Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Mwantumu Mzamili Zodo (27 total)

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo. Swali la kwanza; je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka watumishi wengi zaidi katika Mkoa wa Tanga, hasa ikizingatiwa kuwa Mkoa wa Tanga ndio mkoa wenye halmashauri nyingi zaidi nchini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; utoaji wa huduma za afya kwa vituo vya Serikali unakabiliwa na changamoto nyingi tukilinganisha na vituo binafsi. Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha huduma zinaboreshwa kwenye vituo vya Serikali ili kuongeza mapato ya Serikali? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ajira 12,476, Serikali inaenda kuelekeza kwenye maeneo kama aliyoyataja ndio kipaumbele kitakuwa, ukiangalia Mikoa kama Kigoma, Mtwara, Songwe na mingine ambayo kwa kweli ni mikubwa, lakini kuna upungufu mkubwa zaidi, itakuwa ndio priority ya Serikali. Kwa hiyo, tunachukua ushauri wake na utaenda kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile swali lake la pili ameuliza kwamba, alitumia neno mapato kwenye eneo upande wa Serikali. Ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba, ukiangalia kwenye vituo vyetu vya Serikali, hasa ukiangalia kwenye eneo la bima tu, ukiangalia kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge utaona. Tukichukua hata zahanati tu, tuliwahi kuchukua moja, kwenye zahanati tu ya kawaida ambayo wanalipwa bima kidogo ukilinganisha na mkoani, unakuta wanaingiza milioni 84 kwa mwaka, lakini Serikalini wanaingiza 420, lakini ukigawa kwa idadi ya watumishi Serikalini tulijua walikuwa 187 huku kwenye private walikuwa 17, lakini utakuta kwa mwaka wanaingiza shilingi 5,300,000/=, lakini huku serikalini tena mkoani wanaolipwa zaidi wanaingiza shilingi 2,000,000/=

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunafikiri kuna umuhimu wa kwenda kufanya kazi kuhakikisha productivity ya watu wetu inaongezeka. Tukiongeza kwenye eneo la productivity maana yake hata kuna mahali ambapo prpductivity ndio inasababisha ionekane kwamba kuna upungufu, lakini upungufu sio halisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile kuna eneo la watumishi; tutaenda kuchukua modal ya Wizara ya elimu. Wizara ya elimu wameshirikiana vizuri sana na private sector kwamba, private sector wana shule, lakini na Serikali ina shule, lakini wamekuwa wanashirikiana vizuri sana bila kuwepo anayenyonya upande huu. Hivyo, kwenye afya tutaenda kudhibiti hasa kwenye eneo la kwamba, unakuta kuna watumishi wakati wa kufanya kazi Serikalini wako eneo la private sector wakati wameajiriwa ndani ya Serikali. Nalo hilo litaenda kufanyiwa kazi kwa nguvu na litatusaidia sana kuweka mambo sawa. Ahsante. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kuuliza swali la moja la nyongeza. Kwa kuwa Mkoa wa Tanga unazungukwa na milima ya Usambara; na kwa kuwa milima hii inatiririsha maji mwaka mzima hasa wakati wa mvua. Je, Serikali haioni haja sasa ya kujenga mabwawa kuzunguka milima hiyo ili kuchochea kilimo cha umwagiliaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zodo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nikiri mbele ya Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba hatuwezi kutoka katika matatizo ya kilimo bila kuwekeza katika umwagiliaji. Huo ndiyo muelekeo wa Serikali na maelekezo ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Jambo la msingi ambalo tunalifanya sasa hivi kama Wizara kwanza ni kubadilisha modal ya Tume ya Umwagiliaji namna ambavyo inafanya kazi yake; mbili tunachokifanya kama Serikali ili kuweza ku-take advantage ya maeneo kama Milima ya Usambara lakini na maeneo mengine ya nchi yetu kwa ajili ya kujenga mabwawa katika bajeti mwaka kesho mtaona tumeweka chanzo kipya cha fedha kitakachokuwa cha Tume ya Umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tutawekeza kununua vifaa wenyewe ili Tume ya Umwagiliaji iwe na uwezo wa kupeleka vifaa kwa ajili ya kuchimba mabwawa na kujenga miradi ya umwagiliaji yenyewe kwa mfumo wa force account ili kupunguza gharama kubwa tunayotumia katika maeneo ambayo tunajenga skimu za umwagiliaji, kwa sababu gharama tunazotumia ni kubwa na hatuoni value for money. Kwa hiyo tunabadilisha mfumo tutatengeneza mfumo wa force account na tutanunua vifaa wenyewe ambavyo vitakuwa chini ya Tume ya Umwagiliaji kama tulivyofanya katika Skimu ya Pawaga na Ruaha ambako tumetumia vifaa vyetu wenyewe kurekebisha skimu hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niwaombe Waheshimiwa Wabunge, wasubiri bajeti ya Wizara, wataona mwelekeo wa Wizara katika Sekta ya Umwagiliaji.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. naomba niulize maswali mawilinya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Kijiji cha Jasini kwa Kata ya Moa na Mayomboni, Wilaya ya Mkinga wanapata usumbufu sana wa kukamatwa na askari wa Kenya na kwenda kushitakiwa Kenya na wakati mwingine mali zao kutaifishwa.

