Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Bahati Keneth Ndingo (1 total)

MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru. Kwenye huo waraka nimeona tumetoa tu adhabu ya viboko, lakini tunatambua watoto wetu wengi ambao wanaonekana ni wakaidi shuleni inatokana kwa sababu wameathirika aidha na makuzi au malezi ya nyumbani. Kwa nini tusiweke pia nafasi ya watoto hawa kupewa ushauri kabla ya kutanguliza viboko; kwamba, kuwepo na ushauri kabla ya kuadhibiwa kwa viboko kwenye huo waraka? Nakushukuru.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ndingo Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye maelezo pia niliyoyatoa hapa nimetoa wito kwa walimu wetu wa shule za msingi, sekondari, lakini hii inaenda hata pia kwenye vyuo vya kati na vyuo vya juu; kwamba tuangalie ukubwa wa makosa, umri, mahali na wakati wa makosa yalipofanyika. Nataka tu nitoe taarifa kwamba kwenye taasisi zetu za elimu tuna walezi wa watoto wa kiume na wa watoto wa kike na tumeweka hii walezi kwa lengo la kutoa ushauri pale ambapo tunaona kuna umuhimu wa ushauri. Kazi hii inaendelea shule ya msingi, sekondari na tunatumia zaidi majina ya kingereza matron na patron ndio ambao wanatumika kutoa ushauri nasaha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo pale ambako mwanafunzi anatenda kosa ambalo linahitaji kushauriwa wanafanya; na ndio hii ndiyo inasaidia kupunguza pia hata mkanganyiko kwenye jamii kutokana na nidhamu za watoto hawa. Hata hivyo bado kwenye taarifa yangu nimeeleza walimu wana kazi nyingi sana wanazozifanya shuleni. Wanatumia muda wao katika kuwafanya watoto kuwajenga katika maadili, pia katika kuwafanya wadumishe mila, desturi na utamaduni tulionao huku pia wakiwapa taaluma mbalimbali. Nimetoa wito pia kwa walezi ambao ndio wana nafasi kubwa ya malezi yam toto huyu kuanzia nyumbani pia hata mwenendo wake na baadaye nimetoa ushauri kwamba ni vyema wazazi na walezi wakawa wafuatiliaji wa karibu wa mtoto huyu badala ya kuwaachia majukumu hayo waalimu pekee ili wasaidie watoto hawa kubadilisha mwenendo. Mzazi akishiriki tunaamini mtoto huyu atabadilika sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tutaendelea kutumia hizo taaisisi na idara hizo za ushauri ambazo ziko katika kutusaidia pia kurekebisha mwenendo wa mtoto awapo shuleni, ahsante.