Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Mary Francis Masanja (212 total)

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba niulize maswali mawili mafupi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nashukuru sana kwamba nimepewa jibu la kina na naamini tutaendelea kulifuatilia suala hili. Zaidi ni kwamba hawa operators wanakuja na watu kutoka sehemu nyingine ambao hawajui hii mikataba. Kwa hiyo, hawaajiri wale vijana ambao wanatoka kwenye vijiji karibu na ule mlima, wao hawaelewi mikataba hiyo hivyo wanalipwa kidogo sana. Je, hatuwezi kuweka uwiano fulani hasa kwa zile shughuli ambazo hazihitaji taaluma kwamba hawa operators waweze kuajiri au kuchukua vijana kutoka kwenye kundi la wale ambao wanatoka karibu na mlima kwa sababu hiyo ni njia mojawapo ya kuwapa motosha? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni nyeti kidogo ni hili suala la nusu mile. Kwa vile tunajua kwamba watu wanaolinda ule mlima ni wale wanavijiji walio karibu na hifadhi ya mlima ule inakuwaje sasa suala la nusu mile. Nusu mile ni suala nimezungumza na Mheshimiwa Waziri na ni nyeti kidogo lakini nafikiri kwamba tusiliangalie kama watu wanaomba kuingia msituni isipokuwa ni ku-review ile mipaka ya msitu na kuongeza sehemu ndogo ambayo inaweza ikasaidia wale wananchi wanaoishi karibu kuweza kupata kuni na kupata malisho ya wanyama bila kuathiri miti. Siyo suala la kuingia isipokuwa ni suala la kupanua…
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kumekuwa na changamoto ya wageni kupata ajira kwenye maeneo ya hifadhi hasa kwenye Mlima Kilimanjaro. Hata hivyo, katika mwongozo wa waongoza utalii kuna kiwango ambacho wamewekewa waongoza utalii ambapo hawa watumishi kwa maana ya wanaoomba ajira wanaomba kwa kuzingatia mwongozo huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto pia kwenye upande wa kiwango kwamba mtu anapokuwa anahitaji ajira basi anapunguza kiwango kinakuwa chini ya mwongozo uliopo. Waongoza utalii (tour operators) wao wanazingatia zaidi kupata faida kwenye biashara zao. Kwa hiyo, huyu mtumishi anapokuwa akiomba ajira na kwa kuzingatia kwamba waombaji wa ajira wanakuwa ni wengi basi anapunguza kiwango ili aweze kupata ajira. Kwa hiyo, kumekuwa na changamoto hii lakini tunawashauri watumishi wanaokutana na changamoto hizi waende kwenye Tume ya Usuluhishi (Mahakama ya Kazi) ambayo inasimamia haki za mtumishi yeyote anapokuwa amedhulumiwa haki yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lingine ni kuhusu nusu mile, naomba itambulike kwamba maeneo ya hifadhi yanapokuwa yametangazwa kuwa hifadhi hairuhusiwi kufanya kitu chochote zaidi ya uhifadhi. Nimuombe sana Mheshimiwa Dkt. Kimei, sisi kama Serikali tunapokuwa tunahifadhi maeneo haya tunatunza ili yawe kivutio na kwa ajili ya kutuletea mapato.

Kwa hiyo, tunapokuwa tunatunza, hairuhusiwi kufanya kitu chochote ndani ya eneo la hifadhi, hata kama ni kuokota kuni hairuhusiwi. Kuna maeneo mengine ambayo huwa tunawatengea wananchi kwa ajili ya kuendelea na shughuli zingine kama ufugaji, uvuvi pamoja na kilimo lakini maeneo yanayotunzwa kama hifadhi hairuhusiwi kufanya kitu chochote.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kifupi sana kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, kwa kweli nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ambayo imeletwa na Mheshimiwa Dkt. Kimei inahusika pia na masuala ya mikataba ya ajira na stahiki za wafanyakazi na mfumo mzima wa uratibu wa ajira katika eneo la Mlima Kilimanjaro.

Mheshimiwa Naibu Waziri ameliweka vizuri, tayari Wizara ya Maliasili na Wizara yetu tumeweka ule mwongozo. Tunawaomba sana wafanyakazi wote wanapokutana na changamoto zozote ambazo pia zinahusiana na Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini, 2004, wajitahidi kuwa wanatoa taarifa mapema sana kwenye ofisi zetu za Idara ya Kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Waziri Mkuu kwa sasa imeamua kufungua kliniki maalum. Kila Ijumaa ya mwisho wa mwezi wafanyakazi wote ambao wanaona wana changamoto zinazohusiana na sheria za kazi watakuwa wanaripoti kwenye ofisi zetu za kazi ili wakaeleze zile changamoto wanazozipata kama ni za mishahara, mikataba na mambo mengine yoyote ili ofisi ya Waziri ya Waziri Mkuu iweze kuchukua hatua haraka ili kuondoa migogoro katika maeneo ya kazi kati ya mfanyakazi na mwajiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunamuomba sana Mheshimiwa Kimei kama ana mambo ya ziada aonane pia na ofisi yetu na tutaweza kulifanyia kazi na tutaagiza utaratibu na mwongozo usimamiwe vizuri. (Makofi)
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa jambo hili ni la dharura kwani kwa sasa wakulima wamelima, wamepanda, wamepalilia na kutia mbolea katika mashamba yao kwa thamani kubwa lakini makundi ya tembo yameingia na kuvuruga mashamba hayo na wakulima wamepata taharuki hasa baada ya mkulima mmoja kuuwawa na tembo hao. Je, Serikali inaweza sasa kupeleka kikosi maalum kufanya operation ya kuwaondoa na kuwafukuza tembo hao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa jambo hili linasababishwa pia na makundi ya ng’ombe waliondolewa katika maeneo ya Mkoa wa Morogoro na kuingia katika maeneo ya hifadhi ya tembo hawa na kuharibu ecology yake na kufanya tembo hawa kufika kwa wananchi. Je, Serikali kwa kutekeleza azma ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa katika hotuba yake ukurasa wa kumi na sita hapa Bungeni kwamba itaongeza maeneo ya hekta kufika milioni sita…

SPIKA: Fupisha swali Mheshimiwa.

MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, Serikali imejipangaje kutekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Rais ya kuongeza maeneo ya wafugaji ili kuondoa mgongano huu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Vita Rashid Kawawa, Mbunge la Jimbo la Namtumbo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la kwanza ambalo amesema kupeleka vikosi kazi kwa ajili ya kwenda kushughulikia uvamizi wa tembo; Serikali ipo tayari na hata leo anavyowasilisha tayari Serikali ilishafanya mchakato wa kuhamisha hao tembo na inaendelea kuwaondoa katika maeneo hayo ya mashamba na shughuli za kibinadamu. Kwa hiyo nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Kawawa, kwenye hili suala la uvamizi wa tembo katika maeneo yanayozunguka au ya kandokando ya hifadhi kwamba, Serikali ina vikosi ambavyo viko katika Wizara ya Maliasili na Utalii, kwa kutumia Jeshiusu inaendelea kuwaondoa hawa tembo na wanyama wengine wakali ili kuwawezesha binadamu kuendelea na shughuli zao za kila siku.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la kundi la ng’ombe kwamba wanahamia kwenye maeneo ambayo yamepakana na hifadhi; naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Vita Kawawa kwamba Kamati ya Mawaziri iliundwa na Serikali kuangalia maeneo yote yenye migogoro ikiwemo migogoro inayozunguka mipaka yote ya hifadhi. Sasa hivi Kamati hii ilishamaliza kazi yake na utekelezaji wake unaenda kuanza baada ya Bunge hili Tukufu kumalizika. Hivyo maeneo yote ambayo yana migogoro kama ya namna hii Serikali inakwenda kuyamaliza na niwaondoe wasiwasi Waheshimiwa kwamba wote ambao wana changamoto hii inakwenda kumalizwa na maamuzi ya Kamati ya Mawaziri. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Majibu ya Serikali hayajaniridhisha kwa sababu wananchi wetu kwenye zoezi hili la kuweka beacon walishirikishwa kuweka beacon tu, hawakushirikishwa kwenye mipaka itawekwa maeneo gani.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari baada ya Bunge hili tuongozane kwenda Makete tukawape majibu wananchi wetu na kurudia zoezi la kuweka beacon? Kwa sababu zoezi hili limesababisha wananchi wangu wengi saa hizi wako ndani lakini sehemu ya shule zimewekwa beacon…

SPIKA: Mheshimiwa Festo…

MHE. FESTO R. SANGA: Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari twende wote?

SPIKA: Nisikilize kwanza; swali lako halijaeleweka kabisa, kwamba wananchi wako wlaishirikishwa kuweka beacon lakini hawakushirikishwa mahali pa kuweka, sasa…

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, kilichotokea wananchi wamefika wamekuta watu wa kutoka Serikalini wanaweka beacon, hawajaambiwa kwamba ni eneo hili la mpaka au wapi. Kilichotokea nyumba nyingi za wananchi ziko ndani ya hifadhi, kitu ambacho hakikuwepo, siku za nyuma mipaka ilikuwa mbali. Leo hii wananchi wangu wengi wako ndani ni kwa sababu ya hilo jambo. Sasa ninachomuomba Naibu Waziri tuongozane baada ya hili Bunge twende Makete akawape wajibu wananchi wetu turudie zoezi; hicho ndicho ninachomwomba. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara iko tayari kuhudumia wateja wa aina yoyote akiwemo Mheshimiwa Sanga, hivyo naahidi baada ya Bunge lako Tukufu nitaongozana naye nikiwa na wataalam kwenda kuonesha hiyo mipaka ili wananchi watambue mipaka ya hifadhi ni ipi na iendelee kuheshimiwa. (Makofi)
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza na linakwenda kabisa sambamba na tatizo alilonalo Mheshimiwa Sanga kule Kitulo. Zoezi la uwekaji mipaka ya Hifadhi za Taifa na maeneo ya jamii halikuwa shirikishi kabisa katika Jimbo langu la Longido katika eneo linalotutenga na Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro. Kuna eneo la buffer zone la hekta 5,000 ambazo lilitengwa tangu Serikali ya Awamu ya Kwanza kwamba liwe ni eneo la buffer zone lakini matumizi yaliyoruhusiwa ni kuchunga tu. Hivi leo baada ya beacon kuwekwa bila kuwashirikisha wananchi wanaanza kupelekeshwa kuchungia katika buffer zone. Naomba kuiuliza Wizara, je, wako tayari kutoa tamko kwamba eneo la buffer zone katika ukanda wa msitu wa Mlima Kilimanjaro na Hifadhi ya Taifa zina access ya wachunga mifugo wa Longido na Siha kuchungia?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kiruswa, Mbunge wa Longido, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, maeneo ya buffer zone yana miongozo yake na Wizara itaangalia kama inaruhusu kutumika kwa shughuli zingine. Hata hivyo, kwa sababu Kamati ya Mawaziri ilishafanya maamuzi ikapitia baadhi ya maeneo ambayo yalikuwa na migogoro na maamuzi hayo tunatarajia kwamba yataanza kutekelezwa baada ya Bunge lako hili Tukufu, nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba awe na subira tumalize Bunge, tuangalie sasa kama yale maeneo anayoyasema yeye yatakuwa ndani ya maamuzi ya Kamati ya Mawaziri ambavyo vijiji 920 tayari vitakuwa vimefaidika na maeneo hayo. Kama kitakuwa hakimo basi Wizara itaendelea kushirikiana naye kuangalia ni kitu gani ambacho tunaweza kufanya ili tusiweze kuathiri maeneo ya machunga (malisho) na kwenye maeneo ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. SILLO D. BARAN: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwa kuwa bado mgogoro huu unafurukuta katika vijiji nilivyovitaja, je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kufanya ziara ili wananchi wapate kutatua migogoro hii?

Mheshimiwa Spika, swali la pili…

SPIKA: Kwa nini Waheshimiwa mnamgombea Mheshimiwa Waziri kama mpira wa kona aje majimboni kwenu?

Endelea Mheshimiwa swali la pili.

MHE. SILLO D. BARAN: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mwaka 2019 ulitokea uharibifu wa mazao ya wananchi katika vijiji nilivyovitaja ambao ulisababishwa na wanyama hasa tembo, je, ni lini Serikali itawalipa kifuta jasho wananchi hawa ambao mashamba yao yameathirika?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sillo Daniel Baran, Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Sillo juu ya kuongozana na mimi maana ni majukumu yangu ya kazi, hivyo hilo niko tayari baada ya Bunge lako hili Tukufu tutaenda naye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili la nyongeza ambalo ameuliza juu ya uharibifu wa wanyama wakali; Serikali inawajali sana wananchi wake na inatambua kwamba kuna uharibifu wa wanyama wakali ambao wamekuwa wakiwasumbua wananchi hasa wale ambao wanakuwa wamepanda mazao yao na wanyama wakali hususan tembo huenda katika maeneo hayo na kuharibu.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua hilo ilianzisha Mfuko ambao huwa tunalipa kifuta jasho au kifuta machozi. Kifuta machozi au kifuta jasho ni kwa ajili ya kuwapoza wale ambao wanakuwa wameathirika na changamoto hii ya wanyama wakali. Hivyo, hadi Machi, 2020, Serikali ilikuwa imeshalipa jumla ya shilingi bilioni 5.9 kwa ajili ya kifuta machozi au kifuta jasho kwa wananchi hawa ambao wamekuwa wakiathirika na changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, napenda nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendelea kuhakiki madai yote ambayo wananchi wameathirika na changamoto hii ya wanyama wakali na itaendelea kulipa kadri inavyopata taarifa.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii niulize maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; katika operesheni za askari wa Wanyamapori kumekuwa na tabia ya askari kunyang’anya wananchi mali ikiwemo mashine za boti, mikokoteni na mali nyingine za wananchi. Nataka kujua kauli ya Serikali ni nini kwa sababu askari hawa wamekuwa wakizikamata hizo mali, wanakuwa nazo zaidi ya miaka miwili mpaka mitatu, ambayo hiyo ni hasara kwa Serikali na kwa wananchi kuwasababishia umaskini?

Swali la pili; naomba kutokana na unyeti wa tatizo hili na hali kuwa tete katika maeneo haya; je, Naibu Waziri yuko tayari kama Wizara kuja baada ya Bunge hili ili wajionee uhalisia wa jambo hili?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, masuala ya kisheria yanapokuwa yako chini ya kimahakama, sisi kama wahifadhi tunategemea zaidi Mahakama jinsi itakavyoamua. Kwa hiyo, ushahidi mara nyingi lazima ubaki kama kielelezo tosha pale ambapo kesi inapopelekwa Mahakamani, basi ushahidi utolewe ukionyesha na vitu ambavyo amekamatwa navyo mtuhumiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala hili, kwa kuwa mhimili wa Mahakama ni sehemu nyingine tofauti na mhimili wa Wizara ya Maliasili na Utalii, hivyo kwenye masuala ya kisheria tunayaacha yanaendeshwa kisheria na vifaa vyote ambavyo amekamatwa navyo mtuhumiwa inakuwa kama ushahidi, hivyo vinaendelea kutumika mpaka pale ambapo Mahakama inakuwa imeshatoa maamuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lingine la kuamba na Mbunge, Wizara iko tayari na tutaenda kuangalia hiyo migogoro iliyoko katika eneo hilo na tutalisuluhisha kadri itakavyowezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona na mimi.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto zilizoko kule Kwela, zinafanana sana na kule Arumeru Mashariki hususan Kitongoji cha Momela ambacho kimepakana na Hifadhi ya Arusha National Park.

Je, Serikali inasemaje kuhusu ule mgogoro ambao umedumu kwa miaka kama mitano sasa hivi, wananchi walikuwa wanaishi kwenye yale mashamba, baada ya ukomo wa umiliki kumalizika, baadae wakaja kuondolewa kwa nguvu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimesema awali kwamba Serikali kwa kutambua umuhimu wa wananchi wake na jinsi ambavyo kumekuwa na migogoro ya ardhi hasa upande wa mipaka ya hifadhi, iliteua Kamati ya Mawaziri nane ambao walitembelea maeneo yote ya hifadhi nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kamati hii tayari imeshamaliza mchakato wake na tumeshaanza kukaa kwa ajili ya kuangalia namna ya kutatua migogoro hii. Namwomba Mheshimiwa Dkt. Pallangyo awe na subira maana Kamati hii tayari imeshaanza kazi na baada ya Bunge lako tukufu hili utekelezaji wake sasa utaanza. Kwa hiyo, sehemu zote ambazo zina migogoro ya mipaka inaenda kutatuliwa na pale ambapo kuna migogoro mipya itakayoibuka, basi Serikali itaona ni utaratibu gani mwingine ambao itafanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe tu rai kwa maeneo mengi nchini ambayo yanakutana na hii changamoto ya mipaka na migogoro ya hifadhi, mara nyingi kumekuwa na tatizo kubwa sana la wananchi kuvamia maeneo ya hifadhi. Maeneo haya kwa asilimia kubwa ni njia za wanyama (shoroba). Kwa hiyo, migogoro mingi tunaianzisha kwa maana ya wananchi kupewa maeneo, lakini kwa upande wa pili tena tunaanzisha mgogoro mwingine wa wanyama wakali kupambana na wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge, tuwe na hiyo tahadhari pia kwamba tunapokuwa tunayaachia maeneo, lakini tunakuwa tumeanzisha mgogoro mwingine tena kati ya wanyama na binadamu. Maana wanyama siku zote wanapita maeneo yale yale ambayo walizaliwa nayo mwanzo na waliwaacha mabibi na mababu zao pale. Kwa hiyo, hili tatizo litaendelea kuwepo tu kama wananchi wenyewe hawatakubali uhifadhi ubaki kuwa hifadhi na maeneo mengine ya wananchi yaendelee kutumika kwa wananchi wa kawaida. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kinipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza niipongeze Serikali kwa juhudi zinazoendelea kuboresha miundombinu katika Hifadhi ya Ibanda na Rumayika.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwenye awamu iliyopita ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, alitoa maelekezo kuwekwa mipaka maeneo ambayo yalikuwa yamevamiwa na wananchi na akaelekeza maeneo haya yawekewe mipaka ili wananchi wasiendelee kuvamia yale maeneo, na Serikali ilileta wataalam wakaja kupitia maeneo yale. Baada ya kupitia, Serikali bado haijaweka mipaka kwenye maeneo hayo ya hifadhi na wananchi wameendelea kubugudhiwa. Je, ni lini Serikali itaweka mipaka inayotambulika ili wananchi hawa wasiendelee kusumbuliwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwenye hifadhi hizi pamoja na kutengwa sisi tunashukuru sana Serikali, lakini bado hatujaona juhudi za Serikali za kuweka vivutio ambavyo vitawavutia watalii. Ni lini Serikali italeta vivutio katika Hifadhi ya Ibanda na Rumanyika ili kuvutia watalii waje katika maeneo hayo? Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Swali lako la pili halijaeleweka Mheshimiwa Bilakwate; Serikali ilete vivutio tena wakati hifadhi zenyewe ndiyo vivutio?

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, samahani, kwenye hizo hifadhi hakuna wanyama, yaani hakuna vile vivutio ambavyo vinaweza kuwavutia watalii kuja kuangalia.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, lenye kipengele (a) na (b), kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nianze na mipaka. Ni kweli Wizara ya Maliasili na Utalii imekuwa ikiainisha maeneo mbalimbali yanayohusiana na hifadhi kwa kuweka mipaka katika maeneo ambayo yanahusiana na uhifadhi. Katika Hifadhi ya Ibanda – Kyerwa na Rumanyika tulifanya tathmini baada ya wataalam wetu kwenda kuainisha mipaka na utekelezaji wake tunaendelea kuandaa mazingira ya kupeleka wataalam kwa ajili ya gharama za uthamini ikiwemo kuainisha maeneo yenye changamoto hizi za uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, lakini tunatoa maelekezo kwenye upande wa maeneo haya ambayo tayari yamesha ainishwa, kwamba wananchi ambao wanazunguka maeneo haya wasiendelee kubugudhiwa mpaka pale ambapo wataonyeshwa eneo ambalo linahitajika kwaajili ya uhifadhi na maeneo ambayo wataachiwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu upande wa vivutio. Serikali inatambua kwenye hifadhi hizi ambazo ni mpya ambazo tayari zimeshatangazwa, zina wanyama lakini baadhi hawapo, hasa vivutio vya wanyama wakali kama simba na tembo. Serikali ina mpango wa kupeleka mbegu za wanyama hawa ili kuimarisha maeneo yenye uhifadhi katika maeneo hayo ili kuendelea kuongeza idadi ya Wanyama katika hifadhi hizi, lakini pia vivutio mbalimbali vinavyohusiana na mambo ya mali kale na mambo mengine ambayo yanahusiana na vivutio. Naomba kuwasilisha.
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro ilianzishwa mwaka 1959 na mgogoro uliopo umekuja mwaka 2003 ambao umeweza kuchukua maeneo ya wananchi wa eneo hili la Kata ya Mbulumbulu, Kijiji cha Lositete. Sasa ni nini majibu ya Serikali kwa sababu mwaka 1959 kuanzishwa kwa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, hakukuwa na mgogoro, lakini mgogoro umekuja baada ya marekebisho ya mwaka 2003.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, ni lini Waziri yuko tayari kuongozana nami ili ajionee katika maeneo ya Kata ya Mbulumbulu, eneo la Lositete ili kuona kwamba wananchi jinsi wanavyopata shida katika eneo hili la Lositete? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Daniel Awack, Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimkumbushe Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati hifadhi hizi zinaanzishwa mwaka 1959, wilaya zilikuwa ziko ndani ya wilaya za zamani. Kwa mfano; Karatu ilikua ndani ya Mbulu na sasa hivi Karatu iligawanywa, lakini pia na Ngorongoro ni Wilaya, kuna Monduli na kadhalika. Kama ambavyo nimejibu kwenye jibu langu la msingi, ni kwamba haya maeneo yalienda kutafsiriwa na Kamati za Ulinzi na Usalama za Mkoa pamoja na Wilaya na walishirikishwa wananchi kutambua ile mipaka.

Mheshimiwa Spika, huu mpaka ambao unagombaniwa ni mpaka ambao ni wa muhimu sana kiuhifadhi; kwanza unatunza maji, unatunza mazingira, lakini pia, hawa wananchi walioko kwenye maeneo yale wanang’ang’ania kuingia mle kuchunga mifugo yao. Hatari itakayojitokeza ni kwamba maeneo mengi tunaenda kuyamaliza na tutasababisha kuwepo na tatizo la kukosa maji na wananchi katika maeneo yale wataweza kuathirika.

Mheshimiwa Spika, niwaombe wananchi watambue kwamba Serikali ina nia njema ya kutunza vyanzo vya maji kwa ajili ya jamii zinazozunguka maeneo hayo. Pia eneo lile tumelihifadhi kwa ajili ya Hifadhi ya Ngorongoro ambapo kuna eneo ambalo ni msitu ambao unahifadhiwa kwa ajili ya kutunza vyanzo vya maji kwa ajili ya wenyeji waliomo ndani yake. Niwaombe sana wananchi watambue kwamba Serikali ina nia njema na inawapenda ndiyo maana inahifadhi maeneo haya kwa ajili ya maisha yao ya kila siku.

Mheshimiwa Spika, ombi lake la pili la kuongozana na mimi, nimtoe wasiwasi tutaongozana wote kama ambavyo nimefanya kwenye ziara zangu nyingi baada ya Bunge la mwezi wa Sita kuisha, kwa hiyo tutakwenda pamoja. Ahsante.
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na niishukuru Serikali kwa majibu mazuri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa tuna vijiji ambavyo vimepakana moja kwa moja na Hifadhi ya Mikumi. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kuweka kila kijiji angalau kuwe na game ambaye ataweza kuzuia tembo mara tu anapotoka kwenye hifadhi na kutaka kuingia kwa wananchi?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili, kwa kuwa tuna wananchi zaidi ya 28 wameshapoteza maisha kwa sababu ya tembo, lakini wananchi zaidi ya 2,000 mazao yao yameharibiwa na tembo.

Je, ni lini sasa Serikali itaenda angalau kuwafuta machozi na kuwafuta jasho kwa kupata uharibifu na tembo katika Wilaya yetu hii ya Mvomero? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jonas Van Zeeland, Mbunge wa Mvomero kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameomba kuwepo na askari maalum kwa ajili ya kuweka usalama wa wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi vikiwemo vijiji ambavyo amevielezea, nimuahidi tu Mbunge kwamba Serikali inatambua changamoto hii na ndio maana tumekuwa tukitoa ushirikiano wa karibu sana na wananchi kuhakikisha kwamba wananchi wanalindwa na mali zao pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba atuvumilie lakini tutaandaa eneo maalum kwa ajili ya kuweka askari game ambao watakuwa standby kwa ajili ya kufanya patrol katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tuna upungufu wa askari kwa maana ya kuweka kila Kijiji, nimuombe aendelee kutuvumilia, lakini tutahakikisha tunaimarisha eneo lile ili wanyama wakali na waharibifu wasiendelee kuvamia wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kifuta machozi nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge hili Tukufu nitazunguka kwenye maeneo yote ambayo hayajapata kifuta machozi. Nimuahidi kwamba nitalisimamia zoezi hili mimi mwenyewe kuhakikisha kwamba wananchi wanalipwa kwa wakati. Ahsante. (Makofi)
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nashukuru majibu ya Serikali, lakini kwa kuwa, mgogoro huu umekuwa ni wa muda mrefu na umechukua eneo kubwa la Jimbo la Igunga, takribani kilometa za mraba 450. Sasa nilikuwa namuomba Naibu Waziri kwasababu, kumekuwa pia kuna mvutano kati ya wananchi na Serikali na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya wilaya yetu, nilikuwa namuomba Naibu Waziri kama atakuwa tayari baada ya Bunge hili la Bajeti niambatane naye tuende Igunga tukakutane na wananchi na Kamati ya Ulinzi na Usalama tuweze kulimaliza? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UTALII NA MALIASILI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ninaomba tushirikiane Waheshimiwa wote Wabunge ambao tunawakilisha wananchi kutoka katika maeneo yetu husika. Suala muhimu la uhifadhi ni wajibu wa kila mmoja wetu kutambua kwamba, Serikali inapohifadhi maeneo husika ni kwa ajili ya faida ya wananchi wa eneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia jibu langu la msingi ambalo nimelijibu mwanzo, nimeelezea kwamba, eneo hili ni moja ya vyanzo vya maji ambavyo vinategemewa katika Mikoa ya Tabora, Simiyu na Singida.

Kwa hiyo, ninakubaliana na wazo la Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutaambatana naye, lakini ni wajibu wa kila Mheshimiwa kuelimisha wananchi wanaomzunguka kwamba, uhifadhi ni wajibu wa kila mtu na faida na hasara za uhifadhi tunaziona, lakini pia tunapohifadhi vyanzo hivi vya maji ni kwa ajili ya wananchi wanaoishi kwenye maeneo husika. Lakini pia tunaepuka mambo mengi ikiwemo kuanzisha majangwa ambayo yanaweza yakasababisha ukame katika nchi yetu. Naomba kuwasilisha.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu ya Serikali. Naomba niulize maswali madogo mawili. Kutokana na Mradi huu wa REGROW tulitegemea sasa wananchi wa Mikoa ya Kusini kuanza kutengeneza ajira nyingi sana kupitia utalii na kuongeza pato la mikoa hii; na tulitegemea sasa ujenzi wa Vyuo vya Utalii Nyanda za Juu Kusini katika eneo la Kihesa Kilolo na Makao Makuu.

Je, ni elimu kiasi gani imetolewa kwa wananchi wa mikoa hii ili kuwajengea uwezo katika kuupokea mradi huu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Biashara ni matangazo. Kwa kuwa mikoa yetu hii ya kusini tunavyo vivutio vingi na vizuri vikiwemo Mbunga za Wanyama Ruaha National Park ambapo ni Mbuga ya pili kwa ukubwa katika Afrika; tunavyo vivutio vingine kwa mfano pale Kihesa kuna Gangilonga, jiwe lililokuwa linaongea, lakini tuna Kitanzini ambayo ni sehemu ambayo watu walikuwa wanajinyongea; na vile vile tunalo fuvu la Mtwa Mkwawa ambalo lipo pale Kalenga…

SPIKA: Sasa swali Mheshimiwa.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, nini mkakati wa kuvitangaza hivi vivutio vya kusini ili kupata angalau tupate watalii wa ndani na kuongeza mapato? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Ritta kwa swali lake zuri, maana hii ni kwa manufaa ya Mikoa yote ya Kusini mwa Tanzania. Mradi huu ni faida kubwa sana kwa wananchi na mikoa ya kusini mwa Tanzania kwani Serikali imewekeza kiasi kikubwa cha fedha ambao ni mkopo.

Mheshimiwa Spika, katika swali la msingi la Mheshimiwa Ritta ameuliza kwamba tuna mkakati gani kuhakikisha wananchi wanapata elimu ya kutosha pindi wanapopokea huu mradi? Pia na namna ambavyo wataenda kutelekeleza.

Mheshimiwa Spika, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ina mpango mkubwa wa kuanzisha vyuo ambavyoo vitakuwa ni campus. Tunaanzisha campus ya Mweka na pia kutakuwa na Chuo cha Mambo ya Utalii ambacho kitaanzishwa kama Campus ya Iringa. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi kwamba wananchi wa kusini mwa Tanzania wataweza kuelimika. Pia tutahamasisha utalii kupitia elimu hiyo.

Mheshimiwa Spika, swali lake lingine alisema biashara ni matangazo. Ni kweli bila kutangaza vivutio vyetu tulivyonavyo hapa nchini, utalii hauwezi kuendelea. Kipindi cha mpango huu wa bajeti, tumetenga kiasi cha shilingi bilioni 46.5 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba utangazaji wa vivutio tulivyonavyo hapa nchini unafanyika kwa nguvu zote.

Mheshimiwa Spika, pia kwenye utangazaji bila kuimarisha miundombinu inakuwa ni changamoto; na hilo nimtoe wasiwasi kwamba tumetenga shilingi bilioni 75.4 ambazo zitaimarisha miundombinu iliyoko kwenye hifadhi hizo ili tuimarishe na kutangaza kwa bidii. Ahsante. (Makofi)
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Moja, hivi tunavyoongea, juzi makundi makubwa ya tembo wamevamia vijiji vyote vitano vya Kata ya Igava na wameshambulia mazao yote; mahindi, mpunga na maboga. Sasa wananchi wale wapo hatarini kupata janga la njaa. Ni lini Serikali itawalipa fidia wale wananchi kuwanusuru wasipatwe na janga la njaa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, kwa kuwa ng’ombe wakiingia hifadhini kwa bahati mbaya, ng’ombe mmoja huwa anatozwa shilingi 100,000/=, sasa makundi ya tembo wale wametetekeza mazao yote na nimeenda juzi nimekuta ni mashimo matupu mashambani: ni kigezo gani au ni thamani gani watalipwa wale wahanga ambao ni wafugaji na wakulima wa sehemu ile? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kuhusu fidia, tumekuwa tukifanya uthamini pale ambapo kunatokea changamoto hiyo ya tembo kuingia kwenye maeneo ya kilimo na tunapofanya uthamini tuna-compensate wananchi kulingana na uthamini ulivyofanyika.

Mheshimiwa Spika, kuna uthamini wa aina mbalimbali; kuna mwananchi kuwa amepoteza Maisha, na upande mwingine kupoteza mazao na pia wananchi kujeruhiwa. Kwa hiyo, tunalipa fidia kulingana na athari ilivyojitokeza.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni kuhusu changamoto ya namna ambavyo tunatoza ng’ombe shilingi 100,000/=; kwanza naomba sana wananchi watambue kwamba sisi tupo kwa ajili ya kuhakikisha kwamba hifadhi hizi zinalindwa na zinatunzwa kwa ajili ya manufaa ya nchi kwa ujumla na wananchi waliopo kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, mara nyingi kumekuwa na sintofahamu hasa kwa wafugaji kwamba wanaingiza ng’ombe zao kwenye hifadhi kwa makubaliano ya watumishi walioko kwenye maeneo husika na matokeo yake wanyama ambao wanahifadhiwa kwenye maeneo yale wanakutana na changamoto za magonjwa. Sasa Serikali inajikuta inagharamia gharama kubwa kufanya utafiti wa gonjwa lililoingia kwenye hao wanyama na kuwatibu. Kwa hiyo, tunajitahidi sana kuzuia wafugaji wasiingize mifugo yao kwenye maeneo ya hifadhi. Tutambue kwamba sheria ni sisi wenyewe tulizitunga, kwa hiyo, sisi ni watekelezaji wa sheria.

Mheshimiwa Spika, kiwango hiki kipo kwenye sheria, siyo kwamba sisi tumekiamua; kipo kwenye sheria ya Wanyama kwamba wananchi wanapoingiza mifugo yao kwenye maeneo ya hifadhi, basi tunatumia hiyo sheria kuhakikisha kwamba inatumika sawa sawa. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza: kwenye Hifadhi ya Kitulo kwa sababu ni hifadhi yenye upekee na hifadhi nyingine za Tanzania: Je, Serikali haioni haja kuwavutia zaidi wawekezaji kwa kupunguza gharama za uwekezaji; kwa sababu, gharama zimekuwa ni kubwa? Kwa maana, ukiangalia kuna wana- Makete na Watanzania ambao wako tayari kuwekeza kwenye hifadhi hizi, lakini gharama kwa mfano za environmental assessment tu ni zaidi ya shilingi milioni 50, kitu ambacho kimekuwa kiki-discourage wawekezaji.

Sasa je, Serikali umuhimu wa kupunguza gharama ili wawekezaji wawe wengi kwenye hifadhi zetu na ziweze kutangazwa?

Swali la pili: Hifadhi ya Kitulo inaenda kupitiwa na barabara ya kiwango cha lami inayotoka Isyonje kwenda Kitulo kupitia Makete, lakini bado miundombinu ya ndani ya hifadhi siyo mizuri kwa maana ya barabara: Ni mpango upi wa Serikali kupitia Wizara ya Maliasili kuhakikisha kwamba miundombinu ndani ya Hifadhi ya Kitulo inaimarishwa ili tuweze kuvutia wawekezaji wengi zaidi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Naibu Spika, ahsante. Kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Sanga kwa kuwa na jitihada nyingi sana za kuhakikisha kwamba hifadhi yetu ya Taifa ya Kitulo inapaishwa vizuri, hasa kiuwekezaji, lakini pia kwenye maeneo ya utalii. Napenda nimweleweshe Mheshimiwa Mbunge kwamba, sisi kama Wizara ya Maliasili na Utalii hatuna gharama yoyote inayohusiana na uwekezaji. Wawekezaji wa aina mbalimbali wa ndani na nje ya nchi wanaalikwa kwenye maeneo yote ya uhifadhi kuja kuwekeza uwekezaji mbalimbali, ikiwemo ujenzi wa hoteli, ma-tent, camps, hostels mpaka na lodge. Sisi tunawaalika wawekezaji wote bila kubagua. Gharama kama gharama ni taratibu za uwekezaji ambazo haziko kwenye Wizara yetu, isipokuwa mwekezaji yeyote anatakiwa kufuata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa miundombinu Serikali imejipanga kwa mwaka wa fedha 2021/2022 kuhakikisha kwamba maeneo yote ya uhifadhi yanatengewa fedha ya kutosha kuhakikisha miundombinu yote ndani ya hifadhi inaimarika vizuri ili kwenye upande wa utalii sasa tuweze kuhamasisha utalii na maeneo yale yaweze kupitika kwa urahisi. Ahsante.
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni hitaji la wananchi wa Kitulo la kuitangaza hifadhi hiyo kama kivutio ambacho kiko nchini kwetu; na kwa kuwa, hitaji hilo linafanana sana na hitaji la wananchi wa Katavi la kuitangaza Katavi National Park ambayo ina vivutio vingi sana vya asili vya utofauti akiwepo twiga mweupe anayepatikana kipekee sana katika Mkoa wetu wa Katavi:-

Je, Serikali ina mikakati gani mipya ya kuitangaza hifadhi hiyo ili iweze kufahamika ndani na nje ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Naibu Spika, ahsante. Serikali ina mpango wa kuipaisha hifadhi ya Katavi kwa kuzingatia bajeti iliyopo kwenye mwaka wa fedha wa 2021/2022. Eneo hili ni eneo zuri sana kwenye upande wa utalii.

Mheshimuwa Naibu Spika, hivyo, nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Martha kwamba Serikali inatambua mchango wa Hifadhi ya Katavi na kwamba ni eneo zuri sana kwenye kuhamasisha utalii. Hivyo, tutajitahidi sana pamoja na maeneo mengine yote yaliyoko Tanzania ambayo yana vivutio kuhakikisha kwamba tunayatangaza ili tuweze kupata watalii wengi na kufikia namba ambayo imekusudiwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Kama unavyokumbuka kwamba mifuko hii imeweza kuchangia maendeleo makubwa katika masuala ya uhifadhi, hususan kupunguza wimbi la ujangili nchini pamoja na kuongeza wigo wa masuala mazima ya miradi ya wanajamii, halikadhalika kuingiza vivutio ambavyo vimetupelekea kufikia lengo la watalii 1,300,000: Je, kutokana na mabadiliko ya sheria hii, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba mabadiliko haya hayaendi kudumaza maendeleo ambayo yamefikiwa katika matumizi ya mifuko inayoathirika kutokana na sheria hii?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kama tunavyofahamu, mwezi wa Pili mwaka huu Mheshimiwa Waziri Mkuu alifungua maonyesho ya mifuko pale Arusha na alitoa wito wa kwamba mifuko hii iweze kuendelezwa ili kufikia malengo yaliyokusudiwa.

Je, tuna mpango gani mbadala wa kuisaidia mifuko hii ili pamoja na mabadiliko haya ya sheria ambayo yamefanyika kuhakikisha kwamba yanakwenda kusaidia mafanikio ambayo yamepatikana hasa tukilinganisha kwamba hivi sasa wenzetu wa CMA wameanza kulalamika kutokana na matatizo ya...?

SPIKA: Ahsante sana. Umeshaeleweka Mheshimiwa.

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. kwanza nashukuru kwa swali la Mheshimiwa Soud, lakini nimtoe wasiwasi kwamba Serikali iliona suala hili baada ya mifuko hii fedha zake zilizokuwa zinakusanywa kupelekwa kwenye Mfuko Mkuu wa Hazina, Serikali ilianza kutekeleza majukumu yake yaliyokuwa yanatekelezwa kwenye mfuko huu kupitia bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, nimtoe wasiwasi kwamba shughuli sasa ambazo zilikuwa zinatekelezwa na mfuko huu ikiwemo uhifadhi, kudhibiti ujangili na shughuli nyingine za kuendeleza utalii, kukuza na kutangaza utalii, Shughuli zote hizi sasa zinatekelezwa na bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Kwa mwaka wa fedha 2021/2022 shughuli zote zilizokuwa zinatekelezwa kwenye mifuko hii, sasa zimeingizwa kwenye bajeti kuu ya Serikali. Naomba kuwasilisha.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Pamoja na kumwalika Naibu Waziri aje kutembelea msitu wa hifadhi wa Rondo, maeneo ya Tarafa ya Rondo, Rutamba, Milola na Kiwawa yamekuwa yakiathiriwa sana na Wanyamapori hasa tembo; na kwa kuwa idadi ya askari wanaohusika na ulinzi wa eneo hili ni kidogo.

Je, Serikali iko tayari kutoa mafunzo na kuwawezesha vijana wa maeneo haya washirikiane na wale askari katika kusaidia kulinda mali na Maisha ya wananchi wa eneo hili?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Spika, ahsante. Ni kweli kumekuwa na matukio mbalimbali ya uvamizi wa tembo. Hii tukumbuke tu kwamba tunaishi maeneo mengi ambayo kihistoria ilikuwa ni mapito ya Wanyamapori wakiwemo tembo. Wizara kwa mara nyingi imekuwa ikipata hizi taarifa na kutoa ushirikiano kwa wananchi ikiwemo kupeleka maaskari kuwaondoa hao tembo.

Mheshimiwa Spika, Serikali iko tayari kushirikiana na vijana wakiwemo kwenye maeneo husika hasa kuanzisha WMA ambazo huwa zinashirikiana na Wizara katika kuhakikisha kwamba zinatunza maeneo husika lakini pia tunashirikiana kudhibiti hawa Wanyama wakali. Hivyo niko tayari kuongozana na Mheshiniwa Nape Nauye kwenye Jimbo lake kuhakikisha kwamba suala hili tunali-solve kwa Pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. JACQUELINE K. ANDREA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, pamoja na jitihada nzuri za Wizara inavyofanya kuzitangaza zao la asali nchini, lakini bado hatujafanya vizuri kwa masoko ya nje ambayo inapelekea wafanyabiashara wengi wa nchini wanashindwa kufanya vizuri kwa masoko ya nje hususan ni Mkoa wa Tabora na tukiangalia kinamama wengi wa Mkoa wa Tabora wamejikita kwenye uvunaji wa asali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, je, Wizara inakuja na mkakati upi kuhakikisha soko la nje la zao la asali linafanya vizuri kama ambavyo zao la asali linafanya vizuri ndani ya nchi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, pamoja na jitihada nzuri zinazofanywa na Wizara ya Maliasili na Utalii katika kuhakikisha zao la asali linaendelea kuwa na thamani, mpaka kupata wafadhili kutoka Umoja wa Ulaya.

Je, Wizara imeweka mikakati ipi na mipango madhubuti ya kutenga pesa kwa ajili ya kuhakikisha mradi huu walioweka kusaidiwa na Umoja wa Ulaya unaweza kuendelea hata kama mradi ule, hata kama wafadhali watachelewesha pesa au hawatoleta pesa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline, Mbunge wa Viti Maalum Tabora kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Tabora Mheshimiwa Jacqueline kwa kuona umuhimu wa zao hili la asali. Ni kweli Tanzania tunafaidika kwa asilimia kubwa kwa soko hili la asali kuuza ndani na nje ya nchi. Mkakakati wa Wizara na Serikali kwa ujumla ni kuhakikisha kwamba asali yetu inakuwa na ubora zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumuhakikishia Mheshimiwa Mbunge ni kwamba kwa sasa hivi wizara inashikirikiana na Umoja wa Ulaya ikiwemo Ujerumani kupeleka sampuli za kemikali za asali ambazo huwa zinachakatwa na kuangalia ubora wa asali ya Tanzania. Na kwa asilimia 90 kwa mwaka wa fedha 2020/2021 tulipeleka asali yetu ya Tanzania na ikaonekana kwa asilimia 90 ni nzuri na inafaa kuuzwa nje ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba Tanzania sasa itaanza kupeleka asali kwenye nchi za Ulaya na Marekani kwa kuwa tumekidhi vigezo vya viwango vya ubora wa asali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwenye mikakati ya kutenga fedha nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwa Wizara ya Maliasili na Utalii kwa sasa tuna mkakati wa kuanzisha viwanda vitano. Viwanda vitatu tayari vimeshajengwa na viwili tunakarabati. Lakini pia hii ni mwanzo wa kuhakikisha kwamba tayari tuna vyanzo vyetu sisi wenyewe bila kutegemea misaada mingine ambavyo vitaweza kukusanya asali yote nchini na itachakatwa kwenye viwanda hivi na kuhakikisha soko la ubora wa asali linapatikana na tunaweza kuuza nje na ndani ya nchi. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali ambayo yametolewa vizuri kwa ufasaha, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; sina tatizo na risiti za MNRT Portal, tatizo langu ni kwa nini mtozaji wa faini asipewe post maalum ili atoe risiti halali badala ya zile za kuandikwa kwa mkono?

Mheshmiwa spika, swali la pili, kwa nini Serikali isitoe mwongozo kwa halmashauri na WMAs zote ili fedha zilipwe kwenye control number maalum benki badala ya kubeba kwenye mabegi na kwenda kulipia porini? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kakunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameongelea ni kwa nini tusitoe risiti za kielektroniki badala ya kutoa risiti za mkono. Kama ambavyo nimejibu kwenye jibu langu la msingi ni kwamba miongozo yote ya sasa tunayofanya ni kwamba Serikali inapokea mapato ya aina yeyote ile kutumia risiti za EFD na kwa upande wa Maliasili na Utalii tunatumia hiyo MNRT Portal ambayo ndio tunayopokelea fedha kwa kutumia control number.

Mheshimiwa Spika, suala analoliongelea Mheshimiwa Mbunge ni kwenye hizi Jumuiya za Hifadhi ya Wanyamapori ambazo zinasimamiwa na Serikali za Mitaa kupitia halmashauri na tunazieleleza sasa halmashauri kwa kuwa fedha zake za jumuiya hizi zinakaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali waangalie sasa utaratibu wa kuhakikisha kwamba malipo yote yanayotokana na faini yapitie kwenye utaratibu wa Serikali yaani EFD.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa mwongozo, mwongozo tulishautoa na utekelezaji wake unaendelea kufanyika isipokuwa usimamizi tu kama ambavyo amesema Mheshimiwa Mbunge kwamba imeonekana kuna wananchi wanabeba fedha kwenye mifuko. Tunatoa maelekezo sasa kwa halmashauri ambazo zinasimamia hizi jumuiya kuhakikisha kwamba usimamizi wa fedha za Serikali unapitia kwenye mifumo ya TEHAMA iliyoainishwa na Serikali, ambayo kwa Maliasili na Utalii tunatumia MNRT Portal ambayo inakusanya kwa kutoa control number na kwa wale wanaotumia EFD, basi Halmashauri zisimamie suala hilo ili fedha hizi sasa ziweze kufika kwenye Mifuko husika na ubadhilifu usiweze kujitokeza. Naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kumekuwa na double standard, mifugo inapoingia hifadhini sio tu wanatozwa fidia na wengine ni fidia kubwa na hata wale wafugaji wamekuwa wakipata mateso, lakini tembo wanapokwenda kuharibu mazao ya wananchi na nyumba za wananchi fidia yake ni kidogo, hususan wananchi wa Serengeti, Wananchi wa Tamau, wananchi wa Nyamatoke, Wananchi wa Kunzugu wote hao wapo kando kando ya Hifadhi ya Mbuga Serengeti. Je, ni lini sasa Serikali itarekebisha fidia ya tembo wanapoharibu mazao au mali za wananchi ili iendane na hali halisi kuliko ilivyo hivi sasa fidia ya Shilingi 100,000/=. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Mbunge wa Viti Maalum Ester Bulaya kwa swali lake zuri.ni kweli kumekuwa na changamoto hii ya kwamba wafugaji wanatozwa fedha kubwa kwa maana ya kiwango ambacho kimewekwa kwenye sheria zetu hizi lakini inapokuja kwa mwananchi inaonekana kwamba Serikali haioni umuhimu.

Mheshimiwa Spika, lakini nimtoe wasi wasi Mheshimiwa Esther kwamba sisi tunachofanya ni kukemea uingizaji wa mifugo kwenye hifadhi na niwaombe wananchi ambao wanaishi kwenye maeneo ya pembezoni mwa hifadhi tembo hawa wanaangalia ni nini ulichopanda kwenye maeneo hayo na tunawahamasisha wananchi wapande pilipili lakini pia waweke mizinga ya nyuki.