Je, ni lini sasa Serikali itahakikisha hali hii inakoma? Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili,...

SPIKA: Wanakamatwa kwa sababu gani?

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, wanaonekana wameingia Kenya, wakivua Kenya, ni eneo la bahari.

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, askari wa Kenya mara kadhaa wanaingia Jasini, hali ambayo ni hatari sana kwa nchi zetu hizi mbili.

Je, ni lini sasa Serikali itachukua hatua za haraka za kuhakikisha inaweka mipaka ili kuhakikisha Serikali ya Kenya na Tanzania zisije zikaingia kwenye migogoro? Asante nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA
MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nikiri ni kweli katika eneo la Jasini kwenye Kata ya Moa na Mayombo mara nyingi kumekuwa kukitokea ukamataji wa wananchi wa eneo hilo na hili pia liliwahi kutokea wakati pia tuko ziara kule, nilishafika mpaka Jasini.

Mheshimiwa Spika, lakini kinachotokea hapa ni kutokana na kwamba katika uimarishaji wa mpaka tumesema tunaimarisha kwanza maeneo ya nchi kavu kwa sababu majini katika kuweka maboya tayari mpaka nchi zote mbili ziridhie wapi maboya yawekwe, pamoja na kwamba, tunajua kuna ule mbali wa nautical miles 200 ambazo ziko kwetu, lakini hii haijaweza kufanyika kutokana na hali halisi ambayo kila ukitaka kuweka alama lazima mkubaliane wote.

Mheshimiwa Spika, lakini napenda kushukuru sana Balozi zetu, Ubalozi wetu wa Kenya pamoja na ule mdogo wa Mombasa. Nimshukuru sana Mheshimiwa Pindi Chana wakati yuko pale wametatua matatizo mengi kutokana na kesi hizi na sasa hivi balozi aliyeko pale, Consular Athumani Haji aliyeko Mombasa, ni juzi toka miezi sita iliyopita wameweza kutatua pia changamoto hiyo ya kuweza kukamatwa.

Mheshimiwa Spika, tatizo lililopo kutokuwekwa kwa maboya pale ni kutokana na makubaliano ya nchi mbili, lazima mkubaliane ndio muweke alama hizo. Bila kukubaliana hakuna nchi itakayoweza kuweka.

