Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Suma Ikenda Fyandomo (13 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi uliyonipatia ya kuweza kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais. Awali ya yote nipende kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye amenijaalia uzima na afya njema hatimaye nimekuwa mmoja wa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuwashukuru sana wanawake wa Mkoa wa Mbeya kwa namna ambavyo wamenipatia kura nyingi ambazo zilisababisha jina langu kupelekwa kwenye Kamati Kuu Taifa. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu ambaye ndiyo Mwenyekiti wetu wa Chama Cha Mapinduzi Taifa. Namshukuru yeye pamoja na Kamati Kuu kwa kupendekeza jina langu nami nimekuwa Mbunge sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nikupongeze wewe kwa kuwa Mbunge wa Mbeya Mjini. Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson Mwansasu hongera sana kwa kuwa Mbunge wa Mbeya Mjini na Mbeya Mjini sasa imetulia kama lilivyo jina lako. Napenda vile vile kuwashukuru sana wananchi wa Mbeya Jiji na wananchi wa Mkoa wa Mbeya wote kwa ujumla kwa namna ambavyo waliweza kukichagua Chama Cha Mapinduzi kwa kura nyingi za heshima. Napenda kuwashukuru Watanzania wote kwa ujumla. Tanzania yetu sasa inapendeza, imekuwa ni ya kijani na ina amani ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi kubwa nzuri anazozifanya ambapo Tanzania yetu sasa inatambulika dunia nzima na inaheshimika dunia nzima kwa namna anavyoleta maendeleo kwenye nchi yetu. Nawapongeza sana Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri kwa nafasi zao hizo. Natambua ni watu makini na ni mahiri sana watazitendea haki kwa maana ya kuisaidia Serikali ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wanawake wa Mkoa wa Mbeya katika kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais, namshukuru sana Mheshimiwa Rais alisema kwamba kwenye hotuba ile atavipa vipaumbele sana vikundi tofauti tofauti kwenye mikopo kwa maana ya kwamba viendelee kusonga mbele. Naomba sana Mheshimiwa Rais kwa hotuba hii awape kipaumbele wanawake wa Mkoa wa Mbeya na Tanzania yote kwa ujumla, maana akiwezeshwa mwanamke, mwanamke ndiyo kila kitu, mwanamke ndiyo mama ambaye anajali familia, anasaidia Watoto, anamjali hata baba pia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuomba asilimia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kengele imenikatili, lakini nitaandika kwa sababu napenda sana kuongelea habari za wanawake namna gani waweze kusaidiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikupongeze wewe kwa kazi nzuri na namna ambavyo unaliongoza Bunge hili Tukufu. Pia nimpongeze Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa vile ambavyo anasimamia Kanuni hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano chini ya uongozi imara wa Mheshimiwa wetu, Dkt. John Pombe Magufuli kwa namna ambavyo ameweza kufanikiwa kuingia katika uchumi wa kati kabla ya kipindi kilichokuwa kimetazamiwa. Kwa namna ambavyo tumeweza kuingia kwenye uchumi wa kati Benki ya Dunia wameshangazwa na kasi ya Mheshimiwa Rais wetu, Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, naomba kuishauri Serikali iendelee kuweka mkazo kwenye Halmashauri zetu ili ziweze kuwekewa fedha za kutolewa kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ili wawe kuendesha maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufanikiwa zaidi kwa namna ya kuendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais kwenye uchumi wetu wa kati, ili kasi iendelee kuhusiana na namna ya kutoza kodi kwa wafanyabiashara, naomba elimu kwa upande wa wafanyabiashara imekuwa ni ndogo. Kipindi cha nyuma mfanyabiashara anapokuwa anafanya biashara mfanyakazi wa TRA alikuwa ni rafiki wa mfanyabiashara lakini sasa hivi hali imekuwa siyo, wafanyabiashara wamekuwa wakilalamika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo napenda kuishauri Serikali kuanzia elimu ya msingi, sekondari na vyuo ikiwezekana kuwe na elimu kuhusu kodi kwa maana Mtanzania yeyote pindi anamaliza chuo asijute kwamba anaonewa namna ya kutoa kodi aone ni uzalendo kutoa kodi kwa maana ya kuendesha nchi yetu. Maana nchi inaendeshwa kwa kulipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa Watanzania wanaelewa vizuri sana kazi ambayo ameifanya Mheshimiwa Rais wetu ya kuijenga nchi yetu ya Tanzania. Mheshimiwa Rais wetu baada ya kuchaguliwa 2015 ndani ya siku mia moja alipongezwa kwelikweli hata wananchi mbalimbali wengine walisema Mheshimiwa Rais akae miaka 100, wengine walisema miaka 40, kila mtu aliongea la kwake kwa namna ambavyo amekuwa akiendesha nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kusema kwamba Mheshimiwa Rais ameweka nidhamu Serikali lakini ameweka nidhamu mpaka kwenye ndoa za Watanzania. Naongea hivyo kipindi cha nyuma watu walikuwa wakilalamika sana baba anarudi nyumbani usiku wa manane, mama anarudi nyumbani muda atakao akilalamika kwamba kuna foleni kubwa. Baada ya kuingia Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kama Rais, baba na mama wanawahi nyumbani kupanga mipango ya maendeleo ya familia zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na hayo miaka ya nyuma mara nyingi sana tulikuwa tukiwashuhudia hawa watu wa Kilimanjaro ikifika Disemba wanarudi nyumbani kwao, kwetu haikuwa hivyo. Hata hivyo, baada ya kuingia Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli sasa hivi wazazi wanafurahia watoto wao, watoto wao walikuwa hawaonekani mikoani mwingine anakuwa hajaenda hata miaka mitano, mitatu mpaka kumi lakini sasa hivi ikifika Disemba magari yanapishana huko mikoani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana sana Watanzania tumuelewe Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Watu wanasema pesa haziko mifukoni lakini maendeleo yamekuwa ni makubwa, ukipita mitaani huko barabarani unaona jinsi wananchi wanavyojenga nyumba tena wanaezeka mabati ya m-South au tunapenda kuita mabati ya rangi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tuendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa kazi nzuri anazoifanya. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema ambaye amenipa afya njema na kuweza kusimama kwenye hili Bunge Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wa Fedha pamoja na viongozi wote wa Wizara kwa namna ambavyo wameiongoza na kusimamia bajeti hii ya Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu ambaye ni mwanamke wa kwanza kuwa Rais katika Taifa letu hili la Tanzania. Mheshimiwa Rais wetu ni mama msikivu, mwenye busara, ana hekima, ni mama ambaye anastahili sifa zote. Napenda kuwashukuru Watanzania wote kwamba wamemkubali sana mama tangu pale ambapo ameapishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuchangia bajeti hii na kuipongeza sana vile ambavyo imeandaliwa hasa kwenye kipengele cha vijana wetu wa bodaboda. Naipongeza sana kwani wameondola mzigo mkubwa sana maana faini ya shilingi 30,000/= ilikuwa ni kubwa sana. Pamoja na kuipongeza kwa kazi nzuri hii waliyoifanya, napenda sana kuishauri pia Serikali, vijana ni nguvu kazi ya Taifa, tunawategemea sana na tunawapenda. Napongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwani ilifanya utaratibu wa kuondoa viroba ambavyo viliendelea kulinda uhai wa vijana wetu wa bodaboda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishauri Serikali kwa yafuatayo: kuhusu watu wa Usalama wa Barabarani, nilikuwa napenda kusimamia haya. Vijana wetu wa bodaboda kama nilivyoanza kwa kusema tunawapenda, hatutaki kuwapoteza. Naomba sana ufuatiliaji wa sheria na taratibu za kupita barabarani hizi bodaboda zetu. Bodaboda zilizo nyingi zinapita barabarani zikiwa hazina taa ya breki ya nyuma ambayo inaonesha kwamba ile ni bodaboda inapita. Pia usiku wakati fulani unapishana na bodaboda haina taa yoyote, ukizingatia zenyewe hazina sehemu ya kuweka reflector. Sasa hiyo ni hatari sana ambayo inaweza kupoteza uhai wa vijana wetu hawa wa bodaboda. (Makofi)

Mheshmiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba sana Jeshi la Usalama wa Barabarani kuwaita vijana wa bodaboda kuweka vikao na wao kuwaelimisha, kuwapa semina, namna ambavyo sheria za barabarani zinavyotakiwa kuwa. Naliongea hili maana kipindi cha kwanza bodaboda zilivyokuwa zinaanza, kulikuwa na utaratibu; wanakuja wilaya kwa wilaya, wanakalishwa vikao vijana wa bodaboda kuwapa elimu. Hapa katikati bodaboda zimeingia kwa wingi sana, sijawahi kuona semina inafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, naomba tuzijali sana afya za hawa watoto wetu. Hawa vijana hawavai sana helmet ambayo inazua kupasuka kwa kichwa endapo watapata ajali. Pia kuna kitu kinaitwa chest coat la kuziba kifua, havijazingatiwa kabisa. Vijana wengi wanaendesha bodaboda bila kukinga kifua. Sasa imeanza kuleta athari ambapo hofu yangu tutapoteza vijana wengi katika Taifa letu hili Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewashuhudia vijana wanne ambao waliathirika na mapafu. Wengine walifanyiwa upasuaji wakapona, lakini wawili walipoteza maisha. Sasa hapo ni hao nimefanikiwa kuwaona, ambao hatujawaona! Hili naliona ni tatizo kubwa sana ambalo tunatakiwa tuwasimamie vijana wetu wa Taifa hili la Tanzania. Pia napenda kuishauri Serikali, naipongeza kwamba wamepunguza hizo faini, lakini vituo vingi vya Polisi vina bodaboda nyingi sana. Nilikuwa naomba sana Serikali yetu hii ni sikivu, hao watu ambao bodaboda zao zimekamatwa wawaruhusu kwenda kufuata bodaboda zao ambazo hazina makosa ya jinai wakalipe faini ya hiyo hiyo shilingi 10,000/=. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, wakati fulani nilikuwa nimechangia kuhusu elimu kwa ajili ya mlipa kodi wa Tanzania. Naomba sana, narudia kusema, elimu ya mlipa kodi wa Tanzania ni muhimu sana. Naomba kwa mara nyingine, elimu itolewe kuanzia Shule za Msingi, Sekondari, Vyuo na Vyuo Vikuu ili vijana hawa wanapokua siku zinavyozidi kwenda, inakuwa inawajenga kwamba kulipa kodi ndiyo uendeshaji wa Taifa letu ya Tanzania. Hivyo napenda sana kuliombea hili lizingatiwe. Naomba sana hawa viongozi wa TRA kuweka mikutano na vikao na wafanyabiashara kuwapa elimu na semina ili wasione kwamba wanaonewa katika kulipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongee lifuatalo; kipindi cha Awamu ya Tano, naomba sana mpango na hali ile ya Awamu ya Tano iendelee hata hii Awamu ya Sita. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan. Sisi ni wanawake, naomba sana kasi ile ile iliyokuwa ya Awamu ya Tano iwe ni hiyo hiyo mpaka kipindi hiki cha Awamu ya Sita. Ofisi zote za Umma za Serikali zinaongozwa kwa kutumia Ilani ya Chama cha Mapinduzi na ofisi zote zinazo. Naomba Watumishi wa Umma tusilegelege, ile kasi na mori ya kufanya kazi kama ilivyokuwa Awamu ya Tano iwe hivyo hivyo na awamu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi baada ya Bunge la Bajeti hili kwisha narudi Mbeya, naomba ofisi vile ambavyo alikuwa akijituma akijihimu asubuhi kwenda kazini na iwe hivyo. Nitapita maofisini kuangalia kama mambo yanakwenda sawa. Naomba sana, vile ilivyokuwa, mtu kama hajafika ofisini kwa wakati, maana yake kipindi cha nyuma ilikuwa tukifika unasubiri, mtu anaambiwa bosi sasa hivi ametoka amekwenda breakfast. Unasubiri, ikifika saa 5.00 anasema hajarudi, basi nifanye kazi mbili tatu, unarudi saa 8.00, wanasema ooh, amekwenda lunch. Naomba hilo lisirudiwe tena . Vile ilivyokuwa Awamu ya Tano na iwe hivyo mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba sana; amani na upendo uliokuwepo Awamu ya Tano uendelee na sasa.

