Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Bakar Hamad Bakar (12 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, kwa kutuamsha na kutufikisha hapa na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Pia kwa vile, ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge lako hili, naomba nichukue fursa hii kuishukuru Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, kwa kunipigia kura za kishindo na kushinda kuja kuliwakilisha Baraza hapa kwenye Bunge hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije kwenye kuchangia Hotuba hii ya Wizara ya Muungano na Mazingira. Kwanza nianze kuwapongeza Waziri na Naibu Waziri kwa kuwasilisha Hotuba yao hii. Hotuba ambayo imesheheni mambo mazuri kwa mustakabali wa mazingira lakini kwa muungano wetu tukufu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye hoja moja kwa moja kwenye masuala haya ya Muungano. Tarehe 17 Oktoba, 2020 Kamati zetu zile za Muungano kwa maana ya SMT na SMZ zilitiana saini kuziondoa hoja (5) za Muungano.

Mheshimiwa Spika, hoja hizi ya kwanza ilikuwa ni ushirikishwaji wa Serikali ya Zanzibar kwenye masuala ya Kimataifa na Kikanda. Lakini ushiriki wa Zanzibar kwenye masuala ya Afrika Mashariki, lakini pia ni uchimbaji na utafutaji wa mafuta na gesi asilia. Lakini pia, kuna jambo kubwa la gharama za mizigo kwa mizigo ile inayotokea Zanzibar kutua katika Bandari ya Dar es Salaam. Mambo haya ni mambo mema sana lakini yanabakia kwenye makaratasi. Kwa nini tunaona aibu, tunaona haya kuweza kuwaelimisha wananchi kufahamu mambo haya? Kufahamu kwanza, kabla ya kuondolewa changamoto hii ilikuwaje? Na baada ya kuondolewa kuna umuhimu gani na changamoto hii sasa ikoje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la gharama za mizigo inayotoka bandari ya Zanzibar kuja bandari ya Dar es Salaam bado kwenye jambo hili kuna changamoto. Pamoja na kuondolewa hoja hii, hatujui kwamba, labda pengine ni suala la elimu, ama ni jambo gani hasa? Lakini kuna changamoto kubwa ambayo inasababishwa, inawezekana na TRA au sijui ni Taasisi gani pale ambayo inahusika na mambo hayo lakini sana sana nadhani ni TRA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwananchi mmoja mmoja anaondoka na mzigo wake mmoja pengine ni TV moja, anatoka nayo Zanzibar anakuja nayo Dar es Salaam akifika pale baada ya kutoa kodi Zanzibar anakuja tena kutoa kodi nyingine pale. Jambo hili naomba liangaliwe tena upya, kama ni jambo ambalo limeshaondolewa kwenye changamoto kwenye hoja hizi za Muungano lielimishwe limeondolewaje? Likoje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunavyofahamu sisi ni kwamba, kwa mizigo ile inayotoka nje kwa mfano, labda magari Zanzibar ikifika inachajiwa asilimia 40 ya Tax. Lakini yanaposafirishwa huku Bara yanamaliziwa difference ambayo ni asilimia 60 lakini je. kwa mizigo hii midogo midogo hali ikoje? Naomba sana Waziri na Naibu Waziri waelimishe jamii, wawaelimishe watanzania kuhusu masuala haya, bado kuna changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ni ucheleweshwaji wa kuwekwa saini mikataba ya Kimataifa ambayo sana sana inahusu Zanzibar. Kwa mfano, ujenzi na ukarabati, kwanza kuna ukarabati wa Hospitali ya Mnazimmoja kule Unguja. Jambo hili limefadhiliwa na Saudia Fund, lakini mpaka leo bado haujulikani mustakabali wa jambo hili ukoje? Lakini kuna ujenzi wa barabara kubwa ambayo inatoka Chakechake-Pemba mpaka Wete, mpaka leo kila siku tunaambiwa tu kesho, kesho! Jambo hili kwa kweli linanisononesha. Nakuomba sana, namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atueleze jambo hili limefikia wapi? Na ni lini hasa jambo hili litaondolewa, litatatuliwa na barabara ile ya Chakechake-Uwete itapata ufumbuzi na kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie jambo moja. Kuuenzi, kuutunza na kuuthamini Muungano wetu ni pamoja na kuwathamini viongozi wa Muungano huu. Dkt. Omar Ali Juma alikuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini ukienda katika Kijiji chake kinasikitisha. Kwanza, kwenye kaburi lake ambalo amelazwa pale, utasikitika sana. Barabara ambayo inaunganisha kutoka barabara kubwa mpaka kufika kwenye kaburi lake ambayo pia barabara hiyo inaunganisha kwenda kwenye shule ambayo ipo kwa jina lake yeye Dkt. Omar Ali Juma barabara hiyo ni chakavu haipitiki. Tunaomba Serikali ilione jambo hili na ithamini kiongozi huyu amefanya kazi kubwa kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namuomba sana Waziri atakapokuja hapa aeleze ni mpango gani uliopo kwenye kuthamini mchango wa Dkt. Omar Ali Juma nakushukuru sana. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii kuweza kuchangia hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Tangia asubuhi leo hapa zinazungumzwa barabara tu hapa, lakini bahati nzuri nitahama kwenye eneo hilo la barabara nitakwenda kuchangia kuanzia haya ya 225 mpaka haya ya 227 ambapo inazungumzwa mamlaka ya hali ya hewa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge la kumi na moja lilipitisha Sheria Na. 2 ya mwaka 2019 Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania, ni matarajio ya Bunge hili pamoja na Taifa kuona kwamba sheria ile inakwenda kuleta tija kwa Taifa lakini tija kwa mamlaka hii ya hali ya hewa Tanzania. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri tangia kupitishwa kwa sheria ile Sheria Na. 2 je ni mafanikiko gani yaliyopatikana kwa Taifa ama kwa mamlaka hii mpaka leo hii 2021? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumza haya kwa sababu kwenye sheria ile Na. 2 wapo wadau mbalimbali ambao wametajwa kwenye sheria ile bandari ni mdau wa hali ya hewa aviation ni mdau wa hali ya hewa mazingira, viwanda watu wa nishati barabara majanga kilimo afya sayansi na teknolojia wote hawa ni wadau wa hali ya hewa hasa namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja atuambie je wanaitumiaje wadau hawa sheria ili Na. 2 ya mamlaka hii ya hali ya hewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba sheria haiwezi kutumika ipasavyo kama haijatengenezewa kanuni, lakini tangia mwaka huo ambapo sheria hii ilipitishwa lakini mpaka leo hakuna kanuni ambazo zinaiongoza kuifanya sheria ile iende ikatumike inavyopaswa. Sasa tunamuomba Mheshimwa Waziri atakapokuja atueleze je kanuni za Sheria Na. 2 ya mwaka 2019 imefikia wapi? imekwamwa wapi? tatizo ni nini kwamba mpaka leo kanuni zile hazijapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tuna bahati tumepata bahati ya kuwa na chuo kinachotoa taaluma ya hali ya hewa kwa nchi za Afrika ni nchi chache sana zenye bahati zenye vyuo ambavyo vinatoa taalum hii. Kwa nchi za Afrika nchi za SADC na hasa nchi za Afrika Mashariki ni nchi chache sana tulitegemea sana kwamba chuo hiki kingeweza kuitangaza Tanzania, lakini kingeweza pia kuongeza mapato ya mamlaka lakini pia kuitangaza Tanzania kupitia taaluma hii ya hali ya hewa. Lakini hatuoni kwamba kuna mikakati ipi ya kukifanya chuo hiki kuwa tija na kuitangaza Tanzania kuongeza mapato ya nchi yetu lakini kuongezea mapato ya mamlaka ya hali Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, endapo tutakiwezesha chuo hiki kimiundombinu naamini kwamba mapato ya mamlaka ya hali ya hewa yataboreka na maslahi yatakuwa mapana zaidi na tija kwa Taifa itakuwa pia itaongezeka. Namuomba waziri atakapokuja atuambie ni mikakati ipi aliyonayo kwenye kukiboresha chuo hiki cha mamlaka ya hali ya hewa ambapo kipo pale Kigoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utakubaliana nami kwamba kipindi hiki tulichonacho ni miaka ijayo ambapo majanga yanatokana na hali mbaya ya hewa taasisi hii ya mamlaka ya hali ya hewa ni taasisi muhimu sana kwa Taifa letu na kwa dunia. Umuhimu wa taasisi hii umeonekana zaidi hata hapa kipindi cha karibuni niipongeze sana Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niipongeze mamlaka hii kipindi cha jaribio cha kimbunga cha jobo walikuwa wanatuhabarisha mara kwa mara bila ya habari zile nchi ingekuwa ipo katika wasiwasi sana watu walikuwa na wasiwasi na mali zao lakini watu walikuwa na wasiwasi na maisha yao lakini kupitia mamlaka hii tulikuwa tunapata taarifa za mara kwa mara na ile presha ilikuwa inashuka kila time ambapo ilikuwa inakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamuomba sana Mheshimiwa Waziri atueleze ana mikakati gani ya kuboresha maslahi ya wafanyakazi hili wafanyakazi wale waweze kufanya kazi zao kwa utulivu na moyo zaidi wa kujitolea. Sasa hivi kumekuwa na wafanyakazi wengi wa mamlaka hii wanatoroka kwa maana wanakimbia wanakimbilia sehemu nyingine ambazo taasisi ambazo zina maslahi zaidi. Lakini pia kuna wafanyakazi ambao wamepewa barua za kupandishwa madaraja tangia 2016 mpaka leo hii 2021 barua zile zinabakia kuwa ni hewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamuomba waziri atakapokuja atueleze ni kwa nini na lini maslahi ya wafanyakazi ni lini madaraja ya wafanyakazi pale ambao wana muda mrefu awajapandishwa madaraja ni lini sasa watapandishwa madaraja lakini ni lini barua zile zitajibiwa tangia 2016 mapaka leo 2021 watu wamepewa barua ya kupandishwa madaraja lakini hadi sasa hakuna kilichofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia tunafahamu taasisi hii ni taasisi ya muungano kama ilivyo sasa namuomba sana Mheshimiwa Waziri naiomba pia Serikali inapoajiri ajira hizi za taasisi ya muungano iangalie zaidi pande zote mbili, za muungano ile ratio ya 79 kwa 21 ianze kutekelezwa hasa kwenye taasisi hizo za muungano. Sasa hivi tunazungumza kwamba kuna ratio 79 kwa 21 maana zile ajira za muungano kwa Tanzania bara zitakuwa ni 79 asilimia lakini kwa Tanzania visiwani itakuwa ni asilimia 21 naomba sana tutakapo ajiri taasisi hizi za muungano basi tutumie hii ratio ili kuweza kuweka usawa kwenye ajira za taasisi zetu za muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya kusema hayo nikushukuru sana ahsante sana. (Makofi)