Mheshimiwa Spika, na kingine ambacho ni changamoto kule sasahivi wameanzisha sheria ya uvuvi ambayo chombo kinapoingia ziwani lazima ulipe dola 500 na ukikamatwa pale fine ni dola 300. Sasa mara nyingi wavuvi wetu wanakuwa hawana, lakini diplomasia imekuwa ikitumika wanajadiliana kati ya ubalozi n akule na watu wanatoka.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba katika swali lake la pili analosema ni lini hii itakomeshwa? Niwaombe tu muwe na Subira kwa sababu mchakato unaendelea katika suala zima la kuimarisha mipaka kama ambavyo nimesema katika jibu langu la msingi. Tukiimarisha mipaka hiyo ya nchi kavu ikikamilika suala la kuweka maboya ndilo limebaki kwa sababu tayari mpaka ulishabainishwa isipokuwa ni kuweka alama tu. Tutaweka mara tutakapokuwa tumekubaliana na wenzetu wa Kenya.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na vyama vya ushirika walivonavyo wavuvi lakini bado wavuvi wetu wana hali duni sana kiuchumi katika ukanda wetu wa Pwani. Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuwakwamua wavuvi wa pembezoni mwa Bahari ya Hindi kwa Mikoa ya Tanga, Dar es Salaam, Pwani, Lindi na Mtwara katika kushiriki kwenye uchumi wa blue.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantumu Zodo; kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan inao mkakati madhubuti au inayo mikakati madhubuti ya kuhakikisha inawasaidia wavuvi wa ukanda wa Pwani hasa kuendana na uchumi wa blue kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti tunayoitarajia ya mwaka 2021/2022, yako mambo ya msingi yatakayofanywa. La kwanza ni kuhakikisha tunaongeza uzalishaji katika miamba ya kuvutia Samaki, tutatengeneza katika Ukanda wote wa Pwani. Vile vile kama haitoshi tutahakikisha kwamba tunatengeneza vichanja vya kukaushia samaki, sababu moja kubwa inayowasumbua wavuvi ni upotevu wa mazao ambao wanayazalisha kwa kuoza na kwa kuharibika. Tunataka tuhakikishe kwamba samaki wote wanaozalishwa na wavuvi wa ukanda wa pwani hawaharibiki kwa sababu tutawaongezea thamani kwa kuwakausha, lakini vile vile tutakwenda kuongeza uzalishaji wa barafu na kuwa na cold rooms za kutosha katika ukanda mzima wa pwani, ili kuweza kuitumia vyema uchumi wa blue na kuongeza kipato cha mvuvi mmoja mmoja na hatimaye kuongeza kipato cha Serikali yetu. Naomba wavuvi watuunge mkono ili kuweza kufikia lengo hilo.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuwa kati ya vikwazo vya zao la alizeti ni upatikanaji mdogo kwenye Mbegu ya alizeti wa mafuta. Je, Serikali haioni haja sasa ya kuja na utafiti wa kina wa kuhakikisha tunapata mbegu bora zinazotoa mafuta kwa wingi ili kuchochea wasindikaji na wakulima wa zao hili la alizeti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza utafiti ni jambo ongoing tunaendelea kufanya utafiti lakini tumeshafanya utafiti wa kutambua aina gani za mbegu, tunazo mbegu aina mbili tuna high hybrid na tuna mbegu za OPV ambazo zinatumika kwenye uzalishaji wa alizeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachokifanya sasa hivi kama mlivyosikia kwenye jibu letu la msingi kwamba mwaka ujao wa fedha tutawekeza kiasi cha shilingi bilioni 10 kwa ajili ya kuzalisha mbegu za kutosha na malengo yetu ni kuzalisha metric tons 5,000 za Mbegu ambazo zitakwenda shambani ambazo zitatupatia metric tons 625,000 za mbegu za kwenda kukamuliwa ambazo zitatupatia metric tons 170,000 za mafuta kupunguza gape yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo suala la uzalishaji wa mbegu tayari tunashirikiana na sekta binafsi tutazalisha mbegu za kutosha katika mwaka ujao wa fedha na hii itatufanya kwamba tutakuwa tumepunguza 50% ya gape yetu, na mwaka unaofuatia nadhani kwamba tutakuwa tumemaliza. Kwasababu mahitaji yetu ni kupata mbegu za kwenda kiwandani kukamuliwa metric tons 1,226,000 ambazo zitatupatia wastani wa tani 400,000 za mafuta ili tuweze kupunguza kabisa tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na sisi tunaamini kwamba kutoka upande wa Serikali ni kwamba ndani ya miaka miwili au miaka miwili ya fedha tutakuwa tumelipunguza tatizo hili la mafuta kwa kiwango kikubwa na priority ni zao la Alizeti yakifuatiwa na mazao mengine, kwa hiyo, utafiti umeshafanyika na mwakani tunaanza uzalishaji. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa changamoto iliyopo Jimbo la Mtwara Mjini la kukosa Hospitali ya Wilaya linafanana sana na changamoto ya Jimbo la Kilindi: Je, ni lini sasa Serikali itapeleka pesa kujenga Hospitali ya Wilaya ya Kilindi ili kuokoa maisha ya akina mama wa Kilindi na Mkoa wa Tanga kwa ujumla? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwamba tunajenga Hospitali za Wilaya na Halmashauri katika Halmashauri zote ambazo hazina Hospitali hizo nchini kote. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika mwaka wa fedha ujao 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya Halmashauri zote ambazo hazina Hospitali za Halmashauri na fedha hizo zitapelekwa kwa ajili ya kuanza ujenzi wa hospitali hizo. Kwa hiyo, pamoja na Jimbo hili la Kilindi kwa maana ya Halmashauri ya Kilindi itatengewa fedha hizo kwa ajili ya ujenzi huo. Nakushukuru.
MHE. MWAMTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa moja ya changamoto ambazo zinasababisha kukosekana kwa watumishi kwenye sekta yetu ya afya ni pamoja na vifo, kustaafu na ujenzi wa vituo vya afya pamoja na zahanati. Na kwa kwakuwa bado tunaendelea na ujenzi wa vituo vya afya, je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kasi ya ujenzi wa vituo vya afya inaendana na kasi ya kuajiri watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa Serikali kwa kushirikiana na wadau mwaka 2017/2020 wameajiri watumishi 12,868 na wadau hao ni kama Benjamin Mkapa, AMREF na MDH. Je, ni upi mchango wa wadau hao katika ajira kwa sekta hii ya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA(MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantumu Mzamili Zodo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi ni kweli kwamba Serikali kwa kujali na kuthamini afya za wananchi imeendelea kujenga, kukarabati na kutanua vituo vya huduma za afya ili kusogeza huduma bora za afya kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuzingatia hilo, Serikali pia imeweka mkakati wa kuhakikisha kasi ya ujenzi wa vituo vya huduma za afya kote nchini inaendana na kasi ya ajira za watumishi ili kuviwezesha vituo hivyo kuanza kutoa huduma za afya katika vituo vyote vinavyojengwa na kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana katika kipindi cha mwaka 2017 hadi 2020 jumla ya watumishi takribani 12,868, wastani ya watumishi 4,200 kila mwaka wameajiriwa lakini hivi sasa Serikali inaendelea na ajira za watumishi 2,726 ambazo pia zitakwenda kupunguza upungufu wa watumishi katika vituo vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuhakikisha kwamba tunaajiri watumishi katika vituo hivyo, ahsante sana.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itajenga soko kuu la kuuzia samaki kwa Mkoa wetu wa Tanga na ni lini ujenzi utaanza?

