Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Kwagilwa Reuben Nhamanilo (27 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi hii. Nikipongeze Chama changu cha Mapinduzi kwa uwepo wangu hapa, kikiongozwa na Mwenyekiti wetu, Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli; lakini zaidi niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Handeni pamoja na familia yangu kwa kunifanya niwepo mahali hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yamezungumzwa mengi hapa kuhusu hotuba ya Mheshimiwa Rais. Hotuba yenyewe ilijielekeza kutoa uelekeo wa nchi yetu kwa miaka mitano ijayo, pamoja na yote ambayo Mheshimiwa Rais anayafikiria ni ya muhimu na ambayo yatatuvusha kama taifa kuelekea miaka mitano na pamoja na hoja zote ambazo Wabunge wamezichangia. Kimsingi ukiangalia ni kwamba mambo haya mwisho wa siku yanahitaji fedha; ili tuweze kuyafanya yanahitaji fedha.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi nataka nichangie ili kujaribu kuishauri Serikali ni namna gani kama nchi tutajidhatiti kuweza ku-raise hizi fedha ambazo zinahitajika kwa ajili ya kuyatekeleza mambo haya ya kutuvusha miaka mitano ijayo.

Mheshimiwa Spika, la kwanza ambalo nataka nilishauri kwa Serikali yangu, tutakumbuka mwaka 2019 Bunge lako lilipitisha Finance Act yenye maboresho ya kikodi mengi sana, na moja kati ya maboresho hayo ilikuwa ni kupendekezwa kuanzishwa kwa Ofisi ya Tax Ombudsman, jambo ambalo mpaka leo halijafanyika.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali yangu sikivu ianzishe ofisi hii muhimu ili kuendana na hotuba ya Mheshimiwa Rais ukurasa wa 12 ambapo ameelekeza kwamba lazima tuwe tunafanya business disputes, njia pekee ya kufikia hapo ni kuanzisha ofisi hiyo muhimu ya Tax Ombudsman.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo nataka nilishauri ni structure yetu ya chombo chetu muhimu cha TRA. Yote tunayotategemea yanategemea makusanyo ya ndani yanayofanywa na ofisi hii ya TRA. Ninachoishauri Serikali yangu ni kwamba TRA isiogope kuajiri vijana kwa sababu waajiriwa wa TRA siyo sawa na waajiriwa wengine wa pande nyingine za idara za Serikali, hawa unaajiri watu ambao wanakwenda kuzalisha moja kwa moja, wanatusaidia kukusanya kodi. Haiwezekani eneo la kimkakati kikodi kama ilivyo Ilala unakuwa bado una ofisi zenye watumishi wasiotosha, tunajichelewesha wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo nataka nilishauri ni habari ya informal sector. Informal sector inafanya biashara kubwa sana lakini haiwi captured kwenye mifumo ya kikodi. Hili ninapendekeza ufanyike utafiti mzuri na wa kutosha ili watu wetu wa TRA waweze kutoza kodi sehemu zote zinazozalisha ambazo ziko kwenye informal sector. Tusipojaribu kuli-balance hili litakuja kutuingiza matatizoni kwa sababu formal sector inayolipa kodi itakuja nayo kugeuka kuwa informal sector, ni lazima tufanye utafiti na tujaribu kuya- balance haya mawili.

Mheshimiwa Spika, pamoja na makusanyo mazuri yanayofanywa na TRA, ninashauri tusiwe tunapima ufanisi wa TRA kwa kuangalia increment ya makusanyo yao, kwamba mwaka jana walikusanya hapa, mwaka huu wameongeza kiwango hiki, hicho si kipimo peke yake cha kuonesha ufanisi wa taasisi hii muhimu kwetu.

Mheshimiwa Spika, naomba TRA na Serikali yetu kupitia Wizara ya Fedha wawe wanaangalia ratio kati ya taxes zinazokusanywa kwa uwiano na GDP ya kwetu. Tusipofanya hivyo hatari yake ni kwamba tutakuwa tuna- impose tax burden kwa walipakodi wachache kwa sababu increment hiyo unaweza ukakuta ni kwa sababu ya vertical raise kwa kuongeza tu makadirio ya kodi kwa wafanyabiashara walewale waliopo badala ya kui-spread ile kodi kwa uchumi wote.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka nilishauri ni habari ya mamlaka za Kiserikali. Mamlaka zetu za Serikali zinakuwa supplied na wafanyabiashara, sasa wafanyabiashara wanapokuwa wame-supply Serikalini ukichelewa kuwalipa maana yake unajichelewesha mwenyewe kuchukua kodi yako. Ni bora hata ukafanyika utaratibu kama fedha ya kuwalipa inakuwa haijapatikana, ile component ambayo ina kodi ndani ilipwe kwanza halafu ndiyo waendelee na procedures nyingine. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Reuben Kwagilwa.

MHE KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi hii. Moja kwa moja nijielekeze kwenye kuchangia lakini sababu dakika tano ni chache sitaingia ndani sana ila nataka nitoe ushauri mmoja kabla sijatoa maelezo yangu ya jumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ambao nataka nitoe, kuna suala hapa limezungumzwa sana nalo ni la maji. Sera ya Taifa ya Maji ya mwaka 2002 pamoja na Sheria ya Maji Na. 5 ya mwaka 2019, Sheria hii ya Maji ya mwaka 2019 ndiyo ilianzisha RUWASA lakini kana kwamba haitoshi ikaenda mbele ikaleta Mfuko wa Maji wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alipokuwa anazunguka kufanya kampeni kwenye hotuba yake amekiri, namnukuu anasema: “Hata hivyo, napenda nikiri nilipokuwa kwenye kampeni moja ya changamoto kubwa niliyoelezwa na wananchi ilikuwa ni shida ya maji hususan maeneo ya vijijini”. Kwa sababu Mheshimiwa Rais ameshaliona hili, nashauri Serikali iirejeshe hapa ile Sheria ya Maji, Na. 5 iliyotungwa na Bunge letu ya mwaka 2019 ili tuirekebishe kidogo. Marekebisho yake yaweje? Tumeweka pale source ya fedha za huu Mfuko; tumesema tutatoza shilingi 50 kwenye petrol na shilingi 50 kwenye diesel. Nachoomba ili tuweze kuisaidia RUWASA lazima sheria ije hapa tuitengeneze iweze ku-state ni asilimia ngapi iende kwenye maji katika hiyo shilingi 100 inayotozwa kwenye petrol and diesel. Kwa sababu tukiiacha hivi miradi ya mjini inatumia fedha nyingi kuliko miradi iliyopo vijijini. Kwa hiyo, kuna haja ya kufanya hayo marekebisho ya hiyo sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la jumla sana mimi nataka tu niseme kwamba ndugu zangu unapopanga la kwanza unatumia takwimu na pili unatumia assumptions. Kwenye hili eneo la takwimu tusipojizatiti vizuri kuboresha namna ya upatikanaji wa takwimu kwenye nchi yetu kila tunapopanga tutakuwa tunajikuta tuko nje ya malengo. Kwa hiyo, ni vema tuboreshe sana eneo hili la takwimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye huu Mpango ambao ndiyo mpango wa mwisho kuelekea Vision yetu ya 2025 kama Taifa kukamilika wakati nimekuwa nikiusoma mara kwa mara na kuurejea sijaona mahali ambapo Mpango huu umeweka provision kwamba baada ya Vision 2025 kukamilika inayotekelezwa mwishoni kwenye huu Mpango ni kitu gani kitafuata? Vision nyingine itakapotengenezwa, sijaona provision kwenye Mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine tunapopanga ni vema tukajua financing mode ya hii miradi tunayoipanga especially hii miradi ambayo tunaita flagship projects. Ukifanya tathmini vizuri kwenye Mpango uliopita utagundua tulikuwa na miradi karibia 20 na yote ni mikubwa. Miradi 20 yote hii hatuwezi kui-finance na kodi za wananchi za kwetu za ndani. Kwa hiyo, ni vema tujikite kama taifa na ni wakati muafaka sasa tukubali tu kwamba ili tuitengeneze hii miradi ni lazima tutafute sources nyingine, namna nyingine ya kuitekeleza ama kwa partnership au kwa kukopa lakini tuifanye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huohuo lazima twende na tahadhari, tumejaribu kufanya partnership pale Liganga na Mchuchuma na mradi huu umezungumzwa sana tokea tuko shule na bado mpaka leo haujatekelezeka. Naishauri Serikali yangu sikivu kama hili la Liganga na Mchuchuma limeshindikana kwa mwekezaji huyo tuliyenaye, ni vyema tukaenda mbele tukatafuta mtu mwingine kwa sababu dunia kwa sasa ni chuma na mafuta. Ni bidhaa mbili tu zinazotawala soko la dunia za mafuta na chuma. Kwa hiyo, tunapochukua muda mrefu miaka 7 toka 2014 tunafanya mazungumzo tunajichelewesha tu wenyewe. Tunahitaji tu- mobilize fedha kutokana na hii miradi ya kimkakati ambayo tunayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, mimi ya kwangu yalikuwa hayo machache. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa fursa hii ili niweze kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupanga ni taaluma, lakini kwa Taifa letu na kwa Serikali yetu kupanga si tatizo. Mpango huu tulionao ni mzuri sana kuliko mipango mingi sana ya nchi nyingi hapa Afrika, lakini shida tulionao sisi kwenye kupanga ni kutekeleza Mpango tuliouweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi sitaongelea mengi isipokuwa nataka nijielekeze eneo moja tu, la Mradi Mkubwa tulionao wa Standard Gauge Railway, tunayoijenga. Standard Gauge Railway tunayoijenga ukijumlisha tu zile njia kilometa zinazojengwa tunatakiwa tujenge kilometa 4,886, hapo naongelea njia tu, siongelei mahala ambapo reli zinapishana. Mpaka sasa tumeshajenga kipande cha Dar es Salaam kuja Morogoro kilometa 300 na tunaendelea na kipande cha Morogoro – Makutupora kilometa 422, lakini vilevile tuko upande ule mwingine wa Isaka na Mwanza kilometa 249.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa aina ya financing ya mradi huu tunavyoindesha tukiendelea nayo tutaujenga Mradi huu wa Standard Gauge kwa nchi nzima kwa miaka 81, miaka 81. Ikiwa miaka mitano tumejenga kilometa 300 ndio ambazo ziko above 90 then kilometa 4,886 tutazijenga kwa miaka 81. Hii katika nchi ambayo inapambana kutafuta maendeleo ni kitu hakikubaliki, ni kitu hakikubaliki. Hivyo vipande nilivyo vitaja ambavyo vinajengwa vimetugharimu takriban trilioni 11. Trilioni 11 ni Idle Investment kwa sababu gani, kwa sababu hatutakamilisha leo ili tuanze kutumia mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachokishauri Serikali yetu iondekane na habari ya Traditional Methods za ku-finance miradi hii mikubwa. Kwanza tunajipa pressure kama Serikali, ya ku-finance mradi huu halafu tunashindwa kupeleka huduma kwa wananchi ambazo ni za kila siku. Kwa hiyo ninachokishauri Wizara ya Fedha waangalie utaratibu wa ku- finance mradi huu Infrastructure Bond. Wamefanya hivyo nchi za wenzetu, ukienda Benin wamefanya, ukienda Tunisia wamefanya. Hii inatupa ahueni ya kutekeleza mradi huu na kuutekeleza kwa wakati. Tunapoendelea kutekeleza mradi huu hivi kidogo kidogo ni hasara kwa Taifa letu, ni vile tu hatui- merge hii hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa faida ya wasiofahamu na Watanzania kwa ujumla, tunatakiwa tuitoe reli itoke Dar es Salaam iende mpaka Tabora kwa kupitia Singida, ikifika Tabora iende Isaka Shinyanga mpaka Mwanza, ikitoka Tabora iende Keeza ili tukahudumie Kigali na Burundi, ikitoka hapo Tabora tuipeleke Kaliua kwa ndugu yangu hapa, iende Uvinza mpaka Kigoma tukaihudumie Kongo na tukitoka Kaliua tuje Mpanda mpaka Katema; hiyo ni Reli ya Kati tunayojenga. Bado kuna kipande cha Tanga, Musoma, Arusha kilometa takriban 1,233; na hapo hapo bado kuna kipande cha Mtwara – Mbambabei kilometa 10,092.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ni kitu serious sana, hatuwezi tu kuendesha mradi huu kwa kutumia mapato ya ndani tutawaumiza Watanzania na tunajichelewesha wenyewe kupeleka maendeleo ambayo yanahusu huduma za moja kwa moja za wananchi za kila siku kama vile elimu na afya; na ndio maana kwa mwenendo huu wananchi wa Handeni mpaka sasa hatuja pata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa mradi huu kwa pamoja kutatusaidia sana kama Taifa kwanza kuifungua Bandari yetu ili iongeze mzigo unaopita pale. Kwa sasa hivi tunapitisha tani milioni 17 ukilinganisha na wenzetu wakenya wanapitisha pale Mombasa tani milioni 37. Kukamilika kwa pamoja na kwa wakati mmoja kutatusaidia sana kupata mapato kupitia mradi huu, kwa maana TRA wataweza kukusanya lakini vilevile wananchi wetu uchumi wao unataweza kuwa activated.

Mheshimiwa Naibu Spika, jinsi tunavyojenga kwa vipande vipande hivi na kuchukua muda mrefu kuna maeneo ya nchi yetu yatabaki kuwa-disadvantaged. Kwa mfano kipande hiki cha Mbambabei – Mtwara kitabaki kuwa ni historia tu ikiwa hatutatekeleza mradi wa Liganga na Mchuchuma, viability ya hii reli hapa haipo. Vivyo hivyo kipande kile cha kutoka Tanga kwenda Arusha kwenda Musoma kama hatukuimarisha vile vipaumbele tulivyoweka ukanda ule ikiwemo soda ash pale Lake Natron hakuna viability ya mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lipo bomba linalotoka Uganda Hoima kuja Chongoleani Tanga. Kwa vyovyote vile mafuta yatakapofika Tanga yatahitaji reli hii hii kuyarudisha yakisha kuwa refind. Kwa hiyo Serikali ione umuhimu wa kwenda kukopa kwa kutumia Infrastructure Bond ili tutekeleze mradi huu kwa pamoja kwa mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo na baada ya kushauri hilo ni malizie kwa kusema; limezungumzwa hapa asubuhi kidogo lakini halikukaziwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo Sheria ya Bajeti ya mwaka 2015 ambayo inatu-guide kuanzia mwanzo tunapotengeneza bajeti mpaka tunapoitisha bajeti hapa Bungeni, lakini sheria tukishapitisha bajeti hapa wenzetu wa Serikali wanapokwenda kutekeleza bejeti hakuna Sheria ya Monitoring na Evaluation. Kwa maana hiyo tunamuomba hapa Waziri wa Sera Serikali yetu hapa walete Sera. Kwanza wao watunge Sera ya Monitoring na Evaluation ili wailete hapa tuitungie sheria. Ndiyo maana ripoti hii ya CAG ambayo tunakwenda kuijadili ni aibu ni aibu ni aibu ni aibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tusipofika mahala tukatunga sheria hiyo; huwezi; kwa mfano mradi wa bilioni 380 unaotekelezwa, wa maji kule Handeni, unaojengwa kutoa Maji Korogwe kuyaleta Handeni eti ukasimamiwe na Mtendaji wa Kata, usimamiwe na Diwani. Lazima tutunge sheria ikae vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono mpango uliopo mezani, naomba kuwasilisha. Ahsante sana. (Makofi).
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii ili na mimi niweze kuchangia Mapendekezo ya Mpango 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 08 Aprili, 2021 Waziri wa Fedha aliwasilisha hapa Mpango mkubwa wa nchi wa Miaka Mitano. Mpango huu wa miaka mitano ndio ambao umesababisha leo tunajadili mpango wa mwaka mmoja mmoja; na mpaka sasa tumekwisha jadili mipango miwili na sasa tuko kwenye mapendekezo ya mpango huu wa tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mpango ule mkubwa wa miaka mitano ambao ulikuwa wa 2021/2022- 2025/2026 uliandaliwa kwa kutumia rejea ya vitabu kadhaa, nitavitaja harakaharaka; Dira ya Taifa ya Maendeleo, Ilani ya Uchaguzi ya CCM, hii niliyoishika na watu waione, kitabu makini kabisa; Mpango Elekezi wa Muda Mrefu, matokeo ya tathmini, sera na mikakati mbalimbali ya kisekta, Dira ya Afrika Mashariki 2050, Dira ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika, Agenda 2063 ya Maendeleo ya Afrika pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu 2030.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hivi vitabu vyote nilivyovitaja hiki kimoja ndicho ambacho tulikwenda nacho kwa wananchi, ndicho ambacho tulikinadi, ndicho ambacho wananchi waliamua kwamba watakichagua hiki na wakaichagua Serikali ya CCM ili iweze kuleta maendeleo. Kwa hiyo mipango yote tunayoipanga lazima ilete tafsiri ya hiki kitabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye huu mpango mkubwa kulikuwa na shabaha za mpango ambazo ziko tano. Na mimi leo nataka tuzipitie vizuri tukirejea mapendekezo haya ya mpango yaliyopo mbele yetu tuone kama yanaleta tafsiri ya hiki ambacho kipo kwenye mpango wetu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shabaha ya kwanza ya mpango ule mkubwa wa miaka mitano inasema, “ukuaji wa uchumi kuongezeka kutoka asilimia sita mwaka 2021 hadi kufikia 58% mwaka 2026.” Ilani yetu ya Uchaguzi ukurasa wa 13 (b)(1) inasema, “kuweka sera madhubuti za uchumi jumla ili kukuza uchumi kwa wastani usiopungua asilimia nane kwa mwaka.” Hiki ndicho ambacho tumewaahidi Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyongea kwa Januari mpaka Machi, 2022, uchumi wetu umeripotiwa kukua kwa asilimia 5.4. Hii ndiyo kusema tuko chini na nje ya mpango wetu ambao tumeuweka sisi wenyewe. Kwa hiyo, Serikali wanayo kazi ya kwenda kufanya kuhakikisha kwamba kitabu hiki wanakitafsiri na wanakitekeleza kwa namna ambavyo kinaelekeza. Kinataka ukuaji wa uchumi kwa asilimia nane, lakini Serikali imeripoti ukuaji wa uchumi wa asilimia 5.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shabaha ya pili ilikuwa ni mapato ya ndani ukijumuisha mapato ya halmashauri kuongezeka kutoka asilimia 15 ya pato la Taifa hadi kufikia asilimia 16. Hivi tunavyozungumza ukisoma haya mapendekezo ya mpango yaliyoletwa mbele yetu, sura ya 3 (3), (2)(i) inasema, mapato ya kodi; kwenye mpango wanatarajia yafikie asilimia 12 ya pato la Taifa. Yaani mpango huu wa mwaka mmoja uko nje kabisa ya mpango mkubwa ambao ndiyo tumekubaliana kuufanya. Wao wanaongelea mapato ya kodi kufikia asilimia 12 ya pato la Taifa ilhali mpango mkubwa unataka tufikie kuanzia asilima 15.9 mpaka 16.8.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuwa na mipango ya hivi. Mipango hii midogo ya mwaka mmoja mmoja inatakiwa itafsiri mpango ule mkubwa tuliojiwekea na ambao tumeupeleka kwa wananchi kuunadi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shabaha ya tatu ya ule mpango mkubwa inasema, “mfumuko wa bei kuendelea kuwa wa tarakimu moja, wastani wa 3% mpaka 5%.” Naipongeza Serikali kidogo hapa kwa sababu wamejitahidi sana kuweka mfumuko wa bei kwenye single digit. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikilizeni niwaambie jambo muhimu unapoongelea mfumuko wa bei na hasa kwa Watanzania. Jambo la muhimu kabisa tunapoongelea mfumuko wa bei kwa Watanzania wa kawaida na wananchi walio wengi tunaongelea mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi. Hicho ndicho kinachogusa Watanzania. Taarifa hii ya mpango mpaka kufikia Agosti, 2022, mfumuko wa bei za vyakula na vinywaji baridi uko asilimia 7.8; it is above 3% to 5%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ya mfumuko wa bei ya chakula, nitumie hii nafasi niiombe sana Serikali, kama kuna vyakula kwenye maghala sasa hivi, waruhusu viende kwa wananchi. Hali ni mbaya sana. Hivi sasa Handeni Mjini… (Makofi)

