Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Furaha Ntengo Matondo (4 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Bunge lako tukufu ikiwa ni mara yangu ya kwanza, lakini pia nipende kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya njema na kuweza kuwa hapa siku ya leo kwa ajili ya mchango wa hotuba ya Rais.

Mheshimiwa Spika, napenda kwanza kumshukuru Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa aliyoifanya kwa wananchi wetu wa Tanzania kwa kuonesha kwamba imani ya Tanzania inapatikana na mpaka leo hii tukiwa Bungeni tuna amani kubwa sana, lakini pia niwashukuru wanawake wa Mkoa wa Mwanza kwa kuniamini na kuweza kunichagua kuwa mwakilishi wao katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakishukuru sana Chama changu cha Mapinduzi kwa kunichaguwa na kunipa nafasi ya kuwa Mbunge katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba moja kwa moja nijikite kwa Wizara ya Mifugo na Uvuvi, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuona kwamba tuna haja ya Wizara hii kupata kipaumbele kikubwa ambavyo vimewapatia katika hotuba yake tumeisoma sote ni hotuba ambayo imelenga kujenga sana kwenye Kanda zetu za Ziwa na hata kwenye bahari.

Mheshimiwa Spika, ninaomba sasa kwa wale wavuvi wadogo wadogo ambao wao bado hawajatizamwa vizuri, waweze kuona ni jinsi gani wanaweza kupatiwa zana za kuweza kufanya kazi ili waweze kuondokana na changamoto za uvuvi harama. (Makofi)