Mheshimiwa Spika, swali namba mbili; ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha wavuvi wa maeneo ya pembezoni kwa maeneo ya Moa, Chongoleani, Kipumbwi na Mkoaja kuuza samaki wao kwenye soko la pamoja kukwepa wachuuzi kuwachuuza kwa bei ndogo? ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantumu Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Tanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika majibu ya msingi nimeeleza kwamba kwenye bajeti ya mwaka huu na kupitia ufadhili wa Shirika la IFAD, upo mpango wa Serikali wa kujenga masoko ya samaki. Na soko hili litajengwa katika Wilaya ya Pangani katika Kijiji cha Kipumbwi litakuwa ni soko zuri kubwa na la Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ameuliza je watauzia wapi wavuvi wa Chongeleani, Mkinga, Kipumbwi na kwingineko. Naomba nimhakikishie kwamba soko hili litakapokuwa tayari, wavuvi wa maeneo yote aliyoyataja watafaidika kwa ajili ya kuuza bidhaa zao, ahsante sana.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante; kwa kuwa Serikali inajenga Hospitali za Wilaya na Vituo vya Afya nchi nzima na kwa kuwa baadhi ya hospitali za Wilaya ni kongwe.

Je, Serikali haioni haja ya kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati hospitali za wilaya ikiwemo Hospitali ya Wilaya ya Pangani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantumu Zodo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumekuwa na Hospitali za Halmashauri kongwe ambazo zilijengwa miaka mingi. Zipo ambazo zimejengwa baada ya uhuru mapema, lakini zipo ambazo, zilijengwa hata kabla ya uhuru na kwa kweli miundombinu yake sasa ni chakavu. Lakini pia haziendani na kiwango cha hospitali za halmashauri ambazo sasa tunazihitaji. Kwa kutambua hilo Serikali tumefanya tathmini ya hospitali zote za Halmashauri kongwe na tumekwisha ziainisha. Tunaweka mpango, baada ya kukamilisha hospitali za Halmashauri 28, sasa tutakwenda kukarabati na kupanua hospitali zile kongwe ikiwepo Hospitali hii ya Pangani. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MWANTUM M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Mkomazi na Kata ya Mkalamo katika Jimbo la Korogwe Vijijini ni Kata ambazo zimepitiwa na Mto Ruvu lakini Kata hizo hazina maji kabisa. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha wanapeleka maji kwenye Kata hizo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, mradi mkubwa wa maji wa Mwanga, Same, Korogwe ni mradi ambao unasuasua. Je, Serikali ina mpango gani wa kwenda kukamilisha mradi huo wa maji ili kuondoa adha ya maji kwa wananchi wa Wilaya ya Korogwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zodo kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninapenda kumpongeza Mheshimiwa Zodo kwa ufuatiliaji mzuri kwani wakinamama lazima tusemeane na tuhakikishe tunawatua ndoo kichwani akinamama wote wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata hizi mbili alizoziongelea za Korogwe Vijijini zipo kwenye mpango, mradi huu ukishakamilika kwa awamu hii ambayo utekelezaji unaendelea awamu inayofuata Kata hizi Mbili pia zitapata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na mradi wa Mwanga, Same, Korogwe nimetoka huko hivi majuzi mradi ni mzuri sana na kazi zinaendelea. Mheshimiwa Mbunge pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote wanaotoka kwenye maeneo ya mradi huu baadhi tuliweza kuongozana mradi ni wa mafanikio makubwa sana na unaendelea kutekelezwa na utakuwa manufaa maeneo yote ambayo unapitia.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, bado Hospitali ya Wilaya ya Pangani inakabiliwa na changamoto ya uchakavu wa vifaa kama vile generator, mashine ya kufulia na ambulance: Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha inaondoa changamoto hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kupitia fedha za tozo, Kata ya Madanga tumepata shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya cha Kata ya Madanga: Je, ni upi mpango wa Serikali wa kuhakikisha inakwenda kukamilisha kituo hicho cha afya kwa haraka ili kuokoa maisha ya wananchi wa Kata ya Madanga, Kimang’a, Bushiri na Masaika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshemiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantumu Mzamilu Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Hospitali hii ya Pangani ni chakavu, sambamba na hilo, ina vifaa tiba na vifaa kama mashine za kufulia chakavu na pia gari la wagonjwa ni chakavu sana. Naomba kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Mwantumu Zodo kwa namna ambavyo anasemea wananchi wa Mkoa wa Tanga na Watanzania kwa ujumla, vile vile kwa namna ambavyo anashirikiana kwa karibu sana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Pangani, Mheshimiwa Jumaa Aweso, ambaye naye pia amekuwa anafuatilia sana kuhusiana na ujenzi na ukarabati wa Hospitali ya Halmashauri ya Pangani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika mwaka huu wa fedha, Serikali imetenga fedha kwa ajili kununua magari 407 na kati ya hayo 195 ni magari ya wagonjwa na Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Pangani itapata gari jipya la wagonjwa na kuondoa changamoto hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la vifaa tiba Serikali imeendelea kutenga fedha na tutahakikisha tunaenda kwa awamu kuboresha vifaa tiba katika hospitali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na kituo cha afya ambacho kimepata shilingi milioni 500, nimhakikishie kwamba kitakwenda kukamilishwa, kutafutiwa vifaa tiba na kuwekwa watumishi ili huduma za afya ziendelee kutolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Serikali katika bajeti yake ya mwaka 2021/2022 ilituahidi vichanja kwa wavuvi wa dagaa; na kwa kuwa hata kwenye bajeti yake ya 2022/2023, bado ametuahidi vichanja na Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kuna vichanja 80 watapeleka. Je, ni lini sasa Serikali itapeleka vichanja hivyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swal la nyongeza la Mheshimiwa Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kabisa mwaka huu niliousema wa fedha wa 2023/2024, baada ya kuwa tumekamilisha taratibu zote za kitaalam, ambazo ndiyo zilizokuwa zikitukwamisha tutakwenda kutekeleza ahadi hii ya Serikali kwa hakika kabisa.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa kuwa, Serikali inaendelea na ujenzi wa Mahakama za Wilaya na kule Wilayani Mkinga Mahakama yetu ya Wilaya iko tayari na imeanza kazi wiki iliyopita. Je, Serikali ina mkakati gani sasa wa kukarabati zile Mahakama za Mwanzo ambazo ni chakavu sana. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mhesimiwa Spika, ahsante sana, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu, Mbunge Viti Maalum kutokea Mkinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sasa hivi katika mpango wetu tunaoendelea nao, tunaendelea kukarabati na kujenga majengo mapya katika maeneo mbalimbali. Hivyo nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba majengo yaliyochakaa yataendelea katika utekelezaji wa mpango tulionao katika kipindi hiki tulicho nacho na kipindi kijacho kwa sababu mwisho wa mradi huu ni 2025 kuhakikisha kwamba huduma za Mahakama zote nchini katika ngazi mbalimbali tutakuwa tumezikamilsha. Ahsante.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali inaendelea na ujenzi wa nyumba za Walimu kidogo kidogo na kwa kuwa, zipo nyumba za Walimu ambazo zimejengwa kabla ya uhuru na mara tu hata baada ya uhuru na sasa hivi ni chakavu sana.

Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati angalau zile zilizopo ili kuboresha makazi ya Walimu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mwantumu Zodo Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja ya maelekezo ambayo ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeyatoa katika Halmashauri zote nchini ni kuhakikisha wanatenga fedha za ndani katika mapato yao ya ndani ili kufanya ukarabati wa nyumba zote ambazo zipo za Walimu katika Halmashauri husika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hata hichi anachokizungumza Mheshimiwa Mbunge ni kwamba ninaendelea kuagiza Halmashauri kutekeleza yale maelekezo ambayo Ofisi ya Rais TAMISEMI iliyatoa ya kutenga fedha ili kukarabati hizo nyumba za Walimu katika maeneo yote ambayo zimechakaa.
MHE. MWANTUM M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Wananchi wa Wilaya ya Handeni Mjini wanapata maji kutoka kwenye Kisima cha Nderema ambao ni Mradi wa Serikali, tunaishukuru sana Serikali. Hata hivyo, kisima hicho maji yake yana chumvi sana, je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha wanaenda kuchuja maji yale ili yawe maji safi na salama?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zodo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kisima chochote ambacho kimechimbwa na maji yake bado yana tope Serikali kupitia Wizara tumeendelea na mipango madhubuti ya kuhakikisha tunapata treatment plant kwenye maeneo hayo, hivyo Mheshimiwa Mbunge, pamoja na hiki kisima ulichokitaja na chenyewe kipo kwenye Mpango wa kuweza kujengewa treatment plant. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Tunaishukuru sana Serikali kwa kutenga hizi fedha milioni 400 kwa ajili ya wakulima wa mwani, lakini fedha hizi bado ni chache, hazitoshi. Wanawake wa pembezoni mwa ukanda huu wa bahari wamehamasika sana kulima mwani;

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha wanakwenda kuwaongezea fedha ili kuongeza tija katika uzalishaji wa mwani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali langu la pili, pamoja na akina mama kuhamasika kulima mwani bado kuna changamoto kubwa ya soko;

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuunganisha wakulima wa mwani pamoja na masoko? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantumu Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, ni kweli, na ndiyo maana katika jibu la msingi nimesema hii ni ya awamu ya kwanza; lakini awamu ya pili ambayo tayari maandalizi yake yamekwisha kukamilika ni jumla ya kiasi cha shilingi bilioni 2.5 zitaongezwa. Na kwa hili tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia kwenye program hii iongezwe fedha ambayo itakawenda kuongezeka kwa vikundi kadhaa vya kina mama watakao nufaika na mkopo huu usio na riba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni changamoto ya soko. Upande wa soko unakwenda sambamba na upande wa uzalishaji. Kwa hatua tunayoiendea ya kuongeza uzalishaji imevutia wanunuzi wakubwa wengi. Hivi ninavyozungumza, ushindani juu ya ununuzi wa zao la mwani umeanza. Kampuni zimekwishafikisha bei ya mwani aina ya spinosum shilingi 900 na kwa upande wa aina ya cottonii ni shilingi 200. Kwa hiyo tunakwenda vizuri. Kwa upande wa Serikali tumejipanga kujenga maghala lakini pia vile vile kutengeneza mashine kwa ajili ya ukaushaji wa mwani, ahsante.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana changamoto za mawasiliano kwa Jimbo la Muhambwe zinafanana sana na changamoto za mawasiliano kwa Jimbo letu la Muheza katika Tarafa ya Amani ambayo ni Kata ya Amani Kisiwani Mbomole, Misalai, Zirai na Kwezitu: -