Maana tumesikia sasa vibaka wanaanza, wizi wizi unaanza. Tanzania inajengwa na sisi wenyewe Watanzania. Haya ninayoongea ninamaanisha. Nalipenda sana Taifa letu la Tanzania, nawapenda sana Watanzania wote na ninaomba amani. Utendaji kazi ndiyo iwe ngao yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Wizara hii ya Ujenzi. Ninamshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali cha kuweza kusimama kwenye Bunge lako tukufu ili nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi lakini pia ninampongeza sana Naibu Waziri kaka yangu Kasekenya kwa namna ambavyo amekuwa akijibu maswali hapa Bungeni, pia ninampongeza sana Mheshimiwa Mwakibete namna anavyojibu maswali hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuishukuru Serikali hii ya Mheshimiwa Rais ya Mama Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo imeenda kuuona uwanja wa ndege wa Mbeya. Tunaishukuru sana Serikali hii kwa sababu wameweza kuweka taa ambapo sasa ndege zinaweza kutua usiku kwenye Mkoa wetu wa Mbeya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana nieleweke vizuri, ninaombi moja uwanja ule wa Mkoa wa Mbeya uwanja wa ndege unaitwa Songwe International Airport nilikuwa ninaomba sana ule uwanja ubadilishwe...

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. SUMA I. FYANDOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ule uwanja jina libadilike na uitwe Mbeya International Airport kwa sababu mara nyingi...

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma kuna taarifa, taarifa Mheshimiwa Neema.

T A A R I F A

MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka nimpe taarifa dada yangu Mheshimiwa Suma Fyandomo Ikenda kwamba suala la uwanja wa Songwe siyo uwanja wa Mkoa wa Mbeya, na ni uwanja wa kanda ya Nyanda za Juu Kusini. Kwa hiyo, wanapotafakari na kusemea uwanja ule wakumbuke kwamba siyo wa kwao Mbeya, ni wa kwetu wote, ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma Fyandomo unapokea hiyo taarifa?

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo taarifa siipokei, ule uwanja ni uwanja wa Mkoa wa Mbeya uko ndani ya Mkoa wa Mbeya na hauko Mkoa wa Songwe, sasa hivi Songwe ni Mkoa.

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vile ambavyo mimi...

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma subiri kidogo.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: ...naweza nikajidanganya kwamba mabasi ya Shabiby ni yangu mimi, badala ya kuanza kutafuta mabasi ya kwangu ambayo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma kuna Taarifa kidogo.

T A A R I F A

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi naomba tu kumpa taarifa mzungumzaji kwamba ule uwanja siyo wa Mkoa wa Songwe, siyo wa Mkoa wa Mbeya ni uwanja wa kanda, kwa hiyo kuuita ule uwanja kwamba jina liwe Mkoa wa Mbeya ni ubinafsi. Nakushukuru. (Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachosikitika hapa hawa ndugu zangu wa Mkoa wa Songwe wanajichelewesha kwa sababu wanajidanganya, ule uwanja ninaomba uitwe Mbeya International.

MHE. CONDESTER M. SICHWALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taratibu, kama ni suala la uwanja naomba tumuachie Waziri atakapokuja atajibu kwa sababu limeshakuwa kubwa.

Mheshimiwa Suma endelea. (Makofi)

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana, taarifa zao nazidi kutokuzipokea na hata ukiangalia hapa wanaelezea kwamba uwanja ule ni wa Kanda, lakini wanaokanusha hili ni Wabunge wa Mkoa wa Songwe. Hivyo, ninasisitiza ninaomba Serikali ule uwanja uandikwe Mbeya International Airport. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mara nyingi tumekuwa na wageni…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Matiko.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unilindie muda wangu tafadhali maana nina mengi ya kuchangia, ahsante. (Makofi)

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa tu taarifa maana yake ulizuia lakini nikaona anaendelea kuchakata kwamba uwe wa Mkoa wa Mbeya. Sasa kuondoa hii mikanganyiko na mgawanyiko na kuleta utofauti kwenye hii mikoa nilikuwa napendekeza huu uwanja ufikiriwe hata kupewa jina la kiongozi ili usiwe na majina ya mkoa ili kuleta umoja. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma taarifa hiyo unaipokea?

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa inaweza ikanikuna kidogo ya Mheshimiwa Esther Matiko. Uwanja ule ninaomba kama mtafikiria kwamba muupatie jina la kiongozi maalum ninaomba basi uitwe Tulia International Airport. (Makofi/Kicheko)

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi wewe mbona unaongea sana?

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma subiri kidogo.

T A A R I F A

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, sipingani na hoja ya dada yangu Mheshimiwa Suma, lakini concept iliyopo kwenye uwanja wa Songwe ni umetolewa kama ambavyo Mkoa wa Kilimanjaro unaitwa kwa jina la Mlima Kilimanjaro, Mkoa wa Rukwa unaitwa kwa sababu ya Ziwa la Rukwa, Mkoa Ruvuma unaitwa kwa sababu ya Mto wa Ruvuma. Kwa hiyo, hata ule uwanja uliitwa kwa sababu kuna mto ambao unaitwa Songwe kama sehemu ya kutangaza kivutio. Kwa hiyo, hatumaanishi sisi Wabunge ambao tunatoka Mkoa wa Songwe tunataka uendelee uitwe kwa mkoa wetu. (Makofi)

MWENYEKITI: Umeeleweka, nimesema kwenye suala la jina la uwanja wa ndege hakuna tena taarifa. Tuendelee Mheshimiwa Suma.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana, ninaomba niseme hivi ninaongea haya kwa msisitizo, mimi binafsi nina wageni wangu walikuwa wanatoka Ulaya kuja kunitembelea, walibaki wanahangaika angani maana walikuwa hawaoni jina la Mbeya International Airport wanaona Songwe hawajui … (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba…

MHE. AHMED M. SHABIBY: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ahmed Shabiby.

T A A R I F A

MHE. AHMED M. SHABIBY: Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wa huko wanang’ang’ani uwanja uitwe Songwe na Songwe nao watakapopata uwanja wao utaitwa nani? (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea taarifa ya Mheshimiwa Shabiby kwa kukupiga magoti, ahsante sana. Nadhani nimeeleweka namna ambavyo wageni wetu wanakuwa wanasumbuka wanavyotaka kutua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitashukuru sana endapo Serikali italichukua hili kwa maana ya kuandika ule uwanja jina stahili Mbeya International Airport kama mnaona kwamba inafaa kuandikwa jina kwa sababu Mheshimiwa Tulia Ackson ni mwenyeji wa Mkoa wa Mbeya basi uitwe Tulia International Airport. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana pale Mbeya sisi tuna tatizo kidogo. Tuna tatizo la usafiri…

MBUNGE FULANI: Toa hoja kuhusu jina la uwanja.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa hoja, naomba uwanja uitwe Tulia International Airport, nimetoa hoja. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Waheshimiwa naomba mkae. Mheshimiwa Suma endelea. (Kicheko)

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwetu Mbeya namna ya kusafiri kufika Dodoma tunazunguka sana, nilikuwa naomba nishauri Serikali watupatie ndege ambayo itatoka Mbeya kuja moja kwa moja Dodoma, maana sasa hivi tunazunguka ukitaka kupanda ndege upande ndege utue Dar es Salaam halafu Dar es Salaam ufike Dodoma. Nilikuwa naomba sana mlichukue hili ili mtuone na sisi wananchi wa Mkoa wa Mbeya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa suala la airport nilikuwa naomba jambo moja ambalo hili jambo halihusu ndege za local kwa maana ndege za ndani ya nchi yetu sisi. Nilikuwa ninaomba sana uwanja wa ndege kwa maana ya ndege zinazotoka nje ya nchi ambazo zinashushia abiria terminal three nilikuwa naomba sana kule tuweke tozo la trolley kwa maana kwamba sisi tunaposafiri kwenda nchi za nje hasa Marekani ukitua pale kwa maana kwamba yaani ndiyo upo immigration huwezi kuruhusiwa kuchukua trolley bila kulipia na trolley lile ukilivuta halitoki mpaka uweke fedha. Kwa hiyo, sisi hii itatusaidia kama chanzo cha mapato ya ndani ya nchi yetu. Narudia kwamba naomba nieleweke ndege zetu za ndani hizi zisiingizwe kwenye hizo tozo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachangia barabara ya Wilaya ya Rungwe ambayo hii ni ya ahadi ya tangu kipindi cha Awamu ya Nne. Ile barabara ni barabara ya Masoko Road kwa maana inaanzia pale Tukuyu Mjini kwenda Luhangwa kupita Mwakareli kupitia Suma kuja kutokea Katumba; ile barabara niyamuda mrefu sana, ile barabara alipatikana mkandarasi, lakini mkandarasi yule anasuasua sana, anakwenda taratibu sana, sijajua tatizo lipo wapi! Sijajua tatizo ni fedha ama tatizo limekaa upande gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Wilaya ya Rungwe wanahamu sana kuhakikisha ile barabara imekamilika ili waweze kujikwamua na kukwama kwama kwa magari, maana mvua ikinyesha ni tatizo kubwa sana. Nitashukuru sana endapo Serikali italichukua hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kwa dhati niliongea kwa uchungu sana kuhusu barabara ya kutoka Igawa mpaka Tunduma. Sasa basi ninaingia kwenye ombi maalum, nilielezwa hapa na Naibu Waziri kwamba tatizo ni mkandarasi hajapatikana, kwa maana hiyo fedha zipo. Nilisisitiza kumuomba mkandarasi apatikane mara moja. Ninaomba mnapokuja kuwasilisha hapa naomba sana nipate majibu kwamba mmeshampata mkandarasi wa kuijenga ile barabara ya kutoka Igawa mpaka Tunduma na kazi itaanza lini ya kujenga ile barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana namna ambavyo Serikali inaendelea kufanyakazi yake, lakini watu wa TANROADS hawa wanafanyakazi nzuri, lakini wanakuwa wanajisahau wakati fulani. Madaraja haya zile kingo za pembezeni mwa barabara kukiwa na daraja zinakuwa zimebomoka, zinakuwa hazipo, wanajisahau sana kurudishia kiasi ambacho kule kwetu kwenye barabara ya uwanja wa ndege ukitokea Ntokela unakuja uwanja wa ndege ule uwanja wa ndege umeitwa uwanja wa ndege kwa sababu gari zinashindwa kukata kona zinapaa, zinapitiliza, zinadodondoka, lakini mbele yake kuna daraja lile daraja kingo ya upande mmoja imevunjika siku nyingi na juzi kati gari ilitumbukia ….

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma, nakuongeza dakika moja kwa sababu ya taarifa zile. Nakuongezea dakika moja, malizia.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ile kingo haipo tena, gari ilitumbukia matokeo yake ikalipuka ikawaka moto na watu waliteketea pale. Ninaomba sana hawa watu wa TANROADS wanapoona kwamba kwenye barabara ambako kuna madaraja kama kingo za daraja lile zimebomoka naomba wawe wepesi wakurudishia ili tuweze kuponya maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia. Kipekee nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na kunitia nguvu ili niweze kuchangia kwenye Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, ninaomba kuchangia kwa namna ambavyo mwenendo wa halmashauri zetu. Halmashauri zetu zina Wakurugenzi ambao ni wachapakazi kwelikweli na vile vile zina Wakurugenzi ambao sio waaminifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali ilianzisha utaratibu wa force account, kwa nia njema kabisa, lakini utaratibu huo kwa upande mwingine Wakurugenzi wanaosimamia hayo wanafanya vizuri sana, lakini kwa upande mwingine Halmashauri nyingine zinafanya vibaya sana. Hizi fedha ni za walipakodi masikini kabisa wa Taifa hili la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, utakuta Mkurugenzi anakutwa na CAG kwenye ripoti zake, CAG anavyokwenda kukagua pale majengo ambayo yamejengwa kwa force account. Hayo majengo ni mapya, hayajaanza kutumika lakini wakati wa yalipokaguliwa yalikutwa na nyufa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, majengo hayo milango inadondoka yenyewe, hayajaanza kutumika, lakini Mkurugenzi alikuwepo kuangalia na kuhakikisha, maana yeye ndiye msimamizi mkuu wa hiyo halmashauri, lakini anakuwa yupo kama hayupo. Inatia uchungu sana na inasikitisha sana. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, utaratibu wa majengo ya Serikali; yanatakiwa kujengewa vifaa ama hivi vifaa vya ujenzi ambavyo ni standard, ni imara kabisa. Kabla ya Force Account, mzabuni aki-supply ama mkandarasi ambaye anapewa jengo kulijenga, kama hajafanya vizuri, ukaguzi ukipita basi mzabuni ama mkandarasi huyo anawajibika kufanya ujenzi mwanzo mwisho ili kuhakikisha anakabidhi jengo hilo likiwa katika hali inayotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa, ujenzi huu wa Force Account jengo ni bovu, unakuta fedha shilingi milioni 800,000/= ama shilingi bilioni 1.2, jengo ni bovu, lina nyufa nyingi. Analaumiwa nani? Matokeo yake ni hasara.

