Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Kwagilwa Reuben Nhamanilo (18 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi hii. Nikipongeze Chama changu cha Mapinduzi kwa uwepo wangu hapa, kikiongozwa na Mwenyekiti wetu, Mheshimiwa Rais, Dkt. Magufuli; lakini zaidi niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Handeni pamoja na familia yangu kwa kunifanya niwepo mahali hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yamezungumzwa mengi hapa kuhusu hotuba ya Mheshimiwa Rais. Hotuba yenyewe ilijielekeza kutoa uelekeo wa nchi yetu kwa miaka mitano ijayo, pamoja na yote ambayo Mheshimiwa Rais anayafikiria ni ya muhimu na ambayo yatatuvusha kama taifa kuelekea miaka mitano na pamoja na hoja zote ambazo Wabunge wamezichangia. Kimsingi ukiangalia ni kwamba mambo haya mwisho wa siku yanahitaji fedha; ili tuweze kuyafanya yanahitaji fedha.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi nataka nichangie ili kujaribu kuishauri Serikali ni namna gani kama nchi tutajidhatiti kuweza ku-raise hizi fedha ambazo zinahitajika kwa ajili ya kuyatekeleza mambo haya ya kutuvusha miaka mitano ijayo.

Mheshimiwa Spika, la kwanza ambalo nataka nilishauri kwa Serikali yangu, tutakumbuka mwaka 2019 Bunge lako lilipitisha Finance Act yenye maboresho ya kikodi mengi sana, na moja kati ya maboresho hayo ilikuwa ni kupendekezwa kuanzishwa kwa Ofisi ya Tax Ombudsman, jambo ambalo mpaka leo halijafanyika.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali yangu sikivu ianzishe ofisi hii muhimu ili kuendana na hotuba ya Mheshimiwa Rais ukurasa wa 12 ambapo ameelekeza kwamba lazima tuwe tunafanya business disputes, njia pekee ya kufikia hapo ni kuanzisha ofisi hiyo muhimu ya Tax Ombudsman.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo nataka nilishauri ni structure yetu ya chombo chetu muhimu cha TRA. Yote tunayotategemea yanategemea makusanyo ya ndani yanayofanywa na ofisi hii ya TRA. Ninachoishauri Serikali yangu ni kwamba TRA isiogope kuajiri vijana kwa sababu waajiriwa wa TRA siyo sawa na waajiriwa wengine wa pande nyingine za idara za Serikali, hawa unaajiri watu ambao wanakwenda kuzalisha moja kwa moja, wanatusaidia kukusanya kodi. Haiwezekani eneo la kimkakati kikodi kama ilivyo Ilala unakuwa bado una ofisi zenye watumishi wasiotosha, tunajichelewesha wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo nataka nilishauri ni habari ya informal sector. Informal sector inafanya biashara kubwa sana lakini haiwi captured kwenye mifumo ya kikodi. Hili ninapendekeza ufanyike utafiti mzuri na wa kutosha ili watu wetu wa TRA waweze kutoza kodi sehemu zote zinazozalisha ambazo ziko kwenye informal sector. Tusipojaribu kuli-balance hili litakuja kutuingiza matatizoni kwa sababu formal sector inayolipa kodi itakuja nayo kugeuka kuwa informal sector, ni lazima tufanye utafiti na tujaribu kuya- balance haya mawili.

Mheshimiwa Spika, pamoja na makusanyo mazuri yanayofanywa na TRA, ninashauri tusiwe tunapima ufanisi wa TRA kwa kuangalia increment ya makusanyo yao, kwamba mwaka jana walikusanya hapa, mwaka huu wameongeza kiwango hiki, hicho si kipimo peke yake cha kuonesha ufanisi wa taasisi hii muhimu kwetu.

Mheshimiwa Spika, naomba TRA na Serikali yetu kupitia Wizara ya Fedha wawe wanaangalia ratio kati ya taxes zinazokusanywa kwa uwiano na GDP ya kwetu. Tusipofanya hivyo hatari yake ni kwamba tutakuwa tuna- impose tax burden kwa walipakodi wachache kwa sababu increment hiyo unaweza ukakuta ni kwa sababu ya vertical raise kwa kuongeza tu makadirio ya kodi kwa wafanyabiashara walewale waliopo badala ya kui-spread ile kodi kwa uchumi wote.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka nilishauri ni habari ya mamlaka za Kiserikali. Mamlaka zetu za Serikali zinakuwa supplied na wafanyabiashara, sasa wafanyabiashara wanapokuwa wame-supply Serikalini ukichelewa kuwalipa maana yake unajichelewesha mwenyewe kuchukua kodi yako. Ni bora hata ukafanyika utaratibu kama fedha ya kuwalipa inakuwa haijapatikana, ile component ambayo ina kodi ndani ilipwe kwanza halafu ndiyo waendelee na procedures nyingine. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Reuben Kwagilwa.

MHE KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi hii. Moja kwa moja nijielekeze kwenye kuchangia lakini sababu dakika tano ni chache sitaingia ndani sana ila nataka nitoe ushauri mmoja kabla sijatoa maelezo yangu ya jumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ambao nataka nitoe, kuna suala hapa limezungumzwa sana nalo ni la maji. Sera ya Taifa ya Maji ya mwaka 2002 pamoja na Sheria ya Maji Na. 5 ya mwaka 2019, Sheria hii ya Maji ya mwaka 2019 ndiyo ilianzisha RUWASA lakini kana kwamba haitoshi ikaenda mbele ikaleta Mfuko wa Maji wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alipokuwa anazunguka kufanya kampeni kwenye hotuba yake amekiri, namnukuu anasema: “Hata hivyo, napenda nikiri nilipokuwa kwenye kampeni moja ya changamoto kubwa niliyoelezwa na wananchi ilikuwa ni shida ya maji hususan maeneo ya vijijini”. Kwa sababu Mheshimiwa Rais ameshaliona hili, nashauri Serikali iirejeshe hapa ile Sheria ya Maji, Na. 5 iliyotungwa na Bunge letu ya mwaka 2019 ili tuirekebishe kidogo. Marekebisho yake yaweje? Tumeweka pale source ya fedha za huu Mfuko; tumesema tutatoza shilingi 50 kwenye petrol na shilingi 50 kwenye diesel. Nachoomba ili tuweze kuisaidia RUWASA lazima sheria ije hapa tuitengeneze iweze ku-state ni asilimia ngapi iende kwenye maji katika hiyo shilingi 100 inayotozwa kwenye petrol and diesel. Kwa sababu tukiiacha hivi miradi ya mjini inatumia fedha nyingi kuliko miradi iliyopo vijijini. Kwa hiyo, kuna haja ya kufanya hayo marekebisho ya hiyo sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la jumla sana mimi nataka tu niseme kwamba ndugu zangu unapopanga la kwanza unatumia takwimu na pili unatumia assumptions. Kwenye hili eneo la takwimu tusipojizatiti vizuri kuboresha namna ya upatikanaji wa takwimu kwenye nchi yetu kila tunapopanga tutakuwa tunajikuta tuko nje ya malengo. Kwa hiyo, ni vema tuboreshe sana eneo hili la takwimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye huu Mpango ambao ndiyo mpango wa mwisho kuelekea Vision yetu ya 2025 kama Taifa kukamilika wakati nimekuwa nikiusoma mara kwa mara na kuurejea sijaona mahali ambapo Mpango huu umeweka provision kwamba baada ya Vision 2025 kukamilika inayotekelezwa mwishoni kwenye huu Mpango ni kitu gani kitafuata? Vision nyingine itakapotengenezwa, sijaona provision kwenye Mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine tunapopanga ni vema tukajua financing mode ya hii miradi tunayoipanga especially hii miradi ambayo tunaita flagship projects. Ukifanya tathmini vizuri kwenye Mpango uliopita utagundua tulikuwa na miradi karibia 20 na yote ni mikubwa. Miradi 20 yote hii hatuwezi kui-finance na kodi za wananchi za kwetu za ndani. Kwa hiyo, ni vema tujikite kama taifa na ni wakati muafaka sasa tukubali tu kwamba ili tuitengeneze hii miradi ni lazima tutafute sources nyingine, namna nyingine ya kuitekeleza ama kwa partnership au kwa kukopa lakini tuifanye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huohuo lazima twende na tahadhari, tumejaribu kufanya partnership pale Liganga na Mchuchuma na mradi huu umezungumzwa sana tokea tuko shule na bado mpaka leo haujatekelezeka. Naishauri Serikali yangu sikivu kama hili la Liganga na Mchuchuma limeshindikana kwa mwekezaji huyo tuliyenaye, ni vyema tukaenda mbele tukatafuta mtu mwingine kwa sababu dunia kwa sasa ni chuma na mafuta. Ni bidhaa mbili tu zinazotawala soko la dunia za mafuta na chuma. Kwa hiyo, tunapochukua muda mrefu miaka 7 toka 2014 tunafanya mazungumzo tunajichelewesha tu wenyewe. Tunahitaji tu- mobilize fedha kutokana na hii miradi ya kimkakati ambayo tunayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, mimi ya kwangu yalikuwa hayo machache. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa fursa hii ili niweze kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kupanga ni taaluma, lakini kwa Taifa letu na kwa Serikali yetu kupanga si tatizo. Mpango huu tulionao ni mzuri sana kuliko mipango mingi sana ya nchi nyingi hapa Afrika, lakini shida tulionao sisi kwenye kupanga ni kutekeleza Mpango tuliouweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi sitaongelea mengi isipokuwa nataka nijielekeze eneo moja tu, la Mradi Mkubwa tulionao wa Standard Gauge Railway, tunayoijenga. Standard Gauge Railway tunayoijenga ukijumlisha tu zile njia kilometa zinazojengwa tunatakiwa tujenge kilometa 4,886, hapo naongelea njia tu, siongelei mahala ambapo reli zinapishana. Mpaka sasa tumeshajenga kipande cha Dar es Salaam kuja Morogoro kilometa 300 na tunaendelea na kipande cha Morogoro – Makutupora kilometa 422, lakini vilevile tuko upande ule mwingine wa Isaka na Mwanza kilometa 249.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa aina ya financing ya mradi huu tunavyoindesha tukiendelea nayo tutaujenga Mradi huu wa Standard Gauge kwa nchi nzima kwa miaka 81, miaka 81. Ikiwa miaka mitano tumejenga kilometa 300 ndio ambazo ziko above 90 then kilometa 4,886 tutazijenga kwa miaka 81. Hii katika nchi ambayo inapambana kutafuta maendeleo ni kitu hakikubaliki, ni kitu hakikubaliki. Hivyo vipande nilivyo vitaja ambavyo vinajengwa vimetugharimu takriban trilioni 11. Trilioni 11 ni Idle Investment kwa sababu gani, kwa sababu hatutakamilisha leo ili tuanze kutumia mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachokishauri Serikali yetu iondekane na habari ya Traditional Methods za ku-finance miradi hii mikubwa. Kwanza tunajipa pressure kama Serikali, ya ku-finance mradi huu halafu tunashindwa kupeleka huduma kwa wananchi ambazo ni za kila siku. Kwa hiyo ninachokishauri Wizara ya Fedha waangalie utaratibu wa ku- finance mradi huu Infrastructure Bond. Wamefanya hivyo nchi za wenzetu, ukienda Benin wamefanya, ukienda Tunisia wamefanya. Hii inatupa ahueni ya kutekeleza mradi huu na kuutekeleza kwa wakati. Tunapoendelea kutekeleza mradi huu hivi kidogo kidogo ni hasara kwa Taifa letu, ni vile tu hatui- merge hii hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa faida ya wasiofahamu na Watanzania kwa ujumla, tunatakiwa tuitoe reli itoke Dar es Salaam iende mpaka Tabora kwa kupitia Singida, ikifika Tabora iende Isaka Shinyanga mpaka Mwanza, ikitoka Tabora iende Keeza ili tukahudumie Kigali na Burundi, ikitoka hapo Tabora tuipeleke Kaliua kwa ndugu yangu hapa, iende Uvinza mpaka Kigoma tukaihudumie Kongo na tukitoka Kaliua tuje Mpanda mpaka Katema; hiyo ni Reli ya Kati tunayojenga. Bado kuna kipande cha Tanga, Musoma, Arusha kilometa takriban 1,233; na hapo hapo bado kuna kipande cha Mtwara – Mbambabei kilometa 10,092.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ni kitu serious sana, hatuwezi tu kuendesha mradi huu kwa kutumia mapato ya ndani tutawaumiza Watanzania na tunajichelewesha wenyewe kupeleka maendeleo ambayo yanahusu huduma za moja kwa moja za wananchi za kila siku kama vile elimu na afya; na ndio maana kwa mwenendo huu wananchi wa Handeni mpaka sasa hatuja pata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa mradi huu kwa pamoja kutatusaidia sana kama Taifa kwanza kuifungua Bandari yetu ili iongeze mzigo unaopita pale. Kwa sasa hivi tunapitisha tani milioni 17 ukilinganisha na wenzetu wakenya wanapitisha pale Mombasa tani milioni 37. Kukamilika kwa pamoja na kwa wakati mmoja kutatusaidia sana kupata mapato kupitia mradi huu, kwa maana TRA wataweza kukusanya lakini vilevile wananchi wetu uchumi wao unataweza kuwa activated.