Katika Kanda ya Ziwa hasa Mkoa wa Mwanza kuna akinamama ambao ni wafanyabiashara na wanafanyabiashara ndogo ndogo, lakini akinamama wale wanaitwa akinamama wachakataji, tunaomba sasa waweze kupatiwa vitendea kazi ili waweze kupata chanja za kuanika dagaa na hata kuanika samaki ili wasiweze kuanika chini na hata samaki wale na dagaa wakawa na mchanga kitu ambacho kinawanyima soko, lakini pia hatupati afya bora kwa sababu tunakula chakula siyo bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba kidogo niongelee suala la elimu; ninashukuru sana Serikali yetu imeweza kutoa vipaumbele kwa wanafunzi wetu ambao wanasoma bure mpaka form six, lakini pia wameweza kujenga majengo ya shule kila sehemu imeonekana. Niombe tu tunawanafunzi wetu watoto wa kike ambao ningeomba kila Wilaya basi angalau ipate shule ya bweni ya kuweza kuwawezesha mabinti zetu waweze kusoma wakiwa wametulia ili waweze kupata elimu bora tunapokwenda kusema hamsini kwa hamsini ili iweze kuwa ratio sawa na hata mabinti zetu waweze kuwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongee kidogo kuhusu suala la afya, naishukuru sana Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa John Pombe Joseph Magufuli kwa kuona kwamba hatuwezi kuenenda bila kuwa na afya njema, hilo ninamshikuru sana. Ameweza kujenga vituo vya afya, hospitali za kanda na kila kata kuna hospitali. Lakini niombe, naomba tuweze kupata matabibu katika vituo vya afya, lakini pia tuweze kupata madaktari watakaoweza kutoa dawa za usingizi kwa sababu majengo yamejengwa, lakini ni madaktari wetu kidogo wamekuwa ni wachache basi niombe Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli iweze kuona kuna haja sasa ya kuajiri madaktari na wanaotoa dawa za usingizi ili wananchi wetu wasiweze kuhangaika kwenda kupata huduma mbali wakati huduma wameshawekewa karibu.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa sababu Serikali yetu imeona ni jinsi gani akinamama tunahangaika ikaona kuna haja ya kuweza kupata mikopo ya asilimia kumi. Sasa niombe Wizara husika iweze kusimamia ili asilimia kumi iweze kutoka kwa wakati na wanufaika waweze kupata kile walichokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kumalizia naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kuweza kuchangia katika Wizara njeti ya Mifugo na Uvuvi. Pia napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipatia afya njema na kuweza kusimama siku ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza, napenda kumshukuru Waziri, Naibu Waziri, Makatibu wetu wote na wadau wa mifugo na uvuvi kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Napenda sana kuishukuru Serikali kwa kazi nzuri ambayo imefanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoka Mkoa wa Mwanza, tumezungukwa na ziwa. Tulikuwa na changamoto moja kubwa sana. Wavuvi wetu hapo nyuma walikuwa wanapata shida sana, wakitoka wilaya moja kwenda wilaya nyingine ni lazima walipe. Tuna wilaya saba katika Mkoa wetu wa Mwanza, unamkuta mvuvi mmoja kwa mwezi mmoja analipa mara saba. Kwa kweli ilikuwa ni kero kubwa sana na iliwasumbua sana wavuvi wetu, lakini nipende kuishukuru Serikali kwa sababu kero ile iliweza kuondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naipongeza Serikali na kuishukuru kwa kazi nzuri ambayo ilifanya kwa wavuvi wetu; tulikuwa na desturi ya mvuvi mmoja ikifika Januari unatakiwa kulipa leseni na ukishindwa unapewa faini mwezi Januari huo huo au Februari. Sasa tumepewa kipindi cha miezi mitatu, mvuvi anajianda na kuweza kulipa kuanzia mwezi wa Kwanza mpaka mwezi wa Tatu wanalipa kwa hiari, lakini kama hatalipa, atakwenda kulipa kwa faini ifikapo mwezi wa Nne. Naishukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuiomba Wizara ya TAMISEMI pamoja na halmashauri zetu, tuna kero kubwa sana katika Halmashauri zetu. Tuna wavuvi wadogo wadogo ambao kwa Kiswahili kizuri, wanavua kwa kasia ambayo ni mitumbwi midogo ya futi 14; lakini tuna mitumbwi mikubwa ya futi 28 mpaka 30 ambayo inatumia engine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajikuta wavuvi wale wanalipa ada ya leseni sawa na mvuvi mwenye mitumbwi ya mashine. Ni kero na inawaumiza sana wavuvi wetu, hawawezi kujikomboa kutoka kwenye hali ya umasikini wakaenda kwenye kipato cha kati. Naomba sana Wizara husika iweze kuingialia kati na kuona hili suala. Napenda kuiambia Serikali, mchango wangu ni kwa wale wavuvi angalau kama Halmashauri inalipa 100,000/=, wavuvi wa kasia waweze kulipa shilingi 50,000/=. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ada ya ushuru kwenye mitumbwi. Wanapewa kulipa mitubwi sawa na mtumbwi wa mashine, kiasi kwamba mitumbwi ya kasia wala haiwezi kwenda sehemu yoyote mbali. Unaukuta mtumbwi wa mashine unatoka Mwanza mpaka Bukoba, lakini unakwenda kuleta mazao unakuja kuuza Mwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtumbwi wa kasia hauwezi kutoka hapa mpaka hata kisiwa kingine, kwa sababu ukipanda kwenye ule mtumbwi kwanza unayashika hata maji; ni mtumbwi mdogo, ni mtumbwi hatarishi, ni mtumbwi ambao watu wanajitafutia chakula. Naomba sana viongozi wetu na Serikali yetu iweze kuliona hili suala. Ushuru unaolipwa kwenye mtumbwi wa mashine wasipewe hata wale wengine kulipa kwenye mtumbwi wa kasia. Hii inawaumiza sana wavuvi wetu wadogo wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimechangia hapa hata muda ulioisha, nikaomba sana, wavuvi wetu wadogo wadogo waweze kutoka kwenye hali waliyonayo, Serikali