Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Eng. Dr. Leonard Madaraka Chamuriho (10 total)

Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii kuchangia hoja hii ambayo naiunga mkono kwa sababu inakwenda kujibu hoja zote ambazo zimetolewa katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, imetolewa hoja ya uboreshaji wa miundombinu ya kusafiri kwa njia ya maji ambayo; kama mlivyoshuhudia wengi tayari tumekwisha rekebisha katika Ziwa Victoria na juzi tarehe 15 Juni, 2021 Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan alizindua pale Mwanza meli ya MV Victoria na MV Butiama pamoja na Chelezo, na huo ulikuwa ndio mwanzo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hoja iliyotolewa ya miundombinu ya maji tulishuhudia tarehe 15 mwezi wa sita Mheshimiwa Rais Wetu Samia Suluhu Hassani alishuhudia utiaji saini wa mikataba mitano ambayo ilikuwa inalenga katika kuboresha usafiri wa maji. Alishuhudia mkataba wa Meli kubwa katika Bahari ya Hindi ambayo ni tani 2,800 ambayo imelenga usafiri kati ya hapa na Comoro. Alishuhudia meli kubwa katika Ziwa Tanganyika ambayo vile vile ina meli yenye uzito wa tani 2,800, alishuhudia utiaji wa saini wa meli kubwa ya abilia 600 katika Ziwa Tanganyika pamoja na uzito wa shehena tani 400. Vile vile alishuhudia utiaji wa saini wa meli mpya ya tani 3,000 katika Ziwa Victoria pamoja na ukarabati wa MV Umoja. Kwa hiyo bajeti hii ambao inakwenda kujibu maswali hayo naiunga mkono kwa sababu hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukienda kwenye Bandari, upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam, Tanga na Mtwara unaendelea na bajeti hii inakwenda kukamilisha; kwa hiyo unakwenda kutatua matatizo hayo. Katika Bandari ya Dar es Salaam lile gati la RoRo limekamika na magati namba moja hadi saba yamekamilika na sasa hivi tunamalizia pale ile yard ya kuelekea makasha. Hivyo bajeti hii itaimarisha kuimarisha lango hilo vizuri sana. vile vile lango la kuingilia katika Bandari ya Dar es Salaam linakwenda kupanuliwa, na sasa hivi pale tutaingiza meli kubwa kabisa ambazo zinaweza kubeba hadi makasha 7,000 hadi 8,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa bajeti hii tutaagiza mitambo mikubwa ya kupakulia na kupakilia mizigo maalufu kama SSG Shore to Sea Gantry ambazo zimeagizwa kwa kutumia na bajeti hii. Katika Bandari ya Tanga vile vile lango la kuingilia pale limechimbwa, ambalo litakamilishwa kwa kuongeza gati mbili kubwa za mita 250, 250 ili tuweze kupokea meli kubwa za mita 300. Vile vile Mtwara tunafanya vivo hivyo tunaongeza magati mawili ambayo tayari yanakamilika na sasa hivi tunaagiza vifaa vya kupakilia mizigo, hivyo bajeti hii inakwenda kutatua hayo matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa reli vile vile tulimshuhudia Rais wetu mpendwa tarehe 14 mwezi wa sita akiweka jiwe la msingi katika Reli ya Standard Gauge kutoka Mwanza hadi Isaka. Kwa hiyo inadhihirisha kwamba bajeti hii ambayo itakwenda kukamilisha kipande hicho inatekeleza mwendelezo wa kazi hizo ambazo tumeziendeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika uchangiaji vile vile iliongelewa hoja ya TARURA, kwamba tuaingalie; na ni kweli katika marejeo ambayo tumeyafanya ya uwiano wa mgawanyo wa fedha za mfuko wa barabara ambao tumebaini kwamba ulifanyika mwezi Disemba, 2020 tumebaini kwamba tatizo kubwa siyo mgao wa fedha bali ni kiasi kidogo cha fedha za mfuko. Tayari mmeona katika bajeti hii hatua zimeanza kuchukuliwa katika kuongeza bajeti hii, ni muhimu tuiunge mkono kwani inakwenda kutatua hayo matatizo yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, imeongelewa miundombinu ya Jangwani pale katika mchango wa bajeti hii. tayari TANROADS inafanya pale usanifu wa kina ili tuweze kupata utatuzi wa changamoto hiyo na ambayo katika ukamilifu wake tutaweza kupata utatuzi, kwamba tufanye nini pale ili mafuriko ya pale Jangwani na ile miundombinu ya Mwendokasi iweze kulindwa na tuweze kuendelea na kutoa huduma pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile katika michango iligusiwa sheria yetu ya barabara ya Namba 13 ya mwaka 2007 ambayo ilikuwa inaongelea kuzuia malori yanayozidi tani 10 kuelekea katika vijiji vyetu ambavyo ililenga kwamba tuiachie. Sheria hiyo imezingatia uwezo wa barabara zetu za kule na kuzilinda hivyo lengo lake ni kulinda miundombinu ya zile barabara hasa madaraja yake. Hivyo, sheria hiyo tutaendelea kuizingatia ili kulinda miundombinu hiyo. Lakini tuendelee kuongeza ulipaji kodi ili tuweze kupata fedha zaidi za kutosha kuweza kuimarisha miundombinu hiyo ili iweze kuwa bora zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile ilitolewa rai hapa kwamba kuna ahadi nyingi katika miundombinu ya barabara ya viongozi wa Taifa. Hapa tunarudia kusema tena kwamba hizi ahadi za kitaifa tunazipangia mkakati wa kuzitekeleza. Imetolewa hoja kwamba tuziwekee database na hilo ambalo tumelifanya. Kwamba ahadi zote za kitaifa zilizotolewa katika ujenzi wa barabara, vivuko nakadhalika tutazizingatia kulingana na vipaumbele vyake katika bajeti zitakazokuwa zinaendelea hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile ilitolewa rai ya kupunguza msongamano wa magari katika babara inayokwenda Tunduma hasa pale Mjini Mbeya katika barabara ya Igawa hadi Tunduma. Hilo nalo tunaenda nalo, na kwa sasa hivi tunamalizia ule upembuzi yakinifu wa ile by-pass ili itakavyokamilika katika bajeti hii tuanze na utekelezaji wa ujenzi wa barabara ile ambayo inaondoa changamoto hiyo ambayo tunayo pale. Hivyo ni bajeti hii hii ndiyo itakayotatua changamoto hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna michango ya bajeti hii ambayo ilihusiana na viwanja vya ndege. Kwa mfano ilitolewa rai kuhusu kiwanja cha ndege cha Sumbawanga na vinginevyo. Tayari vile viwanja ambavyo vilikuwa vijengwe kwa ufadhili wa European Investment Bank, maongezi yameshakamiliaka na sasa hivi tunasubiri wakati wowote waweze kutoa fedha ili vile viwanja vinne viweze kujengwa katika bajeti hii. Kwa hiyo tuna kila haja ya kuiunga mkono bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kisera, bado nia ya Serikali kuunganisha mikoa yote kwa viwanja vya ndege ipo pale pale hivyo tutaendelea kuviboresha viwanja vyote vya mikoa na kuvijenga ili viweze kuendelea; na kwa sasa hivi viwanja vyote tunaviboresha katika kiwango cha kuviwekea taa ili viweze kufanya safari za usiku na tuweze kuongeza safari katika miundombinu ya viwanja hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazo barabara nyingi ambazo Waheshimiwa Wabunge wameziongelea hapa na zote hizo ambazo tumezipanga katika bajeti hii tunaomba kupewe hiyo fursa ili tuweze kuzitekeleza katika bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukienda katika miundombinu ya reli, nikirudia pale, tuna reli ambazo tumepanga kuzifanyia upembuzi yakinifu ambazo ni Reli ya Tabora hadi Kigoma ambayo vile vile inakwenda kufanyiwa katika bajeti hii. Reli ya Kaliua - Mpanda hadi Karema nazo tutakamilisha kuzifanyia upembuzi yakinifu. Hivyo tukimaliza huo upembuzi yakinifu kazi ambayo itafuata katika reli hizo ni ujenzi, na kazi zote hizo zimepangwa zitekelezwe katika bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Apika, huo ndio mchango wangu, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia Mpango huu katika Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, kwa vile ni mara yangu ya kwanza kusimama rasmi kuchangia, napenda kushukuru Mwenyezi Mungu kwanza kwa kutuweka hai na kukutana hapa. Pia kumshukuru aliyeniteua Hayati Rais wetu Mtukufu lakini vilevile kumshukuru Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kunibakiza katika nafasi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kuchangia hoja ambazo zimetolewa katika mjadala huu nikianza na Shirika letu la Ndege la Tanzania. Shirika la Ndege la Tanzania mpango wa kulifufua ulipoanza 2016 haukuanza kwa kukurupuka, kwani tulianza na mpango wa mwaka mmoja wa Oktoba 2016 hadi Oktoba 2017 na mpango mkakati uliofuata ambao ulikuwa ni wa miaka mitano ulianza Julai 2017 na utaendelea hadi Juni 2022. Kwa hiyo, tunaendelea vizuri na tija inaanza kuonekana kwani tulipoanza tulikuwa tuna miruko 576 kwa mwaka, lakini sasa tumefika miruko 4,752 kwa mwaka ambapo lengo letu ni kufika miruko 6,500 kwa mwaka lengo ambalo tumekwama kidogo kulifikia kwa sababu ya changamoto ya COVID ambayo imezuia ndege zetu kuruka kwenda katika destinations mpya za China, Afrika Kusini, Nigeria na London.
(Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kulikuwa na hoja ya ufanisi wa ndege zetu, lakini ndege hizi japokuwa tulianza na ndege moja mwaka 2016 na sasa hivi tuna ndege nane hazikuja kwa siku moja, kwa hiyo, kuchukua wastani wa pamoja siyo sawa. Ndege mbili za kwanza tulizipokea Septemba 2016, ndege iliyofuata ilikuwa Aprili 2018, Boeing ya kwanza tuliipokea Julai 2018 na zile Air Bus ya kwanza tulipokea Desemba 2018 na ya pili Januari 2019. Dreamliner ya pili tulipokea Oktoba 2019 na Bombardier ya mwisho tulipokea Desemba 2019. Kwa hiyo, utaona hizi ndege zinakuja kulingana na mpango na tatu zilizobaki zilikuwa zije mwaka jana lakini zimekwamishwa na COVID. Hivyo mipango yetu inakwenda vizuri na miruko hiyo inadhibitiwa kisheria hivyo hatuwezi kuruka kukiuka Sheria za Udhibiti wa Marubani pamoja na Wahudumu wa Ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiangalia kwa wastani miruko ya Bombardier ya kwetu sasa hivi inaruka saa kumi na nusu kwa siku lakini saa ambayo inapendekezwa huwa ni saa nane, kwa hiyo, tumezidisha tunafanya vizuri sana. Kwa Boeing 787 ambayo ni Dreamliner tunaruka sasa hivi saa tatu na nusu inapendekezwa saa 12 na Air bus tunaruka saa sita lakini inapendekezwa saa 10. Sasa hizi ndege mbili kubwa tumekwamba tufikisha hiyo miruko kwa sababu safari ya China ambayo ndiyo ilikuwa imepangiwa na ya Uingereza na Afrika Kusini ndio imesababisha changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea vizuri na ufanisi unajidhihirisha wazi kwani ukiangalia umiliki wa soko tulivyoanza mwaka 2016 ulikuwa ni asilimia 4.5 lakini leo tunaongelea umiliki wa soko wa asilimia 75. Hakuna Shirika la Ndege ambalo limeweza kufikia ufanisi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile tukiangalia jinsi ilivyochangia watalii wetu, tulikuwa na watalii milioni 1.2 lakini sasa hivi tuna watalii wanaokaribia milioni mbili. Hawa wote wamesababishwa na hizo ndege zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile ndege zetu zimeweza kutoa huduma kwa Watanzania waliokwama nje ya nchi wakati wa janga la COVID. Vilevile zimechangia vizuri katika soko la mazao ya mifugo na uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na hoja za uendelezaji wa bandari. Uendelezaji wa bandari zetu unaendana pamoja na Mpango wa Taifa wa Uendelezaji wa Bandari yaani National Port Master Plan ya mwaka 2020-2040. Ukiangalia kwa sasa hivi bandari yetu ya Dar es Salaam ilikuwa na uwezo wa kubeba tani milioni 11 kwa mwaka lakini baada ya maboresho yatakayokamilika mwaka 2024 itaweza kuwa na uwezo wa kuhudumia tani milioni 28 kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tukiangalia bandari zetu za Mtwara na Tanga; ya Mtwara ilikuwa inaweza kuhudumia tani laki nne kwa mwaka lakini sasa hivi itahudumia tani milioni moja kwa mwaka. Bandari ya Tanga ilikuwa inahudumia tani laki tano kwa mwaka lakini nayo baada ya maboresha tunayofanya sasa hivi itaweza kuhudumia tani milioni moja kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa Bandari ya Bagamoyo na ujenzi na uendelezaji wa bandari zote utazingatia mahitaji na ukuaji wa maboresho tunayoendelea kuyafanya sasa katika Bandari zetu za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara. Endapo atatokea mwekezaji yeyote ambaye ataweza kutusaidia katika kuboresha bandari yoyote kulingana na mahitaji mapya milango ipo wazi na tuko tayari kukabiliana na changamoto hiyo. Katika hoja hii ya bandari, tayari kama Serikali tumeshakutana na hoja hii tunayo kwa Waziri Mkuu ambapo tumeangalia mapendekezo yote na mmetoa mapendekezo mazuri ambayo tutayatumia katika ushirikishaji wa maboresho wa bandari zetu hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo imetolewa ni kuhusu Reli ya TAZARA, ni kweli kwamba reli hii ilikuwa inasuasua hapo mwanzo. Tayari tuna mkakati mzuri wa kuihuisha reli hiyo. Tumeshaanza mchakato wa sheria, sheria hii imechukua muda kidogo kuihuisha lakini imebidi iwe hivyo kwa sababu sheria hii inabidi iwe moja ambayo itapitishwa na Bunge lako pamoja na Bunge la Zambia kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Spika, sheria hii tutakapoirekebisha itaruhusu wawekezaji kwani sasa hairuhusu, vilevile itaruhusu upatikanaji wa watumishi kutoka mahali popote kwani sasa hivi tuna hii changamoto ambayo sheria inasema lazima Mtendaji Mkuu atoke Zambia. Kwa hilo, lipo katika mkakati wetu wa kuendeleza hiyo reli mpya ya TAZARA. Vilevile tunaendelea na majadiliano na wenzetu wa China pamoja na wawekezaji wengine ili tuweze kuirekebisha hiyo reli yetu ili iweze kuwa na ufanisi zaidi kuliko ambavyo ilivyo hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo katika mikakati hiyo, tunaungana na aliyetoa kwamba tuongeze matawi ya Tunduma hadi Kasanga Port, kwani upembuzi huo tunaangalia haya yote ili tuiboreshe reli yetu. Vile vile katika TAZARA tunafanya tafiti za bei ili kuwa na bei shindani ili iweze kushindana pamoja na taratibu nyingine za usafiri.

