Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Felista Deogratius Njau (13 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala Za Mikoa Na Serikali Za Mitaa
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Moja kwa moja niende kwa upande wa TAMISEMI katika kipengele hiki hiki cha TARURA. TARURA imekuwa kama kibogoyo asiyekuwa na meno, lakini analazimishwa kula mifupa. Nasema maneno haya kwa sababu TARURA hawana shida. TARURA siyo tatizo, tatizo ni bajeti wanayopewa. TARURA wapo tayari kabisa kufanya kazi, lakini fikiria bajeti nzima ya barabara, TARURA wanapewa asilimia 30 badala ya kupewa asilimia 40 mpaka 50. Mimi napendekeza TARURA waongezewe fedha kwa sababu wanachezea nafasi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilimsikia Mheshimiwa Waziri akisoma hapa, anasema TARURA kwenye kilometa za mraba, wako 144,000. Sijui kama ni kweli, lakini pia ina wingi sana wa barabara. Kwa hiyo, TARURA watengewe fedha za kutosha ili kilio hiki cha Watanzania basi waweze kufutwa machozi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakwenda Dar es Salaam katika jiji ambalo ni kubwa, ambalo ni kitovu cha biashara na ni muunganiko wa Mikoa yote ya Tanzania. Dar es Salaam kumekuwa na msiba na kilio katika majimbo yote ya huko kuhusiana na barabara hasa zile za mitaa na barabara kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, barabara za Dar es Salaam nyingi ambazo hazipitiki ni suluhisho la foleni za Mkoa wa Dar es Salaam. Kwa mfano, Barabara inayotokea Kairuki kupitia Mikocheni, barabara ile inayopitia shoppers ilikuwa suluhisho kabisa la foleni za Dar es Salaam. Mtu anayesafiri Dar es Salaam kutoka Bunju kuelekea Posta ambapo ndipo kwenye Ofisi za Serikali, anachukua masaa matatu kama anatoka hapa kwenda Morogoro.

Mheshimiwa Spika, mtu huyu anafika ofisini anasinzia, akili imechoka, uwezo wake wa kufikiri umeshapotea. Tunaanza kusema watu wetu hawa-perform vizuri, hawa- perform kwa sababu hawapo active, wakifika pale kama mtu ametoka kulala kwenye msiba. Barabara nyingi ni kilio. Kuna barabara moja ipo Ununio; mwaka 2020, baada ya mvua hizi kunyesha nyumba 10, yaani familia 10 zilihama kabisa zikaondoka wakaenda TARURA wakaambiwa chimbeni mfereji. Hakuna miundombinu pale ya mfereji kuelekeza maji baharini. Wale watu wanapeleka wapi haya maji? Familia 10 zipo juu ya nyumba. Sasa hivi wanapiga simu wanasema Mheshimiwa Njau, tunaondoka sasa, wananiaga niwapeleke wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme kitu kimoja. Barabara ni kwikwi Tanzania nzima. Nikisema za vijijini, Mikoa inayohusiana na Kilimo, inayohusiana na biashara na mazao, hakika tunadumaza pato la Taifa. Kwa sababu kama vijijini barabara ni mbovu, hawawezi kwenda kwenye Wilaya, hawawezi kwenda kwenye Mikoa kupeleka mazao yao, tunasema hatupati mapato. Barabara ni suluhisho la biashara na barabara ni suluhisho la kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wengi wanaosimama hapa wanalia juu ya bajeti sehemu fulani. Twende tukatoe mzizi wa fitina kwenye miundombinu. Tukitoa hapa kwenye barabara, tunaweza kwenda vizuri. Pia niseme, hata wakijenga barabara hizi, kama Serikali hatujaweka nguvu kubwa katika kujenga mifereji, ni kazi bure. Barabara zinachongwa leo, baada ya siku tatu maji yanajaa na barabara zinakuwa vile vile. Kwa hiyo, lazima tuweke miundombinu ya mifereji. Kwa mfano, pale Mikocheni Shoppers, kuna adha ya mafuriko; pale ni mifereji tu ndiyo mchawi.

Mheshimiwa Spika, ikipatikana mifereji thabiti, barabara zikajengwa vizuri, barabara hizi zitakuwa imara. Barabara zinaharibika kwa sababu hakuna mifereji. Tuna wataalam wetu, wakandarasi; kuna msiba na kilio cha Makandarasi. Kwenye ripoti ya CAG ameainisha zaidi ya shilingi bilioni 81.52 hazijalipwa kwa Makandarasi, tunategemea kupata matokeo chanya kwa mtu ambaye anakudai na unampa kazi mpya! Hatuwezi kupata matokeo chanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukalipe madeni haya ya Makandarasi ili tuweze kuanza nao vizuri na kumaliza vizuri. TARURA hawa hawa ambao wanatengewa asilimia 30, wanaidai Serikali shilingi 125,854,000/=. Hivi kweli hawa ambao fedha zao hazitoshi, bado wanadai; tukawalipe TARURA Ninaongea haya kwa sababu tuna barabara za kimkakati; wakati tunatenga bajeti, hebu tuweke kipaumbele kwenye barabara za kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Kawe tuna barabara inatoka Mabwepande kuelekea Kibamba - Mbezi, ile barabara ni ya kimkakati kabisa kwenda kupunguza foleni, lakini barabara ile imekaa kama haina mwenyewe. Kuna barabara zimejengwa nusu; barabara ya Shoppers imejengwa kwa lami nusu, mwaka wa nne leo watu wanachungulia na kurudi, iko nusu. Twendeni tukamalize miradi baada ya kuianza, ndipo tuweke miradi mipya.

Mheshimiwa Spika, nashauri wakati tunaanza kupanga bajeti, tuangalie miaka ya nyuma: Je, tulikuwa tuna kiporo? Siyo kila siku tunaibua miradi mipya wakati ya zamani imesimama. Tutakuwa kila siku tunaelemewa na tunaonekana hatufanyi kazi, lakini watu wanachapa kazi.

Mheshimiwa Spika, ninakwenda kwenye ulipwaji wa motisha na madeni. Viongozi kama alivyosema msemaji aliyepita, Madiwani hawana thamani. Kwa sababu hawa ndio wanaosimamia mapato yetu, twendeni tukawape motisha, tusimame nao, tuwasemee. Madiwani ukikaa nao anakwambia posho yangu; ananung’unik! Tunakutana na Madiwani, anasubiri apate huruma ya Mkurugenzi wakati yeye ndiye anatakiwa kumwajibisha Mkurugenzi. Hatuwezi kufika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, twende tukapange upya. Nina imani na Serikali hii, sasa nina imani Mheshimiwa Mama Samia amesimama na viongozi wake, siwezi kuwakosoa kwa sababu ndiyo wameanza, nawaona wanaweza kufanya mabadiliko makubwa na nchi hii ikaenda kuona maisha mengine tofauti.

Mheshimiwa Spika, nasemea Jiji la Dar es Salaam kwa sababu mwisho wa siku Jiji la Dar es Salaam ndiyo jiji ambalo limekusanya mapato ya ndani makubwa kwa asilimia 104, limevuka asilimia 100. Kama Jiji hili ndivyo lilivyo, basi turudishe mapato kule chini, kwa maana ya miundimbinu. Miundombinu ikipatikana, wafanyabiashara watafanya biashara zao na wafanyakazi watafanya kazi vizuri wala hutasikia minong’ono.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ninakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na nakushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu ambayo kimsingi inagusa jamii kubwa ya Watanzania.

Kwanza kabisa kabla ya kwenda mbele ni lazima tuangalie huku nyuma tulifanya vizuri kiasi gani au vibaya kiasi gani ili tuweze kujisahihisha. Nikisema hivyo ninakwenda moja kwa moja kwenye mpango wa utekelezaji wa bajeti wa miaka ya fedha ya mwaka 2016/2017 ambayo bajeti ya Wizara hii ilikuwa ni asilimia 44; mwaka 2017/2018 ilikuwa ni asilimia 9.51 mwaka 2018/2019 ilikuwa ni asilimia 6.5; ukijumlisha kwa wastani wake miaka hii minne mfululizo unakuja kupata asilimia 20 tu ya bajeti katika sekta muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwendaje mbele katika kauli hii ya nchi ya viwanda huku tukiweka asilimia 20 miaka minne mfululizo. Hatuwezi kwenda kwa sababu mwisho wa siku mipango hii ni lazima itekelezwe, pesa ni lazima ziwepo ili maendeleo yawepo. Kwa tathmini hii ya mpango target yetu ni nini? Mpango wa Pili tulikwama wapi leo tunakwendaje mbele? N lazima tu-refer tulikotoka ili tuangalie tulikwama wapi twenda mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema haya kwa sababu hapo nyuma wakati wa kauli mbiu ya nchi yetu ya viwanda ilivyopamba moto, kuna Waziri alisimama kwenye matamko yake akasema tutakwenda kujenga viwanda 100 kila mkoa; alikuwa ni Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Jafo, akasema tutakwenda kujenga viwanda, hizi kauli hizi zisiwe mapambio zikawaponza Watanzania wakatuona huku tunapiga mapambio tu, haiwezekani. Hizi kauli ziende na vitendo, na alivyosema hivi nilikumbuka Kiwanda cha Tanganyika Packers nikasema kiwanda hiki kikifufuliwa wananchi wa Jimbo la Kawe na Dar es Salaam wanakwenda kupata ajira nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikasema kiwanda hiki kimebeba jina la Kawe maana ya Kawe ni njia ya kupita ngo’mbe (cow way) ni Kawe nikasema kiwanda hiki kikifufuliwa tutakwenda kupata ajira nyingi kwa sababu viwanda vingi vimekufa. Siweze kurejea haya kwa sababu viongozi na Wabunge wengi wameongea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawezaje kufikia malengo wakati sekta ya kilimo tumeiacha nyuma, hawa ni mapacha ni lazima tuangalie kilimo tunatengaje bajeti yake inatekelezwa vipi hili twende mbele kwa sababu kama hatuna raw material hatuwezi kwenda na viwanda. Na ukiangalia kwa miaka mitano mfulululizo sekta ya kilimo wametengewa asilimia 17 tu; tunakwendaje kwa namna hiyo? Hatuwezi kwenda kwa sababu hawa ni mapacha bila raw materials viwanda haviwezi kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikisema hayo najielekeza kwenye nafasi yetu ya kidunia ambayo wengi wameiongelea ya 141 kati ya nchi 190; tunakwenda hivyo tulikuwa tumejiwekea malengo kama Tanzania twende kwenye double digit position, hatuwezi kwenda kama malengo yetu hatuwezi kuyatekeleza vizuri wakati tunapanga. Nikisema hayo ninaangalia mazingra ya biashara na viwanda kwa Tanzania ni rafiki? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekwama kwa sababu mazingira si rafiki, Tanzania kuna utitiri mkubwa wa kodi, ukileta uwekezaji anaaanza kujiuliza wazawa wameshindwa kuwekeza kwa sababu ya utitiri wa kodi. Nikianza kutaja hatutamaliza, ukitaka kufungua kiwanda au kuanzisha biashara ni lazima uende ukasajili BRELA kule ni pesa, ni lazima ulipe kodi ya zuio, hiyo ni pesa; ni lazima ulipe kadiri unavyopata hiyo ni pesa; ni lazima ulipe gharama za OSHA hiyo ni pesa; ni lazima ulipe kodi ya ujuzi hiyo ni pesa; bado Manispaa wanakusubiri ulipe leseni hiyo ni pesa; gharama za Zimamoto, ada za Mamlaka ya Chakula; hiyo ni pesa na gharama lukuki ambazo ziko hapa. Mlundikano huu wa kodi, mwananchi wa kawaida mwenye mtaji wa kawaida hawezi kuwekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda namna hiyo Mheshimiwa Waziri nikuombe wakati unakuja na mkakati wako, una-wind up hapa, utueleze ni mkakati gani ulionao ili kuwezesha Watanzania waweze kuwekeza. Tusiimbe tu nchi ya viwanda kwa mdomo, tukatekeleze kwa vitendo kwa sababu…

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mzungumzaji anayezungumza anasema kwamba Serikali haijajenga viwanda kwa maana kauli ilipamba tu moto, lakini viwanda vingi havijaanzishwa. Nataka nimpe taarifa kwamba kutokana na Tanzania National Business Portal, ripoti inayozungumzia kwamba toka Awamu ya Tano ilipoingia madarakani, viwanda 4,877 vimejengwa. Kati ya viwanda hivyo, viwanda 201 ni viwanda vikubwa, viwanda 460 ni viwanda vidogo, viwanda 3,406 na viwanda 4,401 ni viwanda vidogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimpe taarifa kwamba Serikali ya Awamu ya Tano na Awamu ya Sita imefanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba mazingira ya viwanda yanakuepo na viwanda vingi vimeshajengwa nchini. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Felista unaipokea taarifa hiyo?