Je, ni lini sasa Serikali inakwenda kujenga minara ya simu ili kutatua changamoto ya mawasiliano kwa wananchi wa Tarafa ya Amani?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuwekeza kuhakikisha kwamba inatatua changamoto ya mawasiliano kulingana na maelekezo ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Jimbo la Muheza tumeliingiza katika mpango wa utekelezaji wa mradi wa Tanzania kidigitali, hivyo tunaamini kwamba kabla ya mwaka wa fedha huu haujaisha zabuni hii itakuwa imeshatangazwa na hatimaye mtoa huduma atapatikana kwa ajili ya Jimbo la Muheza. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, changamoto ya mawasiliano kwa maeneo ya Kwekivu, Kimbe, Namkindi katika Jimbo la Kilindi ni kubwa na usikivu ni mdogo sana. Je, ni lini mtakwenda kutujengea minara kwa ajili ya kupata mawasiliano?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Kilindi, tumeshaliweka katika utekelezaji wa Tanzania ya Kidigitali, kwa hiyo, nimwombe tu Mheshimiwa Mbunge tuendelee kushirikiana ili kuhakikisha kwamba wataalam wetu watakapofika katika maeneo yao, watoe ushirikiano na kutoa maeneo kwa ajili ya kusimika miradi hii ya minara.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuwa kwenye majibu ya Waziri katika ukarabati wa awali nimesikia baadhi ya Vyuo Vikuu ambavyo vimekarabatiwa, lakini sikusikia Chuo Kikuu cha UDOM na kwa kuwa Chuo Kikuu cha UDOM kina changamoto sugu ya uhaba wa maji kwa miaka kumi na sita sasa toka 2007, ambayo inapelekea uchakavu wa majengo yale. Swali la kwanza; je, ni lini Serikali inakwenda kuondoa changamoto ya miundombinu ya maji katika Chuo Kikuu cha UDOM? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; kwa kuwa Chuo Kikuu cha UDOM kilikuwa kinajengwa kwa phase na kwa kuwa ujenzi wake bado haujakamilika, kuna uhaba wa madarasa na hakuna kabisa nyumba za watumishi. Je, Serikali imejipangaje sasa kwenda kumaliza phase za ujenzi wa Chuo Kikuu cha UDOM?
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nilitaja baadhi ya Vyuo ambavyo tayari Serikali imeshapeleka fedha kwa ajili ya ukarabati na ku–improve miundombinu chakavu lakini sikutaja vyuo vyote ambavyo vimenufaika na fedha za Mradi wa HEET. Chuo Kikuu cha UDOM ni kati ya vyuo ambavyo vimenufaika na fedha za mradi huu wa HEET na tayari fedha zimeshapelekwa kwa ajili ya ujenzi. Suala la maji UDOM kwa ujumla wake tunaendelea kulishughulikia kwa kushirikiana na Wizara husika kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunapata utatuzi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla wake tunaongeza jitihada kuhakikisha kwamba vyuo vyote ikiwa ni pamoja na UDOM tunamaliza ujenzi na ukarabati katika maeneo ambayo yalikuwa hayajakamilika ili wanafunzi wetu waweze kupata huduma nzuri ya elimu ya juu.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Miradi hiyo iliyotajwa hapo ni kwa ajili ya uboreshaji wa stendi za majiji na manispaa na kwa kuwa halmashauri ninazoziongelea haziangukii kwenye majiji wala manispaa. Je, Serikali inampango gani wa makusudi sasa kuhakikisha wanakwenda kuboresha stendi kwenye Halmashauri zetu za Wilaya ya Mkinga, Pangani, Muheza, Lushoto pamoja na Kilindi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa maeneo ya stendi pia ni moja ya chanzo cha uzalishaji wa ajira hasa kwa kina mama na vijana. Je, Serikali sasa ina mkakati gani wa kuhakikisha miundombinu ya stendi inakuwa rafiki kwa wajasiliamali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantumu Mzamili Zodo, Mbunge wa viti maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, halmashauri ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja ni kweli hazipo kwenye category ya majiji na manispaa na halmashauri hizi kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, kwamba tutaendelea kutenga fedha kupitia mapato ya ndani lakini pia kupitia Serikali kuu kwa awamu kuhakikisha kwamba stendi hizo zinajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni mhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba halmashauri hizo pia zipo kwenye mpango, tutaendelea kujenga kwa awamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili kuhusiana na miundombinu inayowezesha wafanya biashara. Serikali imekuwa ikijenga stendi, inajenga maeneo kwa ajili ya mama lishe na baba lishe, inajenga maeneo ambayo yanaweza ku–accomodate Machinga na wafanyabiashara wadogowadogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo suala hili litaendelea kutekelezwa, ahsante. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Serikali imepeleka shilingi milioni 470 kwa shule za Kata 231. Je, ni lini sasa Serikali itapeleka fedha za mabweni kwa ajili ya shule hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, shilingi milioni 470 zilizopelekwa kwenye shule hizi 231 nchini ilikuwa ni kwa ajili ya kata ambazo hazina sekondari bado katika Taifa letu hili la Tanzania. Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliona kuna umuhimu wa kuhakikisha kata ambazo bado hazikuwa na sekondari zinapata sekondari na ndiyo maana ametoa shilingi milioni 470 na mwaka huu kuna shilingi milioni 560 na kuna wengine wamepata hadi shilingi milioni 603 kwa ajili ya ujenzi wa shule hizi za Kata.