Mheshimiwa Spika, vile vile napenda kuchangia kuhusu reli. Tuna reli za aina tatu hapa kwetu. Kwanza nianze na hii reli ya kisasa, standard gauge ambayo awamu ya kwanza ni kutoka Dar es Salaam hadi Mwanza na ina vipande vitano. Kipande cha kwanza ni kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro, sasa hivi tumefikia asilimia 92; kipande cha pili ni kutoka Morogoro hadi Makutupora, tumefikia hatua ya asilimia 58; kipande cha tano ambacho ni Mwanza hadi Isaka, tumefikia hatua ya mobilization na tayari mkandarasi ameshalipwa malipo ya awali tarehe 1 Aprili, mwaka huu 2021. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ilizuka hoja ya ujenzi wa reli kwa muda mrefu lakini kwa ujenzi wa awamu ya kwanza imepangwa kukamilika 2025. Hivyo, tunaendelea na kutafuta wawekezaji ambao watatusaidia katika kumalizia kipande cha tatu na kipande cha nne kutoka Makutupora hadi Tabora na kutoka Tabora hadi Isaka. Awamu ya pili itakuwa ni kutoka Tabora hadi Kigoma pamoja na Mpanda hadi Kaliuwa. Kwa hiyo, sasa hivi tunaendelea na upembuzi yakinifu pamoja na usanifu wa kina ili itakapokamilika tuweze kupata wawekezaji wa sehemu hizo. Hivyo mtandao wa reli nzima utajengwa kulingana na uwekezaji lakini mradi huo utakuwa ni mchanganyiko pamoja na fedha za ndani, kwenye mikopo, PPP, pamoja na fedha za ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile, kulikuwa na hoja ya wafanyakazi wa kigeni kuwa wengi kule lakini hili linadhibitiwa kwa mkataba na tunahakikisha kwamba wafanyakazi wa kigeni ni asilimia 20 tu katika ujenzi huu na wazawa wanakuwa asilimia 80. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile, tuna mpango wa reli yetu ya Mtwara hadi Mbambabay na Matai kuelekea Mchuchuma hadi Liganga. Hii imepangwa kujengwa kwa ubia kwa sekta binafsi na Umma. Tayari tulikuwa tuna Mshauri Mwelekezi KPMG JV ambaye alitufanyia kazi ambayo hatukuridhika nayo, tayari tumeshamwondoa na sasa hivi tunatafuta Mshauri Mwelekezi mwingine ambaye atatupatia mwekezaji mahiri ili tuweze kuendelea na mradi huo kama ambavyo tumekuwa tumepanga.

Mheshimiwa Spika, vile vile napenda kuongelea masuala ya barabara ambayo tumeendelea na vipaumbele…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kutuwezesha kufika hatua hii ya mwisho katika kuhitimisha hoja yangu ambayo niliiwasilisha jana tarehe 17 Mei na kujadiliwa na Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa napenda kuchukua fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini kuongoza Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, Wizara ambayo ni kichocheo cha ufanisi wa utendaji wa sekta zingine za kiuchumi na kijamii. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru pia Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maelekezo na miongozo yake ambayo imenisaidia wakati nikitimiza majukumu ya Serikali katika kipindi hiki kifupi kutoka ateuliwe kuwa Makamu wa Rais.


Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumpongeza Kiongozi wa Shughuli za Serikali Bungeni Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa Mbunge, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutumia uzoefu wake wa uongozi katika kutuongoza kwa umahiri na kimkakati kutekeleza majukumu yetu kila siku hapa Bungeni.


Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii pia kumshukuru Mheshimiwa Spika na pia kukushukuru wewe binafsi Naibu Spika na Wenyeviti wa Wabunge kwa ushirikiano mnaoipatia Wizara hii ninayoiongoza katika kutekeleza majukumu mbalimbali ya Serikali ndani na nje ya Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, nichukue fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano wao wa dhati wanaonipatia kutoka nilipoteuliwa kuwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, nimejifunza masuala mengi kutoka kwao, ujuzi ambao utaniwezesha kutekeleza majukumu yangu kwa sasa kwa kiwango cha hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia kipekee nimshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu, Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso pamoja na Wajumbe wa Kamati yake ambao wamepitia bajeti ya Wizara kwa niaba ya Bunge lako Tukufu na kuanisha namna bora ya kiutendaji kazi kufikia malengo ya Taifa letu. Naahidi kwamba Wizara itazingatia maoni, ushauri na mapendekezo ya Kamati hii kwa weledi wa hali ya juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee niwashukuru Mheshimiwa Engineer Godfrey Msongwe Kasekenya na Mheshimiwa Mwita Mwikwabe Waitara pamoja na Makatibu Wakuu Mhandisi Joseph Christopher Mwalongo na Gabriel Joseph Migile wa Ujenzi na Uchukuzi kwa ushirikiano wao katika kutekeleza majukumu yangu. Aidha, nawashukuru Wakuu wa Idara, Vitengo, Wenyeviti wa Bodi zilizo chini ya Wizara, Viongozi wa Taasisi na Watendaji wote wa wizara kwa ushirikiano mzuri na juhudi walizozifanya kuhakikisha kwamba tunatimiza majukumu tuliyokabidhiwa na Taifa ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu na Watanzania kwa ujumla kwamba, Wizara ninayoisimamia itatimiza matarajio ya Serikali na kuhakikisha kazi inaendelea. Mimi kama waziri mwenye dhamana nitatekeleza wajibu wangu kwa ufanisi na weledi wa hali ya


juu kwa kushirikiana na wenzangu katika Wizara yangu. Ni imani yangu tutafikia matarajio ya Taifa ikiwa ni pamoja na yale ya Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru tena Waheshimiwa Wabunge waliochangia hoja ya Mpango wa Bajeti ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, michango ambayo itanisaidia sana katika kuboresha hoja niliyoiwasilisha. Naomba sasa nijielekeze katika kutoa maelezo kwenye hoja mbalimbali zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutumia fursa hii kuwatambua Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika bajeti yangu. Waheshimiwa Wabunge 59 waliochangia wakati wa majadiliano ya hoja ya Waziri Mkuu na Waheshimiwa 158 wamechangia wakati wa hoja ya Wizara yangu ambapo 84 wamechangia kwa kuzungumza na 14 wamechangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi punde Waheshimiwa Manaibu Mawaziri wa Wizara yangu wameanza kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge. Nawashukuru sana kwa jinsi ambavyo wamejibu baadhi ya hoja zilizojitokeza wakati wa kujadili hoja hiyo niliyoitoa hapa Bungeni wakati nawasilisha hapo jana, hoja kuhusu mpango wa bajeti wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa mwaka 2021/ 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, naomba kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba Wizara itajibu hoja zote za Waheshimiwa Wabunge kwa maandishi na kuziwasilisha kwao kabla ya kuhitimisha kwa Mkutano wa Bunge hili la Bajeti unaoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nianze kuhitimisha hoja yangu kwa kutoa ufafanuzi wa kiujumla wa baadhi ya hoja zilizojitokeza. Bajeti ya Wizara imejikita katika kutengeneza Dira ya Maendeleo ya Taifa ya mwaka 2025, Mpango wa Taifa wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano kuanzia 2021/2022 hadi 2025/2026, Ilani ya Uchaguzi wa


Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020, maagizo mbalimbali ya Viongozi Wakuu wa Serikali na Sera, Mikakati na Miongozo Mbalimbali ya Kitaifa na Kimataifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa Taifa wa Maendeleo pamoja na Ilani ya Uchaguzi zina lengo kuu la kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu. Wizara ninayoiongoza ina jukumu kuu la kuwezesha kufikiwa kwa lengo hili kwa kuwa inawezesha sekta nyingine kufikia malengo yao ikiwa ni pamoja na kuunganisha maeneo ya uzalishaji na masoko. Hii ina maana kwamba ufanisi wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi utawezesha Sekta nyingine za uchumi na kijamii kuwa na ufanisi.


