Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ameir Abdalla Ameir (2 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. AMEIR ABDALLAH AMEIR: Mheshimiwa Spika, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ametukutanisha hapa leo. Zaidi napenda kuwapongeza Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar ambao wamenipa imani kubwa na kunichagua kuweza kuliwakilisha Baraza katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nitakuwa mtovu wa nidhamu kama sitawashukuru wananchi wa Jimbo langu walionichagua wa Jimbo la Mwanakwerekwe. Ni mara yangu ya kwanza kuchangia humu ndani ndiyo maana natoa shukrani hizo.

Mheshimiwa Spika, niende katika mchango wangu na nitagusa mambo matatu. Kwanza nitagusia suala zima la historia ili watu wajue ni kwa kiasi gani huu Muungano una umuhimu katika maisha ya Watanzania kwa ujumla. Katika kipengele cha pili nitajaribu kueleza angalau mafanikio yaliyopatikana katika kila awamu; kuanzia awamu ya kwanza mpaka awamu ya tano ili pia tuone kwamba Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika suala zima la maendeleo ya kiuchumi linakua kwa hali ya juu.

Mheshimiwa Spika, katika historia mimi ni muumini wa faida kubwa zinazopatikana kutokana na Muungano huu. Naomba nitamke hilo wazi na sitatafuna maneno kwamba naziona faida kubwa zaidi na changamoto ambazo zinaelekea ukingoni katika kukamilishwa, kuratibiwa na kuondolewa kabisa. Nikianza katika historia yetu kidogo tu ni kwamba mahusiano ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar hayakuanza tarehe 26 Aprili, 1964 bali yalikuwa yameshajengeka tangu siku za nyuma. Kilele kile ilikuwa ni kuhitimisha tu lakini mahusiano ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar yalianza mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nieleze katika karne ya pili ambapo tulishuhudia biashara (commercial contact) ikifanyika baina ya Zanzibar na nchi zile za Uajemi kama Syria, Iraq, Iran ambao hawa sasa walileta bidhaa zao Zanzibar lakini zikifika Zanzibar zilikuwa zikiletwa maeneo ya ndani kwa Ndugu zetu huku Tanganyika tukishirikiana nao kwa pamoja. Kwa hiyo, hata suala la uchumi halikuanza leo; mashirikiano ya uchumi yalianza kipindi kirefu tangu siku za nyuma.

Mheshimiwa Spika, vilevile Profesa Felix Chami, Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam wakati anafanya utafiti wake wa ecological excavation katika eneo maarufu Zanzibar, Mkoa wa Kusini linaitwa Kuumbi Cave, naomba mnisikilize kwa makini sana Waheshimiwa Wabunge kuna jambo la msingi sana nataka kusema hapa; katika hili pango Profesa aliweza kugundua kwamba binadamu pale aliishi miaka 30,000 iliyopita.

Vilevile iliweza kugundulika mifupa ya wanyama kama twiga, pundamilia na nyati. Sasa kwa akili ya kawaida unajiuliza wanyama hawa wanapatikana Tanzania Mainland tu imekuwaje leo Profesa Chami katika utafiti wake akagundua wanyama wakubwa wakubwa walikuwa wanaishi maeneo ya Zanzibar. Hii ni kutokana na ile theory kwamba eneo lote hili lilikuwa moja lakini baadaye likatawanyika na likagawa visiwa vidogo vidogo vikiwemo vikubwa Zanzibar na vingine, nadhani jamani tumefahamiana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine Muungano huu wa Tanzanyika na Zanzibar naomba tuelewe kwamba ni wa kipekee sana ambapo ni nadra duniani kukuta Muungano umefanyika kwa siku 100 lakini Muungano wetu ulifanyika kwa siku 100 kama na siku 12 hivi kuonesha kwamba ulikuwa ni wa ridhaa, wa damu na wa udugu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, yalianza mashirikiano ya udugu, damu baadaye tukaja tukamalizia na suala la documentation. Msingi wa Muungano huu ni maridhiano na ridhaa na hiyari, kwa hiyo, ni vigumu sana kuona kwamba kuna siku Muungano huu utaweza kuvunjika, hilo jambo haliwezekani. Ni sawasawa na kusema mgonjwa wa akili achukue bunduki halafu apige mbu itawezekana wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nachotaka kuzungumza ni kwamba tumepata baraka kubwa kutokana na Muungano huu, tumepata heshima kubwa duniani kutokana na Muungano huu, miungano mingi imeshavunjika lakini huu bado unadumu na unaendelea na utaendelea. Tumeona mfano Muungano wa Syria na Misri, tumeona Sudan ambayo imekatika na kuwa na Sudan ya Kusini na Sudan ya Kaskazini; tuna mifano mingi kama hiyo. Mfano mdogo tu East Africa Community tulianza nayo lakini baada ya muda ili- collapse kidogo kwa changamoto mbili, tatu ambazo hazikuwa-handled vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana viongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba wanausimamia Muungano huu kidhati kabisa na tuna imani kubwa utadumu kwa maslahi ya pande zote mbili. Hakuna sababu hata moja ya mtu ambaye anatoka Tanganyika au Tanzania Mainland akamdharau mtu anayetoka Zanzibar Visiwani wala Zanzibar Visiwani akamdharau mtu ambaye anatoka Tanzania Mainland sote ni kitu kimoja.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, muda wako umeisha.