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nimefurahishwa sana na mchango wa kaka yangu, Mheshimiwa Mbunge ninayemheshimu sana, lakini napenda kumpa taarifa kwamba analolizungumza, tayari Serikali ya CCM wameshaliona. Leo ninavyozungumza, Ikungi tumepokea Tani 100 za mahindi kuwauzia wananchi kwa bei ambayo itapunguza tension. Kwa hiyo, kwa kweli Serikali na Wizara ya Kilimo tunaIshukuru sana. Naomba nimpe taarifa hiyo. Sasa itakuwa ni vyema na kule kwake wapeleke. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Reuben.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawazungumzia wananchi wa Handeni ambao mpaka leo asubuhi wamenunua kilo ya sembe kwa shilingi 2000. Sasa kama Mheshimiwa Mbunge, mahindi yamefika kwake Ikungi, hilo ni jambo la kuishukuru Serikali ya CCM. Ninachosema hapa ni kwamba Mpango huu uwe wa Kitaifa na siyo wa Ikungi peke yake. Kwa hiyo, ni muhimu sana tukazingatia kilichopo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo, hili la chakula narudia tena, naomba Serikali kama ina chakula kwenye maghala, i- offload ili mahindi yawafikie wananchi kwa bei ambayo itakuwa ni elekezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shabaha namba nne ambayo mpango mkubwa umeuweka inasema, akiba ya fedha za kigeni kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa. Hili nalo naipongeza Serikali. Mpaka sasa wamejitahidi sana ku-mantain akiba ya fedha za Kigeni around 5.1 billion US Dollars ambazo zina uwezo wa kuagiza vitu kutoka nje monthly kwa asilimia 4.6. Kwa hiyo, hili nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kwenye ule mpango mkubwa, ni sekta binafsi kuzalisha ajira zipatazo 8,000,000, ndicho tulichokubaliana na ndicho ambacho tumekipeleka kwa wananchi. Ukifungua Ilani ya Uchaguzi ukurasa wa nane kipengele cha f(1) hadi (4) inasema, “kutengeneza ajira zisizopungua 8,000,000 katika sekta rasmi na isiyo rasmi kwa ajili ya vijana.” Wamesema, hayo yanaweza yakafikiwa endapo tutawekeza kwenye kilimo, mifugo, uvuvi, madini, maliasili, sekta za huduma na utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ajira 8,000,000, mwaka wa kwanza wa mpango umepita, na mwaka wa pili wa mpango umepita. Tafsiri yake ni nini? Ni kwamba mpaka sasa Serikali ilitakiwa iwe imezalisha ajira milioni 3,200,000. Namtaka Waziri mwenye dhamana ya huu mpango atakaposimama hapa atuambie wamezalisha ajira ngapi? Kwa sababu kama ni 8,000,000, maana yake kila mwaka ni 1,600,000. Kwa hiyo, kwa miaka miwili ambayo tayari tumeshaimaliza, ilitakiwa tuwe tumeshatengeneza ajira 3,200,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili nisiishie tu kukosoa, niwashauri pia kwamba hatuwezi kuzalisha hizi ajira ikiwa hatukufanya uwekezaji. Siongelei ule uwekezaji ambao ninyi mna mtazamo nao Serikalini; siongelei ule uwekezaji wa mtu anatoka nje na fedha anakuja kufanya jambo hapa. Naongelea uwekezaji wa kuwawezesha Watanzania kuzalisha. Tunaongelea habari ya kilimo, tunataka Serikali yetu iwawezeshe Watanzania kwenye kilimo, tuwe na millionaires na billionaires kwenye kilimo ambao ni Watanzania. Ukiongelea mifugo, tunataka tumwone tajiri mmoja Mtanzania ambaye Serikali hii imemtengeneza. Tunataka tumwone mvuvi mmoja, vivyo hivyo na kwenye madini. Kwa hiyo, lazima tuwe na uwekezaji ambao ni very strategic. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikilizeni niwaambie; ukanda wote huu wa Bahari kuanzia Dar es Salaam, shuka Tanga nyumbani pale, mpaka Mtwara na Lindi, ni aibu kwamba hatuna hata kiwanda kimoja kikubwa cha ku-process Samaki. Ni aibu! Sasa tunaongelea uchumi gani kama hilo hatuwezi kufanya? Uwekezaji ninaousema ni ule unaojikita kwenye big production chains. Mfano mzuri, tazama Kiwanda cha Cement kilivyo pale, uone chain ambayo iko involved kwenye kiwanda. Vivyo hivyo ndiyo itakuwa kwenye Kiwanda cha Samaki na maeneo mengine. Kwa hiyo, tujikite kwenye maeneo hayo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nimepitia vyema taarifa ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji kuhusu Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2024/2025. Vilevile nimepitia vyema Taarifa iliyosomwa na Waziri wa Fedha, Taarifa ya Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali 2024/2025; na vilevile nimeshiriki katika maandalizi ya Taarifa yetu ya Kamati ambayo imewasilishwa na Makamu Mwenyekiti kwa niaba ya Mwenyekiti wetu, na nimemsikiliza vyema pia alipokuwa anaisoma hapa mbele ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri sana tunapojadili mapendekezo ya mpango, tukaifahamu historia kidogo ya chombo ambacho kimekuwa kikipanga mipango toka tumepata uhuru. Ni muhimu kujua historia hii kwa sababu lipo jambo ambalo mimi nafikiri na ninaamini hatulifanyi kwa usahihi, tunalikosea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1961 mpaka 1964 mipango yetu imekuwa ikipangwa na Tume ya Maendeleo ya Uchumi, tukaona haifai, tukabadilisha. Mwaka 1965, mwaka mmoja tu mipango yetu tukaipeleka Ofisi ya Rais, Idara ya Mipango na Maendeleo; tukaona haifai tukahama. Mwaka 1965 mpaka 1975, miaka 10 hapo tukakaa, mipango yetu ikawa inapangwa na Wizara ya Uchumi na Mipango ya Maendeleo; tukaona haifai tukahama. Mwaka 1975 mpaka 1980, miaka mitano mipango yetu ikawa inapangwa na Wizara ya Fedha, Uchumi na Mipango; tukaona haifai, tukahama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, 1980 mpaka 1985, 1985 mpaka 1989 tukarudi kwenye Wizara ya Fedha, Mipango na Uchumi, tukaona haifai tukahama. Mwaka 1989 mpaka 2000 mipango yetu ikawa inapangwa na Tume ya Mipango, tukaona haifai tukahama tena. Mwaka 2000 mpaka 2005 tukaenda Ofisi ya Rais, Mipango na Ubinafsishaji, haikutosha, tukaona haifai tukahama. Mwaka 2008 mpaka 2016 mipango yetu ikawa inapangwa na Ofisi ya Rais, Tume ya Mipango, tukaona haifai, tukahama. Mwaka 2016 mpaka 2023 mipango yetu ikawa inapangwa na Wizara ya Fedha na Mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwa historia hiyo ya kuonesha namna ambavyo Taifa limehangaika kupata wapi mipango ipangwe, nani asimamie mipango; nimesimama hapa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. Maeneo yote haya ambayo nimeyataja na kuhamishwa kwa Idara hii ya Mipango imekuwa ikifanyika tu kwa Presidential Decree. Rais anakuja anatoa tamko, mipango ihamie sehemu fulani kama ambavyo nimeonesha. (Makofi)

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kakunda, taarifa.

TAARIFA

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpe taarifa mzungumzaji kwamba confusion kubwa ilitokea mwaka 2001 wakati ambapo Idara ya Kuondoa Umaskini ilipelekwa katika Ofisi ya Makamu wa Rais nayo ikawa inapanga mipango. Hiyo ni taarifa. (Kicheko/Makofi)

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo, na pana story ndefu sana kwenye hili ambalo amelisema Mheshimiwa Kakunda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimempongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa sababu mwaka 2023 amerejesha Tume ya Mipango chini ya Ofisi ya Rais na siyo tu by Presidential Decree, ameirejesha kwa sheria. Kwa hiyo, hivi sasa tunayo Sheria ya Bunge tuliyoitunga hapa juzi ya kuanzishwa Tume ya Mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya pili ya sheria ile inasema, Tume ya Mipango, Kuanzishwa kwa Tume; kipengele cha 4(1) na (2) kinasema; “inaanzishwa Tume itakayojulikana kama Tume ya Mipango. Tume itakuwa Idara itakayojitegemea chini ya Ofisi ya Rais.” Sasa nimepongeza hatua hii ya kurejeshwa Tume ya Mipango na kutungiwa sheria ya uwepo wake, lakini kuna jambo moja ambalo nataka nilishauri na Serikali mlichukue. Hili litatusaidia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, usipokuwa na chombo imara cha kupanga mipango, definitely huwezi ukaisimamia mipango hiyo. Huwezi kuifanyia tathmini mipango hiyo. Kwenye hili siyo, tu kwamba nashauri kama Mbunge wa Handeni Mjini, lakini nashauri kama mtu aliyesoma Mipango. Hapa tuliposema tume itakuwa Idara itakayojitegemea chini ya Ofisi ya Rais, natamani sana Serikali na Bunge tukafanya marekebisho. Tume hii ili tuwe na mipango mizuri na tuweze kuisimamia, twendeni tukaifanye kuwa taasisi (an institution). Ikiwa ni taasisi itatusaidia mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, itatusaidia kuandaa wataalamu watakaopata uzoefu wa muda mrefu, lakini kutakuwa na urahisi wa kufanya transitions kutoka kizazi na kizazi, pia kutakuwa na mwendelezo hata wa mipango yenyewe kwa sababu ni taasisi. Hivi sasa kwenye hii Tume ambayo ipo chini ya Mheshimiwa Prof. Kitila kwenye Wizara yake, hii Tume inayojitegemea, ukiuliza leo wafanyakazi wa Tume hii, atakwambia anaokotaokota kutoka idara nyingine za Serikali. Haipaswi kuwa hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, angalieni maeneo ambayo tumetumia taasisi kufanya jambo na mwone ambavyo tumefanikiwa. Angalia leo TRA kama taasisi, angalia leo NBS kama taasisi. Ni muhimu Tume hii ya Mipango ikawa ni taasisi wala siyo Idara chini ya Ofisi ya Rais. Ikiwa taasisi, hatuiondoi pale kwa Rais. Inakuwa ni taasisi inayojitegemea ambayo iko chini ya Rais kwa sababu mipango ni instrument ya Rais katika kuleta maendeleo kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitawapeni mfano wa wenzetu ambao wamefanikiwa sana. Mfano nchi ya India, Mheshimiwa Rais alikwenda kule na bahati nzuri niliona Mheshimiwa Prof. Kitila aliambatana na Mheshimiwa Rais kule. Nina imani kwamba yapo ambayo mmejifunza. Pale India wana Tume ya Mipango (Planning Commissioner) ambaye leo hivi nilivyosimama imetimiza miaka 73. Ipo toka mwaka 1950 ipo pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi miaka yote 62 ambayo nimeitaja kwenye ule mlolongo toka mwaka 1961 mpaka leo tunatangatanga wapi pa kuiweka Tume ya Mipango, halafu wakati mwingine inakuwepo, wakati mwingine haipo. Sasa unaandaa vision ya miaka zaidi ya 20 halafu msimamizi ndani ya miaka mitano amefutwa! Unaandaa Mpango wa miaka mitano mitano ili kutekeleza vision ndefu ya miaka mingi, halafu Tume ya Mipango haipo, imefutwa. Definitely mpango wako huwezi kuusimamia. Ninatoa mifano michache hapa kuonesha namna gani tumeshindwa kuusimamia mpango kwa sababu ya structure yenyewe ya wapi chombo cha mipango kikae. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna madini. Ameongea Mheshimiwa Mzee Njeza, tuna madini tusiyoweza kuyachimba miaka 62. Hii ni mifano michache sana natoa ili tuone kwamba tusipokuwa na chombo madhubuti, taasisi ya kusimamia na kuandaa mipango tutakuwa tuna-miss target na indicators nyingi ambazo tunakuwa tumejiwekea wenyewe. Tuna madini tusiyoweza kuyachimba, tuna samaki tusioweza kuwavua. Kwenye hili nimpongeze Mheshimiwa Rais. Just imagine kwa mara ya kwanza ndiyo Serikali imenunua vyombo vya uvuvi na kuvigawa nchi nzima. Yaani Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anafanya kana kwamba tumetoka msituni au tumepata uhuru leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, aliongea Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwenye ziara ya Mheshimiwa Rais kule Singida, hata yale yanayofanyika kwenye Afya, yote yanafanyika kana kwamba tumetoka msituni na tumepta uhuru leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vifaa ambavyo Mheshimiwa Rais anapeleka, zahanati na vituo vya afya vinavyojengwa, lakini vyote hivi tungekuwa na Tume ya Mipango ambayo ni taasisi tungekuwa tumeshajenga uwezo wa kusimamia na kuyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, angalieni mambo ambayo tume-miss target. Tuna hekta milioni 29.4 ambazo zinafaa kwa umwagiliaji, lakini muulize Waziri wa Kilimo tumeweza kumwagilia ngapi kwenye hizo hekta milioni 29? Tumeweza kumwagilia hekta 822,000. Tuna-miss target kwa sababu ya kukosa mipango mizuri na taasisi ya kusimamia mipango hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna vivutio vya utalii vingi sana, na tumshukuru Mheshimiwa Rais kwa ile Royal Tour ambayo imetusaidia kuongeza watalii, lakini angalia; tuna vivutio vya utalii vingi sana ambavyo malengo yetu tulitaka tufikie watalii milioni tano na tupate fedha za kigeni six billion USD na tutengeneze ajira 1,750,000. Fanya tathmini leo, tuko mbali mno ya malengo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa mwisho, tuna Gridi ya Taifa ambayo haijakamilisha urefu wa 9,351 kilometa na tuna uzalishaji wa umeme ambao haujafika megawati 4,915. Tusipokuwa na taasisi na tusipoifanya Tume hii kuwa taasisi tutaendelea kuya-miss malengo na tutashindwa kuyasimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo ningependa kwenye mpango huu lijitokeze ukiacha huu ushauri wa kuifanya Tume kuwa taasisi huru, taasisi inayojitegemea, taasisi inayoripoti kwa Mheshimiwa Rais, taasisi ambayo ni instrument ya Mheshimiwa Rais, jambo lingine kwenye mpango huu ambao tulitaraji kuliona lakini halija-surface ni tathmini ya mpango wenyewe. Tunafunga vision 2025 na ni miaka miwili tu baadaye, ni mwaka mmoja baada ya mpango huu kupita mwezi wa tatu, lakini hatujapata kufanya tathmini ya ule mpango. Kwa kweli siyo tu tathmini ya miaka mitano hii ya mwisho, tunataka tuone tathmini ya jumla ya miaka yote hii ambayo tumei-practice vision 2025. Hii tathmini inatakiwa ifanyike mapema ili ituwezeshe kuandaa vision nyingine ya mbele. (Makofi)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

TAARIFA

MWENYEKITI: Mheshimiwa Taarifa.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka tu nimpe taarifa mzungumzaji kwamba tunashindwa kufanya tathmini hiyo Mheshimiwa Kwagilwa kwa sababu hatuna taasisi inayojitegemea. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa taarifa hiyo unaipokea?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hii. Unajua ukiwa unaongea hapa Bungeni, unamuambukiza mwenzako umeme hapa. Kwa hiyo, ameelewa kabisa nilichokuwa nakisema kwamba ni muhimu tukawa na taasisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukosekana kwa taasisi kumefanya hata mpango wetu tukiuandaa, Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, Ilani ya chama changu mimi ndiyo imekuwa kiongozi wa mipango ya nchi hii. Ndiyo Ilani ya Chama, wakati kumbe it was supposed to be the opposite. Inatakiwa Ilani zote za vyama zi-refer kwenye mpango, yaani chama A kituambie tu wanafanyaje kufikia mpango wetu wa Taifa kuukamilisha, chama B watuambie hivyo. Hata ukisoma mpango leo watakwambia rejea yao walitumia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Vyama vingine ndiyo kabisa hata rejea hazipo, maana ni vyama hata Ilani havina. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo, nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Ununuzi wa Umma wa Mwaka 2023.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nipate kuchangia Sheria ya Ununuzi ya Umma ya mwaka 2023. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa dhamira na nia ya dhati ya kuhakikisha fedha za Watanzania zinapokwenda kwenye manunuzi zinatumika kwa usahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sheria hii ya Ununuzi, Bunge lako limeipigia kelele kwa miaka mingi sana. Sheria hii ya Ununuzi, ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa hesabu ya Serikali, imekuwa ikitoa msisitizo jinsi ambavyo ilivyo na madhaifu. Hakuwepo mtu miaka yote wa kusikiliza na kulibeba jambo hili kwa udhati kama ambavyo Mheshimiwa Rais, amefanya sasa. Kkwa hiyo ni vyema Watanzania wakafahamu aina ya Rais tuliyenaye na dhamira aliyonayo kwa maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye maeneo haya 12 ya sheria hii tunayoiandika upya, nitachangia maeneo mawili, eneo la pili na eneo la saba. Eneo la pili linaweka Idara ya Sera ya Ununuzi wa Umma. Amezungumza Mheshimiwa Kimei, kutangulia kusema kwamba tunaanzisha idara hii lakini bahati mbaya iliyopo ni kwamba hatuna Sera ya Taifa ya Ununuzi wa Umma. Kwa sababu ya umuhimu wenyewe wa jambo lenyewe, ndiyo maana tumefikia hapa kwamba ni lazima tuwe na sheria, wakati wenzetu wa Serikali wakiandaa sera.

Mheshimiwa Spika, utaratibu ulipaswa uwe ianze sera, tutunge sheria halafu ndiyo mambo mengine ya mikakati na kanuni yaendelee. Nitumie nafasi hii kuiomba Serikali kufanya haraka iwezekanavyo kukamilisha mchakato wa utungaji wa sera ya manunuzi ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, uwepo wa sera utatusaidia kuwa na maelekezo mahususi kwenye mambo ya manunuzi yanayogusa uadilifu, ufanisi, ushirikishwaji, mikakati ya kukuza makampuni yetu ya wazawa wa ndani kwenye manunuzi. Vilevile, matumizi ya rasilimali zetu za ndani yanapokuja manunuzi kwenye uzalishaji pamoja na mambo ya utawala bora na kuondoa migongano ya kimaslahi kwenye manunuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri pekee tuliyonayo ni kwamba wenzetu wa Wizara ya Fedha pamoja na kutokuwepo na sera wamejaribu sana kuyagusa maneno haya niliyoyataja. Mambo ya uadillifu, mambo ya ufanisi, yote tumeyagusa kwenye sheria hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo ningependa nichangie ni ile sehemu ya saba ya Muswada tulionao mezani, ambayo ni usimamizi wa mikataba. Eneo hili kwa kiasi kikubwa linazungumzia wajibu wa kusimamia utekelezaji wa mikataba. Sasa kwa sababu jambo hili linahusisha sekta kubwa kwa nafasi kubwa, linahusisha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali tusingeweza kuyaandika kwenye Sheria hii ni vema sasa wakati tukiangalia wajibu na usimamiaji wa utekelezaji wa mikataba ni vema kuona umuhimu wa kuiwezesha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa sababu sheria ya manunuzi haikamiliki bila kuwa na mikataba. Kwa hiyo, lazima kuiboresha sana Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kuiwezesha kibajeti, kusomesha vijana wetu, wataalam. Vilevile, kuisimamia kwa ukaribu kama Bunge.

Mheshimiwa Spika, nitatoa mifano ambayo Sheria za Manunuzi zinatupeleka kwenye mikataba ambayo mikataba hiyo tukishindwa kuifuata au Ofisi ya Mwanasheria Mkuu isipopewa nafasi ya kuisimamia, mikataba hiyo inaingizia hasara Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitatoa mifano ya mikataba mitano maarufu kwenye nchi yetu . Mkataba wa kwanza ambao ulitokana Sheria ya Manunuzi iliyopita ulikuwa kati ya Heritage Rukwa Tanzania Limited wakiwashtaki TPDC pamoja na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kukiuka mkataba wa uwekezaji jambo ambalo lilisababisha maamuzi yake Serikali ilitakiwa kulipa dola milioni 72.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana nasisitiza kuiboresha na kuiwezesha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, kama tunataka Sheria hii tunayoitunga ikafanye kazi hii kwa usahihi na hizi asilimia 70 za mapato yetu yote na makusanyo tunayopeleka kwenye manunuzi zikasimamie vizuri, lazima ofisi hii tuiwezeshe kibajeti iwe na wataalam wa kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo, nitumie fursa hii kuipongeza Ofisi ya Mwanasheria Mkuu pamoja na kwamba wapo watu wanabeza Wanasheria wetu huko nje, wapo watu wanaobeza Ofisi hii ya Mwanasheria Mkuu, ninataka niwaambie kwenye kesi hii Ofisi yetu ya Mwanasheria Mkuu ilisimama na kushiriki kesi pamoja na majadiliano na kuokoa kiasi chote hiki cha fedha ambacho ilikuwa tukilipe.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano wa mkataba wa pili, ambao ulisababisha nchi yetu kushitakiwa, ili tuone umuhimu kwamba Sheria hii ya Manunuzi haikamiliki bila mikataba na sehemu pekee ya kuisimiamia mikataba ni Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Shauri Namba ICSID kesi Namba ARB1733 kati ya Eco Energy akiishitaki Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kosa lipi, kwa kosa la kukiuka mkataba wa kulinda uwekezaji, angalieni hiki Waheshimiwa Wabunge pamoja na Watanzania wanaonisikiliza hapa kukiuka mikataba. Unajua kuna watu wanafika mahala wanaona tu kunaweza tu kukawa na mkataba na mtu akaamua tu akalala akaamka amekiuka, it is not that way! Haiwi hivyo, mikataba ina taratibu zake siyo habari tu ya kuamka, mtu ametoa tamko kwamba futa mkataba.

Mheshimiwa Spika, kesi kati ya Eco Energy na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kukiuka mkataba wa kulinda uwekezaji, kampuni moja ya Uswisi, baada ya mashtakiano Serikali ilikuwa inadaiwa, ilitakiwa ilipwe dola milioni 166 zote hizi ni fedha, ndio maana nasema Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, kama kweli haya manunuzi na sheria tunayotunga tunataka ifanye kazi lazima tuisimamie na kuiwezesha iweze kusimamia haya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, dola milioni 166 na hapa naipongeza tena Ofisi ya Mwansheria Mkuu wa Serikali kwa mara ya pili kwa kupambana sana na kuhakikisha tumeokoa dola karibia milioni 37 kwenye hili shauri. Yote hii iliyotupeleka ni Sheria ile ya Manunuzi ya zamani. Ndiyo maana nikasema Rais, pekee Mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, ameliona hili ni tatizo na ameamua kuleta Muswada hapa wa kuandika upya Sheria hii ya Manunuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkataba wa tatu uliovunjwa na ambao ulituingiza kwenye matatizo, mkataba wenye shauri namba ICC kesi Namba 22261/TO hii ni ya Symbion Power Limited wakiwashtaki TANESCO, kwa nini wamevunja mkataba wa uwekezaji wa umeme hii ni power purchase agreement. Madai ya dola milioni 355. Sikilizeni niwaambie haya mambo yalikuwepo toka zamani, Bunge limepiga kelele toka zamani, ripoti ya CAG imeandika toka zamani na sisi tumeonge hapa toka zamani hizo, lakini sheria ilibaki vilevile, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, mwenye kuona uchungu wa mambo haya ameleta Muswada wa Sheria hapa iandikwe upya, halafu anatokeaje Mtanzania anakuwa na mashaka na Rais huyu?

Mheshimiwa Spika, kwenye usimamizi wa rasilimali za nchi yetu, ataokeaje mtu anakuwa na mashaka na Rais huyu. Kesi ile Ofisi ya Mwanasheria Mkuu niipongeze tena, wamepambana natukaokoa katika dola ambazo tulitakiwa tulipe milioni 355, tumeokoa dola millioni 202, so these people are doing their job, last time walikuja hapa wanomba milioni 300 tu tuwaongeze, lakini haikuwezekana this is very sad. Mheshimiwa Waziri wa Fedha tunaomba sana kwenye Mid - Year Budget Review ya Mwezi wa 12 pamoja na mambo mengine yatakayoletwa Bungeni, Serikali mlete namna ya kuiwezesha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu, kitengo kinachosimamia mikataba, ikafanye kazi ya Watazania.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano wa mkataba wa nne, shauri Namba ICC Arbitration Award 15947/VRO hii ni kati ya Dowans Holding, haya kampuni yote ninayoyataja ni maarufu, mnayajua vizuri na sarakasi zote. Dowans Holding SA Tanzania Limited, wote hawa kwa pamoja wanaishitaki TANESCO. Shauri ambalo iliamuliwa tulipe dola millioni 77. Ofisi yetu ya Mwansheria Mkuu, wamepambana kwenye hizo tumekoa dola milioni 25, lakini mashtaka haya yote mnayoyaona Mheshimiwa Rais , amefika mahala akona hakuna namna zaidi ya kuandika sheria upya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kesi na mfano wa mwisho, Mohamed Abdulmohsin Al-kharafi and Sons, General Trading, General Contructing and Industrial Stucture WLL, watu wa Kuwait, walishitaki Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, pamoja na Wizara ya Kazi lakini na Wakala wa Barabrara Tanzania na tulihukumiwa kulipa dola milioni 30.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Mbunge, ahsante sana, kengele ya pili imeshagonga.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu na nyeti kwa nchi yetu. Awali ya yote, naomba niunge mkono hoja.

