Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Minza Simon Mjika (32 total)

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Katika Hospitali ya Wilaya ya Meatu tuna machine ya X-Ray tuliletewa toka mwaka 2002. Swali langu ni hili, katika hospitali hiyo hatuna mtaalam wa X-Ray:-

Je, ni lini Serikali italeta mtaalam wa X-Ray katika Wilaya hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika Hospitali ya Wilaya ya Meatu wana mashine ya X-Ray ambayo kwa kipindi kirefu imekosa mtumishi kwa maana ya mtalaam wa X-Ray. Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeendelea kuwasiliana kwa karibu na Wizara ya Afya, lakini pia na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuona namna gani tunapata watumishi hawa ili tuweze kupata mtumishi mmoja na kumhamishia katika Halmashauri ya Wilaya ya Meatu. Wataalam hawa bado ni wachache lakini jitihada za Serikali ni kuendelea kuwasomesha ili tuweze kupata wataalam wengi ili waendane na kasi ya ujenzi wa vituo vya afya ambavyo kimsingi vitahitaji kupata watalaam hawa wa X-Ray.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeshalifanyia kazi na tulishaainisha mtumishi kwa ajili ya kumpeleka Meatu na wakati wowote atakwenda kuanza kutoa huduma ya X-Ray katika Hospitali ya Wilaya ya Meatu. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na nashukuru sana.

Kwa niaba ya wakazi wa Wilaya ya Meatu sasa napenda niulize kwamba ni lini sasa zoezi hili litaanza kwa sababu yapata wiki mbili hivi sasa hatujapata maji katika Wilaya ya Meatu na kuna vijiji ambavyo vinaukame sana kwa mfano Bukale, Mwambegwa na Chambara ni vijiji vingi sana hatuna maji kabisa leo yapata wiki mbili wakazi wa kule tunahangaika, tunapata taabu. Serikali ituambie sasa ni lini itatuletea maji huko kwetu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza Mjika kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama jibu langu la msingi nilivyosema mwezi Agosti, 2021 mradi huu unakwenda kuanzwa na suala hili ni jana tu jopo kamili la wizara liliweza kukaa na hawa wenzetu wa KfW na Mheshimiwa Waziri aliwahitaji watoe commitment yao namna ya kuweza kutekeleza mradi huu kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge nafahamu namna ambavyo unafuatilia suala hili ninakupongeza sana. Nikutoe hofu nitaongozana na wewe tutaenda kuhakikisha kwamba kila namna ambavyo ilikuwa imepangwa inakwenda kutekelezwa kwa wakati.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante na nashukuru sana kwa majibu ya Waziri, lakini sasa napenda nijue ni lini zoezi hili litaanza la ujenzi wa hiyo barabara? Naomba kupatiwa majibu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Minza Mjika kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika jibu langu la msingi nimeainisha kwamba tayari tumeshaanza ujenzi kwenye baadhi ya maeneo na katika bajeti tutakayoanza kuitekeleza ambayo Bunge lako limepitisha, tumetenga fedha, kwa hiyo, mara tu bajeti itakapoanza kutumika barabara hiyo itaanza kujengwa, ahsante.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nina penda kushukuru sana kwa majibu mazuri ya Waziri. Lakini nina maswali mawili tu ya nyongeza. Katika Mkoa wa Simiyu kuna Wilaya tano lakini Wilaya ya Meatu ndio ina ukame sana kuliko Wilaya zote hizo tano. Nilipenda kujua ni lini sasa Serikali itachimba visima virefu vya maji na kusambaza katika vijiji hivyo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, Naibu Waziri yuko tayari kuambatana pamoja nami twende naye katika Wilaya ya Meatu aone wakina mama wanavyopata adha ya maji katika Wilaya ya Meatu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Minza Mjika kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nipende kupokea pongezi kutoka kwa Mheshimiwa Mbunge. Lakini vile vile nipende kumpongeza na yeye, kwa kazi nzuri anayoifanya kwa ushirikiano mkubwa ndani ya Wizara ya Maji. Amekuwa mfuatiliaji mzuri sana akisaidiana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo kaka yangu Simon wanafanya kazi nzuri kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Serikali katika mwaka huu wa fedha 2021/2022 ni kuchimba visima virefu katika Wilaya ya Meatu. Tunatambua namna gani wakinamama wanapata shida ya maji katika Mji ule. Hivyo, tumshukuru Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan, ameliona hili na ameshatupatia fedha tutaenda sasa kifua mbele kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kuambatana kwangu ni kawaida. Hivyo, niseme Mheshimiwa Minza usiwe na wasiwasi baada ya Bunge hili, baada ya kumaliza ratiba ya Mikoa niliyoipanga nitakuja kwako Simiyu hususani Meatu. Lengo ni kuona hali halisi na kuongeza chachu na ufanisi wa miradi yetu ya maji. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante, napenda kushukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, majibu yenye matumaini. Lakini nina swali moja tu la nyongeza.

