Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Amber. Mbarouk Nassor Mbarouk (4 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia na kutoa ufafanuzi wa hoja ambazo zimetolewa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniruzuku uhai na afya njema na kwa kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu.

Aidha, nichukue fursa hii kwa kipekee kumshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na kwa kuniteua kwanza kuwa Mbunge na pili kuwa Naibu Waziri wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaahidi kuwa nitaitumikia nafasi hii kwa weledi na juhudi kubwa nikiongozwa na falsafa ya kutanguliza mbele maslahi ya Taifa na nitatumia uzoefu wangu wa muda mrefu katika diplomasia na uhusiano wa kimataifa kwa maslahi mapana ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kukushukuru wewe binafsi na Mheshimiwa Spika kwa kuliongoza Bunge hili kwa umahiri, hekima, busara na umahiri mkubwa. Aidha, ninaomba kuishukuru Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa maoni na ushauri wao walioutoa kupitia taarifa iliyowasilishwa asubuhi hii. Hii ni Kamati makini kwani wajumbe wake wana uelewa mkubwa wa masuala ya kidiplomasia na hivyo wamekuwa wakitoa mchango mkubwa ambao umeendelea kusaidia kuboresha utendaji kazi wa Wizara na diplomasia ya nchi yetu kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kumshukuru Mheshimiwa Balozi Liberata Mulamula, Mbunge na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki kwa uongozi wake mahiri ndani ya wizara na ushirikiano mkubwa anao nipatia. (Makofi)

Pia ninamshukuru Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara na taasisi zote zilizochini yake kwa ushirikiano mkubwa ninaoupata katika kutekeleza majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia kuishukuru familia yangu kwa upendo na uvumilivu wao na kuendelea kuniunga mkono wakati wote nikitekeleza majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri nijielekeze katika kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge. Kwanza nitoe shukrani kwa Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia na kutoa maoni na ushauri katika kikao hiki ambacho kimejadili hotuba ya bajeti ya Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, michango ya Waheshimiwa Wabunge wote tumeipokea, na ninaahidi kuijumuisha katika utekelezaji wa mipango ya Wizara, naomba nitolee ufafanuzi wa baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, naomba nichangie issue au hoja ya itifaki; hoja hii imeongelewa asubuhi hii kwa hisia kubwa, hapa bora nimtaje ni Mheshimiwa Jerry Silaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli Wizara inasikitika sana na mapungufu yaliyojitokeza na ili kuepusha changamoto hiyo nakuhakikishia kwamba itifaki inazingatiwa katika shughuli zote za kitaifa ambazo zinawahusisha viongozi wetu wakuu, hususan viongozi na mhimili wa Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inaandaa mkutano ambao utajumuisha stakeholders wote wanaohusiana na mambo ya itifaki na tutawajumuisha pia na Ofisi ya Bunge, Ofisi ya Waziri Mkuu, tutazungumza kwa pamoja ili kuboresha utendaji wa Serikali na kuimarisha uhusiano uliopo katika mihimili yote ya dola katika kuratibu shughuli za kitaifa. Na hiki kikao kitafanyika tarehe 14 mpaka 18 hapa Jijini Dodoma kwa ajili ya kujadili masuala haya ya kiitifaki ya viongozi na tunaahidi kwamba suala hili tutajitahidi lisitokee tena. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kukamilisha Sera ya Mambo Nje na kujumuisha masuala ya diaspora; Wizara ipo katika hatua za mwisho kukamilisha Sera ya Mambo ya Nje ya mwaka 2021 pamoja na mambo mengine sera hiyo pia itatoa mwongozo wa utekelezaji wa masuala ya diaspora kisera na kimkakati kwa manufaa mapana ya diaspora.