa ajili ya kuratibu na kuharakisha miradi, maana yake tunayo miradi kwenye majimbo yetu ambayo kwa kweli kasi yake haifurahishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hivi karibuni tu miliona vibonzo vinapita vikionesha vumbi la Kibondo. Hata sisi watu wa Kibondo hatujisiki vizuri, tunatamani lile vumbi liishe. Tunaomba miradi yetu ya kimkakati ya barabara yetu ya kuunganisha Kasulu, Kibondo, barabara ya kuunganisha Kigoma, Tabora, zipelekewe pesa, wakandarasi walipwe pesa zao ili hizi barabara ziweze kuisha na sisi tusiwe vibonzo kwenye mitandao kwa ajili vumbi linaloendelea katika majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, miradi hii ya kimkakati inayojengwa katika Mkoa wa Kigoma inayo miradi ya complementary ambayo inategemea kujengwa Kasulu, Buhigwe na Kibondo. Barabara zipo asilimia 60, 70, 80, lakini miradi hii haijaanza kabisa. Tunaiomba Serikali miradi hii ianze, kwa sababu kama hizi barabara zitaisha halafu miradi haijafanyiwa chochote matokeo yake hii miradi itakwenda kupotea. Na sisi tulishawaambia wananchi wetu kwamba hii miradi ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia niombe Mheshimiwa Waziri, bajeti ya mwaka 2021/2022 majimbo yote ya Mkoa wa Kigoma yalipewa milioni 150 kwa ajili ya kumalizia maboma ya zahanati, kasoro Jimbo la Muhambwe. Nimeshakwenda TAMISEMI zaidi ya mara nne, nimeshakwenda Wizara ya Fedha zaidi ya mara nne, naambiwa vifungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi pesa mlitupa ninyi na majimbo yote yamepewa. Afisa mipango vifungu anavitoa wapi? Nilishakwenda Kumkuyu nikafanya mkutano; Rukaya nikafanya mkutano, tena kwa kujinasibu jamani naleta milioni 50 ya zahanati, leo hii naambiwa vifungu ambavyo hizo pesa mmeleta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuomba Mheshimiwa Waziri unavyokuja kuhitimisha hapa naomba milioni 150 yangu kama ambavyo majimbo mengine yamepewa ili na mimi niende kutimiza zile ahadi ambazo niliwaahidi wananchi wa Jimbo la Muhambwe. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja asilimia 100. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ili niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu sana. Nami nianze kwa kumpongeza Rais wetu, Mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo anaendelea kujali maisha ya Watanzania na kipekee kwa jinsi ambavyo ametoa pesa kwa ajili ya kupunguza makali ya bei ya mafuta. Niwaombe watendaji bei hii iwanufaishe watu wote na siyo wa mijini tu. Kwa sababu tayari kumeshakuwa na malalamiko kwamba huko kwetu vijijini imepungua Sh.150. Naomba taasisi husika tulifuatilie kwa sisi tunaotoka vijijini ili keki hii basi wote tuweze kufaidika sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Waziri wa Nishati na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara hii. Kipekee pia nimpongeze Mkurugenzi wa REA kwa kazi nzuri anayofanya, lakini na Mkurugenzi wa TANESCO, ndugu yetu Maharage Chande ameanza vizuri, amekuja na mikakati mizuri tunaiona, Nikonekt, Mita Janja tunaamini zitaenda kuondoa changamoto kubwa tulizokuwa nazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisimama katika Bunge hili mwaka jana kama sasa ambapo Jimbo langu la Muhambwe lilikuwa lina vijiji sita tu vilivyowekewa umeme, lakini leo nisimame kuishukuru Serikali na kuipongeza