Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Nusrat Shaaban Hanje (31 total)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa kuwa Naibu Waziri amekiri kwamba anatambua uhitaji wa kuweka life skills na soft skills kwenye elimu yetu Tanzania.

Je, Serikali iko tayari sasa kwa ajili ya kuendana na mabadiliko ya mfumo ya Sayansi na Teknolojia pamoja kizazi kipya kwa sababu generation inabadilika. Serikali sasa ipo tayari kulifanya, kuifanya topic ya soft skills ambayo inafundishwa kwenye somo la civic kwa form one topic ya kwanza form two topic ya kwanza na form three topic ya kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ipo tayari sasa kufanya topic ya life skills iwe somo maalum sasa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba inatengenezewa utaratibu mzuri wa upimaji wa uelewa na kuhakikisha kwamba vijana wanapata maarifa zaidi kuliko kusoma kwa ajili ya kujibu mtihani?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili, je, lini sasa Serikali itaanza mchakato wa kushirikisha wadau wa elimu wakiwemo wanafunzi wenyewe na watu wa ku-develop mitaala ili kuhakikisha kwamba wanayoyasema yanatekelezwa kwa vitendo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nilivyoeleza katika jibu langu la msingi kwamba katika mwaka wa fedha 2021/2022 tunakwenda kufanya maboresho na mapitio ya mitaala kama nilivyozungumza hapo awali. Kwa hiyo, suala la kuingiza life skills, suala la kuhuisha mitaala ni suala ambalo lina mchakato mrefu ukiwemo na huo Mheshimiwa Mbunge aliouzungumza.

Kwa hiyo, tutahakikisha tunaenda ku-absolve au kuhusisha na mawazo hayo ambayo ulikuwa nayo maadam tayari hili lilishakuwa ni topic kwenye masomo naweza vilevile tukaifanya kama somo kwa kadri utafiti utakavyotuelekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala kwamba ni lini, kama nilivyoeleza kwenye majibu ya msingi kwamba katika mwaka wa fedha 2021/2022 tutakwenda kuianza kazi hiyo kwa kadri itakavyowezekana. Ahsante.

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwanza nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri aliyotoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika mwaka ujao wa fedha tutafanya mapitio ya mitaala. Lakini swali la nyongeza la pili la Mheshimiwa Nusrat alikuwa ameomba kwamba wadau washirikishwe. Nilikuwa nataka kumtoa hofu kwamba Serikali inapoandaa mitaala huwa inawashirikisha wadau na hata sasa hivi tutawashirikisha. (Makofi)

Kwa hiyo, nitumie Bunge lako Tukufu kuwaomba Waheshimiwa Wabunge kama kuna mambo yoyote ambayo wanadhani yanapaswa kuingia katika mitaala yetu Wizara ya Elimu tupo tayari kupokea maoni yenu. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa kuna umuhimu sana katika barabara ya Singida – Supuka – Ndago ambayo kimsingi inapita katika Jimbo la Waziri wa Fedha pia.

Je, ni lini sasa Serikali itaichimba angalau kwa kiwango cha changarawe barabara hii ambayo zaidi ya miaka kumi haijafanyiwa marekebisho yoyote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mheshimiwa Mbunge ameuliza barabara ya Supuka – Ndago ambako ni Jimbo la Iramba Magharibi ambapo anatokea Waziri wa Fedha wa sasa Mheshimiwa Mwigulu Nchemba. Niseme tu kabisa kwamba barabara hiyo itajengwa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri kuhusiana na upatikanaji wa mbegu ya alizeti kwa wananchi wa Mkoa wa Singida naomba nimuulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mkoa wa Singida wamekuwa wakilima kwa utaratibu wa kawaida kabisa ule ambao wanalima wakimaliza wanaweka mbegu baada ya kuuza wanabakiza kidogo kwa ajili ya kwenda kulima tena mwakani ndio utaratibu wanaoutumia mpaka sasa hivi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Naibu Waziri sasa yupo tayari kwa ajili ya kwenda kukutana na wakulima wa alizeti wa Mkoa wa Singida hususan jimbo la Singida Magharibi kwenye kata za Mwaru, Mgungia, Muhintiri, Minyukhe kwa ajili ya kwenda kuzungumza nao sasa kuona namna gani ambavyo ku-in cooperate mawazo yao na ya Wizara kwa ajili ya kuhakikisha kwamba upatikanaji wa mbegu ya alizeti, zinapatikana zenye tija ili walime kilimo ambacho sio cha desturi? Ahsante sana.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hanje kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwenda ku-visit tupo tayari na tutafanya hivyo na Mwenyezi Mungu akijaalia mwezi huu wa Juni tutakuwa na Mkutano mkubwa utakaoongozwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu katika Mkoa wa Sindiga kwa ajili ya suala la zao la alizeti na kukutana na wazalishaji na wakulima wa alizeti. (Makofi)
MHE. NUSRAT SH. HANJE: Mheshimiwa Spika ahsante, pamoja na majibu Mheshimiwa Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Mkoa wa Singida ni mkoa muhimu sana pamoja na Mkoa wa Dodoma na Simiyu katika uchumi wa nchi, kwa sababu inatambulika kwamba Singida sasa hivi ni pilot kwenye zao la alizeti mahususi kwa ajili ya nchi, kwa hiyo pamoja na jibu lake kwamba mwaka 2022/2023 kwamba ndio ataweka kwenye mpango.

Je, Wizara haioni umuhimu wa kutafakari upya jambo hili kulinganisha na umuhimu wa Mkoa wa Singida kwa sasa kwenye bajeti ya mwaka huu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mkoa wa Singida kwenye miundombinu ya barabara bado kuna changamoto sana. Je, Wizara ina mpago gani wa kuhakikisha kwamba inaunganisha Mkoa wa Singida kwa barabara za lami ili kuhakikisha kwamba wakulima wa alizeti na vitunguu wanafikiwa mpaka kwenye vijiji vyao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, ahsante na naomba nijibu mswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge Nusrat kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nifanye marekebisho huu mwaka unasomeka 2021/2022; maana yake kuanzia Julai tathmini inafanyika tuweze kupata gharama ili tulipishe eneo la kipande cha reli ambacho kimetajwa.