Mheshimiwa Naibu Spika, katika uchaguzi wa mwaka 2020 Chama cha Mapinduzi kilipata ushindi wa kishindo ngazi ya Urais, Wabunge na Madiwani. Hii ilitokana na ubora wa Ilani yake ya Uchaguzi ambayo kiujumla inalenga kujenga uchumi imara na kuwawezesha wananchi kunufaika nayo ikiwa ni pamoja na kuondoa kila aina ya kero za wananchi kuliko ilivyokuwa kwa Ilani nyingine. Kwa kuzingatia hili nina wajibu wa kueleza vitu ambavyo Wizara ninayoiongoza itatekeleza katika kipindi cha miaka mitano ijayo kuanzia 2021/2022 hadi 2025/2026 tukianza na mwaka wa fedha 2021/ 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wameitaka Serikali ya Awamu ya Sita kuendelea na utekelezaji wa miradi ya kimkakati iliyoanza kutekelezwa kipindi cha kwanza cha Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, kwa kuwa miradi ndiyo msingi wa ukuaji wa uchumi wa Taifa letu. Miradi hiyo ni pamoja na kuendelea na ujenzi wa ukarabati wa barabara kuu za mikoa ili kuiunganisha nchi, ujenzi wa madaraja ya muhimu ya barabara na vivuko, kuendelea na ujenzi wa reli ya Standard Gauge, uboreshaji na upanuzi wa Bandari ya Dar es Salaam na kuendelea na ujenzi wa ukarabati wa meli katika maziwa.


Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi thabiti wa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, imedhamiria kuendelea kutekeleza miradi yote ya kimkakati ili Taifa liweze kunufaika nayo kwa kujenga uchumi endelevu. Miradi hiyo inatekelezwa na Wizara yangu kama ilivyoanishwa kwenye Mpango wa Taifa wa Maendeleo na Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 kwa umakini na umahiri mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa mazuri tunayoyaona, lakini tumedhamiria kazi iendelee ili mazuri zaidi yaje kuonekana ifikapo mwaka 2025. Serikali zilizopita za Chama cha Mapinduzi zilijiwekea dhamira ya kuunganisha Makao Makuu ya Mikoa yote nchini kwa barabara kuu za lami. Dhamira hii inakaribiwa kufikiwa ambapo kwa uchache kwa nchi ambapo kazi inaendelea. Kazi hizo zinahusisha ujenzi wa barabara za kuunganisha Mikoa ya Tabora na Kigoma, Mikoa ya Kigoma na Kagera, Mikoa ya Tabora na Mbeya. Aidha, maeneo mengine ni pamoja na kuunganisha na Mkoa wa Manyara, Mkoa wa Morogoro ambao utapewa kipaumbele ndani ya kipindi hiki cha utekelezaji wa Ilani ya CCM ya mwaka 2020-2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi na wasaidizi wangu tutakuwa karibu sana, karibu sana na mahali pa kazi za ujenzi wa barabara zinazofanyika ili kuhakikisha zinafanyika kwa ubora kama walivyoshauri Waheshimiwa Wabunge. Ningependa kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba tayari tunatangaza miradi 16 ya barabara ambayo tumeanza kuitangaza wiki hii, ambayo ni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa kwanza, ni Barabara ya Ntendo hadi Muze kilometa 25; Barabara ya Isonje hadi Makete kilometa 25; Barabara ya Mianzini hadi Ngaramtoni kilometa 18; Barabara ya Bigwa – Kisaki kilometa 15; Barabara ya Uvinza – Malagarasi kilometa 51.1; Barabara ya Mbulu – Hydom kilometa 25; Barabara ya Matai – Kasesya kilometa 25; Barabara ya Ntyuka Junction – Mvumi Hospital


hadi Kikombo Junction kilometa 25; Barabara ya Tarime - Mgumu kilometa 25; Barabara ya Vikonje hadi Uvinza kilometa 25; Barabara ya Kibondo hadi Mabamba kilometa 10; Barabara ya Noranga – Itigi hadi Mkiwa kilometa 25; Barabara ya Itoni hadi Lusitu kilometa 50; Barabara ya Handeni hadi Kibereshi kilometa 20; Barabara ya Kitai hadi Litai kilometa 35; na Barabara ya Kibaoni hadi Stalike kilometa
50. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Bunge lako Tukufu wataona kwamba kazi inaendelea na tunaendelea kuZitendea haki barabara kama ambavyo zimepangwa katika bajeti yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Viwanja vya Ndege vina uhusiano wa karibu sana na huduma za usafiri kwa njia ya anga. Baadhi ya Waheshimiwa Wabunge kwa nyakati tofauti ikiwa ni pamoja na kwenye Bunge hili la bajeti wameainisha umuhimu wa usafiri wa njia ya anga. Kiutalam ndege inatakiwa kuwa angani kwa wastani wa masaa 12 hadi 15 katika saa 24 za siku, hiki ni kigezo kimoja muhimu cha matumizi sahihi ya ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, nchi yetu ina urefu wa zaidi ya kilometa 1,200 Mashariki hadi Magharibi na zaidi ya kilometa zaidi 1,700 kutoka Kaskazini Magharibi hadi Kusini Mashariki. Umbali huu ni stahiki sana kwa matumizi ya usafiri wa njia ya anga, hata hivyo ni viwanja vile tu, vya Julius Nyerere International Airport, Kilimanjaro International Airport, Mwanza na Dodoma ambavyo kwa sasa vinaweza kutumika kwa saa 24 kwa siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili Shirika letu la Ndege linufaike na uwepo wa viwanja hivi vya ndege, napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba Wizara kwa kushirikiana na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege itawekeza vifaa muhimu vyenye kukidhi mahitaji ya utoaji huduma wa ATCL ikijumuisha taa za kuongoza ndege kwenye viwanja vya kimkakati kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022. Viwanja ambavyo vipo kwenye mpango huo ni Uwanja wa Ndege


wa Kigoma, Uwanja wa Ndege wa Mbeya, Uwanja wa Ndege wa Mtwara, Uwanja wa Ndege wa Bukoba na Uwanja wa Ndege wa Geita.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Viwanja vya Ndege vya Tabora, Shinyanga, Sumbawanga, Songea na Iringa navyo wakati wa ukarabati wake vitafanyiwa utaratibu wa kuwekewa taa za kuongozea ndege. Ukamilishaji wa mradi huo wa kuweka taa za kuongozea ndege kwenye viwanja vya ndege utaongeza ufanisi kiutendaji kwa Kampuni ya Ndege ya Tanzania (ATCL). Maelekezo yangu ni kwamba kabla ya mwisho wa mwaka wa 2021 Mamlaka ya Viwanja vya Ndege, TANROADS na ATCL zikutane ili kujipanga kufikiwa kwa lengo hili mahsusi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi nyingi duniani zilizopiga hatua kubwa za kimaendeleo zimefanya hivyo kutokana na sababu kadhaa mojawapo ikiwepo ni kuwepo na huduma za reli zenye uhakika, gharama nafuu na salama. Kwa kulitambua hilo moja ya vipaumbele kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022 ni kuendelea na ujenzi wa reli ya SGR.


Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kulihakikishia Bunge hili Tukufu kwamba tutaendelea na ukamilishaji wa ujenzi wa vipande viwili vya reli vya SGR ambavyo ni Dar es Salaam hadi Morogoro kilometa 300, ambapo kwa sasa imefikia asilimia 91 na kipande cha Morogoro hadi Makutupora kilometa 422 kilichofikia asilimia 60.2 ya ujenzi na kipande cha Mwanza hadi Isaka kilometa 341 ambacho kwa sasa Mkandarasi yupo katika hatua za awali ya kuanza kazi.


Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango itaendelea na kipaumbele cha kutafuta fedha za ujenzi wa reli ya SGR kwa vipande vitatu vya Makutupora hadi Tabora kilometa 294, Tabora hadi Isaka kilometa 133 na kile cha Tabora hadi Kigoma kilometa 411.


Mheshimiwa Naibu Spika, ukamilishwaji wa reli hizi utaziingizia Taifa kipato kikubwa cha fedha za kigeni kutokana na kusafirisha mizigo ya nchi jirani za Burundi, Rwanda, Uganda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo. Kwa sasa wataalam wanakamilisha taratibu za kuanza kumtafuta mkandarasi wa kujenga kipande cha Uvinza hadi Msongati kwa ajili ya kubeba tani milioni tatu kwa mwaka za mizigo ya kwenda na kutoka Burundi hadi Jamhuri ya Demokrasia ya Kongo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu kwa kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango itafanyia kazi ushauri wa Waheshimiwa Wabunge katika kutumia mbinu mbalimbali za kupata fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa vipande vilivyobaki kwenye mtandao wa Standard Gauge.

Mheshimiwa Naibu Spika, usafiri wowote unatakiwa kuwa na vigezo vikuu vitatu; uhakika, gharama nafuu na usalama. Kwa upande wangu nitalisimamia kwa umakini suala la usalama wa usafirishaji na usafiri, nitaendelea kuhakikisha kwamba matumizi bora ya TEHAMA katika kuboresha huduma za uchukuzi unafanyika. Aidha, changamoto katika matumizi ya mifumo ya ufuatiliaji wa mabasi na tiketi za kielektroniki zitafanyiwa kazi kwa karibu na kushirikisha wadau wote hususani wasafirishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu taasisi za mafunzo Sekta ya Uchukuzi nchini itazidi kuboreshwa kwa kiwango kikubwa kutokana na ukuaji huo, ukuaji wa mahitaji ya wataalam wenye weledi wa kusimamia na kuendesha miundombinu na huduma za uchukuzi yanazidi kukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua hili Wizara itazidi kuboresha vyuo vya mafunzo ili viweze kuzalisha watalaam wenye weledi unaotakiwa kukidhi haja hii. Aidha, tutafanya jitihada za makusudi kukamilisha uanzishwaji wa Bodi ya Watalaamu wa Logistic na Usafirishaji ili watalaam wa sekta ya uchukuzi waweze kusimamiwa vizuri na sheria hiyo.


Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kuhitimisha, ningependa kuongelea hoja mahsusi ambazo zimetolewa na Wabunge, kwanza nikianza na hoja ya daraja la JPM ambalo tuliambiwa lina changamoto kwamba kuna mkandarasi ambaye hawajibiki vizuri, lakini ukweli ni kwamba mkandarasi yule ameahidi kuchangia huduma kwa jamii, kwa Kijiji cha Bukumbi kwa kuchangia milioni 50 na analipa mrabaha wa kila tripu ya kokoto kwa Halmashauri ya Wilaya ya Misungwi na hadi hivi sasa amekwishalipa jumla ya milioni
20. Vilevile mkandarasi huyo ameajiri wakandarasi wazawa wanne ambao wanamsaidia katika kazi hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile wazawa ambao wameajiriwa katika shirika lile wanafikia asilimia 90, kwani kuna wafanyakazi 274 ambao ni wa Kitanzania kati ya wafanyakazi 350 ambao wanafanya kazi pale. Mnamo tarehe 12 Januari mwaka huu nilitembelea daraja lile na taarifa hizi nilizipata pale mimi mwenyewe.


Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu ATCL tayari tunafanya kila tunaloliweza kuhakikisha kwamba mifumo ambayo inafanya kazi pale hairuhusu watu kufanya hujuma za kujaza ndege bila sisi wenyewe kutarajia. Mifumo ile hairuhusu kukata tiketi kama ndege imejaa lakini kuna station ambazo zina adhabu ya kuwa haziwezi kujaza ndege, vituo hivyo ni kama Bukoba, Songea, Mbeya na Iringa ambapo kiutalaam huwezi kujaza ile ndege na ukaondoka nayo kwa usalama, hivyo huwa haijai na pengine wananchi hudhani kwamba ndege ile imeachwa bila kujaa kwa makusudi, lakini siyo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri umetolewa kuhusu viwanja vya ndege, ujenzi wake, tutakwenda kulifanyia kazi hilo, kwamba kuangalia ni wapi waendelee kuvijenga ni TAA au TANROADS kulingana na ushauri ambao Wabunge wametupatia. Vilevile zile bypasses katika Miji ya Mbeya, Songea, Dodoma, Mwanza na Arusha na Iringa tutakwenda kuzifanyia kazi ili tuweze kuendana na ushauri wa Bunge lako Tukufu. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, ugawaji wa rasilimali vilevile utazingatiwa kulingana na ushauri walioutoa Wabunge hapa Bungeni na hakutakuwa na tashiwishi katika suala hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumeongelewa vilevile ucheleweshaji wa kutolewa GN kwa ajili ya barabara mbalimbali. Hili suala nalo tunaenda kulifanyia kazi tayari, tumekwishaongea na wenzetu wa Wizara ya Fedha na umeandaliwa mpango maalum ambao utahakikisha kwamba hizi GN za misamaha ya kodi zinatolewa mapema ili tuweze kuharakisha katika mijengo hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hitimisho, mwisho ninawaomba Waheshimiwa Wabunge waipitishe hoja yangu kwa kuwa tunataka kusimamia kwa niaba ya wananchi wote utekelezaji wa maendeleo na ya Ilani ya uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi ya mwaka 2020 pamoja na mpango wa Taifa wa Maendeleo wa Tatu wa mwaka 2021/2022 hadi 2025/ 2026.

Mheshimiwa Naibu Spika, nyenzo ya kutuwezesha sisi pamoja na watumishi wenzetu katika Wizara hii ni bajeti hii na kupitia kwake Serikali itafanya kila iwezekanalo kuhakikisha kwamba, miundombinu ya sekta ya ujenzi na uchukuzi na huduma zake zinaboreshwa na kulingana na matakwa ya sasa na miaka ijayo. Hivyo, kwa niaba ya wenzangu katika Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na kwa niaba yangu mwenyewe ninaomba sana bajeti hii ipitishwe ili kazi iendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hoja zingine ambazo zimetolewa na Wabunge zote tutazizingatia kwa mfano hii ya viwanja vinne ambavyo ni viwanja vya Sumbawanga, Kigoma, Tabora na Shinyanga ambavyo vina ufadhili wa benki ya EIB tunakwenda kumalizia maongezi nao ili tuweze kuhakikisha kwamba vile vikwazo ambavyo vilikuwepo tunaviondoa vyote na viwanja hivi vinaanza kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, kwa reli yetu ya TAZARA ambayo imeonekana ni kiungo muhimu kwa nyanda


za juu, tayari tuna mpango wa open access ambao tunaruhusu watu binafsi kuendelea na kupitisha mizigo yao pale. Tayari kuna kampuni moja ambayo inaitwa Calabash inafanya kazi hiyo na tayari tumetoa zabuni ambapo wauzaji wawili wa kizawa wako tayari kujiunga pale na kuweka treni zao binafsi ili ziweze kusaidia katika kuendesha pale TAZARA.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vile vile tunaendelea na ukarabati wa reli ya TAZARA ili kuhakikisha kwamba reli hiyo inatoa huduma nzuri katika mikoa ya nyanda za juu na kote inakopita.


Vilevile, tunalipa madeni ya TAZARA hasa ukizingatia kwamba tunatoa ruzuku ya mishahara kwa wafanyakazi wa TAZARA ili tuweze kuhakikisha kwamba TAZARA yetu inaendelea. La mwisho kwa TAZARA tunamalizia marekebisho ya sheria mpya ili tuweze kuboresha uwekezaji ndani ya TAZARA lakini vile vile tuwezeshe kuruhusu mambo ambayo yataongeza tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.
(Makofi)
Azimio la Bunge Kuhusu Mapendekezo ya Kurejea Katiba ya Tume ya Usafiri wa Anga ya Afrika ya Mwaka 2009
MHE. ENG. DKT. LEONARD M. CHAMURIHO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniruhusu kuwa mchangiaji wa kwanza kwenye suala hili. Huu mkataba ni mzuri kwa AU kwa maudhui yake na utakwenda kutoa fursa nyingi kama ambavyo imetamkwa kuhusu faida zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna masuala ambayo yamo ndani ya hii itifaki ya kuridhia ambayo hayakuelezwa sawasawa, ambazo ni changamoto tunazoweza kuzipata katika kutekeleza hiki kitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nitajikita kwenye Mkataba wa Yamoussoukro ambao umeongelewa katika itifaki hii, ambao maudhui yake ni kufungua usafiri wa anga kwa Afrika nzima. Huko nyuma tuliona kwamba hili ni jambo jema lakini kwa mataifa ambayo yana mashirika ya ndege machanga inakuwa ni changamoto kidogo na ni hatari.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii Yamoussoukro Decision kama ambavyo imeonekana kwenye hii itifaki, tulikubaliana mwaka 1999 lakini bado sisi tulikuwa hatujaridhia kuitekeleza. Tulisaini lakini hatujaridhia kwa sababu ya athari zake ambazo tuliziona kule nyuma, ilikuwa ni kwamba, tunapokuwa na shirika dogo linaloanza tukifungua anga moja kwa moja, mashirika makubwa yatatumeza na tutashindwa kukua kwa haraka. Tulikuwa tunaona kwamba tungepata muda fulani ili tuweze kukua ili tuweze kuingia katika ushindani huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maelezo yaliyotolewa sikupata hiyo comfort kwamba kuna muda fulani ambao tutajizatiti katika kujenga uwezo wa shirika letu la ndege ili tusimezwe na mashirika makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa Yamoussoukro Decision, una maana kwamba mashirika ya nje kwa mfano yanaweza yakapita ndani yakachukua abiria katika vituo vyetu vya ndani. Hiyo inafaa kwa nchi ambayo haina shirika la ndege, lakini kama una shirika lako la ndege inakuwa ni changamoto kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukienda katika kifungu cha tatu ambacho ni objectives, yaani malengo. Nikiangalia kifungu cha 3 (b) nikisoma kama kilivyoandikwa ni “Facilitating, coordinating and ensuring their successful implementation of Yamoussoukro Decision by supervising and managing African liberalise Air Transport Industry”. Hapa ndipo penye changamoto. Tukishachukua tungeambiwa vizuri kwamba tumejipangaje katika kulinda shirika letu la ndege lisimezwe wakati linakua.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, nikiangalia Article No. 4 (j) ambayo inasema, katika kazi mojawapo nikisoma hapa kama ilivyoandikwa ni “Pursuant to provision of the Article 9 of the Yamoussoukro Decision to discharge the duty of the executing agency of air transport in Africa”. Kwa hiyo bado tunasukuma kwamba, kama lengo litakuwa ni kusukuma utekelezaji wa hii Yamoussoukro Decision.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile nikiangalia Article 11 (i) function of the plenary nayenyewe inaonesha kwamba itahakikisha utekelezaji wa hiyo Yamoussoukro Decision. Pia nikiangalia Article 18 ambayo inaongelea vikwazo ambavyo unaweza kufanyiwa. Kuna vikwazo ambavyo tunaweza tukawekewa kama tutashindwa utekelezaji wa hiyo kitu. Kwahiyo, ina maana kama tukishakubaliana na ile halafu tukasema anga linafunguliwa, huwezi kulizuia shirika la ndege la nchi nyingine, kwa mfano kupita Dar es Salaam likachukua abiria likawateremsha KIA au Mwanza na ambapo hiyo ilikuwa ni majukumu ya mashirika yetu ya ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tungepata maelezo mafupi tujue kwamba katika kuridhia hii, je, ulinzi wa shirika letu dogo ambalo linakua litakuwaje na tumechukulia vipi? Kwa hali ilivyo na bado tunakua; nilikuwa nashauri kwamba, tuweke muda wa kuruhusu shirika letu kukua kabla ya kuingia katika huu mradi ambao utahusisha ku-liberalise Air Transport Industry kwani katika ukuaji huo tunaweza tukamezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Sita na Mkutano wa Saba wa Bunge pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa kwenye Mkutano wa Tatu na Mkutano wa Nne wa Bunge
MHE. ENG. LEONARD M. CHAMURIHO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ili na mimi niweze kuchangia hoja hii ya Taarifa ya Kamati ya Sheria Ndogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kumshukuru sana Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya ya kuliongoza Taifa letu vizuri na kuwa msikivu katika changamoto mbalimbali ambazo zinajitokeza katika taarifa hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kumpongeza Mwenyekiti wetu wa Kamati Dkt. Rweikiza kwa kazi nzuri aliyofanya ya kutuongoza sisi wanakamati katika kutekeleza jukumu hili adhimu ambalo la uchambuzi huu wa sheria ndogo kazi ambayo tumepewa na Bunge lako tukufu na ambayo tumeifanya kwa ukamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, madaraka ya kutunga sheria zote yanatolewa na Katiba yetu katika Ibara ya 4 na Ibara ya 64 ambayo Bunge lako tukufu limepewa lakini katika Ibara ya 97 ya Katiba hiyo hiyo imetoa fursa ya kukasimu madaraka hayo kwa Idara au mtu yoyote ambaye itaona inafaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, ningependa kuchukua fursa hii kuwapongeza hawa waliokasimiwa kufanya kazi hiyo ambayo wengi ni Mawaziri, Naibu Mawaziri pamoja na watumishi kwani wamefanyakazi hiyo kwa umakini. Wametuletea sheria nyingi sana sheria ndogo lakini ni sheria 11 tu ambazo zimeweza kuleta tashiwishi na kuweza kuleta uchambuzi huu hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuzingatia vigezo vya uchambuzi ambao tumefanya katika Kamati yetu mimi nitajikita zaidi katika usahihi na ufasaha wa uandishi wa majedwali katika sheria ndogo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi sheria ndogo zinapotungwa lengo lake kuu ni kurahisisha utekelezaji wa sheria mama ili ziweze kueleweka vizuri zaidi na kuelezeka kwa urahisi zaidi. Hivyo ikiwa sheria hizo hazikuandikwa kwa usahihi na kwa umakini mkubwa, basi zinaweza zikaleta mkanganyiko katika utekelezaji wake au changamoto vilevile katika ulewela ulio sahihi.

