Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Humphrey Herson Polepole (6 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia na kwa sababu ni mara yangu ya kwanza namshukuru sana Mungu wa Mbinguni kwa kunipa nafasi hii. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kunipa heshima ya kuwa sehemu ya Bunge hili tukufu, nami nawaahidi Watanzania lakini pia Bunge hili kuendelea kuchapa kazi ili tuweze kufikia malengo ya Watanzania kama ambavyo wanatarajia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia hotuba aliyoitoa Mheshimiwa Rais katika Bunge hili la Kumi na Mbili lakini nikirejea hotuba aliyoitoa katika Bunge la Kumi na Moja na nitajielekeza katika mambo matatu. La kwanza ni kuhusu viwanda vidogovidogo, vya kati na vikubwa. Mheshimiwa Rais ameeleza katika hotuba yake umuhimu wa viwanda na mchango wake mkubwa katika kutengeneza ajira zaidi hapa Tanzania na tukitazamia ajira milioni nane ambazo Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi inalenga kuzitengeneza katika miaka hii mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu kwa Serikali; tukiunganisha viwanda vidogo vidogo na vya kati na Sekta ya Kilimo kuna faida kubwa sana na tutaweza kuona tija ya viwanda hivyo. Natoa mfano mmoja; mahitaji yetu ya mafuta ya kula hapa Tanzania sasa hivi ni wastani wa tani laki tano na uzalishaji wetu wa ndani wa mafuta ya kula ni wastani wa tani laki mbili na nusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali ikifanyia kazi yenyewe na kwa kushirikiana na Sekta Binafsi pale inapowezekana na pale isipowezekana Serikali yenyewe ichukue dhamana hii kushirikiana na wananchi kutengeneza viwanda vidogo vidogo na vya kati katika maeneo wanapolima alizeti na mawese, ili wakulima ambao wamekosa fursa ya kuuza mazao haya ya alizeti na mawese kwa muda mrefu wawe na soko la uhakika kwa sababu kuna viwanda vya kuchakata alizeti na mawese na kutengeneza mafuta na hatimaye mafuta haya yatapata soko kwa sababu mpaka sasa hivi tuna nakisi ya mafuta ya kula wastani wa tani laki tatu. Maana yake wakulima watapata fedha yao, viwanda hivi vilivyowekeza na Serikali vitarejesha fedha yake na kujiendesha kwa faida, lakini pia walaji watapata mafuta.

