Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Regina Ndege Qwaray (15 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa nafasi uliyonipa. Nami niungane na wenzangu kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi aliyonijalia hadi siku ya leo nimeweza kuwepo hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee pia nikishukuru chama changu kwa kuniteua na kunipendekeza katika ngazi zote na hatimaye leo niko hapa. Pia niwashukuru kwa namna ya pekee sana akina mama wa Mkoa wa Manyara kwa imani kubwa waliyoonesha juu yangu na kuniona natosha kuwa mwakilishi wao katika Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee niishukuru pia familia yangu; mume wangu na watoto wangu ambao wamekuwa bega kwa bega na mimi muda wote wa mchakato na hata sasa wamekuwa wavumilivu kipindi chote ambacho niko katika majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee, niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa iliyoifanya kwa miaka mitano ya kuhakikisha Tanzania inasonga mbele kimaendeleo. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli, kwa hotuba nzuri iliyosheheni matumaini kwa Watanzania ambayo inaonesha dira kwa nchi yetu. Kwa namna ya pekee, tunamwomba Mwenyezi Mungu aendelee kumjalia afya njema, busara na hekima ili yale yote aliyoahidi na aliyoyasema katika hotuba yake yaweze kutekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijikite katika kipengele cha elimu. Kwanza niipongeze sana Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi ambayo imeona ni vyema kuwa na Watanzania wenye elimu na kuhakikisha kila mtoto wa Kitanzania ambaye ana umri wa kwenda shule anaweza kwenda shule na kupata elimu bure kuanzia darasa la awali mpaka kidato cha nne; si kazi rahisi. Ndugu zangu, Tanzania imesonga mbele. Ukiangalia miaka ya nyuma waliokuwa wanapata elimu walikuwa wachache sana lakini leo kila Mtanzania ana uhakika wa kupata elimu na anasoma bure. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na jitihada zote za Serikali bado tuna changamoto ndogo ndogo ambazo Serikali yetu inapaswa ione kwa jicho pevu kwamba bado tuna miundombinu mibovu, madarasa ni machache msongamano ni mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuna upungufu mkubwa wa madawati na wataalam kwa maana kwamba walimu ni wachache. Kuna shule ambazo wanafunzi ni wengi darasani, unaweza kuwa na wanafunzi 200 lakini walimu ni wachache sana. Kwa hiyo, uwiano kati ya mwalimu na mwanafunzi bado haujazingatiwa. Hii inabidi Serikali iangalie uwiano huo ili utendaji kazi kati ya ufundishaji na ujifunzaji uwe mrahisi na wanafunzi wetu waweze kufanya vizuri huko madarasani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nashauri Wizara hii ya Elimu iangalie upya mtaala wa elimu unaotumika. Elimu yetu inayotolewa kwa sasa haimuandai mwanafunzi kwenda kusimama mwenyewe na kujitegemea. Kwa hiyo, napendekeza Wizara ione namna gani elimu inayotolewa kwa sasa inaweza kumuandaa mwanafunzi ili aweze kujitegemea. Kwa maana ya kuboresha vyuo vya ufundi, wanafunzi wapate ujuzi wa kutosha ili waweze kujianzishia maisha kwa maana ya kuwa na ujuzi wa kwenda kujitegemea na kuanzisha ujasiriamali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo basi nashauri Serikali iboreshe vyuo vya ufundi vilivyopo, lakini ihakikishe inaanzisha vyuo vya ufundi katika kila wilaya vikiwa na taaluma na ujuzi ambapo kila mwanafunzi anaweza kupata ujuzi tofauti tofauti. Kwa hiyo, wanafunzi wetu wanapomaliza kidato cha nne ni vyema akaamua kujichagulia kuingia kidato cha tano na cha sita ama kwenda kwenye vyuo vya ufundi kujipatia ujuzi hatimaye aweze kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo Wizara ya Elimu inapaswa sasa kuanzisha au kusimamia kuwepo na kitabu kimoja cha kiada. Kwa maana kwamba tuwe na kitabu kimoja cha kiada kuanzia shule za msingi za Serikali pamoja na shule za msingi za binafsi. Hii itasaidia kuwa na uniformity katika elimu badala ya kuwa na vitabu tofauti vya kiada mwisho wa siku wanafunzi wanafanya mtihani unaofanana lakini wakiwa wanawezeshwa kwa kutumia vitabu tofauti tofauti. Angalizo kwa Serikali pia iangalie vitabu vinavyotumika katika shule za private viwe na ithibati za Kamishna wa Elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais mama yetu mpendwa kwa kusikia kilio cha wananchi. Nampongeza pia Waziri wa Fedha na wasaidizi wake kwa kutuletea bajeti nzuri inayokidhi mahitaji ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia natoa pongezi kwa Serikali kusikia kilio cha bodaboda, Madiwani, Watendaji wa Kata na Vijiji. Ushauri wangu kwanza Serikali ipange maeneo ya kutosha ya kilimo na kupunguza au kuondoa migogoro kati ya wakulima na watumiaji wengine wa ardhi (matumizi bora ya ardhi) ili kupunguza migogoro kati ya wafugaji na wakulima ambayo pia imekuwa kikwazo kati ya wafugaji na wakulima katika ustawi wa maendeleo ya sekta ya kilimo na mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingi tumeona makundi haya mawili kuwa na uhasama mkubwa. Mipango ya matumizi bora ya ardhi yaainishwe kwa mpango wa ramani ili kila mmoja ajue mipaka yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, masoko endelevu ya mazao; wakati tunapitisha bajeti ya Wizara ya Kilimom, Waziri alisema tunataka Bunge hili la Kumi na Mbili liwe la mapinduzi, naishauri Serikali ihakikishe inatafuta masoko ya uhakika ya mazao ya wakulima wetu. Wakulima waruhusiwe kuuza nje ya nchi na masoko mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, bajeti ya Wizara ya Kilimo ya shilingi bilioni 294.1 ni ndogo sana, Serikali ijipange kwa bajeti zijazo kuongeza bajeti ya Wizara ya Kilimo angalau ifike asilimia tano ya bajeti yote kwani kutokana na ufinyu maeneo haya huathiriwa na upungufu wa wataalum, zana za kilimo /vyombo vya usafiri na OC na kutokuwepo kwa mashamba ya kuzalisha mbegu ndani ya nchi hali ambayo pia itafanya mkulima kupata pembejeo za kilimo hususan mbegu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Afya. Awali ya yote napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyoendelea kuboresha sekta hii ya afya ili afya ya wananchi wetu iendelee kuimarika. Nasema haya kwa sababu tumeona ni jinsi gani Mheshimiwa Rais ameendelea kuboresha afya ya wananchi hata kwa kusogeza huduma katika makazi ya wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hilo tu, Mheshimiwa Rais ameongeza jitihada ya pekee kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma hapa nchini badala ya kusafiri kwenda nje ya nchi kuendelea kupata huduma za afya. Kwa namna ya pekee nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Ummy na Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Wizara kwa ujumla, kwani wamekuwa washauri wazuri kwa Rais, lakini wameendelea kumsaidia kufanya kazi kwa bidii, kumsaidia Rais ili afya ya wananchi iendelee kuimarika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nisipotoa shukrani kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan nitakuwa sijatenda haki. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutuletea CT-Scan katika Hospitali yetu ya Mkoa wa Manyara. Kabla hatujaletewa CT-Scan katika hospitali yetu, wagonjwa walikuwa wakihangaika kwenda Hospitali ya Benjamin Mkapa, KCMC na wakati mwingine walikuwa wanaenda Muhimbili, lakini hivi sasa huduma inatolewa pale mkoani, wananchi wetu wanapata huduma kwa ukaribu na pia imewapunguzia gharama ya kusafiri umbali mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutujengea jengo la OPD. Bahati nzuri alikuja Rais mwenyewe akalizindua jengo lile na sasa hivi linafanya kazi vizuri. Pia namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutujengea jengo la Radiology, na jengo la ICU pamoja na damu salama. Hapa naomba sasa, majengo haya ya ICU na Damu Salama hayajakamilika. Namwomba Mheshimiwa Waziri atupelekee pesa pale Mkoani Manyara ili jengo hili liweze kukamilika na liweze kufanya kazi kama ilivyopangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutupatia jengo la wagonjwa wa dharura na tayari limeanza kufanya kazi, wagonjwa wanapata huduma. Pia hospitali yetu ya mkoa kulingana na wingi wa watu katika mkoa, hatuna watumishi, waliopo ni wachache sana. Tuna watumishi 250, tunahitaji watumishi wafike 468 ili hospitali hii iweze kutoa huduma vizuri. Tunaposema huduma ya afya inalegea, ni pamoja na kutokuwa na watumishi wa kutosha katika hospitali. Kwa hiyo, mkituongezea watumishi, tunaamini huduma itatolewa vizuri na wagonjwa wataendelea kupata huduma, itawapunguzia wagonjwa kwenda kutafuta wataalam katika hospitali nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, naombe Wizara ituletee daktari bingwa wa magonjwa ya watoto, daktari bingwa wa magonjwa ya mifupa, madaktari bingwa wa macho, daktari bingwa wa usingizi na daktari bingwa wa mionzi. Mheshimiwa Waziri aone ni namna gani tuna upungufu mkubwa kwa sababu hatuna madaktari bingwa katika hospitali yetu. Kwa hiyo, akitupatia hao madaktari, tutakuwa na uhakika kwamba wagonjwa wetu watapata huduma kwa ukaribu na huduma sahihi kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, pamoja na kwamba hospitali yetu imeanza toka 2008, tunaishukuru Serikali imeendelea kuleta fedha siku hadi siku. Kila mwaka katika bajeti ya Serikali tumeendelea kuletewa fedha. Naomba, kuna upungufu mkubwa wa wodi. Hatuna wodi ya wanawake, wodi ya wanaume na wodi ya watoto. Ukiwa huna wodi hizo, moja kwa moja ujue kwamba hospitali yetu haijakamilika bado. Kwa hiyo, naiomba Serikali ituletee fedha kwa ajili ya kukamilisha au kujenga hizo wodi ili wagonjwa waweze kuhudumiwa pale na waweze kupata huduma ya malazi kama wagonjwa ambao wanatakiwa kulazwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, naomba gari kwa ajili ya uendeshaji katika hospitali yetu ya mkoa. Ili kuendelea kutoa huduma hizi katika maeneo mengine, basi ni vyema hospitali ikapata huduma hizi ili huduma za afya zitolewe kwa ukamilifu zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusemea hospitali yangu ya mkoa, niende moja kwa moja kwenye changamoto ambayo naiona siyo kwa mkoa wangu tu, bali katika maeneo mengi; suala zima la vifaa. Utakuta katika maeneo mengi vifaa tiba au vifaa vile vya vipimo vinaharibika, lakini vinachukua muda mrefu kutengenezwa. Mfano, unapoongelea X-Ray, inaharibika, na CT-Scan inaharibika, lakini haitengezwi. Wagonjwa wanaenda hospitalini hawapati huduma, hawapati vipimo kila akienda anaambiwa kifaa kimeharibika, anaenda wiki inayofuata, kifaa kimeharibika. Kwa hiyo, hii imeleta usumbufu katika maeneo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe tu mifano hai. Kwa mfano, tuna hospitali yetu hapa ya afya ya akili ya Mirembe. Tunapozungumzia hospitali ya magonjwa ya akili, moja kwa moja kifaa kinachoitwa EEG ni kifaa muhimu sana katika hospitali, lakini jambo la kushangaza ni miezi karibia sita tunaelekea miezi saba hospitali ile haina kipimo hicho cha EEG. Sasa hebu fikiria, mgonjwa anatoka mkoani, analetwa hospitali, hapati kipimo, anatibiwaje? Zaidi tumesema ni hospitali special kwa ajili ya magonjwa ya akili. Kwa hiyo naombe Serikali iliangalie hili, kwa sababu tusipoliangalia wagonjwa watalundikwa pale hospitalini, hawapati matibabu na hawapati vipimo sahihi. Kwa hiyo, madaktari watapima kulingana na maelezo, badala ya kupima na kujua tatizo hasa ni nini? Kwa hiyo, naomba sana, vifaa tiba vinapoharibika, ni lazima Serikali ichukue jukumu la haraka sana ili vifaa vile vitengenezwe kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa tunayoiona ni kwamba, vifaa vile vinashindwa kutengenezwa kwa sababu hatuna wataalam wa kutengeneza vile vifaa katika vituo hivyo. Kwa hiyo, niombe wizara ijipange ni namna gani kuhakikisha wakipeleka vifaa tiba, pale pale kuwe na mtaalam wa kutengeneza vile vifaa pindi vinavyoharibika. Wapo vijana wetu waliomaliza vyuo wamemaliza mafunzo DIT wamekaa mtaani. Serikali kwa nini isiwatumie wale vijana wakawepo kwenye vituo au hospitali zetu za referral ili kifaa kinapoharibika tu, iwe rahisi kutengenezwa na huduma kuendelea kutolewa kwa wakati? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, kuna changamoto ya ukosefu wa madawa. Pamoja na kwamba Rais amefanya kazi kubwa sana kujenga vituo vingi vya afya, lakini bado madawa kule ni changamoto, hasa maeneo ya vijijini. Kwa hiyo, naomba Wizara ilichukue hili kuhakikisha kwamba wagonjwa wanapoenda katika vituo vyetu vya afya wanapata madawa muhimu yale ya binadamu ili watu wasipate tena usumbufu mwingi wa kutembea hapa na pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nilizungumzie na nilishawahi kulizungumzia hapa Bungeni, ni suala zima la Sera ya Huduma Afya ya Mama na Mtoto. Wamama wajawazito bado wanapata changamoto wanapoenda kujifungua, kwa sababu mama anatakiwa abebe vifaa yenye mwenyewe kama gloves, pamba na vitu vingine ambavyo vinahitajika wakati wa kujifungua. katika vituo vyetu vya afya na maeneo mengine, hasa katika jamii zetu za kifugaji na umbali wa kwenda hospitali inawalazimu wale wamama kujinyima baadhi ya vyakula ili mtoto awe mdogo tumboni ili aweze kujifungulia nyumbani badala ya kwenda hospitali. Sasa matokeo yake watajifungua watoto ambao hawana afya na ambao hawajatimiza umri kwa kuwa amekosa virutubisho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya yanachangiwa na gharama za hospitali. Hizi gharama kuna familia nyingine hawaziwezi kabisa. Kwa hiyo, naomba sera ya afya ikasimamiwe. Sera ya afya ni kwamba mama anapoenda kujifungua, basi apate zile huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukija kwa mtoto mdogo wa umri chini ya miaka mitano, naomba sasa Wizara pia iliangalie hili, kwa sababu wapo watoto wadogo ambao familia zao ni duni pia, wanashindwa kugharamikia matibabu. Kwa hiyo, Serikali ione ni namna gani ya kuendelea kuwahudumia wale watoto kwa kuwapatia huduma ya afya ili waweze kuishi kama binadamu wengine ambavyo tunaishi kwa sasa. Kwa hiyo, naomba sana Wizara iweze kusimamia sera hii ili Watanzania waendelee kupata huduma hii na afya ya wananchi wetu iendelee kuimarika.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hii ili nami niweze kuchangia katika Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumpongeza Waziri wa Fedha kwa taarifa yake nzuri aliyoianda. Pia niipongeze Kamati ya Bajeti kwa kuandaa vizuri taarifa yao. Kwa namna ya pekee pia, niipongeze Serikali hii ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa inayofanya kuhakikisha Tanzania inazidi kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite katika sekta ya kilimo. Kilimo ni msingi wa uchumi wa viwanda na uti wa mgongo wa Taifa letu. Wananchi wengi wa Tanzania tunategemea kilimo ili kujikwamua kiuchumi, hasa wananchi wa vijijini wanategemea kilimo kujipatia mahitaji yao. Mwananchi wa kijijini anategemea kilimo kusomesha mtoto, kupata mahitaji yake ya msingi ikiwemo afya, yaani kilimo ndiyo kila kitu kwake. Pamoja na hayo yote bado wanakumbana na changamoto nyingi ikiwemo soko kwa maana kwamba baada ya mavuno, wananchi hawana soko la uhakika. Wanavuna lakini mwisho wa siku mazao yao hayapati soko kama inavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kilimo wanacholima kwanza kinakuwa hakina tija. Wanatumia vitendea kazi vilivyopitwa na muda. Akina mama wengi wa kijijini wanajihusisha sana na kilimo lakini hawana vitendea kazi vinavyowarahisishia kufanya kilimo kile kuwa chepesi zaidi. Hivyo inakuwa vigumu sana kupata tija au kupata manufaa kupitia kilimo. Wamama hao leo wanahangaika kutumia jembe la mkono katika kilimo, hawawezi kulima mashamba makubwa hivyo, wameishia kulima mashamba madogo madogo ambayo sasa mazao wanayoyapata ndio hayohayo wanatumia katika chakula na katika mahitaji mengine, mwisho wa siku wanaendelea kudhoofika kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo bado naendelea kushauri Serikali kuona ni namna gani watainua sekta hii ya kilimo ili wananchi wetu wa vijijini waweze kujikwamua kiuchumi. Kwanza nishauri Serikali iwekeze katika utafiti wa mbegu tunazozitumia. Mbegu zetu nyingi tunazotumia zinatoka nje ya nchi, asilimia kubwa mbegu za mahindi na mbogamboga hazizalishwi hapa nchini hivyo, husababisha wananchi kutumia gharama kubwa kupata mbegu na kutumia mbegu ambazo sio bora katika kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nashauri Serikali ifundishe wakulima wetu kuhifadhi na kusindika mazao ili waweze kuuza bidhaa badala ya malighafi. Pia nishauri pia Serikali kujenga mabwawa ya kuvunia maji ili kuboresha scheme za umwagiliaji. Mfano, katika Wilaya ya Babati kuna Vijiji vya Shauri Moyo, Masware, Kisangaji, Bonde la Kiru, Madunga, Narkash, vyote vinategemea kilimo cha umwagiliaji, lakini hawana uwezo mkubwa au teknolojia ya kutosha kuvuna maji ili waweze kuendesha kilimo cha umwagiliaji katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wengi hawana elimu ya kutosha. Hawaelewi ardhi yao wanayoitumia ni mazao gani hasa yanastawi, hivyo wanastawisha mazao ambayo wakati mwingine hayaendani na maeneo yao. Maafisa Ugani katika maeneo yetu bado ni wachache sana. Niishauri Serikali kuongeza Maafisa Ugani katika kila kijiji ili waweze kuwaelimisha wananchi wajue ni mazao gani yanastahili kustawishwa katika maeneo yao, lakini pia waweze kutoa shamba darasa. Yale mafunzo ya shamba darasa yanasaidia wananchi kuona kwa vitendo ili waweze kuzalisha mazao yale yanayoendana na maeneo yao na pia yaweze kuwaletea tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri pia vyuo vya kilimo viboreshwe. Vyuo vyetu vya kilimo haviendi kulingana na ukuaji wa teknolojia. Bado tunatumia mbinu zile za zamani katika kuwapa mafunzo wale wataalam wa kilimo ambao wana kazi ya kwenda kuwaelimisha wakulima hawa, ili waweze kuzalisha mazao kwa kiwango kikubwa. Mfano, Chuo cha Sokoine nashauri Serikali ione ni kwa namna gani kiendelee kubaki na kutoa taaluma inayohusiana na kilimo, uvuvi badala ya kujikita katika kutoa fani ya ualimu. Kama inavyotambulika ni Chuo cha Kilimo, kibaki katika kutoa fani ya kilimo badala ya kujishughulisha na fani nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, katika Mkoa wetu wa Manyara, tunaomba Chuo Kikuu cha Sokoine kuanzisha shamba darasa katika mkoa wetu, ili wananchi wa mkoa ule waweze kufaidika na mafunzo ya kilimo na mwisho waweze kulima kilimo chenye tija na kufaidika na kilimo hatimaye kuleta maendeleo na mapinduzi katika viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nishukuru kwa nafasi uliyonipatia niweze kuchangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Nami niungane na wenzangu katika kuwahakikishia Watanzania kwamba nchi yetu ipo katika mikono salama ya mama yetu, Samia Suluhu Hassan. Matumaini makubwa Watanzania waliyonayo kwa mpendwa wetu, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, na kazi kubwa aliyokuwa ameifanya katika nchi hii, niwahakikishie kwamba Tanzania kamwe haitafutika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Taifa lolote linapozungumzia maendeleo au vipaumbele vya nchi katika maendeleo ya wananchi wake pamoja na kiuchumi, kamwe huwezi kuacha kuzungumzia suala zima la elimu. Mabadiliko ya mtaala wa elimu 2005 yaliyofanyika yalisisitiza Masomo ya Stadi za Kazi na TEHAMA yafundishwe kikamilifu katika shule zetu za msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, masomo haya yalikuwa na nia kubwa sana ya kuwandaa wanafunzi wetu kutoka shule za msingi kupata stadi mbalimbali ambayo ingewawezesha wenyewe waweze kuja kupata maarifa, ujuzi ili waweze kuutumia katika maisha yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna masomo ya TEHAMA na Stadi za Kazi; haya masomo yanapofundishwa kikamilifu katika shule zetu wanafunzi hupata ujuzi mbalimbali. Mfano, Somo la Stadi za Kazi, kupitia somo hili leo hii somo hili lingekuwa limefundishwa kwa ukamilifu na watahiniwa wakafanyiwa mitihani ya kuwapima kama wamepata ujuzi na maarifa, tungekuwa na wasanii mbalimbali, wanamuziki, wachoraji, mafundi ujenzi na wapishi waliobobea. Kutokana na changamoto mbalimbali somo hili leo halifundishwi kikamilifu na limekuwa ni somo la option, kwamba kuna shule zinafundisha lakini kuna shule zingine pia hazifundishi.