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia hotuba hii ndani ya Bunge hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, aliyenipa uhai na uzima leo hii kuweza kusimama ndani ya Bunge hili la kuweza kuchangia hotuba hii nzuri ambayo ni very participative ambayo imeshirikisha mawazo ya Wabunge wote katika Bunge hili, wale ambao walichangia kwenye hotuba mbalimbali za kisekta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Mwananchi, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba kwa uwasilishaji wake mzuri wa hotuba hii. Lakini pia nimpongeze Naibu Waziri wake kwa msaada mkubwa sana kwenye uwasilishaji wa hotuba hii. Sambamba na hilo niwapongeze timu yao yote; Makatibu Wakuu na Manaibu wao, kuweza kusaidiana kuweza kuiandaa na kuiwasilisha hotuba hii nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba hii ni hotuba ya kwanza kwa Serikali hii ya Awamu ya Sita. Nimpongeze mama yetu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama Samia Suluhu Hassan, kwa majibu mengi sana ya Watanzania, hususan wanyonge kupitia hotuba hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba hii imejibu majibu mengi sana, changamoto nyingi sana za wananchi kwenye majimbo yetu kupitia Wabunge wengi ambao walichangia, nikiwemo mimi mwenyewe. Niliweza kuchangia suala la gharama za mizigo inayotoka Zanzibar kuja Bandari ya Dar es Salaam wakati nachangia hotuba ile ya Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili limepatiwa ufumbuzi, na nimpongeze sana mama yetu, Samia Suluhu Hassan, tuko pamoja. Nawaomba sana wenzangu, Wabunge na wananchi tuendelee kumtakia dua, Mungu amlinde, ampe afya njema ili aendelee kutujengea nchi yetu hii kwa uchumi endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii imebeba dhima kubwa ya uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu. Hatuwezi kujenga uchumi shindani ambao utakuwa na viwanda na kwa faida ya maendeleo ya watu kama hatujajenga mazingira rafiki kwa wawekezaji wa ndani na wa nje kuja kuwekeza ndani ya nchi yetu. Ukiangalia sasa hivi mazingira yaliyopo hatuwezi kusema kwamba ni mazingira rafiki kwa wawekezaji kuja kuwekeza ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunataka kuwekeza katika uchumi wa viwanda na uchumi shindani, ni lazima tupunguze suala la riba. Riba kwenye benki zetu ni kubwa, Waheshimiwa Wabunge wengi wamechangia jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na tunampongeza na kumshukuru mama yetu Samia, juzi naye pia amelizungumza jambo hili. Lakini pia Naibu Waziri wakati una-wind up ile hotuba yako ya Wizara ya Fedha ulilizungumza jambo hili na ukasema kwamba mna nia ya kukutana na Benki Kuu pamoja na wadau wote wa benki kuweza kuangalia namna ya kupunguza riba hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu ambao tunashindana nao wkenye viwanda riba zao ziko chini. Sisi bado riba yetu iko juu sana. Hatuwezi kwenda kushindana nao kama hatujaweza kuondoa jambo hili, kama hatujaweza kupunguza riba hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la urasimu; wanapokuja investorswaliomo ndani au walioko nje wanaokuja hapa, bado kuna suala la urasimu, mara pale mara hapa mara huku, anapoona hivyo investor anaondoka na fedha zake anakwenda kuwekeza maeneo mengine, nchi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawaomba sana, tunaiomba sana Serikali, tunaiomba sana Wizara iondoe suala hili. Ikiwezekana basi iweke one stop center ili anapokuja investor basi iwe ni rahisi kwake kufuata zile procedures za kinchi na kuweza kuwekeza. Wanapowekeza hawa wanatuletea faida nyingi sana kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la malighafi. Viwanda hivi ambavyo vinawekezwa ni lazima viwe na malighafi ya kutosha. Ni lazima twende kama Serikali tukawaelimishe na kuwahamasisha wananchi, hususan katika suala la kilimo maana malighafi nyingi zinatokana na kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunaomba sana Serikali ijiwekeze kwenye kuwawezesha na kuwajengea mazingira bora na rafiki, hususan vijana, kwenda kwenye sekta ya kilimo na kujiandaa kwenye malighafi za viwanda hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna uchumi wa buluu (blue economy). Kule Zanzibar, Dkt. Hussein Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kwenye hotuba yake ile ya fedha ya mara hii, amejielekeza katika uchumi wa buluu. Na hii ndiyo agenda kubwa sana kule Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana jambo hili tulibebe kwa sababu bahari ndilo eneo kubwa sana ambalo limezunguka ndani ya nchi yetu. Naomba sana tuwe na dhamira thabiti ya kuliendea suala hili la uchumi wa buluu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona kwenye bajeti kuna target ya kununua meli nne zinazokwenda kwenye deep sea. Naomba sana jambo hili tulianze kwa kutenga fedha zetu za ndani, tusitegemee misaada kutoka nje kuja kutuletea meli hizi, tuanze sisi. Mimi naamini kwamba kwa dhamira ya Serikali tuna uwezo wa kufanya jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeweza kununua ndege 11, tunashindwaje sisi wenyewe kununua meli za kwenda kwenye deep sea. Naamini kama tuna dhamira kweli ya dhati ya kwenda kwenye uchumi wa buluu, hatuwezi kushindwa kununua meli zetu sisi wenyewe na kwenda kwenye uchumi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usimamizi wa matumizi ya fedha; hapa tunajadili matumizi haya ya fedha, tunajadili kupitisha bajeti hizi, lakini jambo kubwa sana ambalo tunalipitisha halitaonakana na maana kama hatuendi kusimamia fedha hizi ambazo tunazipitisha hapa. Nashauri kwamba kuwe na chombo cha tathmini na ufuatiliaji, Wizara ya Fedha iwe na chombo hiki ambacho kinaifuatilia miradi yote wakati wa utekelezwaji wake ili kuona kwamba fedha hizi tunazozipitisha zinakwenda kuzingatia nidhamu ya fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana kuna vitu viwili tofauti; kuna nidhamu ya fedha, lakini kuna namna ya kuweza kuitumia fedha kwa mujibu wa taratibu na sheria. Watu wetu wa procurement walioko huko kwenye maofisi wanajaribu kutumia sheria na taratibu lakini hawazingatii nidhamu ya matumizi ya fedha. Naomba sana Serikali twende tukazingatie nidhamu ya matumizi haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukienda kwenye maofisi unaweza ukakuta kwa mfano kitu cha kununua 500 kimenunuliwa shilingi 1,500, mara tatu au nne ya bei halisi. Tunaomba sana twende tukazingatie nidhamu ya fedha na thamani halisi ya fedha hii ambayo tunaipitisha. Tutakapofanya hivyo, naamini tutapiga maendeleo kwa hatua kubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba atakapokuja Waziri hapa anipe ufafanuzi kuhusu jambo la punguzo hili la PAYE kwa wafanyakazi. Kule Zanzibar wafanyakazi wa Muungano ambao wanafanya kazi kule mapato yale yanakwenda kwenye Serikali ya Zanzibar. Hata hivyo tunaona kwamba hakuna utofauti baina ya mwaka jana na mwaka huu; mwaka jana tulipeleka kule bilioni 21, ikiwa ni PAYE za wafanyakazi wa Muungano walioko kule, lakini mwaka huu pia tunaona kima ni kilekile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najiuliza, na hapa naomba pia nipate ufafanuzi, kwamba je, wafanyakazi kwa maana ya watumishi wa Muungano, kule Zanzibar hawajaongezeka? Au hawapandi madaraja, au labda kima cha mshahara hakipandi? Tatizo hasa ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba mwaka jana ni bilioni 21, lakini hata mwaka huu ni bilioni zilezile 21; tatizo hapa ni kiyu gani. Je, zimebakia pale kwa sababu ya punguzo la asilimia moja au tatizo ni lipi? Naomba pia hapa atakapokuja Waziri atupe ufafanuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri sana Serikali na Wizara za Muungano na zile ambazo siyo za Muungano ziendelee kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja. Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Jamahuri ya Muungano tukifanya kazi kwa pamoja naamini tutapunguza gap kubwa sana la maendeleo katika maeneo yetu haya mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano yapo maeneo ambayo Tanzania Bara yako juu lakini kule Zanzibar bado wapo chini, lakini kuna maeneo ambayo kule Zanzibar tumepiga hatua lakini huku bado.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kule Zanzibar tuna posho za wazee, huku bado jambo lile halijatekelezeka. Kwa hiyo tukishirikiana naamini tunaweza tukapeana mawili matatu tukajua kwamba na huku tunaweza kulitekeleza jambo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la gharama za kuunganisha, huku ni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Bakar kwa mchango wako mzuri.

MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ninakushukuru siyo tu kwa sababu ya kunipa nafasi hii, lakini pia kwa namna bora ambavyo unaongoza Bunge hili kwa hekima na busara nyingi sana. Kwa hiyo, nikupongeze sana na nikushukuru sana kwa namna bora ambavyo unaongoza Bunge letu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninampongeza na ninamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa namna anavyoendelea kutupigania Watanzania na maendeleo ambayo anaendelea kutuhangaikia na tunavyopiga hatua hizi za kimaendeleo. Bajeti hii ambayo iko mbele yetu ni bajeti ambayo inaenda kutatua changamoto za Watanzania, inaenda kumgusa kila Mtanzania. Bajeti hii imewagusa wamachinga, bajeti hii imewagusa wakulima, bajeti hii imewagusa watumishi wa umma, lakini bajeti hii imeyagusa makundi yote, vijana, walemavu, wanawake, hata wanamichezo bajeti hii haiwaacha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunasema kwamba, bajeti hii imekuja katika right time, lakini pia ni bajeti ambayo inaenda kutatua changamoto za Watanzania. Nikupongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha, wewe na timu yako, kwa namna ambavyo umewasilisha na umeandaa bajeti hii nzuri sana kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja ya industry ambayo inakua kwa kasi ya kiuchumi sasa hivi duniani ni Islamic Financing System. Islamic Financing System sasa hivi inakadiriwa taasisi karibia 400 duniani tayari zinafuata mfumo wa Islamic Financing duniani, lakini pia inakadiriwa ukuaji wa system hii kwa mwaka ni karibia asilimia 20 kwa mwaka, lakini na nchi nyingi ambazo sasa hivi zinatumia siyo tu zile nchi za kiislamu, lakini hata nchi ambazo siyo za Kiislamu zinatumia mfumo huu. Ukienda South Africa wanatumia Islamic Financing System, ukienda UK, ukienda Nigeria na nchi za Afrika nyingi hata Kenya wanatumia mfumo huu, lakini kwetu sisi Tanzania bado hatujaweza kuu-recognize mfumo huu uweze kutumika katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, bado tunahitaji kufanya mabadiliko kwenye sheria zetu. Kwa mfano, Banking Act, hii inatakiwa pia ifanyiwe marekebisho ili kuutambua mfumo wa Islamic Financing ili uweze kutumika Tanzania kwa sheria, pia tufanye marekebisho kwenye Insurance Act ili pia iweze kutambua takaful kama ni Islamic Insurance ambayo inakwenda kutatua matatizo mbalimbali yanayohusiana na insurance za kiislamu, pia tunahitaji tufanye mabadiliko kwenye capital market and security ili kuweza kutambua Islamic bond ambayo inaitwa sukuk ambayo itawawezesha wawekezaji wengi ambao hawatumii mifumo iliyoko sasa, wanatumia mifumo ya Kiislamu kuja Tanzania kupiga hodi na kuweza kuwekeza kwa bond hizo ambazo na zikonchi nyingi ambazo zinatumia Islamic Bond kuweza kutekeleaa miradi yao mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda Nigeria wanatumia mfumo huo, ukienda UK pia wanatumia mifumo hii ya Islamic Bond ambayo ni Sukuk, lakini Tanzania bado hatujaweza kuitambua mifumo hii kisheria. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri tuende tukapige hatua.

Mheshimiwa Spika, siyo kwamba tunakwenda kulitekeleza jambo hili from nowhere, kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, ukienda Ibara 159 (f) imezungumzia juu ya mifumo ya Islamic Finance na CCM imeahidi kwamba, ifikapo 2025 jambo hili tayari litakuwa limeshafanyiwa kazi. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, nakupongeza sana kwa sababu umeshapiga hatua kwenye bajeti yako hii umeweka, umefanya amendment kwenye TRA Act ile ya mwaka 2008 tayari kuna kipengele umekiweka pale, lakini kile kipengele bado hakijatosha. Financing System ina faida kubwa sana kwa Tanzania, lakini pia ina faida kubwa sana kwa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna hofu sana kwenye jambo hili na Watanzania wengine wanahofu kwamba, aah, kwa nini Islamic System? Islamic System hizi benki ni huduma kama huduma nyingine. Ukienda kwa Tanzania tunazo system za kidini ambazo zinafanya kazi bila ya ubaguzi na zinatumika kwa watu wote. Ukija tuna shule mbalimbali za kikristo, tuna shule pia za kiislamu, lakini tunasoma kwa pamoja bila ya kubaguana. Pia, tuna hospitali na vituo vya afya mbalimbali ambavyo ni vya kidini, tunaenda kutibiwa kwa pamoja bila kubaguana kidini. Hii pia ni huduma kama huduma zingine na watatumia watu wote au yule ambaye anahitaji na ambaye hahitaji halazimiki kutumia huduma hii. Ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri kwa sababu 2025 tutaenda kuhojiwa na Watanzania kwamba, kwa nini hatukutekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwenye jambo hili. Nikuombe sana tuende tukalitekeleze jambo hili kama ambavyo limeahidiwa na Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa nini sasahivi mifumo hii inakwenda kwa kasi sana? Ni kwa sababu ya faida zinazopatikana kwenye products ambazo zinazalishwa kwenye Islamic Banking. Kwa mfano, miongoni mwa products ambazo zinazalishwa kwenye Islamic Banking ni product ambayo inaitwa Mudharaba. Mudharaba ni product ambayo benki wanampa mtaji mteja anaenda kufanya biashara, lakini kwa kugawana faida. Product kama hii ipo kwenye conventional bank kwa maana wao wanapewa mkopo, wakishapewa mkopo wanachokijua wao ni riba na marejesho ya mkopo ule. Hawashughuliki na biashara yako wanavyofanya, vyovyote itakavyokuwa, umepata hasara, umepata faida ni wewe mwenyewe, lakini mudharaba ambayo ni product ya Islamic hii benki na wewe, benki na mteja wanashughulika pamoja kwenye biashara yako na mwisho mnagawana faida.

Mheshimiwa Spika, endapo imetokea hasara kwenye biashara yako hiyo, haulazimiki kulipa isipokuwa kwamba, isiwe negligence ya kwako wewe kama mteja, lakini kama imekwenda vizuri biashara kwa misingi ambayo mmekubaliana na benki na haikutengeneza faida, hulazimiki kulipa. Leo ukiangalia mifumo yetu ya conventional kama hukwenda kulipa ama watakuja kukufilisi au watakupiga mnada yale ambayo umeweka kama dhamana ya mkopo wako, lakini kwenye Islamic Banking haipo hivyo, kama umepata hasara, ukipata faida mnagawana na benki na hiyo ni moja katika product. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini zipo products nyingi. Kuna mudharaba, kuna musharafa, lakini pia kuna murahaba, ziko nyingi sana. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri jambo hili tulifanyie kazi na tulifanyie kazi kwa wakati na kwa haraka sana.