iweze kuwatambua na kuwapatia mitaji waweze kutoka, lakini kila wakati wanabanwa. Wakitaka kujikwamua huku, wanabanwa, kweli watatoka? Hili suala ni gumu, lakini nina imani Serikali ikiingilia kati, hili suala litakuwa jepesi na watafanya kazi kwa weledi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba, tuna vijana wetu ambao wamemaliza vyuo vikuu, lakini hawajapata ajira. Ni wafugaji wazuri sana wa samaki, tunapata shida. Wananchi wengi wanatafuta jinsi gani ya kuweza kujikwamua kuchimba mabwawa hata kupata kipato, lakini hakuna wataalamu. Halmashauri zetu hazina wataamu wa ufugaji wa Samaki. Hebu niiombe Serikali iweze kuwachukuwa wale vijana, waweze kuji-organize, wapewe mtaji, wataweza kuwasaidia hata wananchi wetu ambao wanahitaji kufanya ile kazi, lakini hawana utaalamu. Unakuta hata kwenye Halmashauri husika, mtaalam ni mmoja, Halmashauri nzima inawezaje kuhudumiwa na mataalamu mmoja wa ufugaji wa Samaki? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Wizara husika iweze kuliangalia hili suala angalau ipitie kila Halmashauri waweze kuajiriwa hawa vijana waweze kuleta weledi katika nchi yetu. Nina imani kubwa ufugaji wa samaki unaleta pato kubwa sana katika nchi yetu na walaji wetu wa samaki wanaweza kupata protein za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la ulinzi au salama wa wavuvi wetu wakiwapo ziwani. Wavuvi wetu wameachwa sana. Wavuvi wetu wanaliletea Taifa letu pesa nyingi sana, lakini hawajaliwi kabisa. Nikitoka Goziba nikija Ukerewe, Rolia, Muleba hakuna Kituo cha Polisi (Police Marine) cha kuangalia usalama wa wavuvi wetu na wafanyabiashara wanaoishi kandokando ya ziwa. Hii inaumiza sana kwa sababu wale watu wasipoangaliwa kila wakati wanavamiwa ziwani; kila wakati wananyang’anywa mashine; kila wakati wanaumizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iweze kufuatilia hili suala, iweze kuwapatia hawa watu waweze kuwa na ulinzi ambao utawasaidia hata wakiwa wanafanya kazi zao waweze kufanya kazi zao lakini wakiwa wametulia na akili zao zikiwa kabisa ziko vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wanawake wenzetu ambao wako katika hali ya kufanya biashara ndogo ndogo katika mihalo. Wale akina mama ni wachakarikaji, nilishasema last time wakati naongea hapa. Naomba sana Serikali iweze kuona hili suala waweze kupatiwa mitaji wana biashara ndogo ndogo za kuchukua dagaa, lakini unawakuta wale akina mama wanaanika dagaa kwenye mchanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wale dagaa wanakuwa ni wachafu na hata hawawezi kuliwa wakawa ni chakula cha binadamu. Naomba wapatiwe mitaji waweze kutengenezewa chanja. Zile dagaa wakianika kwenye chanja wanaweza kujipatia kipato kikubwa, lakini pia wakaingia hela Serikalini, nao wenyewe wakajikwamua kutoka kwenye umasikini walionao wakaingia hata kwenye hali nyingine. Wanahangaika sana siku hadi siku. Siku zinavyozidi kukatika lakini hawapati chochote, hali inakuwa ni ile ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, Serikali yetu ni sikivu, imejaribu kutusikiliza sana kila wakati. Kwa hiyo, naomba sana kuhusiana na hii kero ya wavuvi wadogo wadogo kutoa tozo. Kwa kweli inaumiza. Hata ukiuliza, yaani inaumiza sana. Waweze kutoka katika sehemu ya tozo ambazo ni sawa na mitumbwi mikubwa, angalau wapate tozo ambazo ni tofauti na wengine. Nina imani sana, ikiwa hivyo itasaidia sana wavuvi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wavuvi wetu wanakwenda ziwani, wanafanya kazi ngumu, wanafanya kazi kubwa, lakini wanapoleta mazao yao, hawana sehemu ya kuonesha kwamba tuna masoko yetu ya kuuzia samaki ambayo nikileta mzigo wangu, nikipeleka soko fulani nitapata faida.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia katika Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nipende kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipatia afya njema lakini kunipa ridhaa na kibali cha kuweza kusimama katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nikushukuru wewe mwenyewe kwa kazi yako nzuri ya weledi ya kuliendesha Bunge hili lakini nimshukuru Mheshimiwa Waziri kaka yangu Simbachawene, nimshukuru pia Naibu Waziri kaka yangu kwa kazi kubwa ambazo anazifanya. Katibu Mkuu na timu yao nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya kwa wananchi wa Tanzania kuhakikisha wananchi wako salama na wanafanya kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kuagiza watumishi wote walioondolewa kwenye utumishi wa umma kuweza kupata mafao yao. Ni jambo ambalo ni zuri sana kwa watumishi wetu ambao waliachishwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nipende kumshukuru Mheshimiwa Rais kuagiza watumishi ambao walikaa zaidi ya miaka mitano bila kupandishwa madaraja kuweza kupandishwa madaraja. Ninamshukuru sana sana kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naendelea tena kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa juzi tu kutangaza ajira nyingi, ajira 21,200 kwa vijana wetu wa Tanzania. Kwa kweli ni jambo kubwa kwa sababu ni muda mrefu ajira zilikuwa hazijatangazwa. Ajira hii ni kada ya afya na kada ya elimu. Ajira 13,130 kwa kada ya elimu, lakini tuna ajira 8,070 kwa kada ya afya. Ni jambo kubwa na ni jambo la kumshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia napenda niongelee katika Mkoa wangu wa Mwanza. Katika Mkoa wangu wa Mwanza, walimu wa shule ya msingi tunauhitaji wa walimu 19,842. Walimu waliopo ni 12,529, tuna uhitaji wa walimu 7,313.

