Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Hamis Mohamed Mwinjuma (11 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Umenipiga ambush kusema ukweli. Cha kwanza kuongea kwenye Bunge lako tukufu ni kumshukuru Mwenyezi Mungu, pili, kukishukuru Chama changu cha Mapinduzi na kipekee kabisa Rais wangu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ambaye aliongoza vikao vyote vya uteuzi vilivyohakikisha jina langu linarudi. Tatu, niwashukuru wananchi wenzangu wa Muheza kwa kunipa imani kubwa. Nne, niishukuru familia yangu na nichukue fursa hii sasa kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2021/2022 mpaka 2025/2026. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la mchango ni kuisaidia Serikali kuongeza wigo wa ukusanyaji wa mapato. Niseme kwamba nimeusoma Mpango na naona kwamba kuna maeneo mengi ambayo tunaweza kama Wabunge tukachangia na tukaisaidia Serikali kufanya hilo ili iweze kutekeleza miradi ya maendeleo kwa ufanisi kadri inavyokusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kwa sababu ya muda sitaweza kuongea mambo mengi, lakini niseme kwamba eneo ambalo nataka kulichangia ni hasa la walionitumia, wananchi wa Muheza. Pamoja na kwamba nchi hii inaonekana kwamba asilimia 65 ya wananchi wa nchi hii wanapata riziki zao kwa kutumia kilimo, wananchi wa Muheza ni takriban asilimia 90 ama zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Muheza kama ambavyo najua wananchi wengine wengi wa nchi hii wanataka kuchangia mapato ya Serikali zaidi ya wanavyofanya sasa hivi. Mazingira yanawapa wakati mgumu. Ningependa kuchukua nafasi hii kuiomba Serikali ijue kwamba haiwezi kukwepa moja kwa moja kwenye mazingira kuyafanya rafiki ili kuwezesha kuingiza fedha zaidi baadaye. Ndivyo biashara zinavyofanywa, unawekeza ili upate zaidi huko mbeleni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni nilihudhuria Mkutano wa wadau wa mkonge na Waziri Mkuu na moja ya vitu ambavyo vilinishangaza lakini kwa wema, ni suala kwamba wakulima wadogo wanazalisha zaidi ya wakulima wakubwa, kwamba katika top four ya wazalishaji wa zao la mkonge nchini wakulima wadogo ni namba moja, wakifuatiwa na Mboni wakifuatiwa na na METL na wengineo wanafuata. Hii inaonesha kwamba mahali ambapo tunafanya kosa labda ni kutotoa macho kwenye kuhakikisha wakulima wadogo wanawezeshwa na kupewa nafasi ya kuzalisha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba ya Rais Magufuli ya kufungua Bunge la 12 tarehe 13 Novemba, 2020, katika ukurasa wa 27 na 28 Rais anasema kwamba moja ya vitu ambavyo vinatu-cost ni kwamba, naomba ninukuu: “Takwimu zinaonesha kuwa kila mwaka nchi yetu inapoteza wastani wa kati ya asilimia 30 – 40 ya mavuno yake kwa sababu mbalimbali ikiwemo kukosekana kwa miundombinu ya kuhifadhi” mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais pia kwenye ukurasa wa 27 ameweka wazi kwamba lengo la Serikali ni kukifanya kilimo kuwa cha kibiashara, sasa kuna miradi mbalimbali ambayo ilisitishwa, mathalani Mpango wa Marketing Infrastructure Value Addition and Rural Finance - MIVARF kwamba baada ya awamu ya kwanza Serikali haikusaini kuendelea na awamu ya pili. Sijui sababu zake, lakini nafikiri moja ya vitu ambavyo Serikali ingeweza kufanya ni ku- take over kwenye mpango huu, badala ya kuwaacha wale wa-Finland watuendeshee, Serikali ingeendeleza kwa sababu ni Mpango ambao ulikuwa unaonekana una manufaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, post-harvest centres ambazo zilikuwa zinatumika kama masoko zilikuwa zinawekwa mahali kuhakikisha soko la wafanyabiashara wa mbogamboga, kwa mfano maeneo kama Lushoto, linakuwa la uhakika. Miundombinu ya kufikisha kwenye soko lile wale watu wa Finland walikuwa wanahakikisha wanatengeneza. Kwa hivyo, tunaweza kuua ndege wawili kwa jiwe moja. Kwanza tukahakikisha miundombinu ya wafanyabiashara, wakulima kufikisha kwenye soko inapatikana na pia soko la wazi la wafanyabiashara wakulima hawa wa mboga mboga liko wazi. Kwa mfano kulikuwa na barabara ya kutoka Mkatoni kwenda Kwai kule Lushoto au Chanjamjawiri mpaka Pujini kule Pemba hizi zote zilitengenezwa kwa ajili ya Mpango huu. Kwa hiyo tungeweza kuhakikisha kwamba wana soko na miundombinu inatengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya vitu ambavyo vinaniumiza moyo ni kwamba hii asilimia 30 mpaka 40 ambayo Mheshimiwa Rais alisema inapotea ni ya wakulima wadogo. Wakulima wa ndizi kule kwetu Amani kwa mfano, ukienda wakati wamvua unaona jinsi ambavyo ndizi zimeoza barabarani kwa sababu zinashindwa kufikishwa sokoni. Kwa hiyo, naomba Serikali iwekeze kwenye kuhakikisha kwamba tunawafaidisha, tunawanufaisha wakulima wadogo na wanaweza kupata masoko…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia kwenye hotuba hii ya Wizara na Mawasiliano na Teknolojia ya Habari. Kwanza nichukuwe nafasi hii kuwapongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. Faustine Ndugulile, na wasaidizi wake Engineer Kundo Mathew, dada yangu Dkt. Zainab Chaula na Mwalimu wangu Jim Yonazi kwa hotuba nzuri yenye matumaini inayoonyesha kwamba nchi yetu inajielekeza kwenda sawa sawa na dunia nzima kwenye upande wa teknolojia. Tuna walakini hapa na pale lakini lengo lenu linaonekana wazi kabisa ni kwamba mmekusudia tusiachwe na kasi ya dunia hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina mambo mawili ya kuchangia japokuwa nina mengi kwa sababu nimekuwa hapa toka asubuhi leo na michango mingi ya Waheshimiwa Wabunge imekuwa ya kitaalamu na iliyojitosheleza sana, sitaki kuijazia nzi, kuipigia miluzi mingi na kumpotosha Waziri, nafikiri ameandika mengi na anajua mahali pa kushughulikia ili kupata mwelekeo ambao tunaokusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo limesemwa na Waheshimiwa Wabunge wengi na mimi napenda nilitilie msisitizo ni kuhusiana na udhaifu au kukosekana kabisa kwa mawasiliano sehemu kubwa ya vijijini katika nchi yetu. Mimi natoka Jimbo la Muheza ambapo kimsingi zaidi ya nusu ya Jimbo la Muheza aidha lina mawasiliano dhaifu sana ya simu ama hakuna kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mahali ukiambiwa mtu yupo halafu ukampata kwenye simu unaanza kumuuliza kwanza unatumia simu ya aina gani mpaka inapatikana hapo ambayo inaweza kushika mtandao kibabe namna hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna tarafa, kata vijiji na vitongoji vingi ambavyo havina kabisa mawasiliano. Kwa mfano tuna Kata ya Kwezitu iliyopo katika Tarafa ya Amani sehemu yake kubwa haina mawasiliano, Lanzoni kule Kwemingoji hakuna mawasiliano, Kiwanda na Mangugu kwenye Kata ya Tongwe hakuna mawasiliano, Magoroto na Ufinga, Mtindiro, Kwemhanya, Kwebada, Songa, Kwafungo; zote aidha hazina mawasiliano kabisa ama mawasilisano ni dhaifu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi binafsi nikienda kijijini kwangu yaani simu inakuwa ni ya kuchezea game ama kama unataka kufanya shughuli yenye manufaa kwenye simu hiyo uwe umesha-download kitabu uende ukaitumie kusomea lakini suala la kuitumia kwa ajili ya mawasiliano halipo kabisa. Nimuombe Mheshimiwa Waziri, sitaki kulalamika tu na kuliacha hili suala linaelea, kwa sababu najua kimsingi operators wetu wanafanya biashara na pengine wanasema kwa sababu ya gharama ya kusimika aidha minara hii na gharama ya kuiendesha inawafanya wasifike baadhi ya sehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu ninyi ni watu wa kisasa sana, mimi katika pitapita zangu nimeshakutana baadhi ya watu ambao wanatoa teknolojia mbadala ya kufanya shughuli hizi ili tupate matokeo hayahaya tunayoyalilia na wananchi wote waweze kupata mawasiliano kwa kadri inavyotakikana. Mheshimiwa Waziri nikuombe suala la mawasiliano kwenye nchi hii tusilifanye baadhi ya sehemu likawa ni jambo la anasa. Kwa hisani yako nakuomba wewe na Wizara yako sasa muangalie namna ambavyo mnaweza kupata teknolojia mbadala na kuhakikisha hili suala linatatulika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mtu alikuwa ananiambia kuhusiana na teknolojia ya new line wireless na kwa jinsi gharama alivyokuwa anazilinganisha japokuwa mimi sio injinia nilikuwa najiuliza kwa nini tumechelewa, kwamba gharama ya kusimika minara hii ni ndogo sana, teknolojia hii haitumii umeme ama mafuta kama inavyotumia hii minara mikubwa ya makampuni kwa maana ya ma-operator wetu wa sasa na uwezekano wa kufanya project ndogondogo kwa ajili ya kutatua kero za sehemu husika ni mkubwa vilevile. Kwa hiyo, nawaomba muangalie namna ambavyo tunaweza kupata teknolojia hii na nyingine nyingi za aina hii, najua ziko nyingi na ninyi ni watu wajanja, watu wa kisasa mnaweza kuzipata kwa sababu mme-specialize kwenye Wizara mnayoishikilia, mnaweza kutupatia ufumbuzi. Narudia tena Mheshimiwa Waziri tusiache mawasiliano ya kueleweka yakaonekana ni kitu cha anasa kwenye nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni suala la YouTube. Nimekuwa kwenye Bunge lako Tukufu hili toka asubuhi na nimesikiliza michango mingi, nimefurahishwa na concerns za Wabunge wengi kuhusiana na mapato yanayopotea ya Serikali na wasanii husika kwenye makusanyo ambayo yanaweza kupatikana kwenye mtandao wa YouTube. Kwanza, niseme kwamba ni kweli YouTube ina hela lakini kuna misconception kubwa, sio hela hizo ambazo Waheshimiwa Wabunge wengi wanaziona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, YouTube ni miongoni mwa platforms ambazo zinafanya shughuli ya kuuza muziki (streaming) lakini sio peke yake, kuna platforms nyingi ambazo zinafanya shughuli hii na kimsingi platforms ambazo zinapatikana kwenye nchi hii YouTube ni ya mwisho kwenye kuingiza mapato yaani inalipa kidogo kuliko platforms zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano, YouTube kwa views milioni moja kwa nchi yetu inalipa kati ya dola 400 na 500. Kimsingi YouTube inalipa kutokana na nchi ambayo aliyei-upload yuko. Kama kuna nchi nyingine ambazo matangazo mengi yanaweza kuwekwa wanalipwa Zaidi, kuna mahali wanalipwa mpaka dola 1,000 kwa views milioni moja lakini kwetu ni kati ya dola 400 na 500 kwa views milioni moja. Wakati Spotify wanalipa kwa namba hiyohiyo ya views kati ya dola 7,000 mpaka 10,000 kwa streams hizohizo. Tofauti ya YouTube na hizi platforms zingine ni kwamba YouTube yenyewe ni visual hizi nyingine unaweza kusikiliza peke yake. Kina Spotify, Apple Music, Napster, Deezer, Tudor, zote hizi zinafanya shughuli hiyohiyo na zinalipa zaidi ya inavyolipa YouTube. Kwa hiyo, niwaombe Waheshimiwa tusitoe tu macho kwamba YouTube ndio platform peke yake inayolipa, kuna sehemu nyingi sana ambazo wasanii wanaweza kupata kipato kikubwa na zinatakiwa kutolewa macho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi YouTube inabidi kuwa na aggregator lakini nchini kwetu hatuna aggregator hata mmoja. Nilimsikia Mheshimiwa mmoja asubuhi ameliweka kama wasanii na content creators ni kosa lao au ni ufahamu wao kuwa mdogo. Sisi wengine tumejaribu kuhakikisha nchi hii inakuwa na aggregator kwa miaka karibuni minne au mitano iliyopita, siyo suala rahisi, haliwezekani kirahisirahisi. Pengine nimuombe Mheshimiwa Waziri kama tunataka kuwa na aggregator basi Serikali iingilie kati ijaribu ku-harmonize haya majadiliano kati yetu na YouTube tuone kama tunaweza kupata aggregator kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Afrika Mashariki na Kati yote aggregator ni mmoja tu Mkenya Ngomma VAS lakini wasanii wote wengine wanatumia Believe ambayo ni ya Ufaransa agent wao ni Zeze ambao wako Kenya, Spice Digital ambayo ni ya South Africa ambaye agent wao kwa hapa ni Muziki, Metal Music ya Nigeria ambayo haina agent hapa na Ngomma ambayo ni ya rafiki yangu CLEMO ndiyo ya Kenya. Kimsingi sisi hatuna aggregator na watu wengi naowafahamu nikiwemo mimi mwenyewe tumejaribu kupata aggregator kwenye nchi hii imeshindikana. Ndugu zangu Wasafi watakuwa mashahidi, Diamond Platinum najua alienda mbele sana lakini kuna mahali alikwama mpaka leo hana hiyo huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali yetu iangalie namna ambavyo inaweza kulinda content creators wake lakini pia na walaji, yaani watazamaji na wasikilizaji wa kazi hizi zinazowekwa kwenye mitandao. Kwa mfano, YouTube ukiwa na views zinaonyesha kabisa nyimbo imesikilizwa mara ngapi nchi gani. Kwa hiyo, Marekani wao wanachukua kodi asilimia 30 ya content zote zinazoangaliwa ikiwa zimeangaliwa nchini Marekani. Wao wanachukulia kwamba kama mlaji ni Mmarekani basi ametumia facilities zetu kuitumia hii YouTube kwa hiyo asilimia 30 yetu tunaitaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali na sisi tuna wasanii wetu wengi na wasanii wa nje ambao wanaangaliwa hapa. Kwa mfano DJ Khaled akiangaliwa Tanzania si inakuwa imeonekana kwamba ameangaliwa mara ngapi na sisi tupate percent yetu kama sio 20, 30 lakini tuichukue. Kwa nini Wamarekani wachukue asilimia 30 na sisi tusipate hata percent moja wakati walaji ni wetu, fedha na facilities walizotumia ni za kwetu na sisi tunastahili kupata fedha hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna platforms zingine nyingi ambazo ni plugs ambazo wasanii wetu wanaweza kuweka mziki wao na wasikatwe hata senti moja yaani wasipite kwa hawa aggregators. Ndio maana kwa sasa tumepunguza sana kufuatilia kuwa na aggregatoror kwa sababu tunaona kwamba kuna namna mbadala tunaweza tukaendesha shughuli zetu bila kuwa nao. Kwa mfano, Caller Tune wanakutoza kwa wimbo unao-upload ama album na ni dola kumi ama dola 100 kwa album na unapata ingizo lako lote ya nyimbo zako namna ambavyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Nakuongeza sekunde ishirini.

MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nihitimishe kwa kusema kwamba naiomba Serikali hasa Wizara ya Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari iweke dawati maalumu la kwa ajili ya kuwasaidia watu wetu hasa wasanii na content creator kuhusiana na ufahamu wa masuala haya. Nasema hivyo kwa sababu tunapoteza pesa nyingi na tuna vijana wengi wa Kitanzania ambao ufahamu wao kwenye masuala haya ni mkubwa wanaweza kutusaidia kutuongezea pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii na mimi niweze kuongeza senti 50 zangu kwenye bajeti hii ya Wizara ya Habari, Utamaduni Sanaa na Michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asubuhi wakati wa michango, moja ya wachangiaji dada yangu Ester Bulaya aliongelea wanahabari na kidogo kukawa na lawama ya kwamba Wabunge wote ambao walitangulia kutoa michango hawakuwa wamewaongelea wanahabari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme hili ni suala ambalo tumekuwa tukilifikiria kwa muda mrefu ya kwamba Wizara hii ina matawi mengi kiasi kwamba matawi mengine yanafichwa sana. Ningetoa pendekezo heshima kwa mamlaka husika kuona kama tunaweza kuipunguzia matawi Wizara hii kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano habari imekaa sana kama inafanana na Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari na hali kadhalika utamaduni umefanana sana na Maliasili na Utalii ili tubaki na Michezo na Sanaa ambavyo kusema kweli asilimia 98 ya michango iliyotoka leo ilikuwa inaelekea huko, kama itazipendeza mamlaka kwa hisani yao naomba waliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nitoe pongeze kwa Serikali na Azam Media kwa mkataba mzito wa haki za television za ligi yetu kuu, mkataba ule ambao haujawahi kutokea kwa nchi za Afrika Mashariki ni mkubwa sana na sisi watu wa mpira tunaimani kwamba unakwenda kusaidia mpira wetu. Watu wa mpira tunafahamu masuala ya fedha yalivyokuwa yanaathiri ubora wa ligi yetu, timu nyingi zilikuwa haziwezi hata kusafiri zenyewe mpaka zichangishe washabiki wake na hili lilikuwa linafanya michezo mingi iamuliwe siyo kwa sababu ya ubora wa michezo yenyewe, ubora wa wachezaji na ubora wa timu, isipokuwa kwa uwezo ama kutokuwa na uwezo wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na ndiyo maana unasikia kila siku kuna maneno maneno mara huyu anasema ametaka kupewa milioni 40, hivi vitu ni vya kweli na ninaamini sasa Azam kwa namna moja ama nyingine wamekwenda kuzirekebisha. Kule kwetu tunasema kila harusi inamshenga wake na sisi tunaamini ya kwamba Azam Media ndiyo washenga wa mpira wa nchi hii, kwa hiyo, hii naomba nichukuwe nafasi hii kupitia Bunge lako Tukufu kuwapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo langu kwa Wizara ni iwekeze nguvu zake kwenye kutafuta fedha zaidi kwa ajili ya kuwekeza kwenye ngazi za chini, mashuleni na huku kwenye field. Ukienda majimboni moja ya matatizo makubwa ambayo unaulizwa kila siku na vijana ni vifaa vya michezo na viwanja; hawataki nyasi, hawataki viwanja vya milioni 300 kama alivyopendekeza ndugu yangu Senator Sanga asubuhi wanataka tu viwanja vinavyotosha kuweza kufanyia kazi vipaji walivyojaliwa na Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kusema ukweli ni gharama kubwa, naona Wabunge hawana uwezo wa kuyamudu hayo. Mimi mara ya mwisho kuna kata inaitwa Kwaibada katika jimbo la Muheza vijana waliniomba niwasaidie wakati TARURA wakienda kule wawasaidie kuchonga/kurekebisha uwanja wao ambao umekaa upande mmoja uko mlimani, upande mmoja uko chini, nilivyowaomba TARURA wakaniletea bill ya milioni 13 kwa ajili ya kurekebisha uwanja ule, nikaona sasa TARURA nao hawataki uwanja utengenezwe bado nawaza namna ya kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nipendekeze kwamba Wizara ione namna ambayo kama inaweza kupeleka fedha zaidi mashuleni na majimboni ikiwezekana kwa ajili ya vifaa na kurekebisha viwanja hivi sehemu za vijana kufanya michezo hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni ushiriki wa wachezaji wa nje kwenye ligi zetu, ukiangalia ligi yetu na idadi ya wachezaji wa nje ambao wanatupa burudani kubwa naweza kuwataja wengi hasa walioko katika timu ya Simba unaweza kuona kabisa kwamba kama siku moja wachezaji wale wa nje wataondolewa kwenye ligi yetu, ligi yetu itakuwa na ladha tofauti na itakuwa kwenye kiwango kidogo kuliko ilivyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushiriki wa wachezaji wa nje ni mzuri sana, unawapa changamoto wachezaji wetu, lakini niiombe tena Serikali namna ya kulifanya hili ni kuhakikisha kwamba tunapeleka nguvu huku chini ili na sisi tutengeneze wachezaji ambao wanaweza kucheza nje ya nchi ama ambao peke yao kama wataweza kucheza kwenye ligi yetu basi ligi yetu itakuwa na msisimko kama iliyonayo sasa hivi. Lakini bila Serikali kutilia mkazo michezo ngazi hizi za nchini, uwezo wa timu yetu ya Taifa utaendelea kuwa dhahifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni hili jambo la BASATA; kwanza niseme kwamba mimi bado niko kwenye majukwaa mengi ya wasanii na asilimia 98 ya wasanii wa nchi hii tunakubaliana mambo mawili; aidha, BASATA inahitaji major reform ama sheria inayowekwa kuundwa kwa BASATA iondolewe kabisa tuwe na chombo kingine kwa ajili ya kulea wasanii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Baraza hili liliundwa mwaka 1984 kwa sheria namba 23 na liliunganisha Baraza la Muziki Tanzania - BAMUTA na Baraza la Sanaa la Taifa kwa wakati huo, na malengo yake ukiyasoma kwenye sheria ya mwaka 1984 ambalo ililiunda unaweza kuona kabisa hayakuwa na walakini, hayakuwa na viashiria, hayakuwa na maelekezo ya moja kwa moja kwamba baraza hili linakwenda kuwa polisi kama ambavyo liko sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa sheria ya mwaka 1984 kazi za baraza ni pamoja na kufufua na kukuza maendeleo na utengenezaji wa kazi za sanaa, kufanya utafiti wa maendeleo kutoa huduma za ushauri na msaada wa kiufundi kwa ajili ya maendeleo na shughuli za biashara na sanaa, kupanga na kuratibu shughuli za sanaa na nyinginezo nyingi, lakini hakuna mahali popote kwenye sheria hii ya mwaka 1984 ambapo baraza lilikuwa na kazi ya kusajili na kuhakikisha kwamba linapitia na kupitisha mashahiri ya nyimbo kama linavyofanya sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wengine tumefanya muziki kwa takribani miaka 19; sijawahi kukaguliwa wimbo wangu na sijawahi kufungiwa wimbo wangu kwamba nimewahi kutumia lugha ya matusi. (Makofi)

