Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Minza Simon Mjika (5 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru sana kwa kunipatia nafasi hii, lakini kulingana na ufinyu wa muda nitaenda haraka sana na nitasema tu baadhi ya vitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru sana Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa hotuba yao nzuri iliyosheheni matumaini kwa Watanzania. Nimefurahi sana kwa mambo mengi ambayo wameweza kuyasema mle, kama yatatekelezeka hawatakuwa na ugomvi na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaingia moja kwa moja katika Mkoa wangu wa Simiyu. Mkoa huu una wilaya tano, lakini wilaya nne ndizo zinazoshambuliwa na Wanyama. Kuna Wilaya ya Busega, Bariadi, Itilima na Meatu. Maswa tuko vizuri tunamshukuru Mungu. Nashukuru kwa upande wa Wilaya ya Busega, Mheshimiwa Songe ameweza kuongea kwa hiyo, sina haja ya kurudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie katika Wilaya ya Bariadi. Bariadi tunashambuliwa sana na wanyama, tembo hawa. Kwa mfano, Kijiji cha Nyawa, Gibeshi, Kindwabihe, Mwasenase pamoja na Ihusi, kule kuna mashambulizi makubwa sana ya tembo. Tunaomba Serikali iangalie sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda niingie moja kwa moja tena kwenye Wilaya ya Itilima. Napenda tuishukuru kwanza Serikali yetu. Ninashukuru kwamba tuna gari la wanyamapori katika Wilaya ya Itilima, tayari wameshaleta, tunashukuru. Kwa hiyo, msaada mkubwa umepatikana pale japokuwa kuna vijiji ambavyo vinahangaishwa sana na hawa wanyama; kuna Mwaswale, Nyantuguti, Nkuyu; hivyo ni baadhi ya vijiji tu ambavyo vinashambuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiingia katika Wilaya ya Meatu ninashukuru Mheshimiwa Mpina ameongea na baadhi ya vijiji amevitaja pamoja na changamoto zake. Tunaomba kupata msaada, katika hivyo vijiji tunahangaika sana. Vijiji ni vingi sana; tukiangalia kwa mfano katika Wilaya ya Meatu kuna Mwasengela, Mbuga ya Banyha, kuna Sakasaka, Nyanza, Igobe, Longaloniga; vijiji ni vingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiingia kwangu ninakotoka Meatu kuna Mwanyahina, Makao, Mwagwila, Mwajidalala, Busia, Mwanzagamba, Mwangudo, kote kule wanyamapori hawa tembo wamesambaa sana. Tunaomba msaada kutoka Serikalini.