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu umuhimu wa kujenga Ofisi ya Idara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa Zanzibar ambayo ina hadhi, kwa sasa Wizara inamiliki jengo la Ofisi ambalo sasa hivi lipo katika ukarabati na ukarabati wake unaendelea kwa nguvu. Naona muda unakwenda sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba kutoa ufafanuzi hapa kidogo kuhusiana na issue ya Palestina ambayo imeongelewa na Wabunge hapa. Ni kweli kwamba hivi karibuni mgogoro kati ya Israel na Palestina umeongezeka na kusababisha madhara makubwa kwa pande zote mbili ikiwemo vifo na uharibu wa miundombinu katika miji ya Gaza, Tel Aviv, Jerusalem na Ukingo wa Magharibi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania muda wote imekuwa ikilaani mapigano hayo, dhamira ya Tanzania ni kuona mgogoro huo unatatuliwa kwa njia ya amani na utulivu na usalama unashamiri. Tanzania haijakaa kimya kwenye suala hili, tumeendelea kushiriki na kushawishi Jumuiya za Kikanda na za Kimataifa kuchukua hatua zaidi na za pamoja ili kuona mgogoro huo unatatuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa mantiki hiyo Tanzania inaendelea kuunga mkono maazimio ya Umoja wa Mataifa na Umoja wa Afrika kuhusu mgogoro huo ambao unazitaka pande husika kuheshimu makubaliano ya kuwepo kwa nchi mbili ikiwa ni Palestina huru na Israel salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Tanzania haijabadili msimamo wake kutoka hapo awali na kuhusu msimamo wa Tanzania kuhusu Sahara Magharibi haujabadilika pia. Serikali yetu imeendelea kutambua haki ya msingi ya watu wa Jamhuri ya Kiarabu wa Demokrasia ya Sahrawi kujiamulia mambo yake wenyewe kupitia kura ya maoni na tunaendelea kuunga mkono juhudi zinazofanywa na Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na Umoja wa Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha ufunguzi wa ubalozi wa Morocco hapa nchini si ishara ya kubadili msimamo wetu, bali ni hatua ya kuimarisha uhusiano wa kidiplomasia na kutoa fursa kujadili masuala mbalimbali ya ushirikiano ikiwemo suala la utatuzi wa mgogoro wa Sahara Magharibi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze kidogo kuhusu ahadi ya msaada wa Falme za Kiarabu. Ni Wizara yetu kupitia ubalozi wake wa Abudhab imekuwa ikifanya juhudi kuhakikisha kwamba msaada wa fedha uliotolewa na mifuko hiyo miwili inapatikana mapema inavyowezekana. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba taratibu zote zimekamilika kwa upande wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar na kinachosubiriwa sasa ni Khalifa Fund kutoa fedha hizo ambazo ni dola za Kimarekani milioni mbili kila mwaka kwa muda wa miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha kuhusu hospitali ya Wete mchakato unaendelea, ulikwama kutokana na Covid, lakini hii ni ahadi iliyotolewa na viongozi wa UAE na ahadi hii tunahakikisha kwamba inatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha kuhusu barabara ya Chakechake hadi Wete tayari Serikali imeshasaini mkataba na Saudi Fund tarehe 19 Aprili, 2020 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Chakechake hadi Wete - Njia Kongwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mengine yaliyobakia tutayajibu na kuyawasilisha kwa Wabunge wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru sana kwa kunipa hii fursa na mimi niweze kuchangia kidogo katika hii hoja. Sisi kwa Wizara ya Mambo ya Nje, jukumu letu moja kubwa ni kuhakikisha kwamba, diplomasia ya uchumi inaendelezwa kwa nguvu zote, lakini nashukuru kwamba, kazi hii sasa imekuwa rahisi kwa sababu, hapo kabla kidogo tulikuwa tunasuasua, lakini sasa kwa kweli tunafanya kazi vizuri sana na hii yote ni kutokana na Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kusafisha njia na huko tunakopita sasahivi tunapita vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nifahamishe kwamba, hivi sasa katika balozi zetu kuna msururu mkubwa sana wa wawekezaji ambao wanataka kuja kuwekeza nchini Tanzania. List ni kubwa sana na tunafanya kila juhudi kuhakikisha kwamba, wawekezaji hawa wanakuja Tanzania na kuchangia uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine, katika kipindi hiki tumeshuhudia biashara na nchi jirani imeongezeka sana mpaka kufikia kipindi kwamba, wengine wanalalamika, mbona bidhaa nyingi zaidi zinakuja kutoka Tanzania kuliko sisi tunavyopeleka Tanzania? Na hizi zote ni juhudu za Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, na suala jingine ni kwamba, hizi ziara ambazo Mheshimiwa Rais anafanya tayari zimeanza kuleta matunda na zimekuwa zikizidisha ufanisi wa Wizara yetu. Kwanza, nitataja mfano mmoja tu; ziara yam waka jana ya Mheshimiwa Rais ambayo aliifanya China, makubaliano 15 ya ushirikiano walikubaliana na tayari utekelezaji wa makubaliano hayo umeshaanza na hasa ikiwemo upelekaji wa bidhaa nyingi kwenda nchini China. Hizi zote ni fursa ambazo nchi yetu inatakiwa izitumie kikamilifu.

