Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Amb. Liberata Rutageruka Mulamula (5 total)

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. BALOZI LIBERATA R. MULAMULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa shukrani, maana katika diplomasia tunachojua zaidi ni kushukuru na kushukuru tena kwa kila jambo. Nakushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia kwenye taarifa ya Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira, na kama back bencher kwa mara ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijazungumzia mada zenyewe, naomba kupitia kwako, namshukuru kipekee Mheshimiwa Spika, kwa kunipokea nilipotoka katika Uwaziri na kunipangia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira. Namshukuru sana Mheshimiwa Spika na nakiri kwamba Kamati hii imepanua sana uelewa wangu wa mambo mengi kuhusu sekta tunazozisimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru pia Mwenyekiti wa Kamati yetu, Mheshimiwa David Kihenzile na Makamu wake, Mheshimiwa Eric Shigongo na Wajumbe wenzangu wa Kamati pamoja na Makatibu wetu, Ndugu Anjelina Sanga na Ndugu Chipanda kwa mbeleko kubwa walionipatia na kuniwezesha kujifunza kuwa Mjumbe wa Kamati hii katika kipindi kifupi. Nimejifunza mengi, tumeenda kwenye ziara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa kwenye Posta sikujua kwamba Mheshimiwa Spika uliwachagua Wajumbe wa Kamati hii pamoja na ujuzi wao wa biashara lakini wanajua ku-entertain. Kwa hiyo, nakushukuru kwamba nimejifunza mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kupoteza muda, naomba niunge mkono hoja ya Kamati yetu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira pamoja na mapendekezo yaliyowasilishwa na Mwenyekiti wetu. Pia naunga mkono hoja ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kuongeza mchango wangu kwenye maeneo matatu yanayohusu Sekta zetu za Viwanda, Biashara na Mazingira kwa ajili ya tafakuri ya Bunge lako Tukufu na pia kuishauri Serikali yetu sikivu. Kama mwanadiplomasia mmoja alivyosema, yamesemwa mengi, lakini naomba niseme yale ambayo hayakusemwa katika kuweka msisitizo kwa taarifa ya Kamati yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita katika maeneo matatu. Moja, ni mabadiliko ya viwanda duniani. Kwa lugha ya siku hizi inaitwa fourth industrial revolution. Pia nitajikita kwenye eneo la biashara bunifu, yaani kwa Kiingereza startups. Mwisho nitajikita katika uchumi wa viwanda vya kijani (green industries) lakini kupitia Sera yetu ya Mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kamati tumepata wasaa wa kutembelea viwanda, tumepokea ripoti za Serikali na mipango iliyonayo. Nafurahi kuwa wote tuliopo hapa leo tunaelewa umuhimu wa viwanda katika kukuza uchumi wa nchi yetu. Viwanda vinasaidia kutengeneza ajira, kutupatia kazi, lakini napenda sana kuishauri Serikali kutupia jicho na kujiandaa na mabadiliko makubwa ya viwanda ambavyo nimesema yanapewa kipaumbele duniani (fourth industrial revolution). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pengine tutakuwa na semina, tutaomba watupe semina kuhusu hii, lakini kwa kifupi niseme, tofauti na karne ya 19 na 20, viwanda vya leo vinapigana vikumbo kutengeneza bidhaa zinazohusika sana na electronic na pia zinazoongeza thamani ya bidhaa. Kwa mfano, katika hiyo fourth industrial revolution yameanza kutengenezwa magari yanayotumia umeme, robot na vifaa vya kieletroniki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili hiyo, niseme kwamba nchi yetu imejaliwa rasilimali zote katika kwenda njia hiyo ya fourth industrial revolution. Mtakumbuka katika Mkutano wa Davos wa World Economic Forum, Mheshimiwa Rais aliongelea rasilimali tulizonazo. Nchi yetu imebahatika kuwa na nickel, graphite na earth minerals ambazo sasa hivi zinatumika katika kutengeneza viwanda vya sasa vyenye supply chain, na kufanya hivyo, tutajihakikishia nafasi yetu katika mapinduzi ya nne ya viwanda yajayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu startups, namshukuru Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara alitupa faraja kwamba mmeanza kuangalia jinsi ya kupitia sera na kutoa umuhimu kwa zile startups ambazo zaidi zinatumia teknolojia, ubunifu na zenye uwezo wa kuumuka kulinganisha na biashara za kawaida. Nisingependa tukawa tunachanganya kuhusu startups na SMEs. SMEs zinaweza kuwa startups, lakini startups siyo SM’s.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mnavyoona facebook, uber, zote hizo zilianza kama startups, lakini mnaona sasa ziliweza kuendelea kufanya biashara ya hali ya juu. Kwa Watanzania tuna kampuni ambazo zilikuwa kwenye incubators kama Max Malipo, Kopa Gas na Nala, lakini bahati mbaya biashara hizi bado hatujazipa kipaumbele na wala hazina sera. Nchi nyingi zimeweza kuvutia wawekezaji, (financial Investment) katika hizo. Kwa mfano, kama Nigeria sasa hivi wametangaza karibu Dola bilioni 100.37 ambazo zime-attract baada ya kupitisha sheria ya startups. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine, pia Mheshimiwa Rais amekuwa mwepesi, anajenga chuo. Ameelekeza tujenge Chuo cha Digital Technology Institute ambacho kitasaidia vijana katika kuendeleza ubunifu na teknolojia na tayari Serikali ya Jamhuri ya Korea imekubali kusaidia kujenga chuo hiki. Kwa hiyo, rai yangu kwa Serikali ni kuifanyia kazi ili tuwe na sera mapema iwezekanavyo, tufungulie fursa kwa vijana wabunifu waweze kubuni na kuvutia mitaji mikubwa kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, lakini siyo wa umuhimu, ni eneo la mazingira. Tuendapo, ajenda ya mazingira na viwanda inaenda sambamba. Nampongeza sana Mheshimiwa Spika kwa kuweza kuliona hili na kuunganisha hizi Kamati ya Viwanda na Biashara na Mazingira. Ila tumekuwa tunaangalia katika upande wa kuchafua mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafasi ya viwanda katika hii inayoitwa nishati jadifu (green energy), nchi nyingi au makampuni mengi kusudi waweze kuwekeza kwenye viwanda vyetu lazima tuzingatie hii green energy. Ndiyo maana inaitwa green energy industries, tuliangalie na tulipe umuhimu. Maana yake hakuna mtu atakayetaka kuwekeza viwanda ambavyo