Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Mwantatu Mbarak Khamis (2 total)

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. MWANTATU MBARAK KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii kwa mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu nami kuweza kuchangia bajeti iliyoko mbele yetu. Kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu Muumba Mbingu na Ardhi ambaye amenijalia pumzi na wakati huu nikaweza kusimama hapa kuelezea mchango wangu juu ya bajeti yetu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na walionitangulia kwa kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan pamoja na wasaidizi wake wakiwemo Waheshimiwa Mawaziri, Manaibu Mawaziri kwa namna ambavyo wameanza kutelekeza majukumu/kazi yao na kuwajengea matumaini zaidi Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Naibu wake Mheshimiwa Masauni pamoja na Watendaji wa Wizara ya Fedha kwa kuandaa pamoja na kutuwasilishia bajeti hii ambayo leo tuko hapa katika kuijadili; bajeti iliyojaa matumaini na bajeti iliyobeba dhamira ya kuwaendeleza Watanzania. Hii ni ishara njema ya namna ambavyo Serikali yetu ya Awamu ya Sita inavyokwenda kutatua shida za wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze mchango wangu kwa suala zima la uimarishaji wa elimu. Nichukue nafasi hii pia kuipongeza na kuishukuru Serikali kwa namna ilivyojipanga katika suala zima la kuimarisha elimu Tanzania kwa kujenga Shule za Sekondari nyingi, Shule za Msingi pamoja na kukarabati shule za zamani na isitoshe kuajiri walimu wengi kwa lengo la kuimarisha elimu na kuona watoto wetu wanapata elimu iliyo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika suala hili zaidi nitazungumzia wanafunzi wenye ulemavu. Nachukua nafasi hii pia kuipongeza Serikali kwa namna walivyojali wanafunzi wenye ulemavu na wakaweza kuwajengea mazingira mazuri. Ukiangalia uhitimu wa wanafunzi wenye ulemavu kipindi cha nyuma na sasa hivi ni tofauti. Kwa sasa kila mwaka ufaulu wa wanafunzi wenye ulemavu umekuwa ukiongezeka kwenda sekondari na hata vyuo, na wewe mwenyewe nadhani utakuwa shahidi. Hii yote inatokana na juhudi za Serikali kusomesha walimu wa kutosha ambao wanasomea kuwafundisha watoto wenye mahitaji maalum. Pia hii inatokana na jitihada za walimu hawa. Bila ya jitihada hii, hawa wanafunzi wasingefika hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Serikali kuangalia walimu wanaofundisha wanafunzi wenye ulemavu kwa sababu walimu hawa wana kazi kubwa. Kumfundisha mwanafunzi mwenye ulemavu ni tofauti na kumfundisha mwanafunzi wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwalimu anayefundisha mwanafunzi mwenye ulemavu anatumia masaa mengi zaidi. Kwa hiyo, tunahitaji kuwajengea uwezo lakini pia kuwapa motisha ili waweze kuwasaidia watoto wetu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo sasa, nataka kuzungumzia suala la tozo. Naunga mkono mapendekezo ya Waziri kuhusu kufanyia marekebisho Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani kwa bidhaa zinazonunuliwa Tanzania Bara kwenda Zanzibar na zinazonunuliwa kutoka Zanzibar kuja Tanzania Bara. Napongeza marekebisho haya kwa sababu yatakwenda kuondoa kero ya muda mrefu ambayo ilikuwa ikilalamikiwa na wafanyabiashara. Siyo tu kwa wafanyabiashara, hata kwa wananchi wa kawaida ambao walikuwa wakinunua bidhaa zao kutoka upande mmoja wa Muungano kwenda upande wa pili wa Muungano.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, suala hilo pia litaondoa zile hoja kwa wale wasioutakia mema Muungano wetu waliokuwa wakilitumia sana suala hili. Kwa hiyo, nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huwa tunatengeneza sheria nyingi na nzuri na pale ambapo tunahisi zinahitaji marekebisho tunafanya hivyo, lakini tunatengeneza sheria, tunafanyia marekebisho, lakini shida inakuja katika utekelezaji wa sheria kutokana na baadhi ya Watendaji wetu kutokuwa na uaminifu na hii usababisha mambo yasiende kama yalivyopangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu katika hili, namwomba Mheshimiwa Waziri baada ya kufanya marekebisho haya, awe mfuatiliaji mzuri na timu yake hili kuona malengo ya Serikali yameweza kufikiwa. Pamoja na hayo, pia namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja, atupe ufafanuzi wa kina juu ya tozo hizi: Je, sitahusika mpaka kusafirisha magari? Kwa sababu unapotoa gari Zanzibar kule Bara ni shughuli; au unapotoa gari Bara kuleta Zanzibar ni shughuli. Aje atufafanulie, tozo hizi ni vipi zitagusa masuala ya magari unapotaka kusafirisha? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu mwingine nitajikita katika suala zima la tozo katika kufanya miamala ya matumizi ya simu. Hili suala ni jema sana, Serikali yetu ipo katika kuona inatengeneza mazingira kwa maslahi ya wananchi wake. Kuna miradi mingi imepangwa, kuna shughuli nyingi zimepangwa katekelezwa na zote hizi zinategemea mapato. Kwa hiyo, naunga mkono suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya Mheshimiwa Waziri kuwasilisha hotuba yake hapa, kumekuwa na uelewa tofauti tofauti na watu wanazungumza maneno tofauti juu ya tozo hizi. Namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya majumuisho basi aje atoe ufafanuzi wa kina juu ya tozo hizi kwa lengo la kuleta uelewa mzuri kwa wananchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika mchango wangu mwingine ambao unazungumzia miradi ya kimkakati inayoibuliwa na Halmashauri zetu. Kuna miradi ambayo huwa inaibuliwa na Halmashauri. Miradi hii inaibuliwa lakini kuna vigezo maalum. Kigezo cha kwanza, Halmashauri iwe na uwezo wa kuongeza mapato, iwe na uwezo na mpango wa kujitegemea na pia iwe na uwezo wa kuandika andiko la mradi. Hata hivyo, kuna Halmashauri zetu nyingine tunaona hazitaweza kukidhi hivi vigezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumetunga sheria ya kuzitaka Halmashauri kuchangia asilimia 10 ya mapato yake. Tumeona katika ripoti, inaeleza kwamba kuna Halmashauri zimetimiza asilimia 100, kuna Halmashauri asilimia 30, na nyingine asilimia 50. Hata hivyo, kuna Halmashauri zimewezesha vikundi vingi, lakini kuna Halmashauri zimewezesha vikundi kidogo. Hii inatokana na uwezo wa Halmashauri zenyewe.

Kwa hiyo, kutokana na vigezo hivi, nahisi bado hazijatendewa haki zile Halmashauri zenye uwezo mdogo; na lengo letu ni kuziwezesha Halmashauri kukusanya mapato na kuhudumia wananchi pamoja na kuleta maendeleo katika Halmashauri zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi, naomba sana iundwe timu ya wataalam iende kwenye Halmashauri, tuziangalie Halmashauri ambazo hazina uwezo, zijengewe uwezo hili waweze kuzitambua fursa zinazowazunguka ili nao waingie katika ushindani wa makusanyo. Kwa hiyo, Halmashauri hizi nazo zitaongeza uwezo wake na wataweza kutimiza matakwa ya sheria ya kukamilisha kwa asilimia 100 yale makusanyo ya asilimia 10 ya Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi/Vigelegele)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. MWANTATU MBARAK KHAMIS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenijalia pumzi kwa wakati huu nikaweza kusimama mbele ya Bunge lako hili Tukufu. Aidha nikushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mkosefu wa shukrani kama sitamshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, mama mpambanaji ambaye anatupambania sisi Watanzania kwa jitihada zake za kuhakikisha huduma muhimu zinatufikia wananchi wa Tanzania popote tulipo. Aidha, niwapongeze Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na Naibu Waziri wake na watendaji wote kwa kusimamia vema majukumu yao na leo hii tukasikia Wizara hii imeanza kuonekana, hii yote ni jitihada yao wao kwa namna ambavyo wanaisimamia Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuipongeza Serikali kwa kupeleka miradi ya maendeleo 691, miradi ambayo ina lengo la kuhakikisha huduma muhimu zinapatikana kupitia Wizara hii. Huduma hizo ambazo zimeelezwa katika ukurasa wa 11 wa randama ni vituo vya huduma ya afya, madarasa ya shule za msingi, pamoja na shule za sekondari. Mpango huu ni mwema sana na unaleta matumaini katika kupatikana kwa huduma ambazo zinakwenda moja kwa moja kuimarisha maisha ya wananchi, lakini pia kuleta manufaa makubwa kwa wananchi wetu kupitia miradi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kupongeza naomba nishauri. Kwa upande wa vituo vya afya; kuhakikisha wataalamu wanakuwepo, lakini pia na vifaa tiba vinapelekwa kwa lengo la kufikia malengo ya kujengwa vituo hivi, lakini kwa upande wa shule, pia, kuhakikisha Walimu na vifaa vya kufundishia vinakuwepo, lakini pamoja na kuwepo vizingatie mahitaji ya wanafunzi wote wakiwemo wanafunzi wenye ulemavu kwa sababu, wanafunzi wenye ulemavu wanapata changamoto kubwa katika kujifunza kwa kutokupatikana kwa uhakika kwa vifaa ambavyo vinaweza kuwasaidia kufikia malengo yao ya kujifunza kama walivyo watoto wengine wasio na ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze Wizara kwa kufuatilia na kubaini Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ambayo yanafanya shughuli