Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Husna Juma Sekiboko (20 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa fursa ya kuzungumza katika Bunge lako hili tukufu. Kama ulivyotamka majina yangu naitwa Husna Juma Sekiboko, ni Mbunge wa Viti Maalumu kutoka Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Spika, nina na mambo machache ya kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Rais zilizowasilishwa katika Bunge la 2015 na hotuba yake mwezi wa kumi na moja 2020 kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda napenda nitumie kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hotuba nzuri ambayo imetoa mwelekeo wa namna ambavyo Serikali ya Awamu ya Tano katika kipindi chake hiki cha pili inakwenda kutekeleza masuala mbalimbali ya kimaendeleo katika nchi yetu. Vilevile nikupongeze wewe Mheshimiwa Spika kwa namna ambavyo umeonesha uhodari mkubwa katika kuongoza shughuli za Bunge hasa kwa sisi ambao ni wapya tunaendelea kujifunza na kuimarika kwa haraka, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ya kwanza imezungumzwa sana na Waheshimiwa Bunge waliokwishatangulia kuchangia kuhusiana na uchumi wa nchi yetu. Mheshimiwa Rais katika hotuba yake ameeleza namna ambavyo Serikali anayoiongoza angependa ipige hatua kubwa zaidi katika masuala mazima ya uchumi. Katika kuelezea hilo Mheshimiwa Rais amekazia katika sekta ya kilimo na ameeleza kabisa kwamba Wizara atakayoiunda ambayo tayari ameshaiunda sasa atatamani ishughulike moja kwa moja na ile mifuko ambayo inasaidia ukuaji wa sekta ya kilimo hasa kwa wananchi wa hali ya chini kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuseme kweli kabisa sekta ya kilimo ambayo ndiyo inaajiri Watanzania walio wengi katika nchi yetu bado haijafanya vizuri kabisa. Namna nzuri zaidi ya kuweza kufanya vizuri ni kuhakikisha kwamba tunaweka mkazo kwenye yale mazao ya kimkakati kama mkonge, mahindi, mazao ya matunda ambayo yanazalishwa kwa wingi sana katika Mkoa wa Tanga, lakini vilevile mazao ya alizeti na korosho ikiwa hayo ndiyo mazao makubwa ya biashara katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namna ya kutekeleza haya nilidhani niishauri Serikali kwamba kwa miaka mingi sasa tumekuwa tunazungumzia namna ya kuboresha kilimo katika nchi yetu lakini yawezekana hatujaona tija kubwa siyo kwa sababu pengine bajeti inayotengwa haikidhi mipango ambayo inapangwa juu utekelezaji wa shughuli za kilimo lakini bado wananchi wetu hawajajuwa kilimo ni fursa na ni ajira ya uhakika. Namna ya kufanya kilimo kuwa ajira ya uhakika ni kutengeneza mipango mikakati ya kuidhinisha maeneo ya mapori ya yaliyojaa kwenye nchi yetu na kupanga mazao ambayo yanaweza yakalimika katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kule Handeni wakazi wengi wa Wilaya ya Lushoto kutokana na Lushoto kule ni milima mitupu wanaenda Handeni kulima mahindi lakini wanapata shida sana namna ya kupata ardhi ya kilimo pale Handeni kwa sababu siyo wenyeji pale na ukifika pale bado kuna tozo mbalimbali kwenye vijiji na Serikali za Mitaa ambayo bado inamrudisha nyuma, inamkatisha tamaa huyu mwananchi mdogo ambaye anahemea kule kwenda kufanya kilimo katika wilaya ambayo siyo ya nyumbani kwake. Pangekuwa na mkakati wa Serikali wa moja kwa moja kuwasaidia wale wote ambao wana nia ya dhati ya kufanya kilimo hata kwenye wilaya ambazo si za nyumbani kwao, wakaenda wakafanya kilimo chenye support kubwa ya Serikali kwa maana ya pembejeo na vifaa vingine vya kilimo pengine tungetoka kwenye hali ya sasa ambayo inaonyesha dhahiri kwamba bado hatujafanikiwa sana kuajiri vijana wengi kwenye kilimo kutokana na mikakati ambayo ipo sasa.

Mheshimiwa Spika, nimejaribu kufanya tathimini, ukiangalia matokeo ya kidato cha nne mwaka 2020, kuna wanafunzi zaidi ya 280,000 walipata division four na zero. Takwimu hiyo ya wanafunzi takribani laki tatu wanaotengenezwa kila mwaka na kutupwa na mfumo kuwa nje ya system nzima ya ajira rasmi baada ya miaka kumi unaweza kuwa na watu wengi sana ambao ni walalamishi kwenye nchi, hawana shughuli maalumu ya kufanya. Kama wangetengenezewa utaratibu maalumu wakawa wanawekwa kwenye sekta za ujasiliamali, sekta za kilimo na wakawa wanapewa mafunzo pengine ingewasaidia vizuri zaidi kupata ajira na kuacha kuilalamikia Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia limeuliziwa katika swali asubuhi na Mheshimiwa Hawa Chakoma Mchafu kuhusiana na vituo vyetu vya kutolea huduma ya afya. Katika hotuba ya Mheshimiwa Rais ukurasa wa 64 ameelezea namna gani Serikali imefanikiwa kujenga vituo vingi vya afya na zahanati katika nchi yetu ndani ya miaka mitano. Tumejengewa zahanati 1,998 lakini vituo vya afya 487. Hii ni hatua kubwa mno ambayo nchi yetu ndani ya miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini bado tuna shida kubwa katika utoaji wa huduma katika vituo hivi. Baba mtu mzima ambaye anaenda kuhemea huduma kwenye kituo cha afya kilichopo pembezoni takribani pengine kilometa 90 mpaka 100 kwenda kwenye hospitali ya wilaya anashindwa kabisa kupata huduma za msingi kama vile dawa za presha na vipimo vingine ya kawaida ambavyo viwengeweza kufanyika kwenye ngazi ya kituo cha afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namna pekee ya kuweza kuondoa tatizo hili ni sasa Wizara ya Afya kuamua kubadilisha mfumo wa utekelezaji wa majukumu kutoka kwenye kuyagawa kwa hospitali na baadaye wayagawe kwa kada za watumishi au madaktari ambao wanapatikana kwenye hivyo vituo. Kwa sababu wapo madaktari wazuri na wasomi kwenye vituo vya afya, kwa nini wasipewe jukumu la kuweza kumpima mtu presha na kumpatia dawa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano mtu ambaye amepata shida labda ya kuvunjika mkono au mguu, tunavyoenda sasa, kama Serikali itapeleka vifaa tiba kwenye vituo vyetu kama ambavyo mwongozo wa afya unazungumza maana yake utakuwa na X-Ray mashines na vifaa vingi kwenye ngazi za vituo vya afya. Sasa akishapima hapo atakwenda wapi?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Husna.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuweza na mimi kuchangia kwenye mjadala huu muhimu wa bajeti ya Serikali, lakini kabla ya kwenda kwenye mchango wangu moja kwa moja nitumie fursa hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania, mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan. Bajeti ambayo imewasilishwa mbele yetu ni bajeti ambayo imeonesha nia ya dhati ya Mheshimiwa Rais ya kuendeleza kazi ambazo zilikuwa zimeshaanzishwa katika Awamu ya Tano, lakini ya kuweka mkazo katika utekelezaji wa miradi na majukumu mbalimbali ambayo yana tija kwa Watanzania kwa kipindi hiki cha Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii pia kumpongeza sana Waziri, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba. Hotuba hii mbali na uwasilishaji wake ulikuwa wa tofauti na hotuba nyingine ambazo nimeshuhudia zikiwasilishwa humu, lakini ni hotuba ambayo imebeba mawazo, maono na michango ya Waheshimiwa Wabunge waliokuwa wanajadili katika kipindi chote tangu tumekuja kuanza Bunge hili la bajeti. Hii imeleta matumaini, imeleta ari, lakini inatuongezea nguvu kuona namna gani ambavyo tunaweza tukachimbua mambo zaidi kwa ajili ya kuishauri Serikali kwa imani kwamba haya ambayo tunayazungumza ndani ya Bunge Serikali inachukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimshukuru na kumpongea sana Naibu Waziri, Mheshimiwa Masauni; wanafanya kazi nzuri na kwa kweli, combination yao watu hawa wawili, Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, itatuletea tija na matunda makubwa sana katika kipindi hiki cha Awamu ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia Bajeti Kuu ya Serikali; bajeti ambayo ina mambo mawili makubwa, jambo la kwanza ni ukusanyaji wa mapato, lakini jambo la pili ni matumizi ya mapato ambayo yanakusanywa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ukusanyaji wa mapato chombo chetu, mamlaka ambayo tunaitumia katika ukusanyaji wa mapato nchini ni Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), lakini katika michango ya Waheshimiwa Wabunge wengi ambao walikuwa wanazungumza tangu mjadala huu umeanza umeonesha kuna upungufu mkubwa wa watumishi TRA na hii inawezekana ndio sababu tunasuasua katika ukusanyaji wa mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kutoa ushauri kwa Serikali. Kutokana na upungufu huo wa watumishi na taarifa niliyonayo ni kwamba tuna uhitaji wa watumishi 7,406 nchi nzima kwa Mamlaka ya TRA peke yake, lakini watumishi waliopo ni 4,733 na upungufu ni 2,673, lakini ukiangalia hali halisi ya watumishi kwenye maeneo yetu hususan kwenye Wilaya zetu unakuta Ofisi ya TRA ya Wilaya ina mtumishi mmoja kwa maana ya Meneja wa TRA wa Wilaya au wawili, yeye na msaidizi wake jambo ambalo kwa kweli linazorotesha sana ukusanyaji wa mapato kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wilaya nyingine ina kata zaidi ya 30, lakini yuko meneja mmoja tu, I mean mtumishi ambaye ni Meneja tu wa TRA, ndio anafanya kazi ya kutoa elimu, kukagua, kutoa tathmini, kwenda kuhamasisha na kuelimisha watu watumie mashine za EFD na kadhalika ili aweze kukusanya mapato. Sasa ili tuweze kusaidia Serikali najua kwamba, hatuna uwezo wa kuwaajiri watu 2,600 TRA peke yake kwa wakati mmoja na wala simaanishi kwamba, hao watu wasiajiriwe, lakini nafikiri tunaweza tukaitumia Mamlaka ya Serikali za Mitaa tukaondoa hili ombwe la upungufu wa watumishi katika ukusanyaji wa mapato kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mfumo wetu wa utawala nchini umeanzia kwa Mjumbe wa Nyumba Kumi, umeenda kwenye Kitongoji, unaenda kwenye Kijiji, unakwenda kwenye Kata mpaka kwenye Wilaya na ngazi ya Taifa. Na huko kote kuna viongozi na watumishi wa Serikali, viongozi ambao wangeweza kutoa taarifa za ukusanyaji wa mapato wakazipeleka kwa Meneja wa TRA wa Wilaya akapata taarifa ni duka gani jipya limefunguliwa, ni duka gani limefungwa, ni kwa namna gani watu wanakwepa kodi. Tayari ikawawezesha hawa watumishi wachache wa TRA kuweza kufanya kazi yenye ufanisi katika ukusanyaji wa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi ningeishauri sana Serikali tuwatumie watendaji wa kata, tuwatumie watendaji wa vijiji, tuwatumie Wenyeviti wa mitaa, tuwatumie Wenyeviti wa vitongoji na wajumbe wa nyumba kumi-kumi na namna nzuri ya kuwatumia ni kuwatengea kibajeti kidogo tukawawezesha sasa kama ambavyo tumeona kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri kwamba wanakwenda kulipa posho ya madaraka kwa Watendaji wa Kata. Tushuke twende mpaka kwa Mtendaji wa Mtaa au wa Kijiji, twende mpaka kwa Mwenyekiti wa Kijiji na kitongoji watusaidie na tuwa-task hii kazi ya kutoa taarifa ya walipa kodi, ili kurahisisha hili suala la ukusanyaji wa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna ombwe kubwa kati ya Serikali za Mitaa na Mamlaka ya Mapato – TRA. Unakuta wanakwenda kufanya ukaguzi eneo hilo hilo moja, pengine duka hilo hilo moja watu wa TRA, lakini hawezi kukagua lile jambo ambalo limekuwa tasked kwa halmashauri labda ya Wilaya au ya Jiji. Akienda mtu wa jiji ameenda kukagua labda anataka kwenda kukusanya service levy, lakini hana muda kabisa wa kuangalia kama je, kodi ya mapato imekwenda TRA. Sasa hawa watu tukiwa-link ikawa mtumishi wa Halmashauri akienda kukagua masuala yanayohusu Halmashauri akapewa na kazi ya kuangalia masuala mengine ya Serikali kwa sababu hawa wote ni watumishi wa Serikali, wote wanalipwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wote wanawajibika kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa nini watengane? Kwa nini wasifanye hizi kazi kwa pamoja kukapatikana mazingira ya ufanisi mwisho wa siku tukapunguza hili ombwe la watumishi katika Mamlaka ya TRA?

Mheshimiwa Mwenyekiti, huku TRA zamani tumezoea, ukimuona mtu anafanya kazi TRA utaona ana gari zuri, anaishi kwenye nyumba nzuri, tofauti na mazingira yalivyo sasa. Maeneo ya pembezoni hawa watumishi wa TRA wanaishi kwenye mazingira magumu mno, nyumba zimechakaa, hazijakarabatiwa, magari yamechakaa na ndio ambao tunawategemea waende wakakusanye mapato kwa ajili ya Serikali yetu. Kwa hiyo, ningeomba sana na wao waweze kutizamwa, nyumba zao ziweze kufanyiwa ukarabati maeneo ambayo hamna nyumba waweze kujengewa, ili waweze kufanya kazi hii kwa ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo ningependa kulizungumza leo ni upelekaji wa fedha kwenye maeneo ya matumizi. Huko nyuma palikuwa na maelekezo na ninashukuru kwa kweli ilitekelezwa vizuri kwenye baadhi ya maeneo kwamba ikiwa mradi unajengwa kwenye shule, basi fedha ya mradi hata kama ni ya darasa iende moja kwa moja kwenye shule husika ili kuondoa ile process ndefu ya kuweza kutoa fedha kwenda kwenye ngazi moja iende kwingine iende kwingine mpaka ikifika kule inachukua muda mrefu sana. Sasa ili kupunguza hiyo bureaucracy hela iende moja kwa moja kwenye eneo la matumizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tumeweza kufanya hivyo kwenye shule, tumeweza kufanya hivyo kwenye zahanati, lakini tuna shida kwenye hela ya matumizi mengineyo (OC). Ofisi za Wakuu wa Wilaya hawapelekewi fedha moja kwa moja mpaka ipitie kwa Katibu Tawala wa Mkoa. Fedha yenyewe unakuta ni milioni tano, milioni sita, milioni mbili, imeshindikana kwenda kwa Accounting Officer wa wilaya pale (DAS), inapita kwa Accounting Officer wa mkoa, ana miradi mingapi ya kuweza ku-manage hiyo fedha? Ana watu wangapi anaokwenda kuwalipa hiyo fedha? Lakini hiyo fedha ingeenda moja kwa moja ingerahisisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Niliwahi kuuliza humu swali pia kwamba, kuna haja gani ya fedha ya matumizi ya kituo cha polisi, Mkuu wa Polisi wa Wilaya, ipitie kwa Mkuu wa Polisi wa Mkoa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni urasimu ambao kimsingi hauna sababu, kwa sababu yule aliyeko pale kwenye kituo cha kazi akiipata ile fedha kwa wakati maana yake ataweza kutatua changamoto zake kwa wakati. Na ndio sababu tunaona maeneo mengine unampigia OCD kuna ajali, kuna janga, kuna nini, anakwambia sina mafuta, mipira ya gari imechakaa, fedha bado haijaja, lakini fedha imepelekwa mkoani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa mujibu wa taratibu za wenzetu hawa huwezi kum-question RPC kwamba niletee fedha ukiwa wewe ni OCD uko chini yake kwa mujibu wa taratibu zao za kijeshi. Sasa ili kuondoa huo urasimu wote ni vyema sasa Mheshimiwa Waziri tuone umuhimu wa kupeleka fedha hizi moja kwa moja kule kwenye maeneo ya matumizi ili kuwasaidia wenzetu kuweza kufanya kazi zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini napongeza pia namna ambavyo mmeamua kupeleka fedha za Maafisa Tarafa na Watendaji wa Kata, lakini Mheshimiwa Waziri nataka nikwambie, sio jambo jipya sana huko nyuma limefanyika, lakini halijafanyika kwa usahihi sana kwa sababu zinapitia kwenye ofisi nyingine. Mimi nikiwa DAS unaniletea milioni tatu, unaweza kukuta pale umepita mwenge umeniachia deni, wamepita pale viongozi wameniachia deni, sikumbuki kupeleka fedha kwa Afisa Tarafa naitumia palepale Wiayani inaisha, lakini kama mmeipeleka moja kwa moja kwa Afisa Tarafa maana yake ni kwamba, siwezi kwenda kuichukua kule tayari atakuwa amepata ile haki yake na kazi zake zitafanyika vizuri. (Makofi)

Kwa hiyo, nashauri sana fedha ziende huko moja kwa moja badala ya kupitia kwenye mamlaka nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mwisho ambalo ningependa kulizungumza; siasa,uendeshaji wa nchi kwa akili yangu ya kawaida kabisa kila jambo linakwenda kwa wakati. Siasa yetu ya sasa kwa kauli mbiu ya mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan tunaendeleza kazi ambazo tulizianza katika Awamu ya Tano, lakini kwa namna ambavyo mama anaenda kufanya kazi anataka kuacha legacy kama mama wa kwanza kuiongoza nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, ili aweze kuweka legacy lazima tumsaidie katika eneo la maji tufanye vizuri, bajeti ya maji iende vizuri akamtue mama ndoo kichwani. Lazima tumsaidie katika eneo la afya, vituo vya afya ambavyo vimejengwa vipelekewe vifaa tiba, akinamama waweze kujifungua salama na wajifungue kwa mazingira ambayo yanatakiwa, lakini lazima tupeleke bajeti na ifike ile ambayo inalenga kuwawezesha akinamama kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiyafanya haya mambo matatu tutakuwa tumemsaidia mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan, kuacha legacy katika nchi hii katika muda wake wote ambao atakuwa amekuwa madarakani. Ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nikushukuru sana kwa kunipa fursa ili na mimi niweke mchango wangu kwenye Wizara ya Elimu ambayo ni Wizara nyeti na nichanzo kikubwa cha maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaenda kwenye mchango wangu naomba nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuingilia kati na kuona namna ya kupunguza makali ya bei za mafuta nchini, jambo ambalo lisababisha unafuu katika mfumuko wa bei.