havikidhi masharti ya green energy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nihimize Ofisi ya Makamu wa Rais wachangamkie fedha za kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi ambazo zimekuwa zinatangazwa kwenye mikutano mikubwa, lakini pia kupitia Green Climate Fund na Global Environment Fund. Fedha hizi ni kwa ajili ya nchi zilizoendelea, lakini wawekezaji wetu wa ndani wanaweza kupata fedha hizi ikiwa wanaweza kuwa na viwanda mbali mbali ikiwemo recycling plants. Kwa hiyo, ni wakati wa sasa Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira ifungulie fursa za aina hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona biashara ya carbon. Kabla hujanitoa, nilikuwa nasema tumepewe Mwongozo wa Kitaifa wa Biashara ya Carbon. Sijui wangapi wanajua, lakini tumeambiwa pia Kanuni za Udhibiti na Usimamizi wa Biashara ya Carbon imekuwa mfano kwenye Mkutano wa COP27. Mimi nataka wote tuweze kujua kwamba hii ni biashara, lakini kampuni za nje ndiyo zimekuwa zinafaidika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimalize kwa kushukuru tena, lakini pia niseme naunga mkono hoja mia kwa mia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo Kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Kumi na Mkutano wa Kumi na Moja pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Nane na Mkutano wa Tisa
MHE. BALOZI LIBERATA R. MULAMULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi nami nichangie kwenye taarifa ya Kamati yangu ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kama ilivyowasilishwa na Mwenyekiti wetu, Mheshimiwa Dkt. Jasson Samson Rweikiza.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, naomba kipekee nimshukuru Mheshimiwa Spika kwa kunipangia Kamati hii, kwa sababu imepanua wigo wa uelewa wangu wa umuhimu wa Sheria Ndogo katika ustawi wa jamii na maendeleo ya wananchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mwenyekiti wa Kamati yetu, Makamu wake, Wajumbe wenzangu wa Kamati na Makatibu kwa ushirikiano mkubwa walionipatia na kuniwezesha kujifunza mengi kama Mjumbe wa Kamati katika kipindi kifupi na kutambua umuhimu wa Sheria Ndogo ambazo zinagusa moja kwa moja maisha ya wananchi katika utekelezaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kupoteza muda, naunga mkono hoja ya Kamati yetu ya Kudumu ya Sheria Ndogo na ninakubaliana na taarifa na mapendekezo kama yalivyowasilishwa. Naomba pia nitumie fursa hii kwanza kuipongeza Serikali kupitia Wizara husika kwa taarifa walizotupatia pamoja na semina zilizotolewa na taasisi mbalimbali za Serikali katika kutuelimisha, kutuhabarisha kuhusu utekelezaji wa majukumu yao kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu kama zilivyopitishwa na Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kamati tumepata wasaa wa kuchambua Sheria Ndogo zilizowasilishwa kwenye Bunge lako Tukufu pamoja na uchambuzi wa taarifa za utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kama ilivyoelezwa na Mwenyekiti wa Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema, mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni, naomba kutoa pongezi kwa Serikali kwa hatua nzuri ya kukamilisha marekebisho ya Sheria Ndogo mbalimbali kutokana na dosari zilizobainishwa katika utekelezaji wa kutangazwa katika Gazeti la Serikali, kama zilivyowasilishwa leo kwenye Bunge lako tukufu kupitia Hati iliyowasilishwa Mezani na Waziri Mkuu. Leo tumeshuhudia kwamba kumekuwa na Matoleo 22 ya Gazeti la Serikali, kuanzia mwezi Aprili mwaka huu 2023 hadi Mwezi huu wa Septemba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua ya kutangaza marekebisho katika Gazeti la Serikali ambayo imefikiwa na Wizara zinazohusika katika kipindi husika, ni mwitikio mzuri wa utekelezaji wa Maazimio ya Bunge yanayolenga kuondoa changamoto zilizobainishwa katika Sheria Ndogo kama ilivyooneshwa kwenye jedwali la utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kwenye taarifa ya Kamati. Hatua hii inastahili kupongezwa kwa kuwa ni hatua ya juu ya uzingatiaji wa Maazimio ya Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kujibu hoja mbalimbali za Kamati, mamlaka zinazohusika zimeweka juhudi ya kusahihisha dosari zilizobainishwa na Kamati. Kwa kufanya hivyo, madhara ya dosari hizi yameondolewa kwa kiasi kikubwa. Kwa mfano, Sheria Ndogo ya Afya na Usafi wa Mazingira ya Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi mwaka 2022, kifungu cha 14(3) ambacho Mheshimiwa mwanakamati mwenzangu, Mheshimiwa Maryam alikigusia, kinaeleza kwamba iwapo abiria atakayetupa taka nje ya chombo cha usafiri, kilikuwa kimeweka sheria kwamba mmiliki wa gari, dereva au kondakta ndio aweze kulipa faini isiyozidi shilingi 50,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwamba Serikali imelisikia hili na imeweza kutekeleza maagizo au Azimio la Bunge iliyoitaka kufanyiwa marekebisho ili kumtaka mkosaji mwenyewe aweze kuadhibiwa kwa kosa alilolifanya. Kwa hiyo, tumeona leo kwamba marekebisho ya kifungu hicho yamefanyika kwa kufuta kifungu hicho na kukiandika upya kwa kumwondoa mmiliki na dereva katika makosa yanayotendwa na abiria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua hiyo inaakisi misingi ya haki ya mtu kuadhibiwa iwapo ametenda kosa na siyo vinginevyo. Pamoja na kuipongeza Serikali kwa hatua hiyo, Kamati kama Wajumbe wenzangu walivyosema, imebaini ucheleweshaji katika kurekebisha dosari zilizobainika katika utekelezaji wa Sheria Ndogo. Ucheleweshaji huo unasababisha athari hasi za dosari zilizobainishwa katika Sheria Ndogo mbalimbali na hivyo kushindwa kutatua kero ambazo Bunge lako tukufu lililenga kuziondoa kwa ustawi wa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, zimetajwa sheria mbalimbali ambazo zinacheleweshwa au hazijatekelezwa kutokana na Maazimio ya Bunge, lakini naomba nitoe mfano tu kuhusu hii Sheria ya Environmental Management Control and Management Carbon Trading Regulation of 2022, hii inahusu maombi ya biashara ya carbon. Tumekuwa tukiongelea hilii hata wakati nikiwa kwenye Kamati ya Viwanda na Biashara, kwamba hii iweze kutungiwa kanuni ambayo inaeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nafurahi