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye suala la ushirikiano au ushirikishwaji wa taasisi zetu za Serikali zote mbili; ziko taasisi za Zanzibar ambazo sasahivi zinafanya kazi zake huku Tanzania Bara. Kwa mfano tunayo taasisi ya ZIC, Zanzibar Insurance Company, lakini pia tunayo PVZ ambayo pia inafanya kazi huku tunakuomba sana Serikali kwa pamoja tuendelee kushirikiana na taasisi hizi, bado mashirikiano ya taasisi hizi kwa taasisi ambazo ziko Bara ni madogo sana. Kwa hiyo, nikuombe sana na niiombe sana Serikali tuongeze ushirikiano kwenye taasisi zetu hizi za Zanzibar kwa sababu zote hizi ni taasisi za Serikali na zinamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100 kwa hiyo, hatuna haja ya kuziwekea hofu au kuzijengea hofu. Tuzitumie taasisi hizi kama ni taasisi zetu za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie jambo moja, kuna suala la Foreign Currency Exchange Market. Ni jambo ambalo limefungiwa sasa kwa muda mrefu na sasa hivi huduma hii inahitajika sana. Mama Samia amekwenda mbio sana amefanya Royal Tour kutangaza utalii, watalii watakuja na wameanza kuja, kwa hiyo, tunaziomba hizi taasisi za foreign exchange kwa maana ya Bureau De Change zirudi na zirudi katika masharti ambayo siyo yale kandamizi kama ambavyo yako sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano eneo maalum la Zanzibar, kumuwekea mzanzibari mtaji wa Bilioni Moja ndiyo aanzishe taasisi hii ya Bureau De Change kwa kweli, si jambo rahisi kwa wazanzibari kwa mujibu wa uchumi ambao tukonao bilioni moja ni hela nyingi sana hatuwezi tukapata hata kampuni moja ambayo itaweza kufungua, itakidhi sharti hili la kuweza kufungua hii Bureau De Change kwa Zanzibar. Kwa hiyo, nikuombe sana masharti haya yalegezwe, hasa kwa upande wa Zanzibar, kwa kweli Bilioni Moja ni nyingi sana kuweza kufungua Bureau De Change kwa upande hasa wa Zanzibar.

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii, ninaunga mkono hoja hii, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili kuweza kuchangia ripoti hizi za Kamati tatu ambazo zimewasilishwa ndani ya Bunge letu leo asubuhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehma; ambaye ametuwezesha kuwa wazima na afya njema na kuweza kukutana hapa katika kutekeleza majukumu yetu mbali mbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ripoti hizi ambazo zinasomwa na hoja hizi ambazo tangu asubuhi leo zinaendelea kutolewa hapa zinaonyesha mapungufu mbalimbali yaliyomo ndani ya Serikali yetu. Si kwamba Serikali yetu haifanyi kazi, tunaamini kwamba Serikali yetu inafanya kazi nzuri na mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anafanya kazi nzuri sana. Tunaendelea kumpongeza na kumtakia afya njema ili anendelee kuwatumika Watanzania kwa umakini sana na kuendelea kutekeleza miradi mbalimbali ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia dosari hizi ili Serikali yetu iendelee kufanya kazi vizuri zaidi; iendelee ku-perform na iendelee kukusanya fedha za umma na kusimamia fedha za umma ili kuweza kutekeleza miradi kwa kasi na pia, kuwatumikia Watanzania kwa weledi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mapungufu mbalimbali ambayo yamebainishwa na ripoti za CAG; nami nitazungumzia machache. Kwanza nitaanza kwenye bohari ya dawa (MSD). Tarehe 12 Oktoba, ya mwaka 2021 MSD iliingia mkataba na kampuni ya Misri ya Alhandasya. Mkataba na kampuni hii ulikuwa ni kwa ajili ya kusambaza dawa na vifaa tiba kwa items 75.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkataba uliingiwa tarehe 12 mwezi wa kumi, lakini malipo kwa ajili ya kazi hiyo yalifanyika siku moja kabla ya mkataba kuingiwa. Kwa maana tarehe 11 Oktoba MSD walimlipa Alhandasya bilioni 3.4 advance payment kwa ajili ya kazi hiyo. Tunaona hapa kwanza tu kuna jambo huko mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Alhandasya Kampuni ya Misri, kampuni hii ilishindwa kutekeleza jukumu lake wakati tayari imeshalipwa 3.4 bilioni, na ikatoweka na fedha hizo mpaka leo fedha hizi hazijulikani ziko wapi na hawa Alhandasya hawajulikani hata walipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, MSD walipofuatilia, Alhandasya kule Misri kupitia mabalozi wetu kule walishindwa kuipata kampuni hii. Kwa maneno mengine ni kusema kwamba kampuni hii ilikuwa ni kampuni hewa; kwa maana haipo na fedha hizi za umma zaidi ya bilioni 3.4 zimelipwa na zimepigwa, hazipo tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mchato huo na Alhandasya kushindwa kutekeleza majukumu yake MSD walimpata mkandarasi mwingine; kampuni nyingine ambayo inaitwa EIPICO ambapo yeye alikubali kuweza kusambaza vifaa tiba na kupewa mkataba mwingine wa kuweza kufanya kazi na MSD. Hapo ndipo na yeye alipopewa mkataba wa bilioni 10.8 kuweza kusambaza vifaa mbalimbali kwa makubaliano kwamba ataanza kusambaza vifaa ambavyo alipewa Alhandasya; ambazo zilikuwa ni item 75. Ndani ya item hizo 75 kwa mkataba huo, pia na yeye huyo EIPICO alisambaza item 12 kwa fedha ileile ya 3.4 bilioni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona haya ni mapungufu makubwa na madhaifu makubwa ndani ya Serikali yetu. Tunaiomba sana Serikali iweze kusimamia mikataba hii na iweze kufanya kazi hizi kwa ufanisi mkubwa. Hizi fedha ni nyingi sana kwa ajili ya kuweza kuwatumikia Watanzania. Tunazo shida na changamoto nyingi sana, sasa unapoona mambo haya yanatokea ndani ya Serikali, ni kuitia doa Serikali yetu na ni kumtia doa Mheshimiwa Rais wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais wetu ana nia ya dhati ya kuwatumikia Watanzania lakini mambo haya ambayo yanatokea ni mambo ambayo yanendelea kumtia doa Mheshimiwa Rais wetu. Tunaiomba sana Serikali isimamie mikataba, isimamie fedha za umma kama vile Bunge linavyotaka, kama vile Bunge lilivyoidhinisha fedha hizi ndani ya bajeti ambayo inaendelea na tumeipitisha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi ambazo zililipwa, zililipwa kinyume na taratibu. Kwanza, hakukuwa na dhamana kutoka kwa benki ambayo ililipwa lakini pia, hakukuwa na dhamana ya utendaji kazi wa hizo kampuni ambazo zimelipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo yanatokea hapa hapa Tanzania na hawa hawa Watanzania ambao wanalalamika ndio hao hao ambao wanamkwamisha Mheshimiwa Rais wetu. Kwa hiyo, tunaomba sana kuweza kufanyika marekebisho makubwa ndani na kusimamia fedha hizi za umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye jambo lingine. Kuna nakisi ya ukusanyaji wa kodi wa zaidi ya bilioni 887 ambazo hazikukusanywa kutokana na mambo mbalimbali na changamoto mbalimbali zilizoko pale TRA na kila siku tunakuwa tunapiga kelele kuhusiana na mifumo ya ukusanyaji na usimamizi wa fedha za umma zilizopo pale TRA…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba sana Serikali, fedha hizi ni nyingi sana. Kwa mfano kuna mafuta ambayo yaliingizwa nchini kwa ajili ya kusafirishwa kwenda nchi nyingine lakini mafuta hayo hayakusafirishwa kwenda nchi nyingine na badala yake yalitumika ndani ya nchi na kuisababishia Serikali kukosa kodi stahiki kwenye mafuta hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo yanatokea hapa na sisi tupo na wasimamizi wa mambo haya Maafisa Masuuli wapo. Kwa hiyo tunaiomba sana Serikali iweze kurekebisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato na kuweza kusimamia zaidi ukusanyaji wa mapato ndani ya nchi yetu ili kuweza kufanikiwa zaidi kwenye utekelezaji wa majukumu yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mchakato wa ajira BOT. Pia ni moja kati ya mambo ambayo CAG alibainisha, BOT walitangaza ajira kwa utaratibu wa kawaida na Watanzania walio wengi ambao wana sifa ya kuomba ajira zile, waliomba, lakini cha kushangaza ni kwamba baadaye katika mchakato baada ya Watanzania kuomba, katikati ya mchakato walibadilisha sifa huko ndani kinyume na utaratibu, kinyume na sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu na sheria inasema kwamba, ajira kwa maana ya Watanzania wanatakiwa kuajiriwa chini ya miaka 45, lakini BOT walikwenda kubadilisha hiki kipengele cha umri kutoka miaka 45 wakasema mwisho miaka 30. Tunajiuliza ni kwa nini kipengele hiki cha umri kisiingizwe kabla ya mchakato wa ajira kuanza, kwa nini hakikuwemo ndani ya zile sifa ambazo zilibainishwa pale awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwenye hili tunaona kulikuwa na mkakati makusudi wa kuwakosesha baadhi ya Watanzania fursa hizi za ajira na kuweza kuwanufaisha baadhi ya watu ambao inawezekana wanajulikana. Haya ni malalamiko na changamoto hizi zipo kwa muda mrefu kwamba BOT na taasisi zinazofanana na hizi kuwa watu wanaoajiriwa ni watu ni wa wakubwa ambao wanajulikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapungufu haya ni makubwa ambayo yanaisababishia Serikali yetu doa kubwa na tunaiomba sana Serikali iweze kujirekebisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naunga mkono mapendekezo yote ambayo yametolewa na Wenyeviti wetu hapa kwenye Kamati zetu tatu. Nashukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii ya kuweza kunipa fursa nami kuweza kuchangia kwenye hoja ya Kamati yetu ya PAC.