Nimesimama hapa ili niweze kuzungumzia mradi mkubwa wa kihistoria ambao nchi yetu inaendelea nao wa SGR. Nilisamama hapa mara ya mwisho nikauzungumzia, lakini leo nataka nizungumzie na niishauri Serikali namna bora ya ku-finance mradi huu wa SGR.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu mkubwa na mzuri kwa nchi yetu kama hatukujipanga vizuri na namna ya kuu- finance vilio vitakuwa vikubwa sana huku kuhusu barabara na mambo mengine ya miundombinu mingine. Hii ni kwa sababu fedha nyingi tunayoipata itakuwa inakwenda hapa, halafu tunashindwa kupeleka maendeleo kwenye maeneo mengine ya miradi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipo kitu kinaitwa credit rating, nimesimama hapa niishauri Serikali kufanya mchakato wa kufanya credit rating ya nchi yetu. Zipo kampuni duniani zinazofanya mchakato huu wa kui-rate nchi na faida ya kui- rate nchi ni kwamba utakuwa na uwezo, ukishakuwa rated una uwezo wa kwenda kwenye masoko ya mikopo makubwa na ukapata fedha kwa kiwango kikubwa na cha uhakika zaidi kuliko ambavyo sasa tuna-finance mradi huu kwa kutumia concessional loans.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza concessional loans zenyewe zilivyo zina masharti mengi na ambayo zinafanya sekta zetu binafsi zisiweze kushiriki kwenye maendeleo. Unapokuwa umechangua finance kwa kutumia concessional, yule anayekupa fedha ndiye anayechangua kampuni ya kusimamia, ndiye anayechagua kampuni ya kujenga pia. Tungekuwa tumejielekeza kwenye kufanya credit rating ili tuweze ku-issue infrastructure bonds, ingetuwezesha sisi kuamua nani tumpe kazi gani kwenye mradi upi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunavyozungumza nitatolea mfano Standard Charted Bank kwa kushirikiana na Export Credit Agencies walitupa sisi kama nchi mkopo wa bilioni 1.46. Mkopo huu ambao tumepewa kwa ajili ya kujenga hii SGR ni gharama kubwa ku-service mkopo huu kwa sababu gani, kwa sababu ukitumia njia hii ya kupata mkopo ni kwamba unaruhusu madalali katikati Standart Charted hana hela ya…

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kwagilwa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nampa taarifa mdogo wangu Kwagilwa kwamba tunapozungumza habari ya miradi ya kimkakati ya kimaendeleo katika nchi za kiafrika, bora uchague moja, upewe mkopo kutoka nje wenye masharti ya kwamba mradi ukiisha ukishindwa kulipa wauchukue au utafute mkopo wa bei nafuu kwenye nchi yako mradi uendelee kuwa wako. Kwa hiyo ndio mambo tunayopewa kuchagua hayo.

NAIBU SPIKA: Kabla sijakuuliza Mheshimiwa Kagilwa, Mheshimiwa Getere na Waheshimiwa Wabunge wote niwakumbushe humu ndani tumekuwa na mazoea si mabaya tukiitana nje lakini humu ndani ni Waheshimiwa, kuna wakati huwa inaleta changamoto kidogo mtu akiitwa mdogo wa mtu, kaka wa mtu, shemeji wa mtu na mambo kama hayo au mke wa mtu kwa maana hiyo hiyo.

Mheshimiwa Kwagilwa unaipokea taarifa hiyo.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge aliyezungumza inaelekea hajui hiki ninachokiongea, kwa hiyo taarifa hiyo siipokei. Nazungumzia infrastructure bonds, ni mkopo kama ulivyo mkopo mwingine na mkopo huu hauna sharti lolote la kwamba ukishindwa kulipa mradi huu unachukuliwa haiko hivyo. Uki-issue infrastructure bonds kunakuwa na watu wanao-subscribe wengi kutoka nje wenye fedha wanakupa. Hiki ndicho ninachokizungumzia.

Mheshimiwa Naibuu Spika, nilikuwa natolea mfano kwamba tulipata ile 1.6 kutoka Standard Charted, yupo Standard Charted pale, maana yake tumemlipa fedha wako Export Credit Agencies maana yake tumewalipa fedha na yote hii inaenda ina amount kwenye deni letu la Taifa, ungekuwa ume-issue bond ungekuwa umechukuwa tu fedha moja kwa moja kutoka kwa yule anayekukopesha bila kupita kwa mtu mwingine. Hiki ndicho ninachokizungumzia.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hivyo tutaweza kujenga barabara zetu za ndani kwa makusanyo yetu sasa, haya tunayokusanya kupitia TRA. Kwa mfano, Barabara ya Handeni – Kiteto – Kibirashi – Kondoa - Singida itaweza kujengwa, lakini ilivyo hivi sasa tumefanya bajeti allocation ya bilioni nne, hapo hapo kuna miradi mingine ya barabara kwa fedha hizo, tutakamalisha lini ujenzi wa barabara hizi ambazo ni za muhimu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nashauri kama tutaweza tufanye credit rating kwa kutumia Kampuni ya Standard and Poor, kama tukiweza tufanya credit rating kwa kutumia moody kama tukiweza tufanye credit rating kwa kutumia fitch.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaweza kufanya kwa kutumia kampuni mbili au tukiona ni gharama tufanye kwa kutumia kampuni moja. Tafsiri ya credit rating ni kwamba mnakuwa declared kama nchi ambayo ina uwezo wa kuhimili deni na kulipa pale inapogoma. Hiki ndio tunachokishauri na ndicho ninachokishauri kifanyike na Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunapozungumza kwenye huu mradi huu wa SGR mpaka sasa loti Na.3 haina fedha na haina mkandarasi. Mpaka sasa loti Na.4 Tabora - Isaka haina fedha na haina mkandarasi, hata hii unayoongelea loti Na.5 ya Isaka - Mwanza wamekuja Wachina hapa wameahidi kutupa 1.32 bilioni, hiyo ni concessional loans, sharti la kwanza kampuni zao mbili ndio zijenge. Ndugu zangu hatutaweza kulinda hata ubora wa mradi wenyewe, yaani mtu anapokupa, ajenge yeye, asimamie yeye, sasa wewe ushiriki wako ni upi kwenye hii? Tukiangalia kwenye sekta ya ujenzi ndio sekta ambayo imekuwa mfululuzo kwenye miaka hii ya karibuni lakini watanzania wanashiriki vipi kwenye sekta hii ya ujenzi, hawawezi kushiriki kama tunaendelea kuchagua financing za namna hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nimeongea kwa wakati, nikushukuru sana kwa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii adhimu nipate kuchangia katika bajeti ya nchi yetu kwa mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kuunga hoja mkono hoja zote mbili zilizowasilishwa ya kwanza ya Waziri wa Fedha na ile yetu ya Kamati ya Bajeti. Nimpongeze sana sana Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea bajeti yenye maono makubwa kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii imebeba mahitaji ya Watanzania, bajeti hii imebeba matumaini ya Watanzania, bajeti hii imebeba maoni ya Wabunge, bajeti hii imebeba Ilani ya Uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi, lakini bajeti hii imebeba dira ya Taifa letu, bajeti hii imebeba maono ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan. Nasema hivyo kwa sababu bajeti hii inakwenda kutupelekea barabara zetu zote mijiji na vijijini Mheshimiwa Rais kupitia bajeti iliyowasilishwa hapa anatengua Sheria ya Usalama barabarani ili tuweze kupata Bilioni 322 kwa ajili ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais amebeba maono makubwa kwa Taifa letu kwasababu kupitia bajeti hii tunapeleka maji safi na salama kwa nchi nzima, kupitia hiyo ameamua kutengua Sheria ya Posta na Mawasiliano Sura Na. 306 ili tuweze kukusanya Trilioni 1.3 kwa ajili ya kuyafanya haya. Mama yetu amebeba maono makubwa kupitia bajeti hii kwa sababu anakwenda kufanya jambo ambalo limeshindikana kwa miaka mingi bima ya afya kwa kila Mtanzania, Mheshimiwa Rais anakwenda kutekeleza miradi yote ya kimkakati ikiwemo mradi maarufu ambao mimi huwa ninasimama hapa kuuongelea kila mara mradi wa SGR unakwenda kutekelezwa kupitia bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii inakwenda kututengenezea miundombinu ya elimu, kwenye hili upande wa elimu ya juu kupitia bajeti hii watoto wote wa Kitanzania ambao walikuwa wameshapata udahili kwenye vyuo na wakakosa nafasi ya kusoma kwa sababu ya fedha, bajeti hii inakwenda kuwarudisha katika vyuo. Kwa hiyo, bajeti hii ni ya Watanzania na bajeti hii ni ya kwetu na tunakwenda kuijenga nchi yetu kwa kujifunga mikanda wenyewe kama ambavyo Waziri wa Fedha alituambia hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali ukiacha maeneo haya mapya ambayo yametengua sheria nne na yakatupatia Trilioni mbili, TRA ina department Nne ukiangalia hizi department kuna moja ya muhimu sana inaitwa department ya customs na excise hii inakusanya asilimia 38 ya mapato yote ambayo TRA inakusanya yanatoka kwenye hii department hii inatafsiri kwamba kwa lengo tulilojiwekea la kukusanya mapato ya ndani Trilioni 26 ina maana kwamba Trilioni 8.4 zitakusanywa na department ya customs na exercise duty. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaitaja hii department kwa sababu ndiyo inayohudumia bandari yetu, na ndio inayohudumia viwanja vyetu vya ndege lakini ndio inayohudumia mipaka yetu, Mheshimiwa Waziri wa Fedha twendeni tukafanya mapinduzi kwenye Bandari yetu. Haiwezekani eti bandari yetu ya nchi haina vifaa vya kisasa vya kupakua mizigo na kupakia mizigo. Twendeni tukanunue vifaa hivyo ili mizigo mingi ipite kwenye bandari yetu. Hali ilivyo hivi sasa Bandari yetu inapitisha tani Milioni 17 kwa mwaka, kiwango hiki ni kidogo sana ukilinganisha na bandari ambazo tunashindana nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukafanya mapinduzi kwenye bandari kwa kununua vifaa vilevile tutafanya mapinduzi kwenye bandari kwa kuziangalia vizuri sheria tunazozitunga kwenye Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge sikilizeni niwaambie Sheria hizi za Afrika Mashariki Tanzania trading yetu kubwa ya kibiashara tunafanya na SADC tuna trade kidogo sana na East Africa, wenzetu wamekuwa wajanja sana wana tu-fix kwenye sheria hizi hasa hasa zile zinazohusu usafirishaji wa mizigo kutoka bandarini kwenda kwenye nchi tunazozihudumia. Kwa hiyo, tujipange vizuri kwenda kusimamia eneo hilo ili bandari yetu ipitishe mizigo mingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile baada ya kupitisha bajeti hapa wenzetu wa Serikali tunawapa kazi ya kwenda kuitekeleza bajeti, siku zote hapa tumekuwa tukitaja suala la monitoring and evaluation, budget circle yetu ilivyo, ina sheria hapa Bungeni kupitia Sheria yetu ya Bajeti, inaangazia draft ya budget, inaangazia approval ya bajeti ndiyo tunachokifanya hapa sasa hivi tupo kwenye hiyo stage ya approval, vilevile inapoingia stage ya execution kwenye stage ya bajeti ndipo ambapo Sheria yetu inakosa nguvu, inakosa nguvu. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali ikalete policy ya monitoring and evaluation ili tutunge sheria na hili hapa limekuwa likizungumzwa na kukosewa kosewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuhitaji kutengeneza independent board yeyote hapa, Bunge ndiyo jukumu lake hili yaani tunachotakiwa sasa sisi ni kuendelea kusimamia Serikali kwa maana ya monitoring and evaluation kipindi tutakapokuwa tumeitunga sheria hiyo ya monitoring and evaluation ili tuweze kuisimamia Serikali vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho niipongeze sana Serikali, nimpongeze sana Mama yangu Samia Suluhu Hassan Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa sababu mimi ni shahidi tosha kwamba bajeti aliyoileta hapa imezingatia maoni yote ya Wabunge yakiwemo maoni ambayo tumeshauri hapa ya ku-finance miradi mikubwa kwa kutumia infrastructure bond, ipo hapa imetajwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze sana Serikali nimpongeze sana mama yangu Samia Suluhu Hassan Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano, kwa sababu mimi ni shahidi tosha kwamba bajeti aliyoileta hapa imezingatia maoni yote ya Wabunge yakiwemo maoni ambayo tumeyashauri hapa yaku-finance miradi mikubwa kwa kutumia infrastructure bond, ipo hapa imetajwa. Bajeti pia imechukua maoni yetu Wabunge ya kufanya credit rating ya nchi yetu, ipo hapa imekaa. Mheshimiwa Waziri nikupongeze sana, ondoa mashaka hautakuwa unpopular, utakuwa ni popular finance Minister kwa sababu umeyabeba maono ya Mheshimiwa Rais ukatuletea hapa kwa kadri ambavyo alielekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo nikushukuru sana ahsante sana kwa fursa.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nichukue nafasi hii nikushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuchangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mchango wangu ni mfupi sana. Ukurasa wa 116 wa Mapendekezo yaliyosomwa, yaliyoletwa hapa na Serikali, kipengele cha 3.3.7.3 - Ubia kati ya Sekta Binafsi na Sekta ya Umma; pana miradi pale imeorodheshwa kama 11. Sisi kwenye Taarifa ya Kamati tumeeleza jinsi ambavyo miradi hii ya PPP imeorodheshwa kwa miaka na miaka bila kutekelezwa na matokeo yake kwenye Mpango huu tunaotarajia kwenda kuwa nao, Serikali imeongeza mradi mwingine mmoja mpya. Mradi huu ndiyo umenisukuma nizungumzie eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu, kipengele K, unasema: “kuendeleza upembuzi yakinifu wa mradi wa kusimika boya la kuegesha meli za mafuta katika Bandari za Dar es Salaam na Bandari za Tanga.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu una conflict of interest na maslahi ya nchi, kuuweka kwenye utekelezaji wa kutumia sekta binafsi na kwa maneno rahisi, kuandaa huu mradi kwa kumpa mtu binafsi aufanye, kwa maneno rahisi kabisa naweza kusema hii ni hujuma kwa nchi yetu na ni jambo halikubaliki. Tusipoangalia, tunakwenda kutengeneza TICTS nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko hivi, mradi huu wa kutengeneza boya la kuegesha meli za mafuta, unagusa bandari, tena bandari mbili. Bandari ni uchumi… (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kwagilwa tuwekee vizuri ili uende tu vizuri, yaani kwamba Serikali hapa imeweka katika orodha ya PPP. Kwa hiyo, ni orodha ya watu binafsi na Serikali yenyewe. Nawe unasema kwamba ni binafsi peke yake, labda tuwekee vizuri tu.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nasema hivyo kwa sababu mradi upo kwenye upembuzi yakinifu, inamaanisha mradi haujaanza kujengwa, ina maana unaikaribisha Sekta Binafsi au mtu binafsi ashiriki kuanzia kwenye kujenga hilo boya na kwa lugha nyingine kujenga kipande cha bandari; umkabidhi kipande cha bandari ili ajenge gati kwa ajili ya meli kubwa za mafuta na gesi kuja kushusha pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inagusa habari ya usalama wa nchi, lakini inagusa habari ya uchumi wa nchi, vile vile bandari ni lango la nchi yetu. Kumpa mtu binafsi au kumshirikisha kwenye hizi hatua za awali za kujenga, kumpa miundombinu ile ya bandari, siyo jambo sahihi sana kwa mustakabali wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaelezea jambo hili kwa sababu ukiongelea meli kubwa za mafuta unaongelea pia na meli kubwa za gesi. Sisi tunazalisha gesi. Tumetoa gesi, tumeshaichimba, tumewekeza billions of money kwenye gesi na kila mwaka shirika letu linaloshughulika na habari za gesi na mafuta linatumia bilioni 50 kila mwaka kwa ajili ya utafiti kwenye mafuta na gesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kana kwamba hiyo haitoshi, tayari tumeshakopa Benki ya Exim, Dola za Kimarekani bilioni 1.2 kuitoa gesi kutoka Madimba pale Mtwara, kuitoa Songosongo Lindi, kupitia Somanga Fungu, tumeifikisha Pwani na iko Dar es Salaam. Sasa gesi yetu ile ni natural gas. Tumeshaifikisha Dar es Salaam, Serikali haina juhudi yoyote inayofanya ya kuisambaza gesi kwa wateja. Imeshafika Dar es Salaam, lakini badala yake imerukia inataka impe mtu binafsi aingize gesi nchini. Hiki kitu hakiko sawa. Hakiko sawa kwa sababu huyu mtu au hii sekta binafsi ikipewa kuwaruhusu…

MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji, Mheshimiwa Reuben, Mbunge wa Handeni Mjini, kwamba anapoendelea kushangaa hilo ashangae pia kwamba gesi hiyo ambayo inatoka Mtwara kuja mpaka Dar es Salaam inatumika kwa asilimia 20 tu. Maana yake bado gesi yetu ya ndani haijapata soko. Ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kwagilwa, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hii, tena naipokea kwa uzito sana, hasa ukizingatia kwamba taarifa hii imetolewa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tuwe wazalendo kwenye mambo haya. Mambo haya kwa sababu yanashirikisha mikataba na experience inaonesha kwamba tumekuwa tukifanya vibaya sana kwenye mambo ya mikataba, hasa inayogusa rasilimali kubwa kama hii. Nashauri hapa tusiingie kwenye huu mtego. Tulishaingia huko tukafanya mambo ya hovyo na ya ajabu ambayo hayawezi kuzungumzika, tusirudi huko. Tusirudi huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu, upembuzi yakinifu uendelee na ukikamilika ufanywe na Serikali. Kwa hiyo naishauri Serikali iondoe huu mradi kwenye hii orodha ya miradi inayopanga kuitekeleza kama PPP. Ni muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewashauri hili kwenye Kamati, tulifikiri wameelewa lakini wamekuja nalo kwenye floor huku na ndiyo maana na sisi tumeona tusione haya tuje tuseme hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nataka niliseme ni kwamba katika Mpango huu uliopita kwa maana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, mchango huu unatosha. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. KWAGILWA R. NHAMILO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana niungane na wenzangu kukupongeza kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika wa Bunge letu la Jamhuri ya Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana kamati yako ya bajeti pamoja na Bunge kwa ujumla tulifanya Amendment of the Road and Fuel Tolls Act Cap. 220. Marekebisho haya yalilenga kuipatia TARURA fedha kwa ajili ya barabara zetu za vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitoe taswira ndogo sana ya TARURA tunapozungumza TARURA ili angalau tufanye mapinduzi kwenye eneo hili la barabara zetu za vijijini. Handeni hususan Jimbo la Handeni mjini barabara zetu za TARURA barabara za vumbi ni 88%. Kwa Mkoa wa Tanga barabara zetu za TARURA, barabara za vumbi ni 79% na kwa Tanzania nzima TARURA ina mtandao wa barabara unaofika kilometa 144,429 zinahudumiwa na TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hizo 76% ni barabara za vumbi kwa maana ya kilometa 111,197, TANROADS inahudumia barabara zote kilometa 36,000 na katika hizo zenye lami ni kilometa 11,000 what is the myth ni kitu gani cha ajabu kwenye hiki ninachojaribu kukizungumza tumeipa TARURA jukumu kubwa sana lakini hatujaweka juhudi kubwa za kibajeti na za kitaasisi za kiteknolojia na kwa nguvu zote kujaribu kuibadilisha ili iweze kuhudumia barabara zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa takwimu hizi nilizotoa hapa ndiyo kusema kwamba barabara nyingi mtandao mkubwa wa barabara Tanzania uko chini ya TARURA. Sasa the opposite ndiyo tunachokifanya tunapeleka nguvu kubwa sana TANROADS na natambua kwamba barabara wanazohudumia ni za lami, lakini haiondoi fact kwamba kilometa hizi 144,429 ndiko ambako Tanzania waliko na ndiko ambako uchumi uliko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kusema ni nini ninachotaka kusema ni kwamba lazima tufanye mapinduzi ya namna ya approach ya kutengeneza barabara zetu kuanzia kwenye bajeti yetu inayokuja lazima tufikirie kwa namna ya tofauti. Tathmini ya dharura iliyofanywa juzi kwa uharibifu unaofanywa na mvua uliosababishwa na mvua tathmini iliyofanywa ya haraka inahitajika bilioni 120 kufanya tu marekebisho .(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukichukulia sasa ile amendment tuliyofanya ya kutoka bilioni 322 na hizo kwa hakika hatutaweza kuzikusanya zote, 120 yote inaenda kufanya marekebisho yaliyosababishwa na mvua. Which means tunakwenda ku-miss target yetu ambayo tulijiwekea kufungua barabara zetu za vijijini ninachotaka kusisitiza kama ambavyo tumefanya jitihada za makusudi kwenye SGR, jitihada za makusudi kwenye bwawa la Mwalimu Nyerere, vivyo hivyo moyo wa uchumi wa nchi yetu ni hizi barabara hizi kilometa 144,000 ambazo ziko chini ya TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo lazima tufanye mapinduzi ya namna ya kufikiri na lazima tufanye mapinduzi ya namna ya kutenga bajeti yetu. Tusii-treat TARURA kama kachombo kadhaifu dhaifu hivi ambako kako chini ya Wizara ya TAMISEMI ambako hata hivyo hata kwenye hiyo Wizara yenyewe tuna Waziri wa TAMISEMI na Manaibu Waziri wawili mmoja anajulikana ni wa afya na mwingine anajulikana ni wa elimu. Yaani hata hiyo TARURA pale huioni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dhati kabisa ni lazima tufanye mapinduzi bajeti inayokuja tutenge fedha nyingi lakini zienda angalau zikabadilishe barabara zetu zitoke kuwa za vumbi ziende kwenda kuwa changarawe. Lakini na siku za usoni siku za baadae tujifunze teknolojia kwa wenzetu tutengeneze barabara zetu kwa teknolojia ambayo ni cheap.

NAIBU SPIKA: Malizia.