Jambo alilolifanya Mheshimiwa Rais ni kubwa. Sisi Wabunge tupo tayari na tuko nyuma yake kuhakikisha kwamba tunaendelea kwenda kuyazungumza hayo mazuri ambayo ameanzisha kuyafanya katika hali hii ya taharuki ya uchumi katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri wa Elimu na Naibu Waziri kaka yangu Kipanga kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya. Mheshimiwa Mkenda tangu amefika pale, na mimi ni mjumbe wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii yapo mambo mengi ambayo wajumbe tunamshauri na tunaona hata kwenye taarifa yake amewasilisha kuona kwamba anaithamini kamati yetu na anaona mchango mkubwa unaowasilishwa kupitia kamati na mpongeza na ninamshukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa leo nimeupa jina la quality education, ni namna gani nchi yetu tunaweza kusogelea elimu yenye viwango. Quality education inategemea vitu vingi na ukitaka kumuuliza mtu yoyote maana ya elimu atakwambia ni kuhamisha maarifa kutoka eneo moja au kwa mtu mmoja kwenda kwa mtu mwingine. Lakini vitu ambavyo vinahusika katika kuhamisha maarifa haya ni mazingira ambayo kwa kiasi kikubwa sana naomba nimpongeze Mheshimiwa Rais na Wizara kwa ujumla kwa namna ambavyo wameimarisha mifumo na miundombinu ya elimu katika maeneo yetu. Zimetumika fedha nyingi sana, zimewekezwa katika kujenga miundombinu ya madarasa, miundominu ya vyuo na ofisi mbalimbali kwenye Idara ya Elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jumapili nilikuwa Wilaya ya Kilindi. Nilitembelea Halmashauri ya Wilaya ile na nilikutana na akina mama wa Wilaya ya Kilindi. Moja ya eneo ambalo walinituma kuja kuzungumzia ni namna gani tunaweza tukaboresha elimu hasa katika Wilaya za Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Kilindi kwa mfano, wao wamefanya utafiti na wamegundua kwamba watoto wa Kilindi hawafeli tu kwa sababu hawana uwezo wa kufaulu wao kama wao, isipokuwa mazingira yao, ukosefu wa vitendea kazi na homa ya mitihani ndiyo inayowafikisha katika hali hiyo ya kushindwa kufanya vizuri kwenye mitihani.

Mheshimiwa Naibu Spika, wameenda mbali, wataalam wa elimu, Afisa Elimu Msingi na Sekondari wameeleza ya kwamba wameunda Jukwaa la Wazalendo wa Elimu wa Kilindi. Lengo lao ni kutafuta photocopy machine kwa ajili ya kuziweka kwenye Tarafa zao, kwa ajili ya kuzalisha mitihani. Kwa sababu baada ya kufanya utafiti wamegundua ya kwamba watoto wengi wanafeli mitihani kwa ile homa, taharuki kwenye mitihani kwa kuwa hawana uzoefu wa kufanya mitihani iliyochapishwa. Wamezoea kunakiliwa mitihani ubaoni, wamezoea kufanya mitihani kwenye madarasa ambayo darasa moja watu 80 watu 90.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ukimuweka mtoto kwenye dawati peke yake na ukampa mtihani ambao uko kwenye karatasi umechapishwa tayari anapata taharuki na pengine inaweza kumsababishia kwa kiasi kikubwa kufeli mtihani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu wazo ambalo wamelianzisha Kilindi ni wazo zuri sana. Kwamba moja ya eneo ambalo tunaweza tukaisaidia Serikali kupata elimu bora kwa watoto wetu na tukapunguza failure kwa watoto wetu ni kuwapa mitihani mingi zaidi, wapate mazoezi mengi zaidi. Tunaweza kufanya hilo kama tutapeleka hizo photocopy machine walau kwenye Tarafa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajenga madarasa ni vizuri na tumefikia kwenye hatua nzuri sana lakini tupeleke hivyo vitendea kazi ambavyo sasa angalau vitaifikisha elimu hii inayotolewa na Shule za Serikali ifanane na zile Shule za Private. Watoto wanaosoma Anne Maria wanafanya mitihani hata weekly test iliyochapishwa. Mtoto anayesoma shule ya kwetu ya Serikali anakutana na mtihani uliochapishwa siku ya NECTA.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ili aweze kuzoea hali hiyo ya mitihani, aweze kuwa settled ni muhimu sana kwenda kufanyia kazi wazo hili ambalo limeanzishwa Kilindi na pengine liambukizwe kwenye nchi nzima ili tufanye vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ninatamani kulizungumza ni kuhusu Walimu bora na wanaotosheleza. Zimetolewa takwimu mbalimbali, ratio ya Mwalimu mmoja kwa Shule ya Msingi ni kufundisha watoto 45 lakini ratio ya Mwalimu mmoja kwa Elimu ya Sekondari ni kufundisha watoto 45. Kwa Mkoa wa Tanga, ratio ya Mwalimu mmoja anafundisha watoto kuanzia 80 mpaka 200 shule nyingine hii inaleta shida.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna upungufu mkubwa sana wa Walimu. Walimu ambao tunahitaji siyo chini ya 200,000 kama ambavyo takwimu zinaonesha. Pamoja na kwamba kasungura ketu ni kadogo, ajira zinatolewa kulingana na upatikanaji wa fedha kwenye Bajeti. Kuna haja ya kuweka utaratibu wa wazi kupunguza minong’ono, kupunguza Wabunge kuendelea kupigiwa simu mara kwa mara kuombwa ajira na vijana wetu. Kwa mfano, tunao watoto ambao wamehitimu vyuo tangu mwaka 2013, 2014, 2015 ni kwa nini sasa Serikali isitangaze kwamba mwaka huu itawaajiri waliohitimu 2015 peke yake au 2013 au 2014? Tukaweka nafasi ya kupunguza simu na meseji kwa Wabunge wanaombwa kusaidia watoto hao kuajiriwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watoto wenye umri mkubwa na unafahamu kwamba mtanzania kwa mujibu wa Sheria ya Ajira anaeajiriwa permanent employment ni chini ya miaka 45. Kadri wanavyokaa nje ya soko umri unakwenda kwa hiyo, mwisho wa siku watakosa nafasi ya kuajiriwa. Je, kwa nini sasa tusiwaajiri hata wale wenye umri mkubwa kwanza kwa sababu tunaajiri kwa awamu ili kuweza kuwaondoa kwenye hilo wimbi la kukosa sifa ya kuajiriwa na Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitazama katika watoto ambao wanaajiriwa wapo vijana wengi ambao wanajitolea kwenye shule zetu za Serikali, lakini bado kila siku tumekuwa tukiimba humu ndani wapewe kipaumbele wale wanaojitolea. Kwa sababu tuna upungufu wa Walimu na wao tayari walishaamua kujitolea kutusaidia kuziba hizo nafasi za upungufu. Kwa nini zinapotoka ajira wasiangaliwe wakaanza kuajiriwa hao kabla hawajatazamwa watu wengine? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukitaka elimu bora, tukitaka quality education tunahitaji pia kuwa na Quality Insurers wazuri, bora, wanaowajibika na sisi kuwajengea mazingira ya wao kuwajibika. Katika nchi yoyote elimu hailindwi au haisimamiwi na mtutu wa bunduki. Hutamkuta Polisi anamsimamia Mwalimu afundishe, hutamkuta Afisa wa TAKUKURU wala Afisa wa Usalama wa Taifa wala wa Magereza akimsimamia Mwalimu afundishe.

Mheshimiwa Naibu Spika, chombo cha usalama kinachosimamia elimu nchini ni Uthibiti Ubora (Quality Insurers) wao ndiyo wanaangalia namna gani elimu inatolewa, wana- assure elimu itolewe ambayo inahitajika yenye viwango. Lakini kitu cha kusikitisha hatujawawezesha Wathibiti Ubora, tumewaacha katika mazingira ambayo pengine tumeshindwa kutambua uwezo wao au nafasi yao katika kutekeleza majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma majukumu ya Quality Insurers jukumu lao la pili linasema carrying out periodic school and center physical conditions survey, anapaswa kutembelea shule moja au kituo cha kutolea elimu kimoja baada ya kingine lakini hawana magari. Wanaokwenda kumkagua ni Mkurugenzi mwenye shule zake, Mthibiti Ubora anaenda kuomba mafuta, anaenda kuomba gari kwa Mkurugenzi ili aende amkague shule zake. Tutapata vipi hapo elimu bora? (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa mchango wako mzuri.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba dakika mbili niweze kumalizia. Tafadhali.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Kengele ya pili hiyo.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, awali ya yote ninamshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na wewe nikushukuru sana kwa kunipa fursa ya kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu leo kwa ajili ya kuweka mchango wangu kwenye Bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, leo nimepanga kuzungumzia mambo matatu. Jambo la kwanza ni kuhusiana na hili ambalo limewasilishwa kupitia bajeti hii kwa maana ya kupunguza gharama za uendeshai Serikalini. Kupitia fursa hii naomba nimpongeze sana Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa maono, namna ambavyo bajeti hii imeletwa na kukidhi mahitaji ya maeneo mengi, hasa kwa watu wale wenye kipato kidogo kwa maana ya wenzetu kule chini.

Mheshimiwa Spika, ukizungumzia kupunguza gharama za uendeshaji maana yake unataka kuleta tija katika wale ambao wanategemea huduma za kijamii zinazotolewa na Serikali huko kwenye ngazi za chini. Nimeona katika bajeti hii, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, amekuja na mkakati wa kupunguza matumizi Serikalini kwenye magari, kwa watumishi, vilevile jambo kubwa ambalo nimeliona ni lile la kupunguza vikao na kuhamia kwenye TEHAMA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhamia kwenye TEHAMA kwa ulimwengu tulio nao sasa ni kama vile tumechelewa, ni jambo ambalo ningeshauri liende kwa spidi kubwa sana. Nitakupa mfano, wakati wa maandalizi ya bajeti zetu za halmashauri, halmashauri zetu almost zote huwa zinahamia Dodoma.

Mheshimiwa Spika, wanakaa kwa zaidi ya wiki tatu, wiki tano na wengine miezi miwili, hapa Dodoma kwa ajili ya maandalizi ya bajeti, jambo ambalo lingeweza kufanyika huko kwenye Halmashauri zao taarifa zikaletwa kwenye Kamati za Bunge, michakato ikaenda kimtandao kutumia TEHAMA na mwisho wa siku tukatengeneza tija kubwa sana na tukabana matumizi, fedha hizi tukapeleka kwenye maeneo mengine ambayo yana uhitaji. Kwa hiyo, ninaipongeze sana Serikali na Wizara ya Fedha kwa kuona namna gani tunaweza tukabana matumizi kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Spika, kipindi kifupi kilichopita tuliona Katibu Mkuu Hazina alitoa tangazo la kuongeza hizi posho za viongozi. Hizi ukiziongeza na bado ukaendelea ku-entertain vikao vingi, tunapeleka mzigo mkubwa sana kwa Mtanzania. Ili kuweza kupunguza huu mzigo, pamoja na kwamba hizi posho zimeongezwa, ni vizuri sana Mheshimiwa Waziri akaona namna nzuri ya kutekeleza hili jambo kwa haraka kuleta tija na nafuu ya maisha ili kuendeleza kupeleka fedha kwenye miradi ya maendeleo na kuboresha maisha ya Watanzania zaidi.

Mheshimiwa Spika, eneo hili naona changamoto moja tu, kwamba tumezoea kutumia mtandao wetu kwenye mawasiliano ya Serikali, hata kwenye mifumo ya fedha tunatumia TTCL, lakini TTCL haifanyi vizuri sana, maeneo mengine hayana mtandao kabisa, maeneo mengine mtandao ni hafifu, jambo ambalo litatusababishia sasa kusuasua tunapokwenda kutekeleza vikao kwa kutumia TEHAMA.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ili tuende kwa ufanisi, jambo la kwanza ningeishauri Serikali kuangalia namna bora ya kuboresha mfumo wa mawasiliano kupitia TTCL. Wakiboresha mtandao wa TTCL ukawa unapatikana, bado itakuwa tena ni fursa, badala ya fedha kutumika kwenye mitandao mingine ya kibiashara, hiyohiyo fedha ambayo tunakwenda kufanyia TEHAMA itarudi tena kwenye Mfuko wa Serikali kupitia TTCL. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ninapenda kulizungumza siku ya leo ni namna ya kuongeza mapato. Wakati inawasilishwa Bajeti ya Afya nilisimama katika Bunge lako na nikaiomba sana Serikali kuangalia namna ya kuboresha huduma ya mama na mtoto.

Mheshimiwa Spika, katika kuzungumza hayo tuliona mifano mbalimbali, kwamba pamoja na sera nzuri za Serikali na maelekezo ya Wizara kwamba akina mama na watoto wapate matibabu bure, lakini maeneo mengi akina mama wanafanyiwa operesheni kwa gharama kubwa sana wanapojifungua, watoto bado wanatozwa, ukiuliza wanasema ni uwezo mdogo wa kifedga lakini muda mwingine vituo vyetu vinakosa kabisa dawa.

Mheshimiwa Spika, namna bora ambayo nimeiona ya kwenda kuongeza mapato kwenye vituo vyetu vya kutolea huduma za afya ni kufunga mfumo wa GoT-HoMIS. GoT-HoMIS ni mfumo ambao unaunganisha utoaji wa huduma kwenye kituo cha afya tangu mgonjwa anasajiliwa mpaka anakwenda kwa daktari, anakwenda maabara, mpaka anarudi tena kwa daktari kwa ajili ya majibu. Kwa hiyo, huo mfumo ukiwekwa vizuri maana yake hakutakuwa na uvujaji wa mapato kwenye kituo cha afya.

Mheshimiwa Spika, tumeona kwenye maeneo mengi ambapo huo mfumo umefungwa mapato yameongezeka zaidi ya mara tano, mara sita. Kituo ambacho kilikuwa kinakusanya 100,000 kwa siku kikifungiwa GoT-HoMIS kinakusanya mpaka 500,000, 600,000 kwa siku.

Mheshimiwa Spika, jambo hili likiwekewa mkazo, pamoja na maelekezo ya Serikali, lakini bado Halmashauri hazijatekeleza vizuri huu mfumo, yakipelekwa maelekezo mahususi wakafunga huu mfumo, ninaamini hata yale malalamiko ya kukosekana kwa dawa au kutozwa fedha kwenye vituo vya afya yataondoka kwa sababu tayari kutakuwa na uwezo wa kupata fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ninataka kulizungumza siku ya leo ni hii asilimia 10. Naifahamu dhamira njema sana ya Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, kwamba angetamani kuwawezesha na wamachinga, na mimi najua. Kwenye asilimia 10 ya halmashauri imewataja akina mama, vijana na watu wenye ulemavu, kwenye kundi la vijana wametajwa wenye kuanzia miaka 18 mpaka miaka 35 wakati Baba kwa maana ya mwanaume ambaye anatamani kupata huo mkopo wa halmashauri wa asilimia 10 lakini hawezi kuupata kwa sababu tayari pengine amevuka miaka 35. Changamoto inakuja hapa, Baba mwenye miaka 35 akikosa huo mkopo nadhani inawezekana ndiyo sababu Serikali imefikiria sasa waone namna ya kutengeneza miundombinu kwa ajili ya wamachinga na watu wa namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, nataka niwaambie, chanzo cha mikopo hii ya wanawake na vijana ilianzishwa mwaka 1993 na Kanuni zake nadhani zilianza mwaka 1994, lakini maboresho yaliyofanyika 2018 na kanuni za 2019 yalitoa malengo kwamba kwa mwanamke siyo mtu ambaye ana msuli, baba kwenye familia au kijana mwenye nguvu angalau hawezi kufa njaa kwa sababu ana uwezo wa kwenda kubeba gunia, ana uwezo wa kwenda kuchimba sehemu kazi yoyote ya kutumia msuli na akawezesha familia yake kupata mlo wa siku hiyo. Lakini kwa mama uwezo huo hana.

Mheshimiwa Spika, sasa ili aweze kujikimu, aweze kuendeleza familia, mama ambaye anategemewa na familia, ilionekana ni vyema apewe mkopo ndiyo tukaenda kutenga hizo asilimia 10 tukazigawanya zilivyogawanywa kwa ajili ya kuwezesha yale makundi maalum.

Mheshimiwa Spika, sasa changamoto inayokuja hapa ni kwamba hii fedha haitoshi, kuna halmashauri za pembeni, kwa mfano Halmashauri za Wilaya za Lushoto, Kilindi, Korogwe, Mkinga na kadhalika na pengine nchini halmashauri nyingi ambazo pengine kwa mwaka hata zinakusanya chini ya Bilioni Moja. Sasa kama mapato ya ndani yako chini ya Bilioni Moja, maana yake ni kwamba asilimia 10 inaweza isifike hata Milioni 200 lakini wananchi wanaohitaji pale ni zaidi ya inavyotegemewa, kwa hiyo mwisho wa siku wanazigawanya zile fedha kwa kuwakopesha wengine Milioni Moja, Milioni Mbili, hela ambayo haileti tija au tija yake inachelewa sana kwa sababu mkopo huo unakuwa na fedha kidogo.

Mheshimiwa Spika, sasa nini kifanyike? Kwa kuwa mwaka 1993 lengo lilikuwa ni vijana na akina mama, na kwa sababu mwaka 1993 ulianzishwa mfuko wa vijana na unafanya kazi mpaka leo kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, ninashauri kwamba pamoja na asilimia 10 kubaki kama ilivyo kwenye Halmashauri zetu kwa ajili ya kuwasaidia akina mama, vijana na watu wenye ulemavu, lakini uanzishwe Mfuko mwingine na uwe unatengewa fedha kama unavyotengewa huu wa vijana kwa kila bajeti kwa ajili ya kuwasaidia hawa wamachinga kujenga miundombinu, vilevile mfuko huo uwasaidie akina mama kupata mikopo kama ambavyo wanapata hili kundi la vijana, kwa sababu wanapata ile asilimia 10 ya halmashauri, at the same time wanapata mikopo kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ninapenda kulizungumza siku ya leo ni upande wa watumishi. Ni dhahiri kwamba tuna upungufu mkubwa wa watumishi katika sekta mbalimbali, Wizara imeona na imeleta namna ambavyo wanaweza wakakabiliana na namna ambavyo wanaweza wakaajiri kadri muda unavyokwenda gradually. Mimi naona kuna haja ya kufanya kitu kwenye eneo hili. Kwa mfano, unakuta kwenye Halmashauri ya Wilaya tunazo taasisi zetu kama Halmashauri, kuna RUWASA, TARURA, kuna taasisi nyingi zipo kwenye Halmashauri, unaweza kukuta pengine kuna Mhandisi wa Ujenzi mmoja yupo pale Halmashauri pengine upande wa RUWASA, ni vizuri tukaenda kwenye kanuni zetu za utumishi wa umma tukaangalia namna ya kuwaazima watumishi kwenye taasisi zingine waende wafanye kazi kwenye taasisi mojawapo ili kuweza angalau kupunguza upungufu wa watumishi na mwisho wa siku kuleta tija katika utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, vilevile inaenda pamoja na upande wa Madaktari. Tumezoea kuona Madaktari wengi wameajiriwa kwenye hospitali zetu za Serikali, wakimaliza ule muda waliopangiwa kuwepo pale unamkuta yuko part-time kwenye hospitali binafsi, lakini huwezi kumkuta yuko part-time kwenye hospitali nyingine ya Serikali. Kwa nini, pengine kuna mgongano hapo wa kikanuni na kimaadili kwenye Kanuni za Utumishi wa Umma, kwa hiyo tuki-harmonize haya mazingira ya utumishi wa umma tutawaruhusu watumishi wetu kutumika kwenye taasisi au kwenye maeneo zaidi ya moja na mwisho wa siku kupunguza uhaba katika utumishi wa umma.

