Contributions by Hon. Zaytun Seif Swai (8 total)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Awali ya yote, naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu na vilevile naomba niwashukuru wananchi wangu wa Mkoa wa Arusha hususan kinamama wa Mkoa wa Arusha kwa kuniamini kuwa mwakilishi wao katika Bunge hili. Nawaahidi wananchi wangu hususan kinamama wa Arusha sitawaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee kabisa, naomba nishukuru familia yangu wakiongozwa na mama yangu mpendwa mama Sifa Swai, mume wangu na mtoto mpenzi Alina. Wote hawa kwa nyakati tofauti wamekuwa wakinishauri vyema jinsi gani ya kuwaongoza wananchi wetu na vilevile wananiongezea busara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie hotuba ya Rais, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na suala la elimu. Serikali imefanya mambo makubwa sana kwenye awamu zilizopita kwenye suala la elimu na yote haya imeyafanya kwa sababu inatambua umuhimu wa elimu na mchango wake mkubwa katika uchumi wa Taifa letu. Kutokana na umuhimu huu, Rais ameeleza mambo mbalimbali yanayohusiana na elimu katika hotuba yake na majawapo ikiwa ni kuanzisha shule za sayansi za watoto wa kike katika kila mkoa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, binafsi ni mnufaika wa elimu iliyotolewa bure na Serikali katika masomo haya ya sayansi na hisabati. Kwa hiyo, natambua vizuri changamoto wanazozipata watoto wa kike katika masomo haya na naipongeza Serikali kwa kuamua kuanzisha shule hizi ili kutatua changamoto zile. (Makofi)
Mheshimia Naibu Spika, naomba niishauri Serikali, suala la shule za sayansi ni muhimu sana na linatakiwa lichukuliwe kwa umuhimu wake. Shule hizi zinahitaji umakini mkubwa kwenye kuziendesha. Kwa kuanza zinahitaji kuwa na ubora wa hali ya juu, maabara zenye viwango vya juu na walimu wenye uwezo mkubwa wa kuwafundisha wanafunzi hawa. Vilevile shule hizi zinahitaji nyezo mbalimbali kama vitabu na kadhalika. Kwa hiyo, naiomba Serikali isikurupuke kwenye suala hili, iliangalie kwa umakini na tuhakikishe shule hizi zinajengwa kwa umakini wa hali ya juu tukizingatia hayo mambo niliyotaja ili basi lengo la Serikali liweze kutimia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi sote ni mashuhuda, tumeshuhudia jinsi halmashauri zetu zinavyopata shida sasa hivi kujenga madarasa na kutafuta madawati katika shule mbalimbali na wananchi wetu pia wanalalamika kwa sababu michango ni mikubwa kusaidia maendeleo haya. Kwa hiyo, naiomba Serikali suala hili la ujenzi wa shule za sayansi kwa watoto wa kike isilichukulie juu bali ilichukulie kwa umakini na tulianze suala hili mapema tusisubiri mpaka mwisho wa miaka mitano ili tuweze kuzijenga shule hizi.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba vilevile niongelee suala la mikopo ya asilimia 10 inayotolewa kutokana na mapato ya halmashauri. Tumeona jitihada kubwa sana za Serikali inazofanya kuwawezesha wananchi wake kiuchumi kupitia mikopo isiyokuwa na riba na mikopo mingine yenye riba nafuu na vilevile kupitia mifuko na program mbalimbali zilizoanzishwa na Serikali. Mikopo hii ya asilimia 10 inatolewa kulingana na mapato ya halmashauri husika na sisi sote tunajua kwamba halmashauri zote hazilingani kimapato. Kwa hiyo, formula hii haizingatii halmashauri zenye changamoto ya vyanzo vya mapato. Mikopo hii isiwe ni adhabu kwa wanufaika walioko vijijini na sehemu zenye changamoto za mapato. Naiomba Serikali iweze kuangalia formula hii kwa undani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitatolea mfano mdogo tu, hauwezi kulinganisha mapato ya Ilala, Kinondoni na halmashauri za Ngorongoro, Longido au Monduli na sehemu zingine za vijijini. Kwa hiyo, tunaomba Serikali yetu iangalie fomula hii na iweze kugawa mikopo hii kwa usawa. Suala hili pia litapunguza gap lilipo la umaskini wa vijijini na mijini ambapo nadhani ndiyo lengo kubwa la Serikali yetu, tupunguze gap la umaskini lililopo kwa sasa vijijini na mijini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile naomba nichangie kwenye sekta ya maji. Nashukuru Mheshimiwa Rais bado anatambua kuna changamoto nyingi za maji, hususan vijijini. Serikali yetu imefanya mambo mengi sana hasa kutekeleza miradi mikubwa ya maji ikiwemo mradi wa shilingi bilioni 520 ulioko Mkoani Arusha. Naomba niishauri Serikali isiwekeze tu kwenye miradi mikubwa kama hii vilevile iangalie vyanzo vingine vya maji ikiwemo uchimbaji wa visima virefu. Nitatolea mfano tu, mradi huu wa shilingi bilioni 520 unapita Wilaya ya Arumeru lakini kuna kata katika Wilaya ya Arumeru kama Kata ya Nduruma haina maji. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie pia vyanzo vingine vya maji ukiachia mbali miradi hii mikubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia katika bajeti ya Wizara hii na Maliasili na Utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, huwezi kuongelea maendeleo ya Wizara hii bila kutaja Kanda ya Kaskazini hususani Mkoa wa Arusha. Wameongea vizuri sana Wabunge wa Majimbo wa Mkoa wa Arusha, jana ameongea kaka yangu Mrisho Mashaka Gambo, ameongea vizuri kuhusiana na Wizara hii, umuhimu wa Wizara hii katika mkoa wetu. Vilevile baba yangu Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, Mbunge wa Longido ameongea vizuri sana kuhusiana na umuhimu wa Wizara hii na mimi kama mwakilishi wa Mkoa wa Arusha, naomba nisisitize umuhimu wa Wizara hii katika Mkoa wetu wa Arusha (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba pia niwashauri Wizara hii ya Maliasili na Utalii waendelee kuwashirikisha wadau wakuu wa maendeleo wa Mkoa wa Arusha katika maendeleo ya Wizara hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda naomba niongelee suala moja tu la sintofahamu iliyoko katika Wilaya ya Longido kuhusiana na maamuzi ya Serikali kutenga maeneo yao kuwa Mapori ya Akiba. Naomba niikumbushe Wizara kwamba asilimia 95 ya wakazi wa Longido wanajihusisha na ufugaji na wanategemea sana mapori haya kwa ajili ya malisho ya mifugo yao. Maamuzi haya ya Wizara yataathiri Zaidi ya vijiji 19, vya Tarafa ya Ketumbeine na vijiji 11 vya Tarafa ya Engarenaibor na kijiji kimoja cha Tarafa ya Longido. Tukumbuke kwamba pia katika maeneo haya kuna wakazi zaidi ya 90,000 ambao wanategemea pori hili katika masuala yao mbalimbali ya kuishi na katika kuinua kipato cha uchumi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hawa pia kwa juhudi zao binafsi wameendeleza miundombinu ya masuala ya kijamii kama afya, elimu na kadhalika. Kwa hiyo sidhani kwamba ni suala la busara kuwaondoa katika maeneo haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, Rais wetu wa Awamu ya Tano yake alifanya jitihada kubwa sana kurudisha zaidi ya vijiji 900 kwa wananchi ili waweze kupata maeneo ya kuishi na kufanya shughuli zao mbalimbali za kiuchumi. Vile vile katika hotuba ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, aliyoisoma tarehe 22 Aprili, hapa Bungeni alionyesha dhamira kubwa ya Serikali katika kuongeza maeneo ya wafugaji hapa nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, hatua hizi za Wizara hii ya Maliasili na Utalii, naona dhahiri zinakinzana na dhamira njema ya Serikali kwa wananchi wetu. Naiomba sana Serikali yangu sikivu kupitia Wizara hii, itumie busara katika jambo hili ili basi lisiweze kuleta madhara kwa wananchi wetu. Naomba pia wizara hii kabla ya kufanya maamuzi kama haya iweze kuwashirikisha wadau mbalimbali hususani wa maeneo yale ili waweze kutoa maoni yao juu ya mambo haya. Vile vile naomba sana Wizara kabla ya kufanya maamuzi haya iweze kutembelea maeneo haya ili ijue basi, kama kweli maeneo haya ni mapori ama ni makazi ya wanadamu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naomba kutoa hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza kabisa naomba nimpongeze Waziri wa Fedha kwa uwasilishaji uliotukuka wa rasimu ya mpango. Mimi binafsi kama Mjumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bajeti pamoja na wenzangu tulipokea mapendekezo yale na tuliyafanyia uchambuzi wa kina. Nashukuru na pia, naipongeza Serikali kwa kuchukua mawazo yet una kuyajumuisha katika rasimu ile. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wowote ule unahitaji rasilimali fedha na Waheshimiwa Wabunge hapa wameongea mambo mengi sana ya kimkakati, jinsi gani tutapata fedha kwa ajili ya kuwezesha Mpango wetu utekelezeke kwa kiwango cha juu. Naomba nijikite kwenye suala la udhibiti wa mapato. Mambo yote haya yaliyoongelewa na Wabunge mambo mazuri yatakuwa hayana maana sana kama tutashindwa kudhibiti mapato yetu tutakayoyapata. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee suala la GePG, yaani Government Electronic Payment Gateway. GePG ni mfumo wa Serikali wa kukusanya mapato kielektroniki. Naweza kusema kwamba, Serikali imeshindwa kudhibiti mapato yetu kupitia mfumo huu kwa kiasi kikubwa. Ni kweli, mfumo huu umeisaidia Serikali kuongeza mapato yake, lakini vilevile inabidi tuufanyie kazi zaidi kuhakikisha tunadhibiti mapato yetu mpaka mwisho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu tumewaamini na tumewaachia sekta binafsi watusaidie kukusanya mapato haya, hususan sekta ya simu, makampuni ya simu na mabenki mbalimbali, lakini inavyoonekana makampuni haya binafsi yamewekeza sana kwenye rasilimali watu pamoja na teknolojia ukilinganisha na wafanyakazi wa Serikali wanaohusika moja kwa moja na mifumo hii. Kwa hiyo, kuna mwanya mkubwa sana hapo wa kupoteza mapato kwa sababu ya tofauti ya kiufahamu wa mifumo hii. Naishauri Serikali iweze kuwekeza kwa rasilimali watu na teknolojia kwenye mifumo hii ili basi tuweze kuitumia mifumo hii kwa ufasaha na ufanisi zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia niongelee suala la mawasiliano. Naweza kusema kwamba, sekta hii ya mawasiliano ni moja ya sekta ambazo zinachangia kodi kubwa na uchumi wa nchi hii, lakini Serikali yetu sijaona jitihada zake za dhati kuisaidia sekta hii ili iweze kukua zaidi na Serikali iweze kukusanya mapato zaidi kwa sababu mbalimbali, ikiwemo kodi kubwa, tozo mbalimbali na masharti mengi yanayowekewa sekta hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naweza kutolea mfano tu, kuna maeneo mengi ya vijijini, kwa mfano kule Longido kuna Kata ya Nondoto Matale, hata Wilaya ya Meru kuna Kata ya Ngabobo, hakuna mawasiliano ya simu, lakini sekta hii mdhibiti, ndio kazi yake kubwa kuhakikisha kwamba, sehemu mbalimbali zinapata mawasiliano, hususan sehemu za vijijini. Kampuni hizi za simu zinakatwa tozo ya asilimia tatu katika mapato yake inaenda kwenye mfuko unaitwa USCAF (Universal Fund) na lengo kubwa la Mfuko huu ni kuendeleza mawasiliano sehemu za vijijini na mijini. Sasa napenda kujua kwamba, Mfuko huu unafanya kazi gani hasa kama kuna sehemu nyingi tu za nchi hii ambazo hazina mawasiliano ya kutosha? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Wizara hii muhimu ya Elimu. Mchango wangu utajikita hasa kwenye kuishauri Serikali katika mambo kadhaa ambayo yanaweza kuinua ubora wa elimu yetu ili kutoa wahitimu wenye weledi na wenye ujuzi sahihi ambao unahitajika katika soko letu la ajira. Naomba vile vile, niwapongeze Kamati ya Huduma za Jamii kwa maoni yao ambayo yanaonesha dira ya kuinua kiwango cha elimu katika nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kuongelea suala la mikopo ya elimu ya juu. Naomba kwanza nianze kwa kumshukuru Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kuweza kufuta ile retention fees ya 6% iliyokuwepo katika mikopo ya elimu ya juu. Tunamshukuru sana mama. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, vilevile naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Elimu, nimesikiliza hotuba yake leo na ameweza kufuata maoni ya Wabunge wengi na kuifuta ile asilimia 10 ya penalty, tunashukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwenye suala la mikopo bado kama Serikali, inabidi tufanye kazi sana, tuendelee kuondoa vikwazo na changamoto mbalimbali ikiwemo masharti magumu kwa wahitimu wetu wenye kupata mikopo hii ya elimu ya juu. Asilimia 15 ya marejesho ya mikopo hii bado ni kubwa kwa wahitimu wetu. Wahitimu wetu wengi wakiajiriwa wanapata mishahara ya kima cha chini na walio wengi hawazidi shilingi laki tano. Kuwatoza asilimia 15 ya marejesho ya mikopo ya elimu ya juu, bado kuna kodi na pensheni pamoja na tozo nyingine kwa kweli hatuwatendei haki wahitimu wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali kupitia Bodi ya Mikopo iweze kupunguza asilimia hii hadi kufikia basi angalau asilimia 10 ili tuweze kuwawezesha wahitimu wetu waishi maisha mazuri. Vilevile, tuwape nafasi wale ambao wanaweza kuchangia zaidi ya asilimia 10, basi wapeleke marejesho yao katika Bodi ya Mikopo. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, tatizo la ajira kwa wahitimu wetu bado ni changamoto. Naishauri Serikali, ili kukabiliana na tatizo hili, basi Serikali ianzishe scheme maalum ya mikopo kwa wahitimu wetu ili basi, wakimaliza pale vyuo vikuu kama hawajapata ajira, waweze kujiajiri wenyewe katika sekta ambazo siyo rasmi. Vile vile, nashauri mikopo hii tuishushe kwenye vyuo vyetu vya kati ikiwemo VETA ili basi wahitimu wetu wa-apply ujuzi wao na kwa kutumia mikopo hii waweze kujiajiri na kujitegemea. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la TEHAMA. Sasa hivi dunia yote inaelekea kwenye digital economy. Naomba Serikali kupitia Wizara ya Elimu iweze kuwekeza katika masomo ya TEHAMA hususan katika shule za sekondari ili basi, tuweze kuwawezesha vijana wetu kupambana na huu uchumi wa kidijitali. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, leo hii ukitaka kuongeza ukusanyaji wa mapato kidijitali, unahitaji wataalam wazuri wa TEHAMA; ukitaka kupata wataalam wa masoko ya mazao yetu na bidhaa nyingine, tunahitaji wataalam wazuri wa TEHAMA. Kwa hiyo, basi naweka msisitizo katika Wizara hii ya Elimu tuweze kuwekeza kwenye masomo ya TEHAMA ili tuwasaidie vijana wetu wapambane na changamoto za uchumi wa kidijitali. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa ujumla, ili kuinua elimu yetu ya msingi na sekondari, nashauri, tuweze kuboresha mazingira mbalimbali ya utoaji wa elimu ikiwemo kuweka miundombinu ambayo ni bora zaidi, ikiwemo nyumba za walimu, madarasa na maabara hususan kwenye shule zile za sayansi. Tukiweka mazingira bora ya kufundishia na vile vile, tukiwapa motisha walimu wetu hususan wale wenye kufundisha vizuri na kufaulusha na wale wenye kufundisha kwenye mazingira magumu labda shule za pembezoni, sasi tutaweza kuinua elimu yetu kwa kiasi kikubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, hata kule Loliondo Ngorongoro, Karatu, Mang’ola, Lokisale, Monduli walimu wetu watapenda kwenda kufundisha wanafunzi wetu na kwa ujumla tutaweza kuinua kiwango chetu cha elimu.
Mheshimiwa Spika, nakushukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa maoni yangu katika mapendekezo ya Mpango wa Taifa wa Maendeleo wa 2022/2023.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Arusha vilevile naomba niendelee kumpongeza Mama yetu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutuongoza kwa weledi mkubwa na vilevile kwa kuendeleza diplomasia ya kimataifa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kwa kuchangia kwenye sekta muhimu ya afya. Naipongeza Serikali kwa kuendelea kuboresha huduma hizi za afya pamoja na maboresho yote yaliyofanyika bado kuna changamoto nyingi sana kwa wananchi wetu kupata huduma bora za afya. Changamoto hizi ni pamoja na gharama kubwa za afya kwa wananchi wetu, ubora wa afya wanaopata wananchi wetu na vilevile kupata kwa huduma za afya kwa wakati. Changamoto zote hizi suluhisho lake ni moja tu ni kuwapatia wananchi wetu bima ya afya kwa wote. Taarifa za kutoka Wizara ya Afya mpaka leo hii ni asilimia 12 tu ya Watanzania ambao wananufaika na huduma hizi za bima ya afya kwa wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Kamati ilivyoshauri kwenye mapendekezo yake na mimi naomba niweke msisitizo kwa Serikali kutuletea Muswada wa Sheria wa Bima ya Afya kwa wote ili basi sheria hii iweze kwenda sambamba na Mpango wetu wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa na vilevile wananchi wetu waweze kunufaika na huduma bora za afya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba vilevile niweze kuchangia katika mwenendo wa riba za mabenki. Jana tulimsikia Mheshimiwa Waziri hapa akisema moja ya mafanikio ya sekta hii ya mabenki ni kushuka kwa riba kutoka asilimia 16.8 hadi asilimia 16.6, punguzo la asilimia 0.2 tu. Sisi kama wawakilishi wa wananchi hatuwezi kwenda kusema kwamba punguzo la asilimia 0.2 tu ni mafanikio ya sekta hii ya kibenki. Wananchi wetu bado wanateseka na riba kubwa za mikopo ya kwenye mabenki nasi Wawakilishi wao inabidi tufanye jitihada za makusudi kuhakikisha riba hizi za mabenki zinashuka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumemsikia Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwenye hotuba zake nyakati tofauti akiagiza Benki Kuu ya Tanzania iweze kushusha riba hizi za mabenki hadi kufikia asilimia 10 au chini ya hapo. Asilimia 16.6 inayosemwa hapa hii ni wastani tu, bado kuna wananchi wengi wanakopa kwa riba ya zaidi asilimia 18. Natambua sana jitihada zinazofanywa na Serikali yetu kuhakikisha riba hizi za mabenki zinashuka, wamesema wenzangu hapo ikiwemo mojawapo ni kupunguza kiwango cha chini cha akiba ambazo mabenki haya yanawekeza BOT yaani Statutory Minimum Reserve hadi kufikia asilimia Nane, lakini bado tumeona hili siyo suluhisho la kushusha riba za mabenki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, bado Serikali yetu imetoa Shilingi Trilioni Moja imewapa Benki Kuu ya Tanzania ili kuweza kushusha hizi riba za mabenki, lakini bado tumeona siyo suluhisho pia ya kushusha riba hizi. Pamoja na hayo jitihada zote zilizofanywa bado tunaona ni punguzo la asilimia 0.2 tu ambayo bado sidhani kama tunaweza tukajisifia kuwa ni mafanikio ya sekta hii ya kibenki. Naamini Benki Kuu ya Tanzania pamoja na Wizara yetu ya Fedha