Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Dr. Thea Medard Ntara (1 total)

MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Na mimi naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri Mkuu swali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa na mkakati wa kutekeleza miradi mikubwa kupitia Mtwara corridor lakini mpaka sasa wananchi hawana uelewa juu ya miradi inayojumuishwa na iliyotekelezwa angalau kwa asilimia 50;

Je, Serikali inatoa maelezo gani juu ya utekelezaji wa hiyo Miradi ya Mtwara Corridor?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Thea Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Mtwara Corridor ambao pia na mimi mdau ni mradi ambao unaasisiwa na Serikali yetu. Mradi huu una maeneo mengi yanayotekelezwa ili kusheheneza mahitaji ya Mtwara Corridor. Mtwara Corridor inatazamiwa kuimarisha huduma mbalimbali kutoka Mtwara kuelekea Mkoani Ruvuma, na pale Ruvuma tuna Mkoa jirani wa Njombe kwa kutumia fursa zilizopo kwenye maeneo haya. Kwa hiyo mikoa hii minne Lindi, Mtwara, Ruvuma pamoja na Njombe ni wanufaika wakubwa wa mradi huu.

Mheshimiwa Spika, kwanza tuna mradi wa kuimarisha barabara ambayo tunayo sasa ya lami inatoka Lindi, Mtwara inafika Ruvuma kupitia wilaya zake hapa katikati za Masasi na Tunduru. Na baada ya kufika Songea Mjini Mkoani Ruvuma tuna barabara inakwenda Mbinga mpaka Mbamba Bay, na wale wenyeji mnajua na mimi nimepita huko kuona na kukagua miradi yote hiyo. Sasa tuna barabara inatoka Songea kuelekea Njombe na barabara nzuri inajengwa kutoka Njombe kwenda Ludewa na barabara kote huko tumepita na tumeona kazi nzuri inafanyika.

Mheshimiwa Spika, lakini pia eneo la pili tunaimarisha bandari zetu zilizoko kwenye maeneo haya. Tumeona na wote mashahidi Bandari ya Mtwara imeimarishwa na leo inaanza kupokea meli kubwa; na lengo bandari hii iweze kuhudumia Mikoa hii ya Lindi, Mtwara mpaka Ruvuma pia na nje ya nchi kwenda Malawi na Msumbiji. Tuna bandari nyingine mbili zimeimarishwa, ile ya Mbamba Bay tumeona imeimarishwa, na bado itajengwa kubwa; lakini pia Lihuli au Litui, moja kati ya miji hii tumeona inaimarishwa. Pia Mkoani Njombe kule Ludewa Tungi kuna bandari pale; lakini pia hata Mkoani Mbeya Wilaya ya Kyela nako pia Ziwa Nyasa kuna bandari pale tumeenda na tumejenga na meli zinatoa huduma na nchi ya jirani.

Mheshimiwa Spika, pia tunataka tuimarishe kazi kubwa ya ujenzi wa reli inayotoka Mtwara kwenda Ruvuma na kwenda Mkoani Njombe kule Liganga Mchuchuma kwa ajili ya kuchukua mawe, na reli hii pia itakwenda mpaka Mbamba Bay. Kwa hiyo hii yote hii ndio inaitwa Mtwara Corridor, chini ya program ambayo Mheshimiwa Mbunge anahitaji kujua. Kwa hiyo tumeshaanza kazi hiyo na tunaendelea.

Mheshimiwa Spika, sasa ili wananchi wajue Mtwara Corridor ni nini, sasa Serikali inajipanga, tunapoendelea kwenda kujenga SGR kutoka Mtwara mpaka mikoa ya Ruvuma pamoja na Njombe kule Mchuchuma tunaendelea sasa kujipanga kutoa elimu ya nini Mtwara Corridor inahitaji na namna gani wananchi watanufaika kwa fursa za Mtwara Corridor ili tuweze kupata maslahi mazuri kupitia program hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Serikali tunajipanga sasa kutoa elimu, kutoa hamasa kwa wananchi kuwa tayari kupokea mpango huu wa Mtwara Korido. Kwa hiyo malengo ya Serikali bado yamebaki palepale na utekelezaji unaendelea hatua kwa hatua, na pindi utakapokamilika wananchi wote watakuwa wanajua umuhimu wa Mtwara Corridor, ahsante sana. (Makofi)