Mheshimiwa Spika, nimeliona hili kwa upande wa TRA pia. Kwa mfano, unakuta kwenye maduka yetu anakwenda kutembelea mtu wa TRA kwa ajili ya kukagua kama kuna EFD machine inatumika vizuri, lakini kama huyo mwenye duka analipa kodi vizuri, akitoka anakwenda mtu wa mapato wa Halmshauri, anachokwenda kufanya yeye ni kuangalia service levy peke yake, akitoka atakwenda Afisa Biashara, anachokwenda kufanya ni kuangalia leseni peke yake, akitoka ataenda mtu wa Zimamoto anakwenda kukagua mtungi peke yake, sasa badala yake yangeunganishwa haya yote akienda mmoja wao akapewa nafasi ya kukagua hayo mengine yote kuliko kulazimu kila ofisi, kila idara, kila taasisi kutembelea duka moja. Hii naona kama vile ni matumizi mabaya ya ofisi na kushindwa kutumia watumishi wachache tulionao, ku-utilize resources tulizonazo katika kuleta tija kubwa zaidi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ninapenda kuzungumzia, hapohapo kwenye utumishi wa umma, tuna idara kwenye elimu inaitwa Quality Insurance (Wathibiti Ubora wa Shule). Kwa mujibu wa Waraka wa 2015 hawa ni watumishi viongozi na waraka umewaelekeza kwamba wao watalipwa mishahara yao kwa LSSE II lakini….

Mheshimiwa Spika, naomba sekunde mbili tu niweze kuhitimisha.

SPIKA: Endelea.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, mpaka tunapozungumza sasa wao hawajapelekwa kwenye hiyo ngazi mpya ya mshahara. Ninaiomba Serikali ione namna ya kuwatia moyo watu hawa. Kwa sababu Waraka umetoka tangu 2015, ni nini kinazuia hawa watu wasipelekwe kwenye mishahara mipya kwa miaka Sita ya kubaki kwenye mishahara ya zamani?

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA ELIMU, UTAMADUNI NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuja kuhitimisha Hoja ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo iliyowekwa Mezani mapema leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kuwashukuru wachangiaji wote wa hoja hii na wachangiaji wa hoja hii kwa siku ya leo walikuwa wachangiaji 16. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Waziri wa Sayansi na Teknolojia, Mheshimiwa Adolf Mkenda, kwa kufafanua hoja mbalimbali ambazo zimeulizwa na Waheshimiwa Wabunge, hali hii itarahisisha sana kuacha mambo mengi ambayo tayari yameshafafanuliwa. Vivyo hivyo, namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro, kwa ufafanuzi alioutoa Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza kwa kusema, kupanga ni kuchagua; kama Taifa na kwa kunukuu maelezo au maneno aliyoyasema Mheshimiwa Profesa Sospeter Muhongo asubuhi ya leo kwamba ili kupata Taifa lililoelimika, lenye maendeleo endelevu, msingi wake mkubwa ni kuwa na elimu bora. Elimu bora ni ile ambayo inazingatia ubunifu, inazingatia uvumbuzi, inazingatia utayari wa Taifa kutengeneza wasomi ambao ni creative na ni innovative. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema Kamati inapokea mchango wa Mheshimiwa Sospeter Muhongo na iko tayari kutoa maazimio ambayo yatatolewa baadaye, lakini kwa hapa nasema maneno machache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia mitaala mipya ya elimu, sera na mitaala ya elimu, mabadiliko haya tuna Imani yatazingatia ubunifu, uvumbuzi, yataipa nguvu COSTECH kuendeleza kufanya tafiti na kubaini bunifu zote nchini kwa lengo la kuweka msingi bora kwa ajili ya kuimarisha maendeleo endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kufanya hayo, ni vyema Serikali ikaona umuhimu wa kuwekeza katika elimu. Kuwekeza kwa maana ya miundombinu, kuwekeza kwa maana ya walimu, kuwekeza kwa maana ya mambo mbalimbali ambayo yanagusa ukuaji wa sekta ya elimu hususani katika kuboresha sekta hii na mwisho wa siku kupata matokeo ambayo yatalisaidia Taifa kusonga mbele kimaendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya elimu, sayansi na teknolojia, yamezungumziwa hususani mambo saba makubwa; la kwanza ni lile ambalo nimeeleza la Mabadiliko ya Sera na Mitaala, lakini suala la ajira ya walimu, elimu ya watu wazima, elimu maalum, bajeti ya miradi ya Wizara kwa ujumla, bajeti ya elimu ya juu na elimu ya kati na VETA kwa maana ya Mamlaka ya Vyuo vya Ufundi na katika eneo hili yamezungumziwa zaidi masuala ya vifaa, walimu na mitaji mbegu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nasema Kamati inaunga mkono mawazo na michango iliyotolewa na Waheshmiwa Wabunge wote 16 juu ya maeneo haya saba katika eneo hilo la Elimu, Sayansi na Teknolojia na Kamati itatoa Maazimio hivi punde. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la Utamaduni, Sanaa na Michezo; mambo makubwa matatu yamezungumziwa na Waheshimiwa Wabunge na tunawapongeza wote ambao wamechangia katika hoja ya Kamati. Sitaweza kuwataja wote, lakini nawashukuru wote ambao wameweka msisitizo katika suala la ukomo wa bajeti ya Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, wote ambao wameweka Hoja katika Sports Betting asilimia tano ya fedha inayotoka kwenye Gaming Board au Bodi ya Michezo kubahatisha lakini wote ambao pia wamechangia na kutoa msisitizo katika ujenzi wa viwanja vya michezo na miundombinu ya michezo kwa ujumla. Hapa napo niseme, kama Taifa, Taifa lolote ambalo linataka kupiga hatua ya maendeleo kwa haraka, ni lazima kuwekeza katika soft power au nguvu laini na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo ndiyo soft power ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, soft power ikifeli, Taifa lolote linalazimika kwenda kwenye hard power kwa maana ya…, ikishindwa kutumia nguvu laini, itakwenda kutumia nguvu ngumu. Nguvu ngumu ni nguvu ya kutumia mabomu, mitutu ya bunduki na kadhalika.

Sasa ili tusiende huko, ni vyema Serikali ikatoa fedha zinazohitajika katika kukuza sekta ya michezo, utamaduni na sanaa ili kuwezesha Wizara hii kutekeleza miradi yote ambayo inategemewa kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda, naomba sasa kujikita moja kwa moja kwenye Maazimio ya Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ufinyu wa bajeti ya Sekta ya Elimu;

Kwa kuwa, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ambayo sehemu kubwa ya bajeti yake ni kwa ajili ya mikopo ya elimu ya juu inakabiliwa na changamoto ya ufinyu wa Bajeti;

Na kwa kuwa, hali hiyo inakwamisha dhamira ya kuimarisha na kuendeleza kujielimisha na kuongeza tija katika maendeleo ya Taifa.

Hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali iendelee kuongeza fedha zinazotengwa kwa ajili ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia; na

(b) Hazina ijitahidi kutoa fedha za Wizara hii kwa wakati kama ambavyo imeidhinishwa na Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu upungufu wa walimu wa amali nchini;

Kwa kuwa, licha ya Serikali kuanza kutekeleza Mtaala Mpya wa Elimu, na kusisitiza mafunzo ya amali, lakini taarifa zimeonesha kuwa kuna upungufu mkubwa wa walimu wa amali;

Na kwa kuwa, kutokuwa na walimu wa amali kwa idadi inayohitajika ni jambo linaloathiri madhumuni ya mitaama mipya na kwamba inaathiri manufaa ya elimu wanayopatiwa wanafunzi;

Kwa hivyo basi, Bunge linaazimia kwamba: -

(a) Serikali iongeze fedha na uwezo wa Vyuo vya Ualimu kuandaa walimu wa amali;

(b) Na hivyo vyuo vya ualimu nchini viweke mkazo katika mafunzo yanayoendana na mitaala mipya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa walimu nchini; kwa kuwa, taarifa ya Serikali imeonesha changamoto ya Sekta ya Elimu ikiwemo: -

(i) Upungufu wa walimu wenye ujuzi unaostahili hususan katika masomo ya Hisabati, Fizikia na masomo mengine ya sayansi;

(ii) Upungufu wa miundombinu na vifaa vya elimu; na

(iii) Uchache na uduni wa zana za kufundishia na kujifunzia.

Na kwa kuwa, hali hiyo inaathiri ubora wa elimu nchini, na kwamba inachangia ufaulu usioridhisha wenye madhara kwa hazina na wataalamu wa Taifa.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba, Serikali iandae mkakati wa kuongeza ajira kwenye sekta yenye mahitaji yanayowezesha utekelezaji bora wa mitaala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ufanisi mbovu wa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu;

Kwa kuwa, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu inayotegemea kuweka mifumo ya taratibu kupata idadi kubwa ya wananchi walioelimika inakabiliwa na changamoto za ufinyu wa bajeti kwa ajili ya kuwezesha upatikanaji wa mikopo ya wanaostahili, kutokupata marejesho ya mikopo ya wanaonufaika na wanaweza kurejesha kupata bodi kuweza kuweka mkazo katika jambo hili ipasavyo.

Na kwa kuwa, mambo hayo yamebainishwa na bodi kushindwa kutekeleza azma yake na kusababisha idadi kubwa ya watanzania wanaostahili kupata mikopo wanufaika wa mikopo hiyo.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba,

(a) Serikali iongeze bajeti ya Bodi ya Mikopo kwa ajili ya kuongeza idadi ya wanafunzi wa elimu ya juu wanaopata mikopo.

(b) Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu iongeze juhudi ya utoaji wa elimu kwa umma kuhusu umuhimu na ulazima wa wanafunzi wanaopata mikopo kurejesha fedha hizo kama sheria inavyoelekeza.

(c) Serikali kwa kutumia balozi iandae taratibu madhubuti ya kufatilia wanufaika wa mikopo ya bodi walioko nje ya nchi ili kuweza kurahisisha urejeshwaji wa mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu sheria, kanuni na taratibu za Bodi ya Mikopo kuendana na wakati;

Kwa kuwa, sheria, kanuni na taratibu zinazotumika na Bodi ya Mikopo zimekuwepo kabla ya bodi kuanza kutoa mikopo kwa wanafunzi wa vyuo vya elimu ya kati na kwamba haziendani na masharti ambayo yanahitajika kwa sasa.

Na kwa kuwa, hali ya sheria na taratibu kupitwa na wakati haitoi mwongozo stahiki kwa sasa na hali inayoweza kuathiri ufanisi.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba, Serikali ifanye mapitio ya sheria, kanuni na taratibu ili kuzihaisha kulingana na mahitaji ya sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchakavu wa miundombinu na upungufu wa wahadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Dodoma;

Kwa kuwa, taarifa za Serikali zimeonesha kuwa Chuo Kikuu cha Dodoma kinakabiliwa na uchakavu wa miundombinu ikiwemo miundombinu ya maji; upungufu wa wahadhiri, uhaba wa mabweni kutokana na badhi ya majengo yake kutumika kama Ofisi za Serikali.

Na kwa kuwa, mambo haya yanakwamisha madhumuni ya chuo katika kutoa elimu bora.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba;

i. Serikali iwezeshe Chuo Kikuu cha Dodoma kuajiri wahadhiri kulingana na uhitaji;

ii. Serikali iongeze jitihada na kuwa na mkakati wa dhamira wa kutatua changamoto ya maji katika Chuo Kikuu cha Dodoma; na

iii. Serikali iongeze kasi ya kukamilisha majengo ya ofisi kwenye Mji wa Serikali ili kuacha kutumia majengo ya Chuo Kikuu cha Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa vyuo vya mafunzo ya ufundi usioendana na mahitaji ya wanafunzi na vitendea kazi;

Kwa kuwa, Serikali imefanya kazi nzuri ya ujenzi wa vyuo vya ufundi kwa maana ya VETA, lakini haijatatua changamoto za idadi ndogo ya wakufunzi, upungufu wa vitendea kazi na ukosefu wa zana za kufundishia na kujifunzia.

Na kwa kuwa, changamoto hizo zinahitajika zisipotatuliwa tija wa ujenzi wa vyuo hivyo itakosekana.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba;

(a) Serikali iwezeshe upatikanaji wa fedha na ununuzi wa vitendea kazi na uandaaji wa zana za kufundishia na kujifunzia; na

(b) Serikali iweze kuajiri wakufunzi wa mafunzo ya ufundi kulingana na mahitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ufinyu wa bajeti kwa ajili ya uendeshaji wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima;

Kwa kuwa, Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima imebainika kukabiliwa na ufinyu wa bajeti.

Na kwa kuwa, ufinyu wa bajeti unaathiri uwezo wa taasisi kuendelea kutoa elimu nje ya mfumo rasmi wa elimu bila malipo na kwamba athari hiyo imekwamisha nia ya kuwezesha wanafunzi walioacha shule kwa sababu mbalimbali ikiwemo ujauzito na kadhalika.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba, Serikali itenge bajeti kwa ajili ya elimu inayotolewa nje ya mfumo rasmi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya uendeshaji wa Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia;

Kwa kuwa, Taasisi za Serikali zinasababisha ufinyu wa bajeti ya COSTECH, hususan eneo la utafiti.

Na kwa kuwa, ufinyu huu wa bajeti unaathiri mwelekeo wa COSTECH, kuwezesha nchi kujielekeza katika sayansi ya teknolojia na ubunifu kwa maendeleo ya haraka ya kiuchumi na kijamii.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba Serikali iendeee kuongeza bajeti inayotengwa kwa ajili ya COSTECH kila mwaka na COSTECH ijiimarishe kuratibu bunifu zote vyuoni na katika jamii kwa lengo la kukuza vipaji na kuleta tija inayotegemewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mradi wa EASTRIP;

Kwa kuwa, utekelezaji wa mradi huu umeripotiwa kuwa wa kusuasua.

Na kwa kuwa, hali hiyo inatokana na tofauti ya mifumo ya kifedha kati ya Benki ya Dunia na Tanzania, taratibu za manunuzi nchini zinasababisha tofauti ya bajeti inayotekelezwa na bei halisi ya vifaa vya ujenzi kuchelewa kukamilika kwa miradi.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba;

(a) Serikali itatue changamoto na tofauti za mifumo ya kifedha ya Benki ya Dunia na Tanzania pamoja na kushughulikia taratibu za ununuzi unavyostahili; na

(b) Serikali iongeze mkazo katika utekelezaji wa Miradi ya EASTRIP ili kuwezesha wanafunzi wengi hususan wanawake kujiunga na vyuo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maazimio kuhusu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo; kukosekana kwa fedha ya miradi ya maendeleo zilizoidhinishwa na Bunge:-

Kwa kuwa, taarifa za Serikali zimeshakuwa; Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo haipokei fedha za miradi ya maendeleo zilizoidhinishwa na Bunge.

Na kwa kuwa, kukosekana kwa fedha hizo zilizoidhinishwa na Bunge ni jambo linalikwamisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo iliyopitishiwa fedha.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba, fedha zote zilizoidhinishwa na Bunge kwa ajili ya miradi ya maendeleo inayotekelezwa na Wizara hii kwa mwaka wa fedha 2023/2024 zitolewe ipasavyo na kwa mwaka wa fedha 2024/2025 Serikali iongeze bajeti ya Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukosekana kwa viwanja vya mpira vyenye hadhi inayokubalika kimataifa:-

Kwa kuwa, Tanzania imefuzu kuwa mwenyeji wa michuano ya AFCON kwa mwaka 2027 lakini haina viwanja vyenye hadhi inayokubalika.

Na kwa kuwa, hatua ya Serikali zilizoanza kwa lengo la kujenga viwanja vya mpira vya Dodoma, Arusha haziridhishi, kutakuwa na ugumu kuendelea kuwa mwenyeji wa michuano ya AFCON, uchumi wetu utapoteza fursa muhimu kutokana na michuano hiyo kutokufanyika Tanzania kama viwanja havitapatikana, na itaathiri heshima na hadhi ya Taifa letu katika masuala ya michezo.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba;

(a) Serikali itoe fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa viwanja hivyo; na

(b) Serikali ijipange kuwa na usimamizi madhubuti wakati wa utekelezaji wa miradi hiyo ili kuwa na ujenzi wenye thamani halisi ya fedha (value for money). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali isiyoridhisha ya Uwanja wa Benjamin Mkapa:-

Kwa kuwa, uchambuzi wa taarifa na hali halisi umeonesha kuwa Uwanja wa Benjamin Mkapa unakabiliwa na changamoto za uchakavu wa eneo la kuchezea mpira (pitch); changamoto ya kutumika kupita kiasi na mfumo wa makusanyo kutokuruhusu viwanja kubaki na sehemu ya makusanyo.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba;
(a) Fedha zinazotengwa kwa ajili ya ukarabati na uendeshaji wa miundombinu ya viwanja, uwanja huo wa Benjamin Mkapa zipatikane kwa wakati;

(b) Serikali iweke utaratibu wa sehemu ya makusanyo kubaki kwa uwanja (retention); na

(c) Serikali iandae mkakati wa kuboresha viwanja vingine ili kupunguza matumizi ya Uwanja wa Benjamin Mkapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Sera na Sheria ya Baraza la Michezo kutoendana na hali halisi:-

Kwa kuwa, uchambuzi umebainisha kwamba, Sera na Sheria ya Baraza la Michezo haziendani na hali halisi licha ya kuwa michezo inachangia takribani asilimia 19 katika Pato la Taifa.

Na kwa kuwa, hali hiyo inayotokana na sheria kuwa zoefu tangu 1976 wakati wa mtizamo tofauti wa kiuchumia inakosesha uzingatiaji wa mchango wake katika Taifa.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba, Serikali ianze mchakato wa kuboresha sera na sheria inayohusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa fedha na watumishi wa Baraza la Kiswahili Tanzania:-

Kwa kuwa, Baraza la Kiswahili Tanzania (BAKITA) linategemea kuwa na mfumo madhubuti wa kusimamia na kukuza maendeleo ya Kiswahili Kitaifa, Kikanda na Kimataifa lakini inakabiliwa na ukosefu wa fedha za kutosha, inakabiliwa na upungufu wa walimu au wakalimani wa lugha mbalimbali.

Na kwa kuwa, hali hiyo ina kasi ndogo ya kubidhahisha Kiswahili na juhudi ndogo za BAKITA kuelimisha wananchi kuhusu matumizi sahihi ya lugha ya Kiswahili na fursa ya kiuchumi kutokana na lugha ya Kiswahili.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba;

(a) Serikali iwezeshe BAKITA kuajiri wataalamu wa lugha ya Kiswahili wenye ujuzi wa lugha nyingine ili kuongeza kasi ya ukuaji wa lugha sanifu ya Kiswahili;

(b) Serikali izingatie ahadi iliyotolewa kwenye Ilani ya CCM aya ya 283(d) kuhusu kuimarishwa kwa mila, desturi, utamaduni na kujenga Taifa lililobora na kuiwezesha BAKITA kuongeza wigo wa kuelimisha umma; na

(c) Serikali iwezeshe BAKITA kufanya tafiti katika nchi ambapo Kiswahili kinabidhaishwa ili kubaini fursa manufaa na namna ya kuwezesha kukistawisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwango duni vya filamu Tanzania:-

Kwa kuwa, Bodi ya Filamu Tanzania yenye dhamira ya kuweka mazingira bora na wezeshi kwa utoaji wa Tasnia ya Filami haijaweza kufanikisha ubora wa filamu Tanzania, kushawishi wasanii kuongeza upeo wao kuhusu filamu na Sanaa Tanzania. Kutoa msukumo kwa wasanii kuwa na script au maandiko yenye ufasaha wa lugha.