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, sipokei taarifa hiyo kwa sababu sizungumzii viwanda vinavyofichwa chumbani, nazungumzia viwanda vyenye tija kwa wananchi, nazungumzia viwanda ambavyo vilikuwepo na hatujaviona. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Felista, viwanda vipi vinafichwa chumbani? Naomba uondoe hilo neno.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema huwezi kuwa na blender useme una kiwanda; huwezi kuwa na cherehani moja unaajiri watu wangapi?

MWENYEKITI: Basi tumia lugha nyingine, lakini siyo ya chumbani.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, blender hata ndani si unajua. Kwa hiyo…

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Naomba nimpe Mheshimiwa dada yangu taarifa kwamba hivi tunavyozungumza bajeti iliyoko mezani kwake hapo zimeshatengwa shilingi bilioni 1.6 kwa ajili ya kufufua kiwanda kikubwa sana cha Kilimanjaro Machine Tools, kiwanda ambacho kilikufa miaka mingi, sasa kimeshatengewa hela. Kiwanda hiki kinatengeneza viwanda vingine vidogo vidogo, kazi yake ni kuunda vyuma na fedha imeshatengenezwa pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba kumpa taarifa kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inaendeleza kujenga viwanda vikubwa vikubwa kama hiki ambavyo havipatikani kwingine duniani. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Felista.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naona kaka yangu Mheshimiwa Mafuwe, alikuwa anataka kuchangia kwa sababu hayuko kwenye list. Mimi niendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba maneno haya siyasemi mimi; kupitia Ripoti ya CAG anasema kwamba kumekuwa na utekelezaji mdogo wa bajeti ya maendeleo kwa viwanda vidogo vidogo katika ngazi zote za Serikali; mfano, kwa miaka minne ya nyuma mfululizo, Wizara ya Viwanda na Biashara imetumia asilimia 16 tu ya fedha za maendeleo zilizopelekwa kwa ajili ya maendeleo ya viwanda vidogo vidogo. Maneno haya si ya kwangu, ni maneno ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali (CAG). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikisema hivyo ninasema tujielekeze kwenye ukweli, tunavyopanga hapa tuweke bajeti na ile bajeti iende na ikatekelezwe. Sisemi mapambio ya kuweza kumfurahisha mtu. Watanzania huko nje wanalia, akina mama huko nje wanalia kwa sababu hata akiwa na biashara yake ule utitiri wa kodi kwa miaka mitano iliyopita hii Watanzania wengi biashara zao zimefungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi mtakuwa ni mashahidi, hamuwezi kusema lakini mnajua kwenye majimbo yenu kilio cha Watanzania ni kikubwa kuliko tunavyofikiri. Twende tukarekebishe kwa sababu kazi ya Bunge ni kuielekeza Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda kuielekeza Serikali ikaangalie utitiri huu wa kodi, ipunguze ili wananchi wetu wapate nafuu na waweze kuwekeza. Nia yetu ni njema kwa sababu Tanzania yetu ni moja, tunahitaji maendeleo, hatuhitaji malumbano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hapa hatuhitaji ahadi, tunahitaji utekelezaji. Utekelezaji ni jambo la msingi kwa sababu baada ya kutoka hapa tutakuwa na dhambi ya kujibu kwa Mwenyezi Mungu. Wale watu wenye imani kila siku unamwambia mtoto wako utanyonya kesho kama mtoto wa kuku halafu mwisho wa siku Watanzania wanakosa imani na Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, twende tukatekeleze vile tulivyovipangilia ili tuweze kufikia azma ya Serikali ya viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema maneno hayo, ninakushukuru sana kwa nafasi hii. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa pumzi alizoweza kunipa siku ya leo lakini nami niweze kuchangia katika bajeti hii. Kwa leo, nishukuru kwa kidogo, wanasema usiposhukuru kwa kidogo hata kwa kikubwa huwezi kushukuru. Niweze kushukuru kwa mawazo haya yaliyochukuliwa kwa sababu nimekuwa ni mdau wa barabara nimekuwa nikichangia kwenye barabara katika TAMISEMI na Wizara ya Ujenzi nimejikita sana kwenye barabara. Kwa hiyo, nimeona hapa mrejesho uliokuja umekwenda kuleta suluhu kama tutakwenda ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilieleza jinsi Serikali inavyopoteza wawekezaji, nikaeleza jinsi inavyoweza kufikia kukosa pato la Taifa na pato la mtu mmoja mmoja kama hatutatengeneza miundombinu thabiti ya barabara. Lakini nikaeleza ni jinsi gani tutashindwa kwenda kufikia kauli mbiu ya Tanzania ya Viwanda kama hatutatengeneza miundombinu; nikaeleza ni jinsi gani hatutafanya kilimo chenye tija kama hatutatengeneza miundombinu ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyoongea hivi narejea kwenye hotuba ya bajeti kwenye ile para ya 39. Nimeona pale kwamba Serikali inakwenda kuomba mikopo ya bei nafuu kwenye Benki ya Dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imeainisha pale kiasi cha dola za Kimarekani milioni 120 imeelekezwa itakwenda Dar es Salaam. Ikaelekezwa kiasi cha dola za Kimarekani milioni 300 zitakwenda mikoani kwa lengo la kukuza uchumi. Lakini pale ikaelekezwa milioni 50 dola za Marekani Serikali itakwenda kuweka pale; lakini mwisho wa siku tunapata jumla ya dola za Kimarekani milioni 470. Tukienda kubadilisha kwa fedha zetu za Kitanzania kwa rate ya leo ni shilingi 2,300 tunapata trilioni 1.081. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukihama twende ile para ya 88 ambapo kuna tozo ya mafuta. Serikali inaendelea kutafuta fedha mbadala ili tuweze kupata suluhu ya kero ya barabara. Kwenye tozo ya mafuta ya petrol na diesel tumesema pale kila lita moja itatozwa shilingi 100. Serikali ikadadavua ikapata 322,158,000.20, ukijumlisha unapata trilioni 1.403 fedha hizi ni nyingi sana na zote zinatakiwa zielekee TARURA ndio lengo la Serikali. Na ukiangalia asilimia ya barabara zetu za vumbi ni asilimia 72.4 Nchi nzima kwenye mtandao wa TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi ni nyingi naomba nishauri jambo. Kwa sababu fedha hizi ni nyingi na zikiwekezwa kweli kwenye TARURA zitaleta tija, ninaomba fedha hizi ziwekwe kwenye ring-fence ili zisitumike kwenye matumizi mengine lakini jinsi zilivyotengwa ziende eneo husika. Namba mbili, fedha hizi jinsi Mheshimiwa Waziri alikuja hapa akadadavua vizuri aje hapa wakati wa kuhitimisha fedha hizi zianishe barabara zinazokwenda kujengwa. Lakini pia zianishwe zinakwenda kujengwa kwa kiwango kipi cha lami, cha changarawe au kiwango kipi ili tuangalie thamani ya fedha zetu zinakwenda kufanya nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikifanya hivyo ninarejea pale ambapo Serikali iliona inakwenda kukuza fursa ya kiuchumi ndio maana fedha hizi zikaelekezwa zile dola milioni 300 zikaenda mikoani. Kuna mfano wa barabara ambazo ni kwikwi tutakuwa tunaimba mapambio hapa kila siku kama hatutekelezi wajibu wetu na kutenda kile ambacho tunachokisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo barabara za mikoani ambayo mikoa inalima, inalima mazao ya biashara, inalima mazao ya mbogamboga, kwa mfano; kama Morogoro kuna barabara ile ya Bigwa – Kisaki ile barabara ni kwikwi lakini wakulima walioko kule ni wengi na barabara ile ikijengwa inaweza kuleta tija ni kwa Mheshimiwa Babu Tale. Lakini ipo barabara ile ya Iringa ambayo inapita Lujewa, Madibila mpaka Mafinga ile barabara ni ya kibiashara kule wapo wakulima, wapo watu ambao wako pale wanalima mahindi ikitengenezwa vizuri inaweza kuimarisha pato la mtu mmoja mmoja lakini kuimarisha pato letu la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipo barabara ya Njombe – Kibena kuelekea Lupembe mpaka Madeke kule kuna wakulima wa parachichi. Tunaachaje kutengeneza barabara hizi za kimkakati. Kama lengo letu ni kukuza fursa za kiuchumi na kibiashara twende tukaangalie hizi barabara za kimkakati. (Makofi)