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu; ingependeza sana baada ya kuwa tumefikia kiwango kikubwa cha kuzalisha mafuta nchini, kama zilivyo nchi zingine ambazo zina sera za kulinda masoko ya ndani, (protectionist policies), tuseme marufuku sasa kuagiza mafuta kutoka nje kwa sababu tunazalisha hapa hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ni kuhusu uvuvi; Mheshimiwa Rais ameeleza vizuri sana kuhusu uvuvi wa bahari kuu na katika maziwa yetu makuu ikiwemo ununuzi wa meli, vifaa vya kufanyia uvuvi wa kisasa na kadhalika. Rai yangu kwa Serikali; tulitazame sana Ziwa Victoria na tufanye uvuvi wa kisasa wa vizimba (aquaculture fish farming). Serikali kupitia halmashauri zetu zishauriwe wawekeze kwenye uvuvi wa vizimba (aquaculture fish farming), ni uvuvi wenye faida kubwa na tija kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi mahitaji yetu ya sato hapa nchini bado ni pungufu. Tukiwekeza katika Ziwa Victoria kwa vizimba na tukafuga samaki sato wengi zaidi si tu tutaongeza mapato ya wale ambao wamewekeza wakiwepo watu wa halmashauri, tutaongeza lishe kwa watu wetu wa Tanzania lakini pia tutauza nje sato hao kwa sababu hata katika eneo la maziwa makuu, bado uwekezaji katika ufugaji wa samaki kupitia vizimba haujafanyika vizuri sana. Kwa hiyo tutaongeza pia fedha za kigeni kwa maana hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni ufugaji. Hapa niseme tu kwa ufupi kwamba kazi nzuri imefanyika. Sisi tunaongoza kwa kuwa na ng’ombe wengi Afrika na hili limeelezwa vizuri sana katika hotuba ya Mheshimiwa Rais. Rai yangu mimi, kitu kimoja hatujafanya vizuri; ufugaji wa sasa ni wa kuhamahama, unafanya tija ya ng’ombe ishuke. Kama tukiwekeza kwenye mashamba ya kulima majani, chakula cha ng’ombe (hay) ambapo sasa hivi kwa utafiti niliyoufanya kuna mashamba mawili tu, nafikiri moja liko kule Mbeya. Kama tukilima hay tukawapatia wakulima, ng’ombe wao hawatahitaji kutembea kila mahali na kuleta migogoro kati ya wakulima na wafugaji. Hata hivyo, hay ikilimwa vizuri hapa Tanzania tukaweka mashamba mengi zaidi ya hay, hay ni fursa kubwa na uwekezaji huu utaweza kutuwezesha sisi kuuza hay kwenda nje ya nchi kwa sababu ni zao ambalo linahitajika sana, si tu hapa Tanzania lakini nchi za nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo matatu nigusie moja ambalo limesemwa na wengi, lakini nami niongezee tu kwa uzito. Mwaka 2000 kiongozi wa UAE, Al-Maktoum alifanya uamuzi wa kununua ndege 59 za Shirika la Emirates. Mwaka kati ya 2000…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mchango wangu nitauwasilisha kwa maandishi. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mimi naomba kuungana na Wabunge wenzangu kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa mwaka 2021/2022 na 2025/2026 na nitapenda kujikita katika maeneo manne kwa ufupi.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ni ukweli usiopingika ya kwamba ulimwenguni biashara ndogo ndogo, biashara ndogo na biashara za kati ndizo zinachukua asilimia kubwa ya uchumi ulimwenguni. Kwa lugha ya Kiingereza Micro small and medium enterprises ndizo ambazo zina-constitute most of the economies Ulimwenguni, na neno biashara, ukisema enterprises kama ni biashara, lakini nikisema enterprises inaweza kuwa kampuni ndogo enterprises inaweza kuwa mradi fulani wa uzalishaji enterprises inaweza kuwa shughuli ambayo mtu anaifanya kujiletea kipato. Nitatumia neno enterprises nikimaanisha kwa maana ya tafsiri hiyo pana.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wote waliofanikiwa ulimwenguni ma-bilionea ma-trilionea kwa mtindo huo wote walianza kama micro entrepreneurs ama unasema small entrepreneurs. Mimi ushauri wangu kwenye mpango, tujikite sana kwenye kuwezesha micro-small and medium enterprises kwasababu hawa ndio injini ya uchumi wowote na ikiwepo hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa takwimu za tangu mwaka 2010 micro small medium enterprises zilikuwa kama 2,700,000, kwa maana ya wale ambao wamezianzisha; lakini kwa sera yetu hapa Tanzania ukitazama tafsiri wanasema micro enterprises ni zile ambazo zinawamiliki chini ya watano halafu wale wanaokuwa small wanakuwa watano mpaka hapo mbele kumi, halafu wale wakubwa wanaanzia kumi na kuendelea mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa Tanzania watu wengi wanaosimama katikati ya ama mazao ya shambani na bidhaa inayokwenda kutumika nje ni hawa watu wa Micro small and Medium Enterprises. Iwapo tukiwawezesha vya kutosha hili ni eneo lingine kubwa sana la kikodi ambalo linaweza kuchangia vikubwa sana katika Pato letu la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachotakiwa kufanyika, kwanza, ni kuwatambua watu hawa. Watu wengi katika eneo hili bado siyo rasmi wanasema ni informal sector lakini kimsingi ajira karibia zote, kwa takwimu za mwaka 2010 Micro, Small and Medium Enterprises peke yao walikuwa wana-constitute kwa zaidi ya 31% ya ajira zote hapa Tanzania na hawa ni watu milioni 2,700,000 peke yake. Kama tungekuwa tumewafanya wawe mara mbili maana yake wakawa kama milioni 6 hivi wale waanzishaji wa biashara, nazungumzia biashara hizi zote kwa maana kuanzia Micro, Small and Medium ni wale wenye kipato kisichozidi bilioni 1 basi tungeweza kuona ajira zaidi ya 70% zinatoka katika eneo hili la biashara hizi ndogo ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu kwa Serikali tuwapatie uwezeshaji bila mizengwe, milolongo mirefu na bureaucracy. Utaratibu ambao tayari Serikali imeanza kuufanyia kazi ni mzuri sana na umekuwa na matunda ni kuwatambua Watanzania. Sasa hivi asilimia kubwa ya Watanzania wana vitambulisho vya NIDA. Kitambulisho cha NIDA unaweza ukamfahamu mtu jina lake ukiacha taarifa zile za msingi lakini unaweza kufahamu anatoka wapi, ana shughuli gani na tukiendelea kuboresha tunaweza hata kupata taarifa za kifedha na za kibenki za kila Mtanzania; benki yake ni wapi, anashughulika na jambo gani. Kwa hiyo, tutakuwa tumewaondoa watu hawa wengi kwenye Micro, Small and Medium Enterprises kwenye kigingi kikubwa cha kupata uwezeshaji wa kifedha kwa msingi wa collateral ama wanasema dhamana.