Mheshimiwa Naibu Spika, jinsi tunavyojenga kwa vipande vipande hivi na kuchukua muda mrefu kuna maeneo ya nchi yetu yatabaki kuwa-disadvantaged. Kwa mfano kipande hiki cha Mbambabei – Mtwara kitabaki kuwa ni historia tu ikiwa hatutatekeleza mradi wa Liganga na Mchuchuma, viability ya hii reli hapa haipo. Vivyo hivyo kipande kile cha kutoka Tanga kwenda Arusha kwenda Musoma kama hatukuimarisha vile vipaumbele tulivyoweka ukanda ule ikiwemo soda ash pale Lake Natron hakuna viability ya mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lipo bomba linalotoka Uganda Hoima kuja Chongoleani Tanga. Kwa vyovyote vile mafuta yatakapofika Tanga yatahitaji reli hii hii kuyarudisha yakisha kuwa refind. Kwa hiyo Serikali ione umuhimu wa kwenda kukopa kwa kutumia Infrastructure Bond ili tutekeleze mradi huu kwa pamoja kwa mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo na baada ya kushauri hilo ni malizie kwa kusema; limezungumzwa hapa asubuhi kidogo lakini halikukaziwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo Sheria ya Bajeti ya mwaka 2015 ambayo inatu-guide kuanzia mwanzo tunapotengeneza bajeti mpaka tunapoitisha bajeti hapa Bungeni, lakini sheria tukishapitisha bajeti hapa wenzetu wa Serikali wanapokwenda kutekeleza bejeti hakuna Sheria ya Monitoring na Evaluation. Kwa maana hiyo tunamuomba hapa Waziri wa Sera Serikali yetu hapa walete Sera. Kwanza wao watunge Sera ya Monitoring na Evaluation ili wailete hapa tuitungie sheria. Ndiyo maana ripoti hii ya CAG ambayo tunakwenda kuijadili ni aibu ni aibu ni aibu ni aibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tusipofika mahala tukatunga sheria hiyo; huwezi; kwa mfano mradi wa bilioni 380 unaotekelezwa, wa maji kule Handeni, unaojengwa kutoa Maji Korogwe kuyaleta Handeni eti ukasimamiwe na Mtendaji wa Kata, usimamiwe na Diwani. Lazima tutunge sheria ikae vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono mpango uliopo mezani, naomba kuwasilisha. Ahsante sana. (Makofi).
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii ili na mimi niweze kuchangia Mapendekezo ya Mpango 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 08 Aprili, 2021 Waziri wa Fedha aliwasilisha hapa Mpango mkubwa wa nchi wa Miaka Mitano. Mpango huu wa miaka mitano ndio ambao umesababisha leo tunajadili mpango wa mwaka mmoja mmoja; na mpaka sasa tumekwisha jadili mipango miwili na sasa tuko kwenye mapendekezo ya mpango huu wa tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mpango ule mkubwa wa miaka mitano ambao ulikuwa wa 2021/2022- 2025/2026 uliandaliwa kwa kutumia rejea ya vitabu kadhaa, nitavitaja harakaharaka; Dira ya Taifa ya Maendeleo, Ilani ya Uchaguzi ya CCM, hii niliyoishika na watu waione, kitabu makini kabisa; Mpango Elekezi wa Muda Mrefu, matokeo ya tathmini, sera na mikakati mbalimbali ya kisekta, Dira ya Afrika Mashariki 2050, Dira ya Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika, Agenda 2063 ya Maendeleo ya Afrika pamoja na Malengo ya Maendeleo Endelevu 2030.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hivi vitabu vyote nilivyovitaja hiki kimoja ndicho ambacho tulikwenda nacho kwa wananchi, ndicho ambacho tulikinadi, ndicho ambacho wananchi waliamua kwamba watakichagua hiki na wakaichagua Serikali ya CCM ili iweze kuleta maendeleo. Kwa hiyo mipango yote tunayoipanga lazima ilete tafsiri ya hiki kitabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye huu mpango mkubwa kulikuwa na shabaha za mpango ambazo ziko tano. Na mimi leo nataka tuzipitie vizuri tukirejea mapendekezo haya ya mpango yaliyopo mbele yetu tuone kama yanaleta tafsiri ya hiki ambacho kipo kwenye mpango wetu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shabaha ya kwanza ya mpango ule mkubwa wa miaka mitano inasema, “ukuaji wa uchumi kuongezeka kutoka asilimia sita mwaka 2021 hadi kufikia 58% mwaka 2026.” Ilani yetu ya Uchaguzi ukurasa wa 13 (b)(1) inasema, “kuweka sera madhubuti za uchumi jumla ili kukuza uchumi kwa wastani usiopungua asilimia nane kwa mwaka.” Hiki ndicho ambacho tumewaahidi Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tunavyongea kwa Januari mpaka Machi, 2022, uchumi wetu umeripotiwa kukua kwa asilimia 5.4. Hii ndiyo kusema tuko chini na nje ya mpango wetu ambao tumeuweka sisi wenyewe. Kwa hiyo, Serikali wanayo kazi ya kwenda kufanya kuhakikisha kwamba kitabu hiki wanakitafsiri na wanakitekeleza kwa namna ambavyo kinaelekeza. Kinataka ukuaji wa uchumi kwa asilimia nane, lakini Serikali imeripoti ukuaji wa uchumi wa asilimia 5.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Shabaha ya pili ilikuwa ni mapato ya ndani ukijumuisha mapato ya halmashauri kuongezeka kutoka asilimia 15 ya pato la Taifa hadi kufikia asilimia 16. Hivi tunavyozungumza ukisoma haya mapendekezo ya mpango yaliyoletwa mbele yetu, sura ya 3 (3), (2)(i) inasema, mapato ya kodi; kwenye mpango wanatarajia yafikie asilimia 12 ya pato la Taifa. Yaani mpango huu wa mwaka mmoja uko nje kabisa ya mpango mkubwa ambao ndiyo tumekubaliana kuufanya. Wao wanaongelea mapato ya kodi kufikia asilimia 12 ya pato la Taifa ilhali mpango mkubwa unataka tufikie kuanzia asilima 15.9 mpaka 16.8.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuwa na mipango ya hivi. Mipango hii midogo ya mwaka mmoja mmoja inatakiwa itafsiri mpango ule mkubwa tuliojiwekea na ambao tumeupeleka kwa wananchi kuunadi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shabaha ya tatu ya ule mpango mkubwa inasema, “mfumuko wa bei kuendelea kuwa wa tarakimu moja, wastani wa 3% mpaka 5%.” Naipongeza Serikali kidogo hapa kwa sababu wamejitahidi sana kuweka mfumuko wa bei kwenye single digit. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikilizeni niwaambie jambo muhimu unapoongelea mfumuko wa bei na hasa kwa Watanzania. Jambo la muhimu kabisa tunapoongelea mfumuko wa bei kwa Watanzania wa kawaida na wananchi walio wengi tunaongelea mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi. Hicho ndicho kinachogusa Watanzania. Taarifa hii ya mpango mpaka kufikia Agosti, 2022, mfumuko wa bei za vyakula na vinywaji baridi uko asilimia 7.8; it is above 3% to 5%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ya mfumuko wa bei ya chakula, nitumie hii nafasi niiombe sana Serikali, kama kuna vyakula kwenye maghala sasa hivi, waruhusu viende kwa wananchi. Hali ni mbaya sana. Hivi sasa Handeni Mjini… (Makofi)

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nimefurahishwa sana na mchango wa kaka yangu, Mheshimiwa Mbunge ninayemheshimu sana, lakini napenda kumpa taarifa kwamba analolizungumza, tayari Serikali ya CCM wameshaliona. Leo ninavyozungumza, Ikungi tumepokea Tani 100 za mahindi kuwauzia wananchi kwa bei ambayo itapunguza tension. Kwa hiyo, kwa kweli Serikali na Wizara ya Kilimo tunaIshukuru sana. Naomba nimpe taarifa hiyo. Sasa itakuwa ni vyema na kule kwake wapeleke. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Reuben.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawazungumzia wananchi wa Handeni ambao mpaka leo asubuhi wamenunua kilo ya sembe kwa shilingi 2000. Sasa kama Mheshimiwa Mbunge, mahindi yamefika kwake Ikungi, hilo ni jambo la kuishukuru Serikali ya CCM. Ninachosema hapa ni kwamba Mpango huu uwe wa Kitaifa na siyo wa Ikungi peke yake. Kwa hiyo, ni muhimu sana tukazingatia kilichopo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo, hili la chakula narudia tena, naomba Serikali kama ina chakula kwenye maghala, i- offload ili mahindi yawafikie wananchi kwa bei ambayo itakuwa ni elekezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shabaha namba nne ambayo mpango mkubwa umeuweka inasema, akiba ya fedha za kigeni kukidhi mahitaji ya uagizaji wa bidhaa. Hili nalo naipongeza Serikali. Mpaka sasa wamejitahidi sana ku-mantain akiba ya fedha za Kigeni around 5.1 billion US Dollars ambazo zina uwezo wa kuagiza vitu kutoka nje monthly kwa asilimia 4.6. Kwa hiyo, hili nawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kwenye ule mpango mkubwa, ni sekta binafsi kuzalisha ajira zipatazo 8,000,000, ndicho tulichokubaliana na ndicho ambacho tumekipeleka kwa wananchi. Ukifungua Ilani ya Uchaguzi ukurasa wa nane kipengele cha f(1) hadi (4) inasema, “kutengeneza ajira zisizopungua 8,000,000 katika sekta rasmi na isiyo rasmi kwa ajili ya vijana.” Wamesema, hayo yanaweza yakafikiwa endapo tutawekeza kwenye kilimo, mifugo, uvuvi, madini, maliasili, sekta za huduma na utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ajira 8,000,000, mwaka wa kwanza wa mpango umepita, na mwaka wa pili wa mpango umepita. Tafsiri yake ni nini? Ni kwamba mpaka sasa Serikali ilitakiwa iwe imezalisha ajira milioni 3,200,000. Namtaka Waziri mwenye dhamana ya huu mpango atakaposimama hapa atuambie wamezalisha ajira ngapi? Kwa sababu kama ni 8,000,000, maana yake kila mwaka ni 1,600,000. Kwa hiyo, kwa miaka miwili ambayo tayari tumeshaimaliza, ilitakiwa tuwe tumeshatengeneza ajira 3,200,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili nisiishie tu kukosoa, niwashauri pia kwamba hatuwezi kuzalisha hizi ajira ikiwa hatukufanya uwekezaji. Siongelei ule uwekezaji ambao ninyi mna mtazamo nao Serikalini; siongelei ule uwekezaji wa mtu anatoka nje na fedha anakuja kufanya jambo hapa. Naongelea uwekezaji wa kuwawezesha Watanzania kuzalisha. Tunaongelea habari ya kilimo, tunataka Serikali yetu iwawezeshe Watanzania kwenye kilimo, tuwe na millionaires na billionaires kwenye kilimo ambao ni Watanzania. Ukiongelea mifugo, tunataka tumwone tajiri mmoja Mtanzania ambaye Serikali hii imemtengeneza. Tunataka tumwone mvuvi mmoja, vivyo hivyo na kwenye madini. Kwa hiyo, lazima tuwe na uwekezaji ambao ni very strategic. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikilizeni niwaambie; ukanda wote huu wa Bahari kuanzia Dar es Salaam, shuka Tanga nyumbani pale, mpaka Mtwara na Lindi, ni aibu kwamba hatuna hata kiwanda kimoja kikubwa cha ku-process Samaki. Ni aibu! Sasa tunaongelea uchumi gani kama hilo hatuwezi kufanya? Uwekezaji ninaousema ni ule unaojikita kwenye big production chains. Mfano mzuri, tazama Kiwanda cha Cement kilivyo pale, uone chain ambayo iko involved kwenye kiwanda. Vivyo hivyo ndiyo itakuwa kwenye Kiwanda cha Samaki na maeneo mengine. Kwa hiyo, tujikite kwenye maeneo hayo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye Wizara hii muhimu na nyeti kwa nchi yetu. Awali ya yote, naomba niunge mkono hoja.

Nimesimama hapa ili niweze kuzungumzia mradi mkubwa wa kihistoria ambao nchi yetu inaendelea nao wa SGR. Nilisamama hapa mara ya mwisho nikauzungumzia, lakini leo nataka nizungumzie na niishauri Serikali namna bora ya ku-finance mradi huu wa SGR.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu mkubwa na mzuri kwa nchi yetu kama hatukujipanga vizuri na namna ya kuu- finance vilio vitakuwa vikubwa sana huku kuhusu barabara na mambo mengine ya miundombinu mingine. Hii ni kwa sababu fedha nyingi tunayoipata itakuwa inakwenda hapa, halafu tunashindwa kupeleka maendeleo kwenye maeneo mengine ya miradi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipo kitu kinaitwa credit rating, nimesimama hapa niishauri Serikali kufanya mchakato wa kufanya credit rating ya nchi yetu. Zipo kampuni duniani zinazofanya mchakato huu wa kui-rate nchi na faida ya kui- rate nchi ni kwamba utakuwa na uwezo, ukishakuwa rated una uwezo wa kwenda kwenye masoko ya mikopo makubwa na ukapata fedha kwa kiwango kikubwa na cha uhakika zaidi kuliko ambavyo sasa tuna-finance mradi huu kwa kutumia concessional loans.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza concessional loans zenyewe zilivyo zina masharti mengi na ambayo zinafanya sekta zetu binafsi zisiweze kushiriki kwenye maendeleo. Unapokuwa umechangua finance kwa kutumia concessional, yule anayekupa fedha ndiye anayechangua kampuni ya kusimamia, ndiye anayechagua kampuni ya kujenga pia. Tungekuwa tumejielekeza kwenye kufanya credit rating ili tuweze ku-issue infrastructure bonds, ingetuwezesha sisi kuamua nani tumpe kazi gani kwenye mradi upi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunavyozungumza nitatolea mfano Standard Charted Bank kwa kushirikiana na Export Credit Agencies walitupa sisi kama nchi mkopo wa bilioni 1.46. Mkopo huu ambao tumepewa kwa ajili ya kujenga hii SGR ni gharama kubwa ku-service mkopo huu kwa sababu gani, kwa sababu ukitumia njia hii ya kupata mkopo ni kwamba unaruhusu madalali katikati Standart Charted hana hela ya…

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kwagilwa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nampa taarifa mdogo wangu Kwagilwa kwamba tunapozungumza habari ya miradi ya kimkakati ya kimaendeleo katika nchi za kiafrika, bora uchague moja, upewe mkopo kutoka nje wenye masharti ya kwamba mradi ukiisha ukishindwa kulipa wauchukue au utafute mkopo wa bei nafuu kwenye nchi yako mradi uendelee kuwa wako. Kwa hiyo ndio mambo tunayopewa kuchagua hayo.