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, TAARIFA.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kumpa taarifa Mheshimiwa mzungumzaji anayezungumza hivi sasa kwamba barabara ile ya Kibena stop Lupembe, Madeke barabara ambayo inaunganisha mkoa na mkoa. Kweli kuna umuhimu sana wa barabara hizi kujengwa kwa kiwango cha lami na Serikali ipo hatua nzuri ya kutengeneza barabara hizi kwa kiwango cha lami. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa taarifa hiyo.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, napokea taarifa hii kwa sababu ni kati ya wadau ambao wanalalamika juu ya barabara hizo. Niendelee, naendelea kuainisha barabara za kimkakati kwenye mkoa ule wa Kagera kuna barabara ya Mulushaka, Ukwenda, Mrongo, barabara hii inaelekea mpaka mpakani mwa Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naongea haya sehemu hizo tumefika sisi wanasiasa tumetembea mtaa kwa mtaa, mkoa kwa mkoa, kwa hiyo tunafahamu kero za nchi hii. Barabara hii ukifika kule mpakani kuna wakulima wa ndizi, kuna wakulima wa kahawa, barabara hii ikitengenezwa tunakwenda kukuza pato la Taifa lakini pato la mtu mmoja mmoja ambayo ndio dhamira yetu ambayo Wabunge tuko hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema pia bajeti hii iainishe madaraja. Kuna madaraja ambayo ni sugu watu wanaongea huku kipindi hicho cha bajeti ya Wizara ya Ujenzi na TAMISEMI watu wengi wanaongea juu ya madaraja, vilio kwa kina mama wajawazito wanajifungulia barabarani. Tuainishiwe na madaraja haya ili tuweze kujua fedha zetu inakwenda kutumika vipi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sasa naelekea Dar es Salaam. Katika Mkoa wangu wa Dar es Salaam, Dar es Salaam ni mkoa wa kimkakati na ni mkoa wa biashara na ni kitovu cha biashara Nchi nzima. Dar es Salaam huwezi kusikia mtu anasimama hapa anaomba viatilifu, anaomba mbolea, anaomba pembejeo. Dar es Salaam tunaomba miundombinu thabiti. Tunaomba miundombinu kwa sababu mpaka Dar es Salaam inaibuka katika Majiji yote kwamba ndio Jiji ambalo linakusanya ushuru mwingi kila siku na kimkoa inashika namba moja ni kwa sababu Dar es Salaam ndio mkoa wa biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dar es Salaam kuna tatizo la miundombinu, nikipita kwako kwenye mitaa ile ya Ilala, ninaona barabara za mitaa bado haziko sawa. Pia maji taka Dar es Salaam ni asilimia 14 tu tumeunganishwa katika mfumo wa maji taka, asilimia 86 ule mfumo wa maji taka umeingiliana na maji masafi huko huko tunakutana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna tatizo la mlipuko wa magonjwa ya kipindupindu na magonjwa ya homa ya matumbo. Kila mwaka kipindupindu kinaazia Dar es Salaam, siyo kwa sababu nyingine bali ni mfumo wa maji taka ambayo siyo rafiki. Niombe wakati Waziri anakuja, aje na utaratibu mzuri kwa jinsi gani maji taka yataelekezwa baharini au sehemu nyingine kuliko ilivyo hivi sasa. Dar es Salaam mvua ikinyesha ndiyo wakati wa wananchi wa kupumua na kuanza kucheulisha vyoo vyao na yale mambo yanatapaa barabarani, kwa hiyo siyo salama sana. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kwa sababu Dar es Salaam ndio Jiji la kimkakati, wawekezaji wanapokuja kitu cha kwanza wanaangalia miundombinu, kama miundombinu siyo rafiki wawekezaji wanatukimbia. Na Dar es Salaam ndipo wawekezaji wanaanza kushukia pale, kwa hiyo wanaangalia mandhari, pia wafanyakazi wa Dar es Salaam ni uchovu kwa sababu mvua ikinyesha inakuwa ni jam kunakuwa na foleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe wakati Mheshimiwa Waziri unakuja kuhitimisha, uje na mkakati wa miferiji Dar es Salaam, mifereji ambayo inasababisha barabara zetu za lami zinakatika, hakuna miundombinu thabiti ya mifereji, mvua ikinyesha mafuriko watu hawapiti mijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami nichangie kwenye wizara hii muhimu. Ninapozungumzia kwenye ujenzi na uchukuzi moja kwa moja tunaelekeza kwenye mambo ya miundombinu kama barabara, reli na vitu vinginevyo. Katika sekta hii, imeonesha kukua mfululizo ndani ya miaka minne, imekuwa ikikuwa kwa asilimia 14.4 tangu 2016/2017, 2020/2021. Hii sekta inakua bila kigugumizi pamoja na janga la corona lakini imeiongezea Nchi pato la Taifa asilimia 14.8. Hii ni sekta ya pili kwa kuongezea Nchi pato la Taifa ukitoka kilimo lakini kwa kukua imeibuka kinara sekta hii ni muhimu inahitaji jicho la tatu kwa mustakabali wa Taifa na maendeleo ya mwananchi mmoja mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaposema hivi ninaona kuna changamoto chache ambazo tunaweza tukizimaliza hii sekta inayoenda kukua na kuwa kinara na pato la Taifa litakuwa zaidi na mwananchi mmoja mmoja ataweza kumiliki uchumi. Nikisema hivyo, ninaweza kusema wakandarasi walioingia mkataba, wakandarasi waliosajiriwa kwenye nchi yetu asilimia 10 tu ndio wageni kwa nchi za nje, asilimia 10. Asilimia nyingine ni wazawa lakini ukifanya upembuzi pale unakuta asilimia 60 ya miradi mikubwa inashikiliwa na asilimia 10 ya wakandarasi wageni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunashindwa kuwa wazalendo kwasababu Wakandarasi wetu hawakidhi vigezo, kigezo cha kwanza hawana mitaji, hawana mitaji mizuri kwahiyo hawawezi ku-afford kuweza kushika hii miradi mikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine hawana ujuzi wa kutosha, hawana ujuzi wa kutosha kwa hiyo mwisho wa siku tunatakiwa tukae chini tuweze kuwawezesha wakandarasi wetu wawe na ujuzi wa kutosha ili kuweza ku- afford ushindani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ni vifaa vya ujenzi havikai kwenye level moja bei zake zinapanda na kushuka na sometimes hazipo kabisa. Kwa hiyo, mwisho wa siku hawa wataalam wetu wanashindwa kwenda kwenye ushindani wa wakandarasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapoongea haya ninasema kwasababu Wakandarasi wetu wakiweza kushika hizi tenda uchumi wa mtu mmoja mmoja ndani ya nchi yetu utakua, lakini pato la Taifa litaongeza kwa sababu watu wetu watakkuwa na fedha mfukoni. Niishauri Serikali katika hili, tunavyoona namna hii tuweze kuwawezesha Wakandarasi wetu waweze kumiliki hii miradi mikubwa ili tuweze kuona matunda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ninapotoka mahali hapo, ninaona kabisa barabara nyingi, vilio vingi vya Wabunge humu ndani wanalia juu ya barabara, hawatoki kwenye reli wanaingia kwenye reli ya barabara kwa sababu ndio kero inayomgusa mwananchi wa kawaida kule chini vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara zinazounganisha mikoa kwa mfano barabara zinazounganisha mikoa kuja Dar es Salaam, barabara hizi ni mbovu za mikoa ya kimkakati mikoa ya kilimo. Mikoa ya Njombe, ya Iringa, Mikoa ya Singida barabara hii si salama kwa hiyo wananchi wa kawaida hawawezi kuleta mazao yao Dar es Salaam. Wakifika Dar es Salaam wanakutana na adha nyingine ya mafuriko, Dar es Salaam miundombinu ya mafuriko hakuna mifereji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wanatengeneza mkakati huo wa barabara waangalie mifereji kwasababu maji haya ya mifereji yamekuwa ndio chanzo cha kukata barabara katika Mkoa wa Dar es Salaam. Lakini mafuriko ukifika Jangwani eneo lile la mkutano kuelekea Kariakoo pale hapapitiki wakati wa mvua ni kwa sababu hakuna miundombinu ya mifereji ambayo ni imara. Ukija barabara ya Tegeta kuelekea Bunju, Boko, Basihaya mifereji hakuna barabara zimejengwa zipo vizuri lakini unakuta magari yame- stuck hayawezi kutembea kwa sababu maji yanajaa barabarani, barabara zinakatika kuisababishia Serikali kupata hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuone namna gani bora wakati tunapokwenda kuweka miundombinu ya barabara tuona namna bora ya kutengeneza mifereji. Jiji la Dar es Salaam halina miundombinu rafiki, ukiangalia Jiji la Dar es Salaam watu wanasema kuna lami lakini ni asilimia 14 tu ya Jiji la Dar es Salaam wananchi wake wameunganishwa kwenye maji machafu, maji taka asilimia 14. Asilimia nyingine tunachanganyika na maji hayo hayo tunakunywa, magonjwa ya mlipuko Dar es Salaam, wanaotoka mikoani wanakutana nayo, basi ni vurugu tupu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali, wanajua Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri mnajua, miundombinu ya Dar es Salaam si rafiki kila siku watu wanaugua vipindupindu, wanaugua UTI, wanaugua magonjwa kadha wa kadha kwasababu tu ya miundombinu, lakini sio adha nyingine. Niombe kwa sababu ni kitovu cha biashara, twende tukaitengeneze Dar es Salaam na mikoa yake inayounganishwa kuja Dar es Salaam ili tuweze kuimarisha uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyoongea hapa kuna wananchi wangu wa Ununio hawana pa kukaa, barabara hazina mifereji, watu wapo pembezoni wamekaa wametulia hawana pa kwenda mbele wala kurudi nyuma, nyuma zinaelea. Ni Dar es Salaam hapo sio mikoani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikiangalia kiini naona ni mitaro niiombe Serikali chonde chonde kipindi kilichopita niliongelea juu ya mitaro pale Nyamachabisi alikuja waziri kipindi kile nafikiri waziri wangu anafahamu. Alikuja kipindi kile Nyamachabisi miundombinu ya mitaro hakuna watu wanaelea. Niombe, niombe Serikali hii ya Mama Samia Suluhu Serikali Sikivu na Mawaziri wake waweze kuweka mikakati mizuri ili wananchi waweze kufanya biashara zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyoongelea miundombinu, ninaongelea viwanda huwezi kuwa na viwanda imara kama huna miundombinu. Ninavyoongelea mbiundombinu ninaongelea kilimo, huwezi kuuza mazao yako ya kilimo kama huna miundombinu. ninapoongelea hiyo miundombinu naongelea uwekezaji, wawekezaji wanaanglia miundombinu ndio wanakuja kwenye nchi yetu. Naomba kuwasilisha, ahsante sana. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye amenisaidia kufika mahali hapa hii leo. Naishukuru pia familia yangu ambayo kimsingi imekuwa nyuma yangu kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakwenda moja kwa moja kwenye hotuba ya Rais ambayo imeeleza kwenye ile page ya 21 namna gani wanawake na vijanawanakwenda kupata mikopo ya asilimia 10. Nimesema kuhusiana na hili linatakiwa jicho la tatu kwa sababu wanawake wengi ndiyo wanaoonekana kwenda mbele kwenye hii mikopo na wanawake hawa wamepata changamoto lukuki. Changamoto hizi hazitatuliwi kwa muda mrefu, kwa sababu wanawake hawa wanaenda kupewa vigezo ambavyo haviko kwenye utaratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza wanadaiwa kadi za Chama Cha Mapinduzi, kama hauna kadi ya Chama Cha Mapinduzi hupati mkopo. Lakini wanawake hawa hawa baada ya kupata mikopo hawana mtu wa kuwafundisha ni namna gani watakwenda kufanya biashara kwa kiwango kidogo wanachopewa ili kuleta tija kwenye jamii. Kikubwa zaidi hawa wanawake wanaopata mikopo au wengine wanaokosa wanakimbilia kwenye microfinance...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Felister Njau, kuna Kanuni inavunjwa. Mheshimiws Jenista Mhagama Kanuni inayovunjwa.

KUHUSU UTARATIBU

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (SERA, BUNGE, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kwenye utaratibu. Kanuni ya 71 mambo yanayokatazwa Bungeni lakini 71(1) ambacho Mbunge haruhusiwi kusema taarifa ambazo hazina ukweli, lakini kiambatane na Kifungu cha 70(4) ambacho kinamtaka kuthibitisha ni kwa kiasi gani jambo linalosemwa kwamba si sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niliambie Bunge lako Tukufu, kwa mujibu wa miongozo tuliyojiwekea inayosimamia utoaji wa mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu katika halmashauri zetu, kigezo cha uanachama wa mwombaji wa mikopo hakipo na hakijawahi kutumika. Halmashauri zote zimekuwa zikitoa mikopo hiyo kwa uwiano ulio sahihi kabisa. Kinachozingatiwa ni taratibu zile za kimiongozo ambazo zinatakiwa kila mwombaji mkopo aweze kuzifuata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Bunge hili lisitumike kuzungumza mambo ambayo hayana uasili na uhalisia. Mara nyingi tumekuwa tukimsikia Mheshimiwa Rais akisema maendeleo ya taifa hili hayatazingatia chama, dini, ukabila wala jambo lolote ni maendeleo huru kwa Watanzania wote kwa mambo yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge alikuwa anachangia Mheshimiwa Felister Njau, ameeleza maelezo kuhusu mikopo inayotolewa na vigezo vinavyozingatiwa. Akasimama Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa mujibu wa Kanuni ya 71 na 70, ametoa maelezo ambayo sote tumeyasikia, sitayarejea lakini hoja ya msingi iliyotolewa hapo ni kwamba, Mheshimiwa Felister Njau wakati anachangia amezungumza taarifa kuhusu mikopo ambazo hazina ukweli kwa mujibu wa Mheshimiwa Jenista. Kanuni yetu ya 70 inatuongoza namna ya kwenda na jambo ambalo limezungumzwa hapa, lakini Mbunge ataamua sasa kusimama kama alivyofanya Mheshimiwa Jenista kuonesha kwamba jambo hilo linalosemwa halina ukweli na ametoa ufafanuzi kwa nini anasema halina ukweli.