kusema kwamba kama Wajumbe wa Kamati, sote tunaelewa umuhimu wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo ambayo imekuwa engine ya Bunge lako katika uthibiti wa Sheria Ndogo na utekelezaji wake ulio na tija kwa kuwa sheria hizo zinazogusa moja kwa moja maisha ya wananchi. Ibara ya 8(b) ya Katiba inaeleza kwamba lengo kuu la Serikali ni ustawi wa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia naomba nirudie kwamba naunga mkono hoja ya Kamati yetu mia kwa mia, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee naomba nichukue fursa hii kukushukuru sana kwanza kwa kunipatia nafasi asubuhi ya leo kuwasilisha mbele ya Bunge lako tukufu hotuba ya bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kukushukuru kwa dhati kwa kusimamia kwa umakini mjadala wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Umeonesha unaifahamu sana Wizara hii kutokana na kwamba ulikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuishukuru tena kwa dhati Kamati ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama chini ya uongozi mahiri wa Mwenyekiti wa Kamati, Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo na Mheshimiwa Vincent Mbogo, Mbunge wa Nkasi Kusini na Wajumbe wa Kamati kwa ushauri na maoni yao. (Makofi)

Niwahakikishie Wajumbe wa Kamati kuwa Wizara imepokea taarifa ya Kamati, tumepokea ushauri, tumepokea na maoni na tutayazingatia wakati wa kutekeleza majukumu ya Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Balozi Nassor Mbarouk, Mbunge na Naibu Waziri kwa kazi kubwa anayoifanya na kwa kunisaidia kutekeleza majukumu ya Wizara, kwa hakika ni jembe. Ninamshukuru kwa majibu yake na ufafanuzi alioutoa kwenye hoja zilizoibuliwa kwenye mjadala huu. (Makofi)

Aidha, nawashukuru tena watumishi wa Wizara na taasisi zilizo chini ya Wizara chini ya uongozi wa Katibu Mkuu, Balozi Joseph Sokoine na Naibu Katibu Mkuu, Balozi Fatma Rajabu kwa kusimamia kikamilifu maandalizi ya bajeti ya Wizara. Nimefarijika sana kwa pongezi ambazo mmezitoa kuhusu uongozi wa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho lakini siyo kwa umuhimu naomba kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge waliochangia kwa ujumla wenu kwa kuzungumza na wale waliochangia kwa maandishi. Nadhani haijawahi kutokea, leo tumepata michango kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge 21, kwa kawaida huwa hatufiki hata kumi. Kwa hiyo, naomba niwashukuru sana sana sana Waheshimiwa Wabunge na niwahakikishie kabisa na kwa moyo mkunjufu kwamba michango ambayo mmeitoa tumeipokea na tutaifanyia kazi, maoni na mapendekezo yaliyotolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kutokana na ufinyu wa muda, Wizara yangu haitaweza kuzijibu hoja zote kwa hapa, lakini tutazitolea maandishi na tutaweza kuwasilisha kwenu. Nipende pia kuwahakikishia Wabunge kwamba sisi pamoja na kwamba ni Wabunge lakini ni watendaji, ni watendaji ambao tunazingatia yote ambayo tunazingatia Ilani ya Chama cha Mapinduzi, tunazingatia mpango wa maendeleo, tunazingatia sera yetu ya mambo ya nje, tunazingatia maagizo yanayotolewa na viongozi wa kitaifa lakini tunazingatia maelekezo na maoni na mwongozo kutoka Bunge hili tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo ya utangulizi, naomba nitoe ufafanuzi kwenye masuala machache yaliyoibuliwa kwenye mjadala wa hotuba ya bajeti yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Naibu Waziri kwamba amepitia hoja ambazo zilikuwa zimechangiwa na Wabunge wengi lakini naomba nimshukuru kwa aina ya pekee Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu kwa kutolea maelezo kuhusu jukumu la Mahakama ya Haki za Binadamu na Watu na jinsi gani ushiriki wa NGOs na watu binafsi wanaweza kupeleka kesi zao huko, umelitolea maelezo mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumuhakikishia Mheshimiwa Mbunge ambaye ameliongelea hili kwamba tutaendelea na nitaomba kwamba tuendelee kuweza kuwasiliana maana Serikali imejipanga tunaendelea kuliangalia kwa mapana yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na pengine Mheshimiwa Salome nikufahamishe kwamba tumepata heshima kubwa ya kuwa na Jaji ambaye ni Rais wa Mahakama hiyo, Mheshimiwa Iman Aboud ambaye tuko naye. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge napenda baada ya kikao hiki unaweza pia na wewe ukatumia fursa hii ukaweza kuongea na Rais wa Mahakama hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingi zilitolewa lakini naomba nijikite kwenye hoja moja ambayo ilikuwa specific kuhusu suala la barabara ya Singomakua kwa upande wa Tanzania kama alivyoeleza Mheshimiwa Yahya Ally Mhata kwa upande unaohusu Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tayari imeshajengwa na Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, napenda kulifahamisha Bunge lako tukufu kwamba Serikali ya Msumbiji tayari imetenga fedha za kujenga barabara zake ili kuunganisha na barabara zetu kwa lengo la kurahisisha mawasiliano na biashara kama alivyosisitiza Mheshimiwa Mhata. Leo hii nimeletewa taarifa kutoka Serikali ya Msumbiji kwamba barabara hizo ambazo zinafanyiwa matengenezo ni barabara ya Negomano mpaka Muenda ambayo ni kilometa 200, barabara ya Muenda mpaka Mount Pwezi ambayo ni kilometa 150 nayo inafanyiwa kazi na barabara ya kutoka Mount Pwezi mpaka Singomankua ambayo ni kilometa 90 tayari zimetengewa pesa kwa taarifa niliyoipata kutoka Serikali ya Msumbiji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge ambao wameliongelea vizuri sana au wameliweka vizuri sana diplomasia yetu ya uchumi ambayo ndiyo sera yetu ya mambo ya nje imejikita katika utekekezaji wa diplomasia ya uchumi. Tuliulizwa kuhusu mchango wa Wizara na balozi zetu nje na taasisi hizo chini ya Wizara katika kutekeleza diplomasia ya uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapenda kulijulisha Bunge lako tukufu na kuwahakikishia kwamba tumejipanga vizuri katika kuteleleza hii diplomasia ya uchumi na mifano ipo mingi, lakini kwa uchache wa muda naomba tu kuainisha michache.