Mheshimiwa Spika, sambamba na somo la TEHAMA ambalo ni Teknolojia ya Habari na Mawasiliano basi niombe Serikali ione umuhimu sasa wa kuhakikisha kwamba haya masomo yanafundishwa kikamilifu katika shule zetu ili Watoto waanze kupata ujuzi katika umri ule wa shule za msingi na kuendelea. Hii itasaidia Watoto wetu wapate ujuzi na mwisho waweze kujitegemea katika maisha yao, ukilinganisha na kwamba sasa hivi tuna tatizo kubwa la ajira katika nchi yetu tukiwapatia taaluma hii Watoto wetu watapata maarifa na ujuzi wa kutosha ili waweze kusimama wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sera ya nchi yetu ni elimu bure kuanzia darasa la awali mpaka kidato cha nne na hii elimu ni haki sawa kwa watu wote. Naomba nijikite kwenye elimu maalum kwa watu wenye ulemavu, pamoja na kwamba Serikali ni yenye jukumu la kuhakikisha kwamba watu hawa wenye ulemavu wanapata elimu stahiki na watu ambao hawana ulemavu lakini bado kuna changamoto nyingi mno katika utekelezaji wake. Na hii imesababisha kwamba hata watu wale wenye ulemavu Watoto hawa hawapelekwi shule, imebidi wazazi sasa ukipata Watoto wenye ulemavu ni kuwaficha, hatimaye wale Watoto hawapati haki zao za kupata elimu hii inayotolewa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata maeneo yale ambayo elimu hii hutolewa bado kuna changamoto nyingi mazingira yao si rafiki kwa Watoto hao kupata elimu, ikiwepo madarasa wanayotumia, ukosefu wa meza za kusomea, hata wale ambao wenye uoni hafifu hawana lenzi za kusomea pamoja na vitabu vile ambavyo ni sahihi kwa ajili ya Watoto wale wenye ulemavu wa macho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe hawa Watoto ili waweze kupata elimu sawa kama Watoto wa kitanzania ni vema Serikali sasa ione ni namna gani kuweka karibu huduma hii ya elimu maalum katika maeneo yetu ikipendeza nishauri kwamba shule zetu za elimu maalum walau kila wilaya ipate shule maalum ili kila mtoto ambaye anapata ulemavu aweze kupata elimu hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii itaturahisishia kwamba hata walimu ambao wamesomea elimu maalum sasa hivi wanapelekwa kwenye shule zetu za mchanganyiko ambao hawana tatizo hilo la elimu ya watu wenye ulemavu. Walimu hawa watumike ipasavyo endapo tutakuwa na shule zenye elimu, watu wenye elimu maalum.