Mheshimiwa Felista Njau, ili twende vizuri na kwa sababu sisi wengi hapa ndani ni wageni tutaelekezana tu vizuri hizi Kanuni taratibu, lakini Kanuni ya 70, Mheshimiwa Jenista ametumia fasili ya (4) na (7) inakupa fursa ya aidha kufuta kauli yako kama hilo jambo lililosemwa huna uthibitisho nalo, ama kama hutafuta hiyo kauli hapo nitatoa mimi maelekezo ya nini kifuate baada ya hapo.

Kwa hiyo, nakupa fursa kama huna uthibitisho ufute hiyo kauli, kama utakuwa hufuti kauli nitasimama tena kutoa maelekezo. Nakupa fursa ya kufuta kauli. (Makofi)

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Sifuti kauli kwa sababu nina uthibitisho na kimsingi nilikuwa nashauri kwa sababu watu wengi wanaweza wakatumia hiyo lakini ngazi za juu hawajui. Kwa hiyo, natoa ushauri mamlaka husika ifuatilie, hilo tu. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Sawa, sasa ukae Mheshimiwa Njau. Waheshimiwa Wabunge, naenda taratibu kwa sababu sisi wengi humu ndani ni wageni.

Mheshimiwa Felista Njau matakwa ya Kanuni ya 70, ukikataa kufuta kauli maana yake mimi naweza kukuelekeza uniletee ushahidi. Ushahidi utakaoniletea si wa maneno wa kuniambia kuna watu waliambiwa, hapana; utatakiwa ulete ushahidi wa kulithibitishia Bunge hili kwamba hicho ni kigezo cha mikopo mahali fulani na mahali fulani. Kwa hiyo, tuelewane vizuri Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Kwa hivyo, unavyopewa hii fursa ni fursa ya muhimu sana lakini kama unao uhakika Bunge hili kwa sasa hivi haliwezi kukulazimisha kufuta kauli kwa sababu, wewe umesema unao uthibitisho. Sasa kwa sababu ya ugeni nakupa tena fursa ya pili, kama unao uthibitisho nitatoa maelekezo. Karibu, sekunde 30, unao uthibitisho?

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kuondoa mlolongo nafuta lakini naomba… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Haya, kaa niiweke vizuri, kaa niiweke vizuri, eeh.

Waheshimiwa Wabunge, Kanuni zetu namna zinavyotutaka kuenenda niwashauri sana sote tuzipitie, Wabunge wageni lakini sisi sote kwa sababu hili ni Bunge jipya. Kanuni hizi ni toleo jipya kwa hiyo, ziko Kanuni ambazo zimebadilika hapa na pale niwasihi sana tukazipitie.

Masharti yaliyoko humu huwa yanafuatiliwa nukta kwa koma, kwa hivyo, ukifuta kauli unafuta bila masharti. Hakuna neno lakini ama nafanya hivi, aahh-aa, isipokuwa yale uliyokuwa unayasema maelezo yako ya pili, sasa hii natoa Mwongozo; ungeweza kusema naishauri Serikali wakati wa kutoa mikopo wajaribu kuangalia hiki na hiki na hiki, lakini ukionesha kwamba kuna shida mahali ni lazima hiyo shida iletewe uthibitisho.

Waheshimiwa Wabunge, kwa muktadha huu na ili tuweze kwenda mbele, Mheshimiwa Felister Njau amefuta kauli yake. Kwa muktadha huo Mwongozo wa Kiti kuhusu huo utaratibu aliokuwa ameomba Mheshimiwa Jenista Mhagama ni kwamba taarifa hiyo haitakuwepo kwenye Taarifa Rasmi za Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Njau endelea na mchango wako.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nakwenda kwenye kipengele kingine page number 72 ambapo kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Rais kumeeleza kulinda demokrasia, uhuru, haki za wananchi na vyombo vya Habari. Mpaka sasa navyoongea mimi nilikuwa meneja kampeni wa Jimbo la Kawe, Mheshimiwa Halima James mwana wa Mdee, haki, demokrasia, usawa havikulindwa na havikulindwa toka uchaguzi mdogo wa mwaka 2014 uliofutwa, 2019 uliofutwa, lakini 2020 kulikuwa kuna mambo ya ajabu. Mimi ni kati ya watu niliyekamata kura fake mabegi matano kwenye vyombo vingi, lakini nikasema kwa sababu tunakuja kwenye Bunge hili ni lazima tuseme ukweli, demokrasia tunayoiimba tuifuate kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mtu anajua kwenye Bunge hili amekuja vipi, ameshinda vipi, kwa njia zipi, lakini demokrasia ikaseme na mioyo yetu. Haki ya vyombo vya habari, kuna kipindi sisi tulikuwa tukisimama kwenye majukwaa mwandishi akaonekana amepiga picha, humuoni hata siku tatu, nne, ukimpigia simu anakimbia anasema nina kigugumizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme kama ni haki tunaitangaza, kama ni demokrasia tunaisema, tuiishi kwa vitendo kwa sababu hapa kila mtu ana imani yake. Kila mtu ana imani kwenye Bunge hili kwa hiyo, tuiishi kwa vitendo tusiimbe kwenye makaratasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa minajili hiyo kuna watu lukuki, kuna wananchi waliokamatwa kipindi cha uchaguzi…

KUHUSU UTARATIBU

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, Kuhusu Utaratibu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Gwajima, Kanuni inayovunjwa?

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama kwa Kanuni ya 71(1)(a). Inasema: “Mbunge hatatoa ndani ya Bunge taarifa ambazo hazina ukweli.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mbunge aliyekuwa anazungumza, bahati nzuri mimi ndiye Mbunge halali wa Jimbo la Kawe niliyeshinda kwa kura 194,000 dhidi ya mpinzani wangu aliyepata 30,000 peke yake. Naomba alithibitishie Bunge lako kwamba alikamata kura maboksi 50 kama alivyosema. (Makofi/kicheko)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, bahati nzuri hizi kanuni tutazifahamu tu, Bunge hili ni la miaka mitano, Mwenyezi Mungu atujalie uhai na uzima. Kanuni ya 71 inampa fursa Mbunge kusimama ukisoma fasili nyingine zinazofuata baada ya hapo na kusema kuhusu utaratibu, kwa maana ya fasili ya (2) inampa fursa Mbunge kusimama kusema Kuhusu Utaratibu ili kueleza mambo haya yasiyoruhusiwa Bungeni kwa lile ambalo linakuwa linazungumzwa.

Mheshimiwa Gwajima, Mbunge wa Kawe, amesimama kueleza kwamba taarifa zilizokuwa zinatolewa na Mheshimiwa Felista Njau za kuhusu vitu vilivyokamatwa huko Jimboni Kawe kipindi cha uchaguzi ama siku ya uchaguzi hazina ukweli. Sasa mimi siwezi kufahamu ukweli, anayeufahamu ni Mheshimiwa Felister Njau. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, kabla hamjapiga makofi, hili jengo letu hili kuna muda kuna maneno fulani hivi yanaweza kusemwa pamoja na mambo mengine kwamba hili jumba ni jumba la kisiasa, lakini hili ni jumba ambalo ndiyo maana wanasema Mheshimiwa Spika Bunge lako Tukufu. Haiyumkiniki kwamba mtu anayesimama kuchangia humu ndani atazungumza mambo ambayo yanazungumzwa bila ushahidi, bila uhakika kwa sababu kila mmoja wetu anaitwa Mheshimiwa kwa maana ya ni kiongozi anaweza kusimamia kile anachokisema, anaweza kuthibitisha kile anachokisema.

Mheshimiwa Felister Njau huu ni utaratibu wa pili kwamba Kanuni inavunjwa. Humu ndani huwa ni kawaida watu wanaweza kusimama hata mara nyingi, lakini tazama michango yako isikupeleke mahali ambapo kuna Kanuni humu ndani zinakupeleka nje ya hili Bunge. Isitokee kwamba kila unachokisema tutafika mahali pa kwenda hapo, siyo kwa maana ya utoke nje, aah-aa, kwa maana ya uende huko Kamati ikajiridhishe, ulete huo ushahidi na mambo kama hayo. (Makofi)

Kwa hivyo, kwa muktadha wa Kanuni hizi kwa sababu, sasa husemi ukweli maana yake unarudi tena kwenye 70. Kama unao uthibitisho utasema hivyo, mimi nitaagiza utoe huo uthibitisho. Kama huna uthibitisho futa kauli yako kwa mujibu wa Kanuni ya 70 kama nilivyokusomea Fasili ya (7).

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Uthibitisho ninao na nikiambiwa nilete nitaleta uthibitisho. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, Kanuni hii ya 70 inakataza Mbunge kusema uwongo…

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Tusikilizane Waheshimiwa Wabunge, tusikilizane. Kanuni ya 70 inakataza kusema uongo Bungeni na fasili ya (4) ya (5) na ya (6) ukizisoma zote kwa pamoja utapata picha kwamba Kiti kitaagiza Mbunge ambaye amekataa kufuta kauli kuleta ushahidi kwa kiwango cha kuliridhisha Bunge na siyo kumridhisha mtu mmoja.

Kwa muktadha huo fasili ya (6) inanitaka mimi nitoe muda wa kufanya hivyo. Mimi sitataka nimwambie alete ushahidi hapa kwa sababu naweza kumwambia alete sasa hivi ama alete baadae, kwa sababu alikamata maboksi na mabegi hataweza kuwa nayo humu ndani maana yatakuwa hayakupita pale nje kuingia humu ndani. Kwa muktadha huo, hayo mabegi, hayo masanduku yaliyokamatwa naiagiza Kamati yetu ya Maadili, itamsikiliza yeye halafu mimi nitaletewa huo ushahidi. (Makofi)

Kwa hiyo, Mheshimiwa Njau utapeleka ushahidi wako kwenye hiyo Kamati yetu. Muda ninaoutoa kwa sababu leo ni siku ya Jumatano ndiyo kwanza tumeanza Bunge jana, kufikia Jumatano ijayo huo ushahidi uwe umeshauleta na Kamati yetu ya Maadili ikae wakati huo na kabla Bunge hili halijaisha tutatoa maamuzi kuhusu jambo hilo. (Makofi)

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba dakika zangu zilindwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo niombe mamlaka ambayo inaweza kushughulika, kuna vijana wengi katika kanda mbalimbali na mikoa wako ndani kwa kesi za kisiasa za uchaguzi na zinapigwa tarehe, ushahidi unakosekana. Katika kanda mbalimbali, Kanda ya Kusini 34, Kanda ya Nyasa 36, Viktoria 16, Serengeti 34, Pwani nane, wale vijana ni wa CCM na CHADEMA. Kwa hiyo, naomba mamlaka husika iwaondoe vijana hawa ndani kwa sababu shughuli au mtanange umekwisha. (Kicheko)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Njau, hao washauri wako wa hapo karibu wanatakiwa wakushauri mambo mengi sana ikiwa ni pamoja na mambo yaliyoko mahakamani. Mambo yaliyoko mahakamani hayatolewi maamuzi hapa ndani.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, sorry, wako mahabusu.

NAIBU SPIKA: Mambo yaliyoko mahakamani hayatolewi maamuzi hapa ndani. Mheshimiwa Esther Matiko na Ester Bulaya msimpoteze Mheshimiwa Felister Njau.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Njau malizia mchango wako.

MHE. ESTHER N. MATIKO: No, please, sasa mimi umeniingizaje hapo, I did not say anything.

MHE. ESTER A. BULAYA: Sijawasha microphone hapa, kichwa yake yeye mwenyewe iko vizuri.