inao wachumi wabobezi wengi na kwa pamoja wanaweza kushirikiana kuhakikisha riba hizi za mabenki zinashuka kwa asilimia kubwa. Ili uchumi wetu uweze kuwa uchumi shirikishi na jumuishi lazima wananchi wetu waweze kwenda kwenye mabenki mbalimbali na kuwa na uwezo wa kukopa kwa riba nafuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya Bajeti tuliweza kukutana na Umoja wa Mabenki ya Tanzania (TBA) na walitupa changamoto zao nyingi ambazo zinachangia gharama kubwa za uendeshaji wa mabenki na hivyo wao wanalazimika kuongeza riba katika mabenki yetu. Sababu nyingi walizotupa kati ya hizo kuna sababu mbili ambazo zipo ndani ya Wizara ya Fedha ambao wao wanaweza kuzitatua ili basi kuhakikisha riba hizi zinaweza kushuka kwa wanachi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu walizozitaja moja wanasema kupishana kwa sera kati ya Mamlaka ya Mapato ya Tanzania na Benki Kuu ya Tanzania, zote hizi ni Taasisi za Serikali naamini Waziri wetu hapa anaweza kukaa na taasisi hizi na kusuluhisha na kufanya riba za mabenki ziweze kushuka. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu nyingine waliyoitaja Umoja wa Mabenki, walisema vilevile ni kutokuwa na ushirikiano kati ya Mamlaka ya Serikali na mabenki ya biashara. Naamini pia hii sababu iko ndani ya Wizara ya Fedha, wanaweza kwa pamoja wakashirikiana na umoja wa mabenki haya ili basi watafute suluhisho la kushusha riba hizi za mabenki kwa wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo pia namuomba Mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha hotuba yake aweze kutueleza hapa mikakati Serikali iliyonayo itakayofanya kwa ajili ya kushusha riba za mikopo kwa wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nikushukuru kwa fursa hii uliyonipa ya kuweza kutoa maoni yangu kwenye Mapendekezo haya ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2023/2024. Kama Mjumbe wa Kamati ya Bajeti nami nilishiriki katika uchambuzi huu na ninaunga mkono mapendekezo yote ya kamati yaliyotolewa. Nikianza na hali ya uchumi wa Taifa, naomba nianze kwa kuipongeza sana Serikali kwa juhudi zake za kuendeleza ukuaji wa uchumi chanya na tuko kwenye mwelekeo sahihi kabisa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hadi robo ya mwaka tulifikia ukuaji wa uchumi wa asilimia 5.4 kutoka asilimia Tano kipindi kama hichi mwaka jana. Ukiangalia nchi nyingi katika ulimwengu huu sasa mwaka 2021 walikuwa na ukuaji wa uchumi kwenda kwenye uelekeo hasi wa hadi wastani wa asilimia 3.1. Kwenye hili utaona kabisa jitihada kubwa zilizofanywa na Serikali yetu katika ku- maintain uelekeo mzuri wa ukuaji wa uchumi wa nchi yetu. Hii yote imechangiwa sana na juhudi za Serikali katika kukabiliana na majanga makubwa na changamoto za kidunia ikiwemo UVIKO-19, kwa hiyo ninaipongeza sana Serikali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Sheria ya Bajeti, Sura Namba 439 utaona uandaaji wa mapendekezo haya umetumia mambo mbalimbali ikiwemo Dira ya Taifa ya Maendeleo, Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya 2020, vilevile tumeangalia mikakati mbalimbali ambayo tumejiwekea kama Taifa ya maendeleo. Nitaomba nizungumzie jambo moja la mikakati ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia, juzi tu hapa, Rais wetu amezindua mkakati kabambe kwa ajili ya Taifa kuhakikisha Watanzania wote wanatumia nishati safi na salama kwa ajili ya kupikia. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa uamuzi huu na huu ndiyo mwelekeo wa kidunia. Ajenda hii ya nishati safi na salama kwa ajili ya kupikia ndiyo mjadala unaoendelea dunia nzima hivi sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu alisema kwamba katika mkakati huo kama Watanzania basi Serikali itahakikisha kwamba Watanzania wote wanatumia nishati safi na salama hadi kufikia mwaka 2032. Kwa hiyo, hii ni dira ya miaka 10 kwa hiyo ninaimani kwamba mkakati huu lazima tuuone kwenye mpango wetu wa mwaka mmoja mmoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Mheshimiwa Rais alienda mbali zaidi na kuzitaka taasisi zote zenye kulisha watu zaidi ya 300 kuweza kutumia nishati safi na salama ndani ya mwaka huu mmoja yaani 2023. Katika hotuba yake Mheshimiwa Rais aliahidi wananchi kwamba Serikali itatenga bajeti kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024 zaidi ya Bilioni 23 kwa ajili ya Watanzania waweze kutumia nishati hizi safi na salama kwa ajili ya kupikia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia mapendekezo haya ya mpango na hotuba ya