Mheshimiwa Spika, Mtendaji Mkuu wa PPRA alipotutembelea kwenye Kamati yetu, nilivyokuwa nikichangia juu ya Force Account, namna ambavyo majengo mengi yanakuwa mabovu mapema kabisa kabla ya kuanza kutumika, nilivyokuwa namhoji kwamba moja ya halmashauri imepewa fedha zaidi ya shilingi bilioni 3.0, lakini jengo sio imara. Jengo wakati fulani limeshaanza kujengwa, fedha zimeisha jengo halijakamilika na fedha hazijulikani zimekimbilia wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inasikitisha sana. Mtendaji Mkuu yule wa PPRA akanijibu akasema, Mheshimiwa Mbunge, unachoongea kuhusu Force Account ni tatizo kubwa. Anasema mahali pengine wamepita wamepewa fedha shilingi bilioni 8.0, jengo halijakamilika. Shilingi bilioni 8.0 jengo halijakamilika, tunakwenda wapi? Watanzania tunatakiwa tufike mahali uzalendo ujae ndani ya mioyo yetu. Hizi fedha zinalipwa na mlipakodi. Kwenye halmashauri kuna matatizo makubwa sana. Kwa kweli matatizo ni makubwa, ni makubwa, ni makubwa, sijui ni namna gani tufanye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hizo fedha nyingi sana zinakwenda mabilioni kwenye Force Account. Sioni kama inatusaidia. Natamani sana kuishauri Serikali, fedha za Force Account angalau basi tuweke limit. Kama ni mambo ya Force Account, basi isizidi shilingi milioni 100, lakini kwa mabilioni eti Force Account, usimamizi unakuwa sifuri kabisa. Hilo linakuwa ni tatizo kubwa sana, mioyo inauma. Tunatakiwa tuwaonee huruma hawa walipakodi.

Mheshimiwa Spika, nakwenda kuchangia eneo la madeni ya wazabuni na wakandarasi…

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika Taarifa.

TAARIFA

SPIKA: Mheshimiwa Suma Fyandomo, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Charles Kajege.

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nataka nimuunge mkono msemaji. Force Account siyo kwamba tu miradi haikamiliki lakini hata ubora wake. Sehemu nyingi unakuta majengo yameshaharibika within mwaka mmoja. Kwa hiyo, nashauri kwamba ikiwezekana tuondoe kabisa mambo ya Force Account. (Makofi)

SPIKA: Sawa. Sasa, mwenye hoja yake alikuwa ameshatoa ushauri wake. Naona na wewe umeongeza wa kwako. Mheshimiwa Suma Fyandomo, endelea na mchango wako.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante.

NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Inatokea wapi taarifa.

NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, hapa.

SPIKA: Sasa, Mheshimiwa Waziri, ili nielewe taarifa unampa Mheshimiwa Kajege au Mheshimiwa Suma?

NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, wote wawili. (Kicheko/Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI, wote wawili! Haya.

NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kuwapa taarifa Waheshimiwa wachangiaji kwamba, kimsingi ukifanya tathmini ya utekelezaji wa miradi kwa kutumia Mfumo wa Force Account, kuna faida kubwa zaidi kuliko hasara. Kwa mfano, zahanati ambazo tunajenga kwa takribani shilingi milioni 100, ukichukua nguvu za wananchi na shilingi milioni 50 inaongezwa na Serikali, ukipeleka kwa mkandarasi zahanati ile siyo chini ya shilingi milioni 250 hadi shilingi milioni 300. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vituo vya afya ambavyo tunajenga kwa shilingi milioni 500, ukipeleka kwa mkandarasi si chini ya shilingi bilioni 2.0 hadi shilingi 2.1/=. Sasa, kuhusu udhaifu wa ubora wa miradi inategemea. Si kwa sababu ya Force Account, ni udhaifu wa usimamizi ambayo lingeweza kutokea pia, hata mkandarasi asiposimamiwa kuna miradi inakuwa na udhaifu wa aina hiyo. Kwa hiyo, naomba niwape taarifa Waheshimiwa Wazungumzaji kwamba, jambo la msingi ni usimamizi wa wataalam wanaokuwa katika maeneo yale badala ya mfumo kuwa Force Account au kuwa Contractor. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, tutatamani baada ya huo uzembe au udhaifu wa usimamizi, ni hatua gani zinachukuliwa ili wengine sasa wasiendelee na huo uzembe. Kwa sababu, haya yanayosemwa ya mabilioni hakuna mtu anayefurahi pesa iende halafu jengo lisikamilike. Pesa iende halafu jengo liwe halina viwango. Kwa hiyo, lazima tuone Serikali inachukua hatua gani kwa hao waliozembea ili huu mfumo uzuri wake uendelee na ule ubaya wake uondolewe kwa kuondoa hawa watu ambao wanaufanya mfumo mzima uonekane uko vibaya. (Makofi)
Mheshimiwa Suma Fyandomo, endelea na mchango wako.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, nilidhani kwamba unaniuliza kama napokea taarifa ama sipokei, ama maamuzi yameshatolewa. (Kichecho)

SPIKA: Nimeshindwa kukuuliza hilo swali, kwa sababu taarifa ya kwanza iliyotolewa ulikuwa umeshaingia kwenye hoja nyingine. Halafu Mheshimiwa Naibu Waziri amekuja baada ya ile taarifa nyingine na ushauri wa yule mwingine lakini naona kama wewe unakusudia kuipokea, basi nikuulize. Mheshimiwa Suma Fyandomo, unaipokea taarifa ya Mheshimiwa Naibu Waziri Kwa sababu, mchango ulikuwa wa kwako? Ahsante sana. (Kicheko)

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, naongea kwa uchungu mkubwa kwenye hili Taifa, nina uchungu moyoni. Siwezi kuipokea taarifa hii. Siwezi kuipokea kwa namna ambavyo Mheshimiwa Naibu Waziri, ni kaka yangu, namheshimu sana, ameongea anasema inatakiwa utafutwe utaratibu wa watu wa kwenda kusimamia fedha hizi. Utafutwe na nani na lini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunatakiwa tuwe makini sana na hizi fedha, tuwe na uchungu. Natamani sana na natamani wanaonipa taarifa, kwa maana wanaguswa na ninachokisema, wajiorodheshe na wenyewe waingie kwenye michango, ilikuwa njema sana. (Makofi/Kicheko)

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

TAARIFA

SPIKA: Mheshimiwa Fyandomo, kwa utaratibu wetu hii itakuwa ni taarifa ya mwisho. Mheshimiwa Mwanaisha, nimesikia kama sauti ya Mheshimiwa Mwanaisha Ulenge.

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba nimpe taarifa dada yangu Mheshimiwa Suma Fyandomo kwamba, maneno anayoyasema ni sahihi na ni kwa mujibu wa tafiti. Aliyoyazungumza hapa Mheshimiwa Naibu Waziri, atuletee tafiti. Tafiti zimefanywa na PPRA ambaye ndiyo mwenye dhamana ya kusimamia manunuzi ya umma. Tafiti zimefanywa na Bodi ya Wahandisi. Tafiti zimefanywa na Baraza la Ujenzi Nchini kwamba, Force Account hazina tija kwa Taifa hili. Kwa nini tunaendelea kung’ang’ania? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiyo ndiyo taarifa ambayo nataka kumwongezea dada yangu Mheshimiwa Suma. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Haya. Mheshimiwa Waziri kaa kidogo. Mheshimiwa Suma Fyandomo, unaipokea taarifa hiyo ya Mheshimiwa Mwanaisha?

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ndiyo, naipokea kwa mikono miwili kabisa.

SPIKA: Ahsante sana. Sasa, kaa kidogo, nakulindia muda wako. Mheshimiwa Waziri wa Fedha naona umesimama, sijui umesimama kwa taarifa, utaratibu ama?

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, nilitaka kutoa taarifa na ufafanuzi. Pamoja na kuheshimu…

SPIKA: Sasa, ngoja tuliweke vizuri. Ufafanuzi utapata nafasi ya wewe kuchangia, ila kama unatoa taarifa, unaruhusiwa kuitoa sasa. (Makofi)

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, natoa taarifa.

TAARIFA

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Spika, pamoja na maoni haya yanayotolewa na Waheshimiwa Wabunge, kuanzia mtoa hoja pamoja na Engineer ambayo yanalenga kusimamia rasilimali fedha za walipa kodi na value for money. Naomba tu kutoa taarifa kwamba, si kweli kwamba jambo hili halina tija yoyote. PPRA pamoja na Bodi ya Wahandisi waliishauri Serikali kuendelea kulifanyia maboresho na hicho ndicho tulichofanya, hata kwenye sheria tuliyoipitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge, utaratibu huu wa Force Account unatusaidia kujengea uwezo wananchi wetu kule majimboni. Utaratibu wa kutumia wakandarasi hata kwenye shughuli zinazotokea kwenye grassroot, unawafanya wananchi wetu wa kawaida wakose kazi. Utaona tulivyotumia Force Account kwenye fedha zile takribani shilingi trilioni moja, tuliweza kutengeneza mgawanyo wa fedha ziende kwenye kila wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kutumia wakandarasi, kuna baadhi ya maeneo huwa inaweza ikatokea mkoa mzima, wakandarasi wanaofanya shughuli hata za kujenga vyoo, hata za kujenga madarasa wanatoka mikoa mingine. Ni lini utajenga nguvu ya kazi na sasa hivi tumeshasomesha vijana karibu kila kata? Kwa hiyo, tutaendelea kuboresha na kusimamia mapungufu, lakini tutaendelea kuwatumia pia mafundi kujenga majengo yanayopatikana katika maeneo kule wanakoishi. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Tabasamu, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba alikuwa anatoa taarifa. Kwa hiyo, taarifa haiwezi kuwa juu ya taarifa nyingine. Muda wako Mheshimiwa Suma naulinda. Taarifa ya LAAC ukurasa wa 38 mpaka 39 unaonesha changamoto za matumizi ya Force Account na huku mbele umeeleza kuhusu maazimio, wanapendekeza nini kwa Bunge. Kwa hiyo, tunaweza kupitia hayo maeneo halafu tuone nini tunataka kufanya. Kwa sababu, ni kweli kwa upande mmoja kama alivyosema mchangiaji, inafanya vizuri. Kwa upande mwingine kuna changamoto. (Makofi)

Hizi changamoto siyo kwamba ni ndogo, ndiyo maana zinasemwa ili zifanyiwe kazi. Hakuna namna itaonekana huu mfumo uko vizuri kwa sababu tu maeneo yetu yale kuna watu wanaguswa, hapana. Tunataka tija kwenye matumizi ya huu mfumo. Nadhani ndicho ambacho Kamati inajaribu kusema kwenye hii taarifa yake. Kwa hiyo tupitie hayo maeneo ambayo taarifa ya Kamati imeyasema ili tuweze na sisi kujielekeza vizuri kwenye yale mapendekezo yetu kwa Serikali. (Makofi)

Kwa sababu, maeneo mengine inajengwa shule, Mwalimu Mkuu sijui Mkuu wa Shule ndiyo msimamizi. Sasa, yule siyo mtaalam. Kwa hiyo, mazingira kama hayo kidogo ni changamoto kubwa, kwa sababu, hata yeye ukisema unataka kumwajibisha unamwajibisha vipi? Yeye siyo mtaalam wa hilo jambo. Yeye kazi yake ni kufundisha lakini umempa kazi ya ziada. Kwa hiyo, kidogo inakuja hiyo changamoto kwa sura hiyo. (Makofi)