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo hawa tembo na Wanyama wengine wana Serikali yao na Serikali yao hii na wenyewe wanajadili kama ambavyo tunajadili sisi hapa. Na ukumbuke maeneo mengi ambayo ni ushoroba wa wanyama sisi wananchi ndiyo tumeenda kuwafata kule hata wao wanatushangaa kwamba kwanini sisi maeneo yetu wananchi wameyasogelea. Ndivyo sasa sisi kama Serikali tunajitahidi angalau kuwa tunawaondoa wale tembo kuwarudisha kwenye maeneo ya hifadhi. Lakini tutambue kwamba wananchi ndiyo tunaowafuata hawa tembo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, lengo la kutoza hiki kiwango ni kuzuia hawa wafugaji sasa kutoingiza mifugo yao kwenye hifadhi, na niombe Waheshimiwa kwenye hili tushirikiane lisionekane kama ni la Wizara ya Maliasili ya Utalii sheria hizi tumezitunga sisi wenyewe na utekelezaji wake basi tutekeleze sisi wenyewe. Wafugaji wanaaswa kutoingiza mifugo yao kwenye maeneo ya hifadhi ahsante.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, ndiyo, ndiyo kabisa!

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na nitumie fursa hii kuiasa Wizara ya Maliasili na Utalii kwamba wanapofanya kila jitihada kuzuia mifugo isiingie ndani ya hifadhi hawafanyi juhudi kuzuia wanyama wasiingie ndani ya maeneo ya jamii.

Mheshimiwa Spika, kwa taarifa hiyo watambue pia kwamba mifugo na wanyamapori wote ni wanyama kuna maeneo ambayo wanaingiliana vizuri kiasi kwamba hata ningependekeza kwamba maeneo ambayo hamna wanyamapori kama misitu asili mifugo waruhusiwe kulisha kwasababu wanatengeneza mazingira ya ekolojia ya majani katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwamba kwa vile kuna hako kafuta jasho au kifuta machozi hawa wanyama wanapoingilia katika maeneo ya jamii.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba hicho kifuta machozi au kifuta jasho kinawahishwa kwasababu kuna tabia ya kuiweka mpaka hata mtu anakuja kupewa ameshasahau na maumivu aliyoyapata?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ni kweli wananchi wanapokutana na adha hii ya tembo kuingia kwenye mashamba yao Wizara ya Maliasili na Utalii ina utamaduni wa kulipa kifuta jasho, na kifuta jasho kinategemea ni aina gani ya uharibifu uliofanyika.

Mheshimiwa Spika, kuna waliopata adha ya kupoteza maisha, lakini kuna wale ambao wamepoteza mazao huwa tunafanya tathmini pale tu ambapo tembo wanakuwa wameingia kwenye maeneo hayo na baada ya kufanya tathmini basi Serikali huwa inachukua jukumu la kulipa kifuta jasho.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka huu wa fedha tumetenga bilioni mbili kwa ajili ya kulipa kifuta jasho. Nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kifuta jasho cha aina yoyote ambacho kinatokana na uvamizi wa tembo Serikali itakilipa ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa katika majibu ya Serikali wanaonesha kabisa kwamba mbadala wa wanyama hawa kutokuingia kwenye maeneo ya wananchi ni kutumia mbinu zilizoainishwa hapa, lakini mbinu hizi zinahitaji wananchi waelimishwe na wawezeshwe kwa sababu unapomwambia afuge nyuki na kadhalika, mwananchi huyu hana huo uwezo. Sasa je, Serikali inafanya nini kuwawezesha wananchi hawa kama kweli wana uhakika hili ndiyo litakuwa suluhisho ya kuondoa kero hii ya muda mrefu ya wanyama kuingia kwenye maeneo ya wananchi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; wananchi wanapoingia kwenye maeneo wakaribu mazao, fidia inayolipwa hailingani na uharibifu uliotokea, lakini hata fidia hiyo inayolipwa inachukua miaka na miaka mwananchi kupata fidia hiyo. Je, ni lini sasa Serikali italeta sheria hapa Bungeni tuifanyie marekebisho ili wananchi waweze kupata haki yao kwa jinsi ambavyo wanastahili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cecilia, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali imekiri kwamba kumekuwa na changamoto ya hawa wanyama wakali wakiwemo tembo kuendelea kuvamia mashamba ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hii tumeendelea kuiongelea hata katika Bunge lako hili Tukufu kwamba kwa kuwa wananchi wameendelea kusogea kwenye maeneo ya hifadhi na asilimia kubwa ya maeneo ambayo shughuli za kilimo zinafanyika ni ushoroba wa wanyama.

Mheshimiwa Naibu Spika, imekuwa ni changamoto kwa sababu wanyama hao sasa badala ya kupita yale maeneo wakaenda kwenye shughuli zao zingine zikiwemo pamoja na kutafuta madini pamoja na dawa asili wanazotumia ambazo sisi wanadamu hatuwezi kuzitambua, lakini wao kama nilivyokuwa nikiendelea kusema, wana Serikali yao, basi yale maeneo sasa wanapokutana na mazao wanafanya vurugu ambayo sio ya kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuendelee kuhamasisha wananchi kama wataweza waachane na mazao yanayohamasisha tembo kupita katika maeneo ya mashamba yao. Kama itashindikana sana basi kwenye jibu langu lile la msingi nimeelezea mbinu mbadala ya kuweza kusaidia ili angalau kuepuka hili tatizo linaloendelea kujitokeza kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaendelea kutoa elimu kwenye maeneo husika na kupitia vyombo vya habari na hata hapa naendelea kutoa rai kwa wananchi kwenye maeneo ambayo mashamba yao yanavamiwa na tembo, wafuate haya tunayoelekeza ili wasaidie. Wapande pilipili, waweke hiyo mizinga ya nyuki, lakini pia waendelee kutoa taarifa kwa Serikali kwa sababu Serikali iko kwa ajili yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kuhusu fidia. Lengo la Serikali si ku-compensate mpaka mwananchi afurahi. Tukisema kila mwananchi apate kile ambacho anakusudia, basi hii Wizara haina haja ya kuwepo kazini kwa sababu uhifadhi ni gharama kubwa sana, lakini pia hata tunapotekeleza tunahakikisha kwamba tunahifadhi ili kuendelea kuiongezea Serikali mapato kupitia utalii, lakini kwa wakati huo huo tunaendelea ku-compensate wananchi wanaoathirika na hao wanyama. Kwa hiyo niombe rai kwa wananchi…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Mbunge, ameelewa.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa fursa hii. Niseme kwamba kutokana na jitihada za wananchi wetu kule Vunjo kupanda miti na kuitunza kwenye mashamba yao ya kahawa na ndizi, ngedere na tumbili wameongezeka sana mpaka wamekuwa tishio kwa maisha ya watoto wachanga wanaoachwa nyumbani na ni vigumu sana kupambana na ngedere na tumbili kwa vile wana akili kama binadamu. Sasa nataka nijue, je Serikali ina suluhisho gani kuhusiana na ongezeko hili kuwaondoa hawa ngedere na tumbili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kimei kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli changamoto hii ipo katika Mkoa wa Kilimanjaro na wiki iliyopita tu tulienda kuangalia changamoto hii katika Wilaya ya Rombo na kukawa kuna changamoto ya nyani pamoja na hao ngedere. Wizara ya Maliasili na Utalii ilitoa tamko kwamba tutaenda kuwahamisha hao nyani pamoja na ngedere, tuwapeleke kwenye maeneo ya hifadhi ambako kutafaa zaidi. Ahsante. (Makofi)
MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kadhia inayowapata wananchi wa Karatu ndiyo hiyo inayowapata wananchi wa Mkoa wa Lindi Wilaya ya Kilwa, Liwale, Lindi Vijijini, Nachingwea. Hata hivi juzi tu Wilaya ya Liwale, Kata ya Mbaya kuna mwananchi kule ameuawa na tembo. Pia wanaharibu mashamba ya vyakula na mazao kiasi kwamba wananchi wanaendelea…

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa.

MHE. TECLA M. UNGELE: Je, Serikali ina mpango gani wa kumaliza tatizo hili la wanyama kule Nachingwea, Liwale na Kilwa ili wananchi wa huko nao wawe na maisha mazuri? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum Lindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimekwishakuelezea kwenye jibu langu la msingi nimetoa rai kwa wananchi kupanda mazao ambayo yanaweza yakaepusha hawa wanyama. Hata hivyo, tukumbuke kwamba tunaishi kwenye maeneo ambayo yalikuwa ni njia za wanyama na tukumbuke kwamba hawa wanyama walikuwepo kabla hata ya sisi kuwepo.

Kwa hiyo, wanyama siku zote wanaenda kwenye maeneo yao ya siku zote ambayo sisi ndiyo tumefanya mashamba. Niwaombe wananchi tena kwamba waendelee kupanda mazao haya ambayo tunahamasisha, lakini ikishindikana basi wasilime kwenye maeneo ambayo yako kandokando ya hifadhi. Ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, dhumuni la eneo kinga (buffer zone) siyo kuzuia wanyama kuingia vijijini. Ni kwa jinsi gani Serikali imejipanga kuangalia usalama wa wananchi kwa sababu tembo hawa wanaingia katikati ya vijiji kule Kilangali, Tindiga, Malolo hata Yogo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ikumbukwe tarehe 15 Januari 2019 Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo kwa Wizara saba kukaa chini na kupitia upya mipaka na kuangalia usalama wa watu katika vijiji vinavyopakana na hifadhi. Hata hivyo, mpaka sasa hatujasikia ni vijiji gani vimeshughulikiwa zaidi ya kuona wananchi wakinyanyasika na pia hakuna alama za kudumu ambazo zimewekwa kwenye eneo la kinga (buffer zone) katika vijiji vinavyopakana na mpaka.

Ni lini Serikali inaenda kuweka alama lakini pia inaenda kuanzisha game ranger post pamoja na kuanzisha vikundi vya kuzuia wanyama waharibifu katika vijiji vyetu? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dennis Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpe pongezi Mheshimiwa Mbunge Dennis Londo kwa kuendelea kutoa rai kwa Serikali jinsi ambavyo wanyamapori hasa waharibifu na wakali wanavyoendelea kuathiri wananchi. Hata hivyo, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi ni kwamba sasa Serikali imejipanga kuandaa mkakati ambao utawawezesha hawa wananchi kutambua ni namna gani ya kukabiliana na wanyamapori hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri tumeshaanza kutoa mafunzo katika Mikoa ya Simiyu, tumeshafanya katika Wilaya ya Busega, Wilaya ya Bariadi na maeneo mengine ambayo yanazunguka mkoa huo, lakini pia awamu inayofuata tutaenda katika Mkoa wa Ruvuma, Morogoro na maeneo mengine hapa nchini. Lengo kuu ni kuhakikisha hawa wanyamapori ambao wamekuwa changamoto kwa Tanzania na kwa nchi kwa ujumla wanadhibitiwa kwa kushirikiana na wananchi ambao wanazunguka maeneo ya hifadhi.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, huu uharibifu unaoletwa na wanyamapori ni mkubwa sana kwa nchi nzima na vifo vinatokea karibu kila siku tunaongea humu ndani. Hivi Serikali haioni inastahili kufanya zaidi ya inavyofanya sasa ili kuokoa maisha ya wananchi wetu? (Makofi)
NAIBU WIZARA WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali inatambua changamoto hii na wananchi kweli wamekuwa wakiathirika vikiwemo vifo ambavyo vinatokea. Hata hivyo, naendelea kusema kwamba changamoto ya wanyamapori wakali imekuwa kubwa na sababu kuu ni kwamba tumevamia maeneo ambayo ni mapito ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na Serikali kuona haya yote, kwa sasa hivi tumejipanga kuandaa hivi vikosi kazi vya maaskari na tutagawa orodha ya watumishi wote ambao wanazunguka maeneo ya hifadhi kuhakikisha kwamba inapotokea athari yoyote au kuonekana kwa mnyama mkali yoyote basi taarifa itolewe kwa haraka ili tuweze kudhibiti hawa wanyama wakali. Kingine ni kuhakikisha kwamba tutakapokuwa tumewafundisha hawa wananchi kujua namna ya kujikinga na hawa wanyama wakali, basi tutakuwa tumeshirikiana kwa pamoja kuhakikisha kwamba maeneo yenye hifadhi yanahifadhiwa vizuri lakini na wananchi wanaendelea kujikinga na hawa wanyama wakali.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwape pole sana wananchi wote ambao wamekuwa wakikutana na hii kadhia na hata Serikali siyo kwamba inapenda kuona wananchi wake wanaendelea kupata shida ya namna hii. Tunajipanga ili kuhakikisha kwamba kadhia inapungua ama kutoweka kabisa kwa sababu hata sisi imekuwa ni changamoto kubwa lakini tunajipanga kwa ajili ya kuhakikisha wananchi wanaishi kwa amani.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Licha ya majibu mazuri ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hawa wanaelewa lakini suala hili limechukua muda mrefu, walikuwa wanatumia maeneo haya kulima na wanajua faida ya Bwawa la Mwalimu Nyerere lakini wanachohitaji ni kupata uelewa na kufahamishwa. Kwa kuwa Mawaziri wameshapitisha na suluhisho limeishafikiwa, je, ni lini Mheshimiwa Waziri atakwenda kuongea na wananchi hawa kusudi waweze kupata suluhisho? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, tatizo hili lipo pia katika Kitongoji cha Dutumi, Kata ya Bwakila Chini, Wilaya ya Morogoro Vijijini ambapo kuna tatizo la Hifadhi ya Selous pamoja na wananchi wa Dutumi hasa wakiwemo wakulima na wafugaji kiasi kwamba kuna kijana mmoja alitobolewa macho, mwingine amejeruhiwa mkono, ni lini Mheshimiwa Waziri atakwenda kuwasikiliza kwa sababu vikao vimekaa lakini hakuna suluhisho? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kabla ya bajeti hii kuisha Juni tutaongozana naye kwenda Kilombero lakini pia Morogoro Vijijini ili kutatua mgogoro huu wa wakulima na wafugaji.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa hawa wanyamapori wamekuwa wakivamia vijiji na kushambulia wananchi hususan Wilaya ya Nyang’wale zaidi ya wananchi 10 wameliwa na fisi. Je, Serikali ina mpango gani wa kwenda kuwatembelea na kuwapa pole lakini pia kuwalipa kifuta machozi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Amar, Mbunge wa Nyang’wale, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kumpa pole sana Mbunge wa Nyang’wale na Wabunge wengine wote ambao wamekumbana na athari hii. Nimhakikishie kwamba hawa fisi ambao wako kwenye maeneo ya Nyang’wale na maeneo mengine yote yanayoathiriwa na wanyama hawa tutaenda kuwahamisha na tutawarudisha hifadhini, kwa sababu Nyang’wale ni eneo ambalo kidogo hifadhi ziko mbali na makazi ya wananchi lakini fisi wanaendelea kwenda kwenye maeneo hayo. Pia tutaongozana naye kwenda kuwaona wananchi hao na tutashirikiana kadri itakavyowezekana.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa masuala haya ya mipaka baina ya makazi ya watu na maliasili yamekuwa ni ya kudumu lakini nchi hii inaongozwa na sheria, Sheria Sura 324 inampa Mkurugenzi wa Upimaji na Ramani mamlaka ya kuhakiki mipaka pale panapotokea mgogoro. Kule kwenye Jimbo la Ukonga upo mgogoro mkubwa baina ya Msitu wa Kazimzumbwi na wananchi wa Kata za Buyuni, Chanika na Zingiziwa. Tayari uhakiki ulifanyika tarehe 24 Februari, 2012 na magazeti yote yalitoa tangazo na lipo linafahamika.

Je, ni lini Waziri atakuwa tayari tuambatane na wataalam wa Wizara ya Ardhi kwenda kuhakiki mpaka huu na kuwaondolea kero ya kupigwa, kubakwa na kuchukuliwa hatua kinyume na sheria wananchi Jimbo la Ukonga?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa Ukonga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mbunge Jerry Silaa kwa kuendelea kuwaonyesha wananchi wake kwamba wamemtuma kwa kazi maalum hapa Bungeni. Nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya bajeti hii tutaongozana naye kwenda kutatua mgogoro huu. Ahsante.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Vijiji vyangu vya Ndaleta, Ngabolo, Olkoponi, Pori kwa Pori, Mbeli, Amei, Namelok wanasumbuliwa sana na tembo na hivi tunavyozungumza tembo wako mashambani. Nini kauli ya Serikali kwa wananchi hawa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Olelekaita, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kutoa pole kwa wananchi wanaozunguka maeneo hayo, lakini Serikali kama ambavyo nilisema mwanzo kwamba tumeanza kutoa mafunzo baada ya kuona athari hii inaendelea kuongezeka. Mafunzo haya yatatolewa nchi nzima namna ya kukabiliana na hawa wanyama wakali. Pia tutatoa vifaa maalum kwa ajili ya kudhibiti hawa wanyama wakali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge tuendelee kushirikiana pale ambapo inatokea watupe taarifa na vikosi kazi ambavyo tumevisambaza nchi nzima vitaendelea kufanya kazi kudhibiti hawa wanyama wakali.
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na kwamba sijaridhika na majibu ya Naibu Waziri, nina maswali madogo mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mauaji yamekuwa yakitokea mara kwa mara katika Hifadhi ya Lake Manyara; imetokea mwaka 2005, ikatokea mwaka 2015 na ikatokea tarehe 28/10/2020 ng’ombe wapatao zaidi ya 10 walipigwa risasi wakikutwa kijijini wakidai kwamba wamefuata nyayo. Askari wa Game Reserve wakaenda mpaka nyumba ya mtu huko kijijini na ng’ombe kumi kupigwa risasi.

Vilevile tarehe 28 mwezi wa Novemba, walipigwa risasi watu wanne kule msituni na kuchomwa moto. Nami ni shahidi, nikaenda msituni kule kuwatafuta wananchi hawa na kupata mabaki na mabaki yale yakapelekwa kwa Mkemia Mkuu wa Serikali:-

Je, ni lini wananchi wale watapata majibu ya Mkemia Mkuu wa Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kwa kuwa, Hifadhi ile ya Lake Manyara ikihamishwa mipaka mara kwa mara kila mwaka kutoka Hifadhi ya Lake Manyara:-

Je, Waziri yuko tayari kufuatana nami kwenda kujionea mpaka jinsi unavyohamishwa katika Lake Manyara National Park?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza niendelee kutoa pole kwa wananchi wa Karatu kwa kadhia hii ambayo waliipata. Niwakumbushe tu kwamba, wananchi kwa asilimia kubwa wanatumia nguvu ikiwemo kutotii sheria za uhifadhi na hivyo kusababisha hawa Askari sasa kujichukulia sheria ambazo kimsingi wananchi wangetii kusingetokea vurugu yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tuendelee kushirikiana kuelimisha hawa wananchi. Hili suala la tarehe 28/11/2020 naomba tu waendelee kuwa subira kwa sababu ni taarifa za kiuchunguzi na Askari tayari walishachukua sample na wakapeleka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali. Hivyo, majibu yatatolewa na Jeshi la Polisi baada ya kufanyika uchunguzi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili. Niko tayari kuongozana naye kwenda kuangalia maeneo haya na kuonesha mipaka halisi kama ambavyo ameomba. Ahsante.
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji wa Bunda ina Kata 14 na wakulima wake mazao yao yameathirika sana na wanyamapori, hasa tembo; Kata ya Nyatwali, Bunda Store, Mcharo na Sazila:-

Je, ni lini Waziri atatembelea Halmashauri hii ili aweze kujionea uharibifu huo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nianze kwanza kwa kuwapongeza Wabunge wote ambao wanazungukwa maeneo ya uhifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna sheria ambayo tulishapitisha kwamba wananchi wanapokutana na kadhia hii ya tembo na wanyama wengine tunatoa kifuta machozi. Nampongeza Mheshimiwa Robert Chacha kwamba ameendelea kulizungumzia suala hili la wananchi wake kuhakikisha wanapata kifuta machozi, lakini pia nimwahidi kwamba, nitafika kwenye eneo hilo ili tuweze kuzungumza na wananchi. Ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ubarikiwe sana. Kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Sita inawajali sana wananchi wake wakiwemo wale wanaoishi kwenye Vijiji vya Kata ya Kirua Vunjo, Kilema, Marangu, Mamba na Mwika na wanaoishi kwenye vijiji vinavyozunguka msitu wa Mlima Kilimanjaro:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kutathmini upya msimamo wake na kuwaruhusu wanavijiji hawa kutumia eneo la nusu maili ambalo limeainishwa kwenye mipaka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nitoe rai tu kwa Mheshimiwa Mbunge kwamba maeneo ambayo tayari yanakuwa yameshatangazwa kuwa Hifadhi ya Taifa haturuhusiwi kufanya kitu chochote. Isipokuwa kama ana maombi ambayo anahitaji ifanyike tathmini, basi naomba kupitia Serikali ya Wilaya na Vijiji walete maombi kwenye Wizara, halafu tutaangalia tathmini kama itawezekana; na pale ambapo haiwezekani pia, tutawapa majibu. Ahsante. (Makofi)
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, kwanza naanza kumshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri kwa kuitangaza hifadhi yetu ya Taifa ya Katavi lakini nina maswali mawili ya nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Swali la kwanza ilikuwa ni ahadi ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, mwaka 2019 ya kujenga hoteli ya Kitalii katika Mkoa wa Katavi katika Kata ya Magamba, ili hoteli hiyo iweze kuwavutia zaidi watalii kwa kupata malazi yaliyo bora na malazi yanayoridhisha. Je, huo mpango wa kujenga Hoteli ya kitalii katika Kata ya Magamba ambapo tulishatenga eneo umefikia wapi Ukizingatia hoteli hii itakwenda kuibua fursa nyingi kwa vijana wanaozunguka katika Mkoa wa Katavi kuweza kuapta ajira? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili vijiji vinavyozunguka hifadhi ya Taifa ya Katavi vikiwepo vijiji vya Mwamapuri, Chamalindi, Ikuba, Starike, Mangimoto, na Kibaoni vijiji hivi kwa muda mrefu vimekuwa havinufaiki na ujirani mwema kwa kupata miradi ya maendeleo kupitia TANAPA. Je, Serikali inatoa tamko gani ili vijiji hivi viweze kunufaika na hifadhi hiyo ukizingatia vijiji hivyo ndivyo vinavyotunza hifadhi hiyo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Martha Maliki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la hoteli ya kitalii kujengwa katika hifadhi ya Katavi ni kweli Hayati Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, aliahidi katika ziara zake kwamba kujengwe hoteli ya kitalii katika hifadhi ya Taifa ya Katavi. Mpango huo umeshapangwa na kwenye mpango wa bajeti wa mwaka 2021/2022 mpango huu tumeuweka na hoteli hii ya kitaifa itaanza kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu ujirani mwema, ujirani mwema ni kweli Serikali imekuwa ikisaidia vijiji vyote vinavyozunguka maeneo ya hifadhi ikiwemo hifadhi ya Taifa ya Katavi lakini kwa mwaka wa fedha 2021 tulikuwa na changamoto ya Korona hivyo tulishindwa kuhudumia haya maeneo ya hifadhi kama ambavyo Serikali imekuwa ikipanga. Lakini nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili sasa tunaenda kulitekeleza katika mpango wa fedha wa mwaka 2021/2022 vijiji vyote vinavyozunguka hifadhi za Taifa, ujirani mwema utaenda kutekelezwa kwa kiwango cha juu, ahsante, (Makofi)
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana Mheshimiwa Rais alipokuja Mkoa wa Katavi aliagiza Wizara ya Maliasili na Wizara ya Ardhi kumaliza tatizo la migogoro ya ardhi kati ya mapori ya akiba na hifadhi ya Taifa ya Katavi. Lakini utekelezaji mpaka sasa bado haujafanyika ni lini Mheshimiwa Waziri atakuja Mkoa wa Katavi ili asimamie zoezi hili?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge wa Katavi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya Bunge hili Tukufu tutaongozana naye kwenda kutatua taizo hili kwa hiyo nimuondoe wasiwasi tutaondoka naye, ahsante. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Hali ya madhara yanayotokana na wanyamapori yamekuwa ni makubwa sana. Leo hii kwenye Vijiji vya Ngumbu, Kibutuka, Kiangala na Ngatapa, wananchi wameshahama wamerudi majumbani kwao kutoka mashambani, baada ya tembo kumaliza mazao yote. Sasa naomba Serikali ituambie, je, ina mkakati gani wa kuhakikisha usumbufu huu wa wanyamapori unapungua hasa kwenye hivi vijiji vichache nilivyovitaja? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuwapa pole wananchi wa Liwale, lakini pia niendelee kutoa pole kwa wananchi wengine wote wanaozunguka maeneo ya hifadhi, zikiwemo Hifadhi ambazo nimezitembelea jana za Mwanga na Same.

Mheshimiwa Spika, changamoto hii inasababishwa na wananchi kusogelea maeneo ya hifadhi, hasa maeneo yenye ushoroba, njia za wanyama pori hususani tembo, wanatembea kwa speed ndefu na wanatembea katika maeneo marefu na shoroba hizi zimezibwa na wananchi ambao wanafanya shughuli za kilimo lakini wengine wamejenga kwenye maeneo ambayo ni mapito ya wanyama.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaweka mkakati wa kufanya mafunzo kwa wananchi ya namna ya kudhibiti hawa tembo, lakini pia tunagawa vifaa, lakini pamoja na hilo tumeimarisha dolia za askari, kuhakikisha kwamba hawa wanyama wanapoingia kwenye maeneo ya wananchi basi askari wa doria wanakuwepo kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, nimtoe wasiwasi Mbunge kwamba suala hili Serikali inalitambua na tunaendelea kufanya kazi na hatulali mchana na usiku tunahakikisha wananchi waishi kwa amani. Ahsante.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na jitihada ambazo zinafanywa na Serikali, Wizara imekuwa ikisema kwamba upandaji wa pilipili kwenye maeneo ambayo yanakaribiana na vijiji una uwezo wa kuzuia tembo kuingia vijijini. Sasa, je Serikali hiko tayari kupitia TANAPA na taasisi zake wakapanda wao hizi pilipili ili wawasaidie wananchi wetu wasihangaike, mazao yao yasiliwe na wao wasiuliwe?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nape, Mbunge wa Mtama, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulishabuni mbinu mbadala za kuhakikisha kwamba hawa wanyama wakali wanapunguza kasi ya kuathiri wananchi ikiwemo pilipili lakini pia kuna mizinga ya nyuki ambao ni njia bora zaidi ya kuwafanya hawa wanyama wasiweze kusogelea makazi ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, tunalipokea wazo lake, lakini kulingana na gharama Serikali itaendelea kuangalia tathmini na tunaweza tukafanya kwa awamu, kwenye maeneo ambayo yameathirika Zaidi. Hata hivyo, niwaombe tu Waheshimiwa tuendelee kushirikiana kwenye hizi mbinu ambazo tunaendelea kuzielekeza wakati Serikali sasa inaangalia mbinu ya kudumu ambayo inaweza ikasaidia wanyama hawa kuishi katika maeneo yao na wananchi wakaishi kwa amani.
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri na juhudi za Wizara ambazo tunaziona, lakini kwa kuwa mipaka ya hifadhi hii iliwekwa mwaka 1954 na idadi ya watu imezidi kuongezeka kiasi kwamba sasa hivi Makao Makuu ya Mji Mdogo wa Same yapo kilometa nne tu kutoka kwenye mpaka wa hifadhi.

Je, Serikali haioni kwamba suala la eneo hili la Same Magharibi lichukuliwe kama special case ili kuwapa watu nafasi ya kuweza kufanya kazi zao kwa sababu mpaka upo karibu sana na Makao Makuu ya Mji Mdogo wa Same? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Malisisli na Utalii naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tadayo, Mbunge wa Mwanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, ni kwamba Same ipo kilometa sita kutoka maeneo ya makazi ambayo wanaishi wananchi mpaka kwenye eneo la hifadhi. Kama ambavyo nimeelezea kwamba sasa hivi tuna changamoto ya tembo na hawa tembo wanarudi kwenye maeneo yao ya zamani, kwa hiyo, kuendelea kumega hili eneo ni kuendelea sasa kuongeza migogoro kati ya wananchi na wanyama.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati Serikali inaangalia utaratibu mwingine basi wananchi waendelee kuishi kwenye maeneo hayo kuliko kuendelea kuwasogeza kwenye hatari zaidi kuliko ilivyo sasa, ahsante.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, kwa kweli wakazi wengi wa Same ambao wanaishi karibu na Mkomazi National Park wapo kwenye risk kubwa ya kupata matatizo na kupoteza maisha yao. Kwa sababu Mheshimiwa Waziri tulikuwa naye Jumamosi na Jumapili kule Same na ameona hali ilivyo, haoni kwamba ni vyema zile sehemu zote ambazo zina risk kubwa kukawepo askari ambao wanakuwepo kuwafukuza wale tembo kuliko kuacha hali ilivyo mpaka sasa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anne Kilango, Mbunge wa Same Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulienda ziara na Mheshimiwa Anne Kilango, changamoto ya tembo ipo, ni kweli na ni kubwa, lakini tulitoa maelekezo na naomba hili niendelee kuelekeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwamba tutaweka kambi ambazo zitakuwa ni za doria kwa ajili ya kuhakikisha wananchi wanaishi kwa usalama.

Mheshimiwa Spika, na hili nikuahidi kwamba maeneo yote ambayo yana risk kubwa ya tembo, tutahakikisha kwamba askari wanaishi maeneo yale ili changamoto hii hasa kipindi hiki cha mavuno tuweze kuidhibiti na wananchi waishi kwa amani, ahsante. (Makofi)
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushuru na ninaishukuru Serikali kwa kuleta shilingi milioni 51 kwa ajili ya kulipa fidia na kifuta machozi.

Je, ni lini Serikali italeta muswada Bungeni wa kuongeza viwango vya kifuta machozi pamoja na fidia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na watumishi wa Idara ya Wanyamapori Halmashauri ya Wilaya ya Meatu ambao ni wawili tu wameelemewa kutokana na upungufu wa vitendea kazi.

Je, Serikali haioni kwa kipindi hiki cha miezi miwili watumishi wa TAWA wakawepo doria wakati wa usiku ili kusaidiana na wananchi wanaokesha ili wananchi waweze kuvuna mazao yao katika kipindi hiki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Uatlii naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Leah Komanya, Mbunge wa Meatu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nianze na hili la pili; ninaomba nimuahidi Mbunge na Wabunge wengine wote ambao wana changamoto ya tembo kwamba kipindi hiki ambacho ni cha mavuno, askari watasimamia zoezi mpaka pale ambapo wananchi watatoa mazao yao na hili litaanza kuanzia sasa. Nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge hili tutalitekeleza sisi kama Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili la kwanza ambalo alisema kuleta muswada wa kuongeza kifuta machozi na kifuta jasho kwa wale ambao wameathirika na wanyama wakali hususan tembo; nimelipokea lakini wakati huo huo Serikali inaendelea kuangalia tathmini ya namna ya kufanya, lakini wakati huo huo tunaangalia nchi zingine wamefanyaje.

Mheshimiwa Spika, suala hili kwenye nchi za wenzetu/ majirani zetu ambao wana changamoto kama hii, wao liliwashinda wakaamua kuachana na mambo ya kifuta machozi kwa sababu kadri changamoto inavyozidi kuongezeka, ndivyo gharama zinavyozidi kuongezeka. Serikali ya Tanzania kwa kuwathamini wananchi wake iliona bora iweke hili eneo ili angalau wananchi waweze kufaidika. Kwa hiyo, tunalipokea lakini tutaenda kulichakata na tuone faida na hasara kwa pande zote mbili, ahsante. (Makofi)
MHE.CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona na kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli kwamba idadi ya watu nchini inaongezeka, lakini ardhi tuliyonayo haiongezeki na yapo mapori kama hayo na mengine ambayo kwa namna moja ama nyingine hayana tija kwa Taifa.

Je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa kufanyia tathmini mapori mengine kuyagawa kwa wananchi ili waweze kuyatumia?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Maliaisli na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inapokea mawazo hayo na hata sasa kwa sababu kuna changamoto na migogoro mingi kati ya wananchi na maeneo ya hifadhi, Serikali inaendelea kufanya tathmini na yale maeneo ambayo yanaonekana sio ya faida sana, Serikali itaangalia na italeta mapendekezo kwenye Baraza la Mawaziri na mwisho Mheshimiwa Rais atatoa maelekezo, ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali.

Mheshimiwa Spika, haya mambo ya wanyamapori mimi naona kwamba sasa tunapokwenda tutabakiza nchi ya wanyamapori. (KIcheko)

Sasa mimi najiuliza hivi ni tembo wangapi wanatosha kuishi katika mapori ya Tanzania ambayo watalii watakuja kuona, kwa sababu kama tembo hawa hawana uzazi wa mpango maana yake sasa tuwaruhusu waishi kwa wananchi, ni tembo wangapi wanatosha ili watalii waone kwamba hawa tembo wametosha tunakwenda kuwaona. Maana yake tunapoamini tembo wakiwa wachache ndio watalii watawatafuta, sasa wakiwa wengi … kwenye utalii gani?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba nimpe tathmini ya idadi ya tembo mpaka sasa; mwaka 2009 kulikuwa na idadi ya tembo 134,000 lakini kabla ya hapo walikuwa wanafika tembo 300 na kadhalika, lakini walishuka mpaka kufikia 134,000. Toka mwaka 2009 mpaka 2014 ambapo kulikuwa na poaching kubwa, tembo walishuka mpaka wakafika 43,000. Kutoka mwaka 2014 mpaka 2020 wanakadiriwa sasa
wameongezeka kufika 60,000.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utaangalia hata ile idadi ya mwaka 2009 bado hatujaifikia; kinachotokea hapa ni kwamba tembo anahamasika hasa kipindi cha mavuno, anaweka kambi kwenye maeneo ambayo ni shoroba zao na anapoweka ile kambi basi wanahamasika kula mazao ambayo pengine huyu tembo toka azaliwe hajawahi kukutana na hindi, muhogo anahamasika ndiyo maana sasa changamoto sasa hivi imekuwa ni kubwa kwa sababu ni kipindi hiki hasa cha mavuno, ahsante.
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, wakati tunasubiri hatma ya mgogoro wa bonde hilo na mipaka hiyo kutoka kwa Kamati ya Mawaziri Wanane maisha yaliendelea na wananchi wa kule tulilima na sasa mpunga uko tayari kwa ajili ya kuvunwa. Je, Wizara haioni haja ya kutoa ushirikiano na wananchi tuweze kuvuna mpunga huo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Antipas, Mbunge wa Malinyi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli bonde hili kuna baadhi ya wananchi walikuwa wamevamia kwa ajili ya kilimo na sasa hivi ni kipindi cha mavuno. Kama alivyoomba Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inaweza ikawaruhusu na sisi kwa sababu, yale ni mazao na ili kuepuka njaa kwa wananchi wetu. Na kwa kuwa Serikali hii inawathamini wananchi, tutatoa vibali maalum ambavyo vitawasaidia kwenda kwenye maeneo hayo wavune kwa utaratibu ambao utasimamiwa na Serikali.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Liwale inazungukwa na Pori la Selous, lakini sasahivi mkakati wa Serikali ni kuimarisha utalii wa picha badala ya utalii wa uwindaji na sisi kwenye Kanda ya Kusini kuanzia ukanda wa Kilwa mpaka Tunduru hakuna lango la utalii wa picha.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kutuwekea sisi lango la utalii wa picha na sisi tuweze kunufaika na uwepo wa Selous?

SPIKA: Mheshimiwa kule Liwale unadhani lango lingeweza kukaa wapi kwa mfano?

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, palepale Liwale Mjini ndio panafaa kwa sababu, Kambi ya Selou iko palepale Liwale.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Kuchauka kwa maswali yake mazuri, lakini pia kwa kutambua wananchi wanaoishi Liwale. nimuahidi tu kwamba, mageti yanayohusiana na hii hifadhi yatafunguliwa kwa mwaka wa fedha 2021/2022 na mageti mengine yote.

Mheshimiwa Spika, hili naliongea kwa kujiamini kwa sababu, wiki iliyopita tu nilikuwa katika Mkoa wa Kilimanjaro, Same pamoja na Mwanga, pia kuna maombi hayo ya kufungua mageti mbalimbali kwenye Hifadhi ya Mkomazi. Kwa hiyo, niwaombe Waheshimiwa Wabunge kwenye maeneo yale ambayo yanahitaji kufunguliwa mageti ya ziada, ili kurahisisha watalii mbalimbali waweze kuingia na kurahisisha namna ya kuingia kwenye hifadhi, tutayafungua na bajeti hii itakayoanza keshokutwa imezingatia kufunguliwa kwa mageti hayo. Naomba kuwasilisha.
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Serikali nina maswali mawili ya nyogeza.

Mheshimiwa Spika, kutokana na kwamba mipaka ya Hifadhi hii ya Kitulo ilikosewa kwa sababu walikuwa wanatumia vijana ambao walikuwa wakibeba zile zege au beacon na kwa kuwa zilikuwa ni nzito sana walikuwa wanatua mahala ambapo siyo mipaka. Maana wanapotua ndiyo hapo hapo wanafanya mpaka na kusababisha baadhi ya taasisi kama shule mbili pamoja na jamii/familia/kaya kuwa ndani ya hifadhi. Je Serikali iko tayari sasa kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi kwenda kurekebisha mipaka hii ili iwe na uhalisia ama original yake ilivyokuwa inatakiwa iwe? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Hifadhi ya Kitulo inajulikana kama bustani ya Mungu kwa sababu ina maua ambayo yanachua na ni hifadhi pekee kwa Afrika ambayo ina maua mazuri sana na kwa bahati mbaya sana haijatangazwa ipasavyo. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba Hifadhi hii ya Kitulo inatangazwa ili ijulikane kama zilivyo hifadhi nyingine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Atupele Mwakibete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu mipaka kwamba ilikosewa, nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaongozana na yeye pamoja na watalaam wa Wizara ya Maliasili na Utalii lakini pia nitaomba wataalam wanaotoka katika Wizara ya Ardhi ili twende kuangalia. Pale ambapo itathibitika kwamba mipaka hii ilikosewa basi tutaweza kuirekebisha.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala hili linalohusiana na utalii, nimhakikishie tu Mbunge kwamba bajeti ya mwaka 2021/2022 imezingatia maeneo muhimu likiwemo eneo hili la Hifadhi ya Kitulo kuitangaza kwa nguvu zote na ukizingatia kwamba hifadhi hii ni ya kipekee hapa nchini. Kwa hiyo, nimhakikishie tu kwamba hifadhi hii itatangazwa kwa nguvu zote ili watalii waweze kufika katika hifadhi hiyo.

NAIBU WAZIRI WA ARDHI: Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii. Kutokana na changamoto zinazojitokeza katika tafsiri hasa ya mipaka kwenye maeneo ya wananchi pamoja na hifadhi, Wizara ya Ardhi kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii tutaweka utaratibu ambao tunakwenda kupitia mpaka mmoja baada ya mwingine ikiwemo hata ile ya Kazimzumbwe ambayo imekuwa na shida nyingi. Kwa hiyo, tutaifanya kazi hiyo tukishirikisha na wananchi wa maeneo husika ili tuweze kupata tafsiri sahihi tujue ni kweli mipaka imehama au namna gani kwa sababu kumekuwa na kelele nyingi kuhusiana na maeneo ya hifadhi na wananchi. (Makofi)
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, na nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni kwamba, kwa vile imeshathibitika kwamba jambo hili halina madhara yoyote kimazingira na kwenye idadi ya vipepeo, na kwamba kwanza ukiachilia mbali kuongeza vipato vya wananchi lilikuwa linasaidia kwenye idadi ya vipepeo kwa vile kwa kawaida kipepeo anayetaga mayai mpaka 500 kwa njia zake za kwaida huweza kuzalisha vipepeo wawili, lakini kwa njia hii ya msaada wa wananchi huweza kuzalisha mpaka vipepeo 300.

Je, Serikali haioni kwamba, ilishauriwa tu vibaya kwenye suala hili kwa kutotenganisha kati ya wanyama wakubwa kama chui, twiga na swala na hawa vipepeo wetu na kwamba inatakiwa kurudi nyuma na kutenganisha sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwa vile ni nchi chache sana duniani ambazo zinaweza kuzalisha vipepeo kama sisi, na ni biashara na utalii mkubwa duniani; Serikali haioni haja sasa ya kuwekeza kwenye kuanzisha utalii wa vipepeo, ili kuongeza vivutio vya utalii nchini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hamis Mwin’juma, Maarufu kama “Mwana FA”, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Hamis Mwin’juma, lakini pia nimpongeze sana kwa kuendelea kusimamia eneo hili la wanyamapori hai, lakini nimpongeze pia kwa kuendelea kupigania wananchi wa Muheza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo ameshauri Mheshimiwa Mwinjuma, kwamba Serikali inawezekana ilishauriwa vibaya. Nimtoe wasiwsi kwamba Serikali iko makini na Serikali iko kazini na ina wataalamu wa kutosha. Suala hili limekuwa likichunguzwa na wataalamu mbalimbali. Muhimu ni kuangalia kipi faida na hasara ambayo inaweza ikapata Serikali. Tunapoendelea kuhamisha wanyama mbalimbali kutoka ndani ya nchi kupeleka nje ya nchi ina maana tunazidi kuuwa utalii wa hapa Tanzania. Hata hivyo nimtoe wasiwasi, kwamba suala hili tunaendelea kulifanyia tathmini, tutachakata kuangalia faida na hasara ya eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimpongeze pia, kwa kuendelea kuhamasisha utalii kupitia vipepeo ambavyo amevitamka yeye mwenyewe. Kwa hiyo, kama kweli tutaanzisha utalii wa vipepeo haina haja sasa hata kuendelea kuvitoa hivi vipepeo viende nje ya nchi kwa sababu tunapoendelea kuvitoa tunauwa soko la utalii wa ndani.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa
Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Naomba niulize swali.

Je, Serikali ina mpango gani wa kutumia wazawa katika kukuza utalii wetu hasa cultural tourism? Kwa mfano kutumia wazee wa kimila kama wazee wa kihehe ambao walianza kutunza Mbuga ya Ruaha wakati wa Chief Mkwawa na kutumia wazee wengine kama Wamasai, ili kuhakikisha kwamba utalii wetu unakua, kwa kuwa wao wenyewe wanakuwa tayari ni kivutio?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jesca, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli sasa hivi Serikali ina mpango wa kutumia watu maarufu, wazee wa kimila kama ambavyo amewaainisha Mheshimiwa Mbunge na watu maarufu wakiwemo wasanii ambao tutawatumia kama mabalozi wa hiyari. Kwa hiyo nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, suala hili Serikali inalishughulikia; na tulishukuru sana Bunge hili limetupitishia bajeti nzuri ambayo sasa mwaka wa fedha 2021/22 tunaenda kutekeleza maeneo yote haya. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Naipongeza Serikali kwa majibu mazuri sana ambayo wameyatoa hapa mbele ya Bunge, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza; miti hii inapatikana kwenye maeneo yaliyohifadhiwa na maeneo ambayo hayajahifadhiwa, yakiwemo mashamba ya watu binafsi na ardhi ambayo inamilikiwa na watu binafsi. Sasa swali langu; kwa nini Serikali isitoe ruhusa maalum itakayosimamiwa na Serikali za vijiji kwenye maeneo hayo ambayo hayajahifadhiwa ili watu waruhusiwe kuvuna miti wanayoimiliki kihalali kwa ajili ya matumizi ya ujenzi wa nyumba za asili pamoja na nyumba za kisasa bila kwanza kupata vibali vile vya maliasili kwa sababu maeneo hayo hayahusiani na maliasili? Kwa sababu matumizi yale siyo ya kibiashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili; kuhusu uvunaji wa miti kwenye maeneo yaliyohifadhiwa; kwa nini Serikali isitoe elimu kwanza kupitia mikutano ya hadhara na njia nyingine za mawasiliano ili wananchi wapate ufahamu wa kutosha wa namna ya kuomba vibali ili wasiingie migogoro mara kwa mara ya kuvunja sheria za nchi? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, kwamba Serikali ipo kwa ngazi zote. Kuhusu swali lake linalosema kwa nini Serikali isitoe ruhusa kwenye maeneo yasiyohifadhiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yote ambayo yana rasilimali za misitu yanahifadhiwa na Serikali ikiwemo Wizara ya Maliasili na Utalii, lakini kwenye ngazi za vijiji na maeneo ya wilaya, zinahifadhiwa na Serikali za Mitaa, zikiwemo halmashauri za wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maeneo haya ambayo vibali vyake vinatolewa na Maliasili ni yale maeneo ambayo yanahifadhiwa na Wizara. Hata hivyo, kuna yale ambayo yanahifadhiwa na Serikali za Mitaa, vibali vyote huwa vinatolewa kwenye level ya vijiji na wilaya. Kwa hiyo wale wote ambao wanahitaji kupata vibali basi wawe wanakwenda kwenye maeneo hayo na pia watapata hivyo vibali.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwakumbushe tu kwamba maeneo yote yanahifadhiwa, siyo kwa ajili ya kutunzwa peke yake, lakini pia na uhifadhi wa mazingira pamoja na utunzaji wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili, ameuliza kuhusu elimu; ni kweli kwamba Serikali imeendelea kutoa elimu mbalimbali kwa wananchi ili watambue umuhimu wa utunzaji wa miti. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mpango wa bajeti na fedha zilizoidhinishwa kipindi hiki tumeweka eneo la elimu ambalo tutapita kila maeneo ambayo yanazunguka hifadhi kuhakikisha kwamba wananchi wanapata elimu ya kutosha na namna ya kuomba hivi vibali vya ukataji miti. Ahsante.
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Wananchi wangu wa Jimbo la Bunda Mjini, Alhamisi ya wiki iliyopita tembo wamekula mazao yao, hasa Kata za Bunda Stoo, Balili na Kunzugu. Wapo baadhi ambao wamefanyiwa tathmini ya mazao yao, je, ni lini Serikali itawalipa fidia yao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Robert Maboto, Mbunge wa Bunda Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeshaanza kulipa malipo haya ya kifuta jasho na kifuta machozi na kulikuwa kuna malipo ya kipindi cha nyuma ambayo walikuwa wanadai na niliahidi hata kwa Mbunge mwenzie Mheshimiwa Esther Bulaya, kwamba nitafunga safari niende kwenye maeneo husika tukaangalie ni madai gani ambayo wanadai kisha Serikali iweze kuyalipa. Ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Kwanza nisikitike kwa majibu yasiyoridhisha au niseme labda ya sitaki kutumia kauli kama ya uongo dhidi ya matukio haya ambayo yametolewa na Serikali, na imekuwa ni rahisi sana askari wa TANAPA kujichukulia sheria mkononi kuliko majeshi mengine yoyote, na hii inafanyika maeneo mbalimbali nchini.

Sasa swali langu la kwanza; tarehe 29 Desemba, 2020 wananchi saba waliingia hifadhilini ikisadikika wanakwenda kuchimba madini, wananchi wanne mpaka leo hawajulikani walipo na inasemekana wamechomwa moto hadi kufa na askari wa TANAPA.

Je, hao nao waliamua wenyewe kujichoma au askari wa TANAPA waliwachoma wananchi hao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; tarehe 22 Oktoba, 2020 siku ya kupiga kura askari wa TANAPA waliwapiga risasi ng’ombe kumi wa mama mjane kwenye eneo hili mpaka leo mama huyu hajafidiwa wale ng’ombe sasa hawa ng’ombe nao walijipiga risasi wenyewe au askari wa TANAPA waliwapiga risasi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba maelezo yote niliyosema hapa ni kweli na akihitaji ushahidi tutautoa kama Serikali. Askari wetu ni wengi sana wanauawa na tumekuwa tukishambulia zaidi askari, lakini haya matukio yanatokea pande zote mbili kwamba askari wanakuwa kwenye sheria na kukabiliana na maeneo yao ya hifadhi kwa maana ya kuyalinda yale maeneo lakini inapotokea sasa wananchi kutotii sheria basi huu mtafaruku unatokea.