Katika Wilaya ya Meatu hatuna hata gari la wanyamapori. Askari wapo, lakini hakuna usafiri. Hata tembo wakionekana wanafanya uhalifu sehemu, akipigiwa hana usafiri, inakuwa ni shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali iliangalie sana hili. Hatuna ugomvi na Serikali, lakini tunaomba watutendee ilivyo sahihi. Akina baba wengi katika Mkoa wa Simiyu, hususan hizo wilaya nne ambazi nimezitaja wameshakuwa doria, hawana combat, hawana silaha, hawana usafiri, lakini ni watu wa kulinda wanyamapori. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuomba tuone. Watu wengi sana wamepoteza maisha, akina baba, akina mama na watoto, hususan wanafunzi wanapoenda shule. Kwa mfano, mwaka juzi 2019 kuna mwanafunzi mmoja aliuawa katika Kijiji cha Mwangudo, mtoto wa Darasa la Pili anaenda shule. Alikutana na tembo, alimjeruhi vibaya sana yule mtoto, alimsaga na akaisha kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba vitu kama hivi tunavyoviongea tunaweza tukaona rahisi, lakini wananchi wanalia sana na wanateseka sana. Tunaomba basi Serikali ifanye hima itufanyie msaada huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa mambo makuu ambayo ameendelea kutupatia. Tuna afya njema na ndiyo maana tuko hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kuifanya katika nchi yetu ya Tanzania. Wala haina sababu ya kueleza, wote tuanaona mambo makuu ambayo anaendelea kuyafanya. Vilevile namshukuru dada yangu, Waziri wa TAMISEMI kwa ajili ya kazi nzuri ambazo anaendelea kufanya pamoja na Naibu Mawaziri. Endeleeni kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza kwa upande wa TARURA; TARURA ni watu ambao wanafanya kazi vizuri sana. Barabara zetu zimefunguka, ziko vizuri, japokuwa ni za changarawe, lakini tunaenda vizuri utadhani ni barabara ya lami, tunashukuru kwa hilo. Tunapenda kumshukuru sana kiongozi wetu wa mkoa, Meneja wa TANROADS Gaston Gasana anafanya kazi nzuri sana, ikiwa ni pamoja na Mkuu wetu wa Mkoa anafanya kazi nzuri sana, anasimamia vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa afya, namshukuru Rais wetu ametupatia hospitali kubwa mbili tena za wilaya; Wilaya ya Itilima na Wilaya ya Busega. Meatu, Maswa pamoja na Bariadi tuna hospitali hizo za muda mrefu na zina vifaa, tunashukuru sana kwa kazi nzuri ya Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali hizi mbili ambazo zimejengwa bado ni mpya na bado ni changa zinahitaji wafanyakazi wa kutosha, tunaomba tupate wafanyakazi katika hospitali hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia vifaa vya kufanyia kazi katika hizo hospitali, tunaomba vifaa vipatikane kwa ajili ya kazi hiyo. Vinginevyo ninapenda tu nimshukuru sana Mama kwa kazi nzuri ambazo anaendelea kufanya. Wafanyakazi ni wachache sana katika hospitali, kwa mfano Mkoa wa Simiyu una asilimia 33 ya wafanyakazi mkoa mzima una wafanyakazi 1,500 tu. Kwa hiyo, tuna upungufu wa asilimia 65, ni upungufu ambao ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana Waziri wa TAMISEMI, Dada yangu Angellah jitahidi sana kutupatia wauguzi katika Mkoa wa Simiyu. Tunawapenda sana kazi mnazozifanya lakini tunaomba tuongezewe wafanyakazi. Nadhani ajira zimetangazwa nyingi tunaomba basi na sisi katika mkoa wetu tuweze kupatiwa wafanyakazi wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, basi ninahama hapo naenda upande wa barabara, kuna barabara ambayo imekuwa ni ahadi ya muda mrefu sana, Kolandoto – Lalago inapita mpaka Kishapu – Lalago mpaka Meatu. Barabara ile iko katika Ilani na ni ya muda mrefu, miaka mingi. Tunaomba mtupatie lami na sisi ili nasi tujisikie kwamba ni miongoni mwa Watanzania, kutoka Meatu mpaka Kolandoto tunaomba tupate barabara ya lami lakini pia kuna barabara inayotoka Bariadi inapita Itilima – Meatu mpaka Singida. Tunaomba barabara ile pia tuwekewe lami. Tunahangaika sana barabara ile ni nzuri sana na ni shortcut nzuri haina sababu ya kuzunguka Mwanza au Shinyanga tukishatengenezewa ile barabara magari mengi yatapita pale na uchumi wa nchi yetu utaendelea kuwa juu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naingia upande wa elimu, ninashukuru Rais wetu ametupatia madarasa mengi ya kutosha. Sekondari na primary madarasa ni mengi tu yanatosha vizuri lakini tatizo ni moja, changamoto hatuna walimu wa kutosha. Walimu ni wachache sana, wanafunzi ni wengi ndio wanakaa kwenye madarasa lakini hata yale madarasa yana upungufu tena wa madawati. Tunaomba wanafunzi wakae katika sehemu ambazo ni nzuri ili anapojifunza basi ajisikie vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna upungufu wa vifaa vya kufundishia na kujifunzia tunaomba walimu muwasaidie waweze kupata na wawe na ofisi za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu ambacho napenda niseme ni kwa upande wa maji. Katika Mkoa wa Simiyu tunachangamoto kubwa sana ya maji. Maji ni tatizo sana yaani wakinamama wa Mkoa wa Simuyu, kina baba tunahangaika sana juu ya maji. Tunaomba msaada mkubwa ambao ni mwarobaini utakaotibu hili tatizo ni kupata maji ya kutoka Ziwa Victoria.