Je, ni lini Serikali sasa itajenga chuo cha VETA katika Wilaya ya Meatu na Wilaya ya Busega? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante, naomba sasa kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Minza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi, kwamba ujenzi wa vyuo hivi unalingana sawa au unaendana sawa na upatikanaji wa bajeti na upatikanaji wa fedha. Lakini naomba nimpe tu taarifa Mheshimiwa Mbunge na Bunge lako tukufu, hatuishii tu kwenye ujenzi wa vyuo hivi tunakwenda mbali zaidi kwa sababu tukishajenga ni lazima tuweze kuangania namna gani ya upatikanaji wa vifaa lakini vile vile upatikanaji wa walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa Serikali imejikita katika umaliziaji wa vyuo hivi 25 na baadae sasa tutakwenda kwenye mkakati wa kuweka bajeti kwa ajili ya kufikia Wilaya hii ya Meatu, Busega na Wilaya nyingine nchini zilizobaki kwa sababu Wilaya bado ziko nyingi, nakushukuru sana.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Ninapenda kutaka kujua jibu la uhakika leo, ni lini barabara ya kutoka Kolandoto-Kishapu-Lalagwa hadi Meatu itajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza la Mheshimiwa Minza, Mbunge wa Viti Maalum Simiyu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumetenga fedha kuanza ujenzi wa Kolandoto hadi Lalago, bababara hii ambayo ni barabara kuu na tutaanza kwa kilometa 10 kwa sababu fedha tumetenga katika bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kushukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Swali langu ni moja tu la nyogeza. Je, ni lini malipo hayo yataanza kwa sababu yamechukua muda mrefu sana. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza Simon Mjika, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba maombi tayari tumeshayapata na Serikali imeanza kuyahakiki na kabla ya kuisha mwaka huu wa fedha 2022 wananchi hawa watakuwa tayari wameshalipwa.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii. Napenda kuuliza swali moja.

Ni lini barabara ya kutoka Kolandoto mpaka Meatu itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kolandoto kwenda Meatu ni kati ya barabara ambazo zimeainishwa kwenye Ilani, na pia zipo kwenye mpango wa kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami kuanzia na kilometa 92. Kwa hiyo, sasa hivi kinachosubiriwa ni Serikali kupata fedha ili ujenzi wa barabara hii uanze. Ahsante. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kuishukuru Serikali kwamba katika Mkoa wa Simiyu tuna madarasa mengi sana, lakini kuna upungufu wa Ofisi za Walimu. Walimu wetu hawafanyi kazi kwa furaha kwa sababu hawana ofisi wengi wanakaa kwenye miti. Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusu ujenzi wa Ofisi za Walimu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Minza Mjika, Mbunge wa Viti Maalum, kutoka Mkoa wa Simiyu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumeziagiza halmashauri kujenga ofisi kwa kila halmashauri kutenga mapato yao ya ndani kwa sababu moja ya jukumu letu sasa ni kujenga madarasa, mabweni, mabwalo ya chakula ambayo ndio kazi kubwa tunayoifanya sasa ikiwemo na majengo ya utawala kwa baadhi ya shule. Kwa hiyo kwa kadri tutakavyokuwa tunatafuta fedha tutakuwa tunapeleka, lakini tumeziagiza halmashauri kutumia mapato yao ya ndani kufanya hivyo. Kwa hiyo tunafanya hivyo kwa Mkoa wa Simiyu na mikoa yote nchini, ahsante sana. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza. Napenda kuuliza, katika Wilaya ya Meatu tuna shida sana ya maji. Kwa Mkoa mzima wa Simiyu Wilaya ya Meatu inaongoza: Je, ni lini Serikali italeta maji safi na salama katika Wilaya Meatu ili wananchi wa kule wanufaike? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Simiyu una bahati sana. Una mradi mkubwa ambao unaenda kutekelezwa kwa kutumia kigezo cha mabadiliko ya tabia ya nchi. Mradi ule utafikisha maji maeneo ya Meatu, Maswa na maeneo yote yaliyo karibu kuhakikisha wananchi wanapelekewa maji safi na salama. Nafahamu Mheshimiwa Minza nawe pia umefuatilia sana suala hili, na nilifika Meatu na tunaendelea na kazi. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kuuliza swali.