NAIBU SPIKA: Kabla sijakuuliza Mheshimiwa Kagilwa, Mheshimiwa Getere na Waheshimiwa Wabunge wote niwakumbushe humu ndani tumekuwa na mazoea si mabaya tukiitana nje lakini humu ndani ni Waheshimiwa, kuna wakati huwa inaleta changamoto kidogo mtu akiitwa mdogo wa mtu, kaka wa mtu, shemeji wa mtu na mambo kama hayo au mke wa mtu kwa maana hiyo hiyo.

Mheshimiwa Kwagilwa unaipokea taarifa hiyo.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge aliyezungumza inaelekea hajui hiki ninachokiongea, kwa hiyo taarifa hiyo siipokei. Nazungumzia infrastructure bonds, ni mkopo kama ulivyo mkopo mwingine na mkopo huu hauna sharti lolote la kwamba ukishindwa kulipa mradi huu unachukuliwa haiko hivyo. Uki-issue infrastructure bonds kunakuwa na watu wanao-subscribe wengi kutoka nje wenye fedha wanakupa. Hiki ndicho ninachokizungumzia.

Mheshimiwa Naibuu Spika, nilikuwa natolea mfano kwamba tulipata ile 1.6 kutoka Standard Charted, yupo Standard Charted pale, maana yake tumemlipa fedha wako Export Credit Agencies maana yake tumewalipa fedha na yote hii inaenda ina amount kwenye deni letu la Taifa, ungekuwa ume-issue bond ungekuwa umechukuwa tu fedha moja kwa moja kutoka kwa yule anayekukopesha bila kupita kwa mtu mwingine. Hiki ndicho ninachokizungumzia.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hivyo tutaweza kujenga barabara zetu za ndani kwa makusanyo yetu sasa, haya tunayokusanya kupitia TRA. Kwa mfano, Barabara ya Handeni – Kiteto – Kibirashi – Kondoa - Singida itaweza kujengwa, lakini ilivyo hivi sasa tumefanya bajeti allocation ya bilioni nne, hapo hapo kuna miradi mingine ya barabara kwa fedha hizo, tutakamalisha lini ujenzi wa barabara hizi ambazo ni za muhimu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nashauri kama tutaweza tufanye credit rating kwa kutumia Kampuni ya Standard and Poor, kama tukiweza tufanya credit rating kwa kutumia moody kama tukiweza tufanye credit rating kwa kutumia fitch.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaweza kufanya kwa kutumia kampuni mbili au tukiona ni gharama tufanye kwa kutumia kampuni moja. Tafsiri ya credit rating ni kwamba mnakuwa declared kama nchi ambayo ina uwezo wa kuhimili deni na kulipa pale inapogoma. Hiki ndio tunachokishauri na ndicho ninachokishauri kifanyike na Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunapozungumza kwenye huu mradi huu wa SGR mpaka sasa loti Na.3 haina fedha na haina mkandarasi. Mpaka sasa loti Na.4 Tabora - Isaka haina fedha na haina mkandarasi, hata hii unayoongelea loti Na.5 ya Isaka - Mwanza wamekuja Wachina hapa wameahidi kutupa 1.32 bilioni, hiyo ni concessional loans, sharti la kwanza kampuni zao mbili ndio zijenge. Ndugu zangu hatutaweza kulinda hata ubora wa mradi wenyewe, yaani mtu anapokupa, ajenge yeye, asimamie yeye, sasa wewe ushiriki wako ni upi kwenye hii? Tukiangalia kwenye sekta ya ujenzi ndio sekta ambayo imekuwa mfululuzo kwenye miaka hii ya karibuni lakini watanzania wanashiriki vipi kwenye sekta hii ya ujenzi, hawawezi kushiriki kama tunaendelea kuchagua financing za namna hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nimeongea kwa wakati, nikushukuru sana kwa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii adhimu nipate kuchangia katika bajeti ya nchi yetu kwa mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kuunga hoja mkono hoja zote mbili zilizowasilishwa ya kwanza ya Waziri wa Fedha na ile yetu ya Kamati ya Bajeti. Nimpongeze sana sana Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutuletea bajeti yenye maono makubwa kwa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii imebeba mahitaji ya Watanzania, bajeti hii imebeba matumaini ya Watanzania, bajeti hii imebeba maoni ya Wabunge, bajeti hii imebeba Ilani ya Uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi, lakini bajeti hii imebeba dira ya Taifa letu, bajeti hii imebeba maono ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan. Nasema hivyo kwa sababu bajeti hii inakwenda kutupelekea barabara zetu zote mijiji na vijijini Mheshimiwa Rais kupitia bajeti iliyowasilishwa hapa anatengua Sheria ya Usalama barabarani ili tuweze kupata Bilioni 322 kwa ajili ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais amebeba maono makubwa kwa Taifa letu kwasababu kupitia bajeti hii tunapeleka maji safi na salama kwa nchi nzima, kupitia hiyo ameamua kutengua Sheria ya Posta na Mawasiliano Sura Na. 306 ili tuweze kukusanya Trilioni 1.3 kwa ajili ya kuyafanya haya. Mama yetu amebeba maono makubwa kupitia bajeti hii kwa sababu anakwenda kufanya jambo ambalo limeshindikana kwa miaka mingi bima ya afya kwa kila Mtanzania, Mheshimiwa Rais anakwenda kutekeleza miradi yote ya kimkakati ikiwemo mradi maarufu ambao mimi huwa ninasimama hapa kuuongelea kila mara mradi wa SGR unakwenda kutekelezwa kupitia bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti hii inakwenda kututengenezea miundombinu ya elimu, kwenye hili upande wa elimu ya juu kupitia bajeti hii watoto wote wa Kitanzania ambao walikuwa wameshapata udahili kwenye vyuo na wakakosa nafasi ya kusoma kwa sababu ya fedha, bajeti hii inakwenda kuwarudisha katika vyuo. Kwa hiyo, bajeti hii ni ya Watanzania na bajeti hii ni ya kwetu na tunakwenda kuijenga nchi yetu kwa kujifunga mikanda wenyewe kama ambavyo Waziri wa Fedha alituambia hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali ukiacha maeneo haya mapya ambayo yametengua sheria nne na yakatupatia Trilioni mbili, TRA ina department Nne ukiangalia hizi department kuna moja ya muhimu sana inaitwa department ya customs na excise hii inakusanya asilimia 38 ya mapato yote ambayo TRA inakusanya yanatoka kwenye hii department hii inatafsiri kwamba kwa lengo tulilojiwekea la kukusanya mapato ya ndani Trilioni 26 ina maana kwamba Trilioni 8.4 zitakusanywa na department ya customs na exercise duty. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaitaja hii department kwa sababu ndiyo inayohudumia bandari yetu, na ndio inayohudumia viwanja vyetu vya ndege lakini ndio inayohudumia mipaka yetu, Mheshimiwa Waziri wa Fedha twendeni tukafanya mapinduzi kwenye Bandari yetu. Haiwezekani eti bandari yetu ya nchi haina vifaa vya kisasa vya kupakua mizigo na kupakia mizigo. Twendeni tukanunue vifaa hivyo ili mizigo mingi ipite kwenye bandari yetu. Hali ilivyo hivi sasa Bandari yetu inapitisha tani Milioni 17 kwa mwaka, kiwango hiki ni kidogo sana ukilinganisha na bandari ambazo tunashindana nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukafanya mapinduzi kwenye bandari kwa kununua vifaa vilevile tutafanya mapinduzi kwenye bandari kwa kuziangalia vizuri sheria tunazozitunga kwenye Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge sikilizeni niwaambie Sheria hizi za Afrika Mashariki Tanzania trading yetu kubwa ya kibiashara tunafanya na SADC tuna trade kidogo sana na East Africa, wenzetu wamekuwa wajanja sana wana tu-fix kwenye sheria hizi hasa hasa zile zinazohusu usafirishaji wa mizigo kutoka bandarini kwenda kwenye nchi tunazozihudumia. Kwa hiyo, tujipange vizuri kwenda kusimamia eneo hilo ili bandari yetu ipitishe mizigo mingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile baada ya kupitisha bajeti hapa wenzetu wa Serikali tunawapa kazi ya kwenda kuitekeleza bajeti, siku zote hapa tumekuwa tukitaja suala la monitoring and evaluation, budget circle yetu ilivyo, ina sheria hapa Bungeni kupitia Sheria yetu ya Bajeti, inaangazia draft ya budget, inaangazia approval ya bajeti ndiyo tunachokifanya hapa sasa hivi tupo kwenye hiyo stage ya approval, vilevile inapoingia stage ya execution kwenye stage ya bajeti ndipo ambapo Sheria yetu inakosa nguvu, inakosa nguvu. Kwa hiyo, tunaiomba Serikali ikalete policy ya monitoring and evaluation ili tutunge sheria na hili hapa limekuwa likizungumzwa na kukosewa kosewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuhitaji kutengeneza independent board yeyote hapa, Bunge ndiyo jukumu lake hili yaani tunachotakiwa sasa sisi ni kuendelea kusimamia Serikali kwa maana ya monitoring and evaluation kipindi tutakapokuwa tumeitunga sheria hiyo ya monitoring and evaluation ili tuweze kuisimamia Serikali vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho niipongeze sana Serikali, nimpongeze sana Mama yangu Samia Suluhu Hassan Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa sababu mimi ni shahidi tosha kwamba bajeti aliyoileta hapa imezingatia maoni yote ya Wabunge yakiwemo maoni ambayo tumeshauri hapa ya ku-finance miradi mikubwa kwa kutumia infrastructure bond, ipo hapa imetajwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze sana Serikali nimpongeze sana mama yangu Samia Suluhu Hassan Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano, kwa sababu mimi ni shahidi tosha kwamba bajeti aliyoileta hapa imezingatia maoni yote ya Wabunge yakiwemo maoni ambayo tumeyashauri hapa yaku-finance miradi mikubwa kwa kutumia infrastructure bond, ipo hapa imetajwa. Bajeti pia imechukua maoni yetu Wabunge ya kufanya credit rating ya nchi yetu, ipo hapa imekaa. Mheshimiwa Waziri nikupongeze sana, ondoa mashaka hautakuwa unpopular, utakuwa ni popular finance Minister kwa sababu umeyabeba maono ya Mheshimiwa Rais ukatuletea hapa kwa kadri ambavyo alielekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo nikushukuru sana ahsante sana kwa fursa.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nichukue nafasi hii nikushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuchangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mchango wangu ni mfupi sana. Ukurasa wa 116 wa Mapendekezo yaliyosomwa, yaliyoletwa hapa na Serikali, kipengele cha 3.3.7.3 - Ubia kati ya Sekta Binafsi na Sekta ya Umma; pana miradi pale imeorodheshwa kama 11. Sisi kwenye Taarifa ya Kamati tumeeleza jinsi ambavyo miradi hii ya PPP imeorodheshwa kwa miaka na miaka bila kutekelezwa na matokeo yake kwenye Mpango huu tunaotarajia kwenda kuwa nao, Serikali imeongeza mradi mwingine mmoja mpya. Mradi huu ndiyo umenisukuma nizungumzie eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu, kipengele K, unasema: “kuendeleza upembuzi yakinifu wa mradi wa kusimika boya la kuegesha meli za mafuta katika Bandari za Dar es Salaam na Bandari za Tanga.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu una conflict of interest na maslahi ya nchi, kuuweka kwenye utekelezaji wa kutumia sekta binafsi na kwa maneno rahisi, kuandaa huu mradi kwa kumpa mtu binafsi aufanye, kwa maneno rahisi kabisa naweza kusema hii ni hujuma kwa nchi yetu na ni jambo halikubaliki. Tusipoangalia, tunakwenda kutengeneza TICTS nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko hivi, mradi huu wa kutengeneza boya la kuegesha meli za mafuta, unagusa bandari, tena bandari mbili. Bandari ni uchumi… (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kwagilwa tuwekee vizuri ili uende tu vizuri, yaani kwamba Serikali hapa imeweka katika orodha ya PPP. Kwa hiyo, ni orodha ya watu binafsi na Serikali yenyewe. Nawe unasema kwamba ni binafsi peke yake, labda tuwekee vizuri tu.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nasema hivyo kwa sababu mradi upo kwenye upembuzi yakinifu, inamaanisha mradi haujaanza kujengwa, ina maana unaikaribisha Sekta Binafsi au mtu binafsi ashiriki kuanzia kwenye kujenga hilo boya na kwa lugha nyingine kujenga kipande cha bandari; umkabidhi kipande cha bandari ili ajenge gati kwa ajili ya meli kubwa za mafuta na gesi kuja kushusha pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inagusa habari ya usalama wa nchi, lakini inagusa habari ya uchumi wa nchi, vile vile bandari ni lango la nchi yetu. Kumpa mtu binafsi au kumshirikisha kwenye hizi hatua za awali za kujenga, kumpa miundombinu ile ya bandari, siyo jambo sahihi sana kwa mustakabali wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaelezea jambo hili kwa sababu ukiongelea meli kubwa za mafuta unaongelea pia na meli kubwa za gesi. Sisi tunazalisha gesi. Tumetoa gesi, tumeshaichimba, tumewekeza billions of money kwenye gesi na kila mwaka shirika letu linaloshughulika na habari za gesi na mafuta linatumia bilioni 50 kila mwaka kwa ajili ya utafiti kwenye mafuta na gesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kana kwamba hiyo haitoshi, tayari tumeshakopa Benki ya Exim, Dola za Kimarekani bilioni 1.2 kuitoa gesi kutoka Madimba pale Mtwara, kuitoa Songosongo Lindi, kupitia Somanga Fungu, tumeifikisha Pwani na iko Dar es Salaam. Sasa gesi yetu ile ni natural gas. Tumeshaifikisha Dar es Salaam, Serikali haina juhudi yoyote inayofanya ya kuisambaza gesi kwa wateja. Imeshafika Dar es Salaam, lakini badala yake imerukia inataka impe mtu binafsi aingize gesi nchini. Hiki kitu hakiko sawa. Hakiko sawa kwa sababu huyu mtu au hii sekta binafsi ikipewa kuwaruhusu…

MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji, Mheshimiwa Reuben, Mbunge wa Handeni Mjini, kwamba anapoendelea kushangaa hilo ashangae pia kwamba gesi hiyo ambayo inatoka Mtwara kuja mpaka Dar es Salaam inatumika kwa asilimia 20 tu. Maana yake bado gesi yetu ya ndani haijapata soko. Ahsante.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kwagilwa, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hii, tena naipokea kwa uzito sana, hasa ukizingatia kwamba taarifa hii imetolewa na Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tuwe wazalendo kwenye mambo haya. Mambo haya kwa sababu yanashirikisha mikataba na experience inaonesha kwamba tumekuwa tukifanya vibaya sana kwenye mambo ya mikataba, hasa inayogusa rasilimali kubwa kama hii. Nashauri hapa tusiingie kwenye huu mtego. Tulishaingia huko tukafanya mambo ya hovyo na ya ajabu ambayo hayawezi kuzungumzika, tusirudi huko. Tusirudi huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu, upembuzi yakinifu uendelee na ukikamilika ufanywe na Serikali. Kwa hiyo naishauri Serikali iondoe huu mradi kwenye hii orodha ya miradi inayopanga kuitekeleza kama PPP. Ni muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewashauri hili kwenye Kamati, tulifikiri wameelewa lakini wamekuja nalo kwenye floor huku na ndiyo maana na sisi tumeona tusione haya tuje tuseme hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nataka niliseme ni kwamba katika Mpango huu uliopita kwa maana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, mchango huu unatosha. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. KWAGILWA R. NHAMILO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana niungane na wenzangu kukupongeza kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika wa Bunge letu la Jamhuri ya Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana kamati yako ya bajeti pamoja na Bunge kwa ujumla tulifanya Amendment of the Road and Fuel Tolls Act Cap. 220. Marekebisho haya yalilenga kuipatia TARURA fedha kwa ajili ya barabara zetu za vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitoe taswira ndogo sana ya TARURA tunapozungumza TARURA ili angalau tufanye mapinduzi kwenye eneo hili la barabara zetu za vijijini. Handeni hususan Jimbo la Handeni mjini barabara zetu za TARURA barabara za vumbi ni 88%. Kwa Mkoa wa Tanga barabara zetu za TARURA, barabara za vumbi ni 79% na kwa Tanzania nzima TARURA ina mtandao wa barabara unaofika kilometa 144,429 zinahudumiwa na TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hizo 76% ni barabara za vumbi kwa maana ya kilometa 111,197, TANROADS inahudumia barabara zote kilometa 36,000 na katika hizo zenye lami ni kilometa 11,000 what is the myth ni kitu gani cha ajabu kwenye hiki ninachojaribu kukizungumza tumeipa TARURA jukumu kubwa sana lakini hatujaweka juhudi kubwa za kibajeti na za kitaasisi za kiteknolojia na kwa nguvu zote kujaribu kuibadilisha ili iweze kuhudumia barabara zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa takwimu hizi nilizotoa hapa ndiyo kusema kwamba barabara nyingi mtandao mkubwa wa barabara Tanzania uko chini ya TARURA. Sasa the opposite ndiyo tunachokifanya tunapeleka nguvu kubwa sana TANROADS na natambua kwamba barabara wanazohudumia ni za lami, lakini haiondoi fact kwamba kilometa hizi 144,429 ndiko ambako Tanzania waliko na ndiko ambako uchumi uliko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kusema ni nini ninachotaka kusema ni kwamba lazima tufanye mapinduzi ya namna ya approach ya kutengeneza barabara zetu kuanzia kwenye bajeti yetu inayokuja lazima tufikirie kwa namna ya tofauti. Tathmini ya dharura iliyofanywa juzi kwa uharibifu unaofanywa na mvua uliosababishwa na mvua tathmini iliyofanywa ya haraka inahitajika bilioni 120 kufanya tu marekebisho .(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukichukulia sasa ile amendment tuliyofanya ya kutoka bilioni 322 na hizo kwa hakika hatutaweza kuzikusanya zote, 120 yote inaenda kufanya marekebisho yaliyosababishwa na mvua. Which means tunakwenda ku-miss target yetu ambayo tulijiwekea kufungua barabara zetu za vijijini ninachotaka kusisitiza kama ambavyo tumefanya jitihada za makusudi kwenye SGR, jitihada za makusudi kwenye bwawa la Mwalimu Nyerere, vivyo hivyo moyo wa uchumi wa nchi yetu ni hizi barabara hizi kilometa 144,000 ambazo ziko chini ya TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo lazima tufanye mapinduzi ya namna ya kufikiri na lazima tufanye mapinduzi ya namna ya kutenga bajeti yetu. Tusii-treat TARURA kama kachombo kadhaifu dhaifu hivi ambako kako chini ya Wizara ya TAMISEMI ambako hata hivyo hata kwenye hiyo Wizara yenyewe tuna Waziri wa TAMISEMI na Manaibu Waziri wawili mmoja anajulikana ni wa afya na mwingine anajulikana ni wa elimu. Yaani hata hiyo TARURA pale huioni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dhati kabisa ni lazima tufanye mapinduzi bajeti inayokuja tutenge fedha nyingi lakini zienda angalau zikabadilishe barabara zetu zitoke kuwa za vumbi ziende kwenda kuwa changarawe. Lakini na siku za usoni siku za baadae tujifunze teknolojia kwa wenzetu tutengeneze barabara zetu kwa teknolojia ambayo ni cheap.

NAIBU SPIKA: Malizia.

MHE. KWAGILWA R. NHAMILO: Kama ambavyo alishauri Mheshimiwa Rais barabara zetu tuzifanyie mapinduzi tuende kwenye teknolojia ya kati ambayo siyo gharama sana lakini barabara tuzijenge ziweze ku-survive na ku-sustain kwa muda mrefu.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia ripoti za Kamati zetu tatu. Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa, Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma na Kamati ya Hesabu za Serikali. Mimi nitajielekeza zaidi kwenye Kamati hii iliyochambua ripoti ya CAG ya Hesabu za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili nimeisoma vema ripoti ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwenye eneo la Mashirika ya Umma. CAG amepitia Shirika la Bandari (TPA), TTCL, TANESCO, Shirika letu la Nyumba - NHC na TRC. Nitajielekeza kwenye Shirika la TANESCO na hususan kwenye mradi mkubwa tulionao. Mradi wa Trilioni 6.5 wa Bwawa la Umeme la Mwalimu Julius Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, CAG anasema alivyokwenda kuangalia bwawa hili alikuta ujenzi umechelewa kuisha kwa asilimia 46.45. Bwawa hili ni la muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu, Watanzania wanahitaji bwawa hili likamilike ili tuweze kupata umeme wa uhakika. Viwanda vyetu vinahitaji bwawa hili likamilike ili viweze kufanya uzalishaji. Miradi yetu ya REA tunayoitengenza sasa inahitaji bwawa hili likamilike ili iweze kupata source ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, gridi yetu ya Taifa ili iwe na umeme stable inahitaji bwawa hili likamilike ili tuweze kupata umeme wa uhakika. Vilevile, gharama zetu za umeme ziko juu, umeme wa maji ni umeme cheap kuliko umeme wowote, Watanzania wanahitaji bwawa hili likamilke ili waweze kupata umeme wa gharama nafuu. Sasa taarifa zilizopo hivi sasa, ukizingatia hii taarifa ya CAG, kwamba ujenzi umechelewa, bwawa lilitakiwa likamilike mwaka huu mwezi wa Sita, mwezi wa Sita umepita bwawa halijakamilika, hivi sasa ujenzi uko asilimia 74 na bado hujakamilika, Mkandarasi na Serikali wanabishana. Mkandarasi anaomba kuongezewa miaka mingine miwili zaidi na kwa maana hiyo kwa mujibu wa Mkandarasi, bwawa hili litakamilika mwaka 2024. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali wao wanasema kwamba wamekataa kumwongeza miaka miwili, badala yake wamemwongeza mwaka mmoja. Nataka nilipitishe Bunge hili sababu ambazo zimetolewa na Mkandarasi na mpaka wakafikia kumwongeza mwaka mmoja, pamoja na kumwongeza huo mwaka mmoja yeye bado mpango kazi ambao ameuweka Serikalini unaonesha ni miaka miwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya kwanza, anaomba nyongeza ya muda na kuongezewa gharama kwa sababu watengenezaji wa mitambo walijitoa. Sababu ya pili, anaomba nyongeza ya muda na gharama kwa Watanzania kwa sababu ya taarifa za miamba. Sababu ya tatu, anaomba kuongezwa muda na ongezeko la gharama kwa sababu pale site anasema umeme haumtoshi. Sababu ya nne na ya mwisho, anaomba kuongezewa muda na gharama kwa sababu njia ya kupelekea vifaa site ni mbaya. Jambo hili halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa Trilioni 6.5, kodi za Watanzania, bado inafanyika janjajanja ya kutaka tena kuongeza gharama ya mradi huu? Kuongeza gharama ya muda na gharama ya fedha? Serikali inasema sababu zilivyotolewa haikukubaliana nazo. Kama hawakukubaliana nazo nataka Waziri mwenye dhamana akija hapa atuambie, kama sababu hizi hamkukubaliana nazo kwanini mmemwongeza mwaka mmoja? Kwa nini mmekubali kumwongeza mwaka mmoja ilihali mpangokazi wake unasema anataka miaka miwili, nani mnamdanganya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali na Mkandarasi wameunda Bodi inayoitwa DAB, (Dispute Adjudication Board) kwa ajili ya kufanya suluhu ya haya. Mkataba Serikali umesema kwamba sababu hukubaliani nazo, inamaana ulitakiwa ukabidhiwe kazi mwaka huu, mkataba unasema nini kama kazi haijakabidhiwa? Kwa nini madai ya Serikali kwa Mkandarasi hapa hatuyaoni? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kushangaza mpaka sasa Mkandarasi tumeshamlipa asilimia 65.9 ya fedha. CAG anasema mradi umechelewa, Mkandarasi tumeshamlipa asilimia 65.9 ya fedha zote yaani Trilioni 4.3, lakini Serikali badala ya kulipa trilioni 4.3, wamemlipa trilioni 4.43. Wamemlipa ziada ya shilingi bilioni 113. Sababu waliyoitoa ya kulipa ziada ya shilingi bilioni 113 wanasema eti ni mabadiliko ya kubadilisha dola na shilingi.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Twaha Mpembenwe.

T A A R I F A

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba tofauti hii anayoizungumzia hapa ya fedha ya Bilioni 113 fedha za walipa kodi zilizolipwa kwa uwiano wa kawaida tu, kwa fedha tulizokuwa tumezizoea kawaida kwa kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI, Shilingi Milioni 500 inajenga kituo kimoja cha afya. Kwa hesabu za kawaida hivi ni vituo 226 vya afya ambavyo vingeweza kujengwa katika Jimbo la Handeni, Kibiti na Majimbo mengine yote hapa Tanzania.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kwagilwa unaipokea taarifa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo taarifa naipokea, shilingi 113,196,370,381.06 eti kwa sababu ya kubadilisha dola na shilingi, mkataba gani huo kwenye nchi ya wanasheria wasomi? Yaani unawezaje kuwa na mkataba wa hivyo? Eti kwenye malipo mkianza kulipana wewe ukianza kutafuta dola unapoteza bilioni 115. Vituo 226 vya afya! Hatuwezi Kwenda hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sisi wengine lazima tuwaambie tu, kazi yetu hapa ni kuwaambieni ukweli. Sisi sote tutapita lakini Tanzania itabaki. Bilioni 113 kubadilisha shilingi na dola, naongelea bilioni; hii si sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu mkubwa mpaka sasa taifa halina uhakika kama utakamilika. Kwenye hili tusitake kuumauma maneno. Kutokukamilika kwa mradi huu kunafanya wananchi wa Handeni hawatapa umeme; kutokukamilika kwa mradi huu kunafanya ndugu Waheshimiwa Wabunge kwenye majimbo yenu miradi ya REA tunayopeleka haitakuwa na source ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka niseme kwa lugha fupi, kwamba hii ni hujuma. Tunanunua umeme kwa gharama kubwa sana kutoka mitambo ya kukodisha. Kwa nini hatumalizi wa kwetu? Kwa nini mtu asishawishike kuamini kwamba hii ni hujuma? we cannot go like that as a nation, hatuwezi kwenda hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa sababu leo tuko hapa kuisimamia Serikali ninamwomba Mheshimiwa Spika, aunde kamati tuchunguze hili. Haiwezekani mradi ambao ni tegemezi kwa taifa usikamilike kwa wakati, na bado panaanzishwa longolongo nyingine zitakazopelekea tulipe zaidi na tukabidhiwe mradi baadaye zaidi, na huenda hata usikamilike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna miradi mikubwa tu nchi hii ya kwanza SGR trilioni 16, huu tunaotengeneza. Mradi wa pili ni huu takriban trilioni saba why can’t we be serious on this.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa muda nawashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa fursa hii ya kunipa kuchangia kwenye ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa uelekeo huu wa bajeti ambazo tumezijadili kwenye Kamati zetu na sasa tunazijadili kwenye Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2011 tulitunga Sheria ya Manunuzi ya Umma na baadae tukaifanyia marekebisho mwaka 2013. Sheria hii ya Manunuzi ya Umma ni sheria muhimu sana kwa sababu zaidi ya asilimia 70 ya fedha zote tunazopitisha hapa kwenye bajeti, tunakwenda kuzitumia kupitia Sheria hii ya Manunuzi ya Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Sheria hii ya Manunuzi ya Umma tunamuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu na Serikali walete Muswada tuifanyie marekebisho kwenye kipengele cha ununuzi wa madawa. Sheria hii tulivyoitunga ni cross-cutting, kununua mabati tunatumia sheria hii, matofali sheria hii, kununua vifaa vingine ni sheria hii pia. Ni lazima sheria hii tuirekebishe ili kipengele cha ununuzi wa madawa kiwe na focus yake, kiwe na umuhimu wake, kiwe na utofauti wake, nitaelezea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii kwenye ununuzi wa madawa inatoa mianya mitatu mibaya. Mwanya wa kwanza unaitwa price rigging au price curtailing. Sheria kwa jinsi ilivyo tunapokwenda kuitekeleza kupitia mtandao wa TANePS, hasa ukizingatia kwamba MSD inanunua madawa asilimia 90 tunayaagiza kutoka nje. Kwa hiyo, sheria hii inaitaka MSD kutangaza tender kupitia mfumo wa TANePS na hapa hushindanisha wazabuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wazabuni hawa kwa mara nyingi kumekuwa na tabia ya watu kujipanga, wakijipanga anayechukuliwa ni yule mwenye bei ya chini, kiuhalisia ukiangalia bei ya chini, ambayo wao wanaiita lowest evaluated bid ukiangalia hii inayoitwa bei ya chini siyo bei ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mifano MSD walipotangaza kununua mashine inayoitwa Hematology Analyzer mzabuni aliye-tender bei ya chini ali-tender kwa Shilingi Milioni 117 wakati bei ya soko halisi ni Shilingi Milioni 20. Nitatoa mfano wa pili, MSD walipotangaza tender ya mashine inayoitwa immunology analyzer, mzabuni aliye-tender kwa bei ya chini ali-tender kwa Shilingi Milioni 149 ilhali mashine hii bei ya soko inauzwa Shilingi Milioni 37. Nitatoa mfano wa tatu, MSD ilipotangaza kununua mashine ya kuchakata maji kwa ajili ya kutumika katika kusafisha damu, mzabuni aliye-tender bei ya chini ali-tender kwa Shilingi Milioni 129 ilhali bei halisi ya mashine hiyo ni Shilingi Milioni 32. (Makofi)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Mpembenwe.