Mheshimiwa Waziri hapa, lakini sijaona reflection ya maagizo haya ya Mheshimiwa Rais kwenye mapendekezo haya ya mpango huu. Namuomba sana Mheshimiwa Waziri akileta mpango wake hapa wa mwaka 2023/2024, basi tuweze kuona mapendekezo haya ya matumizi ya nishati safi na salama kwa ajili ya kupikia yanaingizwa kwenye mpango huu wa Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Taifa tukiweza kutekeleza nishati safi na salama kwa ajili ya kupikia, basi tutaweza kuokoa maisha ya wananchi wetu wengi ambao wanafariki kwa ajili ya magonjwa ya mifumo ya afya. Vilevile tutaweza kuokoa fedha nyingi za kuwatibu wananchi hawa, pia tutaongeza nguvukazi kwa ajili ya kufanya maendeleo mengine ya Taifa. Vile vile tutaokoa muda wanaopoteza wananchi wetu hususani kinamama wanaopoteza kwenda kutafuta kuni porini na hivyo watatumia muda huo kwa ajili ya kufanya shughuli zingine za maendeleo na kujenga nchi. Vilevile tutaokoa muda wanaopoteza wananchi wetu hususan akina Mama wanapoenda kutafuta kuni porini na hivyo watatumia muda huo kwa ajili ya kufanya shughuli zingine za maendeleo na kujenga nchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tutaweza kutunza mazingira yetu ambayo mpaka sasa tathmini zinatuambia kwamba tukihitaji tani moja ya mkaa lazima tutumie tani Saba za magogo. Hivyo, tunaona ni jinsi gani suala hili linavyoweza kuharibu mazingira yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nitoe maoni yangu kwenye ushirikiano uliopo kati ya Wizara zetu za kisekta na Wizara yetu ya Fedha. Tumejionea hapa mara kwa mara tunaona hakuna coordination ya kutosha kati ya Wizara ya Fedha na Wizara hizi za Kisekta. Kama nilivyotoka kueleza hapa, suala la nishati safi na salama unaweza kukuta limebebwa kwa uzito wake na Wizara ya Kisekta lakini halijaweza kuingizwa kwenye mpango.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Vilevile kwenye suala la Royal Tour tumeona kazi kubwa iliyofanywa na Serikali yetu kwa ajili ya kuitangaza nchi yetu kwenye utalii, mpaka sasa hivi tunajivunia kuwa mahoteli yamejaa kwa sababu ya kulaza wageni wetu na booking mbalimbali za watalii tuliowapata lakini suala hili halijaingizwa kwenye mpango na ni suala ambalo hata Kamati kipindi kilichopita kwenye bajeti tulishauri Wizara. Kwa hiy,o lack of coordination ni jambo ambalo linazisumbua Wizara hizi, naomba sana Waziri pamoja na Serikali tuweze kuwa na mahusiano mazuri ili basi mikakati yetu yote ya Kitaifa iweze kuingia kwenye mipango yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kujaza mahoteli tu siyo suala ambalo tunatakiwa tujivunie sana. Mahoteli yakijaa ina maana watalii wetu wakifanya booking wanaweza wakaenda hata nchi jirani kwa sababu hoteli zetu zimejaa. Kwa hiyo, kama taifa naomba tuje na mpangomkakati wa kuweza kuongeza hoteli zenye hadhi ya kulaza wageni wetu na kwenye mpango wa 2023/2024, basi tuone mambo haya yakitekelezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona sekta hii ya utalii ilivyo na nguvu ya kunyanyua uchumi wa nchi na inachangia zaidi ya asilimia 17 ya Pato la Taifa lakini asilimia 25 ya fedha za kigeni, hivyo ni muhimu sana tuweze kujikita kwenye sekta hii ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu. Vilevile tuendelee kuongeza bajeti katika Wizara hii ili basi tuweze kuistawisha sekta hii zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia bajeti ya Wizara hii. Naomba nianze kwa kumpongeza Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuifungua nchi yetu Kimataifa, vilevile kwa nia yake ya dhati aliyotuonesha Watanzania kwa kutuletea maendeleo kwenye hili tumeona kabisa amegusa huduma muhimu zile za msingi ambazo zinagusa wananchi moja kwa moja kama huduma za afya, elimu, barabara, pamoja na maji safi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia, niendelee kuwapongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuhakikisha miradi yote ya kimkakati inaweza kuendelea na kwa ufanisi mkubwa. Vilevile niwapongeze Watendaji wote wa Wizara hii ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa wakiongozwa na Waziri wetu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kwa usikivu wao wa hali ya juu pamoja pia na kuendelea kufuata ushauri wa Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita kwenye kushauri mambo kadhaa ambayo basi yataweza kuendeleza Wizara hii ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Naomba nianze kuchangia kwenye utekelezaji wa program ya kuwarudisha wanafunzi wetu mashuleni, hasa wale waliopata changamoto mbalimbali hususan ujauzito.