kwamba kwa sasa nina vijiji 25 ambavyo vimefikiwa na umeme. Hii ni kazi nzuri inayofanywa na Shirika letu la REA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo ninavyo vijiji 15 ambavyo hivi vinatakiwa kuwekewa umeme kwa sababu vimeshapelekwa nguzo lakini vimekumbwa na hii changamoto ya nyaya, MV na LV imekuwa ni changamoto. Tunaambiwa low voltage na medium voltage imepanda bei. Niombe Wizara, niombe Serikali iingilie kati hili suala la wakandarasi kukosa hizi nyaya. Vijiji vyangu hivi 15 ukivipa hizi nyaya vinaenda kuwashwa umeme, nitakuwa na vijiji 40, hii ni quick win.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba jitihada za makusudi zichukuliwe kabisa kuhakikisha tunapata hizi nyaya kwa wananchi wangu ambao katika Jimbo la Muhambwe ambao wamesubiri umeme kwa muda mrefu sana. Maana vijiji hivi ni utekelezaji wa REA awamu ya III, mzunguko wa kwanza, maana tulipitia changamoto kubwa, naomba jitihada hizi zifanyike kwa haraka ili wananchi waliosubiri umeme kwa muda mrefu wa Muhambwe, Kukinana, Kumsenga, Kwakijina, Lukaya, Magarama, Kumkubwa wanasubiri umeme kwa muda mrefu. Naomba Serikali ichukulie kwa uzito wake ili tuweze kupata umeme katika jimbo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niungane na wenzangu kuhusiana na bei ya kuunganisha umeme. Sisi wananchi wa Muhambwe mradi wetu mzunguko wa kwanza ulichelewa sana, kwa hiyo, hatukufaidika na hiyo shilingi 27,000. Nimpongeze Waziri ameliona hili na amesema ndani ya miezi sita atakuja na jibu zuri. Niombe Jimbo la Muhambwe lipewe upendeleo wa kipekee kwa sababu hatujafaidika na hiyo bei ya shilingi 27,000 ili wananchi wangu waendelee kulipa shilingi 27,000 ili waweze kuunganisha huu umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuiomba Serikali, pamoja na jitihada hizi nzuri bado umeme haujawafikia wananchi. Kipekee niwasemee wananchi ambao wanatumia hizi taasisi mbalimbali ikiwemo taasisi za afya;- mahospitali na zahanati, lakini taasisi za elimu; mashuleni, taasisi za dini; makanisani na misikitini bado ni changamoto kubwa. Naomba REA wachukue jitihada za makusudi kuhakikisha kwamba taasisi hizi zinapata umeme, kwa sababu tunapozipatia taasisi hizi tutakuwa tumewagusa watu wengi kwa wakati mmoja na vilevile tutakusanya mapato zaidi kwa hizi taasisi kwa sababu zina uhakika wa kulipa zaidi. Naomba zipewe kipaumbele cha makusudi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kilio chetu Mkoa wa Kigoma kuunganishwa kwenye gridi ya Taifa. Niipongeze Serikali na kumshukuru Waziri, nimeona kwenye vipaumbele ni kipaumbele cha kwanza kuunganisha Mkoa wa Kigoma kwenye gridi ya Taifa. Namwomba Mheshimiwa Waziri kama walivyotuahidi kwamba mwezi Oktoba, Mkoa wa Kigoma tunakwenda kuunganishwa kwenye gridi ya Taifa, basi bajeti i-reflect kile walichotuahidi kwamba kwa bajeti ambayo wametuwekea basi iweze kuunganishwa kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba tutengewe bajeti ya kutosha ili tuweze kuunganishwa kwenye gridi ya Taifa kama walivyotuahidi mwezi Oktoba ili na sisi wananchi wa Mkoa wa Kigoma basi tuanze hizo biashara wenzetu wanazofanya kama za vinyozi, vijana wanasubiri kwa hamu, basi na sisi tuuze soda baridi, tuuze maji baridi, maana yake tumesubiri kwa muda mrefu, naomba lizingatiwe, kama tulivyopewa kipaumbele