Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Mary Francis Masanja (6 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Awali ya yote nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na leo tumekutana katika Bunge lako hili Tukufu. Kipee nikushukuru sana wewe binafsi, kwa kuendelea kulitumikia Bunge hili Tukufu, lakini pia kwa leo kuwa katika uamuzi au ujumuishi maalum wa Sekta yetu hii ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru sana Wabunge wote waliochangia kwenye sekta yetu hii ya maliasili na utalii na niwapongeze sana kwa kuweza kutupa mawazo chanya ya kuweza kuijenga sekta hii ya maliasili na utalii. Mawazo yao, michango yao na ushauri tumeupokea. Niwaahidi kwamba tunaenda kuufanyia kazi kwa nguvu zote, nikishirikiana na Mheshimiwa Waziri na niwaahidi kwamba sisi tuko imara na tumejiandaa kuhakikisha kwamba tunachapa kazi ili tusiwaangushe wao pamoja na wananchi waliotupa dhamana ya kuwaongoza katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza kuelezea kwenye eneo la maliasili misitu. Jukumu la Sekta ya Maliasili na Utalii kwanza kabisa tunahifadhi maliasili zilizopo nchini, lakini pia tuna malikale, lakini baada ya kuhifadhi tunaendeleza utalii. Kwenye eneo hili la maliasili misitu nitapenda sana kuzungumzia upande wa matumizi ya mkaa na kuni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa asilimia 95 ya Watanzania tunatumia nishati ya mkaa na kuni na naomba nilielezee hili kwa ufasaha kabisa kwa kuzingatia Sheria ya Misitu Na. 14 ya mwaka 2002, Sura 323 inasema kwamba mkaa ni moja ya mazao ya misitu yanayoruhusiwa kuvunwa kisheria. Naomba hili nilifafanue kwa ufasaha kwamba hakuna Waziri wala mtu yeyote ambaye amewahi kuzuia uvunaji wa mkaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naongea hivi kulingana na sheria hii, lakini nitapenda kufafanua kwa nini sisi Maliasili na Utalii tunasimamia eneo hili. Tunaomba sana na sheria hii tunaisimamia pale tu ambapo uvunaji wa mkaa unafanywa kiholela. Tunasimamia kwa lengo la kuhakikisha kwamba tunahifadhi maliasili misitu ili iwe endelevu kwa vizazi na vizazi vijavyo. Kwa hiyo, kwa kuzingatia kwamba zao hili linachangia asilimia 3.5 ya GDP lakini pia kwa asilimia 43 ya GDP inachangia pato ghafi la sekta ya misitu ikiwemo mbao na mkaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili tunawahamasisha wavunaji wa mkaa na watengenezaji wa mkaa kwamba pale tu ambapo wanahitaji kwenda kuvuna mkaa, basi watapata vibali maalum ili kuonyesha maeneo stahiki ambayo yanapaswa kuvunwa, lakini pia kuendelea kusimamia maliasili misitu kwa ajili ya maendeleo ya baadaye.

