Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Esther Edwin Maleko (12 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ESTHER E. MALEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuzungumza katika Bunge hili, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, niwashukuru sana Chama changu Cha Mapinduzi kwa kunipa nafasi kwa kuteuliwa kugombea. Zaidi niwashukuru akinamama wa Kilimanjaro kwa imani kubwa waliyonipa, wakanipa kura za kishindo na mimi nikaweza kuwa Mbunge wao na kuja kuwawakilisha katika Bunge hili Tukufu. Pia nisiwasahau wazazi wangu, mume wangu, watoto wangu, ndugu jamaa na marafiki, kwa namna walivyonisaidia kwa maombi na kwa ushauri mpaka leo niko hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kuchangia katika hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa wakati anafunga Bunge la Kumi na Moja, lakini wakati anafungua Bunge la Kumi na Mbili Novemba 13. Katika hotuba yake Mheshimiwa Rais ambayo imetoa dira, mwelekeo na mustakabali wa Taifa, Mheshimiwa Rais alisema katika ukurasa wa 10 kwamba wataongeza jitihada za kuwasaidia wananchi kiuchumi kwa kuwapa mikopo ambayo haina riba au yenye riba kidogo. Naomba basi niende moja kwa moja kuishauri Serikali yangu sikivu, ifanye utaratibu wa namna gani hiyo mikopo ambayo inatolewa na halmashauri 4% kwa wanawake, 4% kwa vijana na 2% kwa wenye walemavu, iangalie basi ni namna gani mikopo hiyo inaweza kuongezwa. Zaidi ya hapo iangaliwe ni namna gani mikopo hiyo haitatolewa kwa masharti ya kupewa kwa vikundi, ikatolewe kwa mtu mmoja mmoja kwa sababu ni wanawake wengi ambao wanahitaji mikopo hiyo lakini wakati mwingine wanakosa kwa sababu ya masharti ambayo yamewekwa kwamba ni lazima mkakope kwa vikundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu najua Serikali yangu ni sikivu naamini itazingatia suala hilo na kwasababu akinamama wa Kilimanjaro wengi ni wakulima, lakini wengi ni wafanyabiashara wakipatiwa fursa hiyo adhimu wataweza kukwamua familia zao. Kama unavyofahamu mwanamke ndiye anayeinua uchumi wa familia, hivyo mwanamke akiguswa familia itaguswa lakini pia na Taifa litakuwa limeguswa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nisiache kulisema hili pia, kule kwetu Kilimanjaro akinamama wengi wanauza ndizi lakini ndizi haina bei kabisa inapopelekwa sokoni. Mwanamke anapopeleka ndizi sokoni anaenda kuiuza kwa shilingi elfu moja na wakati mwingine wanunuzi wanamkopa, anaweza kukaa na hiyo ndizi ikaiva kwa hiyo hivyo inabidi aitoe kwa wale wanunuzi ambao wao wakienda kuiuza wanaenda kuiuza kwa zaidi ya shilingi elfu ishirini na tano. Basi tuone ni namna gani tunaweza kuwapatia akinamama hawa elimu ya namna gani wanaweza kuchakata ndizi hizo na wakaweza kupata kipato zaidi na siyo kuonewa kwa namna ambavyo wanaonewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hali ya hewa ya Kilimanjaro tunaweza kulima kilimo cha mbogamboga, kilimo cha bustani. Naiomba Serikali yangu Tukufu iweze kuongeza bajeti kwenye Wizara ya Kilimo ili sasa wanawake hawa ambao ni wakulima wapate elimu bora juu ya kilimo hicho wanacholima kwenye matunda, kwenye mbogamboga na tukaende kuongeza pato la Taifa. Kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais amesema leo Tanzania iko nafasi ya 20 kidunia kwa kuzalisha mazao haya, lakini imeingiza zaidi ya dola milioni 412 kwa mwaka 2015; mwaka 2018/2019 imeingiza zaidi ya dola milioni 779. Je, hatuoni…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda wako umeisha Mheshimiwa.

MHE. ESTHER E. MALEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa fursa hii ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Elimu. Kwanza nianze kwa kutoa pongezi nyingi sana kwa utekelezaji wa elimu bila malipo kwa sababu kwa sasa wanafunzi ambao wanahitimu wameongezeka na wataendelea kuongezeka kwa kasi kubwa. Sasa ni vyema basi Serikali ijipange ni namna gani basi itaweza kukabili mahitaji haya makubwa ya miundombinu ambayo tayari imeanza kuelemewa. Wizara imeomba kuidhinishiwa kiasi cha shilingi trilioni 1.384 ambazo zina ongezeko la shilingi bilioni 42.4 ikilinganishwa na bajeti ya mwaka 2020/2021, nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya fedha hizo matumizi ya kawaida ni bilioni 480.5 ambayo ni sawasawa na asilimia 34.7 na maendeleo ni bilioni 903.9 ambayo ni sawasawa na asilimia 65.3 tunawapongeza sana kwa uwiano huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kati ya fedha hizo fedha za maendeleo ni bilioni 403, lakini bilioni 500 zinakwenda kwenye mikopo ya elimu ya juu. Sidhani kama ni sahihi fedha za mafunzo au training kuitwa fedha za maendeleo maana matumizi yake ni ya kawaida na matumizi ya fedha za maendeleo hayawezi kwenda kuwekwa kwenye fedha ambazo tunasema zinapelekwa kwenye mikopo ya elimu ya juu. Kwenye mafungu mengine ya fedha za kugharamia mafunzo ziko recurrent, ndio maana fedha zisipotolewa zote kinacho-suffer ni ile miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, katika mwaka huu mpaka Machi, 2021 miradi sita tu kati ya miradi 33 ya mikakati ya maendeleo ndio imepata fedha, lakini hii mingine mpaka sasa haijapata. Miradi hiyo ni EP4R na Equip T haijapata chochote mpaka sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu, ni vyema basi zile fedha za mikopo ya elimu ya juu zipewe fungu lake tofauti ya kujitegemea ili zile fedha za miradi zisiweze kuguswa na ziende kwenye ile miradi, ili iweze kutekelezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo linguine, TAMISEMI tunaomba waboreshe ushirikiano kati yao na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ili waweze kushirikiana vyema kutoa huduma hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, sina uhakika sana kama Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia wanajua mahitaji makubwa ambayo yanatokana na kuanzisha utekelezaji huu wa elimu bila malipo. Kwa sababu katika kipindi hiki cha miaka minne tutakuwa tunahitaji madawati 41,333; tutakuwa tunahitaji matundu ya vyoo 75,300; vitabu 18,000,825; na walimu 41,833; na fedha za ruzuku ya wanafunzi bilioni 1,882,000,500; ambayo hiyo ni sawa na trilioni 1.476 ili kuweza kukamilisha shughuli hii ya wanafunzi watakaoongezeka katika kipindi hicho cha miaka minne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunaomba ushirikiano bora kati ya TAMISEMI, watakaowasaidia kufuatilia miradi inayotekelezwa kwenye wilaya mbalimbali mfano VETA na vyuo vikuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kufikia hapo, huo ndio mchango wangu. Naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuchangia kwenye Wizara ya hii ya TAMISEMI. Moja kwa moja nijikite kuchangia upande wa elimu. Naipongeza sana Serikali yangu sikivu kwa kuweza kusimamia kujenga shule kwenye kila kata. Suala hili la kuwa na shule kwenye kila kata limetupunguzia adha kubwa ya wanafunzi kupata au kwenda mwendo mrefu kwa ajili ya kwenda shule. Pamoja na Serikali kufanya kazi hii kubwa ikatenga shilingi bilioni 23 kila mwezi kwa ajili ya elimu bure, imefanya kazi kubwa sana naipongeza sana Serikali yangu. (Makofi)