Mheshimiwa Naibu Spika, si kila Mtanzania atakuwa na hati ya nyumba rasmi ya kwenda kupata mkopo lakini siku hizi kwenye masoko ya kileo ya mikopo tumeanza kuzungumza kuhusu mbadala wa collateral kwa maana ya dhamana ile ya kidesturi kama hati ya nyumba kwa kuanza kutoa ama mikopo midogo midogo ama kutumia utambulisho ambao hauna shaka. Sasa hivi ukitumia kile kitambulisho chako cha NIDA na tukiweka vizuri zaidi watu wetu wa TEHAMA Serikalini, inawezekana kujua mwenye kitambulisho hiki cha NIDA amekopa mkopo benki kwenye eneo fulani na hajalipa au mwenye kitambulisho hiki cha NIDA ana perform mkopo wake mahali fulani vizuri zaidi. Kwa hiyo, unapokwenda kwa mkopeshaji yeyote rasmi kwa maana ya Taasisi kwa kitambulisho tu kile kinaweza kukupatia uhalali wa wewe kupata mkopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia wanaoingia kwenye soko la ajira ni zaidi ya watu milioni 1 kila mwisho wa mwaka, hawa watu wanaoingia huku ni vijana na hawa vijana hawana hati za nyumba. Kama tukiweka utaratibu mzuri wa kuwatambua wakapata vitambulisho na tukapata wanasema guarantees kutoka kwa ndugu wa karibu na ndivyo ambavyo wenzetu wa Mashariki ya Mbali, Thailand wamefanikiwa kuwakopesha watu wengi sana na kufanikiwa ni kwa sababu ya kutumia utaratibu kama huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili litatoa ajira nyingi sana. Hawa ndiyo ambao baada ya kiwanda kutoa bidhaa wao ndiyo watachakata, watasambaza kidogo kidogo; hawa ndiyo ambao mgodi ukianza ndiyo watakaokwenda kuchukua madini yatakayotolewa na kuyauza kidogo kidogo. Ushahidi upo kwenye eneo la madini hizi bilioni nyingi zimetokea ni kwa sababu tumewarasimisha wachimba madini wadogo wadogo kwa kuwawekea masoko ya madini na tumeona pesa nyingi sana imepatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ilikuwa ni kuhusu uchumi. Ni muhimu sana tukafahamu kwamba uchumi wetu umekuwa madhubuti kwa sababu tumewekeza katika ujenzi kama eneo moja kubwa na ni kigezo cha ukuaji wa kiuchumi. Ujenzi huu umesambaa nchi nzima; barabara, miundombinu ya reli, tumetengeneza meli maeneo mengi kabisa na sasa tuna Bwana la Mwalimu Nyerere na vitu kama hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia amesema lazima mambo haya yaendelee na Watanzania wanafahamu hivyo. Ujenzi mkubwa ni kigezo kikubwa sana cha ukuaji wa kiuchumi na uchumi ukikua ndiyo tutapata fedha, watu watapata ajira nyingi za muda mfupi na muda wa kati na hatimaye mwisho wa siku watu watapata kipato na wataweza kumudu maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu kwa Serikali, ziko fikra kadhaa lakini napenda kusisitiza kwamba ni muhimu tukaendelea kusimamia nidhamu ya kusimamia uchumi wetu. Tumefanikiwa sana kuufanya mfumuko wa bei kwua single digit na kuna fikra nyingi kwenye eneo hili lakini fikra moja ni bayana ni kwamba mfumuko wa bei unapokuwa chini mnufaika ni mwananchi wa kawaida na hasa mnyonge. Ndiye ambaye mkate utaendelea kuwa bei ileile ndani ya muda mrefu, ataongeza kipato lakini bei ya mkate itabaki palepale. Pia wale wakubwa wakiuza mikate mingi kwa sababu wananchi wote wanaweza kununua na wao hatimaye wanaweza kutengeneza faida kwa maana hiyo. Kwa hiyo, kuendelea kuweka nidhamu ya usimamiaji wa uchumi na hasa kuhakikisha kwamba inflation haiongezeki katika kiwango ambacho tume-maintain ni muhimu sana kwa ukuaji wetu wa kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la tatu ni masoko. Hapa Tanzania hatuna tatizo la uzalishaji, wakulima wanalima mazao kila mwaka. Kinachotakiwa sasa hivi ni kutumia mageuzi makubwa ya ki-TEHAMA kumuunganisha mkulima moja kwa moja na soko na kuondoa ukiritimba wa madalali. Wakulima wengi hawafahamiani na mnunuaji wa mwisho lakini kama hapa tungekuja na private sector wakatengeneza mifumo ya ki-TEHAMA ambayo inaweza kumwezesha mkulima akasema nina magunia 100 ya mahindi nika-post hapa kwenye application fulani halafu mtu fulani akasema nataka magunia 50 ya mahindi akaingia kwenye application hiyo wataonana kama ambavyo mifumo hii duniani ipo. Ali Baba alianza kidogo hivi mwaka 1999 yeye na mkewe na anakubaliana na hiki tunachokisema kwamba biashara ndogo sana na za kati wanaanza watu wachache. Hapa Tanzania kwa takwimu ni 2.9% tu ya biashara hizi zote za kati na hizi ndogo zaidi ndiyo zina watu zaidi ya watu watano mahali kwingine kote ni watu wachache sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ni kuhusu utawala bora na uwajibikaji. Mimi napenda kusema kwamba wakati wa msiba wa Hayati Magufuli wale watu walikuwa wanalia siyo kwa sababu Rais Magufuli ametangulia mbele ya haki, mimi nasema hapana. Wale watu walikuwa wanalia kwa sababu Rais Magufuli na Mama Samia walikuwa wana jambo lao na wananchi wale. Wale wananchi walikuwa wanalia wakionyesha concern yao kama yale ambayo Rais Magufuli na Mama Samia waliwaahidi hayo ndiyo yatakayoendelea hata wakati Magufuli hayupo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mama Samia ameeleza msimamo, amesema kazi iendelee. Rai yangu kwa Serikali, usimamizi mzuri wa rasilimali za Taifa letu unatokana na nidhamu nzuri ya viongozi wetu. Vita dhidi ya rushwa, ufisadi, matumizi mabaya ya rasilimali za umma; mambo hayo hatutakiwi kurudi nyuma kamwe, asilani! Kinyume na hapo, Watanzania wale walilia watalia na baadhi yetu humu muda si mrefu kwa sababu watasema tumewageuka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu tumsaidie Mheshimiwa mama yetu Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ili ile ndoto ambayo walituletea yeye na Mzee Magufuli, tukawaamini na tukawapenda ikatimie chini ya uongozi wake katika kipindi hiki na kwa kadri ambavyo Mungu itampendeza na yeye mwenyewe kwa maana hiyo na Chama chetu cha Mapinduzi. Umuhimu sana kuliko yote, nimefurahia sana Mheshimiwa Rais amesema kukumbuka kuzingatia haki za watu wetu na hasa wanyonge. Ni muhimu sana viongozi wakaendelea kusimamia hilo wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi. Nami naomba niungane kwanza na Wabunge wenzangu kuunga mkono kazi nzuri ambayo inafanywa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi kupeleka maendeleo kwa watu wetu wa Tanzania.