Mheshimiwa Naibu Spika, itakumbukwa kwamba wiki moja iliyopita ambayo tulikuwa kwenye Wiki ya Mazingira Duniani ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pia alitoa tamko juu ya tujiandae sasa kuanza kuhama kutoka kwenye matumizi ya nishati ya mkaa na kuni twende kwenye nishati mbadala ya gesi. Aliagiza taasisi mbalimbali vikiwemo vyuo, mashule, mahospitali na magereza kwamba tuendelee sasa kuhamasisha wananchi waanze kuhama kutoka kwenye matumizi ya mkaa na kuni, tuelekee sasa kwenye kutumia gesi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo ni kupunguza ukataji wa miti holela, lakini pia pale panapo umuhimu sana wa uvunaji wa mkaa, basi utoke kwa vibali, si kama ambavyo sasa hivi wananchi wamekuwa wakijichukulia kwa namna ambayo si stahiki sana na inasababisha sasa uvunaji unakuwa ni holela, miti inakatwa ovyo na mwisho wa siku itasababisha jangwa litokee hapa nchini na tutaonekana sasa sisi kwenye usimamizi wa maliasili misitu kwamba tumelegea kidogo. Kwa hiyo niwaombe sana na katika hili tuendelee kuwaelimisha wananchi, yeyote yule ambaye anahitaji kwenda kuvuna mkaa, basi apate kibali aelekezwa na eneo ambalo anapaswa kwenda kuvuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitapenda kuongelea kwenye eneo la utalii, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwenye eneo hili, wametupanua mawazo mengi na wametupa michango mingi sana ya kwenda kuboresha kwenye sekta ya utalii. Tumeyapokea mawazo yao, lakini nitapenda tu kuwakumbusha kwamba, sisi kama Watanzania, nitaomba sana uzalendo uanze na kwetu sisi. Nikisema hivyo, naamini kabisa utalii ukianza na sisi wenyewe, tutachangia pato kubwa sana hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, uzalendo uanze na sisi Wabunge tuliomo humu ndani na kwa ridhaa yako, nitaomba baada ya kumaliza Bunge lako hili Tukufu, tumeandaa safari, Wabunge tuwe mfano, Wabunge wazalendo naamini wote humu tuko ni Wabunge wazalendo tutembelee maeneo yetu ya vivutio na sisi tuwe mabalozi namba moja wa kutangaza utalii ndani na nje ya nchi. Naamini kabisa sisi wenyewe tukiwa wazalendo, utalii utakua kwa kasi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeandaa mikakati mingi ya ku-promote utalii na vivutio vilivyomo hapa nchini na niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba baada ya Bunge hili nadhani wataanza kuona tu amshaamsha zitakazokuwa zinaendelea. Pia tulikuwa tumeshaandaa mipango mikakati ya kukutana na watu mbalimbali wakiwemo Waandishi wa Habari. Hata hivyo, tuna mkakati wa kusambaza vipeperushi mbalimbali hasa kwa wale ambao wanapokea wageni wetu wanapoingia hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naweza nikatolea mfano, kwa mfano, tunaweza tukaandaa hata vipeperushi kwa hawa vijana wetu au wananchi ambao wanapokea wageni wetu kutoka nje ya nchi, wakawa na vipeperushi maalum lakini pia wao wenyewe kwa uzalendo kama Watanzania, pale ambapo unambeba abiria yeyote yule aliyetoka nje ya nchi mueleze kwamba tuna Mlima Kilimanjaro, tuna hifadhi, tuna malikale, tuna kila aina ya vivutio hapa nchini. Kwa hiyo ile elimu wakati unampeleka kule anakoenda kupumzika, anakuwa tayari ameshaanza kujua kwamba Tanzania ina vivutio vya namna gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tutasambaza vipeperushi ambavyo vitasaidia pale ambapo abiria wa kutoka nje ya nchi anaingia ndani ya nchi, basi ataonyeshwa Ngorongoro crater iko wapi, kama ni Serengeti iko wapi, lakini pia ataonyeshwa vivutio mbalimbali vinavyotokana na malikale. Hii yote ni kuhakikisha kwamba mgeni yeyote anayeingia hapa nchini, basi aelezwe Tanzania ina mazao gani ya utalii ambayo yatamhamasisha yeye aende kwenye kutalii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitapenda pia kuongelea kwenye swahili tourism, hili nalo litakuwa ni eneo mojawapo la kuhamisha utalii, ambapo tutandaa vitu mbalimbali ikiwemo maonyesho ya mavazi, lakini pia tutaanda matamasha mbalimbali ya vyakula vya asili, ngoma na utalii wa utamaduni. Haya yote ni maeneo ambayo tumejipanga, sisi kama Wizara kuhakikisha kwamba sekta hii ya maliasili na utalii inakuwa kwa kasi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge, pale ambapo tuna uhitaji wa kuonyesha ubalozi katika maeneo yetu, naweza nikaja kwenye wilaya mojawapo nikataka kucheza hata zile ngoma zetu ili kuhakikisha kwamba utalii wa utamaduni unakua, tushirikiane kwa pamoja kuhakikisha kwamba tunauendeleza utalii wa Tanzania na vivutio vyake vilivyomo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitapenda pia kuongelea eneo la miundombinu; niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba eneo hili tumezingatia bajeti hii mtakayoipitisha ninyi kuhakikisha kwamba maeneo yote yenye vivutio yanapitika kwa ufasaha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeandaa bajeti ambayo itakidhi kulingana na maeneo yote ambayo yana changamoto ya miundombinu. Kwa hiyo hifadhi zote na maeneo yote ya malikale tumezingatia. Tutawaomba tu Waheshimiwa Wabunge kwamba tunapopitisha bajeti hii basi muipitishe tu vizuri mkiamini kwamba tunakwenda kutekeleza na kuhakikisha kwamba miundombinu itapitika na watalii waweze kuingia hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo napenda kuliongelea ni kuhusu mapendekezo ya Waheshimiwa Wabunge ambayo wamependa kuyaongelea kuhusu ufunguzi wa mageti. Eneo hili…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. Nawashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya bajeti ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ya mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo ameendelea kutupa maelekezo lakini kutekeleza shughuli mbalimbali za Serikali ikiwemo utekelezaji wa miradi ya maendeleo ambayo kwa kusema ukweli tumeiona jinsi ambavyo inaenda kwa kasi.

Mheshimiwa Spika, napenda pia kuongelea suala la Maliasili Mheshimiwa Rais amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kwamba Maliasili tunazilinda, tunazitunza pia tunaendeleza masuala mazima ya utalii. Kwenye upande wa sekta ya Maliasili na Utalii tumekuwa na changamoto nyingi sana hususani za Wanyama wakali na waharibifu na hili limeweza kujitokeza hata kwenye hotuba hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ambapo tuna maeneo mengi yenye changamoto za Wanyama wakali na waharibifu pia kumekuwepo na vyakula mazao yanaliwa na wanyama wakali na kwa bahati mbaya kabisa inapelekea mpaka vifo vinatokea.

Mheshimiwa Spika, Serikali inayongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan inajitahidi sana kupunguza athari hizi ikiwemo kuanzisha vituo mbalimbali vya kudhibiti wanyama wakali na waharibifu, hili tunaendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu mwaka wa fedha ulioisha aliweza kutoa fedha na tumeweza kujenga vituo takribani 16 tukavielekeza katika maeneo hususani yenye changamoto hizi.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo mwaka huu wa fedha tunatarajia pia kujenga vituo 13 na tutaelekeza hukohuko kwenye maeneo ambayo yana changamoto hizi. Niwaombe wananchi kwamba tumeanzisha pia programu ya kufundisha vijana ambao tunawaita VJS walioko kwenye maeneo yetu hayahaya tunayoishi, lengo ni kuhakikisha kwamba jamii zinazozunguka maeneo ya hifadhi zitambue namna ya kujikinga na wanyama wakali na waharifu. Tayari tumeshaanza na kila kituo, vile vituo ambavyo tumeshavijenga tayari tumepeleka vijana wanne wanne kila kituo ambao wanatoka katika maeneo husika. Hii inasaidia kwa sababu tumeanzisha utoaji wa ajira katika maeneo hayo lengo ni kudhibiti hao wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, ninaendelea kutoa ahadi kwa wananchi na Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali ipo na inaendelea kulifanyia kazi suala hili kwa nguvu zote na Mheshimiwa Rais analiangalia kwa ukaribu sana, hata mtakumbuka mwaka jana alifanya ziara katika Mkoa wa Simiyu, ahadi yake ilikuwa ni kuajiri askari takribani 600. Tayari tumeshaanza kupata vibali vya kuajiri.