T A A R I F A

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba kidonge cha kilo moja cha kuweza kutengeneza dawa ya kutoa madoa yaani ile JIKI soko halisia inauzwa kwa Shilingi Milioni Nne lakini MSD wamenunua kwa Shilingi Milioni 262 na ushahidi upo. (Makofi)

MWENYEKITI: Unapokea taarifa hiyo Mheshimiwa Kwagilwa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii naipokea na ninataka nisisitize kidonge kimoja cha kilo moja cha kutengeneza JIKI bei sokoni ni Shilingi Milioni Nne na MSD kidonge hiki wamepelekewa bei ya Milioni 262! (Makofi)

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili halikubaliki duniani wala mbinguni. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa subiri kidogo Mheshimiwa Kwagilwa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ummy Mwalimu, Waziri wa Afya.

T A A R I F A

WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mchangiaji. Ni kweli Sheria ya Manunuzi ya Umma inaweza ikawa na changamoto lakini bado haizuii MSD kununua dawa moja kwa moja kutoka kwa wazalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2016 Rais Magufuli alituelekeza tuachane kununua dawa kutoka kwa madalali, tununue kutoka kwa wazalishaji, mwaka 2017 angalieni vyombo vya habari. Tulifanya press tuliweza kushusha bei za dawa kwa zaidi ya asilimia 40, kidonge cha Amoxicilline kilichokuwa kinauzwa Shilingi 11,000 tulikinunua kwa Shilingi 4,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mashuka kutoka Shilingi 22,000 tuliyashusha mpaka Shilingi 11,000. Tatizo lililopo MSD siyo tu Sheria ya Manunuzi ya Umma, mipango mibaya ya utekelezaji wa manunuzi ya umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, MSD hiyo hiyo kwa Sheria hii ilianza kufanya vizuri. Kwa hiyo, hiyo ni taarifa nataka kusema sheria ipo lakini tunaweza tukabadilisha sheria, lakini kama hatuna mipango mizuri ya procurement ya dawa, vifaa na vifaa tiba tatizo la MSD litaweza kuendelea. Mheshimiwa Rais alishatoa maelekezo Wizara tunayafanyia kazi. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Waziri kwa taarifa. Mheshimiwa Kwagilwa unapokea taarifa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea taarifa kwa maana moja nzuri sana kwamba Mheshimiwa Waziri…

MWENYEKITI: Haya na ninakuongezea dakika moja na nusu kwa kumalizia hoja yako.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anakubaliana kwamba lipo tatizo, kama tunataka kumsaidia Mheshimiwa Rais, ambaye amekwishatoa maelekezo ya kwenda kumulika MSD tumsaidieni sisi kwa sababu sehemu yetu ni kutunga sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria hii inayo shida, shida hii inatupeleka hata Bima yetu ya Afya haifanyi kazi. Huwezi kuwa na Bima ya Afya inayohudumia vifaa ambavyo viko overpriced. Madawa yapo overpriced, vifaa vinavyotumika viko overpriced, Bima yako ya Afya itashindwa ku-cover haiwezi! Siyo tu hivyo, namuongelea mwananchi wa Kata ya Kwamagome anayeumwa figo akafanye diagnosis kwa Shilingi 300,000 haiwezekani! Shilingi 500,000 haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuongelea mwananchi wa Kata ya Malezi, namuongelea mwananchi wa Kwaluala, mwananchi wa kwa Sindi haiwezekani! (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MWENYEKITI: Taarifa kutoka wapi?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili...

MWENYEKITI: Mheshimiwa Naibu Waziri Daktari Godwin Mollel una taarifa?

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti…

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilindie muda wangu umechukuliwa. (Makofi)

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wa Afya ameshalielezea vizuri, jambo lenyewe liko straight forward na akasema Rais wetu wa Awamu ya Tano alishaeleza kwamba tuendeni viwandani. Kwa hiyo, anachochangia ni kizuri sana hatuna shida, lakini tukishatoka tukaelekea upande wa viwanda tumekata huo mzizi wa fitina, na vyombo vyetu vingine vikifanya kazi vizuri kuhakikisha wanasimamia hakuna namna yoyote hayo yanayosemwa wakati hii Nchi ina vyombo vyake ninakuhakikishia hakitatokea hicho. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri wa Afya ameshatoa maelekezo na kazi hii inaendelea.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Mollel kwa taarifa yako. Mheshimiwa Kwagilwa, unapokea taarifa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, jitihada zote hizi za Serikali inaonesha kwamba lipo tatizo. Ninachotaka niseme ni nini?

Mimi nitamshangaa sana Mtanzania yeyote ambaye haelewi hiki ninachokisema hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia kwamba Mheshimiwa Rais amepeleka Shilingi Bilioni 200 MSD na bado Watanzania hawana madawa kwenye hospitali! Mheshimiwa Rais amepeleka shilingi bilioni 200 na bado hazitoshi kununua dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fikiria mazingira ambayo mwongozo uliotolewa na Serikali… (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Kwagilwa kwa mchango wako sasa namuita Mheshimiwa…

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia ripoti zetu za Kamati zetu hizi mbili na specifically nataka nichangie ripoti ya Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukurasa wa kumi na moja wa taarifa iliyowasilishwa na Mwenyekiti wetu wa Kamati hii unaongelea habari ya utekelezaji wa miradi ya kimkakati katika halmashauri nchini. Wanasema Bunge limeazimia kupitia upya miongozo ya namna ya kutekeleza miradi hii, na kwamba Kamati imejulishwa na Serikali kwamba tayari imeshafanya mpango wa kushirikiana na UNCDF kwa ajili ya kuandaa mipango hiyo mipya ili miradi hii iweze kutekelezeka fairly.

Mheshimiwa Spika, miradi hii ya kimkakati ni kielelezo kinachoishi, kinachoonesha namna gani kama Taifa hatuko sawa katika ugawaji wa rasilimali za nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, miradi hii ya kimkakati ni kielelezo kinachoishi, kinachoonesha kwamba kama Taifa hatuko sawa katika ugawaji wa rasilimali zetu, nitaelezea.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia miradi hii ya kimkakati sharti lake kubwa la kwanza lilikuwa ni halmashauri itenge fedha, halafu ipeleke andiko. Kwa jinsi halmashauri zetu zinavyotofautiana kimapato mathalani unapozungumzia Halmashauri ya Handeni Mjini own source yetu hata milioni 700 haifiki, tutaigawaje gawaje hiyo fedha mpaka tupate fedha ya kuwekesha ili Serikali ije kutuunga mkono kupata mradi wa kimkakati. Hiyo ndiyo kusema wale giants wote wataendelea kupata miradi hii, halafu sisi ambao siyo giants tutaendelea kukosa miradi hii. Tunatengeneza Taifa ambalo linawapendelea wengine na kuwatweza wengine. (Makofi)

Kwa hiyo, nilikuwa naomba na naiomba sana Serikali huu mwongozo wanaouandaa kwanza pana kitu cha ajabu sana, mimi nilifikiri kwamba mwongozo wanamna ya kugawanya miradi hii Wizara tu ingeweza kufanya kwa maana Serikali tu inaweza kufanya. Yaani sisi kuandaa muongozo wawape Mradi uende mpaka tulete UNCDF? Yaani ndiyo Serikali mmefikia hapo? Yaani kwamba ninyi hamuwezi kufikilia kabisa namna gani tugawanye fairly mpaka tulete hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu jinsi ilivyo unavyogawanya kwa kupeleka kwenye miji mikubwa peke yake unasababisha vijana wetu kutoka Handeni na maeneo mengine ya Tanzania wahame kwenda kwenye hii miji mikubwa, unaenda kusababisha mrundikano pale, watoto wetu wanatafuta ajira pale, vijana wetu wamejaa Dar es Salaam, wamejaa Arusha, wamejaa Mwanza wametoka kwenye vijiji huko kwa sababu hatupeleki miradi hii.

Mheshimiwa Spika, nitaongelea kwa pamoja na mradi huu wa TACTIC maana ni yote hii ni miradi inayokwenda sambamba. Mradi huu wa TACTIC unatupa master plan kwenye mradi, unatupa barabara, unatupa soko na unatupa stendi, cha kushangaza hii miji inayosema ni giants na inayopewa hii miradi ya kimkakati ndiyo hii hii tena ambayo ipo kwenye TACTIC na imepewa kipaumbele ya kwanza, yaani kule kwenye mmewaweka tena kwenye TACTIC na ambako nako watapata soko, halafu unaacha miji kama Bunda inashangaa shangaa, Handeni Mjini tunashangaa shangaa, Ifakara tupo tupo tu, Kondoa, Mafinga, Makambako tunatengeneza Tanzania gani hiyo ya kujenga Dar es Salaam kila siku?

Mheshimiwa Spika, lazima tufike mahala rasilimali za nchi yetu tuzigawe kwa usawia na hili niwaombe wenzetu wa TAMISEMI wakae na watu wa Wizara ya Fedha, kaeni na watu wa Wizara ya Fedha kama fedha hizi tulizonazo zetu za mapato ya ndani na hizi tulizokopa World Bank hazitoshi kuendeleza miji yetu, kaeni na Wizara ya Fedha ili twende tukatatue tatizo hili kwa kutumia Sera za Kikodi. Hivi nani hapa anaweza akasimama aniambie eti Mbuga ya Katavi siyo bora kuliko Serengeti? Katavi iko vile leo ni kwa sababu miundombinu iko mibovu tu pale. Kwa nini hatugawanyi rasilimali hizi kwa kufuata huo uhalisia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali na hususani TAMISEMI waachane na hii habari ya kuzunguka nchi nzima eti wanatambua vyanzo vya mapato. Sasa ukienda Handeni unatambua vyanzo vya mapato? Utakuta sisi ni mnada tu pale kila siku sisi ni mnada tu. Kutengenezwe district economic profiles kwa nchi nzima ambazo zitaonesha…

MHE. ENG. ISACK A. KAMWELWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Nhamanilo kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Isack Kamwelwe.