Mhehimiwa Spika, naomba kutoa ushauri kwa Serikali yangu sikivu, kwamba baada ya kujenga shule hizi kwenye kila kata, tuangalie sasa ni namna gani tunakwenda kujenga hostel, mabweni kwenye kila kata sasa ili wale wanafunzi ambao wanatoka umbali mrefu wasipate shida njiani. Nasema hivyo kwa sababu wanafunzi wa kike wanakutana na vishawishi vingi wakati wanakwenda shule. Wakati mwingine kutokana na umbali wanaokwenda wanaweza kurubunika katikati hapo wakaingia kwenye mitego mingine mingi kwa sababu wanaona muda wa kwenda shuleni na kufika kwa wakati unakuwa ni kidogo. Kwa hiyo naiomba Serikali yangu sikivu iweze kuangalia ni namna gani sasa tumemaliza kujenga shule za kata, tunatoa elimu bure, lakini namna gani tunaweza kujenga mabweni ili wanafunzi hawa waweze kupata elimu sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ule muda wanaotoka shule na kurudi nyumbani wanatumia muda mrefu, lakini wangekuwa shuleni wangeweza kusoma kwa bidii, wakapata muda wa kusaidiana na wenzao, wakapata muda wa kufundishwa zaidi, tofauti na hapa ambapo leo wanatoka shule, wanakwenda nyumbani, wanakuta nyumbani kuna kazi ambazo watasaidia wazazi, kwa hiyo wanakosa muda wa kujifunza kwa muda mrefu. Naomba sana dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu sina mashaka naye, najua yeye pamoja na wasaidizi wake wataliangalia hili.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema kuhusu wanafunzi, niseme kuhusu Walimu. Walimu hawa wanatusaidia kuangalia watoto wetu, tunaenda makazini na tunafanya kazi zetu kwa sababu tunajua wapo walimu ambao wanatunza watoto wetu, lakini walimu hao hao wamesahaulika, kiwango chao cha malipo kipo chini. Ni lazima sisi kama Bunge Tukufu tuweze kuangaliana kuwapigania Walimu hawa ili waweze kuongezewa mishahara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, si hivyo tu, Walimu hawa wanakwenda masomoni wakiwa shuleni. Wanapokwenda masomoni wengine wanaobaki shuleni ambao wanaendelea na kazi wanaongezwa mishahara au kupandishwa vyeo, lakini hawa walikwenda kujiendeleza pamoja na kwamba wanajiendeleza kwa pesa zao, tena kwenye kima kile cha mshahara mdogo wanaolipwa, wanaweza kwenda kujiendelea ili wafanye kazi kwa ufanisi mkubwa, lakini shida inatokea wao wakiwa masomoni wenzao wanapandishwa mishahara, wanapandishwa madaraja, lakini wao hawapandishwi wakiwa masomoni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali yangu sikivu iweze kuwaangalia hao Walimu, imekuwa ni kada ambayo imeachwa nyuma, ni kada ambayo haiangaliwi, wengine wakienda masomoni wakirudi mishahara yao inaongezeka, lakini kwa hao walimu ambao wanatuangalizia watoto wetu, hao walimu wanaotusaidia kufuta ujinga, wamesahaulika. Kwa hiyo naiomba Serikali iangalie pia suala hilo la Walimu. (Makofi)

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika. Taarifa.

SPIKA: Uko wapi?

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, niko hapa!

SPIKA: Endelea.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, suala la mishahara na suala la kutokupandishwa vyeo wakiwa shule sio Walimu tu ni watumishi wote Tanzania. Naomba kumpa taarifa hiyo.

SPIKA: Unaipokea taarifa hiyo, Mheshimiwa Esther E. Malleko.

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, ahsante naipokea taarifa hiyo.

Mheshimiwa Spika, kero nyingine kwa Walimu, ni kero kubwa kwa wale Walimu wanaostaafu. Baada ya kustaafu anapotakiwa kubeba mizigo yao na kurudi nyumbani kwao inakuwa wanacheleweshewa kupata yale malipo na hii inaendelea kukatisha tamaa kwa sababu hao watu wamefanya kazi hiyo kubwa kwa maisha yao yote, lakini wanapofika wakati wa kustaafu bado hata ile hali ya kuangaliwa waweze kurudi nyumbani kwao imekuwa ni shida.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nichukue nichukue nafasi hii kumpongeza sana Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuitenganisha Wizara hii na Wizara ya Afya, hakika ameitendea haki ili iweze kusimamia maendeleo ya jamii, kwa kuwa Wizara hii imebeba mwanga wa vizazi vyetu kwa maana jinsia wazee, watoto, na makundi maalum ndio ukamilifu wa maisha ya mwanadamu.

Mheshimiwa Spika, tukielekea kupitisha bajeti hii muhimu ni ukweli usiopingika nchi yetu imepitia vipindi kadhaa vya udhalilishaji wa kijinsia hasa kwa na watoto katika maeneo mbalimbali. Kiukweli katika dunia ya sasa watu wameshabadilika kutoka kwenye dhana ya unyanyasaji wa kijinsia, badala yake wanapigania kuyakuza makundi mbalimbali kwa kuyaongezea nguvu na uwezo hasa wanawake na watoto.

Mheshimiwa Spika, tafiti za hivi karibuni zilizotolewa na Jeshi la Polisi nchini ambao ni chombo kinachohusika kupokea matukio mengi ya unyanyasaji wa kijinsia inaeleza kuwa mpaka Juni, 2021 tayari watu 15,131 walikuwa wamefanyiwa ukatili wa kijinsia hasa wanawake waliouawa katika ndoa. Pia ripoti iliyotolewa Septemba, 2021 na Jarida la Afrika kuhusu hali ya ukatili wa kijinsia Tanzania imeonesha kuwa asilimia 46 ya wanandoa hufanyiwa ukatili wa kimwili na asilimia 32 walifanyiwa ukatili wa kisaikolojia na asilimia 13 wanafanyiwa ukatili wa kingono.

Mheshimiwa Spika, Mungu ameliwezesha Taifa letu kwa kulionesha kuwa mwanamke anaweza kufanya mambo makubwa yanayobeba na kuiheshimisha jamii kwa kutupa Rais mwanamke Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ambaye anatupa tafsiri kuwa mwanamke sio kiumbe anayestahili kunyanyaswa, bali anastahili kuungwa mkono na kufunguliwa milango ya fursa. Sasa inasikitisha sana kuona namna Taifa letu linavyojipambanua juu ya kuheshimu nafasi ya mwanamke na haki za Watoto, lakini jamii zetu zimekuwa kimya juu ya ukatili huu unaojitokeza.