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba hili mlifanyie kazi, TAMISEMI tusaidieni sana Mkoa wa Simiyu tunahangaika sana hasa Wilaya ya Meatu. Wilaya ya Meatu haina vyanzo vya maji muda mrefu tumekuwa tukihangaika tukilia. Nadhani Mheshimiwa Angellah ulifika katika Mkoa wa Simiyu, Wilaya ya Meatu uliona changamoto iliyoko kule ni shida huwezi hata ukapanda miti ukamwagilia. Tuna ukame wa hali ya juu sana lakini hata vile visima tulivyonavyo tena tembo wanashambulia yale maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaomba mtusaidie tunapoongea namna hii kweli masikitiko ukifika katika Mkoa wa Simiyu hizo wilaya zina changamoto kubwa sana, tunaomba Serikali iweze kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho napenda nikiiongee hapa ni kwa upande wa walimu, nirudi samahani kule, walimu wengi wanadai malipo ya muda mrefu, wameenda likizo hawajapewa pesa zao na wengine wanachangamoto nyingi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba kwa upande wa elimu muweze kuwasaidia. Mwalimu anafanya kazi kubwa sana unajikuta mwalimu mmoja anaweza akafundisha watoto 140 darasa moja mwalimu pekee yake lakini bado hata yale malipo yake ni shida anapoeenda likizo hapati chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna upungufu wa nyumba za walimu, walimu wengi wanaishi mijini shule zao zipo vijijini unajikuta kutoka mjini mpaka kijijini kule ni kilometa saba. Mwalimu aende na kurudi kilometa 14, tunaomba walimu wa kutoka kule kwetu Mkoani Simiyu tupate walau hata kila shule hata nyumba kumi kumi za walimu waweze kukaa karibu na mazingira ya shule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda niseme kuhusu upungufu sasa wa hivo vifaa katika hizo hospitali nilizozisema nadhani hilo nimeliongea na ninaamini kwamba nimeelewaka. Napenda kushukuru, naishia hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi hii ya kuweza kuchangia Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda nimshukuru sana Rais wetu kwa jinsi anavyopambana katika sekta hii ya elimu. Mama anajitahidi ametupa fedha nyingi na amejenga madarasa mengi pia. Lakini vilevile nimshukuru Waziri wa elimu pamoja na Naibu wake kwa kazi nzuri ambazo anazifanya, kweli wanapambana na wanaleta maendeleo katika elimu. Nimshukuru pia Katibu wa Elimu pamoja na Manaibu wake kwa kazi nzuri ambazo wanazifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho nasema nishukuru kwa sasa, katika Mkoa wa Simiyu Wilaya ya Meatu tumepata fedha kwa ajili ya kujenga VETA, kwa hiyo nashukuru sana. Mwaka jana nilisimama hapa kuchangia nikaomba hivyo Waziri umetekeleza; wakazi wa Wilaya ya Meatu tunashukuru sana. Lakini vile vile tunashukuru kwa fedha mlizopeleka. Mmepelekea milioni 228, lakini kazi ile ni ya bilioni tatu. Jitahidi sana Waziri kupeleka pesa kule ili yale majengo yajengwe kwa wakati na si kwamba VETA ijengwe kwa muda wa miaka mitano, haipendezi. Jitahidi fedha zile ziende na shughuli ziende vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana kwa kazi nzuri ambazo mnaendelea kuzifanya, mnaelimisha jamii, mnatoa fedha nyingi, tunapata madarasa na madawati pia. Lakini tukumbuke Watanzanjia tuna watoto wengi sana katika shule zetu. Pamoja na kupambana kujenga madarasa miundombinu lakini bado tuna upungufu mkubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuongea juu ya walimu. Walimu kwa kweli wako katika mazingira ambayo ni magumu sana, lazima niwasemee. Walimu wanahangaika wanafanya kazi katika mazingira magumu. Niliona shule moja hapa, niliwasiliana na Mkuu, shule moja ambayo iko katika Wilaya ya Itilima ina watoto1,200 lakini ina walimu 11, just imagine, wale waaalimu wanafanyaje kazi jamani? Mwalimu afundishe kuanzia chekechea, akitoka chekechea ana kipindi cha darasa la kwanza, akitoka kipindi cha darasa la kwanza, ana kipindi cha darasa la tatu yule mwalimu kweli unamuandalia mazingira mazuri hayo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajikuta mwalimu anachoka, anaongea na wale watoto yaani ukiingia darasani katika Mkoa wetu wa Simiyu nisemee, darasa moja lenye wanafunzi wachache labda ni wanafunzi 125 au 130, mwalimu huyu mmoja. Sasa jiulize, darasa la kwanza mwalimu anaandika kengine kanamfinya; yaani mwalimu unamuweka katika mazingira ambayo ni magumu hata kazi yake anaona kwamba jamani nifanyeje. Lakini bado mwalimu yule anatoka mbali, umbali wa kilometa tisa mpaka kumi, mwalimu anaendesha baiskeli ama kabebwa kwa boda boda na kwa hela hiyo hiyo tunayoijua. Afike kule mwalimu amechoka, kanyeshewa mvua, yaani ni vitu vya ajabu. Mwalimu tena aingie darasani lakini akifika darasani na penyewe mwalimu anapata shida watoto ni wengi wengine wamekaa chini mwalimu anaandika wanamvuta sketi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usiombe kufundisha darasa la kwanza, na ndiyo maana walimu wengi huwa wanakimbia sana kufundisha darasa la kwanza la pili na la tatu, ni watoto amabo ni wasumbufu mno. Una watoto 140 mwalimu mmoja unafundishaje? Haya wengine wamekaa kwenye madawati, wengine chini, ni vurugu; kanakolia, kanafanya nini, unajikuta mwalimu hafanyi kazi katika mazingira yaliyo mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamesema habari ya private; private wanajitahidi kweli inabidi Wizara ya Elimu kujiuliza kwamba inakuwaje shule zetu za Serikali zinakuwa na walimu wachache kiasi hicho? na wale wanajitahidi wanakuwa na walimu wengi ambao wanakuwa na mgawanyo mzuri wa masomo, basi mwalimu hata kama amezidiwa namna gani awe na watoto 50; watoto 50 anaweza akajitahidi mwalimu akawafundisha. Mwalimu huyu unampa watoto 130 au 140 lakini atoe maswali 50 kwa kila somo, hasa darasa la saba na la sita, hivi hebu fanya 50 mara 120., atakuwa amesahihisha maswali mangapi? Yule mwalimu akitoka pale atakuwa na hali gani? Waziri wa Elimu naomba ajitahidi sana kwa hilo, atuletee Walimu wa kutosha katika Mkoa wa Simiyu ili tupunguze idadi ya wanafunzi wengi ambao hawaelewi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine napenda niseme, Serikali imefanya vizuri sana katika kuwapatia Walimu vishkwambi kwa ajili ya kufundishia na kujifunzia. Tunashukuru kwa hilo Walimu amewasaidia, lakini kuna sababu ya Serikali isaidie upatikanaji wa wireless internet ili kurahisisha watoto na walimu kusoma kwa kutumia teknolojia mpya hii ya kisasa, Mwalimu asaidiwe. Niliwaona Walimu siku ya Mei Mosi walikuwa wakimwambia mama, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wanasema mama tumepewa vishkwambi tunavyo, lakini tunataka tufundishwe jinsi ya kuvitumia. Kwa hiyo, Profesa