zao kinyume na utaratibu uliowekwa. Kufuatiliwa kwa mashirika haya kumeleta picha ya kuona kwamba, kuna baadhi ya mashirika ambayo yanasajiliwa kwa nia nzuri, lakini matokeo yake vitendo vyake vinaleta athari kubwa katika jamii yetu. Niiombe Wizara kupitia hili kufuatilia zaidi kwa karibu mienendo ya jumuiya hizi ambazo zinasajiliwa ambazo zipo na zile ambazo zinaundwa sasa hivi, kufuatilia kwa karibu ili ihakikishe mashirika yanayosajiliwa yawe na malengo mazuri ambayo yataleta tija kwa jamii yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema haya natambua mchango mkubwa unaotolewa na Mashirika Yasiyo ya Kiserikali, yanasaidia sana Serikali, lakini kuna baadhi wanaunda mashirika haya kwa lengo la kupotosha utamaduni na silika zetu kama wengine walivyoanza kusema. Kwa hiyo, niwapongeze sana Serikali kwa hili, lakini waendelee kufuatilia kwa karibu zaidi na hayo ambayo wameyafuatilia wazidi kuyafuatilia na wawe karibu sana katika kusimamia utekelezaji wa mashirika haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee katika kipengele cha kulinda haki ya mtoto. Serikali imeeleza kwamba, imeunda madawati ya ulinzi na usalama yapatayo 1,393 kwa baadhi ya mikoa kwa shule za msingi na sekondari, lakini pia wameunda Mabaraza ya Watoto 560. Jambo hili ni jema sana kwa sababu, kuundwa kwa madawati haya na mabaraza haya yatakwenda kuwaweka watoto pamoja na kuweza kujadili changamoto zinazowakabili kwa pamoja na italeta picha ya kuwezesha kujua watoto wanakabiliwa na nini, kuliko hivi sasa hivi mpaka mtoto limfike, ndio uchunguzi unafanywa tunajua watoto wanapatwa na yapi, lakini katika mabaraza haya wataweza kutoa fikra zao na kila mmoja ataeleza changamoto.

Mheshimiwa Spika, nataka kujua mabaraza na madawati haya vipi yamemwangalia na kumshirikisha mwanafunzi mwenye ulemavu? Kwa sababu, miongoni mwa wanaopata changamoto kubwa ni wanafunzi wenye ulemavu katika familia zao, lakini pia katika jamii inayowazunguka, wanakumbana na changamoto ya kubakwa, lakini pia na kudhalilishwa kutokana na hali zao. Mheshimiwa Waziri atakapokuja atatueleza kwamba, watu wenye ulemavu au wanafunzi wenye ulemavu wameshirikishwa vipi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niendelee kuishauri Serikali, mabaraza haya na madawati haya yana lengo zuri, lakini hayataweza kusimama na kuendelea bila kuyawekea bajeti ya kutosha. Mheshimiwa Waziri labda atwambie wamejipanga vipi katika kuhakikisha madawati na mabaraza haya yanafanya kazi zake vizuri na yanaendelea ili kufikia yale malengo ya kuundwa kwake? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee na mchango wangu katika Program Jumuishi ya Malezi, Makuzi na Maendeleo ya Awali ya Mtoto. Imeelezwa kuwa elimu ya uelewa imetolewa juu ya program hii, lakini elimu hiyo imetolewa kwa mikoa kumi na ndio iliyofaidika, mikoa yenyewe imetajwa katika randama. Nataka kujua tuna mikoa isiyopungua 32 kama sikosei, je, vipi Wizara imeangalia hii elimu kufikia katika mikoa mingine ambayo imebakia? Kwa sababu, maendeleo yanapokuja yaende kote na Wizara imechagua kwa mikoa kumi, hii mikoa iliyokuja hali itakuwaje, lakini vigezo gani ambavyo vinasababisha hii mikoa kumi ikachaguliwa kuanzishiwa program hii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee na mchango wangu kwa program ya usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake kiuchumi. Tumeelezwa kuwa kupitia randama hii Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake umeweza kutoa mikopo yenye thamani ya shilingi milioni 663.4 kuanzia Julai mpaka Aprili, 2023. Fedha hizi zilitolewa kwa vikundi 11, lakini pia kwa wajasiriamali mmoja mmoja wapatao 14 na ikajumuisha wanufaika 104 kwa mikoa minne. Hapa pia nataka kufahamu je, kwa nini hiyo mikoa minne tu? Ni kigezo gani kilichotumika hata mikopo hii ikatolewa kwa hiyo mikoa minne? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie mchango wangu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja Mheshimiwa, kengele ya pili ilishagonga.

MHE. MWANTATU MBARAK KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mwisho, naomba nimalizie mchango wangu katika makusanyo na mapato ya Wizara hii. Kwa mwaka 2022/2023, Wizara ilikadiriwa kukusanya bilioni 8.5, lakini hadi kufikia Aprili, 23 imekusanya 3,025,562,821. Nataka kujua ni changamoto gani iliyosababisha Wizara kushindwa kufikia malengo hayo iliyojiwekea? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya mchango huo, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Naunga mkono hoja. (Makofi)