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa Mabalozi wetu wote wameelekezwa kwamba wawe na mpango mkakati unaoonesha jinsi gani wanatekeleza diplomasia yetu ya uchumi ikionesha malengo, ikionesha jinsi gani wakiainisha fursa na kujiwekea kama ninavyosema kipimo kwamba wanafanikisha vipi na sasa hivi tumeanza kupata hiyo mipango na kama Wizara inaifatilia kwa karibu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia niseme katika mwaka wa fedha 2021/2022 Mheshimiwa Rais alianzisha Idara Maalum ya Diplomasia ya Uchumi kwenye Wizara yetu ambayo pamoja na mambo mengine inajukumu la kuratibu utekelezaji wa diplomasia ya uchumi. Kwa hiyo, idara hii inaratibu na kufanya ufuatiliaji wa karibu wa fursa za biashara, uwekezaji, utalii na nyinginezo zilizopo ndani na nje ya nchi kwa kushirikia na balozi zetu, taasisi za Serikali na sekta binafsi kwa lengo la kuhakikisha Taifa linanufaika na fursa hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na nilifarijika kumsikia Mheshimiwa Mbunge mmoja akisema kwamba ili kufanikisha diplomasia ya uchumi kwamba Waheshimiwa Wabunge na ninyi muwe mabalozi wetu, tushirikiane kwa pamoja tuweze kufanikisha hii diplomasia yetu ya uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee pia kwamba balozi zetu zinajitahidi sana kutangaza fursa za biashara na fursa za masoko. Na kama mlivyotaja Balozi wetu, Mheshimiwa Kombo alioko Italy hivi majuzi tu ameweza kuwaleta wakulima wa kawaida tu kwenye maonesho ya kilimo na niliwaona wengi wao walikuwa ni kinamama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika mazao yale hasa matunda na mboga zili-attract watu wengi sana. Kwa hiyo, hiyo ninayosema ni jitihada zinazofanywa na balozi zetu kuhakikisha kwamba mazao yetu, bidhaa zetu zinajulikana huko nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme pia katika hotuba yangu nilieleza namna ambavyo nyama na bidhaa za nyama kutoka Tanzania vimepata soko katika nchi za Mashariki ya Kati na hivi karibuni Saudi Arabia imefungua soko la nyama yetu na watakuja kuwekeza kuhakikisha kwamba wanapata nyama ile ambayo inasoko katika nchi ya Saudi Arabia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, soko hilo limepatikana kutokana na jitihada za kutumia diplomasia, kushawishi mamlaka za Serikali na sekta binafsi katika nchi hizo kukubali kununua bidhaa zinazozalishwa nchini. Niseme mwezi uliopita nilienda ziara Saudi Arabia nikifuatana na Waziri wa Mifugo na Uvuvi kuhakikisha kwamba tunafanikisha hili. Serikali ni moja, tunakwenda pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, ninapenda kutambua mchango wa kituo chetu cha AICC ambacho kimekuwa mwenyeji wa kongamano la habari, lakini pia kitakuwa mwenyeji wa Shirikisho la Mpira (CAF). Kwa hiyo, nadhani hii itakuwa karibu sana tutashiriki huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua limeongelewa hili kwa mapana yake suala la diaspora, suala la uraia pacha na hadhi maalum. Kuhusu suala la uraia pacha nimemsikia sana sana na nashukuru kwa mchango wako Mheshimiwa Gwajima, Mchungaji wetu nakushukuru kwa kuweza kufanya tuseme tafiti (research). Umetueleza kwamba karibu nchi 75 duniani zinaruhusu uraia pacha, lakini pia Mheshimiwa Mbunge na Mchungaji wangu nikueleze kwamba kuna nchi zaidi ya 100 ambazo hazikubali uraia pacha. Kwa hiyo, siyo Tanzania tu na sababu ni nyingi. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuhusu suala hili napenda kulialifu Bunge lako tukufu kuwa kwa mujibu wa Sheria ya Uraia ya mwaka 1995 suala hilo linahitaji mjadala mpana wa kitaifa. Tayari Serikali inaendelea na mashauriano ya ndani na wadau mbalimbali wakiwemo wana-diaspora wenyewe ili kuweza kufikia uamuzi utakaonufaisha diaspora kwa kuwapa hadhi maalum hasa ikizingatiwa kuwa siyo nchi zote duniani zinaruhusu uraia pacha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda nimfahamishe pia Mheshimiwa Mbunge kwamba katika nchi za Gulf tukiamua kuwapa Watanzania uraia pacha wanaondolewa uraia wa nchi za Gulf. Sasa ndiyo maana nasema tulifanyie mjadala vizuri tuweze kwamba wengine wasiumie, wengine wakafaidika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimesikia utatoa mshahara, nahitaji mshahara tuendelee na majadiliano na mashauri ili kusudi tuweze kufikia muafaka kuhusu suala hili muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia Waheshimiwa Wabunge wameongelea kuhusu suala la hadhi maalum ambayo inalenga kuwatambua diaspora na kuondoa baadhi ya changamoto mlizozitaja za kisheria na kisera zinazowakwamisha katika kushiriki kikamilifu katika kuchangia maendeleo ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, naomba niwaeleze kwamba tumekuwa kwenye mchakato huu baada ya kuonekana suala la uraia pacha kwa kweli kwa sasa hivi tusingepata kutokana na hayo ambayo nimeyaeleza. Lakini tukafanya utafiti kwamba nchi ambazo hazina uraia pacha zina mpango gani? Kwa hiyo ndiyo tukakuta kwamba hii hadhi maalum pengine ndiyo compromise kwamba Mheshimiwa Mchungaji wangu umesema umeishi Marekani, hadhi maalum ni kama green card ya Marekani ambayo ukipata green card unapata haki zote. Unaingia bila viza, unafanya biashara yako, kwa tukasema kwa nini na sisi tusijikite hapo. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo Wizara inapanga kuwa na Semina kuhusu hili suala lakini suala la mchango wa diaspora kwa mapana yake tutaiangalia uraia pacha lakini hadhi maalum kwa kweli ukiangalia India mmetaja hapa Pakistani, Iran wote wana hadhi maalum ikiwemo hata Ethiopia nayo ina hadhi maalum kwa wale ambao na nini. (Makofi)