Mheshimiwa Naibu Spika, walimu hawa wakipelekwa kwenye shule hizo tunauhakika watafanya kazi zao kwa ufanisi mkubwa mno badala ya kuwachanganya wale Watoto wenye uhitaji maalum na Watoto ambao hawana uhitaji huo inasababisha kwamba yule mwalimu anapewa masomo mengi kufundisha Watoto wenye elimu maalum na wakati huo huo afundishe na masomo mengine. Utendaji wa mwalimu unakuwa mgumu na hivyo kufanya yule mtoto hawezi kufanya vizuri darasani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nigusie suala la Idara ya Udhibiti Ubora wa Shule, huwezi kuongelea elimu bora kama huna udhibiti ubora wa shule. Idara zetu za Udhibiti Ubora wa Shule, niipongeze Serikali kwa kuwanunulia magari, kwa kuwajengea Ofisi, Ofisi zetu za Idara ya Udhibiti Ubora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo Ofisi hizi hufanya vizuri kwa upande wa shule za msingi tu. Ukiangalia shule zetu za msingi asilimia 90 wanakaguliwa. Lakini ukija kwenye shule zetu za Sekondari ni asilimia 30 tu ndo huwa hukaguliwa na hawa wakaguzi wa udhibiti ubora. Hivyo, huchangia kwamba shule zetu nyingi hazikaguliwi katika shule za sekondari hivyo basi, inasababisha kutogundua mapungufu yaliyopo kwenye elimu kule shule za Sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii inachangiwa kwamba hawa watu wa udhibiti ubora wako ngazi ya kanda sasa ngazi ya kanda kuna kanda zingine sina mikoa miwili kuna kanda zingine zina mikoa mitatu. Sasa mfano mkoa wetu wa Manyara ukiangalia kanda ya Kaskazini Mashariki tuna mikoa miwili, leo hii Mkaguzi wa Kanda akague mikoa miwili kwa maana Manyara na Arusha, Mkaguzi huyo atoke Arusha aende mpaka vijijini na hivi sasa hivi katika kila kata kuna shule ya sekondari, lakini mkaguzi huyo huyo alioko kanda akague shule za sekondari zilizopo kwenye kata zetu, kwanza anatembea umbali mrefu sana kwenda kukagua shule zetu lakini pia wanatumia gharama kubwa kwenda kufanya kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nishauri Serikali sasa ione umuhimu wa kuanzisha Ofisi zetu za Udhibiti Ubora kwa kila mkoa ili hawa watu huduma zao ziwe karibu na waweze kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuwa na elimu bora ni lazima pia uangalie maslahi ya walimu. Maslahi ya walimu…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana kengele ya pili imeshagonga.

MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi uliyonipatia nami niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Kwanza nianze kupongeza Wizara hii ikiongozwa na Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Mawaziri na watumishi wote wa Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya kuhakikisha huduma hii ya afya inaendelea kuboreshwa. Pia, niipongeze Serikali yetu kwa kazi kubwa inayofanya kuhakikisha huduma ya afya inaendelea kuboreka ili wananchi wetu waweze kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie kuhusu huduma ya mama na mtoto. Niombe Wizara itueleze wazi dhana halisi ya huduma bure kwa akinamama wajawazito na watoto wa chini ya umri wa miaka mitano. Huduma hii imebaki kuwa nadharia, akinamama wengi wanapokwenda kujifungua wanatakiwa waje na vifaa vyao ili waweze kupata huduma hiyo ya kujifungua, wakati tunasema kwamba huduma hii ni bure kwa akinamama wajawazito, wanapokwenda kujifungua wapewe huduma stahiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, ukienda kwa upande wa watoto chini ya miaka mitano, huduma hii si bure kwa sababu hawapati dawa. Watoto hawa wanapata huduma ya kuwaona Madaktari lakini linapofika suala la dawa wanatakiwa wajigharamie na kwenda kununua.

Mheshimiwa Naibu Spika, basi niiombe Wizara ituweke wazi ni namna gani sasa huduma hii ya akinamama wajawazito inapatikana bure, lakini huduma kwa watoto chini ya miaka mitano inapatikana bure. Katika eneo letu mfano, hususan Mkoa wetu wa Manyara, jiografia yetu ni ngumu na ya mazingira magumu mno. Sasa inapofika hatua mama anaambiwa aje na vifaa vyake anapoenda kujifungua, inabaki akinamama wengine wala hawaendi hospitali, wanajifungulia nyumbani, kitu ambacho kinahatarisha maisha yao. Hatimaye akinamama wengi wanapoteza maisha kwa sababu fedha za kumudu gharama.