Kwa hiyo, nitaangalia katika kurejea kanuni sahihi katika utungaji wake, lakini vilevile kuangalia kama kanuni hizo ambazo zimerejewa zipo au hazipo, lakini vilevile kama maudhui yaliyotakiwa kuwepo katika kanuni hizo ni yale ambayo yalikuwa yamelengwa na sheria mama.

Mheshimiwa Naibu Spika, wajibu uliokasimiwa wa kutunga sheria ndogo unaweza kupoteza maana yake kama haya majedwali ambayo lengo lake lilikuwa ni kurahisisha badala yake linakwenda kuzua changamoto au ugumu wa uelewa katika kanuni hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa mifano michache; katika sheria ndogo ya The Electricity Electrical Installation Services Rules ya mwaka 2022 ambayo imetungwa kupitia Sheria ya Electricity Act, Sura ya 131 kuna majedwali ambayo yamewekwa mle, katika jedwali la nne la kanuni hiyo linamruhusu mwenye leseni ya uunganishaji umeme akishaunganisha basi ampatie mteja wake cheti cha kuonesha nini amefanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, maudhui ya kanuni hiyo yanataka huyo muunganishaji atoe cheti hicho na kuelezea kila kitu kilichopo na yanasema kwamba muonekano wa cheti hicho ni kama ambavyo umeonekana katika jedwali hilo. Ukiangalia jedwali hilo muonekano wa cheti hicho haupo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, unakuta sasa kanuni hii japokuwa imetoa mwelekeo kwamba nini kifanyike, lakini cheti ambacho kinatakiwa kitolewe au muonekano wake haupo katika kanuni hiyo. Kwa hiyo, badala ya kuwa imesaidia imeleta tena mkanganyiko mkubwa zaidi kwani imesema toa cheti kama kilivyooneshwa katika jedwali na kwenye jedwali cheti hicho hakipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mwingine ambao nautoa ni huu wa kanuni ya The Copy Rights Enabling Rights, Licensing and Rights to Benefits Re-Sells Regulation ya mwaka 2022; kanuni hii nayo imetokana na Sheria ya The Copy Right and Enabling Rights Act, Sura Namba 218.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jedwali la sheria hii limetoa mfumo wa kutoa mgawanyo wa mapato, wao wameita distribution rules for public performance and broadcasting, lakini utakuta kwamba kanuni ambayo imetungwa hapo, maudhui yake yanatokana na kifungu cha 29 cha sheria hiyo. Lakini ukiangalia maudhui ya sheria na kanuni iliyotungwa ni vitu viwili tofauti. Kwa hiyo, unakuta sasa badala ya kanuni hiyo kwenda kurahisisha utekelezaji wa sheria hiyo, inakwenda kuleta changamoto kubwa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, umakini mkubwa unatakiwa na tunashukuru sana uongozi wa Mwenyekiti wetu ambaye alituongoza vizuri katika kupitia kanuni hizi ili kuhakikisha kwamba hatuleti mchanganyiko mkubwa na wajibu uliokasimu kwa hawa kutunga sheria ndogo unatekelezwa kwa usahihi na kwa umakini mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mwingine uko katika Sheria ya The Tanzania Shipping Agencies Performance Benchmark Regulations ya mwaka 2022; kanuni hii imetokana na The Tanzania Shipping Agencies Act, Sura Namba 415. Katika kanuni hii, kanuni ya 16 inayohusu utolewaji wa notisi, notisi ya ukubalifu yaani compliance notice ambayo ni kitu muhimu kwamba ameridhia au amefanya kitu ambacho kinatakiwa kufanywa.

Mheshimiwa Naibu Spika, imeelekeza kuwa wakala wa meli atatoa notisi kwa namna ilivyofafanuliwa katika jedwali la tatu. Kwa hiyo, unakuta kwamba jedwali limetamkwa vizuri kwamba notisi itatolewa kwa mfumo huu. Ukienda kwenye jedwali hilo, unakuta kwamba jedwali hilo la tatu halipo. Sasa unakuta huku umeelekezwa uende jedwali namba tatu ukapate mwelekeo wa hiyo notisi, lakini kwenye utekelezaji utakwama kwa sababu jedwali hilo halipo. Kwa hiyo, hiyo italeta usumbufu katika utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mwingine ambao naweza kuutoa ni kuhusu muingiliano au mchanganyiko unaoletwa na lugha katika sheria; hHii nitatolea mfano katika The Mining Government Mineral Warehousing Regulations ya mwaka 2022 ambayo inatokana na The Mining Act, Sura namba 123.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jedwali hilo utakuta linakudai fomu namba tatu ambayo imetungwa kwa lugha ya Kiingereza na Kiswahili, lakini ukiangalia usahihi wa maneno katika fomu ile Kiswahili na Kiingereza unakuta kwamba maana hazilingani au hazishabihiani. Kwa hiyo, unakuta kwamba hii inaleta changamoto katika ule utekelezaji, nini kifatwe, tafsiri ya Kiingereza au tafsiri ya Kiswahili?

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta kwamba katika jedwali hilo hilo, fomu nyingine zimetungwa kwa lugha moja tu ambayo ni Kiingereza, basi Kamati yetu imeona kwamba ni muhimu kabisa kwamba lugha inayotumika ieleweke vizuri na tafsiri zishabihiane ili kutoleta mchanganyiko katika utekelezaji wa hayo mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii na naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ENG. LEONARD M. CHAMURIHO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ili niweze kuchangia katika bajeti hii ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Napenda kukupongeza wewe unavyoongoza Bunge pamoja na Mheshimiwa Spika, Naibu Spika na Wenyeviti wenzako kwa kazi nzuri mnayofanya katika kuendesha Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda vile vile kutumia fursa hii kumpongeza Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya kwa maendeleo ya nchi hii. Tumeshuhudia kwamba anaweka utendaji mkubwa sana wa mara moja katika sekta hii ya elimu na hili ni jambo kubwa ambalo sasa tunaanza kuona matokeo yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimechungulia bajeti ya elimu, katika miaka mitatu kama ilivyo katika vitabu vyetu, inaongezeka kila mwaka, na hii ni dhahiri kwamba Mheshimiwa Rais ana dhamira ya dhati ya kuhakikisha kwamba elimu inakuwa bora katika nchi hii. Vilevile nampongeza Waziri Profesa Adolf Mkenda pamoja na Naibu Waziri Mheshimiwa Omari Kipanga kwa kazi nzuri wanayoifanya, vilevile na wataalam wao, Katibu Mkuu, Profesa Nombo na Manaibu Katibu Wakuu wawili, Makamishna wote nakadhalika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii imesheheni wabobezi na tunaona kweli kazi inakwenda vizuri, tunawapongeza sana. Uwekezaji huu mkubwa ambao umewekwa na Mheshimiwa Rais katika miundombinu ya elimu unahitaji kulindwa na vilevile kupatiwa viwezeshaji. Ulinzi wa miundombinu utawezeshwa katika matengenezo ya mara kwa mara kuhakikisha kwamba miundombinu hiyo inadumu, lakini katika huduma zake viwezeshi kuhakikisha kwamba walimu na vifaa vinapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita zaidi katika elimu ya juu ambayo katika hayo mawili nitaangalia utafiti pamoja na utayarishaji wa walimu. Walimu wa Elimu ya Juu hawana chuo maalum cha kuwafundisha kama ambavyo tunafahamu vyuo vingine vya walimu hapa kwamba kuna chuo kinachofundisha walimu, lakini kwa elimu ya juu ni vyuo vyenyewe ndiyo hutengeneza walimu wake kulingana na hadhi ya chuo. Kwa hiyo, chuo kinaandaa walimu wake na ubora wake unategemea na jinsi ambavyo itapanga yenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, nimeangalia ukurasa wa 34, kwenye utakelezaji wa bajeti iliyopita, nikaona kwamba ndiyo, ameshughulikia mambo ya udahili vizuri, ameshughulikia vilevile na elimu ya wadahiliwa, lakini nilivyoangalia jinsi anavyoshughulikia walimu wa walimu, nikaona hapo kuna ombwe. Nilipoangalia vilevile katika ukurasa wa 76, nikaona mapendekezo ya bajeti hii anayoiomba, nikaona vilevile kwamba ameweka utafiti, ameupa kipaumbele. Kwa hilo nampongeza sana, kwani hilo ndilo ambalo linawezesha ufundishaji wa hao walimu wa walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kwamba bajeti hii haijaweka wazi jinsi wataalam hao, walimu wa walimu wanavyotengenezwa, kwa sababu kama nilivyosema mwanzoni, hakuna vyuo vya kuwaandaa walimu wa walimu. Hivyo, vyuo vinakuwa huru kutengeneza hayo matokeo ya walimu wanaowatengeneza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi kwa sababu walimu hao wanakuwa wana shahada, vilevile ni zao la vyuo vikuu; na kuondoa huu utaratibu wa mwalimu kusoma hapo hapo na kufundisha hapo hapo, ambapo kitaalam wanaita inbreeding, vyuo vingi huhitaji kufundisha walimu katika vyuo vingine, na hapa ndipo changamoto inapoanza, kwa sababu inahitaji aidha watengewe fedha au wapate ufadhili. Sasa hapa kwenye ufadhili, ndipo changamoto inapokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna methali ile inayosema kwamba “anayemlipa mpiga zumari ndiye anayechagua wimbo.” Sasa katika hili, wafadhili wengi huchagua kufadhili fani ambazo wanazipendelea wao, siyo fani ambazo chuo kinazihitaji. Kwa hiyo, hapo ndipo changamoto inapoanzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakuta kwamba fani ambazo hazina mvuto kwa wafadhili zinaathirika katika vyuo vyetu. Unakuta vyuo vinapata wafadhili, lakini walimu wanaokwenda kufundishwa wanalundikana katika fani ambazo ni fani pendwa za hao wafadhili. Kwa hiyo, unakuta kwamba kweli ukihesabu idadi ya Shahada za Uzamivu ni nyingi lakini mchanganuo wa fani katika hiyo fani inakuwa kidogo kuna changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inatokana na vitu viwili. Moja, kuna fani nyingine unaweza kuziona kama ni fani ngumu, ambazo hazina mvuto kwanza kwa wanafunzi wenyewe. Pili, ni fani ambazo ni ghali kuzifundisha. Kuna fani nyingine ambazo kumfundisha mwalimu mmoja au mhitimu mmoja, unaweza ukafundisha wengine watatu. Kwa hiyo, hiyo haivutii wafadhili katika kuwekeza huko. Matokeo yake inakuwa ni nini sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta kwamba katika idara mbalimbali fani ambazo hazina mvuto zinapungua miaka hadi miaka, lakini matokeo tunapata. Wahitimu wanazidi kutoka lakini wamehitimishwa na nani? Wamehitimishwa na walimu ambao, fani zile ambazo hazipo, vilevile zinakuwa vichwani mwao hazipo, na matokeo yake unakuta baadhi ya kozi nyingine zinaahirishwa, kwa sababu wataalam hawa hawapo. Vilevile wanafunzi wa wauzamivu na wa uzamili wanaathirika kwa sababu wanakosa hiyo huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka kushauri Wizara hii ya Elimu, Sayansi na Teknolojia kwamba, moja, vyuo vya elimu ya juu vianishe hizi kozi au utaalam ambao hauna mvuto kwa wafadhili. Baada ya kupata orodha hiyo ya fani ambazo hazina mvuto kwa wafadhili, basi Serikali itenge fedha kwa ajili ya fani hizo, kwani ni muhimu kwa Taifa lakini hazina wa kuzifadhili. Kwa hiyo, hiyo itatuwezesha kuhakikisha kwamba mazao ya chuo yanapotoka, pamoja na hiyo degree kubwa, lakini vilevile fani ambayo iko kichwani kwao imekamilika kama ambavyo tunaitarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa muda mfupi, Serikali iruhusu vyuo viendelee na utaratibu wao wa kutengeneza walimu wao wenyewe bila kuviingilia kwa sababu hilo ndiLo litakaofanya waweze kuainisha hizo fani na kuzitafuta na kuzitengeneza jinsi wanavyoweza. Hii ni pamoja na kuruhusu watoe mikataba kwa watu ambao wanadhani wanaweza kuwa na fani hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, japokuwa utafiti umetajwa mle ndani, vilevile tuondoe hii dhana kwamba fedha za utafiti katika vyuo ni fedha za kuliwa na hawa walimu. Ni fedha muhimu sana ambazo ndiyo chanzo cha kutengeneza utafiti na utafiti huo ndiyo unaofanya kutoa hao walimu bora; walimu wa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona muda wangu unakwisha. Natoa shukurani kwako na kwa hili, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo Kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Kumi na Mkutano wa Kumi na Moja pamoja na Uchambuzi wa Taarifa za Utekelezaji wa Maazimio ya Bunge kuhusu Sheria Ndogo zilizowasilishwa Bungeni kwenye Mkutano wa Nane na Mkutano wa Tisa
MHE. ENG. DKT. LEONARD M. CHAMURIHO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii kuweza kuchangia, nakushukuru kwa hilo. Pili ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuendelea kuliongoza Taifa hili vizuri.