MHE. FELISTER D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, samahani…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Esther Matiko na Ester Bulaya, muacheni mchangiaji amalize mchango wake. Muacheni mchangiaji amalize mchango wake, Mheshimiwa Felista Njau.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

T A A R I F A

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa, niko huku.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunti.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru. Naomba tu nimpe Taarifa mchangiaji Mheshimiwa Njau kwamba watu anaowazungumzia ni pamoja na wakazi wa Wilaya ya Mpwapwa ambao wako 18 walikamatwa, kesi haijaenda mahakamani…

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, tusikilizane vizuri. Bunge hili siyo kazi yake kuingilia michakato ya taasisi zilizoko huko nje, labda kama hapa mbele kuna hoja hiyo, tuelewane vizuri na ninyi mnazifahamu kanuni, tuelewane vizuri. Mheshimiwa Njau malizia mchango wako. (Makofi)

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nishukuru lakini niombe, wako Mawaziri wenye mamlaka hayo wasimame kidete kwa ajili ya kutetea haki za raia na tusiende kwa sababu ya itikadi au chochote. Nakushukuru sana. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nakushukuru kwa ajili ya kunipa nafasi hii. Pia nitoe pole kwa Watanzania wote kwa msiba mkubwa uliotufika. Kimsingi nimesimama mbele yako niweze kuchangia kidogo, lakini niweke msisitizo; naingia moja kwa moja kwenye Sekta ya Kilimo. Natamani kila mtu akisimama aweze kuona upana na ukubwa wa sekta hii ili tuweze kuweka nguvu inayohusika katika sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme sekta ya kilimo inaweza kuchukua asilimia 56.5 ya ajira zote za Watanzania. Nikienda kwenye asilimia; nakwenda kwenye asilimia 20 ya mauzo yote ya nje. Unaona hapa kidogo kuna ufinyu, kwa sababu sekta hii haijachukuliwa kwa uzito wake. Ikichukuliwa kwa uzito wake, hatutalia ajali za boda boda barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wenzetu wa Nairobi wameweza kutenga SACCOSS maalum, wakakusanya vijana katika makundi na wanatengeneza mfumo wa kununua daladala kule wanaziita matatuu ili waweze kuwekeza. Sisi tuna ardhi kubwa ambayo ina rutuba, tuna maji. Kwa mfumo wa umwagiliaji, kama hatuna ile miundombinu, lakini tuangalie hizi mvua zinazonyesha, tunalia mafuriko; haya maji yanayotokana na mvua tungeweza kuweka pale miundombinu ya umwagiliaji tukavuna yale maji yakatusaidia kwenye kumwagilia, tusingelia leo mambo ya mafuta, tungewekeza kwenye alizeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kikubwa hawa vijana wanaokufa kwa boda boda hawajapata Plan B za ajira. Wakipata Plan B hatutalia vifo hivi, kwa sababu kila kijana anafikiria ajira ni boda boda. Pia tungeweza kuwapa elimu, wakaweza kuwekeza kwenye kilimo ambao ni asilimia kubwa sana, hawa vijana wangetoka na wangekwenda kusimama na utaona uchumi unakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakuomba, kuna benki ambazo zinatoa mikopo kwa wakulima, benki hizi hazijaona vijana. Vijana hawawezi kuwekeza kule kwa sababu wanaonekana hawana thamani fulani hivi. Labda wawekwe kwenye vikundi ili waweze kwenda kwenye benki hizi waweze kukopeshwa au waundiwe SACCOSS zao maalum waweze kukopa maana hawana dhamana, ndiyo maana hawakopesheki.

Mheshimiwa Spika, kijana wa Tanzania hata akienda mahali anaonekana muhuni tu, lakini ni Mtanzania ambaye kimsingi tukimpa mbinu, tukampa elimu, tukawekeza kwenye kilimo, hawa vijana wasingelia leo. Kingine, akina mama wengi wanalima kwa jembe la mkono, hawalimi kilimo chenye tija. Hata wakilima hiki kilimo chenye tija, hawajui zao ambalo wanaweza kulima liweze kwenda nje. Tuwekeze kwenye tafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiwekeza kwenye tafiti, tukalima kilimo chenye tija, tutamkomboa mkulima mdogo na mkubwa na wote tutasimama. Niweze kusema hili suala kwa sababu tuna akina mama wengi wanalima kila siku ni kilio. Analima anaambiwa tu kwa maneno, kwa nadharia kwamba kilimo kitakukomboa, lakini haoni ukombozi wa kilimo hiki.

Mheshimiwa Spika, tukienda vijijini tukakusanya akina mama tukawapa elimu, wakalima kilimo ambacho kitakidhi vigezo kule nje, kwa sababu akina mama wengi wanalima, wanaweka mbolea ya chumvi chumvi, wakija kupima wanaona zao hili halifai. Tuwape elimu. Tuna mifugo; tuchukue mbolea za mifugo, tuweke kwa akina mama wale tuwekeze kwenye tafiti, leo kina mama tutawainua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kikubwa ninachoweza kusema kwenye sehemu ya pili ni mambo ya demokrasia. Mheshimiwa ameongea juu ya kuimarisha demokrasia, usawa na amani. Kuna watu wenye makovu, wana makovu yaliyopita huko nyuma. Tuna mategemeo; Tanzania, Taifa hili sasa hivi lina mategemeo makubwa na Rais wa sasa, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu. Lina mategemeo makubwa kutokana na kauli zake, wanasema kimjazacho mtu moyoni ndicho kinachotoka kwenye kinywa chake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu ameonyesha kunyesha suluhu kwa Watanzania. Kwa hiyo, Watanzania waliokata tamaa wamekuja kivingine. Niwaambie, kuna watu walikuwa wanagugumia, wanalia, wanashika matumbo, leo wanatembea vifua mbele, hata hawajaona kitu, kwa kauli ya kiongozi wetu mkuu, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu. Nampongeza lakini tumwombee kama Watanzania mama huyu asimame kwa hizi kauli anazosema azisimamie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipindi kilichopita, watu walipata makovu. Kuna Watanzania wanaogopa kuja kwenye nchi yao, kuna Watanzania wana kesi za kubambikiwa, za kisiasa zisizoisha, kesi hazina ushahidi zinapigwa tarehe, hatuwezi kuzizungumzia. Mheshimiwa Mama Samia Suluhu amesema kesi zile zifutwe. Niweze kusema jambo moja, kwenye demokrasia wanasema, bila haki kuonekana inatendeka, demokrasia itakuwa inambwela mbwela. Najua kwa kipindi hiki cha mama yetu, demokrasia itakwenda ku-take place na haki za watu zinaenda kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba mamlaka husika na viongozi ambao wako hapa wenye dhamana waweze kuangalia hii michango ya Wabunge. Wabunge wanachangia kutokana na mambo yanayowakuta huko na wananchi wao, tuweze kuyachukua kwa u-serious ili tuyatekeleze ku-reflect kule nje ambapo tunapotoka. Vinginevyo tutakuwa tunaimba mapambio na mambo hayachukuliwi, yakibaki pale pale tunaonekana huku tunakuja kula bata, lakini huku tumesimama kwa ajili ya wananchi wetu. Tunaomba yachukuliwe kwa u-serious ili yaweze kutekelezwa na wananchi waweze kuona matokeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nakushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia kwenye sekta hii muhimu.

Mheshimiwa Spika, sekta hii ninaweza kuzungumzia kwa wavuvi wadogo wadogo. Kwenye Jimbo la Kawe ninapotoka wavuvi wadogo wadogo wapo kwenye kata ya Kunduchi na Kata ya Mbweni, lakini wanachangamoto, changamoto yao kubwa ni Sheria ya Uvuvi ambayo inawabana. Wavuvi hawa wanatakiwa wakiingia majini waingie mita 50, mita 50 kwenye kina ni unatoka Kunduchi una fika Unguja ndiyo unakuta hichi kina. Kwa hiyo, wanapata hii changamoto, lakini wana miundombinu hafifu, wanakuwa na bodi, zile boti engine yake ndiyo unashikia mkononi. Kwa hiyo, mawimbi yakimkuta katika ya bahari anazama na kupoteza maisha tuiangalie hii.

Mheshimiwa Spika, lakini pia ushirikishwaji katika utungaji wa sheria tunaomba wavuvi hawa wadogo wadogo washirikishwe kwa sababu kwenye taarifa zetu, wavuvi wadogo wadogo wanachangia asilimia 98 ya pato la sekta hii, kwa hiyo, tuwaangalie kwa uwangalifu mkubwa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, changamoto zote wavuvi hawa wameweza kuvuna wastani wa tani 350 za samaki kwa mwaka hichi ni kiwango kidogo ukilinganisha na jinsi gani tulivyo na maeneo yetu, hiki ni kiwango kidogo na kwa sababu ni kiwango kidogo samaki hawatoshelezi kwa soko la ndani. Imelazimisha Serikali kuagiza samaki kutoka nje, samaki zinaagizwa tani 24 kutoka nje ambapo ni sawa na dola za Kimarekani milioni 25 uki-calculate kwa pesa ya Tanzania ni shilingi bilioni 690,000 kwa mwaka. Pesa hii ni nyingi na inakwenda nje kwa sababu sisi hatuna nyenzo za kutosha kusaidia wavuvi wetu wadogo wadogo.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali yangu kwa sababu naona Waheshimiwa Mawaziri ni wasikivu na wanachukua kwa sababu tunapokwenda ni kuzuri, walikuwa wanalalamika nyavu zinachomwa lakini sasa hivi elimu naona inafika na nyavu hazichomwi na sasa hizi milimita 16 imeshaeleweka kwa wavuvi. Kwa hilo, nawapongeza.

Mheshimiwa Spika, lakini nishauri pia tujue idadi halisi ya wavuvi wetu hili tuweze kuwasaidia wavuvi, wanalalamika hawasaidiki kwa sababu hawakopesheki, hatujui hata idadi yao, hatuna jinsi ya kuwasaidia kuweza kupata nyenzo nzuri na thabiti za kuweza kuingia majini.

Niombe Mheshimiwa Waziri unapokuja ku-wind up uweke vitu muhimu na facilities ambazo zitasaidia hawa wavuvi waweze kuingia kwenye deep sea bila ya kupoteza maisha.

Mheshimiwa Spika, lakini niombe kwa sababu sekta hii ni muhimu sana, tunaweza kutanua wigo, tutanue wigo wa wawekezaji; wenzangu wamesema tutanue wigo kama tunaona tunafika hapa tunaweza kupiga hatua 100 mbele, tutanue wigo, tutafute wawekezaji waweze kuwekeza kwenye hii sekta, tuna utajirisho wa kutosha. Tukiweza kuweza vya kutosha sekta hii inaweza kuwa ya kwanza kwa kuingiza pato la Taifa. Inaweza kuwa ya kwanza kuajiri vijana wetu. Niki-refer kule nyuma kwenye Mpango wetu wa Pili wa maendelea tuli-target mpaka mwaka 2020 asilimia 4.6 ichangie pato la Taifa sekta hii kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, lakini hatukufika kwa sababu hatuna nyezo kwa hiyo hatuna nyenzo, mafunzo na hatuna vifaa muhimu, lakini mpaka 2019/2020 ni asilimia 24 tu ilitengwa katika sekta hii ya uvuvi. Kwa hiyo twende tukapitishe bajeti na itekelezwe ili tuweze kwenda kusaidia watu wetu sekta hii imeajiri vijana, vijana wengi wamekwenda hawana elimu, wapate elimu ya kutosha, lakini tutapata pato la Taifa, tutapata ajira za kutosha, tutapata mapato ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa sababu muda ni mchache, nashukuru sana. (Makofi)
The Fire and Rescue Force (Amendment) Bill, 2021
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami nichangie.

Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mwenyekiti wa Kamati ambaye ametusimamia kwa weledi mkubwa katika Kamati yetu na kuhakikisha mambo haya yanakwenda vizuri. Naenda kwenye kile kipengele cha 9 amendment ya section 22 (a) ambacho kinaonesha moja kwa moja kwamba, kuna vigezo maalum ambavyo vinawekwa ili mtu aweze kufungiwa fire hydrants.