Sasa tunajua umuhimu wa kuangalia maadili na hatuna wasiwasi nao, hatuna matatizo nalo, lakini suala la Baraza kujipa jukumu ambalo linatuongezea urasimu, ambalo linafanya kazi yetu iwe ngumu, wakati halina msaada wowote kwenye maisha ya msanii wa Kitanzania wala sanaa lenyewe ni suala ambalo sisi halikubaliki kwetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi hatuombi haki ya kutukana kwenye nyimbo, wala hatuombi haki ya kuchochea, kuleta uchochezi kwenye nyimbo, tunachoomba ni haki ya kutengeneza muziki, kufanya sanaa yetu bila kuwa na vikwazo vingi ambavyo baraza hili kwa sheria hii ya mwaka 2019 linajaribu kuifanya. (Makofi)

Kwa hiyo, mimi ninachoona ni kwamba Baraza linajaribu kwa nguvu nyingi sana kuichonganisha Serikali na wasanii, hiki kitu wasanii wote nchi hii wamekikataa na tunashukuru hekima za Waziri na Katibu Mkuu wetu wa Wizara hii ambao walikwenda wakahamua kukisimamisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachikiomba ninajua sheria bado ipo na Waziri na Katibu Mkuu wameisimamisha kwa hekima zao kuona namna ambavyo kitu gani kinaweza kufanyika kuirekebisha.

Sasa mimi sitaki kuhitumia hii kama ground ya kushika mshahara wa Waziri, ninachoomba ni commitment ya Waziri wakati hakija kufanya majumuhisho kuonesha commitment ya Serikali kwamba sheria hii inarekebishwa road map ya marekebisho ya sheria hii ili isiende kuendelea kuwakwaza wasanii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na la mwisho ni suala la COSOTA. Nimefurahi kwamba COSOTA sasa inaamka na pamoja na mambo mengine inaanza kukusanya blanks up levy ambayo ni kodi inayokusanywa kwa sababu ya vifaa vyote ambavyo vinaweza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HAMISI M. MWINJUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba dakika moja.

NAIBU SPIKA: Haya, malizia.

MHE. HAMISI M. MWINJUMA: Sasa tunachoomba sisi kwa Wizara kuwe na mgawanyo separation ya copyright office na collective management organization, kwa sababu Serikali najua mnaanza kuchukua fedha kutoka media houses mbalimbali, sisi tunaomba tukusanye fedha kutoka sehemu nyingine ambazo zinatakiwa kupewa leseni ya kutumia kazi za sanaa kama mahoteli, kama mabasi, hair saloon na barber shop. Sheria ya Namba 7 ya mwaka 1999 imeshasema haya waziwazi na kabisa hata uki-charge shilingi 7,000/8,000 kwa haya maeneo haya yote na tumeshafanya research unaweza kujikuta na bilioni 54 kwa units ambazo zipo zinazotakiwa kukusanya mapato haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sisi tunaomba wakati Serikali inatusaidia kukusanya kwenye media houses, sisi tukusanye kwenye haya maeneo mengine na tuisaidie Serikali pamoja na mambo mengine kukusanya kodi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme nina grounds kadhaa ambazo naweza kuzitumia kushika mshahara wa Waziri lakini sitaki kuzitumia ninachoomba..

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, dakika niliyokuongeza imeisha.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii na mimi niweze kutoa mchango wangu kwenye Bajeti ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kutoa pongezi kwa Mheshimiwa Rais tunasema ameanza vizuri mno. Huku mtaani kauli ni kwamba Mheshimiwa Rais anaupiga mwingi, kule kwetu tunasema Mheshimiwa Rais ameanza na mguu wa kutoka na mguu wa kutoka Mtume ameuombea. Mambo mengi ya awali kabisa ambayo Mheshimiwa Rais ameanza kuyafanya yanatupa imani kwamba nchi ipo kwenye mikono salama na sasa Mama ndiyo ameshika usukani na tunako elekea kunatupa matumaini makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, milioni 500 kwa kila Jimbo kwa ajili ya TARURA zimefika hata Wilayani Muheza na Mimi na Engineer wangu wa TARURA Engineer Kahoza pale tumeshajadiliana ziende zikatengeneze barabara zipi tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kupandishwa madaraja kwa wafanyakazi na ahadi ya ongezeko la mishahara mwakani najua wafanyakazi wanalisubiri hili sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nichukue nafasi hii kumpongeza Kaka yangu Comrade Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, Waziri wa Fedha na Mipango, Naibu Waziri Injinia Hamad Masauni, Katibu Mkuu na Wasaidizi wao kwenye Wizara ya Fedha kwa bajeti hii, bajeti iliyonyooka, bajeti yenye matumaini makubwa na ambayo inaonyesha kwamba Wizara ya Fedha na nchi kwa ujumla ipo pia kwenye mikono salama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kusema kweli Comrade Mwigulu ningependa kulisema hili huku namuangalia usoni huku mtaani tunasema hana baya, anafanya vitu vyote, majukumu yote anayoyafanya kwa usahihi mkubwa, shida yake inakuja tu anapoanza mambo yake ya Yanga. Yaani najua amejizuia kwelikweli kutoweka japo Bilioni Tano kwenye hii bajeti kwa ajili ya kuisaidia Yanga kuwa bingwa mwakani, lakini ndiyo hivyo tusingekubali. Nimpe pongezi sana Comrade Mwigulu na naamini kwamba hata namna zake za ukusanyaji wa mapato ambazo amezipanga unaona kabisa bajeti yetu safari hii inaenda kutekeleza kwa zaidi ya asilimia 67.9, ambapo bajeti iliyopita ilitekeleza kwa vile inaonyesha kwamba kasungura kake katakua kakubwa safari hii. Nimpongeze kwa mara nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina machache tu ya kuweka kwenye bajeti hii kwa vile kama nilivyosema bajeti imetimia kusema ukweli, lakini ningeweza kuongezea hakuna ziada mbovu waswahili wanasema na la kwangu ninalotaka kuliweka ni kuhusiana na mifuko yetu ya uwezeshaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa tovuti ya uwezeshaji tunayo mifuko 45 ya uwezeshaji. Hakuna namna tukawa na mifuko 45 na majukumu yake yasiingiliane kwa namna moja ama nyingine. Kuna mifuko ambayo kazi zake zitakuwa zinagongana na kwa namna hiyo inaipunguzia ufanisi na inatupunguzia pia uwezo wa kui-monitor kwa kadri ambavyo tulitakiwa tufanye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua kwamba kuna mchakato wa kuunganisha baadhi ya mifuko maoni yangu ni kwamba mchakato huu uongezewe nguvu na ufanywe kwa makusudi makubwa kabisa mifuko mingi zaidi iunganishwe ili mradi tuwe na mifuko michache ambayo tunaweza kuisimamia, pia ambayo tutahakikisha kwamba ufanisi wake unakuwa wa kiwango cha juu kama lengo la kuanzishwa kwake lilivyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya mifuko hii 45 hatuna hata mfuko mmoja wa ubia venture fund ambacho kimsingi tuna mifuko ya dhamana kwanza hakuna taarifa za kutosha kuhusu uwepo wake, takwimu zinaonyesha kwamba ni asilimia 30 tu ya wananchi wanaufahamu kuhusu mingi ya mifuko hii kati ya mifuko hii 45. Kwa hivyo, haifanyi kazi yake na kuna mifuko ambayo inafikisha mpaka mwaka mzima haijaweka fedha popote na inachofanya ni kuweka fedha benki ili ku-play safe isipate hasara, sasa hili siyo lengo hasa la kuanzishwa kwake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna biashara nyingi huku kwenye field uraiani ambazo kimsingi zinachohitaji siyo tu kupewa mikopo na ikusanywe baadaye, lakini kinachotakiwa hasa ni uwezeshwaji wa moja kwa moja. Biashara nyingi zinafanywa na wajasiriamali ambao hawana kweli ufahamu wa kutosha kuhusiana na biashara na tunaishia tu kwenye kukopesha vijana kwa kutumia mifuko ya Halmashauri, lakini wanafanya miradi ya boda boda na miradi ya kuku na unapata malalamiko mengi kuhusiana na ufanisi wa mifuko hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sijawahi kukaa siku tatu kwenye Ofisi ya Mbunge wa Jimbo la Muheza na nisikutane na malalamiko, mawili ndiyo yanakuja sana either kwamba mifuko hii haijawafikia watu wengi wanakuja watu wengi ambao wametekekeleza vigezo vyote lakini wanashindwa kupata mkopo kwa sababu sasa ukiwa na milioni 200 ambazo unatakiwa kuwakopesha makundi yote haya matatu unawakopesha vijana wangapi kati ya wananchi takribani 300,000 wa Wilaya nzima ya Muheza.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni kuhusiana na wanaopata mikopo hii lakini wanashindwa kuirejesha na hii inatokana na uwezo mdogo wa namna ya kuwekeza kwa hiyo unakutana na kwamba…

(Hapa kengele ya kwanza ililia)

MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kengele ni ya kwanza?

NAIBU SPIKA: Ni kengele ya kwanza.

MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, unakutana na suala kwamba Mkurugenzi wa Halmashauri anamshtaki raia kijana kutoka Wilayani kwako kwa vile wameshindwa kufanya marejesho sasa unakaa katikati unataka marejesho yafanyike ili watu wengine zaidi wafaidike na mikopo hii, lakini juu ya yote hutaki mwananchi wako apelekwe mahakamani kwa kukosa kurejesha mikopo. Kwa hiyo, unakuta upo mahali kama mwanasiasa, kama mtumishi wa wananchi ngoma yako inakuwa ngumu, kwa vile lengo la mikopo hii ikafanye kazi iliyokusudiwa, lakini irejeshwe, lakini kwa sababu hatuna upeo wa kutosha kuhusiana na biashara tunazotaka kuzifanya inaishia kupotea hewani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wiki mbili zilizopita nilimsikia ndugu yangu Waziri Patrobass Katambi anasema Ofisi ya Waziri Mkuu ilikuwa imetoa shilingi bilioni 4.9 na kati ya hizo zilizorejeshwa ni shilingi milioni 700 peke yake, bilioni 4.2 imepotea hewani, hakulisema lakini nina wasiwasi hata yeye anaamini hiyo hela haitarudi na kazi ya Serikali ni kuhudumia wananchi wake, sasa utashindana na wananchi kwenda nao mahakamani kila wakati mpaka lini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maoni yangu ni kwamba sasa ni wakati wa kuzihusisha taasisi binafsi za fedha zitusaidie kufanya jukumu hili badala ya kuwakopesha tu na kukusanya mikopo hii kwa wananchi sasa tunachotakiwa kwenda kufanya ni kuwashirikisha kwa kuwa na ubia kati ya Serikali, taasisi binafsi za fedha na wananchi hawa wajasiriamali ili kuhakikisha kwamba mikopo hii, haiwi ni mikopo lakini inakuwa ni uwezeshaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, biashara nyingi kwa mfano za Katani kule Kigombe, Ngomeni, Pande, Darajani, Wilayani Muheza hata ukiziambia zirudishwe baada ya mwaka mmoja zinakuwa bado hazijakomaa sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Katani inaanza kuvunwa baada ya miaka mitatu unampa mtu mkopo ambao anatakiwa kurudisha baada ya miezi kadhaa anazipata wapi, inabidi atoe kati ya hizo hizo kuanza kufanya marejesho. Kwa hiyo tukiwa na venture fund zitasaidia kwa sababu tunachoenda kufanya sasa inakuwa ni kuwekeza kwa pamoja kati ya Serikali, taasisi hizi binafsi za fedha na wajasiriliamali wale wadogo na marejesho yake yanaenda kupanua zaidi mifuko yetu hii na itasaidia watu wengi zaidi kuliko ambavyo inafanya sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili halitoki tu hewani lipo katika SME Policy ya nchi yetu ya mwaka 2003 na nchi ambayo inafanya vizuri mifuko hii kwa ubia ni Ghana na Ghana walipata sera hii kutoka kwetu, sasa sisi tuliandika lakini hatujawahi kuifanyia kazi wenzetu wameichukua na inafanya kazi sawa sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha, naomba niseme kwamba naunga mkono hotuba ya bajeti ya Waziri Mwigulu na naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kibali kilichotuwezesha wote kuwepo hapa leo, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mama yangu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa imani kubwa anayoendelea kuwa nayo juu yetu na ahadi yangu ni ile ile, hatutamwangusha, tutafanya kila lililo ndani ya uwezo wetu kuhakikisha Sekta ya Utamaduni, Sanaa na Michezo ya nchi hii inaacha alama wakati huu wa utawala wake wa Serikali ya Awamu ya Sita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru pia Mheshimiwa Waziri kwa miongozo mingi ambayo amekuwa akinipa, Mama yangu experience yake na yeye inanifaa mpaka mimi sasa. Kwa kweli namshukuru sana najifunza mengi kutoka kwake na naamini naiva zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru Watendaji wa Wizara wakiongozwa na Katibu Mkuu, Ndugu yangu Saidi Yakubu na Naibu Katibu Mkuu Ndugu yangu Nicholas Mkapa na Watendaji wote kwa ushirikiano mkubwa wanaonipa. Vilevile, naishukuru sana familia yangu, mapenzi ni mengi kwa kweli na wananchi wenzangu wa Muheza kwa kuendelea kuniunga mkono, kuniongoza na kunipa ushirikiano wa hali na mali, ninyi ni vyuma kweli kweli na Muheza inarudi kwenye ramani vizuri kama ambavyo tulikuwa tumekubaliana ndugu zangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii pia kuzipongeza timu zetu. kwanza kabisa, ninaipongeza timu ya Dar es Salaam Young Africans ambao wamekuwa washindi wa pili, niseme tu kikanuni kwa sababu Yanga hawakufungwa kwenye hizi mechi mbili za fainali bali walishindwa tu kuchukua ubingwa kwa sababu ya kanuni. Kwa hiyo, tunakubaliana wamefanya vizuri sana na wameiletea sifa kubwa nchi na hata zile fedha ambazo Mheshimiwa Rais alikuwa anatoa pamoja na ndege matunda yake yameonekana. Hongereni sana Dar es Salaam Young Africans. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niipongeze Klabu ya Simba kwa kufika robo fainali ya ligi ya Mabingwa wa Afrika. Robo fainali ya ligi ya Mabingwa wa Afrika siyo nafasi ndogo na Simba imekuwa wakirudia mara kwa mara kiasi kwamba lengo sasa hivi ni kuivuka na ninaamini mkijipanga vizuri msimu huu unaokuja pengine tunaweza kuona maajabu. Vilevile, niwapongeze kwa outstanding performance consistently kwa miaka mitano iliyopita iliyosababisha mpate nafasi ya kushiriki Super League. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Super League ni league ya vilabu vya Afrika ambavyo vinahusisha timu nane. Tuna nchi Hamsini na kitu kwenye Bara hili lakini vilabu ni nane tu vilivyopata nafasi ya kushiriki. Ni vile vilabu ambavyo performance zao zinaonekana zina mashiko kweli kweli na vigezo vingine vingi ambavyo wameviweka, Klabu ya Simba imevifikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni matumaini yangu kama timu ya Yanga na yenyewe itaendele na performance iliyoifanya mwaka huu basi pengine tutakuwa na timu mbili kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Shirikisho la Soka Afrika wakati naongea nae kwamba, tuna vigezo Klabu ya Yanga inatakiwa ivifikie ili tuwe na timu mbili. Kwa hiyo kila la heri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujibu hoja kadhaa ambazo zimetangulizwa na Waheshimiwa Wabunge kabla Mheshimiwa Waziri kuja kuhitimisha hoja yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikubaliane na hoja ya Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo, kwamba utamaduni ni mtindo wa maisha na ni zile kawaida za watu na namna tunavyoishi, kwamba matatizo mengi ambayo tunayo yangeweza kuondoka kama tungeyatengenezea utamaduni na kuusimamia ukatekelezwa, hili nakubaliana nae.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sisi tuna mambo mengi na miongoni mwa mambo ambayo yamesemwa ni kuhusiana na taasisi zetu kushindwa kufikisha yale malengo ya maduhuli ambayo tulikuwa tumepanga kwamba tutayakusanya. Sasa kwa sababu ya muda nitoe mfano wa taasisi yetu moja tu ya COSOTA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tumekubaliana kwamba COSOTA mwaka 2022 itakusanya shilingi bilioni 1.35 lakini walishindwa kufikisha na sababu zipo wazi. Sababu moja ni kwamba mazingira na sheria ambazo zilikuwa zimetumika kuweka matazamio yale wakati ule yalikuja kubadilika hapo katikati na yakwafanya wawe chini ya kiwango kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano mabadiliko ya Sheria ya Hakimiliki na Hakishiriki ya mwaka 2022 ambayo yalikuwa yanatuelekeza kwamba tutaaanza kukusanya zile kodi kwenye devices ambayo haijaanza mpaka sasa hivi lakini yenyewe tuliijumlisha kwenye makusanyo yao. Vilevile elimu kwa wale ambao wanatakiwa kulipa ile mirabaha na ushirikiano mdogo ambao tunaupata, lakini hilo ndugu zangu Wabunge tunalishughulikia na hasa wana Kamati ambao walilileta. Miongoni mwa mambo ambayo tumeyafanya hivi karibuni kwa maelekezo ya Waziri, nimewaomba COSOTA wanipe majina na idadi ya fedha wanazodai kutoka kwa wale wadaiwa wao sugu na wamefanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nitumie Bunge lako tukufu kutoa salamu kwa wale ambao ni wadaiwa sugu kwa COSOTA kama wanaona kwamba kutumia kazi za sanaa ni halali yao bila kuwalipa hawa wasanii waliozifanya kazi hizi wajiandae. Bunge hili litakapokwisha mimi kwa maelekezo ya Waziri nitakwenda mwenyewe mtaani kuhakikisha kwamba tunazifungia sehemu hizi na hazifanyi shughuli zinazozifanya za kutumia kazi za sanaa za nchi hii bila kuwalipa wasanii ambao wametoa machozi, jasho na damu katika kuzitengeneza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niihakikishie Kamati kwamba hili tutalifanya na mimi kama msanii sitakaa hapa nione kwamba wasanii wengine wanadhulumiwa na haki zao hazipatikani kwa sababu tu ya matakwa ya watu kutotaka kutoa ushirikiano. Hiyo ni moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, ilikuwa ni hoja ya ndugu yangu Mheshimiwa Sanga kuhusiana na CSR za kampuni zinazotekeleza miradi mikubwa nchini zitusaidie kutengeneza miundombinu ya michezo kwenye nchi hii. Huu mpango sijui Mheshimiwa Sanga umeupata wapi lakini ni kweli kwamba sisi tulikuwa nao tayari sijui ni kidege gani kimekuibia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ina maelekezo ya kujenga stadiums mbili Arusha na Dodoma, miongoni mwa vyanzo vya mapato ni CSR za miradi mikubwa katika sekta ya fedha, nishati na madini. Sasa, tayari Wizara imeanza kufanya mawasiliano na Wizara husika nilizozitaja hapo na nikuhakikishie mawasiliano yanaendelea vizuri na tutalifikia lengo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, njia nyingine ambayo tumeipanga ni kuhimiza Corporate Social Investment, Wawekezaji wafanye uwekezaji wa kijamii ambapo unaweza kujenga viwanja ukavipa jina la Kampuni yako na kadhalika. Hilo nalo tunalifanyia kazi na nikuhakikishie tuko katika hatua nzuri na hili tutafanikiwa. Kazi tuliyopewa ni kujenga viwanja na hizi Arena na Mheshimiwa Sanga hizi fedha tutazipa na Arena na Stadium zitajengwa katika nchi kama ambavyo maelekezo ya Mheshimiwa Rais yametoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni mgao wa mapato wa viingilio. Hili ningetaka kujibia. Hili ni suala la kisheria na kikanuni Mheshimiwa Sanga na kitu ambacho hakiwezi kubadilika ni ile asilimia 18 ya VAT na asilimia tatu ambayo inakwenda kwa BMT. Hayo mengine ni ya kikanuni ambayo TFF inakaa na wadau wake ambao ni vilabu kabla ya msimu kuanza na wanakubaliana. Sasa kwa maoni yako na maoni ya Wabunge wengine wengi ambao walishayatoa kuhusiana na jambo hili, sisi tutaielekeza TFF wakati inakaa na wadau wake ambao ni vilabu kabla ya msimu ujao kuanza, waangalie haya makato kuona namna amabayo wanaweza wakawapunguzia vilabu vyetu mzigo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli mimi kwa sababu ya kuwa mtu wa mpira humu ndani ndani, nafahamu namna ambavyo vilabu vinaingia gharama kubwa za kuendeshwa na namna ambavyo zinapitia wakati mgumu hata wakati mwingine kufika kituo kingine kwa ajili ya kucheza mechi zao. Kwa hiyo, tutafanya kadri tunavyoweza TFF waliangalie wasiwape mzigo vilabu vyetu na yale ambayo yanaweza kuongeleka na yakabadilika yatabadilika mtuachie sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la shule za michezo ulisema Mawaziri wawili wamepita. Nikuhakikishie Waziri Balozi Dkt. Pindi Hazara Chana anakwenda kufanya miundombinu ile kwenye shule zetu za michezo hilo halitashindikana. Hivi ninavyokuambia tenda itatangazwa hivi karibuni ya marekebisho kwenye viwanja vyetu vya michezo na ujenzi wa viwanja vipya vya michezo kwenye zile shule zetu 56 utaanza. Kwa hiyo, kama lilishindikana huko sasa hivi halishindikani kaa utulie uone muziki ndugu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dada yangu Mheshimiwa Khadija (Keisha), alizungumzia kuhusiana na tuzo. Hili nalo nililiombea ruhusa maalum kabisa kwa Mheshimiwa Waziri ya kwamba hili suala la tuzo Mheshimiwa Waziri niachie mimi na nimekwishakabidhiwa. Tutakapomaliza Bunge hili la Bajaeti naanza kushughulika nalo kwa ajili ya tuzo zinazofuata. Kwa hiyo, hili niachie mimi wala usiwe na wasi wasi nalo na tutalipatia suluhisho. Tuzo za mwakani nikuahidi Dada yangu zitakuwa za aina yake na zitakuwa za picha tofauti kabisa na ilivyokuwa huko nyuma. (Makofi)