Mheshimiwa Spika, na kwa kumalizia niingine sasa kidogo katika maridhiano ya kisiasa; hili pia limeturahisishia sana kwa sababu, wenzetu wanapokuja katika Wizara zetu suala hili kila siku lilikuwa ndio gumzo, lakini hivi sasa hawalisemi tena kwa sababu, wanaona kwamba, siasa zetu zimekuwa ni za kirafiki, za kindugu, sio tena siasa za ugomvi na sio tena siasa za chuki. Na hii yote inasaidia katika kupaisha diplomasia ya uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu mwingi wa rehema kwa kuturuzuku uhai na afya njema na kutuwezesha kujadili hotuba hii siku ya leo. Aidha, nichukue fursa hii ya kipekee kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini na kuhudumu katika nafasi hii ya Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Hussein Ali Mwinyi, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi pia Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Mbunge na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushauri na maelekezo yao katika kutekeleza majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia napenda kumshukuru Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Spika na wewe binafsi pamoja na wenyeviti wote kwa namna mnavyoliongoza Bunge letu kwa hekima, busara na umahiri mkubwa. Aidha, naomba kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, ulinzi na usalama kwa maoni na ushauri wao ambao wamekuwa wakitupatia na pia kupitia taarifa iliyowasilishwa asubuhi hii ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni Kamati makini sana na Wajumbe wake wana uelewa mkubwa wa masuala ya Kidiplomasia na hivyo wamekuwa wakitoa mchango mkubwa ambao umeendelea kusaidia na kuboresha utendaji wa kazi wa Wizara yetu na diplomasia ya nchi yetu kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Stergomena Tax, Mbunge, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa uongozi wake mahiri na ushirikiano mkubwa anaonipatia mimi binafsi na wenzangu ndani ya Wizara. Kwa hakika uongozi wake, miongozo yake na michango yake kwa kweli inatufanya kwenda katika direction nzuri zaidi na kuwa chachu ya ufanisi wa Wizara yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimshukuru Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara na Taasisi zote zilizo chini ya Wizara yetu kwa ushirikiano mkubwa ninaoupata kutoka kwao, bila kuwasahau Mabalozi wetu wote ambao wanatuwakilisha sehemu mbalimbali duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ninapenda kuishukuru familia yangu kwa upendo na uvumilivu wao kwa kuendelea kuniunga mkono wakati nikitekeleza majukumu yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nijielekeze kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge, lakini kwanza nianze kwa kutoa shukrani kwa Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia na kutoa maoni yao katika hoja ambayo imeletwa na Mheshimiwa Waziri wetu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirkiano wa Afrika Mashariki. Vilevile, ninashukuru kwa pongezi nyingi ambazo Waheshimiwa Wabunge mbalimbali wamezitoa kwa Wizara yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, tunawaahdi Waheshimiwa Wabunge wote kwamba tunapokea pongezi hizi na kutekeleza majukumu yetu kwa bidii na ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba uniruhusu nitoe ufafanuzi wa hoja iliyoelezwa hapa kuhusu kuchelewa kwa ujenzi wa Makao Makuu ya Mahakama ya Afrika ya Haki za Binadamu na Watu. Kwanza naomba nieleze kwamba pamoja na kuchelewa huko Tanzania muda wote huo imekuwa ikitekeleza wajibu wake kama Host Country Agreement kwa kuipatia Mahakama hiyo Ofisi za Mahakama, nyumba ya Rais wa Mahakama na nyumba ya Msajili wa Mahakama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo ili Mahakama hii iwe na majengo yake ya kudumu katika mwaka huu wa fehda kiasi cha shilingi bilioni Nne tayari zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama hiyo ambazo zitakuwa katika eneo la Laki Laki huko Arusha. Hivi sasa Wizara inakamilisha malipo ya awali kwa Mkandarasi na tarehe Mosi Juni, 2023 ambapo ni kesho kutwa tu, Wizara itakabidhi eneo la ujenzi kwa Mkandarasi ili