MHE. KWAGILWA R. NHAMILO: Kama ambavyo alishauri Mheshimiwa Rais barabara zetu tuzifanyie mapinduzi tuende kwenye teknolojia ya kati ambayo siyo gharama sana lakini barabara tuzijenge ziweze ku-survive na ku-sustain kwa muda mrefu.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia ripoti za Kamati zetu tatu. Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa, Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma na Kamati ya Hesabu za Serikali. Mimi nitajielekeza zaidi kwenye Kamati hii iliyochambua ripoti ya CAG ya Hesabu za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili nimeisoma vema ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwenye eneo la Mashirika ya Umma. CAG amepitia Shirika la Bandari (TPA), TTCL, TANESCO, Shirika letu la Nyumba - NHC na TRC. Nitajielekeza kwenye Shirika la TANESCO na hususan kwenye mradi mkubwa tulionao. Mradi wa Trilioni 6.5 wa Bwawa la Umeme la Mwalimu Julius Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, CAG anasema alivyokwenda kuangalia bwawa hili alikuta ujenzi umechelewa kuisha kwa asilimia 46.45. Bwawa hili ni la muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu, Watanzania wanahitaji bwawa hili likamilike ili tuweze kupata umeme wa uhakika. Viwanda vyetu vinahitaji bwawa hili likamilike ili viweze kufanya uzalishaji. Miradi yetu ya REA tunayoitengenza sasa inahitaji bwawa hili likamilike ili iweze kupata source ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, gridi yetu ya Taifa ili iwe na umeme stable inahitaji bwawa hili likamilike ili tuweze kupata umeme wa uhakika. Vilevile, gharama zetu za umeme ziko juu, umeme wa maji ni umeme cheap kuliko umeme wowote, Watanzania wanahitaji bwawa hili likamilke ili waweze kupata umeme wa gharama nafuu. Sasa taarifa zilizopo hivi sasa, ukizingatia hii taarifa ya CAG, kwamba ujenzi umechelewa, bwawa lilitakiwa likamilike mwaka huu mwezi wa Sita, mwezi wa Sita umepita bwawa halijakamilika, hivi sasa ujenzi uko asilimia 74 na bado hujakamilika, Mkandarasi na Serikali wanabishana. Mkandarasi anaomba kuongezewa miaka mingine miwili zaidi na kwa maana hiyo kwa mujibu wa Mkandarasi, bwawa hili litakamilika mwaka 2024. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali wao wanasema kwamba wamekataa kumwongeza miaka miwili, badala yake wamemwongeza mwaka mmoja. Nataka nilipitishe Bunge hili sababu ambazo zimetolewa na Mkandarasi na mpaka wakafikia kumwongeza mwaka mmoja, pamoja na kumwongeza huo mwaka mmoja yeye bado mpango kazi ambao ameuweka Serikalini unaonesha ni miaka miwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya kwanza, anaomba nyongeza ya muda na kuongezewa gharama kwa sababu watengenezaji wa mitambo walijitoa. Sababu ya pili, anaomba nyongeza ya muda na gharama kwa Watanzania kwa sababu ya taarifa za miamba. Sababu ya tatu, anaomba kuongezwa muda na ongezeko la gharama kwa sababu pale site anasema umeme haumtoshi. Sababu ya nne na ya mwisho, anaomba kuongezewa muda na gharama kwa sababu njia ya kupelekea vifaa site ni mbaya. Jambo hili halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Trilioni 6.5, kodi za Watanzania, bado inafanyika janjajanja ya kutaka tena kuongeza gharama ya mradi huu? Kuongeza gharama ya muda na gharama ya fedha? Serikali inasema sababu zilivyotolewa haikukubaliana nazo. Kama hawakukubaliana nazo nataka Waziri mwenye dhamana akija hapa atuambie, kama sababu hizi hamkukubaliana nazo kwanini mmemwongeza mwaka mmoja? Kwa nini mmekubali kumwongeza mwaka mmoja ilihali mpangokazi wake unasema anataka miaka miwili, nani mnamdanganya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali na Mkandarasi wameunda Bodi inayoitwa DAB, (Dispute Adjudication Board) kwa ajili ya kufanya suluhu ya haya. Mkataba Serikali umesema kwamba sababu hukubaliani nazo, inamaana ulitakiwa ukabidhiwe kazi mwaka huu, mkataba unasema nini kama kazi haijakabidhiwa? Kwa nini madai ya Serikali kwa Mkandarasi hapa hatuyaoni? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kushangaza mpaka sasa Mkandarasi tumeshamlipa asilimia 65.9 ya fedha. CAG anasema mradi umechelewa, Mkandarasi tumeshamlipa asilimia 65.9 ya fedha zote yaani Trilioni 4.3, lakini Serikali badala ya kulipa trilioni 4.3, wamemlipa trilioni 4.43. Wamemlipa ziada ya shilingi bilioni 113. Sababu waliyoitoa ya kulipa ziada ya shilingi bilioni 113 wanasema eti ni mabadiliko ya kubadilisha dola na shilingi.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Twaha Mpembenwe.

T A A R I F A

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba tofauti hii anayoizungumzia hapa ya fedha ya Bilioni 113 fedha za walipa kodi zilizolipwa kwa uwiano wa kawaida tu, kwa fedha tulizokuwa tumezizoea kawaida kwa kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI, Shilingi Milioni 500 inajenga kituo kimoja cha afya. Kwa hesabu za kawaida hivi ni vituo 226 vya afya ambavyo vingeweza kujengwa katika Jimbo la Handeni, Kibiti na Majimbo mengine yote hapa Tanzania.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kwagilwa unaipokea taarifa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo taarifa naipokea, shilingi 113,196,370,381.06 eti kwa sababu ya kubadilisha dola na shilingi, mkataba gani huo kwenye nchi ya wanasheria wasomi? Yaani unawezaje kuwa na mkataba wa hivyo? Eti kwenye malipo mkianza kulipana wewe ukianza kutafuta dola unapoteza bilioni 115. Vituo 226 vya afya! Hatuwezi Kwenda hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sisi wengine lazima tuwaambie tu, kazi yetu hapa ni kuwaambieni ukweli. Sisi sote tutapita lakini Tanzania itabaki. Bilioni 113 kubadilisha shilingi na dola, naongelea bilioni; hii si sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu mkubwa mpaka sasa taifa halina uhakika kama utakamilika. Kwenye hili tusitake kuumauma maneno. Kutokukamilika kwa mradi huu kunafanya wananchi wa Handeni hawatapa umeme; kutokukamilika kwa mradi huu kunafanya ndugu Waheshimiwa Wabunge kwenye majimbo yenu miradi ya REA tunayopeleka haitakuwa na source ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka niseme kwa lugha fupi, kwamba hii ni hujuma. Tunanunua umeme kwa gharama kubwa sana kutoka mitambo ya kukodisha. Kwa nini hatumalizi wa kwetu? Kwa nini mtu asishawishike kuamini kwamba hii ni hujuma? we cannot go like that as a nation, hatuwezi kwenda hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa sababu leo tuko hapa kuisimamia Serikali ninamwomba Mheshimiwa Spika, aunde kamati tuchunguze hili. Haiwezekani mradi ambao ni tegemezi kwa taifa usikamilike kwa wakati, na bado panaanzishwa longolongo nyingine zitakazopelekea tulipe zaidi na tukabidhiwe mradi baadaye zaidi, na huenda hata usikamilike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna miradi mikubwa tu nchi hii ya kwanza SGR trilioni 16, huu tunaotengeneza. Mradi wa pili ni huu takriban trilioni saba why can’t we be serious on this.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa muda nawashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa fursa hii ya kunipa kuchangia kwenye ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa uelekeo huu wa bajeti ambazo tumezijadili kwenye Kamati zetu na sasa tunazijadili kwenye Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2011 tulitunga Sheria ya Manunuzi ya Umma na baadae tukaifanyia marekebisho mwaka 2013. Sheria hii ya Manunuzi ya Umma ni sheria muhimu sana kwa sababu zaidi ya asilimia 70 ya fedha zote tunazopitisha hapa kwenye bajeti, tunakwenda kuzitumia kupitia Sheria hii ya Manunuzi ya Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria hii ya Manunuzi ya Umma tunamuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu na Serikali walete Muswada tuifanyie marekebisho kwenye kipengele cha ununuzi wa madawa. Sheria hii tulivyoitunga ni cross-cutting, kununua mabati tunatumia sheria hii, matofali sheria hii, kununua vifaa vingine ni sheria hii pia. Ni lazima sheria hii tuirekebishe ili kipengele cha ununuzi wa madawa kiwe na focus yake, kiwe na umuhimu wake, kiwe na utofauti wake, nitaelezea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii kwenye ununuzi wa madawa inatoa mianya mitatu mibaya. Mwanya wa kwanza unaitwa price rigging au price curtailing. Sheria kwa jinsi ilivyo tunapokwenda kuitekeleza kupitia mtandao wa TANePS, hasa ukizingatia kwamba MSD inanunua madawa asilimia 90 tunayaagiza kutoka nje. Kwa hiyo, sheria hii inaitaka MSD kutangaza tender kupitia mfumo wa TANePS na hapa hushindanisha wazabuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wazabuni hawa kwa mara nyingi kumekuwa na tabia ya watu kujipanga, wakijipanga anayechukuliwa ni yule mwenye bei ya chini, kiuhalisia ukiangalia bei ya chini, ambayo wao wanaiita lowest evaluated bid ukiangalia hii inayoitwa bei ya chini siyo bei ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mifano MSD walipotangaza kununua mashine inayoitwa Hematology Analyzer mzabuni aliye-tender bei ya chini ali-tender kwa Shilingi Milioni 117 wakati bei ya soko halisi ni Shilingi Milioni 20. Nitatoa mfano wa pili, MSD walipotangaza tender ya mashine inayoitwa immunology analyzer, mzabuni aliye-tender kwa bei ya chini ali-tender kwa Shilingi Milioni 149 ilhali mashine hii bei ya soko inauzwa Shilingi Milioni 37. Nitatoa mfano wa tatu, MSD ilipotangaza kununua mashine ya kuchakata maji kwa ajili ya kutumika katika kusafisha damu, mzabuni aliye-tender bei ya chini ali-tender kwa Shilingi Milioni 129 ilhali bei halisi ya mashine hiyo ni Shilingi Milioni 32. (Makofi)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Mpembenwe.

T A A R I F A

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba kidonge cha kilo moja cha kuweza kutengeneza dawa ya kutoa madoa yaani ile JIKI soko halisia inauzwa kwa Shilingi Milioni Nne lakini MSD wamenunua kwa Shilingi Milioni 262 na ushahidi upo. (Makofi)

MWENYEKITI: Unapokea taarifa hiyo Mheshimiwa Kwagilwa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii naipokea na ninataka nisisitize kidonge kimoja cha kilo moja cha kutengeneza JIKI bei sokoni ni Shilingi Milioni Nne na MSD kidonge hiki wamepelekewa bei ya Milioni 262! (Makofi)

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili halikubaliki duniani wala mbinguni. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa subiri kidogo Mheshimiwa Kwagilwa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya.

T A A R I F A

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mchangiaji. Ni kweli Sheria ya Manunuzi ya Umma inaweza ikawa na changamoto lakini bado haizuii MSD kununua dawa moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 Rais Magufuli alituelekeza tuachane kununua dawa kutoka kwa madalali, tununue kutoka kwa wazalishaji, mwaka 2017 angalieni vyombo vya habari. Tulifanya press tuliweza kushusha bei za dawa kwa zaidi ya asilimia 40, kidonge cha Amoxicilline kilichokuwa kinauzwa Shilingi 11,000 tulikinunua kwa Shilingi 4,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mashuka kutoka Shilingi 22,000 tuliyashusha mpaka Shilingi 11,000. Tatizo lililopo MSD siyo tu Sheria ya Manunuzi ya Umma, mipango mibaya ya utekelezaji wa manunuzi ya umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, MSD hiyo hiyo kwa Sheria hii ilianza kufanya vizuri. Kwa hiyo, hiyo ni taarifa nataka kusema sheria ipo lakini tunaweza tukabadilisha sheria, lakini kama hatuna mipango mizuri ya procurement ya dawa, vifaa na vifaa tiba tatizo la MSD litaweza kuendelea. Mheshimiwa Rais alishatoa maelekezo Wizara tunayafanyia kazi. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Waziri kwa taarifa. Mheshimiwa Kwagilwa unapokea taarifa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea taarifa kwa maana moja nzuri sana kwamba Mheshimiwa Waziri…

MWENYEKITI: Haya na ninakuongezea dakika moja na nusu kwa kumalizia hoja yako.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anakubaliana kwamba lipo tatizo, kama tunataka kumsaidia Mheshimiwa Rais, ambaye amekwishatoa maelekezo ya kwenda kumulika MSD tumsaidieni sisi kwa sababu sehemu yetu ni kutunga sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii inayo shida, shida hii inatupeleka hata Bima yetu ya Afya haifanyi kazi. Huwezi kuwa na Bima ya Afya inayohudumia vifaa ambavyo viko overpriced. Madawa yapo overpriced, vifaa vinavyotumika viko overpriced, Bima yako ya Afya itashindwa ku-cover haiwezi! Siyo tu hivyo, namuongelea mwananchi wa Kata ya Kwamagome anayeumwa figo akafanye diagnosis kwa Shilingi 300,000 haiwezekani! Shilingi 500,000 haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuongelea mwananchi wa Kata ya Malezi, namuongelea mwananchi wa Kwaluala, mwananchi wa kwa Sindi haiwezekani! (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MWENYEKITI: Taarifa kutoka wapi?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili...

MWENYEKITI: Mheshimiwa Naibu Waziri Daktari Godwin Mollel una taarifa?

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti…

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilindie muda wangu umechukuliwa. (Makofi)

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Afya ameshalielezea vizuri, jambo lenyewe liko straight forward na akasema Rais wetu wa Awamu ya Tano alishaeleza kwamba tuendeni viwandani. Kwa hiyo, anachochangia ni kizuri sana hatuna shida, lakini tukishatoka tukaelekea upande wa viwanda tumekata huo mzizi wa fitina, na vyombo vyetu vingine vikifanya kazi vizuri kuhakikisha wanasimamia hakuna namna yoyote hayo yanayosemwa wakati hii Nchi ina vyombo vyake ninakuhakikishia hakitatokea hicho. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Afya ameshatoa maelekezo na kazi hii inaendelea.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Mollel kwa taarifa yako. Mheshimiwa Kwagilwa, unapokea taarifa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, jitihada zote hizi za Serikali inaonesha kwamba lipo tatizo. Ninachotaka niseme ni nini?

Mimi nitamshangaa sana Mtanzania yeyote ambaye haelewi hiki ninachokisema hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia kwamba Mheshimiwa Rais amepeleka Shilingi Bilioni 200 MSD na bado Watanzania hawana madawa kwenye hospitali! Mheshimiwa Rais amepeleka shilingi bilioni 200 na bado hazitoshi kununua dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fikiria mazingira ambayo mwongozo uliotolewa na Serikali… (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Kwagilwa kwa mchango wako sasa namuita Mheshimiwa…

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia ripoti zetu za Kamati zetu hizi mbili na specifically nataka nichangie ripoti ya Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukurasa wa kumi na moja wa taarifa iliyowasilishwa na Mwenyekiti wetu wa Kamati hii unaongelea habari ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati katika halmashauri nchini. Wanasema Bunge limeazimia kupitia upya miongozo ya namna ya kutekeleza miradi hii, na kwamba Kamati imejulishwa na Serikali kwamba tayari imeshafanya mpango wa kushirikiana na UNCDF kwa ajili ya kuandaa mipango hiyo mipya ili miradi hii iweze kutekelezeka fairly.

Mheshimiwa Spika, miradi hii ya kimkakati ni kielelezo kinachoishi, kinachoonesha namna gani kama Taifa hatuko sawa katika ugawaji wa rasilimali za nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, miradi hii ya kimkakati ni kielelezo kinachoishi, kinachoonesha kwamba kama Taifa hatuko sawa katika ugawaji wa rasilimali zetu, nitaelezea.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia miradi hii ya kimkakati sharti lake kubwa la kwanza lilikuwa ni halmashauri itenge fedha, halafu ipeleke andiko. Kwa jinsi halmashauri zetu zinavyotofautiana kimapato mathalani unapozungumzia Halmashauri ya Handeni Mjini own source yetu hata milioni 700 haifiki, tutaigawaje gawaje hiyo fedha mpaka tupate fedha ya kuwekesha ili Serikali ije kutuunga mkono kupata mradi wa kimkakati. Hiyo ndiyo kusema wale giants wote wataendelea kupata miradi hii, halafu sisi ambao siyo giants tutaendelea kukosa miradi hii. Tunatengeneza Taifa ambalo linawapendelea wengine na kuwatweza wengine. (Makofi)

Kwa hiyo, nilikuwa naomba na naiomba sana Serikali huu mwongozo wanaouandaa kwanza pana kitu cha ajabu sana, mimi nilifikiri kwamba mwongozo wanamna ya kugawanya miradi hii Wizara tu ingeweza kufanya kwa maana Serikali tu inaweza kufanya. Yaani sisi kuandaa muongozo wawape Mradi uende mpaka tulete UNCDF? Yaani ndiyo Serikali mmefikia hapo? Yaani kwamba ninyi hamuwezi kufikilia kabisa namna gani tugawanye fairly mpaka tulete hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu jinsi ilivyo unavyogawanya kwa kupeleka kwenye miji mikubwa peke yake unasababisha vijana wetu kutoka Handeni na maeneo mengine ya Tanzania wahame kwenda kwenye hii miji mikubwa, unaenda kusababisha mrundikano pale, watoto wetu wanatafuta ajira pale, vijana wetu wamejaa Dar es Salaam, wamejaa Arusha, wamejaa Mwanza wametoka kwenye vijiji huko kwa sababu hatupeleki miradi hii.

Mheshimiwa Spika, nitaongelea kwa pamoja na mradi huu wa TACTIC maana ni yote hii ni miradi inayokwenda sambamba. Mradi huu wa TACTIC unatupa master plan kwenye mradi, unatupa barabara, unatupa soko na unatupa stendi, cha kushangaza hii miji inayosema ni giants na inayopewa hii miradi ya kimkakati ndiyo hii hii tena ambayo ipo kwenye TACTIC na imepewa kipaumbele ya kwanza, yaani kule kwenye mmewaweka tena kwenye TACTIC na ambako nako watapata soko, halafu unaacha miji kama Bunda inashangaa shangaa, Handeni Mjini tunashangaa shangaa, Ifakara tupo tupo tu, Kondoa, Mafinga, Makambako tunatengeneza Tanzania gani hiyo ya kujenga Dar es Salaam kila siku?

Mheshimiwa Spika, lazima tufike mahala rasilimali za nchi yetu tuzigawe kwa usawia na hili niwaombe wenzetu wa TAMISEMI wakae na watu wa Wizara ya Fedha, kaeni na watu wa Wizara ya Fedha kama fedha hizi tulizonazo zetu za mapato ya ndani na hizi tulizokopa World Bank hazitoshi kuendeleza miji yetu, kaeni na Wizara ya Fedha ili twende tukatatue tatizo hili kwa kutumia Sera za Kikodi. Hivi nani hapa anaweza akasimama aniambie eti Mbuga ya Katavi siyo bora kuliko Serengeti? Katavi iko vile leo ni kwa sababu miundombinu iko mibovu tu pale. Kwa nini hatugawanyi rasilimali hizi kwa kufuata huo uhalisia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali na hususani TAMISEMI waachane na hii habari ya kuzunguka nchi nzima eti wanatambua vyanzo vya mapato. Sasa ukienda Handeni unatambua vyanzo vya mapato? Utakuta sisi ni mnada tu pale kila siku sisi ni mnada tu. Kutengenezwe district economic profiles kwa nchi nzima ambazo zitaonesha…

MHE. ENG. ISACK A. KAMWELWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Nhamanilo kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Isack Kamwelwe.

T A A R I F A

MHE. ENG. ISACK A. KAMWELWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kumpa taarifa mzungumzaji anaeendelea kwamba mwongozo wa bajeti ya mwaka ujao wa fedha TAMISEMI wameelekeza halmashauri zinazokusanya mapato chini ya bilioni moja kwenye mapato yake zitenge asilimia 20 tu ya maendeleo, lakini zile ambazo zinapata zaidi ya bilioni tano zinatenga asilimia zaidi 50 kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Kwa hiyo, unachozungumza kama Handeni milioni 700 asilimia ishirini tu zitaingia kwenye maendeleo, lakini zingine zote ziingie kwenye OC. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Nhamanilo unaipokea hiyo taarifa hiyo?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, namuheshimu sana mzee wangu, kama amenisadia nashukuru sana unajua nina moto hapa. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nimepokea taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Reuben, unaipokea taarifa ya Mheshimiwa Isack Kamwelwe?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ninaipokea taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachokisema tusiwe waumini wa vyanzo vya mapato, tunachotakiwa ni kutengeneza district economic profiles na siyo hizi ambazo mmeweka kwenye website eti district economic profile inaongelea tu watu, eti kuna watu idadi kadhaa, idadi kadhaa tengenezeni district profiles ambazo zinaangalia potentials za eneo husika ili mjue ni mradi gani mkiwapelekea unawa-boost. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunacho Chuo cha Mipango, Mheshimiwa Waziri wa Fedha upo, chuo hicho mnacho wenyewe kwa nini makitumii kupanga? Kwa nini hamkitumii kutengeneza hizi Districts profile kwa ajili ya kuangalia potentials za uchumi wa kila eneo ili tupeleke fedha maeneo hayo kwenye miradi hii ya kimkakati tuka- boost eneo lile? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninatamani sana na ninashauri kwenye maazimio yetu tuongezee azimio, ikiwa tu hii miradi ya kimkakati ambayo Serikali imekuwa ikiiendesha miaka yote hawakuwa hata na mWongozo mpaka leo, na yenyewe ni ya bilioni kama 200 na kitu, je, itakuwaje kwenye huu mtadi mkubwa wa TACTIC ambao ni wa karibu bilioni 600? Wanauendeshaje? Ile tu ya kujenga soko, stendi, hapa na pale hawakuwa hata na mwongozo, huu mkubwa! Ni nani aliyewaambia kwamba, hii first tire inatakiwa iwe hii Miji, kwa nini isiwe Handeni na sehemu nyingine? Tuweke azimio la kwamba mradi huu wa TACTIC ukapitiwe upya na upangwe kulingana na namna ambavyo Halmashauri zinazohitaji kusaidiwa kwa uharaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ambalo ningependa nimalizie…

SPIKA: Sekunde 30, malizia.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ambalo ningependa nimalizie ni hapohapo kwenye kuangalia sera za kikodi kulingana na eneo husika. Kwa mfano, Tanga tunalima mkonge, kwa nini isiwekwe sera ya kikodi kuliendeleza eneo la Tanga kwenye uzalishaji wa mkonge? Mathalani, Mwekezaji yeyote atakayewekeza Tanga ndani ya miaka hii 20 hatatozwa corporate tax. Eeh! ni mfano tu, si watu wote wataenda ku-flock huko? Kwa mfano, Katavi unasema Mwekezaji yeyote atakayejenga hoteli corporate tax yake tutamtoza tano siyo kwamba watu watapeleka hoteli huko? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama watu wa Serikali wamechoka kufikiria wapishe hizo siti wakalie watu wengine wafikirie. Baada ya kuyasema haya nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi/Kicheko)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi nichangie Kamati zetu mbili zilizowasilisha hapa leo, Kamati yetu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na Kamati yetu ya Bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia upande wa taarifa iliyowasilishwa na Kamati yetu ya Bajeti na hususan ukurasa wa 62 wa taarifa, kipengele kile cha 6.5. Kamati inazungumzia ujenzi wa barabara kwa mfumo wa uhandisi, usanifu, manunuzi, ujenzi na utafutaji wa fedha kwa maana ya EPC+F. Ninaishukuru sana Serikali kwamba katika mpango huu ipo barabara maarufu ya Handeni - Kibilashi - Kiteto - Kondoa - Singida ambayo nayo imebahatika kuingia humo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na barabara hizi tunazozijenga, lipo jambo moja la ajabu sana tunalifanya kama Taifa. Nchi yetu ina mtandao wa barabara wenye thamani inazofikia Shilingi Trilioni 21. Barabara za kitaifa zina kilometa 36,361 na zina thamani ya Shilingi Trilioni 18. Barabara zetu za Wilaya zina mtandao wa kilometa 143,881 zenye thamani ya Shilingi Trilioni 2.8.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kushangaza pamoja na kuwa na asset hii kubwa ya kitaifa inayosaidia uchumi wetu, hatuifanyii matengenezo. Hivi sasa barabara zetu za kitaifa zile kubwa na ambazo ndiyo mrija wa uchumi wetu zinahitaji matengenezo yanayokaribia Shilingi Trilioni 2.4 na Serikali imekuwa ikija hapa inadai haina fedha hizo za kukarabati barabara hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili tusipoliangalia litakuja kutuingiza kwenye gharama kubwa na litakuja kufanya uchumi wetu udhoofu, wananchi wetu wasafiri kwa shida, mizigo isafiri kwa taabu, vilevile watu waliopo kwenye sekta ya uendeshaji ya usafirishaji wataendesha shughuli zao kwa gharama kubwa sana ya kununua vipuli kwa sababu ya barabara mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakupa mfano, athari ambazo zinaweza zikapatikana tukichelewa kufanya matengenezo ya barabara kwa kadri ya wataalam wanavyoelekeza. Miaka kadhaaa iliyopita tuliacha kufanya matengenezo ya barabara karibia 13, tukaziacha tu mwaka wa 11, 12 nyingine mpaka mwaka wa 20 tukaziacha. Matengenezo yale yalikuwa yagharimu Shilingi Bilioni 250, hatukufanya. Tulivyokuja kufanya, tumekuja kufanya matengenezo hayo kwa Shilingi Trilioni 1.28, ndiyo kusema tulikula hasara ya Shilingi Trilioni Moja nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sielewi kwanini Serikali inajivuta vuta na sielewi kwanini Serikali inajizungusha zungusha kukarabati barabara zetu hizi za kitaifa ambazo nakwenda kuzitaja hapa ziingie kwenye Hansard kwa kumbukumbu.