Mheshimiwa Spika, sasa Wizara ihakikishe inaimarisha uelewa wa Watanzania juu ya kulinda haki za watoto na wanawake kila mahala sambamba na kuwawezesha wanawake na watoto kuweza kujitambua. Kuwe na madawati katika shule za msingi na sekondari yawepo kusaidia watoto hawa kutoa taarifa kwenye mazingira rafiki maana wengine wanaogopa kwenda polisi kwa hofu.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. ESTER E. MALEKO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu sana ya Kilimo. Kwanza naipongeza Wizara kwa hotuba nzuri, lakini nijikite moja kwa moja kwenda kuzungumzia changamoto zinazokabili sekta hii ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, sekta hii ya kilimo inaajiri zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania na pia inatoa pato la asilimia 29 kwenye pato la uchumi wa Taifa, lakini hii ndiyo sekta yenye changamoto kubwa kuliko sekta nyingine zozote. Tunategemea tutapata ajira kutoka kwenye sekta hii, lakini hatujaweka mkazo mkubwa kwenye hii sekta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa sababu gani? Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2022 katika ukurasa wake wa 33 imeeleza kwa kirefu mikakati ya kukifanya kilimo cha kisasa na cha kibiashara chenye tija na ambacho mazao yake yatakuwa yameongezwa thamani, lakini shida kubwa pamoja na hayo, ni masoko. Wakulima wengi wanalima lakini hawajui mahali pa kuuza mazao yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka Mheshimiwa Rais wetu Hayati John Pombe Magufuli alipokuwa anahutubia Bunge tarehe 13 Novemba, 2020 alisema anaomba Wizara ya Kilimo, Wizara ya Biashara na Wizara ya Mambo ya Nje ikishirikiana na Mabalozi waweze kukutana ili kuangalia ni namna gani wanaweza kutatua changamoto zinazokabili kilimo. Ninaamini kabisa Wizara hizi zikikutana zikaweza kuweka mawazo yao ya pamoja tutaenda kutatua changamoto kubwa ya kilimo inayowapata wananchi wa Tanzania. Wengi wanalima lakini hawajui watauza wapi mazao yao.

Mheshimiwa Spika, inawezekana kutokana na uelewa mdogo au kutokujua namna gani ya kuongeza thamani ya mazao yao, wanakuja wafanyabiashara kutoka nje ya nchi; nchi za Jirani hapa, wananunua mazao yanayolimwa hapa Tanzania, wanakwenda wanayaongezea thamani, wanauza nchi za nje na wanapata fedha nyingi, lakini wakulima wanaolima ambao wanatoka Tanzania wanaendelea kubaki nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaiomba sana Wizara ya Kilimo inayoongozwa na kaka yangu Mheshimiwa Prof. Mkenda, ninajua wewe na ndugu yangu Mheshimiwa Bashe ni viongozi makini sana, muende mkaliangalie suala hili kwa makini, wakulima wetu wanapata changamoto kubwa sana, wanaishia kufanya kilimo ambacho hakina tija, wanaishia kulima lakini hawana faida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo Benki ya Kilimo haiwasaidii wakulima wadogo. Inanufaisha wakulima wakubwa na wakulima hawa wadogo ndio tunaotegemea waende kuinua kipato chao na kuchangia kwenye pato la Taifa. Wanachangiaje sasa ikiwa hata hii benki ambayo imewekwa mahususi kwa ajili ya kuwasaidia, haiwasaidii?

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kubwa ambalo linakwaza kwenye kilimo ni upatikanaji wa mbegu bora. Wizara ya Kilimo, nimesikia kwenye hotuba yenu, mmetenga bajeti na mtasimamia kuhusu upatikanaji bora wa mbegu za kilimo, tunaomba mwahamasishe wakulima ni namna gani wanaweza kwenda kulima mbegu bora na sisi tukaweza kupata mbegu zinazohitajika hata tukaacha kulia kama tunavyolia leo nchi haina mafuta, tunaenda kuagiza nchi za nje.

Mheshimiwa Spika, leo tukilima kilimo hiki cha alizeti, ninaamini suala hili la kulia mafuta, mafuta, litakwisha. Haiwezekani nchi kubwa kama Tanzania yenye zaidi ya asilimia 44 ya ardhi yake inafaa kwa kilimo, lakini bado sisi tunaendelea kuagiza mafuta nje ya nchi. Ni aibu kubwa sana. Naomba sana Wizara ya Kilimo iangalie namna ya kuwapatia wakulima mbegu bora na ziwafikie kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, pia suala la Maafisa Ugani, hili ni tatizo lingine. Leo hii Chuo cha Kilimo SUA kinatoa wataalam, lakini kwa sababu wanaona sekta hii haiwalipi, wanaenda kuajiriwa benki badala ya kwenda kusaidia wakulima hawa ambao ndiyo tunasema tutapata ajira, tutakomboa vijana, tutakomboa wanawake ambao wanateseka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siyo hivyo tu, katika mazao saba ya kimkakati yaliyowekwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2025, kuna zao la mkonge. Zao hili linalimwa pia Kilimanjaro, lakini asilimia kubwa ya wananchi hawa wa Kilimanjaro hawajui vizuri juu ya suala hili. Naiomba basi Wizara iangalie namna ya kuwapatia akina mama na vijana fursa ya kuweza kulima zao hili. Zaidi ya yote, tunalima hili zao la kimkakati, lakini pia tunahitaji kufufua kiwanda cha magunia kilichoko Moshi, kwani kimekufa. Tunasemaje tunaenda kutafuta mazao ya kimkakati, tunaenda kuzalisha bidhaa, lakini kile kiwanda ambacho kinatumika kuzalisha bidhaa hizo, hakipo; lakini tuna malighafi na hatuna mahali pa kwenda kuzipeleka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kiwanda cha Magunia cha Moshi ni tatizo. Kimechukuliwa na mwekezaji, lakini mpaka sasa hakijaendelezwa, lakini leo tunasema zao hili ni la kimkakati na pale Kilimanjaro tunataka wakulima wetu waende kulima zao hili. Wapolima, tunategemea wakauze pale na kiwanda kile kiweze kuboreshwa kisitengeneze tu magunia, kikatengeneze na vitu vingine ambavyo vinatokana na zao la mkonge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naishukuru Serikali kwa kuona umuhimu wa kufufua kiwanda cha Kilimanjaro Machine Tools. Huko tutapata vipuri vya matrekta, ma-Power Tiler, lakini hivi hivi ndiyo vitakavyoenda kuwasaidia wakulima wa Kilimanjaro.