Kwa hiyo mimi nazani labda tu kama mlivyotoa mapendekezo kwamba kutoa elimu, tutatoa semina. Napenda niwahakikishie kwamba na tutawashirikisha wana diaspora wenyewe siku hizi wanatuambia msitusemee tulete tuseme wenyewe, kwa hiyo, tutawaleta na tutakuwa na semina. Naomba nisisitize kwamba hili kwa kweli Wizara inalichukulia kwa umuhimu wake na lipo shirikishi na tutakuwa na hiyo semina ukituruhusu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho pengine Sera ya Mambo ya Nje; napenda kurudia kulihakikishia Bunge lako tukufu kwamba Wizara imekamilisha mchakato huu wa Sera ya Mambo ya Nje ambayo inazingatia mabadiliko ya hali ya sasa na tunatarajia katika mwaka ujao wa fedha hii sera itakuwa imepita ianze utekelezaji. Kama nilivyosema sera hii imejumuisha masuala mapya ambayo ni pamoja na uchumi wa kidigitali kama nilivyosema sasa hivi tunajikita kwenye digital diplomacy, lakini pia inazingatia masuala ya mazingira na mabadiliko ya tabia nchi, lakini pia uchumi wa bluu.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tumepitisha sera yetu ya mwaka 2001 kulikuwa hakuna dhana ya uchumi wa bluu. Kwa hiyo sasa sera yetu nayo itajikita katika uchumi wa bluu, lakini pia kukuza Kiswahili kama lugha ya kidiplomasia na biashara. Pengine kuhusu kukuza Kiswahili, Waheshimiwa Wabunge nasema kubwa zaidi na naomba mtusaidie Watanzania hawachangamkii fursa, nchi za jirani zinachangamkia. Kwa hiyo, sisi kama Wizara tunawabeba kama juzi nilivyosema nilikuwa na Malabo, Equatorial Guinea tumewabeba kuhakikisha kwamba katika kikao hicho tuna wakalimani, wasije wakapata sababu kwamba hawapo. Lakini tunasema kwa pamoja kwa kweli tuchangamkie fursa, majirani zetu wanaenda mbio na sisi tuende mbio. Balozi zetu zimeanzisha vituo, juzi nimefungua Kituo katika Ubalozi wetu wa Seoul, Jamhuri ya Korea na nimeweza kutoa vyeti kwa wanafunzi 300 wa Korea waliyojifunza Kiswahili. Lakini pia ndiyo nasema kuna mwalimu mmoja, tumekuwa tunatafuta, Balozi wetu anahangaika lakini bado kwa hiyo mimi ninasema tuchangamkie fursa na Afrika ya Kusini kwenye Balozi yetu nao wamefungua kituo cha kuweza kutoa mafundisho ya Kiswahili, kwa hiyo fursa zipo tuzichangamkie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwishoni nimalizie kwa kusema katika masuala ya utawala na maendeleo ya watumishi kuna swali lilitokea kuhusu kulipa mafao yao. Naomba nilihakikishie Bunge hili kwamba mafao yote sasa hivi ambayo yalikuwa yamechelewesha yanalipwa na mengine yanafanyiwa uchakataji kwa hiyo naangalia sasa katika mwaka ujao wa fedha tutakuwa tumemaliza mafao ambayo watumishi walikuwa hawajalipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ruhusa yako naomba nimalizie kwa kusema kuhusu kuridhia mikataba; kuhusiana na Serikali kuridhia mikataba mbalimbali iliyosaini, naomba kulitaarifu Bunge lako kuwa Wizara itaendelea kufanya kazi kwa karibu na Wizara na Taasisi nyingine za Serikali ili kuhakikisha kwamba Serikali inaridhia mikataba yenye maslahi ya Taifa na kutokana na Mwongozo wa Kamati yetu tayari tulishakuwa na kikao maalum cha kupitia mikataba yote ambayo tulisaini, hatujaridhia au mikataba ambayo hatujasaini na sasa hivi kwa kukaa na wenzetu wa Wizara za Sheria na wengine kwa hiyo mikataba hii ninapenda kukuhakikishia Bunge lako kwamba inafanyiwa kazi kwa manufaa ya Taifa letu.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo napenda kuwashukuru tena kwa kunisikiliza, ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tena kutoa hoja, ahsante sana. (Makofi)

(Hoja imetolewa Iamuliwe)

WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru tena kwa kunipatia nafasi hii ya kuweza kutoa na kufanya majumuisho ya mjadala uliokuwa unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na kupitia kwako kumshukuru Mheshimiwa Spika kwa kuongoza na kusimamia mjadala wa bajeti yetu kwa umahiri sana. Nawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kushiriki mjadala huu, maoni, michango na ushauri uliotolewa yataiwezesha na kuisaidia Wizara yangu kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee naomba kuishukuru tena Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu, Mbunge na Wajumbe wote wa Kamati kwa kuipatia wizara yetu ushirikiano mkubwa na kwa michango yao ambayo mizuri sana, ambayo wameitoa katika mjadala huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba muda nilionao ni mfupi, lakini niwatambue sio kwa majina, lakini niwatambue na kuwashukuru kwa njia ya pekee Waheshimiwa Wabunge waliochangia hoja niliyoitoa leo asubuhi, jumla ya Waheshimiwa Wabunge 25 wamechangia kwa kuzungumza na pia Waheshimiwa Wabunge wengine wamewasilisha michango yao kwa maandishi, naomba niwashukuru sana, sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezitoa zimejibiwa kwa ufasaha muda mfupi uliopita na Naibu Waziri wangu Mheshimiwa Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk, Mbunge, nichukue tu fursa hii kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa hoja zote na maoni ya Waheshimiwa Wabunge zilizotolewa zitazingatiwa na zimepokelewa kwa moyo mkunjufu na zitazingatiwa na Wizara katika kuboresha utekelezaji wa majukumu ya Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ambazo hazitapata majibu ya kutosheleza katika hitimisho langu tutazijibu na tutaziwakilisha katika Ofisi ya Bunge kwa maandishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze katika kutoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezitoa; kwanza kabisa nitambue mchango wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nje, Ulinzi na Usalama. Maeneo waliyoyagusia ambayo mengi yao pia yamegusiwa na Wabunge, kubwa zaidi niseme ni suala la kuhusu majengo; kuhusu kuwekeza katika vitega uchumi katika kujenga ofisi za balozi zetu na makazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba katika mwaka wa fedha 2021Wizara imetenga shilingi bilioni 20 kwa ajili ya kuendeleza viwanja na ukarabati wa majengo balozini. Hadi kufikia sasa Wizara ilitoa kazi ya usanifu na uandaaji wa mahitaji ya ukarabati wa majengo ya balozi mbalimbali kupitia kwa Mshauri Elekezi Chuo Kikuu cha Ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari mshauri elekezi ameshawasilisha mchoro na makisio ya gharama kwa ajili na ukarabati wa majengo wa Balozi zifuatazo; moja ambayo imekuwa inasemeka muda mrefu sana ni Ubalozi wetu Mascut - Oman. Ujenzi wa jengo la Ubalozi na makazi ya Balozi Mascut ambao utagharimu shilingi trilioni 3.6 zimeshatengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Ubalozi wetu wa Nairobi ujenzi wa jengo la ubalozi shilingi trilioni 3.9 na pia Kinshasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, asubuhi hii Wabunge waliongelea kuhusu ujenzi wa jengo la ubalozi na kitega uchumi Kinshasa DRC; fedha tayari imeshatengwa na pia, Moroni - Comoro kuhusu ujenzi wa jengo la ubalozi tayari pia fedha imetengwa karibu shilingi trilioni 1.8.