Sehemu ya pili; Mheshimiwa Mbunge amesema kuunganisha barabara hizi za lami kwenye eneo lake Mkoa wake wa Singida, ni kweli kwamba tunao utaratibu mzuri wa kila Mkoa, kwa maana Meneja wa TANROADS Mkoa anapaswa kuratibu zoezi la barabara katika Mkoa wake husika. Sasa tupokee hoja yako kama kuna eneo ambalo halipitiki kabisa kwa sasa, nielekeze Meneja wa TANROADS wa Mkoa wa Singida afanyie kazi kama kuna sehemu ya kuchukua dharura tufanye hivyo ili kufanya maboresho kwa wakulima wa alizeti, vitunguu na maeneo mengine wapate huduma nzuri ya usafiri, ahsante.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri kuhusiana na hatua mbalimbali ambazo, tayari wameshaanza kuzichukua kwa kuona umuhimu wa kufanya mapitio ya mitaala yetu ya elimu.

Mheshimiwa Spika, lakini naomba nikufahamu kwa sababu kimsingi wameshafanya makongamano kadhaa ya wadau na marafiki wa elimu kwa ajili ya kukusanya maoni. Lakini wamepitia elimu ya awali, msingi na sekondari kimsingi vyuo na vyuo vikuu bado. Kwa hiyo, niulize sasa Wizara ama Serikali ina mpango gani wa kutuletea pia kufanya mapitio ya kozi ambazo zinatolewa kwenye vyuo vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu, kuna maoni ya watanzania wametoa mbalimbali kuna masuala ya kilimo, kuna masuala ya ujasiriamali pamoja na stadi za kimaisha na mambo mengine mengi yote yamejadiliwa. Lakini vyuo na vyuo vikuu ambavyo ndio kimsingi vinatoa watu ambao ndio watenda kazi kwenye nchi. Ni lini sasa Serikali italeta kufanya marekebisho pia ya mtaala na masuala ya kozi ambazo zinatolewa kwenye vyuo hivyo. Ahsante. (Makofi)
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nitoe ufafanuzi na kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat Hanje. Utaratibu wa vyuo vya kati na vyuo vya elimu ya juu wana taratibu zao za kuanzisha mitaala.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano katika vyuo vikuu seneti ndio chombo kikuu ambacho kina mamlaka ya kuangalia mitaala katika vyuo vikuu na vyuo vya kati vina nyanja tofauti, vyuo vya kilimo viko chini ya Wizara ya Kilimo, vyuo vya utalii viko chini ya Wizara ya Utalii, vyuo vya afya viko chini ya Wizara ya Afya na wote wana taratibu zao. Wizara husika ndio zinakuwa na mabaraza kwa mfano Wizara ya Afya, Baraza la Madaktari ndio linaangalia mitaala ya madaktari, Baraza la Wauguzi linaangalia mitaala ya manesi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kiasi fulani hili jambo labda nilipokee kama Serikali tuangalie namna ya kuliratibu. Kwa sababu, kwa sasa hivi sio vyuo vyote vya kati vinasimamiwa moja kwa moja na Wizara ya Elimu na wala Wizara haihusiki moja kwa moja na kuidhinisha mitaala. Ila imekasimisha mamlaka kwa seneti za vyuo vikuu pamoja na vyombo ambavyo vimewekwa, kwa mujibu wa sheria katika vyuo husika kushughulika na mitaala.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tu tuangalie namna gani labda kwa kuongezea kabla sijamalizia. Ni kwamba nako pia tumeelekeza wafanye mapitio ya mitaala na katika huu Mradi wa Higher Education tuna fedha ambazo tumetenga, kwa ajili ya kufanya mapitio makubwa na ndio maana mradi unaitwa mageuzi ya kiuchumi na yanajikita katika kuimarisha uchumi wa viwanda. Kwa hiyo, mapitio ya mitaala yanafanyika kwa hiyo tutaangalia utaratibu mzuri wa kuratibu tupate mapitio yanayofanyika. Ili tuweze kuja kutoa taarifa kwenye chombo muhimu, ambacho ndio kinasimamia sheria na kusimamia utendaji wa shughuli za Serikali. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante kimsingi suala la uraia pacha na Diasporas limefanyiwa mjadala mpana sana kwa muda mrefu sana. Sasa kwa sababu Serikali na niipongeze kwa kufanya jitihada ya kutambua mchango wa Diasporas na tunaamini kwamba wakifungua wakipewa hati maalum ama uraia pacha pamoja na kwamba kuna restriction ya katiba hawaoni sana ifike hatua lifike tamati suala la kujadili masuala la uraia pacha na Diaspora tulifanyie kazi sasa kwa sababu tumeona impact yake ni kubwa zaidi kwa sababu Serikali yenyewe ndiyo imetuambia sasa hiyo ni ndogo tu tukifungua tutapata faida nyingi Zaidi.