Kwa hiyo, katika yale maboresho itazamwe kwa sura hiyo pana anayochangia Mheshimiwa Mbunge. Mheshimiwa Suma Fyandomo, malizia mchango wako. Kwa maana ya kwamba muda wako ulikuwa umelindwa. Kwa hiyo, endelea kwenye hoja yako nyingine. Ahsante. (Makofi)

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Mheshimiwa Waziri wa Fedha Mwigulu Nchemba, ilitosha kabisa ile aliyoniambia kwamba wanafanya maboresho. Sasa, kwa sababu amejazia kitu kingine kaka yangu Mheshimiwa, basi naomba nimwambie. Unajua vifaa mfano vifaa vya bomba, inatakiwa kama ni koki ile ya bomba inunuliwe kifaa halisi. Sasa, hawa watu wakitumia Force Account kwenda kununua vifaa vya bomba, wananunua local kabisa, kiasi kwamba maji yanaanza kumwagika hovyo, mipira inapasuka na kila kitu. Ndiyo maana ya msisitizo kwamba, kwa sababu umesema maboresho boresheni kwa uhakika na kwa uhalisia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili suala lichukuliwe kwa uharaka sana na kwa umakini. Lichukuliwe kwa uharaka kwa sababu, kama ni maboresho watuambie ni lini ukomo wake wa maboresho kwamba, kufika kipindi fulani tutakuwa tumeshakamilisha maboresho, kila kitu kitakuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna upande wa madeni ambayo wazabuni wanadai. Inasikitisha sana na inatia uchungu sana. Kuna wazabuni ambao wali-supply vifaa vya ujenzi ama makandarasi kwa miaka mingi. Wengine miaka 10, miaka mitano na miaka 15, fedha zao mpaka sasa hawajalipwa. Ukimuuliza Mkurugenzi, kwa nini unadaiwa mpaka shilingi bilioni 4.0 na wazabuni pamoja na wakandarasi, tatizo ni nini? Kwa nini usilipe fedha zao na ni muda mrefu umepita? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, anakujibu kirahisi kabisa anasema mimi sikuwepo kipindi hicho. Sasa kama ulikuwa haupo kipindi hicho, wanavyokabidhiana ofisi wanakabidhianaje? Yaani kwamba hawakai wakakabidhiana haya madeni wanadai hawa, haya wanadai hawa, haya anadai huyu? Siyo tu madeni, kwa utaratibu mzima wa kila kitu kilichoko pale. Kukabidhiana kwao ni kama vile, akifika Mkurugenzi mwingine anamwambia hii ndiyo ofisi karibu, kwa heri naondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya madeni, hawa wazabuni wa Taifa letu la Tanzania wataendelea kuwa maskini, maskini, mpaka kwa sababu fedha zao hawalipwi. Halafu Mkurugenzi anakujibu swali lingine ukimuuliza. Kwa nini imefikia hapa shilingi bilioni tano au shilingi bilioni tatu? Anasema, unajua hapa Mheshimiwa Mbunge, mimi hapa upande wa hizi fedha shilingi bilioni tatu kama halmashauri, natakiwa nilipe shilingi bilioni mbili ama shilingi bilioni moja, shilingi bilioni mbili inatakiwa illipe Serikali ama Wizara husika. Huyu mkandarasi au mzabuni anajua wapi pa kuingilia Wizarani au huko kwenye ofisi anakosema kwamba, wafuate kwenye Serikali, anafuta wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba tuokoe maisha ya wazabuni na wakandarasi, kwa sababu fedha hizo wanakuwa wamekopa, fedha hizo mwisho wa siku wanauziwa nyumba zao, wanakuwa hawajui wataishi vipi, hela za kwenda kupanga hawana, wanabaki wanapigwa stroke, wanabaki wana presha, mwisho wake unakuwa ni kifo. Tuwanyanyue hawa wakandarasi wa Taifa hili la Tanzania lakini tuwanyanyue hawa wazabuni ma-supplier. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, lakini naomba haya wayatendee kazi. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza namshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehema amenipa kibali nami niweze kusimama kuchangia kwenye Bunge hili Tukufu. Awali ya yote ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan na Amiri Jeshi Mkuu, ambapo ametusaidia sana kwenye Hospitali ya Mkoa wa Mbeya. Kwenye hospitali ile ametupatia fedha kiasi cha shilingi bilioni tano kwa ajili ya kujenga jengo la upasuaji, lakini pia ametoa milioni 800 kwa ajili jengo la emergence.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye jengo lile tuna upungufu. Nilikuwa naomba sana, jengo lile halina wodi ya wanawake. Ninaomba sana kwenye bajeti hii tusiache kuweka fedha kwa ajili ya kujenga jengo la wodi ya wanawake, ni matatizo. Hii ni kwa sababu wanawake wanapata tabu sana maana wakiuguwa sehemu ya kuwalaza wanawake inakuwa ni tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuchangia suala la TASAF. Ninaishukuru sana Serikali kwa sababu inatoa fedha kwa ajili ya watu wasiojiweza na wazee. Ninaishukuru na kuipongeza sana na Serikali.

Mheshimiwa Mwneyekiti, hata hivyo hatujaiangalia kwa mapana. Nimejaribu kupita kwenye kaya tofautitofauti ambazo zinasaidiwa na hizi fedha za TASAF; unapita kwenye kaya unamkuta bibi ama babu amekaa upenuni hawezi kutafuta hata kuni hawezi kuwasha moto hawezi kufanya chochote. Fedha wanaweze wakawa wamemfikishia, lakini anaweza akaa upenuni kwakwe anavizia either apite kijana ambaye akimuona ampatie fedha akamsaidie akanunue sukari. Sasa inawezekana akapita kijana ambaye ni mcha Mungu, wakati huo huo anaweza akapita kijana ambaye si mcha Mungu; hiyo pesa imeondoka anabaki tu kusikitika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuishauri Serikali ninaomba sana hizi fedha TASAF ninaomba kila wilaya wafanye mpango wa kujenga hostel kwa ajili ya kutunza hawa wazee wetu. Itawasaidia sana hawa wazee. Naamini wakikaa kwenye hostel watapata huduma zote, na fedha hizi zitakwenda moja kwa moja kwenye vituo vya hosteli ili wazee wetu waweze kupata huduma stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nimeuliza swali, lakini katika kuuliza lile swali nilijibiwa. Kwenye Wizara ya Ujenzi kuna sehemu ambayo sikuielewa vizuri, sehemu yenyewe ninaomba sana tuchukulie kwa uzito. Ni kuhusu hii barabara ya kutoka Igawa mpaka Tunduma hapa ninachangia, ninaomba sana hiyo barabara mtu anapotoka Dar es Salaam, anatoka Dodoma akifika Igawa kuanza safari ya kuelekea Mbeya Mjini mpaka Tunduma moyo lazima ulipuke, moyo unafanya fya’ fya’ kwa sababu anakuwa hana uhakika wa kufika salama nyumbani kwake. Yaani hakuna alama za barabarani, barabara ni finyu na ina mashimo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikwambie hali ni mbaya sana. Mtu akitoka Mbeya Mjini anakwenda Mbalizi ni lazima aage, amuage mtu yeyote, kama mke wake hayupo ama mume wake ametoka anampigia simu, hata kama yuko Dar es Salaam amesafiri anasema natoka kidogo hapa Mbeya Mjini naenda Mbalizi. Hii ni kwa sababu ile barabara haamini kama anaweza kurudi salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakati huo huo hiyo barabara ya kutoka Mbalizi kuelekea Tunduma ni finy, ajali zimekuwa nyingi sana, ndugu zetu wanakufa wengi sana kwa sababu ya barabara finyu. Ninaomba tuchukulie kwa uzito. Bunge la Bajeti ya mwaka jana nilisikitishwa sana kwamba ilitengwa bajeti ya km tano za lami; km tano kutoka wapi mpaka wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoomba hapa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante!

MHE. SUMA I. FYANDOMO: …dakika moja tafadhali. Walisema kwamba wanatafuta mkandarasi; ninaomba tuchukulie serious sana, mkandarasi atafutwe haraka ili ile barabara ianze kujengwa Mbeya tunalia jamani, Mbeya tunateseka sana na ile barabara. Madereva wanajua lakini na sisi tunaosafiri tunajua kwa sababu mioyo yetu haikai sawasawa tunapopita zile barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nashukuru sana.

MWENYEKITI: Umemaliza ee!

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.

MWENYEKITI: Umemaliza maana nilikuwa nimekuongeza dakika moja.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

MWENYEKITI: Si unaongelea Mbeya Mjini!

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Ninakushukuru sana.

MWENYEKITI: Nilikuwa nimekuongeza dakika moja kwa sababu nimeona pale bosi wangu naye anapiga makofi, na mimi napenda kibarua changu.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana, hata Mheshimiwa mwenyewe akifika maeneo yale lazima ashike kiti sawasawa kwamba nitafika salama, na ndiyo maana na yeye inamgusa sana ile barabara ya kutoka Igawa hadi Tunduma. Ninaomba sana; wananchi wa Mkoa wa Mbeya tuna kilio, na machozi. Naomba Serikali ichukulie kwa uzito sana, tafadhali sana sisi kule Mbeya hatuko mikono salama kwa sababu maisha ya watu wengi sana yanaathiriwa na barabara, watu wanakufa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafadhali sana, naomba sana, ninaunga mkono hoja juu ya hili; lakini pia ninaomba kwa upande wa Serikali.