Mheshimiwa Spika, tunaishukuru Serikali kwa kuajiri lakini tunaona ni jinsi gani changamoto ya ajira ilivyokuwa kubwa katika nchi yetu. Huu ni Mkoa tu mmoja wa Mwanza ambao shule za msingi tuna uhitaji wa walimu 7,313. Unaona ni jinsi gani hata weledi wa watoto wetu kupata elimu inakuwa ni changamoto kwa sababu ya walimu ambao bado ni wachache. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikitoka hapo, walimu wetu wa sekondari kwa maana ya sayansi tunao wachache sana. Kwa Mkoa wangu wa Mwanza uhitaji ni 3,750 lakini walimu tulionao ni 1,731. Upungufu tuna 2,019. Unaona ni jinsi gani changamoto ya walimu wetu wa sayansi katika Mkoa ilivyo ni kubwa. Hii inaonyesha wazi tutakuja kukosa vijana wetu madaktari lakini pia tutakosa ma-engineer, hata watu ambao wanatusaidia kwa maana ya kada muhimu kama hii kuweza kuwa na shida. Kwa hiyo, nizidi kuiomba Serikali yangu tukufu pamoja na kwamba ajira zimetolewa lakini ione changamoto hii tunaweza kwenda kuitatua vipi kwa kuongeza watumishi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa Mkoa wa Mwanza tuna changamoto kubwa sana tena kwa watu wa afya. Watumishi tulionao, waliopo ni 3,411; wanaohitajika ni 10,136 lakini upungufu tuna watumishi 6,975. Huo ni mkoa mmoja tu na tumeajiri 8,070. Utaona ni jinsi gani tuna mahitaji makubwa ya wataalam wetu, madaktari wetu. Tunajenga vituo vya afya lakini tunajenga zahanati. Bila kupata wataalam hawa tutakwenda kufanya kazi gani katika hizo zahanati zetu na vituo vya afya? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizidi kuiomba Serikali yangu tukufu iweze kuliona hili changamoto ni kubwa. Tusije tukajenga majengo yakaja kuishia kwenye popo tu. Bila kupata wataalam hatuwezi kufanya kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali yangu iendelee na mkakati huu maalum ambao wanao wa kuweza kuendeleza wataalamu wetu ili angalau tuweze kuendana na kasi ya wananchi wetu tuliopo huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niongee kidogo kuhusu suala la wastaafu wetu. Wafanyakazi wetu wanaajiriwa. Anaajiriwa mtu akiwa na miaka 20, anaajiriwa kwenye Mfumo wa LAWSON wote wanajua wanaingia mle lakini hata kabla hajastaafu, ndani ya miezi sita anaandika barua ya kustaafu lakini inakuja kufika kipindi anatakiwa kustaafu, anaanza kuambiwa mfumo wako hauonekani vizuri, mara barua zako hazionekani. Tuliwezaje kumlipa huyu mtu mshahara wakati anafanya kazi kama barua zake hazikuwemo kwenye mfumo? Tuliwezaje kuwa na huyu mtu miaka 20,30 kazini kama tulikuwa tunajua ana matatizo? Wazee wetu wamehangaika sana. Walipata changamoto kubwa sana, walimu shule zilikuwa ni mbali, mtu anatembea kwa baiskeli kwa mwendo mrefu saa 10 usiku anaamka. Inakuja kufika mwisho ameishiwa nguvu anaanza kuambiwa barua zako hazionekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inaumiza sana, tuone ni jinsi gani tutaendelea kuwasaidia wazee wetu waliotufikisha hapa kuweza kuwaachia maisha yao ya baadaye yaweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishukuru sana Serikali yangu kwa kuleta Mfumo mzuri wa TASAF kwa ajili ya kupunguza umasikini kwenye kaya zetu. Mfumo wa TASAF ni mzuri sana na ninaupongeza sana lakini changamoto iliyopo kwa wananchi wetu ni kukosa elimu.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali yangu tukufu kuona kuna haja sasa ya kuwapelekea wananchi wetu elimu, waweze kujua nini maana ya TASAF? Pia waweze kujua TASAF ina malengo gani kwao?