Mheshimiwa Spika, sasa Serikali haioni kama imefika hatua tulifanye sasa kwa vitendo suala la kutambua kuwapa hadhi maalum ama kutambua mchango wa Diaspora kiuhalali? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nusrat Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua na kuthamini mchango mkubwa wa watanzania wanaoishi nje ya Nchi na kama nilivyojibu hapo awali ni kwamba tayari saa hivi Serikali inafanya tafiti ya kuangalia vipi tunaweza tukaangalia uwezekano wa watanzania hawa kupewa hadhi maalum. Hivyo namuomba Mheshimiwa Mbunge atupe muda kidogo ili kumaliza tafiti na taratibu hizo ahsante sana.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nami nitauliza maswali pamoja na majibu hayo, nitauliza maswali mawili ya nyongeza kutokana na majibu ya Mheshimiwa Waziri, pamoja na kwamba amezungumiza suala la Kanuni za Magereza ambazo zinataka watoto watengwe tofauti na watu wazima wanapokuwepo Mahabusu. Mlundikano wa Mahabusu kwenye magereza zetu hauruhusu jambo hilo ni kwa nini sasa Serikali isiongeze au isipeleke Maafisa Ustawi wa Jamii ambao watakuwa wanashughulika na Watoto wanapokuwa kule kwa sababu ni vigumu sana ku-monitor. Kwa mfano, Gereza la Segerea kuna mahabusu si chini ya mia moja watoto na Maafisa wapo wawili tu ME na KE. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili; kwa nini sasa Serikali isipitie upya kujua idadi ya watoto ambao wana kesi kwenye Mahakama zetu na kwenye Mahabusu zetu yaani kwa maana ya Magereza ili sasa ile sheria kwa jinsi ilivyowekwa na ni nzuri, lakini utekelezaji wake ni mgumu ni kwa nini sasa wasipitie upya ili kuhakikisha kwamba watoto hawa wanasaidiwa kwa sababu hali za watoto wetu kwenye Magereza zetu ni mbaya mno. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat Shaaban Hanje Mbunge wa Viti Maalum, nayo nayajibu kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, kama Mheshimiwa atarejea kwenye jibu langu la msingi atagundua kwamba kuna sehemu nimesema kutakuwa kuna Maafisa wa Ustawi ambao watakuwepo maalum katika magereza kwa ajili ya kusimamia haki na maslahi na kuwalinda watoto hawa. Kwa hiyo, kama changamoto ni Maafisa hawa kuwa kidogo basi nimhakikishie tutajitahidi Serikali kupitia Jeshi la Magereza ili kuona kwamba tunaongeza Maafisa hawa ili watoto wetu waweze kupata huduma nzuri za kuweza kusaidiwa na Maafisa hawa pamoja na kwamba kuna nafasi nyingine ya kushughulikiwa na wazee wao na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine Mheshimiwa amegusia suala la kwa nini isipitiwe upya sheria au tuone namna, nimwambie kwamba sheria hii kwamba ipo vizuri, lakini kwa kuwa na yeye ameshauri tuipitie upya basi tutakaa tutaipitia sheria hii ili kama kutakuwa kuna mapungufu basi tutajua namna ya kuifanyia marekebisho.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge pia aliuliza umuhimu wa kujua idadi ya kesi za watoto. Kesi zote zinazokwenda Mahakamani zinasajiliwa kwa namba, kwa hiyo kama atauliza swali mahsusi kwa Mahakama maalumu au kwa Gereza maalum idadi hiyo itapatikana kwa namba na kwa majina ya wahusika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili; Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009 inaweka misingi ya kulinda maslahi ya mtoto. Kwa hiyo, kwa mtu aliyechini ya kizuizi cha magereza anapopelekwa mahakamani kama hapati huduma inayostahili akiwa magereza anayohaki ya kutoa hiyo hoja kwa Hakimu ambapo shauri hilo lipo mbele yake na maelezo ya kisheria kwenda kwa wanaosimamia hizo selo yakatolewa. Nninakushukuru. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza kwenye Wizara ya Viwanda na Biashara. Kwa kuwa mifuko hii imeonekana haina tija ya kutosha kwa sababu zinatolewa fedha taslim, ni kwa nini sasa Serikali isije na mpango mbadala wa kutoa facilities (vitendea kazi) na kuwawezesha vijana badala ya kuwapa fedha taslimu ambazo pia zimekuwa hazirudi kwenye Serikali lakini pia haziwafikii vijana wa kutosha. Ni kwa nini sasa wasilete utaratibu wa kuwapa vitendea kazi ili waweze kufanya kazi na tuone kitu kinafanyika?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nusrat Hanje Mbunge kama ifuatavyo. Ni kweli kumekuwa na changamoto nyingi kama ambavyo nimesema kwa maana ya kutokuwa na fedha za kutosha mahitaji ya wananchi ambao wanataka kukopeshwa au kupata fedha kutoka kwenye mifuko hii. Lakini lengo la Serikali ni lile lile kuimarisha na kuwasaidia kwa ukaribu zaidi wananchi katika kuwawezesha.

Mheshimiwa Spika, moja ya mifuko ambayo inatoa mikopo hii ni NEDF kupitia SIDO pia tumekuwa tukiwapa ujuzi lakini na wengine vitendea kazi. Lakini sasa baada ya kuwa na lengo hili la kuona namna gani kuunganisha mifuko hii naamini taarifa hiyo ndiyo itakuja na utafiti rasmi wa namna gani ya kuboresha ikiwemo kama ni kuwasaidia vitendea kazi hasa vijana ambao wanakuwa wanakopa fedha hizo au wengine na kutokutimisha lengo la mikopo hiyo nakushukuru.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa lengo ni kuboresha elimu yetu nchini. Ni kwa nini sasa Serikali isipandishe hadhi Shule ya Sekondari Sepuka ambayo ipo Jimbo la Singida Magharibi ambayo kwa sasa ndiyo shule kongwe kuliko shule zote katika Tarafa ya Sepuka ambayo imebeba nusu ya Kata za Jimbo la Singida Magharibi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kwamba ombi la Mheshimiwa Mbunge ni Shule ya Sepuka sijajua ni sekondari ama msingi, lakini naamini ni Sekondari kwenda Kidato cha Tano na cha Sita ambao wanataka tupandishe hadhi na kuwa kidato cha tano na cha sita kwa sababu inapokea wanafunzi kutoka maeneo mbalimbali. Moja ya mpango wa Serikali ni kufanya upanuzi wa shule za sekondari za Kata 100 katika mwaka 2022 ili tuongeze wigo wa kuongeza wanafunzi wa kwenda kujiunga na kidato cha tano na cha sita.

Mheshimiwa Spika, naamini kama lipo katika mpango, basi maana yake tutalifanyia kazi katika mwaka huu fedha 2022/2023, lakini kama halipo maana yake tutalifanyia kazi katika mwaka wa fedha unaokuja 2023/2024. Kwa hiyo, nitayapitia ili niweze kujiridhisha nione kama halipo katika mwaka huu, kama litakuwepo mwakani maana yake tutaliingiza, kwa hiyo ni hilo tu. Ahsante.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu hayo naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

(a) Je, wanafunzi wanaosoma Chuo cha Diplomasia wanafanya wapi mafunzo kwa vitendo ili sasa lengo la kuanzisha Chuo cha Diplomasia liwe limetimia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Serikali imekubali kwamba yaliyokuwa malengo ya msingi kuanzia Chuo cha Diplomasia kwa sasa yamebadilika kutokana na mahitaji ya nchi na pia kutokana na masuala mengine ambayo Serikali wanajua kwanini walipadilisha.