atumie muda wako apate timu ambayo itawasaidia Walimu ili waweze kufanya kazi katika njia iliyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni upungufu wa miundombinu kwa Walimu. Walimu wengi hawaishi shuleni, wanaishi mbali sana. Angalia mazingira ya kule kwetu, Mwalimu anatoka pale Bukundi anaenda Lukale Shule ya Msingi, ni mbali sana ni kama kilometa kumi na tatu, kumi na nne, anaendesha baiskeli, akifika kule Mwalimu amechoka hawezi kufanya kazi na bado mazingira yetu sisi ni magumu sana kule. Walimu wangepata nyumba, wangefanya kazi vizuri, wakae katika maeneo ya shule ili Mwalimu aweze kutekeleza majukumu yake vizuri. Naomba Waziri alichukue hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona Rais wetu amejitahidi amejenga madarasa mengi sana, basi uwepo na utaratibu wa kujenga nyumba za Walimu ili wakae katika maeneo ya shule, maeneo ya shughuli zao. Walimu wanaishi mbali sana, unakuta anatoka pale Mwanuzi Shule ya Msingi anaenda mbali, umbali wa kilometa kumi na mbili, kumi na tatu, hivyo, Mwalimu anafika amechoka hata ule ufundishaji wake unakuwa uko chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho nataka niseme ni changamoto ya madarasa. Madarasa kweli Serikali imejitahidi kujenga, lakini bado kuna upungufu mkubwa. Walimu wanahangaika katika madarasa na watoto wengine wanasoma nje kwa sababu vile vyumba vya madarasa havitoshi. Serikali ilijitahidi kumweka Mwalimu katika mazingira mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande mwingine nataka kuzungumzia habari ya hawa watoto wenye mahitaji maalum, watoto hawa wanahangaika sana. Unakuta Mwalimu anafundisha hana darasa la watoto hao, anavamia hapa, yuko hapa, mara yuko nje. Basi Serikali ijitahidi ijenge madarasa maalum kwa wale watoto wenye mahitaji maalum ili nao wasome katika hali nzuri na wajisikie vizuri, pia hata Walimu wawe na mazingira mazuri ya kuwafundisha watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine Mheshimiwa Waziri nataka nishauri juu ya hawa watoto wa MEMKWA. Watoto wa MEMKWA ingependeza nao waandaliwe miundombinu yao, wawe na madarasa yao special kwa ajili ya kufundishiwa. Kwamba, hii ni MEMKWA wafundishwe, sio mpaka wasubiri watoto wengine wamalize, wamechelewa, anaingia Mwalimu akiwa amechelewa na ufundishaji wake unakuwa haujakaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho napenda niseme, Walimu wetu wanalalamika sana juu ya mafao yao, hasa wanapostaafu. Wanapostaafu inaonekana kwamba, Walimu tunawasahau na tunawatelekeza, lakini wamefanya kazi nzuri sana na kazi ya hali ya juu ya kuinua elimu ya nchi yetu ya Tanzania. Mwalimu anapostaafu pension yake inakuwa ni matatizo, wengi wanalia, kila siku napigiwa simu, tusaidie huko. Jamani Mwalimu anapokaribia kustaafu kabla hata ya miezi mitatu mwandalie pension yake, apewe hela yake yote aifanyie kazi yeye mwenyewe, sio aanze tena mizunguko ya kuja Dodoma mara mbili, mara tatu, mara nne, hata hela hana, anakopa. Tunaomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hilo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende kuishukuru sana Serikali yangu kwa utendaji mzuri ambao unaendelea. Serikali imefanya vizuri sana kuwapatia Walimu hivyo vishkwambi, kama nilivyosema, lakini hapa kuna message nyingi, wanasema, mwambie Waziri ajitahidi tuelewe vizuri kuvitumia vile vishkwambi. Kwa hiyo, wengi hawaelewi. Waziri apate muda, atafute timu yake, iwafundishe Walimu ili waweze kuvitumia vizuri vile vishkwambi na viwe msaada kwao wao na kwa wanafunzi ambao wanawafundisha, litakuwa ni jambo jema sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi hii. Napenda niunge mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ya kuweza kuchangia. Napenda kumshukuru Mungu kwa vile amenipatia nafasi nzuri na siku njema kama hii ya leo kuweza kusimama hapa na kuongea yale niliyonayo. Pia ninamshukuru Mwenyezi Mungu kwa ajili ya Rais wetu Mama Samia, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi nzuri ambazo anaendelea kufanya katika nchi yetu. Ni kweli amekuwa mama wa mfano kiongozi wa mfano Rais wetu, tuzidi kumuombea awe na afya njema na aweze kutimiza maono yake kwa Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ninakushukuru sana Spika wetu kwa kazi kubwa ambayo iko mbele yako, tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu asimame na uweze kushinda, hakika tunapoomba muda wote Mungu anasikia maombi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende kumshukuru Waziri Mchengerwa pamoja na Naibu wake, Katibu, Naibu Makatibu kwa kazi nzuri ambazo wanazifanya. Nimeendelea kumwambia Mheshimiwa Waziri kwamba kazi anayoifanya ni nzuri. Wizara hii ni nyeti sana, ina muingiliano mkubwa sana na ina ugomvi mkubwa sana, lakini Mungu awaongoze katika hilo mkubali kushauriwa na mkubali kubadilika mambo yenu yataenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuipongeza Serikali yangu kwa kazi ambazo zinaendelea kwa sasa, Rais yetu Mama Samia royal tours imeleta mambo mazuri sana, tumeona wageni wengi wanaongezeka kila leo na tunapata fedha za kigeni tunashukuru kwa hilo. Pesa zile zimeingia katika maendeleo ya nchi tunapata barabara, tunajenga hospitali, tunajenga vituo vya afya na maendeleo mengine mengi nchini yanapatikana kulingana na hii ziara ya mama yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninapenda kuwashukuru wawekezaji wetu ambao wapo katika nchi yetu ambao wanakuja kwa ajili ya kutembelea na kutupatia fedha nyingi. Sitaki niongee zaidi kwa sababu naona muda wote ni mdogo nataka niseme habari ya Simiyu. Simiyu ina Wilaya Nne ambazo zinachangamoto kubwa sana ya tembo. Kuna Wilaya ya Busega, Bariadi, Itilima, Meatu. Wilaya hizi zinazo changamoto kubwa sana kila leo wananchi wanauawa ni hakika nadhani hata wewe Waziri taarifa hizi unazipata.