T A A R I F A

MHE. ENG. ISACK A. KAMWELWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kumpa taarifa mzungumzaji anaeendelea kwamba mwongozo wa bajeti ya mwaka ujao wa fedha TAMISEMI wameelekeza halmashauri zinazokusanya mapato chini ya bilioni moja kwenye mapato yake zitenge asilimia 20 tu ya maendeleo, lakini zile ambazo zinapata zaidi ya bilioni tano zinatenga asilimia zaidi 50 kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Kwa hiyo, unachozungumza kama Handeni milioni 700 asilimia ishirini tu zitaingia kwenye maendeleo, lakini zingine zote ziingie kwenye OC. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Nhamanilo unaipokea hiyo taarifa hiyo?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, namuheshimu sana mzee wangu, kama amenisadia nashukuru sana unajua nina moto hapa. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nimepokea taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Reuben, unaipokea taarifa ya Mheshimiwa Isack Kamwelwe?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ninaipokea taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachokisema tusiwe waumini wa vyanzo vya mapato, tunachotakiwa ni kutengeneza district economic profiles na siyo hizi ambazo mmeweka kwenye website eti district economic profile inaongelea tu watu, eti kuna watu idadi kadhaa, idadi kadhaa tengenezeni district profiles ambazo zinaangalia potentials za eneo husika ili mjue ni mradi gani mkiwapelekea unawa-boost. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunacho Chuo cha Mipango, Mheshimiwa Waziri wa Fedha upo, chuo hicho mnacho wenyewe kwa nini makitumii kupanga? Kwa nini hamkitumii kutengeneza hizi Districts profile kwa ajili ya kuangalia potentials za uchumi wa kila eneo ili tupeleke fedha maeneo hayo kwenye miradi hii ya kimkakati tuka- boost eneo lile? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninatamani sana na ninashauri kwenye maazimio yetu tuongezee azimio, ikiwa tu hii miradi ya kimkakati ambayo Serikali imekuwa ikiiendesha miaka yote hawakuwa hata na mWongozo mpaka leo, na yenyewe ni ya bilioni kama 200 na kitu, je, itakuwaje kwenye huu mtadi mkubwa wa TACTIC ambao ni wa karibu bilioni 600? Wanauendeshaje? Ile tu ya kujenga soko, stendi, hapa na pale hawakuwa hata na mwongozo, huu mkubwa! Ni nani aliyewaambia kwamba, hii first tire inatakiwa iwe hii Miji, kwa nini isiwe Handeni na sehemu nyingine? Tuweke azimio la kwamba mradi huu wa TACTIC ukapitiwe upya na upangwe kulingana na namna ambavyo Halmashauri zinazohitaji kusaidiwa kwa uharaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ambalo ningependa nimalizie…

SPIKA: Sekunde 30, malizia.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ambalo ningependa nimalizie ni hapohapo kwenye kuangalia sera za kikodi kulingana na eneo husika. Kwa mfano, Tanga tunalima mkonge, kwa nini isiwekwe sera ya kikodi kuliendeleza eneo la Tanga kwenye uzalishaji wa mkonge? Mathalani, Mwekezaji yeyote atakayewekeza Tanga ndani ya miaka hii 20 hatatozwa corporate tax. Eeh! ni mfano tu, si watu wote wataenda ku-flock huko? Kwa mfano, Katavi unasema Mwekezaji yeyote atakayejenga hoteli corporate tax yake tutamtoza tano siyo kwamba watu watapeleka hoteli huko? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama watu wa Serikali wamechoka kufikiria wapishe hizo siti wakalie watu wengine wafikirie. Baada ya kuyasema haya nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi/Kicheko)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii na mimi nichangie Kamati zetu mbili zilizowasilisha hapa leo, Kamati yetu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama na Kamati yetu ya Bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia upande wa taarifa iliyowasilishwa na Kamati yetu ya Bajeti na hususan ukurasa wa 62 wa taarifa, kipengele kile cha 6.5. Kamati inazungumzia ujenzi wa barabara kwa mfumo wa uhandisi, usanifu, manunuzi, ujenzi na utafutaji wa fedha kwa maana ya EPC+F. Ninaishukuru sana Serikali kwamba katika mpango huu ipo barabara maarufu ya Handeni - Kibilashi - Kiteto - Kondoa - Singida ambayo nayo imebahatika kuingia humo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na barabara hizi tunazozijenga, lipo jambo moja la ajabu sana tunalifanya kama Taifa. Nchi yetu ina mtandao wa barabara wenye thamani inazofikia Shilingi Trilioni 21. Barabara za kitaifa zina kilometa 36,361 na zina thamani ya Shilingi Trilioni 18. Barabara zetu za Wilaya zina mtandao wa kilometa 143,881 zenye thamani ya Shilingi Trilioni 2.8.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kushangaza pamoja na kuwa na asset hii kubwa ya kitaifa inayosaidia uchumi wetu, hatuifanyii matengenezo. Hivi sasa barabara zetu za kitaifa zile kubwa na ambazo ndiyo mrija wa uchumi wetu zinahitaji matengenezo yanayokaribia Shilingi Trilioni 2.4 na Serikali imekuwa ikija hapa inadai haina fedha hizo za kukarabati barabara hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili tusipoliangalia litakuja kutuingiza kwenye gharama kubwa na litakuja kufanya uchumi wetu udhoofu, wananchi wetu wasafiri kwa shida, mizigo isafiri kwa taabu, vilevile watu waliopo kwenye sekta ya uendeshaji ya usafirishaji wataendesha shughuli zao kwa gharama kubwa sana ya kununua vipuli kwa sababu ya barabara mbaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakupa mfano, athari ambazo zinaweza zikapatikana tukichelewa kufanya matengenezo ya barabara kwa kadri ya wataalam wanavyoelekeza. Miaka kadhaaa iliyopita tuliacha kufanya matengenezo ya barabara karibia 13, tukaziacha tu mwaka wa 11, 12 nyingine mpaka mwaka wa 20 tukaziacha. Matengenezo yale yalikuwa yagharimu Shilingi Bilioni 250, hatukufanya. Tulivyokuja kufanya, tumekuja kufanya matengenezo hayo kwa Shilingi Trilioni 1.28, ndiyo kusema tulikula hasara ya Shilingi Trilioni Moja nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sielewi kwanini Serikali inajivuta vuta na sielewi kwanini Serikali inajizungusha zungusha kukarabati barabara zetu hizi za kitaifa ambazo nakwenda kuzitaja hapa ziingie kwenye Hansard kwa kumbukumbu.

Barabara ya Kibaha - Mlandizi, Chalinze - Ngerengere, Melela - Iyovu, Igawa -Uyole, Uyole - Songwe, Mlandizi - Chalinze, Same - Himo, Himo - Arusha, Rusahunga - Rusumo, Shelui – Malendi - Nzega kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Nyanguge – Mwanza – Mara - Border, Makutano - Sirari, Usagara-Mwanza, Mtwara – Mingoyo - Masasi, Madaba - Makambako, Songea -Madaba, Ipole - Miemba, Rungwa - Ipole, Nzega - Manonga, Mwanza - Shinyanga - Usagara, Uyole - Kasumulu, Kobelo - Nyakasanza, Songea - Peramiho, Mikumi - Kidatu, Lupilo - Mahende na Himo -Marangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hizi ukikuta barabara ya chini ina umri wa miaka 17. Barabara yenye umri mkubwa katika hizi kuliko zote ina umri wa miaka 37. Kwa nini tunakuwa hivi? Yaani ni kweli kwamba hatuoni umuhimu kabisa wa kutafuta hii Shilingi Trilioni 2.4 tukafanya ukarabati wa barabara hizi? Mfuko wetu wa Bodi ya Barabara, kwa mwaka makusanyo yake ni kama Shilingi Trilioni moja. Vyanzo vyake vya mapato ni tozo za mafuta ambazo zina-constitute karibia asilimia 97 ya fedha zote wanazopata, tozo za magari ya kigeni na tozo za kuzidisha uzito.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa vyanzo hivi havitatosha kukarabati barabara zetu na barabara ukiitengeneza leo ukaikarabati unaipa uhai mrefu mwingine wa kuishi. Kwa hiyo, ninaiomba sana Serikali na kwenye maazimio yetu kama Bunge tuweke maazimio kwamba Serikali lazima ije hapa na mapendekezo siku zijazo ya vyanzo vipya vingine vya mapato kwa ajili ya Bodi ya Mfuko wa Barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bodi ya Barabara wanafikiria kutumia infrastructure bond kama sehemu mpya, nakubaliana nao ni chanzo kizuri, wanataka kwenda kutoza, kuweka tozo kwenye gesi asilia, kwenye yale magari ambayo yanatumia gesi asilia, siyo jambo baya. Wanataka kutoza kwenye toll bridge na wanataka kutumia hizi njia ya EPC+F.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba nilishukuru barabara ya Handeni – Kibilashi - Kiteto kwenda kwenye hii njia ya EPC+F, kuna haja kubwa kama nchi, huu mfumo tunaotaka kuuendea wa EPC+F tukaupitia upya. EPC+F ina- implication moja kwa moja kwenye Deni la Taifa. Kwa hiyo, ni vizuri Bunge lako likaambiwa, kwa mfano zile barabara Nane ambazo zimetajwa kwamba zinajengwa kwa EPC+F mpango huo umefikia wapi na implication yake itakuwaje? Watawezaje ku-spread hiyo? Kuliko tukawa tunakuja hapa kuwaaminisha wananchi barabara zinajengwa halafu hazijengwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema haya, nakushukuru sana, nilitamani kushauri eneo hilo, matengenezo ya barabara, Shilingi Trilioni 2.4, Serikali itoe maelezo na iweke kwenye mikakati yake kuja hapa na vyanzo vipya kwa ajili ya Bodi yetu ya Mfuko wa Barabara. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii ambayo iko mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, moja kati ya maeneo ambayo yanahitaji sana kusaidiwa ni Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kwenye maelezo yao kwenye Kamati mbalimbali ambazo wamefika na kwa mujibu wa taarifa ya Kamati yetu ya Bunge inayosimamia Wizara hii ya Katiba na Sheria, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali inahitaji ipewe fedha kwa ajili ya kwanza, mafunzo maalum kwenye maeneo ya Uandishi wa Sheria; Pili, kwenye eneo la masuala ya utawala; na Tatu, ni katika eneo la mikataba. Kwamba wanahitaji wapewe fedha kwa ajili ya mafunzo maalum kwenye hayo maeneo matatu niliyoyataja.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nisizungumzie hili la Uandishi wa Sheria na naomba pia nisizungumzie hili la masuala ya utawala, nataka nizungumzie hili la eneo la mikataba.

Mheshimiwa Spika, kutoiwezesha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, kutoipatia fedha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ili wataalam wake wakapate mafunzo kwenye eneo hili la mkataba ni gharama kubwa sana kwa nchi yetu. Fedha ambazo walikuwa wameomba Milioni 300, kutokuwapa Milioni 300 ni gharama kubwa sana kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, wakati naendelea kuelezea nitatoa mfano kwa nini ni gharama sana kwa nchi yetu, kwa maana hiyo nimesimama hapa siyo tu kuchangia, lakini kulishawishi Bunge kwamba ni lazima tusimame kidete kuhakikisha kwamba Serikali inapeleka fedha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ajili ya kuwapeleka Wataalam wetu wajifunze mambo ya mikataba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tusipo-train watu wetu kwenye eneo hili la mikataba nchi yetu itashindwa kunufaika na rasilimali tulizonazo. Hivi sasa kama Taifa tunajielekeza kwenda kuwekeza kwenye LNG, tunajielekeza kwenda kuwekeza kwenye Uchumi wa Blue ambao ni Uchumi wa Bahari. Kote huku tutatakiwa kuingia mikataba mbalimbali, tusipoiwezesha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Sheria, tutaishia kuwa watazamaji na rasilimali zetu hatutanufaika nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano mmoja tu ili niijenge hoja yangu vizuri na Bunge hili liweze kunielewa kwa nini nasisitiza tupeleke fedha Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali Milioni 300 iliyokuwa imeombwa na majibu ya Serikali yamekuwa tu ni mepesi, eti ukomo wa bajeti umefikia hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano ninaotaka kuutoa ni kwamba, majuzi Serikali yetu iliingia mkataba na kampuni ya Baker Botts ya Uingereza kwa ajili ya kutusaidia ile Government Negotiation Team itakayopatikana, kwenye hili nimshukuru sana Mheshimiwa Rais na nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kumteua Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi kuwa Mkuu wa Government Negotiation Teams ambazo zitakuwa zinatengenezwa. Sasa kampuni hii ya Baker Botts ikitufanyia kazi kwa miaka miwili tunailipa Dola Milioni Tatu na Nusu hiyo ni takriban Bilioni Nane ya kitanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunafanya hivyo kwa gharama tu ya kushindwa ku-train watu wetu! Umeombwa Milioni 300 unashindwa ku-allocate, halafu uko willing kulipa Bilioni Nane kwa kampuni moja kwa mkataba mmoja, this is ridiculous. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaingia mkataba wa aina hiyo tukiwa na facts hizi zifuatazo: Nchi yetu ina Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali toka mwaka 1961 miaka 60 sasa; Nchi yetu imeshakuwa na Geology Department kwenye University of Dar es Salaam toka mwaka 1974 which means tuna wataalam wa geology, tuna wataalam wa mambo ya Oil and Gas na ambao pengine hawapo nchini kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, nilibahatika wakati mmoja kwenda Texas - Marekani nikakutana na Watanzania wengi sana wenye utaalam wa mambo ya Gas and Oil, sasa tunapoingia mikataba hii halafu kwa kisingizio tu cha kusema eti hatuna wataalam! Tusiwe tunajiangalia kwenye Wizara za Serikali kwamba kama hatuna mtaalam ndiyo tuna- assume nchi nzima haina wataalam. Tujengeni utamaduni wa kuwatumia watanzania wenzetu ambao wana ujuzi hata kama wako nje ya nchi, we can access them! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naongea haya tumeingia mkataba huu tukiwa na TPDC, Shirika ambalo lina wataalam wa Oil and Gas, Shirika lipo toka mwaka 1969, lina miaka 53 tunaongelea jambo hili tukiwa tunayo Faculty of Law ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambayo ilianza hata chuo chenyewe kabla hakijaanza mwaka 1961, ina miaka 61.

Mheshimiwa Spika, wataalam wote hawa tunao wamefika mpaka level ya PhD, eti leo kwenye mkataba Watanzania hatuwezi kusimama kusema mpaka tutafute mtu atusemee, atufundishe cha kusema, atufundishe ku-negotiate, ilihali tuna wataalam wa kwetu! Tunalipa fedha halafu tumeacha kupeleka halafu tumeacha kupeleka bajeti kwa wataalam wetu kuwa-enhance what is this? Tumuungeni mkono Mheshimiwa Rais yeye ameshaonyesha njia nasi wasaidizi wake twendeni tumuunge mkono.

Mheshimiwa Spika, naomba niishie hapa, nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii angalau ya dakika chache nami niweze kuzungumzia mambo ya maji Jimboni kwangu Handeni Mjini.