(b) Je, ni kwanini sasa Serikali isione haja ya kupitia upya mfumo wa utoaji elimu kwenye chuo hiki ambacho lengo lake lilikuwa ni kutoa viongozi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwasababu hata wanaotolewa katika chuo hiki wahitimu wengi hawatumiwi kama ambavyo lengo la kuanzisha chuo hicho lilivyokuwa. Sasa ni kwanini wasipitie upya ili wanaohitimu katika chuo hicho wawe na tija kwa taifa na Serikali ifikie malengo yake inayosema kwamba inazalisha viongozi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat Shaaban Hanje, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza ni kuhusu mafunzo kwa vitendo. Chuo hiki kimsingi kinapowatoa wale wanafunzi wanakwenda kwenye maeneo mbalimbali kwa ajili ya field zao, moja ya eneo ambalo wanapewa nafasi ni Wizara ya Mambo ya Nje yenyewe ambako wanafunzi wachache huwa wanapewa nafasi kutokana na ukweli wa uwezo wa Wizara yenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini maeneo mengine ni kwenye taasisi mbalimbali zenye sura ya Kimataifa, vile vile kule kwenye NGO na maeneo ambayo utendaji wake upo katika sura ya kimataifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la tija, ni kwamba chuo hiki kina tija kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba kwa sasa kimezalisha wanadiplomasia wengi sana ambao wanatumika katika maeneo mbalimbali. Na ukizingatia kwamba tuna hiki chuo kiliboreshwa na kufanyiwa maboresho ya uhakika kimekuwa na sura ya chuo kikuu, na sasa hivi kinatoa hadi shahada ya juu, kama nilivyoieleza hapo, wanatoa hadi masters pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninachoweza kusema ni kwamba mafunzo wka vitendo wanapatiwa lakini vile vile tija inaonekana kwenye Nyanja za kimataifa na wasomi wengi sana tumekuwa tukiwatumia katika maeneo mbalimbali, ahsante.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ni kwa nini sasa Serikali isione haja ya kushirikisha taasisi binafsi za fedha ili ziweze kutanua wigo wa kupata fedha zaidi kwa ajili ya kutoa mikopo na yenyewe ibaki ku-regulate tu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge hivi sasa tunaendelea na mazungumzo na taasisi mbalimbali za fedha, lakini katika bajeti yetu ya mwaka 2022/2023 tayari wenzetu wa NMB wameweza kuongeza bajeti yetu ya mikopo kwa ajili ya vijana wetu wa elimu ya juu pamoja na elimu ya kati zaidi ya shilingi bilioni 200. Kwa hiyo kama Serikali tunalifanya hilo na tutaendelea kulifanya.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu ya Serikali kuhusiana na utayari wao kwenye suala la madini muhimu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tumeona thamani ya fedha kwenye ongezeko la asilimia 9.4 kwenye bajeti ya GST mwaka wa fedha huu unaoendelea ambapo mapato yame-shoot mpaka asilimia 141.
Ni kwa nini sasa Serikali isilete mkakati wa dharura kwa ajili ya ku-fund GST ili iweze kufanya tafiti za kisayansi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili; sasa hivi tunapozungumza GST imefikia wapi na Serikali imefikia wapi kwenye masuala ya critical minerals kwenye utafiti na uchimbaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat Hanje, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa swali lake la kwanza; ili kuboresha teknolojia ya kutafuta madini na hasa tafiti ya madini haya ya kisasa, GST kupitia Wizara yetu ya Madini imeanza mkakati rasmi wa kuanzisha mashirikiano na wadau mbalimbali wa ndani na nje na kuandika maandiko mahsusi ambayo yatatusaidia kupata fedha za kuwekeza katika utafiti wa madini ya kimkakati. Tuna Kampuni ya Noble Helium ambayo inashirikiana na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na GST, tuna Kampuni ya Rocket Tanzania Limited.

Mheshimiwa Spika, kwa swali lake la pili kuhusu hatua ambazo tumeshafikia katika kutafiti na kuzalisha madini ya kimkakati; ni kwamba sisi kupitia Tume yetu ya Madini kama Wizara, tayari tunatoa leseni za utafiti wa madini ya kimkakati kwa ajili ya utafutaji wa madini na uchimbaji wa madini. Na Serikali imekuwa na ubia na baadhi ya kampuni hizo na kwa ruhusa yako naomba nitaje chache.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Mkoa wa Lindi, tuna kampuni inayoitwa Lindi Jumbo Limited wenye leseni ya uchimbaji wa kati na wanaendelea na utafiti na sasa hivi wamefikia hatua ya kuendeleza ujenzi wa eneo la mradi.

Mheshimiwa Spika, hapo hapo Mkoani Lindi tuna Kampuni inaitwa Ngwena Tanzania Limited, wana leseni za utafiti wa madini ya kinywe na sasa hivi wako katika hatua ya uthamini kwa ajili ya ulipaji wa fidia. Na pia wale wa Jumbo nao wanafanya utafiti wa madini ya kinywe.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa hizi chache nipende tu kumhakikishia kwamba sasa hivi Tanzania imeamka na wawekezaji wakubwa wa ndani na nje wanajihusisha na utafutaji wa madini ya kimkakati. Ahsante sana.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi nami niulize maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri alisema kuna ngazi mbalimbali ambazo zinashughulika na hayo, lakini wanaonaje sasa wakati huu wasianzishe jeshi la jamii kama lilivyo Jeshi USU kwa upande wa Maliasili, kwa ajili ya kuhakikisha kwamba jamii inalinda watoto wetu dhidi ya ukatili pamoja na wanawake? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Ni kwa nini sasa Serikali isiende kwenye shule zetu kwa ajili ya kuanzisha klabu za stadi za maisha na majukwaa ya stadi za maisha kwa ajili ya kuwajengea watoto wetu uwezo wa kujilinda wenyewe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Nusrat kama ifuatavyo. Swali lake la kwanza kuhusu Jeshi Jamii; Wizara imejipanga na mpango kazi wa Taifa wa kutokomeza ukatili dhidi ya wanawake na watoto (MTAKUWWA) ili kuhakikisha kwamba wanakuwa na usalama. Mpango huu umejielekeza kuanzia ngazi ya vijiji hadi mkoa na kuhusisha vyombo vya ulinzi na usalama katika kila eneo.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu jukwaa la watoto; Wizara yetu ina majukwaa ya watoto ambayo yanahimiza ulinzi na usalama. Pia yapo mabaraza na clubs za watoto kuanzia shule za msingi, sekondari hadi Vyuo. Klabu hizi zinawafunza watoto na kuwaelimisha waweze kujitambua, kujielewa, kujiamini na kujieleza wakati wowote katika kujikinga na ukatili dhidi ya watoto. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali inaonesha kusua sua kwa ufanisi wa mifuko hii, na ni tangu Bunge la Kumi na Moja tumekuwa tukizunngumza kuhusu kuunganisha mifuko ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, mifuko ya ujasiriamali.

Je, ipi kauli ya Serikali, kwa kutumia muda mrefu kiasi hiki, wanasemaje kuhusiana na kuharakisha mchakato kwa sababu ni fedha za Serikali zinazoenda huko?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema Serikali tumeshaanza na tumeshafika hatua ya mwisho. Naamini katika mwaka wa fedha ujao kutakuwa na taarifa kamili ya nini mfuko huu pia utapunguzwa. Kwa sababu tuna mifuko zaidi ya 72 lakini kati ya hiyo tisa ni ya sekta binafsi, 63 ndiyo ya Serikali. Kwa hiyo, tunaanza kwanza hii ya Serikali 63 tuone namna gani tunapunguza ili iweze kuwa na tija kama ambavyo Bunge lako limeendelea kushauri, nakushukuru.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini ni kweli kwamba GST ina uwezo mdogo sana wa kiteknolojia kulingana na maendeleo makubwa teknolojia duniani. Sasa Serikali ina mkakati gani wa dharura kuiokoa GST kiteknolojia kwa sababu uwezo wake ni mdogo sana kiasi kwamba hata minerals zile certified mineral chemicals ambazo zinasaidia kuthibitisha ubora wa sampuli haina uwezo huo.