Mheshimiwa Spika, Kilimanjaro tunalima ndizi na parachichi. Katika kulima ndizi, wakulima wetu mfano wanaotoka Jimbo la Hai wanauza mazao yao ya ndizi katika soko la Kwa Sadala, lakini soko hili limekwisha kabisa, hawawezi hata kuhifadhi vitu vyao. Mvua ikinyesha, ni shida hata mchuuzi kuingia kwenye lile soko kwenda kununua bidhaa. Ninaiomba Wizara iangalie kwa jicho la tofauti soko hili la Kwa Sadala ambalo linawasaidia akina mama wengi na vijana, kujikwamua kiuchumi waweze kupata…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ESTER E. MALEKO: ahsante sana naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ESTER E. MALEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika Wizara hii nyeti ya Maliasili na Utalii. Kwanza nianze kwa kutoa pongezi kwa Waziri Mheshimiwa Dkt. Ndumbaro pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Mary Masanja kwa kazi nzuri wanayoifanya. Pia nitoe pongezi za dhati kwa timu nzima ya Wizara kwa sababu wamekuwa wakifanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye kuchangia kwa sababu mud ani mfupi sana. Naomba nichangie kupitia utalii kwa sababu kwa kwetu sisi Tanzania ni nchi ya pili duniani kwa kuwa na vivutio vingi vya asili ikianza Brazil ambayo ni nchi ya kwanza duniani kuwa na vivutio vingi vya asili. Pamoja na hayo sekta hii ya utalii inachagia pato la 17% katika pato la Taifa. Si hivyo tu, inachangia ajira zisizopungua milioni 1.6, zile za moja kwa moja na ambazo siyo za moja kwa moja. Kwa hiyo, Wizara hii ni nyeti kwa sababu pia inaingiza asilimia 25 ya fedha za kigeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwenye kuchangia kwenye vivutio vyetu vya asili. Tuna kivutio kikubwa sana katika Mkoa wetu wa Kilimanjaro. Kivutio hiki ni mlima Kilimanjaro, mlima huu kwa takriban watalii 45,000 mpaka 50,000 wanapanda kwa mwaka. Hata hivyo, kiikolojia mlima huu unaweza kupokea takriban watalii 300,000 kwa mwaka mmoja. Hivyo, unaona idadi ya watalii wanaopanda mlima huu ni 45,000 mpaka 50,000, ina maana kuna nafasi hapo ambayo hatufanyi vizuri. Nadhani hatutangazi vizuri mlima wetu au matangazo yako chini sana, kwa hiyo tujitahidi sana kutumia media. Leo media ni kitu kikubwa sana, watu wanashinda kwenye media, tukiweza kutumia tu Instagram kuutangaza mlima wetu, ambapo hatutumii gharama yoyote kubwa, tunaweza kuutangaza kwa kiasi kikubwa lakini pia hatuwezi kutumia gharama kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tukachukua watu maarufu mfano Ronaldo, Messy na wengine wengi tukawafanya wao wakaja Tanzania, tusiwatoze hata senti tano, tukachukua wao wanapokuja Tanzania wakalala bure wakapata huduma zote bure, lakini yule mtu aka-post tu kwenye page yake yenye followers zaidi ya milioni 50 kwamba yuko Kilimanjaro, tayari tumetangaza mlima wetu na hatutumii gharama kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu, nimeona Wizara inafanya vizuri sana, wamemleta Mamadou kama balozi wa utalii, lakini si hivyo tu jana amekuja Zari the boss lady kama balozi wa utalii. Namshukuru Mungu nilipata nafasi ya kuzungumza naye na kubadilishana mawazo. Kama Mbunge ninayetoka Kilimanjaro nilimwalika aweze kuupanda Mlima Kilimanajro na amekubali, hivyo nawahamasisha Wabunge tuungane pamoja kwenda na Zari kuupanda Mlima Kilimanjaro kwa sababu sisi ni vivutio na sisi ni wawakilishi wa wananchi. Wananchi wakiona sisi tunaenda kupanda mlima Kilimanjaro, nao watahamasika na wataenda kupanda mlima. Kwa hiyo nawaomba Wabunge tuungane pamoja kupanda mlima Kilimanjaro. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu, tunapaswa pia kuboresha rescue system katika mlima wetu wa Kilimanjaro. Watalii wanapokuja wakapata shida wakiwa kule mlimani wanapaswa kupata huduma sahihi. Ninaposema rescue system iboreshwe, naamini Wizara inajua namaanisha nini. Kwa hiyo ninaomba Wizara iboreshe rescue system iwape wale watoa huduma elimu bora zaidi ili iweze kuwahudumia watalii wanaopata shida wakiwa kule mlimani.

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu tuwe na information center…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga.

MHE. ESTER E. MALEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Sasa Mheshimiwa Ester hujatuambia kama na wewe utakuwa unapanda, kwa sababu wako Wabunge hapa ambao watatamani kujua kama na wewe unapanda ili waambatane na wewe.

MHE. ESTER E. MALEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, nimewahamasisha kwa sababu na mimi nitakuwa mmojawapo kwa sababu nimemhamasisha Zari apande Mlima Kilimanjaro, nitakuwa pamoja nao. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia katika Wizara hii ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Spika, naomba kuchukua nafasi hii kuipongeza sana Wizara hususan Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Naibu wake pamoja na Watendaji wote kwa kazi nzuri wanayoifanya. Moja kwa moja niende kwenye hoja yangu kutokana na muda huu mchache.

Mheshimiwa Spika, napongeza sana Jeshi la Polisi kwa kazi nzuri wanayoifanya, lakini pamoja na kupongeza jeshi hili kwa kazi nzuri wanayofanya tunajua kazi kubwa ya Jeshi la Polisi ni kulinda rai na mali zake. Sasa, cha kushangaza hawahawa Polisi ambao tunategemea ndio watakaotulinda sisi na mali zetu sisi hatujui wao wanaishije. Nyumba zao ni mbaya na hazifanani na kazi kubwa wanayoifanya, lakini pia mishahara yao na posho zao haziendani na kazi wanazozifanya nah uku tukitaka wafanye kazi hii kwa weledi mkubwa. (Makofi)

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Esther Malleko, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jerry Slaa.