Kwa upekee mkubwa sana, napenda kumpongeza kwa dhati mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi kwa matukio makubwa ya kihistoria ambayo ameyafanya katika ziara yake ya Mwanza kwa siku tatu mfululizo. Hapa napenda kuweka msisitizo katika uzinduzi na ufuatiliaji wa miradi mikubwa ya kimkakati itakayokwenda kubadilisha maisha ya watu wetu Watanzania na hasa katika kanda ya ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ameshuhudia utiwaji saini mikataba mitano ya ujenzi wa meli kubwa katika Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika na bahari ya hindi. Meli hizi, katika uchumi kuna njia kama tatu za usafiri; ya kwanza ni usafiri wa maji; pili ni usafiri wa reli; tatu ni usafiri wa barabara; nne ni usafiri wa ndege. Zimepangika hivyo kwa maana ya unafuu wa njia za usafiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhamira njema ya Serikali ya Chama cha Mapinduzi kuwekeza zaidi katika usafiri wa kwenye maji, unadhihirisha mwelekeo mzuri wa kusafirisha mizigo mikubwa kwa bei nafuu; na hapa ninaangazia soko lote la Afrika Mashariki. Tutaweka wagon ferry pale yenye kubeba tani 2,800 maana yake hiyo ni sawasawa na kuingiza treni kama tatu hivi za mizigo zitakazotoka Tanzania kwenda Kenya au kwenda Uganda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile itajengwa meli ya kubeba uzito hivyo hivyo wa tani zaidi ya 2,800 ambayo sasa ninaona makaa ya mawe kutoka kusini mwa Tanzania mpaka bandari ya Mtwara kama alivyosema pacha wangu pale, yatatembea kwa maji kutoka Mtwara mpaka Dar es Salaam na mpaka Tanga Cement badala ya kutumia usafiri wa barabara ambao unagharimu nchi yetu fedha nyingi kwa kufanya routine maintenance. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuweka jiwe la msingi la kuzindua ujenzi wa reli ya kutoka Mwanza mpaka Isaka, reli ya kiwango cha Kimataifa, Standard Gauge Railway. Hapa nataka nimtie moyo kwamba akifika Isaka atusaidie kutafuta fedha akamilishe kipande kutoka Isaka mpaka huku Dodoma; na tutoke Dodoma mpaka Tabora - Kaliua hiyo mpaka Kigoma na tukitoka Kaliua twende mpaka Mpanda, tukitoka Mpanda twende mpaka Kalema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa kupeleka meli mpaka Kalema ni kwasababu tayari ameshaweka meli pale, itaanza kujengwa hivi karibuni na tutapitisha kwenye bajeti hii. Maana yake, meli itakayokuwa inabeba mizigo katika Ziwa Tanganyika yenyewe zaidi ya tani 2,800 itatoka Bandari ya Kalema itakwenda Bandari ya Kalemii upande wa DRC Kongo na huko ndugu zetu wale ambao hawana masoko sasa hivi, watatumia masoko yetu ya dhahabu katika eneo la Kalema na mizigo ya mbao. Kwa hiyo, meli italeta hapo Kalema tutabeba na Standard Gauge Railway na italetwa mpaka Dar es Salaam kwa kwa ajili ya kupeleka ng’ambo ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda ifahamike kwamba reli tunayoitumia sasa hivi ni narrow gauge, inaweza kubeba ujazi kama wa tani 1,200 hivi. Pia reli ya TAZARA nayo inabeba kama 1,200 mpaka 1,400 hivi. Kipindi fulani tumezungumza na balozi ya nchi ya kimagharibi sitamtaja hapa, alisema “The East Africa sub-region is too small to support two standard gauge railways,” akimaanisha Afrika Mashariki uchumi wake ni mdogo sana ku-support Standard Gauge Railway mbili kwa maana ile ya Kenya na hii inayojengwa hapa Tanzania. Yule hakuwa na dhamira njema na alikuwa muongo. Kwa sababu sijamtaja nina hakika sijakosea sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukiwa na mzigo wa tani 50 Mbeya au Kapirimposhi, Zambia unataka kuuleta Dar es Salaam, itakuchukua zaidi ya miezi sita kuusafirisha na wakati huo utakuwa umeshakosa masoko huko mbele ya safari. Kwa hiyo, kujenga Standard Gauge Railway, ndiyo njia muafaka ya kuchagiza na kuchochea ukuaji wa kiuchumi katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshmiwa Mwenyekiti, napongeza pia kazi kubwa ameifanya alipotembelea daraja la Kigongo, Busisi. Jana Mheshimiwa Kanyasu alisema vizuri sana kwamba wale ambao wamekuwepo pale wanaweza wakaelewa tatizo lililokuwepo sasa hivi la kutumia vivuko vya maji. Wakati mwingine foleni pale ni masaa matatu kuvuka, lakini sasa tunabadilisha maisha ya watu kwa kuvuka kwa dakika nne tu. Hilo ni jambo kubwa sana katika ustawi wa maisha ya watu wetu wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ningependa kusema baada ya pongezi, niendelee kumpongeza pia Mheshimiwa Rais, Mheshmiwa Mama Samia Suluhu Hassan ambaye alikuwa Makamu wa Rais wa Awamu ya Tano. Yapo mambo yaliyofanyika mwaka jana 2020 ambayo ni vizuri tukayafahamu ya kwamba mama yetu ndiye alikuwa ndiye mshauri mkuu wa Rais wa Awamu ya Tano. Mafanikio yale hatuwezi kumtenganisha nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nieleze jambo moja. Mwaka 2020 dunia ilikumbwa na janga la Corona na Tanzania iliamua kutoka na suluhisho lake la ndani la kukabiliana na Corona. Nakumbuka Serikali ilitoa maelekezo kwamba tufanye mambo makubwa matatu; moja, tumwombe Mungu; pili, tuzingatie ushauri wa wataalamu wa afya na Serikali; na tatu, tuendelee kuchapa kazi. Hakufungiwa mtu ndani hapa, wala hatukuweka measures ambazo ni gandamizi na zinarudisha watu wetu nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda ieleweke kwamba Ndugu Bashiru yuko hapa, Katibu Mkuu Mstaafu, mwaka jana, 2020 alitoa maelekezo kwamba humu ndani msitoke, mwendelee kujadili mpaka mpitishe bajeti, hakuna cha Corona; na mlipitisha na wengine tumewakuta kipindi hiki. Hakuna sababu ya kuogopa jambo hili. Mwaka 2020, kwa mbinu tulizozitumia hapa nyumbani, wakiwemo ndugu yangu hapa, alitoka na ile dawa moja inaitwa Bosnia na nyingine nyingi tu; na Covido na akina nani, zimefanya maisha yamekwenda vizuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachotaka kusisitiza ni kwamba nchi nyingine zote walitumia mbinu zilizoelekezwa na ndugu zetu wa Magharibi. Nikwambie, wote waliotumia mbinu za Magharibi waliharibikiwa vibaya mno. Hizi taarifa siyo longo longo, ni taarifa za kiutafiti na ziko. Nitatoa mfano ambao ni halisi. Nchi zinazotuzunguka, ninyi mnafahamu, zilitumia mbinu za kimagharibi kukabiliana na ugonjwa wa Corona. Wote wali-experience negative growth mwaka 2020 by end of December. Ni Tanzania peke yake iliyotumia local solutions iliyobaki na uchumi chanya, kwa takwimu za Benki ya Dunia na kwa takwimu zetu za NBS. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa Serikali, yako mambo tulifanikiwa sana mwaka 2020, msiyaache, tuyatumie mwaka huu pia kupiga hatua kwa maana hiyo. Bajeti ambayo tunakwenda kuipitisha hapa iliyoletwa na ndugu yetu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa maelekezo ya mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, imepokelewa vizuri sana na Umma kwa sababu inakwenda kufanya mkate mdogo kuu-share na watu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu, tunapo-share mkate, ni vizuri tukajiwekea utaratibu mzuri wa kusimamia nidhamu ya makusanyo na matumizi. Tusipofanya hivyo, tutaumaliza mkate na tusiweze kuwekeza mkate mwingine na kuifanya dhamira njema ya mama yetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan isifike. Sisi tuko hapa kama askari wake wa mwamvuli kuhakikisha ya kwamba tunafika huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haraka haraka nitoe rai pia kwa Wizara ya Fedha, hawa wanaoitwa micro, small and medium enterprises ulimwenguni ndiyo wana-constitute asilimia 90 ya chumi zote. Hapa Tanzania tuwawezeshe zaidi, ndiyo walipa kodi. Mpaka takwimu za mwaka 2010 ambazo ndiyo tunazo, ziko zaidi ya micro, small and medium enterprises kama milioni tatu na zinamilikiwa na watu 2.7 million.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeambiwa hapa walipa kodi ni milioni tano, kama tukiwajengea mazingira mazuri ya kuweza kupata fedha, mitaji na mikopo nafuu; nami nakumbuka kulikuwa kuna maelekezo kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu, nina uhakika katika majumuisho litawekwa sawa, kwamba ile mifuko yote ambayo inatoa fedha hapa nchini inakaribia 20 haisomani, haitambuani na hairipoti kwa wakati mmoja. Ijumuishwe ili hilo fuko lote la fedha tulisukume kwa wajasiriamali wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwa Serikali, unajua wakati mwingine wala siyo tunachohitaji ni benki hapa. Hapa tunahitaji fuko moja kubwa la fedha ambalo litaweza kusukuma kazi za wajasiriamali wadogo ama kwa kuwapatia fedha au kwa kuwapatia guarantee kwa maana hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie jambo moja hapa. Sasa tupo katikati ya kipindi kingine tunaambiwa Corona inaendelea. Rai yangu ni kwamba Wizara ya Afya; hapa mimi ningepeleka Wizara ya Afya zaidi na Wizara ya Fedha. Ilani ya uchaguzi imeeleza katika fungu la 84 kwamba lazima tutengeneze kiwanda cha kimkakati cha kuchakata mimea dawa. Hatujatenga fedha vya kutosha. Ilani inasema kuanzisha kituo kikubwa cha utafiti na uchunguzi wa mimea dawa na kuanzisha kiwanda cha kimkakati cha kuzalisha dawa zitokanazo na mimea yetu. Mbona tunatibiwa, tutapona na hizi mimea dawa? Rai yangu, hiki kiwanda msikiweke huku uraiani, mkakifiche sehemu fulani kwenye Kambi ya Jeshi ambako hakuna mtu anaweza kufika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni vita, wakijua mnatengeneza dawa hapa za kupambana na UVIKO watakuja kutuhujumu, lakini tukikificha sehemu mahsusi, hakuna mtu anaweza kufika, tutatengeneza dawa, tutatengeneza tiba, watu wetu watakaoonekana wamepata tatizo, watapewa dawa hizo na hakuna mtu atakuja kutuzingua hapo baadaye. Ila tusipokuwa makini, umeshasikia wakubwa jana wamesema tupewe chanjo bilioni moja, tuje kudungwa hapa.