Mheshimiwa Spika, napenda niseme kwamba wananchi wa kule wamekuwa na tatizo kwa muda mrefu sana, kila siku wakinababa ni kulala nje kwa ajili ya kulinda tembo, tembo ni wengi kupita kiasi. Tembo wameleta madhara makubwa sana katika Mkoa wetu wa Simiyu, wameua akina baba, akina mama, watoto na wanafunzi wakati wanaenda shule, imefanya hata maendeleo ya baadhi ya wanafunzi kutokuwa mazuri kwa sababu hawaendi shule kwa ajili sababu ya tembo kuwa wengi kupita kiasi.

Mheshimiwa Spika, tembo hao wameleta madhara mengine ya kula chakula kikiwa shambani na kikiwa nyumbani. Tembo ni mnyama mwenye vurugu sana kwa kweli, ni ambaye kweli anavuta watalii wengi wanakuja kumuona hapa Tanzania lakini ni mnyama ambaye analeta madhara makubwa sana, amesababisha vifo vingi sana, ulemavu, ameleta njaa ameleta shida mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri napenda nikuambie kwamba katika Mkoa wa Simiyu kweli watu wengi wameuawa sana, lakini kumbuka kwamba katika Mkoa wetu wa Simiyu tunahangaika na hawa wanyama kwa muda mrefu sana. Mwaka jana tulisema walau mtupatie magari ya askari game hakuna hata gari katika Wilaya ya Meatu na Wilaya ya Bariadi lakini wanyama muda wote wapo wanaingia mpaka sokoni ni muda wa kukimbia tu kina wakimama, wakibaba hawapati amani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanyama hawa wamekula sana mazao unakuta katika Wilaya zetu hizo kuna njaa kubwa sana kwa ajili ya ukosefu wa chakula kwa ambao wanakaa pembezoni mwa sehemu hizi zenye wanyama hawa. Tunaomba Serikali iweze kutusaidia hili, ninaamini kiongozi wetu Waziri wewe ni msikivu, nilikuambia hata siku moja kwamba jamani mjitahidi kuleta amani hata maandiko matakatifu yanasema katika “Waebrania 12 – 14 tafuteni kwa juhudi kuwa na amani na watu wote” tunapokuwa na amani ni jambo ambalo ni jema hawa watu wanalala nje, akinamama wanabaki wenyewe nyumbani, watoto wanashindwa kwenda shule, lakini Waziri ukifika pale na Naibu Waziri wako mkawasaidia hawa watu ni jinsi gani hawa wanyama basi waweze kulindwa na watu ambao wamesomea yale mambo ili kwamba wale watu waweze kupata amani. Kweli imekuwa ni shida ni kukimbizana muda wote watu hawana hata kazi za kufanya. Mheshimiwa Waziri jitahidi kwa hilo, (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna Mbunge mmoja hapa amesema mimi hilo jambo kila siku nilikuwa nawaza akili kwangu, kwanini msijenge fence kwa ajili ya hawa wananyama wasiwe wanavuka kuingia kwenye makazi ya watu? Zijengwe fence kama vile yalivyo Magereza ya nchini Tanzania fence ndefu mnyama hawezi kuvuka ili tuleta amani katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, familia nyingi kule zinalia zimepoteza watoto kinababa wamefariki, kinamama wamefariki wengine wamepata ulemavu. Kwa hiyo, unakuta kwamba hata wale manyama watu wanawachukia kwa sababu ya changamoto kubwa kama zile. Waziri wetu jitahida sana kufatilia mambo kama haya. (Makofi)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, taarifa hapa Jacquline Ngonyani Msongozi.