Mheshimiwa Naibu Spika, huyu mama mjamzito, kwanza kutoka kwenye eneo lake analoishi kwenda kwenye hospitali ni zaidi ya kilometa 70, 80 hadi 100. Sasa mama wa kijijini unapomwambia sasa aje na vifaa, kwanza akiangalia gharama zile za usafiri, aje agharamie vifaa vya kwenda kujifungulia, kiujumla wanashindwa kumudu hizo gharama. Kwa hiyo, naomba iwekwe katika utekelezaji, tusibaki katika nadharia, iwekwe kwa vitendo kwamba akinamama wapatiwe huduma na watoto wale chini ya miaka mitano wapatiwe huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hospitali zetu za Wilaya na vituo vyetu vya afya hakuna vyumba vya kuhudumia watoto njiti. Watoto njiti wanapopatikana wanahudumiwa locally, lakini naomba sasa Serikali ihakikishe vituo vyetu vya afya, hospitali zetu za Wilaya, vyumba vile vya kuhudumia watoto njiti pamoja na wataalam wale wa kuwahudumia wale watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kuna huduma ya phototherapy unit, wale watoto ambao wanapata homa ya manjano. Maeneo yetu mengi hasa Mkoa ninaotoka mimi, watoto hawa wanapopata tatizo hilo la homa ya manjano kiukweli hawapati hiyo huduma inayostahili kwa sababu hatuna mazingira wezeshi, hatuna vifaa, hizo phototherapy unit hazipatikani. Kwa hiyo, Serikali ione namna gani basi angalau hata hospitali zetu za wilaya na rufaa ambazo ni hospitali za mikoa ziwepo hizo phototherapy unit ili watoto wetu wanapopata tatizo hilo basi wahudumiwe kitaalam zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijikite zaidi kwenye huduma ya wazee. Kiukweli huduma hii ya wazee bado niishauri Serikali ione namna bora ya kuwahudumia hawa wazee wetu wa miaka 60 kwenda juu. Wazee hawa wanateseka mno wanapofika kupata huduma hizo katika hospitali zetu. Ukizingatia hospitali zenyewe hizi bado tuna upungufu mkubwa wa dawa, lakini yule mzee anapohitaji ile huduma akijua kwamba Serikali yetu inamhudumia bure, anapofika ile huduma haipati, kiujumla wananyanyasika na kufedheka hawa wazee. Naomba tuwatunze hawa wazee wetu kwa sababu na wenyewe walikuwa vijana kama sisi. Sasa wanapofika katika ule umri mkubwa, naomba Serikali itusaidie basi kuhakikisha ile huduma inapatikana kikamilifu ili wazee wetu nao waendelee kuishi wakiwa na afya njema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami niungane na wenzangu walioongolea suala la Bima ya Afya. Kiukweli hili suala la Bima ya Afya ni kilio kikubwa. Hii Bima ya Afya CHF ambayo inatakiwa kwa wananchi wote bado kuna tatizo kubwa. Bado kuna tatizo kubwa. Tunaomba Wizara sasa ione mkakati upi wa namna gani ya kuboresha hiyo huduma ya Bima ya Afya. Utaona hata mwitikio kwa wananchi unaenda kuwa mdogo kwa sababu mtu anapokata ile Bima ya Sh.30,000 akitegemea anapata huduma katika zahanati au kituo cha afya, matokeo yake hapati dawa. Anabaki na ile hali kama ni mgonjwa atabaki na ugonjwa wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hata unapompa rufaa kwenda hospitali ya wilaya anapata tabu ya kwenda hospitali ya wilaya kwa sababu hata nauli ya kwenda huko hana. Kwa hiyo, yule mtu anaendelea kupata tabu huku akiwa mgonjwa, anahitaji kuhudumiwa lakini huku anahitaji kutoa fedha zake ili aweze kupata huduma hiyo. Naomba huduma hii ya Bima ya Afya iboreshwe ili walau kama kweli tunahitaji wananchi wetu wapate huduma kwa kupitia Bima ya Afya, tuwe serious na jambo hili ili huduma hii itolewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye suala la NHIF. Ukiangalia huduma ya NHIF, watu wengi wamezungumzia humu ndani. Ni kwamba huduma hiyo bado inatakiwa iangaliwe tena upya. Kuna baadhi ya dawa ambazo ni muhimu, zinatakiwa ziwepo kwenye huduma hiyo ya Bima ya Afya. Mfano kuna dawa za sukari, pressure ambazo ni muhimu wananchi wapate. Tena ikiwezekana wapate bure maana ni magonjwa ambayo yanajitokeza, sio magonjwa ya kuambukizwa. Kwa hiyo, unakuta hiyo huduma haipo kwenye Bima ya Afya na inalazimu watu wanaanza kununua zile dawa kitu ambacho sasa ni gharama. Mtu anajiuliza kwa nini anakuwa na Bima ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nishauri, kama itapendeza Serikali ione namna ambavyo yule ambaye ni mchangiaji tunakuwa na wale wategemezi. Sasa wale wachangiaji unakuta mtu hana mtoto, hana baba, mama, hana mume, hana mke lakini yeye ni mchangiaji namba moja. Wakati huo huo anakuwa na mtu ambaye anamtegemea kama mlezi wake aliyemlea, bima inamkataa yule mtu. Nafikiri tuangalie mfumo upya kwa sababu yule mtu ataendelea kuwa mtegemezi kwake na ataendelea kumhudumia na wakati huo yule mtu anaendelea kuchangia bima ya afya lakini hanufaiki, atanufaika yeye peke yake wategemezi watakuwa hawajanufaika na huduma hiyo ya bima ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo naomba nichangie suala la ukosefu wa vituo vya afya katika maeneo yetu. Pamoja na jitihada kubwa ya Serikali, lakini bado katika maeneo yetu tuna changamoto kubwa ya ukosefu wa vituo vya afya. Natolea tu mfano katika Mkoa wetu wa Manyara, Wilaya ya Kiteto pale tuna vituo viwili vya afya. Sasa ukizingatia vituo viwili vya afya na zahanati 23 katika kata 23 kiukweli wananchi wetu bado wanafuata huduma mbali sana. Huduma hizi zisogezwe karibu na wananchi. Mheshimiwa Naibu Spika,

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile hata kwa zahanati zilizopo hatuna vifaatiba, wananchi bado wanateseka kwa sababu vifaa tiba havipo na dawa hazipo na wakati huo huo tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi wa huduma ya afya. Kuna zahanati zingine hata Madaktari tu hawapatikani, wamebaki kuwa watoa huduma. hivyo inawalazimu watu kwenda hospitali zingine na wengine kukosa hiyo huduma ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana na naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi uliyonipatia niweze kuchangia bajeti ya Wizara ya Kilimo kuwasemea waajiri wangu hususan wakulima na wananchi wetu wa Mkoa wa Manyara na pia nichukua nafasi hii kuipongeza sana Serikali kwa kazi kubwa inayofanya kupigania hii Wizara ya Kilimo, nimpongeze sana Waziri na Naibu Waziri wake kwa kazi kubwa waliyoifanya na kusaidia hasa Mkoa wetu wa Manyara kipindi ambacho tulikuwa tumepata janga la kuvamiwa na nzige kwa kweli walifanya kazi kubwa sana hawakulala walihakikisha wamelitatua jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba Wizara hii ya Kilimo inatakiwa sasa iweke jitihada za pekee kuhakikisha kilimo kinamkomboa mwananchi ambaye anayejishughulisha na kilimo. Mkoa wetu wa Manyara ni Mkoa uliobarikiwa sana ni Mkoa ambao una ardhi nzuri sana lakini ni Mkoa ambao unajishughulisha na kilimo cha mazao ya aina yote yanayolimwa Tanzania hii.

Mheshimiwa Spika, lakini kulingana na changamoto inayoikumba hii sekta ya Kilimo wananchi wetu wengi wamekata tamaa na hasa kazi hii ya Kilimo, ikiwepo baadhi ya mazao sasa hivi katika Mkoa wetu watu wengi wameacha kushughulika nayo kwa maana ya kwamba wanakosa vitendea kazi wanakosa pembejeo ikiwepo mbegu na mbolea. Mbegu na mbolea katika Mkoa wetu wa Manyara vinachelewa sana kufika kwa muda muafaka wa wakulima.

Mheshimiwa Spika, hii imesababisha wananchi wetu wameacha sasa hivi kujishughulisha na Kilimo cha Ngano, wameacha kujishughulisha na Kilimo cha Pareto wamekatishwa tamaa kabisa na kujishughulisha hata na kilimo cha vitunguu saumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata mbolea zinapofika au mbegu zinapofika katika maeneo yetu upatikanaji wake ni mgumu lakini pia gharama ni kubwa ukilinganisha na hali halisi ya wakulima wetu. Sasa hivi ukiangalia wananchi wetu wanaojishughulisha hata na Kilimo cha ngano wanaojishughulisha na Kilimo cha Pareto Kilimo cha vitunguu saumu wale wachache waliobaki wanalima kilimo ambacho hakiendani hasa na hali halisi au kilimo kinachowaletea tija wananchi hawa wameendelea kutumia mbegu ambayo haistahili kabisa mwisho wa siku wanafanya kazi kubwa na matokeo ni madogo mno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi hawa wanalima wanatumia nguvu kubwa sana wanatumia gharama kubwa sana lakini hawanufaiki na Kilimo hicho. Niende sambamba katika kuelezea katika suala zima la masoko tunasema jembe halimtupi mkulima kiukweli sasa hivi kilimo kimekuwa ni kilio kikubwa sana kwa wananchi wetu, wananchi wetu wanatumia gharama kubwa sana katika kulima lakini wanapofika katika suala la masoko kiukweli mazao yao yananunuliwa kwa gharama ndogo mno kitu ambacho kinawakatisha tamaa kuendelea kufanya kazi ya kilimo lakini pia kuendelea kumdidimiza na kumgandamiza huyu mkulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna watu wanaitwa madalali hawa watu wanafika kwenye maeneo yetu kule mashambani wananunua mazao yakiwa mashambani, mkulima kwa sababu hana uhakika wa masoko anaamua kuuza kwa gharama ndogo sana na wanaofaidika ni wale madalali ambao wakishafanikiwa kununua kutoka kwa mkulima wanaenda kuuza kwa gharama kubwa kwa hiyo faida kubwa inakwenda kule kwa madalali. Sasa ni muda muafaka Wizara hii kuwahakikishia wakulima masoko yenye uhakika ili kama kweli tuna nia ya dhati kabisa kumkomboa mkulima, tuna nia ya dhati kabisa kufanya wananchi wetu na Watanzania na vijana wetu wafurahie kilimo ni kuwapatia soko la uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni namna gani sasa Wizara imejipanga kuangalia masoko ya uhakika ukizingatia kwamba katika ndani ya Afrika tuna masoko mengi ukiangalia kama nchi ya Congo, Zimbabwe.

Je, Wizara imejiandaaje sasa kutafuta masoko nje ili wananchi wetu wanapofika ule muda wakishavuna mazao yao waweze kupata soko la uhakika na kuuza mazao yao ili waweze kupata faida. Sambamba na hilo imeongelewa sana kuhusu kuamini kwamba tukitegemea mvua katika kilimo imekuwa sio njia sahihi na yenye uhakika kwanini sasa Wizara isione tuwekeze nguvu kubwa katika kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Regina.

MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi uliyonipa. Naunga Mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali chini Rais Mama yetu shupavu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuwaletea Watanzania maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri wa TAMISEMI, Naibu Mawaziri TAMISEMI pamoja na uongozi wote wa Wizara kwa kufanya kazi nzuri kuhakikisha maendeleo na huduma inasogezwa karibu na wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizo bado kuna changamoto kwa upande wa afya, elimu, mikopo ya asilimia 10 kwa makundi maalumu. Katika afya bado mkoa wetu wa Manyara tuna jiografia ngumu mno kutoka kata moja kwenda makao makuu ya Wilaya ni umbali zaidi ya kilometa zaidi ya 100 hivyo kuwa na kituo kimoja katika Tarafa bado ni changamoto kubwa mno, mfano katika mkoa wetu kuna tarafa kubwa zaidi ya baadhi ya Wilaya hivyo ombi langu ni kuwa angalau kituo kimoja kila kata, hii itasaidia kupunguza vifo vingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika Wilaya ya Simanjiro hakuna gari la wagonjwa hivyo wananchi wetu wanateseka sana na wengi kupoteza maisha. Tunaomba kupatiwa gari la wagonjwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la asilimia 10 ya kina mama, vijana na watu wenye ulemavu nashukuru Serikali kwa kuendelea kuwapatia makundi haya ili kujikwamua kiuchumi, lakini bado asilimia nne kwa kina mama haitoshi ukizingatia kina mama ndiyo wana majukumu makubwa kwenye familia na vigezo vinavyotumika kupewa mikopo inatakiwa kufanyika marekebisho.

Ushauri wangu ni kuongeza asilimia 10 iwe kwa kina mama tu na vigezo vya mikopo isiwe lazima kukopa mpaka vikundi, akinamama wapewe mikopo hata mtu mmoja badala ya vikundi, hii itasaidia kuinua uchumi wa mtu mmoja mmoja na urahisi wa marejesho.

Kwa upande wa elimu bado tuna changamoto, ukosefu wa madawati bado kuna watoto wanakaa chini hasa shule za misingi, elimu bora ni pamoja na mazingira mazuri ya kufundishia na kujifunzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika hoja mbili zilizotolewa kwa siku ya leo.