Mheshimwia Mwenyekiti, nilikuwa natoa rai, tuwekeze vya kwetu, local solutions, for local problem.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuungana na wenzangu kuchangia Mpango huu Maendeleo kwa Miaka Mitano kwa kuanza na kuainisha kazi nzuri ambayo imefanyika katika Mpango wa Pili chini ya uongozi wa Serikali ya Chama Cha Mapinduzi na ningetamka mambo mawili muhimu, kazi kubwa imefanyika katika Mpango wa Pili katika kuimarisha uchumi mkubwa na umadhubuti wake (Macro level economy performance) ambayo ukifanya vizuri hapo inakwenda kwenye uchumi mdogo unaohusisha watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kimoja cha kipekee kimefanyika hapa Tanzania ni kufanya haya mambo yote kwa wakati mmoja na nitatoa viashiria vichache kuonesha kwamba katika uchumi mkubwa kazi kubwa sana imefanyika katika Mpango wa Pili na tuna kila sababu ya kuendeleza mafanikio hayo katika Mpango wa Tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kiashiria kimoja cha ukuaji wa uchumi na katika uchumi mkubwa na ufanisi wake ni ujenzi; tumefanya ujenzi wa bandari kubwa na ndogo, tumefanya ujenzi wa viwanja vya ndege, tumefanya ujenzi wa barabara kote nchini Tanzania, tumefanya ujenzi wa reli ya kiwango cha kimataifa, lakini ukiacha ujenzi imefanyika kazi kubwa sana ya kudhibiti mfumuko wa bei kutoka asilimia tano mpaka asilimia tatu kwa maana ya mfumuko wa bei wa jumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi nyingine kubwa imefanyika katika kuimarisha uchumi mkubwa ni kuweka nafuu ya kikodi kwa watumishi katika Pay As You Earn kutoka 12% mpaka 9%. Pia kumepunguzwa kwa kiasi kikubwa sana kwa tozo zenye kichefuchefu katika eneo la kilimo na madini na hapa ni makumi ya tozo ambazo zimefutwa. Kubwa kuliko yote ni uzalishaji wa umeme usafirishaji na usambazaji na hapa kazi kubwa imefanyika kufikia vijiji vyote na tumebakiza kama 2,000. Hoja ninayojaribu kuisema hapa ni kwamba umeme ambao tumezalisha mpaka sasa hivi tuna ziada, tulianza na megawatt 1,300 na sasa tuna 1,600 na hiyo ni ziada ya matumizi ambayo tunayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni kwamba, uchumi mkubwa unakwenda sambamba na uwekezaji na katika sekta binafsi na hapa utagundua kwamba mazingira wezeshi tumeyaweka katika kodi ya makampuni (corporate tax) ambayo tumeipunguza kutoka asilimia 30 mpaka asilimia 20 kwa viwanda vinavyohusika na kutengeneza madawa. Hii itawezesha viwanda hapa Tanzania kuanza kutengeneza dawa na kupunguza changamoto ya upatikanaji wa dawa kama ambavyo imepatikana wakati mwingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tulinde viwanda vya ndani kwa kuweka sera ambazo zitahakikisha kwamba bidhaa zinazoweza kuzalishwa ndani haziagizwi kutoka nje. Hapa napenda kupongeza uamuzi wa Serikali kuongeza kodi katika kuingiza sukari kutoka asilimia 25 mpaka 35 ili viwanda vya ndani viweze kuzalisha na kuuza sukari hapa nchini. Katika uchumi mkubwa pia utaangalia mzunguko wa fedha, wako watu wanapotosha wakati mwingine, lakini ukweli ni kwamba nikitoa kiashiria kimoja tu ya fedha tu zilizowekeza katika mawakala wa benki kutoka mwaka 2013 mpaka mwaka 2019, mzunguko wa fedha ambazo ameziweka mle ndani zilikuwa bilioni 28 tu, lakini mwaka 2019, zimefika trilioni tano, hili ni ongezeko kubwa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sasa nijielekeze katika ushauri; rai yangu kwa Serikali ni kwamba, tufanye itakavyowezekana, miradi ya uzalishaji wa nishati tuikamilishe kabla Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli hajaenda. Sasa hivi tunatengeneza Stigler’s pale bwawa la Mwalimu Nyerere, megawatt 2,115, hiyo inakwenda tayari. Kwenye hotuba ya