Tatu, ninapenda kuwapongeza Mawaziri wote waliofanikiwa kuhudhuria katika vikao vyetu vya Kamati ya kudumu ya Sheria Ndogo, kwani kwa kufanya hivyo wamekuja kujadili dosari mbalimbali ambazo tumeziona katika sheria ambazo wamekasimiwa kuzitengeneza na Bunge lako hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, dosari hizi kwa kweli huwa zinakwamisha utekelezaji wa sheria mama au zinaleta usumbufu katika utekelezaji wa sheria hizi kwa wananchi. Katika Sheria Ndogo hizi huwa kuna majedwali mbalimbali ambayo hukusanya taarifa mbalimbali ambazo zipo kwa wingi na ambazo zinahusu mambo yanayofanana.

Mheshimiwa Naibu Spika, dosari katika majedwali haya huwa yanaathiri sana au kwa kiasi kikubwa utekelezaji wa sheria hizo, ambazo huwa zimetungwa kutokana na Sheria Mama na kama nilivyosema awali zinaleta usumbufu mkubwa katika utekelezaji wake. Nitatoa mifano ya majedwali mawili, kwanza nitaanzia kanuni za usafirishaji wa mazao ya misitu kuingia ndani ya nchi na kutoka nje ya nchi, ambazo ni tangazo la Serikali Namba 266 iliyotolewa tarehe 31 Machi, mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la kanuni hizi ilikuwa ni utekelezaji wa Sheria za Misitu, Sura Namba 323 ambayo katika hizo tunapatia mapato ambayo yanachangia katika uendeshaji wa kila siku wa Serikali na Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jedwali hilo kuna vituo vya kuingia na kutoka nchini kwa mazao ya misitu, ukiangalia njia mbalimbali za kutokea nje ya nchi ambazo ni njia za usafiri utaona kila aina ya usafiri, aidha imewekewa au kuna nyingine hazikuwekewa. Nitapitia moja moja, tukianza na barabara, katika njia ya barabara kanuni hizi zimetoa vituo vya kutosha ambavyo vinaweza kutumika katika kukagua bidhaa hizo. Tukienda kwenye usafiri kwa njia ya reli, vituo vilivyotolewa ni Moshi, Arusha, Tunduma na Kahe junction tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa unaona dhahiri kwamba kuna vituo vingine ambavyo vinahusisha mazao kutoka nje ya nchi ambavyo havikuwekwa, hivyo kutokuwemo katika vituo hivyo, aidha kutaleta usumbufu kwa wananchi kwamba wakifika katika vituo hivyo itabidi wasafiri umbali mkubwa kwenda kwenye vituo vingine ambavyo vinaweza kusababisha ukaguzi wa mazao hayo kitu ambacho ni usumbufu. Kwa hiyo, hili limebidi Kamati yetu imeshauri lirekebishwe na tungeomba Wabunge mtuunge mkono ili dosari hiyo iweze kusahihishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika usafiri wa njia ya maji ambao unahusisha bandari, katika Bahari ya Hindi vituo vimewekwa vya kutosha kutoka kaskazini hadi kusini. Vilevile katika Ziwa Tanganyika ambapo ni mpaka kati ya nchi yetu na nchi zingine vituo vimewekwa. Ukiangalia Ziwa Victoria ambalo tunapakana nalo katika nchi mbili, hakuna kituo ambacho kimewekwa kwa kusafirisha mazao hayo. Hivyo basi inamaana wananchi wakitaka kusafirisha mazao yao ya misitu nje ya nchi kwa njia ya maji usafiri ambao unajulikana ulimwenguni kwamba ndiyo usafiri wa rahisi kabisa hakuna vituo. Kwa hiyo, inabidi huyo mwananchi asafiri kwenda katika vituo ambavyo vinaruhusiwa kitu ambacho ni usumbufu mkubwa wakati ambapo vingeweza kuwekwa vituo katika njia hizo za usafiri wa maji katika Ziwa Victoria na ikaweza kurahisisha jukumu hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika Ziwa Nyasa hakuna kituo ambacho kimewekwa na wakati Ziwa hilo ni mpaka kati yetu na nchi ya jirani. Kwa hiyo, kukosekana kwa vituo hivyo mazao ya miti kuingia au kutoka kupitia Ziwa hilo ni usumbufu au inamuongezea gharama huyo mtumiaji wa usafiri huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, usafiri wa anga. Vilevile katika usafiri wa anga ambao husafirisha kupitia viwanja vya ndege hakuna kituo hata kimoja ambacho kimewekwa kwa ukaguzi wa mazao hayo. Hiyo nayo inaleta usumbufu kwani ina maana kwamba, unaweza kupata usumbufu mkubwa ukiwa pale wakati ambapo ukaguzi huo ungeweza kufanyika pale kwani inafahamika kabisa kwamba ule ni mpaka ambao unaweza kutumika katatika kusafirishia mazao hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mwingine unatokana na majedwali ambayo yametengenezwa katika Kanuni ya The Law School of Tanzania Admission Fee and Conduct of Practical Legal Training Kanuni za mwaka 2022. Katika kanuni hizo ukiangalia majedwali pale hakuna form maaalum itakayotumika katika maombi kulingana na kanuni ambayo imetengenezwa, Kanuni Namba Nne. Huu ni usumbufu mkubwa kwani unaweza ukakuta kwamba katika maombi yale muombaji akashindwa kuweka vitu ambavyo vinavyotakiwa ambayo italeta usumbufu katika udahili wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika kanuni hizohizo ukiangalia jedwali la ada limetumia maneno ambayo hawakutoa maana yake ambayo yanaweza kuleta mkanganyiko mkubwa. Kwa mfano, wametumia neno Tanzanian students bila kueleza maana yake. Katika uchambuzi wetu tumeona hili neno linaweza kuleta usumbufu kidogo, kwamba je, linamaanisha ni raia wa Tanzania au linamaanisha mtu aliyesomea Tanzania au vinginevyo? Sasa hiyo ili isiweze kuleta huo mkanganyiko katika hayo mambo tulikuwa tumeazimia kwamba maneno ambayo yanaweza kuleta utata katika matumizi yake yaweze kutolewa tafsiri katika kanuni ili kuwafanya watumiaji waweze kuyatumia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ikiambatana na hiyo vilevile kuna neno non-Tanzanian student ambayo katika uchambuzi wetu tuliona kwamba linaweza kutafsiriwa kwamba ni mwanafunzi ambaye hakusomea Tanzania. Anaweza kuwa mtanzania ndiyo lakini hakusomea Tanzania na akaambiwa wewe ni non-Tanzanian student kwa hiyo, tukasema hii tafsiri zitolewe ili mkanganyiko huu usiwepo kabisa katika kanuni hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jedwali la kwanza vilevile za kanuni hizo ziliwekwa ada mbalimbali ambazo zinatumika katika chuo hicho, lakini unaona ada ya maombi ya kujiunga haina form wakati ambapo imeainishwa kule ndani na inaweza kuleta usumbufu. Katika jedwali hilo hilo vilevile imeoneshwa changamoto ya kuomba ada kwa Wanasheria Wasaidizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika Sheria Mama ambayo ni The Law School of Tanzania Act, Sura ya 425 katika kifungu cha pili, kinatamka waziwazi kwamba sheria hiyo inatumika kwa wanasheria tu, sasa ukikuta kwenye jedwali wameweka ada za Wanasheria Wasaidizi wakati sheria mama inadai sheria hiyo itumike kwa Wanasheria tu wenye shahada ina maana kwamba Kanuni hizi zimevuka mipaka yake na kufanya kitu ambacho hakiruhusiwi, hivyo inabidi ifanyiwe marekebisho ya kuweza kuondoa kasoro hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo tumeliona waziwazi ni kutohuishwa kwa majedwali kwa wakati. Katika jedwali hilohilo ambalo lilikuwa linahusu ada, kuna ada ya mapitio yanayofanywa na NACTE, taasisi ambayo haipo kisheria sasa hivi na imebadilishwa, hivyo uhuishwaji wa Majedwali haya ni muhimu kwa wakati ili yasilete usumbufu katika utekelezaji wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mchango huu wa majedwali, tumeazimia kwamba majedwali haya yarekebishwe kwa wakati ili tuweze kupata utekelezaji mzuri wa sheria hizi kama ambavyo Bunge liliazimia kwenye kutunga sheria mama.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini
MHE. DKT. LEONARD M. CHAMURIHO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuweza kuchangia hoja hii muhimu ambayo imewekwa mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze na preamble ya haya makubaliano tukiangalia ile ya kwanza kabisa chimbuko ni ziara ya Mheshimiwa Rais alipokwenda kule Dubai. Kwa hiyo, kwa ziara hilo tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kututafutia rasilimali za kuweza kuendeleza miundombinu ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, katika preamble hiyo hiyo kifungu cha pili kinaongelea chimbuko lingine ambalo ni maombi ya TPA na DP World. Ningependa kuwapongeza Wizara pamoja na TPA kwa kuweza kufahamu udhaifu uliokuwepo TPA na kutafutia changamoto cha kuweza kutatua.