Na kwa kuwa, mambo haya yanasabisha mchango hafifu wa tasnia ya elimu katika biashara ya kimataifa na uchumi hasa kwa wasanii na ustawi wa watu wa Tanzania.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia kwamba;

(a) Bodi ya Filamu ifatilie uzingatiaji na uhalisi wa filamu na kutoa msukumo stahiki kwa wasanii; na

(b) Bodi ya Filamu ihakikishe kuwa kuna mwongozo wa wasanii wanaoandaa andiko la filamu (script) ili kuzingatia ufasaha wa lugha na mvuto katika soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Samia Scholarship:-

Kwa kuwa, Mama Samia amefanya jambo jema la kutoa fedha maalum kwa ajili ya motisha kwa vijana kujikita katika masomo ya sayansi.

Na kwa kuwa, hali hii imeonesha uhitaji mkubwa kwa jamii kuhitaji hii sponsorship ya Mama Samia.

Kwa hiyo basi, Bunge linaazimia;

(a) Kumpongeza Mama Samia kwa jambo hili jema kwa jamii ya Tanzania;

(b) Kuhimiza Serikali kuongeza fedha za mfuko huu ili wanufaika waweze kuongezeka zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na michango mingi iliyochangiwa na Waheshimiwa Wabunge wengi kuhusu Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania (Gaming Board of Tanzania), naomba kuongeza Azimio ili Bunge liweze kuazimia azimio hilo lisomeke kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Michezo ya Kubahatisha Tanzania (Tanzania Gaming Board):-

Kwa kuwa, Serikali ilipitishia Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo kupokea asilimia tano ya mapato yatokanayo na kubashiri matokeo ya michezo (sports betting) inayosimamiwa na Bodi ya Michezo ya Kubahatisha.

Na kwa kuwa, Wizara haipokei fedha hizo kwa mtiririko unaoeleweka na hivyo kuathiri utekelezaji wa shughuli za michezo.

Kwa hiyo basi, Bunge liazimie kwamba:-

(a) Serikali ipeleke fedha kwa wakati kama ambavyo inapeleka fedha za OC kila mwezi;

(b) Bunge liazimie kwamba, Serikali ianze mchakato wa kuihamisha Gaming Board kutoka Wizara ya Fedha na kwenda Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo ili kuongeza ufanisi wa michezo ya kubahatisha, lakini vilevile kuongeza tija na kukuza mapato ya Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja kwamba, Bunge lako sasa lipokee Taarifa ya Kamati na likubali maoni na mapendekezo yote ya Kamati kama yalivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja. (Makofi)

(Hoja ilitolewa iamuliwe)

MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kukushukuru kwanza wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii adhimu, hasa tunavyotazamia kupiga hatua kubwa ya maendeleo katika nchi yetu.

Lakini vilevile nitumie fursa hii kuwapongeza sana Waheshimiwa Mawaziri, Waziri Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa; pamoja na Naibu wake Deogratius Ndejembi kwa kazi nzuri ambayo wameanza kuifanya hususani nikiakisi hotuba nzuri ambayo imewasilishwa jana hapa Bungeni. Kimsingi mambo mengi ambayo nilitamani kuyazungumza Mheshimiwa Rais ameyatolea maelekezo jana na nitumie fursa hii kumshukuru na kumpongeza sana japo bado hatujaingia katika mjadala wa kuijadili hiyo hotuba ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumze mambo machache kwa ajili kuendelea kujenga na kuimarisha utumishi wa umma katika nchi yetu. Jambo la kwanza, tuna uhaba mkubwa sana wa watumishi katika sekta zote. Nitakupa mfano, katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto hatuna kabisa Engineer wa Ujenzi. Hakuna Engineer wa Ujenzi kabisa, lakini tunapeleka fedha nyingi kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, tunapeleka fedha nyingi kwa ajili ya vituo vya afya na zahanati. Sasa unaweza kufikiria ni namna gani au ni miujiza gani inatumika kwenda kusimamia ujenzi wa fedha zote hizo za Serikali ambazo zinapelekwa kwenye Halmashauri zetu ikiwa hatuna wataalam kabisa katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sio huyo tu, Halmashauri hiyo hiyo haina Mwanasheria wa Halmashauri, haina mkusanyaji mapato kwa maana DT, hatuna treasurer kabisa kwenye Halmshauri ile. Sasa unaweza kudhani namna gani tuna upungufu mkubwa wa watumishi nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitoka kwenye uhaba huo wa watumishi ambao kimsingi inabidi kutumia nguvu ya ziada kama Taifa, pamoja na vipaumbele ambavyo vimepangwa katika miaka hii mitano, lakini tuwe na namna nzuri kubwa ya kuweza kuongeza na kujaza nafasi hizo za watumishi ili kusudi nguvu kubwa ambayo inawekwa hasa ya uwekezaji wa miradi na fedha nyingi iweze kuwa na tija kwa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maslahi ya watumishi bado ni changamoto, lakini nashukuru limeshatolewa maelekezo, lakini nisisitize tu kwamba hakuna wajibu bila haki kama ambavyo mama jana amesema. Ili tuweze kupata watumishi waweze kuwajibika vizuri ni vyema tukatoa haki kwa watumishi hawa, kwa maana ya malimbikizo ya madeni, wanadai fedha nyingi za likizo, wanadai fedha nyingi za overtime, wanadai fedha watumishi wa umma kwa miaka mingi, sasa pawe na kusudio maalum la kulipa haya madeni ili tuweze kwenda nao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nilitamani kulizungumza ni ushiriki wa watumishi kwenye uchaguzi, kwa maana ya ushiriki kwenye siasa. Ndugu zangu mtakumbuka mwaka jana wakati tunakwenda kwenye Uchaguzi Mkuu, ndipo ulipoanza kutumika rasmi Waraka wa Utumishi wa Umma Na. 1 wa mwaka 2015. Waraka ambao ulitoa maelekezo ni namna gani mtumishi wa umma anakwenda kugombea nafasi za kisiasa hasa ya Ubunge na Udiwani. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; Watanzania wote wanahaki ya kuchagua na kuchaguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa mujibu wa Sheria ya Utumishi wa Umma, mtumishi wa umma anayo haki ya kuwa na chama cha siasa, lakini anayo haki ya kuchagua na kuchaguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watumishi wa umma kwa mujibu sheria hiyohiyo, wamewekewa utaratibu wa namna gani wanaweza kwenda kuchagua na namna gani wanakwenda kuchaguliwa. Namna nzuri ambayo imewekwa kwa mujibu wa sheria ni kwamba, mtumishi ataomba likizo bila malipo kwa miezi miwili na baada ya miezi miwili kwa maana ya ndani ya mchakato huo wa uchaguzi, kama atakuwa ameteuliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi kwenda kugombea kwenye jimbo au nafasi ambayo anakwenda kugombea maana nafasi yake pale itakuwa imekoma ile nafasi ya utumishi. Lakini wapo watumishi wa umma ambao mpaka sasa huu ni mwezi wa kumi wapo likizo ambayo hawajaiomba tena likizo ambayo haina mshahara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa tunatengeneza threat, tunatengeneza uoga kwa watumishi wa umma kwamba wasishiriki kwenye hizi nafasi za kisiasa. Mwisho wa siku, leo tunajisifu ndani ya Bunge letu Tukufu tuna watu wa mchanganyiko tofauti tofauti, tuna wataalam aina tofauti tofauti, hata Mheshimiwa Rais anavyoamua kufanya uteuzi hapati shida, watu wapo wenye taaluma tofauti tofauti. Lakini kama tunatengeneza huu uoga kwa watumishi wa umma kwenda kushiriki uchaguzi, maana yake ni kwamba miaka ijayo, tusishangae tukawa na hao darasa la saba walio wengi zaidi kwenye Bunge hili au kwa sababu ya kukosa ile motisha na namna ambavyo wanaweza wakalindwa wakiwa kwenye utumishi wa umma watakavyokuwa na nia ya kwenda kugombea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Waraka wa Utumishi wa Umma Na. 1 wa mwaka 2015 mtumishi wa umma ikitokea hajachaguliwa kwa maana hajabahatika kupata nafasi yake anapaswa kurejea kwa kuomba kurejeshwa kwenye nafasi yake kwa mujibu wa waraka huo. Lakini kama hajapata nafasi ya kurejeshwa, anapaswa kulipwa mafao yake. (Makofi)

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Husna Sekiboko kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kumpa taarifa mchangiaji. Anachangia vizuri anasema kwamba na….

MBUNGE FULANI: Declare interest.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu spika, na-declare interest kuwa mimi ni darasa la saba. Anasema kwamba humu ndani kuna watu wenye taaluma tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania nafasi ya Ubunge ilitajwa kwamba mgombea Ubunge awe anajua kusoma na kuandika na sisi darasa la saba tunajua kusoma na kuandika, kwa hiyo asitutishe kwamba ikitokea tumekuwa yaani wataalam wamepungua wamebaki darasa la saba, hata sisi tunao uwezo wa kuiongoza Serikali. Nakushuruku sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, huo huwa ni mjadala mrefu, lakini kimsingi hili jumba hili ni la wa wawakilishi.

Kwa hiyo, wananchi yule wanayemleta ndio wanayeona ndio anaweza kuwakilisha hoja zao, yaani hoja ni uwakilishi, ndio maana Rais anakuwa na nafasi zake akiona humu kwenye uwakilishi hakutoshi analeta wa kwake anawapa hizo nafasi.

Kwa hiyo, kila kundi lina umuhimu wake humu ndani na wale wanao wachagua wanajua wanampeleka nani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Sekiboko malizia mchango wako.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, dakika zangu zimepungua naomba unilinde.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimalizie hii hoja kwa kuiomba Serikali sasa, Wakurugenzi hao ni watumishi wa umma na hata kabla ya kuteuliwa kuwa wakurugenzi walitokea kwenye Kanuni za Utumishi wa Umma, na namna ya wao kuingia na kutoka wanasimamiwa na Kanuni za Kudumu za Umma na Standing Order.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Makatibu Tawala wa Wilaya ambao nao ni watumishi wa umma per se, kuna Katibu Tawala wa Mkoa na wa Wilaya, kwa maana ya Makatibu Tawala. Sasa hao wote ningeiomba Serikali kutizama namna nzuri ya ku-handle hili suala lao. Ni kweli waliomba ruhusa wakaenda kugombea, lakini waraka umesema ni miezi miwili huu ni mwezi wa kumi. Ni vyema sasa Serikali itakoa hatma ya hawa watu kwasababu pamoja na kwamba baadhi yao wanatafsirika kama wateule wa Mheshimiwa Rais, lakini wanashughulikiwa kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, awali ya yote niitumie fursa hii kuipongeza Wizara ya Elimu na Serikali kwa ujumla, kwa maamuzi yaliyofanyika kupitia sera ya elimu ya kuanzisha shule za kata, ambazo zinasaidia wanafunzi wengi hasa wale wanaotoka kwenye familia za masikini. Uamuzi huu ulikuwa uamuzi mzuri sana kwa Taifa letu hili linaloendelea kwasababu, imetoa fursa ya watoto wengi wanaoishi kwenye mazingira ya chini kupata fursa hiyo ya kupata elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimejaribu kupitia takwimu takribani kwa sasa tuna shule za kata 3,900, shule hizi zimejengwa kwa nguvu za wananchi na kumaliziwa na Serikali kupitia Wizara yetu ya Elimu na Wizara ya TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hoja yangu leo katika shule hizi ninajaribu kutizama ni namna gani tunaweza tukafanya maboresho na kuzalisha watoto wenye elimu inayostahili, kwa maana ya elimu bora kutoka kwenye shule zetu hizi. Ni mwalimu by professional, shule ili iitwe shule lazima iwe na walimu na wanafunzi lakini lazima iwe na madarasa, maktaba na maabara. Kwa sababu, tunaamini katika elimu, elimu anayopata mwanafunzi darasani ya kufundishwa na mwalimu ni asilimia 25 peke yake zaidi ya asilimia 75 ya ujuzi anaoupata mwanafunzi, inatokana na mazingira yanayomzunguka. Kwa maana anajifunza kutoka kwenye maabara, lakini anajifunza kutoka kwenye maktaba ili kuweza kupata ubunifu na stadi ambazo anastahili kuzipata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye shule zetu hizi zaidi ya 3,900 tunakosa hayo mazingira ya kumuwezesha mwanafunzi kujifunza, kwa maana shule zetu hazina maabara na shule zetu hazina maktaba. Mazingira ya kujifunzia ni magumu sasa nini kifanyike? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe sana Serikali kupitia Wizara ya Elimu na pengine kushirikiana na TAMISEMI ambayo ndio wasimamizi wa hizi shule za kata. Kuangalia sasa namna gani Serikali inaweza kuweka malengo ya makusudi, kukamilisha maabara katika maeneo mengine ambayo zimeshaanza kujengwa. Lakini kuweka maktaba kwa ajili ya kuwasaidia watoto hawa wa wakulima na wanyonge wa Tanzania, waweze kupata elimu sawasawa na watoto wa matajiri na wale wanaoishi kwenye miji mikubwa ambayo ina shule nyingi ambazo zina hali nzuri ya kutolea elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipenda kulizungumza hili kabla sijakuja kwenye hoja yangu ambayo nilitamani kuizungumza zaidi leo kuhusiana na specialization. Namna ya kupanga michepuo kwenye shule zetu na hii sio tu kwa zile shule maalum zinazosimamiwa moja kwa moja na Wizara ya Elimu, lakini vile vile, kwenye hizi shule zetu za kata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kipindi ambacho sisi tulikuwa shuleni tunasoma tulikuwa tunaona, ukienda kwenye shule fulani utakuta kuna mchepuo wa kilimo, ukienda shule nyingine utakuta kuna mchepuo wa ufundi, unaenda shule nyingine ni mchepuo wa sanaa. Haikuwekwa bahati mbaya ilikuwa inawafundisha wanafunzi kujiendeleza kutengeneza ujuzi na maarifa tangu wakiwa katika ngazi za chini kabisa za kupata elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na ukiwa mwalimu ukifundisha kidato cha kwanza mtoto anasoma pale kwa takribani mwaka mmoja, akienda kidato cha pili tayari umeshamfahamu kwamba, huyo mtoto anaweza kwenda kwenye mchepuo gani? Na unamshauri kwenda ku- specialize kupunguza mzigo wa masomo ambao mwisho wa siku hauwezi kumsaidia. Mtoto anapangiwa anakwenda kwenye combination za sayansi, mwingine anakwenda kwenye combination za sanaa, mwingine za biashara. Na mwisho wa siku ndio tunakuja tunapata ma-accountants, tunapata hawa madaktari, tunapata na watu wa namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niiombe na niishauri sana Serikali hoja hii pia ameizungumzia vizuri Mheshimiwa Charles Mwijage, hatuna sababu ya kuwafundisha watoto wetu general education, tutengeneze specifically tunataka mtoto ahitimu akiwa ameiva kwenye eneo gani mahsusi katika elimu anayopata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la specialization kwenye elimu ni suala muhimu sana. Hivi tunalalamika leo tunataka kubadilisha mfumo wa elimu, tunataka kubadilisha mtaala wa elimu, kwa mashaka tu kwamba pengine huu mtaala haumsaidii mtoto kuweza kukabiliana na mazingira anayoyaishi. Lakini kiukweli mtaala hauwezi kutusaidia, kama hatujaamua kumuandaa huyu mtoto kwenye mazingira yake tangu mwanzo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tulikuwa tunasema jana, Mheshimiwa mmoja alizungumza humu ndani, kuna dhambi gani mmasai kuingia darasani na kumfundisha mtoto namna ya kufuga ng’ombe? Kuna dhambi gani kumuita mvuvi, baharia akaingia darasani akamfundisha mtoto namna nzuri ya kuvua samaki? Hata wakati tunasoma walimu walikuwa wanakaa pembeni anamuita traffic anafundisha watoto namna ya kuvuka barabara, ni elimu. Elimu tusiiwekee mipaka kiasi cha kuwafanya wanafunzi wetu kukariri, tutengeneze mazingira ambayo mtoto anaweza kujifunza kadri mazingira yake yanavyomruhusu na kutengeneza ujuzi wa kuweza kuendeleza maisha yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya jambo hilo nizungumze kidogo kuhusiana na soko la elimu. Tumeingia kwenye mazingira ambayo elimu sasa inakwenda kuwa ni biashara. Tuna shule za private na tuna shule za Serikali. Shule za private Mheshimiwa Waziri pia uje ulitizame vizuri, inawezekana kuna namna fulani inatengenezwa siasa ya kuwaaminisha umma kwamba, shule za private ndio zinatoa elimu nzuri kuliko shule za Serikali. Lakini ukweli ni kwamba, shule za Serikali zina mazingira mazuri, zina walimu wa kutosha, zina maeneo mazuri ya watoto kujifunzia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ukitaka kumfundisha mtoto masuala ya kilimo shule ya kata ya msingi labda, Kwemakame ina eneo zuri la kuweza ku-practice kilimo kuliko shule ambayo inapatikana pale Dar es Salaam. Kwa hiyo, tuna haja pia ya kuuza na kutoa namna gani shule zetu zina mazingira mazuri ukilinganisha na hizi za private, mwisho wa siku tutakuwa… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa kengele ya pili imegonga.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa na mimi kuchangia kwenye Wizara yetu hii maalum kabisa ambayo tunatarajia inakwenda kumkomboa mwanamke wa Kitanzania kwenye jambo hili la shida ya maji.

Mheshimiwa Spika, kabla ya kutoa mchango wangu nimpongeze sana kaka yangu Mheshiwa Jumaa Aweso kwa kazi kubwa ambayo ameifanya kwenye Wizara hii, hakika nchi yetu sasa imekuwa na matumaini makubwa ya kutatua kero ya maji, pamoja na Naibu wake dada yangu kipenzi kabisa Engineer Mahundi. Uwezo wao na namna ambavyo wanaongoza hiyo Wizara inatusaidia sana kuwasemea akinamama kwenye jambo hili la maji.