Mheshimiwa Rais ameeleza miradi mingine karibu kumi ambayo itazalisha umeme na kuongeza uzalishaji wa umeme nchini kifani na kwa sababu tunazungumzia a competitive industry economy, yaani uchumi shindani wa viwanda, umeme ni kigezo muhimu sana cha kufanikiwa kwa viwanda nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilipokuwa nikisoma Mpango, nimeangalia katika ukurasa wa 129, kiashiria cha Serikali hapa kinasema tunataka tuongeze umeme kutoka 1,600 ya sasa mpaka 4,900. Nikizitoa hapa tutabaki na 3,000 nikitoa 2,100 za Stigler’s tutabaki na 1,000, aah jamani! Mheshimiwa Rais ameeleza hapa Ruhuji megawatt 358, Rumakali megawatt 222, Kikonge megawatt 300, Mtwara gesi megawatt 300, Kinyerezi III na IV megawatt 600 na 300 mtawalia; na Somanga Fungu kwa gesi megawatt 330. Naishauri Serikali itazame ile miradi strategic ya kuzalisha umeme katika hii ambayo Rais ameelekeza ili tusije tukafika 2025 tumechukua ile ambayo kwa hakika haitaweza kutuvusha kwa maana hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nieleze tu katika viwanda na kilimo tujikite kwenye eneo moja kubwa, kutehamisha uunganishaji wa wakulima na masoko. Siku hizi Alibaba ni tajiri kwa sababu mtandaoni mtu unaweza kuuza korosho, mahindi na vitu kama hivyo. Nashauri, siku hizi simu hizi za kupangusa kila mtu anazo, lakini pia matumizi ya USSD code, inawezekana mkulima akawa na nyanya Ilula, asihangaike kuchukua lori zima kulipeleka Dar es Salaam, akatazama mle ndani akaona kuna soko, Dodoma au Morogoro… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kengele imegonga, basi nitaleta mchango wangu kwa maandishi. Naomba kuunga hoja. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuanzia Januari, 2021 hadi Februari, 2022 pamoja na Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa Kipindi cha Januari 2021 hadi Januari 2022
MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikupongeze sana kwa kuchaguliwa kwa kishindo na ahsante sana kwa nafasi ya kuchangia. Nipongeze sana Wenyeviti wa Kamati wamesema mambo makubwa sana yaliyonipelekea kubadilisha kidogo mtiririko wa namna ambavyo ningependa kuchangia na ningependa kwanza kusema kama ifuatavyo: -