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wa Simiyu tuna Wilaya Tatu ambazo zina upungufu wa watumishi wa afya. Wilaya ya Meatu, Bariadi na Maswa.

Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli katika Halmashauri hizi za Mkoa wa Simiyu kuna upungufu wa watumishi kama ilivyo kwenye Halmashauri nyingine zote hapa nchini, mpango wa Serikali ni kuendelea kuajiri watumishi kwa awamu na ndiyo maana ajira 7,612 zimetangazwa na Halmashauri hizi pia zitapewa kipaumbele katika kuwapelekea watumishi hao. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mhesimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona, naomba niulize swali la nyongeza, je, ni lini Serikali itaongeza watumishi wa afya katika Wilaya ya Meatu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu kwamba Halmashauri ya Meatu ina upungufu wa watumishi na itapewa kipaumbele kwenye ajira hizi ambazo zimekwishatangazwa.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Katika Mkoa wa Simiyu tuna Wilaya Tano, lakini Wilaya ya Meatu inaongoza kwa ukame wa maji.

Je, ni lini sasa tutapata maji ya kutoka Ziwa Victoria maana juzi tu Naibu Waziri amefika pale tumepata maji lakini maji yenyewe yameshakuwa ni ya mgao mtatusaidiaje katika Wilaya ya Meatu?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Meatu ni kama alivyoeleza Mheshimiwa Mbunge, niliweza kufika mimi mwenyewe na ninakushukuru sana Mheshimiwa Minza kwa ushirikiano wako kwa namna ambavyo tumeweza kupunguza ile changamoto ya maji machafu na sasa hivi angalau mnapata maji kwa zamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ya uhakika kutoka Ziwa Victoria tayari unaendelea kufanyiwa kazi, kama unavyofahamu tayari watu wameshaanza kulipwa fidia zao na ule ni mradi maalum kwa ajili ya mabadiliko ya tabianchi, hivyo tutarajie mwaka huu ujao wa fedha shughuli zote zitakwenda kufanyika vizuri.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, ni lini Serikali itakarabati majengo ya Kituo cha Polisi Maswa ili yaweze kuendana na hadhi ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kutoka Mkoa wa Simiyu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Maswa kweli ni cha siku nyingi na kimechakaa. Maelekezo yetu kwa IGP na wasaidizi wake kule mikoani wafanye tathmini ya kiwango cha uchakavu na kubaini gharama zinazohitajika ni kiasi gani ili kiweze kupangiwa matengenezo kadiri tutakavyopata fedha.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kumshukuru sana Waziri kwa majibu yake mazuri. Nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Busega na Wilaya Itirima tuna hospitali nzuri sana za wilaya, tatizo ni moja majengo ni mazuri na yanapenda hatuna watumishi wa kutosha. Kwa hiyo hospitali zile hazina hadhi ya kuitwa hospitali ya wilaya kwa sababu watumishi hawatoshi;