Kwanza kabisa nipongeze Kamati mbili zilizowasilisha taarifa yao hapa siku ya leo, lakini kazi kubwa ya Bunge ni pamoja na kutunga sheria, lakini Katiba yetu imekasimisha madaraka, imelipa uwezo Bunge hili kukasimisha madaraka

katika mamlaka nyingine za Kiserikali. Lakini kwa bahati mbaya sana mamlaka zetu zilizopewa jukumu hili la kutunga sheria ndogo katika maeneo yao zimekuwa zikitunga sheria ambazo hazina uhalisia kulingana na maisha halisi ya Mtanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesema hayo na nitaendelea kuelezea haya kwa kutumia mifano michache. Mfano Sheria ya Ushuru wa Nyumba za Kulala Wageni katika Manispaa ya Temeke; sheria hii iliyotungwa pale inaweka katazo kwa wageni kulala katika chumba kimoja na kulalia kitanda kimoja, wageni hawa ambao ni wa jinsia moja, lakini sheria hii haikuzingatia watu wenye mahitaji maalum, sheria hii haikuzingatia kwamba kuna ulazima, kuna mazingira ambayo yanamlazimisha mtu kulala katika kitanda kimoja watu wa jinsia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, mama amekuwa akisafiri na mwanaye, hakuna namna unamzuia mama yule kulala na mtoto wake, lakini pia kuna mgonjwa anayehitaji msaada kutoka kwa msaidizi wake, huwezi kumzuia kulala katika kitanda kimoja au chumba kimoja na huyo msaidizi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwneyekiti, hivyo sheria hii katika utekelezaji wake inaleta ukakasi kwa sababu unapoenda kutekeleza sheria ya namna hii wapo wananchi watakaoumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunaelewa maisha ya Mtanzania halisi yalivyo, wakati mwingine inawalazimu watu wa jinsia moja kama ni mama na mtoto wake kulala chumba kimoja ili kuokoa gharama, lakini ukisimamia sheria hii maana yake yule mtu ataingia gharama zisizokuwa na msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kupitia uchambuzi wa Kamati yetu pia tumegundua Sheria ya Afya ya Usafi wa Mazingira katika Halmashauri ya Nsimbo; sheria hii imeweka katazo kwa mtu yeyote kuuza vyakula kwa kubeba kwenye ndoo, kwenye sufuria hata kama imefunikwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaelewa maisha ya Watanzania wetu, lakini hebu fikiri maisha ya Mtanzania ambaye ni mama ntilie, unamwambia usihifadhi chakula kwenye sufuria, hata kama umefunika, asihifadhi chakula kwenye ndoo hata kama imefunikwa. Unampa maisha gani huyu Mtanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, sheria hii ukienda kwenye utekelezaji wake huwa ni mgumu sana. Ni mgumu kwa sababu mlaji wa hii sheria unaenda kumpa adhabu zisizokuwa na msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika Halmashauri ya Msalala kuna sheria ya Ukusanyaji na Kuzoa Taka; sheria hii inaweka katazo kwa mwananchi ambaye atatupa taka hovyo ambacho ni kitu kizuri, lakini sheria hiyo imetamka kwamba mwananchi au kaya lazima iwe na chombo cha kuhifadhia taka chenye mfuniko, lakini sheria haijatamka kwamba chombo hicho ni chombo cha aina gani? Na ni mfuniko wa aina gani, lakini sheria haielekezi baada ya kukusanya zile taka, akishamaliza kukusanya anapeleka wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa mazingira halisi ya kijijini tunaelewa kwa watu tuliotoka kijijini, kaya zote za vijijini wanachimba mashimo ya taka, ili kuhifadhi takataka. (Makofi)

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Iddi Kassim?

T A A R I F A

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpa Taarifa mchangiaji kwamba sheria hizi, mamlaka haya ambayo tumeyakasimu kwenye Halmashauri zetu, utaratibu wa kutunga sheria hizi haufuatwi, hasa kuwashirikisha wananchi katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo Halmashauri ya Msalala ni Halmashauri iliyo katika maeneo ya vijijini na hivyo ninashauri sheria hii ifanyiwe marekebisho kwani haitatekelezeka kwenye maeneo hayo, ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante, Mheshimiwa Regina unapokea Taarifa?

MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea hiyo Taarifa kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii kwa uhalisia wake unaona ni kwa namna gani kwanza wananchi wanaenda kunyanyasika. Halmashauri ya Msalala haina gari la kubebea taka, wakati huo umetunga sheria kwamba kila kaya wahakikishe wana chombo cha kuwekea taka. Sasa baada ya kuweka hizo taka watazibeba kwenda wapi? Dampo liko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukiitizama kwa undani hii sheria, mamlaka hizi zinazotunga sheria zinatunga sheria ambazo hazina uhalisia kulingana na wakazi wa eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sheria nyingine ni Sheria ya Ada na Ushuru katika Halmashauri ya Mvomero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii inaeleza kwamba ada ya kibali cha upimaji wa afya, maana yake kila mtu anayehitaji kibali cha kunyunyiza viuatilifu atapata kibali kwa gharama ya shilingi milioni moja. Kama kibali tu anaenda kupata kwa shilingi milioni moja, anapotaka kutoa huduma kwa wananchi atatoa kwa gharama gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Halmashauri lazima ipange gharama ambazo hata yule ambaye amepata kibali tayari anapotaka kutoa huduma kwa wananchi atoe gharama ambazo hazitamuumiza mwananchi huyo. Katika uchambuzi wetu wa Kamati kulingana na huu udhaifu uliojitokeza katika mamlaka waliyopewa, jukumu la kutunga sheria ndogo bado kuna haja ya Bunge sasa kufikiria upya namna ya kuendelea kusimamia hizi mamlaka ili wasije wakatutungia sheria ambayo inaumiza wananchi wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema haya kwa sababu sheria hizi mpaka kufika kwetu kwa Wabunge tayari kule imeshaanza kutumika, jambo ambalo wananchi wameshaanza kuumizwa na hizo sheria na mpaka hatua ya kukataza au kuondoa ile sheria ije iwafikie wananchi, tayari wananchi wengi wameshapata madhara makubwa.

Kwa hiyo, ombi langu ni kwamba Bunge hili tuna jukumu kubwa bado la kuendelea kusimamia hizi mamlaka tuliowapa jukumu la kutunga hizi sheria, ili wananchi wetu wasiendelee kupata madhara makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikifika hapa niseme naunga mkono hoja, lakini nikushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Wizara hii ya Madini. Kwanza kabisa nampongeza sana Waziri pamoja na timu yake kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara hii. Kwa niaba ya wananchi wote wa Mkoa wa Manyara namshukuru sana Rais, Mama yetu mpendwa, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia maombi ya soko la madini kubaki pale Mererani. Kwa nini tunasema kwamba, soko la madini libaki pale Mererani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati wanagawanya Mkoa huu wa Manyara kutoka Mkoa wa Arusha, waliangalia vigezo vingi sana na ndiyo maana Wilaya ya Simanjiro imeendelea kubaki Mkoa wa Manyara badala ya Mkoa wa Arusha kwa sababu kijiografia Wilaya yetu ya Simanjiro iko karibu sana na Mkoa wa Arusha, lakini waliangalia ni vigezo gani au ni shughuli gani za kiuchumi zinazoweza kubeba mkoa kwa mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wetu wa Manyara, mkoa wetu unabebwa na madini ya Tanzanite; mkoa wetu unabebwa na shughuli za kilimo; na mkoa wetu unabebwa na Hifadhi ya Wanyama ya Tarangire. Hivyo basi, busara ya Serikali ya Awamu ya Tatu chini ya Mheshimiwa Benjamin William Mkapa waliona kabisa ni muhimu suala zima la madini ya Tanzanite yabaki eneo la Manyara. Hivyo basi, tunaishukuru sana Serikali kwa kuendelea kubakiza soko hili katika eneo la Mererani na tunaendelea kuwaomba libaki pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Serikali ni kwamba, lile soko la eneo la Tanzanite City limeshatengwa, mfumo wa maji umekamilika, mfumo wa umeme umekamilika, barabara zimechongwa, lakini bado kazi ya ujenzi haijaanza. Kuna uzio umewekwa pale wa bati, lakini hayo mabati yameanza kudondoka. Tunaomba kujua, ni lini Serikali itaenda kuanza ule ujenzi mara moja ili kuwatoa hofu wafanyabiashara wa Mererani? Kwa hiyo, Waziri anapokuja kuhitimisha, naomba sana atueleze, ni lini ujenzi utaanza pale ili wafanyabiashara wafanye kazi zao wakiwa na matumaini makubwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, soko hili kuwa pale Mererani inatusaidia kuendeleza Mji wa Mererani, inasaidia vijana wengi kupata ajira pale Mererani, na kusaidia mapato makubwa kubaki katika Mkoa wa Manyara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la wageni kufika Mererani usalama wao umeboreshwa sana. Kwanza wageni wengi wanatua katika uwanja wa ndege wa KIA ambapo ni kilometa 20 tu kufika Mererani. Kwa hiyo, wafanyabiashara wa madini wa Mererani wanaendelea kuomba kwamba soko hili libaki pale, lakini Serikali itukamilishie mara moja ujenzi huu ili soko lile liweze kufanya kazi kwa ubora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi la pili. Wamama wengi katika eneo lile la Mererani wanajishughulisha sana na uchimbaji wa madini. Wako wamama wanamiliki migodi na wako ambao ni wachimbaji wadogo wadogo. Changamoto wanazokutananazo wamama hawa ni ukosefu wa mikopo. Naiomba Serikali sasa ione namna ya kuwawezesha akinamama, wale wachimbaji wadogo wadogo ili waweze kujishughulisha kikamilifu na waweze kujikwamua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini tunasema haya? Shughuli ya madini ya Tanzanite upatikanaji wake kwanza kwa sababu hawana vifaa vya kutambua kwamba eneo hili ndiyo kuna madini, hiyo inawakosesha wamama wengi wanapoteza hela nyingi wakiwa wanachimba yale madini halafu hawafanikiwi. Serikali ione namna ya kuwapatia vifaa na wataalam pamoja na mitaji ili wale wamama wanapochimba madini yale wawe na uhakika wa kupata madini na waweze kujinyanyua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala la usafiri. Katika lile eneo la ukuta wa Mererani ambalo tunasema geti la Magufuli, tuna usafiri wa bodaboda mle ndani; tuna wamama ambao wanafanya biashara ya Mamantilie, tuna wamama ambao wanabeba matunda kichwani wakiwa wanaenda kuwauzia wachimbaji wadogo wadogo mle kwenye eneo la ukuta, lakini changamoto kubwa ni bodaboda zinazotumika mle ndani, wanalipishwa shilingi 2,000 kuwapeleka na shilingi 2,000 kurudi; wanapoingia tu getini, kitu ambacho kinasababisha wale akinamama wanashindwa kufanya zile biashara ili kujikwamua kiuchumi kwa sababu wanatumia zaidi ya Shilingi 8,000 hadi shilingi 10,000 kwa siku.