Kwa maana njema kabisa kama Serikali isiposikiliza mapendekezo ya Kamati hizi mbili kwa umakini, tutaelekea kubaya na mimi ningesema jambo moja ambalo labda linaweza likaonekana lisieleweke, lakini kama tusipoweka dhamira ya dhati kwenye mradi mmojawapo tu wa chuma tunatumia pesa nyingi kuleta chuma hapa na inaathiri kitu kimoja kwenye uchumi kinaitwa balance of payment yaanitunatumia pesa nyingi sana kuagiza bidhaa kutoka nje kuja ndani kuliko ambavyo tunauza bidhaa za ndani kwenda nje, kiuchumi unapokuwa na nakisi kwenye balance of payment si afya kwenye uchumi na ni kitu ambacho kinaweza kikatufikisha siku moja tukashindwa kuwa na fedha ya nje ya kutosha kuweza kufanya majukumu yetu mengine ikiwemo kulipa madeni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ningependa niseme katika hili la kuweka nidhamu ya namna ambavyo tunazalisha ndani, ifike pahala tukubaliane kama Taifa yako mambo tuweke sera za ulinzi (protection policies) katika nchi yetu kwamba bidhaa hii na hii hatuta agiza kutoka nje tutaizalisha kutoka ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakupa mfano mafuta ya kula yanatuongezea nakisi kwenye balance of payment, mbolea inatuongezea nakisi kwenye balance of payment, hiyo chuma nimeisema, sukari inatuongezea nakisi kwenye balance of payment, mchele unalimwa hapa Tanzania lakini bado tunaagiza inatuongezea nakisi kwenye balance of payment, ngano/shairi ambayo inaweza kulimwa hapa Tanzania inatuongezea nakisi kwenye balance of payment.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii nakisi kubwa nikipitia pitia nyaraka hapa za Wanakamati na nini inaonekana bado ni tatizo baadhi yenu mtafahamu ya kwamba dhamira nzuri ya Mheshimiwa Rais kwenda kukopa kule IMF pamoja na mambo mengine ilikuwa ni kuweza kushughulika na nakisi kubwa inayoongezeka kwenye balance of payment. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, rai yangu kwa Serikali ziko bidhaa ambazo tukiwekeza vya kutosha hapa hapa nyumbani tutajitosheleza na tukijitosheleza fedha nyingi itabaki hapa hapa nyumbani na hapo ndiyo inapokuja kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, duniani kote wale wanaitwa micro small and medium enterprises ndiyo wanashika zaidi ya asilimia 90 ya chumi zote. Hapa Tanzania hawa micro small and medium enterprises ndiyo ambao wanashikilia viwanda vingi vidogo na vya kati ambavyo vina jukumu la kuchakata mazao mbalimbali na huduma na bidhaa ambazo zinahitajika hapa nyumbani. Ifike pahala hawa micro small and medium enterprises yaani biashara ndogo sana, ndogo na za kati ziwezeshwe kwa makusudi na Serikali yenyewe, mabenki hayawezi kuweka pesa kule kwa sababu watasema hakuna usalama. Lakini Serikali ndiyo baba yao, ndiyo mama yao na hapa katika Wizara ya Fedha na Mfuko ule wa Uwezeshaji iko mifuko zaidi ya 50 ya kuwezesha wananchi kiuchumi haisomani, haijuani, malengo yake hayashabihiani, sasa unapokuwa una mifuko zaidi ya 50 yenye fedha za mamia ya mabilioni ambayo haisomani nafahamu yaliwahi kutoka maelekezo hapa kwamba mifuko hii ihuishwe, lipatikane fuko moja kubwa la kwetu la ndani ambalo tutalitumia kuwawezesha wajasiriamali wadogo ambao hawa kimsingi ndiyo engine ya uchumi wetu. Tukifanya hivyo hata wigo wetu wa kodi na mapato utaongezeka. Nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na mimi nianze kwa kupongeza kazi nzuri sana ya Kamati.

Mheshimiwa Spika, Ibara ya 8(1)(b) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inazungumzia lengo kuu la Serikali itakuwa ni ustawi wa wananchi wetu. Katiba inaeleza lengo kuu ni ustawi na lengo hilo linafanyika kwa kutunga sera zinazolenga kuleta ustawi wa watu wetu katika maeneo kadhaa wa kadhaa. Baada ya sera tunatunga sheria ili kuhakikisha kwamba yale ambayo tumeyaweka kwa maana ya ustawi na maendeleo ya watu yanaweza kuwa na nguvu ya kisheria kutekelezwa. Ili sheria ziweze kutekelezwa Katiba inatoa utaratibu wa Bunge ambalo ndilo lina mamlaka ya kuweka utaratibu wa kutekeleza sera na sheria kutunga kanuni.