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee kabisa kwenye hili naomba nianze kwa kumpongeza na kumshukuru Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu basi wa kuwarudisha wanafunzi wetu shuleni na kuwapa fursa nyingine mabinti wetu waweze kupata fursa ya kuendelea kielimu na baadaye kuweza kujikwamua kiuchumi. Kwenye program hii changamoto bado ni kubwa katika utekelezaji wake. Kwenye Halmashauri zetu nyingi hakuna miongozo madhubuti ya kuweza kufuatilia masuala haya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Halmashauri zetu nyingi hakuna taarifa rasmi za wanafunzi hawa, wanafunzi ambao wamekatiza masomo yao, wanafunzi ambao wamerudishwa shuleni kwa kipindi chote hiki. Na ukiangalia taarifa ya Mheshimiwa Waziri hapa katika ukurasa wa 21 hadi wa 27 kwenye hotuba yake utaona ametueleza data mbalimbali za uandikishwaji wa wanafunzi kuanzia elimu za awali mpaka kidato cha tano, idadi ya wanafunzi waliohitimu, elimu ya watu wazima na taarifa za wanafunzi waliopata elimu nje ya mfumo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri hapa hatujaona taarifa za wanafunzi hawa waliokatisha masomo yao katikati na vilevile wakarudishwa katika mfumo huu rasmi wa elimu. Hapa tunawanyima sana fursa mabinti zetu waliokatisha masomo na wenye hamu bado ya kuendelea kusoma. Tunawanyima fursa kwa sababu, hawana taarifa ya jinsi gani waweze kurudi kwenye mfumo rasmi. Nikichukulia mfano tu kwenye Mkoa wangu wa Arusha, Halmashauri zetu nyingi ikiwemo Longido, Ngorongoro, Meru, Arumeru, hakuna taarifa hizi, nimefuatilia binafsi, lakini sijapata taarifa hizi.
Naomba nitoe ushauri wangu kwa Mheshimiwa Waziri wakati anahitimisha hapa basi aweze kutuambia mikakati yake aliyonayo, mikakati ya Wizara iliyonayo kwa ajili ya kuhakikisha taarifa hizi zinapatikana rasmi na kunakuwa na miongozo rasmi kwa ajili ya kufuata kwenye Halmashauri zetu ili basi wanafunzi wetu hawa waweze kupata nafasi nyingine ya kurudi katika mfumo rasmi wa elimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala jingine naomba nichangie na kutoa ushauri wangu ni kuhusiana na mikopo ya asilimia 10 ambayo inatolewa na Halmashauri zetu. Changamoto za mikopo hii bado ni nyingi sana, kama Kamati ya Serikali za Mitaa ilivyoainisha hapa changamoto hizi ni nyingi na ushauri wake kwa Serikali basi Serikali inabidi ije na mikakati madhubuti kwa ajili ya kuweza kufuatilia utekelezaji wa mikopo hii ili iweze kuleta ufanisi kwa wananchi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ya Kamati inaonesha kuna Halmashauri zaidi ya 24 ambazo zimekopesha chini ya asilimia 50 ya mapato ya fedha zilizotengwa hadi kufikia Februari 20/22.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutenga kwa asilimia 10 ya mikopo ya Halmashauri ni takwa la kisheria kwa hiyo sioni sababu ya kwa nini Halmashauri zetu zinaacha kutenga asilimia 100 ya fedha zote zilizotengwa kwa ajili ya mikopo ya Halmashauri kwa makundi yale tajwa ya wanawake, vijana na walemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia changamoto nyingine ya marejesho wamesema wenzangu hapa hii ni changamoto kubwa sana ukiangalia kwenye taarifa tumeona kwamba kuna zaidi ya asilimia 50 ya fedha zote zilizokopeshwa kwa wananchi kuanzia mwaka 2018 hadi Februari, 2022 bado ziko mikononi kwa wananchi hawajaweza kurudisha na hakuna mikakati madhubuti basi ya Serikali kufatilia marejesho ya mikopo hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama utoaji wa mikopo ni takwa la kisheria basi tunaomba pia tuweke kanuni kali na miongozo ya kufuatillia marejesho ya mikopo hii ili basi ziweze kurudi kwenye mfumo ule revolving fund na wananchi wengi zaidi waweze kukopeshwa mikopo hii. Ukiangalia tu katika Mkoa wa Arusha tokea mwaka 2018 tumeweza kutoa mikopo takribani bilioni 12.7 lakini ni bilioni tano tu ambazo zimerejeshwa zaidi ya Bilioni Saba bado zipo mikononi mwa wananchi na hakuna kanuni maalum ya kuweza kuifuatilia hii mikopo iweze kurudishwa kwa wakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto zote hizo nimeona kamati pia imetoa ushauri mzuri mojawapo ni kuwepo kwa mifumo imara ya TEHAMA ili kuweze kufuatilia mikopo hii vilevile Mheshimiwa Waziri hapa wakati anatoa hotuba yake alitueleza hapa kwamba wataweka kigezo cha kuwapima Wakurugenzi wetu kutokana na ufanisi wa mikopo hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wakurugenzi wetu tayari wana kazi za kuwatosha na kazi hizo ndiyo zinapelekea