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali ione namna ya kuongea na wamiliki wa usafirishaji, yaani magari, ili magari yaruhusiwe kufanya kazi kule ndani ya ukuta; wamama hawa waweze kupata usafiri ili waweze kujikwamua kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, naiomba Serikali; kuna hawa wafanyakazi wa migodi ambao wanafanya mkataba kati ya wamiliki wa migodi pamoja na wale wafanyakazi wa migodi. Wale wafanyakazi wa migodi wana changamoto nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri hili anafahamu ni kwa namna gani wale wachimbaji wadogo wadogo ambao wanazama kwenye mashimo wanakosa haki zao za msingi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. REGINA N. QWARAY: Muda umeisha? Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hii Wizara nyeti, Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya katika nchi yetu. Pia nimpongeze sana Waziri wa Elimu pamoja na timu yake yote ya Wizara kwa kazi nzuri wanaoyofanya katika Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba, ukitaka kuwa na elimu bora lazima uangalie walimu bora. Usipo andaa walimu bora huwezi kuwa na elimu bora; na walimu bora hutokana na mafunzo bora wanayopata katika vyuo.

Mheshimiwa Naibu Spika, walimu wetu kwa sasa ubora wao unapungua siku hadi siku. Nasema hivi kwa sababu gani; tunashukuru Wizara ya TAMISEMI imetoa ajira kwa walimu wapya, lakini walimu hawa wapo waliomaliza elimu yao au mafunzo ya ualimu kwa miaka mitano au saba. Walimu wale wamekaa nyumbani wakiwa wanafanya shughuli zingine za kiuchumi. Wapo wanaofanya shughuli za mama ntilie, wapo wanaofanya shughuli za bodaboda, wapo wanaofanya shughuli za kilimo na mifugo. Walimu hawa kwa miaka saba au kwa miaka mitano waliokaa nyumbani ni ukweli kwamba wameshasahau yale yote waliyofundishwa katika mafunzo yao ya ualimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa basi, ni wakati wa Serikali kuweka utaratibu, kwamba wanapoajiri walimu wapya wawapeleke kozi fupi fupi ili waweze kufanya kazi yao na kuleta tija. Lakini sambamba na hilo ni miaka mingi sasa walimu hawapati semina, ni miaka mingi walimu hawapati kozi fupifupi. Serikali iangalie namna gani ya kuwa- brush walimu ili waweze kuwaongezea maarifa na ujuzi katika kufanya kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walimu pia bado wanamazingira magumu ya kazi. Mazingira ya walimu yasipoboreshwa bado elimu yetu haitakuwa bora. Tunapoongelea elimu bora ni kumuongelea pia na mwalimu yule anayetoa hiyo elimu. Mazingira yao bado ni magumu ukizingatia na kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwalimu bado ana majukumu mazito sana. Mwalimu anaandaa lesson notes, lesson plan pamoja na scheme of work. Vilevile mwalimu anatakiwa asahihishe, na pia anatakiwa afundishe. Kazi zote hizi zinamtegemea mwalimu. Sasa, ukiangalia mazingira hayo inamuia vigumu kwa sababu uwiano kati ya mwalimu na mwanafunzi haupo. Mwalimu mmoja anakuwa na wanafunzi zaidi ya 200 au 100 darasani. Ukiangalia kazi ya namna hiyo ni ngumu sana mwalimu kufanya kazi yake ili kuleta tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Serikali basi iangalie mazingira ya ufanyaji kazi ya walimu ili walimu hawa waweze kufanya kazi. Vilevile kuangalia uwiano kati ya mwalimu na mwanafunzi. Tukifanya hivi tutaenda mbele kwenye hii sekta ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo nizungumzie suala la motisha; walimu wanahitaji kupata motisha kwa sababu ni muda sasa walimu hawapati motisha. Wapo walimu wanaofanya vizuri, hivyo Serikali iangalie namna nzuri ya kuwapa motisha wale walimu ili waweze kufanya kazi yao kwa moyo. Katika suala zima la kufanya kazi motivation ni muhimu sana. Motivation moja wapo ni pamoja na kuwaongezea mishahara lakini na kupandisha madaraja. Niishukuru Serikali kwa mwaka huu na mwaka jana imepandisha madaraja. Hata hivyo bado tunahitaji kuwapa motisha walimu wale wanaofanya vizuri kwa kuwanafanya wanafunzi wetu wafaulu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine nishauri Serikali kuna TRC vituo vile vya mafunzo au vituo vya walimu wanaofanyia mafunzo, TRC ziboreshwe katika kila kanda, zikiboreshwa walimu watapata muda wa kwenda kujifunza baada ya masomo. Watajifunza, watabadilishana mawazo, walimu watakusanyika pale, watajadili mada zile ambazo zinawasumbua ili waweze kufanya kazi zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nipongeze Serikali kwa kuanza mchakato wa mtaala mpya wa elimu. Tunapongelea mtaaala mpya wa elimu ni mtaala unaoenda kuendana na mahitaji ya jamii husika. Mtaala huu ulenge nini jamii inahitaji. Tunapozungumzia elimu bora ni lazima tuanze kuanzia chini. Tunapoanza kuboresha elimu ya vyuo tukasahau huku madarasa ya awali, shule za msingi na sekondari hakika hatutafanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iangalie namna ya kuboresha kuanzia darasa la awali, tunaboreshaje? Tunahitaji mwanafunzi anapomaliza au anapohitimu elimu yake aweze kujitegemea. Yale masomo ambayo yanatakiwa apewe ujuzi wa mwanafunzi kwenda kujitegemea akiwa uraiani yaanzie kuanzia darasa la awali ili kuendelea kuwajengea uwezo wanapoendelea kujifunza anapomaliza elimu yake ya msingi anakuwa tayari amepata ujuzi na maarifa; anapoenda chuoni anakuwa tayari anaujuzi na maarifa kuanzia kule chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumesahaulika kwa sababu kuna masomo ambayo walikuwa wanafanya wanafanya vizuri. Yapo masomo ambayo yalikuwa yanawashughulisha watoto wanafanya kazi za mikono, siku hizi hakuna. Turudishe yale masomo ambayo yanawafanya wanafunzi wanafanya shughuli za mikono ili kuweza kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima sasa tuanze reforms kuanzia chini kwenda juu. Tukifanya hivi ninaamini kwa kiasi kikubwa tutafanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikisema haya naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya TAMISEMI. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, Mama yetu mpendwa Daktari Samia Suluhu Hassan, kwa namna anavyofanya kazi, kiukweli Watanzania tunafarijika sana na namna ambavyo Mama ameendelea kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninampongeza sana Waziri wetu wa TAMISEMI pamoja na Naibu Mawaziri wote wawili kwa namna wanavyoendelea kumsaidia Mama kufanyakazi na kutatua kero za wananchi hapo kwa hapo.

Mheshimiwa Spika, baada ya shukrani hizi na pongezi hizi naomba nijikite katika vipengele vichache ambavyo ningependa kuchangia kwa siku ya leo.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa ya kujenga shule nyingi za sekondari na kwa kujenga shule nyingi za msingi. Madarasa aliyojenga Mheshimiwa Rais ni madarasa yanayovutia na kupendeza sana. Tunapotaka kupandisha hadhi ya elimu yetu ya Tanzania ni pamoja na kuangalia mazingira ambayo watoto wetu wanayasomea. Nasema haya kwa sababu shule zetu nyingi za Kata zimejengwa katika Makao Makuu ya Kata jambo ambalo linawapelekea watoto katika mazingira haya kutembea umbali mrefu kufika katika Makao Makuu ya Kata ili kwenda kupata elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yapo maeneo ambayo watoto wanatembea kilometa 20, 30 hadi 50 kutoka kwenye vijiji kuja kwenye Makao Makuu ya Kata ambayo ndiyo shule zetu za sekondari zilipo. Watoto hawa wameendelea kukumbana na changamoto nyingi mno ni kitu ambacho kimewapelekea watoto wameamua kupangisha wanaita gheto. Yale maisha ya geto watoto wanajipikia, watoto wanajitafutia mahitaji yao lakini usalama ni mdogo sana.

Mheshimiwa Spika, usalama huu tulikuwa tunawalilia watoto wa kike lakini sasa hivi mpaka watoto wa kiume wamekuwa wakijiingiza katika matendo ambayo hayapendezi. Watoto wetu wa kike waliopangisha katika maisha haya ya geto wanaendelea kuvamiwa kule wanabakwa, wanapata mimba na wengine kuambukizwa magonjwa. Jambo hili linawafanya watoto wengi wasitimize malengo yao na wasifikie ndoto zao. Wapo watoto ambao wamefikia kuacha shule kwa sababu pia kutembea kwa umbali mrefu kwenda kufata elimu. Ninaombe sasa Serikali imefanya kazi kubwa ya kujenga madarasa mazuri. Sasa niombe nguvu hiyo hiyo iliyotumika kujenga madarasa yapelekwe sasa kujenga bweni ili watoto wapate mazingira ya kusomea na waweze kutimiza ndoto zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo Wabunge wenzangu wameongelea mengi watumishi. Mimi katika Mkoa wangu wa Manyara hali ni mbaya zaidi. Ninasema haya kwa sababu kuna wilaya zetu hasa Wilaya zile za kifugaji, ukienda shule moja unakuta ina walimu watano, shule ina darasa la kwanza mpaka la saba. Mwalimu mmoja anafundisha wanafunzi wa darasa la kwanza wanafunzi wako 100 darasani halafu unataka mwanafunzi yule ajue kusoma na kuandika, jambo ambalo haliwezekani.

Mheshimiwa Spika, mimi niombe kulingana na upungufu mkubwa wa watumishi tulionao sasa Serikali iwekeze katika kuona namna ya kurekebisha Ikama katika idara ya elimu. Tusipofanya hivi tutaendelea kuboresha mitaala lakini hatutafanikiwa na hatutafikia malengo kwa sababu mwalimu mmoja kufundisha wanafunzi 100 kwa darasa moja ni jambo ambalo haliwezekani.

