Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Bahati Keneth Ndingo (8 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kupata fursa ya kuchangia katika Wizara hii ya Afya na Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuipongeza sana Wizara kwa kazi nzuri na nzito ambayo wameendelea kuifanya. Pia nimpongeze Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan kwa hotuba yake aliyoitoa tarehe 7 kuhusiana mambo ya masuala mazima ya wazee. Kwa kweli, hotuba ile iliwapa matumaini makubwa wazee na tunashukuru kwa kutambua thamani kubwa ya wazee wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua tuna Sera ya Wazee iliyotungwa mwaka 2003 lakini mpaka sasa hatujaitengenezea sheria ya kusimamia utekelezaji wake. Hata kama tuna mipango mizuri na mikubwa kwa ajili ya wazee wetu kama tunakosa sheria ya kusimamia utekelezaji wa sera hizi, itakuwa ni ngumu sana changamoto za wazee kupata muarobaini. Kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anakuja ku-windup atuambie ni lini ataleta Bungeni sheria ya kusimamia utekelezaji wa Sera hii ya Wazee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze sasa kwenye vituo vya kulelea wazee vinavyomilikiwa na Serikali. Nitambue kwamba Serikali inafanya kazi kubwa kwa ajili ya wazee wetu na sasa hivi tuna vituo takriban 16 nchi nzima vya kulelea wazee, lakini hali ya vituo hivi kwa kweli inasikitisha. Mimi binafsi nimeshatembelea baadhi ya vituo vya kulelea wazee, niliwahi kwenda pale Fungafunga Morogoro miundombinu ya pale si rafiki. Ilani ya Chama cha Mapinduzi imetuelekeza kwamba wataenda kukarabati vituo 5 kama ifuatavyo: Kituo cha Kolandoto (Shinyanga); Kituo cha Nunge (Dar es Salaam); Kituo cha Njoro (Kilimanjaro); Kituo cha Magugu (Manyara) na Kituo cha Fungafunga (Morogoro). (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba wanapokwenda kufanya maboresho ya vituo hivi pia waangalie sana miundombinu ambayo itakuwa rafiki kwa wazee. Kwa mfano, pale Fungafunga (Morogoro) ukiangalia kile Kituo cha Wazee vyoo vyao viko nje kabisa ya sehemu wanazolala na wale wazee wanahitaji kusaidiwa kwa sababu ni watu ambao umri wao umekwenda sana.

Mheshimiwa NaibU Spika, kwa hiyo, niombe sana wanapofanya marekebisho ya vituo hivi waangalie miundombinu rafiki ambayo haitakuwa vikwazo kwa wazee wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na miundombinu kuwa rafiki vifaa vya kuhudumia wazee kwenye hivi vituo hakuna, hata gloves za kuwasaidia wale wazee hakuna. Kwa hiyo, niombe sana sana Serikali vifaa viwepo kwenye vituo hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwenye vituo hivi vya Serikali huduma zinazotolewa mle ndani ni huduma za kwanza yaani mzee atapewa tu Panadol, ndio zinazokuwepo pale lakini ile huduma angalau inakuwa ni ngumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi vituo vingi vyao vipo nje sana ya miji na kusababisha wazee wengi kupoteza maisha kwa sababu ya umbali. Kwa mfano, hiki cha Fungafunga (Morogoro) kwa sababu nimeshakwenda hata barabara ya kufika pale kituoni hakuna, watu wanapita chini ya lile bomba la reli, hata gari zikifika pale kuleta dawa wanaenda na pikipiki wanavuka wanachukua ndio wanakuja kuzileta kituoni. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri muangalie sana miundombinu ya hivi vituo vya wazee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilifurahi kusikia kwamba mna utaratibu wa kuanzisha uniform kwenye vituo vyetu vya afya, kwamba watu wanaohudumia wazee mtatoa uniform maalum ili mzee akifika pale ajue hawa ndio wanaohudumia wazee. Naomba katika utaratibu huo mwaangalie pia walemavu na viziwi ili wajue kabisa, kama mtaweka sare hizo kwa wazee muweke na sare pia kwa watu wengine ambao wanauhitaji maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, naomba niongelee kuhusu mambo ya vyoo. Magonjwa mengi sana yanatokana na ukosefu wa vyoo; usambazaji wa uchafu kutoka vyooni. Kuna kampeni moja ilikuwa inaongelea “Nyumba ni Choo.” Kampeni ile ilifanyika, lakini kwa vijijini kule bado suala la vyoo ni shida. Kwa hiyo, naomba sana, kampeni hizi za nyumba ni choo iendelezwe ili iweze kuleta tija mpaka kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kule vijijini hakuna vyoo na maradhi mengi yanatokana na kukosa vyoo. Endapo Serikali mtaichukulia uzito hii Kampeni ya Nyumba ni Choo na vyoo vikawepo kwenye kila maeneo, itatusaidia sana kupunguza magonjwa mengi na itaisaidia pia Serikali kutopoteza fedha nyingi kwa sababu ya kukosekana magonjwa ambayo ni hatarishi. Kwa hiyo, niwaombe sana Serikali mjitahidi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, kengele imeshagonga.

MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kupata fursa, nami nianze kwa shukrani kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza tangu niingie hapa Bungeni nikiwa Mbunge wa Jimbo la Mbarali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kukishukuru Chama changu, ninashukuru Halmashauri Kuu ya Chama changu na ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa imani kubwa waliyonayo na kurejesha jina langu ili nikawanie kiti hiki kwa kupitia tiketi ya Chama cha Mapinduzi. Pia ninawashukuru sana wana CCM wenzangu wa Jimbo la Mbarali kwa imani yao kwangu na ninawashukuru sana wananchi wa Mbarali kwa kunipa heshima kubwa ya kuwa mwakilishi wao Bungeni. Niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa uwakilishi baadhi ya Wabunge walifika Mbarali kusaka ushindi wa Chama cha Mapinduzi, ninawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho siyo kwa umuhimu niishukuru familia yangu inayoongozwa na mume wangu kipenzi kwa mapenzi, umoja na mshikamano wao, kwa niaba yao ninawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze sasa mchango wangu, msingi wa maendeleo duniani ni watu, msingi wowote wa utawala duniani ni watu na maendeleo yoyote ambayo yanaweza yakafanyika yakaacha uchungu na maumivu kwa wanadamu au wananchi, hayo maendeleo si yenye tija. Ili maendeleo yawe yenye tija ni lazima yawe yanafurahiwa na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wowote ili utekelezeke, lazima uwe mpango shirikishi, ushirikishe wananchi. Vilevile ili mpango uweze kupangika na ukatekelezeka ni lazima mpango huo sekta zote zichukuliwe kwa uzito unaostahili. Nikianza kwa sisi Mbarali, mfano mwaka 2006 Mpango wa Serikali ulikuwa ni kutanua Hifadhi ya Ruaha. Utanuzi wa Hifadhi ile ulienda kuhamisha vijiji 10 na kata moja nzima ya kule kwetu Mbarali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango ule lengo lake, pamoja na kwamba mpango ulikuwa ni kuhakikisha mnaweka uhifadhi kwenye Bonde la Ihefu na mtiririko wa maji kwenda kwenye Mto Ruaha, mpango ule haukufanikiwa. Kwa sababu gani? Ni kwa sababu hamkushirikisha watu. Badala yake, mpaka sasa uharibifu kwenye Bonde la Ihefu umeongezeka kwa kasi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa suluhu ya wataalam wa Taifa hili, wanataka tena kuwahamisha wana-Mbarali kwenye maeneo yale. Hili jambo likanifanya niwe msomaji sana wa matatizo kama haya kwenye mataifa mengine. Ni lazima tukubaliane, sekta na mchango wa chakula kwenye Taifa hili na kwenye Bonde la Mbarali siyo jambo la kupuuzwa hata kidogo, pia sekta ya uhifadhi siyo jambo la kupuuzwa; sekta ya utiririshaji maji kwenye Mto Ruaha pia siyo jambo la kupuuzwa. Mambo haya yote matatu yana uzito sawa. Kwa hiyo, wataalam wa Taifa hili na ninyi mliopata fursa ya kumshauri Mheshimiwa Rais, ni lazima msiwe wavivu wa kufikiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nasoma ripoti, mnamo mwezi wa Pili mwaka huu nchi sita zilienda kupeleka Umoja wa Mataifa mipango yao ya kurejesha maeneo oevu. Mheshimiwa Prof. Kitila hapo unapenda sana kusoma vitabu, sasa nami nakuomba ukasome ili mkashauriane vizuri kuhusiana na Mbarali. Nenda kasome mpango wa Zambia walivyofanya kurejesha maeneo oevu, kasome mpango wa Gabon, kasomeni mpango wa DRC Congo, kasomeni mpango wa Mexico, walifanya yafuatayo, na Mbarali inawezekana kufanyika ili wananchi waendelee kufanya shughuli zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, walivyofanya na nilivyosoma ripoti kwa udogo kabisa, na ni mambo ya kawaida, gharama ndogo kabisa kuliko gharama za kuhamisha watu kila baada ya muda fulani. Kwanza, walianza kujenga miundombinu ya umwagiliaji. Hiyo kazi Mheshimiwa Rais ameshaifanya Mbarali na anaendelea kuifanya. Leo Waziri wa Kilimo yuko pale, kaka yangu Mheshimiwa Bashe, tuna miradi sita ya umwagiliaji inaendelea, Dkt. Samia Suluhu Hassan ameleta shilingi bilioni 78. Mnatuhamisha twende wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya hivyo, juzi nilikuwa namwuliza hapa kaka yangu Mheshimiwa Bashe, mna mpango gani wa kutujengea mabwawa? Akaniambia wanakuja Mbarali kujenga mabwawa ya umwagiliaji. Sasa mnawapeleka wapi hawa watu wakati Mheshimiwa Rais ameshaanza mipango?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, wenzenu walichofanya, tunajua sheria za kufanya kazi pembezoni ya mito ni mita 60. Twendeni tukapande miti pembeni ya hizo mita. Nasi wana-Mbarali tuko tayari kuongoza zoezi hilo, lakini siyo kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, wenzetu wanachofanya ili kurejesha maeneo hayo wanasema wanalima kwa msimu mmoja wa mvua. Wakulima wadogo wa Mbarali ndicho wanachofanya, wanalima msimu mmoja wakati wa mvua peke yake. (Makofi)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

TAARIFA

MWENYEKITI: Mheshimiwa taarifa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, anachokizungumza Mbunge wa Mbarali, nami ni Mjumbe wa Kamati ya Ardhi, uvivu wa wataalam wetu Mheshimiwa Waziri Mchengerwa tulivyoenda kule, anawauliza kwa nini hapa mnawahamisha na hawa mnawaacha? Mtaalam anasema hawa hawana miundombinu mizuri ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, anachokizungumza Mheshimiwa Mbunge ni sahihi, wataalam wetu ni wavivu wa kufikiri. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa unaipokea taarifa hiyo.

MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, suala la Mbarali kama mlivyotuhamisha mwaka 2008, uharibifu uliongezeka zaidi. Leo ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja ni zaidi ya 170,000. Upi mkakati wa ku-recover hizo ajira? Eti tunaenda kupoteza ajira 170,000 kwa ajili ya kuhamisha watu. Kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu nakuomba, ungesitisha hata zile fedha zile za tathmini, mgeendelea kutujengea miundombinu Mbarali ili tuendelee kuwa salama. Tathmini hizo za nini wakati utaalam unajulikana? Kasomeni ripoti, wenzenu wa nchi hizi wamefanya haya na yamewezekana. Leo wananchi wa Mbarali wamesimamishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Rais, alimtuma Makamu Mwenyekiti wa Chama hiki awaambie wananchi wa Mbarali walime, lakini yako maeneo ambayo walikatazwa kulima. Leo hii ugonjwa wa sukari na Mheshimiwa dada yangu Mheshimiwa Ummy ungepeleka vipimo kule. Katika Wilaya ambayo watu wanaumwa sukari na pressure, Mbarali inaweza ikaongoza. Kwa hiyo, naomba sana, jambo hili hebu wataalam wa Taifa hili msiwe wavivu kufikiri. Yanapokuja masuala magumu ya wananchi, twendeni tukahakikishe wananchi wanafurahia maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la utiririshaji wa maji ni muhimu. Nimezunguka Mbarali wakati wa kampeni, hata kabla ya hapo tumezunguka maeneo mbalimbali. Tumewashauri watu wa mazingira, Mbarali inapokea maji kutoka maeneo tofauti tofauti, ina vijito; mito ile imeziba. Mnasema utiririshaji wa maji kwenda Ruaha ni mbaya, tumewaambia nendeni mkachimbue ile mito vizuri ili mtiririko wa maji uende vizuri. Leo hii tunakwenda kuwaadhibu masikini wenye heka mbili, tatu, nne. Ina maana kweli sisi hatuwajui watumiaji wa maji wakubwa Mbarali? Hapana, siyo sawa. Ni lazima ifikie wakati tumshauri Mheshimiwa Rais kwa kuangalia maslahi mapana ya wana-Mbarali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hili inawezekana labda wenzetu, sijui, mnaogopa kuliwasilisha. Mimi binafsi nimemwandika barua Mheshimiwa Rais nikamwone kuhusiana na hili ili nikamweleze kama ninyi mnashindwa kutusaidia wataalam wa Taifa hili kupeleka maoni ya wana-Mbarali na utaalam halisi unaonekana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemeandikia nimwone. Naamini Mheshimiwa Rais atanipa fursa nimwone, nimwelezee nini wana-Mbarali wanataka? Naamini kwa usikivu wake, kwa upendo wake wana-Mbarali atatupa fursa tutaliangalia upya suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashukuru sana kwa kupata fursa hii. Nawaomba sana wataalam na mnaoweza kumshauri Mheshimiwa Rais, mkiwa mnakaa, suala la Mbarali siyo la kujadiliana kwenye karatasi kirahisi, siyo suala la kukaa na kujadiliana kwenye makaratasi. Chama cha Mapinduzi chenye Serikali hii, kiko na wananchi kwenye suala hili.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge waliokuja Mbarali wako na wananchi, lakini Wabunge waliofika Mbarali kwenye kampeni ni mashahidi. Wameona hali halisi ya wana-Mbarali. Vilevile CCM, mimi Mbunge wao tuko na wananchi na suala la kuhamisha siyo suala jema na wanaofikiria kumshauri Mheshimiwa Rais hivyo hawawatendei haki wana-Mbarali na hawamtendei haki Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, tushauri vitu ambavyo vitakwenda kujenga hata morally ya wananchi. Twendeni mkamshauri vitu vya msingi Mheshimiwa Rais. Fikirieni wataalam wa Taifa hili, nendeni mkaanzishe vituo vya kufuatilia uhifadhi. Niwaambie kabisa, katika mpango wenu Waheshimiwa sijaona mkakati madhubuti wa mambo ya uhifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnapenda kufanya vitu simple, yaani tunafanya tu uhifadhi kwa maneno. Uhifadhi unataka investment. Wekezeni kwenye uhifadhi. Kuhamisha watu siyo suluhu la uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashukuru sana kwa kupata fursa hii, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kupata fursa nami niungane na Waheshimiwa Wabunge kuendelea kuipongeza Serikali ya Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa bajeti yake hii ya kwanza, nzuri kabisa ambayo imepokelewa kwa bashasha kubwa huko mtaani. Lakini pia niendelee kuipongeza Wizara ya Fedha kwa kazi kubwa ambayo wameifanya kutuletea bajeti ambayo inakuwa ni chachu ya maendeleo kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali kwa kuongeza vyanzo vya mapato ya ndani. Tunaona bajeti hii inayokwenda kuisha tarehe 30 Juni, tulikuwa na vyanzo vya mapato ya ndani kwa asilimia 69, sasa kwenye bajeti hii tunatarajia kuwa na vyanzo vya mapato asilimia 72. Kwa hiyo ina maana tunakwenda kupunguza utegemezi wa bajeti na mikopo ya nje na wahisani kwa asilimia tatu. Siyo kazi ndogo niwapongeze sana kwa ubunifu wa kuibua vyanzo vipya vya mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtakubalina na mimi na Waheshimiwa Wabunge ni kwamba kwa takribani miaka mitano iliyopita kuanzia 2014 mpaka 20219 Halmashauri zetu bado zimekuwa na changamoto ya kuweza kupata mapato ya kutosha. Kwa hiyo tumekuwa tukiipa Serikali Kuu mzigo mkubwa kwenye Halmashauri zetu. Tumeona kwamba kwa takriban kuanzia mwaka 2014 mpaka 2019 zaidi ya asilimia 85 ya Halmashauri zilishindwa kujigharamia matumizi yake ya kawaida. Hivyo zilipelekea kwamba Serikali Kuu iendelee kuzisaidia hizi Halmashauri. Kwa hiyo, utaona kwamba bado Serikali Kuu ina mzigo mkubwa ambao ni lazima kama Taifa tuje na mbinu mbadala za kuendelea kutafuta vyanzo vya mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe kuishauri Serikali, niliona katika Mpango wa Pili wa Serikali mliongelea Hati Fungani za Manispaa (Municipal Bonds) lakini pia niliona katika bajeti ya mwaka 2018/2019 Mheshimiwa Waziri wa Fedha kipindi hicho ni Makamu Rais sasa, alisisitiza kuendeleza Mpango ule wa kuanzishwa kwa Hati Fungani za Manispaa, ilielezwa Bunge lako Tukufu kwamba mmekwenda kufanyia training karibia Manispaa ya Mwanza, Arusha na nyinginezo na Tanga. Sasa, naona hili jambo pia limekuwa kama linasinzia. Hii nchi ni kubwa lazima tubuni halmashauri hizi zijiendeshe kibiashara. Tukisema halmashauri zote nchini ziweze kujiendesha kwa kutegemea Serikali Kuu tutakuwa tunajidanganya. Kwa hiyo niiombe sana Serikali iweke mkazo kwenye kuhakikisha wanamalizia uanzishwaji wa hizi Hati Fungani za Manispaa au Municipal Bonds.