Mheshimiwa Spika, hivi ninavyoongea kuna Askari 271 tayari tumeshapokea vibali vyao ambao watasambazwa katika maeneo yenye changamoto. Kwa hiyo, ninaendelea kuwatoa wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwamba changamoto hii tunaendelea kuiangalia kwa karibu sana na tunaendelea kufikisha huduma kwa wananchi ili tuweze kuokoa maisha ya Watanzania pia na mazao ambayo yameendelea kupata kadhia hii.

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba ardhi haitoshi na mahitaji ya ardhi ni makubwa, kila mtu anatamani sana kuongezewa maeneo. Tutakumbuka kwamba Mheshimiwa Rais aliruhusu kusamehe vijiji takribani 920 na baadhi ya vijiji hivyo vingi vilikuwa vimesajiliwa ndani ya hifadhi. Tunaposema tunaachia hivi vijiji kwa upande mwingine tunakaribisha changamoto ya wanyama wakali na waharibifu. Niendelee kuwaomba wananchi pale ambapo Kijiji kiliachiwa kikasajiliwa ndani ya hifadhi lakini tunakutana na changamoto hizi, basi tushirikiane pamoja kudhibiti hawa wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Spika, kile tunachotaka sekta ya maliasili na utalii ni kuangalia maeneo mahsusi ambayo ni shoroba za wanyama wakali na waharibifu ambao wanahama kutoka eneo moja kwenda eneo jingine basi tuachie maeneo hayo ili kuruhusu mzunguko wa wanyama kiikolojia waweze ku- move kutoka sehemu moja kwenda nyingine.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde thelathini malizia mchango wako.

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kulikuwa pia na hoja iliyojitokeza katika Jimbo la Biharamulo ambalo ilielezewa na Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa. Kwanza ninampongeza Mheshimiwa Mbunge kwamba kumekuwepo na tuhuma ambazo zinaidhalilisha Serikali, kwamba kuna watumishi ambao wamekuwa wakipokea kiasi kidogo wanaruhusu wananchi wanaenda kulima katika maeneo ya hifadhi. Ninaahidi kwamba hili tutaenda kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, pia nataka nitoe taarifa tu kwamba tarehe 24 Oktoba, 2022 tulikamata baadhi ya wakulima ambao walikuwa wamechangishana fedha na wakataka kumrubuni Mhifadhi wa Biharamulo, taarifa hizi ziko TAKUKURU ninavyoongea na hawa watuhumiwa walifikishwa Mahakamani. Tunachoomba ni ushirikiano, anayetoa rushwa
na anayepokea wote wako matatani. Kwa hiyo, kama wananchi wanashiriki kutoa rushwa ili waende kulima kwenye maeneo yale, sheria zitachukua mkondo wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kumekuwa na changamoto ya wakulima ambao wanaingia kisirisiri wanalima, tunapoenda kuyazuia yale maeneo tayari wanakuwa wamefika kwenye hatua ya kuvuna, tunaporuhusu sasa kwamba mkimaliza kuvuna sasa msiingie tena, wanaweka kwenye makoti yao mbegu tena ambayo hiyo mbegu anapovuna anapanda tena kule halafu anakuja analalamika kwamba kwa nini tumezuia haya mazao,

Mheshimiwa Spika, kupitia Bunge lako Tukufu hili naomba...

SPIKA: Sawa Mheshimiwa, nilishakuongeza sekunde thelathini naona umejiongeza dakika nyingi zaidi. Haya malizia sentensi yako.

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, tunaomba wakulima tunapozuia basi wasiingie hifadhini kwa sababu haya maeo tunayalinda kwa maslahi ya taifa letu.

Mheshimiwa Spika, naunga hoja. Nashukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante nami nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa namna ambavyo ameendelea kutulinda hadi ameweza kutufikisha siku hii ya leo ambapo tunakwenda kuhitimisha Bajeti yetu ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, kipekee nimpongeze na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa namna ambavyo amekuwa mstari wa mbele wa kuhakikisha kwamba uhifadhi na dhamira yake kuu ya kuendeleza utalii inazingatiwa katika sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuwapongeza Mheshimiwa Makamu wa Rais na Waziri Mkuu kwa jinsi ambavyo wanaendelea kuipigania sekta hii ukizingatia kwenye masuala mazima ya uhifadhi wa mazingira, lakini pia Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kwamba migogoro mbalimbali iliyokuwa kwenye sekta yetu hii ameendelea kuisimamia na kuitatua kwa ufasaha zaidi.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipokupongeza wewe kwa uthubutu ambao umeuonesha kama mwanamke mwenzetu. Tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu kwa harakati hii unayoiendea, tuna imani na wewe na tunaamini ushindi unarudi Tanzania. Tunakuombea sana na Mwenyezi Mungu akakufanikishe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kwa moyo wa dhati kabisa nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri wangu, Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa na nimpongeze kwa namna ambavyo ameipokea Wizara lakini kwa jinsi ambavyo ameipokea Wizara lakini kwa jinsi ambavyo ameichukua kwa muda mfupi na kuielewa vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara yetu ina changamoto nyingi sana, lakini kwa muda mfupi tayari tumekwishaanza kuiona nuru na Waheshimiwa Wabunge tayari wameonesha kwamba wanakwenda kushirikiana na sisi kwa nguvu zote. Niendelee kumuahidi Bosi wangu kwamba tutashirikiana vizuri na nitampa ushikiano wa kutosha kuhakikisha kwamba Wizara hii tunaipigania na kuivusha hapa ilipo na tunaipeleka mahali fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii ya dhati kabisa kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge lakini niwapongeze sana kwa namna ambavyo wametupa ushauri, kwa namna ambavyo wametupa maelekezo, lakini kikubwa wametuonesha wapi tulipo.