Mheshimiwa Spika, tutakapomaliza ujenzi wa shule hizi za kata Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya mabweni kwenye shule hizi.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Zao la mkonge ndiyo dhahabu yetu ya Mkoa wa Tanga kwa sasa. Zao la mkonge linachukua miaka mitatu toka kulihudumia mpaka kuanza kuvuna. Wakulima wengi wadogo wadogo wanaoanza wanashindwa pale mwanzo kwa sabbau ya kusubiria miaka mitatu kabla ya kuvuna;

Je, Wizara haioni haja sasa ya kuja na mkakati wa kuwawezesha wakulima wadogo wadogo ili kuedelea kuleta hamasa kwenye zao hili?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye zao la mkonge Serikali imefanya yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza, tumeendelea kuongeza uzalishaji wa miche ya kutosha kupitia TARI Mlingano pale Mkoa wa Tanga, na hivi sasa tunajenga maabara ya tissue culture kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa miche hii ya mkonge ili wakulima wengi zaidi waweze kuhamasika. Pili; tunahakikisha ya kwamba katika mwaka huu wa fedha tunanunua decorticators mbili, ile corona, kwa ajili ya uchakataji wa mkonge ili mkonge mwingi zaidi uweze kuchakatwa na kuongeza hamasa ya wakulima kulima zaidi; na la tatu, tunaendelea kuunganisha wakulima wetu na taasisi mbalimbali za kifedha ili waweze kukopesheka na kuongeza tija katika uzalishaji wa zao la mkonge. Na la mwisho, kwa sababu katika ulimaji wa mkonge kuna spacing tumekuwa pia tukiwahamasisha pale katikati kulima mazao mengine ya haraka ili yawasaidie kuiongeza tija na kuongeza kipato katika aina ya zao ambalo wanalilima.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kuuliza swali moja dogo la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali toka robo ya tatu imesitisha kutoa mikopo hii ya asilimia 10 mpaka sasa na kwa kuwa akina mama wanahangaika na mikopo ya kausha damu huko mitaani; je, ni lini sasa Serikali inakwenda kuanza kutoa mikopo hii ya asilimia 10?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali ilisitisha utoaji wa mikopo hii ili kufanya tathmini na mapitio ya namna ambavyo mikopo hii inatolewa na hili lilikuwa ni agizo la Kamati ya Kudumu ya Bunge lako tukufu ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Hivi sasa timu ile imeshaundwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tayari wameanza kufanya kazi ya kufanya mapitio na vilevile ilikuwa ni malekezo yake Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha mapitio haya yanafanyika haraka ili fedha zile nyingi zisipotee pale mikopo inapotolewa. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, tayari tumeshatoa maelekezo kwa Wakuu wa Mikoa wote, Makatibu Tawala wa Mikoa na Wakurugenzi Watendaji wa Halmashauri. Kwa mujibu wa kifungu au Kanuni ya 24(2) ya kanuni za utoaji wa mikopo hii, tayari kila Halmashauri ina akaunti mahususi kabisa ya mikopo hii na tumewaelekeza hakuna kusimama katika kupeleka asilimia 10. Kwa hiyo hela zitapelekwa na pili utaratibu mpya utakapotangazwa, basi tutakuwa tuna hela tayari kwa ajili ya kupeleka kwenye huo utoaji wa mikopo.