Vilevile Wizara inafanya ukarabati wa jengo la ofisi ya Mambo ya Nje ya Zanzibar kama ilivyoelezwa, shilingi bilioni tatu badala ya trilioni tatu samahani nilikuwa namaanisha bilioni sio trilioni, shilingi bilioni tatu. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, iliongelewa kuhusu jengo la ofisi yetu Zanzibar ambayo Naibu wangu ameieleza, lakini napenda nilihakikishie Bunge kwamba, ukarabati wa jengo hilo umeanza. Pamoja na ukarabati wa jengo la Ubalozi wetu Washington DC ambalo ukarabati wa jengo hilo unategemea utagharimu kiasi cha shilingi bilioni 5.8 na unatarajiwa kukamilika hivi karibuni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nieleze tena pia, kuna Mpango wa mwaka 2018/2032 wa ujenzi, ununuzi na ukarabati wa majengo ya ofisi na makazi balozini ambapo Wizara inatenga fedha za maendeleo kwenye bajeti ya Wizara kila mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, imeongelewa sana kwamba tumekuwa tunatenga hizi fedha kwenye bajeti, lakini hatupati, lakini napenda kushukuru Wizara ya Fedha imetuona. Wametenga karibu shilingi bilioni 20 ambazo zitatusaidia kuweza kukarabati hayo majengo na kujenga mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja kwamba, Serikali ikamilishe mchakato wa kuandaa sera ya mambo ya nje; kama alivyoeleza Naibu Waziri wangu, hii rasimu imekamilika, kinachosubiriwa sasa ni kuweza kuridhiwa na mamlaka katika mwaka huu tutakuwa tumeikamilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, sera hii ina sehemu kubwa ya diaspora kwa hiyo, sera ya diaspora itakuwa sehemu ya Sera ya Mambo ya Nje. Nataka kuihakikishia Bunge Tukufu kwamba sera hii kwa kweli haitamaliza mwaka huu tutakuwa tumeimaliza. Hii ni kwa kutambua umuhimu wa diaspora katika kuchangia maendeleo ya nchi yetu, masuala ya diaspora kwa kweli yanapewa kipaumbele na kama alivyosema Mheshimiwa Kimei, mimi nilikuwa mdau sana, nimekuwa mdau sana wa masuala ya diaspora na nitahakikisha kwa kweli kama sikutunguliwa suala la diaspora kwa kweli nitaipa umuhimu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na niseme pia kuhusu uraia pacha, hili ni suala lilishafanyiwa kazi kweli, iliyopo tu ni maamuzi ya kisera liweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hoja ya kwamba, Serikali iweke mpango mkakati wa kushughulikia changamoto ya muda mrefu ya uchakavu wa uhaba wa magari, hususani katika balozi zetu; naomba kukuhakikishia kwamba changamoto hii tayari tumeishughulikia Wizara imepata kibali kutoka Ofisi ya Waziri Mkuu kununua magari 67 katika mwaka huu wa fedha. Tayari fedha zimeshatumwa kwenye balozi zetu 18nje, kuweza kununua magari na bado tunaendelea kufuatilia magari mengine ambayo tumeagiza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imeanza pia, kupeleka vituoni watumishi 137 katika kipindi hiki. Tumesikia kilio cha Waheshimiwa Wabunge kuhusu balozi zetu kwamba hazina watumishi.

Sasa mimi nitumie pia nafasi hii kuweza kuishukuru Wizara ya Fedha. Wizara ya Fedha imetuwezesha, tutapeleka watumishi 137 katika mabalozi zetu na tumezingatia weledi, tumezingatia uzoefu na tumezingatia ujuzi, kwa hiyo, sio kupeleka tu. Lakini kwa kweli tutakuwa tumeziimarisha balozi zetu na kila tunapopata rasilimali zaidi ya fedha, tutakuwa tunawaongezea uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, iliongelewa asubuhi hapa pia kwamba Wizara yetu iweze kufuatilia baadhi ya Wizara za kisekta, ambazo zikifanya kazi kwa juhudi na ufanisi zitaongeza pato la Taifa, kwa kusimamia uzalishaji wa mazao ya kilimo na mifugo ambayo yana soko kubwa nje ya nchi kama vile, nyama ya mbuzi katika masoko ya nchi za Kiarabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwaambie Wabunge kwamba, ushauri umepokelewa na unazingatiwa, lakini pia ulishaanza kufanyiwa kazi. Niwashukuru pia Mawaziri wenzangu kutoka hizi Wizara za kisekta, tumekuwa na ushirikiano wa karibu, tukiwa na ugeni tunakaa pamoja kimkakati na kuweza kuweka yale maslahi, ambayo kila sekta inaona inaupa kipaumbele, kwa hiyo, tunafanya kazi kwa karibu sana na sekta zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, pia katika ushirikiano huu Wizara ilifanikisha upatikanaji wa vibali kwa kampuni nane za Tanzania kuuza minofu ya samaki aina ya sangara katika nchi ya Saudi Arabia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Serikali kuzidisha juhudi kusimamia balozi zetu za nje, kutangaza fursa za kitalii na vivutio mbalimbali zilizopo nchini kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii, tumepokea ushauri huu na kwamba utazingatiwa, lakini niwahakikishie kwamba tayari Balozi zetu kwa kweli zinafanya mambo mengi makubwa sana katika kuvutia utalii na kama mtakumbuka tulieleza hapa asubuhi kwamba mathalani balozi zetu zimepeleka sampuli za zao za korosho, lakini pia ubalozi wetu wa Malaysia umeweza kufanikisha kwamba ndege ya Malaysia inaweka matangazo ya utalii wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na hoja mbalimbali kuhusu Wizara iendelee kuwapa viwanja mabalozi wa nje hapa Dodoma, kwa ajili ya kujenga ofisi na makazi ili balozi zihamie hapa. Napenda kukufahamisha kwamba Serikali tayari ilishatoa viwanja Jijini Dodoma kwa balozi zote na tayari ilishatoa hati kwa balozi zote zinazowakilishwa nchi zao hapa nchini. Kwa hiyo, sisi ni kuhamasisha kwamba wajenge ili waweze kuhamia makao makuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, iliulizwa pia kwamba Wizara ihakikishe inapeleka taarifa za kutosha ubalozini kuhusu mazao na fursa za biashara ili kufanikisha utekelezaji wa diplomasia wa uchumi. Kama nilivyoeleza hapo awali kwamba Wizara imeendelea kushirikiana na Wizara za kisekta na taasisi za biashara za sekta binafsi nchini kutafuta masoko ya mazao ya kilimo, mifugo na uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia imeshiriki pamoja na TANTRADE katika maonesho mbalimbali ya kibiashara. Kwa hiyo, balozi zetu zimepeleka sampuli za zao la korosho kwa ajili ya kuwasilisha katika nchi mbalimbali ikiwemo Vietnam, India na China. Aidha, balozi zetu zote zimeendelea kutangaza bidhaa za kimkakati zinazopatikana Tanzania. Vilevile Wizara imeendelea kuhamasisha taasisi za Serikali zinazohusika na biashara, kushirikiana na sekta binafsi kushiriki katika maonesho mbalimbali ya Kimataifa, ambayo yanatoa fursa kwa nchi kutangaza bidhaa zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara pia, imeendelea kufungua of course Balozi mpya kama ilivyoelezwa na mwenzangu. Lakini nisisitize pia kwamba kwa kipindi hiki Wizara ipo katika hatua za mwisho kufungua consul kuu huko Guangzhou nchini China, niwahakikishie kwamba tuko katika hatua za mwisho. Pia Lubumbashi Jamhuri ya Demokrasia ya Congo baada ya kupata vibali kutoka katika nchi husika, maana yake katika kufungua hizi consul au balozi, lazima mpate pia kibali kutoka kwenye nchi zinazohusika. Hamuwezi kwenda mnaingia tu mnasema tumefika tunaanzisha na wenyewe inabidi watukubalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kama sisi kwa upande wetu tumeshamaliza mchakato huo, lakini tunasubiria hizo nchi husika na wenyewe waweze kuturuhusu wamalize mchakato wao, kusudi tuweze kufungua hizi balozi. Nina imani haitapita mwaka huu kabla hatujazifungua hasa Guangzhou na Lubumbashi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo mengine of course yameongelewa kuhusu kutangaza Kiswahili na kupeleka walimu na kufundisha lugha hiyo nje ya nchi, tayari mikakati hii imefanyika. Balozi zetu zimejipanga, tayari vyuo vikuu vya nchi za SADC karibu nyingi sana zimeanza mtaala/curriculum ya Kiswahili. Kwa hiyo, sasa iliyopo ni sisi huku wenyewe kujipanga na walimu wakaweza kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maana nilikuwa juzi Afrika Kusini wameniambia Afrika Kusini tayari vyuo vyao vimeshaanzisha tayari curriculum ya Kiswahili. Botswana imeanza, Lesotho inaanza, lakini shida ni kwamba walimu wako wapi. Kwa hiyo, sisi tunaomba tushirikiane na sekta zote zinazohusika tuweze kuwapata walimu waende kufundisha Kiswahili kwenye hizo nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kuhusu hili suala la Wizara kwamba iweke mkakati of course niliyosema ya kutangaza utalii nimeshaiongelea. Lakini niseme pia kwamba juhudi zinaendelea kwa mfano, Ubalozi Tanzania nchini Malaysia kama nilivyosema imeshawishi Kampuni ya Ndege ya Lion Group Air ya nchini Indonesia inayomiliki zaidi ya ndege 350 kuweka video kwenye ndege zao zinazoonesha utalii wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilimsikia Mbunge hapa nakumbuka mimi nilikuwa mmoja wa mwanachama wa Mozambique na Tanzania, kile chama kitafufuliwa Mheshimiwa Mbunge, maana mimi nilikuwa mjumbe, nilikuwa kwenye bodi lakini kwa uhusiano wetu wa Mozambique tena uko karibu sana na kutokea na yale yanayotokea Mozambique nadhani hiko chama kinahitajika sana, kutoa msukumo na kuweza kusimamia yanayoendelea katika nchi ya rafiki yetu hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nikuhakikishie hayo ya DRC hatuna tatizo kabisa kama ninavyosema tunamalizia mchakato wa kufungua hiyo consul kuu nchini Lubumbashi kwa ajili ya kuendeleza mahusiano ya biashara, lakini najua tena kuna mambo mengi kati ya DRC na Kigoma. Kwa hiyo, tunayatambia na tuna consul kule ya DRC, kwa hiyo, wanataka nao kuanzisha mahusiano hayo. Kwa hiyo, kwa kweli tutaendeleza na kwa mchango wenu kwa kweli mimi naona kwamba kuna fursa nyingi sana ambazo saa nyingine wengi hawazifahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sijui nina muda gani, lakini naomba kwa hitimisho niruhusu kwamba baada ya maelezo hayo, ninaliomba Bunge lako Tukufu lipitishe na kuunga mkono bajeti ya Wizara yangu kwa mwaka 2021/2022 ili niweze kutekeleza yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, tunapende kutekeleza ipasavyo masuala yote yaliyoainishwa katika Sura ya Saba ya Ilani ya CCM yam waka 2020/2025 inayohusu mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa.

Pili, tuko tayari kutekeleza majukumu ya msingi ya Wizara kama ambavyo Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mkazo aliouweka katika hotuba yake hapa Bungeni tarehe 22 Aprili, 2021 ambapo ndio msingi wa mpango wa bajeti niliouwasilisha. Vipaumbele hivyo ni pamoja na kuimarisha na kukuza uhusiano na mataifa mengine pamoja na jumuiya za kikanda na taasisi za kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, tumejipanga kuimarisha utendaji kazi wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki pamoja na balozi zetu zote zilizoko nchi mbalimbali. Yale yote ambayo tumepata hapa leo kwa kweli itasaidia sana katika kujipanga na kuweza kuimarisha utendaji wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, tutaendelea kushirikiana na Wizara za kisekta na sekta binafsi katika kutangaza vivutio vyetu vya utalii, kuvutia uwekezaji na kutafuta masoko ya bidhaa zetu nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, nne, tutaendelea kushiriki kikamilifu kwenye shughuli za Kimataifa ikiwemo ushiriki wa Tanzania kwenye kulinda amani duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba yale yote ambayo wameyasema tumeyachukua hasa yale ambayo wametaka kwa mfano, Zanzibar kwamba tuwe tunawapa taarifa mapema kuhusu ushiriki wao katika hii mikutano ya kikanda, lakini pia kuweza kuangalia nafasi za ajira watu wetu waweze kufanya na wenyewe kazi nje, lakini pia kuweza kuwapeleka watu wetu waweze kupata ujuzi na uzoefu kutoka katika nchi za nje hasa katika mahusiano yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, Wizara yangu imeongeza kasi ya kutekeleza majukumu yake kwa kufanya maboresho makubwa ili kufikia malengo yake pamoja na matarajio ya Watanzania. Hivyo kwa timu niliyonayo na kikosi nilichoongezewa na Mheshimiwa Rais, naomba Bunge lako lituunge mkono na kutupitishia bajeti niliyoiomba ili tukachape kazi, kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kutoa hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. BALOZI LIBERATA R. MULAMULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa hii niweze kuchangia kwenye hoja iliyoko mbele yetu. Nimefuatilia kwa umakini sana wasilisho la Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji na mjadala unaoendelea niseme tu kwamba wasilisho lake ni zuri sana. Linatupa mwanga wa mbele tunapokwenda na kutupa matumaini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake wa kuiondoa mipango katika Wizara ya Fedha na kuiweka chini ya Ofisi yake. Niseme katika nchi zilizoendelea mipango ndiyo huwa inaelekeza, inaongoza hazina na siyo vinginevyo. Nimefurahi sana kuwaona Waheshimiwa Mawaziri hao wawili Mheshimiwa (namwitaga pacha) Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo wakiwa wameketi pamoja kama mapacha kwa kuwasilisha Mpango wa Maendeleo na Mtazamo wa Bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile ni mara yangu ya kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Kitila Mkumbo kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kuongoza Wizara hii. Kama wengi walivyosema ni msomi mwenye upeo na mawazo mapana, ana uwezo mkubwa na ushawishi mkubwa. Kwa hiyo, sifa zote hizi niseme ni muhimu sana kwa Waziri wa Mipango na sifa hizi zinaonekana pia katika wasilisho lake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kusikiliza wasilisho la Mheshimiwa Mkumbo na Mpango wenyewe niseme nimevutiwa na mambo matatu. Moja ni kuhusu maendeleo vijijini, lakini ya pili ni mabadiliko ya tabianchi, ya tatu ni uchumi wa kijani na uchumi wa buluu (green economy and blue economy). Najua wamegusa maeneo mengi lakini nasema maeneo haya matatu yakisimamiwa vizuri yanaweza kuwatoa Watanzania wengi kwenye wimbi la umasikini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia nimesikitishwa kwamba Mpango huu bado haujaupa umuhimu wa kutosha shughuli za utafiti na maendeleo (research and development) imepewa pesa kidogo sana chini ya Sekta ya Elimu ambayo ni kama 0.003% wakati lengo ni kuwa na 1% ya pato la Taifa. Bahati nzuri nimekaa hapa na Mheshimiwa Profesa Mkenda na ninaamini kwamba na yeye pengine ana uchungu kuona kwamba Sekta hii imepewa hela kidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi bahati nzuri nimekuwa kwenye vyuo vikuu kwa Chuo Kikuu cha George Washington University na nikatumia muda pia kwenye Massachusetts Institute of Technology nikiona wenzetu hela kubwa sana inaenda kwenye R and D. Kwa hiyo, wito wangu kwamba Mheshimiwa Profesa Mkumbo kwa kweli hii muipe umuhimu sana ili tutoboe. Hii kwa kweli hatuwezi kuendelea kuipa peanut. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema nimevutiwa maeneo matatu muda ukinitosha nitaweza kuyaongelea lakini nianze na kuhusu maendeleo vijijini. Tumesikia shule nyingi zimejengwa, vituo vya afya vimefunguliwa, maji yanasambazwa, mambo mazuri sana na kwa lugha nyepesi tuseme Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameonyeshwa kuguswa sana na wananchi vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeguswa pamoja na kwamba nimekuwa na nyadhifa mbalimbali nimekuwa nimekaa nchi za nje lakini mimi ni mtoto wa kijijini kama pengine walivyo wengi hapa na nilikuwa najiita I am a rural girl kwa hiyo, nafuatilia sana. Mzee wangu marehemu Mheshimiwa wakati ule marehemu sasa Novat Rutageruka alikuwa akisema, “Ukitaka kupima maendeleo tumefikia wapi tumetoka wapi, tumefika wapi angalia hali ya kijijini.” Kweli alikuwa ananiasa kila wakati anasema nakusikia kwenye mihadhara huko na watu wa World Bank mnatoa takwimu, mnazipata wapi mbona hamtuulizi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nasema naguswa sana na hali ya umasikini of course na maendeleo vijijini yanayoendelea na ninaamini kama tutajielekeza kuwapa maarifa na mtazamo wanavijiji baada ya kuwapelekea hizi huduma mbalimbali. Tumesema sasa hivi vijiji vingi vimepata umeme, minara ya mawasiliano imesambazwa lakini wanaitumiaje katika kupata maendeleo ambayo tunayataka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kijijini kwetu sehemu imeweza kupata umeme lakini kwa watu wetu umeme ni taa na sisi ni watu ambao siyo kama watu wa Kilimanjaro siyo watu wa biashara sana kwa hiyo mtu anafurahia na anawasha taa pengine anaweka na TV. Nadhani wananchi wetu wanataka elimu tuwaelimishe kwamba huu umeme waanzishe viwanda vidogo vidogo, waongeze thamani kwenye mazao yao katika maeneo waliyonayo na hiyo BBT nasema kwamba hiyo BBT ya kilimo ipelekwe pia kwenye masuala haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nilikuwa natoa ushauri tu kwamba pengine tufikirie kuanzisha Mamlaka ya Maendeleo Vijijini (Rural Development Authority). Maana yake huko nyuma tulikuwa na Wizara zinazohusika na maendeleo vijijini. Nchi zilizopiga hatua kwenye maendeleo vijijini nyingi zina Wizara na taasisi hizi. Sasa sisi shughuli hii imesambaa kwenye TAMISEMI, Wizara mbalimbali kwa hiyo inakuwa ni vigumu katika kuratibu. Kwa hiyo mimi naamini pengine Mheshimiwa Profesa Kitila anaweza akamshauri Mheshimiwa Rais kuangalia uwezekano wa kuanzisha Rural Development Authority, namuona ana-note kwa hiyo nadhani umelipata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tabianchi pia haina mwenyewe na yenyewe. Mabadiliko ya tabianchi na yenyewe muangalie jinsi gani inaweza ikawa na taasisi mbali na NEMC ya kuweza kuangalia maana yake ni eneo kubwa zuri sana hasa tukiangalia katika carbon credit. Sasa hivi mkutano wa COP 28 unakuja, itatoka maazimio mengine nani anayachukua? Kwa hiyo, nadhani itakuwa vizuri pia katika kutazama uchumi wa green economy. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nadhani itakuwa vizuri pia kuwa na hiyo katika kutazama green economy. Mambo ya uvuvi yameongelewa, lakini nasema hiyo ni sehemu ambayo kwa kweli hatujaitendea haki. Uvuvi tunauona kama ni wa watu maskini lakini ndiyo potential kubwa iliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabla hujanigongea kengele nyingine, niseme uchumi wa blue nao kwa kweli tujifunze mengi kutoka Zanzibar kwamba wameanzisha Wizara inayohusika na uchumi wa blue. Hii ni kweli kuna fursa nyingi sana ambazo hatujazitendea haki. Maana yake nayo imesambaa katika Wizara mbalimbali na sekta mbalimbali. Tuondokane na dhana ya sector approach. Profesa Mkumbo tuondokane na sector approach tutazame dhana ya uchumi in a holistic manner. Kwa namna hiyo nadhani itaweza kuleta yale ambayo tunatarajia kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naomba nimpongeze Mheshimiwa Tulia Akson kwa kuchaguliwa kuwa Rais wa IPU. Ushindi wake umenipa hamasa kwamba mgombea wa nafasi ya Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Madola kwamba inawezekana. Tukijipanga vizuri na kutumia ushawishi wetu mkubwa kidiplomasia na Kimataifa aliotujengea Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan. Naomba mniunge mkono, ahsanteni sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa balozi umesema tukuunge mkono au umeunga mkono?

MHE. BALOZI LIBERATA R. MULAMULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.

MWENYEKITI: Sawa.

MHE. BALOZI LIBERATA R. MULAMULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo yote, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)