Mheshimiwas Spika, lakini kwenye hili analoliongelea kwamba waliingia na kuchomwa moto, mimi hilo siwezi kuliongelea hapa kwa sababu taarifa zake tulishawahi kuziongelea hapa kwamba ziko kwenye uchunguzi na DNA ilishapelekwa kwenye maeneo yetu ya uchunguzi na taarifa hizi ni za kiusalama zaidi, kwa hiyo, tamko la Serikal litakuja kutolewa baada ya uchunguzi kufanyika.

Mheshimiwa Spika, na hili la risasi kwamba kuna ng’ombe walipigwa risasi pengine labda nimuombe Mheshimiwa atuletee uthibitisho kwamba wakati ng’ombe hawa wanauawa kama alikuwepo basi tuweze kulishughulikia, lakini vinginevyo ninaomba sana na nimuombe kama anavithibitisho vyovyote ambavyo askari walienda kupiga hao ng’ombe atuletee na Serikali itachukua hatua, ahsante. (Makofi)
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; swali langu linahusiana na suala la maaskari.

Mheshimiwa Spika, nini kauli ya Serikali juu ya kutuletea kituo katika Tarafa ya Milola, sababu ya msingi ni kwamba ndani ya tarafa ile kila usiku uchao, kila asubuhi kuna taarifa ambayo ninaipata juu ya wanyama hasa tembo kuja kuzunguka katika maeneo yale ambayo watu wanaishi na matokeo yake watu wanapoteza maisha yao na nilishasema watu wamepoteza maisha, mazao yanaharibika kila siku na tunaambiwa tulime, sasa hata kama watu watalima nini matokeo yake.

Naiomba Serikali inipe tamko au inihakikishie juu ya kuleta kituo katika eneo letu lile ili askari wale waweze kushughulika na wale wanyama, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Mama Salma ni askari anakuwa wa Halmashauri au unataka wa Wizara?

MHE. SALMA R. KIKWETE: Ikiwa wa Halmashauri sawa, ikiwa ni wa Wizara sawa, lengo ni kuhakikisha kwamba askari wanakuwepo na maisha ya wananchi yanakuwa salama. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na utalii naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, niwape pole kwanza wananchi wa eneo lile kwa kuendelea kuvamiwa na tembo, lakini Serikali itapeleka askari pale ambao wataenda kulinda ili kupunguza kadhia hii ya wanyama wakali na waharibifu kama tembo.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Mkalama ni wilaya mpya na ina mapato madogo sana. Naomba tu niseme Wizara itakuwa tayari kulipokea boma hili kama sisi Halmashauri ya Mkalama tutaamua kuwakabidhi ili walikarabati liweze kuleta manufaa kwa nchi na kwa jamii ya Mkalama; swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Naibu Waziri atakuwa tayari baada ya Bunge twende naye mpaka Mkalama ili akaone hali halisi ya boma hili na aone umuhimu wake ili aharakishe mchakato wa kulichukua kama tutawakabidhi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Mtinga, Mbunge wa Iramba Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Francis Mtinga, amekuwa ni mfuatiliaji sana kwenye eneo hili la kuboresha malikale likiwemo hili boma la historia lililoko katika Wilaya ya Mkalama. Nimpongeze sana na pia niwapongeze wananchi wa Mkalama Iramba Mashariki kwa kuwa na Mbunge mahiri anayefuatilia maeneo haya ya kihistoria ambayo ni mojawapo ya chanzo cha mapato katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa haya maeneo ni maeneo muhimu kwa ajili ya kuhamasisha utalii lakini pia kuongeza mapato katika sekta zetu hizi, nimuahidi kwamba tutaenda kulitembelea lakini pia kama Halmashauri itashindwa kulikarabati boma hili basi Wizara iko tayari kulipokea na kulikarabati na liwe eneo mojawapo ya chanzo cha mapato katika Serikali, ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, ahsante; Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ni mtu ambaye anaheshimika Tanzania na duniani kote na kwa kufanya hivyo kule Butiama ni sehemu ambayo amezaliwa lakini pia ni sehemu ambayo amezikwa.

Je, ni kwa nini sasa Serikali haioni umuhimu wa kuboresha maeneo yale ya Hayati ili pawe ni historical site ambapo ataelezea kila kitu ili tuweze kupata watalii wengi na kuongeza mapato kama vile ilivyo kwa mwenzetu Hayati Mandela wa Afrika Kusini ambapo watu wengi wanakwenda wanamimika kuweza kujifunza zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali ina maeneo mengi ya kihistoria, lakini tuna eneo muhimu la kumbukumbu ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere lililoko kule Butiama. Serikali ina mpango wa kuanzisha utalii wa Kiswahili, tuanita Swahili Tourism ambayo kwenye maeneo haya yenye kumbukumbu tutaanzisha Swahili Tourism iwe ni motisha; mtalii anapofika kwenye maeneo hayo basi kwanza atajifunza Kiswahili lakini atasimuliwa historia na kumbukumbu ya waasisi wetu walikuwaje na walifanya nini na ukizingatia kwamba Mwalimu Nyerere alikuwa ni mmojawapo wa waasisi wa kuboresha lugha yetu hii ya Kiswahii.

Nimhakikishie tu Mbunge kwamba eneo hili ni la muhimu na Mbunge wa eneo hilo alishanialika kwenda kule kwa ajili ya kuangalia namna ya kuboresha eneo hili ili liwe chanzo cha mapato ya Serikali. Kwa hiyo, niwatoe wasiwasi Wabunge na hata wale wengine ambao wana maeneo mengine yenye historia kupitia bajeti hii mliyotupitishia tutahakikisha kwamba maeneo haya tunayasimamia kikamilifu ili kuweza kuboresha sekta yetu hii ya utalii, ahsante. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; sera yetu ya utalii mbali ya kwamba inatuingizia mapato, pia wananchi wanaozunguka maeneo yenye hifadhi pia wananufaika. Halmashauri ya Mji wa Bunda imezungukwa na mbuga ya Serengeti.

Sasa swali langu, Mheshimiwa Waziri mbali ya kwamba wananchi wanalinda Hifadhi ya Serengeti lakini tembo wanapokuja kwa wananchi kuharibu mazao pamoja na nyumba zao wamekuwa hawalipwi fidia. Kwa mfano, Mcharo wananchi 350, Guta, 403, Bunda Store, 86, Kunzugu 65, Nyatwali 51 na Mheshimiwa Waziri nimeshaleta ofisini kwako watu hawa wanadai fidia kwa muda mrefu takriban watu 900. Lini watalipwa fidia yao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimtoe wasiwasi Mbunge. Mbunge wa Jimbo alishawahi kunifuata akanipa orodha ya wanaodai, lakini pia hata yeye mwenyewe ameshanipa orodha ya wanaodai. Kwa hiyo, tulikubaliana kwamba nitaenda mimi mwenyewe kuongea na wananchi, lakini wale wote wanaodai nitahakikisha kwamba Serikali imewalipa, lakini pia tutaongea na wananchi waendelee kuwa wahifadhi, maana hao ndiyo wanaotusaidia sisi hata kuhifadhi maeneo yanayozunguka hifadhi, ahsante. (Makofi)
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu ambayo siyo ya matumaini sana kwa wananchi wa Tarafa ya Umba, hasa Kata ya Mnazi na Lunguza, tunayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; kwa kuwa shughuli za wananchi hawa wanaozungukwa na hifadhi ya Taifa Mkomazi sehemu yao kubwa ni ufugaji na eneo lao ni dogo, lakini uanzishwaji wa hifadhi haujawatendea haki kwa sababu hakuna mlango hata mmoja wa kuingilia hifadhini kutokea upande huu wa Lushoto.

Je, ni lini sasa Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga geti la kuingia Hifadhi ya Taifa ya Mkomazi katika eneo la Kamakota, Kijiji cha Kivingo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa ukaribu huu wa Hifadhi na makazi ya watu unasababisha mara kwa mara wanyama waharibifu, hasa tembo, kuvamia mashamba katika Vijiji vya Mkundo- Mbaru, Mkundi-Mtae, kiasi kwamba zaidi ya ekari 3,000 za matikiti maji na mkonge zimeharibiwa vibaya na tembo.

Je, Waziri yuko tayari sasa kuwatembelea wananchi wale ili angalau akawaone na kuweza kuwafariji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Shangazi kwa kuendelea kuhamasisha utalii, hasa katika maeneo ya Jimbo lake la Mlalo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu Wilaya ya Lushoto ni eneo moja wapo ambalo linasaidia sana kuongeza mapato ya Serikali, hasa kisekta, na Mheshimiwa Shangazi amekuwa mara nyingi akitutembelea katika ofisi zetu kuelezea changamoto za maeneo hayo. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba Serikali inatambua mchango wkae, lakini pia tuko bega kwa bega kuhakikisha kwamba utalii unasonga mbele, ikiwemo eneo hili la Mlalo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo ameomba kuhusu kuweka geti katika eneo la Kamakota, nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti hii ambayo mmetupitishia, geti hili litafunguliwa ili kurahisisha watalii wanaoelekea maeneo ya Lushoto, hususan Mlalo, basi iwe rahisi sana kupita katika eneo hili la Kamakota.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, utalii tutaufungua katika eneo hilo na tuna uhakika kwamba tutaweza kupata mapato mengi yanayotokana na Hifadhi yetu hii ya Mkomazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ameuliza kama Waziri yuko tayari; nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba nitafika Mlalo, kama siyo basi atakuwa ni Waziri, kuongea na wananchi na kuendelea kuwapa pole hata wananchi wengine wenye maeneo ambayo wanakutana na changamoto hizi za wanyama wakali na waharibifu kama tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na idadi kubwa ya vifo ya karibu watu 60 ndani ya mwaka mmoja na watu 30 kupata vilema vya kudumu, Serikali inakuja na majibu ya kusema kwamba inafanya tathmini. Ni tathmini gani ambayo inataka kuifanya ili kujiridhisha ili waende wakavune na ni lini watakamilisha hiyo tathmini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, ni lini Serikali itatoa kifuta machozi kwa watu ambao ndugu zao wamefiwa au wameliwa na mamba na wengine wamepata majeruhi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Morogoro Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ufafanuzi katika eneo la kufanya tathmini. Maeneo ambayo anayaongelea Mheshimiwa Mbunge ni maeneo ambayo kiuhalisia, ni maeneo ya Mito na maeneo mengi ya Mito mamba wengi wanapenda kuishi maeneo hayo. Sekta ya Maliasili na Utalii tunahifadhi maeneo mbalimbali ambayo yanakuwa yamehifadhiwa. Lakini maeneo ya Mito ni maeneo ya mtiririko ambapo ukiangalia Mto kutoka eneo moja kwenda lingine ni eneo refu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunafanya tathmini kuangalia namna ya hawa mamba wanavyoishi majini kwa sababu, wanasafiri wanatoka njia moja kwenda njia nyingine. Unaweza ukamuona mamba yuko Morogoro lakini baada ya muda fulani ukamkuta yuko Pwani au yuko Mkoa wa Dar es Salaam. Kwa hiyo, tunafanya tathmini kuangalia hii namba ya hawa mamba ni kubwa kiasi gani. Kwa sababu, nao wana umuhimu fulani ambao katika maeneo hayo wanapaswa kuwepo sio kuwaondoa kabisa, kwa sababu vile vile, hiyo tunatambua kwamba ni moja ya maliasili ambayo inapaswa kuhifadhiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa hiyo, tukishakamilisha tathmini tutaangalia kama idadi ni kubwa basi tutawavuna. Swali la kwamba ni lini ni pale ambapo tutakamilisha tathmini ambayo sasa hivi mchakato wake tumeshaanza na kama ambavyo nimesema ni Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Katavi na Rukwa ambako ndio inasemekana kuna mamba ambao wanasumbua sana. Ikishakamilika tu ndani ya mwaka huu wa fedha tutawavuna ama kuwapunguza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lingine ameongelea kuhusu kifuta machozi nimtoe wasiwasi tu Mbunge kwamba, suala la kulipa kifuta machozi tumelianza toka mwaka wa fedha ulioisha na sasa hivi kuna maeneo yanaendelea kulipwa. Kwa hiyo, hata kwenye eneo lake kama wananchi hawajapata kifuta machozi basi ninawaelekeza Idara ya Wanyama Pori, wataenda katika eneo hili na wataenda kulipa wale wananchi ambao wameathirika na tatizo hili. Ahsante. (Makofi)
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nilikuwa nina maswali mawili ya nyongeza. Swali langu la kwanza, Serikali ina mpango gani pia kuendelea kutoa vibali kwa ajili ya wale wawindaji waliokuwa wakifanya uwindaji katika mbuga zetu za nyanda za juu kusini?

Mheshimiwa Spika, pia Serikali ina mkakati gani wa kushirikiana na Wizara ya Fedha ili kuboresha huduma za upatikanaji wa fedha za kigeni ili kuwarahisishia watalii nchini hasa kwa kuruhusu maduka ya kubadilisha fedha za kigeni?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jesca Jonathan Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge ameulizia kuhusu vibali vya uwindaji. Vibali vya uwindaji vimeendelea kutolewa na Wizara kama kawaida na wafanyabiashara kwa maana ya wawekezaji wote ambao wanatamani kuja kuwekeza kwenye eneo hili la uwindaji, tumekuwa tukitoa vibali kupitia mbinu mbalimbali ikiwemo ya kupitia manunuzi ambayo tunatangaza kwa njia ya kieletroniki. Kwa hiyo, ninawaalika tu wawekezaji ambao wanataka kuwekeza katika sekta hii ya uwindaji waje na kila baada ya muda tunapokuwa tumefanya matangazo haya kuna ambao wanapata lakini wanaochelewa, tunaendelea kutangaza kila baada ya muda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa kubadilisha fedha kwenye maduka haya ya fedha za kigeni, mpaka sasa Serikali imeendelea kushirikiana na hao wafanyabiashara ikiwemo kuandaa mazingira mazuri kwa ajili ya kuendelea na biashara hii ya kubadilisha fedha. Tunawaomba tu wale wafanyabiashara wote ambao wanafanya biashara hizi waendelee kufuata taratibu wa Serikali kama ambavyo imeendelea kuelekezwa na Wizara ya Fedha. Nasi Sekta ya Maliasili na Utalii tutaendelea kuungana nao pamoja ili kuhakikisha kwamba biashara hii inaendelea kufanyika ili tuweze kukuza utalii katika nchi yetu. Ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru Serikali kwa majibu mazuri, na nimpongeze Naibu Waziri kwamba naye ameshafika Liwale kwa hiyo ninachokizungumza anakifahamu. Lakini hii sehemu ya pili anayosema kwamba Madiwani na Wabunge wanahusika, kwamba wanapata hizi taarifa, mimi nimekaa Liwale miaka sita, sijawahi kupata hii taarifa zikiletwa kwenye Baraza letu la Madiwani. Kwa hiyo jambo hili labda leo aagize hili jambo lifanyike lakini hili jambo halifanyiki kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili, kwamba Kamati hii ya Uvunaji anayeingia mwanakijiji ni Mwenyekiti wa Kijiji peke yake, sasa wanaovuna hesabu zinakuja pale wanaambiwa cubic meters yule mwanakijiji cubic meters hajui, magogo mangapi yanaondoka hajui, matokeo yake kuna magogo yale makubwa ambayo yana mashimoshimo wanayaacha, kwa hiyo uharibifu ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kufahamu, ni lini Serikali italeta fedha za upandaji miti kwenye vile vijiji ambavyo vina uvunaji huo ambao mimi nausema kwamba ni uvunaji wa holela?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kuchauka Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba Kamati hii ni Kamati ambayo inaundwa katika level ya Wilaya, lakini washiriki wa Kamati hii ni pamoja na Wenyeviti wa Vijiji na Watendaji wa Vijiji, pia inajumuisha Meneja wa Misitu ambaye anatoka Makao Makuu TFS lakini yuko pale Wilayani, kuna Afisa Misitu ambaye anakuwa ni mjumbe, vilevile kuna Afisa Tawala wa Wilaya ni mjumbe pia kuna Afisa Ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaitamka hii Kamati ili afahamu Wajumbe wanaoingia mule ambao sasa ndiyo wanapeleka taarifa kwenye Baraza la Madiwani kama taarifa ya wale wote tu waliopitishwa kwenye orodha ya uvunaji wa mazao ya misitu na anayekuwa Mwenyekiti wa Kamati hii ni Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya na Katibu ni Meneja wa Misitu anayetoka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa hii inapokuwa imekamilika inapelekwa kwenye Baraza la Madiwani. Baraza la Madiwani Wabunge ni Madiwani, wanashiriki pia Mwenyekiti wa Halmashauri ni Diwani na hawa Wenyeviti na Watendaji wa Vijiji wanapopeleka maombi yao kwenye hii Kamati ya Wilaya tayari wanaonekana ni wajumbe ambao watapeleka tena kwenye WDC kama taarifa. Kwa hiyo taarifa hizi kuanzia level ya kijiji kwenda WDC na mpaka kufika kwenye Halmashauri, Mbunge na Mwenyekiti anakuwa ameipata kupitia Mabaraza yanayofanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi niwaombe tu, kwa kuwa huyu Mjumbe ambaye ni Afisa Ardhi wa Wilaya anaingia kwenye hii Kamati na kama hafanyi hivyo basi anafanya makosa ni kwamba hii taarifa baada ya kukamilika inatakiwa ikasomwe kwenye Baraza la Madiwani ili Waheshimiwa Wabunge wafahamu lakini pia na Mwenyekiti wa Halmashauri afahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivyo kwa sababu Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana ya Mwenyekiti wa Halmashauri ama Mbunge, wale ni wasimamizi, hawawezi kuingia kwenye mchakato kama ilivyo maelekezo na miongozo ya uvunaji wa misitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ameongelea kuhusu fedha, ni kweli kulikuwa kuna changamoto ya fedha, tukipeleka kwenye Halmashauri, halmahsauri zilikuwa hazifikishi kwenye maeneo husika ambayo kunatakiwa kuanzishwa vitalu na kupandwa hii miti ili kuziba yale maeneo ambayo yamekwisha vunwa. Kwa sasa tutapeleka hizo fedha lakini tutaleta mwongozo mahsusi wa kuhakikisha fedha hizi zinawafikia wale tu ambao wanahusika na fedha hizi na siyo Halmashauri kuelekeza kwenye matumizi mengine.Naomba kuwasilisha.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza naishukuru Serikali kwa kuifanya Iringa kuwa kitovu cha utalii kusini, lakini mradi huu ambao GN hiyo imetangwazwa Julai, 2021 ulizinduliwa tarehe 12 Februari, 2018 na Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassain akiwa Makamu wa Rais. Sasa swali langu ni moja tu kwa Serikali, je, inaridhika na speed ya utekelezaji wa mradi huu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa David Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi huu utakamilika kwa wakati. Nasema hivyo kwa sababu mradi huu una-cover maeneo manne ya Kusini mwa Tanzania ambako ndiyo unatekelezwa. Mradi huu kwenye maeneo haya ni pamoja na Hifadhi ya Nyerere, Ruaha, Udzungwa na Mikumi.

Mheshimiwa Spika, eneo analoliongelea Mheshimiwa Chumi ni eneo mojawapo ambalo ni ujenzi wa kituo mahususi kwa ajili ya kutunza information za masuala ya utalii. Hivyo, maeneo mengine mradi huu unaendelea ambapo mitambo mbalimbali imeshanunuliwa, magari lakini pia kuna viwanja vya ndege ndani ya hifadhi vimeendelea kukarabatiwa na miundombinu mingine mingi inaendelea kufanyika. Hivyo, eneo hili lilikuwa linasubiri tu GN iweze kukamilika, lakini wakati huo huo tuna mshauri mwelekezi ambaye tayari ameshaanza zoezi na tumeshaanza kupokea ripoti. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakamilisha mradi huu kwa wakati bila wasiwasi. Ahsante. (Makofi)
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kuwa, miongoni mwa viumbe hai waliozuiliwa ni pamoja na vipepeo ambao sio maliasili, vipepeo wanaozalishwa na watu binafsi Wilayani Muheza, Mkoani Tanga. Je, Serikali iko tayari kutoa tamko rasmi kwamba, masharti waliyoyatoa yatawahusu viumbe hai ambao ni maliasili na vimbe hai wanaozalishwa na watu binafsi hayawahusu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Mto Zigi, Mkoani Tanga, una mamba wengi ambao wanaua watu wengi kwa muda mrefu sana. Tangu nikiwa binti mdogo watu wanafariki na juzi tu kuna mtu ameliwa na mamba na vilevile watu watatu wameshaliwa na mamba miezi miwili iliyopita. Je, Serikali haioni haja ya kwenda kuvuna mamba wale hata kama mto ule hauko ndani ya hifadhi, lakini mamba ni maliasili? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Engineer Mwanaisha Ulenge, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mwanaisha kwa maswali mazuri ambayo ameyaelekeza kwa Serikali, likiwemo hili la wanyamapori hai. Nataka nimwondoe wasiwasi, tunaposema wanyamapori hai ni wanyama wa aina yoyote iwe mdudu, nani, anaposafirishwa nje ya nchi sisi kama Maliasili na Utalii tunatambua kwamba, hiyo ni rasilimali ya nchi na haipaswi kuhamishwa kutoka eneo moja kwenda nje ya nchi. Kwa hiyo, nataka nimtoe wasiwasi na ndio maana hata hawa mamba pengine hawapo hata kwenye hifadhi, lakini kwa kuwa ni maliasili za Taifa lazima tuzilinde. Tunazilinda ili tuweze kuleta watalii ndani ya nchi waje kuona na tunapata mapato kutokana na vivutio hivi tulivyonavyo.

Mheshimiwa Spika, kwa kifupi maswali yote nimeyajibu kwa pamoja, lakini hili la kuvunwa mamba nimtoe wasiwasi, mwezi uliopita tulikuwa tuna tathmini ya kukusanya data ya mamba wote ambao wamekuwa wakisumbua wananchi. Tayari tuko kwenye mkakati wa kwenda kuwavuna, hivyo muda wowote ninavyosema kuanzia sasa, tutatuma wataalam wa kwenda kuvuna mamba hao. Naomba kuwasilisha.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na ninashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa na tatizo kubwa sana katika eneo hili la hifadhi hii ya Burigi Chato na tunashukuru kwa fedha ambazo zimetolewa na kutoa elimu kwa umma unaozunguka hifadhi ile. Kumekuwa na kesi kubwa sana pale za mifugo ya watu kukamatwa ndani ya hifadhi lakini baada ya kukamatwa zinapopelekwa kesi mahakamani, watu wale wamekuwa wanatozwa fine ya Shilingi 100,000/= kwa kila ng’ombe na wengi wanalipa baada ya kutozwa ile fine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa shida imekuja unatoza fine mahakamani ulikamatiwa ng’ombe 100 unapopewa barua ya mahakama, umeshalipa fedha ya Shilingi Milioni 10 ukarudishiwe ng’ombe wako unaenda unakuta ng’ombe wako 70, ng’ombe wako 80 badala ya ng’ombe waliokamatwa.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba kusikia kauli ya Serikali juu ya vitendo hivi ambavyo vimesababisha wananchi wa Biharamulo kuteseka na hatimae kupoteza fedha zao na ng’ombe hao ambao wamekuwa wanapotea huko. Nisikie kauli ya Serikali juu ya hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kumekuwa na kesi pia wananchi wananifuata ninapokuwa Jimboni, saa nyingine wanapiga simu na kwa DC kesi zipo. Mwananchi anakuja analalamika kwamba, Mheshimiwa Mbunge nimekamatiwa ng’ombe wangu 50 bado tuna kesi mahakamani, lakini ng’ombe wangu nimewaona kwenye mnada wanauzwa. Sasa naomba kusikia kauli ya Serikali juu ya hili jambo ambalo limesababisha watu sasa wanaona taabu kabisa na wanatuchonganisha na wananchi. Tukisikia kauli ya Serikali juu ya hili pia hao ng’ombe ambao wamekuwa wanauzwa kwenye mnada je, hatuoni haja ya Serikali kuunda Tume Maalum, kwa ajili ya kwenda kuangalia hivi vitendo vya wananchi kulalamika? Kwamba, ng’ombe wao wanauzwa kwenye mnada na ilhali bado kesi zinaendelea mahakamani.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kuwasilisha. (Makofi)
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika,
ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza niendelee kutoa pole kwa wale wananchi ambao wameendelea kukutana na kadhia hii, ya kudhulumiwa mifugo yao na kumekuwa ndiyo na malalamiko mengi na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walishawahi kunifuata kwamba, kuna baadhi ya wahifadhi wasio waaminifu ambao inapelekea mifugo yao kutotimia kama ambavyo imekamatwa awali.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tunafahamu Sheria za Utumishi wa Umma, watumishi hawa tumekuwa tukiwachukulia hatua wale ambao wanahusika na kadhia hii ikiwemo upotevu wa mifugo. Lakini pia kumekuwa na changamoto ya baadhi ya mifugo ambayo huwa inakufa wakati ikiwa inasubiri kupelekwa Mahakamani kwa maana ya kesi inapochukua muda mrefu Mahakamani inapelekea baadhi ya mifugo kupoteza maisha. Lakini kwa upande mwingine ambao amesema Mheshimiwa Mbunge kwamba mifugo mingine inaonekana iko minadani, basi Serikali itaendelea kufuatilia na wale watumishi ambao wanahusika na changamoto hizi tutawachukulia hatua. Na inapothibitika basi wengine tunawasimamisha kazi na hata kufukuzwa kazi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge ambao wana changamoto hii, niwaombe pale kuna mfugaji ambaye amekutana na changamoto hii basi watusaidie kutupa hizi taarifa. Lakini pia niwaombe Waheshimiwa tuendelee kuelimisha hawa wafugaji pia, wakifuga kwa kufuata Sheria na taratibu za nchi ninaamini kabisa kadhia hii tutaipunguza kabisa ama kuimaliza. Ahsante. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, katika harakati za Serikali kuhifadhi mazingira na maliasili yetu ilihamasisha wananchi kufungua mabucha ya wanyamapori. Wananchi wa Jimbo langu walihamasika na walifungua mabucha tatizo ni upatikanaji wa leseni kutoka Wizara husika.

Je, ni lini wananchi wangu watapatiwa leseni ili shughuli hii ya kuuza nyamapori iweze kuanza ndani ya Wilaya yangu?
NAIBU WAZIRI, MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali imeendelea kutoa leseni za mabucha kwenye maeneo mbalimbali ya hapa nchini na hizi bucha ni kwa ajili ya wanyamapori. Mwaka wa fedha 2020/2021 tuliweza kutoa leseni zaidi ya 46 na tuna masharti ya namna ambavyo wanapaswa kuomba hawa wafanyabiashara wanaofanya biashara hizi za wanyamapori. Lakini kumekuwa na changamoto ya ukosefu wa wanyamapori wenyewe, kwa maana unapowinda kuna- target ambazo wanazifahamu wawindaji. Sasa kumekuwa na malalamiko kwa wale wenye leseni wanakosa nyama na matokeo yake wanarudisha wanashindwa kuendelea na biashara hii.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Mbunge kama kuna yeyote ambaye anahitaji leseni, Wizara ya Maliasili na Utalii iko tayari wakati wowote kutoa leseni. Lakini changamoto inayojitokeza ni kwamba upatikanaji wa wale wanyama wenyewe ndiyo changamoto halisi inayojitokeza. Kwa sababu, uwindaji kuna maeneo ambayo tunayatenga lakini inapokosekana basi malalamiko yanarudi kwa Serikali, lakini leseni zipo tunawakaribisha wafanyabiashara wote waje. (Makofi)
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana. Kwa kuwa, ukosefu wa vitalu vya kufugia mifugo na maeneo ya malisho ndio sababu kubwa ya kupeleka mifugo hifadhini na kwa kuwa, elimu inayotolewa na Wizara ya Maliasili inatolewa kwa binadamu na siyo ng’ombe na kwa vile ng’ombe wao wanataka kula majani na wakati wa kiangazi hakuna sehemu ya majani na majani yako porini.

Je, Wizara ina utaratibu gani ama ina mpango gani wa kuhakikisha eneo lile la hifadhi linamegwa, tunapata vitalu kwa ajili ya kufugia mifugo yetu ng’ombe kwa upande wa Biharamulo na Ngara? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndaisaba, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kumekuwa na changamoto ya ukosefu wa malisho na imepelekea kuwepo na migogoro baina ya Wahifadhi na Wafugaji. Serikali inatambua changamoto za ukosefu wa maeneo ya mifugo, lakini kupitia Kamati ya Mawaziri Nane ambao tumekuwa tukizunguka nchi nzima, tayari Serikali imetoa maeneo ambayo yatamegwa kwa ajili ya wananchi kutumia. Hivyo tunaendelea kuelekeza wananchi wayatumie vizuri ikiwemo kutenga maeneo hayo kwa ajili ya malisho na kuandaa matumizi bora ya ardhi kwa ajili ya wafugaji na matumizi kwa ajili ya kilimo. Hivyo, Serikali imeshaliona hili na tumeendelea kutoa elimu lakini pia kumega maeneo ya hifadhi. (Makofi)
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Wizara lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; je, Wizara ina mkakati gani kuongeza watalii kwa sababu kutokana na UVIKO-19, idadi ya watalii wanaopanda Mlima Kilimanjaro imepungua sana kutoka 50,000 mpaka 12,000 kwa mwaka 2020. Je, Serikali sasa ina mkakati gani wa kuweza kuongeza watalii na kusaidia ajira kwa vijana wanaotegemea mlima huo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; akinamama wajasiriamali wa Kilimanjaro wanaojishughulisha na shughuli za utalii tunaomba na wao waweze kupatiwa mikopo ili waweze kutangaza zaidi mlima wetu, mbuga zetu na utalii kwa ujumla. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Edwin Malleko, Mbunge wa Viti Maalum Kilimanjaro, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Esther kwa juhudi nzuri anazozifanya za kuendelea kutangaza vivutio vya utalii ukiwemo Mlima Kilimanjaro. Nampongeza sana kwa sababu amekuwa ni balozi mzuri wa kuhakikisha eneo hili linaendelea kuvutia watalii wengi.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo ameuliza kwamba tuna mkakati gani wa kuendelea kuongeza watalii na kuongeza ajira kwa vijana. Eneo hili Wizara imekuwa ikibuni mbinu mbalimbali zikiwemo kuanzisha marathons mbalimbali katika maeneo mbalimbali ya hifadhi, lakini lengo ni kuhakikisha kwamba watalii wengi wanakwenda kuviona vivutio lakini pia kuwa mabalozi wa kuendelea kuvitangaza.

Mheshimiwa Spika, hili ni shahidi hata Watanzania wa leo wamekuwa wazalendo na kila mtu sasa hivi anamhabarisha mwenzake kuhakikisha kwamba wanafika kwenye vile vivutio, lakini siyo kufika tu, kuisemea Tanzania ndani ya nchi na maeneo mengine ya nje ya nchi na lengo ni kukuza utalii na kuongeza pato la Taifa. Ahsante.
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na kuutangaza Mlima Kilimanjaro ningependa kufahamu, je, Serikali ina mkakati gani wa kutangaza vivutio vidogovidogo ambavyo vipo katika mikoa hasa Mkoa wa Ruvuma, Wilaya ya Mbinga, yenye vivutio vidogo vingi vya kihistoria vyenye kuvutia ili kupata watalii na kuongeza mapato ya ndani?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kapinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na vivutio vidogovidogo ambavyo kwa nia moja au nyingine Serikali ilichelewa kuviibua, lakini Wizara ina mkakati wa kuhakikisha inaibua na kuvitangaza vivutio hivi katika kila mkoa, wilaya na kata.

Mheshimiwa Spika, vivutio vingi vidogovidogo havina GN, hivyo tumeendelea kuelimisha wananchi, kuelimisha Serikali za Vijiji, kata na halmashauri kuhakikisha kwamba yale maeneo ambayo yanasimamiwa na halmashauri ama vijiji wayaibue na Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii itatoa wataalam wa kuweza kushauri na kutoa usaidizi wa kuhakikisha kwamba haya maeneo yanapata GN na kuyatangaza na wale watalii waweze kufika katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. NORAH W. MZERU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, je, kuna mpango gani wa kuwavutia wawekezaji katika sekta ya utalii Morogoro? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Norah Mzeru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Norah kwa kuendelea kuimarisha utalii, lakini pia kuendelea kuhamasisha katika maeneo mbalimbali ikiwemo maeneo yaliyohifadhiwa katika Mkoa wa Morogoro.

Mheshimiwa Spika, nipende tu kumtaarifu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeweza kuainisha maeneo mbalimbali kwenye maeneo yaliyohifadhiwa kwa ajili ya kuwekeza na shughuli hizi za uwekezaji zinahamasishwa katika maeneo mengine mengi ambayo utalii unafanyika. Hivyo, nimtoe wasiwasi katika hifadhi ya Udzungwa, Mikumi, pamoja na Nyerere, tumetenga maeneo mahususi kwa ajili ya uwekezaji. Hivyo, tunaendelea kuwaalika wawekezaji wa ndani ya nchi na nje ya nchi waweze kufika katika maeneo hayo na kuwekeza kwa ajili ya kuongeza na kukuza utalii. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza, napongeza majibu mazuri ya Serikali. Labda kabla sijauliza maswali ya nyongeza, nina maelezo ya ziada kwamba eneo la Uwanja wa Ndege wa Ipole liko chini ya Ofisi ya TAWA Kituo cha Ipole cha Pori la Akiba la Ugalla. Nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa kutoka Tabora mpaka Ipole ni kilomita 100; na kutoka Koga mpaka Ipole WMA ni kilomita 90: Je, Serikali haioni kwamba kujenga uwanja huo wa ndege pale Ipole kutakuwa na faida zaidi katika kuvutia watalii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: kwa kuwa huyu mwekezaji ameshajenga uwanja mdogo pale Koga na inaonekana kabisa Serikali haina nia ya kuendeleza ujenzi wa Uwanja wa Ndege pale Ipole: Je, Serikali iko tayari kuyarudisha mashamba na ardhi ya wananchi wa Ipole waliyoitoa mwaka 1996 kwa nia njema kwa Serikali kwa ajili ya kujenga Uwanja wa Ndege, kuwarudishia ili waendelee na shughuli zao za kiuchumi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nampongeza sana Mheshimiwa Kakunda kwa kuwa mhifadhi na pia ameendelea kuhamasisha utalii, ikiwemo maeneo haya yaliyopo katika Wilaya ya Sikonge hasa katika Pori la Akiba la Ugalla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kutoka Tabora mpaka Ipole ni kilomita 100 ambazo huwa zinasaidia watalii wanaofika Tabora kuelekea katika eneo hili la WMA. Sambamba na hilo, Mheshimiwa Kakunda ameomba Serikali iweze kujenga kiwanja katika eneo la Ipole ili kurahisisha watalii waweze kupita njia ambayo ameisema ya kilomita 90.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshauri tu kwamba maeneo yenye uhitaji ni mengi; na kwa kuwa kiwanja cha Tabora kinatosheleza maeneo haya kwa hizo kilomita alizozisema, basi naomba wananchi au wawekezaji waliopo katika maeneo hayo, waendelee kuvumilia wakati tunaangalia namna ya kuweza kuboresha, kiwanja kidogo kilichopo katika Kituo cha Ipole ili kuwawezesha wale watalii wanaotaka kuingia kwenye hiyo WMA ama kwenda kwenye Pori la Akiba la Ugalla waweze kufika kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tu kwamba Pori la Akiba la Ugalla limeshapata mwekezaji na tayari huyo mwekezaji yupo tayari kuendelea kuboresha kiwanja hicho. Hata Serikali tutajipanga katika maeneo hayo kuhakikisha kwamba tunaboresha viwanja hivyo ili kurahisisha watalii waweze kufika katika maeneo hayo. Ahsante (Makofi)
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi. Mahitaji ya uwanja katika Wilaya ya Sikonge ni sawa kabisa na mahitaji, ambayo yapo katika Jimbo letu la Biharamulo ikizingatiwa kwamba Hifadhi ya Burigi, Chato ipo Biharamulo na mageti yote yapo Biharamulo; hata hivyo, tumekuwa na uwanja wetu wa muda mrefu pale eneo la Katoke ambao ungesaidia zaidi kukuza utalii hasa kwa wageni ambao watahitaji kutembelea Hifadhi ya Biharamulo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu: Ni lini mpango wa Serikali kusogeza huduma pale katika eneo la Katoke kwa kukarabati ule uwanja ili uweze kutumika na watalii wanaotembelea hifadhi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, namshukuru sana Mheshimiwa Engineer Ezra kwa kuwa ni mdau mkubwa wa kuhamasisha utalii katika maeneo ya Burigi Chato; na hili ni eneo mojawapo ambalo tumeendelea kulihamasisha; na kwa bahati nzuri sasa hivi tumeshaanza kupata watalii wengi katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakumbuka kwamba tuna kiwanja kizuri sana ambacho kimejengwa na Serikali maeneo ya Chato. Uwanja huu ni mkubwa ambao ulikuwa na lengo la kuhakikisha wale watalii wote ambao wanataka kuingia lango la Chato na Biharamulo waweze kufika kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iliweka mkakati kwamba pamoja na watalii wengi wanaopita maeneo hayo, wengi wao wakiwa wanunuzi wa madini, basi wanapopita kwenda kununua madini na uwanja wa ndege wa Taifa uko pale, basi ni rahisi kupita maeneo yale na pia kuona vivutio vilivyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, namwomba Mheshimiwa Eng. Ezra awe na subira kidogo wakati tunaangalia mafungu mbalimbali ya kuweza kuboresha eneo hili la Biharamulo – Katoke, tuendelee kutumia huu uwanja wa Taifa uliopo ambao ni mzuri zaidi kwa ajili ya kuwezesha watalii waweze kuingia katika malango haya yote mawili. Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mbuga ya Serengeti ni maarufu sana duniani na watalii wengi sana huvutiwa kuja kutembelea mbuga ile, lakini kumekuwa na changamoto mbalimbali ikiwepo ukosefu wa uwanja wa ndege: -

Mheshimwia Mwenyekiti, kwa kuwa tangu Bunge la Kumi chini ya Mwenyekiti wa Wabunge wa Mkoa wa Mara, Mheshimiwa Wasira, tumekuwa tukifuatilia Serikalini kuhakikisha kwamba ile mbuga ndani ya Serengeti inajengwa uwanja wa kimataifa ili watalii wanaotoka nchi nyingine waje moja kwa moja watue kwenye huo uwanja wa kimataifa wa Serengeti kuliko ilivyo sasa hivi ambapo wanapita Kenya kwa njia za barabara: Ili kuongeza mapato ya nchi, kwa nini Serikali haioni umuhimu sasa wa kujenga uwanja wa Serengeti kuwa uwanja wa Kimataifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge kutoka Mkoa wa Mara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Esther kwa kuendelea kuwa mdau katika Hifadhi ya Serengeti. Tunamshukuru sana kwa sababu ameendelea kutoa mchango mzuri katika Taifa letu ikiwemo Mbuga hii ya Serengeti ambayo imekuwa ikiongoza Kimataifa na duniani kote kama ni Mbuga bora. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimtoe wasiwasi Mbunge kuhusu suala la ujenzi wa Kiwanja cha Kimataifa cha ndege ambacho Serikali inafikiria kujenga. Suala hili tumepanga kuweka uwanja wa ndege wa Kimataifa kwenye Wilaya ya Mugumu; na tayari Serikali tumeshapeleka maombi ya kuandaa eneo kubwa la uwekezaji, likiwemo eneo la uwanja wa ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili tunalishanya kwa sababu wenzetu majirani tayari wameshaanza mchakato wa ujenzi wa uwanja wa kimataifa na lengo ni kuiua Mbuga ya Serengeti kwa kuleta watalii upande wao, lakini pia iwe rahisi kuingiza Tanzania. Nasi tumeona ni bora sasa tukaingia kwenye ushindani ikiwemo kujenga uwanja huu wa kimataifa ili ndege zinapokuja ziende moja kwa moja kwenye Hifadhi yetu ya Taifa ya Serengeti na moja kwa moja iwe rahisi kuingia kwenye Hifadhi ya Serengeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, tunafanya hivyo ili kupunguza kelele na miungurumo mbalimbali inayofanyika kwenye uwanja mdogo ule wa Seronera ambao umekuwa ni kero kwa wanyama na hata kiuhifadhi. Hivyo, tunataka kuuhamishia maeneo ya Mugumu ili iwe rahisi kuleta wasafiri/watalii mbalimbali wanaotoka nje ya nchi waje kwa ajili ya kutuletea mapato nchini. Ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Inaelekea kuna mkanganyiko kidogo kwenye majibu ya Serikali, kwa sababu mwaka 2007 wananchi wa Kata ya Ilungu hususan Kijiji cha Kikondo walifanyiwa tathmini ya kupewa fidia kwa yale maeneo yaliyochukuliwa na DAFCO ambayo sasa hivi ndiyo Hifadhi ya Taifa ya Kitulo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na hali hiyo wenzetu wa TANAPA walishindwa kuwafidia wale wananchi, kwa hiyo yale maeneo hasa Kijiji cha Kikondo bado yanatumika ni kijiji ambacho kina shule kina zahanati. Pia kuna maeneo ambayo yalichukuliwa na watu wa TFS kwenye Misitu ya Mwambalis na hayo maeneo yamekuwa yakitumiwa na wananchi hata kabla ya hapo na mpaka leo yanatumiwa.

Sasa kutokana na mkanganyiko wa majibu, naomba Mheshimiwa Waziri apange ziara akayatembelee hayo maeneo ili afanye tathmini yeye mwenyewe ili kujua uhalisia, lakini hali siyo nzuri kuna mgogoro na wananchi kwa kweli wanapata shida sana. Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwa na changamoto hizi ambazo mara nyingi wananchi wamekuwa wakihitaji ardhi wakati huo huo maeneo haya yalichukuliwa na Serikali. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba changamoto hizi tutaenda kuzifuatilia, lakini pia tutaenda kukutana na wananchi ambao wamekutana na kadhia hii na lengo ni kukaa pamoja ili kuweza kutatua changamoto hii. Hivyo nitafika kwake kwenda kutatua changamoto hii. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante hili suala la Hifadhi ya Kitulo liko pia Makete ambako ni wilayani kwangu. Kuna mgogoro mkubwa kati ya wananchi na Hifadhi ya Kitulo kwa sababu uwekaji wa beacon ya mipaka haukushirikisha wananchi kitu ambacho kimesababisha mgogoro mkubwa. Pia tuna hifadhi ya Mpanga Kipengele ambako kuna Vijiji vya Ikovo, Kimani na kwenye Hifadhi ya Kitulo mgogoro mkubwa uko kwenye Vijiji vya Chankondo, Misiwa kule Itelele.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Bunge hili ilituahidi kwamba itakuja Makete kutatua hii kero na haijaja hadi leo. Ile timu ya Mawaziri Nane pia ilisema itafika Makete haijafika hadi leo.

Je, ni lini Serikali itakuja kutatua changamoto hii ya migogoro ili wananchi wangu waweze kupata maeneo kwa kufanya kazi kwa sababu ndiyo waliotumia kuhifadhi hii Hifadhi ya Kitulo hadi Serikali imekuja kuichukua mwaka 2005?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na maelekezo ya Mheshimiwa Rais ambaye aliandaa Kamati ya Mawaziri Nane ambao walikuwa wanapaswa kuzunguka nchi nzima. Zoezi hili tulilianza kipindi cha mwaka uliopita na tulizunguka kwenye baadhi ya maeneo. Nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Sanga kwamba zoezi hili bado ni endelevu tutafika kwenye maeneo yote yenye migogoro na tutatatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, yale ambayo yameshapitiwa na kamati hii tutahakikisha kwamba yanarudishwa kwa wananchi. Yale ambayo ni migogoro mipya Mheshimiwa Waziri ameshaunda kamati nyingine ambayo tumeanza kupitia tena upya maeneo ambayo yana migogoro ili kuhakikisha kwamba wananchi na maeneo ya hifadhi yanahifadhiwa vizuri na wakati huo huo wananchi wanaendelea na shughuli zao za kila siku. Ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kama kuna mkoa ambao ulikuwa unasubiri kwa hamu ile Timu ya Mawaziri Nane ni mkoa wa Morogoro. Jimbo la Mikumi, Kata za Zombo, Muhenda, Kisanga na Mikumi zimekuwa katika changamoto ya muda mrefu ya mipaka kati yao na TFS, kati yao na TANAPA.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba kuna timu ambayo imeundwa na Waziri kuorodhesha migogoro hiyo. Je, kata hizo na vijiji hivyo vya kata hizo zinaenda kuingia katika orodha ndefu ya vijiji vyenye migogoro? Nawakilisha.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili naomba nilifafanue kwa ufasaha zaidi kuna ile migogoro ambayo inapitiwa na Mawaziri Nane. Hii migogoro Mawaziri Nane watapita kwenye maeneo nchi nzima na watatatua hii migogoro. Hata hivyo, kuna migogoro mipya ambayo haikuwahi kupitiwa na Kamati ya Mawaziri Nane. Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii ameunda Kamati ndani ya Wizara imehusisha na maeneo mengine kwa maana ya watumishi wa ardhi na maeneo ya mazingira kupitia mapori ya hifadhi, kupitia ramani moja baada ya nyingine kuangalia huu mgogoro unatoka wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna migogoro mingine ni ya beacon, kuna migogoro mingine wamesogea kidogo, kwa hiyo kuna mabishano kati ya mipaka na mipaka. Kamati hii itapita tena upya na itaangalia pale ambapo pana mgogoro tutautatua kwa pamoja na tutazisoma ramani tuta- define mipaka na baadaye tutatoa majibu sahihi ili wananchi waridhike na maeneo ya hifadhi, lakini wakati huo huo watendewe haki kuliko ilivyo sasa. Ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kwanza nianze kuipongeza Wizara ya Maliasili kwa kushirikiana na wananchi wa Jimbo la Nyangh’wale kuweza kutokomeza wanyama wakali kama vile fisi ambao walipoteza maisha ya wananchi wangu wa Jimbo la Nyangh’wale. Sasa swali, je, ni lini Waziri atapanga ziara ya kuja kuwapa pole wananchi wa Jimbo la Nyang’wale lakini pia kifuta machozi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hussein, Mbunge wa Nyang’wale, kama Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuelezea changamoto hii ya fisi. Ni kweli kumekuwa na changamoto, fisi wanakuwa wamebaki kwenye maeneo ambayo siyo ya hifadhi na wamekuwa wakiwadhuru wananchi. Zoezi hili tulishaelekeza watendaji, pengine na hapa tena nitoe maelekezo kwamba watendaji walioko Kanda ya Mwanza, nikimaanisha magharibi tuandae operation ya kwenda kuwasaka wale fisi wote ambao hawako kwenye maeneo ya hifadhi na kuwarejesha kwenye maeneo ya hifadhi ili kunusuru hali za wananchi wa Jimbo la Nyang’wale. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali ya nyongeza. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri yanayoeleweka na ambayo yamenijenga zaidi.

Mheshimiwa Spika, maswali yangu mawili ni kwamba; kwa kuwa fursa kwa watu binafsi ya kuanzisha ranchi, mashamba na bustani za wanyamapori imetolewa.

Je, hadi sasa ni watanzania wangapi wamepata fursa hiyo?