Mheshimiwa Spika, namwomba Waziri aende mbali zaidi kwa sababu tumeona majanga ya moto yakienda kwenye mabweni ya watoto wetu, masoko makubwa, mabenki na kusababisha athari kubwa sana, lakini ukiangalia kwenye level hizo wanaweza wasifikie kwenye vigezo hivi. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri itolewe elimu maalum na wale watu waweze kujilinda ili kuepukana na hasara itakayoweza kutokea; mali au watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru pia katika kipengele hiki ambapo Jeshi la Zimamoto limekuwa jeshi kamili kwa mujibu wa sheria. Tumeshuhudia uhalifu mkubwa wa kiwango kikubwa. Hata juzi tu Karikoo pale wakati soko linaungua huku vibaka wanaingia kwenye ATM Machines wanavunja wanachukua. Kwa hiyo, kitendo cha Jeshi la Zimamoto kupata silaha na kuweza kujilinda na kulinda mali za watu, ni kitendo ambacho kinatakiwa kiungwe mkono kwa sababu jeshi hili kuitwa jeshi bila silaha ni sawa na kibogoyo kupewa mfupa atafune. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba Bunge lako Tukufu liridhie jeshi hili kupewa instruments zake zote ili liweze kusimama kama jeshi. Kwa sababu, sometimes wanawaona kama wako legelege, lakini nafikiri utaratibu utafuatwa ili jeshi hili likasimame imara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Mpaka hapo sitakuwa na mengi ya kusema zaidi ya kushukuru kwa nafasi hii. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia katika hotuba ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, najikita kwenye ukurasa 33 ambapo ameainisha kwamba Serikali imeendelea kutekeza miradi ya ujenzi wa Mahakama mbalimbali nchini. Tuna kero kubwa ambayo ni kwikwi katika Taifa ni mlundikano wa mahabusu ndani ya Mahakama na wafungwa, hii ni kero kubwa kwa Taifa na inasababisha athari kubwa.

Mheshimiwa Spika, mpaka hapa tunapoongea mahabusu na Mahakama ndani ya nchi yetu wako zaidi ya 30,000 hawa zaidi ya 30,000 ni kiwango cha juu kabisa tumeshazidi yaani Mahakama zetu zimekosa uwezo na Magereza wa kuweza kumudu hawa watu.

Mheshimiwa Spika, nilijua mkakati utakuja madhubuti katika kutekeleza hili ili tuweze kupambana na adha hii, kwa sababu ndani ya Magereza kuna vitu vingi. Kuna kesi ambazo ni kesi za ajabu, yaani unakwenda Magereza unaenda kutembelea wafungwa unakutana na msichana amepoteza 10,000 ya bosi wake, yuko pale miezi nane, ni kesi ngumu.

Mheshimiwa Spika, ninapendekeza kwa sababu wale wakiwa kule tayari wana-adopt tabia ngumu na mbalimbali mbaya ambazo kwenye jamii hazikubaliki, ni bora tungekuwa na sera maalum au utaratibu wa kuweza kuchukua haya makosa madogo madogo na kuwafunga vifungo vya nje. Tukifanya hivi tunaweza kusaidia kupunguza adha ya mlundikano wa Magereza zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine kikubwa Magereza yetu pia yamejaza katika hao 30,000 kuna wakimbizi ndani yake ambao hapa nchini kwetu wanapita tu au hii ni njia. Kwa hiyo, hapa wanatokea Nairobi, wanakuwa-charged hela wanapita, hapa sisi tunaenda kuwekeza pesa tunajenga self- house tunawaweka, wanakula pesa za Watanzania, pesa za walipa kodi, halafu kifungo kikiisha wanaangalia tu kama kawaida. Kwa hiyo, tunapoteza fedha nyingi kutumia kwa hao watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa tuna takwimu ya wakimbizi 5,756 wako Tanzania na kwa siku mtu mmoja anakula shilingi 2,500 mara idadi hiyo, kwa siku wanakula zaidi ya shilingi milioni 14, ukihesabu kwa mwaka ni zaidi ya shilingi bilioni tano. (Makofi)

SPIKA: Sawa. Mheshimiwa Felista Njau tusaidie jambo moja, hawa ni Wakimbizi au wahamiaji haramu?

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ni wahamiaji haramu.

SPIKA: Eeh! Ni lazima taarifa yako iwe inawasema hivyo kwa sababu Wakimbizi kuwekwa ndani tena inakuwa kidogo siyo sahihi.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, sawa. Hao wahamiaji haramu ambao wanaopita, kwa hiyo wanatumia shilingi zaidi ya bilioni tano milioni mia moja kumi na moja ambazo ni pesa za walipa kodi ya Watanzania. Ukikaa ukafikiria unaweza ukaona labda, halafu hakuna mtu anayeshtuka wala hakuna hatua, kikubwa ingewezekana wakifika hapa wachukuliwe na escort mpaka mpakani wanapoelekea ili tuokoe hii pesa ya Watanzania ambayo inachukuliwa bure na hawa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati tunazungumza haya ziko hospitali hazina dawa, wakati tunazungumza haya ziko barabara mbovu, pesa hii ingeweza kuelekezwa kule na ikaleta tija. Ukijumlisha hii pesa kwa pesa ya Tanzania kwa darasa moja la Shilingi Milioni 20 unajenga madarasa 250, kitu ambacho hili tungelichukua kama special case tukaenda nalo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine gumu wahamiaji hawa haramu wapo waliotumikia kifungo chao, wamemaliza kifungo na wapo nchini 2,200 wanakula pesa za walipa kodi, wanakula pesa za Watanzania, wahamiaji haramu 2,200 wapo tu wamemaliza kifungo, hawapelekwi kwao, hawako ndani wako tu pale wanambwela wanakula hela za Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba hatua zichukuliwe Uhamiaji, Mambo ya Ndani na Polisi washirikiane katika hili ili kuokoa pesa nyingi za walipa kodi zinazopotea. Tunalia adha ya umaskini, tunalia janga, sasa hivi tuko kwenye umaskini mkubwa huko nje kila mtu ana kilio, lakini pesa hii ingeweza kuwezesha hata vikundi vya akina mama ambao leo wanatembea wana adha kubwa, hili tulichukue kwa unyeti wake ili lilete tija kwa Taifa letu. (Makofi)

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Felista Njau, kati ya hawa Wahamiaji Haramu ambao wamemaliza kifungo chao wamekuja jamaa zao kuwataka wasafirishwe, basi bado kuna ugumu wa kuwatoa na bado tumewashikilia. Nataka nimuongezee hiyo taarifa. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Felista Njau unaipokea taarifa hiyo?

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, naipokea kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika suala hili niombe Wizara ziungane ili kulitatua kwa wakati na kwa muda ili kuokoa pesa hizi zinazopotea.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo ninataka nilichangie kwa ufupi ni kwamba kuna kipande cha barabara inayotoka Morogoro kuja Dodoma, hiki kipande ni kama vile watu hawaoni, lakini ni kipande kigumu ambacho kina mabonde, ukisafiri usiku unaweza ukafikiri haupo Tanzania, lakini kwenye barabara hiyo kwa siku unakutana na malori manne, matano yamedondoka yako chini, hakuna effort zozote zinazochukuliwa katika kurekebisha barabara hii ambayo umuhimu wake mkubwa kwanza ni barabara inakuja Makao Makuu ya nchi.

Mheshimiwa Spika, pili, barabara hii inaunganisha nchi za jirani kwa maana ya Uganda, kwa maana ya Congo, kwa maana ya Rwanda, kwa maana ya Burundi. Barabara hii ni ya msingi kwa maana ya diplomansia yetu ya kiuchumi, inasafirisha malori yanayosafirisha bidhaa kuelekea nchi mbalimbali, lakini imesahaulika kabisa.

Mheshimwia Spika, lakini kwenye barabara hiyo kwa siku unakutana na malori manne mpaka Matano yamedondoka, na hakuna efforts zozote zinazochukuliwa katika kurekebisha barabara hii ambayo umuhimu wake ni mkubwa. Kwanza inakuja makao makuu ya nchi, pili, barabara hii inaunganisha nchi za Jirani za Uganda, Congo, Rwanda pamoja na Burundi. Kwa hiyo, barabara hii ni ya msingi, kwa maana ya diplomasia yetu ya uchumi kwa sababu malori yanasafirisha bidhaa kuelekea nchi mbalimbali, lakini imesahaulika kabisa.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana, nafikiri ni Oktoba, Msemaji wa Serikali alisema tayari upembuzi yakinifu umefanyika tunatafuta Mkandarasi, lakini naona kuna ukimya mkubwa katika barabara hii. Naomba tulichukulie kipaumbele kwa sababu Wabunge wanapita hii barabara na watakuwa ni mashahidi wangu, barabara ni mbovu kwa kiwango cha tofauti. Naomba hilo lichukuliwe kama ushauri wangu. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwa uchache kulingana na dakika zilizoko mbele yangu. Kwanza kabisa nipongeze Vyombo vyetu vya Ulinzi na Usalama kwa kazi kubwa ya kutukuka na ya kizalendo wanayoifanya katika Taifa letu. Natangulia kupongeza kwa sababu vyombo hivi havina bajeti ya kutosha lakini kazi wanayoifanya ni kubwa sana. Nafikiri wangekuwa wanafanya kazi ambayo haina mashiko tusingekuwa tuko salama leo. Kwa heshima hii nawapa kwa sababu wanafanya kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naenda moja kwa moja kwenye Bajeti ya Maendeleo. Tumesikia maoni ya Kamati, nami naungana nayo asilimia 100, lakini kwa masikitiko yangu makubwa, tumeangalia Ngome fungu namba 28 wamepokea asilimia 17.74 tu. Kwenye hii Jeshi letu liko hoi bin taabani, lakini wajibu wake ni mkubwa mno kulingana na bajeti ambayo wameipokea. Tunaelekea Bunge la Bajeti na hawa watu hawajapokea hata robo ya bajeti yao, ni hatari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua JKT ni eneo ambalo kila mtu anaangalia baada ya Taifa letu kuonekana kwamba ajira imekuwa ni duni kwenye Taifa letu, vijana hawana ajira hata awe na kitu gani, lakini nafasi ya ajira kwenye Taifa letu ni ndogo, wako mtaani, wana fani zao, lakini hawaajiriki mahali popote, hawawezi kuajiriwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekimbilia kwenye chaka la Vyombo vya Ulinzi na Usalama ambao wameonesha kuajiri vijana wengi kwenye Taifa letu. Hii siyo siri ni lazima tuseme ili tuone ni wapi palipotoboka? Eneo kubwa zaidi ni JKT ambao kimsingi mpaka sasa hivi vijana wetu wako huko kwenye mafunzo kwa maaana ya uzalendo lakini baadaye wataingia kwenye ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, JKT pesa walizoomba jana za bajeti mpaka leo naongea hapa wamepata asilimia sifuri, the shame. Asilimia sifuri, tukajiuliza maswali kwamba hawa watu huenda vigezo hawajatimiza wakaja kwenye Kamati, tukawahoji wakasema na certificate walishapeleka, kuna nini kinaendelea kwenye Jeshi letu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawawezi kulia wakasikika au kusema popote kutokana na ethics za kazi zao, lakini sisi kama Taifa tunalionaje Jeshi hili ambalo linalinda ulinzi, mali zetu, uraia na watu wetu, wamepata asilimia sifuri? Mwaka jana walikuja hapa wakaleta Miradi yao ya Maendeleo wanayotaka itengewe fedha, Chita ambapo kuna Kilimo wameweka hekari 12,000, tukiamua kuhudumia eneo lile hata mfumuko wa bei utapungua. Tunafikiria nini kuhusu Taifa kama Vyombo vya Ulinzi na Usalama hatuwezi kuviangalia, hatuwezi kuvitengea bajeti kwa manufaa ya Taifa letu. Mama yetu kipenzi anazunguka kutafuta pesa huku na kule, nia yake ya dhati ni kulisaidia Taifa, Taifa linasaidikaje kama usalama wa nchi unakuwa tete? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia hili naona kuna la kufanya. Juzi Waziri wa Fedha Mheshimiwa Mwigulu Nchemba alikuwa hapa akasema fedha hazigawiwi tu kama peremende, ni lazima kuwe na utaratibu umefuatwa, utaratibu umefuatwa fedha ziko wapi? Akamjibu Mheshimiwa Bashe, hapa akamwambia kwa kuwa wewe hujatimiza vigezo fedha zimejaa, zilizojaa zielekee kwenye Vyombo vya Ulinzi na Usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na muda naelekea maeneo yetu ya Jeshi la Magereza. Kwenye nchi yetu, kwenye Taifa Jeshi la Magereza mpaka sasa…