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa nini? Unapokuwa umevaa nguo yako unaweza ukaona umevaa vizuri na umependeza, lakini ukikutana na mwenzio akakwambia hapa kuna doa huyo anakupenda sana. Vile vile, sisi tunawashukuru Waheshimiwa Wabunge wametuonesha ni namna gani tunapaswa kwenda. Niwaahidi kabisa kwa moyo wa dhati kwamba, yale yote ambayo wametuelekeza, wametushauri na yale ambayo wametupatia kama mapendekezo tumepokea na tutayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kazi ya uhifadhi na hususani kulinda rasilimali za Taifa ni kazi kubwa sana na inahitaji ushirikiano wa kutosha. Kuna milima na mabonde, hizi rasilimali tulizonazo tunazozilinda, tunazitunza si rasilimali za mzaha. Tunakutana na milima, mabonde na changamoto nyingi, lakini tunaamini kwa maelekezo waliyotupatia Waheshimiwa Wabunge na kwa namna tunavyokwenda kushirikiana na wananchi kuzungumza, kushuka nao huko chini ili tukae nao kwa pamoja tutahakikisha kwamba migogoro mingi tunakwenda kuipunguza ama kuimaliza kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sekta yetu hii inategemewa na sekta nyingi. Ukiangalia katika maliasili hatuhifadhi wanyamapori peke yake. Hatuhifadhi kwa ajili ya utalii, lakini ndani ya sekta hii kuna sekta nyingi zinaitegemea. Sekta ya nishati, usipokuwa na eneo maalum ulilohifadhi vyanzo vya maji na kadhalika hakika sekta ya nishati haiwezi kuendelea. Vilevile tuna sekta ya mifugo, sekta ya kilimo, tuna maji, mazingira na kwenye mazao pia tuna uchavushaji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunatunza haya maeno sio kwa ajili ya kuendeleza utalii peke yake ni kwa sababu tunaishi na uhai wetu unategemea sana maeneo hayo. Kwa hiyo, ningependa hili tulielewe sisi kama wawakilishi wa wananchi kwamba maeneo haya tunayatunza kwa ajili ya Watanzania wote, ni kwa ajili ya maslahi yetu wote ni kwa ajili ya uhai wetu wote Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kuna suala la migogoro Waheshimiwa wameliongelea. Natambua kwamba Mheshimiwa Waziri atalifafanua, lakini pia kwa yale yote ambayo wametuelekeza tutaendelea kuyafanyia kazi na tunatamani sana migogoro hii iishe. Niendelee kuchukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, uthubutu huu wa kutatua migogoro hii ni mwanamke jasiri na wa kwanza aliyeamua kutekeleza wazo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukikumbuka migogoro hii imekuwa na historia ndefu sana. Iliundwa Kamati ya Mawaziri Nane ikaingia uwandani ikaanza kuibua migogoro. Hata hivyo, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa unyenyekevu mkubwa ameingia ndani akaamua yeye mwenye kuitekeleza. Ndani ya miaka miwili sasa hivi tunaelekea kutatua migogoro yote.

Mheshimiwa Spika, tumpongeze sana Mheshimiwa Rais ndani ya mwaka mmoja tumezunguka na tumekwenda mkoa kwa mkoa, tumezungumza na wananchi, lakini hatuwezi kukataa mapungufu yapo, lakini tunaendelea kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa namna amabavyo anaendelea kutuelekeza na sisi tunaendelea kuahidi kwamba kwa ile migogoro ambayo bado ipo, tutashuka na tutakwenda kuzungumza na wananchi na kuhakikisha kwamba migogoro hii inakwisha kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mikakati mingi ambayo Waheshimiwa Wabunge wameweza kuifafanua na kuielekeza katika Wizara yetu ya Maliasili na Utalii, tumeipokea. Kuna suala zima la kuimarisha Utalii wa Fukwe. Kwa sasa Wizara imejipanga kuanisha maeneo ambayo yanaweza kuwa mahususi kwa ajili ya fukwe. Tumeainisha fukwe hizi katika Mkoa wa Mtwara, Lindi, Dar es Salaam, Pwani na Tanga, lakini pia tunakwenda kuangalia maeneo ya Kanda ya Ziwa ili fukwe hizi sasa ziweze kutumika ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, pale ambapo kama walivyopendekeza Waheshimiwa Wabunge kwamba fukwe hizi zikimilikiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii basi itakuwa ni rahisi sana kwenye utekelezaji wa uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, kuna wazo lingine limetolewa la Kiberenge (Utalii huu wa cable car). Kwa sasa hivi Wizara imeshaweka mshauri mwelekezi ambaye ameshaanza kufanya upembuzi, kupata mawazo ya wadau mbalimbali na kuangalia namna ya masuala mazima ya mazingira.

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kupokea mawazo na ushauri kutoka kwa wadau. Muda wa utekelezaji ukifika na wadau watakapokuwa wameshatupatia mawazo ya kutosha, zao hili la utalii la cable car litakwenda kutekelezwa kwa nguvu zote. Tunaamini kwamba kwa sasa hivi asilimia 80 ya utalii tunategemea sana utalii wa hifadhi kwa maana ya wanyamapori. Kwa hiyo sasa hivi tunajikita sana katika kutanua wigo katika mazao mengine ya utalii ikiwemo utalii huu wa kiberenge (cable car).

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo tumepata maoni mengi kutoka kwa Wabunge hususani suala zima la mali kale. Kwenye suala hili la malikale tumeanza kujitanua na hivi sasa ukienda hata Kilwa tumeshaanzisha utalii wa meli na sasa hivi tunapata watalii wengine kutoka nje ya nchi. Hii yote ni kuboresha maeneo mbalimbali ya kihistoria lakini wakati huo huo tunatanua wigo wa utalii.