Swali la pili nilitaka kujua, kutokana na utaratibu huo hadi sasa hivi Serikali imepata faida kiasi gani? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa sasa jumla ya ma-butchery 71 ambayo yamekwisha sajiliwa na yanafanya kazi na kwa ujumla sasa siwezi kujua idadi lakini wamiliki ni pamoja na kuwa na leseni na kwa sasa hivi leseni zilizosajiliwa ni 71. Lakini pia faida zake tulizozipata ni pamoja na kupokea mapato jumla ya shilingi 229,500,000; lakini pia tumeweza kuongeza ajira kwa wananchi ikiwemo Madaktari wa Mifugo ambao wanapaswa kuajiriwa kwa kila mwenye butchery au shamba, bustani au ranchi ili kuwezesha hawa wanyama kupata huduma za kitabibu. Lakini pia tumeongeza ajira katika wahudumu wanao wahudumia hao wanyamapori ambao wapo katika ranchi hizo ama bustani. Ahsante. (Makofi)
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nitoe pia shukrani zangu za dhati kwa hatua hiyo iliyofikiwa ambapo sasa wanyama kama vile tembo, twiga, swala na wengineo wameongezeka sana. Sasa naomba kuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, je ni kwa namna gani sasa wananchi wanaozunguka msitu ule wameshirikishwa ikiwa ni pamoja na kupewa elimu ili kuepusha migogoro na migongano isiyokuwa na lazima inayoweza kujitokeza? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pili, je, Serikali inatoa commitment gani wakati wa kutoa tangazo sasa la kuumiliki ule msitu, kupeleka mizinga ili wananchi waone fursa yaani wanufaike na zile fursa zinazotokana na huo msitu ili nao wawe sehemu ya kuutunza huu msitu? Naomba kuwasilisha. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abeid Ramadhani, Mbunge wa Singida Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye majibu yangu ya msingi ni kwamba Serikali tumeendelea kupongeza Serikali za Vijiji, Wilaya na Mikoa kwa hatua ambayo wamefikia kwamba maamuzi waliyoyafanya kwanza ni mazuri; lakini pia nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakapokuwa tumeshakamilisha tangazo na kuwa na GN ya eneo lile basi tutaanza kuelimisha wananchi wanaozunguka maeneo hayo kuangalia na kuona faida za kuhifadhi huo msitu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia faida nyingine zinazopatikana katika maeneo hayo ikiwemo kuhamasisha wananchi kujiendeleza na faida ya ufugaji nyuki ili kuweza kupata zao la asali lakini kwa wakati huo huo tunaweza tukaendelea kutangaza utalii na likawa eneo mojawapo la kuhamasisha watu kwenda kutembelea katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika hizi zote ni faida kwa wananchi na watarajie kwamba watafaida nae neo hili kwa sababu uhifadhi ni moja ya maeneo ambayo tunaendelea kuhamasisha nchini kote. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Nitambue kazi kubwa inayofanywa na Wizara hii, pamoja na kutambua mikakati hii ambayo itasaidia kutangaza na kuviendeleza lakini bado sisi tulioko kwenye maeneo yale ikiwa ni pamoja na wataalam wa halmashauri hawana uelewa wa mikakati hii.

Sasa Mheshimiwa Waziri yupo tayari baada ya Bunge hili kuja Ukerewe ili kwa pamoja sasa wao na sisi pamoja na wataalam wa halmashauri tuweze kushirikishana mikakati hii ili iweze kuwa na tija?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; moja kati ya vivutio vilivyoko Ukerewe ni pamoja na beach ya Rubya ambapo pia kuna msitu ulio chini ya TFS. Lakini kwa kuwa Ukerewe tuna upungufu wa madawati karibu 6,000; Mheshimiwa Waziri kupitia CSR, TFS wako tayari kutusaidia kuondoa upungufu huo wa madawati 6,000? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph Mkundi, Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, niko tayari kuambatana na Mbunge kwenda katika Kisiwa cha Ukerewe kuibua vivutio vilivyopo, lakini pia kuvitangaza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini suala hili la pili la kuhusu beach ya Rubya ni kweli tuna hifadhi ya Rubya ambayo ni hifadhi ya msitu unaosimamiwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania na tumekuwa tukitoa CSR katika maeneo hayo na hivi karibuni tunakwenda kuzindua Kituo cha Polisi ambacho kimejengwa kutokana na hii Hifadhi ya Rubya. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba wajibu wa Serikali ni kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo tunayahifadhi wananchi walioko kwenye maeneo hayo wanafaidika na rasilimali iliyoko pale. Kwa hiyo, suala la madawati tutakwenda kulishughulikia na tutakwenda kuzungumza na wananchi ili waone umuhimu wa kuendeleza hifadhi hiyo.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushuruku sana lakini pia nashukuru sana majibu mazuri ya Serikali, hata hivyo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwanza, kutoka barabara kuu kufika Kitulo pana mlima wenye kona 54 na nyani wa kutosha. Je, Serikali ina mpango gani wa kutengeneza barabara ile kwa kiwango cha lami ili watalii wakafurahie nature ya uumbaji wa Mwenyezi Mungu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili; je, Wizara ina mpango gani wa kujenga ofisi walau ndogo pale Chimala ili kuamsha ari ya wananchi pale kujenga mahoteli ya kitalii jambo ambalo litaleta fursa ya ajira kwa vijana na kuinua uchumi wa Wanambarali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Mbalali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna changamoto ya barabara hii na tutazungumza na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi ili tuone namna ya kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami na hii itasaidia kuvutia utalii katika maeneo yanayozunguka Hifadhi ya Kitulo.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la ujenzi wa ofisi ninaomba nilichukue tukafanye tathmini kuangalia namna iliyo bora ya kufikika kiurahisi, lakini pia kuwepo na hicho kituo ambacho kinawezesha muendelezo wa utalii. Naomba kuwasilisha.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA, Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Kuna mpango gani wa kuboresha miundombinu ya Hifadhi za Ibanda na Rumanyika zilizopo Wilaya ya Kyerwa ili kuvutia watalii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oliver Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna hifadhi nyingi ambazo tumeshazitangaza ikiwemo ya Ibanda, Rumanyika, pia Kyerwa. Nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa Mkakati wa Serikali ni kuhakikisha tuna zindua Phase II ya programu ya Royal Tour. Kwa hiyo, maeneo haya pia tutaweza kuyaingiza ili yaweze kuwa ni ya kimkakati katika kuhakikisha kwamba vivutio hivi tunavitangaza vizuri. (Makofi)
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; Mawaziri wale nane walikuja Mkoani Geita, kule Mbongwe kuna changamoto ya migogoro ya watu wenye uhifadhi, kuna Kijiji kimoja cha Sango, majuzi kimewekewa vigingi katikati ambapo kilishapata GN toka mwaka 1976. Je, Waziri, msimamo huu ukoje, maana wananchi mpaka sasa hivi wana hofu kulingana na kigingi kilichowekwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa amesema kumekuwa na wimbo la ukataji wa mkaa, lakini kuna utaratibu wa kisheria hawa wananchi huwa wanazifuata. Ila kuna hawa Askari Mgambo ambao pengine hawana mafunzo vizuri ya kusimamia hizi sheria; kumekuwa na mgongano pale wanapofanya hizi operation wanawakamata wananchi ambapo wanavibali tayari lakini wanaonekana kuwaumiza na kutowatendea haki. Je, ni nini kauli ya Mheshimiwa Waziri ili kusudi wananchi hao pale wanapofuata sheria zote wafanye shughuli zao vizuri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nicodemas Maganga, Mbunge wa Mbongwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli katika maeneo ya Mbongwe, baadhi ya vijiji vimeingizwa kwenye Kamati ya Mawaziri Nane na hivi ninayoongea tayari mikoa 13 imekwishatembelewa na maelekezo ya Serikali ni kwamba tunafanya tathmini na wataalam wako katika mikoa hiyo 13 wanafanya hizi tathmini, lakini pia kuona sasa namna ya maeneo ambayo yamehalalishwa kumegwa, yamegwe kwa ajili ya kuachia wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, kwamba kwa kuwa maeneo hayo yako ndani ya tathmini ambayo inasimamiwa na Kamati ya Mawaziri Nane wa kisekta, tutaendelea kutoa maelekezo kwamba wananchi wasibughudhiwe wakati tunasubiri majibu ya tathmini hiyo. Kwa hiyo, vigingi visiwafanye wananchi wasifanye shughuli zao za kila siku, na hao wahifadhi tunawaelekeza wasilete vurugu yoyote mpaka pale ambapo tathmini ya Mawaziri nane itakapokamilisha kazi zake.

Mheshimiwa Spika, kauli ya Serikali kwa hawa wananchi ambao wanakutana na changamoto ya kukabiliana na askari pamoja na wananchi. Niendelee kutoa rai kwa wananchi, kwamba tuendelee kufuata sheria, taratibu na kanuni zinazosimamia uvunaji wa mazao ya misitu.

Mheshimiwa Spika, tumekuwa na changamoto, tunatoa vibali tukiamini kwamba vibali hivi vitatumika ipasavyo, lakini tumekuwa na changamoto ya uanzishwaji wa usafirishaji wa mazao ya misitu kwa kutumia pikipiki. Pikipiki inapita inaenda inavuna mti ambao haujaruhusiwa na wanapita njia zao za uchochoro, wakikamatwa wanasema wameonewa. Tuwaombe wafuate utaratibu na vibali vitolee kwa usahihi, ndivyo hawatakutana na changamoto ya kukamatwana na mazao haya ya misitu.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Licha ya kupewa vibali na sheria ilivyo lakini hawa askari, wakiwakamata watu hasa wenye baiskeli wanaobeba mkaa wanaharibu hata vyombo vyao vya usafiri. Je, Serikali inataka kutuambia kwamba sheria inaelekeza hivyo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Askari wa Mazao ya Misitu wanapokuwa wanasimamia kwenye mageti, tuna changamoto kubwa sana ya usimamizi wa mazao haya. Ndani yake tuna askari wanaotoka kwenye halmashauri na kuna askari wanaotoka kwenye Wizara yetu ya Maliasili na Utalii. Kwa hiyo, kuna mkanganyiko hapa katikati ambao unajitokeza wakitaja maliasili, hata kama angekuwa ni Mgambo basi lawama inarudi Wizara ya Maliasili.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, niendelee kuwaomba wananchi, kwa kuwa tuna vyombo vya dola; pale ambapo unatendewa vivyo sivyo ripoti na taratibu za kisheria ziweze kuchukuliwa haraka.
MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, wafanyabiashara wengi hawa ambao walikuwa wanategemea kuuza nyamapori walishajenga mabucha kwa ajili ya kuuza nyamapori, kama ambavyo Serikali ilikuwa imewahamasisha. Mpaka sasa hivi vibali havijatolewa kwa muda mrefu na hasa kwa hawa wawindaji wa kawaida ambao wanalipa na leseni. Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba hawa wafanyabiashara wa nyama ya pori wanapata hivyo vibali ili waweze kufungua mabucha yale ambayo walishayajenga?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; hata pale nyama hiyo inapokuwa imepatikana kwa hao wachache ambao wanauza, bei yake inakuwa ni ghali sana, na wananchi wengi wa kawaida wangependa kula hii nyama ya porini. Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka mazingira mzuri kwa ajili ya kufanya hii nyama ya pori nayo iwe na bei ya kawaida ambapo kila mmoja anaweza kununua? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba tu niwatoe wasiwasi Watanzania na Mheshimiwa Mbunge kwamba vibali hivi vitatolewa baada ya mapitio ya Kanuni kukamilika. Tulikuwa na changamoto ya namna ya ugawaji wa vibali hivi kwa kuwa tuliweza kuanzisha makampuni ambayo tuliyakaribisha ili yaweze kuomba vibali vya uwindaji wa kienyeji. Lakini tumegundua changamoto inayojitokeza ni namna ambavyo tunaweza kuwanyima haki ya Kikatiba wananchi kuweza kupata kitoweo ambayo iko ndani ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tumepata maoni kutoka kwa wadau na sasa tumepitia Kanuni hizi, tunatarajia sasa kuzirejesha kwa maana tutoe ile haki ya wananchi, nao wawe na haki ya kuweza kupata kitoweo hiki.

Mheshimiwa Spika, kuhusu bei ya nyamapori, suala hili baada ya kuwa tumepitia Kanuni hizi na wananchi kuruhusiwa nao kuwinda uwindaji wa kienyeji, basi tunatarajia bei ya nyamapori kushuka kuliko ilivyo sasa ambapo tulikuwa tumependekeza makampuni pekee yaweze kuingia katika biashara hii. Ahsante.(Makofi)
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa kuna malalamiko mengi sana ya wananchi kwa ajili ya kuruhusiwa uwindaji wa kienyeji, kwa nini Serikali sasa isiharakishe huo mchakato wa mapitio ya Kanuni usiku na mchana ili wiki ijayo waweze kutoa hicho kibali?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba mchakato umeshakamilika na hivi sasa uko kwenye level ya Waziri, wakati wowote tutaweza kutoa mapendekezo au maelekezo ya utekelezaji wake.(Makofi)
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa Msitu wa Mpanda North East ulishapoteza hadhi ya uhifadhi kutokana na shughuli za kibinadamu, pamoja na Serikali yenyewe kuchangia kwa kugawa maeneo kuyafanyia shughuli za maendeleo ukiwemo Mji wa Mpanda pale Mpanda Mjini ni eneo la TFS, makazi ya Katumba na vijiji vilivyotajwa.

Je, ni lini Serikali itakuja kutatua huo mgogoro kumaliza mgogoro huo kwa kupitia timu ya Mawaziri wanane ambao Serikali ilielekeza?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa TFS imekuwa na tabia ya kuwapiga wananchi, kuwaibia mali zao kila wanapozalisha mali, kipindi cha uzalishaji mali hawaendi kuwapiga na kipindi cha uvunaji wanakwenda kuwanyang’anya mali zao. Ni lini tabia hii itakomeshwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kakoso, Mbunge wa Mpanda Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba pamoja na majibu ya msingi maeneo haya yaliingizwa kwenye timu ya Mawaziri wa kisekta nane ambao walikwenda kuchakata na pia wameweza kufika katika mikoa 13 kutoa maelekezo ya namna ya kutatua changamoto hizi za migogoro. Hivi ninavyoongea sasa kuna wataalam wako katika maeneo hayo ikiwemo Mpanda Vijijini ambako wataalam wamekwenda kufanya tathmini hiyo. Maeneo haya kama kweli yanakosa sifa ya kuwa hifadhi basi yataingizwa kwenye utatuzi wa migogoro ya Mawaziri nane na kisha yataingizwa kwenye ufutaji wa GN ambazo zipo tangu mwaka 1947.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa TFS kunyang’anya mazao, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kama kuna changamoto ya namna hii ambayo imejitokeza, basi naomba nilichukue, twende kulifanyia kazi na wananchi waweze kuendelea na shughuli zao za kila siku. Ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kunipa nafasi hii.

Kwa kuwa na sisi katika Kijiji cha Luhimbalilo, Kata ya Mputa, Wilaya ya Namtumbo kumekuwa na fukuto la mgogoro kati ya TFS na kijiji hicho kuhusiana na hifadhi ya Matogolo kuingilia eneo la Kijiji cha Luhimbalilo.

Je, Serikali inaweza kuelekeza sasa kikosi cha wataalam wakaja kufanya mazungumzo na kutafsiri hiyo mipaka ili kuondosha mgogoro huo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe tu kwamba migogoro yote ambayo inatuletea changamoto katika uhifadhi niwaombe Waheshimiwa Wabunge tuipokee ili tuweze kuleta wataalam waweze kufafanua mipaka na pale ambapo pana uhitaji wa namna ya kuachia maeneo kwenye maeneo ambayo yamevamiwa zaidi tutakaa chini, tufanye tathmini na kisha tuondokane na hii migogoro ya kila siku ili maeneo ambayo tumeyahifadhi basi yaendelee kuhifadhiwa vizuri kwa maslahi ya Taifa letu.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Waziri mlikuja kwenye Kijiji cha Handa Kata ya Lahoda pamoja na timu ya Mawaziri watano na wewe ukiwemo mlikutana na changamoto kubwa sana, kuhusiana na Hifadhi ya Swagaswaga na wananchi walieleza changamoto wanayoipata kutokana na hifadhi hiyo na mkaunda timu ya wataalam kwa ajili ya Kwenda kutafsiri mipaka.

Je, ni lini Serikali itakwenda kuwaeleza wananchi tafsiri ya mipaka hiyo kwa sababu bado wananchi wale wanapigwa, bado wananchi wale wananyang’anywa mazao yao, wanadhalilishwa; nataka kujua ni lini mtakwenda kutoa hayo majibu kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kunti, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya wataalam kufika katika maeneo hayo na kufanya tathmini niwaombe wananchi waendelee kusubiri maamuzi ya Serikali, wasiendelee kuvamia maeneo hayo na kujichukulia mamlaka ya kwamba tayari tumeyaachia. Ni mpaka pale Serikali itakapotoa tamko kwamba sasa tunaachia eneo hili, basi wananchi waendelee kufanya shughuli hizo.

Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge wasubiri kuwa tunachakata tutayaleta majibu.
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, huoni kwamba kuvua samaki usiku wakiwa wamelala unaweza ukavua samaki hata wale ambao hawajalengwa? Swali la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, ni lini Serikali itabadilisha au itafanya marekebisho ya kanuni ya mwaka 2020, kipengele cha 66(b)(b), 66(f)(f), 66(g)(g) na kipengele 128(1) ambacho kina faini ambayo haitekelezeki kwa wavuvi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maimuna Pathan, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nitoe ufafanuzi katika suala hili la kuvua samaki usiku. Kuvua samaki usiku kuna uwezekano wa samaki wale wadogo kuwa karibu zaidi ya kina 50 kuliko wale samaki wakubwa, lakini pia uvuvi wa kutumia ring net unasababisha kuchukua mazalia ya samaki pamoja na mayai ambayo yanaweza yakaondoa uvuvi endelevu katika mazalia ya samaki na hivyo kufanya maeneo haya yasiwe endelevu kiuchumi na kiuvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala la lini Serikali itabadili kanuni; mchakato wa kanuni hizi unaendelea, hivyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Bunge, muda ukifika zitakuja kwenye kamati husika na kanuni hizi zitafanyiwa marekebisho, ahsante.
MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, Serikali imefikia wapi katika kuwasaidia wavuvi ili waweze kupata vifaa vya kisasa na waweze kuvua uvuvi wenye tija?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa mwaka wa fedha 2022/2023 imetenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaa na zana bora za uvuvi, na kwa mwaka huu wa fedha tayari wavuvi wameshapata taarifa na wameshaanza kufanya maombi na zana hizi watakazopewa zitakuwa hazina riba, watapewa mikopo ambayo haina riba ili kufanya uvuvi uwe ni uvuvi endelevu na wa kisasa, ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, majibu ya Mheshimiwa Waziri kuhusiana na uvuvi wa mita 50 yanaenda kinyume kabisa na uhalisia katika maeneo yote ya ukanda wa pwani. Wavuvi wetu wa Mtwara, Lindi, Pwani, Kilwa, Tanga ni wavuvi wa kawaida ambao hawana uwezo wa kuvua kina cha mita 50 ambayo ni bahari kuu. Katika mabadiliko ya kanuni yanayokuja, Serikali iko tayari kuondoa kikwazo hiki cha uvuvi wa mita 50?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kassinge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tulipokee wazo lake na tutalifikisha kwa wataalamu, watalichakata na majibu yatatoka katika Bunge lako tukufu.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kanuni hizi ambazo zinaandaliwa, Ziwa Tanganyika tuna-share zaidi ya nchi moja, lakini nchi nyingine kwenye ziwa hilo hilo wanavua mchana. Hamuoni kama zuwio hilo linawapa umasikini wavuvi wa nchi yetu na mbadilishe ili waendelee kunufaika na Taifa letu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba Waheshimiwa Wabunge watambue kwamba rasilimali za uvuvi ni rasilimali za muhimu sana ambazo zinahitaji kuwa na uvuvi endelevu. Kwanza Serikali inafanya kuyalinda maeneo haya, kuyasimamia vizuri, lakini pia kuyahifadhi ili kuwepo na uvuvi endelevu. Hivyo tunavyoelekeza namna ya kutumia uvuvi wa kisasa na ni uvuvi endelevu kwa kuyafanya mazalia ya samaki yaendelee kuwa endelevu wananchi wanapaswa kufuata taratibu na sheria zilizopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na hii ina lengo la kuhakikisha kwamba, tunalinda maeneo haya ili tuwe na uvuvi endelevu, tunapoyamaliza haya mazalia ya samaki tutahakikisha uvuvi usiwepo kabisa hapa nchini. Kwa hiyo, tunaendelea kuwaomba wananchi waendelee kufuata sheria zilizopo ili kufanya uvuvi uwe uvuvi endelevu.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri tu lakini nina maswali madogo mawili kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili la Bondo katika Kata ya Mswaki ni eneo muhimu sana kwa ajili ya mvua, halikadhalika kwa ajili ya mazingira. Lakini eneo hili ni la Serikali na lina GN 341 toka 1960. Swali langu je, nini mpango madhubuti na endelevu wa Serikali wa kulinda maeneo haya ili yasiweze kuvamiwa na wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; moja ya ahadi ya wenzetu wa TFS juu ya eneo hili walikuwa wajenge Kituo cha Afya lakini naipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwamba tayari tumekuwa tukipata Milioni 500 Kituo cha Afya kwenye kijiji cha Mswaki kimejengwa. Je, nini kauli ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba wako tayari sasa kutujengea bwawa kwa ajili ya kitu kinaitwa CSR? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa jinsi ambavyo ametoa ushirikiano kwetu kuhakikisha kwamba eneo hii tunalirudisha Serikalini, wananchi ni kweli walikuwa wamevamia eneo hili lakini kwa kutambua umuhimu wa hifadhi basi tumeanza kuwatoa hawa wavamizi na kuweka vigingi ili maeneo haya yaweze kutambulika rasmi kama ni eneo la hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango madhubuti wa Serikali ni kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo ni mazuri na ya muhimu katika kuhifadhiwa vizuri tumeendelea kutoa elimu kwa wananchi, na kwa kutambua kwamba wananchi pia ni sehemu ya uhifadhi, hivyo tumekuwa tukishirikiana na wananchi kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo tunayatambua na ni ya muhimu tunayahifadhi vizuri kwa maslahi ya Taifa. Kwa hiyo nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge Serikali inaendelea kuhakikisha kwamba wananchi wanatambua umuhimu wa uhifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala lingine ambalo amelisema la Kituo cha Afya, ni kweli Serikali iliwahi kuahidi kuwajengea Kituo cha Afya katika Wilaya ya Kilindi katika Kijiji cha Mswaki na kwa bahati nzuri Serikali imetimiza ahadi hiyo. Kwa kuwa, tumekuwa tukitoa CSR katika maeneo mbalimbali ambayo yanazunguka maeneo yaliyohifadhiwa Mheshimiwa Mbunge nimuombe tulichukue ombi lake tuende tukachakate na hatimay tutampa majibu yaliyo sahihi lakini tuwahakikishie wananchi wa Kilindi na Mswaki kwamba tutahakikisha wanapata CSR kama moja ya wajibu wa Wizara ya Maliasili na Utalii. (Makofi)
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana; nimeyapokea majibu ya Serikali. Kwa kuwa kwenye jibu la msingi amesema Serikali inaruhusu shughuli za kiuchumi kuweza kufanyika kwenye eneo la misitu zikifuata sheria, lakini sheria hizi zimekuwa ngumu sana kwa wachimbahi wadogo hawa kuweza kuzi-meet ili waweze kupata hivi vibali. Je, serikali haioni haja sasa kuweza kupunguza masharti ya kutoa vibali vya kuingia ndani ya misitu ili wananchi wetu hawa waweze kupata vibali hivyo waweze kufanya shughuli zao za uchumi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Serikali imekuwa inaendesha zoezi la kuweka beacon katika mipaka kati ya vijiji pamoja na hifadhi. Zoezi hili limeweza kufanyika katika Kata za Mafyeko, Kambikatoto pamoja na Matwiga. Zoezi hili limeweza kufanyika bila kuwashirikisha wananchi wa maeneo husika.

Je Serikali haioni haja sasa kuweza kuweka bikon zile upya katika maeneo yale ya mipaka ya asili ili wananchi hawa waweze kufanya shughuli zao vizuri bila kuleta taharuki?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Masache N. Kasaka, Mbunge wa Lupa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza aliloliongelea Mheshimiwa Mbunge, kuhusu kupunguza masharti ili kuruhusu wachimbaji wadogowadogo waweze kuingia katika maeneo yaliyohifadhiwa. Nimtaarifu tu Mbunge kwamba, masharti haya tuliyoyaweka, yanazingatia pia kuhifadhi maeneo ya misitu na masharti haya kwa wachimbaji wadogowadogo tumeyaweka ni machache sana.

Mheshimiwa spika, kwa mfano, kwa ridhaa yako napenda tu nielezee kuhusu suala la masharti ya wachimbaji wadogowadogo ambao wanapaswa kupata leseni. Pia wanatakiwa kufanya Environmental Protection Plan (EPP), ambayo huwa haifanani na EIA, ni masharti madogo ambayo yanamfanya mchimbaji aweze kufuzu ili aweze kupata kibali cha kuingia kuchimba. Kwa hiyo sisi tunaona masharti haya ni nafuu sana na tunaendelea kuhamasisha wananchi kwamba tunapohifadhi ni kwa ajili ya uhifadi endelevu na wakati huo huo tunaruhusu shughuli za uchimbaji ndani ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili zoezi la beacon, nimfahamishe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tunapokuwa tunaweka mipaka, tunashirikisha pia Wizara ya Ardhi, ambapo wanakuwepo wapima ardhi ambao wanazisoma na kutafasiri ramani ambazo zinaonyesha ramani kamili ya hifadhi husika. Endapo kama kuna mgogoro uliojitokeza, basi nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge, kwamba tutawashirikisha tena Wizara ya Ardhi ili tujiridhishe na wananchi kwamba mipaka hii ni sahihi ama siyo sahihi. Kama itaonekana bikon zimewekwa nje ya mipaka hiyo, basi tutafanya marekebisho. Ahsante sana.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; ni kweli sheria inataka hivyo, lakini kwa kuwa shughuli za kibinadamu zinaendelea kama uvunaji wa mikaa na kuvuna miti katika misitu hiyo ya TFS, je, Serikali hawezi kuona sasa wakati umfefika wa ku-review sheria hiyo ili kwenda na wakati?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; tunaona hifadhi nyingi ambazo zinachomwa kwa makusudi katika utaratibu wa kuachia muda majani yaote. Je, Serikali haioni kwamba hata utaratibu huo pia umepitwa na wakati, wakati umefika sasa wa kuruhusu watu kuvuna majani ili kutoa suluhisho ya malisho ya ng’ombe ambao sasa hivi wanahangaika hasa katika maeneo ya wafugaji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent Kalogeris akiwakilishwa na Mheshimiwa Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nijibu haya maswali mawili kwa pamoja kwamba ni kwa nini tunafanya usafi kwenye maeneo ya hifadhi hususani kuchoma majani na Mheshimiwa Mbunge amesema badala ya kuchoma hayo majani basi yangetumika kwa ajili ya mifugo. Kiutaalam wa kiuhifadhi, wanashauri endapo kuna na mahitaji ndani ya hifadhi, ikiwemo mbolea, lakini pia kuna calcium ambayo wanaitumia wanyama pori, basi huwa kuna maeneo ambayo yameainishwa ambayo yanatengeneza hiyo calcium kwa kuchomwa jivu, ili wanyamapori waweze kupata calcium waendelee ku- survival kwenye maeneo yao ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo jivu hili huwa linatengeneza mbolea ili iweze kusaidia kuendelea kumea kwenye yale majani ambayo yanatumika kwa ajili ya malisho ya wanyamapori.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Kwanza naishukuru sana Serikali kwa namna ambayo kwa kweli wameweza kudhibiti moto uliokuwa unawaka ndani ya Mlima Kilimanjaro. Katika dhana hiyo hiyo ya kudhibiti, je, Serikali haioni iko haja ya kufanya mabadiliko ya sheria ili wananchi wanaozunguka Mlima Kilimanjaro waweze kupata service levy kama ilivyo kwenye maeneo mengine yenye mgodi ili kuongeza sense of ownership ya wananchi wanaozunguka kuona mlima ule ni mali yao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunapokea mawazo yake, lakini bado tunatambua kwamba wananchi wanaozunguka maeneo ya Mlima Kilimanjaro, ni sehemu ya hifadhi na mara nyingi tumekuwa tukihamasisha upandaji wa miti ili kulinda hifadhi hii ili iweze kutunzwa vizuri. Kwa hiyo, tunalipokea hili pia la sheria ili tuweze kuangalia utaratibu mwingine kuhakikisha mlima huu tunautunza vizuri.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; pamoja na uharibifu huo uliojitokeza wananchi hawa walihamishwa kwenye vitongoji vile kwa sababu ya uharibifu wa wale tembo. Mpaka sasa hivi wananchi wale wanaendelea kupata shida hakuna walicholipwa. Je, ni nini mpango wa Serikali angalau wa kuwapa fidia hawa wananchi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwenye Kata ya Businde, Kata ya Bugara pamoja Kikwechenkura, tembo wanaendelea kufanya uharibifu mkubwa, taarifa zinaendelea kutolewa lakini hakuna chochote ambacho Serikali inafanya. Je, ni nini mpango wa Serikali wa kudumu kuweza kuwahamisha wanyama hao waharibifu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nitoe pole kwa wananchi wote ambao wamekuwa wakikutwa na kadhia hii ya changamoto ya wanyama wakali na waharibifu. Serikali inatambua changamoto hizi na ndio maana tumeanza ujenzi wa vituo vya askari ili kusogeza huduma hii kwa ukaribu zaidi na wananchi waweze kutoa changamoto zao na huduma hii iweze kutolewa kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo tumeanza kufundisha vijana kwenye maeneo husika hususan vijana wa kwenye maeneo ya vijijini kama VGS ambao watashirikiana na askari kuhakikisha kwamba, wanyama wanaposogea katika maeneo ya shughuli za kibinadamu, basi iwe rahisi kuwaondoa.

Mheshimiwa Spika, nimwahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inachukua hatua na suala la kifuta machozi na kifuta jasho, tayari tumeshaanza kufanya tathmini na utekelezaji wake utafanyika hivi punde. Ahsante.
CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Wananchi 71 wa Kata ya Busindi, Kijiji cha Businde na Kitongoji cha Nyakabumbwe, pia katika Kijiji cha Nyakashenye, waliambiwa wapishe eneo lao kwa sababu ni ushoroba wa kupita tembo na waliahidiwa kupewa maeneo mengine, lakini hadi sasa pamoja na kupita katika mamlaka mbalimbali hawajapewa mahali popote. Je, ni lini Serikali itawapatia eneo la kuishi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna maeneo ambayo yamevamiwa na shughuli za kibinadamu ikiwemo hata ujenzi wa nyumba. Eneo la Kitengule ni eneo ambalo ni ranch ambapo sasa wananchi walipoyavamia yale maeneo tembo wakawa kama wako kwenye kisiwa. Moja ya tiba ambayo tulitaka kuifanya ni kufungua ule ushoroba ili tembo waweze kuruhusiwa ku-move kwenda kwenye Hifadhi ya Burigi Chato. Tulielimisha wananchi katika eneo hilo na utaratibu sasa wa kufungua hizi shoroba ni pamoja na wananchi kukubali kupisha zile shoroba.

Mheshimiwa Spika, tunafanya tathmini na tukishafikia muda ambao ni muafaka fedha na namna ya kuwahamisha wale tembo basi tutarudi kwa wananchi kuwafahamisha zoezi hili. Ahsante.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa nchi yetu Tanzania hivi sasa inakabiliwa na wimbi kubwa la ukataji na uchomaji moto wa misitu ya asili. Je, Wizara ina mkakati gani wa ufuatiliaji kuona mpango huu wa AFR 100 unakwenda kufanikiwa ili kukabiliana na tatizo la uharibifu wa misitu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa utekelezaji wa lengo la mpango huu linajumuisha nchi nzima pamoja na Zanzibar. Naomba tu kujua tumeishirikishaje Zanzibar ili kuona mpango huu tunautekeleza kinchi zaidi ili kuweza kukabiliana na tatizo la uharibu wa misitu kule Zanzibar? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Soud Mohammed Jummah, Mbunge wa Donge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa mhifadhi mzuri kwenye masuala haya ya misitu kwa sababu kwa asilimia kubwa amekuwa anatoa mchango mzuri sana kwenye eneo hili la uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, Serikali ina mikakati mingi na mikakati hii tayari ilishaanza kutekelezwa tangu mwaka 2018 ambapo Serikali iliingia mkataba na dunia. Mkakati huu ni wa kidunia lakini kwa Afrika tumeelekezwa kutekeleza jumla ya hekta milioni 100 kuziongoa ili ziingie kwenye uhifadhi. Tanzania ni moja ya nchi ambazo zimeingizwa katika mkakati huo ambapo jumla ya hekta milioni 5.2 tumeziwekea mkakati huo na malengo yetu ni kuhakikisha tunaziongoa.

Mheshimiwa Spika, mikakati hii imeendana sambamba na zoezi la uongoaji na urejeshaji wa maeneo ya hifadhi. Hivi karibuni utashuhudia ziara ya Mawaziri Nane wamekuwa wakitembea kila mikoa kuhakikisha kwamba maeneo yale ambayo yanastahili kurejeshwa, yarejeshwe ili tuweze kuingia kwenye mpango huu wa kidunia ambao tunaongoa jumla ya hekta milioni 350.

Mheshimiwa Spika, swali lake lingine ambalo ameuliza, je, Zanzibar ni miongoni mwa nchi ambazo ziko ndani ya mkakati huu. Zanzibar ni kweli ipo na kwa kuwa Zanzibar ni sehemu ya Muungano zoezi hili linafanyika kama Tanzania Bara na Zanzibar hivi karibuni kuna Mradi wa FAO ambao umeunganisha Zanzibar na Kigoma na tayari wanatekeleza katika maeneo mbalimbali ikiwemo kurudisha maeneo ya hifadhi ili kurejesha uoto wa asili.
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Spika, kwanza nawashukuru Wizara kwa majibu mazuri ambayo umeyatoa kulikana na utekelezaji wa kazi waliyoifanya. Nina swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa jukumu kubwa la Wizara ni kuhakikisha wanatoa elimu kwenye maeneo yanayopakana na kandokando ya hifadhi kama vijiji alivyovitaja, lakini kupitia taasisi yake, TAWA aliweza kutoa fedha kwa ajili ya kuanzisha Shule ya Sekondari katika Kijiji cha Nkuyu, Kata ya Nkuyu kwa kushirikiana na wananachi. Sasa Wizara iko tayari kukamilisha ile Sekondari?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Njalu Silanga, Mbunge wa Itilima kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tuliwahi kuweka mradi kwenye shule hiyo aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge na tukajenga madarasa manne; nimwahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaenda kumalizia yale maeneo ambayo yamebaki ili shule hii iweze kufanya kazi.
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, pamoja na Serikali kuwa tayari kuhamisha makundi hayo ya tumbili hao katika Kisiwa cha Juma, lakini bado kuna tatizo la mamba katika mialo yetu hasa mwalo wa Buyagu, Irunda pamoja na Rugongo.

Je, Serikali ipo tayari kutujengea vizimba kwa ajili ya kuondoa huo usumbufu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili ni kwamba tunalo eneo katika Wilaya ya Sengerema kule kwa mwenzangu Ndugu yangu Eric Shigongo tunaeneo la Kichangani ambalo linatumika kwa ajili ya uvuvi. Jimbo la Sengerema linapata samaki kutoka katika eneo hilo.

Je, Serikali iko tayari kutuachia lile eneo likaondoka katika game reserve kwa sababu linatoa usumbufu watu walioko pale wanalipa kama wako nchi nyingine?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tabasam Hamis Mwagao Mbunge wa Sengerema kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na tatizo la mamba na si sehemu ya Sengerema peke yake, ni maeneo mengi ambayo yana mito na maziwa na Serikali imeendelea kujenga vizimba vya mfano. Lakini tunaelekeza pia Serikali za Mitaa tushirikiane nao ili kuhakikisha maeneo haya tunayaimarisha vizuri na wananchi waweze kupata huduma bora ya maji na pia tutashirikiana na Wizara ya Maji ili kuona kwamba wananchi wanaweza kupata maeneo mazuri ya kuchota maji badala ya kutumia maeneo ambayo yanawanyama wakali na waharibifu hususani mamba.

Mheshimiwa Spika, swali lingine ameongelea kuhusu eneo la Kichangani; eneo hilo liko katikati ya pori ambapo ni hifadhi na tuliweza kuwaruhusu wavuvi waweze kulitumia kwa utaratibu maalum kwa sababu tunatunza mazalia ya samaki na uhifadhi mbalimbali, hivyo nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge na wananchi kwamba eneo hili liko purposely kwa ajili ya uhifadhi.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Serikali ambayo yatakwenda kuzua mgogoro mwingine; katika vijiji alivyovitaja hapo ni kijiji kimoja tu ambacho kipo kwenye Jimbo la Igalula. Kuna Kamati ya Mawaziri nane ilikuja kule na ikatoa maelekezo kuwa itaenda kugawa maeneo katika maeneo haya, lakini katika jibu lake wanasema hawaoni haja.

Je, Serikali haioni sasa kuweka kauli inayoeleweka kwa wananchi ili waweze kutoa mkanganyiko ambao unajitokeza?

Swali la pili, Jimbo la Igalula limezungukwa na vijiji vingi vyenye mgogoro kama huu hasa katika Kata ya Miswaki, Loya, Igudi, Mwamabondo na vijiji vingine. Je, Serikali haioni haja ya kwenda kupitia mipaka upya ili kila mwananchi ajue ni wapi anaishia na hifadhi inaishia wapi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Venant Daud Protas, Mbunge wa Igalula kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu kauli ya Serikali iweke kauli sahihi kuhusiana na vijiji vilivyotajwa; kuna mapori matatu yapo ndani katika Jimbo la Igalula, kuna Pori la Iwembele, Uyui, Kigwa, Lubuga, kuna Nyahua.

Mheshimiwa Spika, swali la Mheshimiwa Mbunge la msingi halikuhainisha ni vijiji gani hasa ambavyo analenga. Lakini nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba eneo la Igalula kwa maana ya Jimbo la Igalula kuna vijiji ambavyo vinaenda kunufaika na Kamati hii ya Mawaziri nane, kuna kijiji cha Miswaki, Igudi, Mwamdalaigwe, Loya na Mwamabondo, vijiji hivi vinatoka katika Jimbo la Igalula na vitaenda kunufaika na kumegewa kwa maamuzi ya Kamati ya Mawaziri nane.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuonesha mipaka, niwatoe wasiwasi Wabunge pamoja na Mbunge aliyeuliza swali kwamba kwa utaratibu tulionao sasa ni kuhakikisha kwamba yale mapori mapya ambayo tutayapa GN mpya tutaweza kushirikisha wananchi namna ya kutambua mipaka mipya na yale ambayo yatatangazwa na Serikali kwamba haya sasa ni mapori halali basi wananchi watafahamu mipaka yao ili iwe rahisi kutoingiliana tena na kuanzisha migogoro mipya.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Ardhi.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa namna alivyojibu swali la Mheshimiwa.

Mheshimiwa Spika, labda nijibu kwa ujumla kulingana na changamoto iliyokuwepo katika maeneo ambayo Mheshimiwa Rais ameridhia kati ya vijiji 975, vijiji 920 wamekubaliwa kubaki kwenye maeneo yao. Kitakachofanyika ili kuondoa hizi changamoto ni ushirikishaji wa wananchi katika maeneo watashirikishwa wote na wataalam wote watakuwepo na katika maeneo ambayo tumekwishapita tayari wapo ili kuweza kubaini mipaka kwa pamoja. Na hii inafanyika hivyo ili baadae kusijekutokea lawama pengine kwamba hawakushirikishwa katika kubainisha mipaka mipya.

Kwa hiyo, tunaimani maeneo ambayo Mheshimiwa Rais ameridhia na ameongeza hata pale ambapo alikuwa amesema kwamba wangeishia, imewapa pia fursa ya kuwa na maeneo ya akiba ya wao pia kuweza kuyawekea mpango wa matumizi ambao Serikali itafanya kwa kushirikiana na wao ili basi wasiendelee kuwa na ugomvi na hifadhi ambazo ziko zimetengwa kwa kazi maalum.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kushukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Swali langu ni moja tu la nyogeza. Je, ni lini malipo hayo yataanza kwa sababu yamechukua muda mrefu sana. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza Simon Mjika, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba maombi tayari tumeshayapata na Serikali imeanza kuyahakiki na kabla ya kuisha mwaka huu wa fedha 2022 wananchi hawa watakuwa tayari wameshalipwa.
MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza suala la kuvunja sheria hapa halipo kwa sababu tayari hawa wananchi wameshashinda kesi mahakamani na Mahakama ikawapa ushindi na ikaamuru mifugo yao warejeshewe.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; Waziri wa Maliasili na Utalii wakati anahitimisha bajeti yake alisema mifugo hiyo itarudishwa mara moja; na Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokutana na kikao cha wafugaji wote nchini aliagiza mifugo hiyo wairejeshwe lakini sasa hivi…

SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa Mpina ulishatoa maelezo marefu sana.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, swali ninaloliuliza hapa orodha ipo Wizarani na Waziri anayo orodha kwa nini anakwepa hapa kuwalipa hao wafugaji wanyonge ambao wameshashinda kesi mahakamani na kutudanganya hapa kwamba hiyo orodha hana?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina, Mbunge wa Kisesa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi ni kwamba mpaka sasa hatujapata orodha ya wafugaji ambao wanalalamika hawajarejeshewa mifugo yao. Kama ambavyo nimeeleza kwamba kesi inapopelekwa mahakamani sisi tunapeleka vielelezo tu lakini kesi inabaki kuwa ni chini ya hakimu, DPP na sisi tunakuwa kama mashahidi, kwamba tumekamata mifugo hii, baada yah apo hakimu ndio anayetoa hukumu. Aidha, hukumu inakuwa ni kurejeshewa hiyo mifugo kwa faini au mifugo kutaifishwa.

Nimesema endapo kama kuna mfugaji ambaye ana kesi ambayo inatudai sisi Wizara ya Maliasili na Utalii basi waje wizarani tutakaa pamoja tuichambue hiyo kesi na tutaweza kutekeleza kama Serikali.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Swali langu pale Makete tuna pori la Mpanga Kipengele ambalo linazunguka vijiji vya Ibaga, Ikovo, Kiimani na Kigala. Pori hili limegeuka ni mwiba kwa wananchi wa Makete kwa sababu mifugo yao imekuwa ikiingia na watu wanakamata lakini bikoni zimewekwa kwenye maeneo ya wananchi; na nililalamika hapa Bungeni na ukaniahidi Mheshimiwa Waziri utakuja.

Je, ni lini Serikali itekwenda kuweka bikoni ili wananchi wangu wawe salama katika eneo hili?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tulikuwa kwenye ziara ya Mawaziri nane ambao wanatatua changamoto hizi za migogoro ya ardhi.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu kwamba nitafika kama sio mimi basi ni Mheshimiwa Waziri kuhakikisha kwamba tunafafanua wapi mipaka ilipo ili wananchi waweze kuielewa na hatimaye tuendelee kushirikiana kulinda maeneo ya hifadhi.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa vile Serikali inasema itawarudishia ng’ombe wao je, itakaporudisha itawalipa na fidia?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu Mbunge wa Simiyu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nifafanue hapa nimesema hapa kwamba tunapokamata mifugo kesi zao tunazipeleka Mahakamani hukumu inakuwa kati ya Hakimu na sisi tunasimama pale kama mashahidi tu ambao tunaonyesha vielelezo. Kwa hiyo suala la kwamba tutarejesha mifugo ni pale ambapo Serikali itajiridhisha kwamba hawa wahalifu watakaoingiza mifugo yao kwenye hifadhi wanastahili kurejeshewa hiyo mifugo na tunapopeleka kesi Mahakamani tunakabidhi vielelezo vyote, kwa hiyo sisi hatukai na mifugo. Ahsante.
MHE. RASHID ABDALLA RASHID: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina swali la nyongeza. Ni kweli vikundi vimepatiwa mafunzo haya na vinapatiwa tunzo, lakini ni lini vitapatiwa fedha ili ziweze kuwasaidia katika shughuli zao badala ya kukaa na mafunzo kwa takribani miaka miwili bila kupata fedha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Abdalla Rashid, Mbunge wa Kiwani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali tayari imeshafanya mafunzo kwa vikundi hivi vya uhifadhi wa mazingira na tayari tumeshafanya uwezeshaji wa wataalam, hivyo Serikali sasa kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakishirikiana na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais, Zanzibar watafanya uwezeshaji wa vikundi hivi ili viweze kutekeleza miradi hii.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Nimesikia majibu ya msingi ya swali hili. Kwanza naomba kabisa kabla sijauliza swali; Mheshimiwa Waziri tunaomba ufanye ziara kwenye vijiji vyetu ili hayo matamko ambayo wewe unayatoa hapa uweze kuwaambia wananchi wenyewe wasikie kama sehemu ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu: Je, ni lini Serikali itavimegea nafasi za kulima wananchi wa Itumbula, Ivuna, Mlomba, Itelefya pamoja na maeneo mengine yote ambayo yapo ndani ya Jimbo la Momba ambayo yanahitaji kumegwa kupata maeneo ya kulima kwa sababu maeneo yao yote yamezungukwa na hifadhi na maeneo hayo wananchi wenyewe walitoa kwa Serikali kwa ajili ya kulinda misitu; na sasa hivi wamezaliana? Wataenda wapi ili waweze kulima na kuendeleza shughuli zao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Condester, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya Wizara ya Maliasili na Utalii ni kulinda meneo yaliyohifadhiwa. Kama kuna ombi la wananchi kumegewa, basi walete maombi hayo yataangaliwa, lakini pia na sisi tutaangalia kama maeneo hayo yana vyanzo vya maji, yana shughuli ambazo zinapaswa kuhifadhiwa vizuri, basi tutawataarifu wananchi namna iliyo bora.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshiniwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kituo cha Doroto ambacho kimetajwa kwenye majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ni kituo kikubwa ambacho kinasimamia Game Reserve ya Muhesi lakini hakina gari: Je, Serikali ipo tayari sasa kupeleka gari jipya kabisa katika kituo hiki?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: kuna wananchi ambao walifariki kutokana na wanyama hao wakali katika Kijiji cha Nyabutwa katika Kata ya Mgandu na maeneo mengine mazao ya watu yaliliwa: Je, ni lini Serikali itawalipa kifuta jasho na kifuta machozi kwa ajili ya kuwafariji wananchi hao kutokana na matukio hayo ya wanyama wakali?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahaya Omari Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeshapokea magari 59 ambayo yatasambazwa kwenye vituo vilivyo na athari ya wanyamapori wakali na waharibifu, hivyo nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba priority itapelekwa katika Kituo hiki cha Doroto.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili lingine la kifuta machozi na kifuta jasho, tulikuwa na changamoto kidogo ya fedha na kufanya tathmini na tayari tumeshakamilisha. Hivyo, wakati wowote tutaanza kulipa wathirika wa changamoto hii. (Makofi)
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza kabisa napenda niipongeze Serikali na kuishukuru kwa sababu Bunge lililopita nilieleza kadhia ya tembo ambao wanawaua watu, kula mazao na kuleta uharibifu mkubwa. Naishukuru Serikali kwa kuniletea kile kituo na sasa hivi kituo kimekamilika zaidi ya asilimia 95.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, niliomba gari na askari. Gari bado sijapata na maaskari bado sijapata, lakini kitu cha kusikitisha, tarehe 6 Novemba, 2022 mwananchi wangu aitwaye Mwanahawa Mohamed Likenge ameuawa na tembo katika eneo la Lucheme Kitongoji cha Ndulima na tarehe 7 Novemba 2022 amezikwa. Sasa kwa kuwa Askari ni wachache, naomba niongezewe Askari ili waweze kufanya patrol kuhakikisha wananchi hawa wanapata manusra na hatimaye tujue hatma yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete, Mbunge wa Lindi Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nitoe pole kwa mwananchi huyu ambaye tulipata taarifa ndani ya siku tatu kwamba ameuawa na wanyama wakali na waharibifu. Namwomba tu Mheshimiwa Mbunge kwamba maombi yake yote tutayatekeleza kwa wakati; na kwa kuwa tayari tumeshapata magari, basi tutayaelekeza katika eneo hilo na maeneo mengine yenye changamoto hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo tumeshaanza ku-train VGS, hawa Askari wa Vijiji na tayari vijiji tisa tumeshamaliza kuwafanyia mafunzo na hawa wote watapelekwa kwenye maeneo ambayo yana changamoto hii. Tutaongeza askari katika maeneo yenye changamoto na nguvu ili kuhakikisha kwamba tunathibiti wanyama wakali na waharibifu. (Makofi)
MHE. ANGELINA A. MALEMBEKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Halmashauri ya Manyoni ilitangaza nafasi au fursa ya kuwekeza kwenye Halmashauri yake hususan kwenye zao la korosho, lakini yale maeneo waliyoyapanga ndiyo njia kuu ya kupita tembo. Kwa hiyo, ukipanda, wakipita wanavunja, wakirudi tena wanakula yale majani. sasa nataka kujua Wizara hii lini itawasiliana na Halmashauri ya Manyoni ili wale ambao wamepata mashamba kwenye eneo lile ambalo ni njia ya tembo waweze kubadilishiwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwa na changamoto ya uvamizi wa wanyama wakali na waharibifu katika mashamba ya uwekezaji yaliyoko Manyoni. Tayari tumeshaanza kuimarisha doria kwa kuanzisha usimamizi wa doria kuzunguka mashamba hayo na tuna mpango sasa wa kuweka kituo ambacho kitakuwa ni kituo cha kudumu kwa ajili ya kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mepesi ya Serikali naomba nitoe ushauri mmoja lakini pia niwe na swali moja la nyongeza. Kwanza tuwaombe Wizara ya Maliasili, pamoja na dhamana kubwa waliyopewa ya kulinda maliasili za Taifa letu, lakini wajue wana wajibu pia wa kuruhusu Watanzania wahudumiwe bila wao kuwa kikwazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, eneo la Hifadhi ya Msitu Kihesa, Kilolo ni eneo ambalo limepitia mchakato mkubwa mpaka kutengwa kwa ajili ya kujenga Kituo cha Utalii Kusini. Nilikuwa nataka kuuliza, maana swali hili tunaliuliza tangu Januari, 2021 na tunapata majibu yasiyokuwa straight; naomba leo Mheshimiwa Naibu Waziri atuhakikishie hapa: Ni lini hasa ujenzi wa Kituo cha Utalii Kusini Kihesa, Kilolo utaanza chini ya mradi wa REGROW kwa sababu miradi mingine yote ya REGROW inaendelea na imeanza, kasoro Kituo cha Utalii Kusini cha Kihesa, Kilolo.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jesca Jonathani Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Jesca kwa namna ambavyo anaendelea kufuatilia mradi huu wa ujenzi wa Kituo cha Information Center ambacho kitasaidia upatikanaji wa ofisi mbalimbali na pia kuwezesha masuala ya utalii ili yaweze kuendelea vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba natambua kwamba wananchi wa Iringa wana hamu kubwa sana ya ujenzi wa jengo hili ambalo linatarajiwa kujengwa ghorofa tano pamoja na jengo lingine la Kituo cha Utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba ujenzi huu unatarajiwa kuanza mwezi Mei na sasa hivi tulikuwa tuna mkandarasi ambaye alikuwa anaangalia michoro, na michoro tayari imeshakamilika, na kulikuwa kuna marekebisho kidogo na utaratibu sasa wa kumpata mkandarasi kwa ajili ya ujenzi umeshaanza. Hivi ninavyoongea, tunatarajia kumpata na mwezi wa Tano ujenzi unaanza. Pia nimhakikishie kwamba tuko ndani ya muda, na ujenzi huu unatarajiwa kukamilika mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine amesema ni ushauri, tunaupokea lakini nataka nimkumbushe tu kwamba utaratibu wa utoaji wa vibali kwenye maeneo ya misitu ambapo unatarajiwa miti kukatwa, unategemea hasa hasa mteja anayetarajia kupitisha nguzo za umeme awe amekamilisha kulipa tozo zote zinazotakiwa.