Je, Serikali ina mkakati gani wa dharura kuokoa GST?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia swali la pili, mpaka sasa Serikali imetoa leseni ngapi ambazo ziko kazini sasa hivi za madini ya kimkakati ambayo tunategemea GST itusaidie kuyabaini?
WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, la uwezo mdogo wa GST wa kufanya utafiti, naomba nimuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba GST kama taasisi ya utafiti itashirikiana na sekta binafsi. Kama nilivyoeleza kwenye jibu langu la msingi, tunazo kampuni mbalimbli ambazo ziko ndani na nje ya nchi ambazo zinafanya kazi ya utafiti kusaidia Taifa letu. Hivi sasa tumeshazungumza na kampuni mbalimbali kubwa duniani kwa akjili ya kufanya utafiti huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kwamba tumetoa leseni ngapi; tumeshatoa leseni kadhaa, naweza nisijue kwa idadi, lakini madini yote ya mkakati anayoyafahami iwe nickel, iwe graphite iwe rare earth, iwe helium na kadhalika; yote haya kuna leseni na makampuni mbalimbali yanaendelea na utafiti hapa nchini. Kwa hiyo naomba nimuhakikishie, demand ya madini mkakati ambayo anahitaji sasa hivi ni jambo ambalo halikuwa la muda mrefu, na wawekezaji wengi walikuwa busy na madini mengine. Sasa hivi muelekeo mkubwa ni kufanya haya madini mkakati na kampuni nyingi zipo zinafanya hizi kazi. Baada ya muda ataona migodi mingi inajengwa kama ambavyo kabanga inajengwa.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mpaka sasa hivi Blueprint inaonekana ni document ya Serikali na watu hawaimiliki. Ni yapi sasa mafanikio mpaka sasa hivi tangu tufanye reforms kwenye blueprint, Serikali imefanikiwa nini kiuchumi ili at least sasa tuanze kuona value for money na hayo marekebisho ambayo tumeyafanya?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, napenda kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafanikio yako mengi kama ambavyo nimesema. Moja ya maeneo ambayo yalikuwa yana angaliwa ni zile Sheria zilizoanishwa kwenye mpango ule au kwenye document hiyo, ambayo kimsingi iko public na kila mtu anaweza ku-access na sio ya Serikali. Ni zaidi ya sheria na kanuni 88, ambazo katika hizo sheria na kanuni 40 zimeklwisha ratibiwa na kufanyiwa marekebisho. Hata hivyo katika mambo ambayo yalikuwa yameibuliwa ni mwingiliano kati ya taasisi za Serikali moja wapo mi TBS na TMDA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengi yameweza kurekebishwa; lakini moja ni uanzishwaji wa mifumo ambayo ilikuwa na changamoto kwa wafanyabiashara kwa mfano Wafanyabiashara wakitaka kulipia ilikuwa ni changamoto kubwa. Kwa hiyo mifumo 42 imerekebishwa, moja wapo tunaona ni hii GEPG ambayo ni malipo ya Serikali na yameboreshwa na hii imepunguza sana manung’uniko kwa wananchi kupanga foleni Kwenda kulipa katika taasisi mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi katika utekelezaji huo ndiyo tunaona kwamba tumeanzisha idara hizi na vitengo ambavyo vitakuwa mahususi sasa kusikiliza na kutatua kero za wafanyabiashara maeneo yote. Kuanzia wizarani kuna kitengo hicho lakini pia tunaenda kwenye halmashauri tunaweka kitengo ili kuhakikisha tunapunguza manung’uniko na changamoto ambazo wafanyabiashara wa Tanzania walikuwa wanakutana nazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo taarifa hizo au kitabu hicho au document hiyo ni ya wananchi wote. Kwa hiyo popote utakapotaka unaipata na taarifa hizi kama ulivyosema kama ukihitaji tutaileta hapa Bungeni; lakini Kamati yako ya Viwanda, Biashara na Mazingira wamekwisha ipata na wameijadili na mambo mengi yanaendelea kurekebishwa.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu hayo, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa mpaka sasa Serikali inatoa mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vitatu ambavyo ni vya Serikali MUST, DIT na Arusha Technical College ambao ni 2,435 pekee. Ni nini sasa maandalizi ya msingi ambayo Serikali imeshafanya mpaka sasa kuhakikisha kwamba inatoa mikopo kwa wanafunzi wote wa vyuo vya kati ikiwepo wa private? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa nini sasa Serikali isione namna ambavyo inaweza kushirikisha Sekta Binafsi ikiwemo benki ili na wao waweze kushiriki katika kutoa mikopo kwa vyuo vya kati kwa riba nafuu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la kwanza anataka kufahamu maandalizi au mkakati wa Serikali kwa upande wa utoaji mikopo katika elimu ya kati. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, eneo la kwanza kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi, tumeendelea au tutaendelea kupeleka ruzuku kwenye vyuo hivi vya elimu ya kati kwa lengo la kuhakikisha kwamba kwanza tunaenda kushusha zile gharama za uendeshaji au ile gharama ya ada ambayo wanafunzi wanalipa.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, tulilofanya kama Serikali, Serikali tayari imeshafanya mabadiliko ya Sheria ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu ili kuhakikisha sasa tunaenda vilevile ku-cover elimu ya kati. Kwa hiyo ile Sheria ya Bodi ya Mikopo nayo tayari tumeshaifanyia marekebisho.

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu, Serikali inafanya mapitio ya uwezo wa Bodi ya Mikopo namna gani inaweza kuratibu utoaji wa mikopo katika vyuo hivi vya kati.