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa nimpongeze sana dada yangu Engineer Upendo Omari Lugongo, Mhandisi Mkuu wa Maji, Mkoa wa Tanga. Anafanya kazi kubwa sana, lakini kazi hii anayoifanya itakuwa na tija kama mambo haya mawili ambayo natamani kuyazungumza yatafanyiwa kazi katika Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza, shida ya maji ni kubwa, pamoja na jitihada kubwa ambazo zinafanywa na Serikali lakini huwa tunapeleka fedha nyingi kwenye kuanzisha miradi mipya lakini tumekuwa tukiiacha miradi ya zamani bila ukarabati. Ukiangalia kwenye Idara zingine kwa mfano Idara ya barabara tukishajenga barabara tunakuwa na ruzuku ya ukarabati wa barabara. Tukijenga vituo vya afya tunakuwa na bajeti kwa ajili ya ukarabati wa vituo vya afya vivyo hivyo kwenye mashule na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, lakini fedha ambazo tunatenga kwa ajili ya ukarabati wa miradi ya maji ni ndogo sana, muda mwingine tunaziachia Jumuiya za Watumia Maji ambazo hazina uwezo. Hizi Jumuiya za Watumia Maji ambazo kwa utaratibu wa sasa tunajenga miradi kwa kutumia fedha nyingi, lakini tunawakabidhi wenzetu waweze kuisimamia na kutumia charges ndogo ndogo ambazo wanachangia wakati wa kuchota maji waweze kukarabati hiyo miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni utaratibu ambao kwa kweli unaweza kutukwamisha katika kutatua tatizo hili la maji katika nchi yetu kwa sababu hizo jumuiya kwanza hazina elimu, hazijaelimishwa vya kutosha, lakini jumuiya hizo zina-charge hao tunaowaita Watanzania wanyonge, Watanzania wa hali ya chini, ukienda huko vijijini hao wanaoenda kuchota maji kwa shilingi 200, mia 300 mpaka 500 ndiyo wale wale ambao tumeona kwamba hawawezi kulipa ada tunawapa elimu bure. Ndiyo wale wale ambao tunawapelekea ruzuku ya TASAF kwa kushindwa kukimu miasha yao. Sasa bado tumewawekea huu mzigo wa kuwa wanachangishana fedha kupitia kwenye visima vya maji, lakini baadaye wakusanye kwa ajili ya kukarabati jambo ambalo tungelifanya sisi kama Serikali, lingekuwa na mantiki kubwa sana katika kutengeneza uendelevu, (sustainability) ya miradi ya maji vijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niishauri sana Serikali ione namna gani sasa inaweka kusudi la dhati katika kukarabati miradi hii hasa visima vile vya vijijini kabisa, kuwapunguzia huu mzigo akina mama wa vijijini ambao wanashindwa kuoga, wanashindwa kunywa maji, wanashindwa kulea watoto wao vizuri. Utakutana nao barabarani wamebeba madumu ya maji kama watoto mgongoni, wanahemea maji mbali kwa kushindwa kulipia gharama za maji muda mwingine lakini kukosa maji maeneo ya Jirani. (Makofi)


Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilitamani kulizungumza ni ukarabati wa mabwawa. Kule Tanga hususani kwenye Wilaya ya Mkinga kuna bwawa pale Duga, kule Handeni kuna mabwawa ya Mandera, Masomanga na Gendagenda. Kule Kilindi kuna bwawa la Kwamaligwa, Kwadudu na Mkuyu, mabwawa haya ni ya siku nyingi yamejengwa takribani kipindi cha uongozi wa Mwalimu Nyerere. Ni mabwawa ambayo yalikuwa na uwezo wa kutoa maji kwenye jamii nyingi, lakini hayajawahi kukarabatiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo sasa wanashindwa kupata maji lakini haya ukijumlisha na ile miradi mikubwa kama Potwe kule Muheza, Maramba kule Mkinga, Magina na Kwesine kule Lushoto ikikarabatiwa hii miradi ya siku nyingi ambayo ilikuwa inazalisha maji na kuhudumia kwa watu wengi zaidi inaweza kutatua kwa sehemu kubwa sana tatizo hili la maji. Lakini kwa sababu, muda ni mfupi sana nimeipitia hiyo hotuba ya Mheshimiwa Waziri inshallah Rais ajaye labda, lakini kuna hii miradi ya payment for result P4R. mikoa nane haijaguswa na hii miradi ikiwemo Mkoa wa Tanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Mkoa wa Tanga ina vijiji 846 lakini kati ya hivyo ni 400 tu vina mtandao wa maji na angalau watu wanapata maji safi na salama. Zaidi ya vijiji 400 kwenye Mkoa wa Tanga hawapati maji kabisa vijiji hivyo havina miundombinu ya maji kabisa, hawapati maji safi na salama. Sasa kwa nini tusipeleke huu mradi niiombe Wizara ya Maji na Serikali ione umuhimu wa kupeleka hii miradi ya P4R kwenye Mkoa wa Tanga. Lakini mwisho kabisa gharama ya maji ni kubwa sana, maeneo mengine tunaona mvua zikinyesha watu wananyanyua mikono juu wanamshukuru Mungu na hapo hawachukui tena maji ya RUWASA wala ya DAWASA wanatumia maji ya mvua kwasababu ya kutafuta ahueni.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Mawasiliano ambayo ni moja ya Wizara muhimu sana katika uchumi wa nchi yetu. Napenda kupitia kwenye mambo mawili, lakini kabla sijapitia huko naomba nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambayo wameanza kuifanya katika Wizara hii mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza ambalo napenda kulizungumza limezungumzwa na Wabunge wengi ni kuhusiana na mawasiliano kwenye baadhi ya vijiji. Actually, inasikitisha na inashangaza sana kwa nchi ya Tanzania nchi ambayo sasa tunajinasibu kwamba tuko kwenye uchumi wa kati lakini tunashindwa kukusanya mapato haya yaliyo wazi kabisa kutoka kwenye simu, kwa kutokupeleka mawasiliano kwenye baadhi ya maeneo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kata nyingi zinakosa mawasiliano lakini pamoja na kukosekana kwa hayo mawasiliano tunayo kampuni yetu ya Serikali ya simu ya TTCL ambayo ingeweza kuchukua hiyo fursa, hiyo changamoto ikageuza kuwa fursa na kwenda kuwekeza kwenye hayo maeneo kwa maana ya kujenga minara na kuweka mawasiliano ya simu na internet kwa ajili ya kurahisisha huduma kwa wananchi, lakini vilevile kupata soko na kuimarisha uchumi wa Shirika hilo. Hata hivyo, hilo halifanyiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii sasa kuishauri Serikali na Shirika letu la TTCL, kuamua kwa dhati kabisa kwenda kuwekeza huduma hii ya mawasiliano katika yale maeneo ambayo mitandao mingine haijafika. Nina mfano wa baadhi ya maeneo kule Lushoto Jimbo la Mlalo kuna maeneo ya Bustani kule Rangwi na kuna maeneo ya Umba kule Mlalo, kuna shida kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia kwenye maeneo ya Muheza kuna Kata inaitwa Kwemigondo ni around kilometa 30 tu kutoka Makao Makuu ya Wilaya pale Muheza, lakini uwezi kuamini kwamba ukaribu wa kiasi hicho kutoka kwenye Makao Makuu ya kwenda kwenye hiko kijiji ama hizo kata hakuna mawasiliano ya simu kabisa siyo makampuni mengine wala siyo kampuni yetu ya TTCL. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii kidogo inaleta shida ni vizuri wenzetu wakaona sasa umuhimu wa kwenda kuwekeza huko siyo tu kwa ajili ya kukusanya mapato kwa sababu wakitumia simu wanalipia siyo tu kwa ajili ya kurahisisha mawasiliano. Lakini vile vile, kwa ajili ya kuwasaidia hawa watu kuwaweka salama kwa maana watakuwa wanapata nafasi nzuri ya kutoa taarifa ya kiusalama pale ambapo panakuwa na changamoto kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ambalo nilitamani kulisema ni kuhusiana na uwekezaji ambao kwenye kampuni ya TTCL. Kampuni kwa kipindi kirefu sasa tangu uhuru, tangu tupate uhuru kampuni hii imekuwa ikifanya kazi kwa mazoea kiasi cha kutokuwa na mabadiliko makubwa ukiendana na uwekezaji mwingine unaofanywa kwenye makampuni ya binafsi. Sasa nishauri Serikali kuwekeza kwa maana ya kufanya pia mapinduzi kwenye utumishi wa kampuni ya hii kwa maana ya kuajiri vijana ambao wanahari na uwezo wa kuwajibika na ambao wako tayari kuwa na mawazo mapya ya kimtandao kama ambavyo yanaonekana sasa kuliko kuendelea kuwekeza fedha nyingi kwenye kampuni hii tunaipa mishahara mingi, lakini hakuna mabadiliko eneo linaloleta tija katika kampuni hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo nilipenda kulizungumzia kuhusiana na gharama za mawasiliano. Hapo kati pametokea sana sinto fahamu ya kupanda na kushuka kwa gharama za mawasiliano hasa kwa maana ya muda wa mazungumzo na bando, lakini bado hatujawa na utaratibu ambao kweli unatu-guide namna gani ambavyo tunaweza tukatumia hizi bando hizi dakika kwenye mitandao mingine ambayo wanafanya biashara, mitandao mingine unakuta wana bei tofauti na mitandao mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama Mtanzania mlaji tuko kwenye soko huria, lakini je kama nchi tunapaswa kununua vifurushi hivi angalau isizidi kiasi gani na isipungue kiasi gani? Ni jambo muhimu sana wananchi wetu wakalifahamu hilo ili waweze kupata huduma hiyo wakiwa wanafahamu kiunagaubaga namna gani inatakiwa kugharamiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumza hayo naomba nikushukuru kwa fursa hii naunga mkono hoja. (Makofi)

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Uchambuzi wa Sheria Ndogo Zilizowasilishwa katika Mkutano wa Pili wa Bunge
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru sana kwa kunipa fursa na mimi kuchangia katika mjadala huu muhimu sana wa sheria ndogo na awali ya yote niwapongeze sana Wajumbe wote wa Kamati hii kwa namna ambavyo wamechakata na kuleta mapendekezo yao juu ya nini sasa kifanyike kwa ajili ya kufanya marekebisho ya sheria hizo.

Mheshimiwa Spika, jambo ambalo limenisimamisha hapa leo ni ushirikishwaji wa wadau kwenye kutunga hizi sheria ndogo kwenye mamlaka zetu. Tumeshuhudia maeneo mengi sheria hizi zimetungwa katika mazingira ambayo hazitekelezeki, lakini katika mazingira mengine sheria hizi zinakinzana moja kwa moja na Katiba na sheria mama.

Mheshimiwa Spika, sasa ninaomba sana Bunge lako pamoja na Kamati hii ya Sheria Ndogo kuzichambua zile sheria ndogo ndogo zote ambazo zinakinzana na sheria mama lakini zinatengeneza mtafaruku kwa wananchi katika utekelezaji wake ili kuendelea kuishi katika nchi ambayo ina amani na utawala wa kisheria.

Mheshimiwa Spika, nitakupa mfano wa sheria moja ndogo ya rumbesa. Kuna sheria ambayo inazuia kupakia mzigo kwenye magunia isizidi kilo kati ya 100(+5 na -5). Lakini namna wanavyotekeleza hii sheria, wanapima yale magunia baada ya kupakiliwa kwenye magari badala ya kupima uzito wa gari kwenye mizani.

Mheshimiwa Spika, mimi ninachofahamu, kama unataka kudhibiti rumbesa na kwa sababu rumbesa imewekwa kwa ajili ya kuwasaidia wakulima wasilanguliwe kwenye biashara ya mazao, pale wakati wa ununuzi wa mazao, kama unanunua mahindi kwenye eneo la soko pale ndipo ambapo vipimo vinasimamiwa, mnunuzi anunue kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizowekwa katika soko lile.

Mheshimiwa Spika, lakini wakati ameshapakia ule mzigo, kwa sababu unakuta mnunuzi mwingine amenunua mahindi au kabichi au karoti, amekwenda kuzimwaga kwenye chumba kimoja halafu baada ya kununua mazao yake yote anakwenda kuyapaki kwenye magunia na kusafirisha. Wakati anapaki kwa kuwa tayari alikuwa ameshapima wakati wa kununua, wakati wa kupaki anaweza kupaki kienyeji kadri ambavyo anaweza ili kuweza kupunguza gharama pia ya vifungashio.

Mheshimiwa Spika, sasa kinachotokea wenzetu wana-block barabarani, wanaweka vizuizi barabarani na kuanza kupima gunia mojamoja ambalo liko ndani ya gari, kinyume na utaratibu ambao umewekwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninaomba sheria hizo zote kwa sababu zimewekwa kwa nia njema na ni sheria nzuri na lengo ni kumlinda Mtanzania aweze kufanya shughuli zake katika mazingira yenye ustawi, ziangaliwe na zitengenezewe kanuni nzuri za utekelezaji ili tusiwaumize hawa pia wanaofanya biashara ya usafirishaji wakati wa kusafirisha mazao haya.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo ninapenda kuchangia ni hili la kuandaa sheria hizi kwa mujibu wa sheria mama. Tumeona katika mazingira mengi, na moja amelizungumza Mheshimiwa Naibu Spika kwenye taarifa yake, uki-park gari vibaya Dar es Salaam, gharama ambayo unapigwa inakwenda tofauti na gharama ile ya tozo/faini za magari kwa maana ya makosa barabarani; zinakwenda tofauti.

Mheshimiwa Spika, lakini sheria ambayo tunaifuata ya msingi ni ile ya faini za barabarani. Kwa nini huyu wa jiji akamate tozo kubwa ya faini unapo-park sehemu pengine ambayo siyo rasmi, au unapofanya kosa lolote la matumizi ya magari kwenye maeneo hayo, tofauti na ile tozo mama ambayo imekuwa-defined kwenye sheria.

Mheshimiwa Spika, maeneo hayo yote yakifanyiwa kazi tutaendelea kuishi kwenye mazingira ambayo kila mmoja ataiheshimu sheria na mwisho wa siku tutaendelea kufanya vizuri.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Taarifa, Mheshimiwa Ester Bulaya.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nilikuwa tu nampa taarifa kwa sheria ndogo ndogo ambazo zinakera, kulikuwa na mgomo wa waendesha bajaji wa Musoma Mjini, Manispaa ile Halmashauri ni ya Chama cha Mapinduzi. Bajaji akimpeleka mteja haruhusiwi kumpakiza mtu, arudi kwenye kituo chake bila abiria, akipakiza faini shilingi 3000. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Husna, unapokea Taarifa hiyo?

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, ubaya wa hizi sheria ndogo nyingi zimetungwa kipindi cha miaka mitano iliyopita ambapo halmashauri zetu nyingi zilikuwa na mchanganyiko wa vyama vingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee mchango wangu kwenye eneo la elimu, tuna sheria nzuri sana nchini, lakini wananchi hawazifahamu sheria kwa sababu hakuna utolewaji …

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Esther Matiko.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe tu taarifa Mheshimiwa Husna kwamba tukiangalia michango yote ni kwamba kweli hizi sheria ndogo ndogo zinakera, lakini ukitaka kuweka mizania ya vyama mchanganyiko na nini kwa zaidi ya asilimia 80 Halmashauri zilikuwa chini ya Chama cha Mapinduzi na sheria nyingi ambazo zinakera nyingi nyingi Tanzania zimetungwa na hao wa Chama cha Mapinduzi.

Kwa hiyo tuondoe mambo ya uvyama tuangalie nini solution kubwa kwa kuondoa hizi kero ndogo ndogo tukianza kuchagiza CHADEMA, CCM mtajikuta mnajimaliza, maana yake zaidi ya asilimia 80 ilikuwa chini ya Chama cha Mapinduzi, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Taarifa hiyo Mheshimiwa Husna unaipokea?

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, siipokei hiyo taarifa kwa sababu Mheshimiwa Esther Matiko alikuwa ana nafasi ya kuomba kuchangia, nimuombe tu aheshimu nafasi yangu ya kuchangia ili niweze kumaliza mchango wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatizo kubwa la utekelezaji wa sheria nchini ni watu kukosa elimu juuu ya sheria na unafahamu kabisa kwamba kutokujua sheria siyo utetezi mbele ya sheria. Ningeomba sana Kamati ya Sheria Ndogo hii ya Bunge kuelekeza mamlaka zetu kutoa elimu kwa wananchi kabla ya utekelezaji wa sheria iliyotengenezwa kwenda kutekelezwa, hii itatusaidia sana kupunguza migogoro, kupunguza manung’uniko na mwisho wa siku kutekeleza sheria hizi katika hali ambayo ni salama kwa ajili ya malengo ya sheria zilizotengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana kwa kunipa ruhusa ya kuzungumza, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa fursa na kuweza kuweka mchango wangu katika hoja zilizowasilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naunga mkono hoja. Baada ya kuunga mkono hoja naomba nijikite katika mambo makuu matatu; jambo la kwanza ni afya, hususan katika taasisi ya MSD, jambo la pili nitazungumzia kidogo kuhusu elimu na baadaye nitazungumzia kuhusu Baraza la Michezo Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika taarifa ya huduma na maendeleo ya jamii iliyowasilishwa, moja ya changamoto kubwa ambayo imekithiri ni upungufu wa dawa nchini. Ukifuatilia hata katika ground, huko site, utakubaliana na mimi kwamba, pamoja na upungufu mkubwa wa dawa zipo dawa ambazo katika maeneo yote hazikuwahi kuwa tatizo, dawa hizo ni kama panadol na paracetamol.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siri ya uwepo wa hizo dawa muda wote ni kwa sababu, sehemu kubwa ya dawa hizi zinazalishwa nchini kupitia Kiwanda cha MSD pale Keko. Kupitia kiwanda cha Idofi kule Makambako Njombe ambacho kinazalisha vifaatiba na tayari kinajiwekeza katika kuzalisha dawa zaidi nchini. Tumekuwa na fursa nzuri ya kuweza kupata baadhi ya dawa ambazo zinatosheleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni nini maoni yangu katika jambo hili; Serikali sasa iamue kwa dhati kuwekeza kwa nguvu katika kuanzisha viwanda vya dawa nchini. Viwanda vya dawa nchini ndio njia pekee ambayo itatuondosha kwenye kadhia hii kubwa nchini ya upungufu wa dawa kwa binadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, anafanya kazi kubwa sana katika ujenzi wa miundombinu ya kutolea huduma nchini. Tumeona madarasa mengi sana yamejengwa katika eneo la elimu, tumeona vituo vya afya na zahanati zinaendelea kujengwa kwa wingi sana, lakini majengo hayo hayatakuwa na tija ya kutisha kama hatutakuwa na vifaa pamoja na dawa katika zahanati na vituo vyetu vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya eneo ambalo linakwamisha sana upatikanaji wa dawa ni namna ambavyo dawa zinaingizwa nchini. Imeelezwa kwamba, dawa mpaka ifike kwa mlaji ikiagizwa kutoka nje inachukua kati ya miezi sita mpaka miezi nane. Kipindi hicho inawezekana dawa nyingine ikawa tayari imeanza kuelekea kwenye kwisha kwa muda wake wa matumizi. Hali hii imesababisha hasara kubwa kwa Serikali kupitia MSD na dawa nyingi zimeangamizwa kwa kupita muda wake wa matumizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia kwamba, bado tuna upungufu mkubwa wa dawa katika maeneo yetu, ushauri wangu ni kwamba, namna ambavyo tunaweza tukatatua jambo hili ni kuhakikisha kwamba, sasa tunaenda kwa dhati kuwekeza katika ujenzi wa viwanda vya dawa nchini. Hilo liende sambamba na ajira za watumishi wa idara ya afya, hilo liende sambamba na ule Muswada wa kuhakikisha kwamba, sasa tunapitisha huduma ya afya kwa wote nchini. Tukiwezesha hayo, tutakuwa tumetatua kadhia hii ya huduma ya afya kwa wananchi wetu hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni katika suala la elimu. Kwa kipindi kirefu binafsi tangu nimeingia kwenye Bunge hili nimekuwa nikiuliza maswali, lakini nilikuwa nikichangia ni namna gani Serikali ina-accommodate wale vijana ambao wanashindwa kuendelea na masomo baada ya kuwa wameshindwa mitihani katika level ya darasa la sab ana kidato cha nne au kidato cha sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namna pekee ya kwenda ku-accommodate vijana hawa ni kutoa elimu ya ufundi kwa mikopo. Nashukuru sana maoni ya Kamati yamelimeweka hili jambo vizuri. Nisisitize, kwa kuwa, Serikali hii ni ya watu wote si ya wale ambao wanafaulu peke yake, Serikali hii inawahusu wale pia wanaoshindwa mitihani, ni vizuri sasa ikaja na utaratibu mzuri wa kuweza kuwa-accommodate hao kupitia vyuo vya ufundi kwa kuwapa mikopo ya kufanya masomo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya muda suala la BMT nitalizungumza siku nyingine. Naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kutofuata Maelekezo ya Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kupata nafasi ya kuchangia mjadala huu muhimu sana kwa mstakabali wa Wizara ya Elimu na Taifa letu kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii, na mimi nataka nielekee moja kwa moja kwenye hadidu ya rejea iliyotokana na maelekezo yako ndani ya Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Spika, itakumbukwa kwamba maelekezo yaliyokuja kwenye Kamati yalikuwa ni kuona na kusikiliza Wizara pamoja Bodi ya Mikopo kama kuna pingamizi, kuna resistance au kuna kupingwa kwa maelekezo ya Wizara. Hata hivyo, kabla sijaendelea nataka kulithibitishia Bunge lako, mimi ni msema kweli na nitasema kweli daima, hakuna chembe chembe za kuzuia au kutokutekelezwa kwa maelekezo ya Wizara kwenye Bodi ya Mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Waziri alipofika mbele ya Kamati alieleza kwa uwazi kwamba yeye hana shida na Bodi ya Mikopo. Na maelezo yake alithibitisha kwa kuonesha kwamba yeye ndiyo mwenye mamlaka ya kuiwajibisha Bodi, na kwamba kama kungekuwa na namna yoyote ya kupingwa na Bodi angechukua hatua kwa sababu ipo kwenye mamlaka yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini alikwenda mbali zaidi, akasema maelekezo aliyoyatoa yote yalitekelezwa na Bodi, kwa hiyo hakuna suala la resistance. Hii inakinzana na maelezo ambayo yalitolewa mbele ya Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Bodi ya Mikopo walithibitisha kwamba siku ambayo Wizara iliitembelea Bodi, ilikuwa ni mwaliko wa Bodi ya Mikopo kwa ajili ya kwenda kuzindua utaratibu mpya wa utolewaji wa mikopo kwa mwaka 2022/2023. Wakati Wizara imefika kwenye Bodi, ilienda pamoja na Wajumbe wa Kamati ambao Mheshimiwa Waziri aliwateua na Waziri alitoa maelekezo. Kwamba analeta Kamati husika ambayo aliitambulisha katika mkutano huo kwa ajili ya kufanya uchunguzi wa mambo kadhaa, lakini hapakuwa na maandishi.