MWENYEKITI: Mheshimiwa nakuongeza dakika moja maana muda wako umekwisha.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshazidiwa…

MWENYEKITI: Malizia sasa.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, uwezo wa Magereza ni watu 29,902, leo tuna watu 321,146. Tuliojaza kule siyo Watanzania, wako wahamiaji haramu 3,809 wako pale. Tuliomba tukasema kuwa kuna mkakati wa ziada wa kuwaondoa wahamiaji haramu, wahamiaji wale kwa siku wanatumia Sh.15,540,000, kwa mwaka wanatumia billion 5.6, bajeti ambayo tungeipeleka kwenye vituo vya afya, tukaipeleka kwenye madawati, tungepata madawati 81,000. Tungepeleka kwenye nyumba za Walimu tungepata nyumba za Walimu 62,200. Leo tunalia lakini watu wako picnic, wale wahamiaji haramu pale hatuwezi kuwapeleka shambani wakalime. Kwanza wako weak na wanafurahia kwa sababu wamepumzika, sisi tunapumzisha watu, wanakula pesa za Mama yetu, anakwenda kuzitafuta Ughaibuni, tuwe na uchun gu na pesa hizi za Rais wetu anatafuta Ugaibuni ili watoto wake wale. Nauliza swali, kiko wapi cha kumpikia mgeni wenyeji kulala na njaa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuwe na utaratibu wa vyombo vya sheria wawaondoshe watu hawa, tayari Jeshi la Uhamiaji wamechukua hatua, wameanza kutoa Visa rejea, nawapongeza sana. Hoja hii ilikuwa ya kwangu mwaka jana, wameanza, lakini walioko ndani waondoshwe waende kwao tubaki sisi tubanane humu humu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii jioni ya leo ili niweze kuchangia kidogo. Mwaka 2022/2023, Bunge letu Tukufu liliidhinisha kiasi cha shilingi bilioni tano milioni mia moja na arobaini na nane ikiwa ni mpango wa kuboresha elimu ya sekondari katika shule zilizojengwa katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka ilipofika Februari, haikupelekwa hata shilingi mia. Ipo desturi ya Bunge lako Tukufu kuidhinisha fedha kuelekea kwenye miradi ya maendeleo na fedha hizi haziendi, umekuwa kama ni ugonjwa sugu, lakini pia tunafifisha maendeleo yetu. Katika hili kuna shida kwa sababu fedha hizi zilikuwa zinatakiwa ziende kwenye kununua vifaa vya maabara, lakini zikanunue kemikali ili watoto wetu ambao wanasoma shule za sekondari waweze kusoma kwa ufanisi na kwa vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wetu walikosa fursa hii mwaka jana. Kuna tatizo ambalo linatokea baada ya watoto wetu hawa kukosa vifaa vya sayansi. Kuna athari kubwa 2021 wanafunzi 158,185 walipata daraja la sifuri na daraja la nne katika shule za sekondari. Huu ni ukosefu wa vifaa, tumemwona Mama yetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan, siwezi kubeza jitihada zake, huyu Mama amejitolea kwa kiwango kikubwa kuilinda na kuitetea Tanzania kwa wivu mkubwa. Kwa sababu tu Rais Samia, aliidhinisha ujenzi wa majengo ya shule za msingi na sekondari kila Mbunge akisimama anajinasibu katika hilo na nitakuwa ni mchoyo wa fadhila kama sitamshukuru katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wanafunzi asilimia 66 mwaka 2021, walipata madaraja haya zaidi ya nusu ya watahiniwa. Maana yake nini? Tunakwenda nje ya malengo ya ushindani wa kielimu, kwa nia njema na thabiti kabisa ya Taifa langu naomba nishauri, zipo shule za private ambazo zinafanya vizuri. Zikifanya vizuri siyo kuzifichia matokeo twende tuka–compete nao tuwe partners nao tusi–compete nao, tuwasaidie ili wasaidie Serikali kuweza kufanya vizuri katika matokeo ya watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na shule nyingi za private zinazofanya vizuri, siyo uchawi ni jitihada katika miundombinu ya elimu, Walimu wanalipwa vizuri, wanalipwa mafao vizuri, ndiyo wanafanya vizuri. Kujenga majengo pekee haitoshi katika elimu. Katika shule za private kumekuwa na mlolongo wa tozo na kodi hii ni kuwarudisha nyuma, tuna–compete nao hawa tunawaweza tuungane nao, tuboreshe elimu ya Tanzania, tuondoe tozo na kodi, ziko zaidi ya 15, akija mtu anawekeza kwenye elimu anaanza kuogopa, tuige kwa wenzetu Uganda na Kenya waliwaleta karibu, wakaungana nao, elimu imeboreshwa. Tuungane na private sector twende tukadumishe elimu kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo kuna shida kwenye elimu. Watu wengi wameitika elimu bila ada, wameitika siyo siri. Hata hivyo, wanaokwenda kumaliza shule elimu ya msingi na sekondari wanakuwa ni nusu ya wale walioanza. Katika Ripoti ya CAG inaeleza katika halmashauri 11 za shule ya msingi tayari wanafunzi zaidi ya nusu…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Njau, Ripoti ya CAG ya mwaka gani?

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ya mwaka 2021. Halmashauri ya Kwimba wanafunzi waliandikishwa 6,950, waliomaliza shule ya msingi ni 3,783 sawa na asilimia 49, ndiyo iliyoongoza kwa wanafunzi kuacha shule. Huenda ni miundombinu lakini sisi kama Taifa tuboreshe miundombinu yetu ili tuweze ku–compete na elimu yetu. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

TAARIFA

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Nataka kumpa taarifa muongeaji kwamba Wilaya ya Kwimba wanafunzi ambao hawakwenda kumaliza elimu yao ya msingi ni kwa sababu ya fisi walikuwa wametanda maeneo hayo kwa muda mrefu, lakini siyo kwamba labda eti watoto wale wameshindwa kumaliza elimu ya msingi kwa sababu wamekwenda kuchunga ng’ombe, Hapana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Njau, unapokea taarifa?

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, amenibeza. Inayofuata ni Halmashauri ya Kinondoni Mjini, ambayo wanafunzi walioandikishwa kuanza shule walikuwa 15,000, waliomaliza ni 4,652. Tayari tumeshuka sawa na asilimia 46. Kwa hiyo tunaweza kusema ni kijijini lakini pia mijini lipo hili tatizo, kuna nini? Ni lazima tufuatilie kwa ukaribu ili tujue kwa nini watoto wetu hawamalizi shule? Kwa nini wanakuwa na ari ya kwenda shule lakini hawamalizi shule. Kwa hiyo kuna tatizo ambalo liko hapa katikati, tutakapoacha tutaliacha Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea. Katika shule za sekondari walioanza katika Halmashauri ya Newala, kati ya wanafunzi 7,950, waliomaliza ni elfu nne na kitu. Hii idadi bado inazidi kupungua. Kwa hiyo ushauri wangu tuungane na sekta binafsi, tuboreshe elimu yetu, tuangalie changamoto iko wapi, twende tuka–solve changamoto, lakini tusisahau maslahi kwa Walimu. Walimu wana wakati mgumu japo hawatoshi, lakini wale waliopo wanalia ukata. Mishahara midogo, pesa zao za malimbikizo ya kupandishwa vyeo hawana, miundombinu ni mibovu. Tukienda kuboresha hapa nafikiri tunaweza tukapata kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naenda kwenye asilimia kumi ya mikopo. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu na Serikali kwa ujumla, jana walitoa kauli thabiti ambayo akinamama waliokuwa wanategemea wa waliyokuwa wanayategemea walisikia ile kauli wakawa na wasiwasi. Nasema leo nawaondoa wasiwasi, kauli ya Serikali ni thabiti kwa sababu kulikuwa na mianya ya rushwa, pesa zilikuwa zinapewa watu, si wahusika, kwa hiyo kimsingi ni lazima ufuatiliaji upatikane na watu waanze kufanya utafiti, ndipo pesa hizi zitolewe tena. Naiungana mkono Serikali katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii muhimu sana, kwa maslahi mapana ya Taifa letu. Awali ya yote kwanza nitambue mchango mzuri na kazi, ufanisi, tija pamoja na uzalendo unaofanywa na vyombo vyetu vya ulinzi na usalama. Pia nitambue na nipongeze jitihada za Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambaye hivi karibuni siku ya Muungano Aprili 26, aliweza kutoa msamaha kwa wafungwa 376. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amekuwa na tabia ya kuingia moja kwa moja kwenye kero na kuzitatua. Mimi kwa hilo nampa hongera lakini si kwamba tu aliwaondoa wafungwa na kupunguza msongamano bali aliweza kupunguza gharama za matumizi ambazo kwa mwaka ni bilioni 338 ambazo zinatumiwa na hao tu 376.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tatizo la msongamano wa wafunga magerezani bado halijapatiwa jibu sahihi, ndiyo maana naona Mheshimiwa Rais alielekeza nguvu zake kule ili kuonyesha njia ili na sisi wenye dhamana tuweze kupita huko kuona namna gani tunaweza kwenda kupunguza msongamano huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, idadi inayotakiwa kwa wafungwa ni 29,902 lakini iliyopo sasa ni 32,140, tayari tumezidiwa. Tusiende tu kukimbilia kwenye kujenga magereza lakini tutafute mwarobaini. Sisi tuliona kwamba Bodi ya Parole inaweza ikawa mwarobaini lakini zipo Sheria katika Bodi ya Parole ambazo zinakwamisha wasiweze kuchukua hatua. Sheria hizi zinatakiwa bodi ikae iweze kuzichakata ili kuona sheria rafiki zitakazosaidia ili kuweza kupunguza msongamano wa wafunga magerezani. Nikisema hivyo nirejee kipo kifungu ambacho kinaonyesha kwamba lazima aliyemshtaki mtuhumiwa aweze kuridhia na kusaini ndipo mtuhumiwa aweze kupata msamaha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kuna mambo mengi, wanaweza kuwa na chuki, anaweza kuwa na hasira na asikubali. Kwa hiyo, wale watu wanabaki magerezani. Kwa hiyo kwa kiipengele hicho niombe Bodi ya Parole itakavyokaa ianze kuchakata sheria ziwe rafiki kwa ajili ya kupunguza msongamano kwa wafungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, msongamano huu wa magereza unajumlisha Wahamiaji haramu. Bunge liliopita nilisimama kwenye Bunge lako Tukufu nikazungumza ni namna gani Wahamiaji haramu wanakomba pesa za walipa kodi na kwenda kukaa kwenye picnic, kwa sababu watu hawa hawawezi kufanya kazi ya uzalishaji. Tayari wamemaliza vifungo vyao, tuna wahamiaji haramu 2,609 wako wamekaa wanastarehe wanakula chakula, hawa wahamiaji haramu 2,609 wanatumia pesa za walalahoi, pesa za walipa kodi, pesa za watu wadogo wadogo ambao wanalazimishwa kulipa kodi wasipolipa kodi watachukuliwa hatua. Sisi tunachukua hatua gani kuwaondoa wahamiaji haramu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wahamiaji hawa haramu kama ilivyosema Kamati, wanatumia pesa nyingi kwa mwaka, wahamiaji hawa haramu wanatumia bilioni 2.3. Bilioni 2.3 ni pesa nyingi, ni pesa nyingi ukilinganisha na maisha yetu ya sasa, fedha hizi zingeweza kuelekezwa kwenye madarasa zingejenga madarasa 117 na watoto wetu wangekaa sehemu salama, zingeweza kuelekezwa magereza huko huko zikaenda kwenye miradi ya maendeleo nao magereza wangeweza kufanya mambo makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, itumike busara wakati Waziri anakuja ku-wind up aweze kuonyesha dira ya wahamiaji haramu, kwa sababu zipo hapa Wizara ya Mambo ya Nje, Wizara ya Mambo ya Ndani, Wizara ya Mambo ya Ulinzi, kaeni muone namna gani mnakwenda kutoa hii kansa ambayo imeenea kwenye Nchi yetu. Nikisema hayo naenda ku - reflect kwenye bajeti ya magereza, bajeti yao ni ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bajeti ya Maendeleo mwaka 2022/2023 wameomba shilingi 21,300,069,000. Hizi zilitengwa na Bunge, lakini fedha walizopata ni shilingi milioni 100. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Hee! Loh!