Mheshmiwa Mwenyekiti, misitu hii inasimamiwa na Serikali Kuu kupitia Wakala za Huduma za Misitu Tanzania, lakini kuna misitu mingine inasimamiwa na Halmashauri na mingine ni misitu ya vijiji. Kwa misitu ya Halmashauri na Vijiji, tuna kamati za uvunaji ambazo zinasimamiwa, ziko chini ya Wilaya. Kamati hizo pia zinatoa vibali baada ya kuwa mteja amekamilisha taratibu zote za ulipaji wa tozo. Tozo hizi zinasimamiwa na Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri amelieleza Bunge lako Tukufu hapa kwamba hamna ucheleweshaji wa kutoa vibali vya kupitisha umeme kwenda vijijini. Sasa nataka kujua, Wizara ya Nishati ilikuja kwenye Kamati ya Bajeti, wakaeleza kwamba moja ya kikwazo kikubwa cha kuchelewesha kupeleka umeme vijijini ni kuzuiwa au kucheleweshwa kwa vibali na TFS. Leo Mheshimiwa Waziri anaeleza kwamba hakuna huo ucheleweshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua katika hizi Wizara mbili ambazo ni za Serikalini, ni yupi anaongea uongo katika kuhakikisha kwamba umeme unafika vijijini kwa wananchi? [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MWENYEKITI: Mheshimiwa Matiko hilo neno la uongo naomba uliondoe.

MBUNGE FULANI: Uongo!

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujua Wizara ya Nishati na Wizara ya Maliasili na Utalii ni Wizara ambazo ziko ndani ya Serikali...

MWENYEKITI: Imeshaeleweka, ipi ipo sahihi?

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naondoa “uongo”, sasa nanyoosha vizuri swali.

MWENYEKITI: Eeeh, ndiyo.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mnaliambia nini Bunge na wananchi kinachochelewesha umeme kwenda vijijini wakati nyie ni Wizara mbili ambazo mpo ndani ya Serikali, siyo kwamba ni kutoka hata kwenye sekta binafsi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII, Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kusema Wizara zote mbili; ya Nishati na ya Maliasili na Utalii zimesema ukweli. Nataka nimhakikishie tu kwamba Wizara hizi zinafanya kazi kwa ushirikiano. Kabla Wizara ya Nishati haijatekeleza miradi yake, ni lazima mteja awe amekamilisha taratibu zote ikiwemo malipo ya tozo. Kama hajalipa tozo, basi vibali hawezi kuvipata kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nataka niliseme hili wazi kwamba wateja wengi wanasingizia kwamba vibali vinacheleweshwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, lakini ili nikupe kibali, ni lazima uwe umetekeleza masharti yote ikiwemo ulipaji wa tozo. Sasa kama tozo umeshamaliza kulipa, kwa nini mimi nikunyime kibali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndivyo utaratibu unavyotakiwa na wateja wengi wanataka tusamehe ulipaji wa tozo. Kwa hiyo, kama mteja anahitaji kusamehewa tozo, basi awasilishe kwenye mamlaka husika ambayo ni Wizara ya Fedha, na Waziri mwenye dhamana ataangalia kama kuna haja ya kutoa msamaha, ahsante. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Mheshimiwa Kunambi, swali lake hapa linauliza ni lini Serikali itatatua mgogoro huu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; ili kupunguza migogoro na kuimarisha sense of ownership kati ya Mlima Kilimanjaro na Vijiji vya Foo, Mkuu, Ndoo, Kilanya, Sawe, Ng’uni na kule Kieli, Serikali ilituahidi kutuletea fedha za CSR ili tujenge madarasa; nawe Mheshimiwa Naibu Waziri uliahidi hapa Bungeni kwamba mtatupa fedha hizo: Je, ni lini Serikali itatuletea fedha hizo za CSR? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Saashisha kwa niaba ya Mheshimiwa Godwin Emmanuel Kunambi, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nifafanue kwenye suala la lini Serikali itatatua mgogoro? Kwenye jibu langu la msingi nimeeleza kwamba, kwa sasa hivi Kamati ya Mawaziri nane imeshapita maeneo takribani yote hapa nchini, na imeacha kila mkoa kamati inayofanya tathmini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya maeneo tayari uthamini umeshaanza, lakini kuna maeneo ambayo tayari wananchi walikuwa wameshavamia kwenye maeneo kama hilo la kilombero. Tunafanya tathmini kuangalia eneo lipi ambalo litakuwa ni la muhimu kuokoa kile kiini ambacho kitatunza haya maji kwa ajili ya kuyapeleka katika Bwawa la Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tathmini hii iko uwandani inafanyika na inashirikisha wananchi wa Mlimba hatua kwa hatua ili kuangalia nini kilicho sahihi ili kusije kukaleta mkanganyiko tena kwamba kamati hii haikushirikisha wananchi. Kwa hiyo, ni lini? Ni pale ambapo tu kamati hii itakapokamilisha uthamini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la CSR, naomba tu tena niendelee kuelekeza TANAPA; nakumbuka tulifanya ziara na Mheshimiwa Saashisha katika maeneo ya hai, lakini tukaangalia, kweli kulikuwa kuna uhitaji wa wananchi katika eneo hilo ambalo wanatakiwa wapate CSR.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nielekeze TANAPA tukamilishe ahadi hii kwa wananchi ili tuweze kuwa na ushirikiano mzuri na wananchi waweze kuwa ni sehemu ya uhifadhi kwa ajili ya kizazi cha sasa na cha baadaye, ahsante.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nataka nimwulize Mheshimiwa Waziri kwamba ni lini Serikali itakuja kutatua mgogoro uliopo katika Halmashauri ya Ushetu pamoja na Kariwa ambao unazidi kuchukua sura mpya na sasa mpaka wananchi wangu zaidi ya 17 wamekamatwa na kuwekwa ndani bila sababu zozote za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nipate majibu ya Serikali.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cherehani, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nampa pole Mheshimiwa Mbunge, na pia nawaomba wananchi wa Ushetu wawe na subira. Tulipanga kwenda kufanya mazungumzo na wananchi, lakini ratiba zikaingiliana. Nawaomba wananchi wa Ushetu wawe wavumilivu, baada ya Bunge hili, tutaondoka na Mbunge wao kwenda kuzungumza na kutatua changamoto hii, ahsante. (Makofi)
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Kumekuwa na mgogoro wa muda mrefu kati ya Hifadhi ya Tarangire na Vijiji vya Olasiti, Kakoyi na Vilima Vitatu.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kumaliza kabisa ule mgogoro wa eneo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Regina, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imejipanga kupunguza ama kumaliza kabisa migogoro iliyopo baina ya hifadhi zinazozunguka maeneo ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hili nimuahidi kwamba kupitia Kamati ya Mawaziri nane lakini pia kwenye migogoro mipya inayokuja tumejipanga kuitatua bila kuleta taharuki kwa wananchi. Kwa hiyo, nitaenda na nitashirikiana na wataalam kuangalia wapi penye marekebisho na tutazungumza na wananchi tutaitatua hii changamoto.
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Moja; kwa kuwa kiwango wanacholipwa wakulima walioharibiwa mazao na wanyama ni kidogo sana.

Je, Serikali ina mpango gani wa kubadili sheria, ili kuweza kuwalipa wananchi kulingana na thamani ya mali zao zinazoharibiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa, pamekuwa pakitokea matukio haya ya tembo mara kwa mara katika maeneo hayo hususan Kijiji cha Chemchem, ni lini Serikali sasa itatujengea kituo cha Askari wa Hifadhi, ili kuweza kuzuia athari zaidi katika mzao ya wananchi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza mawili, ya Mheshimiwa Ally Makoa, Mbunge wa Kondoa Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wananchi wamekuwa wakilipwa kiwango kidogo. Na kiwango hiki cha kifuta machozi ama kifuta jasho ni ile tu kutoa pole kwa wananchi na kuweka mazingira ya ushirikiano baina ya uhifadhi na wananchi, lakini tulipata maelekezo katika Bunge lako hili Tukufu wakati wa bajeti kwamba, tupitie kanuni za sheria hizi na tayari Wizara imeshaanza kuzipitia kwa ajili ya kurejea upya kanuni hizi, ili kifutajasho basi kiweze kuongezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ninamuahidi Mheshimiwa Mbunge wa Kondoa Mjini, Mheshimiwa Ally Makoa kwamba, katika bajeti hii ya 2022/2023 tumeoanga kujenga vituo 13, vituo hivi vitapelekwa katika Jimbo lake ili tuweze kupeleka Askari waweze kuendelea na zoezi la kuzuia wanyamapori wakali na waharibifu.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Waziri umeshafika kwenye Jimbo langu ndani ya Kata ya Maore, umeona ni kiasi gani wananchi wangu wanauawa na kuharibiwa mazao yao. Je, huoni umuhimu sasa kujenga kituo pale ndani ya Kata ya Maore ili uepushe maisha ya wananchi wangu na hatari? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mama Anne Kilango, Mbunge wa Same, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nilifika katika eneo hilo la Maore na kuna changamoto kubwa sana ya wanyama wakali na waharibifu. Tuliahidi kujenga bwawa lakini pia tutapeleka kituo ambacho kitasaidia hawa wananchi kupunguza adha hii ya wanyama wakali na waharibifu. (Makofi)
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu ya Serikali lakini bado nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Msitu wa Mbiwe ilianza rasmi mwaka 1995, wakati shughuli za kibinadamu za kiuchumi katika mamlaka ya Mji Mdogo Makongolosi hasa kilimo zilikuwa zinafanyika: -

Je, Serikali haioni haja sasa kwa kipindi hiki kuweza kuweka utaratibu maalum kama ilivyofanya kwenye uchimbaji wa madini ili na hawa wananchi wanaoshughulika na shughuli za kilimo waweze kufuata hizo taratibu waweze kufanya shughuli zao za kilimo kwenye maeneo yanayofaa kwa kilimo?

Swali la pili, Wilaya ya Chunya imekuwa muhanga wa kupokea wahamiaji wengi waliotoka maeneo mbalimbali walikofukuzwa huko hasa maeneo ya Usangu pamoja na Wilaya ya Songwe: -

Je, Serikali haioni haja sasa kuweza kuona utaratibu maalum hawa wananchi ambao wametoka kwenye maeneo hayo, wanafika Wilaya ya Chunya na kuharibu mazingira hasa na mifugo yao kuweza kuingia kwenye maeneo ya mashamba kuweza kutoa tamko rasmi ili wananchi wetu wale wasiweze kuathirika na mifugo hiyo inayoingia ndani ya Wilaya ya Chunya.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Masanche Njeru Kasaka Mbunge wa Rupa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu utaratibu wa kuruhusu shughuli za kilimo ndani ya hifadhi, taratibu na kanuni zinaelekeza kwenye uapnde wa misitu ya TFS kwamba kunapokuwa na uchimbaji wa madini basi wale wachimbaji wanaruhusiwa kuchimba na wakati huohuo kurudishia miti ili kuendelea kuhifadhi maeneo hayo. Kwa hiyo, sheria na taratibu zinazoongozwa na Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania ni kwamba hairuhusiwi kufanya shughuli za kilimo isipokuwa uchimbaji wa madini, ambalo ni eneo maalumu lililo ndani ya hifadhi ya misitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu wahamiaji, binadamu au wananchi kulingana na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania haimzuii mwananchi yoyote kuishi eneo lolote analohitaji. Katiba inaruhusu mtu yoyote kuishi pale ambapo anaona panafaa, isipokuwa kwa wale ambao wanavamia maeneo ya hifadhi sheria na taratibu zitafuatwa ikiwemo kuwakamata na kuwachukulia hatua za kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo nawaomba wananchi waheshimu maeneo ya hifadhi kwa mustakabali wa Taifa letu na kwa faida ya wananchi wenyewe.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa vijiji vya Twentela, Mbalwa, Ntungwa, Mbawo, Moraviani na Itumbula wamezungukwa na hifadhi, hapo nyuma wananchi hao wenyewe kwa ridhaa yao walitoa maeneo hayo ya hifadhi ambayo yalikuwa ni ya kwao.

Je, Serikali haioni ipo haja ya kumega kipande kidogo tu cha hifadhi kuwasaidia wananchi hawa wapate eneo la kulima kwa sababu wamezaliana na hawana sehemu nyingine ya kwenda kwa ajili kuendesha shughuli zao, lakini kwa kufuata utaratibu na kutoa elimu bila kuathiri sheria zetu. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Condester kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali hili pia aliwahi kuuliza Mheshimiwa Mbunge na taratibu nilimwelekeza kwamba, maombi yanatakiwa yaletwe na sisi tutaangalia tathmini, kama kuna umuhimu wa kumega eneo hilo basi tutapeleka mapendekezo kwa Mheshimiwa Rais, lakini pale ambapo tutaona kuna haja ya kutunza vyanzo vya maji basi wananchi wataelimishwa na maeneo haya tutayahifadhi kwa ajili ya kizazi hiki na kinachokuja.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunatangaza Hifadhi ya Nyerere, National Park tayari kuna maeneo ya WMA, mfano kama Wma ya Magingo katika vijiji vya Mpigamiti, Barikiwa na Mlembwe tayari vimechukuliwa na TANAPA.

Je, ni lini Serikali itakuja kuhakiki hiyo mipaka ili yale maeneo yaliyokuwa yamehifadhiwa na vijiji yaendelee kuwa yanahifadhiwa na vijiji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu wananchi wa Liwale niwaahidi kwamba kwa kuwa taratibu za kuainisha mipaka ni kazi inayoshirikisha Wizara ya Ardhi pamoja na Wizara ya Maliasili na Utalii, tutaenda kuhakiki hiyo mipaka ili kuruhusu wananchi watambue maeneo yao na kisha yaendelee kuhifadhiwa vizuri.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itamaliza mgogogro wa mpaka kati ya TANAPA na wananchi wa Momela ambao unatokana na TANAPA kutwaa mashamba Namba 40 na Namba 41 bila kushirikisha Serikali ya Kijiji.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Pallangyo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuahidi Mbunge tutaenda kuzungumza na wananchi nikishirikiana na wataalamu tupate maelezo ya kutosha.

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa shughuli zote zilizotajwa ambazo zimeanza kufanyika ndani ya Pori la Akiba la Mabwepande, tayari wananchi wengi hawajui na hata wananchi wa Jimbo la Kibamba pia hawajui;

(a) Je, Serikali ipo tayari kufungua geti upande wa Jimbo la Kibamba ili wananchi wengi sana waweze kushiriki kwenye shughuli zilizotajwa kwenye jibu la msingi?

(b) Kwa kuwa katika kila uwekezaji tunategemea mapato na seerikali imejibu hapa imeshatumia shilingi 710,789,122. Je, ni yapi makadirio ya mapato katika mwaka 2022/2023?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Issa Mtemvu Mbunge wa Kibamba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, pori hili la Mabwepande ni pori ambalo limepekena na Mikoa jirani ikiwemo Pwani na pori hili lipo katikati ya Dar es salaam, kwa sasa tumeshaanza kufanya hamasa mbalimbali na kwa kuwa mwanzoni tulikuwa hatuna miundombinu tumeweza sasa kuwekeza na sasa hivi tuna miundombinu ya kutosha na hivyo watalii wameshaanza kuingia na matamasha mbalimbali yameshaanza kufanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshaanza pia kutumia mitandao ya kijamii kuhamasisha wananchi, pia tunatumia televisioni matamasha mbalimbali kama ambavyo nimeyataja ikiwemo nyama choma festival hii yote ni kuwafanya wana Dar es salaam wawe na maeneo maalum ya kupumzika ikiwemo kulala ambapo tumeshaandaa maeneo ya camp site kwa ajili ya wananchi kulala.

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kuhamasisha Watanzania wote unapofika Dar es Salaam basi tembelea Pori la Pande utapata huduma zote za kiutalii na utaweza kuwa umepumzika kama vile upo Serengeti National Park.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa mapato tangu tulipowekeza katika pori hili kwa sasa tumesha kusanya jumla ya shilingi milioni 4.9 na kwa kuwa uwekezaji ni endelevu tunaendelea kuwekeza ili kuhakikisha kwamba eneo hili linakuwa ni kivutio kikubwa katika mkoa wa Dar es Salaam. (Makofi)
MHE. VINCENT P. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Nina swali moja;

Kwa kuwa robo tatu ya Pori Tengefu la Lwafi la Wilayani Nkasi halina wanyama na wananchi wameshaingia wanafanya shughuli zao za kiuchumi; na mipaka hiyo tangu 1948 kipindi cha ukoloni iliwekwa, lakini baadaye ikaja ikabadilishwa ikasogezwa kwa wananchi.

Je, Mhesimiwa Waziri haoni kuwa ni kukwamisha juhudi za wananchi wa Wilaya ya Nkasi wanaojitafutia riziki zao?

Je, ni lini tutakuja kupitia upya ili mipaka irekebishwe, wananchi wameongezeka ili wapate maeneo ya kulima? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vicent Mbogo, Mbunge wa Nkasi, akiwakilishwa na Mbunge wa Nkasi Kaskazini Aida Khenani, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka tu nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Wilaya ya Nkasi haina uhaba wa maeneo, isipokuwa kuna changamoto ya mtawanyiko. Wananchi wanaishi pale ambapo wanahitaji kukaa, kitu ambacho tunaipa mzigo Serikali kupeleka huduma kwa wananchi tukiendelea kuwaruhusu waendelee kutokomea kwenye maeneo ya hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachoelekeza Serikali ni kwamba wananchi wapangwe kwa kuangalia matumizi bora ya ardhi ili kuwepo na miundombinu inayowezesha huduma bora za wananchi ziweze kuwafikia wananchi. Hili swali analolisema kwamba robo tatu ya Lwafi haina wanyama. Ili eneo lihifadhiwe vizuri na ili liwe na madhari nzuri ni pale tu ambapo litaachana na shughuli za kibinadamu. Ndiyo maana yale maeneo ambayo tunayatunza vizuri wanyama huwa wanarudi taratibu na uhifadhi unakuwa ni endelevu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nataka niwaambie tu wananchi wa Nkasi kwamba maeneo ambayo tunayahifadhi mengine tunayachukua yakiwa hayastahili kuwa hifadhi; lakini yanapotunzwa kwa muda mrefu uoto wa asili unarudi, madhari inarudi na wananyama wanaanza kurudi. Kwa maana nyingine wanyama wanatoweka baada ya shughuli za kibinadamu kuingilia maeneo ya hifadhi. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa sababu kwa sasa kuna migogoro mingi inayoendelea nchini ambayo inapelekea mpaka mauaji kwenye maeneo ya hifadhi na wananchi;

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kupitia upya sheria za uhifadhi ili ziweze kuendana na nyakati za sasa na kupunguza migongano kati ya wananchi na wahifadhi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na changamoto hizi Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati John Pombe Magufuli aliunda Kamati ya Mawaziri nane ambao walipita nchi nzima. Na utekelezaji wake ni kama ambavyo umeona, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imetekeleza kwa kwenda kijiji kwa kijiji, kata kwa kata, wilaya kwa wilaya, kutoa ufafanuzi. Yale maeneo ambayo yameonekana wananchi wanaweza kuachiwa; tumeachia jumla ya vijiji 975 vimerudi kwa wananchi. Kuna yale maeneo ambayo ni ushoroba wa wanyama, ni mahitaji mahsusi kwa ajili ya uhifadhi endelevu yamerudishwa kwa Serikali; na ndiyo maana maeneo ambayo tumeyaachia wananchi walishangilia na tulivyokuwa tunapita wananchi wamefurahi kwamba Serikali imewasikiliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya machache ni kwa ajili ya uhifadhi mahsusi ili kutunza vyanzo vya maji lakini kuhifadhi mazingira pamoja na uhifadhi endelevu, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza ninaipongeza Wizara, walituma timu kwa ajili ya kutatua mgogoro kwenye Hifadhi ya Kitulo na Mpanga Kipengele. Swali langu; ni lini wananchi hawa wa maeneo ya Ipelele, Ikovo na Mfumbi ambao wanapakana na Hifadhi ya Kitulo pamoja na Pori la Mpanga Kipengele mtawapatia barua, kwa sababu mlionesha nia ya kuwaongeza maeneo, ili waanze kufanya shuguli zao za kichumi kwa kuwa muda mrefu sasa wameendelea kusubiri barua lakini hawajapata maamuzi ya Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Jimbo hili kwamba, Serikali iliunda Kamati ambayo ilienda kufanya tathmini uwandani, na Kamati hii imeshapita maeneo takribani nchi nzima, ikiwemo eneo la Mheshimiwa Sanga. Kwa hiyo, sasa hivi kinachofanyika ni utekelezaji wa uchambuzi uliofanyika uwandani. Wakati wowote naomba nimuahidi Mheshimiwa Mbunge na wananchi wanaozunguka Hifadhi ya Kitulo kwamba kuanzia sasa utekelezaji wake utafanyika na tutawajulisha wananchi maeneo husika, kwamba sasa tathmini imeenda hivi. Tutapita pia kijiji kwa kijiji, hifadhi kwa hifadhi, tunashirikiana kuweka vigingi ili kuondoa hii taharuki ya wananchi kutofahamu mipaka halisi. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro wa Hifadhi ya Serengeti na Kata za Nyanungu, Goroma na Kuhihancha, ni mgogoro wa muda mrefu na mipaka iliwekwa mwaka 68 bila kushirikisha wananchi. Naomba nijue Wizara ya Maliasili; ni lini sasa itaenda katika kata hizo ikae na wananchi pamoja bila kutumia mzinga na bunduki wasikilize wajadiliane kumaliza mgogoro katika eneo hilo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Waitara, Mbunge wa Tarime, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna changamoto kubwa katika Jimbo la Mheshimiwa Waitara; na hivi karibuni tu askari wetu ameuwawa kwa kupigwa mshale. Hili kwa kweli sisi kama Serikali tunasikitika sana wananchi wanapojichukulia mamlaka ya kudhuru wahifadhi ambao wanalinda rasilimali zetu sisi kwa faida yao wenyewe. Hili naomba niliseme hadharani kwamba wale askari wako kwa ajili ya kulinda rasilimali za Taifa na si vinginevyo. Kwa hiyo tunaomba tuheshimu mipaka, tuheshimu hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapomuua askari hauwezi kuibadilisha ile ramani. Askari atakufa lakini ramani itaendelea kuwepo; ni mpaka pale Serikali itakaporudi kuutatua huu mgogoro. Kwa hiyo tunaomba wananchi wasijichukulie sheria mkononi, hilo ni la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la pili, nataka nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tunaenda wenyewe kwenda kutatua ana kwa ana na wananchi na kuwatahadharisha kwamba kuendelea kuua askari wataishia jela, kwa sababu lazima sheria ichukue mkondo wake. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ningependa kumuuliza swali la nyongeza Mheshimiwa Naibu Waziri. Naipongeza Serikali kwa kumaliza Mgogoro wa Ngorongoro vizuri kabisa kwa kuwahamisha wale wananchi waliokuwa Kata ya Ngorongoro kwenda Kilindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Nyatwali iliyopo Bunda ni sawa sawa na kata iliyoko Ngorongoro. Ile kata ina hamishwa yote ikiwa na miundombinu ya shule, hospitali na vitu vyote, na ni kata ya enzi na enzi. Hata hivyo, kuna double standard ya Serikali. Inaonekana kule watalipwa milioni mbili ilhali kule watu walihamishwa kistaarabu mpaka na ng’ombe wakabebwa kwenye gari.

Je, Serikali ina mpango gani wa kumaliza Mgogoro wa Nyatwali?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Musukuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Nyatwali na vijiji jirani vinavyozunguka kata hiyo, Serikali ilitoa mapendekezo ya kulichukua eneo hilo kutokana na changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa zikijitokeza katika eneo hilo. Wananchi hawa wako kihalali na hii sentensi Serikali kila siku tumekua tukiiongelea; wako kihalali sio wavamizi na vijiji vilivyoko pale vimesajiliwa kihalali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu uliopo, Serikali inapoona kuna umuhimu wa eneo lile kulichukua kwa maslahi ya Taifa, hapa nikisema maslahi ya Taifa, tuna resources nyingi ambazo tunazitumia kwa maslahi ya Taifa. Kwa hiyo, hata hili eneo tunaliangalia kwa upana zaidi na si kwa wananchi wachache.
Kwa hiyo, tunachofanya, tumefanya uthamini na wananchi waliomba mapendekezo kwamba badala ya heka kulipwa milioni mbili basi wanaomba milioni tatu. Ahadi tuliyoitoa ni kwamba tathmini ifanyike watathmini waingie uwandani waone halafu Serikali itaona nini kifanyike na tutarejesha kwa wananchi mrejesho ambao utakuwa ni muafaka kati ya wananchi na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa tahadhari tu, hawa wanaohamishwa ni kwa mujibu wa sheria za nchi. Ngorongoro imekuwa treated tofauti na maeneo mengine. Mara nyingi Waheshimiwa Wabunge wanadai pale ambapo wananchi wanahamishwa wanataka walinganishe na Ngorongoro. Suala la Ngorongoro lipo tofauti kabisa na maeneo mengine, ahsante.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Naibu Waziri, lakini mimi nina swali moja tu la nyongeza, linaweza kuchukua muda kidogo, naomba unilinde.

Mheshimiwa Spika, mgogoro huu upo kati ya mwanakijiji na wanakijiji na umechukua muda mrefu zaidi ya miaka 15 na mgogoro huu unafahamika katika Serikali ya Kata, Serikali ya Wilaya, Serikali ya Mkoa na wameshindwa kufanya suluhu yeyote.

Kwa hiyo, sasa nomba Serikali sasa ione muda muafaka kwa Wizara ambayo wanaona inahusika na swali hili, wafike katika kijiji hicho, wafanye suluhu ili huyu mwanakijiji apate haki yake na wanakijiji wapate haki yao, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mhesimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Conchesta, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, niziombe tu Serikali zilizoko kwenye Mamlaka ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa wakishirikiana na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi washughulikie mgogoro huu ili sasa wananchi waweze kupata haki yao na huyo mwekezaji aliyeko katika maeneo hayo pia aweze kufanyiwa haki yake, ahsante. (Makofi)
MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, ni lini Serikali itashughulikia migogoro ya wafugaji na wakulima inayoendelea katika maeneo yanayozunguka Hifadhi ya Serengeti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Agnes Marwa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na changamoto kubwa katika Hifadhi ya Serengeti na wananchi ama vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo na changamoto hizi zimesababisha kuwepo na vurugu nyingi ikiwemo wananchi kuuawa lakini pia na askari wameendelea kuuawa.

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imeshaanza kuchukua hatua na kama siku tatu zilizopita Serikali ya Mkoa ilienda kuzungumza na wananchi ili kutatua mgogoro huu. Kimsingi hakuna mgogoro wowote isipokuwa wananchi hawataki kukubaliana na mipaka iliyopo na kibaya zaidi tunapoweka vigingi wananchi wanaenda wanang’oa vile vigingi na kuendelea kufanya vurugu ikiwemo kuingiza mifugo hifadhini.

Kwa hiyo, niendelee kuwaomba wananchi wafuate sheria na taratibu zilizopo nchini, kwenda kinyume na sheria ni kujitakia sababu nyingine ambazo Serikali itachukua hatua.

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Naibu Waziri namshukuru sana, lakini naomba nitumie nafasi hii kusema kwamba eneo la Serengeti ni miongoni mwa maeneo ya vivutio vyetu ambavyo vinajulikana kimataifa. Hili ni eneo ambalo tunapaswa kulilinda na kuliendeleza, lakini hili ni eneo pia ambao kumekuwa na changamoto kama alivyosema Naibu Waziri, askari wetu mara kwa mara wamekuwa wakipigwa mishale na wananchi wanaozunguka.

Mheshimiwa Spika, wiki iliyopita Askari Deus mwenye umri wa miaka 42 amepigwa mshale wa sumu eneo lile na tumekuwa tukiendelea wananchi na kutoa matamko na kulaani hali hii.

Mheshimiwa Spika, hivyo nitumie nafasi hii kusema kwamba kimsingi Serengeti haina mgogoro wowote wa mpaka, wananchi wanapaswa kufahamu na niishukuru sana Kamati ya Ulinzi na Usalama ikiongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Mara wamepita juzi na wataalam wetu, kuwaonesha wananchi eneo la mpaka ili wasipate kuingia katika hifadhi.

Hivyo ni muhimu kuheshimu maeneo haya ya hifadhi ili hifadhi zetu ziwe salama, wafugaji wawe salama na wakulima wawe salama. Nimeona niongeze msisitizo huo, nashukuru sana. (Makofi)
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa, hili zoezi ambalo linaendelea sasa hivi la kuweka mipaka ndiyo limeenda kuchochea kabisa mgogoro uliopo kati ya vijiji hivi 24 na Hifadhi ya Wamembiki. Na kwa kuwa Mheshimiwa Rais anazamira ya dhati kabisa kumaliza huu mgogoro uliopo pale. Je, Serikali haioni kuna haja ya kwenda kuhakiki upya hii mipaka kwa kufuata mipaka ile waliyokubaliana wananchi mwaka 97 kati ya wananchi na Hifadhi ya Wamembiki? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili Mheshimiwa Waziri kwa kuwa wananchi wanayozunguka Hifadhi ya Wamembiki wana changamoto nyingi sana. Uko tayari kuongozana nami baada ya Bunge hili la Bajeti kwenda kuzungumza na hawa wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jonas Zeeland, Mbunge wa Mvomero kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Mvomero kwa kukubali kuruhusu pori hili ambalo lilikuwa ni Hifadhi ya Jamii ya Wanyamapori (WMA) kuwa Pori la Akiba ambalo kwa kusema ukweli Serikali inawashukuru sana wananchi hawa. Kwa sababu umuhimu wa eneo hili kwanza ni mapito ya wananyama wengi wakiwemo wanyama wakali na ni ushoroba ambao unapita katika maeneo ya Hifadhi ya Selou, Mikumi, Tarangile na Saadan. Lakini pia katika maeneo haya kuna umuhimu wa utunzaji wa vyanzo vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo nimhakikishie tu Mbunge kwamba wananchi hawakukosea kukubali kupandisha eneo hili kuwa Pori la Akiba. Sasa ile changamoto ambayo inaonekana kwamba tumeenda kuibua migogoro mipya niwahakikishie tu wananchi wa Mvomero kwamba tutaenda kuishughulikia na kwa kuwa wataalam wako uwandani basi tutahakikisha hii migogoro inakoma na wananchi waendelee kuishi maisha yao vizuri na wakati huo huo pori hili tunalihifadhi kwa faida ya wananchi wanayozunguka maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, swali la pili niko tayari tu kuambatana na Mheshimiwa Mbunge pia kwenda kuwaona wananchi, kutatua na kuelezeana namna ya umuhimu wa kutunza maeneo haya kwa ajili ya vizazi vinavyokuja. (Makofi)
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa hii nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, matatizo yaliyoko kwenye hili Pori la Wamembiki yanafanana na matatizo yaliyoko katika Wilaya yangu ya Mbozi kwenye Pori la Isalalo kati ya wananchi wa Kata ya Isalalo na Mbinzo na Itaka na TFS.

Je, ni lini Serikali itatatua huu mgogoro wa Pori la Isalalo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George, Mbunge wa Mbozi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niwaombe wananchi wafahamu kwamba migogoro mingi ambayo inasemekana kuwa ni migogoro ni migogoro ambayo ni nani amemkuta mwenzie? Pori analoliongea Mheshimiwa George ni eneo ambalo lina GN ambayo GN ni ya miaka ya nyuma na wananchi wamesogea katika maeneo hayo. Kwa bahati mbaya kabisa Kamati ya Mawaziri Nane haikuweza kupita katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimuombe kwa kuwa huu ni mgogoro mpya, Serikali itaenda kuhakiki yale maeneo na kuyaangalia umuhimu, kwanza tunaangalia umuhimu wa eneo lile kama ni vyanzo vya maji na kuna wanyamapori na mazalia ya wanyamapori yako katika maeneo hayo, tunaendelea kuwashauri wananchi kuyaachia yale maeneo pamoja na kuwa tunawaita sisi ni wavamizi. Linapoonekana eneo halina umuhimu sana basi Serikali inapitia na kumega yale maeneo nakuwaachia wananchi.

Mheshimiwa Spika, hivyo nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaenda kuyahakiki hayo maeneo na kama yanaendelea kuwa yanafaa katika uhifadhi basi tutawashauri wananchi lakini kama yatakuwa yaruhusu kumegwa basi tutayaachia. Ahsante.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, vijiji vya Ngomalusambo na kijiji cha Vikonge ni miongoni mwa vijiji ambavyo Serikali ilitoa maelekezo kupitia kwa Mheshimiwa Rais Hayati Dokta John Pombe Magufuli viachiwe vibaki kuwa kwa matumizi ya wananchi, lakini mpaka sasa bado vijiji hivyo vina mgogoro kati ya TFS na vijiji hivyo.

Ni lini Serikali itakuja kutatua mgogoro huu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kakoso kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimuahidi tuu Mheshimiwa Kakoso kwamba tutafika katika maeneo hayo nakuyaangalia kama yana umuhimu wa kuyaachia tutaendelea kuyaachia. Ahsante.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nishawahi kuuliza swalli hapa Bungeni la Msitu wa Kazimzumbwi na Mheshimiwa Waziri aliniahidi kwamba Kamati ya Mawaziri Nane itafika kwenda kutatua mgogoro baina ya Msitu wa Kazimzumbwi na wananchi wa Kata ya Zingiziwa, Chanika, Buyuni na Pugu, lakini mpaka ninapozungumza hapa Mawaziri Nane hawajafika.

Naomba kujua, Je, ni lini Mawaziri hawa nane watafika kwenda kutatua mgogoro huo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa Ukonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ziara ya Mawaziri wa Kisekta hivi sasa ninavyoongea wako safarini kuelekea Arusha na nimuahidi tu Mheshimiwa Jerry kwamba, kwa kuwa oparesheni hii imeshaanza na tunaendelea na zoezi hili tutafika katika msitu huo na tutatatua changamoto hiyo. Ahsante.
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.

Vijiji vya Ntwigu, kijiji cha Ng’wandwe, kijiji cha Mwanduti na Kipendamoyo ni miongoni mwa vijiji ambavyo vilikuwa kwenye orodha ya kupatiwa usajili kipindi cha usuluhishi wa migogoro ya Mawaziri nane, lakini baada ya lile zoezi vijiji hivi havijapatiwa usajili.

Mheshimiwa Spika, je hivi vijiji baada ya kuwa vimekosa hadhi ya kuwa kwenye Hifadhi kwa sababu hakuna wanyama na wale wananchi wameshakuwa wengi wamevamia hilo eneo. Ni lini sasa hivi vijiji vitapewa usajili wa kudumu ili wananchi wajue mipaka yao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rehema Migilla kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, usajili wa vijiji unafanywa na Serikali za Mitaa. Hivyo nimuombe Mheshimiwa Rehema kwamba atawasiliana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuangalia kama kuna umuhimu wa vijiji hivi kusajiliwa. Na niombe vijiji hivi vinavyosajiliwa viwe na hadhi inayolingana. Kwa sababu kuna vijiji vingine vinapelekwa kwenda kusajiliwa kumbe viko ndani ya hifadhi. Nitoe tahadhari hiyo kwa wananchi kwamba wanapopeleka vijiji hivi kwenda kusajiliwa wajiridhishe kwamba je, wako ndani ya vibali vinavyoruhusiwa kusajiliwa? Ahsante.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, naomba nimuulize Waziri wa Maliasili na Utalii ni lini itafika katika Jimbo langu la Nanyumbu kutatua mgogoro wa mipaka katika vitongoji vya Wanika na Malomba na kijiji cha Mbangala Mbuyuni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahya, Mbunge wa Nanyumbu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, kabla ya bajeti hii kuisha basi nimuombe tutafute hata weekend moja tuende tukatatue mgogoro huu. Ahsante. (Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni kweli Mamba wawili walikutwa wamekufa ziwani, si kwamba walivunwa kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema, na kwa kuwa akina mama wananchi wa Buchosa bado wanaendelea kuliwa na Mamba mpaka sasa; swali la kwanza;

Je, Waziri anaweza kuchukua hatua kwa watumishi wake ambao nina uhakika kwamba wamemdanganya ili jambo hili lisitokee siku nyingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; wananchi wa Buchose wanahitaji commitment ya Serikali ya kwamba ni lini sasa vizimba hivi vitajengwa ili kuokoa maisha yao wakati wanateka maji? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Eric James Shigongo Mbunge wa Jimbo la Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Erick Shigongo kwa kuendelea kufatilia eneo hili ambalo kumekuwa na changamoto ya wanyama wakali hususan mamba. Ni kweli alikuja na alimwona Mheshimiwa Waziri, lakini pia tulipeleka askari kule, wamekuwa wakifatilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikidhibitika kweli kwamba hawa askari wamedanganya kwamba hawakwenda na wale mamba wamekutwa wako pembeni wamekufa, hatua za kinidhamu na za kiutumishi ninamwelekeza Katibu Mkuu azichukue haraka mara moja; kama itathibitika tu kwamba hawa askari wamedanganya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la pili nimwahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii tumekuwa tukijenga vizimba vya mfano kuonyesha namna ambavyo hawa wanyama wanaweza wakadhibitiwa na wananchi wakaendelea na shughuli zao za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwahidi tu kwamba tutapeleka wataalamu wataenda kujenga kizimba cha mfano ambacho kanda ya ziwa pia wataenda kujifunza pale. Lakini kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, ni kwamba kwa kuwa haya maeneo kwa asilimia kubwa yanamilikiwa na Serikali za Mitaa zikiwemo Halmashauri. Tunazielekeza Halmashauri ziweze kutenga fedha kwa ajili ya kujenga vizimba ili kusaidia hawa wananchi waendelee na shughuli za kibinadamu, ahsante.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Tangu mwaka 2019 mpaka sasa watu watatu wamethibitika kufa kwa sababu ya tembo kwenye kata za Mkomazi na kata za Mkumbara kule Korogwe Vijijini na sasa hivi tunapozungumza hali ya uharibifu wa mazao ni kubwa sana. Ni upi mkakati madhubuti wa Serikali kuhakikisha kwamba tunawasaidia wananchi wetu kudhibiti tembo na wanyama wengine wasiendelee kuathiri mazao lakini na maisha ya wananchi wetu? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Timotheo Mnzava Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali la yote nimpongeze Mheshimiwa Mbunge. Ni kweli wiki iliyopita tu tulikuwa tuna changamoto ya tembo ambao walivamia katika maeneo ya mashamba ya katani na mashamba ya mipunga, lakini tulipeleka askari.

Changamoto iliyopo ni kwamba wale askari walikuwa ni wachache. Lakini nimuahidi Mheshimiwa Mnzava wananchi wa Korogwe zoezi linalofuata sasa hivi ni kwamba tumeamua kutafuta askari wa ziada ambao tutakuwa tunawaajiri kwa muda ili kuongeza nguvu katika maeneo ambayo yana changamoto ya wanyama wakali ili hawa wananchi katika kipindi cha mwezi wa nne mpaka wa saba waweze kuvuna mazao yao bila tatizo. Hili naliweka ni commitment ya Serikali tunaenda kulitekeleza mara moja.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuulizwa swali la nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuzuia simba na tembo wanaoharibu mazao pamoja na mifugo katika Kata ya Magugu pamoja na Vilima Vitatu Jimbo la Babati Vijijini pamoja na Jimbo la Kiteto? Ahsante.
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asia Halamga Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba katika Kijiji cha Magugu tulikuwa na changamoto ya simba ambayo sisi tuliiona ni changamoto ngeni sana kwa sababu tumezoea ni tembo, mamba na viboko; lakini tulipeleka askari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto tunayoipata ni kwamba hawa wenyeji baada ya kuonesha kwamba mipaka ya hifadhi inakuwa maeneo fulani wenyeji wanasogea karibu sana wanaweka mazizi kando kando ya hifadhi. Sasa Simba anapotoka cha kwanza anaona kitoweo kiko karibu, kwa hiyo ‘mimi niwaombe wananchi wanaoishi maeneo hayo kwamba tunapoweka kando kando ya hifadhi beacon hii unaweka zizi la ng’ombe hapa. Na hili limekuwa ni changamoto kubwa kwa sababu hao hao wanatega ikifika maeneo kadhaa basi anaingiza hata ng’ombe hifadhini anaweza wanapata chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niwaombe wafugaji, kwamba kuweka zizi kando kando ya hifadhi ni kuleta hatarishi ya wanyama wakali kusababisha kuliwa hii mifugo na wanyama hatarishi kama simba. Lakini tumeendelea kutoa ushirikiano na askari wataendelea kuwepo katika maeneo hayo ili kudhibiti simba wanaotamani kula mifugo.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa. Kumekuwepo na ongezeko kubwa la kima, ngedere na nyani kwa vijiji vinavyopakana na Mlima Kilimanjaro na wanyama hawa wamekuwa wanasababisha uharibifu mkubwa sana wa mazao ikiwa ni pamoja na kula kuku na kusababisha umaskini.

Je, Serikali ina mpango gani kusaidia wananchi wetu kukabiliana na changamoto hii?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Moshi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna changamoto ya ngedere, nyani na kadhalika katika maeneo ya Mlima Kilimanjaro; lakini tumeanzisha utaratibu wa kugawa miti ambao tunatarajia kuanza ili kuwepo na upandaji wa miti katika maeneo ambayo tunaamini haya tukiweza kuyazuia na kuyahifadhi vizuri basi wanyama hawa wataweza kuishi maeneo salama zaidi kuliko ilivyo sasa ni kweupe zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa wakati huo huo tulishaahidi kwamba hawa ngedere tutatafuta namna ya kwenda kuwapunguza na kupeleka katika maeneo mengine ya hifadhi. Hilo nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutalitekeleza. Ahsante.
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri swali; kwamba kwenye kata za Swaiti Sambao, Lweipiri na Ololosopan, tembo wamekuwa wakiharibu mazao pamoja na kuumiza wananchi.

Je, Serikali ina mkakati upi wa kuhakikisha kwamba wananchi wale wanafidiwa?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Shangai Mbunge wa Ngorongoro kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu mwanzo, kwamba sasa tuna mpango wa kuangalia namna ya kuwa na askari wa kutosha ili kipindi kile ambacho ni cha migogoro kati ya binadamu ya wanyama wakali, basi hawa askari waweze kuelekea katika maeneo hayo na kudhibiti hawa wanyama wakali. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri nataka tu kujua wanasema kubaini maeneo mapya ya uwekezaji kwani yale ya zamani Mheshimiwa Waziri mmeyaendeleza? Hilo swali langu la kwanza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kule kwetu Mtwara hususan wilaya ya Mtwara ambayo inahusisha Jimbo la Mtwara mjini na Mtwara Vijijini kuna fukwe nzuri sana ambayo ikiendelezwa itavutia utalii na hivyo kusababisha shughuli za maendeleo pale Mtwara zipatikane sasa swali langu. Serikali imejipanga vipi kuhakikisha wanatangaza fukwe zile zinaendelezwa ili watalii waje? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Issa Malapo Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Tunza kwa kuliona hili na mimi niseme tu kwamba haya maeneo ambayo ni maeneo ya fukwe kwa asilimia kubwa yanamilikiwa na Serikali za Mitaa lakini pia na wananchi binafsi. Kwa hiyo sisi tumekuwa tukitafuta wawekezaji lakini baada ya kutafuta wawekezaji tunawapeleka katika wamiliki ambao wanamiliki haya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo baada ya Royal Tour ambayo Mheshimiwa Rais, tunamshukuru sana, ameizindua na pia kutafuta wawekezaji tumetengeneza namna na mbinu bora ya kuwakutanisha sasa hawa wamiliki wa maeneo haya na kuyaweka wazi na kuyasajili ili sasa kuwepo na uwezekano ukipata mwekezaji basi unamuonyesha tu kwamba nenda hapa.