Je ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha ili na wananchi wa kule wafaidike?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Mbunge jinsi anavyofuatilia masuala ya afya kwenye mkoa wake kwa kushirikiana na Wabunge wa majimbo. Kama ambavyo nimesema kwamba kwa mwaka huu tunategemea kupata watumishi takribani 12,000 hivi. Tutaendelea kushirikiana na wenzetu wa TAMISEMI ili tuweze kuona ni namna gani tunaweza kupeleka watumishi maeneo hayo ili wananchi waweze kupata huduma kulingana na ukubwa wa hospitali yenyewe.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itajenga hosteli katika Shule za Sekondari za Meatu na Kimali ili kuwapunguzia wanafunzi adha ya kutembea umbali mrefu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumjibu kwa kifupi Mheshimiwa Minza Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Simiyu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshaeleza nia ya Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuongeza shule za kidato cha tano na cha sita nchi nzima ikiwemo katika Mkoa wa Simiyu. Kwa hiyo niwaondoe hofu Waheshimiwa Wabunge wote kwenye dhana hii, kwa sababu fedha inatafutwa na sehemu ya fedha imeshapatikana ambayo itaelekezwa katika halmashauri zenu kwa ajili ya kuongeza mabweni sehemu zingine mabwalo ya chakula sehemu nyingine madarasa na vyoo ili tuweze kuzisajili na kuzifungua. Kwa hiyo hofu hiyo iondolewe kwa waheshimiwa wote.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mkoa wa Simiyu una upungufu sana wa walimu kwa upande wa sekondari na shule ya msingi. Walimu wa kike ni wachache sana na shule zingine hazina kabisa walimu wa kike.

Je, Serikali ina mpango kutuletea walimu wa kike katika Mkoa wa Simiyu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA YA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, tayari Ofisi ya Rais, TAMISEMI ilishatoa maelekezo kwa Makatibu Tawala wote wa mikoa ya Tanzania Bara. Kuhakikisha wanafanya msawazo katika shule zilizo ndani ya mikoa yao na kupeleka walimu wa kike na wakiume katika maeneo ambayo hayana.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii ya Bunge lako tukufu kwa Niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kumwelekeza RAS wa Mkoa wa Simiyu kuhakikisha anafanya msawazo na kupeleka walimu katika shule ambazo hazina Walimu wa kike wa kutosha.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Majibu aliyoyatoa yako sahihi na kama yatatekelezeka, Meatu tutafaidika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mpango huu wa kujenga madaraja haya kwa kupitia barabara hiyo ya lami itakuwa ni mwezi Oktoba: Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kujenga madaraja haya kwa muda mfupi, Lyusa pamoja na Chobe ili wananchi wa Meatu waendelee kutumia ile barabara kwa mwaka mzima? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Minza yote kwa pamoja, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi, haya madaraja ni madaraja aina ya drift, na katika mpango ambao tutaujenga sasa kwa mpango mkubwa wa EPC+F, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, tunategemea mradi huu usainiwe kabla ya mwisho wa mwezi Juni. Kwa hiyo, tumejumuisha hayo madaraja, yatajengwa wakati huo mradi mkubwa unatekelezwa, ahsante. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika Wilaya ya Itilima kuna shule mbili, shule ya kwanza ni Shule ya Msingi Itubilo ambayo imejengwa mwaka 1965. Majengo yake yamechakaa sana, lakini pia kuna Shule ya Msingi Mwagindu, imejengwa mwaka 1950, nayo majengo yake yamechakaa sana. Je, ni lini Serikali itakarabati majengo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema hapo awali kwamba, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba, inakarabati shule zote ambazo ni za siku nyingi au kongwe katika halmashauri zote nchini. Hivyo basi, Mheshimiwa Mbunge awe na subira, Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kukarabati shule hizi kongwe zilizopo Itilima.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Katika Kata ya Mwandoya kuna kituo kikubwa sana cha afya ambacho kinahudumia zaidi ya watu 3,500, lakini kuna upungufu mkubwa sana wa majengo, hakuna jengo la mama na mtoto wala jengo la x-ray. Je, ni lini Serikali itajenga majengo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba wananchi wake wanapata huduma ya afya iliyo bora hasa Serikali hii ya Awamu ya Sita ya Dkt. Samia Suluhu Hassan na ndiyo maana katika mwaka wa fedha uliopita ilitengwa bilioni 117 ya kuhakikisha kwamba tunajenga vituo vya afya vya kimkakati. Sasa tutaangalia kituo cha afya hiki cha Mwandoya ni namna gani tunaweza tukatafuta fedha kama Serikali ya kwenda kujenga majengo ya mama na mtoto. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsanste na nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; katika Wilaya ya Meatu kuna vituo vya afya ambavyo vimefunguliwa viwili Iramba Ndogo pamoja na Mwasengela. Iramba ndogo ina wafanyakazi watatu; mmoja ni mganga na wawili ni wauguzi, kwa hiyo hawatoshi kabisa, lakini katika Kituo cha Afya cha Mwasengela chenyewe hakina kabisa watumishi wa afya na kinategemewa kufunguliwa tarehe 1 Julai; naomba majibu ya Serikali kuhusu wafanyakazi katika vituo hivi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili liko katika Hospitali ya Wilaya ya Maswa; Hospitali ya Maswa ni kubwa sana lakini watumishi hawatoshi, naomba nipate jibu la uhakika kwamba ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha katika Hospitali ya Wilaya ya Maswa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Minza, la kwanza la Iramba Ndogo kupata watumishi wa ziada na Mwasengela; niseme tu kama nilivyokwishakutoa maelezo kwenye majibu yangu ya msingi kwamba Serikali inaajiri watumishi wa afya 8,070 na katika hawa tutapanga kwanza kwenye maeneo yale yenye upungufu mkubwa ikiwemo Iramba Ndogo, lakini vilevile kwa sababu kituo hiki cha Mwasengela ni kituo kipya ambacho kinaenda kufunguliwa tarehe 1 Julai na kama sikosei kipo Kisesa, tutahakikisha hizi ajira mpya kwa sababu wataingia kazini mwaka huu wa fedha ambao tunautekeleza sasa na tarehe 1 Julai ni mwaka ule mwingine wa fedha, tayari kituo hichi kinapofunguliwa watumishi hawa wa afya watakuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda tu kwenye hili alilogusia la Hospitali ya Wilaya ya Maswa vilevile kwenye hizi ajira tutapeleka maeneo ambayo yana upungufu mkubwa ikiwemo Hospitali ya Wilaya ya Maswa. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante, Kata ya Mwamishali ina changamoto ya daraja la kutoka Mwambiti, Tongoleangamba hadi Buliashi ambayo ni Makao Makuu.