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante ninakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Maji. Kwanza ninamshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye amenipa afya njema niweze kusimama hapa kuchangia jioni hii ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri wa Maji Jumaa Aweso kwa kazi nzuri anayoifanya na ni Kijana mahiri kabisa. Mheshimiwa Waziri Aweso una nidhamu kiasi kwamba wewe ni kijana rijali hata siku hii ya leo umekuja kututambulisha mawifi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maji Maryprisca Mahundi, Mheshimiwa huyu wa Naibu Waziri wa Maji sisi hapa wote ni mashahidi. Wabunge wa Majimbo wanapokuwa wakiomba aweze kuwafikia Majimboni mwao amekuwa hasiti kufika anawaahidi na anafika, nakupongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri Maryprisca Mahundi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mchango mkubwa sana kwenye Mkoa wetu wa Mbeya. Kwanza kabisa lengo kubwa la Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ni Kumtua Ndoo Mama Kichwani, na mama yetu huyu amekuwa na juhudi kubwa sana juu ya hilo. Lakini kwetu Mbeya kuna Mradi wa Kiwira ni Mradi mkubwa sana ambao utalisha Mkoa mzima wa Mbeya, mradi ule ni wa fedha kiasi cha shilingi bilioni 200. Cha kusikitisha mradi ule umetengewa fedha kiasi cha shilingi bilioni tano, napata wasiwasi sana bilioni tano kwa kugawa hiyo bilioni 200 ina maana ni miaka 40 ijayo ndipo mradi huo uje ukamilike nikiwa tayari nimekuwa kikongwe kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake wa Mkoa wa Mbeya wako busy sana kutafuta fedha kwa ajili ya kulisha familia zao. Wanawake wa Mkoa wa Mbeya huwezi ukamkuta mwanamke wa Mkoa wa Mbeya yuko kibarazani anapiga story, anacheza draft, anacheza sijui miboi sijui vitu gani. Wanawake wanatafuta pesa, sasa wanaacha kutafuta pesa kwa ajili ya kulisha familia zao wanahangaika kwenda kutafuta maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata akina baba hapa ni mashahidi kwenye hili siyo Mbeya peke yake ni Tanzania nzima wanawake ndiyo wanahangaika na familia. Sasa wanawake wanabadilika kuacha kutafuta fedha za familia wanahangaika kwenda kutafuta maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaongea hili kwa uchungu sana, Wilayani Rungwe kuna Mradi wa Maji ambao una thamani ya 4,500,000,000.00 niliongea hapa ule Mradi mabomba peke yake kwenye kutandaza kutoka kwenye chanzo cha Mto Mbaka inatakiwa fedha shilingi 1,800,000,000 ilitolewa 5,000,000,000. Lakini wakati huohuo Serikali ikatoa shilingi milioni 200 hiyo shilingi milioni 200 hata Kiwandani kwa ajili ya kwenda kuongeza mabomba haifai, wamekataa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naiomba sana Serikali naomba sana kwa dhati, ninaomba hii fedha kwa ajili ya mabomba ni force account inatumia nilikuwa naomba kwenye suala la kujenga tenki la maji, wamtafute Mkandarasi ili aanze kujenga tenki la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Tukuyu Mjini ni za kwanza kuathirika juu ya kutokupata maji, Kata ya Bagamoyo, Kata ya Msasani, Kata ya Makandana kwenye Kata ya Makandana eneo la Kioski ndiyo shida kabisa. Kuna Kata ya Kawetere, kuna Kata ya Idigi, kwa masikitiko makubwa hata kata ambapo anatoka mama mzaa chema nako maji hakuna ni tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana tuchukulie serious suala hili, sasa hivi kwenye hiyo bajeti imetengwa shilingi milioni 500 peke yake, milioni 500 itasaidia nini. Mabomba yale ile fedha mliyotota kwanza ile milioni 700 ya awali ni kilomita tatu tu kati ya kilometa 9.5. Mheshimiwa Waziri ninakuomba sana, sina lengo hata kidogo la kusema naweza kushika shilingi yako kwa sababu natambua wewe ni msikivu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni msikivu na hapa utakuja kuongea hiyo siku ya kesho wakati unavyohitimisha kwamba utapeleka fedha kwenye Wilaya ile ya Rungwe ili mradi uendelee. Narudia kukuomba tena kuhusu suala la kujenga tenki, kuhusu kujenga ninaomba atafutwe Mkandarasi ninashauri Serikali, naomba suala la fedha ya mabomba iongezeke.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Halmashauri ya Busokero ninazidi kumshukuru Mheshimiwa Rais Mama Samia, nilikuwa nikiwalaumu watumishi kwamba hawafanyi kazi ipasavyo. Lakini fedha Busokero kule kulikuwa na changamoto mwaka jana kulitokea mafuriko kwenye Kata ya Isange na Kata ya Lwangwa. Lwangwa ndiyo halmashauri ndiyo mjini pale, watumishi wa Serikali na wananchi wote wanasumbuka na maji. Fedha ipo lakini utendaji wa kazi haupo, nawapongeza sana na mlipeleke. Kilichosikitisha zaidi Watendaji kwenye halmashauri kumbe wanatakiwa watoke kwenye Wilaya ya Rungwe. Lakini Watendaji hawa wa Wilaya ya Rungwe hawana usafiri wa kufika kule. Hawa watu wa RUWASA fedha za kununulia magari waliomba Benki Kuu ya Dunia walipewa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kupewa fedha zile hawa watu wa GPSA ndiyo walipewa fedha miezi mitano iliyopita mpaka sasa hivi hawajaleta magari yale. Kwa hiyo, nilikuwa naomba Ofisi ya Waziri Mkuu iingilie kati kutoa kibali ili magari yale yaweze kufika na Watendaji wale wapate magari ili waweze kufika site kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitashukuru sana kama hili litachukuliwa kwa uzito. Kwenye Mkoa wetu wa Mbeya nilikuwa naomba sana kuna fedha ambazo zinatoka Benki Kuu ya Dunia kwa mkopo nafuu, kuna Mikoa nane tu ambayo imeingizwa humo kwenye orodha. Ninaomba na Mkoa wa Mbeya uingizwe kwenye P4R ninaomba sana. Mheshimiwa Aweso ni msikivu sana wewe kaka, ninakuomba wakati unakuja kuhitimisha naomba nisikie kwamba Mbeya imeingizwa kwenye utaratibu wa P4R nitashukuru sana. Kwa sababu nitajua kwamba matatizo ya maji Mbeya yanaenda kuisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Kata ya Rujewa kwa maana ya Mbarali pale kuna Mradi ambao umejengwa miaka ya 80 wananchi wameongezeka na sasa hivi ni maendeleo zamani tulikuwa tunakimbilia tukienda washroom nitakimbilia huko nje sasa hivi ni ndani, huko ndani kunatakiwa maji. Pale kile chanzo cha maji sasa hivi kinauwezo wa kutoa lita milioni 200 kwa siku, wakati mahitaji ya watu wa Mbarali kwenye Kata husika ya Rujewa pale wanataka kutumia maji lita milioni 700 kwa siku. Sasa uone ni namna gani upungufu wa maji upo kwa kiasi kikubwa kwenye maeneo yale.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma muda wako umeisha ulipigiwa kengele nilikuachia dakika moja zaidi.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Dakika moja eeh.

MWENYEKITI: Malizia hiyo sentensi yako Mheshimiwa.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali walitoa wazo zuri sana wananchi wanaoishi Wilaya ya Chunya, Wilaya ile ya Chunya walijenga kisima, walichimba kisima lakini kisima kile hakijakamilika kwa sababu ya fedha. Kile kisima kilikuwa na thamani ya shilingi milioni 199 zilizotolewa fedha shilingi milioni 100 peke yake ambapo wamefanikiwa sawa kuweka mabomba. Lakini mambomba ya kuwasambazia wananchi kuwafikishia kwenye nyumba zao ni changamoto kwa sababu fedha hazijakamilika. Ninaomba sana hiyo fedha kiasi cha shilingi milioni 99 ziwafikie wenyeji wa Chunya ili Chunya pale mjini waweze kukomboka waweze kunufaika na maji yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, ninakushukuru sana. Ninaunga mkono hoja, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia Wizara hii ya TAMISEMI. Kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambako ameniwezesha kuwa mzima na kunipa afya njema, ni jambo la kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa sababu tunavuta na kupumua hewa yake bure. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anazozifanya. Kazi hizo zinaonekana kiuhalisia, nimshukuru sana kwa sababu Mkoani kwetu Mbeya amekuwa akitutumia fedha za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wetu Juma Zuberi Homera pamoja na timu yake namna ambavyo wanasimamia vizuri sana shughuli za maendeleo kule Mkoani kwetu Mbeya. Na kupitia Mheshimiwa Mkuu wetu wa Mkoa Zuberi Homera, Mkoa wetu sasa hivi unakwenda kwa kasi na umetulia kweli kweli kama jinsi ambavyo Mbunge wa Mbeya Jiji anaitwa Mheshimiwa Dkt. Tulia na Jiji letu la Mbeya limetulia kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeza sana TAMISEMI, TAMISEMI ambapo wanafanya vizuri wakiongozwa na Mheshimiwa Waziri Kairuki pamoja na Manaibu Waziri wake. Nawapongeza hawa vijana wetu wa TARURA wanafanya kazi nzuri, TARURA Mkoa wa Mbeya ni wachapakazi na wanajituma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bajeti inakuja hapa Bungeni tunaipitisha na tunaamini kwamba fedha zile tunapitisha, zinakwenda kufanya kazi zilizolengwa. Mwaka 2022/2023 tulipitisha hapa kazi za maendeleo matengenezo bilioni 8.4 zimepokelewa bilioni 4.2 sawa na asilimia 51. Fedha za jimbo bilioni 3.5 zimepokelewa bilioni 2.1 sawa na asilimia 60, fedha za tozo bilioni 7.5 zimepokelewa bilioni 4.3 sawa na asilimia 60. Maendeleo bilioni 1.7 zimepokelewa milioni 968 sawa na asilimia 56. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi mwaka unakwendakwisha imebaka kama miezi wiwili tu, fedha zile hazijafikishwa kule TARURA, ambapo wazabuni nikimaanisha makandarasi
wanafanyakazi kwa kujituma kuhakikisha wasikwamishe maendeleo ambayo ni ya mkoa, hasa kwa barabara na wakandarasi hawa fedha wakati fulani wanakua wanakopa na zingine wanachukua fedha za moto. Wanaishia kuuziwa nyumba zao ama mashamba yao waliowekewa rehani. Sasa tunatakakujua Wananchi wa Mkoa wa Mbeya, fedha zinakuwa zinakwenda wapi? Na kwa nini zisifike kwa wakati kule? Zile ambazo tumeshazipitisha hapa. Nini kinasumbua? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, sasa hivi mwaka kesho tunakwenda kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa. Mkoa wetu wa Mbeya unatatizo kubwa sana la Maafisa Watendaji, wamekuwa ni shida hawapo. Ukienda Wilaya ya Rungwe hatuna Maafisa Watendaji 48, Mbeya Jiji Maafisa Watendaji 60 hawapo, Chunya 10 hawapo, Mbeya DC 16 hawapo, Busokelo 12 hawapo. Jumla Mbeya tuna upungufu wa Maafisa Watendaji 146 na sasa mwaka kesho tu tunakwenda kwenye chaguzi za Serikali za Mitaa, tunaomba sana mliangalie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo nimeongea kuhusu TARURA. Sasa hivi vyakula vipo bei juu, wazabuni ambao wanapeleka vyakula kwenye shule za kwetu kwa maana shule za Serikali. Fedha zilizokuwa zikipelekwa zimepunguzwa sana. Chakula kipo bei juu, chakula kipo baharini kabisa kule bei zake lakini fedha zinapelekwa kidogo. Sasa hivi Serikali inatengeneza madeni kwa mazabuni. Mazabuni wanapata shida sana namna ya kuendesha biashara zao namna ya kuendesha kazi zao.

Mheshimiwa Spika, tulikuwa tukiongelea sana kuhusu mabweni ya watoto wa kike. Kwa namna ambavyo walikuwa wakipata changamoto huko mitaani lakini sasa hivi ninaomba sana Serikali iwekee mkazo hili, ione jicho la huruma. Sasa hivi changamoto iko kwa watoto wa kike, ipo kwa watoto wa kiume. Naomba sana tunapoelekeza kuendelea kujenga mabweni tuelekeze kujenga mabweni kwa ajili ya watoto wa kike na watoto wa kiume. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaipongeza sana Serikali ninampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, Samia Suluhu Hassan, amesema kazi iendelee na nimefanya msisitizo hata kuvaa nguo hii ambayo niivaa mitaani kote kuonyesha kazi iendelee na kweli kazi itaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunafanya kazi nzuri naipongeza Serikali kwamba wamejenga zahanati, vituo vya afya lakini watumishi wamekuwa ni changamoto nikimaanisha kwamba vile vituo vya afya vimejengwa lakini madakatari ni tatizo. Tunaomba sana mpeleke madaktari, mmpeleke manesi lakini pia hata vitendea kazi vimekuwa ni duni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali iweke jicho la huruma juu ya haya ninayoyaongea hapa. Naomba sana jambo lingine kwa upande wa ndugu zetu hawa wa TAMISEMI. Nimeongelea suala la barabara, naomba nijaribu kuongelea kwa upana wake. Safari hii tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa fedha ambazo amezipelekea TARURA, lakini hazijafika zote ila barabara zile ambazo zilifikiwa kiukweli zimekuwa nzuri na mafuriko kidogo yamepungua hata usumbufu umepungua.