Mheshimiwa Spika, wapo vijana wetu wanaojitolea katika maeneo yale mimi niombe katika ajira hii waangalie hasa waliotoka maeneo yale wanayojitolea. Nasema hivyo kwa sababu wapo vijana ambao wanaomba ajira hizi wakishafanikiwa wakipangwa katika mazingira yale ambayo sio wenyeji wenyewe wanaanza kuomba kuhama kwa sababu mbalimbali. Sasa wakianza kuhama kumbuka umewanyima vijana ambao tayari walikuwa wamekwishajitolea mwaka wa kwanza wa pili na wa tatu.

Mheshimiwa Spika, katika ubora kijana aliyejitolea kwa miaka miwili mfululizo ukienda kwenye ujuzi na maarifa yule ameboresha zaidi kwa vitendo, kwa hiyo anakuwa na uwezo mkubwa wa kufundisha kuliko yule ambaye amekaa mtaani na kuja kuanza kazi. Yule ambaye amejitolea atakuwa na uwezo mkubwa wa kufundisha na atatoa elimu bora kwa watoto wetu. Kwa hiyo, niombe sana Wizara iliangalie hili ili kuona namna gani vijana wetu wazalendo waliojitolea, tusiwakatishe tamaa ili waweze kujitolea na wengine waone mfano kwamba mtu akijitolea mwisho wa siku atafanikiwa, atapata ajira, badala ya kuwaacha tena katika nafasi hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa ya kutujengea vituo vingi vya afya. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa sababu ndoto yake kubwa na malengo yake makubwa ni kupunguza kwa kiwango kikubwa vifo vya mama na mtoto, lakini vituo hivi haviwezi kwenda kufanya na kutoa huduma bora kama hatuna watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vipo vituo vyetu vya afya, unakuta ina daktari mmoja au nurse mmoja, jambo ambalo linakuwa ni gumu sana katika utoaji huduma. Kwa hiyo, wagonjwa wanafika kwenye kituo lakini hakuna madaktari. Wagonjwa wanapewa rufaa kwenda maeneo mengine kwa sababu tu kituo chao cha afya hakina wataalam. Kwa hiyo, naomba, ili kuleta ufanisi katika utoaji wa huduma za afya katika vituo vyetu vizuri vilivyojengwa, ni lazima pia kurekebisha ikama katika Idara hii ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais na ninamshukuru sana kwa sababu aliamua na kukubali kwamba vijana wetu amboa walikatizwa masomo kwa sababu mbalimbali ikiwemo mimba, warudi shuleni. Vituo hivi ambavyo sasa wale vijana wetu wamerudi kwenda kusoma, bado vimekuwa na changamoto. Kuna mafanikio, lakini kuna changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto wanazokutana nazo, wale vijana wanaenda kujifunza kwenye Vituo vya TRC. Sasa katika vile vituo, unakuta wamepewa chumba kimoja cha kujifunzia na kufundishia. Wale wanafunzi wanasoma kwa miaka miwili tu ili aweze kufanya mtihani wake wa Kidato cha Nne. Sasa kwa miaka miwili tu, mwanafunzi anatakiwa awe amemaliza vitu vyote ili aweze kufanya mtihani wake na aweze kufaulu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto wanazokutanazo wale wanafunzi kwanza hawana walimu wa kufundisha, na pia hawana vitabu vya kujifunzia. Naiomba Serikali sasa iwapelekee vitabu kama ambavyo wanapelekewa katika shule hizi ambazo ziko kwenye mfumo rasmi. Tunasema haya kwa sababu kama lengo kweli ni kuwaokoa hawa vijana wetu ambao wamekatizwa masomo waweze kufikia malengo yao, Serikali ni lazima iweke jitihada zake ili kuhakikisha wale vijana wanafaulu na kutimiza ndoto zao. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante ili na mimi kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika bajeti hii ya Wizara ya Mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo ameendelea kuweka mikakati katika Wizara hii na kuhakikisha suala zima la mifugo katika nchi hii linakuwa endelevu na lenye tija. Nimpongeze pia Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na wafanyakazi wote wa Wizara kwa namna walivyoanza vizuri kufanya kazi. Pia nipongeze kwa ripoti nzuri hii ambayo imewasilishwa katika Bunge hili, iliyojaa mikakati na namna ya kwenda kumkomboa hasa mfugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunavyofahamu, wafugaji, hasa wafugaji wa asili, wanategemea mifugo kwa kila kitu. Wanategemea mifugo katika mahitaji ya kujisomesha na kwa ajili ya chakula; na kwa kila kitu mfugaji wa asili anategemea mifugo ili aweze kujikwamua kiuchumi. Kama alivyosema Mheshimiwa Waziri kwamba tunapoongelea mifugo maana yake tunaongelea uchumi, sasa ni uchumi upi tunao uzungumzia katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni kumekuwa na chanagamoto nyingi sana. Jambo ambalo linawakwaza wafugaji wasione suala zima la ufugaji kama linaleta tija na kuweza kujikwamua kiuchumi ni kwa sababu wafugaji wa nchi hii wamekuwa ni watu ambao ni wakukimbizana hapa na pale wakiwa ni watu waliosahaulika, kwa sababu wafugaji wanakuwa ni kama wakimbizi katika nchi yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema haya kwa sababu kumekuwa na migogoro mingi sana baina ya wafugaji pamoja na hifadhi zetu. Lakini tunashukuru kwa sababu migogoro mingi kati ya wafugaji na wakulima sasa imepungua kwa asilimia kubwa. Hata hivyo haya yote yanatokana na sababu kwamba Serikali haijaweka mkazo katika kuhakikisha maeneo yote ya malisho katika halmashauri zetu yametengwa. Haya ninayasema kwa sababu mamlaka zetu hazijasimamia kuhakikisha kila halmashauri kutenga maeneo maalumu kwa ajili ya malisho. Hii imesababisha migogoro kuendelea kila siku katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayasema haya kwa mifano hai. Tuna mifano ya wafugaji ambao wamekuwa wakikamatwa mara kwa mara na mifugo yao ikiendelea kutaifishwa na kupigwa minada. Baada ya kutaifishwa na kupigwa minada wafugaji wanabaki wakiwa maskini, kitu ambacho kinasababisha wale wafugaji waone kwamba kazi ya ufugaji si kazi ya kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu sasa kwa Serikali, niombe sasa mamlaka husika wakasimamie maazimio ya mikutano ilifanyika baina ya wadau wa ufugaji pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye aliongoza ule mkutano uliohudhuriwa na Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya; kwamba kila Wilaya sasa iende ikatenge maeneo ya malisho ili kuondoa migogoro. Migogoro hii inasababisha mifugo mingine kukatwa, kujeruhiwa na kufa. Migogoro hii imesababisha hata wafugaji wengi kupoteza maisha na wengine kuwa walemavu. Kwa hiyo niombe sana mamlaka hizi zikasimamie ili walau wafugaji waone wana haki ya kufuga na kujipatia kipato katika familia zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, nipende kugusia suala zima la utambuzi, usajili na ufatiliaji. Tusiposimamia suala hili katika nchi yetu tuna uhakikia hata masoko ya nje hatutaenda kufanya vizuri. Mheshimiwa Waziri ameeleza hapa kwamba utaratibu wa kuweka hereni katika mifugo ulisitishwa; lakini sasa, mkakati wa Serikali ni nini? Tunaendaje kutambua mifugo yetu? Tusipofanya hivi ni lazima sisi hatutaingia kwenye soko la ushindani na hatma yake hatutaweza kuingiza kipato katika nchi hii na masoko yetu hayatakubaliwa. Tukiweza kuwatambua wanyama wetu itatusaidia kuweka mkakati na kuwatambua, kwa mfano, suala la usalama kwa wanyama wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, wale wanyama kuna nchi zingine bila kuwa na hereni hawawezi kupokea mnyama, hawakubaliki kwa sababu hawatambuliki na hawana uthibitisho. Kwa hiyo niombe Serikali sasa ije na mpango ambao hautakuwa na maumivu kwa wafugaji ili suala hili la kuweka alama na kuwatambua wanyama wetu iende kwa urahisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, pamoja na kuwa na mifugo mingi katika nchi yetu, lakini kama nchi tumeshindwa kupata faida kubwa kutokana na mifugo. Hii ni kwa sababu sisi hatujawekeza lakini tumekuwa na ushuru na utitiri mwingi wa tozo katika nchi yetu ambayo inafanya wafanyabiashara wengi wa nyama kushindwa kufanya biashara ya nyama.