T A A R I F A

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya watoto wa line tulioko humu ndani napenda kumpa taarifa mzungumzaji kuwa hali ya makazi ya Polisi kusema kweli ni mbaya. Tangu zile za pale Ukonga, zile Police Hunger Officers Line, ile namba tano niliyozaliwa mimi, zile za File and Rank na zile za FFU hali ni mbaya. Naomba kumpa taarifa mzungumzaji. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Esther Malleko, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa hiyo kwa sababu ni kweli kwamba askari wetu wanafanya kazi kubwa sana lakini mazingira wanayoishi hayakidhi mahitaji wala viwango vya kuishi mwanadamu. Ukiangalia nyumba wanazoishi kuna nyingine ni za bati, haifai wala haipendezi; huku tukiwataka hawa askari tunataka wakatulinde. Wanaendaje kutulinda sisi ilhali wao wameacha familia zao zikiwa katika mazingira duni? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba sana Wizara hii katika bajeti hii iangalie namna ya kuboresha nyumba za askari wetu, kuboresha maslahi yao pamoja na kuboresha zaidi vitendea. Askari hawa wanaenda kufanya kazi ya kulinda kwenye doria usiku, lakini magari yote ni mabovu. Sasa, wataendaje kufanya kazi hii kubwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini si hivyo tu, tumesikia hata wenzangu hapa wakichangia, hata mafuta wanaenda kuomba kwa wadau. Haipendezi, tunatakiwa tuangalie ni namna gani ya kuwezesha jeshi hili la Polisi ili liweze kufanya kazi yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna changamoto nyingine kubwa sana. Jeshi la Polisi linafanya kazi nzuri, lakini leo kumeibuka wimbi kubwa la matapeli wanaojifanya ni maafisa wa Serikali. Ninaomba sana Jeshi la Polisi liweze kusaidiwa; kama ni sheria haijakaa vizuri iletwe hapa tuirekebishe, lakini kama kuna namna yoyote ile sisi kama Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambao tuliwahi kupitisha hiyo sheria na sasa imepitwa na wakati tuifanyie kazi tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna jambo lingine pia ambalo linawatesa sana wananchi. Jambo hili ni kuhusu matapeli wa mitandaoni. Leo tumeambiwa kwa kupitia vitambulisho vya NIDA watasajili namba za simu na tatizo hili litakwisha, lakini kila kunapokucha tatizo hili linazidi kuongezeka, kila kuchapo tunatumiwa ujumbe kuna babu, kuna bibi anatoa dawa ya mapenzi, sijui ya nini, kila siku. Sasa, mimi ninauliza, hivi TCRA, Jeshi la Polisi pamoja na kampuni za simu ambazo zinawapa wakala wao kwenda kusajili hizi line za simu wanashindwa kudhibiti jambo hili? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa pongezi kwa Wizara hususani kwa Waziri wetu na Naibu Waziri lakini pia na watendaji wote kwa kazi kubwa wanayoifanya katika sekta hii ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali ya Chama Cha Mapinduzi imefanyakazi kubwa ya kujenga shule nchini Tanzania na sasa kila mahali leo tuna shule. Tuna idadi ya shule takribani 24,000; hizi ni shule nyingi sana. Katika shule hizo shule za msingi ni 17,000 na shule za sekondari ni 7,000. Ninakipongeza sana Chama changu Cha Mapinduzi kwa kazi hii nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanafunzi wanaobebwa katika hizi shule tulizonazo tuna takribani wanafunzi milioni 14. Si hivyo tu, kati ya hawa wanafunzi kwenye shule hizi milioni 14 milioni 12 wapo katika Shule za Msingi na milioni mbili katika shule za sekondari. Hapa tunajiuliza swali la msingi, kama wanaandikishwa wanafunzi milioni 12 katika Shule za Msingi lakini wanaokuja kwenye Shule za Sekondari ni milioni mbili, huu upungufu mkubwa hivi katikati hapa hawa wanafunzi wanakwenda wapi? Ni swali la kujiuliza nani lazima Serikali iweze kufuatilia ili tujue upotevu huu wa hawa wanafunzi ambao wanaanza milioni 12 lakini wanakuja kufika Sekondari milioni mbili; tatizo linakuwa wapi tuweze kupambana na tatizo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si hivyo tu, leo elimu yetu ya Tanzania haimuandai mhitimu kuja kujiajiri au kuajiriwa; hiyo ni changamoto kubwa sana. Leo vijana wengi wanahitimu lakini hawa vijana wanapata wapi ajira? Wakati hakuna maandalizi mazuri ya wao kwenda kujiajiri au kuajiriwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa ninashauri kuliko Serikali kupoteza mamilioni ya fedha kusomesha wanafunzi hawa na mwisho wakahitimu na bila kuwa na elimu ambayo au kwenda kuweza kujiajiri inakatisha tamaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu hiyo ninashauri kwamba mitaala iendane na wakati huu uliopo tuibadilishe mitaala yetu iendane na wakati huu uliopo. Lakini si hivyo tu…(Makofi)

MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa taarifa kwa muongeaji kwamba na hao wanafunzi wenyewe bahati nzuri wanasema kama inawezekana waangaliwe somo la Kiswahili kama nchi nyingine wanavyokuza lugha zao iwe ni somo la darasani kwa sababu si elimu ambayo wanakwenda kuifanyia kazi. Ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Malleko, taarifa hiyo.

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante; naomba niendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa ninauliza hivi kuna haja gani kwa Serikali kupoteza mamilioni ya fedha kusomesha wanafunzi lakini hatima yake wanafunzi hao wanaenda kubaki nyumbani hawana ajira, hawawezi kujiajiri inakuwa ni mzigo kwa Tanzania. Hili bomu tunalolitengeneza baadaye litatulipukia sisi. Kuna vijana wengi sana ambao wamehitimu lakini hawana ajira, hawawezi kujiajiri kwa sababu hawajafanyiwa maandalizi hayo tangu wanaanza hizi shule za msingi, sekondari na mpaka wanapoenda kuhitimu katika vyuo vikuu. Kwa hiyo, ninaomba sana Serikali yetu iweze kuwasaidia wahitimu hawa kupambana na changamoto za maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo vijana wengi ambao wamekosa ajira wengi wanakimbilia kwenda kujiajiri kwenye bodaboda; lakini kipato wanachopata ni cha kujikimu kwa wakati ule tu, kwa siku hiyo tu, na si kitu ambacho kinaweza kuwasaidia na kuwajengea uwezo au kuwasaidia kuendeleza maisha yao. Wanaishia kupata chochote kidogo ambacho kitawasaidia kujikimu kwa siku hiyo na kesho asubuhi waende kutafuta sehemu nyingine ya kuweza kuongeza kipato chao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana Serikali yetu iangalie elimu kwa sababu elimu ndicho kitu kikubwa ambacho kinaweza kuwasaidia watanzania kutoka pale walipo kwenda mahali pengine. Elimu hii kama haitazingatiwa kuwasaidia hawa watu ambao wanaenda kuhitimu waweze kujiajiri ajira leo ni shida. Kwa hiyo, tutengeneze mazingira ya vijana hawa wakihitimu waweze kwenda kujiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, mchango wangu wa leo ni huo. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii nyeti na muhimu sana kwa mustakabali wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza nipeleke pongezi zangu za dhati kwa Waziri pamoja na Naibu wake na watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanayoifanya. Najua jukumu la kutunza mazingira ni la nchi nzima, lakini ninasikitika sana, hata Wenyeviti wanapokuwa wanasoma taarifa zao za bajeti hapo, inaonekana bajeti ni finyu sana katika Wizara hii. Tujiulize, Wizara hii ndiyo imebeba Wizara nyingine zote. Bila kuwa na mazingira safi, bila kuwa na kutunza mazingira ya nchi hii, hivi vitu vingine vyote haviwezi kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunaona katika mlima wetu wa Kilimanjaro moto unatokea sana, ni uharibifu wa mazingira. Tunaona Serikali inatumia fedha nyingi katika kuzima moto huo, lakini siyo hivyo tu, hata watu wanakufa wakati wa kuzima moto, na Serikali inapata hasara kubwa sana. Je, imejipanga vipi sasa kuweza kukabiliana na masuala yote hayo kama bajeti inakuwa ni finyu kiasi hiki? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iweze kuangalia suala hili kwa umakini, kwa sababu, bila kutunza mazingira hatuwezi kufanya jambo lolote. Tukumbuke kwamba, hii dunia ni kama nyumba, na jinsi tunavyozidi kuiharibu, iko siku itatuangukia, nasi sote tutakuwa tumeangamia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa masikitiko makubwa sana kwa sababu uharibifu wa mazingira umekuwa ni mkubwa sana. Ninasema tena kwa sababu ya moto unaowaka Mlima Kilimanjaro na uharibifu mkubwa wa mlima ule tunaona hata kiwango cha barafu kinazidi kupungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejipangaje sasa katika kuona namna ya kutoa elimu kwa wale wananchi wetu wa kule chini ambao ndio wahusika wakubwa kabisa wanaohitaji kupewa elimu hii ili waweze kutunza mazingira? Wao ndio wanapaswa kuambiwa ni namna gani watatunza mazingira, ni njia gani mbadala wanazoweza kutumia ili wasiharibu mazingira kwa kukata miti ovyo, lakini elimu kule chini bado haijafika kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naishauri Serikali, leo tunaweza kuuza hewa ya carbon. Ni kwa nini basi Serikali isijikite kwenda kutoa mafunzo na elimu kwa hawa watu wa chini kwenye Serikali za Mitaa ili waweze kujua umuhimu wa kutunza mazingira, na zaidi ni namna gani wanaweza kufaidika kwa kuuza hewa hiyo ya carbon? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma katika andiko moja ambalo linasema, Wilaya ya Tanganyika kuna vijiji nane vimepata takribani Shilingi milioni 380 kwa uuzaji wa hewa hii ya carbon. Kwa nini basi Serikali isione jambo hili ni la muhimu tukaweza kushirikiana na Halmashauri na wengine sasa wakapata hiyo elimu na namna gani wanaweza kupanda hiyo miti na zaidi ya hapo tukaweza kuvuna hiyo hewa na kuiuza? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijikite kwenye suala la uzimamizi na udhibiti wa uchafuzi wa mazingira. Kama nchi, katika eneo hili tumefeli sana. Tanzania kwa mwaka mmoja inazalisha taka ngumu takribani tani milioni saba, lakini cha kusikitisha kiasi kinachoweza kukusanywa, yaani kuzolewa, ni asilimia 35 tu. Hebu tujiulize tunaishije kwenye mazingira kama haya ambayo taka kama hizo nyingine zote zimebaki, hazijapata ufumbuzi wa namna gani zinaweza kukusanywa na kuzolewa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kila kukicha majiji na miji yanakua, ongezeko la watu mjini linakua, viwanda na biashara na kazi nyingine za kuingizia wadamu kipato zinakua, lakini suala la kuzoa taka na kudhibiti taka bado limekuwa ni changamoto kubwa sana. Ninaishauri Serikali, kutokana na sababu hizi kubwa ambazo zinaonekana zinaenda kutuletea shida katika majiji yetu na Halmashauri zetu, Serikali ione ni namna gani basi itaongeza bajeti kwenye Wizara hii ili waweze kufanya kazi yao kwa ufanisi mkubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo, asilimia 30.7 ya utupaji taka nchini ni holela. Watu wanatupa taka kwa maeneo ambayo hayajatengwa. Unaweza mnaweza kuona, hata mnapopita kwenye mifereji au mito imekuwa ndiyo sehemu ya watu kutupa taka. Mvua inaponyesha, yale matakataka yanakuwa yanaziba mifereji ya maji na baadaye kunatokea mafuriko na baadaye tunapata kipindupindu. Hili ni jambo la kulifanyia kazi. Siyo hivyo tu, asilimia 38.4 ya maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya kutupa taka, lakini miundombinu yake haikidhi utupaji taka. Kwa hiyo, hili ni jambo la kulitazama kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya utupati taka, ni asilimia 27.8, lakini hayahudumiwi. Ni kwa nini yatengwe lakini yasihudumiwe? Ni kwa sababu ya ufinyu wa bajeti. Lakini leo tunasema asilimia 5.3 ya utupaji taka nchini ndiyo inahusisha utupati taka salama. Tunakwenda wapi kama asilimia hiyo yote ni sawa na asilimia 90 ya utupaji taka katika nchi yetu siyo salama? Kwa hiyo, tunawezaje kukwepa kupata kipindupindu na magonjwa mengine ya mlipuko? Hivyo naomba sana Wizara hii iweze kuongezewa bajeti ili iweze kufanya kazi zake vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, Halmashauri nyingi hazioni umuhimu wa kutenga fedha za kutosha kwa ajili ya suala hili na ukusanyaji na utupaji wa taka. Mimi ninaishi hapa Mlimwa C, hapa hapa Dodoma, nitolee mfano hapa. Tunaweza kukaa na taka ndani zaidi ya wiki mbili bila kuja kuzolewa, lakini wanapokuja kuzoa, gari linalokuja kuzoa zile taka na lenyewe ni takataka. Hata wale wanaokuja kuzoa taka ukiwaangalia, hawana hata vifaa vya kuwakinga kwa zile taka wanazokuja kuzibeba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu tujiulize, tunakwenda wapi kama Taifa? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante. Kengele ya pili, ahsante kwa mchango mzuri.