Mheshimiwa Spika, kipekee…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa kengele imegonga ya pili.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii lakini ningependa sana kujua anavyokuja kuhitimisha hapa Mheshimiwa Waziri atuambie fedha zile ambazo zinacheleweshwa nini kinasababisha zicheleweshwe hizi fedha
badala ya kwenda kwa muda muafaka ili makandarasi waache kusumbuliwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hii Wizara ya Elimu. Kwanza kabisa nipende kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa namna ambavyo amenipa afya njema nimeweza kupata nguvu ya kusimama, kuchangia wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa namna ambavyo inafanya kazi vizuri ya kuboresha mambo ya elimu kwenye nchi yetu hii ya Tanzania. Mheshimiwa Rais, Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, anafanya kazi nzuri amekuwa akitenga fedha nyingi sana kwa ajili ya elimu na mambo mengine mbali mbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu ninaomba kabla sijaanza kuchangia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, kaka yangu Mheshimiwa Mkenda pamoja na Naibu Waziri, Katibu Mkuu na watumishi wote, wanafanya vizuri sana kusimamia elimu kuhakikisha inakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo kubwa sana kwenye shule za msingi. Shule za msingi zipo lakini ni kama tumezisahau kidogo, shule za msingi madarasa yamekuwa ni machakavu kwelikweli. Madarasa ni machakavu halafu wakati huo huo wanaweza yakawa hayatoshelezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano pale Wilaya ya Rungwe, Kiwila kuna shule ya Mpandapanda ile shule ina wanafunzi jumla ya 1,380 ina vyumba vya madarasa saba kiasi kwamba darasa moja wanakaa wanafunzi 197 hiyo inapelekea shida kweli kweli namna gani ya kukaa wakiwa madarasani ili watoto waweze kuelewa wanavyofundishwa na walimu. Msongamano huo ni mkubwa sana, wakati huo huo kuna shule ambazo zina hali mbaya sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Wilaya ya Kyela kuna shule moja ya msingi inaitwa Makwale ina hali mbaya sana. Lakini wakati fulani hata ofisi zinakosena, wanachukua darasa wanaweka kama ndiyo ofisi, ambapo inaendelea kupungu zaidi idadi ya madarasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuiomba Serikali, naomba itizame kwa upya, maana elimu ya msingi ina matter sana kwa sababu bila msingi hawajafika watoto sekondari, hawajafika chuo, hawajafika maprofesa wanakuwa hawapo wala madaktari bila shule ya msingi. Kwa hiyo, nilikuwa napenda kushauri Serikali shule za msingi hizi tuzitazame ziboreshwe, ziwe mkazo wa kuboreshwa kwa sababu elimu yote inaanzia huku chini ndipo madarasa na vidatu vingine vinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba nishauri Serikali pia, nishauri Serikali kwa upande wa wahasibu. Ninaipongeza Serikali imeweka wahasibu lakini kwenye shule zile kongwe Sekondari ya Rungwe, Iyunga Sekondari, Loleza kuna wahasibu kule na zingine nyingi tu ambazo zina wahasibu. Hizi shule zetu za kata za sekondari zilizo nyingi hazina wahasibu, anateuliwa mmoja wa walimu kwa ajili ya kwenda kufuatilia fedha kwenye halmashauri na mifumo inakuwa inasumbua, anaweza akaenda kwa siku nne mfululizo na mwalimu yule ana vipindi darasani anatakiwa afundishe kwa hiyo, watoto wanakosa vipindi. Kwa sababu mwalimu anaenda kufatilizia mambo ya kiuhasibu kwenye halmashauri na si kwamba halmashauri wanafanya makusudi, hapana ni kwa sababu mifumo inakuwa inasumbua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo basi nilikuwa natamani serikali kama itaona inafaa basi watafutwe ama waajiriwe wahasibu siyo kwa kila shule, anaweza akawa muhasibu mmoja, ambaye anaweza akawa ana shughulikia shule tano mambo ya kifedha nadhani hilo litatusaidia kuiweka elimu yetu katika utaratibu mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mifano ipo hai kabisa, mtu anatoka Kata ya Nzovwe kule Mbeya Jiji au Iziwa nauli ni zaidi ya shilingi 5,000 anakwenda mjini Mbeya Jiji pale kwa ajili ya huduma. Mfumo umegoma basi anarudi kama alivyo kesho hivyo hivyo lakini bado mambo yanakwama kwa sababu vipindi ambavyo alitakiwa afundishe watoto wale wanakwama kupata masomo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuchangia kwenye upande wa vyuo. Serikali inafanya vizuri sana kule Mbeya, Wilaya Rugwe tumebarikiwa, tuna vyuo viwili vya walimu, kuna chuo cha Mpuguso. Chuo cha Mpuguso Serikali imekitizama kwa jicho zuri, imefanya vizuri kwa maana imeboresha majengo lakini pia imeongeza mabweni lakini iliweka lami pia japo kwa sehemu lakini kuna changamoto. Chuo cha Mpuguso cha Ualimu kina wanachuo 670, wapishi wapo wawili, kiuhalisia walitakiwa wapishi wawe watano mpaka sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hicho ni chuo cha Mpuguso nakisema kwa mfano halisia si mfano ni halisia ya hao watumishi hawapo ila na vyuo vingine yamkini vina mapungufu kama haya. Kwa hiyo, nilitamani sana kuhusu upande wa vyuo Serikali itizame watumishi namna ambavyo wapo na wanatakiwa kufanyaje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia chuo hicho kina wakufunzi wa sayansi wawili tu. Kiuhalisia walitakiwa wakufunzi wawe wanne kwa hivyo chuo kina upungufu wa wawakufunzi hao ninaomba sana Serikali itizame upungufu huo wa wawakufunzi kwenye vyuo, ili iweke uhalisia na mambo mengine yaweze kwenda sawa sawa na vile mpango unavyoenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mazuri Serikali inavyofanya uchakavu wa nyumba za watumishi. Kuna nyumba za watumishi lakini ni chakavu sana. Hivyo basi, nilikuwa naomba sana Serikali itazame hili namna ya kuboresha, kufanyia ukarabati nyumba za watumishi. Lakini pia bado azitoshelezi kuna uhaba, kuna uhaba wa nyumba za watumishi pale Chuo cha Walimu Mpuguso. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza Serikali namna ambavyo imeweka vyuo vya VETA. Haijatusahau hata pale Iyunga kuna chuo cha VETA lakini pia kuna Sekondari ya Iyunga, Sekondari ya Iyunga ni sekondari ya muda mrefu sana ni ya tangu mwaka 1925 lakini miundombinu yake si rafiki sana kwa sababu haijafanyiwa ukarabati. Najua hili ninaweza kwenda moja kwa moja TAMISEMI lakini kwa sababu tunaongelea mambo ya elimu na pale ni elimu inapatikana ya sekondari. Ninaomba sana, sana muiangalie shule ya sekondari ya Iyunga ambayo ni shule bora sana kati ya shule nyingi ambazo ziko vizuri. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Suma, kengele imeisha lia.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja hii ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ahsante kwa kunipa nafasi ya kuongea. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Ujenzi. Awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na uzima ambao nipo nao sasa hivi, nimepata nguvu ya kusimama, kuongea kwenye Bunge hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Waziri wa Ujenzi, Mheshimiwa Mbarawa pamoja na Naibu Waziri, kaka yangu Kasekenya; Mheshimiwa Naibu Waziri, kaka yangu Fredy Mwakibete; nawapongeza kwa kazi nzuri mnazozifanya na namna ambavyo mnazipitiapitia hizi barabara zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiomba kitu ukapewa unapaswa kushukuru. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan kwa namna alivyoguswa na barabara yetu ya Inyala. Ajali zilikuwa nyingi sana, akatutumia fedha kiasi cha shilingi 6,998,000,000 tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuokoa uhai wa watu wengi pale Inyara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ahadi ya awamu ya nne, ahadi ile ni ya barabara ya kutoka Katumba kupita Suma kwenda Mwakaleli, Ruangwa, Mbwambo mpaka Tukuyu Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile barabara ni muhimu sana, kwa sababu inapita barabara inatokea Rungwe inatokea Busekelo kule halafu inarudi tena Tukuyu Mjini. Naiomba sana Serikali, sijasikia hapa kwamba kuna fedha yoyote ambayo imetengwa kwa ajili ya barabara hiyo ya kutoka Katumba Suma - Mwakaleli kutokea Tukuyu Mjini. Hivyo, naomba kwenye mipango yenu ya bajeti msiisahau barabara hiyo kwa sababu tumeiomba kwa muda mrefu. Naishukuru sana Serikali kwa kipande kwa sehemu kuanzia Tukuyu Mjini kule imeanza kufanya kazi nzuri ya kuweka lami, ninaishukuru Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ambayo ilikuwa ni korofi sana Barabara ya Ibanda kwenda Itungi Port. Barabara hiyo ni muhimu sana ambayo inapitia Kyela Mjini. Naishukuru Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ni Sikivu, hiyo barabara mkandarasi yuko site inafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya kutoka Igawa kwenda Tunduma Mkoa wa Songwe. Ile barabara ni barabara muhimu sana. Zinapita gari ambazo zinakwenda kwenye border mbili; border ya kwenda Malawi na border ya kwenda Zambia. Ile barabara ni barabara ambayo ninaiongelea kila wakati hapa Bungeni. Ile barabara ni nyembamba ambayo inapitisha makontena ya 40ft, 20ft, pamoja na petrol-tank, lakini na mabasi yote yanapita hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile barabara ni nyembamba halafu ina corrugation ajali kila siku. Wananchi wa Mkoa wa Mbeya kwa tatizo la barabara ile, wengi wamekuwa walemavu, lakini wengi wamepoteza familia zao kwa ajali zinazotokea kutokana na barabara ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Serikali ilipokuwa inawasilisha hapa sijasikia hizo kilometa 181 kwamba ni lini itaanzwa kujengwa hiyo barabara. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, hiyo barabara ni barabara ambayo ina misiba, kila siku tunalia wananchi wa Mkoa wa Mbeya. Tumechoka kulia misiba. Pia walemavu wengi wanapatikana kupitia barabara ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, sijajua kwamba Mheshimiwa Waziri ile misiba ungekuwa unaona namna tunavyolia, ni kwa sababu huoni. Ungekuwa unaona, nakwambia ungepata uchungu kwamba ile barabara uipe kipaumbele. Naongea kwa uchungu kiasi kwamba natamani hata misiba wakati fulani tukiihamishia humu Bungeni kupiga yowe labda ndiyo Serikali itasikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa namna ambavyo imetenga fedha, ile barabara ya kilometa 29 ya Mbeya Mjini barabara nne. Pia namshukuru Mheshimiwa Rais, katuongezea kilometa nne zingine za kuanzia pale Uyole kwenda mpaka Mlima Nyoka. Mheshimiwa Waziri akiwasilisha hapa ameongea kwamba mkandarasi yupo ameishafika na andaa utaratibu. Wananchi wa Mkoa wa Mbeya hatuona kwamba ameshaanza huyo mkandarasi, kwa sababu hatuoni mitambo yoyote, tungeanza kuona mitambo imefika, hekaheka zimeishaanza za kuandaa juu ya barabara ile basi tungejua barabara ile imeshaanza rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa namna ambavyo umenipa hii nafasi, Kkuna barabara ya kutoka Makongorosi – Lupa mpaka Rungwa ile barabara ni kilometa 356 ni barabara muhimu ambayo inakwenda kuunganisha Mkoa wa Singida na Tabora. Ningeiomba sana Serikali angalau kwa kilometa 100 ingewekea bajeti ya kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya Rujewa – Madibila; barabara ya Rujewa – Madibila ni kilometa 92, ni barabara muhimu sana kule kuna mazao mengi, mazao ya kutosha ile barabara ni mbaya. Ninaomba sana Serikali kwa matamko mliyotamka hapa kwamba mnaitambua, naomba muiwekee bajeti ya fedha ile barabara ikikamilika kilometa hiyo 92 inakwenda kuunganisha na barabara kilometa 60 kutoka Madibila mpaka Mafinga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa namna ambavyo unavyoendesha Bunge letu hapa mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wastaafu ambao walistaafishwa Air Tanzania, wana kilio kikubwa sana, mwaka jana kuna fedha za waastafu ambazo tulipitisha hapa Bungeni, wastaafu wale wana kilio kikubwa sana, wafanyakazi ambao walikuwa wakifanyakazi ATC. Ninaomba usikie kilio cha wale watumishi wa Air Tanzania tangu walivyostaafishwa wengine miaka kumi mbili imepita hawajapewa mafao yao, wengine miaka sita na wengine wamekufa bila kupata fedha zao, ninaomba hili ulichukulie kipaumbele. Hawa watu mkiwafuta machozi yao, mkawapatia fedha zao za kustaafu basi watawashukuru sana, lakini sijajua ni nini kina zuia kama mwaka jana tulipitisha bajeti hapa mlisema ni za wastaafu ni kwa nini hamjawafikishia fedha zao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimshukuru na kumpongeza sana Engineer wa TANROADS wa Mkoa wa Mbeya Engineer Masige, amekuwa akisimamia vizuri sana hizi barabara za mkoani kwetu Mbeya, pongezi nyingi sana zimuendee Mheshimiwa Engineer Masige chini ya kiongozi mkuu ambaye ni Mkuu wa Mkoa wetu Homera.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Suma ahsante sana. Muda wako umeisha.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote nipende kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema nami niweze kuchangia Wizara hii ya Fedha kwa maana ya Bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye amekuwa Rais mwanamke wa kwanza East Africa. Ninampongeza sana hiyo ni heshima kubwa sana kwetu lakini pia amekuwa Makamu wa Rais wa kwanza Tanzania. Pongezi nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuridhia kuwa Dkt. Tulia Ackson agombee nafasi ya Urais IPU. Pongezi nyingi sana kwako Dkt. Tulia namna ambavyo unakwenda kugombea hii nafasi tunakuombea sana kwa Mwenyezi Mungu na Mwenyezi Mungu atasimama na wewe atakwenda kutimiza haja ya moyo wako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa. Alifanya kazi kubwa sana pale Dar es Salaam, alisimama kwa muda mrefu sana akiongea na wafanyabiashara. Yote hiyo ni kwa ajili ya kuweka nchi sawa sawa, kutengeneza amani, upendo na mshikamano. Alituliza mioyo ya wafanyabiashara wa Tanzania. Pongezi nyingi sana kwako Mheshimiwa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa Mwenyezi Mungu aendelee kuwa nawe katika majukumu yako popote unapokuwa awe pamoja na wewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaingia kuchangia kwenye Mpango huu wa Serikali. Nipongeze TRA, TRA wanafanya kazi nzuri ya kukusanya kodi ndipo ambapo maeneo mengi wanatimiza malengo yao ni kwa sababu ya utiifu na nidhamu waliyonayo wafanyabiashara kuchangia ama kulipa kodi kwa sababu wanajua kodi ndiyo maendeleo ya Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati fulani wafanyabiashara hawa wanapata changamoto hasa pale wanapokuwa wamejipanga na kujiandaa kwa ajili ya kwenda kulipa kodi kuna tatizo kubwa la mtandao kwa maana ya control number. Control number ni tatizo kubwa. Serikali kwa maana ya TRA wanakuwa na operation ya kukamata vyombo vya moto. Utakuta wamekamata bajaji, magari na wafanyabiashara wale wako tayari kulipa lakini anafika TRA mtandao unasumbua uko chini, wanakwama kulipa kwa wakati lakini bado wanaendelea kushikiliwa vyombo vyao kiasi kwamba wanashindwa kuendelea kufanya biashara kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na wakati huo kwa wafanyabiashara hawa wadogo wa bajaji inawezekana kabisa amekopa hiyo fedha kwa ajili ya kwenda kulipa. Sasa pale akikwama kulipa mtandao uko chini, control number inakwama kutolewa ndipo ambapo shida inapoanzia. Anauhitaji kwa ajili ya kutumia fedha kwa ajili ya familia yake lakini inashindikana sijajua, tatizo liko wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Jeshi la Polisi, Jeshi la Polisi akikamata gari akiona lina makosa, control number inatoka hapo hapo kwa kosa alilonalo anatakiwa alipie lakini nikiangalia na tukiangalia Watanzania kwenye Wizara hii ndiyo wenye kihenge, ndiyo mmeshika fedha zote za nchi. Mnashindwa nini kuboresha utaratibu TRA wa control number kutoka kwa wakati ili Watanzania walipe wakaendelee kufanya majukumu yao? Ni nini kinakwamisha hili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Mbunge wa Wanawake wa Mkoa wa Mbeya. Wakati fulani napata simu za malalamiko hata nje ya Wananchi wa Mkoa wa Mbeya. Nataka nitoe jambo hili ambalo nilipigiwa simu kutoka Dar es Salaam ni kero za wananchi. TRA wanakuwa na operation, siku moja walisimama TAZARA pale wakakamata gari ya mfanyabiashara, ile gari ilikuwa inaenda kupakia mzigo kwa bahati mbaya sana tajiri alikuwa hana taarifa kwamba ile gari inadaiwa kumbe kuna makosa ameyasababisha dereva ambaye wakati huo hakuwa kwenye hiyo gari. Tajiri yuko tayari kulipa hiyo fedha, anamwambia kwamba natuma hiyo fedha ilipwe sasa hivi muachie gari ikafanye kazi, TRA wanamwambia wanasema, “Hiyo gari lazima iende yard Tabata, ikipaki Tabata urudi hapa uende Vingunguti ndipo ukalipie kodi.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa muda wa nani, kwa gharama za nani na kule yard inatakiwa ikalipe kodi? Sasa mfanyabiashara huyu anachelewesha muda, yuko tayari kulipa na pale siyo majembe wapo ni wahusika wa TRA, maafisa wa TRA wako pale wanasema hawawezi kutoa control number kwa wakati, tatizo linakuwa wapi? Mbona Jeshi la Polisi linafanya haya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sisi wenye kihenge ambao ndiyo mnashika fedha za nchi kunakuwa na tatizo gani kulipa, kutoa control number papo kwa papo ili kazi zingine ziendelee? Nashauri sana Serikali mlitazame hili la ukusanyaji kodi, yamkini mapato mengine yanapotea kwa sababu ya kutokupokea fedha kwa wakati, kutokupokea mapato kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja ambalo kidogo imekuwa changamoto. Wafanyabiashara hawa ni wasikivu kwa kulipa kodi. Kuna tatizo moja, kaka yangu pale Mheshimiwa Waziri anafanya kazi nzuri sana. Mheshimiwa Dkt. Mwigulu anafanya kazi nzuri sana, kuna kipengele kimoja kaka yangu ninaomba sana utazame hili. Kuna hii service levy; service levy inakwenda kukata mtaji wa mfanyabiashara. Wafanyabiashara hawakatai kulipa service levy kwa sababu wanajua kodi ndiyo kila kitu. Ninaomba sana service levy mfanyabiashara analipa 0.3. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi, tunaomba yaani ingefaa angalau basi iwe 0.1 kulipa ni ndani ya Wizara yako hizo fedha zinakusanywa zinakwenda zote kwenye kihenge kimoja. Mkiliangalia hili kwa undani tunaomba msaidie hawa wafanyabiashara najua hili liko ndani ya TAMISEMI ndani ya upande wa leseni lakini hili jambo kwa sababu ni Serikali na huu ni mchango wa Bajeti ninaomba mkalitazame. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mwigulu Nchemba amefanya kazi nzuri sana pale alipokuwa akisoma na ipo kwenye maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amewaonea huruma sana, amewajali sana wafanyabiashara ameamuru wasifungiwe maduka yao badala yake wanatakiwa waelimishwe ili waende kulipa kodi. Kwa sababu mfanyabiashara huyu akifungiwa duka lake atatafuta fedha wapi za kwenda kulipa kodi.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeliona hili kwa undani sana.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina taarifa hapa.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaendelea nimekatishwa kidogo hapa maana mimi nilikuwa naendelea kufafanua namna gani umewatendea haki wafanyabiashara wa Tanzania. Mheshimiwa Mwigulu Nchemba umewatendea haki sana. Na mimi kwa niaba ya watanzania, wafanyabiashara ninakupongeza na kukushukuru kwamba hili umefanya vizuri hasa wafanyabiashara wa Mkoa wa Mbeya wanakwenda kufanya kazi zao bila kutishwatishwa bila vitisho…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Suma Ikenda Fyandomo, na muda wako umekwisha.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa muda ulionipatia lakini niseme kwamba Mungu abariki sana mpango huu, na ninaunga mkono hoja, ahsante sana, nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye Bunge lako tukufu kuchangia kwenye Wizara hii nyeti, Wizara muhimu sana ya akinamama. Awali ya yote ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais mama Samia Suluhu Hassan kwa kuunda hii Wizara muhimu sana kwa ajili ya wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanawake wa Tanzania nzima wanatambua sana na wanalijua hili, wanapokuwa wajawazito wanajua Serikali ipo, watajifungua salama na bila gharama yoyote. Kwa bahati mbaya sana kumezuka tatizo ambapo wanawake wanajifungua siyo wote, wanawake wengine watapata bahati mbaya ya kujifungua watoto wakiwa na mgongo wazi, wanawake wale wanakuwa hawajajiandaa chochote kuhusu masuala ya fedha kwamba watatokewa na hilo tatizo.