MHE. AMEIR ABDALLAH AMEIR: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja asilimia mia moja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. AMEIR ABDALLA AMEIR: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, Muumba Mbingu na Ardhi, ambaye leo ameniwezesha kupata afya njema nami kuwa miongoni mwa Wabunge watakaochangia hotuba hii ya bajeti ya mwaka 2021/2022. Napenda kumpongeza sana Rais, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan pamoja na Waziri wa Fedha na Naibu wake, kwa bajeti hii ambayo imeweza kupanga matumizi yake kwa kuyapa kipaumbele maeneo muhimu ambayo yanakwenda kukuza uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya hapo, bajeti hii haijaacha pengo hata moja. Hii ni bajeti ya wananchi, kwa maslahi ya wananchi na kwa neema ya wananchi wa Tanzania wote. Bajeti hii imegusa wananchi wote; imegusa wakulima, wavuvi, wajasiliamali, watu wa makundi maalum, walimu, waendesha bodaboda, akina mama kwa asilimia kubwa sana, mama ntilie na kadhalika. Kwa hiyo, naipongeza sana bajeti hii kwa asilimia kubwa sana na Inshaallah Mungu atatuweza kwamba Taifa letu la Tanzania litapiga hatua kubwa katika maendeleo ya uchumi katika sekta mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi nitachangia katika maeneo machache sana kwa sababu maeneo mengi Waheshimiwa Wabunge wameyazungumza kwa ufafanuzi mzuri na kutoa mapendekezo mazuri, na ushauri mzuri ambao una manufaa makubwa kwa Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mimi nitatoa ushauri nikijikita zaidi kwenye ongezeko la kodi katika suala zima la utalii wa watu wenye mahitaji maalum; vile vile nitaongea kuhusu suala la umuhimu wa kuwekeza viwanda vyetu hususan katika suala la mbolea na jambo lingine ni suala la ajira kupitia lugha sanifu ya Kiswahili na mwisho nitazungumzia kuhusu mahusiano mazuri baina ya sekta ya kilimo na sekta ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya utalii kuna jambo hatujaligusa kwa undani zaidi na tumeliacha kidogo, lakini kama Serikali italitilia mkazo na kulipa kipaumbele suala hili basi litasaidia sana kuongeza thamani na ongezeko la mapato katika utalii wetu. Nalo ni suala la kujikita katika utalii wa watu wenye mahitaji maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wenye mahitaji maalum sasa hivi duniani wanafika takriban bilioni tatu. Ni robo tatu nzima ya population ya watu duniani. Kwa maana hiyo, Serikali kama tutajikita zaidi huku, basi Tanzania itakuwa ni nchi ambayo inapokea watalii mbalimbali duniani katika kundi hili na kwa asilimia kubwa itaongeza thamani kubwa ya pato la nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kukibidhaisha na kufanya lugha ya Kiswahili kama ni sehemu ya ajira. Kiswahili kinapaa duniani; Kiswahili kinasomeshwa katika Vyuo Vikuu mbalimbali duniani hivi sasa, lakini cha kushangaza maeneo mengine, Wazungu kwa Wazungu ndio wanafundisha hicho Kiswahili kwa sababu sisi hatujapanua zile fursa za kufika katika hayo maeneo mbalimbali tukakieneza Kiswahili na walimu wetu ambao wanasomesha Kiswahili Tanzania kule Zanzibar na Tanzania Bara wakapata fursa hii kwa undani. Kwa hili sasa, namwomba sana Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi (ameshageuka) ambaye ni Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje, atutengenezee mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, samahani sana, nimekosea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Waziri anahusiana na mambo ya Nje, aweze kututengenezea mazingira kupitia balozi zetu ambazo zinatuwakilisha nchi za nje. Kila balozi atengeneze fursa za lugha ya kishwahili kwa watanzania jamani, naomba sana tusaidie sana kwa kila balozi hata kama hakuna mazinga hayo lakini atengeneze kuhakikisha kwamba walimu wanaofundisha kiswahili Tanzania wanapata fursa katika balozi zetu hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine napenda kuhangia katika sekta ya maendeleo ya kilimo na viwanda, hatuwezi kuendelea katika sekta ya viwanda bila ya kufanya mageuzi na mapinduzi ya sekta ya kilimo. Bajeti hii inakuja na mageuzi hayo, bajeti hii imeelekeza wakulima wazilishe kwa wingi mazao ya biashara na mazao ya chakula, tukizalisha kwa wingi mazao ya chakula kwa wingi, maana yake ni nini? Maana yake ni kwamba tutaongeza population ya idadi ya watu, na tukiongeza population na idadi ya watu maana yake tutakuwa na soko la uhakika la ndani ya nchi na bidhaa zetu zitauza ndani ya nchi na nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nilizungumzie katika suala la kuwekeza katika viwanda vya mbolea. Tanzania tumejaaliwa kuwa na aina ya madini fulani ambayo yanatumika katika kutengenezea hizi mbolea ambazo nchi nyengine hakuna, na madini haya tukiyatumiwa viwili ambayo yanatumiwa katika mikoa miwili tu, basi ni vyema tukawa na madini haya ambayo yanatuwezesha kuzalisha mbolea zetu sisi wenyewe, na kuondoa ule utegemezi mkubwa wa kuzalisha au kuagiza mbolea kutoka nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa na mbolea zetu wenyewe hapa nchini, basi sekta ya kilimo itakuwa na kuimarika kwa hali ya juu zaidi. Lingine niipongeze sana bajeti hii na Serikali kwa ujumla, kwa kuondoa tozo ya nyasi bandia, jambo hili linaisababishia nchi yetu kukuza sekta ya michezo, hususan mchezo wa mpira wa miguu, na leo hii nataka ni– declare interest, kwamba mimi ni mfuasi wa Simba tangu miaka 12. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa bajeti hii ya kaka yangu Mwigulu Nchemba, bajeti ya wananchi, kwa maslahi ya wananchi, kwa ajili ya wananchi, natangaza rasmi ni mwana Yanga rasmi. Natangaza rasmi kwamba i leo ni mwana Yanga rasmi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kwamba, aah! Ukitoa taarifa unanitatiza kidogo niache. Eneo lingine ni kwamba tuna miradi ya kimkakati na nashukuru kwamba mama bajeti imetuhakikishia kwamba hakuna mradi wa kimkakati hata mmoja utakaosita, miradi yote ya kimkakati itaendelezwa, namshukuru mama na naishukuru bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kushauri hapa katika miradi ya kimkakati, tuwekeze rasilimali watu ambao wataweza kuiendesha vizuri miradi hii, lazima tuhakikishe tunasomesha vijana wetu, na tunasomesha raia wetu wa Tanzania katika zile sekta au taaluma ambazo zina ugumu ndani yake, ili kupunguza utegemezi wa kuajiri wataalam kutoka nje ya nchi mara kwa mara, na tuwe na waalamu wetu kwa asilimia zote ikiwezekana kama siyo asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache naipongeza sana naiunga mkono bajeti hii na ninaimani leo na mimi nitaalikwa chako ni chako, ahsante sana. (Makofi)