Mheshimiwa Spika, sambamba na suala la utalii tumeendelea kuhamasisha masuala mazima ya uwekezaji. Kama ambavyo tumesikia kwamba sasa hivi Tanzania tuna vitanda 132,676. Hiki ni kiwango kidogo sana kwenye masuala mazima ya uwekezaji ukilinganisha na mataifa mengine. Kwa hiyo, tumekwishazindua investment forum lakini pia tumeendelea kuhamasisha wawekezaji mbalimbali na hata humu ndani wawekezaji wamo. Tunaendelea kuwahamasisha tujenge Hotel, lodge, tujenge maeneo ambayo watafikia watalii wetu ili tuweze kupanua wigo wa namna ya kuwahudumia wageni wetu.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni kuhusu miundombinu. Waheshimiwa Wabunge wameongelea sana suala la miudombinu wezeshi ambayo inaweza ikasaidia utalii kufikika maeneo mbalimbali. Tumeshaanza kuboresha miundombinu hii ukizingatia tulikuwa tuna Hifadhi 16 za Taifa na sasa hivi tuna Hifadhi 22, maeneo haya yote tumeshaanza kutengeneza miundombinu ya barabara lakini pia tunaweka uwekezaji ndani yake ikiwemo kujenga lodges na hotels na hii ni maandalizi mazuri sana ya mapokezi ya wageni wanaoweza kuja katika hifadhi hizo.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na suala zima la misitu hususani upandaji wa miti, lakini pia tumeanzisha mpango kabambe unaitwa “Achia Shoka Kamata Mzinga.” Huu ni mpango mahususi wa kuwezesha wenzetu wote ambao wanashughulika na suala zima la ufugaji nyuki wahakikshe kwamba ukataji wa miti tunaukomesha lakini tunafuga nyuki kwa kuachia shoka halafu tunakamata mzinga. Lengo ni kuhakikisha kwamba zao hili…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa.

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: …na mazao mengine yanayotokana na nyuki yaweze kuboreshwa ama kulimwa kwa kiwango cha juu.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Mheshimiwa Waziri aliweza kuzindua mpango huo…

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana.

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutupa kibali cha kuweza kujadili bajeti yetu ya Wizara ya Maliasili na Utalii katika siku hii ya leo, lakini kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini nimpongeze sana kwa kuipa kipaumbele sekta hii ya maliasili na utalii ambapo hivi karibuni ameweza kuzindua filamu ya Royal Tour na kwa kiasi kikubwa na kiwango kikubwa ameweza kuhamasisha utalii wa ndani na nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi ninavyoongea sasa ndani ya miei minne ya Januari mpaka Aprili tumekuwa na ongezeko la watalii wengi sana na kuanzia mwezi Mei mpaka Disemba hoteli nyingi hifadhini zimejaa kwa maana ya booking. Hivyo ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuipa kipaumbele sekta hii ya muhimu ambayo kiukweli sisi tukishindwa kutekeleza majukumu haya basi tulaumiwe sisi. (Makofi)

Kwa hiyo, tumhakikishie tu Mheshimiwa Rais kwamba tutaendelea kutangaza utalii, tutaendelea kuhabarisha habari njema za vivutio vyetu tulivyonavyo hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo nichukue nafasi hii kwanza kuwashukuru Wabunge wote kwa michango yao mizuri sana na mingi imekuwa ni ya kutuelekeza, lakini pia kutuonesha namna ambavyo tunataka kwenda, tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara yetu hii ya Maliasili na Utalii ina changamoto nyingi sana na sisi tunatambua hilo na tumeyapokea mengi ambayo mmetuonesha njia na sisi tunawaahidi kwamba tutaenda kuyatekeleza na yale magumu ambayo tutaona yanatushinda sana basi tutashirikiana na ninyi kuhakikisha kwamba sekta ya utalii inapaa na zaidi tunamsaidia Mheshimiwa Rais kuendeleza sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende tu kusema machache ili niunge hoja; kwanza kabisa nipende tu kusema kwamba jukumu la Wizara ya Maliasili na Utalii ni kulinda, kutunza, kuhifadhi, lakini pia na kuendeleza utalii. Sisi kama Wizara tumepewa jukumu hili la kuangalia maeneo yote yaliyohifadhiwa, tunayatunza, tunayalinda, tunayahifadhi, lakini yanapoleta kivutio kizuri basi tunahamasisha utalii ili watu waone maeneo haya kwamba tumeyatunza kwa namna gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo ndani ya maeneo haya tunatunza vyanzo vya maji, lakini tunatunza misitu, lakini tunadhibiti mabadiliko ya tabianchi, sambamba na hilo tunatunza mazingira. Sekta nyingi zinaitegemea sana sekta hii ya maliasili; nikianza na sekta ya nishati, bila kuwa na vyanzo vizuri vya maji hatuna umeme, kwa hiyo, uchumi wan chi unategemea sana katika sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ninapoenda kwenye misitu pia, misitu yetu tukiimaliza tukashindwa kuitunza vizuri hatutaweza kuishi. Tunasema misitu ni uhai, lakini sambamba na hilo tunapata maji kutoka kwenye maeneo yale kwa hiyo, ningependa kuliweka wazi hili tutambue kwamba tunapoyahifadhi haya maeneo tuna lengo zuri kabisa la kuhakikisha kwamba sisi tunaishi na Mungu aliyaweka haya maeneo ili yaweze kutufanya tuishi vizuri. Tunapata hewa nzuri kutoka kwenye maeneo haya. Wizara ya Muungano na Mazingira wanatutegemea sisi, tukisema leo maliasili tutelekeze haya maeneo hizi sekta nyingine zote haziwezi kuendelea. (Makofi)

Kwa hiyo, niendelee kuwaomba Waheshimiwa Wabunge pamoja na kuwa na changamoto nyingi katika sekta hii, lakini bado tuone na upande wa pili wa umuhimu wa sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wa sekta hii unategemewa sana na sekta mbalimbali. Nikienda kwenye sekta ya mifugo, tunapoleta mtalii hapa ndani lazima mtalii atakula, nikisema uvuvi atakula samaki, nikienda kwenye usafirishaji pia tutasafirisha abiria, nikienda kwenye kilimo pia tutauza mazao yetu kwa huyu mtalii anayekuja, lakini tutauza maji, lakini kwa wakati huohuo sekta hii inatuletea watalii wengi ambao wanatuongezea uchumi wetu katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaenda moja kwa moja kwenye eneo la migogoro ya mipaka; sekta hii ni kweli tumekuwa na changamoto nyingi sana za mipaka, migongano kati ya hifadhi na wananchi na inaleta hatari kubwa na pengine wananchi wanapoteza maisha.