Kwa hiyo nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa hivi Serikali inayashughulikia kwa ukaribu na hivi punde tutaanza kuwaona wawekezaji wengi wanaenda kwenye maeneo haya na tutahakikisha wanayapata kwa sababu tayari tumeshaanza kuyasajili na wamilki wameshakuwa wazi na wameshaanza kuiona Serikali na tayari tuna mpango mzuri ahsante.
MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa nchini kuna maeneo ya fukwe ambayo yameendelezwa kiutalii, lakini maeneo haya yanakabiliwa na changamoto kubwa ya uchafuzi wa mazingira.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuyahifadhi maeneo haya ili kuweza kuwavutia watalii nchini?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asya Mohammed, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jukumu la Serikali kuhakikisha kwamba maeneo yote ambayo tunapeleka watalii lazima yawe ni masafi yenye kuvutia ili tuendelee kupata watalii. Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye yale maeneo ambayo yanaonekana yana changamoto hizo Serikali itaendelea kuchukua hatua ili kuhakikisha kwamba maeneo haya yanavutia na wawekezaji na watalii waendelee kuja.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa ni muda mrefu Nyanda za Juu Kusini tumekuwa tukiainisha vivutio vipya mbalimbali vya utalii, lakini vile vile Nyanda za Juu Kusini tumebarikiwa kuwa na hifadhi ya kipekee ya Kituro ambayo hifadhi hii ulimwenguni ni aina ya kipekee, hakuna ambayo inafanana nayo.

Je, Serikali mmejipanga vipi kuhakikisha kwamba mnakuza utalii wa nyanda za juu kusini?
NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mgaya Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Neema kwa kuendelea kuhamasisha utalii na hili ninalisema kwa dhati kabisa kwa sababu sasa hivi focus yetu ni kuelekea kwenye Nyanda za Juu Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mradi wa REGROW ambao ulishaanza tayari na tayari ni mradi ambao una madhumuni ya kuboresha maeneo ya Nyanda za Juu Kusini hususan miundombinu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kwa kuwa Kaskazini sasa hivi tunaelemewa watalii nikimaanisha kwamba ukipeleka watalii 1000 tayari kule kuna jam; focus ya Serikali ni kuelekeza hawa watalii sasa warudi nyanda za juu kusini na maeneo mengine na ndiyo mkakati wa Serikali. Nimhakikishie kwamba uhamasishaji unaoendelea sasa hivi ni kuwekeza lakini pia na kuhamasisha utalii katika maeneo ya Nyanda za Juu Kusini.

Kwa hiyo hili tumeliona na tunaendelea kulitengenezea mkakati madhubuti. Ahsante sana.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kuwa nia ni kuleta unafuu kwa wananchi wanaozunguka maeneo hayo; na kwa kuwa halmashauri ndio zinazojua zaidi mahitaji ya watu wale, hatuoni kwamba ni muda sasa tuzipeleke fedha hizo kwenye halmashauri badala ya kutekeleza miradi kama inavyofanyika migodi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa katika Mkoa wa Kilimanjaro suala la uoteshaji miti ni hiari, lakini ukataji miti ni suala ambalo lazima upate kibali na miti hiyo wanatumia kwa ajili ya nishati ya moto. Je, Serikali haioni kutafuta namna nyingine ya kuwapatia nishati mbadala kupitia CSR?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuendelea kufatilia hizi CSR katika eneo lake analowakilisha. Katika swali lake ambalo ameuliza Serikali haioni haja kupeleka fedha katika halmashauri. Kwenye jibu langu la msingi nimesema kwamba halmashauri pia zinapata asilimia na pia wananchi wanapata asilimia. Lengo ni kufikisha hii miradi kwa jamii ambao ndio hasa walinzi wa haya maeneo ambayo tunayahifadhi.

Mheshimiwa Spika, jamii ikijisikia kwamba ni sehemu ya uhifadhi sisi kama Serikali tunafarijika kwamba wanaona uthamani wa eneo lile na ni rahisi sasa hata unapowaelezea uhifadhi namna yake ni nini na thamani ya uhifadhi ni nini. Kwa hiyo kupeleka kwenye jamii ni muhimu zaidi kuliko kwenye halmashauri.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kwamba uoteshaji wa miti Serikali kupitia hifadhi ya TANAPA ilianzisha mradi wa majiko banifu katika eneo linalozunguka Mlima Kilimanjaro. Majiko haya yalikuwa ni fanisi na walienda kufundishwa kaya mbalimbali katika maeneo hayo na pia tumeingia kwenye mpango wa kuanzisha upandaji wa miti katika maeneo yanayozunguka hifadhi hiyo.

Mheshimiwa Spika, upandaji huu ulianza toka mwaka jana na sasa hivi ni endelevu. Hivyo nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi huu utatekelezwa ambapo wananchi wengi wanaozunguka maeneo hayo watapata miche ambayo itapandwa katika maeneo ya vijiji nje ya hifadhi ili irahisishe kupata nishati mbadala. Ahsante.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nusu ya Wilaya ya Meatu imepakana na Hifadhi ambazo ni Ngorongoro, Serengeti na Maswa Game Reserve. Je, ni lini Serikali itaendelea kunufaisha miradi katika Wilaya ya Meatu, miradi ile ilikuwa inatolewa na ujirani mwema kutokana na utalii unaofanywa katika Hifadhi ya Serengeti na Ngorongoro ikiwemo ujenzi wa mabweni?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya, Mbunge wa Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimwambie tu kabisa Mheshimiwa Mbunge kwamba, asiwe na wasiwasi na niendelee kumpongeza kwa sababu wananchi wanaozunguka yale mapori ya akiba tunatambua umuhimu wa namna ya kunufaika na CSR. Hata hivyo, kwenye eneo hili Mheshimiwa Leah amekuwa akileta maombi katika ofisi zetu, lakini tutambue tu kwamba katika kipindi cha miaka miwili hii iliyopita tulikuwa tuna changamoto ya UVIKO 19 ambapo hifadhi zetu ziliathirika sana. Hivyo Serikali ilichukua jukumu la kuzisaidia hizi hifadhi ili ziweze kujiendesha.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tumeshaanza kuimarika vizuri, CSR zitarudi kama ilivyokuwa mwanzo na pengine zaidi hasa ukizingatia Royal Tour imeibua mambo mengi, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya swali la nyongeza. Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Mamlaka ya Wanyamapori (TAWA), imefanya maboresho makubwa Kilwa Kisiwani ambao ni mji wa kitalii na Kilwa Kisiwani imetangazwa kuwa ni sehemu ya urithi wa dunia, lakini makubaliano yalikuwa kwamba wananchi wa Kilwa Kisiwani wapate CSR kupitia kujengewa shule pamoja na zahanati, lakini mpaka sasa hawajajengewa shule wala zahanati.

Mheshimiwa Spika, swali langu, je, Waziri yuko tayari kufuatilia kuona kwamba shule na zahanati inajengwa Kilwa Kisiwani?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kuliona hili, lakini kama ambavyo nimeeleza mwanzo kwamba kabla ya UVIKO-19 tulikuwa tunatekeleza kupeleka haya maeneo CSR, lakini hii changamoto ya UVIKO-19 ndio iliyoturudisha nyuma lakini kwa sasa hivi tumeshaanza kuimarika vizuri. Hivyo nimwahidi Mheshimiwa Mbunge katika eneo lake nitaenda pia nitaenda kuongea na wananchi wa jimbo hilo ili kuwaambia umuhimu wa kupata CSR pia umuhimu wa utunzaji wa maeneo ya hifadhi. (Makofi)
MHE. JACQUELINE K. ANDREW: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili. Swali langu la kwanza; katika mikoa yetu ambayo ina hifadhi changa, Wakuu wetu wa Mikoa wamejitahidi kujitokeza

kuhakikisha wanatangaza utalii katika hifadhi hizi changa. Je, Serikali ina mpango gani katika kuhakikisha inasaidia viongozi hawa wa mikoa ili kuweza kukuza utalii katika hizi hifadhi changa na tukizingatia bado miundombinu ni mibovu, magari pia hayatoshi, wanapata wakati mgumu hasa wanapokuwa wanafanya kazi za kutangaza hifadhi hizi kujikuta sasa inabidi waazime magari kutoka sehemu zingine, tunaonaje kama Serikali tuweze kusaidia kutangaza sekta hii ya Maliasili na Utalii?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; bado tunachangamoto nyingi kwenye upande wa ajira. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha ajira zinapatikana na kukuza sekta hii ya utalii hasa katika hifadhi hizi changa, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacquiline Kainja, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali kwa sasa imejikita katika maeneo mapya ya utalii zikiwemo hifadhi hizi ambazo imezitaja na malengo makuu ni kuhakikisha kwamba tunapanua wigo wa namna ambavyo watalii wataweza kufika katika maeneo hayo. Mikoa yote ya Tanzania tumeendelea kuwahimiza waendelee kuhamasisha utalii ikiwemo utalii wa ndani lakini pia tumejikita kuboresha miundombinu zikiwemo barabara, maeneo ya malazi na chakula ili sasa iwe rahisi kwa watalii kuweza kufika katika maeneo hayo. Kwa hiyo tunaendelea kuwahimiza Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya waendelee kuhamasisha masuala mazima ya utalii.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ameongelea kuhusu ajira. Tumeendelea kuwasiliana na Ofisi ya Rais, Menejimenti Utumishi na Utawala Bora kuangalia namna ya kuongeza watumishi ambao tutawasambaza katika maeneo mapya yaliyoko katika hifadhi hizo.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je Serikali haioni iko haja sasa ya kuondoa hizo sheria, miongozo na kanuni ili wananchi wa Kaole waweze kupatiwa gawio kwa kile ambacho kipo katika mji wao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je ni lini Serikali sasa ina mpango wa kuwatumia wazee wa Kaole kuelezea historia ya magofu ya kale pamoja na kaole kwa wageni wanaokuja badala ya kuwatumia waajiriwa ambao historia hiyo wameisoma kwenye vitabu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mharami Shabani, Mbunge wa Bagamoyo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa namna ambavyo sasa hivi Wizara ya Maliasili na Utalii makusanyo yake yanaenda Mfuko Mkuu hatuoni haja ya kurekebisha sheria hii kwa sababu makusanyo yote yanayokusanywa yanaenda Mfuko Mkuu na yanapofika kwenye Mfuko Mkuu, halmashauri zinapokea ruzuku mbalimbali ambazo zinatoka katika Mfuko Mkuu. Kwa hiyo fedha yote inayokusanywa katika maeneo haya tuna uhakika kwamba inaenda kulenga wananchi wa Tanzania nzima kutokana na masuala mazima ya utalii.

Mheshimiwa Spika, hili lingine alilosema la kutumia wazee tunalipokea, tutawashirikisha wazee wa Bagamoyo pamoja na maeneo mengine zilipo malikale ili tuweze kuipata historia kamili ya Tanzania pamoja na wazee wetu waliotutangulia, ahsante.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa. Swali la kwanza; je, Serikali ina mpango gani wa kufungua VIP route ya Kibia ambayo hupeleka watu maalum kupanga Mlima Kilimanjaro ili tuweze kupata fedha za kigeni kama ambavyo tume-plan.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili mti mrefu kuliko yote Barani Afrika wenye mita 81.5 upo katika msitu wa Mlima Kilimanjaro katika Kijiji cha Pema, miundombinu ya kufika katika eneo hili na mazingira ya eneo hili ni mabaya. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuboresha eneo hili ili tuweze kupata fedha za kigeni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Profesa Patrick Alois Ndakidemi, Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba tu nimtaarifu Mheshimiwa Profesa Patrick pamoja na wananchi wa Moshi kwamba kwa sasa hivi tayari Wizara imeshaanza ukarabati wa lango hili la VIP route ambapo lipo takribani asilimia sabini na kwa sasa tunatafuta Wawekezaji kwa ajili ya kujenga huduma za malazi na chakula. Pia kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024, tutajenga lango kuu linalopitia katika hiyo VIP route ambayo itawasaidia wageni kuingia katika Hifadhi ya KINAPA.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili lingine mti mrefu zaidi hapa Afrika tumeshaanza kutenga kutenga fedha kwa ajili ya kuweka miundombinu sahihi katika eneo hilo ili Wataliii waweze kufika kwa urahisi. Kwa hiyo, kwa bajeti hii ambayo itapitishwa na Bunge lako hili tunatarajia kwamba zoezi hili litaanza kwa mwaka wa fedha unaokuja, ahsante. (Makofi)
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali ambayo sijaridhika sana. Kimsingi nilitarajia nijibiwe swali na Wizara ya Fedha, lakini hamna shida kwa sababu Serikali ni moja. Ilikuwa ni nia njema ya Serikali kuokoa Jeshi la Uhifadhi kwa maana ya kufanya operesheni zake kutokana na uwezo wao mdogo wa kuingiza mapato kipindi cha COVID. Sasa hivi kuna jitihada mbalimbali ambazo zinafanywa na Serikali hasa Mheshimiwa Rais katika kuifungua nchi. Tunatarajia wageni watakuwa wengi na Jeshi la Uhifadhi litaweza kujiimarisha. Je, Serikali haioni haja sasa kubadilisha sheria ili TANAPA na TAWA waweze kukusanya fedha zao wenyewe na kuendelea kupeleka gawio Serikalini?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Antipas Mgungusi, Mbunge wa Malinyi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye jibu la msingi nimesema wazi kabisa kwamba ni vyema fedha yote inapokusanywa ikaingia kwenye kapu moja ili kuona hata vyanzo vyetu vya mapato tunapataje. Pamoja na yote hayo maelezo yangu yalikuwa ni kwamba kipindi hiki ambacho sasa tumeanza kuimarika, bado tunachechemea, nikimaanisha kwamba Serikali bado inalisaidia hili Shirika la Uhifadhi (TANAPA). Kwa hiyo tutakapofikia mahali ambapo tunasimama wenyewe basi Serikali itaona kama kuna haja ya kubadilisha sheria tutaleta ndani ya Bunge lako Tukufu na sheria itaendelea kurekebishwa. Ahsante.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Mgogoro kati ya Pori la Usumbwa Forest Reserve na Pori la Hifadhi ya Taifa Kigosi Moyowosi umedumu kwa muda mrefu sana. Sasa je, ni lini Serikali itaushughulikia mgogoro huu ili kuwapa nafasi wananchi wa Jimbo la Ushetu hasa wanaozunguka Kata za Idahina, Nyankende, Ulewe pamoja na Ubago waendelee na shughuli zao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cherehani, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niendelee kuwaomba wananchi ambao wanaishi kwenye maeneo haya waendelee kuwa na subira wakati Serikali inaendelea kuangalia namna iliyo bora ya kutatua migogoro hii.

Mheshimiwa Spika, tuna Kamati ya Mawaziri Nane ambayo ina maelekezo kutoka kwa Mheshimiwa Rais kwamba tuzunguke nchi nzima kuhakikisha kwamba tunatatua migogoro hiyo. Sambamba na hilo tumezielekeza taasisi, endapo kuna migogoro mipya ambayo haimo ndani ya hii migogoro inayotatuliwa na Kamati ya Mawaziri Nane basi tuanze pia kuangalia mchakato mpya kuangalia namna iliyo bora ili tuweze kutatua migogoro hiyo. Kwa hiyo, niwaombe wananchi wote ambao wana migogoro mipya katika maeneo yao Serikali inaendelea kuyafanyia kazi ili tuone njia iliyo bora ya kutatua migogoro hiyo.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii, nina swali dogo gu. Kwa vile Serikali imetuhakikishia kwamba Mamlaka za Hifadhi za Misitu na Wanyamapori wana wajibu wa kutoa CSR kwa vijiji vinavyozunguka hifadhi hizi. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuziagiza mamlaka hizi ziweke bayana kiasi cha ufadhili ambazo zimetolewa kwa vijiji hivyo ndani ya miaka mitatu iliyopita? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, awali ya yote niwaombe sana wananchi wanaozunguka maeneo ya hifadhi waamini kwamba Serikali inatambua umuhimu wa mashirikiano ikiwemo miradi ya ujirani mwema.

Mheshimiwa Spika, bajeti zote tunapozileta hapa Bungeni huwa tunaweka kipengele cha miradi ya CSR. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba hata bajeti hii tutakayoisoma hivi karibuni itazingatia hilo. Hivyo, niwaombe wananchi wote na Waheshimiwa Wabunge ambao wanazungukwa na maeneo haya yaliyohifadhiwa watarajie kuona CSR katika maeneo yao. Ahsante sana.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Jitihada za Serikali ni pamoja na kuhakikisha kwamba mapato yatokanayo na utalii yanaendelea kuongezeka kwa kuboresha miundombinu na kufanya marketing ya utalii. Je, ni lini Serikali itaanza utekelezaji kikamilifu wa Mradi wa REGROW ambao ulizinduliwa tarehe 12 Februari, 2018 na Mheshimiwa Makamu wa Rais ambaye sasa ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi wa REGROW ulianza kutekelezwa mwaka 2017, lakini kutokana na changamoto ambazo zilijitokeza, Benki ya Dunia iliweza kuongeza muda mpaka mwaka 2025, ambapo tutamaliza mradi huu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara imeunda Kamati Maalum ambayo itafanya kazi bega kwa bega kuhakikisha eneo hili tunasimamia vizuri kama ambavyo tunasimamia fedha za UVIKO ili kuhakikisha mradi huu unakamilika haraka na kuhamasisha watalii waweze kufika katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kuuliza swali moja la nyongeza. Sote tunajua kwamba bado kuna changamoto kubwa sana ya madawati hapa nchini na wananchi wamekuwa ni wahifadhi namba moja wa misitu pamoja na miti mingine ambayo inapandwa na Watanzania wenyewe. Serikali ina mpango gani sasa wa kutumia miti mingine ambayo inataka kufanana na mininga ambayo iko maeneo mengi ili kuweza kuondoa changamoto hiyo ya madawati?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kaboyoka, kwa niaba yake ameuliza Mheshimiwa Aida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza niweze kuifahamisha jamii na Watanzania wote kwamba, Serikali imefanya utafiti wa miti 19 na moja ya utafiti huu ni pamoja na mti wa mtiki. Tunaangalia namna iliyo bora ya kufanya mazungumzo na Wizara ya Fedha kupitia PPRA ili kuwe na mwongozo maalum wa kuhakikisha kwamba miti hii sasa inatumika kwenye furniture. Kwa hiyo nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba changamoto ya madawati ambayo imekuwa ikijitokeza katika jamii inaenda kupungua kwa sababu aina ya miti 19 kama itaenda kutengeneza haya madawati, basi kutakuwa na aina mbalimbali ya miti ambayo ni mizuri na bora na imefanyiwa utafiti na wataalam kutoka Maliasili na Utalii. Ahsante.
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana; pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri mimi nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, mkandarasi wa mradi huo wa Kabanga hajalipwa fedha zake kwa mwaka mzima. Naomba kujua ni sababu gani zimesababisha mkandarasi huyu asilipwe fedha yake kwa mwaka mzima?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; naomba kujua, Wizara ya Maji na Serikali wana mfumo wa kuweza ku-track status ya miradi ya maji ili kuepukana na changamoto hizi za miradi kusimama na mkandarasi kutokuwa site kwa mwaka mzima? Naomba kupata majibu ya Serikali ya maswali hayo mawili.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ndaisaba George Ruhoro, Mbunge wa Ngara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niendelee kuwaomba tu wakandarasi ambao wanaidai Serikali kwamba kwa sasa Serikali imeshaanza kulipa na tayari fedha zimeshaanza kupelekwa katika maeneo husika. Kwa hiyo wakae mkao wa kupokea fedha hizo ili waweze kuendelea na kazi ambazo ziko katika site hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa strategy, tunaamini kwamba lengo la Serikali ni kumtua ndoo mama kichwani, na strategy mojawapo ni kuhakikisha huduma ya maji inawafikia wananchi kwa ukaribu zaidi. Hivyo nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa Serikali imeshaweka mikakati mahususi ya kuhakikisha maji haya yanawafikia wananchi tutaendelea kusimamia kwa ukaribu zaidi ili miradi hii iweze kukamilika na wananchi waweze kupata huduma iliyo bora.
MHE. IDD K. IDD: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana. Kwanza kabisa tunaipongeza Serikali kwa majibu mazuri haya na kwa kuwa mradi huu tayari umekamilika, sasa ni lini Wizara itatenga fedha ili kupeleka maji katika Kata ya Shabaka, Kata ya Kaboha, Kata ya Busolwa na Kata ya Mwingiro?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili la nyongeza; kwa kuwa Mradi huu wa Mangu – Ilogi umeshakamilika, je, ni lini sasa Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kupeleka maji katika Kata ya Runguya na Kata ya Segese? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Idd kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, kwa kuwa tunaendelea na mpango na bajeti wa mwaka huu unaokuja wa 2023/2024, maombi yake tutayaingiza katika bajeti hiyo ili wananchi wa maeneo husika waweze kufaidika na huduma bora ya maji. (Makofi)
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa muda mrefu sana Jimbo la Monduli hasa katika Kata ya Sepeko, Mswakini, Lepulko, Narami na Lemoti kumekuwa na changamoto kubwa ya maji. Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi zake katika maeneo haya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Catherine Magige, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee tu kuwakumbusha wananchi kwamba miradi ya maji imeweza kutekelezwa katika miaka hii iliyopita, lakini kuna baadhi ya maeneo ambayo bado hatujawafikia. Tuwaahidi tu kwamba kwa kuwa tunaenda kwenye bajeti husika tutawaingiza katika bajeti hii inayokuja ili waweze kupata huduma bora ya maji safi.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; Mheshimiwa Waziri amezungumzia suala la historia, simba wa jina la Bob Junior aliyekufa siku za karibuni tumeona mataifa mbalimbali, vyombo vya habari zikichukua habari zake kama simba ambaye ni shujaa. Hivi ni kweli hatuna mashujaa hapa Tanzania ambao watapewa majina kama huyo simba aliyekufa? Ambaye pia watoto wake wanaitwa Rihana na majina mengine ya kizungu, hatuna watu mashuhuri kama kina Mkwawa, akina Mwansasu, aakina Mwakatumbula wakapewa majina hayo na mwisho tukaweza kufanikiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; ukishasoma historia Livingstone na majina mengine kama hayo tuna Machifu katika maeneo yale ambao wangeweza kupewa majina yao. Je, ni lini Serikali italeta Muswada wa kubadilisha majina kama hayo yaliyopewa wakati wa kikoloni ili watu wetu waweze kupewa hizo nafasi na majina yao ya Kiafrika yakasimama zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimkumbushe tu Mheshimiwa Mbunge kwamba utalii wa Tanzania au utalii wowote hapa duniani ni utalii unaohusisha wazawa kwa maana ya wenyeji, lakini pia na watalii wa nje. Tunapotumia majina maarufu hatutangazii Watanzania peke yake, tunatangazia ulimwengu, kwa hiyo hiyo historia inabebwa kiulimwengu. Kwa mfano tuna mchukulia Bob Junior ambaye ni simba ambaye amekufa hivi karibuni na alikuwa na watoto wake mmoja alikuwa anaitwa Rihana. Tunapotumia jina Rihana ina maana hata mtalii anetoka Marekani anaweza kuja kumwangalia Rihana, lakini tutakapompa let say Masanja, aliyesimama hapa watakao mfahamu wa hapa hapa Tanzania, kwa hiyo tunatangaza utalii duniani ili kuonyesha jinsi gani Watanzania tumejaliwa na rasilimali tulizonazo hapa nchini, ahsante. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Itigi baada ya kuliwa mazao yao na hawa wanayama wanategemea kile kidogo ambacho Serikali imekiweka kwenye sheria ikiwemo kifuta machozi na kifuta jasho;

Je, ni lini sasa watamalizia kulipa wananchi ambao wameliwa mazao yao miaka miwili iliyopita?

Mheshimiwa Spika, swali la pili Serikali imegawa pori kubwa la akiba la Rungwa, Muhesi na Kizigo kuwa mapori yanayojitegemea. Rungwa peke yake, Muhesi peke yake na Kizigo peke yake. Muhesi imepakana sana karibu na vijiji vingi vya Itigi;

Je, ni lini sasa wataongeza askari wa wanyamapori ili angalau waweze kuwadhibiti hawa wanyama wanapotoka kule kuingia kwenye makazi ya watu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Jimbo la Manyoni Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni mwezi wa tatu tumemaliza kulipa kifuta jasho na kifuta machozi katika Wilaya ya Manyoni hususan katika maeneo ya Vijiji vya Njiri, Rungwa, Sanjaranda na Itigi Mjini ambao walipata madhara makubwa ya wanyamapori wakali na waharibifu. Hivyo nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge, kwamba kwa sasa hivi tumeshafanya tathmini kwa wale ambao wamebaki tutawalipa katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la askari, tumeshaomba tayari kuongezewa tena kwa mwaka huu askari waajiriwa ambao tayari tumeshapata kibali tunaamini kwenye maeneo ambayo yana changamoto za wanyama wakali na waharibifi tutaendelea kuongeza nguvu na vituo kujengwa ili angalau tupunguze athari hii ya wanyama wakali na waharibifu.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, hata hivyo nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kuwa Bwawa la Olua ambalo lilizinduliwa na Mwalimu Nyerere tarehe 15 Julai, 1977, yeye mwenyewe aliahidi kwamba atatoa eneo kwa ajili ya scheme ya umwagiliaji kwa kutumia maji ya bwawa hilo.

Je, ahadi ya Rais tangu lini ilifutwa?

Swali la Pili; kwa kuwa Mawaziri sita wa Maliasili wameshalitembelea eneo hilo tangu mwaka 2010 na Waziri wa mwisho alikuwa Mheshimiwa Dkt. Hamis Kigwangalla mwaka 2019: -

Je, ni lini ahadi ile ya Mheshimiwa Rais na ahadi ya Waziri wa Maliasili itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph George Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nirejee tu kwenye jibu langu la msingi kwamba maeneo haya yanapokuwa yameombwa mara nyingi wataalam wanaenda kuhakiki na wanaangalia kama kuna maeneo ambayo ndani yake kuna wanyama wakali na waharibifu hususani tembo, pia tunaangalia vitu mbalimbali ikiwemo masuala ya ikolojia wataalam walipoenda kuangalia walikuta umuhimu wa maeneo haya kuendelea kuhifadhiwa, na hii ahadi iliyotolewa ilikuwa ya mwaka 1977, tunatambua kabisa hifadhi hizi zinasimamiwa na Halmashauri lakini pale ambapo kunakuwa na umuhimu wa kuwaachia wananchi basi Serikali inafanya tathmini na inarejea na kuwarudishia wananchi waendelee kuyatumia kwa ajili ya shughuli nyingine.

Mheshimiwa Spika, naendelea kumuomba tu Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi bado ipo, tathmini itaendelea kufanyika na pale ambapo tutaona kuna umuhimu wa kuyarejesha haya maeneo basi tutafanya hivyo.
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini mwaka 2021/2022 ambao mashamba yao yaliliwa mashamba yao hawajalipwa fidia yao. Je, Serikali itawalipa lini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maboto Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumejitahidi sana kupunguza madai ya kifuta machozi na kifuta jasho, kwa upande wa Mkoa wa Mara ninaahidi tu kupitia Bunge lako hili ndani ya kipindi hiki tunachoendelea na bajeti tutaenda kumalizia madai haya. Ahsante.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Swali la kwanza; je, Serikali yetu sikivu ninavyoielewa mimi, haioni umuhimu wa kujenga mahusiano mema kati ya hifadhi na wananchi kwa kuwapa eneo la kuweka mizinga yao na kufuga mifugo yao kama walivyozoea na hasa kutokana na ongezeko la watu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; hivi Serikali haioni kuna haja ya kumaliza suala ambalo linaulizwa kila mwaka kwa kulipatia ufumbuzi wa kudumu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika,
ahsante. Naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Jimbo la Urambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, niahidi tu kwamba tutaangalia maeneo mengine yaliyo jirani na eneo hilo ili warinaji wa asali, hususan wale wafugaji wa nyuki, tuweze kuwahamisha ili tuwapeleke katika misitu ambayo inaendana na uhifadhi wa mazingira yanayohusiana na ufugaji nyuki.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Timu ya Mawaziri Nane ilikuja katika Kata ya Kigwa na kutuahidi kutupa eneo katika Kigwa Rubuga. Je, ni lini Serikali itaweka mipaka mipya katika maeneo hayo ili wananchi wajue mipaka yao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika,
ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Venant Daud Protas, Mbunge wa Igalula, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tulikuwa na kazi ya kufanya tathmini, kamati hii iliandaliwa na Kamati ya Mawaziri Nane na tayari wengi wameshamaliza kazi yake. Kazi inayofanyika sasa hivi ni kuainisha mipaka na kuweka vigingi. Hivyo, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Igalula kwamba wakati wowote tutaendelea kufanya kazi ya kuweka vigingi.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, naomba niulize maswali yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; takwimu ananzozieleza Naibu Waziri sio sahihi. Takwimu ambazo ninazo za waathirika wa wanyama waharibifu ni zaidi ya watu 200.

Je, Waziri yupo tayari kumwagiza Afisa wake aliyopo pale Masasi aende akafanye mapitio mapya ya waathirika wote walioathirika na Wanyama waharibifu hasa tembo katika Kkata ya Sengenya, Kijiji cha Mkumbaru, Chinyanyera, Igunga; Kata ya Nangomba Kijiji cha Chihuve; Kata ya Luimesule; na Kata ya Masugulu? Takwimu hizi sio sahihi kwa hiyo namuomba Waziri afanye hayo kama nilivyomwelekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili; fidia wanazolipwa waathirika ni ndogo kuliko hali halisi ilivyo. Waathirika hawa wanaopoteza maisha yao fidia ni ndogo, wanaopata ulemavu fidia ni ndogo na wanaoharibiwa mashamba yao fidia ni ndogo. Je, Waziri yuko tayari kuleta Muswada hapa wa kurekebisha viwango hivi ili wananchi walipwe haki sawa kulingana na hali halisi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahya Ally Mhata, Mbunge wa Jimbo la Nanyumbu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Mbunge kwenye hili suala la takwimu nitazichukua kutoka kwake, lakini pia tutaenda kuhakiki upya katika maeneo hayo ili wananchi waweze kulipwa stahili yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande huu wa fidia sheria ya mwaka 2011 iliyopitisha kifuta machozi na kifuta jasho ilikuwa na madhumuni ya kumshika mkono mwananchi, lakini ukiangalia namna ya kufidia mfano maisha ya mwananchi ambaye amepoteza maisha ni ngumu sana kufidia au mtu ambaye amepata ulemavu, hivyo sheria hii ilipitishwa kwa ajili ya kumshika mkono mwananchi kumwonesha kwamba Serikali iko pamoja naye.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo katika Bunge lako hili mwaka jana tulipewa maelekezo ya kuzipitia upya Kanuni zake zinazohusiana na masuala ya kifuta machozi na jasho na hivi karibuni tutaileta katika Bunge lako hili kwa ajili ya kuipitia ili tuweze kuongeza kiwango hiki na Kanuni zirekebishwe, ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Endapo ikitokea mwananchi ameua tembo au gari limegonga tembo au mnyama yoyote faini anayotozwa ni kubwa sana, lakini ikitokea vinginevyo kwamba mnyama amemuua mwananchi au ameharibu mazao yake, sheria haimpi haki mwananchi. Je, nini kauli ya Serikali ku-balance haya mambo ili kuhakikisha kwamba Mtanzania anapata haki yake ndani ya nchi yake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Paresso, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tutambue kwamba hawa wanyama ambao tunao katika nchi yetu ni rasilimali za Taifa na wanalindwa kisheria kama ambavyo tunawalinda wanadamu na tutambue kwamba changamoto hii ya wanyamapori wakali na waharibifu imeanza hivi karibuni. Miaka ya nyuma wanyama hao walikuwa wanaishi kwa uhuru na salama kabisa na hatukuwahi kuwa na changamoto hizi. Kwa hiyo ukiangalia mahitaji ya ardhi, ongezeko la watu tumeendelea kusogea katika maeneo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukisema leo hii changamoto hii tuielekeze kwenye faini, mzigo ni mkubwa sana kwa Serikali hautaweza kugharamia hasara ambayo itaweza kujitokeza. Kwa hiyo tunaendelea kuhamasisha wananchi kwamba tusiendelee kuyasogelea maeneo haya na ndio maana kanuni hii ilitungwa kwa wale ambao Wanyama wamewafata basi tunawashika mkono ili kuhakikisha kwamba Serikali inaonesha kwamba iko nao.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri kuna kero ya popo Kata ya Kivukoni Jimbo la Ilala. Hawa popo ni waharibifu, wanachafua mazingira na wananchi walishalalamika mpaka leo bado. Hebu tueleze mnachukua hatua gani kwa upande wa popo Kata ya Kivukoni? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Naibu Spika, ni kweli kuna changamoto ya popo ambao wamezunguka katika maeneo ya Dar es Salaam hususan maeneo yanayozunguka Ikulu. Serikali imeshaanza kuyafanyia kazi tulishawahi kufanya kazi ya kuwapuliza kwa maana ya kuwapunguza, lakini changamoto tunayoipata ni kwamba tunapowaondoa wanaruka wanaondoka, lakini kuna muda ambao wanarudi. Sasa tumeshaanza utaratibu na Taasisi ya TAWIRI kutafuta mbinu mbadala kuhakikisha tunawaondoa kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuahidi kabla ya Bunge lako hili la bajeti kwisha, tutakuwa tayari tumeshakamilisha utaratibu wa kuwaondoa.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Je, ni lini mifumo ya malipo ya TANAPA, TAWA, Ngorongoro pamoja na ile ya Wizara itaunganishwa na kuwa mfumo mmoja wa malipo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ni lini Serikali itaruhusu uhai wa leseni za TALA uwe kwa mwaka ambao leseni imekatwa tofauti na sasa hivi ambavyo leseni inakuwa ni kalenda ya mwaka?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mifumo ya malipo katika taasisi zetu tayari imeshaanza kutumika. Baadhi ya taasisi kama Ngorongoro na TANAPA utekelezaji wake unaendelea, lakini baadi ya taasisi tayari tulishaunganisha. Kwenye upande wa leseni; sasa hivi leseni inatoka kwa mfumo mmoja tu ambapo imeunganishwa mifumo yote. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye suala la leseni wadau wote wanafaidika na mfumo huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye suala hili lingine la TALA, tumeshaanza kupokea maoni kutoka kwa wadau mbalimbali hususan wadau wa masuala ya utalii na tunaangalia tupitie kanuni upya tuone kama zitaleta tija katika marekebisho ya utoaji wa leseni. Nawakumbusha tu wadau hawa kwamba Serikali ina calenda year ambapo ndiyo huwa inakusanya mapato yake na imejiwekea mipango yake. Kwa hiyo, kama tutaona kuna haja ya kurekebisha kanuni hizi, basi tutawashirikisha kwa kuchukua maoni yao, lakini kwa kuangalia pia Serikali katika ukusanyaji wa mapato, ahsante. (Makofi)
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Ni standard ya kawaida kwa taasisi zote za Serikali, lakini hasa majeshi, kuwa na kiongozi mkuu wa taasisi husika kwa ajili ya chain of command, lakini Jeshi la Uhifadhi halina kiongozi mkuu kwa maana ya divisheni zile TFS, TAWA, TANAPA, kila mtu ana-operate mwenyewe anavyoona inafaa. Sasa ikitokea viongozi wakuu wa nchi wanataka kuongea na majeshi wao Jeshi la Uhifadhi wanampeleka nani kuwawakilisha?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mheshimiwa Naibu Waziri amejibu kwamba wakiona changamoto wataanzisha mchakato wa kubadilisha sheria ili kupata kamishna. Anataka aone changamoto gani ilia one sasa kuna uhitaji wa kuwa na Commissioner General wa Jeshi la Uhifadhi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Antipas Zeno Mgungusi, Mbunge wa Malinyi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeeleza kwenye jibu la msingi ni kwamba taasisi hizi zina majukumu tofauti. Ukiangalia utekelezaji wa majukumu yao unaendana sambamba na namna ambavyo majeshi haya yameundwa. Kwa mfano kwenye Taasisi za TANAPA na Ngorongoro, taasisi hizi zina baadhi ya vitu ambavyo vinaruhusiwa kutumika lakini kuna baadhi ya taasisi ambazo zinazuia kama TAWA na TFS.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano kwenye upande wa TAWA na TFS tunaruhusu masuala ya uvunaji na uwindaji wa kitalii. Kwa hiyo, utaona yale majukumu yenyewe ya taasisi yanatofautiana. Kwa hiyo, kila kamishna wa uhifadhi anatekeleza majukumu kulingana na muundo wa taasisi husika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa sasa hivi tunaona bado wanafanya kazi vizuri na wote wanaripoti kwa Katibu Mkuu, kwa hiyo mkuu wa nchi anapotaka kuzungumza na majeshi haya anazungumza na Katibu Mkuu ambaye ndio msemaji wa Wizara kwa upande wa utendaji.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa maoni yake, tunayapokea na pale ambapo tutaona kwamba kuna uhitaji sasa wa kuunda jeshi ambalo litakuwa na mwakilishi ambaye ni Kamishna Jenerali, basi tutafanya hivyo na tutapitia kanuni zetu ili tuendane sambamba na majeshi yaliyopo.
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri Kijiji hiki cha Ngaresero bado kina changamoto kubwa na ndio msingi wa swali la Mheshimiwa Mbunge wa Ngorongoro. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari kuambatana na mimi pamoja na Mbunge wa Jimbo la Ngorongoro kwenda kujionea hali halisi ya kijiji hiki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwashukuru na kuwapongeza Wabunge wa Mkoa wa Arusha hususan katika Jimbo hili la Ngorongoro na Mbunge wa Viti Maalum, Mheshimiwa Zaytun. Kama ambavyo Serikali imeendelea kutatua migogoro mbalimbali, mgogoro huu tutaenda kuushughilikia ili tukae na wananchi, tuweze kufikia muafaka na hatimaye pori hili liweze kufikia hadhi iliyotarajiwa.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nimeyasikia majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini nataka tu kumwambia kwamba, migogoro ipo kwa sababu wananchi wanachukuliwa wanawekwa ndani. Sisi hii tunai-term kama mgogoro. Maswali yangu mawili ya nyongeza ni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ameshawahi kutuambia tulete maombi Wizarani. Tumeshaleta maombi: Ni lini maombi yetu yatajibiwa ili kuwapa wananchi kipande cha ardhi ili waendelee kuendesha shughuli zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Je, kama maombi haya yakitoka yatakuwa hapana, Serikali inachukua hatua gani kuendelea kuwasaidia wakulima hawa wapate maeneo ya kulima kwa sababu, ni Watanzania na hawana mahali pa kwenda ili kuendelea kulea watoto wao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Condester, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Mheshimiwa aliwahi kuleta maombi yake na haya maombi mchakato wake unaendelea. Ila kwenye upande wa matokeo ya haya maombi kwamba, yatakuwaje, inategemea sasa na maeneo ambayo sisi tunayaona kama ni ya muhimu, hususan kwenye maeneo ambayo tunatunza vyanzo vya maji na maeneo ambayo ni muhimu kwa kuhifadhiwa. Kwa hiyo, Serikali itafanya tathmini na itaangalia umuhimu wa maeneo haya kwa ajili ya kutunzwa na Serikali na yale ambayo tutaona tunaweza tukayaachia, basi wananchi wataweza kufaidika na maeneo ambayo tutaweza kuyaachia.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku ya tarehe 22 Jumatatu, kumetokea vurugu na sintofahamu kubwa sana kati ya wananchi wa Kijiji cha Jangwani Eneo la Mto wa Mbu na Askari wa Uhifadhi wa Eneo la Ziwa Manyara na kusababisha mwananchi mmoja kufariki na wananchi kadhaa kujeruhiwa kwa risasi za moto: Je, ni kwa nini askari hawa wa uhifadhi wamekuwa wakitumia nguvu kubwa kukabiliana na hii migogoro kati ya wananchi na maeneo ya hifadhi kiasi kwamba, wananchi wanapoteza maisha na wengine wengi kujeruhiwa? Kwa nini kusiwe na njia nyingine mbadala kukabiliana na changamoto hizi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nifafanue kidogo kwa ridhaa yako. Kwa kawaida wahifadhi wanakuwa kwenye maeneo yao ya kutekeleza majukumu yao ya kawaida ya kila siku. Mgogoro huu ulijitokeza katika ziwa Manyara ambapo askari walikuwa katika shughuli zao za doria na waliweza kukamata wahalifu watatu ambao walikuwa wamevamia katika hifadhi hiyo. Baada ya wahalifu hawa kukamatwa ili wafikishwe kwenye vyombo vya kisheria kwa mujibu wa taratibu na sheria zilizopo, wavuvi zaidi ya 30 walijiunga kwa pamoja na wakaenda kuwavamia wale wahifadhi ambapo walikuwa katika maeneo yao ya doria ya kawaida. Kwa bahati nzuri walikuwa tayari wameshawafunga pingu wale wahalifu watatu, lakini wananchi walienda kuwashambulia hao askari. Katika kujiokoa, waliweza kuwaachia hao wahalifu wakakimbia na pingu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichotaka kusema hapa ni kwamba, suala linapofika kwenye vyombo vya sheria ama wahalifu wanapokutwa na hatia, basi tuache sheria ichukue mkondo wake; lakini inapofika wananchi wanaungana pamoja, wanalishambulia jeshi, jeshi lenyewe sasa linakuwa linaonekana halina nguvu. Kizuri zaidi na kwa kuwa, maelekezo ya Mheshimiwa Waziri yameshaelekeza kwamba tusitumie nguvu, hawa askari waliweza kukimbia na hawakuweza kufanya vurugu yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maandamano hayo, ilisababisha askari kujumuika na wahifadhi ili kuwatawanya watu. Watu walikuwa wengi sana kwa sababu waliungana, ni wanavijiji wa maeneo yale waliwazingira na kufanya maandamano, na walikuwa wanavunja magari, wakikutana na gari wanafanya uhalifu. Kwa hiyo, katika vurugu zile ndiyo zilisababisha sasa huyo mwananchi kufikwa na maafa hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunawaomba sana wananchi wajitahidi sana kuheshimu vyombo vya Dola vilivyopo kwa sababu, viko kisheria na vinatekeleza majukumu yaliyokasimiwa. Kizuri zaidi, hawa tumewakasimisha madaraka kulinda rasilimali za nchi. Kwa hiyo, tunapowashambulia, tunawapunguzia nguvu ya kulinda rasilimali zilizopo hapa nchini.
MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi. Kwa kuwa chanzo kikubwa cha migogoro ya wananchi na wanaoishi katika maeneo ya hifadhi na wahifadhi ni mipaka pamoja na alama zinazoonekana, lakini pia ni pamoja na kuzuia matumizi mseto katika maeneo ya WMA kinyume na mikataba iliyofungwa katika uanzishaji wa WMA hizo: Je, Serikali ina mkakati gani mahususi wa kuondoa changamoto hizo ili kuwezesha wananchi kuishi kwa ushirikiano mwema na wahifadhi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kimsingi Serikali inatamani sana kuimaliza hii migogoro, lakini tunatambua kwamba mahitaji ya ardhi sasahivi ni makubwa, wananchi wanaendelea kuongezeka na kila mtu anatamani kumiliki ardhi. Ardhi iliyobaki ni ardhi iliyohifadhiwa ambayo ni inasimamiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii na utalii. Kwa hiyo, kumekuwa na hizi changamoto za hapa na pale na mara nyingi wananchi wanasema ni migogoro, lakini sisi tunasema siyo migogoro kwa sababu, maeneo yana mipaka yake, yana ramani zake, yana GN zake. GN zipo na zinajulikana, isipokuwa pale ambapo kunakuwa na sintofahamu ya mpaka, tunaenda kuufafanua kwa kuweka vigingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naendelea kuwaomba wananchi kwamba sisi tunaendelea kuongezeka, lakini ardhi ni ile ile. Tuendelee kuheshimu haya maeneo kwa mustakabali mzima kabisa wa Serikali na kwa vizazi vinavyokuja. Tunatunza haya maeneo siyo kwa sababu tu yameangaliwa, tunatunza kwa sababu tunaendelea kuongezeka.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wilaya ya Liwale ina WMA ya Magingo, lakini uanzishwaji wa TANAPA, ile Hifadhi ya Mwalimu Nyerere imeingia kwenye maeneo ya WMA ya Magingo katika Kitalu cha Nachengo, Kijiji cha Mpigamiti na Ndapata na Kimambi: Je, Serikali inachukua hatua gani kwenda kutatua migogoro hii iliyoletwa na uanzishwaji wa Hifadhi ya Mwalimu Nyerere?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaenda kuufafanua huo mpaka na kutafsiri mpaka ili WMA ziweze kufanya kazi zake na Hifadhi ya TANAPA iendelee na shughuli zake.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, licha ya majibu mazuri ya Serikali ya kuitangaza Hifadhi ya Kitulo lakini Serikali ina mradi wa regrow mradi ambao umejikita kwenye kutangaza utalii Kusini mwa Tanzania na hifadhi hii ni hifadhi ya kipekee Barani Afrika na Tanzania, kwa nini mradi regrow haujaenda kwenye Hifadhi ya Kitulo ili uweze kuisaidia hifadhi hii kutangazwa kwa ukubwa zaidi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwenye Hifadhi ya Kitulo kumekuwa na changamoto ya kimahusiano kati ya wananchi na hifadhi kwa maana ya migogoro ya mipaka. Sasa katika jitihada za kutangaza utalii ni upi mkakati wa Serikali kutatua migogoro iliyopo kwenye vijiji vya Misiwa, Ujuni, Nkondo, Makwalanga, Lugoda na Igenge. Vijiji hivi kwa muda mrefu vimekuwa na mgogoro na hifadhi, upi mkakati wa Serikali kutatua mgogoro huu ili mahusiano yaweze kuimarika kati ya hifadhi na Wananchi wa Wilaya ya Makete?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Richard Sanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa miradi ya regrow, mradi wa regrow phase one ulikuwa unawezesha kufanya maboresho katika hifadhi nne ambazo ilikuwa ni Mikumi, Nyerere, Udzungwa na Ruaha, lakini Serikali inatarajia kuingia mkataba tena kwenye REGROW Phase Two ambayo Hifadhi ya Kitulo pia itaingizwa katika mradi huo. Kwa hiyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Kitulo itaingizwa kwenye phase two na maboresho yatafanyika.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa migogoro tulishapeleka tathmini tayari ilishafanyika na sasa hivi ni utekelezaji tu wakuainisha mipaka mipya. Kwa hiyo, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi sasa naomba nielekeze tu TANAPA waende kuweka vigingi katika maeneo ambayo yameainishwa baada ya tathmini kuwa imefanyika lakini na sisi pia tutaenda kujihakikishia.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwanza niseme siridhiki na majibu ya Serikali kwa sababu hizo jitihada zimefanywa na wananchi na takribani watu 24 ndani ya miaka mitatu wakiwemo Watoto wameuawa na fisi. Sasa swali langu;

a) Je, ni lini na kwa uhakika hilo jeshi la uhifadhi litafika katika eneo hilo na kuwavuna fisi hao ili wananchi waendelee kukaa kwa amani?

b) Je, ni lini, Serikali itakuja na mkakati wa kutoa elimu kwa wananchi ili yanapotokea majanga kama hiyo waweze kujihami na kukabiliana na Wanyama wa namna hiyo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwenye swali lake la nyongeza linalohusiana na lini Jeshi la Uhifadhi litaenda kuwasaka, naomba tu niendelee kuelekeza kuanzia sasa kwamba Jeshi la Uhifadhi Kanda ya Kaskazini waelekee Karatu, wakaamnze kufanya msako wa fisi hao ili wananchi waweze kuona umuhimu wa uhifadhi lakini pia fisi hao waweze kurudishwa hifadhini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala hili la elimu. Kwa sasa hivi tumeanza programu za kufundisha au kuelimisha wananchi namna ya kujikinga na wanyama wakali na uharibifu. Kwa hiyo naendelea kuelekeza kwenye upande wa Kanda ya Kaskazini kwamba, pamoja na msako huo utakaofanyika pia watoe elimu kwa wananchi ili tuweze kuwa na mashirikiano ya pamoja.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Mbali na fisi kusumbua wananchi na kuleta madhara kwa watu wenye hifadhi pia kumekuwa na tatizo kubwa la mamba katika Ukanda wa Ziwa Victoria hasa maeneo ya Tairo na Guta Pamoja na Wilaya ya Bunda upande wa Mwibala;

Je, nini tamko la Serikali katika kuhakikisha mnaenda kuvuna mamba hao?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwenye upande wa mamba tumeshaanza programu ya kutengeneza vizimba na kuwafundisha wananchi namna ya kujikinga nao. Kwa sababu tatizo linajitokeza ni pale ambapo wananchi walizoea kuogelea ziwani, wengine wana mazoea ya kwenda kucheza kandokando ya ziwa. Nakumbuka enzi za zamani hasa wale tulioishi Kanda ya Ziwa, tulikuwa tuna maeneo yetu ambayo huruhusiwi kwenda kucheza maeneo hayo kwa sababu kuna Wanyama wakali hususan mamba na viboko.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kadri tunavyozidi kuongezeka wananchi wanaendelea kuyasogelea yale maeneo. Kwa hiyo tunaendelea kuwaelimisha wananchi kama yale mazoea ya wananchi ya kila siku ya Kwenda kuogelea kama ilivyo zamani tuyaache, na matokeo yake tunatengeneza vizimba kama wanaenda kuchota maji basi waende kwenye maeneo yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kadri tunavyozidi kuongezeka wananchi wanaendelea kuyasogelea yale maeneo. Kwa hiyo, tunaendelea kuwaelimisha wananchi kwamba, yale mazoea ya kila siku ya kwenda kuogelea kama ilivyokuwa zamani tuyaache na matokeo yake tunatengeneza vizimba, kama wanaenda kuchota maji, basi waende kwenye maeneo yale tu ambayo yameainishwa, ili kuepuka hii athari inayojitokeza ya hasa watoto wanachukuliwa na mamba na inakuwa ni athari kwa wazazi pia na kwa jamii kwa ujumla. Kwa hiyo, tunawaelimisha wananchi pia waendelee kuyaheshimu haya maeneo.
MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia kwenye mbuga zetu kuna Askari pamoja na Maafisa wengine ambao wanazilinda hizo mbuga. Ukienda kule kwenye mbuga utakuta kuna vibanda vya wafugaji wanaishi huko pamoja na rundo la mifugo wakati Serikali wanasema kwamba wameweka zuio. Je, hao wafugaji walioko kule na hivyo vibanda hawa Askari hawawaoni? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili. Inasemekana kuna baadhi ya Maafisa Wanyamapori ambao siyo waaminifu, wanashirikiana na wale watu wenye mifungo kuwaingiza katika hifadhi zetu. Je, Serikali inasemaje katika hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aleksia Kamguna, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hawa Askari wanakuwepo katika maendeo ya hifadhi, changamoto ambayo tunakutana nayo hasa kwenye mapori ambayo yameungana na mapori ya Halmashauri na mengine ni mapori ya Vijiji. Kwa mfano, kama Hifadhi ya Nyerere, tuna Hifadhi ya Selous lakini kuna mapori ambayo yameungana na Hifadhi ya Nyerere. Kwa hiyo, utakuta kwamba kwenye Pori la Selous Askari wanafanya operesheni, pale ambapo kunakuwa na mifugo, inakamatwa na inachukuliwa hatua lakini wale wamiliki wahiyo mifugo wanaenda wana-pause kwenye yale mapori ya Halmashauri pamoja na Vijiji ambapo sasa kule askari wetu hawafiki katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, changamoto hiyo imekuwa kubwa kwa sababu hii mifungo ipo na inakuwa kando kando tu inakuwa imeegeshwa pale ambapo Askari wetu wanapoondoka tu tayari mifugo inaendelea kuingia hifadhini, lakini kulingana na sheria zetu, nadhani wanafahamu wafugaji namna ambavyo tunasimamia kanuni, taratibu na namna ambavyo tunaendelea kuzishughulikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hili suala la Askari kushirikiana na Wafugaji. Ni kweli tuna sheria kali sana na pale inapogundulika kwamba Askari anashirikiana na kukiuka kanuni na taratibu zilizopo, tunamchukulia hatua mara moja na wengine wanafukuzwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii sheria tunatumia Sheria ya Jeshi ambayo tayari sisi tumeshaanza kuingia katika utaratibu huu na wengi wameshachukuliwa hatua. Kwa hiyo, ikithibitika kwamba kuna Askari amefanya hivi basi tupate taarifa mara moja na tuweze kuchukua hatua. (Makofi)
MHE. RIZIKI S. LULIDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Lindi sasa hivi, eneo la Selous pamoja na Mbuga ya Tendeguru kuvamiwa na wafugaji. Mheshimiwa Naibu Waziri ni shahidi, alikwenda akawakuta wafugaji wako ndani ya mbuga, wakichoma mikaa katika Misitu ya Tendeguru na kumaliza Miti ya Mipingo lakini kusababisha sasa hivi taharuki, Wafugaji kutoka katika misitu, kwenda kuvamia mashamba ya watu. Sasa hivi Mkoa wa Lindi tuko katika taharuki kubwa ya mapigano ya wafugaji na wananchi.