Mheshimiwa Naibu Spika, natoa mfano; ukiangalia tozo zilizopo katika nchi yetu na nchi jirani ya Kenya, Tanzania kuna tozo zaidi ya kumi lakini wenzetu wa Kenya wenyewe wana tozo tatu. Hii inasababisha na kurahisisha sasa hata mfanyabiashara wa nyama wa Tanzania kuona ugumu kufanya biashara Tanzania na kukimbia nchi za jirani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ghrama zetu pia ziko juu sana. Kwa mfano suala la kuchinja mbuzi; Tanzania tunachinja mbuzi kwa shilingi 6,500 lakini Kenya wao wanachinja kwa 150 ambayo ni sawa na shilingi 2,700 kwa bei ya Tanzania. Hili suala naomba Wizara iliangalie ili kurahisisha wale wafanyabiashara wanaosafirisha nyama waweze kufanya biashara hii zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile kuna tozo ambazo hata hazina umuhimu sana. Kwa mfano autonics certificate kuna hizi za meat crown ambazo zingeweza kufanywa kupitia zile tozo za uchinjaji ili kumrahisishia mfanya biashara aweze kufanya biashara bila kupata maumivu yoyote. Pia suala pia la usafirishaji limekuwa la gharama kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nizungumzie namna Wizara inavyoweza kufanya ili kuweza kuinyanyua hii sekta ya mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu, kwanza kuhusu minada. Minada yetu haimpi faida mfugaji, anayepata faida ni yule anayeuza nyama. Mfugaji anapokwenda mnadani kuuza nyama hawatumii kipimo chochote isipokuwa ni makubaliano tu, kwamba huyu ng’ombe anafaa kuuzwa laki tano au milioni; lakini yule anayeuza nyama lazima aweke kwenye kilo. Kwa hiyo moja kwa moja ukiangalia mfugaji hapati faida, anayepata faida ni yule anayeuza nyama. Sasa, niiombe Serikali iweke mizani katika minada yetu ili ng’ombe wapimwe kilo wakati wa mauzo, walau hata sasa na mfugaji anaweza akapata faida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni ombi, hasa katika Mkoa wetu wa Manyara. Kwamba, katika miaka miwili mitatu tumekumbwa sana na suala la ukame. Niiombe Serikali iwachimbie wafugaji mabwawa ya kutosha ili inapofika msimu ule wa ukame wanyama waweze kupata maji ya kutosha na waweze kuhimiri... (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze katika kuchangia katika Wizara hii ya Kilimo. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuona kwamba kilimo ndio kipaumbele katika nchi yetu, ukizingatia kwamba wananchi wetu wengi asilimia 60 wanajihusisha na shughuli nzima ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuipongeza sana Wizara nimpongeze kaka yangu Hussein Bashe Waziri wa Kilimo pamoja na Naibu Waziri kwa kufanya kazi kubwa kuhakikisha kilimo kinaenda kusonga mbele. Kwa kupitia Mawaziri hawa tulionao nina uhakika kutakuwa na mapinduzi makubwa katika sekta hii ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, usalama wa nchi yetu unategemea usalama wa chakula na usalama wa chakula unategemea kuwa na mbegu bora na mbegu bora upatikana kwa Serikali yetu kuamua tuzalishe mbegu hapa nchini. Asilimia 45 ya mbegu ya mahindi hutoka nchi za nje, lakini asilimia 95 mbegu ya mboga mboga inazalishwa nchi za nje. Hivyo basi inapelekea tunapokea mbegu ambazo si bora na wakulima wengi wanapopata zile mbegu na kwenda kufanya shughuli za kilimo uzalishaji unapungua siku hadi siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali iwekeze katika utafiti. Tukiwekeza katika utafiti tutawasaidia wakulima wadogowadogo. Sasa hivi wakulima wetu wanafanya kilimo kisichokuwa na tija. Wanalima bila ya kuelewa ardhi hii inastahili kuotesha nini, kwa sababu hawajui udongo ule unafaa kwa zao lipi. Kwa hiyo niombe sana Serikali iwekeze sana katika Vituo vyetu vya Utafiti ili wananchi wetu wapewe elimu kulingana na ardhi iliyopo. Wananchi wetu wapewe elimu kuangalia ni mbegu gani inastahili kuoteshwa katika eneo hilo, tukifanya hivi tutawasaidia wakulima wengi na hatimaye suala zima la kilimo kitakuwa kinapanda siku hadi siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la utafiti, Vituo vyetu vya Utafiti havifanyi kazi vizuri hii ni kwa sababu kuna kodi kubwa katika vifaa vile vya utafiti. Niiombe Serikali ipunguze au iondoe kabisa kodi katika vifaa vile vya utafiti. Utashangaa sana katika Serikali yetu hata vifaa vinavyoletwa na taasisi za kiserikali vinatozwa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ambalo linapelekea vituo vyetu vya utafiti vinashindwa kufanya kazi. Sasa ni muda muafaka tuelekeze kwenye suala zima la utafiti, nina uhakika tutafanya mapinduzi makubwa katika suala zima la kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Serikali kuwekeza katika kilimo cha mbogamboga na matunda (horticulture). Sasa hivi kuna mwamko mkubwa sana kwa wananchi hasa vijana wengi na akinamama, wamepata mwamko mkubwa wa kujishughulisha na shughuli nzima ya kilimo cha horticulture, kwa sababu ni kilimo pekee ambaye unapata matokeo kwa muda mfupi, ni miezi mitatu hadi miezi sita unapata mavuno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuwekeza kule, tatizo kubwa lililopo ni kwamba hawana mitaji na hawana vitendea kazi. Naiomba Serikali iwekeze kule ili angalau vijana wengi na akinamama wengi waweze kujiajiri na kukuza mapato yao ili kuendeleza maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine niendelee kuipongeza Serikali kwa kuweka msukumo mkubwa katika kilimo cha umwagiliaji. Hii hapa itasaidia sana wananchi kujikwamua kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, si kila jambo litafanywa na Serikali, niiombe Serikali iweze kuondoa kodi katika mitambo ya uchimbaji wa mabwawa ili wananchi wenyewe au wakulima waweze kununua hiyo mitambo na kuweza kujishughulisha na shughuli za umwagiliaji. Ukiondoa kodi katika mitambo ya uchimbaji itapunguza bei kwa asilimia 30 hadi 40. Kwa hiyo tuwasaidie wakulima wetu ili waweze kununua mitambo hiyo na kujishughulisha na shughuli nzima kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufikia hapa naomba niunge mkono hoja. Nashukuru. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia mpango wa Serikali. Kwa kuanza, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo anaendelea kuipambania nchi yetu kwa kutuletea maendeleo katika kila sekta. Lakini nimpongeze sana kwa kurejesha Tume ya Mipnago, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kuanzisha Wizara hii ya Mipango. Kupitia Wizara hii ya Mipango, tunaamini kabisa kwamba sasa maendeleo na mipango itaenda kupangika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta inayobeba watanzania wengi ni kilimo, uvuvi na ufugaji, na mimi nimeweza kupitia katika ripoti ya kamati na niungane na kamati kwamba bado kasi ya sekta ya umwagiliaji iko chini mno. Serikali inahitaji kuwekeza kwa kiwango kikubwa katika sekta hii ya umwagiliaji, kwa sababu nchi yetu mpaka sasa suala la mvua sio suala lenye mashaka. Kwa hiyo, Serikali ikiwekeza kwenye kilimo cha umwagiliaji tuna uhakika wa kupata chakula cha kutosha lakini pia sekta ya mifugo itakwenda kustawi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sio kila jambo lazima Serikali ifanye, Serikali inaweza kutengeneza mazingira wezeshi katika private sector, wakawekeza katika private sector kwenye sekta hii ya umwagiliaji. Uwezeshaji wake huo ni kupunguza kodi katika mitambo ya uchimbaji wa visima na mabwawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiweza kupata mabwawa ya kutosha, tuna uhakika wafugaji watafuga vizuri. Tuna uhakika tunaweza kufuga Samaki, tuna uhakika tutapata maji kwa ajili ya matumizi ya binadamu. Lakini hivyo hivyo tukiweza kuwekeza kwenye visima tutakuwa tumetatua tatizo la kilimo na uzalishaji. Kwa hiyo, ushauri wangu mkubwa ni kwamba bado Serikali iwekeze kwa nguvu kubwa katika kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali na kuishukuru sana kwa kuendelea kutupatia mbolea ya ruzuku, kwa sababu wananchi wanapata mbolea, lakini bado ninatamani kuona kwenye mpango, Serikali iende kwenye kuwekeza katika viwanda vinavyochakata gesi asilia. Tukiwekeza kwenye viwanda vya kuchakata gesi asilia tunapata nishati mbadala lakini tunapata mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi nchi yetu tunaagiza mbolea aina ya urea nje ya nchi kwa asilimia mia moja, jambo ambalo linafanya gharama kubwa Serikali kuagiza hiyo mbolea ya urea, lakini tukizalisha hapa nchini ni uhakika kwamba mbolea hiyo itapatikana kwa urahisi na wananchi watakuwa wamepata hiyo mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunatakiwa kuwekeza kwenye matumizi ya mbolea ya asili kama mbolea ya samadi na mboji kwa kuwaelimisha wananchi wakulima na wafugaji kwamba baada ya mavuno zile takataka za mashambani, wapewe elimu namna ya kuhifadhi na baadae kuzitumia kama mbolea katika kilimo. Pia, mbolea ya samadi tunaweza kupata kupitia mifugo, mifugo nchi hii bado ni mingi sana lakini wananchi bado hawajapata elimu ya kutosha namna gani tunaweza kutumia mbolea ya samadi katika kilimo chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia inaweza kuwekeza katika majiji makubwa kama Jiji la Dar es Salaam, Jiji la Dodoma, Jiji la Mwanza, kwa sababu haya majiji makubwa kuna ukusanyaji mwingi wa taka ngumu, lakini Serikali ikiamua kuwekeza kwa kupitia viwanda, tukawekeza kwenye kuchakata taka ngumu kupata nishati mbadala, hapo hapo tuna uwezo wa kupata mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, badala ya taka ngumu kutupwa na kuziba mitalo na nini. Serikali ianzishe viwanda ambavyo vitaweza kuchakata hizo taka ngumu ili kujipatia nishati mbadala, lakini pia tuna uwezo wa kuzalisha mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wetu hasa wakulima wadogo wadogo wamekuwa wakilima kilimo kisicho na tija na hii inasababishwa na nini? Hii inasababishwa na kwamba wakulima wanalima bila kujua ardhi yao inahitaji kustawishwa mazao ya aina gani. Wakulima wanalima bila kujua kwamba udongo ule unafaa kustawisha mbegu za aina gani na hii kazi ilitakiwa ifanyike, kwamba maabara zetu zifanye kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, maabara zimewekwa katika ofisi za kanda, maabara ziko mbali na wananchi. Mfano, sisi Mkoa wa Manyara, maabara tunayoitegemea ni maabara iliyoko Arusha Serian Tengeru au uende Tanga. Jambo ambalo unampa mkulima gharama kubwa kwenda kufanya vipimo vya udongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, amewawezesha Maafisa Ugani pikipiki pamoja na vifaa vya kupimia udongo lakini jambo la kusikitisha sana, Maafisa Ugani mpaka sasa ukienda kuuliza huko kwa wakulima kazi hiyo haifanyiki. Kwa hiyo, wakulima wamekuwa wakilima bila kujua kwamba udongo wake unatakiwa kustawisha zao gani lakini mbolea ya aina gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri ifike wakati Maafisa Ugani warudishwe chini ya Wizara ya Kilimo ili waweze kusimamiwa ipasavyo, kwa sababu sasa hivi wanawajibika kwa Mkurugenzi, jambo ambalo linakuwa gumu sana kuwafuatilia mpaka ngazi za chini. Hivyo, wakulima wadogo wanatakiwa wapewe elimu kwa sababu wakulima wakubwa wana uwezo wa kupeleka hizo sample za udongo katika maabara na kuweza kufanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nishauri vile vituo vyetu vya utafiti viboreshwe, hata vile vifaa vinavyotumika bado havikidhi haja. Wakati mwingine hawapati majibu yanayoendana na uhalisia. Hata mtu akisema apeleke udongo, ukiwa na hekari kumi, ukichukua udongo wa sehemu moja yawezekana ndani ya hekari kumi labda una udongo wa aina tatu, kuna udongo wa kichanga, labda una mfinyanzi, ukipeleka udongo wa aina moja maana yake hutapata matokeo mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kilimo cha mbogamboga. Kilimo hiki cha mbogamboga ni kilimo ambacho watu wanalima bila kuwa na usimamizi hawana bodi ni watu wanaamua kujilimia tu lakini ndio kilimo ambacho kinazalisha kwa wingi zaidi, kwa hiyo niombe Serikali iwawezeshe wakulima wadogo wadogo kupata mbegu kwa urahisi.

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kumetokea…

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Ndege kwa mchango mzuri.

MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)