mpaka tumefika leo hapa mikopo hii imeshindwa kufanyakazi kwa ufanisi. Kwa hiyo naomba kwa sababu changamoto hizi za mikopo zinajulikana kwenye Halmashauri zote 124 ni changamoto ambazo ziko common tuwatafutie Halmashauri zetu solution ambazo ni common pia ili basi Halmashauri zetu zote ziweze kufuata ili mikopo hii iweze kuwa na ufanisi zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia kwenye bajeti hii muhimu ya Wizara ya Elimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika maendeleo endelevu ya dunia na sisi kama nchi ambayo tunapaswa kuyatekeleza, lengo Namba Nne tunapaswa kuzingatia ubora wa kiwango cha elimu tunayoitoa kwa wanafunzi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni dhahiri kwamba katika maendeleo ya nchi yoyote ile ubora wa kiwango cha elimu unamchango mkubwa katika maendeleo ya nchi husika. Ili Walimu wetu waweze kutoa kiwango bora cha elimu ni lazima wao wenyewe wawe bora zaidi kwa kuwa na ujuzi stahiki vilevile sisi kama Serikali tuweze kuwaendeleza Walimu hawa mara kwa mara ili waendane na mabadiliko mbalimbali ya kidunia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia Bajeti ya Elimu kama Wizara, Wizara hii ni nyeti sana lakini mara zote tumekuwa tukitoa Bajeti ambayo ni ndogo ya Wizara hii ili kuendeleza elimu yetu. Hata ukilinganisha katika nchi za Afrika Mashariki, Tanzania bado tuko chini kwenye bajeti tunayoitoa katika Wizara hii muhimu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kiwango kile kidogo cha bajeti tunayotenga bado hatukipeleki kwenye eneo husika ili kuweza kuboresha kiwango cha ubora wa elimu tunayoitoa. Naishauri Serikali kwenye bajeti zijazo tuweze kutenga kiasi kikubwa cha bajeti kwa ajili ya kuboresha kiwango cha elimu tunayoitoa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika vitu ambavyo vinaboresha moja kwa moja elimu yetu ni lazima tuwape mafunzo mara kwa mara Walimu wetu ili waweze kuendana na matakwa ya kidunia vilevile ni lazima tuwe na nyenzo za kutosha ikiwemo vitabu ili tuweze basi kutoa elimu hii yenye viwango.
Naishauri Serikali kwenye bajeti zijazo iangalie na ihakikishe pia inatenga bajeti ya kutosha kwenye miundombinu laini ili basi tuweze kuendana na matakwa haya ya kidunia. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangie pia kwenye ufanisi wa Vyuo vyetu vya Kati ikiwemo VETA. Kama Kamati ilivyoshauri, imeshauri vizuri sana kwamba ujenzi wa Vyuo hivi vya Kati uendane sambamba na kuajiri Walimu wa Vyuo hivi. Natolea mfano tu pale Wilayani Ngorongoro - Samunge kuna Chuo cha VETA, chuo kizuri sana, kina majengo mazuri, chuo kina mandhari nzuri lakini kina uhaba mkubwa wa Walimu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, chuo hiki kina uwezo wa kutoa wahitimu zaidi ya 500 kwa wakati mmoja ambapo pia kwenye hili, chuo hiki kingeweza kuhudumia hata Wilaya tatu ikiwemo Ngorongoro, Karatu na Monduli kwa wakati mmoja. Tungeweza kukitumia chuo hiki vizuri tungeweza kutatua tatizo kubwa la ajira kwa wanafunzi wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Chuo hiki ukiangalia kwa sasa kina Walimu Watano tu, idadi ya Walimu inayohitajika ni ziadi ya Walimu 30 mpaka 40. Naomba Wizara hii iweze kuzingatia maoni haya ya Kamati ili basi Vyuo vyetu hivi vya VETA viweze kuleta tija kwa wahitimu wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la mikopo ya NMB ambayo Mheshimiwa Waziri ameeleza jana kwa kifupi sana kwa wahitimu wetu.
Kwanza kabisa naomba niwapongeze Benki ya NMB kwa kuona umuhimu wa kuwekeza katika elimu yetu. Japo kuwa Waziri jana alieleza kwa kifupi sana lakini jambo hili ni jema na linaonesha kabisa dhahiri kwamba litaenda kutatua tatizo la mikopo kwa wahitimu wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama wawakilishi wa wananchi tunahitaji kulijua hili jambo. Hili ni jambo jema na zuri kwenye sekta hii ya elimu, kulijua vizuri na kupata ufahamu mpana ili basi tuweze kwenda kuwaambia wananchi wetu ambao tunawawakilisha fursa hizi watazipataje, ikiwemo tuweze kujua vigezo na terms mbalimbali ili wanafunzi wetu waweze ku-access mikopo hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa ninaouwakilisha, Mkoa wa Arusha wanahitaji kufahamu watapataje mikopo hii ambayo inatolewa kwa riba nafuu na Benki yetu ya NMB. Naishauri Wizara pamoja na Benki hii ya NMB kwa pamoja waweze kuendesha semina kwa Wabunge kama wawakilishi wa wananchi ili tuweze kujua vizuri wananchi wetu watapataje fedha hizi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)