Lakini tatizo hilo mtoto akizaliwa ana mgongo wazi anapelekwa hospitali, anafanyiwa operation kwa gharama ya shilingi 500,000 mpaka shilingi 1,000,000 wanawake wale uwezo huo wanakuwa hawana. Ninaomba sana Mheshimiwa Waziri alichukue hili kwa umakini sana, hili tatizo ni la Tanzania nzima hasa wanawake wa Mkoa wa Mbeya wamepata matatizo makubwa sana juu ya kujifungua watoto wenye mgongo wazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitafurahi sana na nitashukuru endapo Mheshimiwa Waziri atalizingatia hili kuangalia namna gani watapunguziwa gharama ama kuimaliza kabisa gharama za matibabu hayo ya kutibu watoto hao. Ninaipongeza sana Serikali na ninaishukuru sana kwa namna ambavyo wametoa fedha kwenye halmashauri zetu zile asilimia 10. Ile asilimia 10 ni kwa ajili ya wanawake 4%, vijana 4% na kundi la walemavu 2%.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba kuishauri Serikali juu ya hili, ninaomba sana kwenye 10% ile iongezwe iwe 15%. Asilimia 15 kwa maana ipi? Asilimia 15 ili kwa wanawake maana wanawake wana majukumu mengi sana, wana mzigo mkubwa sana wa kutunza na kulea familia, ninaomba kwenye 15% hiyo 9% iende kwa wanawake, 3% iende kwa vijana, 3% iende kwenye kundi la walemavu. Ninamaanisha kwamba mwanamke hata mtoto mdogo maadamu amezaliwa ni mwanamke ni kama anaanzia majukumu yake hapo.

Mheshimiwa Spika, ninamaanisha kwamba kundi la vijana watoto wa kike nilikuwa naomba hao waingie kwa upande wa wanawake, nina maana kwamba mabinti hao wakiingia kwenye kundi la wanawake mpaka sasa hivi hiyo fedha inaonekana kama ni ya 4% ni ya wanawake, lakini pia tunakuwa na mabinti huko ndani, kwa hivyo wasichana waingie kwenye kundi la wanawake kwenye mkopo huo ambapo 9% iwe wanawake wakijumuisha na mabinti, vijana lakini vijana ambao ni wa kiume wapate 3% ninamaanisha kwamba mama endapo atasikia mtoto wake anaumwa ambaye ni kijana, mama ndiyo anashughulikia mwanzo mwisho, siyo kwamba atam-charge kijana kwamba nipe fedha zako....

SPIKA: Mheshimiwa Suma kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jackson Kiswaga.

T A A R I F A

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, ninapenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba katika lile kundi kubwa la vijana, pia wapo akinamama humo na nina wasiwasi aina ya mchango huu wakati mwingine unaweza ukatugawa namna unavyowasilishwa kwa sababu pia kundi la vijana ni kubwa, lakini ndani ya vijana pia wapo wakinamama humo. Kwa hiyo ndiyo hiyo nilipenda kumpa taarifa ahsante sana.

SPIKA: Ndiyo maana niliacha amalizie ile hoja yake kama umemsikiliza vizuri anataka hiyo asilimia iongezeke halafu hao mabinti waondolewe kwenye hiyo 4% wanayopewa pamoja na vijana wengine waingie kwenye wanawake. Kwa hiyo, ukitaja wanawake wote wawe kundi moja, ndiyo hoja yake ndiyo maana nilitaka umsikilize amalize halafu ndiyo umpe taarifa.

Kwa hiyo, hoja yako wewe ndiyo ambayo kidogo inaweza ikaleta mushkeli yeye anaenda na hoja yake ya kuongeza asilimia.

Mheshimiwa Suma Ikenda Fyandomo.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa ufafanuzi huo na hilo ndiyo lilikuwa lengo langu sana kwamba vijana wa kiume watakapokuwa wamebakiwa na hiyo 3% naamini itawatosheleza sana kwa sababu tutakuwa tumeondoa kundi kubwa la vijana kwa maana mabinti zetu kuingia kwenye kundi la akinamama.