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana, kwenye bajeti tukatoe kipaumbele kwenye miradi ambayo itakwenda kuchochea uchumi kwa haraka. Leo hii tuna mradi mkubwa unakwenda kuanza wa Liganga na Mchuchuma lakini kama Serikali imeandaa mazingira ambayo yatakuwa wezeshi kwa mradi huu kutopatikana kwa vikwazo. Barabara zipo, miundombinu rafiki kwa ajili ya mradi huu ipo? Ni vitu ambavyo kama Serikali lazima tuhakikishe tunatoa vipaumbele kwenda kutekeleza bajeti yetu kwenye vyanzo ambavyo vitakwenda kuchochea uchumi wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii ukienda kule kwenye barabara za huko vijijini utaona jinsi kuna uwekezaji mkubwa kwa mfano, kuna uwekezaji mkubwa ulifanywa na Serikali ya Awamu ya Tatu kule kwetu Madibila, Mbarali. Waliwekeza zaidi ya bilioni 28 lakini leo hii hata barabara kufika kwenye yale mashamba hakuna. Ni jinsi gani Serikali inapoteza mapato kule kwa kukosekana tu barabara ile barabara ipo tangu Serikali ya Awamu ya Tatu imeahidiwa kwa wananchi kilomita 151 kutoka Rujewa, Madibila mpaka Mafinga kule kuna wakulima wa mbao, kuna uwekezaji mkubwa Serikali imetengeneza skimu za umwagiliaji kubwa lakini hakuna barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana Serikali, leo hii lango kubwa la biashara kwenye nchi za Southern Africa, Kusini mwa Afrika, (SADC) leo hii lango kubwa la biashara ni kule, barabara ile haifai kutoka pale Igawa mpaka Tunduma ni shida. Kwa hiyo, ni lazima kama Serikali tutoe vipaumbele kwenye maeneo ambayo yataweza kuchochea uchumi wa Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze TAMISEMI kwa kuwashirikisha Waheshimiwa Wabunge katika miradi mbalimbali inayoendelea. Niombe sana na Wizara nyingine zifanye hivyo kama Wizara ya Ujenzi wakae na Waheshimiwa Wabunge, Wabunge hawa wanajua barabara ambazo zitakwenda kuchochea uchumi kwenye Majimbo yao. Kwa hiyo niwaombe sana na Wizara nyingine muwape kipaumbele Waheshimiwa Wabunge wa Majimbo yao ili waweze kujadiliana nanyi na kuwapa kipaumbele ambacho kitasaidia kujua ni nini kipaumbele cha vitu ambavyo vitachochea uchumi katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ninashukuru sana kwa kupata fursa, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kupata fursa. Nami nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, management yote ya Wizara na taasisi zake kwa kazi nzuri ambazo wanaendelea kufanya katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nita-base kwenye vitu viwili kuishauri na kutoa maoni yangu kwenye Wizara hii. Kwanza ni Chuo chetu cha Utumishi wa Umma na vile vile mafunzo kwa Watumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaona kuna upokwaji mkubwa wa taasisi hii kufanya majukumu yake, kwa sababu chuo hiki kilianzishwa kwa ajili ya kuwafunda watumishi wa umma, lakini sasahivi tumekuwa na utaratibu wa kawaida kabisa kwa mtumishi kuingia ofisi ya umma pasipo kupitia kwenye chuo hiki, na ndiyo maana tunayaona haya ambayo yako kwenye mitandao. Utaona si dhambi sasahivi kuona document ya Serikali ambayo imendikwa siri kwenye Instagram, tunaona kabisa unaingia kwenye ofisi ya umma mtu amevaa kama anaenda disco, ni kawaida kabisa kwa sababu wameacha kukitumia ipasavyo Chuo cha Utumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo zamani ilikuwa kwamba, ili mtumishi yeyote aanze kazi ni lazima apite kwenye chuo hiki kufanyiwa induction program. Kwenye induction program utaelezwa mipaka yako kwa nafasi yako, bosi wako umuheshimu vipi, mipaka yako inaishia wapi. Sasahivi ugomvi mwingi ulio kwenye taasisi mbalimbali ni kwa sababu watu hawapikwi kwenye chuo hiki. Mtu anaona jambo hili napaswa kufanya mimi pasipo kufanya huyu. Kwa hiyo mgongano ni mkubwa. Ni lazima Wizara ikipe msisitizo chuo hiki kuwafunda watumishi wa umma, la sivyo vitu vya kwenye mitandao na tabia za ajabuajabu za kwenye utumishi wa umma hazitakoma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii kwenye hili suala la training tunaona TAMISEMI wanaajiri, wanapeleka watumishi wao Chuo cha Hombolo. Chuo cha Kodi wakiajiri wanapeleka watumishi wao chuo chao cha kodi. Wakiajiri bandari wana chuo chao cha bandari, kila taasisi zina vyuo vyao, lakini kule wakienda ukiangalia program wanazozisoma si za utumishi wa umma, wanasoma program za kama job description zao. Mfano kama bandari utakusanyaje kodi, utafanya hivi, Hombolo vilevile wanafanya hivyo. Sasa utumishi wa umma haupati fursa ya kuwafunda wale watumishi wa-behave vipi kwenye nafazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe coordination ndani ya Serikali. Hawa watumishi wanavyowekwa kwenye hivi vyuo; kama wakiwa Hombolo mfanye coordination mchukue chuo hiki kina wataalam wengi waende wakawape training ya utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu mafunzo kwa watumishi. Ni mashahidi humu ndani ili gari hata liwe zuri ni lazima ufanye service. Unakuta mtumishi wa umma anakaa five years, haendi hata kwenye mafunzo, Kwa sasa mambo yanakwenda yanabadilika, technology zinabadilika. Ni lazima mafunzo nyawe si hiyari yawe ni lazima na wawepo na program maalum, kila baada ya muda fulani watumishi wawe wanaenda kwa kupokezana kupata mafunzo mafupi ili kuwajengea uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo tutapunguza matatizo mengi ambayo yanawakumba watumishi wa umma na utumishi; lakini vilevile Mheshimiwa Waziri ni lazima uwe na wivu na utumishi. Utumishi wowote ndani ya nchi hii uko chini yako. Wewe ndiye unayeteuwa kwenye idara nyingine, Wizara nyingine; kwa hiyo ni lazima kuhakikisha kuna coordination ya kutosha. Hata kama TAMISEMI wanaajiri, lakini wale waishaajiriwa ni watumishi wa umma, lazima wafanye kazi kwa kufuata misingi ya utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru kwa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Pili nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii pamoja na timu yake yote kwa kazi nzuri wanazofanya katika sekta hii muhimu kwa maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, kwanza ni muhimu Mheshimiwa Waziri atambue kwamba jeshi letu la askari wa wanyama pori linahitaji kufanyiwa tathmini ya kina ili lifanye kazi kwa weledi mkubwa na kufuata misingi ya sheria.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto za wananchi kuingia hifadhini, lakini baadhi ya askari hawa wamekuwa wakiua watu, wakijeruhi watu na wakipora mifugo ya watu kiholela. Kwa kweli mwananchi anayeishi karibu na hifadhi mimi naamini ndio wahifadhi wa kwanza kama mahusiano yatakuwa mazuri. Kwa sasa wananchi ni bora akutane na chui au simba ataweza kujiokoa kuliko kukutana na askari wa wanyamapori.