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. FURAHA N. MATONDO: ...Waweze kutambua taratibu zake zikoje kwa wananchi na walengwa ni watu wa namna gani?

SPIKA: Mheshimiwa Furaha Matondo kuna taarifa kutoka Mheshimiwa Waziri wa Nchi.

TAARIFA

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge ya kukubaliana naye kwamba Mfumo ama program ya Mradi wa TASAF ni mradi muhimu sana na unahitaji elimu na jambo hili lilithibitishwa pia na Diwani wa Chama cha CHADEMA katika Kata moja ya Masasi Mjini alipokuwa anaishukuru Serikali kwa kazi nzuri iliyofanywa na Program ya TASAF katika kata yake ya CHADEMA pale Masasi Mjini na akaomba elimu itolewe nchi nzima, Watanzania wote ikiwemo vyama vyote vya siasa waelewe mradi huu wa TASAF ulivyo mzuri na unavyosaidia wananchi. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Tunza Malapo unamfahamu huyo Diwani jina lake ili Mheshimiwa Waziri…

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nashukuru.

SPIKA: Mheshimiwa ngoja, subiri. Mheshimiwa Tunza Malapo unalifahamu jina la huyo Diwani?

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, hapana simfahamu.

SPIKA: Haya ahsante sana. Mheshimiwa Furaha Matondo unaipokea taarifa hiyo ya Mheshimiwa Waziri?

MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo ninaipokea kwa sababu TASAF wanafanya kazi nzuri, changamoto ilikuwa ni elimu tu kama alivyosema. Kwa hiyo, niombe wananchi wetu waweze kupata elimu waweze kujua nini misingi ya TASAF lakini taratibu zake zikoje kwa wananchi na walengwa ni watu wa namna gani?