Barabara ya Kibaha - Mlandizi, Chalinze - Ngerengere, Melela - Iyovu, Igawa -Uyole, Uyole - Songwe, Mlandizi - Chalinze, Same - Himo, Himo - Arusha, Rusahunga - Rusumo, Shelui – Malendi - Nzega kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Nyanguge – Mwanza – Mara - Border, Makutano - Sirari, Usagara-Mwanza, Mtwara – Mingoyo - Masasi, Madaba - Makambako, Songea -Madaba, Ipole - Miemba, Rungwa - Ipole, Nzega - Manonga, Mwanza - Shinyanga - Usagara, Uyole - Kasumulu, Kobelo - Nyakasanza, Songea - Peramiho, Mikumi - Kidatu, Lupilo - Mahende na Himo -Marangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hizi ukikuta barabara ya chini ina umri wa miaka 17. Barabara yenye umri mkubwa katika hizi kuliko zote ina umri wa miaka 37. Kwa nini tunakuwa hivi? Yaani ni kweli kwamba hatuoni umuhimu kabisa wa kutafuta hii Shilingi Trilioni 2.4 tukafanya ukarabati wa barabara hizi? Mfuko wetu wa Bodi ya Barabara, kwa mwaka makusanyo yake ni kama Shilingi Trilioni moja. Vyanzo vyake vya mapato ni tozo za mafuta ambazo zina-constitute karibia asilimia 97 ya fedha zote wanazopata, tozo za magari ya kigeni na tozo za kuzidisha uzito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa vyanzo hivi havitatosha kukarabati barabara zetu na barabara ukiitengeneza leo ukaikarabati unaipa uhai mrefu mwingine wa kuishi. Kwa hiyo, ninaiomba sana Serikali na kwenye maazimio yetu kama Bunge tuweke maazimio kwamba Serikali lazima ije hapa na mapendekezo siku zijazo ya vyanzo vipya vingine vya mapato kwa ajili ya Bodi ya Mfuko wa Barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Barabara wanafikiria kutumia infrastructure bond kama sehemu mpya, nakubaliana nao ni chanzo kizuri, wanataka kwenda kutoza, kuweka tozo kwenye gesi asilia, kwenye yale magari ambayo yanatumia gesi asilia, siyo jambo baya. Wanataka kutoza kwenye toll bridge na wanataka kutumia hizi njia ya EPC+F.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba nilishukuru barabara ya Handeni – Kibilashi - Kiteto kwenda kwenye hii njia ya EPC+F, kuna haja kubwa kama nchi, huu mfumo tunaotaka kuuendea wa EPC+F tukaupitia upya. EPC+F ina- implication moja kwa moja kwenye Deni la Taifa. Kwa hiyo, ni vizuri Bunge lako likaambiwa, kwa mfano zile barabara Nane ambazo zimetajwa kwamba zinajengwa kwa EPC+F mpango huo umefikia wapi na implication yake itakuwaje? Watawezaje ku-spread hiyo? Kuliko tukawa tunakuja hapa kuwaaminisha wananchi barabara zinajengwa halafu hazijengwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema haya, nakushukuru sana, nilitamani kushauri eneo hilo, matengenezo ya barabara, Shilingi Trilioni 2.4, Serikali itoe maelezo na iweke kwenye mikakati yake kuja hapa na vyanzo vipya kwa ajili ya Bodi yetu ya Mfuko wa Barabara. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, moja kati ya maeneo ambayo yanahitaji sana kusaidiwa ni Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kwenye maelezo yao kwenye Kamati mbalimbali ambazo wamefika na kwa mujibu wa taarifa ya Kamati yetu ya Bunge inayosimamia Wizara hii ya Katiba na Sheria, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inahitaji ipewe fedha kwa ajili ya kwanza, mafunzo maalum kwenye maeneo ya Uandishi wa Sheria; Pili, kwenye eneo la masuala ya utawala; na Tatu, ni katika eneo la mikataba. Kwamba wanahitaji wapewe fedha kwa ajili ya mafunzo maalum kwenye hayo maeneo matatu niliyoyataja.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nisizungumzie hili la Uandishi wa Sheria na naomba pia nisizungumzie hili la masuala ya utawala, nataka nizungumzie hili la eneo la mikataba.

Mheshimiwa Spika, kutoiwezesha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kutoipatia fedha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ili wataalam wake wakapate mafunzo kwenye eneo hili la mkataba ni gharama kubwa sana kwa nchi yetu. Fedha ambazo walikuwa wameomba Milioni 300, kutokuwapa Milioni 300 ni gharama kubwa sana kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, wakati naendelea kuelezea nitatoa mfano kwa nini ni gharama sana kwa nchi yetu, kwa maana hiyo nimesimama hapa siyo tu kuchangia, lakini kulishawishi Bunge kwamba ni lazima tusimame kidete kuhakikisha kwamba Serikali inapeleka fedha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ajili ya kuwapeleka Wataalam wetu wajifunze mambo ya mikataba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tusipo-train watu wetu kwenye eneo hili la mikataba nchi yetu itashindwa kunufaika na rasilimali tulizonazo. Hivi sasa kama Taifa tunajielekeza kwenda kuwekeza kwenye LNG, tunajielekeza kwenda kuwekeza kwenye Uchumi wa Blue ambao ni Uchumi wa Bahari. Kote huku tutatakiwa kuingia mikataba mbalimbali, tusipoiwezesha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Sheria, tutaishia kuwa watazamaji na rasilimali zetu hatutanufaika nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano mmoja tu ili niijenge hoja yangu vizuri na Bunge hili liweze kunielewa kwa nini nasisitiza tupeleke fedha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Milioni 300 iliyokuwa imeombwa na majibu ya Serikali yamekuwa tu ni mepesi, eti ukomo wa bajeti umefikia hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano ninaotaka kuutoa ni kwamba, majuzi Serikali yetu iliingia mkataba na kampuni ya Baker Botts ya Uingereza kwa ajili ya kutusaidia ile Government Negotiation Team itakayopatikana, kwenye hili nimshukuru sana Mheshimiwa Rais na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kumteua Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi kuwa Mkuu wa Government Negotiation Teams ambazo zitakuwa zinatengenezwa. Sasa kampuni hii ya Baker Botts ikitufanyia kazi kwa miaka miwili tunailipa Dola Milioni Tatu na Nusu hiyo ni takriban Bilioni Nane ya kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunafanya hivyo kwa gharama tu ya kushindwa ku-train watu wetu! Umeombwa Milioni 300 unashindwa ku-allocate, halafu uko willing kulipa Bilioni Nane kwa kampuni moja kwa mkataba mmoja, this is ridiculous. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaingia mkataba wa aina hiyo tukiwa na facts hizi zifuatazo: Nchi yetu ina Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali toka mwaka 1961 miaka 60 sasa; Nchi yetu imeshakuwa na Geology Department kwenye University of Dar es Salaam toka mwaka 1974 which means tuna wataalam wa geology, tuna wataalam wa mambo ya Oil and Gas na ambao pengine hawapo nchini kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, nilibahatika wakati mmoja kwenda Texas - Marekani nikakutana na Watanzania wengi sana wenye utaalam wa mambo ya Gas and Oil, sasa tunapoingia mikataba hii halafu kwa kisingizio tu cha kusema eti hatuna wataalam! Tusiwe tunajiangalia kwenye Wizara za Serikali kwamba kama hatuna mtaalam ndiyo tuna- assume nchi nzima haina wataalam. Tujengeni utamaduni wa kuwatumia watanzania wenzetu ambao wana ujuzi hata kama wako nje ya nchi, we can access them! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naongea haya tumeingia mkataba huu tukiwa na TPDC, Shirika ambalo lina wataalam wa Oil and Gas, Shirika lipo toka mwaka 1969, lina miaka 53 tunaongelea jambo hili tukiwa tunayo Faculty of Law ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambayo ilianza hata chuo chenyewe kabla hakijaanza mwaka 1961, ina miaka 61.

Mheshimiwa Spika, wataalam wote hawa tunao wamefika mpaka level ya PhD, eti leo kwenye mkataba Watanzania hatuwezi kusimama kusema mpaka tutafute mtu atusemee, atufundishe cha kusema, atufundishe ku-negotiate, ilihali tuna wataalam wa kwetu! Tunalipa fedha halafu tumeacha kupeleka halafu tumeacha kupeleka bajeti kwa wataalam wetu kuwa-enhance what is this? Tumuungeni mkono Mheshimiwa Rais yeye ameshaonyesha njia nasi wasaidizi wake twendeni tumuunge mkono.

Mheshimiwa Spika, naomba niishie hapa, nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii angalau ya dakika chache nami niweze kuzungumzia mambo ya maji Jimboni kwangu Handeni Mjini.

Mheshimiwa Spika, mara ya mwisho wananchi wa Handeni Mjini kupata mradi wa maji ilikuwa ni mwaka 1974, na mradi ule ulikuwa ni wa miaka 20 life span yake. Hiyo ndiyo kusema kwamba tuna miaka karibia 30 wananchi wa Handeni hatujawahi kupata mradi mkubwa wa maji. Sasa nimesimama hapa leo kutoa shukrani zangu nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Rais wa Awamu ya Sita kwa namna ambavyo ameiangalia Handeni kwa jicho la kipekee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kutoa shukrani hizo kwa kaka yangu, ndugu yangu, Waziri wa Maji, Mheshimiwa Aweso pamoja na Naibu wake, na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Eng. Sanga. Niendelee kusema kwamba Wizara hii ya Maji kwa sababu inagusa matatizo makubwa sana ya Watanzania, kwa kweli inastahili kuwa na watu wa aina ya viongozi tulionao hapo kwenye hiyo Wizara. Ingekuwa ni kwa uwezo wangu, na kwa sababu sisi ndio washauri wa Serikali, tunashauri Waziri huyu aendelee kuwepo kuwepo pale aendelee kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwa mara ya kwanza wananchi wa Kata ya Kwamagome, wamepata mradi pale Kwamagome unaopeleka maji Kwamagome na Hedi. Kana kwamba haitoshi, nilipokwenda Ofisini Wizarani, tumeongezwa fedha ili wananchi wa Lusanga, Sasioni, Lolopili na Mji mpya nao wapate maji. Nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa usikivu wako.

Mheshimiwa Spika, nashukuru zaidi kwa mara ya kwanza kwa historia ya nchi yetu Kata ya Malezi wamepata mradi wa maji wa Shilingi 324,000,000/=. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuomba katika kipindi hiki, Mheshimiwa Waziri mradi huu natamani sana tukauzindue kwa pamoja, twende pamoja tukauzindue na ule mradi wa Mabanda ambao wewe siku ile ulipokuja, usiku ule tulipokunywa maji pale, ulipiga simu tukiwa pamoja kwa Mheshimiwa Rais na usiku ule ule alikubali kutoa shilingi 671,000,000 ambazo zimejenga tenki kubwa sana pale Mankinda. Tunapeleka maji kata yote ya Mabanda na tunapeleka maji Kijiji cha Mankinda Kata ya Konje na tunayapeleka maji pale Wanyamakazi. Nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kata ya Kojamba tulipata Shilingi bilioni 1.96 ili kuchimba bwawa kubwa pale Kwinkambala, mkandarasi akatuzingua na sisi tukamzingua mara nne yake. Hivi ninavyozungumza, mkandarasi alishafukuzwa. Nitoe wito kwa Wabunge wenzangu, Mkandarasi akizingua site, tusingoje Serikali. Sisi wananchi tuna mamlaka ya kuwakataa wakandarasi ya ovyo ovyo. Kwa hiyo, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri, ulikuja pale na umeshaweka utaratibu ndani ya wiki mbili kama ulivyoahidi kwamba tunakwenda kupata mkandarasi mwingine pale Kwinkambala. Kwa maana hiyo bado umeendelea kutusikiliza wananchi wa Handeni Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ametupa mradi wa shilingi 857,000,000, kinachimbwa kisima kikubwa pale Ndelema kuyapeleka maji Kwinkambala wakati tukiendelea kusubiri ujenzi wa Bwawa kubwa lile la Kwinkambala.

Mheshimiwa Spika, zaidi naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kufanikisha mradi huu wa miji 28. Mradi huu umezungumzwa hapa Bungeni kwa takribani miaka sita iliyopita. Wito wangu kwenye mradi huu, dola milioni 500 mkopo tunaochukua Serikali ya India, Benki ya Exim, miaka sita iliyopita milioni 500 ingeweza kufanya kazi kubwa zaidi kuliko leo. Kwa hiyo, kama process za mradi huu zimeshakamilika, chonde chonde mradi uanze.

Mheshimiwa Spika, mwisho nimalizie, Waswahili wanasema kushukuru ni kuomba tena. Wananchi wa Handeni Mjini wamenituma niombe tujengewe bwawa pale Mandela Kata ya Kwenjugo, pia tujengewe bwawa pale Kata ya Mabanda Bwawa la Kwamkole. Tukishakuwa na Bwawa na Kwinkambala tukawa na Bwawa la Mandela na tukawa na Bwawa Kwamkole, tafsiri yake ni kwamba tutakuwa na source nyingi za maji kwa Jimbo letu la Handeni mjini plus haya maji ambayo yanatoka kwenye huu mradi wa HTM yanayotoka Mto Ruvu kule Pangani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo napenda nitoe shukrani za dhati kwa Engineer Yohana Mgaza, Meneja wa HTM. Vile vile nitoe pongezi zangu za dhati kwa Engineer Hosea Mwingizi. Mheshimiwa Waziri hawa watu naomba wasihamishwe Handeni, wawepo waweze kutusaidia kwenye haya mapambano ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya, nakushukuru sana kwa fursa hii. Ahsante sana, wananchi wa Handeni wakae mkao wa kula, tunakwenda kuiandika historia ya Handeni Mjini kupitia uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan na ndugu yangu Waziri Aweso.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwenye tovuti ya Wizara ya Fedha, upo mwongozo wa maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali, mwaka 2023/2024. Mwongozo huu wenzetu wa TAMISEMI walikutana kati ya tarehe 17 mpaka 21 kuujadili na kuona namna ya kuutekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mengine, wamezigawa Halmashauri zetu katika makundi manne. Kundi la kwanza ni kundi ambalo ziko Halmashauri tisa. Halmashauri hizi tisa zimewekwa kwenye kundi la kupeleka asilimia 70 ya mapato yasiyolindwa kwenye maendeleo. Kundi la pili, lina Halmashauri 17. Kundi hili limepangiwa kupeleka asilimia 60 ya mapato yasiyolindwa kwenye maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kundi la tatu lina Halmashauri 102. Kundi hili limepangiwa kupeleka asilimia 40 ya mapato yasiyolindwa kwenye maendeleo na kundi la tatu ambalo ndiyo kundi la Halmashauri ya Handeni Mjini iliyopo, kundi hili lina Halmashauri 56 ikiwemo na Korogwe na Halmashauri nyingine nyingi ambazo ningekuwa na muda ningezitaja. Halmashauri 56 zenyewe zimepangiwa kupeleka asilimia 20 tu ya mapato yasiyolindwa kwenda kwenye maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri ya jambo hili ni nini? Jambo hili linapeleka umasikini kwa wananchi wote waliopo kwenye Halmashauri hizi. Jambo hili, literally, halikubaliki! Ukisema kwamba makusanyo yetu ya ndani yasiyolindwa asilimia 20 tu ndiyo iende kwenye maendeleo, tafsiri yake ni kwamba, kwanza tutawa-discourage walipa kodi. Mlipa kodi anataka akilipa kodi yake, ushuru ukikusanywa, aone haspitali pale, kituo cha afya kimejengwa, aone madarasa yanajengwa kwa fedha anayokusanya. Sasa tukiwa tunakusanya halafu asilimia 80 yote tunaenda kuinywa chai, tunaenda kuitumia kwenye mafuta kwa ajili ya usimamizi, hii haitakuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itatusababishia matatizo kwa sababu, mbali na kuwa-discourage walipa kodi, wanufaika wetu wa asilimia 10 zile tunazokopesha; tulipokuwa tunatenga asilimia 40 tulikuwa tunapeleka asilimia 10 kuwakopesha wananchi, kuwakopesha akinamama, vijana na walemavu, lakini ukitenga asilimia 20 inamaanisha hata hiyo fedha ambayo unawapelekea inapungua, wanufaika watakuwa wachache. Tafsiri yake ni kwamba, tunatengeneza nchi yenye matabaka makubwa. Wale wenzetu ambao wamepangiwa kupeleka fedha nyingi kwenye maendeleo, ndiyo na fedha zao za kuwawezesha wananchi wao zitakuwa nyingi, lakini na miradi watakayoitekeleza kwenye maendeleo ni mingi kuliko ambavyo sisi tutatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kufanya hivi halafu eti wao TAMISEMI wanasema, tukishaondolewa zile asilimia 20 tukabaki kwenye 20 ya fedha za maendeleo, eti watalipa madeni ya watumishi wasiokuwa walimu. Ukimlipa madeni mtumishi, huo ni wajibu wako, na ni jambo zuri kufanya. Wanasema wataleta stahiki kwa Wakuu wa Idara; huo ni wajibu wenu na ni jambo zuri kufanya. Nasema ni wajibu wenu kwa sababu, vyanzo vyote vya mapato kwenye Halmashauri mmevichukua nyie, kwa hiyo, mna wajibu wa kufanya haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisema mtaongeza OC proper, vyote hivyo unavyoviongea vinaenda tu kusaidia uendeshaji wa Halmashauri, lakini ikiwa sisi tulikuwa tunatumia mapato ya ndani kujenga zahanati pale kwenye Zando mwaka juzi, 2021; mwaka jana 2022 tukajenga zahanati Mankinda kwa fedha za ndani, na mwaka huu 2023 tumejenga pale Bangu zahanati kwa fedha za ndani; na tulikuwa tunatarajia kwenye mwaka huu wa fedha tunaopitisha bajeti tukajenge zahanati kule Kwalubaka. Sasa nyie mmechukua fedha zote, tunawaambieni sasa: Je, mtatuletea fedha ili tujenge zahanati hizi ambazo… (Makofi)

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka wapi? Haya Mheshimiwa pale.

T A A R I F A

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nataka kumwongezea taarifa Mheshimiwa anayezungumza kwamba, TAMISEMI kuzisaidia hizi Halmashauri ambazo amezipunguzia asilimia 40 kwenda asilimia 20, ni kuhakikisha wanapeleka miradi ya kimkakati ili kupandisha mapato kwenye hizi Halmashauri au kama hizo Halmashauri zilishatengewa miradi ya kimkakati, ikamilike ili kuzisaidia kupandisha Halmashauri hizo, siyo kutoa hizo asilimia 40. Tutasaidiaje wananchi wetu?

MWENYEKITI: Mheshimiwa ni taarifa au ni swali?

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni taarifa nilikuwa namwongezea Mheshimiwa anayeongea.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Reuben unaipokea Taarifa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa ya Mbunge aliyetoka kunipa taarifa ambaye anatokea Momba, na Halmashauri yake ni miongoni mwa Halmashauri ambazo zimetengwa ili ziingie kwenye asilimia 20 na fedha zote ziende kwenye matumizi ya kawaida badala ya kwenda kwenye matumizi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema aliyenipa taarifa, Halmashauri hizi lazima tuje na mpango wa kuzisaidia. Suala siyo kuzifanya ziwe likizo ya maendeleo. Hatuwezi kuzipa likizo ya maendeleo, eti wawe wanakusanya asilimia 80 yote wanakula, 20 ndiyo inaenda kwenye maendeleo. Hii siyo sawa! Hii haikubaliki!