SPIKA: Mheshimiwa Jacquline Ngonyani.

TAARIFA

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nataka nimpe taarifa mzungumzaji anayezungumza sasa kwamba, kutokana na kadhia hiyo kwamba watoto wanashindwa kwenda shuleni lakini pia hao tembo wameweza kufika mpaka majumbani wanavuna mazao na wakati mwingine wanachua vyakula mpaka vya nyumbani wanakula.

Mimi nilikuwa nadhani kwamba sasa hawa tembo wangevunwa ili kupunguza hiyo kadhia wabakizwe wachache, hawa wachache watakaobaki waendelee kuzaa. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Minza Mjika.

MHE. MINZA S. MJIKA: Naipokea taarifa hiyo kwa mikono miwili. Nilikuwa naelekea kusema kwamba kwa mfano mfugaji anapofuga anakuwa na ng’ombe wengi sana, ng’ombe wanazidi inabidi awapunguze wengine aende kuwauza mnadani apate pesa afanyie shughuli zingine za maendeleo. Hata hawa tembo wamekuwa wengi mno na ndiyo maana wanatembea huku na huku, si wavunwe wauzwe basi tupate hata fedha za kigeni? Itakuwa ni jambo jema kuliko kutesa wananchi muda wote wanakimbizana kwa ajili ya tembo, kila leo unapigiwa simu tunaomba hela ya tochi, tunaomba hela ya turubai, tunaomba pesa ya nini?