Mheshimiwa Spika, eneo la nne kama mkakati Wizara sasa inafanya tathmini ya fani gani ambazo tutaanza nazo kwa ajili ya utoaji wa mikopo katika eneo hili la elimu ya kati.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili, anataka kujua mkakati wa Serikali kuhususha Sekta Binafsi, tayari tumeshaanza majadiliano na Sekta Binafsi ikiwemo mabenki na naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari Benki ya NMB imetoa bilioni 200 kwa ajili ya mikopo hii ya Elimu ya Juu pamoja na kati na tunaendelea na juhudi hizo na wadau wengi wameonyesha nia ya kuunga mkono juhudi za Serikali.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na utayari wa Serikali kufanya marekebisho ya Sheria ya Ndoa lakini bado kuna Sheria za Kimila kandamizi kwenye mirathi. Je, ni kwa nini sasa Serikali isione haja ya kupitia upya Sheria za Kimila ili kuondoa ukatili wa kijinsia na ukandamizaji wa wanawake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kunipa nafasi nijibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Nusrat, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni sahihi kwamba sheria zetu za kimila, tuna sheria tatu za mirathi, tuna ya kidini Sheria ya Kiislamu Sheria ya Kimila na Indian Succession Act. Hizi sheria zote zimekuwa zikizungumzia jinsi gani watu wananweza kupata haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa sheria ambazo tumezisema katika Bunge hili kwamba tunazifanyia marekebisho ni pamoja na sheria hizi za mirathi za kimila ili Watanzania wote wapate haki zao. Kwa sababu katika sheria ambayo Mheshimiwa Mbunge ame-refer wanawake wengi hawapati haki zao, wanakuwa katika marriage lakini watoto wanapewa mali wakati wale akina mama ambao wamezaa wale watoto wanakosa haki. Kwa hiyo, tunakuja na marekebisho ya sheria hizo. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa kuwa tunakubaliana kwamba tuna tatizo kubwa la walimu wa sayansi nchini na pia tunatambua kuna maendeleo ya sayansi na teknolojia: Ni kwa nini Serikali isione namna ambavyo inaweza kutumia TEHAMA kwa ajili ya kuhakikisha kwamba inatatua tatizo la walimu kwa mwalimu mmoja kuweza kufundisha shule nyingi kwa wakati mmoja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa TEHAMA, na ndiyo maana Serikali hii ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ilitoa vishikwambi kwa walimu wote kama kianzio cha kwenda kwenye TEHAMA kwa walimu hawa. Kadiri siku zinavyokwenda, kuna shule ambazo zinajengwa za kimkakati kama shule ya mfano iliyokuwepo hapa Iyumbu Jijini Dodoma ambazo zitakuwa ni shule za TEHAMA kuweza kufundisha wanafunzi wetu wengi zaidi, na miaka inavyokwenda, tutazidi kuongeza kama Serikali.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa, tunafahamu kwamba, Serikali inatumia e-Government na TEHAMA kwa ajili ya kutoa huduma za kijamii kiserikali, lakini mara kadhaa wananchi wamekuwa wakikosa huduma kwenye ofisi za Serikali kwa sababu ya kwamba, mtandao uko chini. Ni kwa nini sasa Serikali isije na mkakati mahususi wa kuhakikisha kwamba, utolewaji wa huduma kwa kutumia e-Government na TEHAMA kwenye ofisi za Serikali unatengenezewa upekee na kuhakikisha kwamba, wananchi hawakosi huduma kwa sababu za mtandao uko chini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa, tumekuwa tunaona Serikali inafanya udhibiti wa mitandao, hususan katika kipindi cha uchaguzi, lakini pia tunafahamu kwamba, sasa hivi Serikali inachagiza uchumi wa kidijitali na wananchi wengi wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii kwa ajili ya kuhakikisha wanafanya shughuli zao za kiuchumi. Ni kwa nini sasa Serikali isione umuhimu wa kuhakikisha kwamba, majukwaa haya ya mitandaoni hayakosi mawasiliano, hususan kipindi ambacho Serikali inafanya udhibiti wa kasi hususan kipindi cha uchaguzi?
NAIBU WAZIRI WA WIZARA YA WIZARA YA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa
Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat Shaaban Hanje, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza kuhusu matumizi ya internet katika ofisi za Serikali. Serikali imewekeza katika miundombinu, Ujenzi wa Mkongo wa Taifa. Katika ujenzi huo tuna capacity mbalimbali, tuna kitu kinaitwa Synchronize Transport Module maana yake STMA. Hizi STM kuna 1, 2 na 3; 1, 2, 3, 4 maana yake kwamba, ni capacity na speed ambapo kwa mfano STM 1 ambayo ina MBPS 155 maana yake hiyo ni capacity yake, lakini kuna ya 491, kuna ya 2488, lakini sasa niombe na kuwashauri wataalam wa eGA na wataalam ambao wako katika Wizara mbalimbali, wafanye tathmini ya mahitaji halisi ili waweze kujua kwamba, wanaweza wakapata capacity ipi itakayoendana na traffic wakati wanapokuwa wanahudumia wananchi wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipengele cha pili cha udhibiti. Kuna Profesa mmoja anaitwa Tim Wu kutoka Colombia Law School alisema kwamba, ili ubunifu uendelee na ili tuwe na freedom ya access to information na ili business na innovation zizidi kukua ni lazima tusiweke restrictions katika aina gani ya mtandao tuweze ku-access na aina gani ya contents tuweze ku- access.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali yetu kupitia TCRA tumeweka utaratibu kwa watoa huduma kuhakikisha kwamba hakuna restriction ya aina ya content ambayo mwananchi anaweza kui-access.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ni bahati kubwa kuuliza swali la kwanza kabisa kwenye Wizara mpya ya Mipango na Uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Serikali imefanya utafiti gani mpya na upembuzi wa kina kufahamu fursa mpya za uwekezaji zinazoendana na sayansi na teknolojia? Kama imefanya hivyo, je ni kwa nini sasa Serikali isione umuhimu wa kuweka taarifa hizi zinazoendana na wakati kwenye tovuti za Wizara zinazotangaza masuala ya uwekezaji? Kwa sababu hata hao wawekezaji wanaangalia kwenye tovuti hizo. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nusrat Hanje, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Kituo cha Uwekezaji kila mwezi inatoa taarifa mpya ambayo inaonyesha fursa ambazo zimejitokeza. Pia inatoa taarifa kuhusu aina ya uwekezaji ambao umefanyika katika mwezi huo lakini tupokee ushauri wake kuhusu kuweka kwenye website ya Wizara. Nimtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba ndio kwanza ofisi hii imeanzishwa na tupo katika mchakato wa kuanzisha taasisi mbalimbali ikiwemo suala la website, ahsante. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri mno ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa sababu mradi wa HEET ume-fund vyuo vya umma pekee ambavyo viko 15 kati ya 47 vilivyopo nchini: Ni upi mkakati wa Serikali kuona namna wataweza kuviwezesha vyuo vya private ambavyo kimsingi ni vingi kwa idadi hii ili na vyenyewe viweze kufanya mapitio ya mtaala ili viendane na dira na mwelekeo wa Serikali?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kuna terms of reference zipi ambazo Serikali wameshavipatia vyuo vya private ambavyo waliamua kuanza wenyewe kufanya mapitio, ili sasa kuona namna gani bora tunaweza tukafungamanisha dira na mwelekeo wa Serikali kwenye elimu ambayo inatolewa katika mtaala wa vyuo vikuu nchini? Ahsante.
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Nusrat Hanje, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza pamoja na kwamba, fedha nyingi zaidi za Mradi wa Higher Education for Economic Transformation zimepelekwa katika vyuo vya umma, bado fedha zimetengwa vilevile kwa ajili ya sekta ya vyuo binafsi kwa mfano, kutoa scholarship, lakini na mafunzo ambayo yanaendeshwa kwa ajili ya kubadilisha mitaala yanachanganya vyuo vyote bila kujali kama ni binafsi ama vya umma.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa TOR; vyuo vyote, kama nilivyosema katika kujibu swali la msingi, vinatengeneza mitaala yao kwanza kwa kupitia kwenye seneti zao, baada ya kukamilisha ndio zinapelekwa kwenye Commission ya Elimu ya Juu kwa ajili ya kupata ithibati. Chuo kinapata kibali cha kuwa chuo kikuu kwa sababu, tunaamini seneti yao ina uwezo mkubwa wa kuidhinisha mitaala. Sasa sisi maelekezo yetu ni kwamba, sasa hivi tuanze kuongeza elimu ya mali na kuzingatia vipaumbele vya nchi, hilo tumeshazungumza na ma-vice chancellors wote wa vyuo vyote na wakati wa kupitisha kwenye ithibati kuna fursa ya sisi kuangalia ni kiasi gani wameji-align na muelekeo huo wa kitaifa.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini sasa Serikali itajenga barabara ya Singida – Sepuka – Ndago kwa kiwango cha lami ambayo kimsingi ni barabara muhimu sana kwa wananchi na wakazi wa Tarafa ya Sepuka, Jimbo la Singida Mashariki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja ya Singida – Sepuka – hadi Ndago ni barabara ambayo tunategemea muda wowote kusaini mkataba kwa ajili ya kuanza ujenzi kwani tayari taratibu zote za manunuzi zimeshakamilika. Kwa hiyo, kinachosubiriwa tu ni kuisaini ili ujenzi uanze kujenga barabara hiyo yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.(Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na kusuasua kwa utekelezaji wa bajeti kadri tunavyotenga kwenye Bunge hili kipindi cha bajeti, wakati mwingine kuchelewa kufika au kufika kwa asilimia ndogo. Sasa naomba kufahamu mkakati wa Serikali kutatua changamoto hii, kwa sababu tukitenga bajeti tunatarajia ifike kama tunavyotenga.