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi yote ya kimkakati mmewapelekea ma-giants. Ukija kwenye mradi wa TACTIC; tier one ya TACTIC iko na ma-giants, majiji makubwa. Tier two ya TACTIC iko na ma-giants majiji makubwa, halafu tier three ndiyo tuko sisi wachovu ambao ndiyo tena mnatunyang’anya na mapato, halafu na tier three yenyewe hamuitekelezi. Hii siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu mnapanga wapi? Huu ni utafiti wa wapi mmefanya? Nataka niwakumbushe, ukisoma Five Years Development Plan tuliyonayo ukurasa wa 12, inasema: “The aim of the fifth phase Government was to increase development spending to the tune of 30 - 40 percent.” Huu mpango tuliujadili hapa, tukaupitisha hapa, nyie mnawezaje kujifungia chumbani na kubadilisha bila kuja kutuambia hapa? Yaani mnawezaje kufanya hivyo? Yaani Halmashauri zote 56 zi-paralyze tu kwa sababu nyie mmeamua? Hii siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri atakapokuja kufanya hitimisho hapa atuambie, sisi wa Handeni, pamoja na Halmashauri nyingine nyingi kama ilivyo Mpumbwe, Kasulu, Handeni TC, Nyang’hwale, Nzega, Mpama, Iramba, Ikungi, Longido, Namtumbo na maeneo mengine, mta-compensate vipi kwenye hii fedha tuliyokuwa tunapeleka kwenye maendeleo? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ili nichangie Wizara yetu hii ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara. Mimi ni mmoja wa Wabunge wanaotokea Mkoa Tanga, kwenye hili suala la Kiwanda cha Tanga Cement nafikiri Mheshimiwa Tauhida ameliweka vizuri sana. Naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Tauhida kwamba Serikali inao wajibu ya kutoa ufafanuzi kwa wananchi wapate kulielewa, lakini zaidi taratibu za kisheria ni za muhimu kufuatwa kwa sababu ndio misingi tuliowekeana kama nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichangie kwamba, Wizara yetu hii kwenye suala zima la uwekezaji. Tunao Watanzania ambao ni wawekezaji ndani ya nchi yetu, lakini vile vile tunao wawekezaji ambao sio Watanzania ambao wamekuja kuwekeza ndani ya Tanzania. Sasa nimesoma Hotuba ya Mheshimiwa Waziri inaonyesha pana mapitio mengi ya kisera yanafanyika na pana mapitio mengi pia ya kisheria yanafanyika ili kuboresha mazingira ya uwekezaji nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala hili la uwekezaji ni bahati mbaya sana kama nchi tumekuwa na mtazamo wa outward looking, yaani kila sheria na kila sera tunapojaribu kuileta ya uwekezaji inamwangalia na kumlinda zaidi mwekezaji kutoka nje na inamwangalia kidogo sana mwekezaji ambaye ni Mtanzania. Mwaka jana hapa, nitatolea mfano, tumepitisha Sheria mpya ya Uwekezaji, fikiria ni sheria mpya hii, hata miezi sita haijamaliza, lakini sheria ile ilitoa fursa kwamba ili mwekezaji aweze kupata incentives, aweze kupata vitu vyote vya misamaha ya kikodi na vivutio vya kiuwekezaji akiwa ni Mtanzania, lazima awe na mtaji wa dola laki moja. Akiwa ni mtu kutoka nje anatakiwa awe na dola laki tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaposema dola laki moja kwa Mtanzania ndio aweze kupata incentives, vivutio vya kuwekeza, unaongelea zaidi ya milioni 200 na kitu za Tanzania. Sasa unawaweka wapi Watanzania ambao wana mitaji ya milioni 150, 170, 180. Ndio kusema kwamba sheria hii wao haiwapi fursa ya kuitwa wawekezaji ndani ya nchi yao, wala ya kupata upendeleo na vivutio kama ambavyo mtu kutoka nje anapata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo wenzetu wa Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji lazima sera hizo wanazozifanyia mapitio zije zikimtazama Mtanzania, mwekezaji wa ndani, mzawa, ili aweze kunufaika na uwekezaji ndani ya nchi yake. Nasema hivyo kwa sababu hata Bunge hili ambalo tumekaa hapa kesho kutwa bajeti ikija kusomwa, maeneo mengi ambayo tutakuwa tumetaja yameongeza kodi ni yale yanayoenda kuwaathiri Watanzania wawekezaji ndani ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepambana sana hapa Bungeni kubadilisha sheria pale TIC ili kwamba mwekezaji akitoka nje akiingia ndani ya jengo mmoja apate vitu vyote ndani ya jengo hilo. Kuanzia usajili, kila kitu mpaka anatoka pale na leseni yake ya biashara, anakwenda kufanya biashara, lakini wafanyabiashara wetu wa ndani ambao ndio Watanzania, wawekezaji wa ndani, hatujawapa jicho hilo. Yeye akitaka kuanza kufanya biashara anazunguka, anazunguka mitaa yote mpaka viatu vinakwenda upande hajasajili biashara na hao ndio walio wengi na ndio Watanzania wenye nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hizi sera wanazosema wanazifanyia mapitio ambazo wamezitaja kwenye hotuba yao, ni vyema zikaja na jicho la kumwangalia Mtanzania mwekezaji wa ndani. Mwekezaji wa nje akiingia na huu mtaji wake wa laki tano kwanza kuna wakati anapewa likizo ya kodi, hata miaka mitatu wanaita grace period, lakini hata vifaa anavyonunua vinasamehewa kodi. Nitatolea mfano wa wachimbaji wadogo, mchimbaji wetu mdogo kwa mfano akisema anaagiza grader leo hapa, lazima wataligonga VAT, lakini wale wachimbaji wakubwa waliopo hapa anaagiza yale ma-grader yanaingia bure, anaagiza mpaka magari yanaingia bure na anapewa na msamaha wa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hii haiwezi kuwa sawa. Hatuwezi kuwa na nchi ambayo hatuwajengi Watanzania wenyewe kuwa wawekezaji ndani ya nchi yao. Halafu mbaya zaidi mwekezaji huyu mkubwa wa nje ambaye tunamkimbilia na kuwaacha wa kwetu, sheria hii ambayo tuliitunga hapa inampa free repatriation of profit ambapo faida hii angepata mwekezaji Mtanzania ingebaki hapa hapa. Kwa hiyo ni ushauri wangu kwamba wawekezaji wazawa wa Tanzania ifike mahali kama tunavyotaka kuangalia kwa jicho la pili na kwa jicho la ukaribu wawekezaji wa nje ndio hivyo hivyo tunatakiwa tuwaangalie hawa wawekezaji waliopo ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, langu lilikuwa ni hilo, nashukuru sana kwa fursa hii, shukrani sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa na mimi niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara yetu muhimu ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja katika maeneo ambayo Serikali ya CCM imefanya mapinduzi makubwa ni eneo hili la afya. Mapinduzi haya yaliyofanyika ya kuleta miundombinu vikiwemo vituo vya afya, zahanati, Hospitali za Rufaa za Kanda, Mikoa yamesababisha tuwe na changamoto. Kwa hiyo, wajibu wetu sisi ni kuishauri Serikali hii namna ya kutatua changamoto hizi ili mafanikio haya ambayo tumeyapata yasigeuke kuwa laana.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nitaongelea jambo moja tu ili kuishauri Serikali, jambo la dawa. Mwaka jana nilisimama hapa nikazungumzia kuhusu MSD, ninaipongeza sana Serikali kwamba ilichukua hatua thabiti na bado inaonesha dhamira ya kuleta mabadiliko kwenye Sheria ya Manunuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pale MSD nataka leo tupaangazie upande wa pili, tuuache ule wa MSD tuangazie upande wa pili wa mfumo wetu wa dawa. MSD pana miradi Minne ya kununua dawa. Mradi wa kwanza ni ununuzi wa vifaa na vifaatiba vya huduma za dharura, mradi wa pili ni ule wa mapambano dhidi ya Covid-19, mradi wa tatu ni utekelezaji wa mradi wa mfuko wa dunia na mradi wa Nne ambao ndiyo mimi leo nataka kuuzungumzia ni ule wa fedha zinazolipwa kutoka kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, iko hivi hospitali zetu kwa maana ya Madaktari wetu wa Wilaya, Halmashauri zetu zinapoweka oda kununua dawa MSD uzoefu unaonesha kwamba wakiweka oda ya dawa 10 MSD wanapata Nne, Sita hawazipati. Uzoefu unaonesha kwamba wakitoa oda ya dawa 100 pale MSD wanapata dawa 40, 60 hawazipati, huo ni uzoefu na ndiyo takwimu zilivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa upo mwongozo kwamba zile dawa ambazo Halmashauri zetu zikiweka oda MSD, dawa ikikosekana mwongozo unawataka wataalamu wetu na hospitali zetu zikanunue dawa kwa prime vendors (washitiri). Sasa hili la washitiri ndiyo mimi nataka tulijadili. Mimi hili la washitiri naliona ni tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni tatizo kwa sababu gani, kwanza nitoe takwimu Halmashauri ya Handeni Mjini mwaka 2021/2022 MSD tulinunua dawa za milioni 40 tu, lakini kwa washitiri tulipeleka milioni 60. Mwaka huu wa fedha mpaka as of 31st March MSD tumepeleka milioni 55 kununua dawa lakini kwa washitiri tumepeleka milioni 61.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ndiyo kusema nini? Fedha zetu nyingi za dawa kwenye Halmashauri zetu zinakwenda kwa washitiri. Kwa hiyo, tusipopaboresha hapa kwenye huu mfumo wa washitiri hili tatizo la ukosefu wa dawa tutaendelea kuwa nalo la ukosefu wa dawa.

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini ni tatizo kwa washitiri?

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa msemaji anaongea vizuri sana. Tatizo lililopo MSD hana fedha ya kununua dawa na kuzihifadhi ili anapopata oda kutoka kwenye Halmashauri aweze ku- deliver on time. Halmashauri wanapomkuta MSD hana dawa inawabidi waende wakanunue kwa mshitiri na ndiyo maana tumeomba katika taarifa MSD apewe mtaji awe na dawa ili huyu anapopata order apelike palepale. Ahsante sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Reuben uanipokea taarifa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni mwanamapinduzi, lazima tufanye mapinduzi. Washitiri ni tatizo, na matatizo nayaeleza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza wakienda kununua dawa kwa mshitiri, bei wanayotuuzia washitiri ni kubwa kuliko ambavyo tungenunua MSD. Ni kubwa! Last time nilitaja figures hapa watu wakashangaa, kwa habari ya kidonge cha shilingi milioni nne kununuliwa kwa shilingi milioni 200 na kitu. Leo sitaji figures, nasema tu kwa ujumla, kwamba, tukienda kununua kwa washitiri, bei tunayonunua ni kubwa kuliko ambayo tungenunua MSD, la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, tatizo kubwa ni kwamba, wale washitiri bei wanazotuuzia ni kubwa kuliko za wholesellers wetu wanaopatikana hapa nchini. Ni kana kwamba haitoshi, hata uki-order leo dawa, au kifaa tiba kinaweza kikamaliza mwaka hakijaletwa. Hii siyo sawa. Tuondokane na hii habari ya washitiri. Sasa wenzetu wa Wizara ya Afya wanayo mawazo, wanafikiri kwamba, badala ya kuweka mshitiri mmoja kwenye Mkoa mzima, waweke hata wanne. Hiyo haiwezi kuwa solution namna mlivyofikiria, kwa sababu nyie mnataka wawepo wanne, lakini wa- specialize kwamba huyu awe analeta hivi, huyu alete hivi, huyu alete hivi. Hapo hapatakuwa na ushindani. Kama bado mna idea ya kuwa na washitiri, ruhusuni wawepo washitiri washindanishe bei ili tusiwe tunalanguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaongea hivi kwa sababu Mheshimiwa Rais anapeleka fedha nyingi sana. Sikilizeni niwaambie, bajeti ambayo MSD wanaihitaji ni kama shilingi bilioni 592 tu, lakini miezi sita tu iliyopita MSD wamefanya manunuzi ya zaidi ya shilingi bilioni 257. Hizi zinazonunuliwa na MSD zikiwa managed vizuri, na hizi tunazonunua Halmashauri, zikiwa managed vizuri, dawa zinatosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachofanyika ni kwamba tunanunua bei mara tatu mara nne ya bei halisi. Haitakiwi kuwa hivi, kwa sababu tukifanya hivyo, wananchi wa wa Kwedizandu watapata lini dawa? Wananchi wa Kwalwala, Kwasindi, Kwabaya; haya majina ninayoyataja siyo ya Kongo, ni ya Handeni Mjini msiojua. Wananchi wa Kwedi, kule kwa Magono, hawawezi kupata dawa tukiwa na mpango huu. Kwa hiyo, twendeni tukafanye mapinduzi kwenye huu mfumo wa washitiri tuuangalie upya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, dada yangu Mheshimiwa Waziri namwamini sana, ni mchapa kazi mzuri, ana wasaidizi wazuri, ana wataalam wazuri wamemzunguka, twendeni tukakae chini, tufikirie namna ya kuisaidia MSD. Hii habari ya kukosa dawa wakati tuna fedha, kwa sababu dawa inapoagizwa, ikachelewa kuja kwa miezi tisa, kwa mwaka wakati fedha tunazo, huu ni umasikini mkubwa kabisa wa namna ya kuyatazama mambo. Hivi, huwa najiuliza kila siku, kama magari yanaweza yakaletwa Dar es Salaam, tukawa na bounded warehouse, yako hapo yamekaa, inashindikana nini kwa dawa tukawa na bounded warehouse za dawa?

Mheshimiwa Naibu Spika, asije mtu akachukulia kwamba habari ya bounded warehouse, naongelea godown, dawa zina utaratibu wake wa kutunza, ndiyo naongelea hivyo. Hayo maeneo ya kuhifadhi dawa, kwa nini tusiongee na wazalishaji, order tunazijua, maoteo ya vituo vyetu vya afya yote tunayajua. Tena katika eneo ambalo mnatakiwa mkaboreshe ni namna ya maoteo ya dawa yanavyofanyika, haya ndiyo yanayopelekea dawa zichomwe. Tunaagiza zaidi ya tunavyotumia, tuna-spend fedha nyingi zaidi ya tunavyotumia. Kwa ujumla kinachofanyika hapa ni mismanagement. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wataalam wetu msaidieni Waziri wetu, isije ikafika mahali tukisimama hapa ionekane tunaisema Serikali, tunawasema watu; tunawasema nyie wataalam, tunashindwaje kuji-organize? Fedha zinapoteapotea tu, tumelipa huku, tumelipa huku, nyingine zimechomwa, haiwezi kuwa nchi ya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nahoji tena, kwa nini tusiwe na bounded warehouses za dawa na za vifaa tiba, kwamba mzalishaji akizalisha Urusi aje ahifadhi hapa Tanzania, mzalishaji akizalisha Ujerumani, aje ahifadhi hapa Tanzania ili MSD iki-place order saa mbili asubuhi, saa saba mchana dawa zimeshafika. Nini kinashindikana? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii adhimu ili na mimi nipate kuchangia kwa niaba ya wananchi wa Handeni Mjini kwenye Wizara hii muhimu ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, Ilani yetu ya Uchaguzi ukurasa wa 11, ukisoma kile kipengere cha 67(a), sitakinukuu lakini nitataja kilichoelekezwa kwa sababu ya muda. Ilani inatuelekeza ifikapo 2025 tunatakiwa tuweze kuingiza fedha zinazotokana na Utalii dola za Kimarekani bilioni sita au fedha za Kitanzania karibia trilioni 14 ndani ya miaka mitano ifikapo 2025.

Mheshimiwa Spika, vilevile Ilani inatuelekeza ifikapo mwaka huu wa 2025 nchi yetu iwe imepokea au imepata Watalii milioni tano. Hali ikoje kwa sasa? Hali ilivyo kwa sasa mpaka Aprili 14 taarifa ya Serikali inaonesha kwamba tulikuwa na watalii 1,412,719 pungufu ya lengo kwa 3,500,000. Wakati huohuo inaonyesha tulikuwa tumeoingiza fedha bilioni za Kitanzania 288 ambayo hiyo ni asilimia kidogo sana ukilinganisha na lengo la bilioni sita kwa maana ya trilioni 14. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, takwimu zetu hizi wenzetu wa Maliasili hizi za kusema wanazo 1, 412,719 wanazipataje? Watalii wa Ndani kwenye hiyo 1,400,000 wako 718,299, watalii wa nje na hapa nimpongeze Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake binafsi naomba mninukuu hilo vizuri kwa juhudi zake binafsi za kufanya tukio kubwa lile la Royal Tour na kuwavuta watalii kuja hapa Tanzania, watalii 694,420. Kwa hiyo, watalii 694,420 wameletwa na Mheshimiwa Rais kwa sababu ya Royal Tour hawa wa ndani 718,000 ndio nataka nizungumzia takwimu wanaziptaje hizi.

Mheshimiwa Spika, ni jambo la kusikitisha sana, eti hata mtu akipanda basi anatoka Arusha kupitia Momera kwenda vijijini anahesabiwa ni mtalii, akipanda basi kutoka Bagamoyo au gari binafsi kupitia Saadani, Pangani yaani mimi Kwagilwa naenda Handeni nataka nipite Tanga Mjini niende msibani nahesabiwa ni mtalii.

Mheshimiwa Spika, mtu akipanda basi kutoka Arusha akapita Serengeti Ngorongoro anaenda zake Musoma anaenda kuoa huko, anaenda zake Musoma anaenda kutibiwa, anaenda zake Tarime mahindi yake yameliwa na ng’ombe anawahi, anaenda zake Mwanza anahesabiwa ni mtalii, halafu tunakuja hapa tunasema tuna watalii 1,412,000! Nimesema nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuwaleta hawa 694,420, ninyi mnafanya kazi gani watalii wa kwenu wako wapi? maana hao miongoni mwao ni wasafiri, ni watu wanatoka Dar es salaam wamepanda treni ya TAZARA wanapita Morogoro wanaenda zao Mbeya mnahesabu watalii.

Mheshimiwa Spika, mtalifikiaje lengo la watalii milioni tano, mtalifikiaje lengo! Mtalifikiaje lengo hilo? Sikilizeni niwaambie ni lazima mtekeleze wajibu wenu wa kumsaidia Mheshimiwa Rais, kwenye hii habari ya utalii lazima tufanye mambo yafuatayo badala ya kuwa mnakuja hapa na kutupa takwimu kwamba kuna watalii wa ndani laki saba kumbe mmehesabu na wafugaji ambao wanahamishwa kutoka Ngorongoro wanaenda Handeni wakipita getini mnawahesabu!

Jambo la kwanza la kufanya, ondoeni VAT kwenye Airline Industry. Sikilizeni niwaambie utalii ni export, tunafanya export of service ndiyo maana tunapata Dola katika kipindi ambacho dunia yote ina msukosuko kuhusu forex hatuna fedha za kigeni za kutosha, utalii sisi ndiyo ulitakiwa utulinde tupate fedha za kigeni, acha kuhesabu mtu anakwenda mnadani kuuza kondoo amepita getini unamhesabu.

Mheshimiwa Spika, fanyeni jitihada sekta hii ituokoe, ondoeni VAT kwenye Airline maeneo yafuatayo:-

Kwanza; kwenye Ndege. Kwenye Injini za Ndege, hizi injini zinauzwa gharama kubwa sana ukitoza VAT unafanya hilo jambo linakuwa la anasa, Kwa hiyo matokeo yake Airline Industry ya kwetu iliyo ndani haiwezi ku-compete regionally, ondoeni VAT kwenye spare parts za ndege, ondoeni VAT kwenye aircraft maintenance.

Mheshimiwa Spika, hizi ndege zinasaidia wawindaji kupekewa watalii wao kwenye vituo vya kuwindia, zinasaidia watalii kutoka eneo moja kwenda jingine, sasa leo mtu amekubebea watu anakuletea unamgonga VAT! tutapata wapi mapato? Mtafikaje bilioni sita kwa mwaka? Mtafikaje watalii milioni tano?

Pili; ondoeni VAT kwenye ada za vitalu. Mtu anapokuwa amelipia kitalu kwa mwaka, amelipa ile ada ya kwanza anakuwa amekilipia kwa miaka kumi ninyi hata ile fedha ambayo anawalipa kwa miaka inayofuata mnaipiga VAT 100 percent, that’s wrong! Ilani yetu ya Uchaguzi inasema nini? Tatizo hamsomi hiki kitabu kizuri. Ilani inasema fanyeni mapitio ya Sera, Sheria, Kanuni na Miongozo (c) ukurasa wa 112, Sheria ya VAT siyo msahafu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye Finance Bill, nataka tu nitoe taarifa kwamba nitashika shilingi leo kama Serikali haitaweka commitment kwenye Finance Bill inayokuja hii ili kuondoa VAT kwenye haya mambo ninayoyazungumza hapa. Tunataka fedha za kigeni, hatuwezi tukafika mahala, tutafika mahala tutashindwa hata kuagiza mafuta kwa sababu hatuna Dola, tutafika mahala viwanda vyetu vitashindwa kununua raw materials kwa sababu hatuna Dola lakini tuna nchi ambayo imejaliwa tuna kazi ya kuhesabiana tu mtu kapita anaenda Ngorongoro, mtu kapita anaenda msibani mnasema ni mtalii ameingiza nini cha forex. (Makofi)

Mwisho, watu wa mahoteli, watu wanaosafirisha kwenye tourism industry wanatozwa VAT mahala ambapo siyo sahihi kwa sababu tu ya ubovu wa sheria, ninyi watu wa maliasili na utalii hawa wanaondesha sekta ya utalii, private sector ni watu wenu, simameni muwatetee na ninyi msiwe sehemu ya kuungana kuwakandamiza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ondoeni VAT kwenye deposit. Sheria iliyopo ya VAT inasema hivi: The Value Added Tax imposed on taxable supply shall become payable at the earlier of (A) the time when an invoice of supply is issued; yaani mtu tu akipata mtalii kule nje akimwandikia tu invoice mnakuja mnataka VAT anaitoa wapi? Akakope? Halafu unasoma inasema: the time when consideration of supply is made yaani hata akilipa advance tu ambayo mtalii anakuja miezi sita baadae leo analipa kuwahi chumba analipa kuwahi ndege analipa, ninyi mnataka kodi we cannot work like that! Halafu we are very comfortable eti sheria iko hivyo! Sheria ni kitu gani kwani? Sheria inatungwa hapa! Kwa hiyo, tuondoeni hivi vitu. (Makofi)

MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Kwagilwa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Asya.

TAARIFA

MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji anayezungumza kuhusiana na wadau wa utalii hasa hawa wawekezaji wa tour industry.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala zima la hawa wadau kutozwa VAT kwa sababu wageni wanapokuwa nje ya nchi ni lazima wafanye advance booking kwenye mahoteli, hoteli Sheria ukiisoma ya Utalii, hawa watu wanalipa kodi (VAT) ni mwisho wa mwaka siyo kipindi kile ambacho mgeni ana-book, kwa hiyo asipotoshe.