Mheshimiwa Spika, mara ya mwisho wananchi wa Handeni Mjini kupata mradi wa maji ilikuwa ni mwaka 1974, na mradi ule ulikuwa ni wa miaka 20 life span yake. Hiyo ndiyo kusema kwamba tuna miaka karibia 30 wananchi wa Handeni hatujawahi kupata mradi mkubwa wa maji. Sasa nimesimama hapa leo kutoa shukrani zangu nyingi sana kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Rais wa Awamu ya Sita kwa namna ambavyo ameiangalia Handeni kwa jicho la kipekee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kutoa shukrani hizo kwa kaka yangu, ndugu yangu, Waziri wa Maji, Mheshimiwa Aweso pamoja na Naibu wake, na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Eng. Sanga. Niendelee kusema kwamba Wizara hii ya Maji kwa sababu inagusa matatizo makubwa sana ya Watanzania, kwa kweli inastahili kuwa na watu wa aina ya viongozi tulionao hapo kwenye hiyo Wizara. Ingekuwa ni kwa uwezo wangu, na kwa sababu sisi ndio washauri wa Serikali, tunashauri Waziri huyu aendelee kuwepo kuwepo pale aendelee kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwa mara ya kwanza wananchi wa Kata ya Kwamagome, wamepata mradi pale Kwamagome unaopeleka maji Kwamagome na Hedi. Kana kwamba haitoshi, nilipokwenda Ofisini Wizarani, tumeongezwa fedha ili wananchi wa Lusanga, Sasioni, Lolopili na Mji mpya nao wapate maji. Nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa usikivu wako.

Mheshimiwa Spika, nashukuru zaidi kwa mara ya kwanza kwa historia ya nchi yetu Kata ya Malezi wamepata mradi wa maji wa Shilingi 324,000,000/=. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kuomba katika kipindi hiki, Mheshimiwa Waziri mradi huu natamani sana tukauzindue kwa pamoja, twende pamoja tukauzindue na ule mradi wa Mabanda ambao wewe siku ile ulipokuja, usiku ule tulipokunywa maji pale, ulipiga simu tukiwa pamoja kwa Mheshimiwa Rais na usiku ule ule alikubali kutoa shilingi 671,000,000 ambazo zimejenga tenki kubwa sana pale Mankinda. Tunapeleka maji kata yote ya Mabanda na tunapeleka maji Kijiji cha Mankinda Kata ya Konje na tunayapeleka maji pale Wanyamakazi. Nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kata ya Kojamba tulipata Shilingi bilioni 1.96 ili kuchimba bwawa kubwa pale Kwinkambala, mkandarasi akatuzingua na sisi tukamzingua mara nne yake. Hivi ninavyozungumza, mkandarasi alishafukuzwa. Nitoe wito kwa Wabunge wenzangu, Mkandarasi akizingua site, tusingoje Serikali. Sisi wananchi tuna mamlaka ya kuwakataa wakandarasi ya ovyo ovyo. Kwa hiyo, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri, ulikuja pale na umeshaweka utaratibu ndani ya wiki mbili kama ulivyoahidi kwamba tunakwenda kupata mkandarasi mwingine pale Kwinkambala. Kwa maana hiyo bado umeendelea kutusikiliza wananchi wa Handeni Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ametupa mradi wa shilingi 857,000,000, kinachimbwa kisima kikubwa pale Ndelema kuyapeleka maji Kwinkambala wakati tukiendelea kusubiri ujenzi wa Bwawa kubwa lile la Kwinkambala.

Mheshimiwa Spika, zaidi naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kufanikisha mradi huu wa miji 28. Mradi huu umezungumzwa hapa Bungeni kwa takribani miaka sita iliyopita. Wito wangu kwenye mradi huu, dola milioni 500 mkopo tunaochukua Serikali ya India, Benki ya Exim, miaka sita iliyopita milioni 500 ingeweza kufanya kazi kubwa zaidi kuliko leo. Kwa hiyo, kama process za mradi huu zimeshakamilika, chonde chonde mradi uanze.

Mheshimiwa Spika, mwisho nimalizie, Waswahili wanasema kushukuru ni kuomba tena. Wananchi wa Handeni Mjini wamenituma niombe tujengewe bwawa pale Mandela Kata ya Kwenjugo, pia tujengewe bwawa pale Kata ya Mabanda Bwawa la Kwamkole. Tukishakuwa na Bwawa na Kwinkambala tukawa na Bwawa la Mandela na tukawa na Bwawa Kwamkole, tafsiri yake ni kwamba tutakuwa na source nyingi za maji kwa Jimbo letu la Handeni mjini plus haya maji ambayo yanatoka kwenye huu mradi wa HTM yanayotoka Mto Ruvu kule Pangani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo napenda nitoe shukrani za dhati kwa Engineer Yohana Mgaza, Meneja wa HTM. Vile vile nitoe pongezi zangu za dhati kwa Engineer Hosea Mwingizi. Mheshimiwa Waziri hawa watu naomba wasihamishwe Handeni, wawepo waweze kutusaidia kwenye haya mapambano ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya, nakushukuru sana kwa fursa hii. Ahsante sana, wananchi wa Handeni wakae mkao wa kula, tunakwenda kuiandika historia ya Handeni Mjini kupitia uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan na ndugu yangu Waziri Aweso.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwenye tovuti ya Wizara ya Fedha, upo mwongozo wa maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali, mwaka 2023/2024. Mwongozo huu wenzetu wa TAMISEMI walikutana kati ya tarehe 17 mpaka 21 kuujadili na kuona namna ya kuutekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mengine, wamezigawa Halmashauri zetu katika makundi manne. Kundi la kwanza ni kundi ambalo ziko Halmashauri tisa. Halmashauri hizi tisa zimewekwa kwenye kundi la kupeleka asilimia 70 ya mapato yasiyolindwa kwenye maendeleo. Kundi la pili, lina Halmashauri 17. Kundi hili limepangiwa kupeleka asilimia 60 ya mapato yasiyolindwa kwenye maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kundi la tatu lina Halmashauri 102. Kundi hili limepangiwa kupeleka asilimia 40 ya mapato yasiyolindwa kwenye maendeleo na kundi la tatu ambalo ndiyo kundi la Halmashauri ya Handeni Mjini iliyopo, kundi hili lina Halmashauri 56 ikiwemo na Korogwe na Halmashauri nyingine nyingi ambazo ningekuwa na muda ningezitaja. Halmashauri 56 zenyewe zimepangiwa kupeleka asilimia 20 tu ya mapato yasiyolindwa kwenda kwenye maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri ya jambo hili ni nini? Jambo hili linapeleka umasikini kwa wananchi wote waliopo kwenye Halmashauri hizi. Jambo hili, literally, halikubaliki! Ukisema kwamba makusanyo yetu ya ndani yasiyolindwa asilimia 20 tu ndiyo iende kwenye maendeleo, tafsiri yake ni kwamba, kwanza tutawa-discourage walipa kodi. Mlipa kodi anataka akilipa kodi yake, ushuru ukikusanywa, aone haspitali pale, kituo cha afya kimejengwa, aone madarasa yanajengwa kwa fedha anayokusanya. Sasa tukiwa tunakusanya halafu asilimia 80 yote tunaenda kuinywa chai, tunaenda kuitumia kwenye mafuta kwa ajili ya usimamizi, hii haitakuwa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itatusababishia matatizo kwa sababu, mbali na kuwa-discourage walipa kodi, wanufaika wetu wa asilimia 10 zile tunazokopesha; tulipokuwa tunatenga asilimia 40 tulikuwa tunapeleka asilimia 10 kuwakopesha wananchi, kuwakopesha akinamama, vijana na walemavu, lakini ukitenga asilimia 20 inamaanisha hata hiyo fedha ambayo unawapelekea inapungua, wanufaika watakuwa wachache. Tafsiri yake ni kwamba, tunatengeneza nchi yenye matabaka makubwa. Wale wenzetu ambao wamepangiwa kupeleka fedha nyingi kwenye maendeleo, ndiyo na fedha zao za kuwawezesha wananchi wao zitakuwa nyingi, lakini na miradi watakayoitekeleza kwenye maendeleo ni mingi kuliko ambavyo sisi tutatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kufanya hivi halafu eti wao TAMISEMI wanasema, tukishaondolewa zile asilimia 20 tukabaki kwenye 20 ya fedha za maendeleo, eti watalipa madeni ya watumishi wasiokuwa walimu. Ukimlipa madeni mtumishi, huo ni wajibu wako, na ni jambo zuri kufanya. Wanasema wataleta stahiki kwa Wakuu wa Idara; huo ni wajibu wenu na ni jambo zuri kufanya. Nasema ni wajibu wenu kwa sababu, vyanzo vyote vya mapato kwenye Halmashauri mmevichukua nyie, kwa hiyo, mna wajibu wa kufanya haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisema mtaongeza OC proper, vyote hivyo unavyoviongea vinaenda tu kusaidia uendeshaji wa Halmashauri, lakini ikiwa sisi tulikuwa tunatumia mapato ya ndani kujenga zahanati pale kwenye Zando mwaka juzi, 2021; mwaka jana 2022 tukajenga zahanati Mankinda kwa fedha za ndani, na mwaka huu 2023 tumejenga pale Bangu zahanati kwa fedha za ndani; na tulikuwa tunatarajia kwenye mwaka huu wa fedha tunaopitisha bajeti tukajenge zahanati kule Kwalubaka. Sasa nyie mmechukua fedha zote, tunawaambieni sasa: Je, mtatuletea fedha ili tujenge zahanati hizi ambazo… (Makofi)

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka wapi? Haya Mheshimiwa pale.

T A A R I F A

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Nataka kumwongezea taarifa Mheshimiwa anayezungumza kwamba, TAMISEMI kuzisaidia hizi Halmashauri ambazo amezipunguzia asilimia 40 kwenda asilimia 20, ni kuhakikisha wanapeleka miradi ya kimkakati ili kupandisha mapato kwenye hizi Halmashauri au kama hizo Halmashauri zilishatengewa miradi ya kimkakati, ikamilike ili kuzisaidia kupandisha Halmashauri hizo, siyo kutoa hizo asilimia 40. Tutasaidiaje wananchi wetu?

MWENYEKITI: Mheshimiwa ni taarifa au ni swali?

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni taarifa nilikuwa namwongezea Mheshimiwa anayeongea.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Reuben unaipokea Taarifa?

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa ya Mbunge aliyetoka kunipa taarifa ambaye anatokea Momba, na Halmashauri yake ni miongoni mwa Halmashauri ambazo zimetengwa ili ziingie kwenye asilimia 20 na fedha zote ziende kwenye matumizi ya kawaida badala ya kwenda kwenye matumizi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema aliyenipa taarifa, Halmashauri hizi lazima tuje na mpango wa kuzisaidia. Suala siyo kuzifanya ziwe likizo ya maendeleo. Hatuwezi kuzipa likizo ya maendeleo, eti wawe wanakusanya asilimia 80 yote wanakula, 20 ndiyo inaenda kwenye maendeleo. Hii siyo sawa! Hii haikubaliki!