Tunaomba Waziri Mchengerwa utusaidie na tunakuomba ufike katika Mkoa wetu wa Simiyu. Ufike katika Wilaya zile ambazo zinahangaishwa na hawa Wanyama, utaona heka heka ya kinababa ambao wanayo kule, hawalali nyumbani muda wote wako porini jamani hebu tuangalie hawa watu kweli? Kuna Mheshimiwa mmoja anapenda kusema kwamba changamoto ya akili, matatizo ya akili wale watu hawawezi wakawa na akili nzuri. Kwa sababu hawatulii majumbani kwao na weka zao na familia zao, muda wote wanalala porini je, watapata amani kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kusema kwamba wanyama hawa ndiyo hatarishi sana katika Mkoa wetu wa Simiyu, hakuna mnyama mwingine mwenye vurugu kama tembo. Tunaomba Serikali iangalie kama ni kuwavuna basi wavunwe, sasa hivi wameingia katika hizo Wilaya toka mwezi Novemba mwaka jana, mpaka sasa hivi wako kule wanakula chakula shambani, wanakuja nyumbani, hata akikuta ni kubinua tu lile bati anaanza kula huyo mnyama ni mnyama mwenye vurugu sana, lakini hakuna mtu anayeweza kupiga kwa sababu wananchi wanaogopa sheria. Tunaomba Serikali basi iweze kuwavuna wanyama hao na sisi wananchi wetu waweze kuishi kwa amani na waweze kuwa na amani kama wapo katika nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kusema juu ya hawa wawekezaji wetu, kwa mfano Mwiba. Nashukuru kwamba si kwamba hawasaidii, wanasaidia katika maendeleo na ni wadau wa maendeleo pia. Kwa mfano, katika shule ya sekondari Paji, Mwiba ametoa baiskeli 200. Wanafunzi wamepata baiskeli ambazo zina thamani ya milioni 40 na kuendelea lakini pia wamejenga shule, wamejenga madarasa, tunawashukuru wale wawekezaji, si kwamba tunawachukia lakini kero ni kwa wale wanyama tu basi, ikitoka hiyo kero wala hatuna shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile Mwekezaji huyo tunapenda kumshukuru sana ameamua kuanzia mwezi wa Saba wanafunzi watakula shuleni muda wote. Kwa hiyo, tunashukuru sana kwa huo uwekezaji, wawekezaji wetu waliyopo hapa nchini kwa ajili ya kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, Waziri Mchengerwa ninazidi kukuomba Waziri wangu endelea kuwasaidia wananchi wa Mkoa wa Simiyu na Wabunge wengi hapa wanaongea wanalalamika hilo jambo, tafadhali mtusikilize ili familia za kule ziwe na amani ili familia za kule ziwe na furaha, wanapolima wapate chakula wasije wakawa ombaomba kwa sababu ya kufirisiwa na tembo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante napenda nishukuru sana kwa kunipatia muda huu, lakini vilevile nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa ajili ya wema wake wa pekee ambao ametufanyia katika siku hii ya leo. (Makofi)

Awali ya yote nimshukuru sana Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ambaye anafanya kazi kubwa kwa ajili ya Taifa letu hili. Mama yetu anapambana, anakimbia huku na kule kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu, tunamshukuru sana na zaidi ya yote tunamuombea kwa Mwenyezi Mungu aendelee kumlinda na kumpatia afya njema. Lakini vilevile nipende kuwashukuru akinamama hawa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayofanya. Mama Gwajima na Naibu wako tunakuona sana unavyofanya kazi tunakuombea afya njema na uendelee kuifanya kazi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, basi kulingana na muda wetu mimi napenda niseme sehemu tatu tu; sehemu ya kwanza napenda kuongelea habari ya hawa watu wabakaji. Hakuna watu wananiumiza roho kama hao. watoto wa kike wananyanyaswa sana na vijana wa kiume wananyanyaswa sana, lakini nikiangalia hatima yake naona kama vile yaani hawafanyi makosa makubwa. Mtu yule anatakiwa achukuliwe hatua kama vile anavyochukuliwa muuaji kwamba ameua, apewe sheria kali ya kukaa gerezani hata miaka 20 ili ajifunze kule, kwa sababu mtu anapofanya hivyo wanawaathiri sana watoto wetu wa kike. Wanawaharibu watoto wetu, wanakosa amani na wanakatisha njozi zao kwamba alitaka asome pengine amefanyiwa jambo baya na bado likashindikana hata kutatulika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kingine niseme kuna Mheshimiwa Kapinga kasema mtoto hawezi akaongea maneno yale mahakamani, ndio maana unajikuta kwamba ukisema mahakamani kwamba nilitendewa jambo baya unaambiwa jambo gani hilo baya litaje. Sasa mtoto hawezi kutaja kwa asili yetu sisi Watanzania. Tunaomba watu kama wale washughulikiwe, hata msamaha wa wafungwa unaotolewa wakati mwingine Disemba wakati wa sikukuu, Rais watu kama hao wasitoke ashauriwe kabisa watu hao waendelee kukaa gerezani kwa sababu kosa wanalolifanya ni kubwa lakini unaona mtu kafanya kosa kubwa kama lile unashangaa baada ya miezi mitatu minne unamuona mtaani. Sasa linachukuliwa ni jambo la kawaida kabisa, lakini akipewa adhabu moja tu miaka 20 akakaa gerezani anatoka kule alishachoka hawezi kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba sana hilo mlichukue pamoja na Waziri husika wapewe adhabu za kutosha na wasitoke kwa msamaha wa Rais watu wa namna ile kifungo chao wapigwe miaka 30 akae mle ajifunze. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshsimiwa Spika, naingia kwa upande wa wamachinga. Ninapenda nimshukuru sana Rais wetu amewakumbuka vijana wetu kupata sehemu maalum za kufanyia kazi kwa kweli kwa hilo ninampongeza sana. Vile vile, wameitisha mkutano hapa vijana wetu wamepata semina mbalimbali, jinsi ya kuchukua mikopo na mikopo ile waitumieje, kwa hilo tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende upande mwingine wa wakina mama kweli mikopo wanapata lakini ile mikopo haitoshelezi. Nilikuwa naomba wenzangu wameongea hapa ninashukuru mimi niliona bora iwe asilimia 16 kwa mchanganuo ufuatao; asilimia 10 wanawake na wasichana wapate asilimia 10; lakini asilimia tatu wapate vijana, lakini asilimia tatu tena wapate walemavu; hiyo itapendeza kidogo. Kwa hiyo, mtu atachukua kitu ambacho ni kikubwa na anaweza akafanyia kazi. (Makofi)