Je, Mheshimiwa Waziri aliyepo pale anatoa tamko gani leo hapa kwa vile aliyaona haya lakini utekelezaji wake haukukamilika mpaka hivi sasa?

Mheshimiwa Naibu Spika, nawasilisha swali langu. Ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Sisi kama Serikali tumeshajipanga, kwa maana ya Wizara ya Maliasili na Utalii pamoja na Wizara ya Mifugo na Uvuvi, tukae pamoja kwa sababu suala hili ni suala la wananchi wetu na hao wananchi nao wanayo haki ya kuishi kama Watanzania. Tunachokifanya sasa hivi tunasimamia sheria upande mmoja lakini upande wa pili wanaegesha tu wanasubiria kuingia tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo sisi kama Serikali tukae pamoja, tuone namna iliyo bora ya kuwahudumia hawa wafugaji ili changamoto hii sasa isiendelee kujitokeza. Kwa sababu sasa hivi sisi tumepewa dhamana.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spikja, ahsante, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni nimefanya ziara Wilayani Monduli na moja kwa moja Mheshimiwa Waziri wa Maliasili alizungumza na wananchi wa Monduli, akawaahidi baada ya wiki moja ya ziara yangu ataenda na wataalam wake kutatua kero hii, lakini mpaka leo hii Waziri hajaonekana. Matokeo yake mwezi uliopita mwananchi mmoja katika Kata ya Makuyuni eneo la Ndoroboni ameuawa na tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tatizo la tembo limekuwa kero kubwa sana kwa Tanzania nzima, wamekuwa wanazagaa zagaa ovyo na kuharibu mazao na kuua wananchi, Serikali imekuwa inatupa majibu hatuoni matokeo yake. Sasa leo nataka kufahamu nini kauli ya Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni kweli kumekuwa na tatizo hili la changamoto la wanyama wakali na waharibifu, ni changamoto sasa takribani miaka minne inaendelea kuongezeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imechukua hatua za haraka. Moja ya hatua za haraka ni kwamba tumeanza sasa hivi kuwarudisha hawa wanyama wakali kwa kutumia helikopta, kuna baadhi ya maeneo tayari tulishaanza kwenda. Wakati huo huo tunaendelea kutoa elimu kwa wananchi kwa sababu ukiangalia maafa kwa asilimia kubwa yanajitokeza ni pale wananchi hawana elimu, wengine wanafukuza kwa kutumia fimbo na kadhalika. Kwa hiyo tunaendelea kuitatua hii changamoto wakati huo huo na kutoa elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua nyingine ya haraka ni kwamba sasa hivi tumeamua tutapeleka Askari ambao watakaa katika maeneo husika kwa muda mrefu. Suala la kupigia simu Askari ndiyo wafike sasa hivi tunataka kuliacha na tunataka hawa Askari kwenye maeneo yale hatarishi wakae maeneo yale wakishirikiana na wale VGS (Village Scouts) ili kuondoa hili tatizo kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuna operesheni ambayo tumeipanga na Mheshimiwa Waziri ameelekeza na tayari tutaingia kazini mara moja. Kwa hiyo, naomba niwatoe wasiwasi wananchi kwamba Serikali inalishughulikia suala hili kwa karibu sana na haya ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais, pamoja na Mheshimiwa Waziri Mkuu, umetuelekeza tulishughulikie kwa uharaka, tunatambua wananchi wanaumia lakini naomba nitoe kauli hii kwamba wananchi tutawafikia muda siyo mrefu. Ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na niishukuru Serikali kwa majibu mazuri, lakini niiombe uhakiki huu unaoshirikisha wananchi uhusishe pia Kijiji cha Chunya - Kata ya Mpapa; Kijiji cha Barabara - Kata ya Matili; lakini pia Kijiji cha Kimbindachini - Kata ya Muungano. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mbinga ni milimani, na kwa hiyo, sasa kutokana na uhifadhi maeneo mengi ya milimani tunapewa…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kapinga naomba uulize swali moja kwa moja. Swali la kwanza na la pili, tafadhali; uliza swali lako la msingi.

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio nilikuwa nauliza swali hapo, kwamba basi acha ulivyonielekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango gani wa kutoa elimu kuwafanya wananchi hawa waweze kuishi na misitu katika milima iliyopo Wilaya ya Mbinga? Swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Serikali inatoa kauli gani katika maeneo yaliyoanzishwa Miradi ya Panda Miti Kibiashara bila kushirikisha wananchi, ili kuwarejeshea maeneo haya wananchi husika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kapinga, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mpango wa kutoa elimu, nitoe tu maelekezo kwa watendaji wa Wizara ya Maliasili na Utalii hususan Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania, tunapoenda kuainisha hii mipaka wahakikishe kwamba tunashirikisha wananchi walioko katika maeneo hayo ili kuwepo na urahisi wa kutambua mipaka iliyopo na kuondoa migogoro inayoweza kujitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili nimuahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutalizingatia, lakini pia tutaendelea kutoa elimu ya namna ya uhifadhi wa mazingira kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili la pili ambalo amelisema kwenye Mradi wa Panda Miti Kibiashara; kikawaida mradi huu unawawezesha wananchi kujiinua kiuchumi kupitia mazao ya miti, na mara nyingi tunashirikisha wananchi kabla ya mradi huu kufika katika eneo husika. Kwa hiyo, kama kuna maeneo ambayo tumepeleka mradi huu halafu hatukushirikisha wananchi, basi tumefanya makosa na tutaenda kupitia upya utaratibu uliopo ili wananchi waweze kufaidika na miradi hii ya Panda Miti Kibiashara.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika Awamu ya Tano ambayo kupitia RIGRO walipendekeza kwamba lengo kubwa ni kukuza utalii Kusini na walichagua Mkoa wa Iringa uwe ni makao makuu ya mradi huo. Sasa tumeshatenga eneo lipo na kila mwaka tunaadhimisha wiki ya utalii pale Mkoa wa Iringa.

Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha utekelezaji wa makao makuu haya unafanyika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba wananchi walioko pembezoni mwa mbuga hii wanapata elimu, wanawezeshwa kielimu na kiuchumi kuhakikisha kwamba wao ndio watakaokuwa watangazaji wa mbuga hii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwanza niendelee kuwapongeza Wabunge wote wa Iringa, pamoja na kuwa swali hili na Mheshimiwa Grace Tendega, lakini mara nyingi wanafuatilia sana kwenye mradi huu wa RIGRO na ujenzi wa information center ambayo itajengwa Makao Makuu Iringa uko kwenye hatua za kuanza. Tayari tulikuwa kwenye mkakati wa mkandarasi ambaye tayari tulikuwa tumeshatangaza kazi na tuko anytime kuanza kazi hii. Kwa hiyo, naomba niwataarifu tu kwamba Wana-Iringa na Watanzania wote kwa ujumla kwamba utalii na mkakati wa kukuza utalii Kusini mwa Tanzania uko mbioni kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili la kuwapa elimu wananchi wanaoishi pembezoni mwa hifadhi; kwenye Mradi wa RIGRO zimetengwa fedha kwa ajili ya kuwapeleka training wananchi mbalimbali waliozunguka katika maeneo yanayozunguka mradi huu, na ni shahidi tosha Wabunge wanaotoka katika maeeo hayo wanafahamu kwamba tumekuwa tukipeleka watoto ambao wanapelekwa shuleni kwa ajili ya kujifunza namna ya kuendeleza masuala mazima ya utalii na uhifadhi. Kwa hiyo, faida wameshaanza kuziona na wananchi wameshaanza kuona faida ya mradi huu.
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya changamoto kubwa kwenye sekta hii ya utalii ni uhaba wa hoteli zenye hadhi ya kulaza wageni wetu; je, Serikali ina mkakati gani wa kutatua changamoto hii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa sasa tayari Serikali imeshaanza kutangaza maeneo ya uwekezaji na tayari wawekezaji wameshaanza kujitokeza. Kwa hiyo, suala la uhaba linaenda kupungua ama kuisha kabisa kutokana na uzinduaji wa filamu ya Royal Tour na mkakati wa uwekezaji ambao tayari tumeshaanza kuuweka.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwa ajili ya kuongeza idadi ya watalii na kuboresha uhifadhi katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti; je, ni lini ujenzi wa uwanja wa ndege wa Serengeti utaanza?

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba tu niwataarifu ndugu zangu wana-Serengeti, hususan Mugumu kwamba mchakato unaendelea na uko kwenye hatua za utekelezaji kwa maana ya kuanza. Tayari tulishaanza mchakato na namna ya ku-identify hayo maeneo na lengo ni kuhakikisha kwamba tunapunguza muingiliano wa shughuli za uhifadhi katika Hifadhi ya Serengeti, hivyo uwanja tutauhamisha usogee katika Eneo la Mugumu. Kwa hiyo, mchakato unaendelea.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya jitihada za kuongeza watalii dunia nzima ni kurahisisha miundombinu, hasa barabara na mageti kutokea kila upande. Kuna maelekezo ya Serikali pale Mbuga ya Mikumi kufungua geti lingine kwa upande wa Kilangali na Tindiga ili kurahisisha usafiri wa watalii kutokea Kilosa kwenye station ya SGR itakapokamilika.

Je, Serikali ina kauli gani? Lini geti hili linaenda kufunguliwa kuheshimu maelekezo ya Makamu wa Rais, lakini wewe pia Naibu Waziri ulipoitembelea Mikumi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, tunatambua kwamba, geti hili ni la muhimu sana kwa ajili ya uchumi wa nchi, hususan katika masuala mazima ya utalii na tayari tulishaanza mpango wake. Kwa hiyo, nimuondoe shaka Mheshimiwa Mbunge wa Mikumi kwamba geti hili tutalifungua na pale tu ambapo mchakato wa reli utakavyoanza tayari na sisi utekelezaji wake utakuwa umekamilika.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante, wananchi wa Ushetu wanaheshimu sana mipaka ya Serikali kwenye mapori yetu na ni walinzi wazuri sana, lakini idadi ya ng’ombe wa wananchi wa Ushetu inazidi kuongezeka. Mpaka sasa Wananchi wa Ushetu wana ng’ombe 176,000 na wanapakana na mapori haya hawana kabisa eneo la kuchungia.

Je, Serikali itamaliza lini hii tathmini ili wananchi hawa waweze kupata sehemu ya kulishia mifugo yao, badala ya kuendelea kugombana na watu wa maliasili?

Swali langu la pili, Halmashauri ya Ushetu ina mapori matatu. Inayo pori la Usumbwa Forest Reserve, Ubagwe Forest Reserve pamoja na Mpunze Saba Sabini, lakini Ubagwe Forest Reserve imekuwa na mgogoro mkubwa sana na Halmashauri ya Kaliua ambao umechukua sura mpya. Hata juzi wananchi wangu wamekamatwa wakawekwa ndani bila sababu za msingi, mbaya zaidi juzi kumekuwa na mgogoro kati ya maliasili wa TFS na Askari wa Maliasili wa Ushetu, Mheshimiwa Naibu Waziri huo mgogoro anaujua nilimtaarifu.

Nini kauli ya Serikali na Mheshimiwa Waziri ni lini tutaenda kutatua mgogoro huu kwa wananchi wangu?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Katika eneo hili la kulishia mifugo, ninaendelea tu kumshauri Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Ushetu kwamba, kwa kuwa Wizara ya Maliasili imepewa dhamana ya kuyalinda na kuyasimamia maeneo haya, inapofika suala la mahitaji ya maeneo ya mifugo basi waendelee kuwasiliana na Wizara husika ili tukae Pamoja, tuone namna iliyo bora ya kutenga maeneo haya, tumepewa kazi ya kuyasimamia tu na kuyatunza maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, suala lingine hili la kuhusu mipaka na migogoro kati ya TFS na Pori la Usumbwa Forest Reserve tunaendelea kuangalia namna ya kuainisha mipaka na kwa kuwa sote ni Serikali moja kwa maana ya Halmashauri na TFS, hakuna haja ya kugombania mipaka isipokuwa ni masuala ya kiutawala tu kwamba hawa ni TFS na hawa ni Halmashauri ni kukaa pamoja tu ili sote tulinde haya mapori kwa pamoja.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na uwepo wa mwongozo huo wa mwaka 2017, bado kumekuwepo na ongezeko kubwa la kuvuna miti kiholela. Hata wale ambao wanapatiwa vibali, anapewa kibali cha kwenda kuvuna miti mifu anakwenda kuvuna miti hai. Yametokea kwenye Vijiji vya Mshara na Uswaa, na Mto wote wa Makoa ule unaharibika: -

Je, hamuoni ni wakati sahihi sasa wa kuongeza nguvu wa kushirikisha ODC na mikutano mikuu ya vijiji?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa mwongozo huu ni wa muda mrefu sasa, hamuoni ipo haja ya kufanya maboresho ya mwongozo huu ikiwa ni pamoja na kuongeza kipengele kwamba wale wanaopewa vibali vya kuvuna miti na wao wapewe miti kadhaa ya kupanda kwenye maeneo ambayo wanavuna miti?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kuhusu hili ongezeko la ukataji miti hovyo, hususan kwa hawa wavunaji, ni kweli kumekuwa na ongezeko hili, lakini kwenye ile kamati tulitarajia kwamba mwongozo huu usimamiwe vizuri kwa sababu Mwenyekiti wa Serikali ya kijiji ni mjumbe wa kamati ya uvunaji ya wilaya. Kwa hiyo tunatarajia anapoitisha vikao vya vijiji tayari wanakijiji wote wanakuwa wanajua kwamba eneo lao linakwenda kuvunwa, na ujumbe unaotoka kwa wanakijiji anauchukua mwenyekiti na anaingia kule kama mjumbe anaufikisha.

Mheshimiwa Spika, wakati huohuo kuna kamati ya mazingira na kamati ya maliasili ambazo ziko chini ya Serikali ya kijiji, zote hizi zinapitisha utaratibu wa namna ya kuvuna. Kwa hiyo sisi hatuoni kama kuna haja ya kubadilisha mwongozo, isipokuwa usimamizi wa ule mwongozo ndio tunatakiwa tuuboreshe zaidi, kwa maana ya kwenda chini na kufuatilia zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili suala la pili la kuangalia kipengele kwa wale wanaovuna, kwamba kuwepo na haja ya kurejesha, kwa maana ya kupanda miti; kuna asilimia tano ya mvunaji; anapokuwa ameshapata kibali cha kuvuna anarejesha asilimia tano na inarudishwa kwenye halmashauri ya wilaya. Ile asilimia tano ya fedha zinazotokana na uvunaji inakwenda kurudisha uoto wa asili kwa kupanda miti. Kwa hiyo tunazielekeza halmashauri kwenye ile fedha inayorudishwa ya uvunaji wahakikishe kwamba inakwenda kwenye matumizi ya upandaji miti ili kurudisha uoto wa asili.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza naishukuru Serikali kwa hatua tuliyofikia. Pia namshukuru Naibu Waziri kwa juhudi kubwa aliyoifanya mpaka mahali tulipofika. Naamini hatakata tamaa, tumalizie kabisa.

Mheshimiwa Spika, maswali yangu mawili ya nyongeza: La kwanza, kwa kuwa sasa Iringa inakwenda kuwa lango la utalii kusini. Ni namna gani Serikali imejipanga kuhakikisha kwamba tunaingiza tamaduni, mazingiira ya Iringa, watu wa Iringa, vivutio vya Iringa ili viwe sehemu ya kutoa taarifa au picha halisi kwa watalii watakaokuja kusini?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Mmejipanga vipi kuhakikisha kwamba viongozi wakiwepo Waheshimiwa Madiwani wanapewa semina kuhakikisha kwamba wanaupokea utalii kusini? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza niwataarifu tu wananchi wa Iringa hususan mikoa yote iliyoko kusini mwa Tanzania, kwamba malengo ya Serikali ni kuhakikisha tunatanua wigo kwa masuala mazima ya utalii. Ujenzi wa kituo hiki unaendana sambamba na kutanua wigo wa masuala mazima ya utalii. Kwa hiyo, tuna Hifadhi ya Ruaha katika maeneo yale ya jirani, lakini tutahakikisha tunaunganisha package zote za masuala ya utalii ikiwemo masuala ya utamaduni, masuala ya kihistoria, tunaunganisha na utalii wa wanyamapori. Haya yote yatakuwa yanaunganishwa kwenye package moja ambayo tutaisaidia sasa sekta hii iweze kukua katika maeneo mazima yaliyoko kusini mwa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala lingine hili la viongozi wa kisiasa hususan Waheshimiwa Madiwani, kwa kuwa tunaanzisha kituo mahususi hiki, lazima tutatoa elimu kwa wananchi na viongozi ili nao watusaidie kutoa promotion katika maeneo hayo na pia waweze kutembelea vivutio hivi, kwa sababu tunaamini kiongozi anapofika katika eneo hilo, tayari anawahabarisha hata wengine ambao hawajawahi kufika katika eneo hilo. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, katika kuendeleza utalii ukanda wa kusini, Kata ya Kisaki kuna eneo linaloitwa Kisaki Majimoto ambapo kuna chemchemi inayochemsha maji kiasi hata cha kuweza kulifanya yai likaiva, je, Wizara ina mpango gani wa kutambua eneo hilo na kuliingiza katika kivutio cha utalii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nimtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mkakati wa Wizara ni kuhakikisha maeneo yote ambayo yana vivutio vya kihistoria ikiwemo Majimoto; tuna maeneo mengi ambayo yana majimoto na eneo ambalo anatoka Mheshimiwa Mbunge, lakini tuna maeneo mengine mengi ambayo yana vivutio ambavyo bado hatujaviibua. Tunataka kila Mkoa, kila wilaya angalau mtalii yoyote anayefika katika eneo hilo, basi aweze kuona kivutio kilichopo katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba mkakati tulionao ni mkubwa, tunachotafuta sasa hivi ni fedha ya kutosha ili mambo yasonge mbele.
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na nia njema ya kutumia SUMA JKT kwa ajili ya kuongeza nguvu kwenye jeshi la uhifadhi na ninajua malipo yao kidogo ni makubwa ukilinganisha na watu ambao wana- volunteer; je, Wizara sasa haioni haja ya kutumia vijana ambao wapo kambini au mtaani lakini hawapo SUMA JKT? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, vijana wetu waliomaliza elimu ya wanyapori kwa maana ya Mweka, Pasiansi na Olmotonyi ambao wapo mtaani kwa sasa, Wizara haioni haja ya kuwapa mkataba wa muda mfupi na kuwalipa posho? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, pamoja na kuwa ni Mhifadhi Mkuu na amekuwa akitumikia Serikali kwa miaka ya nyuma akiwa Mhifadhi, lakini kwa sasa hivi Serikali ilishaanza kuwatumia hao vijana wa JKT. Hivi ninavyoongea, tayari taasisi zinaajiri. Pia tumeanzisha makampuni ambayo vijana ambao hawajapata ajira za Serikali wanaingizwa kule na taasisi zetu zinachukua vijana kutoka kwenye makampuni hayo. Kwa hiyo, utaratibu huu tunaendelea nao. Wale waliopo kambini tunawatumia pia kwa ajili ya doria za muda mfupi pale ambapo inapojitokeza changamoto za wanyama wakali na waharibifu.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja la nyongeza pamoja na ombi moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali. Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa kushirikiana na Mji Mkongwe watafanya ukarabati wa lile Jengo la Ngome Kongwe ya Bagamoyo; je, ni lini kazi hiyo itaanza rasmi kufanyika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi. Wananchi wa Kaole na Wazee wa Kaole Bagamoyo wamenituma; wanashukuru sana kwa eneo lao kuwa eneo maarufu kwa utalii wa malikale, lakini ombi lao ni kwamba pale pana msikiti wa miaka mingi, kwa hiyo, wanaomba ule msikiti uhesabike kama misikiti mingine na watalii pamoja na watu wengine watakapokuja wavue viatu ili watakapoingia mle ndani ili kutunza mila na utamaduni wa misikiti katika Mji wa Kaole Bagamoyo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali nampongeza sana Mheshimiwa Muharami, Mbunge wa Bagamoyo kwa namna ambavyo anaendelea kutunza historia hususan ya malikale. Pia nawaomba wananchi wa Bagamoyo tuendelee kushirikiana kwa pamoja, kulinda na kuendeleza hizi malikale tulizoachiwa na waasisi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la lini kazi hii itafanyika kwa mashirikiano na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, niwaahidi tu wanachi wa Bagamoyo, kwa mwaka wa fedha unaokuja ambapo tayari bajeti tumeshapitishiwa, tutaanza ukarabati wa jengo hili. Kwa hili la msikiti natoa tu maelekezo hapa hapa kwamba Mkurugenzi wa Maliakale ashirikiane na viongozi walioko katika Wilaya ya Bagamoyo kuhakikisha anatoa maelekezo kwamba msikiti huu ni sawa na misikiti mingine na heshima zinazotakiwa kama msikiti watu waingie bila viatu, basi utekelezaji wake uanze mara moja, ahsante. (Makofi)
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa wananchi hawa walizoea kufanya shughuli zao za kibinadamu wakati pori hili halijaingizwa kwenye Hifadhi ya Taifa TANAPA; tathmini hii sasa itakamilika lini, kwa sababu nimekuwa nikiahidiwa kila mara, ili wananchi waweze kumegewa eneo lao waweze kuendelea kufanya shughuli za kibinadamu hasa katika Kata ya Ulewe, Kata ya Ubagwe na Kata ya Idahina? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili. Kamishna wa Ardhi katika Mkoa wa Shinyanga kakamilisha tathmini katika Pori la Ubagwe Forest Reserve katika mpaka wa Kaliua ambapo sasa inahitajika gharama ya kwenda kuhakikisha wanaweka mipaka ili kuondoa mgogoro pia uliopo katika eneo hili. Serikali lini sasa itapeleka fedha ili mipaka hii iweze kuwekwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge. Ushetu nilifika na nilizungumza na wananchi wa pale na tuliwaahidi kwamba migogoro hii tunaishughulikia. Kwenye upande wa eneo hili ambalo wananchi wanadai, nataka tu niwaambie wananchi wa Ushetu kwamba wakati Usumbwa Forest Reserve ikiwa kwenye hadhi ya msitu kwa maana ya Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania wanalisimamia, pori hili lilikuwa linaruhusu shughuli za kibinadamu na hadhi yake tulikuwa tunaruhusu ufugaji wa nyuki na wananchi walikuwa wanarina asali katika maeneo hayo. Ndiyo maana leo hii wananchi wanaona ni kama walinyang’anywa, lakini hadhi ya pori ilibadilishwa kutoka kwenye forest reserve, ikapanda kuwa National Park. National Park inazuia shughuli za kibinadamu ndani yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa sasa hivi tunaangalia utaratibu wa kuyashusha hadhi baadhi ya maeneo ili wananchi waendelee kuanza kupata faida ya uhifadhi, na pia waendelee kufuga nyuki kwa ajili ya kurina asali. Kwa hiyo, niwatoe wasiwasi wananchi wa Ushetu, suala hili tunalishughulikia na Mbunge wao amekuwa akiliulizia mara kwa mara. Kwa hiyo, muda siyo mrefu tunatarajia kuleta azimio Bungeni. Nadhani kuna baadhi ya maeneo yatashushwa hadhi na wananchi wataanza kufaidika na urinaji wa asali. Kwenye suala hili la lini tutaweka mipaka, kwa kuwa tathmini tayari imeshakamilika ni wakati wowote tu kuanzia sasa. Kwa kuwa ni jukumu letu Wizara ya Maliasili na Utalii kuweka mipaka, basi tutaendelea kuainisha mipaka halisi, ahsante.
MHE. BUPE N. MWAKANGA’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kumaliza mgogoro wa uwanda wa game reserve Mkoani Rukwa lakini nina swali dogo la nyongeza. Je, ni lini sasa Serikali itapunguza tozo za token ambazo wananchi wanalipa wanapoingia kuvuna na kutoka? Ni lini Serikali itapunguza hizo tozo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru kwa sababu mgogoro huu umeisha. Kwenye suala la token sasa tutaenda uwandani kuangalia ni jinsi gani tukae na wadau ili tuone bei ambayo ni nzuri zaidi kwa wao na kwetu sisi twende sambamba na mahitaji ya wananchi, ahsante.

MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa wananchi waliambiwa kwamba watalipwa kwa ekari moja shilingi milioni mbili, kutokana na uhalisia wa maisha, maisha yamepanda juu sana, wananchi waliomba waongezewe kutoka milioni mbili kulipwa shilingi milioni sita. Je, nini tamko la Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbili, kwa kuwa Kata ile ya Nywatwari kuna wavuvi na wafugaji, je, wafugaji wamekwisha tafutiwa maeneo kwa ajili ya mifugo yao na wavuvi wataangaliwa vipi kwa ajili ya maeneo rafiki ya kuendeleza uvuvi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Agnes na kumpongeza kwa namna ambavyo anaendelea kutetea Wananchi wa Mkoa wa Mara akiwa kama Mbunge wa Mkoa wa Mara. Hili suala la stahili ya hawa wanaopaswa kuhama linafanyika kwa mujibu wa sheria na taratibu zilizopo ambapo Wizara ya Ardhi wamekuwa wakifanya uthamini na miongozo yote wanaitumia ili kuhakikisha kwamba suala hili linaendana sambamba na sheria na taratibu na kanuni zilizopo. Endapo kutakuwa na uhitaji wa kuangalia uthamani au namna ya kuongezewa basi tutakaa na Wizara ya Ardhi ili tuweze kujadili kama kuna uwezekano huo.

Mheshimiwa Spika, kwenye hili la pili la wafugaji na wavuvi, kwenye upande wa kuwahamisha tayari uthamini umefanyika ikiwemo mifugo yao, ardhi yao waliyokuwa wanaitumia. Kwa hiyo, watakapokuwa wameenda kwenye makazi mapya yatazingatiwa hayo ikiwemo kutengewa maeneo ya mifugo lakini kwenye suala hili la uvuvi sheria za uhifadhi zitaongozwa kwa sababu maeneo ambayo tunaenda kuyatwaa mengi tutakuwa tunayahifadhi. Kwa hiyo tutaangalia utaratibu unasemaje ili tuweze kukaa pamoja na wavuvi waweze kuangaliwa. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa majibu yao. Nitakuwa na swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa majibu yameonesha kanuni zipo na wananchi wanafahamu lakini kule bado kuna changamoto kwenye Jimbo la Kibaha Vijijini, je, Waziri atakuwa yuko tayari baada ya Bunge hili twende tukasaidiane kuwaelekeza kanuni na taratibu za uvunaji wa mazao hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa wazo hili tunatamani sana tuendelee kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kufahamu umuhimu wa uhifadhi lakini kuwepo na uvunaji endelevu wa mazao wa misitu. Kwa hiyo natoa ukubali na utayari wa Wizara, tuko tayari kukutana na Wananchi wa Kibaha na maeneo mengine ili kutoa elimu na kuzungumza nao kwa ajili ya kutoa miongozo sahihi, ahsante.
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, wiki iliyopita nilitoa ushauri kwa Serikali kwa kuweka solar electric fence kuzunguka maeneo yote ambayo yana mbuga za wanyama. Je, Serikali haioni sasa ni wakati sahihi wa kuchukua ushauri huo ili kuepuka wanyama kutoka kwenye mbuga za wanyama na kuzunguka hovyo, kuzurua na kuleta maafa na kuharibu mashamba ya watu kwa Watanzania?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, fidia zinazolipwa kwa wahanga ni kidogo sana, haziendani na hali halisi ya sasa; je, Serikali haioni haja ya kuongeza kiwango cha fidia zinazotokana na uharibifu wa wanyamapori?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII, NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mbunge, maswali haya yameendelea kujitokeza katika Bunge lako hili, lakini swali la kwanza linalohusiana na kuweka electric fence, tayari Wizara imeshaanza mkakati huo na kuna maeneo ambayo tumeyatengea bajeti tutaanza kuweka fence kadri bajeti itakavyokuwa inaruhusu.

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye hili la pili la fidia, tayari mlishatupa maekekezo kupitia sheria hii na tuko kwenye hatua za mwisho. Kwa hiyo, tutaileta na tutafanya marekebisho ili kiwango hiki kiweze kuongezwa. (Makofi)

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, changamoto ya tembo kwenye vijiji ambavyo vinazunguka hifadhi ya Mikumi ni kubwa na Serikali imetoa ahadi nyingi; nini kauli ya Serikali kwa madhara makubwa ambayo wananchi wanayapata kutokana na uvamizi wa tembo katika vijiji vya Kilangali, Zombo, Ulaya na Iyombo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea maswali tisa ya nyongeza kwa Waheshimiwa mbalimbali na naomba niyajibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la Mheshimiwa Londo; ameuliza ni nini kauli ya Serikali? Kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi. Ni kwamba sasa hivi tunaangalia njia mbadala wakati huo huo tunaendelea kutatua migogoro hii ya wanyama wakali na waharibifu. Tunajenga vituo, tunaajiri VGS, lakini wakati huo huo tumeshaweka sasa mipango kwenye baadhi ya maeneo tuanze kuweka fence ya umeme ili kupunguza hii athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la Mheshimiwa Anne Malecela, naomba niahidi mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye katika maeneo yale. Lakini pia tumeshaanza kuongeza nguvu kwake, tumepeleka askari na tutaendelea kuajiri VGS katika maeneo hayo ili tuweze kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, wananchi wa Same kilio chenu kimeshasikika Bungeni na tutaongozana na Mheshimiwa Mbunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la Mheshimiwa Vita Kawawa, ni kweli Mheshimiwa Waziri alitoa ahadi ya ujenzi wa madarasa katika jimbo lake, na huu ulikuwa ni mpango wa CSR si kwa ajili ya fidia ya wanyama wakali na waharibifu. Ni kwamba Mheshimiwa Waziri alifanya ziara katika jimbo hilo na akatoa ahadi ya ujenzi wa madarasa ili kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tushirikiane pamoja katika uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuahidi kwamba ahadi ni deni, Wizara itatekeleza. Na kwa kuwa ilikuwa ni kauli ya Mheshimiwa Waziri basi tutafuatilia ili ahadi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dunstan, Mbunge wa Mkinga, yeye ameongelea kuhusu kituo; niahidi tu kwamba katika mpango wa fedha wa 2023/2024 uliopitishwa katika Bunge lako hili, tutapeleka kituo katika Jimbo la Mkinga ili tuongeze nguvu ya kudhibiti wanyama wakati na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Justin Nyamoga, madhara makubwa; naomba niahidi tu kwamba tutaendelea kufuatilia katika maeneo haya ili wananchi waweze kulipwa fidia inayotokana na wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Grace Tendega; naomba tu nilitaarifu Bunge lako, na kwa ridhaa yako, nipe tu nafasi kidogo nitoe ufafanuzi. Tumekuwa na changamoto nyingine imejitokeza katika Mkoa wa Iringa; kuna uvamizi wa simba kwenye baadhi ya maeneo, lakini naomba niwataarifu wananchi, nadhani wameona juhudi za Serikali toka uvamizi huu umejitikeza tumekuwa karibu na wananchi, tunatoa elimu.

Mheshimiwa Spika, naniendelee kutoa elimu kupitia Bunge lako hili, kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa simba, wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku. Lakini pia wenye mifugo wawashe moto kuzunguka maeneo yale ya mifugo ili kuepusha simba wasisogee katika maeneo hayo tunajitahidi sana kulinda maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Wanairinga, Serikali iko kazini na tumeshapeleka helikopta inazunguka usiku na mchana kuhakikisha tunawasaka hawa simba. Tuendelee kushirikiana pamoja ili kuhakikisha zoezi hili tunalikamilisha na simba hawa tunawachukua na kuwarudisha katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Charles, Mbunge wa Mwibara; kumekuwa na changamoto ya viboko na tembo. Naomba niendelee tu kuahidi, nakumbuka tuliwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na tukaongeza nguvu ya askari katika maeneo hayo. Tuendelee tu kuwasiliana, nguvu tutaongeza lakini pia tutaendelea kuajiri VGS ili waweze kusaidia pale inapotokea dharura katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ombi la Mheshimiwa Jimbo la Tunduru kwamba tuongeze VGS (askari wa vijiji). Tunaomba tulipokee hili na tutaweka priority katika eneo hili, tunajua hii changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna shida moja ya mratibu ambaye alihamishwa. Nadhani maelekezo yameshatoka, atarudishwa katika eneo hilo ili aweze kushirikiana na wananchi kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Matiko tayari nimeshalijibu, kwamba tuko kwenye process ya ku-review hizi sheria na kanuni kuangalia sasa angalau tusogeze kiwango fulani ili wananchi nao waweze kuona umuhimu wa namna ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nashukuru, wananchi wa Kata ya Ndungu, Kata ya Kalemawe na Kata ya Maore wanaishi kwa shida sana kwa sababu karibu kila wiki mwananchi anauwawa na mazao yanaharibiwa kwenye mashamba. Serikali niliiomba juzi wakati wa bajeti, Bunge likiisha niongozane na Waziri aende akaone hali yaenyewe, Mheshimiwa Waziri ananiambia nini?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea maswali tisa ya nyongeza kwa Waheshimiwa mbalimbali na naomba niyajibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la Mheshimiwa Londo; ameuliza ni nini kauli ya Serikali? Kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi. Ni kwamba sasa hivi tunaangalia njia mbadala wakati huo huo tunaendelea kutatua migogoro hii ya wanyama wakali na waharibifu. Tunajenga vituo, tunaajiri VGS, lakini wakati huo huo tumeshaweka sasa mipango kwenye baadhi ya maeneo tuanze kuweka fence ya umeme ili kupunguza hii athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la Mheshimiwa Anne Malecela, naomba niahidi mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye katika maeneo yale. Lakini pia tumeshaanza kuongeza nguvu kwake, tumepeleka askari na tutaendelea kuajiri VGS katika maeneo hayo ili tuweze kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, wananchi wa Same kilio chenu kimeshasikika Bungeni na tutaongozana na Mheshimiwa Mbunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la Mheshimiwa Vita Kawawa, ni kweli Mheshimiwa Waziri alitoa ahadi ya ujenzi wa madarasa katika jimbo lake, na huu ulikuwa ni mpango wa CSR si kwa ajili ya fidia ya wanyama wakali na waharibifu. Ni kwamba Mheshimiwa Waziri alifanya ziara katika jimbo hilo na akatoa ahadi ya ujenzi wa madarasa ili kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tushirikiane pamoja katika uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuahidi kwamba ahadi ni deni, Wizara itatekeleza. Na kwa kuwa ilikuwa ni kauli ya Mheshimiwa Waziri basi tutafuatilia ili ahadi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dunstan, Mbunge wa Mkinga, yeye ameongelea kuhusu kituo; niahidi tu kwamba katika mpango wa fedha wa 2023/2024 uliopitishwa katika Bunge lako hili, tutapeleka kituo katika Jimbo la Mkinga ili tuongeze nguvu ya kudhibiti wanyama wakati na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Justin Nyamoga, madhara makubwa; naomba niahidi tu kwamba tutaendelea kufuatilia katika maeneo haya ili wananchi waweze kulipwa fidia inayotokana na wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Grace Tendega; naomba tu nilitaarifu Bunge lako, na kwa ridhaa yako, nipe tu nafasi kidogo nitoe ufafanuzi. Tumekuwa na changamoto nyingine imejitokeza katika Mkoa wa Iringa; kuna uvamizi wa simba kwenye baadhi ya maeneo, lakini naomba niwataarifu wananchi, nadhani wameona juhudi za Serikali toka uvamizi huu umejitikeza tumekuwa karibu na wananchi, tunatoa elimu.

Mheshimiwa Spika, naniendelee kutoa elimu kupitia Bunge lako hili, kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa simba, wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku. Lakini pia wenye mifugo wawashe moto kuzunguka maeneo yale ya mifugo ili kuepusha simba wasisogee katika maeneo hayo tunajitahidi sana kulinda maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Wanairinga, Serikali iko kazini na tumeshapeleka helikopta inazunguka usiku na mchana kuhakikisha tunawasaka hawa simba. Tuendelee kushirikiana pamoja ili kuhakikisha zoezi hili tunalikamilisha na simba hawa tunawachukua na kuwarudisha katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Charles, Mbunge wa Mwibara; kumekuwa na changamoto ya viboko na tembo. Naomba niendelee tu kuahidi, nakumbuka tuliwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na tukaongeza nguvu ya askari katika maeneo hayo. Tuendelee tu kuwasiliana, nguvu tutaongeza lakini pia tutaendelea kuajiri VGS ili waweze kusaidia pale inapotokea dharura katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ombi la Mheshimiwa Jimbo la Tunduru kwamba tuongeze VGS (askari wa vijiji). Tunaomba tulipokee hili na tutaweka priority katika eneo hili, tunajua hii changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna shida moja ya mratibu ambaye alihamishwa. Nadhani maelekezo yameshatoka, atarudishwa katika eneo hilo ili aweze kushirikiana na wananchi kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Matiko tayari nimeshalijibu, kwamba tuko kwenye process ya ku-review hizi sheria na kanuni kuangalia sasa angalau tusogeze kiwango fulani ili wananchi nao waweze kuona umuhimu wa namna ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, alipokuja Mheshimiwa Waziri kutatua na kuzungumza na wananchi kuhusu masuala ya tembo aliahidi pia kwamba TFS na TANAPA watajenga madarasa katika Shule ya Sekondari ya Mkomanule na Shule ya Sekondari ya Mbunga. Je, ahadi hiyo ipoje mpaka sasa hivi, wananchi bado wanaisubiri?

SPIKA: Mheshimiwa Vita Kawawa, hiyo ahadi ni kutokana na madhara ya tembo ndio badala ya yale madhara ya kuwalipa wananchi waliopata athari na mashamba, Serikali itajenga madarasa au ni vitu viwili tofauti? Ili nijue kama na lenyewe liwemo kwenye orodha ua hapana? Mheshimiwa Vita Kawawa.

MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, alipokuja lilikuwa ni suala la kutatua hilo suala la tembo, kwa sababu watu walikuwa wamekufa katika vijiji hivyo tofauti, na katika moja ya shida waliyoieleza wananchi wale, pamoja na tembo, waliomba pia wajengewe madarasa katika shule zao hizo na TFS na TANAPA.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea maswali tisa ya nyongeza kwa Waheshimiwa mbalimbali na naomba niyajibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la Mheshimiwa Londo; ameuliza ni nini kauli ya Serikali? Kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi. Ni kwamba sasa hivi tunaangalia njia mbadala wakati huo huo tunaendelea kutatua migogoro hii ya wanyama wakali na waharibifu. Tunajenga vituo, tunaajiri VGS, lakini wakati huo huo tumeshaweka sasa mipango kwenye baadhi ya maeneo tuanze kuweka fence ya umeme ili kupunguza hii athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la Mheshimiwa Anne Malecela, naomba niahidi mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye katika maeneo yale. Lakini pia tumeshaanza kuongeza nguvu kwake, tumepeleka askari na tutaendelea kuajiri VGS katika maeneo hayo ili tuweze kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, wananchi wa Same kilio chenu kimeshasikika Bungeni na tutaongozana na Mheshimiwa Mbunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la Mheshimiwa Vita Kawawa, ni kweli Mheshimiwa Waziri alitoa ahadi ya ujenzi wa madarasa katika jimbo lake, na huu ulikuwa ni mpango wa CSR si kwa ajili ya fidia ya wanyama wakali na waharibifu. Ni kwamba Mheshimiwa Waziri alifanya ziara katika jimbo hilo na akatoa ahadi ya ujenzi wa madarasa ili kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tushirikiane pamoja katika uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuahidi kwamba ahadi ni deni, Wizara itatekeleza. Na kwa kuwa ilikuwa ni kauli ya Mheshimiwa Waziri basi tutafuatilia ili ahadi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dunstan, Mbunge wa Mkinga, yeye ameongelea kuhusu kituo; niahidi tu kwamba katika mpango wa fedha wa 2023/2024 uliopitishwa katika Bunge lako hili, tutapeleka kituo katika Jimbo la Mkinga ili tuongeze nguvu ya kudhibiti wanyama wakati na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Justin Nyamoga, madhara makubwa; naomba niahidi tu kwamba tutaendelea kufuatilia katika maeneo haya ili wananchi waweze kulipwa fidia inayotokana na wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Grace Tendega; naomba tu nilitaarifu Bunge lako, na kwa ridhaa yako, nipe tu nafasi kidogo nitoe ufafanuzi. Tumekuwa na changamoto nyingine imejitokeza katika Mkoa wa Iringa; kuna uvamizi wa simba kwenye baadhi ya maeneo, lakini naomba niwataarifu wananchi, nadhani wameona juhudi za Serikali toka uvamizi huu umejitikeza tumekuwa karibu na wananchi, tunatoa elimu.