aweze kuanza maandalizi ya awali ya ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuna hoja hapa ilizungumzwa kuhusiana na changamoto za visa hasa kwa vijana wetu wanaokwenda masomoni nje ya nchi. Naomba nikiri kwamba ni kweli baadhi ya muda kumekuwa na changamoto kwa baadhi ya vijana wetu ambao wanakwenda kusoma huko nje. Hata hivyo, Wizara imekuwa ikisaidia kwa kadri inavyoweza ili wanafunzi hao wapate VISA na hivyo kupata fursa ya kwenda kusoma. Aidha, ililetwa rai hapa kwamba Wizara ianzishe Idara ya Fursa lakini naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari kuna Idara ya Diplomasia ya Uchumi na kwa hiyo tunachukua huo ushauri wake ili hizo fursa hizo ziwe katika Idara ya Diplomasia ya Uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nieleze kuhusu Ofisi ya Wizara ya Mambo ya Nje iliyoko Zanzibar. Kwanza, tunashukuru sana kwa Mheshimiwa Mbunge Soud kutambua juhudi za Serikali za kuhakikisha kwamba tuko katika maeneo mazuri ya kufanyia kazi. Pia, naomba kulifahamisha Bunge lako kwamba, suala la wafanyakazi hivi sasa liko katika hatua za mwisho la kulipatia ufumbuzi na hivi karibuni kuna Maafisa kama wanne hivi wataajiriwa hapo. Pia kuhusu suala la samani tayari Wizara imekwishaweka samani nzuri za kisasa katika Jengo la Ofisi zetu huko Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la usafiri wa gari, naomba nimfahamishe Mheshimiwa Mbunge kwamba, tayari mwezi uliopita gari aina ya landcruiser tayari lilishapelekwa Zanzibar kwa ajili ya Ofisi zetu.

Mwisho kuhusu kujenga Ofisi zetu za kudumu, naomba kulieleza Bunge lako tukufu kwamba, hivi sasa tuko na majadiliano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ili waweze kutupatia eneo hilo na tayari eneo hilo linaweza kupatikana eneo la Tunguru kwa ajili ya ujenzi huo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naona muda umekwisha. Kwa hayo machache, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu Mtukufu, Mwingi wa Rehma kwa kuturuzuku uhai na afya njema na kutuwezesha kujadili hotuba hii siku ya leo. Aidha, nichukue fursa hii kwa kipekee kumshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini kuhudumu katika nafasi ya Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia sina budi kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Phillip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushauri na maelekezo yao katika kutekeleza majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumshukuru Mheshimiwa Spika na wewe binafsi kwa namna mnavyoliongoza Bunge letu kwa hekima, busara na umahiri mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, ninaomba kuishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa maoni na ushauri wao walioutoa kupitia taarifa iliyowasilishwa asubuhi hii. Hii ni Kamati makini sana, Wajumbe wake wanauelewa mkubwa wa masuala ya kidiplomasia na hivyo wamekuwa wakitoa mchango mkubwa ambao umeendelea kusaidia kuboresha utendaji kazi wa Wizara na diplomasia ya nchi yetu kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda pia kumshukuru Mheshimiwa Balozi Liberata Mulamula, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa uongozi wake mahiri ndani ya Wizara na ushirikiano mkubwa anaonipatia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ninamshukuru Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na watendaji wote wa Wizara na taasisi zote zilizopo chini yake kwa ushirikiano mkubwa ninaoupata kutoka kwao bila kuwasahau Mabalozi wote ambao wapo nchi za nje wakituwakilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, ninapenda kuishukuru familia yangu kwa upendo na uvumilivu wao na kuendelea kuniunga mkono wakati nikitekeleza majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri nijielekeze katika kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge, lakini kwanza nitoe shukrani kwa Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia na kutoa maoni yao katika hoja ambayo imeletwa na Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru sana pia kwa pongezi nyingi ambazo Waheshimiwa Wabunge mbalimbali wamezitoa kwa Wizara yetu na kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri tunawaahidi Waheshimiwa Wabunge wote kwamba pongezi hizi kwetu ni deni ambalo tutalilipa kwa kutekeleza majukumu yetu kwa bidii na ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jumla ya Waheshimiwa Wabunge 20 wamechangia hoja hii na michango ya Waheshimiwa Wabunge wote tumeipokea na tunaahidi kuijumuisha katika utekelezaji wa mipango ya Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza nianze kuhusu suala la viwanja, ujenzi na ukarabati wa majengo ya Ofisi za Balozi zetu. Suala hili limeongelewa takribani na nusu ya Wabunge ambao wamechangia leo hapa. Wizara tayari imekamilisha taratibu za manunuzi za kuwapata wakandarasi watakaotekeleza miradi ya ujenzi na ukarabati kwenye Balozi zetu nje ya nchi. Miradi hiyo ni ujenzi wa jengo la kitega uchumi katika Ubalozi wa Tanzania Nairobi ambapo mkandarasi aliyepatikana ni SRJE East Africa Limited, ujenzi wa jengo la ubalozi na kitega uchumi katika ubalozi wetu wa Kinshansa mkandarasi ni China Railways Construction Engineering Group Limited na ujenzi wa makazi ya jengo la ubalozi na makazi ya balozi katika ubalozi wetu Muscat mkandarasi aliyepatikana ni Arab Contractors na pia ujenzi wa jengo la ubalozi la kitega uchumi katika ubalozi wa Tanzania Comoro mkandarasi aliyepatikana ni Suma JKT Construction Company Limited, mradi wa ukarabati wa jengo la zamani la ubalozi R Street katika ubalozi wa Tanzania Washington mkandarasi ni Kampuni ya M&R Construction Group. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mikataba ya miradi hii tayari imeridhiwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali na hivi sasa ni Wizara ipo katika hatua za kukabidhi maeneo ya miradi (site possession) kwa wakandarasi ili ujenzi uanze mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika ubalozi wetu wa Msumbiji ambalo kuna jengo lenye ghorofa tisa tayari limekarabatiwa na lipo katika hatua za mwisho kukamilika. Aidha, kuhusu utekelezaji wa kiwanja cha ubalozi mpango wa kukiendeleza umeanza kufanyika kwa kukamilisha michoro na makabrasha ya jengo linalopendekezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ubalozi wetu wa Zambia kesho Wizara yetu ina kikao na Benki Kuu, Shirika la Nyumba la Taifa na Wizara ya Fedha pamoja na Wakala wa Majengo Tanzania kwa ajili ya kujadili namna ya kuviendeleza viwanja hivyo kwenye mwaka huu wa fedha. Hata hivyo, majengo sita yaliyopo Lusaka tayari yamekarabatiwa na yapo katika hadhi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ilielezwa hapa kwamba katika Ubalozi wetu wa Ufaransa tuna jengo bovu. Kwa kweli Ubalozi wetu wa Ufaransa hatuna jengo bovu, Wizara ina majengo mapya ambayo yamenunuliwa mwaka 2015 kinachofanyika ni ukarabati wa mara kwa mara hasa kutokana na vipindi vya joto na baridi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ilizungumziwa kuhusu ukarabati wa jengo la Ofisi ya Wizara iliyopo Zanzibar naomba kulitaarifu Bunge lako kwamba ukarabati wa Jengo la Ofisi ya Mambo ya Nje Zanzibar tayari umekamilika na jengo hilo sasa lina muonekano wenye hadhi ya Ofisi ya Mambo ya Nje. Aidha, kuna utaratibu pia saa hizi unaoendelea wa kuanza kujenga jengo jipya la Ofisi ya Mambo ya Nje ambalo tunategemea litakuwa sehemu ya Tunguu mara tutakapokabidhiwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa zaidi naomba kukufahamisha kwamba hivi sasa Wizara yetu inaendelea na utekelezaji wa maelekezo ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kujadiliana na taasisi za fedha hapa nchini kwa lengo la kuendeleza viwanja kwa kujenga majengo ya ofisi, vitega uchumi pamoja na makazi ya watumishi wa ubalozini. Hadi sasa kwa kutekeleza maagizo hayo tayari tumeshafanya vikao viwili na Benki ya CRDB kwa nia ya kuwa na utaratibu maalum wa kutekeleza maelekezo hayo. Tunafurahi kwamba hata leo hapa wawakilishi wa CRDB walikuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niongelee kidogo kuhusu suala jingine ambalo limechangiwa hapa na Waheshimiwa Wabunge wengi hili ni suala la wafanyabiashara wa Watanzania kuzuiwa kwenda China kwa kipindi hiki.