Kwa upande wa wanawake ninapenda niseme kwamba hakuna mtu anafanya biashara kama mwanamke, mwanamke ni mjasiriamali wa kweli, akipewa mafunzo ya kutosha mwanamke hakosei na anafanya kazi kwa bidii zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, basi mimi naomba kulingana tu na kwamba hatuna wataalam wa kutosha tunaomba Serikali iongeze hawa maafisa maendeleo ya jamii, ili kwamba watu kabla hawajapata mkopo wakina mama wapewe semina mkopo ule ni wa kufanyia nini na ufanyeje lazima ajue. Lakini mtu anaweza akachukua mkopo siku hiyo hiyo anakwenda kujengea nyumba, anakwenda kununua cement anaanza ujenzi wa nyumba, marejesho atatoa wapi? Fedha ya mkopo sio ya kujengea, fedha tunayojengea ni ile inayotengwa kwenye mzunguko yaani ile faida inapopatikana basi iendelee kwenye shughuli za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini unakuta mtu anachukua mkopo, anaingia kufanya sehemu zingine ambazo haziko muhimu na akinamama hawa tunaona wana majukumu mengi. Kina mama kweli tuna majukumu sana yaani kama ni kwenye familia mama anachukua majukumu asilimia 85 baba anachukua tu asilimia 15. Kwa maana hii mama atachukua mkopo akishachukua mkopo chakula cha nyumbani ni mama, mboga ni mama, watoto kwenda shule ni mama, uniform, viatu ni mama, baba hana habari tena hususani kule kijijini hawana habari kabisa. Baba anajua issue ni kulewa tu, hana mambo mengine anamsumbua mama, hiyo ni kweli wala msibishe, ninasema kitu ambacho nimekifanyia utafiti ni kweli, baba anakunywa anarudi anataka chakula huku nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaomba wakina mama hawa wasaidiwe na kingine ninapenda niseme kwamba tunapowapa mkopo basi mkopo ule utolewe kwa wakati. Kwa mfano, mtu anataka mkopo alime nyanya, nyanya inalimwa kuanzia mwezi wa nne na kuendelea huko kwenye kiangazi…

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wakina baba sio wakina baba wote ambao hawajali watoto zao, mimi nasimama nafasi ya baba na mama pia, ahsante. (Makofi)

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana hiyo naipokea lakini ni kwa baadhi ya akina baba…

SPIKA: Mheshimiwa Mjika.

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema sio akina baba wote.

SPIKA: Mheshimiwa Mjika, subiri kidogo.

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, bee.

SPIKA: Mheshimiwa Minza Mjika, unaikubali taarifa hiyo?

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, naikubali sio kwa akina baba wote wanaofanya hayo matendo kama nilivyosema kwamba hususani wengi kule vijijini. Mimi natoka Simiyu nawaelewa ndugu zangu kule, lakini sio kwamba wote sio wote nalitambua hilo.

Mheshimiwa Spia, kitu kingine wakina mama wapewe mkopo kwa muda muafaka. Anapoomba mkopo kwamba pengine anataka kuanzisha biashara yake apewe kwa muda muafaka, lakini anapocheleweshwa kupewa mkopo anajikuta sasa anakuwa nje ya matarajio yake na hafanyi vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, ninapenda niongee juu ya hili jambo kwamba wakina mama wapate muda mzuri wa kuweza kufundishwa ujasiriamali kama nilivyosema hakuna kitu kinapotosha kama hicho. Inapofika marejesho wakina mama wengi tunaona jinsi wanavyohangaika wanakimbia huku na huku kumbe hawakupata shule nzuri kabla ya kuchukua mkopo wao.

Mheshimiwa Spika, basi kwa hayo yote ninapenda nishukuru ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)