SPIKA: Mheshimiwa umepokea taarifa hiyo?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, anasema napotosha siipokei taarifa, nataka nimwambie nimesimama hapa nimesema nasimama kuongea kwa wananchi wa Handeni Mjini watu werevu kabisa wanaelewa ninachofanya hapa ndani ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tufanye mapinduzi kwenye hii sekta ili tumuunge mkono Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, amefanya jitihada kubwa sana why are we lagging behind?

SPIKA: Mheshimiwa Kwagilwa muda wako umekwisha kengele ya pili ilishagonga, ahsante sana.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuchangia kwenye Wizara hii muhimu, Wizara ya Fedha. Mimi ni miongoni mwa Wajumbe wa Kamati yetu ya Bjeti, Kamati ambayo ina dhamana ya kuisimamia Wizara hii ya Fedha. Kwenye majukumu yetu pamoja na maeneo mengine tunasimamia Mafungu mbalimbali kwenye Wizara hii likiwemo Fungu la Hazina, Huduma za Mfuko wa Jamii, Idara ya Mhasibu Mkuu wa Serikali, Msajili wa Hazina, Deni la Serikali, Kitengo cha Kudhibiti Fedha Haramu, Tume ya Pamoja ya Fedha na Wizara ya Fedha yenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa leo nataka nizungumzie Fungu moja katika haya. Fungu namba sita, Idara ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali. Bajeti zetu hizi ambazo tumekuwa tukizijadili hapa mara tu baada ya kuzipitisha, Serikali inakwenda kutekeleza bajeti hizi na kule zinakokwenda jicho letu pekee ambalo tunalitegemea ni Wakaguzi Wakuu wa Ndani kwenye Halmashauri zetu lakini na kwenye Taasisi mbalimbali za Serikali zinazopokea fedha kutoka kwenye bajeti hii tunayopitisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana 2022/2023 kwa maana ya mwaka huu wa fedha unaokwisha. Fungu hili Na.6 kwa maana ya Idara ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali tulimpa fedha bilioni saba, milioni mia nane na themanini na tisa, laki moja na themanini na nne na mwaka huu tumempitishia bilioni tisa, imeongezeka kidogo na tunamshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuliwezesha Fungu hili kwa kuliongezea fedha ili likafanye kazi zake za ukaguzi. Tumewapa bilioni tisa, milioni mia tisa ishirini na saba na elfu nne.

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tukafanye mapinduzi kwenye Idara hii ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali ili jicho letu kwenye fedha za umma likaongezeke. Lazima tuifanyie mapinduzi idara hii ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali. Mapinduzi ya kwanza ambayo tunatakiwa tuyafanye ni ya kimuundo, lazima tubadilishe muundo. Nitatolea mfano, Wakaguzi wetu ambao wako kwenye halmashauri zetu wakishafanya ukaguzi wao, wakamwandikia Mkurugenzi, akajibu na Wakuu wake wa Idara, wakapeleka kwenye Kamati ya Ukaguzi na wakapeleka kwenye Kamati yao ya Fedha, ripoti yao moja kwa moja wakiiandika inakwenda straight kwa Idara ya Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa tafsiri yake ni nini? Tafsiri yake ni kwamba ukichukua ripoti zote za nchi nzima zikapelekwa moja kwa moja kwa mtu mmoja pamoja na kwamba ni taasisi, hawezi kuwa na uwezo wa kuyachakata yote na kutupa majibu. Hawezi kuwa na uwezo wa kuyachakata yote na kuchukua hatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachopendekeza na ninachoshauri hapa huu muundo lazima tuubadilishe. Lazima tuwe na Mkaguzi Mkuu wa Ndani ngazi ya Mkoa ili sasa wale wa Wilaya wakishachakata taarifa zao na kuziandikia, taarifa ikatue pale Mkoani. Ukishakuwa na Mkaguzi Mkuu wa Ndani kwenye kila Mkoa, definitely itakulazimisha kuwa na ofisi za kanda. Kwa hiyo wa Mkoa atazichakata za Mkoa mzima halafu ata-submit kwenye kanda yake halafu wale wa kanda ndio wapeleke kwa Mkaguzi wa Ndani Mkuu wa Serikali. Kwa kufanya hivyo…

MHE.ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

TAARIFA

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa taarifa.

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Naibu Spika, mzungumzaji anaendelea kuchangia vizuri sana. Nataka nimpe tu taarifa hapo anapopaona kwamba patengenezwe au pawe na Wahasibu Wakuu, Wakaguzi Wakuu wa Ndani wa Mikoa. Nataka nimpe taarifa hawa wapo kwenye Ofisi ya Mkuu wa Mkoa, ni Makatibu Tawala Wasaidizi, Ukaguzi wa Ndani wa Mkoa, lakini hawana kazi hiyo. Wana kazi ya kukagua wilayani na Ofisi ya RAS tu, kwa hiyo wapo hao. Wapewe majukumu ya kwenda kusaidia watendaji hao wa halmashauri kwenye ukaguzi.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ruben taarifa hiyo?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa. Ninachokisema hapa, nataka tufanye marekebisho kidogo yule Chief Internal Auditor kwenye Ofisi ya Mkoa, aendelee kubaki pale kwa sababu kila Afisa Masuhuli lazima awe na Internal Auditor, yeye abaki pale afanye mambo yake hayo ya kumwangalia RAS, afanye mambo ya kumwangalia DAS. Sisi tunamtaka Mkaguzi wa Ndani Mkuu Mkoani ajitegemee kabisa separate na yule wa pale kwa RAS.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo ni kwamba, yeye a-consolidate zile zote za wilaya zote ndani ya Mkoa na kuzichakata na kwa muundo huo tukishakuwa na Mkaguzi Mkuu wa Ndani kila Mkoa, definitely itatupeleka kwenye ofisi za kanda ambazo nazo zitachakata, halafu ndio zimpelekee sasa Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Serikali. Tukifanya hivyo tuna-ensure mambo mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, kwenye ukaguzi kinacho matter ni ubora wa taarifa. Tukifanya hivyo tutakuwa tumepata quality assurance lakini tutakuwa tumepata quality control, lakini sivyo hivyo tutakuwa tumeifanya kazi ya Mkaguzi Mkuu, CAG yule kazi yake itakuwa ni rahisi sana anapopita na kazi yake ikiwa rahisi itakuwa accurate, lakini wakati huo huo fedha zetu za wananchi tutakuwa tumezilinda. CAG akishakuwa na kazi ndogo tutataka sasa Serikali imwongezee fedha nyingi ili yeye awe anafanya real time audit. Tukifanya hivyo tutakuwa tumefanikiwa kuzuia majambazi yote yaliyopo ndani ya mfumo wa Serikali ambayo yanaiba fedha zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutakuwa tumefanikiwa kuzuia watu wote ambao sio waaminifu ambao wanaiba fedha zetu na kwa maana hiyo taarifa ya CAG itakuwa inakuja ikiwa safi na fedha za wananchi zikiwa salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, utoaji wa taarifa wa Wakaguzi wetu wa Ndani; moja ya eneo ambalo lazima tulifanyie maboresho, kwamba Mkaguzi wa Ndani mathalani Halmashauri ya Handeni Mjini anaandaa taarifa yake halafu anaipeleka moja kwa moja kule kwa Mkaguzi wa Ndani Mkuu. Taarifa yake anaipeleka moja kwa moja halafu Mkaguzi Mkuu yuko chini ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha. Kwenye ukaguzi huu tunapokagua kuanzia kwa Wakaguzi wa Ndani tunamkagua na huyo Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha. Haiwezekani wewe uwe unajikagua mwenyewe, unajiletea mwenyewe halafu taarifa unakaa nazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu kuna tabia ya watu wakipelekewa hizi taarifa za ukaguzi wanazipiga polish wanazing’arishang’arisha hivi, zinawafurahisha furahisha halafu wanakaa nazo. Haitakiwi kuwa hivyo, tunachotaka, taarifa ikitoka kwa Internal Audit wetu wa halmashauri, iende kwa yule Internal Auditor wa Mkoa. Ikitoka kwa yule wa mkoa, iende kwenye kanda, halafu iende kwa Katibu Mkuu Kiongozi, Pay Master General yeye apewe taarifa tu, kwa sababu ndiye anayekaguliwa pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wafanye hayo mapinduzi, wasipofanya haya tutaamini kwamba wana nia ovu ya kuendelea kufuja fedha za Watanzania. Taarifa zote za kikaguzi na taarifa mbalimbali za wachambuzi wa mambo ya kikodi, ya kikaguzi, ya fedha za wananchi, zimekuwa zikionesha kwamba tumekuwa tukipoteza trilioni nne mpaka tano kila mwaka kwa kuibiwa kwa sababu ya mifumo kama hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mapinduzi ya pili ambayo nataka tuyafanye, ni kuwawezesha wakaguzi kuwa conversant kuijua mifumo inayotumika kwenye taasisi zetu. Mifumo kama vile GePG, mifumo kama vile PlanRep, MUSE, ule unaotumika kwenye afya TANePS na sasa tunaubadilisha kuwa NeST na ule wa TAUSI na mifumo mingine mingi ambayo inatumika…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Reuben, mfumo wa time uko tayari. (Kicheko)

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja na nakushukuru sana. (Makofi)
Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi niwe miongoni mwa Wabunge ambao wamepata fursa hii adhimu ya kuzungumza kuhusu azimio hili ambalo tunakwenda kulipitisha, azimio ambalo limepata kuzungumzwa na Watanzania wengi sana huko nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesimama hapa kuwaomba Watanzania kwamba shughuli ya leo tunayoifanya tunaifanya kwa niaba yao Kikatiba, hofu waliyokuwa nayo na sisi mwanzoni tulikuwa na hofu hiyo hiyo, lakini baada ya kujiridhisha kwa kupitishwa na wataalamu wetu kwenye jambo hili hofu yetu imeondoka, na nataka niseme kuanzia sasa tutaendelea kuwapa elimu wenzetu walioko nje ya Bunge hili na tukitoka hapa tukirudi majimboni tutakwenda kuifanya kazi hiyo vizuri pia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, makubaliano haya ya ujumla sehemu zote ambazo Watanzania wana hofu tutakwenda kuzikazia zaidi kwenye mkataba mmoja mmoja kwenye miradi inayokwenda kuingiwa, na sisi hapa hatupo kwa ajili ya kuyashauri hayo ambayo wao wana hofu nayo na sisi tunaona kwamba ni ya msingi na kwamba Serikali inapokwenda kuingia mkataba mmoja mmoja ikayakazie. Mambo hayo ni pamoja na mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza, Serikali baada ya azimio hili kupita waende wakafanye valuation ya Bandari yetu ya Dar es Salaam, na ambao kwa kweli kwenye appendix I ndipo ambapo mwekezaji au wenzetu wamechagua kwamba tukashirikiane nao. Kwa hiyo, ni muhimu sana kufanya valuation ya bandari ili tujue asset tulizonazo kwenye bandari yetu, tujue reliability zilizopo kwenye bandari yetu na kwa ujumla tuujue mtaji wetu uliopo kwenye bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii ni muhimu sana kufanyika kwa sababu tunakaribisha mwekezaji mwingine na anaondoka mwekezaji mwingine TICTS aliyekuwepo pale. Kwa hiyo ni muhimu tukafanya valuation, tujue mtaji, lakini vilevile tujue future earnings, lakini vilevile tujue market value ya asset zetu, ni muhimu sana jambo hili lifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo ni la muhimu sana kufanyika ni feasibility study. Tufanye feasibility study ya miradi yote ambayo tunafikiri kwamba au ambayo tutakwenda kukubaliana na mwekezaji anayekuja kabla ya kuingia mikataba naye tufanye feasibility study. Kwa nini nasema feasibility study? Feasibility study itatuambia kwamba katika bandari ambazo mwekezaji ameonesha nia na katika maeneo ambayo mwekezaji ameonesha nia anatutoa pale kwa uwekezaji wake kutupeleka wapi? Kwa mfano mpaka sasa bandari zote 86 zinazohudumiwa na TPA zinapokea meli 4,686; feasibility study itatuonesha kwamba kwa uwekezaji anaoenda kufanya atatupeleka kwenye kupokea meli ngapi kutoka hapa tulipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili mpaka sasa tunapokea tani za mizigo milioni 20.709 uwekezaji huu unaokuja feasibility study itatuonesha kwamba ukifanyika tutafikia level ipi? Katika hizo tani milioni 20 tunazopokea za mizigo milioni 18 zote ni za Bandari ya Dar es Salaam ambalo ndio eneo kwa phase ya kwanza mwekezaji ameonesha interest. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine feasibility study ikatuoneshe kwamba kutoka kwenye makontena 823,404 ambayo tunayapokea kwa sasa, uwekezaji huu utatupeleka kwenye makontena mangapi? Kwamba baada ya uwekezaji na baada ya bandari kwenda kwenye full swing tutakuwa na uwezo wa kupokea kontena ngapi?

Ndugu zangu Watanzania na ndugu Wabunge wenzangu hivi ndio vipimo ambavyo kwenye mikataba inayoenda kufanyika mbele lazima tuwe navyo ili miaka kadhaa baadae tuweze kujitathmini kwamba uwekezaji huu tulioupokea na tunaouridhia umetusaidia au umeturudisha nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, uwekezaji huu unaofanyika tukafanye feasibility study ili tujue kwa sasa tuna magari 200,938 hayajahudumiwa na Bandari ya Dar es Salaam, tunatarajia mzigo uongezeke kwa uwekezaji unaokuja na magari yanayohudumiwa waongezeke ajira za Watanzania ziwepo na chain yote ya uchumi ionekane kwa uwekezaji unaokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bandari yetu na katika vitu kwa kweli ambavyo tunahamasika na tunakubalina sote kwamba tunamhitaji mwekezaji ni ili kuongeza mzigo ambao bandari inahudumia wa nchi jirani. Hivi sasa bandari yetu inahudumia mzigo kutoka nchi jirani tani milioni 7.7 tunatarajia baada ya uwekezaji kufanyika na mikataba tunayokwenda kuingia mmoja mmoja ikatuwezeshe kututoa hapa kwenye kupokea tani milioni saba peke yake kwa maana ya mizigo ya Zambia iongezeke, mizigo ya Kongo ikaongezeke, mizigo ya Burundi ikaongezeke, mizigo ya Rwanda ikaongezeke na Malawi ikaongezeke, Uganda ikaongezeke na nchi zingine kama vile Msumbiji, Sudan, Kenya, Comoro, Angola na Zimbambwe, uwekezaji utusaidie kufika hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili watu wengi wamelizungumzia huko nje, wapo waliolipotoshwa, lakini wapo waliokwenda mbali zaidi ya kuzungumza yale ambayo ni hatari kwa umoja wa nchi yetu na mshikamano wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwakumbushe wakati nchi yetu ilipopita kipindi kukubwa cha Covid-19, wakati dunia yote ilikuwa imejifungia ndani haikuzalisha, Watanzania tulikuwa tunatembea mitaani na tulikuwa tunafanya shughuli zetu. Makamu wa Rais wa nchi hii alikuwa ni Dkt. Samia Suluhu ndio alikuwa Mshauri Mkuu wa Rais aliyekuwepo. Tulivuka salama na hatukumtilia mashaka kama ni Mtanzania au siyo Mtanzania. Jambo hili hatupaswi kuliendekeza, yanapokuja mambo ya msingi ya hoja tutofautiane kwa hoja na si kwa kubaguana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawakumbusha Watanzania, miaka miwili iliyopita shughuli za kisiasa hazikuwa zinaruhusiwa kufanyika, hapakuwa na mikutano wa chama cha siasa wala hapakuwa na press conference za kwenye vyombo vya habari, ni Rais huyu huyu ndio alikuja akafungua hiyo minyororo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini wakati ule na yale yalikuwa ni mambo ya kitaifa ni mambo ya kikatiba kama ambavyo tunafanya hili la leo, kwa nini wakati ule hamkuhoji kwamba huyu ni Mzanzibar amekuja kufungulia vyombo vya habari? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi ninavyozungumza miaka miwili iliyopita kulikuwa na magazeti zaidi ya manne yamefungiwa online tvs, online media karibu vyombo zaidi ya 30, 40 vimefungiwa. Hivi ninavyozungumza ni Rais huyu huyu aliyepo amefungulia vyombo vyote vilivyokuwa vimefungiwa. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa kengele ilishagonga, ahsante sana.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie, mpaka sasa...

SPIKA: Mheshimiwa Kwagilwa kwa kuwa umeshaomba, sekunde 30 malizia.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, mpaka sasa hakuna kesi mahakamani ya chombo chochote cha habari wala mwandishi wa habari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya naunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii nipate kuchangia Bajeti yetu ya Serikali ya mwaka 2023/2024. Kwa sababu ya muda nitakimbia kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshika kitabu cha Bajeti aliyoisoma Mheshimiwa Waziri wa Fedha tarehe 15 wiki iliyopita na ninataka nianze kwa kunukuu ukurasa wa 182 unasema. “Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii tena kuendelea kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi kwa uongozi wake bora na thabiti wenye mafanikio makubwa hususan katika kuleta mageuzi ya kiuchumi pamoja na kuimarisha hali ya kisiasa nchini na mahusiano ya kikanda na kimataifa katika kipindi kifupi cha miaka miwili ya uongozi wake. Hakika Mama apewe Maua yake.” Mwisho wa kunukuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli hii ambayo ilitolewa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha katika Bunge hili nimeifuatilia kwa ukaribu sana bajeti hii na nimeisoma vyema sana Finance Bill ambayo tunaendelea Kamati ya Bajeti kuwasikiliza wadau. Ninaungana na Waziri wa Fedha kusema Mama apewe maua yake kwa kupitia Bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza; mwaka jana tulikuwa na Bajeti ya shilingi trilioni 41.48. Bajeti hii tunayokwenda kuipitisha ni ya shilingi trilioni 44.39, hili ni ongezeko la shilingi trilioni tatu nzima na ni ongezeko la almost 7%. Ndugu zangu katika macho ya kibajeti na kitaalamu hili siyo jambo jepesi, ninasema Mama apewe maua yake. Miaka miwili iliyopita tulishauri hapa kwamba nchi yetu ifanyiwe credit rating. Serikali sikivu ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ikafanya jambo hilo. Hivi sasa ninavyozungumza nchi yetu iko rated na makampuni mawili makubwa duniani ya credit rating, Kampuni ya FITCH na Kampuni ya MOODY’S. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mara baada tu Mheshimiwa Waziri wa Fedha kusoma Hotuba yako ya Bajeti siku zile, wenzetu ambao tumewapa kazi ya kutusimamia kwenye mambo haya ya fedha na kutushauri, Kampuni ya MOODY’S wametoa taarifa yao sijui kama umeiona. Taarifa hii na yenyewe imedhihirisha kwamba Mama apewe maua yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wenzetu wame-appreciate kwamba kwenye Bajeti yetu, mapato yameongezeka. Lakini la pili, hatua zote za kikodi ambazo zimechukuliwa zinatufanya Tanzania tuendelee kuwa nchi inayokopesheka. Kwa hiyo, tutaendelea kuaminika kwenye masoko ya kifedha makubwa huko duniani lakini kwa nini Mama apewe maua yake? Wenzetu wa MOODY’S hawa wanastaajabu. Wanashangaa kuna mambo makubwa matatu yanafanyika ndani ya nchi yetu pamoja na ongezeko hili la bajeti na pamoja na kipindi kigumu hiki cha uchumi kwa dunia nzima. Jambo la kwanza wanasema, wanalishangaa, linawezekanaje kwa Tanzania kufanyika? La kwanza; higher spending for ongoing infrastructure projects. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kampuni ya MOODY’S wanashangaa inawezekanaje Tanzania inaongeza bajeti na inaenda kuongeza makusanyo ili hali inapeleka fedha nyingi sana kwenye miradi mikubwa ambayo kwa ukanda wetu wa Afrika na hasa hasa Kusini mwa Jangwa la Afrika haipo miradi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa kwanza ni reli ya SGR na ambayo inajumuisha ununuzi wa vichwa na mabehewa. Kwenye hili ushauri wangu kidogo tu tutafute vichwa na mabehewa angalau kwa root moja tu kwa Serikali halafu tuwaachie private sector. Tuwe na line moja tu inayoweza kutusaidia kufanya kui-regulate biashara lakini tuwaachie private sector ifanye eneo hilo la vichwa na mabehewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo wanatushangaa ni ujenzi wa Bwawa kubwa la Mwalimu Nyerere. Kote huko kunakwenda na trillions. Wanashangaa ujenzi wa Daraja la Busisi kule Kigongo. Wanashangaa skimu kubwa za umwagiliaji ndiyo maana wamekuja na taarifa wanasema Mama apewe maua yake wanaungana na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na mimi naungana naye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile wanashangaa sana fedha zinatoka wapi za kujenga miundombinu kwenye Mji wetu wa Kiserikali pale Mtumba. Unajua, you cannot know what you have until you lose it. Mheshimiwa Waziri wa Fedha wewe ni mwalimu wangu lakini leo naomba nisione haya nikupongeze mbele ya Watanzania. Nakupongeza na ninataka nikwambie una bahati kufanya kazi kuwa Waziri wa Fedha chini ya Rais wa aina hii ambaye tunaye. Naomba nirudie hii statement, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu una bahati sana kuwa Waziri wa Fedha katika kipindi ambacho tuna Rais wa aina hii Dkt. Samia Suluhu Hassan. Wanaendelea kushangaa wanasema inawezekanaje Watanzania wanayafanya haya wanapeleka miradi ya barabara? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesaini hapa miradi ya barabara mingi sana lakini na mwisho kwenye miradi hii mikubwa mikubwa wanasema wanashangaa kuona miradi ya huduma za kijamii. Hakuna mahali Tanzania hii ambapo hapajengwi kituo cha afya, hakuna mahali Tanzania hii hapajengwi hospitali, hakuna mahali Tanzania hii hapajengwi shule, hakuna mahali Tanzania hii hapapelekwi umeme. Hakika Mama apewe Maua yake na kwenye hili. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii nami niweze kuchangia Bajeti Kuu ya Serikali 2022/2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Rais wa Awamu ya Sita, Mama shupavu, Mama mchapakazi kwa kutuletea bajeti ya kizalendo na ambayo ina harufu ya mapinduzi. Bajeti hii imekuwa ya tofauti kwa sababu ya mambo mawili makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ni bajeti inayoelekeza kubana matumizi; na jambo la pili ni bajeti ambayo inakwenda kuimulika Sheria ya Manunuzi na kuiwekea control. Mambo hayo mawili ni mambo makubwa ya msingi sana, naipongeza sana Serikali kwa jambo hili kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2021 bajeti yetu ilikuwa shilingi trilioni 37.99 na makusanyo ya ndani tulilenga tukusanye shilingi trilioni 21, lakini tukaishia kukusanya shilingi trilioni 17 mpaka Aprili. Mwaka huu bajeti yetu ni shilingi trilioni 41.48 na makusanyo ya ndani tunalenga tukusanye shilingi trilioni 28.02. Kwa maana hiyo, katika haya makusanyo ya shilingi trilioni 28.2, TRA inatakiwa ikusanye shilingi trilioni 23.65. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pale TRA zipo department nne za kikodi. Ipo Department ya Custom and Excise, Department ya Domestic Revenue, Department ya Large Tax Payers na Department ya Kikodi ya Tax Investigation. Mimi nitaongelea department moja ya Custom and Excise, Department yetu ya Forodha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye makusanyo ya TRA mwaka 2021 ya shilingi trilioni 17.2 department hii ilikusanya asilimia 40. Vivyo hivyo hata makadirio ya mwaka huu wa fedha shilingi trilioni 23.68 makusanyo ya ndani, tunatarajia Department hii ikusanye asilimia 40, karibia shilingi trilioni 10. Sasa department hii inakusanya wapi? Maeneo yake makubwa ni wapi? Maeneo yake makubwa ya kwanza ni bandari zetu, kwenye airports zetu na kwenye mipaka yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaangazia eneo moja katika hayo niliyoyataja nalo ni la bandari. Natambua kwamba tunazo bandari nyingi, lakini nitazungumzia bandari zetu tatu kubwa; Bandari ya Dar es Salaam, Bandari ya Tanga na Bandari ya Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Bandari ya Dar es Salaam peke yake kwa Tanzania ndiyo bandari pekee ambayo International Trade kwa ukubwa inafanyika kwa karibia asilimia 90. Asilimia 90 ya biashara yetu ya Kimataifa inafanyika Bandari ya Dar es Salaam. Sasa ni nini tunatakiwa tufanye kwenye maeneo haya ya hizi bandari tatu ili tukakusanye zaidi? Maana kupanga matumizi siyo shida, shida ni namna ya kukusanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, tunatakiwa tukanunue vifaa vya kisasa kwa ajili ya ku-deal na containers. Kwenye biashara ya bandari, fedha nyingi ipo upande wa containers. Vifaa ninavyoviongelea hapa, siongelei hizi cranes ambazo tunazo kwa sasa, hizi Gottwald Cranes, tunatakiwa tuwe na vifaa vya kisasa SSG. Hii inaitwa Ship-to-Shore Gantry Cranes.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya gati zetu zilivyo, kwa namna ambavyo Mheshimiwa Rais ameweka fedha pale Bandari ya Dar es Salaam, tumeiendeleza gati ya kwanza mpaka gati ya saba. Tumeweka pale mradi wa dola milioni 420 kwa ajili ya kuendeleza hizo gati. Sasa gati namba sita na namba saba ndizo gati ambazo zita-deal na containers. Tunatakiwa tukanunue hivi vifaa SSG (Ship-to-Show Gantry Cranes). Kifaa kimoja katika hivi, kinagharimu kama Euro milioni 11 hivi au milioni 10 na kitu. Kwa ukubwa wa gati zilivyo pale, gati moja itahitaji angalau kwa uchache, tena hizi SSG angalau tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, upanuzi tuliyoufanya pale, bandari yetu kwa sasa ina uwezo wa kupokea meli kubwa sana zile za post-panamax, na zile meli zikija pale zina urefu mkubwa na zinabeba containers nyingi. Kwa hiyo, kutumia vifaa hivi vidogo vidogo tulivyonavyo pale, tunapoteza biashara. Meli zinakaa muda mrefu kwenye kushusha na zinakaa muda mrefu kwenye kusubiri kuingia. Kwa hiyo, tunapoteza biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiweka SSG tatu tatu kwenye kila gati, tafsiri yake ni kwamba hizi post-Panamax ships huwa zinakuwa na partition tatu. Kwa hiyo, kila crane itashambulia partition moja. Tutashusha mizigo yetu ndani ya muda mfupi, meli zitaondoka na tutavutia watu kuja kufanya biashara na sisi kwenye eneo letu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, tunatakiwa tufunge mifumo ya ku-control containers ambayo ni ya N-generation; mifumo ya kisasa ambayo inai-trace container kutoka the pot of loading mpaka hapa inapofika kwetu na mpaka inaporudi kwa wenye nayo. Biashara ya container duniani ndiyo biashara kubwa inayo-control biashara za meli. Kwa hiyo, tusipofanya hivi tutakuwa hatujawekeza vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni skilled labour. Watu wetu tuwaelimishe, tuwasomeshe wajifunze mambo haya. Sasa ukurasa wa 27 wa Taarifa ya Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti inasema, “Kamati imebaini kwamba Mamlaka ya Bandari, badala ya kuendeleza kuwekeza ili kuwe na ufanisi katika uondoshaji wa shehena bandarini inafikiria kutumia makampuni ya nje kama vile DP World na TICTS. Hatua hii inaweza kuleta mafanikio ya ufanisi lakini itapunguza kwa kiasi kikubwa mapato ya Serikali.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kushauri ni nini? Ninashauri kwa uwekezaji huu ambao tumeufanya bandarini, tusiende kufikiria kuwapa watu kuendesha bandari yetu. Tumeweka hizo Dola milioni 420 Bandari ya Dar es Salaam, tumeweka Shilingi bilioni 256 za Kitanzania Bandari ya Tanga, na tumeweka Shilingi bilioni 157 Bandari ya Mtwara. Sasa uwekezaji huo mkubwa; vifaa hivi kuvinunua hata Shilingi bilioni 500 haifiki. Sasa Shilingi bilioni 500 ndiyo itufanye tuigawe Bandari yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tusifanye hivyo. Twendeni tukafanye utafiti kama ili tuone kama kuna genuine reasons ya kumpa mtu kuendesha bandari yetu. Tunao uzoefu, tuliwapa TICTS, leo ni mwaka wa 22 tunao pale, wakipata Shilingi bilioni 230, sisi tunachoambulia ni Shilingi bilioni thelathi na kitu tu. Ukiweka na hela ya pango ni kama Shilingi bilioni tisini na kitu tu, it is a loss.