Mheshimiwa Spika, inasikitisha sana, jeshi hili kwa jinsi linavyokiuka utawala wa sheria na kunyanyasa sana wananchi. Haikubaliki na haipendezi.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni wanyama kuvamia makazi ya watu hususani tembo. Hili tatizo linaendelea kukua kwa kasi sana na wanyama hawa wakivamia maeneo ya wananchi wanasababisha uharibifu mkubwa wa mazao, lakini wazee na watoto wanapoteza maisha na fidia kwa matukio haya kwanza hayaendani na hali iliyopo ya uhalisia kwa sasa, lakini pia hayatolewi kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, ni muhimu Wizara hii iweke mkakati madhubuti kuweza kushughulikia matatizo makubwa wanayokumbana nayo wananchi waishio pembezoni mwa hifadhi hizi, wananchi hawakupenda kuzaliwa wala kuishi pembezoni mwa hifadhi, ila wamejikuta wamezaliwa karibu na hifadhi. Tunaomba muwasaidie, Mheshimiwa Waziri Mchengerwa nakuamini. rekebisha hii sekta, okoa wananchi walioteseka kwa muda mrefu, angalia kwa jicho la ziada jeshi hili, wananchi wa maeneo haya mioyo yao inavuja damu kwa mateso makali, rudisha mshikamano na umoja wa jeshi hili na wananchi. Nashauri watumie nguvu hizo kupambana na majangiri na sio wananchi ambao makosa yao yanarekebishika.