Kwa hiyo, hawatakiwi kusimama, wanatakiwa kuendelea kuzitenga katika akaunti za mikopo. Kilichosimama tu ni ule utoaji kwenda katika vikundi vya wanufaika, nakushukuru.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa katika majibu ya Naibu Waziri amesema wako kwenye hatua za mwisho kwenda kusaini mkataba wa ujenzi wa daraja hilo: Nataka kujua je, ni lini hasa mkataba huo unatarajiwa kusainiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili: Kwa kuwa ujenzi wa daraja la Bweni Pangani unakwenda sambamba na ujenzi wa barabara ya Tanga - Pangani kilometa 50; na kwa kuwa ujenzi wa barabara hiyo uko asilimia 37: Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kuwa daraja hilo litakwenda kukamilika kwa wakati baada ya mkataba huo kusainiwa? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantumu Mzamilu Zodo, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba muda wowote kabla ya mwisho wa mwezi huu tuna uhakika mkataba huu utakuwa umesainiwa na daraja hili ujenzi wake unafadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia barabara aliyoitaja tuna uhakika itakwenda sambamba na ndiyo maana kwa sababu ya ukubwa wa hili daraja ilipewa lot yake, ni barabara ambayo inajitegemea, ina lot yake. Kwa hiyo, tuna uhakika kwa kuwa ina lot yake na mkandarasi atakayekuwa amepatikana atasimamia hilo daraja tu na barabara za maungio wakati mkandarasi mwingine anaendelea kujenga barabara, kwa hiyo, tuna uhakika wakati mkandarasi anakamilisha barabara, daraja pia litakuwa linakamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa changamoto ya mbolea bado ni kubwa sana nchini; na kwa kuwa Tanga tulikuwa na Kiwanda cha Mbolea na sasa hivi hakifanyi kazi: Je, Serikali haioni haja sasa yakutafuta mwekezaji kwa ajili ya kwenda kuwekeza kwenye kiwanda kile ili kutatua changamoto kubwa ya mbolea tuliyonayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zodo, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama nilivyosema tuna changamoto kubwa sana ya mbolea, zaidi ya tani 600,000 zinahitajika katika kukamilisha mahitaji ya tani 700,000 kwa mwaka ambazo zinatumika katika nchi hii. Kwa hiyo, Serikali ina mpango wa kuendelea kufufua viwanda ikiwemo na hiki ambacho anasema Mheshimiwa Mbunge kule Tanga. Tutaona namna ya kutafuta wawekezaji ili waweze kuwekeza katika kiwanda hicho ili kuendelea kuzalisha mbolea kama ilivyokuwa hapo awali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, toka Desemba, 2022 Mheshimiwa Rais amepeleka milioni hamsini hamsini kwenye maboma ya zahanati. Mpaka leo hayajakamilika ikiwepo Zahanati ya Mpasilasi kwenye Jimbo la Korogwe vijijini. Je, ni upi mkakati wa Serikali sasa kuhakikisha wanakwenda kusimamia ili maboma yale yakamilike?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, Serikali inapeleka milioni 50 kwa ajili ya kukamilisha maboma kwenye maeneo ya halmashauri zetu ambako kuna viongozi. Kuna wakuu wa idara, Wakurugenzi, wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa. Sasa, ni wajibu wao kuhakikisha kwamba, fedha hizi ambazo Mheshimiwa Rais anazipeleka zinafanya kazi kwa wakati na kukamilisha ujenzi kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, nittumie fursa hii kuwakumbusha Wahesjhimiwa wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, Makatibu tawala wa mikoa pamoja na wakurugenzi kwamba, ni wajibu wao na sisi tutafuatilia kuona maboma haya yanakamilika kwa wakati na kuanza kutoa huduma kwa wananchi. Ahsante.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Swali la kwanza; kwa kuwa mchakato huu wa utoaji wa mikopo ya asilimia 10 umesitishwa ni mrefu sasa, na kwa kuwa akina mama bado wanahangaika na mikopo ya kausha damu huko mitaani. Je, ni lini sasa Serikali itaanza tena zoezi hili la utoaji mikopo ili kuondoa adha kwa akina mama wa Mkoa wa Tanga na Watanzania kwa ujumla? (Makofi)

Swali la pili; kwa kuwa Halmashauri huwa zinatenga mikopo ya asilimia 10 kutoka kwenye mapato ya ndani kila robo ya mwaka, na kwa kuwa mchakato huu pia umesimama kwa muda mrefu. Je, Serikali inahakikisha Halmashauri zinaendelea kutenga fedha za asilimia 10 ili wakianza mchakato huu akina mama waweze kupatiwa mikopo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zodo. Swali lake la kwanza juu ya mchakato kusitishwa, ni kweli mchakato huu ulisitishwa baada ya Mheshimiwa Rais kupokea ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) na kuonesha kwamba kuna fedha nyingi ambazo zilikuwa hazijarejeshwa za mikopo hii, hivyo maelekezo ya Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Dkt. Samia Suluhu Hassah yalikuwa, yafanyike mapitio sasa ya namna ya mikopo hii inavyotolewa.

Mheshimiwa Spika, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa aliunda timu, ambayo ilifanya mapitio ya namna ya mikopo inavyotolewa, timu ile ikawasilisha taarifa kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na sasa mapendekezo yale yamewasilishwa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hivi tunavyozungumza Waziri wa nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, amekumbushia kwa Mheshimiwa Rais ili jambo hili liweze kurudi sasa na kuanza utekelezaji wake. Kama kuna Sheria ya kubadilika iletwe mbele ya Bunge hapa ili sheria hizo ziweze kubadilika.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la fedha hizi je bado hutengwa. Ndiyo, fedha hizi bado zinatengwa kwa sababu, kwa mujibu wa Sheria ile ya Fedha ya Serikali za Mitaa, fedha hii iko ring fenced na inaendelea kutengwa. Pale mikopo hii itakapoanza kutolewa tena basi fedha hii ipo, nawatoa mashaka hayo. Ahsante sana.