Mheshimiwa Spika, government works on paper, hapakuwa na maelekezo ya kimaandishi kutoka kwa Katibu Mkuu wa Wizara kwenda kwenye Bodi kuelekeza namna gani timu hiyo itakwenda kufanya kazi na hadidu za rejea ni zipi. Jambo hilo lilisababisha kuchelewa kutekelezwa kwa maelekezo hayo. Mpaka ilipoandikwa barua, Bodi haikuleta resistance, ilitekeleza. Kwa kuthibitisha hayo Bodi iliongeza hadidu za rejea katika hadidu za rejea mbili zilizopelekwa kwenye Bodi na Katibu Mkuu wa Wizara. Hii inatuonesha kwamba Bodi ilikuwa tayari kufanya kazi na Kamati iliyoundwa na Waziri.

Mheshimiwa Spika, lakini mbali zaidi, Bodi imegharimia gharama za Wajumbe wa Timu ya Uchunguzi kwenye Bodi ya Mikopo, Bodi ndiyo imegharamia. Hii inathibitisha pia kwamba hapakuwa na shida yoyote ya utekelezaji wa maelekezo ya Waziri kwenye Bodi.

Mheshimiwa Spika, shida ambayo tumeiona kubwa ni mawasiliano na mahusiano. Mbele ya Kamati tumethibitishiwa hilo, lakini namna ambavyo taarifa zimekuja pia imeonekana kuna namna fulani ama kuna hofu ndani ya Wizara au kuna hofu inatengenezwa kwenye Bodi, jambo ambalo linakwamisha utekelezaji wa majukumu katika maeneo hayo mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ushauri Wangu; Mheshimiwa Kitila Mkumbo ameeleza vizuri, kwamba kama Waziri angetoa tamko hata kwenye vyombo vya habari, ingekuwa ni ngumu kutekelezwa na Bodi kama hapakwenda maandishi mahsusi kwa ajili ya tamko la Waziri. Na kwa kuwa machinery ya Waziri ipo; kuna Katibu Mkuu, kuna Katibu wa Waziri wao wangeweza kushusha yale maelekezo kwa maandishi kwa Bodi ingerahisha utekelezaji wa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri na hizi resistance ambazo zinazungumziwa leo zisingekuwepo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kikubwa ambacho naishauri Serikali ni kuimarisha mifumo ya mawasiliano. Kiongozi anapotoa maelekezo kwenye taasisi, wanaohusika kushusha hayo maelekezo kwa maandishi wafanye jambo hilo kwa wakati ili kuondoa hii mikanganyiko ambayo inaweza kutokea na kupoteza muda kama inavyotokea sasa.

Mheshimiwa Spika, utulivu ulio sasa kwenye Bodi ya Mikopo, mtakumbuka takribani miaka sita sasa inatengenezwa na namna ambavyo machinery ya Bodi inafanya kazi yake vizuri. Twende mbali zaidi, tusije tukahukumu mtu badala ya mfumo. Mfumo uliopo, Bodi ya Mikopo inatekeleza, inatoa mikopo kwa idadi ya wanafunzi kulingana na kiasi cha bajeti iliyopelekewa. Hapa tunaweza kuizungumzia Bodi kama wameshindwa kuwalipa hao watoto kwa wakati, lakini kama watoto wamelipwa kwa wakati hata kama wangelipwa watoto watatu kulingana na bajeti iliyopelekwa, hilo sio jambo la bodi ni jambo la Serikali kukaa chini, kuangalia namna nzuri ya kuongeza wanufaika wa Bodi kwa maana ya kupanua bajeti ya Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu ili kuleta tija zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana naunga mkono hoja ya Kamati. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa fursa kuweka mchango wangu leo kwenye Wizara hii nyeti katika maendeleo ya nchi yetu. Awali ya yote nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais mama yetu shupavu, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara hii ipo Ofisi ya Rais, kupitia Mheshimiwa Rais tumeona fedha nyingi zimepelekwa kwenye halmashauri zetu kwa ajili ya miradi mbalimbali. Zimeenda fedha nyingi kwenye miradi ya afya, miradi ya elimu na miradi ya maji, hususani katika hizo huduma muhimu kwa jamii.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli kwa dhati kabisa ni muda wa kumpongeza na kumtia moyo sana yeye pamoja na wanaomsaidia katika hii ili tuweze kupata tija kubwa zaidi katika maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na fedha nyingi ambazo zinapelekwa kwenye halmashauri zetu, tuna changamoto kubwa sana ya miradi viporo, tuna miradi ya muda mrefu ambayo inasuasua. Inawezekana tunashindwa kusimamia vizuri, namna gani ambavyo tunaweza tukasaidia halmashauri zetu kuhakikisha kwamba miradi inayoanzishwa isikae muda mrefu sana bila kukamilishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ili kuweza kutengeneza usimamizi mzuri, miradi inayoanzishwa iweze kukamilika kwa wakati kuna haja kubwa sana ya kuboresha kada ya Madiwani. Madiwani ndio wasimamizi wakubwa wa shughuli katika halmashauri na kwa mujibu wa majukumu yao, Madiwani ndio kiungo kati ya wananchi na halmashauri yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na majukumu mengine ambayo yameainishwa katika Kanuni za Kudumu za Madiwani namba 72(1) na (2). Madiwani wana hali mbaya, wana hali mbaya kwa sababu hawajawezeshwa kufanya kazi kwa maana ya kuzunguka kwenye kata zao, kijiji kwa kijiji kusimamia miradi ya maendeleo ambayo inaendelea kwenye maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili Diwani aweze kufanya kazi vizuri, anahitaji kusafiri kutoka eneo moja hadi eneo lingine, lakini posho ambayo wanalipwa, ni ndogo sana na mwisho wa siku tumeishia kuwalaumu Waheshimiwa Madiwani katika maeneo yetu kwamba pengine kada hiyo ipo lakini hatuoni tija kutokana na nafasi ambayo wamepewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili tuweze kwenda kupata tija kwenye halmashauri, Wizara ya TAMISEMI, tukizungumzia TAMISEMI, tunazungumzia halmashauri zetu nchini, tunazungumzia Waheshimiwa Madiwani, Waheshimiwa Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa kwa ujumla wake. Sasa ili waweze kuleta tija kwa nafasi zao, kuna haja ya kutazama upya, kuangalia namna gani tunaweza tukasaidia kuboresha maslahi ya Madiwani, maslahi ya Wenyeviti wa Vijiji na Wenyeviti wa Mitaa… (Makofi)

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Husna Sekiboko, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Neema Mwandabila.

T A A R I F A

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nilitaka nimpe taarifa Mheshimiwa Husna Sekiboko kuhusu maslahi ya Madiwani, nataka kumwambia kwamba kazi wanaoifanya yote hiyo lakini bado hawana mshahara na posho wanayopewa ni ndogo sana kiasi kwamba utekelezaji wa kazi kwao unakuwa mgumu. Ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Husna Sekiboko, unapokea taarifa hiyo?

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, naipokea hiyo taarifa kwa mikono miwili. Nataka nimwambie Mheshimiwa Neema, kwa mujibu wa Kanuni za Kudumu za Madiwani, kanuni 84(1) na (2) kifungu cha kwanza kinasema wajumbe wa Baraza la Madiwani watalipwa posho kulingana na mapendekezo ya halmashauri zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili tayari ni tatizo na ni kichaka baadhi ya Wakurugenzi kubana maslahi ya madiwani. Kwa maana kwamba halmashauri inasizingizia kuwa imepewa nafasi itawalipa kulingana na makusanyo au kulingana na uwezo. Hivi, ni nani alichagua kuzaliwa Mbeya, Dar es Salaam au Kakonko ambako makusanyo ni madogo, hakuna ambaye amechagua kuzaliwa Singida, wote hao wamezaliwa kwenye hayo maeneo bila kuchagua. Kwa nini walipwe kulingana na makusanyo ya halmashauri? Ikiwa wanatumika, wanafanya kazi zinazofanana katika muda wote na wanaisaidia Serikali katika majukumu ambayo yameainishwa katika kifungu cha 72A. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili Diwani aweze kufanya kazi vizuri, pamoja na posho ambayo tumeihamisha kutoka kwenye halmashauri inalipwa sasa Serikali Kuu tulete usawa, Madiwani nchi zima walipwe kama ni mshahara, sio kwenye posho waende kwenye mshahara walipwe sawa, lakini posho zao ziwe na tija hapo tutaweza kuona uwajibikaji wao na mwisho wa siku, hizi fedha ambazo tunapeleka TAMISEMI, trillions of money kwenda TAMISEMI, zitakuwa na wasimamizi wazuri na tutaona tija ya miradi ambayo tumeipelekea fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukizungumzia ten percent, ambayo tunazopeleka kwa akinamama, vijana na wenye ulemavu, msimamizi number one ni halmashauri na ndio mtekelezaji, lakini nataka nikuhakikishie wako Waheshimiwa Madiwani ambao hata hii ten percent hawajapata nafasi ya kuelimishwa vizuri na kujua namna gani wanaenda kuisimamia. Hii inatokana na nini? Ni udhaifu, tumeshawatengenezea Madiwani udhaifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekuwa Diwani kwa miaka mitano, tangu 2010 mpaka 2015, Mkuu wa Idara ambaye sasa anapaswa kusimamiwa na Diwani, yeye ndiyo mkubwa kwenye halmashauri. Mtendaji wa Kata ambaye ni Katibu wa Ward C Diwani ni Mwenyekiti, yeye ndiyo mkubwa kwenye kata? Kwa nini? Kinachomjengea heshima ni kipato anachopewa. Madiwani wetu siwasemi kwa ubaya, lakini wanakopa kwa watendaji, hivi leo umetoka kwa Mtendaji wa Kata, umekopa kwa Mkuu wa Idara, kesho utakwenda kumsimamia afanye kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna haja kuamua kwa dhati kabisa kama tunataka kuleta tija, TAMISEMI tuangalie upya kada ya Madiwani. Madiwani wapewe nafasi ya kuwajibika baada ya kuboreshewa maslahi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie kuhusiana na vifaa tiba, pamekuwa na mjadala kidogo baina ya Mheshimiwa Mabula, kuhusiana na Mheshimiwa Mzanva kuhusu vifaa tiba. lakini nataka nikupe mifano, kuna zahanati zimekamilika ni mwaka wa pili sasa hazifanyi kazi, majengo yanachakaa kwa sababu hamna vifaa tiba. Tuna vituo vya afya vimekamilika, tuna hostel, pale Magamba Wilaya ya Lushoto, inaanza kubomoka, hakuna vifaa. Sasa tukianza kujigawanya na kuamua ni wakati gani tununue vifaa tiba na wakati gani tujenge majengo tutakuwa pengine hatufanyi vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la msingi ambalo nataka niishauri Serikali ni kwamba, tukamilishe miradi yote ambayo imeshaanzishwa kabla hatujaanzisha miradi mipya, ili tupate nafasi ya kuhakikisha kwamba miradi iliyopo inakamilika lakini vilevile na vifaa ambavyo vinatakiwa kwenye miradi hiyo na vyenyewe vinaweza kupelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nikushukuru sana lakini niendelee kuipongeza Wizara ila nitoe…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, ila nitoe ombi moja kwa Wizara ya TAMISEMI watazame upya…

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga, ni jambo jipya unaanza au unamalizia sentensi?

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii. Nami nianze kwa kuzipongeza Kamati zote mbili na taarifa zilizowasilishwa, lakini nimpongeze zaidi Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuwaletea maendeleo wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namuomba Mwenyezi Mungu anisaidie lakini leo nina jambo moja tu mahsusi kama nitajaliwa kuongea na lingine basi ni kwa rehema za Mwenyezi Mungu. Jambo lenyewe ni ubora wa elimu yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2022 inaonesha tumeendelea kupata matokeo mabaya hasa kwenye mitihani ya watoto ya sayansi. Tumeendelea kuwa na matokeo mabaya hasa kwenye shule zetu za Serikali. Tumeendelea kuwa na matokeo mabaya ya sayansi lakini tumeendelea kuwa na upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2022 tulihitaji kuwa na walimu 19,216 wa hesabu, tulifanikiwa kupata Walimu 5,537. Tunao upungufu wa Walimu 13,679 kwa asilimia, tuna upungufu wa Walimu kwa asilimia 71, huo upungufu wa walimu asilimia 71 umesababisha watoto kufeli somo la hesabu kwa asilimia 83.

Mheshimiwa Spika, suala la somo la fizikia, (physics) tulihitaji kuwa na Walimu Elfu Kumi na Sita na kidogo, tumekuwa na walimu elfu tatu na kidogo. Tumekuwa na upungufu wa walimu elfu kumi na mbili na kidogo, tumepata upungufu kwa asilimia 77. Failure ambayo imesababishwa na huo upungufu wa Walimu ni asilimia 82, tunawekeza kwenye standard gauge, tunawekeza kwenye ujenzi wa barabara kubwa kubwa fly overs tunawekeza kwenye ujenzi wa mahospitali ya rufaa chungu nzima, tumewekeza kwenye miundombinu mizuri sana excellent nani anakwenda kuihudumia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumewekeza vya kutosha kwenye majengo na mimi nataka nimpongeze sana mama yangu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan tumejennga sana madarasa, mama umefanya kazi kubwa mno kwenye ujenzi wa madarasa! Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge tuishauri Serikali sasa wageukie kuajiri walimu namna pekee itakayo tutoa kwenye hii failure ni kusaidia kuajiri walimu walioko mtaani waende watusaidie kuwafundisha watoto.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana wa 2022, walimu walioomba kuajiriwa TAMISEMI walikuwa 165,948 tumeajiri walimu takribani 16,000 kutoka kwenye 165,948. Katika hao walimu 30,000 ni Walimu wa Sayansi walioajiriwa ni takribani walimu 5000 wa sayansi kutoka kwenye walimu 30,000. Tunataka muujiza, hatutatoka kwenye hizi failures kama hatutawekeza vya kutosha katika kuajiri walimu kwenye nchi hii. Tutaondoa namna ya kuwa grade shule zilizofanya vizuri na ambazo hazijafanya vizuri, tutaondoa wala haina shida. Lakini haitakuwa suluhisho la kufuta sifuri mashuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukizungumzia walimu kuna principle inasema kitu chochote kisipotumika kwa muda mrefu kinakuwa butu hata kisu usipokitumia kwa muda mrefu lazima wakati wa kukitumia lazima ukinoe kwanza. Tunaajiri leo walimu waliohitimu 2015 tunawapeleka shule wanaenda kufundisha hakuna programu yoyote ya kuwanoa, kuwakumbusha kuwarudisha kwenye nafasi yao ya kwenda ku-perform vizuri, hatufanyi hivyo! Mbaya zaidi leo kwa taarifa nilizonazo mara ya mwisho tumewaajiri walimu wa sayansi mwisho tuliishia 2017.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2018, mwaka 2019, mwaka 2020, mwaka 2021na mwaka 2022 miaka mitano au sita hawajaariwa. Hii miaka ya karibuni wote wako mtaani hawajaajiriwa, sasa utakavyowaajiri hawa watu mtu ambaye ameshinda kwenye kijiwe cha kahawa ama cha bodaboda kwa miaka mitano mfululizo unampeleka shuleni akafanye muujiza gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namna ya kwenda kuboresha hili nataka niishauri Serikali, walimu walioko mtaani hawa zaidi ya laki moja. Tunaupungufu mkubwa kuliko hawa walimu walioko mtaani, tukifanya hili tutasaidia Serikali katika mambo mawili. Jambo la kwanza ni kuendelea kuwafanya wawe active, pili tutakuwa tumepunguza pia huo upungufu wa walimu ambao umesababisha hii failure ambayo tunaiona sasa.

Mheshimiwa Spika, jambo lenyewe tuajiri kutumia ajira za muda mfupi. Kwa sababu nchi yetu tunaijua, bado ni nchi inaendelea bado ni nchi maskini uwezo wa kutoa ajira zote hizo kwa wakati mmoja nchi yetu haiwezi tunafanya shughuli nyingine nyingi ambazo zote tunazihitaji. Sasa kwa sababu ya upungufu wa fedha bajeti ndogo tuliyonayo tuwapeleke hawa Walimu wakafundishe kwa maana ya ajira za mkataba za muda mfupi mfupi. Tukiwatawanya kwenye mashule huko kwanza tumepunguza upungufu wa Walimu lakini at the same time tumewasaidia kuimarisha wasisahau, wasibweteke, wasiwe butu na mwisho wa siku kutusaidia katika kuongeza ufaulu mashuleni.

Mheshimiwa Spika,sisi tulitembelea Chuo cha Mwalimu Nyerere pale Butiama. Tulikuta kwa mika kumi na tatu chuo kina watumishi zaidi ya arobaini. Kwa miaka
13 hakijafanya udahili na wale watumishi wanalipwa mishahara ya Serikali OC zinakwenda zinatumika lakini tukija tuna upungufu wa walimu wa hesabu tuna maprofesa tumewaweka pale for 13 years hawajafanya kazi.

Mheshimiwa Spika, tunakwenda wapi? Hebu twende na vipaumbele kama Taifa. Kama lengo letu ni kuisaidia Nchi hii maskini ipige hatua lazima tujiulize changamoto zetu sisi ni zipi? Changamoto yetu kubwa ni elimu, elimu, elimu! Tunahitaji kuelimisha watu wetu kwanza wajitegemee. Tumezoea kuwaambia watu jamani someni mjiajiri, well and good! Tunaweza kujiajiri, hebu niambie mimi Mwalimu wa Historia nimefundishwa niende nikamfundishe mtoto Zinjanthropus ni nini? Niende nikamfundishe mtoto evolution of man ni nini? Haya sijaajiriwa mimi niende nikajiajiri kwenye nini? Wapi nitapewa kazi ya kuelezea evolution of man… wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namna pekee ya kunitumia mimi ni kunipa nafasi ya kwenda kufundisha hiyo evolution of man. Mtume Mohamed Swalala walah wasaalam katika maisha yake alikutana na swahaba mmoja aliyekuwa na busara sana, aliona Mtume anaishi vizuri sana na watu akamfuata akamwambia, Ya Mohammad…’ ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu nipe ushauri, nishauri mimi’. Mtume akamjibu akamwambia la tagadhabu! akarudia tena kwa sababu hakuwa anaamini kwamba huo ndiyo ushauri atakaopewa na Mtume Mohamed.