Kwanza nitoe pole sana kwa wananchi ambao wanakumbana na kadhia hii, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Rais alianzisha Kamati ya Mawaziri Nane na sambamba na hilo tumeendelea kuhabarisha umma, pale ambapo kuna migogoro mipya wailete tuitatue na changamoto hizi tumeshaanza kuzipokea na Serikali ya Awamu ya Sita imeweza kuachia vijiji 920 ambavyo vilikuwa ndani ya hifadhi, lakini kwa huruma ya Mheshimiwa Rais amevirudisha kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo migogoro mipya bado tunaipitia ili tuhakikishe kwamba mwananchi kwanza, hifadhi tunaiangalia baadae. (Makofi)

Kwa hiyo, niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwamba ndio maana kuna Kamati hii ambayo inazunguka nchi nzima, lengo ni kutokuwepo na taharuki kwa wananchi. Na haya ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais na tunayatekelea kwa sababu alisema sitaki kusikia taharuki yoyote. (Makofi)

Niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge, tunaenda kutatua matatizo haya kwa mashirikiano baina ya wananchi na wahifadhi, ili kuleta amani nzuri na wahifadhi wawe na amani ya kuyasimamia yale maeneo ambayo yatakuwa yameachiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuendelee kuipongeza Serikali na tuendelee kuwa-support Maliasili na Utalii ili tuweze kufikia mahali ambapo jamii zitambue uhifadhi ni sehemu ya maisha yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitapenda pia niongelee eneo la tozo. Waheshimiwa Wabunge baadhi wameongelea kuhusu tozo; ni kweli sisi tuna tozo, lakini tunaangalia hizi tozo tukijilinganisha na washindani wenzetu. Tuna washindani wa nchi jirani ambao tunapopanga hizi tozo tunaangalia na wenzetu wana tozo za aina gani.

Mheshimiwa Spika, mfano nitapenda kuongelea katika hifadhi zetu nne ambazo mwaka jana tulipandisha kiwango cha kiingilio kutoka dola 60 kwenda dola 70, tuliongeza dola 10. Ukilinganisha na washindani wetu mpaka sasa nikisema hata Masai Mara sisi tunapotoza Serengeti kwa dola 70 wenzetu wako dola 80. Serengeti ni hifadhi bora Barani Afrika, unapoiongelea Serengeti huilinganishi na Masai Mara, lakini bado Serengeti iko chini ya Masai Mara, kwa hiyo, tunapoongelea hizi tozo lazima tujilinganishe na wenzetu wana kiwango gani na sisi tuna kiwango gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini sambamba na hilo tulipandisha kwenye maeneo ya Tarangire, Arusha pamoja na Ziwa Manyara ambapo tulitoka dola 45 kwenda dola 50, tumeongeza dola tano. Kwa hiyo, tuangalie tozo zetu hizi ziko na ni kipindi cha peak, kipindi cha high season. Tunapoenda kwenye low season tunaenda kwenye tozo ya kawaida ambayo ilikuwa ni ya miaka ya nyuma. (Makofi)

Kwa hiyo, bado ukilinganisha na vivutio vyetu vilivyo bora tuko kwenye standard nzuri na watalii wanaendelea kuongezeka. Niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwenye eneo hili tumejipanga vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo nataka niwaondoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kuhusu miundombinu katika maeneo ya hifadhi. Tumshukuru sana Mheshimiwa Rais amweweza kutupatia fedha shilingi bilioni 90.2 za kujenga miundombinu ya barabara katika maeneo ya hifadhi. Fedha hizi tumezielekeza kununua miundombinu ya mitambo, lakini pia na ujenzi wa barabara. (Makofi)

Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba utekelezaji wa fedha hizi utakapokamilika tutaondokana na kero ya uharibifu wa barabara wa mara kwa mara ndani ya hifadhi kwa sababu tutakuwa na mitambo ambayo hii mitambo itakuwa inatengeneza hizi barabara mara kwa mara na wakati huo huo Royal Tour imeshatufungulia utalii, tunaamini utalii utakuwa juu na barabara zitakuwa zinatengenezwa kila wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna eneo lingine ambalo wameweza kuliongelea…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, muda wako umekwisha. Dakika moja malizia.

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, nilitaka tu niongelee kidogo kwenye eneo la REGROW kwamba, eneo la REGROW lime-cover hifadhi nne ya Ruaha, Mikumi, Nyerere National Park pamoja na Udzungwa, sio Mikumi tu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Mary Masanja, sasa kwa sababu umetaja hapo majina ya hifadhi na kumbukumbu zetu ili zikae sawa sawa hii inayoitwa Selous, hii inayoitwa Nyerere watu wamesema Selous humu ndani wewe umeita Nyerere sasa sema jambo hapo ili Wabunge wajue inaitwa nini sasa hivi.