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Natamani kufahamu mpaka sasa hivi Serikali imechukua hatua gani kwa Watendaji ambao wamekuwa siyo waaminifu na wabadhilifu wa mali za umma hususan bajeti kadri tunavyotenga badala ya kusubiri taarifa ya CAG pamoja na Mwenge? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat Hanje, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutoa fedha kama zilivyotengwa katika bajeti kadri ya fedha zinavyopatikana. Kwa kuwa, mfumo wetu wa bajeti ni cash budget, pesa zitakusanywa ili ziweze kutumika katika bajeti, hivyo Serikali itaendele kukusanya na kuongeza uwezo wa ukusanyaji wa mapato ili tuweze kutekeleza bajeti kama ilivyopangwa.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili. Serikali imechukua hatua mbalimbali kwa wale watumishi ambao siyo waadilifu. Hatua hizo ni pamoja na kuwafikisha Mahakamani, wako wale ambao wamefungwa sasa, wako ambao wamesimamishwa kazi na wako ambao wamefukuzwa kazi. Ahsante. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu hayo wafungwa na mahabusu wamekuwa wakifanyiwa ukaguzi hadharani kwa kuvua nguo zote bila kujali umri wao; na kwa uzoefu wangu mimi, upo uwezekano wa kuwakagua kwa kuwatenganisha lakini kuweka chumba maalum, lakini Serikali imekuwa haifanyi hivyo; pamoja na kwamba Serikali imenunua scanner 12 kwa ajili ya kufanya ukaguzi: Ni kwa nini sasa Serikali isione haja ya kutenga chumba maalum kwa ajili ya kuwakagua na kuwatenganisha ili kulinda staha na haki za binadamu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: mavazi ya wafungwa yamechakaa mno jambo ambalo linasababisha wafungwa wanawake warithi mpaka nguo za ndani za wafungwa wenzao ambao walimaliza muda wao, jambo ambalo kwa kweli siyo sawa: Ni kwa nini sasa Serikali isione haja kwanza ya kuondoa utaratibu huo na pia kupeleka mavazi kwa ajili ya wafungwa, pamoja na magodoro, mablanketi na neti?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mbunge lakini swali letu la msingi lilikuwa linazungumzia kukarabati magereza sasa imeibuka hili la mavazi na kukaguliwa hadharani. Lakini nadhani tupokee katika ukarabati na ujenzi wa magereza yanayokuja tutazingatia umuhimu wa kuwatenganisha wafungwa wote wanaume na wanawake wakati ukaguzi unapofanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mavazi kuchakaa kama mlivyosikia wakati wa bajeti, bajeti yetu mwaka huu imeongezeka kiasi ambacho maeneo ambayo yalikuwa hayapati funding kama haya ya mavazi ya wafungwa yatapewa kipaumbele ili waweze kupata mavazi yanayowastiri nakuleta staha kwa jumuiya hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru; ni lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji vya Jimbo la Singida Magharibi ikiwemo Kintataa, Irisia na Mwasutianga? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mbunge wa Viti Maalum Singida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kuna baadhi ya vijiji ambavyo havikuwa vimefikiwa na miundombinu ya umeme lakini Mradi Kabambe wa Upelekaji wa Umeme Vijijini, Mzunguko wa Tatu, Awamu ya Pili, utakamilisha vijiji vyote kufikia Desemba mwaka huu kwa mikataba tuliyokuwa nayo. Kwa hiyo na vijiji alivyovitaja Mheshimiwa vimo katika mpango huo na vitapelekewa umeme.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa tunafahamu wote kama Taifa hatuna Sera ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu lakini pia Sheria ya Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH) imepitwa na wakati.

Je, Maonesho ya kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu MAKISATU yanatekelezwa kwa sera ipi?