Ninasema hivi kundi la wanawake liongezewe asilimia hizo kwa sababu mama anabeba majukumu mengi sana. Anabeba majukumu ya baba, anabeba majukumu ya hao vijana, anabeba majukumu ya watoto wote kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, mama ana huruma sana kwa watoto kwa baba kwa wamama na kwa kila mtu hivyo basi nitashukuru sana hili likichukuliwa uzito kwamba wapewe akinamama kwa maana ya 15%; ninaomba sana mumshawishi, mshauri hizo halmashauri iongezeke iwe asilimia 15 nasisitiza 9% iwe kwa wanawake, 3% kwenye kundi la vijana wetu lakini 3% kwenye kundi la walemavu nitashukuru sana hili kama litabebwa kwa uzito.

Mheshimiwa Spika, kuna tatizo kubwa sana hapa nchini hasa kwetu mkoa wa Mbeya, anapokuwa akiishi ama wakioana baba na mama wanaishi pamoja, wanaanza kutafuta tangu shilingi moja pamoja baba na mama, lakini mwisho wa siku ikatokea mama ametangulia mbele ya haki baba atasononeka yeye pamoja na familia, lakini maisha yataendelea atakuwa tu burudani raha mustarehe hasumbuliwi na mtu yoyote.

Mheshimiwa Spika, lakini ikatokea amefariki baba ghafla kwa maana ya mume shida inaingia kwenye familia, shinda inaingia kweli kweli, anajitokeza baba hafahamiki kwenye hiyo familia anasema mimi ndio baba mkubwa, mimi ni mdogo wake, mimi ndio natakiwa niwasimamie, kwenye kusimamia mali kuzitafuta walikuwa tu baba na mama na watoto wao wakimuomba Mungu wafanikiwe kwenye hiyo familia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini watu wanajitokeza from nowhere, watoto hawa hawawajui wanasema unasikia mimi ndio baba yako mkubwa, mimi ndio baba yako mdogo hawawafahamu wametokea wapi? Mbona akifariki mama hawa watu hawajitokezi kuja kumbuguzi baba kwenye hiyo familia. (Makofi)

Nilikuwa ninaomba sana kule kwetu Mkoa wa Mbeya wanawake wajane wanasumbuliwa sana na haya, hivyo basi nilikuwa naomba sana kushauri Serikali ijaribu kuweka kama sio kuweka moja kwa moja kwa maana ya kutokujaribu, iweke mawakili kila Halmashauri ambao watakuwa wanawasaidia wanawake wajane ambao wanapatwa na matatizo kama haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii sheria naona iliangalia upande mmoja, unajua kwenye familia yamkini mama ndio mtafutaji mkubwa, baba ni msimamizi sawa kama kiongozi mkubwa kwenye hiyo familia, lakini akifariki baba ni shida, ni shida ni shida. Hivyo basi hiyo sheria kama ilikuwa imewekwa miaka ya nyuma sana kwamba baba ndio hatakiwi kusumbuliwa endapo mke atakuwa ametangulia mbele ya haki, hiyo sheria naomba ibadilishwe, hiyo sheria naomba ibebe uzito kote kote kwamba mama na baba wanakuwepo pale wanakuwa wanatafuta fedha pamoja, kwa ajili ya familia hivyo basi asisumbuliwe mwanamke yeyote pindi baba atakapokuwa ametangulia mbele ya haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanawake wana majonzi makubwa sana, naona taa umeiwasha.

SPIKA: Muda umeisha.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, nilikuwa nimalizie kidogo.

SPIKA: Sekunde 30 malizia.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana hivyo basi nitashukuru sana kama Serikali italichukulia hili kwa uzito mkubwa kuangalia mama anavyoteseka, mama anavyosumbuliwa na Mheshimiwa Rais ameunda hii Wizara kwa makusudi mazima kabisa ili tuendelee kuwatetea wanawake hapa ndani na katika kuwatetea hawa wanawake ninaomba mlibebe muwasaidie wanawake wanaoonewa pindi wanaume zao wanapokuwa wamekufa…

SPIKA: Haya ahsante sana.

MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, maana analia mara analia mara mbili analia msiba wa baba/wa mme wake analia msiba wa kupokonywa mali zake zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia kwenye Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninapenda sana kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa mara nyingine tena, kwa namna ambavyo aliweza kuunda Wizara ya wanawake, jinsi na watu ambao hawajiwezi, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Nimesimama hapa kuomba kuongezewa fedha kwenye asilimia 10. Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, Kaka yangu, ‘Kalumbu’ ulikuwepo nilipochangia hapa kwamba ninaomba sana ile asilimia 10 niliyoiweka kwa ajili ya kusaidia, asilimia Nne wanawake, asilimia Nne vijana na asilimia Mbili watu wenye ulemavu. Niliomba sana kwa dhati ya moyo wangu, kwamba wanawake wana majukumu mazito sana. Majukumu mazito kwa maana ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wewe naamini ni shahidi, mtoto akizaliwa wa kike kitu cha kwanza unamuita mama, umekuja, unamfurahia unamuita mama. Tayari ameshajiunganisha kwenye majukumu, nilitegemea hapa ombi langu la kuongezewa asilimia nyingine badala ya asilimia 10 waweke 15 ambapo asilimia tisa iende kwa wanawake kulingana na majukumu yao, kwenye asilimia hizo ni kwa sababu wanawake hao ndiyo hao hao wajasiriamali, ndiyo hao hao machinga, ndio haohao ambao wanatunza familia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri anavyokuja hapa kuhitimisha alichukulie uzito sana suala la wanawake. Wanawake wana majukumu mazito. Vijana hapa ambapo wanakuwa wanapata hiyo mikopo, akipata tatizo wa kwanza kuhangaika ni mwanamke ambaye ni ama mama yake au dada yake, lakini hatamwambia kwamba naomba fedha ya kukuuguza hospitali, hatamwambia hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa kilio cha Wabunge wote amekisikia, kuhusu kutokuondoa asilimia tano kwenye asilimia 10. Naomba iongezeke, badala ya asilimia 10 iongezeke iwe asilimia 15, Tisa kwa wanawake, Tatu kwa vijana, Tatu kwa watu wenye ulemavu kulingana na majukumu waliyonayo wanawake. Hata mabinti hawa niliomba kwamba mpaka sasa hivi kwa sababu ni wanawake wameshaunganishwa huko, wanakopa fedha kupitia Mfuko huo wa Wanawake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitashukuru sana endapo hapa Mheshimiwa Waziri atalisemea hili, kwamba amebadilisha msemo wake ule wa kuondoa hata asilimia tano, bali ataongeza asilimia nyingine tano ili asilimia tisa iende kwa wanawake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanawake wa Tanzania hasa wanawake wa Mkoa wa Mbeya Wilaya za Kyela, Rungwe, Mbarali, Chunya, Mbeya Mjini na Mbeya Vijijini, wanawake wajane wa Taifa hili wanasumbuliwa sana. Ninaomba sana kwenye hili Serikali iwaone wanawake. Wanapokuja kuhitimisha ninatamani kama inawezekana ile sheria ya kusema mama anapofiwa na mume anasumbuliwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema hapa juzi, imenipasa nirudie kwa sababu baada ya mchango ule nilipotoka nje hapa kumbe kulikuwa na wageni wengi sana wanawake na kati ya wale wengi sana walikuwa ni wajane. Walijitokeza wanawake kuja kunisalimia na kunishukuru sana juzi nilivyowasemea wanawake wajane wa Tanzania hii. Mama mmoja nilipata uchungu sana, kati ya wale wanawake waliokuja kunishukuru, wanawake Wanne walikuwa na kesi Mahakamani za kudhulumiwa zao. Mmoja akaniambia, Mheshimiwa naomba samahani namba yako ya simu, mimi mume wangu nimeishi nae miaka 16 lakini amefariki, kesi ninayo Mahakamani. Baada ya kufariki anakuja Baba yake mdogo anasema mimi hii nyumba lazima iwe mali yangu niimiliki kwa sababu mume wako mimi ndiye liyemtafutia kazi! Ni uonevu wa hali ya juu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba Serikali ichukulie kwa uzito kilio cha wanawake Tanzania nzima, hasa Mkoa wa Mbeya. Wanawake wengi sana hata kabla ya nafasi hii mimi kuwa Mbunge, walikuwa wakija kulia getini kwangu wakiniomba msaada, nilikuwa nikiwasaidia ili wapate haki zao waweze kusaidia watoto wao na familia zao. Nitashukuru sana kama nimeeleweka juu ya hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hili jambo la TCRA. Kwenye Nchi yetu ya Tanzania tumeendelea sana kwa mawasiliano. Sasa hivi mfanyabiashara anakuwa yuko Mbeya, ameingia mteja dukani anahitaji kifaa yeye hana, anapiga simu dukani, anapiga simu Dar es Salaam anakipiga picha anauliza kama kifaa hicho kipo. Ni ndani ya dakika moja jawabu limepatikana na anaweza kukiuza kifaa kile. Mtu anasafiri anaweza akawa yuko Uturuki, anapiga picha vitu ambavyo amevikuta, mali mpya kule Uturuki, anauliza huku maduka ya Dar es Salaam; Je, nikileta hivi ili tuweze kuuza, je tutauza? Ndani ya dakika moja jibu vinapatikana, lete kwa wingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi vifungu wanavyosema viondolewe kwenye TCRA, hivyo vifungu vitaturudisha nyuma, mawasiliano yatapotea, yataisha, tutarudi nyuma. Ishu ya kidigitali hii itakuwa ni historia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake tumeingia kwenye mfumo wa kidigitali lakini matokeo yake tunaambiwa kwamba hivi vifungu viondolewe; TCRA watakuwepo kama nani, watakuwa wanafanya shughuli gani? Tutakuwa tumewaondolea kufanya kazi watu wa TCRA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sijui mlikaa na TCRA lini na wapi mkafikia mwafaka wa haya, lakini kwa vifungu vya sheria jinsi ambavyo tumevichanganua haitawezekana TCRA ikafanya kazi kwa ufanisi endapo vifungu hivi vitaondolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mawasiliano sasa hivi kwa jinsi ambavyo yamekuwa yametuletea, wakati fulani unaweza ukawa una mawazo yako, una mambo mengi kichwani kulingana na hali ya maisha, lakini wakati mwingine unaona kwamba hebu nishike hii simu nijaribu kupata furaha yangu. Ukishika simu utacheka wakati umekasirika, utapata furaha pale, utapunguza stress, utapunguza maradhi, utatoa sumu ya mawazo kwenye mwili wako kwa kucheka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunakotaka kwenda, tukitoa vifungu hivi vya TCRA, vifungu vya sheria, tunakwenda kupoteana. Tutarudi kulekule, ukitaka kufungua mtandao ndiyo ukae baada ya siku moja, mbili au tatu, hatupendi Watanzania turudi nyuma, tunahitaji tusonge mbele kwa ajili ya maendelea ya nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, kulikuwa na kilio kikubwa sana cha wazabuni ambao ni ma-supplier Serikalini, wengine walikuwa wanadai madeni ya hata miaka 20 iliyopita, lakini Mheshimiwa Rais, Mama Samia, baada ya kuliona hili alituma fedha na baadhi yao walipunguziwa mzigo, nadhani yuko kwenye mchakato, ataendelea nalo hili. Ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa haya anayoyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya Watumishi wa Serikali ni wazembe, wanatengeneza madeni wao wenyewe kwa uzembe wao. Baadhi yao wanafanya kazi nzuri, baadhi yao ni wazembe wanaiangusha Serikali. Fedha zinakuwepo kwenye akaunti, wanaagiza vifaa kwa supplier, akishaagiza fedha zipo lakini anafanya uzembe wa kumlipa supplier, mwisho wa siku zile fedha unaingia mwaka mpya wa Serikali zinavutwa zinakwenda Hazina, kuja kurudi ni ndoto. Hilo linakuwa linaunda madeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan nilimsikia hapa akisema Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu, alieleza kwamba wameacha utaratibu kuanzia sasa hakutakuwa na kurudishwa fedha. Fedha zilizoingizwa kwenye Halmashauri zetu, zilizoingizwa Serikalini kwa ajili ya kazi, zitabaki huko bila kurudi kule Hazina. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa sababu ameondoa kilio cha wafanyabiashara walio wengi ndani ya hii nchi. (Makofi)