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kabla ya Nyerere National Park kupandishwa hadhi kuwa national park lilikuwa ni pori la akiba ambalo lilikuwa linaitwa Selous. Baada ya Nyerere National Park kupandishwa hadhi lilimegwa pori la Selous likabaki sehemu kuwa pori la akiba na Nyerere National Park ikapandishwa kuwa Hifadhi ya Taifa, kwa hiyo tuna Game Reserve ya Selous na wakati huo huo tuna Nyerere National Park. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Kwanza kabisa nianze kwa kuunga mkono hoja, lakini pia nianze kwa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo ameendelea kuwa muumini mzuri hususan kwenye masuala mazima ya uhifadhi, lakini na utunzaji wa mazingira, lakini ni dhahiri kwamba uhai wetu kwa ujumla unategemea sana vyanzo vya maji, lakini pia viumbehai wakiwemo wanyamapori na mimea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, michango ya Wabunge imeelekeza zaidi katika Wizara ya Maliasili na Utalii, lakini pia na Wizara ya Ardhi. Sisi ni wadau wakubwa kabisa kwenye maeneo mengi yenye migogoro hususan maeneo ya hifadhi na tunatambua changamoto hizi zipo na ndiyo maana ilimpelekea Mheshimiwa Rais kuunda Kamati ya Mawaziri nane kwenda uwandani kuchunguza kina na kadhia wanayoipata wananchi hususan kwenye migogoro ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niendelee kuwapongeza Wabunge kwa namna ambavyo wameendelea kuwa wavumilivu. Nimejaribu kuongea hapa kwamba chimbuko la migogoro hii ni la muda mrefu. Tunakumbuka tangu Serikali ya Awamu ya Tano iliyokuwa inaongozwa na Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, kulikuwa kuna migogoro hii na aliweza kuunda Kamati ya Mawaziri nane wakaenda uwandani wakaanza kuchunguza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeenda uwandani kwa ajili ya kutekeleza na ninyi mtatambua mwaka jana tumezunguka Mawaziri, tumepita kila sehemu kuangalia hizi changamoto. Niwaombe tu Waheshimiwa Wabunge changamoto hizi ni za muda mrefu na utatuzi wake unahitaji sana busara, lakini na hekima lakini na tuvumiliane kwa sababu unapoenda unakuta mwenzio kaingia huku inahitaji busara sana kutatua changamoto hiyo na ndiyo maana Mheshimiwa Rais alielekeza kabisa kwamba hahitaji kuona taharuki inatokea katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tumeenda hatua kwa hatua na pale ambapo kuna kuwa kuna mabishano, Serikali inaangalia, kama kuna umuhimu sana wa kung’ang’ania hili eneo basi kuna maslahi mapana ya Taifa letu, lakini pale ambapo tunaona tunaweza kuachia, basi tunakaa tunazungumza na Mheshimiwa Rais ameweza kuachia takribani vijiji 975 vilivyokuwa vimesajiliwa ndani ya hifadhi vyote ameviachia. Tumpongeze sana na tuendelee kumtia moyo kwa sababu migogoro hii ni mingi, lakini tunaenda kuimaliza kabisa na Mheshimiwa Waziri wangu ameahidi kabisa kabla ya bajeti ya Maliasili tutakaa na Waheshimiwa Wabunge wote wenye migogoro tutajadiliana eneo kwa eneo ili tufikie mahali migogoro hii tuimalize maana lengo la Serikali ni tutembee pamoja na siyo tena kuendelea na migogoro hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipende tu kuzungumzia suala la Mbarali ambalo lilijitokeza jana na suala kubwa hapa ni kwamba mchakato mzima wa kuainisha hii mipaka tayari umeshakamilika isipokuwa tunachotarajia sasa hivi ni kuleta kwenye Bunge lako hili tukufu ili liweze kuridhia marekebisho ya Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha na kabla ya kuisha Bunge hili tayari azimio hili litaletwa katika Bunge lako hili tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tuwaondoe shaka Wanambarali, tuwaondoe shaka Wanambeya ambao wamekuwa wakishughulika na hizi shughuli za kilimo hususan katika maeneo ambayo yanazunguka Bonde la Usangu kwamba tutakamilisha na kila mtu ataelewa mipaka yake na wale ambao wameainishwa kwamba wataainishiwa mipaka yao basi wataweza kuiona kwa uharaka zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kumejitokeza kwenye suala hili la Nyatwali. Suala la Nyatwali malengo ya Serikali ilikuwa ni kupunguza migogoro ya wanyama wakali na waharibifu. Kama ambavyo umekuwa ukisikia, tumekuwa na changamoto kubwa sana ya wanyama wakali na waharibifu kwa hiyo, tunajaribu kuongoa zile shoroba ambazo tunaweza angalau tukaruhusu wanyama pia nao wakaweza kupita katika maeneo ambayo kusiwe na mgogoro kati ya jamii pamoja na wanyama wakali na tukitambua kwamba Serengeti ni hifadhi maarufu na imekuwa ya kwanza inaongoza kimataifa kwa maana ya uhifadhi bora na ni chanzo kikubwa cha mapato katika sekta ya utalii. Hivyo tunaendelea kuwaomba Wananyatwali kwamba Serikali imeendelea kusikia maombi yao, lakini tunashukuru kwa sababu wamekubali kwa hiari kwa maana tulienda kuzungumza nao na tukawaeleza kwa nini tunaenda kufanya hivyo. Lengo kubwa ni kuokoa maisha ya wananchi. Hakuna mtu anayefurahi kusikia kila siku kilio cha wananchi wanakufa kwa sababu ya wanyama wakali na waharibifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua muda wangu umeisha naunga mkono hoja, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Kufutwa kwa Hifadhi ya Taifa ya Kigosi ili Kuruhusu Kuanzishwa kwa Hifadhi ya Msitu wa Kigosi na Azimio la Bunge la Kuridhia Kurekebisha Mpaka wa Hifadhi ya Taifa ya Ruaha
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Nisiwe mchoyo wa fadhila, nianze kwa kumpongeza sana na kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa namna ambavyo amesimamia mazoezi haya ya migogoro, hatimaye leo tumeanza sasa harakati za kuleta maazimio ili turekebishe baadhi ya maeneo. Nampongeza kwa moyo wa dhati kwa sababu hata Wabunge wenyewe wamekiri leo kwamba safari ilikuwa ni ndefu, lakini hatimaye tunaanza kuiona nuru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikupongeze wewe umekuwa ukitusimamia vizuri sana, miongozo ni mingi sana iliyokuwa inatoka humu Bungeni ikihusiana na maeneo haya yenye migogoro, lakini umetusimamia vizuri sana. Tunakupongeza na tunakuahidi kwamba tutaendelea kushirikiana na Wabunge na wewe binafsi ili kuhakikisha kwamba tunaitendea haki Serikali lakini pia tunawatendea haki Watanzania wote.