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na Wizara ya Habari, Mawasiliano ya Habari na Teknolojia ya Habari yote yana masuala ya teknolojia jambo ambalo linasababisha tushindwe kuelewa nani hasa mhusika wa masuala ya teknolojia kwenye Taifa letu. Je, Wizara ipo tayari sasa kuanza kuishauri Serikali kwa vielelezo hatua kwa hatua waanzishe Wizara mpya ambayo itashughulika na masuala ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu; ukizingatia mabadiliko ya sayansi na teknolojia ulimwenguzi lakini mapinduzi ya nne ya viwanda kama ilivyo nchi za Kenya, Afrika Kusini na Rwanda? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat Shaaban Hanje kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Nusrat kwa ufuatiliaji wake wa karibu wa masuala ya sayansi, teknolojia na ubunifu, lakini kipekee nichukue fursa hii kuwapongeza Wabunge wote ambao waliweza kufika na kutembelea kwenye mashindo yetu ya MAKISATU ambayo yalianza tarehe 16 – 20 Mei, 2022 katika Uwanja wetu wa Jamhuri pale Dodoma.

Mheshimiwa Spika, naomba nimtuoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba dhana hii ya utekelezaji wa mashindano hayo ya MAKISATU ni msimamo au ufuatiliaji wa karibu wa Serikali kuhakikisha kwamba mashindano haya au ubunifu nchini unaweza kuimarishwa.

Mashindano haya yanatekelezwa kwa mujibu wa sera ya ubunifu ya mwaka 1996. Tunakiri kuna mapungufu machache kwenye sera hii, lakini ndio ambayo tunazingatia katika utekelezaji wa mashindano haya.

Mheshimiwa Spika, lakini kama nilivyozungumza katika kipindi kilichopita kwamba, sera hii tunakwenda kuifanyia maboresho makubwa, lakini naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kupitia mashindano haya tumeweza kuibua bunifu zaidi ya 1,785, lakini vilevile zaidi ya bunifu 200 zimeweza kuendelezwa na zaidi ya bunifu 26 zimeweza kuingia sokoni kuona namna gani Serikali inasimamia kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini katika swali lake la pili anazungumzia suala la Wizara ya Elimu pamoja na Wizara ya Habari kuwa na suala hili la teknolojia. Ni kweli, tunaomba tukiri kwamba, Wizara ya Habari na Wizara ya Elimu zote zina teknolojia ndani, lakini utekelezaji wa teknolojia hii unategemea na mawanda yale ambayo Wizara imepewa kupitia hati idhini ya uanzishwaji wa Wizara husika.

Mheshimiwa Spika, kwa vile ametoa ushauri namna gani sasa Serikali inaweza kutenganisha maeneo haya ya ubunifu na Wizara hizi; basi tubebe ushauri huo, twende tukaufanyie tathmini na tuweze kuufanyia kazi ili tuweze kuona namna gani tunaweza tukatekeleza.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa mpango wa REA kwa Mkoa wa Singida mpaka mwezi wa Saba wanatakiwa wawe wameunganisha vijiji 10 na umeme, lakini katika Wilaya ya Ikungi Majimbo ya Singida Magharibi na Mashariki vijiji saba vyote ni vya Jimbo la Singida Mashariki: -

Je, ni nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba wanaongeza idadi ya vijiji katika Jimbo la Singida Magharibi kutoka vitatu na kuendelea ili wananchi wapate huduma ya umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi hii tunayoitekeleza inalenga kupeleka huduma kwa wananchi. Kwa hiyo, kama kijiji kimepata umeme kwenye mradi mmoja, kwa mfano vijiji alivyovisema saba vimepata umeme kutoka kwenye mradi wa backborn wa Mradi wa msongo wa kilovolt 400 kwenda Namanga, then vimeshapata umeme. Vile vijiji vingine vyote vilivyobaki ndiyo vinaingizwa kwenye REA III round II. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hakuna kijiji hata kimoja kitakachobaki bila kupata umeme; kama hakipo kwenye REA III basi kitakuwa kipo kwenye mradi mwingine kwa ajili ya kpatiwa umeme. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuwa Kanda ya Kati hususani Mkoa wa Singida na Dodoma ni miongoni mwa mikoa ambayo ni ya kimkakati hususani kwenye zao la alizeti ukiwemo mkoa wa kwako Mheshimiwa Naibu Waziri.

Je, Serikali haioni haja ya kuhakikisha kwamba sasa tunapata Chuo cha Kilimo kwenye Kanda ya Kati kuhakikisha kwamba fedha zinazotengwa na Serikali zinakuwa na tija?
NAIBU WAZIRI KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mbunge wa Viti Maaalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vyuo vyetu vya kilimo vimegawanya katika kanda na Kanda ya Kati pia yenyewe inapata huduma kupitia vyuo hivi, lakini sambamba na hizo tunazo taasisi mbalimbali ambazo zinafanya kazi katika Mkoa wetu wa Dodoma pamoja na Singida ambazo lengo lake kuu ni kuhakikisha kwamba tunawajengea uwezo wakulima wetu kulima kilimo cha alizeti kwa tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ya kwamba tumezingatia sana ikolojia ya Dodoma na Singida na tumeweka nguvu ya kutosha kuhakikisha wakulima wetu wanapata elimu ya kutosha juu ya kilimo cha alizeti na mwisho wa siku tuondoe tatizo la upungufu wa mafuta ambalo tunalo hapa nchini.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ni lini Serikali itawapa wachimbaji wadogo eneo namba moja, Kata ya Mang’onyi, Jimbo la Singida Mashariki, ambao wameondolewa tangu mwaka 2015?
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo ambalo amelitaja Mheshimiwa Mbunge, nitakwenda kufanya ziara eneo hilo kwa sababu nina ziara katika eneo hilo. Pia, moja kati ya jukumu langu kubwa ni kwenda kuzungumza nao na hasa katika kuhakikisha kwamba tunaendelea kuwapatia maeneo wachimbaji wadogo kwa sababu, haya ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ya kwamba nitafika mwenyewe katika maeneo hayo na kuona namna ya kuweza kutoa utaratibu mzuri kama ambavyo tumefanya katika Mlima wa Sekenke na maeneo mengine ya Sekenke ambayo tulitoa leseni kwa ajili ya wachimbaji wadogo.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ni lini Serikali itawapa wachimbaji wadogo eneo namba moja, Kata ya Mang’onyi, Jimbo la Singida Mashariki, ambao wameondolewa tangu mwaka 2015?
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo ambalo amelitaja Mheshimiwa Mbunge, nitakwenda kufanya ziara eneo hilo kwa sababu nina ziara katika eneo hilo. Pia, moja kati ya jukumu langu kubwa ni kwenda kuzungumza nao na hasa katika kuhakikisha kwamba tunaendelea kuwapatia maeneo wachimbaji wadogo kwa sababu, haya ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ya kwamba nitafika mwenyewe katika maeneo hayo na kuona namna ya kuweza kutoa utaratibu mzuri kama ambavyo tumefanya katika Mlima wa Sekenke na maeneo mengine ya Sekenke ambayo tulitoa leseni kwa ajili ya wachimbaji wadogo.