(Hapa kengele I;ilia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Naibu Waziri, ahsante sana.

NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na mambo mengine ya kusema lakini naamini Mheshimiwa Waziri ameya – capture na atayasema wakati wa kuhitimisha hoja yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa hii na mimi niweze kuchangia kwenya hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi. Sina hakika kuhusiana na mambo niliyoandika yalivyo mengi kwa hiyo nitaenda moja kwa moja kwenye hoja yangu, kama muda utaniruhusu nitaleta pongezi zangu mwishoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukianza kwa nukuu kutoka kwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, anasema: ‘‘Ili nchi iendelee na ipate maendeleo inahitaji watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora.” Kwa kichwa kizuri kama cha Mwalimu Nyerere ambacho tunakubaliana kwamba hata ambao hawakubaliani na siasa zake huko duniani wanakubaliana na ubora wa kichwa chake, kuiweka ardhi miongoni mwa vitu vinne muhimu kwa ajili ya maendeleo ya Taifa siyo kitu kidogo hiki wote tunakubaliana nacho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo mimi ninachoona ni kwamba kwanza suala la ardhi kuwa miongoni mwa vitu vinne muhimu kwa ajili ya maendeleo ya Taifa, ni zawadi na laana. Ni zawadi kwa sababu ardhi tunayo kubwa na kama itatumika ipasavyo kwa sheria tulizojiwekea na wasimamizi wake wakafanya vile ambavyo tumewatuma kufanya, itatuelea maendeleo bila wasiwasi wowote, lakini ni laana kama yatafanyika kinyume chake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa ardhi unafanya uwezekano wa kuepuka kabisa migogoro ya ardhi kutokuwepo, migogoro ya ardhi ni kitu ambacho tunatakiwa kuishi nacho, tuifanyie kazi tuisuluhishe kila wakati kuhakikisha kwamba wananchi wanyonge wanapata haki zao kama wananchi ambao wana nguvu kuliko wengine. Kwa hiyo, ni ongoing nisichokubaliana nacho ni jinsi ambavyo tunatengeneza migogoro na mingine ambayo pengine tungeweza kuitatua wakati ni midogo tunaiacha inakuwa milima mikubwa ambayo inakuwa migumu kuitatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna Mbunge hata mmoja kwenye Bunge hili tufuku wa Jimbo ambae hana mgogoro kimeo wa ardhi kwenye Jimbo lake, hiyo inakuonyesha jinsi ambavyo kuna matatizo makubwa ya ardhi kwenye nchi hii. Sasa pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri alisema kwamba mikutano 1,800 kwa ajili ya usuluhushi wa migogoro ya ardhi ilifanyika mwaka uliopita, lakini bado nimuombe Mheshimiwa Waziri afanye mikutano zaidi aendelee kwa nguvu nyingi asichoke mama yangu na ndugu yangu Ridhiwani pia muendelee kwenda site kuhakikisha migogoro ya ardhi inaendelea kutatuliwa siku hadi siku, siamani kwamba kuna siku tutafika hatuna hata mgogoro mmoja wa ardhi kwenye nchi hii lakini angalau tuibadilishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro iliyokuwapo juzi na siku kabla ya juzi isiwepo leo na kesho. Katika Jimboni la Muheza tuna matatizo makubwa ya ardhi, mathalani naweza kuorodhesha migogoro karibu 15 hapa, lakini kwa sababu ya muda nina miwili ambayo ya mfano, kwanza kwenye Tarafa ya Amani, tuna mwekezaji East Usambara Tea Company ambaye anamiliki hekari 35,000 za ardhi, kati ya hekari 35 kulikuwa na viwanda vitano vyakuchakata chai ni viwanda viwili tu vinafanya kazi sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda vitatu vilivyobaki vimebaki kuwa magofu ambayo yanafungwa yamekuwa majumba ya kifahari pamba na nyoka kule Amani. Kati ya hekari 35,000 ambazo Mwekezaji huyu anazimiliki ni hekari 5,000 tu ambazo zinatumika kulimia chai. Sasa kule Amani kila kitu kinaota, tunayo mashamba mpaka ya mpira huu unaotengeneza matairi, tuna mashamba ya iriki, mdalasini karafuu na kadhalika. Wananchi wa Kata zote Sita za Tarafa ya Amani wanamiliki robo heka, robo heka kwa sababu Mwekezaji ameshikilia ardhi ambayo haifanyii kitu kwa zaidi miaka 25 sasa! Unashirikia hekari 30,000 ambazo huzifanyii kitu katika ardhi ambayo Kata zote Sita hakuna hata hatua moja kwa ajili ya kujenga shule. Kwa mfano, Kijiji cha Magoda Kata ya Kisiwani wanataka hata eneo la kujenga Ofisi ya Kijiji hakuna ardhi ya kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanataka eneo la kujenga Shule ya Msingi na Zahanati hakuna eneo la kufanya hivyo na kuna mtu ameishikilia hekari 30,000, my good guess ni kwamba amelichukua eneo ameenda kulitumia kama collateral kwa ajili ya kupata financing kufanya biashara zake nyingine wakati wananchi wa Tarafa ya Amani wanapata shida! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Misalai katika Kijiji cha Misalai hakuna hata hatua moja kwa ajili ya kufanya shughuli za makazi. Shamba Ngeda wanataka eneo kwa ajili ya kufanya shughuli za kilimo lakini hawawezi, hakuna hata hatua moja. Mbomole wanataka kufanya ujenzi wa shule ya sekondari hakuna ardhi, wanataka kujenga zahanati na shughuli za kilimo lakini hakuna ardhi hata hatua moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nilisema mwanzoni, ardhi hii inasitawi kila kitu. Sasa mwekezaji anapoiwekea ardhi eka 30,000 ambayo haifanyii chochote huku ni kuwaonea wananchi wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma kwenye, naomba niitafute ili nisikosee, ukisoma kweney misingi mikuu ya ardhi kitaifa, ukiacha wa kwanza ambao unasema ardhi yote ni mali ya umma na imekabidhiwa kwa Rais kama mdhamini na msimamizi mkuu kwa niaba ya Watanzania wote, wa nne unasema kudhibiti kiasi ambacho mtu mmoja au taasisi yaweza kumiliki na kutumia kwa mahitaji yake bila kuwaathiri Watanzania na wanajamii wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunapofika mahali wananjamii wengine hawana sehemu hata ya kujenga ofisi ya kijiji ama darasa moja la shule ilhali kuna mtu ana ekari 30,000 ameziweka tu amekwenda kuzichukulia mkopo sehemu huku ni kuwaonea wananchi wanyonge na Kwenda kinyume na misingi ya umiliki wa ardhi ambayo tumejiwekea kwenye nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye taifa ambalo serikali yake inasimama kwa niaba ya wanajamii wote, na inasimama kwa niaba ya watu, linapotokea suala la ukinzani kati ya watu na maendeleo basi Serikali inachagua upande wa watu. Sasa hili limekwenda mbali zaidi, hili ni watu na wanataka maendeleo halafu upande mwingine kuna mtu mmoja anayehakikisha watu hawa hawapati maendeleo.

Mimi niwaomba wawakilishi wa Mheshimiwa Rais kwenye upande huu wa ardhi, Mheshimiw Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri na Katibu Mkuu mfanya mnavyofanya, twendeni site mkawasikilize wananchi, mkawasikilize wasaidizi wenu kwenye halmashauri, na ikiwezekana na Kamishna wa Ardhi wa Mkoa ili kuona namna ambavyo tunaweza kuwasaidia wananchi wale wanyonge.