Mheshimiwa Spika, maana yake ni kweli mikutano inaitishwa na watu wanaitwa lakini wengine hawawezi kuhudhuria maana hawaelewi nini maana ya TASAF. Licha ya hivyo, kuna wazee wengine ambao familia zao vijana na watu wanaowazunguka wanauwezo wa kufanya kazi. Kwa hiyo, wananchi wengi hawajui ni kitu gani kinatakiwa kwa wale baba zetu na ndugu zetu walioko kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hilo naomba niseme kidogo tena kwenye changamoto iliyopo kwenye ajira zetu. Kuna nyumba watu wako wanne, ameanza kuomba ajira wa kwanza huu ni mwaka wa tano mpaka wa sita lakini mpaka na wadogo zake wamekuja kusoma wamekuwa watu wanne wanasomeshwa kwa shida lakini mpaka leo hawajapata ajira. Kila wakiingia kwenye mfumo kuomba ajira, ajira zikitoka hawamo. Inaumiza, ni kweli Wabunge tuliomba humu wote wala siyo wachache, simu zetu zimejaa kuombwa ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wabunge unajua kabisa ni jinsi gani hatuwezi kuajiri lakini tunajua mfumo wetu ni mfumo ambao unatenda haki. Basi ukatende haki kwa wananchi wetu. Kama ambavyo tumesema changamoto kubwa iliyoko hata kwenye Mkoa wangu wa Mwanza, tuna vijana wengi ambao hawajaajiriwa. Wamemaliza wana zaidi ya miaka mitano, miaka sita wanahitaji ajira lakini mpaka leo ajira hazijapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuombe sasa haki ikatendeke, vijana wetu waweze kupata ajira. Changamoto iliyopo iweze kupatikana. Mkate tunaoupata tuweze kugawana wote ratio sawa. Mikoa mingi tuna shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo naunga mkono hoja, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia katika Wizara hii nyeti, Wizara ya Afya. Kwanza kabisa nipende kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipatia afya njema lakini pia kuweza kusimama katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nipende kumpongeza Mheshimwa Rais, Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuhakikisha wananchi wetu wa Tanzania wanakuwa na afya njema ili waweze kutimiza majukumu yao.

Mheshimiwa Spika, naomba nimpongeze Waziri, Ndugu yetu na rafiki yetu, anafanyakazi kubwa sana kuhakikisha wizara hii inafanyakazi nzuri sana kwa wananchi wa Tanzania waweze kuwa na afya njema lakini niishukuru wizara nzima Naibu Waziri, Katibu Mkuu lakini na watendaji wote wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, Kanda ya Ziwa tumekuwa na tatizo kubwa sana na changamoto kubwa ya kansa ya kizazi kwa sisi wanawake. Nimesimama kwenye Bunge lako kuongea tatizo hili kwasababu tumekuwa na changamoto hii wanawake wengi tumekumbwa sana na tatizo hili la kansa ya kizazi hasa Kanda ya Ziwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2021 wanawake 36,224 waliofanyiwa uchunguzi wa kansa ya kizazi waliokutwa na dalili za kansa ya kizazi walikuwa ni wanawake 1,597 na wanawake 252 walidhaniwa kuwa na vimelea vya kansa ya kizazi, wanawake 66 walikutwa tayari na ugonjwa wa kansa. Hii inaumiza sana ukizingatia sisi ni wanawake na ukizingatia ndio tunaotegemewa katika nchi yetu na katika majukumu makubwa ya familia zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kubwa kwa Wizara ya Afya ni kutoa elimu kuanzia kwa mabinti zetu mpaka kwetu sisi akina mama ili kuweza kuelewa ni kwasababu gani tatizo hili limekuwa kubwa sana katika Kanda ya Ziwa.