Je, ni lini Serikali itajenga daraja hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, Serikali itajenga daraja hili la Mwamishali kuelekea Makao Makuu ya Kata kadri ya upatikanaji wa fedha. Tutaangalia katika mwaka huu wa fedha 2023/2024 kuona kama fedha imetengwa kwa ajili ya usanifu na ujenzi wa daraja hili na kama haijatengwa tutatenga katika mwaka wa fedha wa 2024/2025 kadri ya upatikanaji wa fedha hizo.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ninashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

a) Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Afya Udekwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili linatoka katika Mkoa wa Simiyu, Wilaya ya Maswa, Wilaya ya Binza;

b) Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha afya katika Kata ya Binza? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu maswali mawili haya ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kata hii ya Budekwa ipo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo. Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wake kadiri ya upatikanaji wa fedha; na tutaangalia katika mwaka wa fedha unaofuata kama kuna fedha imetengwa, ili iweze kwenda mara moja kujenga.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la kituo cha afya hiki alichokiulizia kilichoko Mkoani Simiyu, tutaangalia vilevile kuona ni namna gani kama fedha imetengwa basi iweze kwenda mara moja kwa ajili ya ujenzi wa kituo hiki cha afya.

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante napenda kuuliza swali. Nyumba za askari polisi Wilayani Maswa ni za siku nyingi sana zimejengwa na mkoloni je, ni lini Serikali itajenga nyumba hizo upya ili ziwe na hadhi ya kuishi askari polisi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WIZARA YA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kwa upande wa Maswa si nyumba tu ambazo zimejengwa wakati wa mkoloni. Hata kituo cha polisi ngazi ya wilaya hakipo chenye hadhi stahiki. Katika bajeti ijayo tutaanza utaratibu wa kuweka fedha kwa ajili ya ujenzi wa hizo nyumba, lakini na kuanza kujenga kituo cha polisi chenye hadhi wilaya kama ambavyo imewahi kuulizwa na Mbunge wa Jimbo husika na tukamjibu hapa, ahsante sana.

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itajenga Mradi wa umwagiliaji katika Kata ya Mwanyahina katika Jimbo la Meatu?

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge alishawasilisha jambo hilo ofisini kwetu na tumekubaliana kwamba, nitawaelekeza wataalam wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kwenda kuangalia lile bwawa lililoko pale kama litakuwa ni chanzo kizuri cha maji kwa ajili ya umwagiliaji. Na baada ya hapo tutawatengea fedha kwenye bajeti inayokuja ili waanze kilimo cha umwagiliaji.