Mheshimiwa Spika, kabla ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa neema yake ya uzima na uhai ambao anaendelea kutujalia hadi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikupongeze wewe binafsi pamoja na Naibu Spika kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi za kishindo na kuweza kushika nafasi ambazo mko nazo. Nikuombeeni kwa Mwenyezi Mungu afya njema lakini busara na hekima ziendelee kuwaongoza katika uongozi wenu.

Mheshimiwa Spika, pia niipongeza Kamati yetu ya PAC lakini kipekee nimpongeza Mheshimiwa Mwenyekiti mama Kaboyoka kwa namna ambavyo ameweza kuiwasilisha ripoti hii kwa ufasaha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye ripoti hii, nitaelekeza michango yangu kwenye kuanzia ukurasa wa 20–24 kwenye ripoti ya Kamati ya PAC. Ukurasa huo unaelezea namna ya ukaguzi uliofanyika kwenye Mamlaka ya Mapato ya TRA. Kwa kweli ukusanyaji wa mapato ndiyo jambo ambalo linaiwezesha Serikali kuweza kutimiza mipango ambayo Bunge lako Tukufu inaipitisha kila mwaka. Lakini bila kukusanya mapato na mapato hata kama hayatatosheleza maana yake ni kwamba mipango ambayo tunaipanga ndani ya Bunge hili Tukufu haitoweza kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika ukaguzi wa CAG wa mwaka 2019/2020 umebaini mambo kadhaa kwenye mamlaka hii ya mapato ambayo sisi kama Kamati tumeona kwamba tuishauri Serikali kuweza kuyachukulia hatua za haraka ili kuongeza mapato ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na trend ya kutokutimia malengo ya ukusanyaji wa mapato, kwa mfano; mwaka 2019/2020 mapato ambayo yalikadiriwa ni trilioni 19.6 lakini ambayo yamekusanywa ni trilioni 17.1. Kutokutimia malengo ya ukusanyaji mapato kwa TRA kuna sababishwa na mambo kadhaa; moja wapo ni mifumo ambayo TRA wanaitumia kwenye kukusanya mapato haya. Kwa mfano; kuna mfumo wa ITAX, mfumo huu unaiwezesha Mamlaka ya Mapato kuweza kukusanya mapato ya wafanyabishara mmoja mmoja. Lakini mfumo huo umegundulika na dosari kadhaa zikiwemo zinazosababisha upotevu mkubwa wa mapato au kutokukusanya mapato inavyopaswa. Kwa hiyo, tunaiomba sana Serikali uupitie upya mfumo huu wa ITAX ili kuongeza mapato yanayotokana na wafanyabiashara kila mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, CIMIS pia ni mfumo mwingine ambao unamilikiwa na TRA. Mfumo huu unalengo la kutatua changamoto za mashauri ya kodi ambayo yanaendelea kurundikana mwaka hadi mwaka. Kwa mfano, mwaka 2018/ 2019 mashauri haya yalikuwa 770 lakini hadi kufika 2019/2020 mashauri haya yameongezeka licha ya kuwa na mfumo huu wa kuwasaidia utatuzi wa makosa haya na kufikia makosa 1097. Kiukweli tulitegemea sana kwamba kuwepo kwa mfumo huu ungeweza kusaidia kutatua mashauri haya lakini tunaendelea kuona trend ya ongezeko ya makosa haya ya kikodi.

Mheshmiwa Spika, mfumo huu pamoja na kusababisha ongezeko hilo la makosa lakini pia kuna trilioni 360 mpaka sasa ambazo zinasubiria kutatuliwa kwenye mashauri haya. Lakini endapo mashauri haya yataweza kutatuliwa Serikali inaweza ikaingiza fedha nyingi sana. Mbali na tatizo hili la mfumo huu, pia kuna udhaifu mkubwa kwenye mfumo huu ambao nimezungumza wa CIMIS ambao unamuwezesha Meneja wa Kanda moja kuweza kuingia mashauri ya kanda nyingine. Kwa kweli kama tutaweza au kama kutakuwepo maafisa ambao siyo waaminifu wanaweza wakabadilisha nyaraka za Ushahidi na kuweza kuisababishia hasara kubwa Serikali yetu. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshmiwa Spika, naunga mkono hoja hiyo. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa Rehema, kwa zawadi ya uhai na uzima na kuweza kuniwezesha kusimama katika Bunge lako tukufu asubuhi hii. Pia, nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii, lakini pia nikupongeze kwa namna ambavyo unaendelea kuliheshimisha Bunge letu ndani na nje ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anaendelea kupambana na kutatua changamoto za Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najiuliza hivi hali ingekuwaje kama Mama Samia asingekubali kuweka na kutoa zile bilioni 100 kila mwezi ambazo zinaenda kutatua na kupunguza changamoto ya mafuta. Najiuliza ingekuwaje kwa wakulima wetu kama Mama Samia asingekubali kuzitoa zile bilioni 150 kwa ajili ya kupunguza changamoto ya bei ya mbolea na bei ya mbegu bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia huwa najiuliza, hivi bei ya unga na mafuta ya kula ingekuwaje kama kodi za bidhaa hizi pamoja na tozo zisingeweza kuondolewa na kuweza kuwawezesha wananchi kuweza kupata bei nafuu angalau kutokana na uchumi ambao kwa sasa hivi unaendelea duniani. Baada ya kujiuliza haya yote, niwaombe sana Watanzania tuendelee kumuunga Mama Samia mkono, tuendelee kumuombea dua ili aweze kuyatekeleza haya ambayo yanapangwa kwa umakini zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mapendekezo ya mwongozo wa maandalizi ya mpango huu ambao tunaenda kuujadili pamoja na bajeti ya mwaka 2023/2024, mimi nitatoa mapendekezo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeelezwa kwamba kuna mwenendo wa sekta za kibenki, kwamba benki sasa hivi zimeanza kupata faida kubwa kupitia return on equity pamoja na return on asset. Hatuwezi kujisifia kwa kuwapa benki hizi kupata faida pekee yao. Kwa sababu ndani ya benki hizi zisingekuwepo kama si wawekezaji. Bado interval na difference kubwa ipo kwenye wawekezaji pamoja na benki hizi. Watu ambao wanawekeza fedha zao, fedha wanayoipata kama faida ni ndogo kulinganisha na pesa wanayoipata benki kama faida. Bado interest cost ambayo waomba mikopo wanaichukua, wanaomba na kupewa ni interest kubwa sana hadi sasa hivi, lakini ukiangalia wale wanaowekeza fedha zao ile interest income wanayoipata ni ndogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa hali hii utakuta kwamba benki zinatengeneza faida kubwa lakini wale wanaowekeza bado pesa wanazozipata na income wanayoipata ni ndogo sana. Kwa hiyo, hatuwezi kujisifia kwa jambo hili. Mimi niombe muongozo wa mpango na tutakapokwenda kutengeneza mpango basi angalau sasa tushushe riba ya mikopo lakini pia tuongeze ile interest income ambayo inapatikana kwa wawekezaji wanaowekeza kwenye benki zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Bunge la Bajeti nilichangia kuhusiana na kuwepo kwa Islamic banking bado naendelea. Kwenye muongozo huu wa mpango ambao tunaenda kuuandaa pamoja na bajeti inayokuja naendelea kulisisitiza jambo hili. Kwa sababu kipindi kile cha bajeti halikuweza kutekelezeka lakini naamini kwa sababu tunaenda kutengeneza mwongozo, tunaenda kutengeneza mpango wa bajeti lakini pia tunaenda kutayarisha bajeti ijayo, naamini jambo hili Mheshimiwa Waziri kutokana na umuhimu wake unaweza kulichukua na kuweza kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ametuambia hapa kwamba mikopo chechefu imetoka kuanzia asilimia 9.3 mpaka sasa hivi ni asilimia 7.8. Mimi nipongeze kwamba inapungua lakini bado hiki kiwango ni kikubwa na ni kikubwa kwa sababu ile ambayo mwanzo niliizungumza, kwamba riba ya mikopo ni kubwa sana, lakini Islamic banking ndiyo ambayo inaenda kutatua changamoto hizi. Mifumo hii ya Islamic banking ipo hapa nchini tangia 2008 lakini tangu kipindi chote hicho inatumika kienyeji. Bado hakuna sheria, bado hakuna miongozo, bado hakuna kanuni ambazo zinaiongoza na kuisimamia Islamic banking ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe sana Serikali, ilichukue jambo hili, nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kuweka kile kipengele kwenye ile financing act ya kuondoa VAT kwenye mikopo ya mrabaha ambayo ni Islamic product. Kuondoa kipengele kile kuanzia mwaka huu 2022 lakini bado tunatakiwa tuwe na sheria ambayo inaongoza namna bora ya kuendesha hizi huduma za mikopo ya kiisilamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichangie jambo moja, nakuomba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante sana naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii ya kuweza kuchangia kwenye hoja hizi za Kamati zetu tatu ambazo ni Kamati ya PIC, PAC pamoja LAAC. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa zawadi yake hii ya uzima na wa afya njema na kuweza kusimama kwenye Bunge lako hili Tukufu jioni hii kuweza kuchangia machache ambayo tumeyaona kwenye Kamati yetu ya PAC.

Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anaendelea kuitumikia nchi yetu. Kwa kweli tunampongeza sana na tunamwambia aendelee kupiga kazi na sisi tuko nyuma yake, tunamuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mchango wangu leo nitaelekeza kwenye Kamati ya PAC na moja kwa moja nitazungumzia mambo matatu. Jambo la kwanza nitaangalia dosari katika usimamizi na ufuatiliaji wa mikataba. Moja ya miongoni mwa eneo ambalo Kamati yetu ya PAC imetumia muda mrefu kuchambua na kuangalia kwa kina ni eneo la namna gani mikataba yetu tunayoingia kwenye taasisi mbalimbali inavyoweza kusimamiwa na inavyoweza kufuatiliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna dosari nyingi sana kwenye eneo hili na naiomba sana Serikali iangalie upya kwa namna ambavyo tunaweza kusimamia kwa sasa kwa kweli bado tuna changamoto kubwa sana kwenye usimamizi wa mikataba yetu na kwenye ufuatiliaji wa mikataba yetu, jambo ambalo linapelekea hasara kubwa kwa Serikali lakini pia upotevu wa fedha nyingi lakini na ucheleweshwaji wa miradi mbalimbali ambayo inatekelezwa kupitia maeneo mbalimbali au sekta mbalimbali ambazo zinatekeleza miradi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni tumepata taarifa kwamba Serikali tutaenda kutekeleza miradi kupitia EPC+F pamoja na PPP. Sasa kama hatukuwa makini sana kwenye suala la usimamizi wa mikataba, kiukweli tutaenda kuisababishia Serikali yetu hasara kubwa sana na mabilioni ya fedha yatapotea kupitia mifumo hii ambayo tunakwenda kutekeleza miradi kupitia mifumo mipya hiyo ambayo nimeitaja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia tu mfano wa fedha ambazo zimepotea. Kwa mfano, ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza ambapo ilitakiwa ilipwe shilingi milioni 134, imelipwa shilingi milioni 154. Hii ni kwa sababu tu ya usimamizi mbovu na ufuatiliaji mbovu wa mikataba yetu. Ukiangalia pia ujenzi wa Hospitali ya Mkoa wa Mtwara, hali iko hivyo hivyo zimelipwa shilingi milioni 200 zaidi. Kwa hiyo hii ni mifano tu kuona kwamba mikataba yetu namna tunavyoweza kusimamia na namna ambavyo tunaweza kuifuatilia, kwa kweli tuna dosari kubwa na tuna udhaifu mkubwa sana Serikalini kwenye jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili niangalie kwenye mwingiliano wa majukumu ya kiutendaji kwenye taasisi zetu, mamlaka mbalimbali na mashirika mbalimbali ambayo yapo Serikalini. Kwenye Kamati yetu sisi hatukatai taasisi kushirikiana, lakini tunakubaliana na jambo hili endapo ushirikiano huo utaenda kuongeza ufanisi, ubora na utaenda kupunguza gharama za utekelezaji wa miradi hiyo ambayo wanaenda kushirikiana. Kwa hali ilivyo sasa, hatuoni kwamba kuna umuhimu kwa baadhi ya mashirika au kwa baadhi ya taasisi kuweza kushirikiana. Kwa sababu kwa mfano tu TAA (Tanzania Airport Authority) pamoja na TANROADS wanashirikiana kwenye ujenzi na ukarabati wa viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulitegemea kwamba ushirikiano wao utupe ufanisi mkubwa kwenye utekelezaji wa majukumu ambayo wamepeana, utupe ubora kwenye kazi hizo ambazo wanazifanya na gharama pia ziwe chini kwenye mambo haya ambayo wanashirikiana, lakini hali ni tofauti sana. Kwa mfano, kuna hasara ya zaidi ya shilingi milioni 236 ambayo Uwanja wa Ndege wa Dodoma, TAA walienda kuondoa taa uwanjani pale ambazo zilikuwa zinatumia nishati ya jua na wakaweka nishati ya umeme, taa nyingine ambazo taa hizo ziliwekwa na TANROADS. Kwa kweli ni hasara kubwa za Serikali, zaidi ya shilingi milioni 236 zimepotea kwa sababu tu ya ushirikiano dhaifu uliopo baina ya taasisi hizi mbili, TAA pamoja na TANROADS.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizo hizo taasisi mbili zimesababisha kuchelewa kwa utekelezaji wa Mradi wa Uwanja wa Ndege wa Shinyanga, kwa sababu mkataba na Benki ya Uwekezaji ya Ulaya uliingia baina yake pamoja na TAA, lakini mkataba huo ukataka kupewa TANROADS jambo ambalo ilichelewesha sana utekelezaji wa mradi huu. Tunaiomba sana Serikali, kwenye ripoti yetu sisi tumeshauri kwamba majukumu yote ambayo yanahusika na ujenzi wa viwanja vya ndege yarudishwe kwa taasisi ambayo inahusika na viwanja vya ndege ambayo ni TAA. Kwa hiyo naiomba sana Serikali izingatie mapendekezo haya, izingatie ushauri huu kwa maslahi mapana ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho ambalo nataka nichangie, ni namna Mifuko ya Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi inavyoweza ku-operate hapa katika nchi yetu. Tunayo Mifuko mingi ambayo hapa imetajwa kwamba kuna Mifuko zaidi ya 52, lakini tunaona ufanisi na utendaji wake bado ni mdogo. Tunaona kwamba control na usimamizi wa Mifuko hii ni jambo linalopelekewa na sababu ya kutosomana kwa mifumo hii na hivyo mtu anaweza akakopeshwa kwenye Mfuko mmoja na mtu huyo huyo akaenda akakopa kwenye mfuko mwingine bila ya kujulikana kwa sababu mifumo hii haisomani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mtu mmoja anaweza akakopeshwa na zaidi ya Mifuko miwili au mitatu, kitu ambacho kinapelekea mikopo chechefu mikubwa ambayo tumeiona. Mfano wa mikopo chechefu hiyo ni Mfuko wa Pembejeo za Kilimo, zaidi ya shilingi bilioni 20.1 zimepotea kwenye mifuko…

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Hamad Bakar.

MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Uwekezaji, Biashara na Viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake pamoja na timu yake nzima ikiongozwa na Katibu Mkuu na Naibu Makatibu Wakuu wote watatu. Tanzania ni miongoni mwa nchi chache ambazo zimebarikiwa na rasilimali nyingi mno, lakini rasilimali hizi tulizonazo bila ya kuweza kuzitangaza kwa nchi mbalimbali na zikajulikana duniani hatuwezi kufikia malengo na kuweza kuzitumia kwa maslahi ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ziara ambazo anazifanya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan, pamoja na kujenga uhusiano mzuri, ziara hizi kati yetu na nchi hizo ambazo anazitembelea lakini pia zinalengo la kutangaza rasilimali zetu kwa ajili ya maslahi ya Taifa letu kupata fursa za uwekezaji, lakini pia kwa kuangalia sana kwa watu wetu wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazo fursa nyingi zikiwemo bahari, maziwa lakini tunayo ardhi, tunavyo visiwa mbalimbali vingi sana bila vitu hivi kuvitangaza haviwezi kujulikana na haviwezi kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi leo nitazungumzia zaidi kwenye suala la uwekezaji; bado pamoja na mama kwenda na kufanya ziara hizi mbalimbali zenye lengo hili la kuzitangaza rasilimali zetu, tunazo changamoto za fursa au zenye kujenga mazingira rafiki kwa wawekezaji ili kuweza kupata fursa hizo kuja hapa. Tunayo changamoto ya urasimu kwa maana ya bureaucracy, bado jambo hili ni changamoto kubwa sana kwa nchi yetu. Endapo tutatatua changamoto hii ninaamini ile kazi ambayo anaifanya mama basi inaweza ikawa rahisi sana kupata wawekezaji wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tuna changamoto ya rushwa, bado rushwa ni tatizo kwa nchi yetu endapo pia tutatatua changamoto hii, tutaweza kuweka mazingira rafiki sana kwa wawekezaji wa ndani na wawekezaji wa nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna changamoto nyingine ambayo tulisema ni political stability, ili nchi yoyote iweze kuvutia watalii na kuweza kuvutia wawekezaji ni lazima kuwe na stability ya political. Tunashukuru sana kwa nchi yetu kwa sasa hivi amani na utulivu ambayo ipo ni jambo la kuweza kupongezwa na kuungwa mkono. (Makofi)