Mheshimiwa Spika, leo hii ukienda Bugando kuna wagonjwa wengi sana wa kansa ya kizazi. Ukienda Ocean Road imejaa wagonjwa wengi sana wanaotoka Kanda ya Ziwa. Hii inaumiza sana, ukizingatia na sisi ni wanawake na Mheshimiwa wetu Waziri wa Afya ni mwanamke mwezetu. Ombi langu ni kuomba sana elimu itolewe kuanzia mashuleni kwa mabinti zetu na hata kwa akina mama ambao watakuwa wanakwenda kliniki hata wanaokwenda hospitali waweze kujua tatizo hili linapatikana vipi lakini pia linatibika vipi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu imekuwa ni nchi ya nne kwa tatizo kubwa la kansa ya kizazi. Tanzania inaongoza kuwa ni nchi ya nne. Kati ya wanawake 100, wanawake 59 wanakufa na kansa ya kizazi nchini kote; na Tanzania ikiwa ni nchi ya nne, hii inaumiza sana na inaumiza kwasababu ni wanawake wengi wanaopoteza maisha kutokana na tatizo hili kubwa. Niombe sana wizara hii iweze kuangalia kwa jicho la tatu tatizo hili kwa wanawake limekuwa ni sugu na linatuangamiza sana sisi wanawake, elimu itolewe sana kwa mabinti zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na tatizo hili nchi yetu ya Tanzania inaongoza kwa vifo vya kansa ambavyo tuna aina tano za kansa katika nchi yetu ya Tanzania. Ukiacha kansa ya kizazi ya wanawake tuna kansa za ngozi, mkojo (kansa ya tezi dume), kichwa, shingo, koo na kinywa, pamoja kansa ya matiti. Magonjwa yote haya hayajatolewa elimu ya kutosha, hayafahamiki ni jinsi gani tunaweza kuyaepuka ili tuepukane na hili tatizo. Kwa hiyo, ombi langu kubwa kwa Serikali niombe sana iweze kutoa elimu kuanzia kwa mabinti zetu lakini pia iweze kuwafahamisha ni kwanini tatizo hili limekuwa sugu katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, vifo hivi vinavyoangamiza wanawake wenzetu na mabinti zetu ni vingi sana. Inavyoonesha tatizo hili ni sugu katika nchi yetu wanawake wanaokufa kwa kansa ya kizazi ni wengi. Kama takwimu zinavyoonyesha, kati ya wanawake 100,000 wanawake 59 wanakufa kwa kansa ya kizazi… (Makofi)

MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Furaha Matondo kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Agnes Marwa.

T A A R I F A

MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Spika, natoa taarifa kwa muongeaji kwamba kutokana tatizo hili kubwa ndiyo maana Mheshimiwa Rais ametoa fedha kwa ajili ya kujenga Hospitali Maalum ya Taifa kwaajili ya wanawake na watoto ikiwemo suala la hili la kansa kwa wanawake.

Mheshimiwa Spika, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Furaha Matondo.

FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo ninaipokea, lakini ninaomba sana elimu itolewe, na hasa chanjo kwa mabinti zetu zipatikane. Kwasababu tatizo hili ni kubwa nasilakufumbia macho. Vifo vya kansa ya kizazi vimekuwa ni tishio katika nchi yetu hasa kwa upande wa Kanda ya Ziwa. Ni vifo ambavyo vinaangamiza sana wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe sana Wizara iangalie tena kwa jicho la tatu.Tunaliongelea suala hili hapa lakini wengi hawana elimu na hawajui kwasababu gani wanapata matatizo kama haya. Wengi wanapata tatizo hili wanatoka wanakwenda kutibiwa kienyeji, na wengi wanakufa kwa kukosa elimu.

Mheshimiwa Spika, tulipata tatizo la HIV katika nchi yetu elimu ilitolewa mpaka mashuleni wakajua nini chanjo cha tatizo la HIV; iweje leo wanawake waangamie kwa kukosa elimu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kubwa ni elimu kwa akina mama na vijana wetu. Chanjo hii kwa vijana inapatikana, kwanini vijana wetu hawapati chanjo? Niombe vijana wetu waweze kupatiwa chanjo hii ya kansa ya kizazi ili tuweze kuepukana na hii changamoto. Sisi akina mama tukimalizika kwa tatizo kama hili nchi yetu itaendeshwa na watu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache lakini naomba sana, Mheshimiwa Ummy amenielewa Waziri wetu naimani atakwenda kulifanyia kazi kubwa ni mwanamke mwenzetu anawatoto wa kike na anajua changamoto ni kubwa. Hoja yangu ninayomalizia ni elimu itolewe sana kwa vijana wetu…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Haya ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)