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi yote ya kimkakati mmewapelekea ma-giants. Ukija kwenye mradi wa TACTIC; tier one ya TACTIC iko na ma-giants, majiji makubwa. Tier two ya TACTIC iko na ma-giants majiji makubwa, halafu tier three ndiyo tuko sisi wachovu ambao ndiyo tena mnatunyang’anya na mapato, halafu na tier three yenyewe hamuitekelezi. Hii siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu mnapanga wapi? Huu ni utafiti wa wapi mmefanya? Nataka niwakumbushe, ukisoma Five Years Development Plan tuliyonayo ukurasa wa 12, inasema: “The aim of the fifth phase Government was to increase development spending to the tune of 30 - 40 percent.” Huu mpango tuliujadili hapa, tukaupitisha hapa, nyie mnawezaje kujifungia chumbani na kubadilisha bila kuja kutuambia hapa? Yaani mnawezaje kufanya hivyo? Yaani Halmashauri zote 56 zi-paralyze tu kwa sababu nyie mmeamua? Hii siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waziri atakapokuja kufanya hitimisho hapa atuambie, sisi wa Handeni, pamoja na Halmashauri nyingine nyingi kama ilivyo Mpumbwe, Kasulu, Handeni TC, Nyang’hwale, Nzega, Mpama, Iramba, Ikungi, Longido, Namtumbo na maeneo mengine, mta-compensate vipi kwenye hii fedha tuliyokuwa tunapeleka kwenye maendeleo? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia mswada wa sheria ya fedha 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme naunga hoja iliopo Mbele yetu naiunga mkono, baada ya kuiunga hoja mkono nijielekeze kuchangia kwenye huu Muswada.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natokea Handeni sehemu ambapo ni Wilaya yenye madini mengi sana, na Muswada huu uliokuwa umeletwa Serikali ilionyesha ni ya kuigusa sekta ya madini kwa maana ya kuongeza kodi. Na hata vifungu ambavyo ame withdraw, wamesema wanakwenda kujipanga ili siku za usoni waweze kuanalia namna nzuri ya kutoza kodi kwenye sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Muswada huu kwenye amendment zilizoguswa ilikuwa ni ile part 3 amendment of the income tax Act cap 332, na ile part 25 ambayo ni amendment of the vocational education and training Act cap 82. Hii ilikuwa inawataka wachimbaji walipe 0.4 kama levy kwa maana ya SDL, na ile nyengine ilikuwa inawataka wachumbaji wadogo walipe asilimia 3 kama income taxi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii nimshukuru sana sana Mheshimiwa Rais mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kuwa msikivu sana, kwa kuwa msikivu sana na kuelekeza kwa Waziri wa Fedha wa withdraw hizi kwa ajili ya kuwalinda wachimbaji wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa Serikali ime-withdraw, na kwa kuwa bado wanafikiria kutoza kodi zaidi siku za usoni, kwa wachimbaji wadogo maana mpaka sasa mchimbaji mdogo analipa asilimia 6 kama mrabaha, analipa asilimia moja kwa ajili ya ukaguzi na analipa 0.3 kama sehemu ya serves levy, inamaana kodi yake yote mpaka sasa mchumbaji ni asilimia 7.3. Sasa kabla ya Serikali kufikiria kuwatoza zaidi wachumbaji wadogo, ninashauri mambo yafuatayo yafanyike:- (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza kumekuwa na taarifa tofauti tofauti za sensa za idadi ya wachimbaji wadogo, hivi tunavyo zungumza si Serikali, si wachimbaji wadogo wenyewe wenye takwimu sahihi za wachimbaji wadogo, kwa hiyo tunaishauri Serikali, sensa hii inayokuja ya Tanzania nzima ikatusaidie kutupa idadi ya wachumbaji wadogo nchi nzima, huwezi kutoza kodi kwenye sekta ambayo hujui idadi ya wahusika, hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili tulitunga sheria hapa mwaka 2017, Sheria ya The Natural Wealth and Resources, Permanent Sovereignty Act 2017, ambayo iliwawezesha watanzania kumili madini kisheria rasilimali zile, madini kisheria. Sasa watanzania wameshamiliki madini kisheria, Watanznia wanamiliki PML Watanzania wanamiliki migodi, lakini hatujawawezesha Watanzania kuyachimba haya madini, hatujawawezesha watanzania kuchimba haya madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata ukiangalia ile Mining Act cap 123 ambayo imtungiwa Regulations Section ya 129, inasema The Mining Act Mineral Value Addition Guidelines ambayo imetolewa kwenye tangazo la Serikali namba 60, tuipitie upya kanuni hii, tumewamilikisha madini na tumewanyang’anya fursa ya kuyatumia madini haya, kwa sababu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, regulation hii ilotungwa na wizara inazuia wachumbaji kusafirisha madini ghafi, sikatai kwamba kuna umuhimu sana wa kuyaongeza madini yetu thamani kabla hatujayasafirisha, sio kila madini tunauwezo nayo leo ya kuyaongeza thamani. Kwa mfano wanaposchimba chuma, ukiongelea valued edition kwenye chuma unaongelea kufunga plant kiwanda cha zaidi ya dola milioni moja, mchimbaji gani mdogo ataweza ku-afford kuongeza value addition ya chuma hapa, tumewafilisi wachimbaji wa kopa kwa hii na tumeshindwa kuyatumia maadini kama vile manganese na zile pressures mentals. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naiomba wizara yenye zamana ikapitie upya kanuni hii, tujaribu kuangalia kwa yale madini ambayo tunaweza kuyaongeza thamani kama ilivyo gold, kama ilivyo tanzanite tuendelee nayo, na kwa madini ambayo bado hatujajipanga tuwaruhusu watu wayachimbe na wayasafirishe yakiwa ghafi. Tukifanya hivyo tutapata kodi nyingi sana zaidi ya hata ambayo mlikuwa mnakadiria kuipata kwa kutoza asilimia tatu, huo ni ushauri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili nawashukuru sana benki ya CRDB kwa kuanza kuwaamini wachimbaji na kuwakopesha, lakini wenzeatu wa Serikali naomba niwaeleze jambo moja, hata kama CRDB wameanza kuwakopesha wachimbaji, wanawakopesha kwenye commercial rate, uchimbaji ni investment huwezi kumkopesha mtu kwa commercial rate afanye uchimbaji, lazima tuangalie namna gani wachimbaji wetu watakopeshwa kwama kufanya investment, kwa kuzingatia kwamba pay back period ya miradi yao ni ndefu sana na hata break event point yao ni ndefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwakumbushe tu hata hizi kodi tunazowatoza sasa hivi wachimbaji, kuna wengine tunawatoza kutoka kwenye mitaji yao kwa sababu inamchukua mchimbaji muda mrefu sana kutengeneza faida.

Kwa hiyo, anapokuwa amekwenda kuuza madini yake aliyoyapata wewe ukitoza ile 7.3 haimaanishi kwamba yeye atengeneza faida, anaweza kuwa ame-invest amepata jiwe ambalo halifanani na thamani ya investment yake kwa sasa, lakini wanaendelea kulipa kodi kizalendo sana, kwa sababu wanalipa kodi kwenye investment zao, kwenye capital. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii industry ni lazima tui-trite with conscious, tusiwe tunakuja tu hapa tunataka kutoza kodi, lazima hii industry tuilee na lazima tufungue milango kwa sababu hawa wachimbaji hatujawa na uwezo wa kuwawezesha kama Serikali, basi tuwalee ili wao wenyewe waendelee kujijenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya nakushuru sana nafikiri nimetumia muda wangu vizuri, ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (no. 6) Bill, 2021
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia fursa hii ili na mimi nipate kuchangia Muswada wa Mabadiliko ya Sheria Mbalimbali Na. (6) wa Mwaka 2021. Niungane na Wabunge wenzangu waliotangulia kuzungumza kuipongeza sana Serikali ya CCM kwa kuwajali wakulima, wafugaji na wavuvi, kuondoa Withholding Tax ya asilimia mbili katika mazao yanayotokana na shughuli hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa salamu hizo za pongezi, mimi nataka nichangie marekebisho ya ile part three, yaliyokuwa yameletwa kurekebisha Sheria ya Usimamizi wa Kodi. Sheria hii imefanyiwa marekebisho na sisi Kamati ya Bajeti tumeshauri sana ili kuondoa vikwazo vyote ambavyo vilikuwa vinakwamisha utekelezaji wa mradi wa bomba la mafuta. Sasa baada baada ya kuipitisha sheria hii hapa Bungeni na wenzetu wa Serikali kwenda kushirikiana na Serikali ya Uganda kuutekeleza mradi huu ninashauri mambo yafuatayo kwenye mradi huu:

Mheshimiwa Spika, mradi huu una gharama ya Dola Bilioni 3.5 karibia trilioni nane hivi. Tafsiri ya hii ni kwamba ni mradi mkubwa na ni fursa kubwa kwa wananchi wetu ambako mradi unapita lakini na kwa Watanzania kwa ujumla. Kwa hiyo, basi ni lazima tuweke mikakati ya makusudi kuwawezesha wananchi wetu ambako mradi unapita ili washiriki kikamilifu kwenye shughuli zote kwenye fursa zote za ujenzi na uwepo wa mradi huu maeneo ambako bomba hili linapopita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hali za wananchi wetu tunazifahamu. Kikwazo kikubwa kwa wananchi wetu kushiriki kwenye fursa za bomba la mafuta hili ambalo tunalizungumzia itakuwa ni mitaji. Tayari Maafisa wetu wa Maendeleo ya Jamii huko tunakotoka ambako bomba linapita wanawahamasisha wananchi wajiunge kwenye vikundi, lakini kikwazo kikubwa, ninarudia tena, kikwazo kikubwa ambacho kitawakumba wananchi wetu ni mitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu sasa kwenye hili la kuwawezesha wananchi wetu mitaji ya kushiriki kwenye fursa za bomba la mafuta, ushauri wa kwanza ni kwamba kwa wale watakaofanikiwa kupata mikataba ya kazi kwenye bomba lile la mafuta kwa maana ya ama ku-supply vitu au kujenga, ninaomba kwamba ufanyike utaratibu maalum ili mikataba ile itumike kama dhamana kwenye mabenki. Kufanyike utaratibu maalum mikataba ile watakaokuwa wamepata itumike kama dhamana kwenye mabenki ili waweze kuchukua mikopo tena yenye riba nafuu. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa unajadili vizuri, lakini tujue kwamba, leo tunajadili sheria. Tunapojadili sheria ni tofauti kabisa na kujadili mada. Hatujadili bomba la mafuta na mambo yake, tunajadili sheria iliyoletwa hapa. Endelea tu Mheshimiwa tumalizie.

MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nakushukuru. Kwa kuwa, umenipa na umeridhia niendelee naomba nimalizie vipengele vinavyofuata.

Mheshimiwa Spika, jambo jingine kwenye bomba hili tunalokwenda kulijenga ni vyema Serikali ikalichukua kama fursa na sisi kama nchi tutazame ushoroba kwa maana ya mkuza. Corridor hii ambayo tunakwenda kuijenga ya bomba la mafuta kutoka Hoima mpaka Chongoleani - Tanga siku zijazo tuifikirie kama fursa ya kupitisha bomba la gesi kutoka hapa gesi yetu ilipo ili tuweze kuipeleka mpaka Uganda na hatimaye Sudan ya Kusini na baadae Congo. Tuitazame kama fursa ya siku zijazo.

Mheshimiwa Spika, mwisho kwenye hili bomba hili linapita kwenye Mikoa Nane na katika hiyo Mikoa Nane Mikoa ya mwisho huku kuelekea Bandari ya Tanga ni pamoja na Tanga yenyewe, Dodoma, Singida na Manyara. Sasa bomba hili litahitaji barabara ya kulihudumia hili bomba, barabara hiyo inayopita maeneo hayo ili kuweza kulifikia hili bomba kwa urahisi ni barabara ya Handeni – Kibilashi – Kiteto
– Kondoa na Singida. Kwa hiyo, ni vyema Serikali inapofikiria kwenda kutekeleza mradi huu ifikirie pia kuitengeneza barabara hii.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipatia muda na kuniruhusu kuchangia haya. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Kudhibiti Utakatishaji wa Fedha Haramu wa Mwaka 2022
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kuchangia Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Kudhibiti Utakatishaji wa Fedha Haramu. Kwanza nitumie nafasi hii nimpongeze sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kulipa uzito jambo hili na kwa kuona umuhimu wa jambo hili na hatimaye kuleta Muswada huu kwa dharura ili kulinda hadhi ya nchi yetu katika uwanda wa Kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma tathmini ambayo ilifanywa na ikapelekea leo Serikali kuleta Muswada huu, tathmini ile inaonyesha maeneo mawili makubwa ambayo ilitutaka kama nchi tuyafanyie marekebisho ili tuweze kuendana na viwango vya Kimataifa. Eneo la kwanza ni eneo la kisheria ambayo ndiyo kazi tunayofanya leo hapa. Kwa hiyo, hapa wala asiwepo mtu wa kumlaumu mtu mwingine kwamba imechelewa kuja, huu ndiyo wakati sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni la kimifumo. Mifumo ya taasisi zetu, namna ambavyo taarifa zinatoka taasisi moja kwenda nyingine, namna ambavyo taasisi zinatoka kampuni moja kwenda nyingine. Haya ndiyo maeneo mawili ambayo utafiti ule au tathmini ile ilitaka tuyaboreshe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 4 ya Muswada ambayo inafanya marekebisho kwenye kifungu cha 3 cha Sheria ile tunayoifanyia marekebisho, imetaja maeneo mawili ya muhimu na ambayo nataka niyajadili kwa huu muda mfupi uliopo. Eneo la kwanza ni eneo la watoa taarifa (reporting persons). Ibara hii imeongeza idadi ya watoa taarifa, Sasa watoa taarifa watahusika zaidi na hili eneo la kimifumo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Serikali baada ya kupitisha Sheria hii hapa itakuwa na kazi kwa kweli ya kwenda kuhakikisha kwamba taasisi zetu mifumo inayotumika inasomana. Tuna mifumo mingi. Ipo mifumo inayotumika kule bandarini ya TANCIS, ipo mifumo inayotumika kwenye mabenki ambayo iko pale BoT na mifumo inayotumika na TRA ya kikodi. Vile vile taasisi yetu hii ya Financial Intelligence Unit inapokuwa imejiridhisha na taarifa zilizopelekwa kwake, inazipeleka kwenye taasisi nyingine mbalimbali kama vile Polisi na vile PCCB. Kwa hiyo, mifumo ya maeneo haya pia lazima Serikali ikairejee iiboreshe ili iweze kusomana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vivyo hivyo, mifumo ya Credit Reference Bureau ambao ameongezwa kwenye kifungu hiki kama sehemu ya watoa taarifa, vile vile tukaiainishe na mifumo ya kiutumishi pamoja na mifumo ile ya Tume ya Maadili ya Umma. Nakumbuka kila mwaka tunajaza fomu zile za Maadili ya Viongozi wa Umma. Tunatakiwa kama nchi tuwe na mfumo ambao taarifa hizi tunazi-update tu, badala ya kuwa tuna-update kila siku. Kwa kufanya hivi, tutakisaidia kitengo chetu cha Financial Intelligence Unit kufanya kazi yake kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipengele kingine ambacho kinatajwa kwenye ibara hii ni hiki cha kufanya Consumer Due Diligence kila biashara inapofanyika. Kwamba unapokuwa unafanya biashara yako, lazima umjue mteja wako. Tumeweka marekebisho pale, tumesema consumer monitoring. Sasa kwenye kufanya consumer monitoring, Watanzania wenye biashara, taasisi zenye biashara zitategemea zaidi taarifa za mtu mmoja mmoja. Kwa maana hiyo, tunaipa Serikali yetu challenge ikafanye kazi kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika nchi hii Mtanzania anamiliki vitambulisho karibia vinane. Nitatoa mfano. Kitambulisho cha NIDA, kitambulisho cha Mpiga kura, kitambulisho cha kazi, kitambulisho cha Bima ya afya, driving license, passport, kitambulisho cha benki, vitambulisho vya mifuko ya Hifadhi ya Jamii. Ni lazima Serikali iwe na mfumo ambao kitambulisho chetu kimoja tu kile cha NIDA kibebe taarifa zote za kila Mtanzania. Kwa kufanya hivyo, tutarahisisha mazingira ya kufanya biashara na kurahisisha kupata taarifa ambazo ndiyo hasa zinahitajika kwenye kitengo chetu hiki cha Financial Intelligence Unit ili tuweze ku-meet masharti haya kama Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka nichangie tu maeneo haya. Nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)