Mheshimiwa Spika, kwa wengi wanaweza kuwa hawafahamu kwa nini hawa waliweza kumtafuta mwekezaji mahiri. Nitatoa mifano mitatu ambayo itaonesha ni kwa nini unahitaji mtu mahiri ili uweze ku-deal na hivi vitu vikubwa vikubwa.

Mheshimiwa Spika, mfano wa kwanza tulitaka kununua spare za engine za TAZARA zinaitwa tracks and motors, tulipotoa ile order tuliambiwa tunaweza tukaipata baada ya miaka mitatu na kosa letu lilikuwa ni moja tu kwamba sisi tulikuwa niwaagizaji wadogo, hatuwezi kuweza kuitoa design team ya wale manufacturer wahame watutengenezee sisi kitu kidogo, kwa hiyo tutakwenda baada ya miaka mitatu.

Mheshimiwa Spika, mfano wa pili ambao nitautoa kwa nini tunahitaji wawekezaji mahiri, ni pale tulipoagiza vichwa vya treni. Tulipoagiza vichwa vya treni tulipata changamoto moja kubwa, klila ukiagiza unaambiwa kwamba order yako ni ndogo mno kuweza kuhamisha design team yetu ikafanya kazi yako ili upate hiyo order yako. Kwa hiyo, unajikuta unawekwa kwenye foleni ya miaka mitatu au minne mbele na ikitokea changamoto yoyote unasukumwa mbele zadi? Ni kwa sababu ni mdogo.

Mheshimiwa Spika, mfano wa tatu ambao ningependa kuutoa utahusu bandari wenyewe. Katika hayo maendelezo ya bandari yaliyofanywa sasa hivi tuliagiza hizo sea to shore gantry ambazo ni crane ambazo zinatumika pale. Tulipata muda ambao ni wa miaka mitatu mbele, kosa letu moja tu ninyi ni wadogo mno kuweza kutoa hiyo order mkapata moja kwa moja. Kwa hiyo, inabidi uwe una mwekezaji mahiri ambaye akiagiza order yake ni order kubwa ambayo itasababisha uweze kupata hiyo order. (Makofi)

Sasa huyu mwekezaji mahiri kama tulivyoambiwa amewekeza kwenye bandari nyingi sana. Kwa hiyo, hata kama akitoa order yake ni kubwa, kwa hiyo uwekezaji wake unakwenda moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile katika uendeshaji huu vifaa hivi huharibika, vinapoharibika tunapambana na changamoto hiyo hiyo kwamba unapoagiza vipuri na wewe ni mtu mdogo unaingia kwenye foleni ndefu sana, imeharibika crane yako moja unataka upate hicho kipuri unaambiwa kipuri chako utakipata baada ya miaka mitatu. Sasa huwezi kuwa unasubiri hapo na wenzako wanapata vipuri kwa sifa moja tu, kwamba wao order zao ni kubwa kwani ni wakubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa nataka kuchukua fursa hii kuwapongeza Wizara kupitia TPA kwamba kwa kutafuta mwekezaji mahiri ili aweze kutuboreshea bandari zetu ili tuweze kupata uendelezaji wa haraka.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu wa tatu utaenda kwa wale waliojadili huu mkataba. Kama ilivyojieleza katika preamble pale, sisi tulikwenda kuomba kusaidiwa. Sasa unapoenda kuomba katika majadiliano huwa uko kwenye weaker position, lakini unaona kwamba katika majadiliano haya hawa waliojadiliana wameweza kabisa kutuletea mfumo mzuri kabisa ambao unaweza kutuondolea changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, mfumo waliouweka ambao unaanzia IGA unatoka kwenye IGA unakuja kwenye Host Government Agreement ambayo ni kwamba mnajadiliana Serikali itampa nini mwekezaji, lakini wa tatu tutakwenda kwenye land lease ambayo utampangisha mwekezaji ili apate sehemu ya kufanyia biashara na mwisho ni hiyo concession agreement, ni mfumo ambao ni mzuri ambao unaweka hatua mbalimbali ambazo zinaweka. Kwa hiyo, ningependa kuchukua hatua hiyo kuwapongeza hao ambao waliweza kufanya hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile pongezi ambazo ninawapa hao ni kuweza kuweka mikataba ijadiliwe wakati ule ambapo inapotakiwa. Hili litawezesha hawa watakaojadili hiyo mikataba inayokuja kuweza kuangalia changamoto za nyuma ambazo tulikuwa nazo na kuweza kuzichukulia katika mukhtadha wakati uliopo. huu nao ni mtindo mzuri sana ambao inabidi tuwapongeze katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano ukiangalia kifungu cha nane ambacho kinaongelea ardhi, maana yake ni kwamba wameweka kwamba kwa sababu kitajadiliwa kwa sheria za kwetu kitajadiliwa kwa mukhtadha wa sheria zilizopo. Ukiangalia kwenye kifungu cha tisa, vivutio; vivutio wamesema vitawekwa kulingana na sheria za kwetu, kwa hiyo kwa sababu wameviweka vitajadiliwa kule mbele, jukumu letu ni kuangalia hizi hofu za Watanzania na kuziingiza katika ile mikataba kama vizuizi hatarishi ambavyo tunavilania. Kwa hiyo, hizi hoja ambazo zinatolewa na hofu za wananchi nashauri tu kwamba Serikali izichukue ili ziweze kuingia katika majadiliano hayo tuweze kupata kilicho bora ambacho Watanzania wote wanakitaka.

Mheshimiwa Spika, vilevile ningependa kuwapongeza kwa kuweza kulinda ajira za Watanzania. Katika miradi hii mikubwa huwa kuna mvutano mkubwa sana katika kulinda hizi ajira. Ukichukulia mfano wa mkataba wa SGR kwa wafanyakazi wa kawaida asilimia 80 wanatakiwa wawe Watanzania na asilimia 20 ndio wawe wageni. Hiyo ni ratio nzuri tu na kwa wale kwa upande wa management asilimia 20 wanakuwa Watanzania, asilimia 80 watakuwa wa kwao.

Kwa hiyo, hii ni mifano ambayo imeangaliwa huko nyuma na sasa hivi inaweza ikaangaliwa vizuri zaidi katika mikataba inayokuja. Kwa hiyo, tuwapongeze hawa kwa kutuwezesha kuruhusu tujadili mikataba hii mbele ili tuangalie huko nyuma tulivyofanya na tuweze kuboresha kwa kadri ambavyo tutaona inafaa.

Mheshimiwa Spika, sitakuwa nimetenda haki bila kuongelea machache ya hofu. Napenda kujadili hofu ambayo imejitokeza katika majadilano huko nje.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa kengele ya pili imeshagonga. Ahsante sana.

MHE. DKT. LEONARD M. CHAMURIHO: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ENG. DKT. LEONARD M. CHAMURIHO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru kwa kuniona na kunipatoa nafasi hii kuchangia hoja hii muhimu. Kwanza ninapenda kuunga mkono hoja bajeti hii kwani ni bajeti ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda vilevile kumpa pongezi Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutuletea bajeti ya wananchi, kwani ni bajeti murua ambayo ukiangalia amefuta ada kwa kidato cha tano na sita, vilevile kwa vyuo vya ufundi ili tuweze kupata rasilimali watu nzuri kwa nafuu kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ametoa mikopo kwa vyuo vya kati na anaendelea kutafuta rasilimali kwa miradi mikubwa ya maendeleo kama vile SGR, Bwawa la Nyerere, na hivi karibuni ametutafutia wawekezaji wazuri katika Bandari yetu ya Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nampongeza Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na timu yake; Naibu Waziri, Mheshimiwa Chande; Katibu Mkuu, Dkt. Natu Mwamba na Naibu Makatibu Wakuu pamoja na timu nzima, kwa kuweza kumsaidia Mheshimiwa Rais kutuletea bajeti hii ambayo ni nzuri kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ntajikita kwenye vifaa vya ujenzi ili kuona ni jinsi gani tutawezesha miundombinu hii ambayo Mheshimiwa Rais anaitolea pesa itakavyoweza kutusaidia ili tuweze kupata value for money.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukurasa wa 107 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri imeelezea vizuri kuhusu cement na jinsi ambavyo inalindwa pamoja na wafanyakazi wake. Lakini ninapenda kutoa mchango wangu kwa kuhakikisha kwamba hii cement ili isipande bei ni nini ambacho tunatakiwa tukifanye kwenye uendeshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia hapa nina orodha ya viwanda 14 vya cement (saruji) kama ambavyo vimewasilishwa, na vilevile nimeangalia hotuba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara ambayo imeonesha kwamba jumla ya uwezo wa uzalishaji (installed capacity) ya viwanda vyetu hivi ni tani milioni 10.48. Lakini uzalishaji wa sasa hivi ni tani milioni 7.6, na matumizi kwa sasa hivi ni tani milioni 7.1. Kwa hiyo, tuna ziada kidogo ambayo inakwenda nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ukiangalia katika hiyo bajeti inasema kwamba bei ya cement imeonesha uhimilivu, kwani ina ongezeko la 0.5 tu. Sasa hii inabidi ilindwe ili tuweze kupata unafuu katika bei ya saruji tuweze kuendeleza miundombinu yetu ambayo tunaijenga kwa pesa ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza Serikali ijikite katika kuhakikisha kwamba hii bei haipandi. Nini kifanyike; ukiangalia uwezo wa kuzalisha saruji na baadhi ya viwanda vyetu utagundua kwamba viwanda vikubwa vinazalisha chini sana ya uwezo wao. Ukiangalia kwa Mfano Kiwanda cha Mbeya Cement, kinazalisha asilimia 43 tu; ukiangalia Dangote Cement, anazalisha asilimia 54 tu. Kwa hiyo, hivi viwanda vikiongeza uzalishaji vitahakikisha kwamba cement (saruji) inakuwepo na haitapungua bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma tumeona ukosefu wa saruji umesababisha bei kupanda, lakini hawa wawekezaji wakubwa kama watapandisha uzalishaji uendane na installed capacity, tunaweza kuhakikisha kwamba tunapata saruji ambayo itakuwa ina bei ambayo inaeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tulishuhudia huko nyuma kwamba viwanda hivi vikipanga matengenezo kwa pamoja vinasababisha uhaba wa saruji, kitu ambacho kinasababisha tena bei hiyo kuweza kupanda. Hivyo, tukiweza kuhakikisha kwamba hivi viwanda tunaviratibu vizuri ili vifanye matengenezo yao makubwa, siyo kwa wakati mmoja ili uzalishaji usiathirike, basi tutahakikisha kwamba upatikanaji wa saruji unaendana vizuri na uwezo wa viwanda hivyo ili viweze ku-maintain hiyo bei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, kama Wizara husika itaangalia, kuna orodha ya kampuni ambazo tayari zimekwishajiandikisha hapa lakini bado viwanda vyao havifanyi kazi. Kama vitaanza kufanya kazi tutahakikisha kwamba saruji itapatikana na vilevile tutaweza kupata bidhaa hiyo kwa bei nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye nondo unakuta kuna changamoto hiyohiyo. Ukurasa wa 144 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri imeongelea hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naona umeniwashia taa.