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ni mimi kuweza kuchangia katika Wizara hii ya Kilimo. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa awamu ya sita, Mama yetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya, na kipekee katika kuongeza bajeti hii ya kilimo kufikia kwa kiwango cha asilimia 29.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri Bashe pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Mavunde pamoja na Wakurugenzi wote kwa kazi nzuri hii wanayoifanya kwenye Wizara kwa sababu leo tunaona mwanga bora katika kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Ilani ya CCM katika ukurasa wa 33, naomba kunukuu, inasema; “35. Kilimo cha kisasa ndio msingi katika kujenga na kina nafasi ya kimkakati katika kukuza ustawi wa taifa.”

Mheshimiwa Naibu Spika, takribani Watanzania milioni 40 wako katika sekta hii ya kilimo. Kati ya wakulima hawa milioni 40 wapo wakulima wanaotoka katika mkoa wa Kilimanjaro. Niende moja kwa moja katika Mkoa wangu wa Kilimanjaro. Kama ambavyo hatuwezi kuitenganisha Kilimanjaro na mlima wa Kilimanjaro ndivyo hivyo ambavyo hatuwezi kuitenganisha kilimo cha kahawa na kilimo cha ndizi na Mkoa wa Kilimanjaro.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niende moja kwa moja katika kuchangia katika kilimo cha ndizi ambacho kinalimwa sana na akina mama wa Kilimanjaro. Kilimanjaro kahawa inalimwa sana na wanaume lakini ndizi ni zao la akina mama, Zao hili ni zao la kibiashara lakini pia ni zao la chakula. Nilikuwa ninaomba Wizara iangalie umuhimu wa zao hili kwa kuwapatia wakulima wa Kilimanjaro mbegu bora zinazoendana na hali ya hewa ya kulimanjaro ili akina mama wetu waache kulima zile ndizi walizokuwa wakilima zamani ambazo kwa sasa zimepitwa na wakati. Kwanza mavuno ni machache lakini zinapatwa sana na magonjwa. Wizara iangalie ni kiasi wanaweza kuwekeza katika eneo la utafiti ili tuweze kupata mbegu bora ambazo zitaenda kutuingizia kipato cha kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, katika zao hili la ndizi akina mama wetu wanahitaji pia kupata umwagiliaji ili waweze kupata mazao ya kutosha. Nilikuwa naishauri Serikali iangalie ni namna gani itaenda kuboresha ile mifereji ya asili ya zamani ili iweze kusaidia katika umwagiliaji na akina mama wetu wakilima mazao haya waweze kupata mazao yenye tija.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, jambo la muhimu ni namna Wizara invayoweza kutupatia masoko, si Tanzania tu na nje ya Tanzania. Tunaweza kutumia Waheshimiwa Mabalozi wetu kwa ajili ya kutangaza zao hili katika balozi za huko na sisi tukaweza kupata biashara; ikizingatiwa kwamba katika Mkoa wetu wa Kilimanjaro tunao uwanja wa ndege, na tutautumia uwanja huu vizuri kuweza kusafirisha mazao haya nje na kuwapatia akina mama wa Kilimanjaro faida kubwa katika zao hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, si hivyo tu katia mazao ya nje, Mkoa wetu wa Kilimanjaro tuna changamoto kubwa sana kwa katika vituo vya kuuzia ndizi zetu. Akina mama hawa wanateseka sana. Ukienda kwa Sadala saa kumi na mbili kamili utakuta tayari akina mama wetu wamefika na mikungu yao ya ndizi, lakini kuna shida; kwa sababu mvua yao jua lao, hakuna soko. Si akina mama wa hapo tu, akina mama wa Mamsera wanateseka sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kati ya wote, akina mama wanaoteseka zaidi ni akina mama wa Mwika. Eneo la Mwika akina mama wanauza ndizi zao barabarani kiasi kwamba kunatokea ajali nyingi na kuna msongamano mkubwa, watu hawaweze hata kupita kipindi cha soko.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Wizara iangalie ni namna gani inaweza kutupatia masoko ili akina mama wetu wasipate shida kwenda kuuza ndizi zao. Lakini wakienda kuuza kwenye vituo watauza ndizi zao kwa bei elekezi; kwa sababu wale wachuuzi wanapikuwa wanakwenda kuwafuata majumbani mwao wanawapa kwa bei wanayoitaka wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hili sitakuwa na mchezo nitashika shilingi ya Mheshimiwa Waziri kama hatatoa maelekezo ya kutosha ni namna gani akina mama wa Kilimanjaro hawatateseka tena katika kwenda kuuza mazao yao hasa ya ndizi. Wanateseka sana kwenda kuuza mazao haya, hawajui watapeleka wapi baada ya kwamba wachuuzi wakiona kwamba jioni imefika bei inakuwa chini; na wakina mama wanaona kuliko warudi na ndizi nyumbani anawauzia kwa bei wanayoitaka. Kwa hiyo nitashika shilingi ya Mheshimiwa Waziri hapa kama hatakuwa ametoa maelekezo yanayoeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji pia teknolojia kwenye zao hili la ndizi, tunahitaji pia tupate mashine za kisasa za kuweza kuchakata na kuongeza thamani ya ndizi hata tukauza ndizi ambazo tayari zimechakatwa zikatengenezwa zikauzwa nje ya nchi kama malighafi ya aina hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo linatatiza akina mama wa mkoa wa Kilimanjaro ni mikopo. Kwa nini basi Wizara isione ni namna gani inaweza kuwakopesha akina mama wa Kilimanjaro ili nao waweze kwenda kufanya biashara yao au kuwekeza zaidi kwenye zao la ndizi? Kwa sababu wao pia ni Watanzania; ukiangalia kule katika Ziwa Victoria wavuvi wanapewa mitumbwi, ukiangalia Ziwa Tanganyika wavuvi wanapewa mitumbwi, kwani kuna shida gani na wakina mama wa Kilimanjaro nao wakaweza kupewa mikopo ili waweze kulima na kupata tija katika kilimo hiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe pongezi sana kwa Wizara kwa Serikali kwa sababu katika kipindi hiki wameweza kutupatia ruzuku ya mbolea tani 14,020. Naomba katika hilo niwapongeze sana kwa sababu katika ruzuku hii hata wakulima wa kahawa wameweza kupata mbolea hii, kwa hiyo ninawapongeza sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa Tanzania tunazalisha kahawa tani 80,000; lakini niwapongeze sana kwa sababu huku nyuma tulikuwa kwenye tani 61,000, kwa kweli tumepiga hatua tunahitaji pongezi. Si hivyo tu fedha zinazoingia za Kimarekani katika kuuza kahawa hii ni takribani Dola za Kimarekani milioni 230. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kule Kilimanjaro, kwa sababu nimesema zao hili ni la akina baba pia akina baba wanahitaji…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa mchango mzuri, kengele ya pili.