Mheshimiwa Spika, naendelea kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, ameendelea kutusimamia kutuongoza pale ambapo tunakwama ametuonyesha njia. Tuendelee kumshukuru na awe na moyo huo huo pale ambapo tunamhitaji hasa kwenye harakati hizi za kutatua migogoro. Pia, niendelee kumshukuru sana bosi wangu Mheshimiwa Waziri Mchengerwa kwa namna ambavyo tunaendelea vizuri kuyaangalia haya maeneo, lakini pia kwa hatima ya zoezi hili la kupitisha haya Maazimio mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikumbuke tu na kumpongeza Mwenyekiti wa Kamati yetu, Makamu Mwenyekiti lakini na Waheshimiwa Wajumbe. Hawa wamekuwa nguzo, wametupa maelekezo mahususi, wametusimamia na hatimaye leo tumeingia Bungeni tukiwa kifua mbele tukitetea Maazimio hayo mawili. Nawapongeza sana Waheshimiwa Wabunge na tunakiri kwamba tutaendelea kushirikiana nao na yale maelekezo yote ambayo wametupa kwenye Kamati na hata yaliyotoka kwenye ripoti yao hapa tumeyapokea na tutaendelea kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wabunge wamechangia, tunawashukuru sana kwa michango yao mizuri na tunaendelea kuwaomba waendelee kutuelekeza ili tuendele kufanya kazi nzuri ili Watanzania wapate haki yao, lakini pia Serikali iendelee kuhifadhi na kulinda rasilimali za Taifa kwa maslahi ya Watanzania wote.

Mheshimiwa Spika, ningependa nitoe mchango wangu katika maeneo mawili, eneo la kwanza linahusiana na Azimio la Kushusha Hadhi Pori la Hifadhi ya Taifa Kigosi kuwa Forest Reserve. Kwenye Sekta yetu hii ya Maliasili na Utalii tumekuwa na mchakato mzima wa uanzishwaji wa viwanda vya uchakataji wa mazao ya misitu hususan mazao yanayotokana na nyuki. Tuna viwanda 97 nchini, lakini tuna viwanda sita katika Wilaya ya Mlele, Kibondo, Bukombe, Nzega, Sikonge na Manyoni. Hivi viwanda vipo kwa ajili ya kuchakata asali na viwanda hivi vipo kwa ajili ya kutegemea rasilimali inayotokana na mazao yanayotokana na nyuki.

Mheshimiwa Spika, niliwahi kutembelea Wilaya ya Bukombe, wazalishaji wakubwa wa zao la asali na ni moja ya wilaya hizi nilizozitaja. Changamoto tuliyoikuta pale ni kwamba tulikuwa tunawaondoa wale wananchi waliomo ndani ya hifadhi, kwa sababu hifadhi hii imepanda hadhi kuwa National Park. Nakumbbuka nilifanya ziara na tukaomba pamoja na kuwa nature ya reserve ile imeshazuia shughuli za kibinadamu lakini uzalishaji wa mazao ya nyuki ulikuwa ni wa hali ya juu. Kwa bahati nzuri kabisa Serikali imepeleka kiwanda pale na kiwanda kinazalisha vizuri na wananchi uchumi wao umeimarika, Watanzania wanapata ajira kutokana na mazao hayo. Kwa hiyo tuliweza kuwaruhusu hawa wananchi waendelee kurina asali na kufuga nyuki, lengo lake ni kuwafanya waendelee kuzalisha mazao hayo.

Mheshimiwa Spika, kushuka kwa hadhi ya mapori haya, kutasaidia sana wananchi kuimarika kiuchumi, kimapato, lakini pia tunaamini ajira za Watanzania zitaendelea kuongezeka. Eneo hili linazungukwa na mikoa minne, Mkoa wa Kagera, Mkoa wa Geita, Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Shinyanga. Kwa hiyo kushuka kwa hadhi kwa pori hili kutasaidia mikoa minne iende kufaidika na mazao ya uchakataji wa asali lakini yanayotokana pia na nyuki.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo hili lingine la Azimio la Ruaha pia niendelee kukushukuru, niwashakuru Wabunge kwa namna ambavyo wamelipokea vizuri. Kama ambavyo nimesema mwanzo, eneo hili limekuwa na mgogoro wa muda wa siku nyingi, lakini niwapongeze sana Kamati ya Mawaziri nane. Tumeenda mara kadhaa kule lakini hatimaye leo tumeleta azimio Bungeni. Kuna mawazo mbalimbali yametolewa na Waheshimiwa Wabunge ikiwemo kuendelea kuwashirikisha wananchi, lakini pia wametuomba sana mipaka iweze kuonekana kwa uwazi zaidi na iwe shirikishi kwa wananchi. Tunaahidi kwamba tutaendelea kuwashirikisha wananchi, lakini pia mipaka tutaweza kuiweka kwa ufasaha kabisa ili kila mtu aone na eneo hili liweze kuhifadhiwa vizuri.

Mheshimiwa Spika, tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo amekubali kupunguza eneo hili kuwaachia wananchi hususan wakulima na tunaendelea kuwaomba wananchi kwamba kila ambacho kinaombwa Mheshimiwa Rais anawasikiliza na anatekeleza. Kwa hiyo tuendelee kushirikiana pamoja na Serikali tuendelee kushirikiana pamoja na Mheshimiwa Rais na tuendelee kumuunga mkono ili migogoro hii ifikie hatma na hatimaye tuweze kuendeleza rasilimali hizi tulizoachiwa na waasisi wetu kwa maslahi mapana ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)