Niwaombe sana Watanzania niwaombe sana wanasiasa tuendelee kuidumisha amani tuliyonayo, tukiidumisha amani hii ndio ambayo tutawahakikishia wawekezaji kuja nchini na kuweza kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna changamoto nyingine ambayo ni miundombinu ambayo bado miundombinu tulizonazo sio Rafiki, ukiangalia barabara zetu bado sio rafiki kwa wawekezaji, ukiangalia umeme, maji na miundombinu mingine. Tukiweza kurekebisha kwenye maeneo haya ya miundombinu ninaamini kwamba wawekezaji watakapokuja na watakapoona kwamba tumeweka sawa kwenye suala la miundombinu, ninaamini kwamba tutaongeza wawekezaji wengi sana wa nje na kuja kuwekeza katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwanza ni wakati sasa wa kuweza kuanzisha system (mifumo mbalimbali) itakayoondoa hivi vikwazo, hizi nenda rudi za wawekezaji, kuwarahisishia wao hizi njia za kuweza kupata vibali, lakini njia za kuweza kuona hizo fursa zinazopatikana katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia sheria tulizonazo ni wakati wa kufanya marekebisho ya sheria ili sheria hizi ziwe na fursa nzuri na ziwe na maslahi mapana kwa wananchi wetu, kwa nchi yetu lakini pia ziwe na maslahi mapana kwa wawekezaji ambao wanawekeza hapa nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia FDI inflow ya trend ya Africa kwa sasa Tanzania ni kama vile haionekani. Unaona nchi kama Egypt, unaona nchi kama South Africa, unaona kama Nigeria, Congo, unaziona hizo kwenye suala hili la Foreign Direct Investment (FDI), sisi bado tuko chini sana. Ni wakati wa kupiga hatua kuondoka hapa tulipo na kuelekea huko mbele zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya kusema hayo niunge mkono hoja hii, ahsante sana nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana nami kunipa nafasi hii ili kuweza kuchangia hotuba hii ya bajeti ambayo iko mbele yetu ambayo inahusu Muungano na Mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, niwapongeze viongozi wetu wawili; Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa namna ambavyo wanaendelea kushirikiana na kwa namna ambavyo wanaendelea kufanya kazi ya kuleta maendeleo kwa Serikali zote mbili; Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri pamoja na timu yao kwa utendaji wao mzuri wa kazi hizi na niwaambie tu kwamba tunaendelea kushirikiana kuhakikisha kwamba mambo haya ya Muungano yanaendelea kuwa mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuwaomba Watanzania wote, hususan vijana, kuendelea kuulinda, kuutetea na kuupigania Muungano wetu huu kwa faida ya nchi zetu zote mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba vikao vya Kamati ya kujadili masuala mbalimbali yanayohusu Muungano vinaendelea na hoja mbalimbali – kama ambavyo Mheshimiwa Waziri leo amewasilisha – hoja mbalimbali tayari zimepatiwa ufumbuzi; niipongeze sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na juhudi hizo bado tunazo kero mbalimbali ambazo zinaendelea kuleta changamoto kwa nchi zetu mbili. Alisema kwamba hoja ya mizigo inayotoka Zanzibar kuja Bara imeondolewa kodi zile ambazo zilikuwa ni kodi mara mbili, lakini bado hoja hii inaonekana kuwa ni changamoto, hasa kwa mizigo midogomidogo ambayo inatoka Zanzibar kuja Bara.

Mheshimiwa Naibu Spika, iliyoondoka ni hoja ya wafanyabiashara lakini haijaondoka hoja ya wananchi wanaosafiri kwenda Zanzibar na kurudi Bara wanaosafiri na mizigo yao midogo midogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani mwananchi amesafiri na kilo mbili za sukari anafika nazo Bara anaambiwa alipe kodi. Haiwezekani mwananchi amesafiri na TV moja, tena used, anakuja kutumia nyumbani, anafika Bara anaambiwa alipe kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ni nchi moja, haiwezekani wananchi hawa anayetoka Morogoro kwenda Dar es Salaam halipi kodi anaondoka na mizigo yake, anaondoka na mambo yake kama hayo lakini hakuna sehemu yoyote ambayo anasimamishwa kulipa kodi. Lakini anayetoka Zanzibar kuja Bara akifika Dar es Salaam anatakiwa alipe kodi kwa TV moja ambayo anakwenda kutumia nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili halijakaa vizuri. Niiombe sana Serikali ilifanyie kazi jambo hili. Bado kabisa halijakaa vizuri na inaleta kero kubwa kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona magari ya nchi jirani mbalimbali yanayozunguka hapa Tanzania na hayana usumbufu wowote, hayaletewi usumbufu wowote, lakini kuna changamoto kubwa kwa usajili na utambuzi wa magari yanayotoka Zanzibar kuja Bara kuweza kutumika hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu hii ni moja, Tanzania ni moja. Ni kwa nini mpaka leo hakujawekwa sheria inayotambua, inayosajili magari yanayotoka Zanzibar kuja kutumika hapa Bara.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana, jambo hili limezungumzwa muda mrefu sana na linaendelea kuwa kero. Niiombe sana Serikali, nikuombe sana Waziri, utuambie ni lini utaleta sheria ya kuweza kuweka wazi masuala ya usajili wa vyombo vya usafiri…

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba juzi tu nilinunua TV nilivyofika bandarini nikachajiwa difference laki mbili. Kwa hiyo, tatizo hili ni kubwa kweli kabisa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Bakar, taarifa.

MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nimepokea taarifa hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado changamoto hii. Kwa hiyo tuombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja atuambie, Sheria ya Usajili wa Vyombo vya Usafiri ni lini italetwa Bungeni kuweza kujadiliwa na kuweza kupitishwa rasmi na kuondoa mkanganyiko na usumbufu huu unaotokea kwa vyombo vya usafiri vinavyotoka Zanzibar kuja Bara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la ajira, hasa kwa taasisi za Muungano. Upo uwiano ambao umebainishwa wa asilimia 21 kwa Zanzibar na asilimia 79 kwa Bara kwa zile taasisi zote za Muungano. Bado pia hapa kuna changamoto; hakuna utaratibu ambao uko wazi unaobainisha hizi asilimia 21 zinapatikanaje na asilimia 79 zinapatikanaje. Kwa hiyo, naomba sana Serikali hebu ifanyie kazi jambo hili, iweke utaratibu ulioko wazi, unaoonekana na ambao hauna mkanganyiko, kwamba tujue asilimia 21 zinapatikanaje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati imeshauri kwamba kuna haja na umuhimu mkubwa wa kufanya tathmini ya watumishi wa Umma wanaofanya kazi kwenye sekta za Muungano; bado. Likifanyiwa tathmini jambo hili naamnini itakuja kutuletea majibu hapa kwamba jambo hili hasa likoje. Ni kweli asilimia 21 inatekelezwa? Ni kweli ajira hizi ziko hivyo ambavyo inazungumzwa? Lakini pia tutapata majibu mengi na tutaondosha manung’uniko mengi ambayo yapo sasa hivi yanayoendelea. Niombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja aje na majibu haya kwa ufasaha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiacha jambo hilo pia kuna suala la ushiriki na ushirikishwaji kwa taasisi ambazo siyo za Muungano. Tunafahamu kwamba ushirikishwaji na ushirikiano wa taasisi za Muungano hakuna shida sana, lakini kwa taasisi zisizo za Muungano, na hasa kwa mikutano inayofanyika ya kimataifa ambapo Tanzania inakwenda kushiriki kule, Zanzibar bado baadhi ya taasisi hazijaweza kushirikishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba baadhi ya taasisi tayari, kwa mfano Ofisi ya CAG tayari mikutano mbalimbali Zanzibar inashirikishwa. Lakini kuna taasisi kwa mfano suala la Mamlaka ya Kudhibiti Dawa za Kulevya, Zanzibar tuna mamlaka yetu na Bara tuna mamlaka nyingine. Kwa hiyo, niombe sana kwa mikutano ya kimataifa ambayo Tanzania inakwenda kushiriki kwa taasisi ambazo siyo za Muungano basi Zanzibar iweze kushirikishwa kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie na suala la mwisho ambalo ni suala la mazingira. Amezungumza hapa Mheshimiwa Simai, Mbunge wa Nungwi, kwamba jambo hili ni changamoto kubwa, hasa kwa visiwani. Mabadiliko ya tabianchi ni jambo kubwa sana kwa visiwa. Visiwa vinaendelea kuliwa na maji. Kwa hiyo, niiombe sana Serikali iweke msisitizo na mkazo mkubwa kwenye suala hili la mabadailiko ya tabianchi na kuongeza fungu hili la bajeti, hasa kwa maeneo ya visiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya kusema hayo, niiunge mkono hoja hii. Nakushukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii nami niwe mchangiaji kwenye Hotuba yetu hii ya Bajeti ya Serikali. Nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anaendelea kutenda mema kwa Watanzania, lakini nimshukuru na nimpongeze kwa bajeti hii ambayo jumla ya zaidi ya trilioni 44 ambayo ametuletea mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru pia na nimpongeze kwa utendaji kazi kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo afya, ikiwemo elimu, ikiwemo ujenzi wa Barabara, lakini reli ya kisasa ambayo inaendelea kujengwa, lakini nimpongeze kwa mambo mbalimbali ambayo yanaendelea kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitatenda haki kama sikumpongeza Waziri na Naibu Waziri wa Wizara hii kwa namna ambavyo wanaendelea kushirikiana kwa pamoja katika kutekeleza majukumu ambayo Watanzania wamewakabidhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze na niwashukuru sana kwa namna ambavyo wanaendelea kushirikiana na Wizara inayohusika na Fedha na Mipango ya Zanzibar. Kwa kweli kulikuwa changamoto nyingi ambazo ziko kwenye maeneo yao, walipoingia wao wamekwenda kushirikiana katika utatuzi na leo hii tunazungumzia mambo mengi ambayo yamefanywa mazuri kwenye ushirikiano huu wa Serikali ya Zanzibar na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Wizara ya Fedha na Mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwatie moyo na niwaombe Wizara hii waendelee kupiga kazi. Sisi tuko pamoja nao na tunawaunga mkono, tunawaombea sana Mwenyezi Mungu aendelee kuwapa afya bora, lakini pia hekima iendelee kuwatawala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la uwekezaji. Hatuwezi kuongeza idadi ya walipakodi, hatuwezi kupiga hatua ya kuongeza watu wenye ajira kwenye nchi yetu kama hatukuhamasisha, kama hatukuendelea kujenga mazingira rafiki, kujenga mazingira mazuri kwa wawekezaji ambao wanakuja kuwekeza ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la uwekezaji haliepukiki, ni lazima nchi yeyote kwanza iangalie wananchi wake na hususani kundi kubwa la vijana. Vijana hawa lazima tuwaangalie kwenye suala la ajira na kwenye suala la ajira hatuwezi kwenda kwenye ajira kama hatukuweza kuwekeza kwenye maeneo mbalimbali ambayo yanazalisha ili kuweza kuwapa vijana wetu ajira. Tunapoongeza ajira maana yake tayari tunaongeza walipakodi na hapo ndipo tunapokwenda kuzungumzia suala la upunguzwaji wa viwango vya kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumza sana kwamba viwango vya kodi bado viko juu, lakini tutafanyaje kwa idadi hii ya walipakodi ambao wanahudumia Watanzania walio wengi? Hatuwezi kupunguza viwango hivi, lakini nadhani dawa ya jambo hili ni kuongeza walipakodi hasa wa kuwekeza maeneo mbambali ili kuweza kupunguza rate ya kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima ifike mahali Tanzania tuache, tubadilike na tubadilishe mindset zetu, tukiona tu hatuwezi kumwona tu Mzungu yeyote au mtu mweupe yeyote tu hapa nchini halafu tukawa tunadhania amekuja kutuibia. Dhana hizi potofu ni lazima tuzipige vita, ni lazima wananchi wa Tanzania wabadilike, hakuna, haiwezekana kwamba nchi yetu sisi tuwe sisi tu wenyewe tu tumejifungia, haiwezekani. Tuna-lack of experience katika mambo mengi sana, tuna-lack mitaji kwa mambo mengi sana lakini tuna-lack teknolojia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wana fedha, wenzetu wana teknolojia nzuri, wenzetu wana uwezo wa kuweza kutekeleza mambo mbalimbali, lazima tuweke mazingira rafiki na lazima tuwavutie. Nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wetu kwa hakika anaendelea kufanya kazi kubwa kwenye kuwavutia wawekezaji kuja nchini kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna eneo moja ambalo mchango wake mpaka sasa ni mdogo kama vile limesahauliwa. Suala la uvuvi, bado rasilimali tuliyonayo kwenye bahari ni kubwa sana, lakini ukiangalia mchango unaochangiwa kwenye sekta ya uvuvi ni asilimia 1.8. Kwa kweli katika eneo hili ni lazima tuendelee kuwekeza ili kuweza kuongeza, kuweza kutumia bandari yetu au kuweza kuitumia bahari yetu katika kuongeza pato la Tanzania, kuongeza ajira, lakini pia kuweza kupunguza ile rate ambayo nimezungumza pale mwanzo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
MUswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Usajili wa Wahasibu na Wakaguzi wa Hesabu wa mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. BAKAR HAMAD BAKAR: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Kwanza na mimi nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema kwa kuniwezesha kusimama ndani ya Bunge hili Tukufu kuweza kuchangia muswada huu wa sheria ambao tunaenda kuujadili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa uwasilishaji wake mzuri wa mapendekezo haya ya muswada huu wa sheria, lakini kipekee sana naomba nimpongeze Mwenyekiti wangu wa Kamati ya PAC, Mama Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, kwa uwasilishaji mzuri na wa fasaha sana kwenye hotuba yake ambayo ametoka kuiwasilisha. Mchango wangu mimi utakwenda kwenye maoni haya ya jumla ya Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia kwenye muswada huu wa sheria, Ibara ya 18 ambayo imefanyia marekebisho kwenye kifungu cha 30, inakwenda kuzifanya au kuzitaka biashara zote ambazo mitaji yake ni kuanzia milioni 700 ama turn over ya milioni 500 kwenda kuwasajili ama kuwaajiri wahasibu ambao wamesajiliwa wenye CPA, lakini tunazo taasisi ama mashirika ya umma makubwa yenye mitaji zaidi ya hizo milioni 700 na zaidi ya hizo milioni 500 ambazo zimetajwa ndani ya sheria hii ambazo zimefanya taasisi zisizokuwa za Serikali ziajiri wahasibu, lakini mashirika haya kwenye kurugenzi zao hayana wahasibu wenye CPA. Kwa hiyo, tumependekeza kwenye Bodi za Wakurugenzi kwenye mashirika haya ya umma angalao na wao wawe na mhasibu japo mmoja kwenye bodi zile ambaye atakwenda kusaidia kwenye masuala haya ya fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bodi nyingi za wakurugenzi kwenye mashirika na mashirika yetu haya ndio ambayo yanakwenda kuzalisha na ndio ambayo yanakwenda kuongeza mapato makubwa kwenye nchi yetu. Sasa kuziacha tu bodi hizi bila ya wenye taaluma hii na jambo hili kuwekwa kwenye sheria kwa kweli ni kuzipa mianya bodi hizi kukwepa wana-taaluma hii wenye CPA. Kwa hiyo, tunapendekeza sana kwamba jambo hili lina uzito mkubwa na liweze kuchukuliwa kuingizwa kwa wahasibu wenye taaluma ya uhasibu wenye CPA kwenye Bodi za Wakurugenzi kwenye mashirika mbalimbali ya umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, NBAA ni taasisi ya kitaifa, lakini sheria hii ambayo tunaenda kuipitisha/kuitunga leo, ni sheria ambayo inahusu Tanzania Bara peke yake. Tunatambua kwamba Zanzibar sasa hivi wapo kwenye mchakato wa kuanzisha bodi kama hii ambayo itahusiana na usajili wa wahasibu na wakaguzi kwa kule Zanzibar, lakini bado kuna ukakasi kwamba, kwa sababu hii ya NBAA ni Bodi ya Taifa, je, recognition ya wana-taaluma hawa itakuwaje? Wale ambao watasajiliwa na Bodi ya Zanzibar watakapokuja huku Bara watatambulikaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hii bado ipo kimya sana, haijaeleza kwamba, tutawatambuaje wana-taaluma hii watakaotoka upande mmoja wa muungano kwenye sehemu nyingine, wale watakaotoka Tanzania Bara kwenda kufanya kazi Zanzibar Bodi ya Zanzibar itakuwaje, lakini wale ambao watasajiliwa na Bodi ya Zanzibar watakaokuja kufanya kazi huku Bara watatambulikaje na sheria hii? Kwa hiyo, tunaomba pia Mheshimiwa Waziri aje atueleze jambo hili kwenye sheria hii litakaaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwa sababu, taasisi hii ni ya kitaifa, tayari ime-comply na imejiunga na taasisi mbalimbali za kimataifa, sasa siamini kwamba taasisi kama hii ambayo itaundwa kule Zanzibar itapata ruhusa wapi ya kuweza kujisajili na taasisi za kimataifa? Ziko taasisi mbalimbali kama IVAC, lakini iko PAFA, kuna INTROSAI na AFROSAI; taasisi zote hizi NBAA ni mwanachama kule, lakini je, Bodi ya Zanzibar ambayo itaenda kuundwa sasa hivi itakuwa mwanachama kule? Itaruhusiwa kuundwa kule?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu, tunaona kwamba, kwa experience tunazo bodi au tunazo taasisi ambazo Zanzibar na Tanzania Bara zinakanganyana kwenye kujiunga ama kupata ushirikiano kwenye mashirika ya kimataifa, nikitoa mfano, tunayo TFF na ZFF kule mpaka leo Zanzibar si mwanachama wa mashirika yale au taasisi zile za kitaifa zinazohusiana na jambo hili. Kwa hiyo, na jambo hili tunaliona kwamba, huko mbele huenda, kuna wasiwasi, ikaja ikatokezea mkanganyiko kama huu na ikatokezea mtafaruku kwenye mambo yetu haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ibara ya 4 kwenye muswada huu imetaja majukumu ya Bodi hii ya NBAA, lakini majukumu haya tunaona kwamba yamechukuliwa/ yamechanganywa majukumu ya udhibiti na usimamizi. Tumependekeza kwamba tuanzishe public oversight body ambayo itaenda kushughulikia baadhi ya majukumu kwamba, tusiipe mzigo mkubwa taasisi hii ya NBAA kufanya mambo yote ya udhibiti pamoja na usimamizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja hii asilimia 100. Ahsante sana. (Makofi)