MheshimiwaMwenyekiti, wito wangu ni kumshauri Mheshimiwa Rais, kwamba mashamba haya ambayo hayatumiki yafutiwe hati na wananchi wagawiwe ili waweze kufanya shughuli zao za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mfano wa pili katika ya 15 ambayo ningependa kuitoa lakini nikasema nitasema miwili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wa pili ni kuhusiana na jinsi ambavyo watu ambao tumewapa mamlaka ya kutafsiri sheria za ardhi kwa ajili ya jamii nzima wanavyotukosea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2017 laliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati John Pombe Magufuli, Mungu amrehemu, alipita Mkoani Tanga. Miongoni mwa vitu alivyovifanya ni kufuta hati sita za yaliyokuwa mashamba ya mkonge kwa sababu yalikuwa hayatumiki. Kwenye mkutano wa hadhara pale Mkanyageni aliamrisha kwamba shamba lililokuwa la Geiglits ambalo lilikuwa katika Kijiji cha Muungano ligawiwe kwa wananchi wa maeneo yale; kwamba kila mwananchi apate eka tatu, na mwenye uwezo wa kuendeleza apate ekari tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2017 mpaka sasa hivi ni mwaka 2022, nikuambie kwamba zoezi hili halijafanyika hata kwa asilimia 20. Sasa unapata walakini, maelekezo yalikuwa wazi, kwamba kuna eneo kuna wananchi, idadi ya kaya inafahamika kwa sababu Mheshimiwa Rais hawezi kufuta, na akaamrisha kwamba kila kaya ipate eka tatu. Vivyo hivyo mchakato ule haujaweza kutimia hadi leo. Sasa una watu, una ardhi, kila kimoja unajua ukubwa wake lakini zoezi hili linashindikana kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili pia nimuombe Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri na wasaidizi wao twende tukawasikilize wananchi. Moja, tupate vielelezo kutoka kwa wananchi, maafisa wa ardhi kule chini na tuone kitu ambacho tunaweza kukifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule chini kuna kamati ya wazee tisa kwenye Kijiji cha Muungano pale Kilapula, mzee mmoja anaitwa Dkt. Mhada amenitumia email 22, yaani imepita juzi tu, na Mheshimiwa Mnzava ni shahidi wangu, sija-exaggerate kituo chochote. Email 22 zenye vielelezo za kwa nini anahisi wananchi wanyonge wanaonewa na wanataka kudhulumiwa ardhi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisemi kwamba iamuliwe tu kwamba wakagawiwe, lakini twende tukawasikilize na tuone vielelezo ambavyo wanavyo na tuamua kwa conscience zetu zikiwa clear kabisa, tukiwa tumejitosheleza na vile vielelekezo ambavyo wanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya ardhi iko mingi sana Wilayani Muheza, na ninaomba Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri wanipe angalau siku tatu za kuambatana nao kule kuhakikisha kwamba tunakwenda kuitatua yote. Sina mpango wa kushika shilingi, kusema kweli kama mtaniahidi hilo wakati mnakuja kufanya majuisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na niwapongeze na Mheshimiwa Rais, na ninaamini mtafanya kazi nzuri. Niwahakikishie, sisi tuko pamoja nanyi. Wananchi wa Wilaya ya Muheza wana Imani kubwa na Serikali yao ya Awamu ya Sita, chini ya Mama, Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Niwahakikishie kwamba kama tutawaondolea kero hizi ndogondogo basi mtashangaa na matokeo ya kuungwa mkono ambayo mtayapata kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana, ninaomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi ili niweze kuweka senti 50 zangu kwenye bajeti ya Wizara hii ya Utamaduni, Sanaa na Michezo.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa ndugu yangu Sharifu wa Kipumbwi kule Pangani Jumaa Hamidu Aweso anasema asiyeshukuru kwa kidogo, hawezi kushukuru kwa kikubwa. Nitambue mchango mkubwa na kazi nzito inayofanywa na wasaidizi wa Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kwenye Wizara hii; ndugu yangu Waziri, Mohamed Mchengerwa; Naibu Waziri, dada yangu Pauline Gekul; Katibu Mkuu, Dkt. Hassan Abbas; na ndugu yangu Said Yakubu, Naibu Katibu Mkuu ya kuitafsiri dira na maono na huruma za Mheshimiwa Rais kwa wanamichezo, wanasanaa na wanautamaduni wa nchi hii. Kazi nzuri wanaifanya na kusema kweli tunaiona na tunawashukuru sana na ushirikiano wanaotupa ni Mungu tu anayeweza kuwalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina mambo kadhaa ambayo napenda kuchangia, kwa hiyo, muda usipotosha mengine nitayaweka kwenye maandishi. La kwanza kabisa ambalo sitaki kuliweka mwisho, usije muda ukaniishia na sijalisema ni hili suala la mirabaha. Kusema ukweli kazi nzuri imefanyika, kazi nzuri imefanyika na hasa kwenye uthubutu. Mirabaha hii siyo mara ya kwanza kugawiwa, lakini mara ya mwisho iligaiwa mirabaha ya mwaka 2018 na kabla ya hapo ilikuwa ya 2014. Kusema ukweli kuna mazingira mengi ambayo yalikuwepo, yalikuwa yanafanya mirabaha ishindikane kugaiwa, lakini pia yalikuwa hayawezi kurekebishwa kama hatutaanza kuigawa, yaani ile lazima mvua inyeshe ndio tujue wapi panapovuja. Sasa hivi mvua imenyesha, tumejua wapi panapovuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa pamoja na kuwa na complain, complain, kutoridhika kwetu kuhusiana na ugawaji wa mirabaha ile, nani kapata kiasi gani, kwa nini na vitu vya namna hiyo, lakini niwapongeze kwa uthubutu ule. Shida yangu kwenye mirabaha ni namna ambavyo tunaifanya tokea mwanzo, ukusanyaji na ugawaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze mwanzoni kabisa, mirabaha iko kwa mujibu wa sheria. Sheria ya Hati Miliki na Hati Shiriki, Sheria Na.7 ya mwaka 1999 na marekebisho yake ya mwaka 2003. Moja ya vitu inachosema ni kwamba maeneo yote ambapo yanatumia kazi za sanaa, yanatakiwa kulipa mirabaha. Maeneo ambayo kusema kweli yanatumia kazi za sanaa yako mengi, hoteli, buses, hair saloons na barbershops, restaurant, cafe, bars and social clubs, radio na televisions, shopping malls, medium size shops, night clubs, telecommunication companies na music festival. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa safari hii COSOTA wamegawa Shilingi milioni 321 na mirabaha ilikuwa haijagaiwa toka mwaka 2018. Kwa hiyo, hiyo milioni 321 hii ni ya miaka minne, ndio tafsiri yangu. Nikajaribu kuchukua effort kupiga simu kwa watu wetu TRA watusaidie kujua sehemu ambazo COSOTA wanatakiwa kuchukua mirabaha. Kusema ukweli tumeshindwa ku-capture kila kitu, lakini beverage servicing activities ziko 3,009 nchi hii. Passenger land and transport ziko 66,738, restaurants mobile food activities ziko 30,957, urban and sub-urban passenger land transport ziko 1,347. Jumla ni biashara ambazo zimesajiliwa TRA ambazo zinatakiwa kulipa mirabaha 102,051. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hii milioni 321 ambayo tunasema ni mirabaha ya miaka minne kwa biashara 102,051 inamaanisha biashara hizi zote zimelipa shilingi elfu tatu tatu kwa miaka minne kutumia kazi za sanaa. Yaani nafikiri hii ni sahani ya chipsi mayai kwa Edo pale. Watu wamelipia kupiga muziki, kutumia kazi za sanaa kwa miaka minne bila kipingamizi, anapiga mtu yoyote, saa yoyote 24 hours a day kwa siku 365. Sasa unaweza kuona jinsi ambavyo COSOTA haijaanza kufanya kazi yake. Ninachojaribu kufanya, ni kulinganisha ile scope ambayo COSOTA wanakusanya na ile potential ambayo tunayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, biashara hizi kama ambavyo zingelipa Sh.30,000 tu ambayo ni Sh.2,500 tu kwa mwezi ambayo hamna mtu yoyote anayeweza kukataa kati ya hawa kulipa, bado tungekuwa na mara 10 ya kiwango ambacho COSOTA wamekikusanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kusema ukweli sheria inasema waziwazi kwenye marekebisho ya mwaka 2003 na nikisoma kipengele cha tatu inasema: “No person shall hold a public performance or a broadcasting of a work in which a copyright subsists except under a license issued by the society.” By the society wanamaanisha COSOTA.

Mheshimiwa Spika, sasa swali la kwanza kuwauliza ni kama COSOTA wametoa leseni za sehemu hizi 102,000 ambazo ni wazi zinatumia kazi za mziki. Kama hawajatoa kwa miaka 23 toka sheria hii ilipotengenezwa, ni wazi COSOTA hawajaanza kufanya kazi yao. Kiwango tunachokusanya hakijafika hata asilimia tano ya hasa ambacho tulitakiwa tuwe tunakikusanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sheria iko wazi haijamumunya maneno, you pay to play as you want na hicho ndio ambacho kinatakiwa kufanyika. Kwa hiyo, kazi za muziki, kazi za sanaa zinatumika na hakuna anayelipa. Maeneo haya yote ya biashara ninayokwambia, OSHA wanakusanya chao, NEMC wanakusanya chao, TRA wanakusanya chao. Watu pekee ambao hawalipwi kutokana na shughuli hizi za kibiashara zinazofanyika ni wasanii wa nchi hii. Sasa unaweza kuona na sheria iko wazi, yaani siyo kitu ambacho tunaenda kuifanya sheria tukae tena tutengeneze sheria upya ama nini. Sheria iko wazi inasema, kwa hiyo, kuna mtu tu hafanyi kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hoja yangu ni kwamba, kwa mujibu wa maelekezo ya sheria, kiwango tunachokusanya ni kidogo sana na tumejaribu kuongea na COSOTA miaka nenda, miaka rudi kujaribu kuwaelekeza hili kuhusiana na uwezekano wa ku-outsource shughuli hii ili watu wengine waifanye. Hata kama ikibidi ku-privatize moja kwa moja, halafu COSOTA ikawa inalipwa kutokana na makusanyo kwa kiwango wanachokiweka, ingekuwa sawa. Serikali inapoteza pesa nyingi na wasanii wanapoteza pesa nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kama Serikali haitaki kukusanya hela yake, wasanii wanataka kukusanya hela zao. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Waziri, akae chini upya na COSOTA, waseme maeneo yote ambayo yanatakiwa kukusanywa mirabaha, wana mpango nayo gani na kama kwa miaka 23 wameshindwa kufanya shughuli hii, wanatuambia nini sababu ambayo itafanya shughuli hii isiwe outsourced na maeneo haya yakaanza kukusanywa na watu binafsi wengine kwa sababu wao shughuli hii imewashinda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, hili ndiyo eneo ambalo lina pesa nyingi kwenye Wizara yake kuliko maeneo yote. Tulijaribu kupiga hesabu maeneo yote kwa ka-research kadogo ambacho siyo rasmi sana, tulipata tunaweza kukusanya takribani bilioni 56 kwa mwaka. Bilioni 56 kwa mwaka Waziri anajua ni kodi ya kiasi gani ya Serikali, anafahamu ni hela ngapi kwa wasanii. Uzuri wa royalties ni kwamba hata wasanii kama wameacha kufanya muziki, familia zao zinaweza kufaidika hata kama wao hawapo duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii familia ya Mzee wangu Waziri Ally, familia ya Remmy Ongala, Marijani Rajabu zingekuwa zinalipwa kwa pesa hizi, lakini baadae unapata malalamiko kuna mtu royalties amepata Sh.50,000 kwa sababu tu COSOTA wameshindwa kufanya kazi yao. Hii siyo ramli, hizi ni hesabu na hiki kitu kiko wazi kabisa kwa mujibu wa sheria, hatuhitaji kupita kokote ili kukifanya kitokee. Hilo ni moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tarehe 31 mwezi uliopita, Mheshimiwa Rais alihudhuria concert ya hip hop pale Dar es Salaam na moja ya vitu alivyosema ni kuhusiana na umuhimu wa kuanza kukusanya blank tape levy na aliisema hii kwa nia njema kabisa. Blank tape levy ni ile tozo ambayo inatakiwa kuchajiwa kwenye vifaa vyote ambavyo vinaweza kubeba kazi za sanaa kama flash disks, memory cards na CDs wakati vinaingia tu. Tukichukulia kwamba asilimia 90 ya vifaa hivi vinakwenda kutumia kuhamisha shughuli za sanaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, hatuna teknolojia, hatuna human resources ya kutosha ya kuanza kupita sehemu moja moja kuhakikisha kila ambaye anahamisha muziki, anahamisha shughuli ya sanaa tunamchaji. Kwa hiyo, namna pekee ambayo tunaweza kufanya ni wakati vifaa vile vinapoingizwa kwenye nchi hii tunaongeza katozo kidogo ili wasanii wa nchi hii nao wakafaidika kwa kazi zile zinazokwenda kuhamishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba dakika moja nimalize.