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujua Serikali inawasaidiaje wanawake wa Mkoa wa Simiyu ambao hawajiwezi kiuchumi na ambao hawapo kwenye mpango wa TASAF?
NAIBU WAZIRI UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni kweli, katika mikoa au majimbo mengi ikiwemo Simiyu kuna wanawake wengi ambao hawana uwezo, hawajiwezi, lakini hawako kwenye ule mpango wetu wa TASAF. Moja ya maeneo ambayo tunayaangalia sasa kama nilivyosema ni kupitia zile 10% ambazo tunaweza kuzifanyia kazi na kuunganisha baadhi ya mifuko ambayo ilikuwa haiwafikii walengwa, ili tuone hawa ambao hawako kwenye TASAF lakini wana uhitaji maalum kama swali la msingi ulilouliza waweze nao kunufaika na fedha hizi za Mifuko ambayo itawasaidia kuweza kuanzisha shughuli mbalimbali za kijasiriamali, lakini pia kuinuka kiuchumi katika shughuli zao za kila siku.

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante, ningependa kuuliza kutoka katika Wilaya ya Busega. Wilaya ya Busega ina changamoto kubwa sana ya maji hasa katika Kata ya Nyaruhande, Rutubija na Ngasangu. Je, ni lini Serikali itapeleka maji safi na salama katika kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Busega binafsi nimeshfika pale na kufanya kazi kubwa sana kuhakikisha kata zote zinapata maji na katika kata hizi alizozitaja tayari tuna mpango madhubuti wa kuhakikisha maji yanawafikia wananchi yakiwa safi na salama na ya kutosha.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda nielekeze swali langu katika Mkoa wa Simiyu Wilaya ya Busega: Ni lini Serikali itapeleka mashine ya X-Ray katika Wilaya ya Busega? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Minza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa sasa hivi tuko katika mchakato wa kufanya manunuzi ya vifaa tiba, ninaamini mara baada ya mchakato huu kukamilika, basi tutalizingatia hilo nao tutawapatia hiyo X-Ray.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na kilio kikubwa sana kwa wakazi wa Mkoa wa Simiyu hususani Wilaya za Busega, Itilima na Meatu; je, ni lini akina mama wa mkoa huo watafaidika na maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Simiyu unakwenda kunufaika na mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoria mradi ambao ni mapambano dhidi ya uharibifu wa mazingira na tunatarajia maeneo hayo yote aliyoyataja yanakwenda kunufaika, Meatu ipo katika mpango huo na tayari wananchi wameanza kulipwa fidia. (Makofi)

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante nashukuru na ninashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali kweli Waziri amekuwa akinipa ushirikiano sana.

Lakini nilitaka nijue sasa ni lini mtaalam huyo ataletwa kwa sababu tatizo hili limekuwa ni la muda mrefu sana leo Wilaya ya Meatu hospitali ina zaidi ya miaka 30 lakini hatujawahi kupata mtaalam wa kudumu wa X-ray, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza Simon Mjika, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Minza amekuwa akifuatilia sana sana kwa kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Meatu kupata mtumishi kwa ajili ya huduma za X-ray kwenye hospitali ya Meatu na nimuhakikishie kwamba katika ajira hizi ambazo tunakamilisha na mpango ni kuanzia Julai watumishi wetu watapelekwa vituoni tutapeleka mtaalam wa X-ray kwenye hospitali hii ya Meatu, ahsante. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, je, ni lini sasa Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa zahanati katika Kata ya Binza Kijiji cha Iyogero?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, ni lini Serikali itapeleka fedha za kukamilisha kujenga zahanati katika Kijiji cha Ng’hami Wilaya ya Maswa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafuatilia kuona hatua ambazo majengo haya ya zahanati yamefikia ili tuweze kuweka kwenye bajeti kwa ajili ya kukamilisha majengo haya, ahsante.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali: -
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kuuliza swali; je, ni lini Serikali itajenga mabweni katika Shule ya Kimali Sekondari, Wilayani Meatu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mwenyekiti, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Minza Mjika, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatafuta fedha, na kwa sababu tuna miradi mingi katika Idara ya Elimu basi tutalipa kipaumbele katika fedha ambazo zinakuja kutoka kwenye wafadhili mbalimbali, ahsante sana.