Mheshimiwa Spika, nashukuru na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kupata fursa. Nami niungane na kaka yangu Mwita Waitara kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais. Tunaona nia ya dhati kabisa ya Mheshimiwa Rais wetu kuhakikisha kwamba anamaliza suala la migogoro ya ardhi ndani ya Taifa hili. Nia hiyo tunaona tafsiri nzuri kabisa ya Mheshimiwa Rais, hataki migogoro ya ardhi ndani ya Taifa, lakini tatizo linakuja kwa wasaidizi wake huku chini kwenye tafsiri ya nia njema ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tarehe 18 mwezi wa kwanza, Mheshimiwa Waziri Mkuu alifika pale Mbarali. Alifika pale Kapunga, Mbarali na Mheshimiwa Waziri alikuwepo Mama yangu Dkt. Angeline Mabula. Aliona kiu ya Wanambarali kutaka kujua hatma ya mgogoro huu. Wanambarali walijitokeza kwa wingi pamoja na shughuli za shamba hawakwenda ili wasikilize Mheshimiwa Waziri Mkuu anasema nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu alituambia kati ya migogoro ya vijiji 34 ambavyo tumedumu navyo Mbarali kwa miaka 15, vijiji 29 vitarudi kwa wananchi na vijiji vitano vitabaki kwenye hifadhi. Sasa kinachoendelea kule Mbarali tunaona watu wa TANAPA wanaendelea kuweka beacon kila mahali. Hata vile vijiji ambavyo Mheshimiwa Waziri Mkuu alitamka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Mama yangu Mheshimiwa Angeline, kesho anavyokuja kufanya majumuisho hapa, tunachotaka sisi Wanambarali na Wanambarali wamesema kesho watakuwa kwenye TV watashika kalamu na karatasi wajue kijiji kwa kijiji, vipi vijiji hivyo 29 ambavyo vinabaki kwa wananchi na vijiji vitano vipi ambavyo vitabaki hifadhini? Kesho tutamsikiliza mama yangu, la sivyo kesho, nitaondoka na shilingi ya Mama yangu mpendwa, asipotutajia vijiji hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo ni salamu za Wanambarali, kesho tunamsubiri mama yangu Mheshimiwa Waziri hapo, atuambie kwa majina kijiji kwa kijiji na vinavyoondoka ni vipi na vinavyobaki ni vipi?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa inatoka wapi? Mheshimiwa.

