Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Bakar Hamad Bakar (1 total)

MHE. BAKAR HAMAD BAKAR aliuliza: -

Je, ni kwa kiwango gani bahari zinachangia kukua kwa uchumi kupitia uvuvi?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bakar Hamad Bakar, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Uvuvi hutoa mchango katika uchumi wa nchi kupitia uzalishaji wa bidhaa na huduma mbalimbali zinazozalishwa ndani ya sekta. Aidha, baadhi ya bidhaa na huduma zinazozalishwa hutumika kama mali ghafi katika uzalishaji ndani ya sekta nyingine kama vile viwanda na kuwa na mchango mkubwa zaidi katika sekta hizo. Katika mwaka 2022, sekta ya uvuvi ilichangia asilimia 1.8 ya Pato la Taifa huku ikikua kwa asilimia 1.9.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka 2022/2023, mazao ya uvuvi kutoka baharini yalichangia jumla ya tani 54,823 sawa na asilimia 10.6 ya mazao ya uvuvi ambayo ni tani 513,525. Vilevile, maduhuli ya Serikali ya shilingi bilioni 1.8 yalikusanywa kutoka katika shughuli za uvuvi baharini. Kiasi hicho cha mazao ya uvuvi kilichozalishwa kutoka baharini kilitokana na uvuvi mdogo na kilikuwa na thamani ya shilingi bilioni 356.3. Naomba kuwasilisha.