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika sekta hii muhimu kabisa ya elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Rais wetu mpendwa, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoifanya. Tumeona bajeti ya sekta ya elimu imeongezwa kwa wastani wa asilimia 18, imetoka bilioni 4.7 kwa mwaka wa fedha 2021/2022 hadi kufikia bilioni 5.7 kwa mwaka huu wa fedha 2022/2023. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nisiache pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Elimu, Kaka yangu, Mheshimiwa Profesa Mkenda, pamoja na Naibu wake, Mheshimiwa Kipanga, kwa kazi nzuri wanayoifanya. Nitakuwa ni mchoyo wa fadhila pia nisipowapongeza Watendaji wote wa Wizara hii kwa sabbau tunaona kazi nzuri sana inayofanyika ya kuendeleza elimu katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuipongeza Wizara ya Elimu kwa kazi kubwa wanayoifanya. Tumeona wigo wa elimu bila ada umeongezwa kwa Kidato cha Nne, Kidato cha Tano na Kidato cha Sita. Serikali inatenga takribani shilingi bilioni 10.3 kila mwaka kwa ajili ya fidia za kulipia ada wanafunzi hawa, tunaipongeza sana Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, mikopo ya wanafunzi wa elimu ya juu imeongezwa sana na sasa imefika asilimia 14.7. Ilitoka bilioni 570 na sasa imefika bilioni 654. Jamani hilo ni jambo kubwa sana la kuipongeza Serikali yetu. Fedha za kujikimu wanafunzi wa elimu ya juu zimetoka kuanzia shilingi 8,500 hadi kufikia 10,000 hii ni hatua kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kazi kubwa inayofanywa na Serikali, lakini bado sekta ya elimu inakabiliwa na changamoto na mahitaji mengi. Niende kwenye changamoto chache. Leo kutokana na ongezeko kubwa la udahili wa wanafunzi wanaoendelea katika ngazi zote, mfano kidato cha kwanza, udahili umeongezeka kutoka wanafunzi 780,376 kwa mwaka 2021 hadi kufikia wanafunzi 173,941 kwa mwaka 2023. Hili ni ongezeko la asilimia 38. Kwa ongezeko hili tunakuwa tunahitaji miundombinu ya madarasa na walimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na changamoto hii ya miundombinu na walimu, nianze na changamoto ya miundombinu. Miongozo inaelekeza kwamba darasa moja liwe na wanafunzi 45, lakini kwa sasa darasa moja lina wanafunzi 74 kwa shule za msingi. Kwa shule za awali mwongozo unasema darasa moja liwe na wanafunzi 40, lakini kwa sasa darasa moja lina wanafunzi 75.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni kutokana na takwimu za BEST, kitabu hiki cha takwimu za elimu ambacho kinatolewa na Wizara ya Elimu pamoja na TAMISEMI. Tunaona kwa uwiano huu tukisema mwalimu amfikie kila mwanafunzi mmoja mmoja, anawezaje kumfikia mwanafunzi mmoja mmoja katika msongamano mkubwa kama huu? Kwa hiyo tunaona ni namna gani elimu yetu haitafikia kile kiwango tunachohitaji kwa sababu huku kwenye msingi ndiko tunakoenda kukuza elimu ya wanafunzi ili waweze kufanya vizuri katika ngazi za juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hali hiyo inafanya shule za msingi kuwa na uhaba mkubwa sana wa madarasa. Na kwa sasa tuna uhaba wa madarasa takribani vyumba 102,485, ni uhaba mkubwa sana. Changamoto hii inasumbua sana katika ufundishaji na kwa utafiti uliofanyika inaonekana kuna vyumba ambavyo wanafunzi wanakaa hata zaidi ya 100 kwenye chumba kimoja. Kwa hiyo tuangalie namna ya kuweza kurekebisha changamoto hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye changamoto ya pili ambayo ni walimu; kwa mujibu wa Hotuba ya Bajeti ya TAMISEMI ya mwaka huu, shule za msingi zina uhaba wa walimu 100,958 na shule za sekondari zina uhaba wa walimu 74,743. Pamoja na TAMISEMI kupata kibali cha kuajiri walimu 13,130, bado uhaba wa walimu utaendelea kubaki kwa sasa tutakuwa na uhaba wa walimu wa takribani 162,551.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiendelea kuajiri kwa utaratibu huu itatuchukua miaka 10 mpaka 15 kuweza kutatua changamoto hii ya walimu. Nasema hivyo kwa sababu wakati Serikali inaajiri kuna walimu wanastaafu na kuna walimu wanaofariki, lakini pamoja na hao wanafunzi bado wanaendelea kudahiliwa kwa hiyo ongezeko la wanafunzi linaendelea kuwa kubwa na wakati changamoto ya walimu ikiendelea kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sensa yetu ya 2012, Watanzania walikuwa milioni 44 na sasa ni milioni 61. Inaonekana hapo katika hiyo miaka kumi hao watu waliozaliwa ni watoto na wanahitaji elimu, sasa tusipotengeneza miundombinu mapema ukifika wakati huo tutapata changamoto, wanasema ukitaka kuliua Taifa uue elimu, kwa hiyo sisi tunataka kuboresha kwenye elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwenye jambo hili, ninaishauri Serikali iweze kuongeza bajeti ya elimu kwa asilimia 20. Kuna Azimio la Incheon la Mwaka 2015 ambalo lilizitaka nchi zote zilizo Ukanda wa Kusini mwa Jangawa na Sahara ziweze kutenga asilimia 20 ya bajeti yote ya Taifa kwenda kwenye sekta ya elimu ili kuweza kukabiliana na changamoto kama hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali itaweza kutoka hapa kwenye asilimia 18 tunayotenga sasa tukaenda kwenye asilimia 20, tunaweza kutatua changamoto hizi ambazo ni za miundombinu na walimu tukaweza kuajiri walimu wa kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ninaishauri Serikali iangalie itakuja na mpango gani mahsusi wa kuweza kuajiri walimu kuendana na ongezeko. Tumeona ongezeko la watoto na upungufu wa walimu. Kwa hiyo, ninashauri Serikali ije na mpango wa miaka mitano, mitano wa kuona katika kipindi cha miaka tunaangalia uhaba wa walimu tulionao tunaugawanya kwa hiyo miaka mitano, tunaona ni namna gani tunaweza kuajiri walimu, hata tukiajiri kila mwaka walimu 25,000 tutakuwa tumepunguza sana tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongeze pale alipokuwa amechangia Mheshimiwa Shangazi. Leo sekta ya elimu inasaidiana sana na wadau hawa wenye shule binafsi, kwa sababu nia yetu ni moja kuweza kuendeleza wanafunzi au Watanzania kupata elimu bora. Sasa inapoonekana upande huu wa wadau wa elimu na Serikali wanakinzana inaonekana kama kuna namna fulani ambayo hawaendi pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mambo ambayo yanafanyika ambayo siyo mazuri, wawekwe pamoja wazungumze, watatue hizo changamoto.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Malleko kwa mchango mzuri.