SPIKA: Sekunde thelethini kengele ya pili imeshagonga.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, akamwambia eeh! Mtume Mwenyezi Mungu nishauri, mara tatu akamwambia la tagadhabu! anamwambia usigadhabike. Nimejitahidi sana hivi nivyozungumza nimejizuia nisigadhabike, lakini hali halisi iliyopo huko tunapotoka, mimi natoka kijiini ndugu zangu, hali halisi iliyoko huko watu wanapata shida.

Mheshimiwa Spika, mtu kasomesha mwanae bado anaenda kumhudumia ‘libaba’ liko pale unalipika ugali, hajaajiriwa, unaangalia aliyeko shule naye anafeli, kwa nini anafeli hamna mwalimu! mwalimu unaye nyumbani unampikia ugali! Inna lillahi Mwenyezi Mungu atusaidie! Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa fursa leo tena kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu na kuchangia Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa maamuzi yake ya upendo sana kwa kuongeza kima cha chini cha mshahara mpaka asilimia 23.3. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri, dada yangu Ummy Ally Mwalimu kwa kazi kubwa anayochapa kwenye Wizara hii akiambatana na kaka yangu pale Mheshimiwa Dkt. Mollel. Kwa kweli katika Wizara ambazo sisi Wajumbe wa Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii tunakuwa comfortable nazo ni pamoja na Wizara ya Afya. Tunawapongeza sana, tunawapongeza sana ongezeni hiyo spirit ya kuwajibika kwa ajili ya nchi yetu ili tuweze kutengeneza maisha bora kwa kila Mtanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesimama leo kwa ajili ya jambo moja tu, huduma ya mama na mtoto. Huduma ya mama na mtoto ukisoma Sera ya Afya, ukisoma miongozo yote ya afya inaeleza namna gani Serikali imepanga kuokoa vifo vya mama na mtoto hasa kwa kuondoa tozo na fedha zote ambazo mama mjamzito na mtoto mchanga wanaweza kugharamia kipindi hicho.

Mheshimiwa Spika, uhalisia ulivyo ni tofauti kabisa na miongozo yetu inavyotolewa. Nimshukuru sana mchangiaji aliyemaliza Mheshimiwa Munde ameligusia na ametoa msisitizo vizuri kwamba hali ilivyo ni tofauti kabisa na miongozo ambayo inawekwa mezani.

Mheshimiwa Spika, nitakupa mfano wa baadhi ya maeneo, Kilindi kuna Kata moja inaitwa Kwasunga ipo zaidi ya kilometa 100 kutoka kwenye Kituo cha Afya Mkata. Akina mama wa Kwasunga wanajifungua njiani kuelekea kwenye kituo cha afya. Lakini pamoja na kwamba wanajifungua njiani wakifika hospitalini kwenye Kituo cha Afya Mkata hawana fedha, hawapati huduma. Kama siyo fedha waende na ile package, gloves na nini kwa ajili ya kwenda kujifungulia. Lakini ukija kwenye utaratibu wa Sera na Miongozo inasema huduma ya mama na mtoto ni bure.

Mheshimiwa Spika, niliombe Bunge na niiombe Serikali kama kuna sehemu tunataka kufanya siasa siyo kwenye huduma ya mama na mtoto. Huduma ya mama na mtoto ni ustawi wa Taifa letu kwa ujumla, ni eneo ambalo ni nyeti na ndiyo inasababisha kwenye ustawi wa shughuli zetu za maendeleo kama tutakuwa na mama mwenye afya akajifungua mtoto mwenye afya bora. Sasa bila kusimamia kwa dhati kwa sababu Sera zipo, Miongozo ipo lakini utekelezaji umekuwa mgumu. Bila kusimamia eneo hili la utekelezaji sawasawa bado tutakuwa tunafanya siasa na kifo cha mama na mtoto nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale Majengo–Korogwe Hospitali ya Wilaya yameshatokea haya akinamama wameenda kujifungua wameombwa fedha bila fedha na wanapiga simu. Mheshimwia Waziri nataka nikwambie moja ya eneo ambalo nimetangaza vita na watoa huduma ya afya kwenye Mkoa wa Tanga ni hili la afya ya mama na mtoto. Nimewapa namba zangu za simu wale akinamama wakishamuingiza kwenye kumi na nane mtoa huduma anayeoomba fedha, Mheshimiwa Waziri nitamsukumia kwako na ikitokea umechukua muda Mheshimiwa dada yangu Ummy Mwalimu nakupenda sana lakini kwenye eneo hili kama haitapatikana tiba ya dhati ya kuondoa kweli kwa dhati na kwenye utekelezaji ikaonekana kwamba mama na mtoto wanapata huduma bure. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sitaki kusema naweza kushika Shilingi ya Mheshimiwa Waziri. Lakini eneo hili ni gumu, eneo hili linatia uchungu akinamama wanapata shida, kipato chao ni kidogo hata hicho ambacho Serikali imeamua kukitengeneza kwa ajili yao na chenyewe hakipatikani. Namuomba sana Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya windup atoe maelekezo ya Serikali ni kwa namna gani wataenda kusimamia perpendicularly kwa dhati kabisa mama na mtoto apate huduma bora bila malipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii. Kwa sababu ya muda naomba niende moja kwa moja kwenye mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan na Serikali anayoingoza kwa kazi kubwa na nzuri ambazo tunaendelea kuzishuhudia huko kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2022 katika Mkutano wa Bunge uliopita kama nakumbuka vizuri ilikuwa ni Septemba au around Desemba, nilizungumzia vigezo na mambo ambayo yanapaswa kuzingatia katika kuboresha elimu. Mchango wangu wa leo naomba niendelee pale nilipoishia mwaka jana 2022.

Mheshimiwa Spika, moja ya eneo ambalo litatusaidia kuboresha elimu Tanzania ni kuhakikisha kwamba kila mtoto anapata fursa ya kusoma au ya kujifunza katika mazingira yanayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, amezungumza Mheshimiwa Regina Ndege, kuhusiana na mabweni au hosteli za watoto wa kike, lakini kwa upande wa Mkoa wa Tanga hususan Wilaya ya Lushoto, jambo hilo ni critical zaidi. Naomba nitoe mfano kwamba, sera au tamko la Serikali kwa sasa elimu inatolewa bila malipo, lakini wapo wazazi ambao wanapeleka watoto shule kwa gharama ya takribani kuanzia shilingi 600,000 mpaka Shilingi milioni moja kwa mwaka na ni shule ya Kata. Kwa namna gani?

Mheshimiwa Spika, Shule ya Sekondari Mlola, watoto wanaotoka Makanya, hilo ni Jimbo la Lushoto, wanakwenda umbali wa zaidi ya kilomita 20 kuifuata elimu ya sekondari. Kinachotokea ni nini? Hawana uwezo wa kutembea kilomita 20, kwenda na kilometa 20 kurudi nyumbani. Wazazi wanalazimika kuwapangishia vyumba waishi karibu na shule ili waweze kupata elimu hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mzazi anakodi pango la chumba cha mtoto aweze kwenda shule, mzazi ananunua godoro, mzazi ananunua vyakula, anamwekea mtoto ili aweze kwenda shule. Huku nyumbani mzazi huyu usisahau ni yule ambaye tunampa TASAF kila mwaka kwa ajili ya kujikimu maisha yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kinachotokea kwenye Wilaya ya Lushoto mahususi, wazazi wengi na nimefanya mikutano nao, wametamka wenyewe. Wamesema, wanafikia mahali hawashawishiki na kuwasaidia watoto wao kufaulu mitihani ya darasa la saba, na wengi wanazungumza na watoto wao wafeli mitihani ya darasa saba ili kumpunguzia mzazi adha ya kuongeza hii gharama ya kumpeleka mtoto shule ya sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili limetokea, Mheshimiwa Mkenda ana taarifa nalo. Kwenye Wilaya ya Lushoto, Tarafa ya Mlola tuna upungufu wa watoto watoto 1,600 ambao walipaswa kwenda sekondari kwa mwaka huu hawaja kwenda, kwa nini? Kwa sababu hawajafikia kiwango cha ufaulu kilichotakiwa kwa mwaka 2022. Kwa nini? Kwa sababu wazazi wamekaa na hao watoto wakakubaliana wafeli. Kwa nini? Kwa sababu gharama ya kumsomesha huyo mtoto kwenye shule ya kata ni kubwa mno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunazungumzia elimu bila malipo, lakini wanaonufaika nayo ni wale ambao wanaishi karibu na hizo shule. Wale wanaoishi mbali na shule hizo, hawafurahii elimu inayotolewa bila malipo. Wanalipa gharama kubwa mno kwa ajili ya kusomesha watoto wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nini kifanyike? Kwanza kabla ya nini kifanyike, hoja hii tafsiri yake ni nini? Halmashauri ya Lushoto kwa mfano, makusanyo yake kwa mwaka ni around Shilingi bilioni 1.5 mpaka point 7. Watoto 1,600 ambao hawafanikiwa, maana yake kuna gap, kwa maana kila darasa lina upungufu wa watoto kuanzia 15 mpaka 20. Kwa maneno mengine, tafsiri yake ni kwamba, kuna vyumba vya madarasa ambavyo havina watoto kabisa wa kusoma.

Mheshimiwa Spika, tumepeleka fedha kila darasa lijengwe kwa Shilingi milioni 20. Ukiangalia hao watoto 1,600 vyumba vya madarasa vinavyohitajika ni takribani 40. Vyumba 40 mara 20,000 ni shilingi milioni 800. Kwa hiyo, tumepata hasara kwa kila mwaka ya shilingi milioni 800. Makusanyo yetu ni Shilingi bilioni 1.5 mpaka
7. Tunakwenda taratibu sana, hatuwezi kupiga hatua ya maendeleo kwa mpango huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeishauri Serikali, kwanza tunapozungumzia suala la ujenzi wa mabweni, tunapozungumza sasa, Wilaya ya Lushoto, Wilaya ya Kilindi na Wilaya ya Korogwe Vijijini, ni jambo ambalo mlichukulie kama special case. Ni jambo ambalo linahitaji jicho la tatu la Serikali. Hali ni mbaya, elimu inashuka, na hatutaweza kuipandisha.

Mheshimiwa Spika, mimi ni mwalimu by professional. Hatutaweza kupandisha kiwango cha elimu kwa kupeleka key performance indicator. Huu unakuwa tayari ni mgogoro. Mheshimiwa Kairuki, nikushauri dada yangu, kama kuna sehemu unataka kutengenezea mtego, ni huu mpango au huu mkataba wa key performance indicator. Mwalimu amekuwa ameshaandaliwa chuoni, ana uwezo wa kumfundisha mtoto afaulu kwa mujibu wa taaluma yake. Ukimpelekea mpango nje ya taaluma yake, unamtoa kwenye reli aache kufundisha, aanze ku-deal na mpango ambao umepelekwa na TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, mara nyingi tunasema, TAMISEMI watusaidie jambo moja, yale masuala yanayohusu taaluma, wawaachie Wizara ya Elimu wayafanye. Wafanye yale mambo ambayo ni ya miundombinu; kujenga madarasa jengeni, kujenga barabara jengeni, lakini suala la taaluma ni sehemu nyeti ambayo inapaswa isimamiwe na wenye taaluma yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo Mheshimiwa Waziri nataka nikwambie, kuna kamgomo baridi, usipoangalia katatokea Dhahiri. Walimu hawaridhiki na namna ambavyo wanapelekewa maagizo na maelekezo mbalimbali kutoka TAMISEMI. Walimu wanaona mnaiacha professional yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niseme wazi, hiki mnachokifanya kwa walimu, hebu mjaribu kupeleka afya, mjaribu kupeleka kwenye taaluma nyingine. Kwa nini muichezee taaluma ya walimu peke yake? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali, kama lengo ni kuongeza ubora, kunyanyua ubora wa elimu Tanzania, boresheni maslahi ya walimu, watajiongeza. Kama lengo ni kuongeza ubora wa elimu Tanzania, pelekeni crash programs, wafundisheni huko, waboresheni na wafundishwe na wataalamu waliowafundisha kwenye vyuo vyao. Wataboreka na elimu yetu itakuwa nzuri zaidi; lakini hili suala la kupeleka mikataba ambayo haipo kwenye taaluma, inakwamisha shughuli za walimu na mwisho wa siku haitatuweka kwenye nafasi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kupata fursa na mimi kuweka mchango wangu kwenye bajeti ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijatoa mchango wangu naomba nitumie fursa hii kuipongeza sana Serikali. Kuipongeza Serikali kwa sababu yapo mambo mengi ambayo tumekuwa tukisimama mbele ya Bunge lako Tukufu tunashauri Serikali namna ya kuboresha elimu ya Tanzania, tumeshuhudia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri lakini tumeshuhudia kwenye mijadala mbalimbali ya Mheshimiwa Waziri na Kamati ya Kudumu ya Bunge, yameendelea kutekelezwa na yanaonesha kuleta tija kubwa katika mabadiliko ya elimu nchini, ninapongeza sana kwa jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote ni mashahidi, binafsi tangu nimeingia kwenye Bunge hili pamekuwa na mjadala mkubwa wa uhitaji wa mabadiliko ya elimu Tanzania. Watu wamekuwa na kiu ya kuona elimu ya Tanzania inatolewa kwa kuleta mabadiliko ya mtu mmoja mmoja baada ya kuhitimu. Tumekuwa na uhitaji wa kushuhudia elimu ya Tanzania inamsaidia kijana wa Tanzania kujiajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mkakati huu wa kutekeleza maombi na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge ndani ya Bunge hili kwa kuamua kuleta mtaala mpya wa elimu, hii ni dhahiri kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi ni Serikali sikivu, ni dhahiri kwamba Wizara hii ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeamua kusikiliza mawazo na kutekeleza kadri ambavyo imeweza. Ninawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wazo hili la kubadilisha mitaala liliafikiwa na Rais wetu kipenzi, Mama Samia Suluhu Hassan na alilitolea maelekezo Madhubuti, na yeye kama Mama, kama Kiongozi alishagundua yapo maeneo ambayo yana mapungufu na yanahitaji kufanyiwa kazi ili elimu yetu iweze kuwa bora. Mimi nataka niseme pamoja na mambo mengi mazuri ambayo yamewekwa kwenye mitaala mipya, lakini jambo la kuweka internship kwa walimu, jambo la kuhakikisha kwamba mwalimu kabla hajaajiriwa anajitolea kwa mwaka mzima kwenda kufanya internship kazini kuimarisha ujuzi wake, ni jambo kubwa ni mabadiliko makubwa na ni jambo ambalo litaboresha sana elimu ya Tanzania. Niendelee kupongeza kwa jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nianze kuchangia. Kama mtakumbuka vizuri kwenye mchango wangu juu ya Wizara, wakati nachangia Wizara ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, niliishauri na niliiomba Serikali ije na mkakati wa maksudi wa kupunguza upungufu wa walimu kwenye mashule yetu. Nilikuja na takwimu, nilionyesha namna ambavyo kuna pengo kubwa kutoka kwa walimu wanaohitimu, walimu walioko mtaani na walimu ambao wanaajiriwa kila mwaka, nikashauri kwamba inawezekana kupunguza hili wimbi au pengo la upungufu wa walimu mashuleni kwa kutengeneza utaratibu wa kuajiri kwa mkataba au kuajiri kwa muda, kuleta ajira za muda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge litakuwa limerekodi kwenye Hansard. Majibu yaliyotolewa na Serikali ilikuwa ni kwamba Serikali haina mwongozo, hakuna utaratibu wa walimu kujitolea lakini walimu wengi wapo mashuleni wanajitolea, nataka niseme jambo moja, tunapozungumza sasa katika ngazi ya awali tunahitaji kuwa na walimu 61,487. Walimu waliopo mashuleni ni 8,619, upungufu wa walimu kwa ngazi ya awali pekeyake ni walimu 52,868. Huu upungufu ni mkubwa sana, upungufu ni mkubwa lakini walimu wapo mtaani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda sekondari vivyo hivyo, tuna uhitaji wa walimu laki tatu na zaidi lakini walimu walioko shuleni ni laki moja na kidogo. Kwa hiyo tuna upungufu wa zaidi ya walimu 100,000. Ukienda kwenye shule za msingi ni hivyo hivyo na inapelekea kama nchi sasa kuwa na zaidi ya upungufu wa walimu 300,000 kwenye mashule yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa nilizonazo Mama yetu, kipenzi chetu Mheshimiwa Rais ametangaza ajira za walimu hivi karibuni. Ajira ni kama 29,000 kama nakumbuka vizuri lakini walioomba ni zaidi ya walimu 300,000. Imagine tatizo ni kubwa namna gani? Tunawezaje kwenda kulitatua tatizo hili kwa kufikiria kwamba hatuwezi kuwa-consider wale ambao wanajitolea kwa sababu hatuna mwongozo. Hii siyo sawa na hii siyo sahihi. Niendelee kusisitiza na kuiomba Serikali tuleteeni mwongozo, walimu waliohitimu vyuo vya ualimu wapate nafasi ya kwenda kujitolea. Wanapojitolea mambo mawili yanatokea kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ni wao kuimarisha ujuzi wao na kujikumbushia yale material yasiweze kupotea, lakini jambo la pili wanatupunguzia upungufu gap ya walimu kwenye mashule yetu. Watoto watapata nafasi ya kusoma. Hili hatuwezi kuliacha pembeni kwa majibu kwamba hatuna mwongozo. Majibu hayo hayatoshi, hayatoshelezi. Kwa hiyo tunaiomba sana Serikali ifikirie namna nyingine ya kuleta mfumo au mwongozo ili tuweze kuajiri walimu wengi zaidi kwa mkataba kwa sababu sisi wote ni Watanzania, tunajua hali ya nchi yetu hatuna uwezo wa kutoa ajira kwa walimu 300,000 kwa pamoja lakini basi walau.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafanya ujasiriamali. Huko kwenye m-pesa tumeajiri walimu wenye certificate, wenye diploma, wenye degree. Unamlipa mwalimu shilingi 100,000 kwa mwezi na anafanya hiyo kazi. Anafanya shughuli ambazo wala hajazisomea lakini yuko pale kwa ajili ya kutafuta angalau tonge la kila siku. Sasa kama Serikali itaamua kuajiri kwa mkataba au kutengeneza utaratibu wa walimu kujitolea maana yake ni kwamba bajeti inaweza kutumika ndogo lakini ikawa imetatua matatizo mawili kwa wakati mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu wadhibiti ubora elimu. Ukizungumzia ubora wa elimu hawa wadhibiti ni kama tunavyochukulia nafasi ya CAG kwenye Hesabu za Serikali. Wao ndiyo wanaangali utaratibu, utekelezaji na namna ambavyo elimu inaendelezwa katika maeneo yetu, katika shule zetu na kadhalika. Nilizungumza mwaka jana katika bajeti iliyopita nikaiomba Serikali, hawa kwa nia njema kabisa huko nyuma Serikali iliamua kuwabadilishia muundo kuwatoa kwenye watumishi wa kawaida kuwapeleka kweye watumishi viongozi ili walau maslahi yao yaweze kuongezeka na mwisho wa siku kazi zao ziweze kufanyika kwa ufanisi. Niiombe Serikali na nimuombe Mheshimiwa Mkenda, Mheshimiwa Mkenda wewe ni Mwalimu na tunafahamu uwezo wako na sasa hivi una mama mmoja jembe sana, Profesa Carolyne Nombo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge, Katibu Mkuu tuliye naye Wizara ya Elimu sasa ni Katibu Mkuu mwenye weledi mkubwa. Mimi nimefanya kazi katika Kamati hii na nimeshirikiana na Wizara hii ya Elimu tangu nimeingia hapa Bungeni, na nimeshapita na Makatibu Wakuu zaidi ya watatu lakini Katibu Mkuu tuliyenaye sasa ni Katibu Mkuu kweli kweli. Anatoa ushirikiano, anajibu hoja za Wabunge, anakerwa na yale ambayo sisi Wabunge tuna kerwa nayo. Hongera sana Mheshimiwa Waziri, hongera sana Mheshimiwa Nombo, lakini mwisho wa siku tunachoomba, yale ambayo tunayashauri kama wawakilishi wa wananchi basi yachukuliwe hatua ili wananchi ambao tunawawakilisha nao waone kwamba tumefanya kazi yetu vizuri. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Husna Sekiboko kengele ya pili imelia.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, naunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. HUSNA J. SEKIBOBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia mchana wa leo. Awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutubariki sote kupata nafasi ya kuongea siku hii ya leo. Nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa bajeti nzuri sana ambayo imewasilishwa kwetu na Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwigulu Nchemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mwigulu bajeti ambayo umewasilisha kwetu, imeleta matumaini makubwa na tunaamini katika mwaka huu wa fedha, kuelekea hata 2025 mambo ya Chama cha Mapinduzi yatakuwa barabara, kwa nini? Kwa sababu bajeti imejielekeza zaidi katika kutatua kero na changamoto za wananchi, kwa nini? Kwa sababu bajeti ambayo umewasilisha inakwenda kupunguza mzigo wa maisha kwa akina mama masikini waliokuwa wanasomesha watoto wao kwenye elimu ya kati kwa gharama kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aliwahi kuishi Mtume Mohammad S.A.W katika maisha yake aliyowahi kuishi zama hizo na maswahaba wenzake. Maswahaba wakawa wanamuuliza, walikuwa wakimuona kila muda anatembea na tasbihi anamuomba Mwenyezi Mungu maghfilla amsamehe, lakini yeye tunaamini katika sisi waislamu ndio kiongozi ambaye ni mwema zaidi katika sisi wanadamu wa kiislamu. Kwamba ni kiongozi wetu katika dini. Wao waliamini ni katika yule ambaye hana makosa, hana dhambi, ni mtu mwema mbele ya Mwenyezi Mungu. Lakini muda wote alitembea na tasbihi na kuomba maghilla Eh! Mwenyezi Mungu nisamehe. Wakamuhoji wewe Mtume wa Mwenyezi Mungu tunajua wewe unaswali unafunga, unafanya sadaka unafanya kila jema ambalo Mwenyezi Mungu ameamrisha lakini mbona muda wote wewe astaghfirullah inakuwaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mtume Mohammad S.A.W akawajibu maswahaba kwamba, bora ni yule anayemjua na kumwabudu Mwenyezi Mungu, bora siyo huyo unayemuona kwamba wewe ni kiongozi wetu lakini yule anayemuogopa mwenyezi Mungu ndio bora. Lakini akasema Mungu tunaemuabudu anapenda kutajwa sana, anapenda kuimbwa, kuombwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikwambie tumpe sifa anayostahili Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, yeye hana sifa ya Mungu kwamba anapenda kusemwa sana, lakini yeye anastahili kusemwa sana kwa nini? Kwa sababu ya yale mema mazuri ambayo anayafanya katika Taifa letu. Mheshimiwa Mwigulu Lameck Nchemba Waziri wa Fedha, na hapa ninukuu maelezo aliyokuwa ametangulia kusema Mheshimiwa Reuben Kwagilwa, amezungumza vizuri sana, ame-narrate vizuri kazi kubwa ambayo inafanyika kwenye Wizara ya fedha. Lakini nataka niseme wewe ni katika watu pia ambao wanastahili kusemwa vizuri, siyo kwa sababu unapenda kusemwa lakini unastahili kwa yale mazuri ambayo unayoedelea kuyafanya katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimesema hapo mwanzo Mungu alisema yeye anapenda sana kuombwa na hivyo hata viongozi wetu wa kidunia msichoke, mpende kuombwa na mimi nakuja sasa kwenye ombi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi juzi Serikali imefanya allocation ya wanafunzi kwenda kidato cha tano katika mashule yetu. Jambo la kusikitisha kweli kweli wapo wanafunzi wenye ufaulu mzuri sana division two, wamekosa nafasi za kwenda kusoma boarding wamekosa nafasi ya kwenda kidato cha tano hata day. Nina mfano wa wanafunzi ambao nimeletewa, lakini nina mwanafunzi hapa ana division two ya point 21 ana C ya Chemistry, ana C ya Biology, ana C ya masomo mengi na combination zaidi ya mbili zime – balance, amekosa shule. Nimefanya consultation kwa Naibu Waziri wa TAMISEMI, Nimezungumza na Naibu Waziri wa Elimu, nimeongea na Naibu Katibu Mkuu - TAMISEMI maelezo ninayopewa hakuna nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi kosa lake yeye ni nini? Kufaulu kupata division two ya point 21 ndiyo kosa lake? Kosa lake ni nini mwanafunzi wa namna hii? Tunapotaka kutengeneza nchi ambayo ina elimu tutakayotaka kuifanya iwe chachu ya kuchachuza uchumi wa nchi hii, lazima tuheshimu maono maombi na fikra za watoto wanazoziweka kwenye malengo yao ya kupata elimu. Mtoto amefaulu vizuri amekosa nafasi ya kwenda shule, je, kosa la kwake ni lipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikizingatiwa mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan anatoa elimu bure kwa kidato cha tano na cha sita. Huyu mtoto wa masikini mama yake anachoma vitumbua, anauza magimbi mtaani, amekosa nafasi ya kupeleka mwanae shule. Mwanae aliyefaulu kwa division two, tunamuweka katika kundi gani? Ninaiomba sana Serikali itoe maelekezo mahsusi kwa watoto ambao wamefaulu vizuri, watoto ambao wanastahili kwenda kidato cha tano kwa mwaka huu watafutiwe nafasi waende, kwa sababu ukimpeleka mtoto huyo kwenye chuo cha kati, siyo lengo lake na nina mfano wa mtoto mwingine ambae amepangiwa Chuo cha Uhasibu Arusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua umewasha mic lakini nirihusu nimalizie. Mtoto amepangiwa Chuo cha Uhasinu Arusha ana F ya hesabu, hajawahi kusoma masomo ya biashara, alifaulu masomo ya arts na masomo ya sayansi. Je, unampeleka kwenye accounts, kwenye chuo cha biashara unategemea akafanye muujiza gani? Je, ule mtaala mpya tunaopigia chapuo humu ndani kwamba tuende kwenye mtaala mpya wa elimu. Je, kama tutawapeleka watoto kwa mtindo huu, amesoma amasomo haya, interest yake ni kusoma kitu hiki wewe umempeleka kitu kingine tofauti. Tunategemea nini kwenye Taifa hili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema ni vyema tukaheshimu maono na maombi ya wanafunzi, kwa sababu kila wanavyomaliza shule huwa wanajaza fomu kipaumbele chake ni kwenda wapi, anapojaza anataka kwenda kidato cha tano. Mtoto apelekwe akasome ili tuweze kuendeleza vipaji vyao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa fursa na mimi kuchangia bajeti hii lakini awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa busara na maamuzi magumu aliyoyafanya kuiweka sekta hii kwenye Wizara kamili, ni jambo kubwa sana na ni jambo la kupongezwa.