Mheshimiwa Spika, kifungu cha 4 cha Sheria ya Tafsiri kinaeleza kwa upana tunapozungumza sheria ndogo maana yake nini, tukasema leo basi kwa kuwa tumepata nafasi kwenye Kamati tulieleze ili tufahamu upana na umuhimu wa sheria ndogo inapokuja kwenye kuhakikisha ustawi wa watu wetu ni halisi.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Tafsiri kifungu cha 4, sheria ndogo inajumlisha amri, viongozi wetu wamepewa mamlaka ya kutoa amri (orders), viongozi wetu wamepewa mamlaka pia ya kutoa matamko (proclamations) na hayo matamko yanaweza yakagusa ustawi wa watu wetu, lakini pia zipo kanuni kwa maana ya rules and regulations, pia zipo notices ambazo pia zinatolewa na mamlaka mbalimbali na viongozi wetu, tunazo pia sheria ndogo kwa maana ya by- laws kwenye Serikali ya Mtaa kama ambavyo wenzangu wametangulia kusema lakini zaidi ya yote zipo hati kwa kiingereza tunasema instruments, zote hizi kwa ujumla ni sheria ndogo na Bunge hili limepewa dhamana ya kusimamia na kuhakikisha ya kwamba hazikinzani na sheria mama, sera zetu na Katiba zetu katika kuleta maendeleo ya watu wetu wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale ambapo tunaziendea ndivyo sivyo shida inaanza kuja, shida inaanzia kwenye Serikali, shida inakwenda Chama cha Mapinduzi na hata Wabunge mmoja mmoja inaweza kuwa mtihani. Rai yangu kwa Serikali, sheria ndogo jambo la msingi kifungu cha 48(1) kinaeleza utaratibu wa namna ambavyo tunapaswa kuziendea sheria ndogo.

Moja, ikitolewa tamko, amri ama ni kanuni zinatakiwa ziletwe hapa katika Mkutano unaofuata ndani ya siku sita. Na mimi ningependa nijielekeze kwamba Serikali izilete na ikizileta tupe nafasi pale kwenye Sheria Ndogo kuna watu wabobezi na mabingwa watazichambua na wataangalia maslahi mapana ya Taifa letu la Tanzania na mimi ningependa niangazie mambo kama matatu hivi: -

Kwanza, tozo kwenye miamala; hii ni kanuni tulipitisha uhalali wa kutoza, Waziri na Serikali wamekwenda kutengeneza kanuni lakini jambo limekuwa kubwa na lina interest kwa umma. Watu ukiwasikiliza hivi wananung’unika na jambo hili, sasa Serikali nafahamu linaweza kuwa ni jambo la kibajeti linagusa pesa za Serikali lakini umesikia hapa pesa imepungua, miamala imepungua liletwe hapa kama siyo kwenye bajeti, kwenye Sheria Ndogo sisi tuwaoneshe namna gani unaweza ukatoza miamala na wananchi wakawa na amani wame-relax vizuri, pesa ikaongezeka na pesa ikiongezeka ndiyo maendeleo ya nchi hii yatakuwa yanakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninashauri jambo hili la tozo ifike pahala, Mheshimiwa Rais alishatoa mwelekeo tufanyie kazi jambo hili, liletwe basi tuweke utaratibu sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni tamko la umeme shilingi 27,000. Hili jambo linaweza likafitinisha watu na Chama chetu cha Mapinduzi, mimi kama mnufaika wa Chama cha Mapinduzi jambo hili limesemwa kipindi hiki liletwe Bungeni, Mkutano unaokuja tuwasaidie wenzetu wa TANESCO maana yake nini kutoza shilingi 27,000 kwa Watanzania ambao wameusubiri umeme kwa miaka mingi sasa umefika huu siyo wakati wa kuwaambia tena shilingi 27,000 inaondoka! Unajua ilikuja kwa sababu kuna mkanganyiko na TANESCO lazima wafahamu, hawatupi umeme bure, tunalipa LUKU tena kwa pesa nyingi.

Mheshimiwa Spika, mwisho…

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Polepole kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Engineer Manyanya.

T A A R I F A

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nadhani unatakiwa kukaa kwanza. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ninapenda kumpa taarifa aliyekuwa anazungumza kwamba jambo hili Kamati imeliangalia kiundani na ilishaongea na Wizara kwamba wao wataweza kuleta ufafanuzi wa bei mbalimbali ambazo zinahitajika ili Kamati kwa pamoja tuweze kuangalia na wenzetu pia kwenye Bunge waweze kupata taarifa.

Kwa hiyo, kimsingi dhamira ilikuwa njema kwamba bei pengine ya umeme sasa imekuwa ni ndogo sana, lakini sisi tumesema tuliangalie kwa mapana ili tuweze kupata namna bora zaidi ya kushughulikia. Ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Humphrey Polepole malizia mchango wako.

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Engineer Manyanya ni mama yangu na nimepokea taarifa yake lakini kule kwenye Sheria Ndogo hili halijaja bado ndiyo maana ninaiomba Serikali ilete kwenye Mkutano unaokuja kama Sheria ya Tafsiri inavyoelekeza ili sisi kama Bunge na Kamati ya Sheria Ndogo tusaidie kusema watu hawa kwanini tunasema shilingi 27,000, Kijijini na maeneo ya pembezoni kwa maana hiyo na kwa maslahi mapana ya Chama chetu cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nizungumzie suala la Sheria ya Madawa na Vifaatiba ipo pale tumeipitia. Wanasema ukitaka kufanya majaribio ya kitabibu au clinical trial Mtanzania, mgunduzi kagundua dawa unatakiwa ulipe kule fees and charges dola karibu 3,000. Nani anaweza kutoa dola 3,000 kwa kugundua dawa ya corona, nani anaweza kutoa dola 3,000 kwa kugundua dawa ya kifua kikuu au na mambo kama hayo?

Mheshimiwa Spika, ninaomba vitu hivi viwe katika namna ambayo itakuza ugunduzi katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana ninaunga mkono hoja. (Makofi)