MWENYEKITI: Ndiyo Mheshimiwa, muda wako umemalizika.

MHE. ENG. DKT. LEONARD M. CHAMURIHO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda tu kumalizia kwa kusema kwamba viwanda tuvijengee uwezo wa kuzalisha bidhaa hizi ndani ili tuweze kupunguza bei na miundombinu anayotafutia pesa Mheshimiwa Rais iweze kudumu. Ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ENG. DKT. LEONARD M. CHAMURIHO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia katika hoja hii ya Bajeti Kuu ya Taifa. Kwanza napenda kuunga mkono hoja ya bajeti hii ambayo ni bajeti ya wananchi iliyowasilishwa na Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, napenda kutoa pongezi kwa Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea bajeti ya wananchi ambayo kwa kweli imekidhi mambo mengi. Kwanza imeongezeka kwa asilimia 8.1 ambayo inaashiria kwamba vitu vingi vimeongezeka, huduma nyingi zimeongezeka. Pili, amefuta ada na mambo mengine mazuri. Pia ni bajeti ambayo ina mambo mengi mazuri ambayo hata muda wa kuyaelezea unakuwa ni kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, nitoe pongezi kwa Mawaziri wote, Manaibu Waziri, Makatibu Wakuu na Manaibu Katibu Wakuu kwa kazi nzuri wanayofanya ya kumsaidia Mama kutuletea maendeleo katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia bajeti yetu ilivyopangwa na kuletwa, utekelezaji wake utahitaji mambo mawili makubwa, ambayo kwanza ni kuongeza mapato; na pili, ni kubana matumizi. Tunanipongeza bajeti hii kwani hayo yote mawili yamejitokeza mabaya na katika uwasilishaji wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia dhima ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa ya Mwaka 2021/2022 hadi 2025/2026 ni kujenga uchumi shindani wa viwanda kwa maendeleo ya Taifa. Sasa mimi nitaelekeza mchango wangu katika viwanda vya vifaa vya ujenzi, wajenzi wenyewe yaani Wakandarasi na tatu, ni uhai wa matokeo yao ya ujenzi huo kwamba ni nini ambacho kinaendelea?

Mheshimiwa Naibu Spika, vifaa vya ujenzi kutoka nje au vyenye kutumia bidhaa nyingi kutoka nje vimepanda sana. Kwa mfano, tukichukua mabati ya kuezekea, bei yake imepanda kidogo. Kwa hiyo, hapa katika bajeti hii, ushauri ambao tunaoutoa ni kwamba tutumie vifaa vingi vyenye asili ya hapa nyumbani ili tuweze kupunguza utegemezi mkubwa kutoka nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano ambao nitautoa hapa ni huo huo wa mabati kwamba kwa miaka ya nyuma tumekuwa tukiona majengo mengi ya Serikali yalikuwa yakiezekwa kwa vigae na kwa kweli yamekuwa yakidumu kwa muda mrefu; na huko nyuma tulikuwa vilevile na viwanda vya vigae. Ukiangalia vigae hivi vinahitaji vitu viwili tu, udongo ambao ni mwingi sana tunao hapa nchini, na vilevile kama ni malighafi ya kuchomea, tukiokoa misitu yetu tunaweza tukatumia hata gesi ili tuweze kuchoma vigae tuvipate kwa bei nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tukipunguza utegemezi wa vifaa ambavyo vinatengenezwa nje na tukaongeza vifaa ambavyo vinatengenezwa ndani ya nchi tutakuwa tumemsaidia sana Mama katika bajeti yake hii ya wananchi kwani tutakuwa tumepunguza utegemezi kutoka nje na vilevile tutakuwa tumepunguza utegemezi wa dhana ya imported inflation kwani bidhaa nyingi kutoka nje zinakuwa na mfumuko wa bei ambao hauko ndani ya uwezo wetu katika udhibiti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili nitajielekeza kwa Wakandarasi. Tumekuwa na miradi mingi ambayo tunaitekeleza hapa nchini, lakini miradi hiyo mingi inatekelezwa na Wakandarasi kutoka nje. Hii inatokana na vigezo ambavyo vinawekwa katika tathmini kwamba uwezo, uzoefu na kadhalika; na katika hilo nashauri tuendelee kujenga uwezo wa makandarasi wetu wa ndani ili waweze kujenga hii miradi mikubwa. Tufanye juhudi za makusudi za kuwawezesha watendaji wa ndani hawa Wakandarasi ili waweze kutekeleza hii miradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mzuri ambao tunaipongeza Serikali kwa kuwa imefanya hilo, imeweza kuwakusanya Wakandarasi katika miradi minne ya majaribio ambayo imewajengea uwezo. Kuna daraja la Mbutu ambalo limejengwa na Wakandarasi wa ndani, wameungana Wakandarasi 10 ambao imewasaidia kujenga uwezo wa kutekeleza mradi mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna barabara ya Dumila - Kilosa ambayo hadi sasa hivi inajengwa na ina mkusanyiko wa Makandarasi 10 ambao nao vilevile tunawajengea uwezo wa kujenga barabara hizo. Barabara ya Urambo - Kaliuwa nayo imejengwa na Wakandarasi wa ndani lakini kwa mkusanyiko huo huo wa kuwajengea uwezo; na vilevile kuna barabara ya Makutano - Sanzate.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa utaona kwamba tukiziendelea juhudi hizi ambazo tunawapa uwezo Wakandarasi wa ndani kuweza kujenga miradi mikubwa, tutapunguza sana gharama za matumizi au utegemezi wa makapuni ya nje ambayo yana bei kubwa, na hiyo itatusaidia kabisa katika kutekeleza bajeti hii ya wananchi ambayo Mama yetu mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ametuletea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda kumshauri Waziri wa Fedha na Mipango kwamba Sheria ya Ununuzi iko Wizarani kwake. Kwa hiyo, anaweza kabisa kufanya juhudi za makusudi za kuweza kulirekebisha hili au kujenga uwezo wa Makandarasi wetu kwa kuwatengea miradi ya mifano au miradi ya kuweza kuwajengea uwezo ili waweze kuendelea na kuhakikisha kwamba katika miradi mikubwa inayofuata au inayokuja tuwe na ushiriki mkubwa zaidi wa Wakandarasi wetu wa ndani ili bei iweze kupungua na vilevile na fedha nyingi zaidi iweze kubaki hapa kwetu nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa tatu, napenda kuelekeza katika matokeo ya ujenzi huu ambao unafanywa. Mama yetu ametoa fedha nyingi sana kwa ajili ya ujenzi wa miradi mingi; zahanati, hospitali, barabara, na kadhalika. Sasa tunajiuliza; je, katika fedha hizo ambazo zimetengwa, miradi hiyo uhai wake utakuwaje? Kwa hiyo, hapo tunatoa tena ushauri kwamba ili tuweze kuwa na matumizi mazuri zaidi ya fedha zetu na kuhakikisha kwamba fedha hii ambayo inatolewa na Mama inatupa value for money, basi tutumie vifaa bora ambavyo vitaakisi matokeo ya kudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hapa ndiyo kuna changamoto kwa sababu vifaa bora vinakuwa na bei kubwa kidogo kuliko vifaa duni, lakini ukiangalia uhai wa vile vifaa unakuta kwamba ni tofauti sana. Sasa katika bajeti yako tumeona kwamba Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG) ameongezewa bajeti na hii inampa uwezo wa kukagua zaidi, basi huyu CAG naye ajengewe uwezo wa kuhakikisha kwamba anapata uwezo wa kutathmini life cycle cost ya mradi mzima. Tusipotoshwe na bei ndogo ya mwanzo ambayo unakuta kwamba mradi huo ukikamilika unaweza kuwa una maisha mafupi zaidi kuliko kutumia vifaa bora zaidi ambavyo vitakuwa na maisha marefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ukikamilisha jengo lako ambalo litakaa miaka miwili halafu linakuwa limekwisha kwa gharama nafuu, lakini ukitumia vifaa bora ambavyo utaweza kupata jengo hilohilo kwa gharama kubwa kidogo lakini likakaa miaka mingi zaidi, utakuta kwamba ukifanya tathmini kwa life cycle cost utakuta ni kwamba ni bora utumie vifaa bora lakini upate kitu kizuri kitakachodumu miaka mingi kuliko kuwa unafanya marekebisho na matengenezo kila wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hili linahitaji tujengeane uwezo kidogo kwani inatia hamasa sana kuchukua vifaa vya bei nafuu ambavyo vina uhai mfupi, badala ya vifaa vya kudumu muda mrefu. Wote ni mashahidi kwamba katika majumba yetu huko unaweza ukanunua bomba la bei nafuu la Shilingi Elfu Tano, lakini kila baada ya miezi miwili au mitatu unalibadilisha, ukinunua bomba la 15,000 ungekuta bomba linakaa miaka mitatu, ukijumlilsha utaona kwamba ni heri ununue kile ambacho kinadumu kuliko kununua kile kitu ambacho ni rahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa Wizara hii kuleta bajeti ambayo imeakisi hayo matakwa na ninaunga mkono hoja. (Makofi)