Mheshimiwa Naibu Spika, wote tumeshakubaliana kama Watanzania, Bandari ya Bagamoyo tutawapa watu. Hakuna mwenye ubishi juu ya hilo. Sasa na hii ya Dar es Salaam nayo tuwape watu? Hata ukiwa na nyumba yako ya kupangisha, unapangisha vyumba vyote mpaka unakosa pakukaa? Haiwezekani! (Makofi)

Mhehimiwa Naibu Spika, nami naishauri Serikali, na huu ushauri ni kwa nia njema, twendeni tukawekeze vifaa ambavyo vinatakiwa ambavyo ni hizi cranes, tuwekeze hii mifumo ya kisasa ambayo ni N-generation na tuwaeleimishe watu wetu halafu tuendeshe bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa uwekezaji huu mdogo hata bila hivyo vifaa, mwaka huu wa fedha, 2022/2023 mpaka kufikia mwezi wa Aprili, Bandari ilikuwa imekusanya Shilingi bilioni 888, ukilinganisha na mwaka 2021 kabla ya uwekezaji ambapo muda kama huu tulikuwa tumekusanya Shilingi bilioni 751. Hapa tuna-handle container 600,000 tu, tukiweka hivi vifaa ninavyovisema, tutaenda kwenye full swing ya ku-handle container 1,500,000. Tukifanya hivyo, hii department ya TRA ambayo naisemea hapa ya Customs itakusanya zaidi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, sijajua ni kengele ya kwanza au ya pili.

MJUMBE FULANI: Ya pili.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa fursa. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia mswada wa sheria ya fedha 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme naunga hoja iliopo Mbele yetu naiunga mkono, baada ya kuiunga hoja mkono nijielekeze kuchangia kwenye huu Muswada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natokea Handeni sehemu ambapo ni Wilaya yenye madini mengi sana, na Muswada huu uliokuwa umeletwa Serikali ilionyesha ni ya kuigusa sekta ya madini kwa maana ya kuongeza kodi. Na hata vifungu ambavyo ame withdraw, wamesema wanakwenda kujipanga ili siku za usoni waweze kuanalia namna nzuri ya kutoza kodi kwenye sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Muswada huu kwenye amendment zilizoguswa ilikuwa ni ile part 3 amendment of the income tax Act cap 332, na ile part 25 ambayo ni amendment of the vocational education and training Act cap 82. Hii ilikuwa inawataka wachimbaji walipe 0.4 kama levy kwa maana ya SDL, na ile nyengine ilikuwa inawataka wachumbaji wadogo walipe asilimia 3 kama income taxi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii nimshukuru sana sana Mheshimiwa Rais mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kuwa msikivu sana, kwa kuwa msikivu sana na kuelekeza kwa Waziri wa Fedha wa withdraw hizi kwa ajili ya kuwalinda wachimbaji wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa Serikali ime-withdraw, na kwa kuwa bado wanafikiria kutoza kodi zaidi siku za usoni, kwa wachimbaji wadogo maana mpaka sasa mchimbaji mdogo analipa asilimia 6 kama mrabaha, analipa asilimia moja kwa ajili ya ukaguzi na analipa 0.3 kama sehemu ya serves levy, inamaana kodi yake yote mpaka sasa mchumbaji ni asilimia 7.3. Sasa kabla ya Serikali kufikiria kuwatoza zaidi wachumbaji wadogo, ninashauri mambo yafuatayo yafanyike:- (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza kumekuwa na taarifa tofauti tofauti za sensa za idadi ya wachimbaji wadogo, hivi tunavyo zungumza si Serikali, si wachimbaji wadogo wenyewe wenye takwimu sahihi za wachimbaji wadogo, kwa hiyo tunaishauri Serikali, sensa hii inayokuja ya Tanzania nzima ikatusaidie kutupa idadi ya wachumbaji wadogo nchi nzima, huwezi kutoza kodi kwenye sekta ambayo hujui idadi ya wahusika, hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili tulitunga sheria hapa mwaka 2017, Sheria ya The Natural Wealth and Resources, Permanent Sovereignty Act 2017, ambayo iliwawezesha watanzania kumili madini kisheria rasilimali zile, madini kisheria. Sasa watanzania wameshamiliki madini kisheria, Watanznia wanamiliki PML Watanzania wanamiliki migodi, lakini hatujawawezesha Watanzania kuyachimba haya madini, hatujawawezesha watanzania kuchimba haya madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata ukiangalia ile Mining Act cap 123 ambayo imtungiwa Regulations Section ya 129, inasema The Mining Act Mineral Value Addition Guidelines ambayo imetolewa kwenye tangazo la Serikali namba 60, tuipitie upya kanuni hii, tumewamilikisha madini na tumewanyang’anya fursa ya kuyatumia madini haya, kwa sababu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, regulation hii ilotungwa na wizara inazuia wachumbaji kusafirisha madini ghafi, sikatai kwamba kuna umuhimu sana wa kuyaongeza madini yetu thamani kabla hatujayasafirisha, sio kila madini tunauwezo nayo leo ya kuyaongeza thamani. Kwa mfano wanaposchimba chuma, ukiongelea valued edition kwenye chuma unaongelea kufunga plant kiwanda cha zaidi ya dola milioni moja, mchimbaji gani mdogo ataweza ku-afford kuongeza value addition ya chuma hapa, tumewafilisi wachimbaji wa kopa kwa hii na tumeshindwa kuyatumia maadini kama vile manganese na zile pressures mentals. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naiomba wizara yenye zamana ikapitie upya kanuni hii, tujaribu kuangalia kwa yale madini ambayo tunaweza kuyaongeza thamani kama ilivyo gold, kama ilivyo tanzanite tuendelee nayo, na kwa madini ambayo bado hatujajipanga tuwaruhusu watu wayachimbe na wayasafirishe yakiwa ghafi. Tukifanya hivyo tutapata kodi nyingi sana zaidi ya hata ambayo mlikuwa mnakadiria kuipata kwa kutoza asilimia tatu, huo ni ushauri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili nawashukuru sana benki ya CRDB kwa kuanza kuwaamini wachimbaji na kuwakopesha, lakini wenzeatu wa Serikali naomba niwaeleze jambo moja, hata kama CRDB wameanza kuwakopesha wachimbaji, wanawakopesha kwenye commercial rate, uchimbaji ni investment huwezi kumkopesha mtu kwa commercial rate afanye uchimbaji, lazima tuangalie namna gani wachimbaji wetu watakopeshwa kwama kufanya investment, kwa kuzingatia kwamba pay back period ya miradi yao ni ndefu sana na hata break event point yao ni ndefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwakumbushe tu hata hizi kodi tunazowatoza sasa hivi wachimbaji, kuna wengine tunawatoza kutoka kwenye mitaji yao kwa sababu inamchukua mchimbaji muda mrefu sana kutengeneza faida.

Kwa hiyo, anapokuwa amekwenda kuuza madini yake aliyoyapata wewe ukitoza ile 7.3 haimaanishi kwamba yeye atengeneza faida, anaweza kuwa ame-invest amepata jiwe ambalo halifanani na thamani ya investment yake kwa sasa, lakini wanaendelea kulipa kodi kizalendo sana, kwa sababu wanalipa kodi kwenye investment zao, kwenye capital. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii industry ni lazima tui-trite with conscious, tusiwe tunakuja tu hapa tunataka kutoza kodi, lazima hii industry tuilee na lazima tufungue milango kwa sababu hawa wachimbaji hatujawa na uwezo wa kuwawezesha kama Serikali, basi tuwalee ili wao wenyewe waendelee kujijenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya nakushuru sana nafikiri nimetumia muda wangu vizuri, ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (no. 6) Bill, 2021
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia fursa hii ili na mimi nipate kuchangia Muswada wa Mabadiliko ya Sheria Mbalimbali Na. (6) wa Mwaka 2021. Niungane na Wabunge wenzangu waliotangulia kuzungumza kuipongeza sana Serikali ya CCM kwa kuwajali wakulima, wafugaji na wavuvi, kuondoa Withholding Tax ya asilimia mbili katika mazao yanayotokana na shughuli hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa salamu hizo za pongezi, mimi nataka nichangie marekebisho ya ile part three, yaliyokuwa yameletwa kurekebisha Sheria ya Usimamizi wa Kodi. Sheria hii imefanyiwa marekebisho na sisi Kamati ya Bajeti tumeshauri sana ili kuondoa vikwazo vyote ambavyo vilikuwa vinakwamisha utekelezaji wa mradi wa bomba la mafuta. Sasa baada baada ya kuipitisha sheria hii hapa Bungeni na wenzetu wa Serikali kwenda kushirikiana na Serikali ya Uganda kuutekeleza mradi huu ninashauri mambo yafuatayo kwenye mradi huu:

Mheshimiwa Spika, mradi huu una gharama ya Dola Bilioni 3.5 karibia trilioni nane hivi. Tafsiri ya hii ni kwamba ni mradi mkubwa na ni fursa kubwa kwa wananchi wetu ambako mradi unapita lakini na kwa Watanzania kwa ujumla. Kwa hiyo, basi ni lazima tuweke mikakati ya makusudi kuwawezesha wananchi wetu ambako mradi unapita ili washiriki kikamilifu kwenye shughuli zote kwenye fursa zote za ujenzi na uwepo wa mradi huu maeneo ambako bomba hili linapopita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali za wananchi wetu tunazifahamu. Kikwazo kikubwa kwa wananchi wetu kushiriki kwenye fursa za bomba la mafuta hili ambalo tunalizungumzia itakuwa ni mitaji. Tayari Maafisa wetu wa Maendeleo ya Jamii huko tunakotoka ambako bomba linapita wanawahamasisha wananchi wajiunge kwenye vikundi, lakini kikwazo kikubwa, ninarudia tena, kikwazo kikubwa ambacho kitawakumba wananchi wetu ni mitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu sasa kwenye hili la kuwawezesha wananchi wetu mitaji ya kushiriki kwenye fursa za bomba la mafuta, ushauri wa kwanza ni kwamba kwa wale watakaofanikiwa kupata mikataba ya kazi kwenye bomba lile la mafuta kwa maana ya ama ku-supply vitu au kujenga, ninaomba kwamba ufanyike utaratibu maalum ili mikataba ile itumike kama dhamana kwenye mabenki. Kufanyike utaratibu maalum mikataba ile watakaokuwa wamepata itumike kama dhamana kwenye mabenki ili waweze kuchukua mikopo tena yenye riba nafuu. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa unajadili vizuri, lakini tujue kwamba, leo tunajadili sheria. Tunapojadili sheria ni tofauti kabisa na kujadili mada. Hatujadili bomba la mafuta na mambo yake, tunajadili sheria iliyoletwa hapa. Endelea tu Mheshimiwa tumalizie.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nakushukuru. Kwa kuwa, umenipa na umeridhia niendelee naomba nimalizie vipengele vinavyofuata.

Mheshimiwa Spika, jambo jingine kwenye bomba hili tunalokwenda kulijenga ni vyema Serikali ikalichukua kama fursa na sisi kama nchi tutazame ushoroba kwa maana ya mkuza. Corridor hii ambayo tunakwenda kuijenga ya bomba la mafuta kutoka Hoima mpaka Chongoleani - Tanga siku zijazo tuifikirie kama fursa ya kupitisha bomba la gesi kutoka hapa gesi yetu ilipo ili tuweze kuipeleka mpaka Uganda na hatimaye Sudan ya Kusini na baadae Congo. Tuitazame kama fursa ya siku zijazo.

Mheshimiwa Spika, mwisho kwenye hili bomba hili linapita kwenye Mikoa Nane na katika hiyo Mikoa Nane Mikoa ya mwisho huku kuelekea Bandari ya Tanga ni pamoja na Tanga yenyewe, Dodoma, Singida na Manyara. Sasa bomba hili litahitaji barabara ya kulihudumia hili bomba, barabara hiyo inayopita maeneo hayo ili kuweza kulifikia hili bomba kwa urahisi ni barabara ya Handeni – Kibilashi – Kiteto
– Kondoa na Singida. Kwa hiyo, ni vyema Serikali inapofikiria kwenda kutekeleza mradi huu ifikirie pia kuitengeneza barabara hii.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipatia muda na kuniruhusu kuchangia haya. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Kudhibiti Utakatishaji wa Fedha Haramu wa Mwaka 2022
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kuchangia Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Kudhibiti Utakatishaji wa Fedha Haramu. Kwanza nitumie nafasi hii nimpongeze sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kulipa uzito jambo hili na kwa kuona umuhimu wa jambo hili na hatimaye kuleta Muswada huu kwa dharura ili kulinda hadhi ya nchi yetu katika uwanda wa Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma tathmini ambayo ilifanywa na ikapelekea leo Serikali kuleta Muswada huu, tathmini ile inaonyesha maeneo mawili makubwa ambayo ilitutaka kama nchi tuyafanyie marekebisho ili tuweze kuendana na viwango vya Kimataifa. Eneo la kwanza ni eneo la kisheria ambayo ndiyo kazi tunayofanya leo hapa. Kwa hiyo, hapa wala asiwepo mtu wa kumlaumu mtu mwingine kwamba imechelewa kuja, huu ndiyo wakati sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni la kimifumo. Mifumo ya taasisi zetu, namna ambavyo taarifa zinatoka taasisi moja kwenda nyingine, namna ambavyo taasisi zinatoka kampuni moja kwenda nyingine. Haya ndiyo maeneo mawili ambayo utafiti ule au tathmini ile ilitaka tuyaboreshe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 4 ya Muswada ambayo inafanya marekebisho kwenye kifungu cha 3 cha Sheria ile tunayoifanyia marekebisho, imetaja maeneo mawili ya muhimu na ambayo nataka niyajadili kwa huu muda mfupi uliopo. Eneo la kwanza ni eneo la watoa taarifa (reporting persons). Ibara hii imeongeza idadi ya watoa taarifa, Sasa watoa taarifa watahusika zaidi na hili eneo la kimifumo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali baada ya kupitisha Sheria hii hapa itakuwa na kazi kwa kweli ya kwenda kuhakikisha kwamba taasisi zetu mifumo inayotumika inasomana. Tuna mifumo mingi. Ipo mifumo inayotumika kule bandarini ya TANCIS, ipo mifumo inayotumika kwenye mabenki ambayo iko pale BoT na mifumo inayotumika na TRA ya kikodi. Vile vile taasisi yetu hii ya Financial Intelligence Unit inapokuwa imejiridhisha na taarifa zilizopelekwa kwake, inazipeleka kwenye taasisi nyingine mbalimbali kama vile Polisi na vile PCCB. Kwa hiyo, mifumo ya maeneo haya pia lazima Serikali ikairejee iiboreshe ili iweze kusomana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivyo hivyo, mifumo ya Credit Reference Bureau ambao ameongezwa kwenye kifungu hiki kama sehemu ya watoa taarifa, vile vile tukaiainishe na mifumo ya kiutumishi pamoja na mifumo ile ya Tume ya Maadili ya Umma. Nakumbuka kila mwaka tunajaza fomu zile za Maadili ya Viongozi wa Umma. Tunatakiwa kama nchi tuwe na mfumo ambao taarifa hizi tunazi-update tu, badala ya kuwa tuna-update kila siku. Kwa kufanya hivi, tutakisaidia kitengo chetu cha Financial Intelligence Unit kufanya kazi yake kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipengele kingine ambacho kinatajwa kwenye ibara hii ni hiki cha kufanya Consumer Due Diligence kila biashara inapofanyika. Kwamba unapokuwa unafanya biashara yako, lazima umjue mteja wako. Tumeweka marekebisho pale, tumesema consumer monitoring. Sasa kwenye kufanya consumer monitoring, Watanzania wenye biashara, taasisi zenye biashara zitategemea zaidi taarifa za mtu mmoja mmoja. Kwa maana hiyo, tunaipa Serikali yetu challenge ikafanye kazi kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi hii Mtanzania anamiliki vitambulisho karibia vinane. Nitatoa mfano. Kitambulisho cha NIDA, kitambulisho cha Mpiga kura, kitambulisho cha kazi, kitambulisho cha Bima ya afya, driving license, passport, kitambulisho cha benki, vitambulisho vya mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Ni lazima Serikali iwe na mfumo ambao kitambulisho chetu kimoja tu kile cha NIDA kibebe taarifa zote za kila Mtanzania. Kwa kufanya hivyo, tutarahisisha mazingira ya kufanya biashara na kurahisisha kupata taarifa ambazo ndiyo hasa zinahitajika kwenye kitengo chetu hiki cha Financial Intelligence Unit ili tuweze ku-meet masharti haya kama Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka nichangie tu maeneo haya. Nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)