cha kwanza, basi na pesa pia tupewe mgao wa kutosha kama kipaumbele cha kwanza kinavyoonesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishukuru Serikali vile vile, mwaka jana tulikuwa na mradi wa kupata umeme kutoka maporomoko ya Mto Malagarasi, megawati 49.5. Nimeona safari hii tumetengewa Bilioni 13. Nichukue nafasi hii kuipongeza na kuishukuru Serikali kwa sababu kupata umeme katika maporomoko ya Mto Malagarasi itakuwa ni suluhisho la kudumu. Naomba tulichukue kwa umuhimu wake ili wananchi wa Muhambwe waweze kupata umeme kutoka katika Mto Malagarasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi zote hizi niendelee pia kuipongeza TANESCO. Mkurugenzi amekuja na mikakati mizuri, lakini nimepitia taarifa ya Mkaguzi Mkuu wa Mahesabu ya Serikali. Ili tuweze kulisaidia hili shirika na tuweze kulikwamua hapo lilipo, lazima tulisaidie hili shirika. Shirika hili la TANESCO ni kati ya mashirika ya Serikali ambayo yana deni kubwa kuliko mtaji. Hii imeoneshwa kwenye ukurasa wa 36 wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shirika hili linadaiwa Tritioni 13.4 na huku likiwa na mtaji wa Trilioni 3.0. Hii ni uwiano wa takribani asilimia 356. Hii ina maana gani? Shirika hili haliko himilivu, shirika hili halijasimama kibiashara. Kwa hiyo, naiomba Serikali iisaidie shirika hili. Tunafahamu katika deni hili liko principle na kuko na interest. Pia yapo na madeni mengine kama hapa Wabunge wengi wamesema jinsi ambavyo wanadaiwa kwenye gesi, basi Serikali ichukue jitihada za makusudi kulisaidia hili shirika ili tuweze kulipima kwa sababu madeni yao wameyarithi, ni madeni ya miaka mingi, mengine ni ya makaratasi lakini mengine ni kama hayo nimesema ni interest.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lisaidiwe hili shirika kuweza kulipa hili deni, aidha Serikali ilichukue hili deni au iligeuzwe hili deni liwe mtaji au iipe ruzuku TANESCO hasa kwenye hii gesi ambayo matumizi ya gesi ni makubwa takribani Bilioni 40 mpaka Bilioni 50 tumeona TPDC wanawadai Bilioni 400 shirika hili haliwezi kwa nini nasema haliwezi, nimepitia mahesabu ya mapato ghafi ya shirika hili, hawa wanakusanya takribani Bilioni 120 hadi Bilioni 150 kwa mwezi ina maana kwa mapato yao hata tukiwaambia wasitumie hizi pesa kwa jambo lolote hili deni watalilipa ndani ya miaka Nane mpaka Tisa, hawawezi kulilipa, Serikali ichukuwe jitihada za maksudi kuisaidia TANESCO ili ilipe hili deni au ilichukue hili deni ili TANESCO iwe na mtaji mkubwa kwa ajili ya uhimilivu wa shirika hili kuweza kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu umeme ni uchumi, umeme ni siasa na wananchi wanahitaji umeme, wanahitaji kuona siyo kuwaambia na Ilani yetu imewaambia tunakwenda kumaliza kupeleka umeme, sasa tukiwa bado shirika haliko imara hivi basi itakuwa ni changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao viongozi wazuri wamewekwa pale katika Wizara Waziri, Naibu Waziri na Wakurugenzi wote, kwa hiyo Serikali itawasaidia waweze kufanya kazi zao vizuri na hii itakuwa kipimo kwamba tutaona matokeo chanya haraka kwa ajili ya ufanisi wa nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache naomba kuunga mkono hoja asilimia 100 nikitegemea yale yote niyoyashauri yataenda kutekelezwa kwa ajili ya maslahi mapana ya Jimbo la Muhambwe, ahsante sana.