Mheshimiwa Spika, mpaka Mheshimiwa Rais anafanya maamuzi ya kusimamisha Wizara hii kuwa Wizara kamili ameangalia mambo mengi, ameona nchi yetu inahitaji ustawi wa hali ya juu na tukiangalia kwenye mazingira yetu tunapotoka tunaona sehemu kubwa ya changamoto zinazokabili Taifa letu ni maendeleo ya Jamii, nataka niseme jambo moja kuna usemi kwamba siasa hapo ulipo; politics is local. Siasa ya nchi yetu locality yetu, changamoto zetu ni changamoto za mwanamke na mtoto wa kike, hizo ndizo changamoto kubwa ambazo tunaza Tanzania na nitasema kwa nini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu na wachangiaji wengi hapa wamezungumzia masuala ya ukatili wa kijinsia wamezungumzia namna ambavyo watoto wetu wananyanyasika kwenye maeneo mbalimbali, lakini nataka niseme ukweli watoto wengi wanaopata hayo manyanyaso ni watoto wa maskini, sijaona mtoto wa tajiri au pengine sio wengi ambao wanapitia kwenye hayo manyanyaso na hii ni sababu ya umasikini. Kama tunataka kutatua changamoto ya unyanyasaji wa kijinsia, ukatili wa aina yoyote, jambo la kwanza kabisa ni kuziimarisha familia zetu kiuchumi. Leo tunazungumzia suala la kusimamisha mawakili kwenye Halmashauri kwenye Idara ya Maendeleo ya Jamii ili kumsaidia mwanamke anapolia na mirathi apate msaada wa kisheria, mtoto wake anapobakwa apate msaada wa kisheria, lakini hii ni nini ni kwa sababu familia zetu nyingi ni maskini, wenye uwezo wa kusimamisha mawakili watetezi, wanasheria kwenye mahakama zetu ni wale ambao wana uwezo wa kifedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nini niishauri Serikali; kwenye Halmashauri zetu tuna asilimia 10 tuliyotenga kwa ajili ya kukopesha vijana, kinamama na watu wenye ulemavu, lakini hile fedha haitoshi, niiombe sana Serikali na niiombe Wizara hii, iangalie namna nzuri ya kuweza kuweka mikopo ya akinamama na hususani akinamama kwenye Halmashauri zetu ili familia zetu ziweze kuimarisha kiuchumi, waweze kusimamia vizuri malezi kwenye familia zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, malezi na mmomonyoko wa maadili kwa namna nyingi na kwa maeneo mengi umesababishwa na akinamama na akinababa kuhemea mpaka usiku wa manane kuwaacha watoto peke yao, watoto wengi ambao unaambiwa wameenda kulelewa na familia nyingine na baba mkubwa na shangazi ni wale ambao unakuta kwenye familia baba, mama ameenda kuhemea anashinda shambani, anarudi usiku, baba anaenda kutafuta anarudi usiku, muda wa kuzungumza na watoto kwenye familia hakuna wote wanakwenda kuhemea. Sasa namna nzuri ni kuimarisha hizi familia kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano Wilaya ya Lushoto, Wilaya ya Kilindi, Wilaya ya Handeni ni Wilaya ambazo zipo pembezoni Wilaya hizi makusanyo yake hayafiki hata shilingi bilioni 1.5 kwa mwaka, mapato ya ndani ukisema hata utenge asilimia 10 haifiki hata shilingi bilioni moja kwa mwaka, lakini akinamama ni wengi, nini sasa kifanyike maana yake Serikali i-subsidize hiyo ten percent, iongozee kwenye zile Wilaya za pembeni kuwawezesha akinamama wengi zaidi kuweza kupata mikopo ya bei nafuu na hili liendane sambamba tumekuwa na wimbo wa muda mrefu wa Benki ya Wanawake Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini mpaka tunavyozungumza sasa hatujaona effectiveness ya hiyo Benki ya Wanawake Tanzania imewakopesha akinamama vijijini huko wangapi, imewawezesha kubadiisha maisha ya akinamama wangapi, hii bado halijaleta tija ningeomba sana ningeishauri Wizara hii iangalie namna nzuri ya kutenga fungu maalum kwa ajili ya kuwakopesha akinamama hasa akinamama maskini ambao wapo Wilaya maskini ambazo zipo pembezoni ambapo mapato yao hayafanani kama Wilaya za mjini, halmashauri zao zina mapato madogo ambayo ukitenga hiyo ten percent haiwasaidii akinamama kuwainua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo la dawati la kijinsia na mwaka jana niliuliza swali la msingi humu ndani, kuna sababu gani lile dawati la kijinsia kukaa polisi? Familia zetu tunafahamiana akinamama na Watoto wengi wanaogopa kwenda kwenye vituo vya polisi, dawati lile lingesogezwa kwenye huduma ya maendeleo ya jamii, kwenye ustawi wa jamii, hospitali matukio mengi yangeripotiwa na tungepata namna nzuri ya kushughulikia hayo matukio na mwisho wa siku jamii yetu ingestaarabika.

Mheshimiwa Spika, kwa ajili ya muda naunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa, 2022
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nami nashukuru kwa kupata fursa ya kuchangia Muswada huu.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, ambaye kiukweli ndiye anayejaribu kuleta furaha kwa Watanzania na kutufuta machozi kupitia Wizara hii kupitia kwa Kiongozi wetu Mheshimiwa George Simbachawene, kwa sababu unapofanyia kazi maafa maana yake unataka kuleta furaha na kuondoa huzuni kwa Watanzania, tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati Mheshimiwa Mwinyi anamalizia, amesema maafa yanakuja kwa dharura lakini maafa yanatokana na majanga mbalimbali. Yapo majanga ambayo yanasababishwa na shughuli za binadamu, lakini yapo majanga ambayo yanakuja kwa kadri ya Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Spika, ukisoma Muswada huu, hasa katika dhumuni, malengo na sababu ya Muswada inalenga katika kuzuia majanga. Ninawapongeza sana Wizara pamoja na Kamati ya Katiba na Sheria, wamefanya kazi nzuri ya kujikita zaidi katika kuzuia majanga na siyo kupambana na changamoto za majanga.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongezee tu jambo kwamba ili kuzuia haya majanga, kuna maeneo mengi ya kufanyiakazi, eneo kubwa na muhimu ambalo ninapenda Wizara walichukue ni matumizi mazuri ya Jeshi letu la Zimamoto, hasa kupitia mipango miji katika Majiji na Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, tumeona changamoto kubwa ya maafa yanayotokana na moto kushindwa kuzimwa ama kudhibitiwa kwa wakati ni kutokana na magari yale kushindwa kuingia katika eneo la matukio kwa sababu ya kukosa njia au barabara ya kufika huko. Kwa hiyo wakati tunapambana na njia za kuzuia, wakati tunapambana namna ya kuelimisha jamii mara kwa mara, tuangalie namna ambavyo Kamati zote hizi ambazo zimetajwa kwenye Muswada huu zitasaidiwa katika kupanga vizuri Miji na kutoa nafasi ya vikosi vyetu vya zimamoto kuweza kufanya kazi kwa ufanisi mara majanga hayo yanapotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, majanga yanatokea kwa dharura, lakini majanga yanaweza kukingwa kama tutatoa elimu ya kutosha. Katika majukumu ya Kamati elekezi za Wilaya, Kamati za Mikoa mpaka kwenye Mitaa na Vijiji, pamoja na majukumu mazuri mengi ambayo yameainishwa pale, sijaliona jukumu la Kamati hizi kutoa elimu za kila siku namna ya kukabiliana na majanga.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninaishauri Serikali kwamba wakati wanajumuisha watusaidie namna ya kuingiza litamkwe kisheria kwamba Kamati hizo zisisubiri janga litokee ili wadhibiti, ziendelee kutoa elimu kadri muda unavyokwenda, kadri hali ya hewa na majanga mbalimbali yanavyotokea ili kuweza kuwasaidia wananchi wetu kutokupoteza maisha.

Mheshimiwa Spika, nimesoma Ibara ya 17, kipengele kile cha Kwanza kinatamka kwamba Kamati ya Usalama ya Wilaya itageuzwa tu kuwa Kamati Elekezi ya Maafa ya Wilaya. Lakini katika Kamati ile elekezi, haijamtaja Mkurugenzi wa Halmashauri, imemtaja Mwenyekiti wa Halmshauri au Meya wa Jiji, imemtaja Mbunge mwenye Jimbo katika Wilaya ile lakini Mkurugenzi wa Halmashauri hajatajwa, pengine ni kwa sababu kuna Kamati elekezi ya maafa kwenye ngazi ya Jiji au Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, nini faida ya kumtaja Mkurugenzi kwenye Kamati ya Wilaya; Kamati ya Wilaya kwa maana ya Kamati ya Usalama itatoa maelekezo, Namna nzuri zaidi ya kufikisha katika utekelezaji kwenye Majiji au Halmashauri ni Mkurugenzi Mtendaji kuwa mule ndani, yeye hajatajwa kwenye ile Sheria ya Baraza la Usalama kama Mjumbe kwenye Kamati ya Usalama, lakini hata katika Wajumbe walioongezwa na kwenyewe hajatajwa. Kwa hiyo, akiunganishwa hapo Kamati hiyo itakuwa na namna nzuri zaidi ya utekelezaji hasa kwa kuwa na yeye ni Afisa Masuuli kwenye ngazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na Ibara ya 17, naomba pia nitoe ushauri katika Ibara ya 34 ambapo amesema kutakuwa na Mfuko wa Taifa wa Usimamizi wa Maafa. Tunazungumzia ile dhana ya ugatuaji wa madaraka. Kama tunataka kwa dhati kabisa kudhibiti maafa kwenye ngazi za chini kabisa, ni vizuri huu mfuko ukapelekwa kwenye ngazi ya Mkoa, huu mfuko uonekane pia kwenye ngazi ya Wilaya, ngazi za Kata na kadhalika huko chini.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini? Tunazungumzia majanga ambayo ni natural, lakini yapo majanga ambayo yanasababishwa na binadamu. Tuna majanga madogomadogo pia, kwa mfano juzi katika Wilaya ya Handeni wananchi kadhaa wamejeruhiwa na tembo pale. Maeneo mengine unakuta upepo tu unaezua nyumba, nyingine ni nyumba za nyasi, nyingine za bati, lakini watu wanapata shida, wanajeruhiwa, wanahitaji msaada. Sasa namna ya Wilaya au Kata kusubiri mfuko ambao upo Wizarani kuja kusaidia wale wananchi pale inakuwa ni shida. Wakati mwingine kukusanya michango kwa maana ya usimamizi wa rasilimali inakuwa ni mtihani mpaka mtu aridhie atoe, lakini inaweza kumchukua muda kutoa chochote kwa ajili ya kwenda kusaidia.

Mheshimiwa Spika, ili kulinda hiyo hali ninashauri sana, kwanza huu Mfuko ionekane ni namna gani utakwenda kwenye ngazi za chini, wawe na uhakika wa matumizi ya dharura panapotokea jambo hili. Pili, sheria itamke kwamba ikiwezekana kwenye Halmashauri zetu kama ambavyo tunatenga asilimia fulani ya mapato ya ndani kwa ajili ya majukumu mengine, hata ikiwa ni asilimia moja tu, itengwe kwa ajili ya kuratibu majanga kwenye Councils zetu. Hii itatusaidia kufanya action ya haraka pale ambapo janga linatokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuzungumza hayo, naunga mkono hoja na sheria hii imekuja wakati muafaka kabisa, ninapenda kuishauri Serikali kwamba utekelezaji wake ufanyike kwa haraka kwa ajili ya kuendeleza au kulinda furaha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana. (Makofi)