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba dakika moja tu nimalizie.

NAIBU SPIKA: Sekunde mbili.

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kuna mbunifu anaitwa Mataka, ameweza kubuni namna gani ya kufanya ufundishaji wa Hisabati, Kiswahili pamoja na Kiingereza…

NAIBU SPIKA: Ahsante, mengine andika.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia katika sekta hii nyeti kabisa ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza sana sana Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuleta maendeleo Tanzania. Tumeona Royal Tour ikitikisa Tanzania nzima, tumeona mishahara ya wafanyakazi inazungumziwa kila mahali hapa Tanzania. Lakini kubwa zaidi ni katika bajeti ya kilimo ya mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu ni maajabu makubwa sana na haijawahi kupatakutokea kwa kuwa bajeti ya kilimo imeongezwa kutoka Shilingi bilioni 294 hadi kufikia Shilingi bilioni 751, sawa na asilimia 155. Kwa kweli Mama yetu anafanya kazi kubwa, wote tunapaswa kumpongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo nichukue pia nafasi hii kumpongeza kaka yangu Mheshimiwa Hussein Bashe, Waziri wa Kilimo pamoja na Mheshimiwa Mavunde kwa kazi kubwa sana wanayoifanya katika sekta hii ya kilimo. Wamekuwa ni wachapakazi lakini si hivyo tu, wamekuwa na ubunifu mkubwa katika kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya kilimo. Ninawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nijikite kuchangia katika zao la kahawa. Zao la kahawa limekuwa ni uti wa mgongo kwa Mkoa wa Kilimanjaro. Mkoa wa Kilimanjaro unalima zao la kahawa tangu kabla ya uhuru. Lakini si Kilimanjaro tu, takribani mikoa 15 katika Tanzania inalima kahawa. Ni sawasawa na kwamba nusu ya Watanzania wanalima kahawa. Hivyo ukigusa kahawa umegusa nusu ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kusikitisha sana kahawa hii ambayo ilikuwa inaiingizia Tanzania pato kubwa kabisa kuliko mazao mengine yoyote limeachwa nyuma na kwa sasa hata ruzuku halipati. Mazao ya korosho, tumbaku na pamba yanapata ruzuku, lakini tunajiuliza ni kwa nini kahawa haipati ruzuku?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri ni rafiki yangu sana, lakini leo bila kupepesa macho, nimepanga kuondoka na Shilingi kwenye mshahara wa Mheshimiwa Waziri kama hatatoa majibu ya kujitosheleza ya kwa nini kahawa haipati ruzuku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo limekuwa ni changamoto kwenye kahawa ni suala la miche. Wananchi hasa wa Kilimanjaro wanahitaji miche bora ya kahawa; ile miche ambayo inaweza kustahimili hali ya hewa ya sasa lakini pia inayoweza kustahimili magonjwa huku ikiendelea kutoa mazao mengi tofauti na ile ya zamani. Mibuni mingi iliyopo katika Mkoa wetu wa Kilimanjaro imezeeka. Leo tunahitaji miche mingine ili tuweze kupata kahawa iliyobora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana Wizara kwa kuwa bajeti ya sasa kwenye uzalishaji wa mbegu imetoka kuanzia Shilingi bilioni 10.58 hadi Shilingi bilioni 43.03, haya ni mapinduzi makubwa sana. kwa hivyo, ninaamini wananchi wa Kilimanjaro Watanzania wote wanaolima kahawa watapata miche bora itakayosaidia zao hili kufika pale lilipokuwa zamani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la taifa lilikuwa ni kufikia kuvuna tani 300,000 ifikapo mwaka 2025. Lakini mpaka sasa mwaka 2021/2022 tumeweza kuzalisha tani 65,235 ilhali tulikuwa tunalengo la kuzalisha tani 72,000. Hatuwezi kwenda kwa staili hii tukaweza kufika huko tulikokuwa tunataka kwa 300,000. Kwa sababu leo tuko tani 65,235 mpaka tufike tani 300,000 itachukua muda mrefu sana. Kwa hiyo, ninaomba zao hili lipewe kipaumbele, zao hili lipewe ruzuku. Leo tuna maafisa ugani ambao tumeona mmewapa mapikipiki wakafanye kazi kubwa kwenye zao hili pia… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante kwa mchango mzuri.

MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Naunga mkono hoja. Ahsante.