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Magereza wana shughuli za kufanya, wana rasilimali watu, wanaweza kufanya mambo makubwa, wamepewa shilingi milioni 100 sawa na 0.46%. Hatuwezi kwenda hivi. Kama tunawapa wahamiaji haramu shilingi bilioni mbili sawa na 20%, tunaachaje kuwapa hawa wazalishaji? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zetu tumewekeza, tunalisha watu wanaopita wanakuja kukaa hapa wanapunga hewa, tunaacha kwenda kuzalisha. Watu wa magereza waliweka mikakati 2020 wakasema wana vituo tisa wanaweza kuzalisha mazao mbalimbali, wakapunguza burden ya mafuta ya kula, wakapunguza burden ya mfumuko wa bei. Tungewapa fedha wakalime. Wana ardhi, wameziainisha vituo tisa. Tumeshindwa kuwapa fedha lakini fedha za kulisha wahamiaji haramu, wapita njia tunazo. Kiko wapi cha kumpa mtoto wa kambo chakula ukamwacha mtoto wako? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba lichukuliwe kwa u-serious kabisa, wakati Mama yetu anazunguka huku na kule ughaibuni kutafuta fedha, sisi tunakwenda kulisha watoto wa jirani wanashiba sisi tunalala njaa. Naomba fedha inayotengwa na Bunge kwa ajili ya Bajeti za Wizara hii na Wizara nyingine kwa maslahi ya Taifa zikatolewe kwa wakati. Hazitolewi. Ukiwapa shilingi milioni 100, wakanunue nini katika shilingi bilioni 21? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka ninavyoongea leo, wako tu wako hapo. Vyombo hivi haviwezi kulalamika kutokana na nature yao ya kazi, lakini sisi tunakuwa midomo yao, tunawasemea. Wanafanya kazi kwa kinyongo, hawafanyi kazi vizuri, wanafanya kwa kinyongo lakini ni kwa sababu wamejawa uzalendo, wanafanya kazi hii na Taifa linaona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Magereza ardhi waliyonayo ni ekari 19,770. Iliyotumika ni 3,850 sawa na 19% halafu mnalalamika hawa Magereza wamekuwaje? Wapeni hela tuwapime kwa kazi zao. Tuwape fedha wakafanye kazi. Wana uwezo mkubwa, wana ufanisi mzuri, wana uzalendo wa kutosha, wanaweza kuliletea tija Taifa, lakini wameshindwa kufanya kwa sababu tu hawana fedha za maendeleo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana. muda wako umekwisha. Tunashukuru sana kwa mchango wako.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Namalizia kwa kusema, Waheshimiwa hawa Jeshi la Magereza wapate stahiki zao, waweze kununua sare zao wenyewe. Wasinunuliwe, wanunue kwa wakati ili wawe smart. Saa nyingine unakutana nao hawaeleweki. Tuwasaidie wakasimame. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye hotuba hii ya Bajeti. Nikianza na hotuba hii ya bajeti, nimeiona imejikita kwenye mambo mengi ikiwemo utalii, uvuvi na mambo mengine. Si mbaya kwa sababu tayari tunatafuta keki pana zaidi kwa ajili ya kugawanya mgawanyo wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa zaidi sijaona kipengele muhimu sana cha diplomasia ya uchumi. Kinachofanyika katika Taifa letu, Mama Samia Suluhu Hassan amekuwa kama assist kwenye ulingo wa mpira. Sasa wanatakiwa ma-striker wa kufunga magoli, hivyo, kila mtu acheze kwenye nafasi yake. Wakati tukiimba royal tour inaleta matokeo ni lazima sasa twende kwenye diplomasia ya uchumi tuangalie tutapataje watu kupitia royal tour, wawekezaji pamoja na fursa mbalimbali katika Taifa letu. Yeye amecheza nafasi yake na sisi tunatakiwa kucheza kwenye nafasi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikisema hayo, naenda moja kwa moja katika balozi zetu. Huwezi kuongelea diplomasia ya uchumi kama usipogusa balozi zetu nje ya nchi. Sasa hivi kuna shida kubwa katika balozi zetu nje ya nchi ambapo kuna uhaba mkubwa wa watumishi. Wale watu wanatakiwa wawe ndiyo reception yetu ya kupokea watalii, wawekezaji na watu wanaokuja kutafuta fursa na kutafuta sisi fursa kwenda nje, lakini kuna uhaba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ukaguzi wa CAG wa Machi, 2022, inaonekana katika balozi sita kuna upungufu wa watumishi 26. Kiwango hiki ni kikubwa kwa sababu walitakiwa wawe watumishi 62 lakini wapo watumishi 38 tu. Hawa ndiyo tunaowategemea wawe reception yetu ya kupokea watalii na kupokea wawekezaji, hili ni janga. Wakati tunakwenda katika nchi ya Kongo, pia tulikutana na hii kesi ya upungufu wa watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilishauri, nikasema katika balozi zetu huwezi kuuza bidhaa zako ukazifungia chumbani, ni lazima uzitangaze. Katika balozi zetu hakuna kitengo ambacho ni cha habari. Ukiangalia blog mbalimbali za Wizara, ukiangalia kwenye social media huoni utangazaji wa fursa za kiuchumi za Tanzania kama ilivyo, huoni watu wamejipambanua. Tunahitajika kujipambanua zaidi kama Tanzania, tusisubiri mtu mmoja atangulie mbele halafu sisi tukarudi nyuma. Tutakuwa tunaharibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiangalia katika suala zima la watumishi. Kama watumishi hawapo wa kutosha, ule mzigo unakuwa ni mkubwa, ufanisi unakuwa duni. Kwa hiyo, naomba wakati Waziri anakuja aweze kutuwekea mkakati bayana ni namna gani tunaenda kujaza hizi nafasi za watumishi katika balozi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, athari hii imekwenda moja kwa moja kwenye utekelezaji wa dhana ya kidiplomasia katika balozi zetu. Mwaka 2020/2021, balozi sita nje ya nchi zilishindwa kutekeleza dhana hii kwa kukosa bajeti. Siyo kwamba zilikosa hakuna, hazikupelekwa, zilitengwa na Bunge lako Tukufu lakini hazikupelekwa nje ya nchi. Nikifika hapa naunga mkono kile kipengele cha ufuatiliaji kwa ajili ya kuangalia bajeti tunazotenga, je, zinafika kwa wakati na zinafika kama tulivyozitenga? Otherwise tutakuwa tunakaa hapa na tunachokisema kinapotelea hewani, bila kipengele hicho hatuwezi kuvuka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, labda niainishe balozi ambazo zilishindwa kutekeleza hii dhana ya diplomasia ya uchumi nje ya nchi kwa vitendo kwa kukosa bajeti. Bunge lako tukufu 2020/2021, lilitenga shilingi 116,200,000 kwenda Ubalozi wa Kinshasa Congo, lakini fedha zilizopelekwa ni Sh.13,000,000, sawa na asilimia 11, tunatokaje hapa? Balozi ya Lilongwe ilitengewa shilingi 57,000,000, zilipelekwa shilingi 12,000,000 sawa na asilimia 21. Tunaondokaje hapa kwenda mbele? Ubalozi wa Doha ulitengewa shilingi 75,600,000, tulipeleka shilingi 10,000,000 tu, sawa na asilimia 14. Tuna move vipi kwenda kufunga magoli, vita iliyopo sasa hivi kwenye Taifa ni vita ya kiuchumi siyo vita ya mtu kwa mtu. Tunaingiaje kwenye ushindani wa kiuchumi kama reception yetu imefungwa na hakuna pakupita? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, Addis Ababa tulitenga shilingi 138,000,000 zimepelekwa shilingi 2,000,000 tu, shame. [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo ni sawa na asilimia 1.8. tunakwenda wapi? Ubalozi wa Washington DC tulitenga shilingi 144,000,000,000 lakini zilizopelekwa ni shilingi 8,000,000, sawa na asilimia saba. How can we move kama nchi kama tunakwenda kufanya mambo kama hayo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikitoka hapo niende kwenye kipengele cha pili. Hawa watu Mabalozi wetu, watumishi wetu wa ubalozi ambao ni pungufu wamebeba mzigo mkubwa lakini wawakilishi hawa wanadai Serikali, kuna nini hapa?

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Njau kuna neno umelitamka ambalo si neno la Kibunge ni neno la kuudhi. Huwezi kusema Serikali imefanya kitu halafu ukatamka neno hilo la shame. Kwa hiyo, naomba ulifute.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, nalifuta.

NAIBU SPIKA: Hapana, tamka kwa maneno yako kwamba hilo jambo unalifuta.

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, niseme ni aibu. [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

NAIBU SPIKA: Futa neno lako hilo. Futa neno lako hilo. Si umeshafuta?

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, nimefuta.

NAIBU SPIKA: Haya, ahsante. Tuendelee. (Makofi)

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, badala yake niseme inasikitisha sana. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea. Madai ya watumishi katika balozi zetu ambayo ni sebule (reception) ambayo tunawapokea wawekezaji na watalii, tuwaangalie kwa jicho la huruma. Kwenye ripoti ya CAG imeainisha balozi nne ambazo zinadai Shilingi milioni 684.17, ni fedha nyingi. Labda niziainishe kwa haraka haraka; ni Ubalozi wa Paris, Ufaransa ambao unadai Shilingi milioni 83.2; Ubalozi wa Kuala Lumper, Malaysia unadai Shilingi milioni 67.3; Ubalozi wa Kinshasa, Congo unadai Shilingi milioni 243; Ubalozi wa Pritoria, South Africa unadai Shilingi milioni 290. Jumla yake ni Shilingi milioni 684.17. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa watu wenye mzigo mkubwa ambao hawatoshi, lakini bado wanadai marupurupu, wanadai posho zao na malimbikizo yao ya mshahara, na bado wanatakiwa waende mbele kupambana; nafikiri kama sijakosea, kwenye Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma za Mwaka 2009 zinaelekeza, kama kuna watumishi wanadai malimbikizo, marupurupu, posho, kupanda vyeo, walipwe mara moja. Kanuni hii imekiukwa kupitia balozi hizi. Tunaendaje kuwabana wakafanye kazi kubwa namna hiyo wakati hata fedha zao hawajapewa?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri anapokuja hapa aeleze ni mkakati gani madhubuti wa kwenda kulipa madeni haya ili balozi zetu ziweze kufunguka na Tanzania iweze kupata neema?

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunaongelea haya, ni kwa maslahi mapana ya Taifa letu, ni kwa maslahi ya nchi yetu ambapo tumeona Kiongozi Mkuu Jemedari ametangulia mbele na wengine wapo nyuma wanarudi nyuma, tukamshike mkono twende wote pamoja. (Makofi)

(Hapa kengele ililila kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)