Waheshimiwa Wabunge ni vizuri tukaelewa kwamba ndugu zetu Wachina ugonjwa huu wa UVIKO ulianzia kwao na ulileta madhara makubwa ikiwemo zaidi ya watu 4,000 kupoteza maisha yao. Hali hiyo iliwafanya waweke masharti magumu ili kudhibiti maambukizo ikiwemo kuzuia raia wa kigeni kuingia China na kuwataka raia wao wanaorudi kwao kukaa quarantine siku 21 hotelini kwa gharama zao na kuyataka mashirika ya ndege ya kimataifa kupunguza safari za ndege hadi kufikia safari moja kwa wiki na katika safari hizo ndege isizidishe ujazo wa abiria kwa asilimia 60 ili kuwepo na social distance ndani ya ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, masharti hayo si tu kwamba yamewaathiri wafanyabiashara wetu bali pia yanawaathiri na raia wao na raia wa mataifa mengine yote ulimwenguni tangu mwezi Machi hadi leo hii tunavyozungumzia jiji la biashara la uchumi la Shanghai lipo kwenye lockdown baadhi ya wilaya za Jiji la Beijing nazo pia zipo katika lockdown na imeelezwa na ubalozi wetu kwamba kwa zaidi ya siku 60 sasa katika Jimbo la Shanghai wananchi wameambiwa wasitoke ndani ya nyumba zao na maduka yote yamefungwa, usafiri wa ndani umesimama, shughuli za mabenki pia zimesimama, shughuli za bandari, soko la hisa na viwanda vingi navyo vimesimamisha uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo inatuonesha dhahiri ni jinsi gani ndugu zetu hawa wanavyochukulia ugonjwa wa UVIKO-19 tofauti na nchi nyingine duniani. Hatua zao si tu zinaumiza wafanyabiashara wetu, bali pia zinawaumiza wananchi wao. Hivyo tuvute subira na tuwe na matumaini kwamba mambo yatafunguka na wenzetu wakiwa tayari watatufungulia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tukisubiria hilo, Serikali imechukua hatua mbalimbali za kuwawezesha wafanyabiashara wetu kutimiza malengo yao ikiwa ni pamoja na kufungua dawati la viwanda na biashara kwa ajili ya kutoa huduma kwa wafanyabiashara wanaotaka kuagiza bidhaa China. Aidha, Serikali imefungua Ofisi ya Ubalozi mdogo Guangzhou ambayo itaendelea kufanya kazi hiyo kwa ufanisi zaidi. Aidha, Serikali imeanzisha safari za ndege za Air Tanzania na kusafirisha mizigo ya wafanyabiashara wetu ili kurahisisha upatikanaji wa mahitaji yao kwa haraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kuna habari njema, na habari ambayo tumeipokea wiki hii ni kwamba kuanzia Juni mwaka huu shirika letu la ndege limeruhusiwa kuanza tena safari za kubeba abiria kwenda China. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kidogo kuna suala hapa pia lilizungumziwa kuhusu kufungua ubalozi nchini Pakistan na Iran. Kwanza nataka nikubaliane na Waheshimiwa Wabunge kwamba Pakistan na Iran tuna mahusiano nao mazuri sana na tumekuwa tukishirikiana katika mambo mbalimbali, lakini kuhusu mpango wa Serikali kufungua ubalozi wake nchini Pakistan na Iran, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki tayari imeanza kufanya utafiti wa kuona namna ya kufungua ubalozi katika nchi hizo kwa kuangalia faida za kiuchumi na maslahi mapana ambayo nchi yetu inaweza kunufaika nazo ikiwa ni pamoja na kuainisha gharama za ufunguzi wa ubalozi na uendeshaji wake, mara zoezi hilo litakapokamilika, basi Wizara itawasilisha mapendekezo na ushauri kwa mamlaka kwa ajili ya maelekezo zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa hoja hapa kuhusiana na fursa za ajira katika nchi mbalimbali huko nje ikiwemo Qatar. Ni kweli kwamba Tanzania na Qatar zilisaini MOU kwa ajili ya vijana wetu wapate fursa za kwenda kufanya kazi nchini Qatar. Hata hivyo, mara tu baada ya kusaini huko kukatokea ugonjwa wa Covid ambao ulizuia kidogo kuendelea na process hiyo. Lakini hivi sasa tayari mazungumzo yameshaanza tena na hivi karibuni tutapata habari njema. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri maliza. Mheshimiwa Waziri, maliza, sekunde 10.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)