TAARIFA

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Anachokizungumza Mheshimiwa Bahati ni sahihi kabisa. Licha ya nia njema ya Serikali ya kutatua mgogoro ambao uko Mbarali, kumekuwa na changamoto ya uwekaji beacon kiholela kwenye maeneo ambayo wananchi wanafahamu kabisa Serikali iliwazuia. Kwa hiyo ni vyema Serikali ikaenda kuangalia, kinachozungumzwa hapa Bungeni na kinachofanyika nje, ni vitu viwili tofauti. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Bahati unaipokea hiyo taarifa?

MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili kaka yangu Festo naye ni muhanga kwa sababu Mbarali na Makete ni watu wale wale wanaingiliana. Kwa hiyo anaijua vizuri hii historia ya kule Mbarali. Namshukuru sana my brother. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, inasikitisha sana kuona kwamba mpaka sasa hivi 25% tu ya ardhi ya Tanzania ndiyo imepimwa. Hii migogoro tunayoimba kila siku humu Bungeni ni kwa sababu tunaenda pole pole sana kwenye kupima ardhi ya Taifa hili. Hivi kwa mfano, kweli tangu tumepata uhuru, leo hii tumepima 25% tu ya ardhi, tunahitaji miaka 180 kumaliza kupima nchi hii, kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo sawa, teknolojia zimekua. Ujuzi wetu umeongezeka, kwa nini hawapimi ardhi? Watu wanashindwa kuendelea, leo hama hapa, ondoka hapa, yaani fujo tu, kwa sababu hawapimi ardhi. Wapime ardhi ya Taifa hili tuondokane na migogoro ya kila kukicha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wanawekeza watu hapa, walime, kesho ondokeni hapa nenda hapa, wamekaa miaka 70, wamezika babu, vijukuu, kesho ondokeni hapa, tunakuwaje hivyo? Why? Kwa nini hatupimi ardhi yetu na wanaangalia kabisa taarifa za Mtakwimu wa Serikali. Sasa hivi…

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa.

TAARIFA

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nataka nimpe taarifa dada yangu Bahati kwamba anachosema ni kwamba itatuchukua muda mrefu kupima ardhi. Leo mpango wa matumizi bora ya ardhi kwenye vijiji vyetu, mfano, Wilaya ya Ikungi, katika vijiji vilivyopo 101, it’s only vijiji vitano tu ndiyo vina mpango wa matumizi bora ya ardhi. Kwa hiyo tusitegemee kwamba bila kupima tutamaliza migogoro. Kwa hiyo migogoro itaendelea, dawa ni kupima ardhi ya nchi hii. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Bahati unaipokea hiyo taarifa?

MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nazipokea taarifa zote, ni kweli kabisa hatuko serious kwenye upimaji wa ardhi ya Taifa letu na hatuwezi kumaliza migogoro ya Taifa hili kama hatupimi ardhi. Kwanza tunawarudisha watu nyuma kimaendeleo kila siku, leo watu wanalima hapa, kesho ondoka hapa nenda hapa, hatuwezi kuendelea kama Taifa. (Makofi)

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Bahati kuna taarifa.

TAARIFA

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba ule mradi ambao Mheshimiwa Waziri ameuzungumza hapa ndiyo una lengo la kwenda kutayarisha miundombinu ya teknolojia bora ya upimaji ili tukimaliza kuutekeleza ule mradi, sasa itakuwa ni rahisi kwa kuweka miundombinu bora ya upimaji na tutakwenda kwa haraka zaidi katika upimaji, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Bahati unaipokea hiyo taarifa?

MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei hiyo taarifa, yaani kweli leo hii ukaende kupima vitu vya hivyo? Hapana, siipokei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni lazima Wizara iwe serious na tuone kwenye mikakati yao wako serious kupima ardhi ya Taifa hili. Hivi wenzenu kila siku ni migogoro, kila siku ni migogoro. Mama yangu atakwenda kule, wapime ardhi, matatizo yote haya yatakuwa hamna. Kwa kweli tunaomba wapime ardhi ya nchi hii. Mipango yao hiyo haionyeshi kama kuna uthabiti kabisa na wana malengo la kweli la kutaka kupima ardhi ya nchi hii. Kwa kweli mama yangu Mheshimiwa Waziri ili na apumue, wapime ardhi ya nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kupata fursa. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana nami kwa kunipatia fursa ya kutoa mchango wangu. Nianze kwanza kwa kuwapongeza sana mtangulizi wa Wizara hii, Mzee wangu, Mheshimiwa Lukuvi alifanya kazi kubwa, lakini nampongeza Mheshimiwa Waziri, Mama yangu Angelina Mabula na Naibu wake Ridhiwani, mnafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri ambazo zinafanyika ndani ya Wizara hii, baadhi ya mambo yanatia dosari, hata ule uzuri wa mambo makubwa ambayo yamefanyika unakuwa hauleti ladha. Jambo hilo ni migogoro ya ardhi. Kila maeneo ndani ya Taifa hili huwezi kukosa migogoro sugu ya ardhi. Pamoja na kwamba kamati zinaundwa, lakini huwa migogoro ya ardhi ndani ya Taifa hili inachukua muda mrefu na hakuna suluhu, wala huoni kama kuna mwaka wa kuleta suluhu kwenye migogoro hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano. Nichukue mfano wa mgogoro mmoja ambao nadhani ni mgogoro kongwe ndani ya Taifa hili ni GN 28 ya kule kwetu Mbarali. Huu mgogoro tangu mimi niko binti, sasa hivi naelekea utu uzima, mgogoro huu bado na hatuelewi hata nini hatima yake. Kwa masikitiko makubwa zaidi, hii Kamati ya Waheshimiwa Mawaziri nane, imefika Mbeya mara mbili na wananchi walikuwa wanaisubiri kwa hamu mno wakijua kwamba sasa ile neema iliyotangazwa na Mheshimiwa Rais kujua ni vijiji gani vitarasimishwa virudi kwa wananchi au vibaki kwenye hifadhi vitatajwa, Mbeya kamati hii imekuja mara mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara ya kwanza walipofika waliishia Mbeya Mjini, wakasema tutarudi tena. Wamefika mara ya pili mwezi uliopita, hakuna majibu. Wamesema sasa hivi tunauachia mkoa, watakuja kupitia upya. Kwa kweli inatia uchungu. Leo hii ukifika kule nyumbani kwetu Mbarali, muulize hata mtoto wa miaka mitano, akutajie matatizo matatu ya wilaya hii, atakwambia la kwanza ardhi, lapili ardhi, la tatu ardhi, atasahau hata shida za maji wala barabara. Ni kwa sababu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mgogoro huu tumepoteza ndugu zetu. Wanawake wamepoteza waume zao, watoto wamepoteza baba zao kupitia mgogoro huu, watu wanapoteza maisha. Siku moja alikuja Mbunge wa Jimbo letu la Mbarali, Mzee Mtega, alileta Taarifa Binafsi humu ndani, Waheshimiwa Wabunge walitokwa na machozi jinsi unyama unavyofanyika kisa mgogoro huu. Inasikitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro wa takribani miaka 15, kila siku wananchi hawajui hatima yao. Halafu wananchi wa Mbarali siyo mara yao ya kwanza kuhamishwa. Walihamishwa; vijiji 10 vilishahamishwa na watu hawapo maeneo hayo waovu, lakini sasa hivi ngoja nikutajie; maeneo kwa mfano, Msangaji, Upagama, Ukwaheri, Idunda, Ikoga, Kapunga, huku kote watu walishaondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafiti zilizoonyeshwa, ni kwamba wakibaki watu maeneo haya wataathiri Mto Ruaha, na maeneo hayo hakuna watu, sehemu kubwa watu waliondoka. Baada ya watu kuondoka maeneo hayo, walikubaliana kati ya mamlaka zilizokuwepo na wananchi. Hawa watu waliondoka bila mtutu, wakaambiwa na wakaelewa. Baadaye wakakubaliana mipaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limekuja kutoka tangazo la GN 28, wamekuja hata lile eneo ambalo hawa wananchi walihamishiwa Luhanga na kwenyewe kukaonekana tena kuko ndani ya hifadhi; vijiji 33 vingine vipo ndani ya hifadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sisi wana-Mbarali hatima yetu ni nini? Kwa kweli tunaumia. Kila siku tunapata misiba. Kweli Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi ishindwe kufanya maamuzi kwenye jambo hilo ambalo linatesa watu hivi! Siyo sawa. Wamekuja Waheshimiwa Wabunge mbalimbali humu ndani, kila siku GN 28, kila siku linaongelewa na taarifa zinaletwa, lakini hakuna. Yaani tunachukulia rahisi tu. Siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekit, tunaamini kabisa viongozi wetu wa juu ambao ni Waheshimiwa Marais huwa wanakuwa ndiyo wamiliki wa ardhi kwa niaba ya wananchi, na kwenye hili tayari kuna matamko mbalimbali ya viongozi wetu ambayo yametolewa kwa kuwaambia; ngoja nianze kwanza kunukuu. Februari, 2015 aliyekuwa Waziri wa Maliasili, Mheshimiwa Lazaro Nyalandu alifika Mbarali, alitumwa na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, alisema haya yafuatayo, nakukuu: “Mheshimiwa Rais wetu ameridhia, baada ya wananchi wa kata hizo zilizoondolewa, hakuna mwananchi yeyote atakayeondolewa katika vijiji vilivyobakia.” Kwa hiyo, wananchi endeleeni na shughuli zenu za maendeleo, akaendelea: “ninaagiza viongozi wa Mkoa wa Mbeya, Njombe na Iringa muanze kuchukua hatua za haraka za kurekebisha tangazo hilo lililoleta mabadiliko ya mipaka ya eneo hili kwa ajili ya kupeleka Bungeni, kwa ajili ya kubadili sheria hiyo.” Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 4 mpaka tarehe 6 mwezi wa Kumi 2018 Hayati Rais wa Awamu ya Tano aliagiza Makatibu 11 waende Mbarali wakiongozwa na Katibu Mkuu aliopo Ofisi ya Waziri Mkuu, Mambo ya Sera na Uratibu Prof. Faustine Kazomola, huyu ndio alikuwa kiongozi wa kamati hiyo, walikaa Mbarali kwa siku hizo tatu; tarehe 4 mpaka tarehe 6 kushughulikia suala hilo. Baada ya hapo, Januari, 2019 tarehe 15, naomba ninukuu maneno ya Mheshimiwa Rais Hayati Dkt. Magufuli ambaye ndio alikuwa guarantor wa land hii hapa, alisema: “Vijiji vyote vilivyobainishwa viko ndani ya hifadhi, visiondolewe. Ninaagiza mamlaka husika zianze kufanya mchakato wa kuvirasimisha vijiji hivyo. Natoa mwezi mmoja mchakato wa kuanza mabadiliko ya sheria ili yapelekwe Bungeni.” Tarehe hiyo hiyo ndiyo aliyoteua kamati ya kwanza ya Mawaziri nane kushughulikia migogoro hii na migogoro mingine ambayo haijapatta ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekit, sisi tulitarajia baada ya kauli ya Mheshimiwa Rais hii, kazi ya kwanza ya Kamati pamoja na migogoro mingine ambayo ipo maeneo mengine, kazi ya Kamati kwa Mbarali ilishatolewa maelekezo na maeneo ambayo ni hatarishi watu walishaondoka. Kuna shida gani Mbarali? Kuna shida gani Mbarali? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kupata fursa nami nianze kwa kuipongeza sana Serikali inayoongozwa na Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaendelea kufanya. Niungane na Waheshimiwa Wabunge kuipongeza sana Wizara ya Fedha kwa kazi nzuri mnayoifanya kwa bajeti nzuri ambayo mmeileta Bungeni, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni dhahiri bajeti hii kama ikitekelezwa kwa ufanisi walau hata kwa asilimia 50, kwa ufasaha, nina uhakikia uhakika kabisa tutapiga hatua kama Taifa. Leo hii mchango wangu niuelekeze kwenye Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika na Waheshimiwa Wabunge, tumekuwa mashuhuda humu ndani na ripoti ambazo zimekuwa zikitolewa na Mdhibiti wa Hesabu. Ripoti zile zinakuwa na upotevu mkubwa sana wa fedha. Laiti kama tungeweza kuwekeza nguvu kubwa kwa huyu Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali kumtengenezea miundombinu rafiki ya ufanyaji kazi wake, ninaamini kabisa tungeweza kuokoa fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi sio mwanasheria, lakini nimejaribu kupitia na kusoma, nimeenda kwenye Katiba yetu ya mwaka 1977 na marekebisho yake, Ibara ile ya 143 imemtaja Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali na imeainisha pale majukumu makubwa matatu. Jukumu la kwanza; ni kudhibiti fedha zote zitakazotoka kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali, lakini jukumu la pili alilopewa mdhibiti huyu ni kuhakikisha matumizi yote ya kwenye mfuko huo wa Serikali yamepitishwa na Sheria ya Bunge. Kazi yake ya tatu, ni kufanya ukaguzi walau mara moja kwa mwaka na kutoa ripoti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napata shida kidogo nikija kwenye Sheria ya Ukaguzi wa Umma. Sheria yenyewe inaitwa Public Audit Act, ile Sura ya 418. Sasa sheria hii ambayo ndiyo inaanzisha Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali, imeshaondoa neno “mdhibiti”; pale ni ku-audit. Nikisoma hiyo sheria hiyo, nimejaribu kusoma, kwa uelewa wangu, sijaona muundo wala uongozaji wowote wa mdhibiti huyo anafanyaje udhibiti wa hesabu. Nilichokiona hapa kwenye sheria hii, ni namna gani atakagua; kwa hiyo, nimeona muundo na utendaji kazi wake katika kukagua peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali anatembelea mguu mmoja wa auditing peke yake, lakini udhibiti sheria hii hatujaweza kuitafsiri vizuri Katiba inavyotaka. Ndivyo nilivyoona mimi kwamba sheria hii imetufanya tusiitafsiri vizuri Katiba, hivyo tumeelekeza majukumu yote ya Mdhibiti na Mkaguzi wa Hesabu za Serikali katika ku-audit lakini kwenye ku-control hatujaweza kulifanya hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine, kwa mfano kwenye ripoti ya ukaguzi, hii ya 2020/2021 CAG anahoji kuwepo kwa Halmashauri 19 ambazo zilipokea shilingi bilioni 47.19 za miradi ya maendeleo zaidi ya bajeti iliyopangwa. Sasa kama huyu ndio controller, ame- control vipi? Kama huyu controller naye anahoji kuzidisha na kuweka matumizi nje ya bajeti, kwa hiyo, tunaona kabisa suala la udhibiti kwa huyu Mkaguzi na Mdhibiti, bado suala la udhibiti hatujalipa nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba nishauri mambo mawili tu kwa Serikali kwenye suala hili. Kwanza, Serikali iangalie uwezekano wa kutenganisha hizi nafasi mbili; ukaguzi na udhibiti; nasi tutakuwa siyo nchi ya kwanza kufanya hivyo. Nchi nyingi tayari zimeshaondoka huko, hata majirani zetu hapo Kenya. Ukishasema kwamba mdhibiti huyo huyo asaini fedha zitoke, huyo huyo akajikague, ufanisi hautakuwa vile kama ulivyo. Kwa hiyo, nilikuwa nashauri tuone uwezekano wa kutenganisha kazi hizi mbili kuleta ufanisi na kupunguza na kutokomeza kabisa upotevu wa mali za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naiomba Serikali ili tuweze kudhibiti mali za umma, waje na miongozo iletwe Bungeni Sheria ya udhibiti ili tumwelekeze huyu atadhibiti vipi na atafanyaje kazi za udhibiti na ripoti zake zitakuwa zinaletwa vipi? Kuliko kusoma tu ripoti za ukaguzi wakati udhibiti tumeuacha pembeni. Kwa hiyo, naomba haya yazingatiwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tatu, hii nchi ni kubwa, lakini nchi yote hii kila Halmashauri inategemea Mfuko Mkuu wa Serikali. Tumeshauri hapa, tunaomba Wizara ya Fedha shirikianeni na TAMISEMI, wekeni mkazo kwenye hati fungani za Serikali za Mitaa. Serikali za Mitaa zianze sasa utaratibu wa kufanya miradi yao kibiashara, watu wanunue hisa zao watengeneze miradi. Hii ya kusema kila Halmashauri kutegemea Serikali Kuu, tunajichelewesha, kwa sababu hatuwezi kama Taifa kila Halmashauri kuitimizia mambo yake. Hatuwezi!

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana mjitahidi, msisitize uwazishwaji wa hizi hati fungani, ukamilike ili Halmashauri zetu ziweze kujiendesha kibiashara. Kwanza kwa kufanya hivyo, mtaweza kusaidia Halmashauri hizi, watu wawe wamiliki wa miradi ile, lakini vile vile watakuwa wanapata fedha kwa riba ndogo. Maana yake ni tofauti na kukopa fedha kwenye benki. Hati fungani zina riba ndogo. Kwa hiyo, mhakikishe hizi Halmashauri zinaweza kujifanyia miradi ya maendeleo na ikabuni miradi mikubwa ambayo baadaye itakuwa ndiyo vitega uchumi vya Halmashauri zetu kuliko Halmashauri zote kutegemea Serikali Kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru, na ninaunga mkono hoja. (Makofi)