Mheshimiwa Spika, naniendelee kutoa elimu kupitia Bunge lako hili, kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa simba, wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku. Lakini pia wenye mifugo wawashe moto kuzunguka maeneo yale ya mifugo ili kuepusha simba wasisogee katika maeneo hayo tunajitahidi sana kulinda maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Wanairinga, Serikali iko kazini na tumeshapeleka helikopta inazunguka usiku na mchana kuhakikisha tunawasaka hawa simba. Tuendelee kushirikiana pamoja ili kuhakikisha zoezi hili tunalikamilisha na simba hawa tunawachukua na kuwarudisha katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Charles, Mbunge wa Mwibara; kumekuwa na changamoto ya viboko na tembo. Naomba niendelee tu kuahidi, nakumbuka tuliwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na tukaongeza nguvu ya askari katika maeneo hayo. Tuendelee tu kuwasiliana, nguvu tutaongeza lakini pia tutaendelea kuajiri VGS ili waweze kusaidia pale inapotokea dharura katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ombi la Mheshimiwa Jimbo la Tunduru kwamba tuongeze VGS (askari wa vijiji). Tunaomba tulipokee hili na tutaweka priority katika eneo hili, tunajua hii changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna shida moja ya mratibu ambaye alihamishwa. Nadhani maelekezo yameshatoka, atarudishwa katika eneo hilo ili aweze kushirikiana na wananchi kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Matiko tayari nimeshalijibu, kwamba tuko kwenye process ya ku-review hizi sheria na kanuni kuangalia sasa angalau tusogeze kiwango fulani ili wananchi nao waweze kuona umuhimu wa namna ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, wananchi wa Mkinga kwenye kata 13 wamepata athari kubwa ya tembo kutoka Mbuga ya Tsavo, Kenya na Mbuga ya Mkomazi na ili kukabiliana na tatizo hilo Serikali iliahidi kuweka kituo maalum Wilaya ya Mkinga. Lini Serikali itatimiza ahadi hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea maswali tisa ya nyongeza kwa Waheshimiwa mbalimbali na naomba niyajibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la Mheshimiwa Londo; ameuliza ni nini kauli ya Serikali? Kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi. Ni kwamba sasa hivi tunaangalia njia mbadala wakati huo huo tunaendelea kutatua migogoro hii ya wanyama wakali na waharibifu. Tunajenga vituo, tunaajiri VGS, lakini wakati huo huo tumeshaweka sasa mipango kwenye baadhi ya maeneo tuanze kuweka fence ya umeme ili kupunguza hii athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la Mheshimiwa Anne Malecela, naomba niahidi mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye katika maeneo yale. Lakini pia tumeshaanza kuongeza nguvu kwake, tumepeleka askari na tutaendelea kuajiri VGS katika maeneo hayo ili tuweze kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, wananchi wa Same kilio chenu kimeshasikika Bungeni na tutaongozana na Mheshimiwa Mbunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la Mheshimiwa Vita Kawawa, ni kweli Mheshimiwa Waziri alitoa ahadi ya ujenzi wa madarasa katika jimbo lake, na huu ulikuwa ni mpango wa CSR si kwa ajili ya fidia ya wanyama wakali na waharibifu. Ni kwamba Mheshimiwa Waziri alifanya ziara katika jimbo hilo na akatoa ahadi ya ujenzi wa madarasa ili kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tushirikiane pamoja katika uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuahidi kwamba ahadi ni deni, Wizara itatekeleza. Na kwa kuwa ilikuwa ni kauli ya Mheshimiwa Waziri basi tutafuatilia ili ahadi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dunstan, Mbunge wa Mkinga, yeye ameongelea kuhusu kituo; niahidi tu kwamba katika mpango wa fedha wa 2023/2024 uliopitishwa katika Bunge lako hili, tutapeleka kituo katika Jimbo la Mkinga ili tuongeze nguvu ya kudhibiti wanyama wakati na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Justin Nyamoga, madhara makubwa; naomba niahidi tu kwamba tutaendelea kufuatilia katika maeneo haya ili wananchi waweze kulipwa fidia inayotokana na wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Grace Tendega; naomba tu nilitaarifu Bunge lako, na kwa ridhaa yako, nipe tu nafasi kidogo nitoe ufafanuzi. Tumekuwa na changamoto nyingine imejitokeza katika Mkoa wa Iringa; kuna uvamizi wa simba kwenye baadhi ya maeneo, lakini naomba niwataarifu wananchi, nadhani wameona juhudi za Serikali toka uvamizi huu umejitikeza tumekuwa karibu na wananchi, tunatoa elimu.

Mheshimiwa Spika, naniendelee kutoa elimu kupitia Bunge lako hili, kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa simba, wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku. Lakini pia wenye mifugo wawashe moto kuzunguka maeneo yale ya mifugo ili kuepusha simba wasisogee katika maeneo hayo tunajitahidi sana kulinda maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Wanairinga, Serikali iko kazini na tumeshapeleka helikopta inazunguka usiku na mchana kuhakikisha tunawasaka hawa simba. Tuendelee kushirikiana pamoja ili kuhakikisha zoezi hili tunalikamilisha na simba hawa tunawachukua na kuwarudisha katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Charles, Mbunge wa Mwibara; kumekuwa na changamoto ya viboko na tembo. Naomba niendelee tu kuahidi, nakumbuka tuliwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na tukaongeza nguvu ya askari katika maeneo hayo. Tuendelee tu kuwasiliana, nguvu tutaongeza lakini pia tutaendelea kuajiri VGS ili waweze kusaidia pale inapotokea dharura katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ombi la Mheshimiwa Jimbo la Tunduru kwamba tuongeze VGS (askari wa vijiji). Tunaomba tulipokee hili na tutaweka priority katika eneo hili, tunajua hii changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna shida moja ya mratibu ambaye alihamishwa. Nadhani maelekezo yameshatoka, atarudishwa katika eneo hilo ili aweze kushirikiana na wananchi kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Matiko tayari nimeshalijibu, kwamba tuko kwenye process ya ku-review hizi sheria na kanuni kuangalia sasa angalau tusogeze kiwango fulani ili wananchi nao waweze kuona umuhimu wa namna ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kata ya Ruaha Mbuyuni ambayo iko tu barabarani kabisa pale kwenye lami, Kijiji cha Msosa, Kijiji cha Ruaha Mbuyuni chenyewe na Kijiji cha Ikula kuna madhara makubwa sana yanayosababishwa na tembo kiasi cha kusababisha chakula kuwa pungufu. Serikali inachukua hatua gani katika kudhibiti tembo hao hasa kuongeza askari katika Kambi ya Mtandika?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea maswali tisa ya nyongeza kwa Waheshimiwa mbalimbali na naomba niyajibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la Mheshimiwa Londo; ameuliza ni nini kauli ya Serikali? Kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi. Ni kwamba sasa hivi tunaangalia njia mbadala wakati huo huo tunaendelea kutatua migogoro hii ya wanyama wakali na waharibifu. Tunajenga vituo, tunaajiri VGS, lakini wakati huo huo tumeshaweka sasa mipango kwenye baadhi ya maeneo tuanze kuweka fence ya umeme ili kupunguza hii athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la Mheshimiwa Anne Malecela, naomba niahidi mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye katika maeneo yale. Lakini pia tumeshaanza kuongeza nguvu kwake, tumepeleka askari na tutaendelea kuajiri VGS katika maeneo hayo ili tuweze kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, wananchi wa Same kilio chenu kimeshasikika Bungeni na tutaongozana na Mheshimiwa Mbunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la Mheshimiwa Vita Kawawa, ni kweli Mheshimiwa Waziri alitoa ahadi ya ujenzi wa madarasa katika jimbo lake, na huu ulikuwa ni mpango wa CSR si kwa ajili ya fidia ya wanyama wakali na waharibifu. Ni kwamba Mheshimiwa Waziri alifanya ziara katika jimbo hilo na akatoa ahadi ya ujenzi wa madarasa ili kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tushirikiane pamoja katika uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuahidi kwamba ahadi ni deni, Wizara itatekeleza. Na kwa kuwa ilikuwa ni kauli ya Mheshimiwa Waziri basi tutafuatilia ili ahadi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dunstan, Mbunge wa Mkinga, yeye ameongelea kuhusu kituo; niahidi tu kwamba katika mpango wa fedha wa 2023/2024 uliopitishwa katika Bunge lako hili, tutapeleka kituo katika Jimbo la Mkinga ili tuongeze nguvu ya kudhibiti wanyama wakati na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Justin Nyamoga, madhara makubwa; naomba niahidi tu kwamba tutaendelea kufuatilia katika maeneo haya ili wananchi waweze kulipwa fidia inayotokana na wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Grace Tendega; naomba tu nilitaarifu Bunge lako, na kwa ridhaa yako, nipe tu nafasi kidogo nitoe ufafanuzi. Tumekuwa na changamoto nyingine imejitokeza katika Mkoa wa Iringa; kuna uvamizi wa simba kwenye baadhi ya maeneo, lakini naomba niwataarifu wananchi, nadhani wameona juhudi za Serikali toka uvamizi huu umejitikeza tumekuwa karibu na wananchi, tunatoa elimu.

Mheshimiwa Spika, naniendelee kutoa elimu kupitia Bunge lako hili, kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa simba, wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku. Lakini pia wenye mifugo wawashe moto kuzunguka maeneo yale ya mifugo ili kuepusha simba wasisogee katika maeneo hayo tunajitahidi sana kulinda maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Wanairinga, Serikali iko kazini na tumeshapeleka helikopta inazunguka usiku na mchana kuhakikisha tunawasaka hawa simba. Tuendelee kushirikiana pamoja ili kuhakikisha zoezi hili tunalikamilisha na simba hawa tunawachukua na kuwarudisha katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Charles, Mbunge wa Mwibara; kumekuwa na changamoto ya viboko na tembo. Naomba niendelee tu kuahidi, nakumbuka tuliwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na tukaongeza nguvu ya askari katika maeneo hayo. Tuendelee tu kuwasiliana, nguvu tutaongeza lakini pia tutaendelea kuajiri VGS ili waweze kusaidia pale inapotokea dharura katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ombi la Mheshimiwa Jimbo la Tunduru kwamba tuongeze VGS (askari wa vijiji). Tunaomba tulipokee hili na tutaweka priority katika eneo hili, tunajua hii changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna shida moja ya mratibu ambaye alihamishwa. Nadhani maelekezo yameshatoka, atarudishwa katika eneo hilo ili aweze kushirikiana na wananchi kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Matiko tayari nimeshalijibu, kwamba tuko kwenye process ya ku-review hizi sheria na kanuni kuangalia sasa angalau tusogeze kiwango fulani ili wananchi nao waweze kuona umuhimu wa namna ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa; pamoja na tembo kuvamia maeneo mbalimbali hivi karibuni katika Kata ya Lyamigungwe na Kata ya Lupota simba wamevamia katika mifugo ya wananchi na wamekula mifugo ile na wananchi wana taharuki kubwa. Nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba wananchi wanakuwa huru? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea maswali tisa ya nyongeza kwa Waheshimiwa mbalimbali na naomba niyajibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la Mheshimiwa Londo; ameuliza ni nini kauli ya Serikali? Kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi. Ni kwamba sasa hivi tunaangalia njia mbadala wakati huo huo tunaendelea kutatua migogoro hii ya wanyama wakali na waharibifu. Tunajenga vituo, tunaajiri VGS, lakini wakati huo huo tumeshaweka sasa mipango kwenye baadhi ya maeneo tuanze kuweka fence ya umeme ili kupunguza hii athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la Mheshimiwa Anne Malecela, naomba niahidi mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye katika maeneo yale. Lakini pia tumeshaanza kuongeza nguvu kwake, tumepeleka askari na tutaendelea kuajiri VGS katika maeneo hayo ili tuweze kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, wananchi wa Same kilio chenu kimeshasikika Bungeni na tutaongozana na Mheshimiwa Mbunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la Mheshimiwa Vita Kawawa, ni kweli Mheshimiwa Waziri alitoa ahadi ya ujenzi wa madarasa katika jimbo lake, na huu ulikuwa ni mpango wa CSR si kwa ajili ya fidia ya wanyama wakali na waharibifu. Ni kwamba Mheshimiwa Waziri alifanya ziara katika jimbo hilo na akatoa ahadi ya ujenzi wa madarasa ili kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tushirikiane pamoja katika uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuahidi kwamba ahadi ni deni, Wizara itatekeleza. Na kwa kuwa ilikuwa ni kauli ya Mheshimiwa Waziri basi tutafuatilia ili ahadi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dunstan, Mbunge wa Mkinga, yeye ameongelea kuhusu kituo; niahidi tu kwamba katika mpango wa fedha wa 2023/2024 uliopitishwa katika Bunge lako hili, tutapeleka kituo katika Jimbo la Mkinga ili tuongeze nguvu ya kudhibiti wanyama wakati na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Justin Nyamoga, madhara makubwa; naomba niahidi tu kwamba tutaendelea kufuatilia katika maeneo haya ili wananchi waweze kulipwa fidia inayotokana na wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Grace Tendega; naomba tu nilitaarifu Bunge lako, na kwa ridhaa yako, nipe tu nafasi kidogo nitoe ufafanuzi. Tumekuwa na changamoto nyingine imejitokeza katika Mkoa wa Iringa; kuna uvamizi wa simba kwenye baadhi ya maeneo, lakini naomba niwataarifu wananchi, nadhani wameona juhudi za Serikali toka uvamizi huu umejitikeza tumekuwa karibu na wananchi, tunatoa elimu.

Mheshimiwa Spika, naniendelee kutoa elimu kupitia Bunge lako hili, kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa simba, wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku. Lakini pia wenye mifugo wawashe moto kuzunguka maeneo yale ya mifugo ili kuepusha simba wasisogee katika maeneo hayo tunajitahidi sana kulinda maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Wanairinga, Serikali iko kazini na tumeshapeleka helikopta inazunguka usiku na mchana kuhakikisha tunawasaka hawa simba. Tuendelee kushirikiana pamoja ili kuhakikisha zoezi hili tunalikamilisha na simba hawa tunawachukua na kuwarudisha katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Charles, Mbunge wa Mwibara; kumekuwa na changamoto ya viboko na tembo. Naomba niendelee tu kuahidi, nakumbuka tuliwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na tukaongeza nguvu ya askari katika maeneo hayo. Tuendelee tu kuwasiliana, nguvu tutaongeza lakini pia tutaendelea kuajiri VGS ili waweze kusaidia pale inapotokea dharura katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ombi la Mheshimiwa Jimbo la Tunduru kwamba tuongeze VGS (askari wa vijiji). Tunaomba tulipokee hili na tutaweka priority katika eneo hili, tunajua hii changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna shida moja ya mratibu ambaye alihamishwa. Nadhani maelekezo yameshatoka, atarudishwa katika eneo hilo ili aweze kushirikiana na wananchi kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Matiko tayari nimeshalijibu, kwamba tuko kwenye process ya ku-review hizi sheria na kanuni kuangalia sasa angalau tusogeze kiwango fulani ili wananchi nao waweze kuona umuhimu wa namna ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante, tatizo la tembo, mamba na viboko ni kubwa sana katika Jimbo la Mwibara na imefikia kwamba wameuwa mpaka wananchi.

Sasa je, Serikali ina mpango gani au inachukua hatua gani ili kuhakikisha kwamba, hilo tatizo linakwisha?

SPIKA: Hao viboko wanavamia mashamba pia? Wanavamia mashamba na wananchi?

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, yes, yaani kwa sababu wanatoka majini kwenda kula vyakula huko nchi kavu.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea maswali tisa ya nyongeza kwa Waheshimiwa mbalimbali na naomba niyajibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la Mheshimiwa Londo; ameuliza ni nini kauli ya Serikali? Kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi. Ni kwamba sasa hivi tunaangalia njia mbadala wakati huo huo tunaendelea kutatua migogoro hii ya wanyama wakali na waharibifu. Tunajenga vituo, tunaajiri VGS, lakini wakati huo huo tumeshaweka sasa mipango kwenye baadhi ya maeneo tuanze kuweka fence ya umeme ili kupunguza hii athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la Mheshimiwa Anne Malecela, naomba niahidi mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye katika maeneo yale. Lakini pia tumeshaanza kuongeza nguvu kwake, tumepeleka askari na tutaendelea kuajiri VGS katika maeneo hayo ili tuweze kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, wananchi wa Same kilio chenu kimeshasikika Bungeni na tutaongozana na Mheshimiwa Mbunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la Mheshimiwa Vita Kawawa, ni kweli Mheshimiwa Waziri alitoa ahadi ya ujenzi wa madarasa katika jimbo lake, na huu ulikuwa ni mpango wa CSR si kwa ajili ya fidia ya wanyama wakali na waharibifu. Ni kwamba Mheshimiwa Waziri alifanya ziara katika jimbo hilo na akatoa ahadi ya ujenzi wa madarasa ili kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tushirikiane pamoja katika uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuahidi kwamba ahadi ni deni, Wizara itatekeleza. Na kwa kuwa ilikuwa ni kauli ya Mheshimiwa Waziri basi tutafuatilia ili ahadi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dunstan, Mbunge wa Mkinga, yeye ameongelea kuhusu kituo; niahidi tu kwamba katika mpango wa fedha wa 2023/2024 uliopitishwa katika Bunge lako hili, tutapeleka kituo katika Jimbo la Mkinga ili tuongeze nguvu ya kudhibiti wanyama wakati na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Justin Nyamoga, madhara makubwa; naomba niahidi tu kwamba tutaendelea kufuatilia katika maeneo haya ili wananchi waweze kulipwa fidia inayotokana na wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Grace Tendega; naomba tu nilitaarifu Bunge lako, na kwa ridhaa yako, nipe tu nafasi kidogo nitoe ufafanuzi. Tumekuwa na changamoto nyingine imejitokeza katika Mkoa wa Iringa; kuna uvamizi wa simba kwenye baadhi ya maeneo, lakini naomba niwataarifu wananchi, nadhani wameona juhudi za Serikali toka uvamizi huu umejitikeza tumekuwa karibu na wananchi, tunatoa elimu.

Mheshimiwa Spika, naniendelee kutoa elimu kupitia Bunge lako hili, kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa simba, wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku. Lakini pia wenye mifugo wawashe moto kuzunguka maeneo yale ya mifugo ili kuepusha simba wasisogee katika maeneo hayo tunajitahidi sana kulinda maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Wanairinga, Serikali iko kazini na tumeshapeleka helikopta inazunguka usiku na mchana kuhakikisha tunawasaka hawa simba. Tuendelee kushirikiana pamoja ili kuhakikisha zoezi hili tunalikamilisha na simba hawa tunawachukua na kuwarudisha katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Charles, Mbunge wa Mwibara; kumekuwa na changamoto ya viboko na tembo. Naomba niendelee tu kuahidi, nakumbuka tuliwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na tukaongeza nguvu ya askari katika maeneo hayo. Tuendelee tu kuwasiliana, nguvu tutaongeza lakini pia tutaendelea kuajiri VGS ili waweze kusaidia pale inapotokea dharura katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ombi la Mheshimiwa Jimbo la Tunduru kwamba tuongeze VGS (askari wa vijiji). Tunaomba tulipokee hili na tutaweka priority katika eneo hili, tunajua hii changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna shida moja ya mratibu ambaye alihamishwa. Nadhani maelekezo yameshatoka, atarudishwa katika eneo hilo ili aweze kushirikiana na wananchi kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Matiko tayari nimeshalijibu, kwamba tuko kwenye process ya ku-review hizi sheria na kanuni kuangalia sasa angalau tusogeze kiwango fulani ili wananchi nao waweze kuona umuhimu wa namna ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, Wilaya ya Tunduru imezungukwa na hifadhi ya wanyamapori na wananchi wa Tunduru wanategemea kilimo. Kutokana na uvamizi wa tembo uharibifu ni mkubwa pamoja na watu kupoteza Maisha, na Serikali inatumia kiwango kikubwa sana kulipa fidia kwa wananchi.

Je, Serikali sasa haioni haja ya kuwaajiri wale askari wa VGS ambao wako vijiji vyote na kuwatengea posho, ili kupunguza hizi athari na kutokana kwamba watumishi hawa wa wanyamapori wako saba tu Wilaya nzima? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea maswali tisa ya nyongeza kwa Waheshimiwa mbalimbali na naomba niyajibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la Mheshimiwa Londo; ameuliza ni nini kauli ya Serikali? Kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi. Ni kwamba sasa hivi tunaangalia njia mbadala wakati huo huo tunaendelea kutatua migogoro hii ya wanyama wakali na waharibifu. Tunajenga vituo, tunaajiri VGS, lakini wakati huo huo tumeshaweka sasa mipango kwenye baadhi ya maeneo tuanze kuweka fence ya umeme ili kupunguza hii athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la Mheshimiwa Anne Malecela, naomba niahidi mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye katika maeneo yale. Lakini pia tumeshaanza kuongeza nguvu kwake, tumepeleka askari na tutaendelea kuajiri VGS katika maeneo hayo ili tuweze kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, wananchi wa Same kilio chenu kimeshasikika Bungeni na tutaongozana na Mheshimiwa Mbunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la Mheshimiwa Vita Kawawa, ni kweli Mheshimiwa Waziri alitoa ahadi ya ujenzi wa madarasa katika jimbo lake, na huu ulikuwa ni mpango wa CSR si kwa ajili ya fidia ya wanyama wakali na waharibifu. Ni kwamba Mheshimiwa Waziri alifanya ziara katika jimbo hilo na akatoa ahadi ya ujenzi wa madarasa ili kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tushirikiane pamoja katika uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuahidi kwamba ahadi ni deni, Wizara itatekeleza. Na kwa kuwa ilikuwa ni kauli ya Mheshimiwa Waziri basi tutafuatilia ili ahadi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dunstan, Mbunge wa Mkinga, yeye ameongelea kuhusu kituo; niahidi tu kwamba katika mpango wa fedha wa 2023/2024 uliopitishwa katika Bunge lako hili, tutapeleka kituo katika Jimbo la Mkinga ili tuongeze nguvu ya kudhibiti wanyama wakati na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Justin Nyamoga, madhara makubwa; naomba niahidi tu kwamba tutaendelea kufuatilia katika maeneo haya ili wananchi waweze kulipwa fidia inayotokana na wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Grace Tendega; naomba tu nilitaarifu Bunge lako, na kwa ridhaa yako, nipe tu nafasi kidogo nitoe ufafanuzi. Tumekuwa na changamoto nyingine imejitokeza katika Mkoa wa Iringa; kuna uvamizi wa simba kwenye baadhi ya maeneo, lakini naomba niwataarifu wananchi, nadhani wameona juhudi za Serikali toka uvamizi huu umejitikeza tumekuwa karibu na wananchi, tunatoa elimu.

Mheshimiwa Spika, naniendelee kutoa elimu kupitia Bunge lako hili, kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa simba, wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku. Lakini pia wenye mifugo wawashe moto kuzunguka maeneo yale ya mifugo ili kuepusha simba wasisogee katika maeneo hayo tunajitahidi sana kulinda maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Wanairinga, Serikali iko kazini na tumeshapeleka helikopta inazunguka usiku na mchana kuhakikisha tunawasaka hawa simba. Tuendelee kushirikiana pamoja ili kuhakikisha zoezi hili tunalikamilisha na simba hawa tunawachukua na kuwarudisha katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Charles, Mbunge wa Mwibara; kumekuwa na changamoto ya viboko na tembo. Naomba niendelee tu kuahidi, nakumbuka tuliwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na tukaongeza nguvu ya askari katika maeneo hayo. Tuendelee tu kuwasiliana, nguvu tutaongeza lakini pia tutaendelea kuajiri VGS ili waweze kusaidia pale inapotokea dharura katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ombi la Mheshimiwa Jimbo la Tunduru kwamba tuongeze VGS (askari wa vijiji). Tunaomba tulipokee hili na tutaweka priority katika eneo hili, tunajua hii changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna shida moja ya mratibu ambaye alihamishwa. Nadhani maelekezo yameshatoka, atarudishwa katika eneo hilo ili aweze kushirikiana na wananchi kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Matiko tayari nimeshalijibu, kwamba tuko kwenye process ya ku-review hizi sheria na kanuni kuangalia sasa angalau tusogeze kiwango fulani ili wananchi nao waweze kuona umuhimu wa namna ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, wanyama wakali wakiwadhuru binadamu kwa maana ya wakivunjika, wakapata ulemavu wanalipwa kifuta jasho cha shilingi 500,000 na wakiuwawa wanalipwa shilingi 1,000,000; wakiharibu mazao ekari moja shilingi 25,000.

Sasa ni kwa nini Serikali isi-review kanuni zao ili ije na uhalisia wa kuweza kutoa kifuta jasho ambacho kinakidhi ustahiki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimepokea maswali tisa ya nyongeza kwa Waheshimiwa mbalimbali na naomba niyajibu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la Mheshimiwa Londo; ameuliza ni nini kauli ya Serikali? Kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi. Ni kwamba sasa hivi tunaangalia njia mbadala wakati huo huo tunaendelea kutatua migogoro hii ya wanyama wakali na waharibifu. Tunajenga vituo, tunaajiri VGS, lakini wakati huo huo tumeshaweka sasa mipango kwenye baadhi ya maeneo tuanze kuweka fence ya umeme ili kupunguza hii athari ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la Mheshimiwa Anne Malecela, naomba niahidi mbele ya Bunge lako hili Tukufu kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye katika maeneo yale. Lakini pia tumeshaanza kuongeza nguvu kwake, tumepeleka askari na tutaendelea kuajiri VGS katika maeneo hayo ili tuweze kushirikiana pamoja. Kwa hiyo, wananchi wa Same kilio chenu kimeshasikika Bungeni na tutaongozana na Mheshimiwa Mbunge (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala hili la Mheshimiwa Vita Kawawa, ni kweli Mheshimiwa Waziri alitoa ahadi ya ujenzi wa madarasa katika jimbo lake, na huu ulikuwa ni mpango wa CSR si kwa ajili ya fidia ya wanyama wakali na waharibifu. Ni kwamba Mheshimiwa Waziri alifanya ziara katika jimbo hilo na akatoa ahadi ya ujenzi wa madarasa ili kuwafanya wananchi wanaoishi katika maeneo hayo tushirikiane pamoja katika uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee tu kuahidi kwamba ahadi ni deni, Wizara itatekeleza. Na kwa kuwa ilikuwa ni kauli ya Mheshimiwa Waziri basi tutafuatilia ili ahadi hii iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dunstan, Mbunge wa Mkinga, yeye ameongelea kuhusu kituo; niahidi tu kwamba katika mpango wa fedha wa 2023/2024 uliopitishwa katika Bunge lako hili, tutapeleka kituo katika Jimbo la Mkinga ili tuongeze nguvu ya kudhibiti wanyama wakati na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Justin Nyamoga, madhara makubwa; naomba niahidi tu kwamba tutaendelea kufuatilia katika maeneo haya ili wananchi waweze kulipwa fidia inayotokana na wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Grace Tendega; naomba tu nilitaarifu Bunge lako, na kwa ridhaa yako, nipe tu nafasi kidogo nitoe ufafanuzi. Tumekuwa na changamoto nyingine imejitokeza katika Mkoa wa Iringa; kuna uvamizi wa simba kwenye baadhi ya maeneo, lakini naomba niwataarifu wananchi, nadhani wameona juhudi za Serikali toka uvamizi huu umejitikeza tumekuwa karibu na wananchi, tunatoa elimu.

Mheshimiwa Spika, naniendelee kutoa elimu kupitia Bunge lako hili, kwamba wakati huu ambapo tunawasaka hawa simba, wananchi wawe na tahadhari ya kutotembea usiku. Lakini pia wenye mifugo wawashe moto kuzunguka maeneo yale ya mifugo ili kuepusha simba wasisogee katika maeneo hayo tunajitahidi sana kulinda maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaombe Wanairinga, Serikali iko kazini na tumeshapeleka helikopta inazunguka usiku na mchana kuhakikisha tunawasaka hawa simba. Tuendelee kushirikiana pamoja ili kuhakikisha zoezi hili tunalikamilisha na simba hawa tunawachukua na kuwarudisha katika maeneo yao.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Mheshimiwa Charles, Mbunge wa Mwibara; kumekuwa na changamoto ya viboko na tembo. Naomba niendelee tu kuahidi, nakumbuka tuliwasiliana na Mheshimiwa Mbunge na tukaongeza nguvu ya askari katika maeneo hayo. Tuendelee tu kuwasiliana, nguvu tutaongeza lakini pia tutaendelea kuajiri VGS ili waweze kusaidia pale inapotokea dharura katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ombi la Mheshimiwa Jimbo la Tunduru kwamba tuongeze VGS (askari wa vijiji). Tunaomba tulipokee hili na tutaweka priority katika eneo hili, tunajua hii changamoto ya wanyama wakali.

Mheshimiwa Spika, pia kulikuwa kuna shida moja ya mratibu ambaye alihamishwa. Nadhani maelekezo yameshatoka, atarudishwa katika eneo hilo ili aweze kushirikiana na wananchi kudhibiti wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Matiko tayari nimeshalijibu, kwamba tuko kwenye process ya ku-review hizi sheria na kanuni kuangalia sasa angalau tusogeze kiwango fulani ili wananchi nao waweze kuona umuhimu wa namna ya uhifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali, naomba niulize swali moja tu la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wananchi wale wa Kibesa sehemu ya Mpiji Magohe, wanatembea kilometa 8.2 kufuata sekodari pale Mpiji Center.

Je, Mheshimiwa Waziri utakuwa tayari kuja ili uone ushuhudie ile adha ya wananchi wale wanayopata ili mimi na wewe tushirikiane kufuata taratibu, sheria na miongozo ili waweze kupewa hilo eneo katika sehemu ya hifadhi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Issa Jumanne Mtemvu, Mbunge wa Jimbo la Kibamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, eneo nalifahamu na nilishafanya ziara mara nyingi. Na ukiangalia jibu la msingi, nimejibu kiufasaha, kwamba maeneo ni machache na Jiji la Dar es Salaam linaendelea kukua, tukikosa maeneo ya kupumulia watu wanazidi kuongezeka lakini tukaendelea kunyima maeneo ambayo angalau watu wanapopumua…

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, ni kwamba haya maeneo tunayatenga, si kwa sababu tu ya msuala ya utalii. Serikali inatambua kwamba kuna umuhimu wa ku-balance ikolojia. Kuna maeneo kama Pugu tumetenga ile Kazimzumbwi na upande wa Kibamba na huku kaskazini tumetenga hili Pori la Mambwepande. Lakini lengo ni kuifanya Dar es Salaam ipate maeneo ya kupumulia kwa sababu watu wanazidi kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimejibu, kilometa za mradba katika eneo hili ni 15 tu, ni chace sana. tulitamani hata ziwe nyingi. Sasa tukiendelea kuzimega tena, kwanza tunawafanya wana-Dar es Salaam wakose pa kupumlia; cha pili, ni kufanya sasa maeneo mengi ambayo tunajitahidi kuyatunza kwa ajili ya ku-balance ikolojia yatakuwa yanazidi kupungua zaidi.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kwa Serikali.

Mheshimiwa Spika, maporomoko ya Kalambo ni miongoni mwa vivutio vilivyo Kusini Nyanda za Juu na ni ukweli usiopingika kwamba maporomoko haya kuachiwa chini ya TFS ambayo siyo kazi yake ya kutangaza vivutio vya kitalii ni kukosesha Taifa hili mapato sahihi.

Je, Serikali iko tayari kuyaondoa maporomoko haya kuwa chini ya umiliki wa TFS na kupeleka katika taasisi ambayo kazi yake mahsusi ni kwa ajili ya kutangaza vivutio vya utalii?

Swali la pili, kwa sababu kutangaza ni pamoja na uwepo wa bajeti na Wizara bado haijaleta bajeti yake. Je, watatuhakikishia kwamba kama maporomoko haya yataendelea kuwa chini ya TFS bajeti yake itaonekana ambayo iko mahsusi kwa ajili ya kutangaza vivutio vya utalii?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kandege, Mbunge wa Kalambo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kuyapeleka haya maporomoko haya maporomoko katika taasisi ya TFS tuliona kuna mbinu nyingine ambazo zinahitaji kusimamiwa na taasisi hii ya huduma za misitu Tanzania. Kwanza, kuna misitu ndani yake lakini pia kuna uoto wa asili ambao ndani yake unatunza vyanzo vya maji, hivyo TFS ni sahihi kabisa kusimamia maporomoko haya.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo taasisi zilizoko chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii zote zinatangaza masuala ya utalii. Tumeanza kujenga miundombinu ya barabara katika eneo hilo, pia tumetengeneza ngazi za kufika chini, tunatarajia pia kuanzisha masuala ya cable car katika maporomoko hayo ambayo tunatarajia kwamba tutapata watalii wengi sana ambao watakuwa wanatoka nchi jirani na ndani ya nchi.

Sambamba na hilo, tunajenga daraja ambalo litaunganisha Zambia na Tanzania, hii yote ni mikakati ambayo imepangwa ndani ya bajeti ya TFS. Kwa hiyo nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaenda kufanya mambo mazuri na Kalambo inaenda kufunguka. Ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wananchi wanaoishi katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Tunduru na Namtumbo wamekumbwa na taharuki kubwa sana wakati wote wa maisha yao kuhusiana na hali halisi ya wingi wa tembo na uharibifu mkubwa unaofanyika, tembo wamefikia hatua ya kufika mpaka majumbani.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwavuna hawa tembo ili waweze kupungua na adha inayowakuta wananchi hawa ipungue? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Msongozi Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la fidia Mheshimiwa Mbunge nimtoe wasiwasi na Wabunge wengine wote. Jana tulikuwa na semina tuliweza kuliongelea hili suala, tulichofanya sisi kama Serikali tumekubaliana na mawazo ya Waheshimiwa Wabunge kwamba tunayachukua kwa umoja wao, tunaenda kuangalia sheria ambayo ilipitisha mwanzo kiwango hicho tuifanyie review kisha tutaleta humu humu Bungeni tuone namna iliyobora ya kuangalia thamani ya hawa wananchi ambao wanapata hasara ya kupoteza mazao na wengine wanapoteza hadi maisha ili angalau hii fidia au kifuta machozi na jasho kiweze kukidhi haja ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, suala lingine la kuhusu taharuki ya tembo, ni kweli hii ni changamoto kubwa na tunawapa pole sana wananchi ambao wamekuwa wakikumbana na changamoto hii ya wanyama wakali hususan tembo. Serikali ina mkakati mahsusi wa kuhakikisha kwamba tunaanzisha vituo viwe karibu sana na maeneo yaliyohifadhiwa ili angalau taharuki hii inapojitokeza basi Askari wawe karibu kutatua tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo tumeendelea kutoa elimu kwa wananchi ili tuwe na ushirikishwaji wa karibu na jamii ili kudhibiti hawa wanyama wakali na waharibifu. Ahsante. (Makofi)
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jamhuri kwa niaba ya Mamlaka ya Uhifadhi kwa maana ya TAWA iliwashitaki Wenyeviti wawili wa vitongoji ndani ya Kijiji cha Mkangawalo, kesi ya jinai namba 281 kwa kosa la kufanya shughuli za kilimo kwenye hifadhi, na tarehe 27 Septemba, 2021 Mahakama iliwaacha huru watu hawa na kuagiza warudishiwe ardhi yao na mali zao kwa maana ya trekta walizonyang’anywa.

Je, ni lini Serikali sasa itarejesha mali zao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi wa Jimbo la Mlimba ni wakulima, wafugaji na wavuvi. Mamlaka hii ya Uhifadhi kwa maana ya TAWA imekuwa ikiwasumbua mara kwa mara. Je, Waziri ni lini sasa atakuwa tayari kuambatana nami kwenda Jimboni pale Mlimba kwenda kushuhudia kero hizi na kuzitatua? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Godwin Kunambi, Mbunge wa Jimbo la Mlimba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala hili ambalo lilikuwa mahakamani na Mheshimiwa Mbunge ametuthibitishia hapa kwamba watuhumiwa hawa wameshaachiwa huru na mali zao zilishikiriwa na TAWA, nitoe tu ufafanuzi katika eneo hili, kwamba mtuhumiwa anapokamatwa ushahidi na vitu vyote vinapelekwa mahakamani. Na pale ambapo inathibitika kwamba mtuhumiwa ameshinda kesi, basi mtuhumiwa anarejeshewa mali zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama mali hizi ziko upande wa TAWA, nimuhakikishie tu Mbunge kwamba tutaenda kulishughulikia suala hili ili mali hizi zirejeshwe kwa watuhumiwa. Lakini ninavyofahamu tunapopeleka kesi hizi mahakamani, tunapeleka na vithibitisho vyote na vinakuwa chini ya Mahakama. Kwa hiyo, kama iko kwetu basi nimuhakikishie kwamba vitarejeshwa kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na suala hili la pili kwamba niko tayari kwenda kutoa ufafanuzi. Nimhakikishe tu Mheshimiwa Kunambi kwamba wananchi wa Mlimba watambue kwamba Serikali iko kazini na kama nilivyosema, Timu ya Kitaifa ambayo imeteuliwa na Baraza la Mawaziri iko uwandani, inafanya tathmini bila kufanya taharuki yoyote na inashikirisha mkoa, inashirikisha wilaya na wale wananchi tukimaanisha viongozi walioko kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukishatambua Serikali inapaswa kurejesha kama wale ambao tunatakiwa kuwaondoa hifadhini kwamba watalipwa ama hawastahili kulipwa, wananchi watapewa taarifa na baada ya hapo tutaanza kutatua hii migogoro kwa kushirikishana, hatutaenda kwa nguvu kwa kuwa Mheshimiwa Rais alishasema, hataki kuona taharuki.

Kwa hiyo, nimhakikishie tu Mbunge kwamba pamoja na kuwa ametaka niende kule, lakini kwa kuwa timu ya tathmini iko uwandani, tuiache ifanye kazi. Tunapoenda sasa kuongea na wananchi tuwe na kitu cha kuwaambia wananchi bila kuweka taharuki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie kwamba tutatatua tatizo hili na tutaambatana naye baada ya tathmini kukamilika.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana; ili kuepusha migogoro na kutengeneza sense of ownership kati ya wananchi wa Jimbo la Hai hususan wanaozunguka Mlima Kilimanjaro na KINAPA. Tuliandika barua ya kuomba fedha za CSR ili kutekeleza miradi kwenye vijiji vinavyozunguka Mlima Kilimanjaro, na tayari Mheshimiwa Naibu Waziri ulipokea, nilikuletea mwenyewe. Je, ni lini Serikali itatuletea fedha hizi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha, Mbunge wa Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Wizara kupitia taasisi zake huwa tunatoa CSR kwa jamii zinazozunguka hifadhi, na Mlima Kilimanjaro una jamii mbalimbali zinazozunguka hifadhi hiyo. Kwa kuwa hapa katikati tulikuwa tuna changamoto ya UVIKO–19 Wizara yetu ilikumbana na changamoto hiyo, hivyo hatukuweza kupeleka CSR kwa wananchi kama ambavyo tulikuwa tumepanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wote wa Hai, kwamba sasa hivi utalii umeanza kuimarika vizuri. Tumeanza kupata wageni wengi, tuna uhakika kabisa kwamba ile sense of ownership ya wananchi wa Hai na maeneo mengine yanayozunguka hifadhi ya Mlima Kilimanjaro wataenda kuiona na watafaidika nayo kupitia CSR.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa migogoro kati ya Hifadhi ya Tarangire na vijiji vya Gijedangu, Hayamango, Vilimavitatu na Salama ni vya muda mrefu.

Je, ni nini mkakati wa Serikali wa kuonesha kwamba migogoro hii inafika mwisho ili wananchi wetu waweze kufanya shughuli zao za kiuchumi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sillo, Mbunge wa Babati kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimeeleza kwenye majibu ya nyongeza kwamba, maeneo yote ambayo yamezungukwa na hifadhi, Serikali itahakikisha wananchi wanafaidika na uhifadhi. Tunatambua kwamba hawa wananchi kwa asilimia kubwa wanatusaidia kusimamia maeneo haya. Sisi tuko huku makao makuu na pamoja na kuwa tuna wataumishi wetu walioko kwenye maeneo ya hifadhi, lakini askari peke yake hawawezi kulinda haya maeneo bila kushikirisha wananchi ambao ndiyo hasa wenye uchungu wa haya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba CSR ni moja ya priority ya Wizara ama Serikali kuhakikisha kwamba wananchi wanajisikia kwamba ni sehemu ya hifadhi. Hivyo, tutahakikisha kwamba wananchi wa jimbo lake wanaona umuhimu wa uhifadhi ili waendelee kutusaidia kusimamia maeneo haya yanayozunguka hifadhi ya Tarangire. Ahsante.
MHE. JEREMIAH A. MRIMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuja kwa timu ya Mawaziri nane ambayo ilitangaza kuongezwa kwa eneo la mita 500 eneo la Kinga katika vijiji vya Mbilikili, Bisarara, Tamkeri, Mbalibali, Gwikongo, Machochwe, Nyamakendo pamoja na Meringa. Pia katika nyakati tofauti mwaka 2008, 2010, 2013 mipaka ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti na vijiji hivyo imekuwa ikibadilishwa.

Sasa je, Waziri wa Maliasili pamoja na Waziri wa Ardhi wako tayari kuja Serengeti wakiambatana nami mapema iwezekanaavyo wakiwa na GN ya mwaka 1968 yenye ramani namba 14, 15, 4 ili kutatuza tatizo hili kwa sababu ni la muda mrefu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali namba mbili; mwaka 1994 Serikali ilipunguza eneo la Grumeti Game Reserve pamoja na Ikorongo Game Reserve kutoka kilometa za mraba 3,600 kuwa 993.4 lakini mpaka sasa kumbukumbu za Serikali bado hazijafanya mabadiliko hayo. Kwa hiyo, wananchi wa Makundusi, Pakinyigoti, Rwamchanga, Rwabando wamekuwa wakizuiwa kufanya shughuli zao. Je, ni lini mabadiliko hayo yatafanyika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jeremiah Amsabi Mrimi, Mbunge wa Serengeti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la mipaka kama ambavyo timu ya Mawaziri nane ilipita kutoa ufafanuzi, lakini pia ikaacha watumishi ambao walikuwa wanafanya tathmini ya namna ya kuja kutoa ufafanuzi juu ya mipaka hiyo. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Serengeti na wananchi wa Serengeti kwamba tathmini sasa hivi imeshakamilika na kinachofuata sasa ni kwenda kuonesha mipaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wizara ya Maliasili na Utalii tukishirikana na wizara ya Ardhi tutaenda kufafanua hii mipaka tukiwa na wananchi wa maeneo hayo na lengo ni kuondoa sasa ile vurugu au taharuki ya kutotambua mipaka kati ya hifadhi na wananchi.

Kwa hiyo, niwahakikishie hawa wananchi kwamba tathmini imeshakamilika tunakuja sasa kufafanua utambuzi wa mipaka ni ipi ya hifadhi ni ipi ya wananchi, hilo linaenda kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na swali lake la pili limehusiana na ufafanuzi wa GN baada ya kurekebishwa eneo la Hifadhi ya Ikorongo; Serikali italifanyia kazi eneo hili na tutapeleka waraka kwa wananchi kwa maandishi sasa kuonesha kwamba eneo hili litakuwa ni la hifadhi na lile ambalo limeachwa kwa wananchi ili wawe na uwezo sasa wa kufanya shughuli zao za kila siku, tutaenda kulifanyia kazi na tutatoa taarifa kwa wananchi wa Wilaya ya Serengeti.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Waziri kumekuwa na mgogoro wa muda mrefu sana kati ya Hifadhi ya Kitulo na Vijiji vya Misilo, Lugoda, Igenge, Nkindo na Makwalanga. Je, lini Serikali itamaliza tatizo hili la mipaka kati ya Hifadhi na vijiji hivi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Neema, Mbuge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwape pole wananchi wa Makete hususan wanaozunguka eneo hili la Kitulo. Nilishawahi kuzungumza na Mheshimiwa Mbunge na nikatoa ahadi kwamba tungeenda kuutatua huu mgogoro, lakini kutokana na changamoto mbalimbali sikuweza kupata huo muda. Lakini ninamuahidi Mbunge na ananitazama hapa kwamba wananchi wa Makete wakae mkao wa kusubiri, tunaenda na Mheshimiwa Mbunge kutatua mgogoro huu. Na mgogoro huu tunaenda kuumaliza ili wananchi waweze kufanya kazi kwa uhuru na hifadhi tuweze kuisimamia vizuri. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza nalo liko hivi; je ni lini Serikali itatua mgogoro kati ya Arusha National Park na wananchi wa Kijiji cha Lukungw’ado ambao unatokana na Serikali haikununua bila kushirikisha Serikali ya Kijiji mashamba Namba 40 na Namba 41 ambayo wananchi walikuwa wanategemea kujikimu nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza na Mheshimiwa Pallangyo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti suala la kutatua migogoro ni wajibu wa Wizara ya yale maeneo ambayo hatujayafikia ni mhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakuja kuyatatua, na ukizingatia maeneo mengi yalikuwa kwenye vijiji 920, lakini kwa yale maeneo ambayo hayakuingizwa kwenye vile vijiji 920, na migogoro yao ni mipya tumeshaelekeza wananchi kupitia wawakilishi wao watuletee malalamiko haya ili tupite katika maeneo hayo tuweze kutatua migogoro hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro mingine ni ya kufika sisi kama viongozi, kukaa na wananchi tukaisikiliza. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaambatana katika Jimbo lake ili tuweze kutatua mgogoro huu.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru; migogoro ya ardhi kati ya Hifadhi ya Serengeti Wilaya ya Serengeti na Wilaya ya Tarime, Bunda umekuwa ni wa muda mrefu na ambao mingine inapelekea hata kuzuia wananchi kufanya shughuli zao, mathalani Kata ya Nyatwali iliyopo Wilaya ya Bunda ambayo ina vijiji vitatu, cha Serengeti, Tamahu na Nyatwali yenyewe ina wakazi takribani 10,000 na Serikali imepeleka miradi ya umwagiliaji takribani wa bilioni 1.7 na maji safi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wakazi hao wamezuiliwa kuendeleza makazi yao takribani miaka 10; tunataka kujua ni kwa nini Serikali isiwaache hao wananchi waendeleze na makazi kwa sababu mmeshindwa kuwalipa fidia ili iweze kuondoka takribani miaka 10 sasa hivi?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna maeneo mengo likiwemo eneo la Nyatwali ambalo kiuhalisia lilikuwa ni eneo la wananchi, na nipende tu kuwaambia wananchi wa Nyatwali kwamba hakuna mgogoro isipokuwa wananchi walioko pale wako kihalali kabisa, wanaishi kihalali na Serikali ilishasajili vijiji na wananchi wapo miaka ya tangu 1974, wapo pale. Hilo niwaondoe wasiwasi, hakuna mgogoro isipokuwa yale maeneo hata wewe ni shahidi umekuwa ukiona malalamiko mengi ya Waheshimiwa Wabunge wananchi wao wanalalamika kwamba kwa asilimia kubwa wanachangamoto ya wanyama wakali hususani tembo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hili wananchi wa Nyatwali ni mojawapo ya maeneo ambayo yana kilio hiki, tathmini ya Serikali ni kuangalia namna iliyobora ya kuepusha hawa wananchi wasiendelee kuteseka na wanyama wakali. Maeneo ni mengi yamezibwa yamewekwa makazi ya kudumu, wananchi wamejenga kwenye maeneo ambayo ni mapito ya wanyama ukiangalia eneo la Nyatwali ni eneo moja wapo ambalo upande mmoja ni Serengeti National Park, upande mwingine ndio Nyatwali ilipo na vijiji vya jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiruhusu pale wananchi kuendelea kuishi changamoto ya wanyama wakali tutaendelea kulia kila siku kwa hiyo mimi niwaombe wananchi, maeneo yote ambayo tumeyainisha Serikali imesitisha kuleta huduma mbalimbali, Serikali imeshaanza kufanya tathmini wananchi watalipwa kupisha maeneo hayo. Na hili ni tamko la Serikali kwamba ili kupunguza athari za wanyama wakali ni vyema tukatafuta eneo maalum ya mapito ya wanyama kuliachia ili wananchi waishi kwa amani na wanyama waendelee kupita katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili tunalishughulikia kwa uhakika na kwa haraka zaidi ili wananchi waweze kuishi kwa amani na Serikali iendelee na taratibu za uhifadhi ahsante.