SPIKA: Sekunde 30.

MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa hivyo, Mheshimiwa Rais ameliweka wazi hili. Pamoja na ile kazi ya COSOTA ambayo tunamwomba Mheshimiwa Waziri akahakikishe inafanyika ya makusanyo, lakini kwenye blank tape levy kwa sababu maelekezo ya Rais ni maagizo tayari, imeshakuwa sheria. Nategemea hili kuliona linaaanza as soon as mwezi Julai na ndugu yangu Mheshimiwa Mchengwerwa asipolifanya hili tunarudi kumsemea kwa Mheshimiwa Rais kwamba amepuuza maelekezo yake. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu mwingine nitauweka kwenye maandishi kwa sababu nina mengi ya kusema na muda haunitoshi. Nakushukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii na mimi niweze kuchangia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha ya Mapendekezo ya Serikali kuhusu Makadirio ya Mapato na Matumizi ya mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali cha kusimama mbele ya Bunge lako hili Tukufu na nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha na timu yake nzima kwa hotuba nzuri iliyobeba dira, dhamira, maono na mwelekeo na huruma ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa Watanzania, inatia moyo na tunachoweza kufanya ni kuendelea kumuombea Mheshimiwa Rais Mungu amuweke kwasababu kuna mahali tunapoelekea na kuna mwanga mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri nimpongeze kwa kuyatafsiri yote haya malengo ya Mheshimiwa Rais kwa matendo katika kipindi cha mwaka mmoja huu, kusema kweli ile kauli ya unaupiga mwingi na wewe inakuhusu moja kwa moja. Mara nyingi mimi nasema Kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu unakuwa huna baya isipokuwa inapokuja mambo yako ya ‘Utopolo’ tu lakini huko kwingine upo safi kabisa. Hongera! (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ni nzuri hata hivyo kuna maeneo kadhaa ambayo mimi nahisi naweza kuweka senti hamsini zangu. Kwanza kabisa ni katika ukurasa wa 69 ambapo Mheshimiwa Waziri anapendekeza kuhusiana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri zetu kwamba tuikate kwa asilimia 50. Asilimia Tano iende kwenye kutengeneza miundombinu ya masoko ya Wamachinga. Kwanza, mimi niseme msingi wa sera ile, msingi wa ule mwongozo ilikuwa ni kuwawezesha wananchi kiuchumi, kuwakwamua kwenye umaskini, kuwaunganisha na Serikali yao moja kwa moja kwa kuwahakikishia kwamba hali zao za kiuchumi binafsi zinaimarika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo ile imekuwa inafanya shughuli nzuri ina changamoto za hapa na pale lakini naamini suluhisho la changamoto zile si kuikata kwa asilimia 50 na kuirudisha kwenye Halmashauri, hili jukumu la kujenga miundombinu ya masoko ya wamachinga ni jukumu la Serikali, Serikali isilikimbie inabidi ilifanye kwa namna yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuchukua asilimia Tano kati ya asilimia 10 zile na kuirudisha Serikalini ni kuwapora akina Mama, Vijana na Watu Wenye Ulemavu fedha ambazo tulikuwa tumeshawaahidi na zinawasaidia kwelikweli. Mimi kwa mfano, Muheza pale mapato yetu ya ndani ya Halmashauri ni takribani shilingi bilioni 2.1 kwa hiyo, kiutaratibu tunatakiwa kutoa shilingi milioni 210 kila mwaka kwa ajili ya kuyawezesha makundi haya. Sasa pamoja na mzunguko na marejesho tunakaribia kutoa shilingi milioni 500. Makundi ambayo yananifuata mimi binafsi, makundi ambayo yanamfuata Mkurugenzi, yanamfuata Mkuu wa Wilaya kumuomba awasaidie kupata mikopo hii kwa ajili ya kujisaidia kwenye shughuli zao za kiuchumi ni mengi mno hata hiyo hela yote ambayo tunayo haiwezi kufika nusu ya haja tuliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, kusema ukweli Mheshimiwa Waziri wa Fedha ninakuomba hii asilimia Tano tusiiguse huku, tusipite njia hii haitoki na Serikali isikwepe kama kuna lolote ambalo lingeweza kufanyika kwanza, ningehisi kwamba ungetoka mwongozo mwingine wa hii fedha iongezwe kwa sababu inawasaidia moja kwa moja inamsemea vizuri Mheshimiwa Rais, inaisema vizuri Serikali, inasema vizuri Wabunge, Madiwani na Halmashauri zetu. Kwa hiyo, badala ya asilimia 10 pengine ingeenda kuwa asilimia 15. Serikali ifanye jukumu lake la kujenga miundombinu kwenye masoko ya wamachinga kwa fedha ambazo yenyewe itazipata wapi hatujui, lakini ihakikishe kwamba fedha hii haiguswi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama kuna uwekezano tena Serikali itoe ruzuku kwa Halmashauri zetu ambazo zinaingiza mapato kwa kiwango ambacho kimekusudiwa, kimekadiriwa basi zipewe ruzuku kwa ajili ya kufanya miundombinu hii ya wamachinga na siyo kutoa kwenye fedha hizi ambazo tulishaahidi makundi haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, pendekezo hili Mheshimiwa Waziri mimi niseme kwamba sikubaliani nalo na ninapendekeza tuachane nalo moja kwa moja lisirudi wakati wa majumuisho yako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri nimemsikia pia akisema kwamba Pato la Wastani la Mtanzania kwa sasa ni Shilingi Milioni 2.8 na hii inamaanisha ni kama 233,000 kwa mwezi, hatupo vibaya kusema kweli dola elfu moja mia moja na kitu, lakini tunaweza kuimarisha kwa kulainisha zaidi mazingira wezeshi yanayomfanya Mtanzania wa kawaida kujiongezea kipato chake, kwenye hili bado hatujafanya vizuri sana kuna maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mfano; kule kwetu Muheza kuna Tarafa inaitwa Amani katika vijiji vya Fanusi, Magoda, Kisiwani na Kavaa kule Amani tulikuwa tunafanya miradi ya ufugaji wa vipepeo kabla ya mwaka 2016, halafu likatoka zuio 2016 la kuzuia miradi ile isifanyike, najua ukisema miradi ya vipepeo watu wanajua kama mnachukua vichujio vile mnaenda kukamata kwenye maua haipo hivyo ni miradi mikubwa ambayo ilikuwa inawasaidia sana wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kaka yangu Mheshimiwa January Makamba alipokuwa Waziri wa Mazingira alishatembelea miradi ile, somo yangu Mheshimiwa Hamisi Kigwangalla alipokuwa Waziri wa Maliasili alishajionea na juzi Mzee wangu Mheshimiwa Jerry Silaa akiongoza Kamati yake ya Uwekezaji walipita pia kule, na wote wamekuja na positive feedback kwamba miradi ile kwanza haina athari za kimazingira, vipato vya wananchi vinaongezeka, shughuli za kijamii kama maji na madarasa yamejengwa na miradi ile pia vilevile na inatusaidia kulinda misitu kwa sababu wananchi wanapata shughuli nyingine za kiuchumi za kufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2016 mpaka sasa hivi ni miaka takribani Sita, pengine mwongozo ulitoka haraka haraka kwa sababu ulikuwa unataka kulinda swala, pundamilia na twiga wetu wasitoroshwe na ukawa haukupata muda wa kutofautisha kati ya pundamilia na vipepeo, lakini mimi ninachosema ni kwamba imechukua miaka sita sasa kwamba wataalam wetu wameshindwa kufanya kazi yao ya kuweza kutofautisha kati ya wanyama ambao wanatakiwa kulindwa wasitoroshwe kwenye nchi hii na hawa Vipepeo wanaoishi kwa siku 14. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Mzigua mmoja hapa nyuma yangu anasema kwamba tunakaa kwa miaka Sita tunabishania kuhusiana na wadudu ambao wanaishi kwa siku 14. Miradi ile ilikuwa inawasaidia wananchi wa maeneo husika wanapata mpaka kiasi cha shilingi milioni moja kwa mwezi, sasa katika nchi ambayo pato la Mtanzania ni shilingi milioni 2.8 kwa mwaka mtu mmoja anapata milioni 12 kwa mwaka na bado tunamzuia, tunamfanyia roho mbaya tu ili mradi asifanye biashara hii kwa sababu ya uvivu tu wakushindwa kutenganisha kati ya swala na vipepeo hii siyo sawa! Hili eneo hatujafanya vizuri Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati mwingine unaona kama kuna masihara yanafanyika mpaka juzi Kamati ya Bunge ya Uwekezaji inayoongozwa na Mzee wangu Jerry Silaa ilitoa maagizo ya kwamba suala hili lifanyiwe kazi na miradi ile ifunguliwe, vipepeo waendelee kusafirishwa lakini mpaka sasa hivi hamna hata mtu mmoja aliyetingisha hata unywele! Sasa hii maana yake ni kama ni dharau kwa Bunge vilevile kwasababu kutenganisha kati ya vipepeo na Swala kusema kweli ….

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa taarifa mchangiaji kwamba siyo tu miradi ya kufuga vipepeo ina faida na tija kubwa kwenye maisha ya wafugaji ambao ni wananchi wa vijiji alivyovitaja, bali pia miradi hiyo inafaida kubwa sana kiuhifadhi na kimazingira. Pia miradi ya vipepeo haihusiani kabisa na sababu zilizopelekea kuzuiliwa kwa wanyama kusafirishwa nje ya nchi ambazo nyingi zilikuwa ni kelele na vilio vya wananchi baada ya kusikia kwamba Twiga na Pundamilia wanasafirishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa apokee taarifa hiyo. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwinjuma taarifa hiyo.

MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, Kigwangalla will always come to my rescue, ahsante sana naipokea taarifa hii kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilichokuwa najaribu kusema ni kwamba hata watoto wa Darasa la Nne wangeweza kutofautisha kati ya Swala, Pundamilia na Vipepeo bila wasiwasi wowote, sasa sisi tuna watalaam ambao kabisa wamesomeshwa na hela za kodi za wananchi wa nchi hii, wameshindwa kufanya shughuli hii wakaandika madokezo na kupendekeza kwamba miradi ile iruhusiwe kwa miaka Sita, haya ni masihara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Bunge lako Tukufu miongoni mwa mambo ambayo tunatakiwa kuyafanya ni kuhakikisha tunawalegezea mazingira wananchi ya kujiingizia vipato vyao binafsi, hili likiwa mojawapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi naomba kuunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi nisema mawili, matatu kwenye hoja iliyopo mezani. Nisije nikafika mwisho muda ukanibana ama nikajisahau niseme kwanza naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nichukue fursa hii kuwapongeza watendaji wetu kwenye Wizara ya Maji; Ndugu yangu Waziri Jumaa Hamidu Aweso na Ma- engineer wake, dada Naibu Waziri Maryprisca Mahundi, Katibu Mkuu Eng. Sanga (Mzee wa Mnadara), dada yangu Nadhifa Kemikimba, Mkurugenzi wa Tanga (UWASA), Eng. Upendo Rugongo, Meneja wa Tanga (UWASA – MUHEZA) Eng. Nyambuka na Meneja wa RUWASA - Muheza Eng. Cleophate Maharangata, kusema kweli mnatutendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua matatizo ya maji nchi hii ni makubwa na pengine ndio tatizo kubwa kuliko yote hasa kwa Wabunge wanaotoka Majimbo ya vijijini kama mimi. Mimi natoka Wilaya ya Muheza ambapo kuna changamoto kwenye kila kitu; elimu, afya, barabara na kadhalika. Akitokea mwananchi mwenzangu yeyote wa Muheza hapa ukamuuliza tatizo la kwanza la Muheza ni nini, naamini atakutajia maji. Akina mama wa Muheza kuna mahali nilifika wakaniambia Mheshimiwa ukiweza kuhakikisha tunaweza kuchota maji kwenye mabomba ikifika mwaka 2025 lete shati lako lisimame hapa wewe ukapumzike na tutalipigia kura. Kwa hiyo, ndugu yangu Mheshimiwa Jumaa na wasaidizi wako nafikiri mnajua kama mpaka Ubunge wangu mmeushika kwenye mikono yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kauli ya Kiswahili wanasema kwamba asiyeshukuru kwa kidogo hawezi kushukuru kwa kikubwa. Pamoja na tatizo kubwa la maji Wilaya ya Muheza kusema kweli watendaji hawa wanatusikiliza na wanapanga kuyatatua matatizo haya kwa moyo wao wote. Unaona hata maana ambapo hawawezi kulifanya kwa asilimia 100 lakini ndimi zao zinakuwa laini na unaona unawahangaisha katika kutafuta suluhisho ya matatizo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Muheza tuna Mradi wa Kilongo ambao umetengewa kiasi cha shilingi milioni 778, tuna mradi wa Kwemdimu una shilingi milioni 649; mradi wa Kwemnyefu, Mdogo, Pongwe una shilingi bilioni 6.1 na ule mradi mkubwa kabisa ambao tunaamini unakwenda sasa kutatua tatizo zima la maji Wilaya ya Muheza wa miji 28 ambao sisi tumetengewa bilioni 40. Tunafahamu mioyo yenu ni mizuri na tunafahamu tatizo liko wapi, ni fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, niliombe Bunge lako Tukufu kama kuna kitu ambacho tunatakiwa kufanya kama Wabunge ni kuhakikisha Wizara ya Maji inapewa fedha zote ambazo tumekubaliana hapa. Kwa miaka 10 mfululizo ikiwemo bajeti yao ya mwaka huu wa fedha unaokwisha wamekuwa hawapewa hata asilimia 60 ya fedha ambazo wanaziomba, kKwa mfano, bajeti ya mwaka huu wa fedha wamepata asilimia 54 tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ufahamu wangu, tunapoamua kwamba tunatenga fedha kwa ajli ya kwenda kutekeleza miradi ya maji tunakuwa tumeamua kwamba kuna asilimia fulani ya matatizo ya maji ya nchi hii tunakwenda kuyatatua siyo yote. Kwa hiyo, kama tumeamua kwamba tunatenga fedha na zinakwenda kutatua asilimia 20 ya matatizo ya maji katika nchi hii tunapowapa asilimia 50 maana yake tunakwenda kutatua asilimia 50 ya asilimia 20 ambayo tulipanga, tunazidi kujirudisha nyuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge tumeingia kwenye Bunge hili hasa Wabunge wa Vijijini kama mimi tukijua kwamba tatizo kubwa ni maji na kama hatutaikomalia Serikali iwe inatoa fedha zote ambazo zimeombwa na Wizara ya Maji ambazo zimepangwa kutekeleza miradi hii tutatoka hapa matatizo yale hayajakwisha. Sidhani kama hiyo ndiyo namna tunataka kukumbukwa, tumeingia tumekuta tatizo la maji, tutoke tuliache tatizo la maji. Naomba tulikomalie au kwa lugha ya mtaani tunasema kidedea Wabunge wote na ukiwemo Naibu Spika kuhakikisha kwamba Wizara ya Maji inapata sehemu kubwa ya fedha ilizoomba ili miradi hii ya maji iweze kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nondo zilikuwa nyingi lakini nashukuru, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Spika, mchango wangu ni kuhusu biashara ya viumbe pori hai, specifically inayohusisha wadudu wadogo yaani vipepeo, mijusi, jongoo, ndege na vinavyofanana na hivyo ifunguliwe.

Mheshimiwa Spika, biashara hii ilikuwa inafanyika kwa miaka kadhaa kabla ya kupigwa marufuku na kusitishwa tarehe 17 Machi, 2016 kwa agizo la Serikali. Watanzania waliokuwa wanashiriki biashara hii wameingia hasara kubwa na kurudishwa nyuma sana kiuchumi, na mfano halisi ni wananchi na wafanyabiashara waliokuwa wanashiriki biashara ya vipepeo jimboni kwetu Muheza, Mkoani Tanga.

Mheshimiwa Spika, ninazo hoja kadhaa za kwa nini Serikali inatakiwa kuirudisha biashara hii. Kwanza, miradi ya kufuga na kusafirisha vipepeo kibiashara haina madhara yoyote ya kimazingira, haipunguzi idadi ya vipepeo na kinyume chake inawaongeza. Kwa kawaida muda wa kuishi wa vipepeo ni majuma mawili na vipepeo hutaga mpaka mayai 400 na kwa njia zao za kawaida hutotoa mawili ama matatu tu, ila wakitotoleshwa kwa njia za kibinadamu zilizokuwa zikifanyika mayai yote hutoa vipepeo.

Pili, inasaidia sana kwenye uchumi wa wananchi mmoja mmoja. Wananchi wa vijiji vyetu walikuwa wana uwezo wa kupata mpaka shilingi milioni moja kwa mwezi ambazo ni fedha nyingi mno kwa mazingira yetu. Kwa kusitisha biashara ile, wananchi wetu wamerudi kwenye ufukara wa kabla haijaanza kufanyika na kwa vile wanaishi pembeni ya hifadhi tunahatarisha mno kwao kuvutiwa na kufanya shughuli za kihalifu kwa misitu yetu. Kwa hiyo, biashara ile ilikuwa inasaidia ulinzi pia kwa misitu yetu.

Mheshimiwa Spika, halikadhalika biashara ile ilisaidia miradi ya kijamii yenye faida kubwa. Tuliweza kujenga madarasa kadhaa, miradi ya maji ya bomba na fedha taslimu zilizolipwa kwa Serikali za Vijiji. Yote hayo yamepotea kwa kusitishwa kwa biashara ile. Kwa kifupi ni kuwa zuio lile lilikosa macho kama lilivyokosa mashiko. Halina faida yoyote iwe ya kimazingira ama kiuchumi na ni wakati sasa wa Serikali kuliondoa. Serikali kama ilivyo kwa wananchi wa maeneno husika Wilayani Muheza, inapoteza fedha nyingi kwa kuendelea kuizuia. Serikali kuruhusu tena usafirishwaji wa vipepeo nje ya nchi kuna mantiki kubwa kwa ustawi wa wananchi wale na pato la Taifa pia kiujumla.

Kwa kuongezea, Kamati ya Bunge ya Uwekezaji chini ya Mwenyekiti wake Mheshimiwa Jerry Silaa ambayo ilitembelea maeneo ya Tarafa ya Amani, Wilayani Muheza kunakofanyika ufugaji wa vipepeo iliishauri Serikali kuondoa zuio na kuifungulia biashara ile. Faida ni nyingi na hakuna hasara yoyote kwa kufanya hivyo.

Niiombe tena Serikali kupitia Bunge lako tukufu, iondoe zuio lile ili kumuunga mkono Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwanza kwenye nia yake ya kuwarahisishia maisha wananchi wa Tanzania, lakini pia kuendelea kuitangaza Tanzania kama alivyofanya kwenye filamu ya Royal Tour kwani vipepeo hawa wanakwenda kutumika kwenye maonesho ya vipepeo nje ya nchi na sifa za uzuri wao zinaipamba nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona na kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara hii ya Maji na nipate kuleta salamu za wananchi wenzangu wa Muheza kwa Serikali yao. Nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali na uwezo wa kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu leo na niwashukuru sana wananchi wa Muheza kwa kuendelea kunipa ushirikiano, imani na kunitia moyo kijana wao niendelee kuwapambania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kututeulia na kuwaacha vijana wake aliowatuma kwenye Wizara hii ya Maji waendelee kufanya kazi aliyowatuma ya Watanzania.

Nitumie fursa hii kumpongeza nugu yangu, kaka yangu, rafiki yangu Mheshimiwa Al-habib Jumaa Hamidu Aweso, kidume kwelikweli kwa kazi kubwa anayoifanya. Pia nimpongeze Mheshimiwa Maryprisca Mahundi, Engineer, Naibu Waziri na Engineer Antony Sanga na Nadhifa Kemikimba na wasaidizi wao wote kwenye Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nina mambo mawili; jambo la kwanza ni kuhusiana na bilioni 6.05 ambazo Wilaya ya Muheza imezipata kwa miezi 18 hii ambayo mimi ni Mwakilishi wao. Bilioni 6.05 ni fedha nyingi na siwezi ku-capture zote kwa mnyumbulisho wake jinsi zinavyoenda kutumika, lakini nina matukio mawili - matatu ambayo nataka kuyataja.

Mheshimiwa Spika, kwanza tulipokea Milioni 300 kwa ajili ya kuimarisha miundombinu kwenye Kata ya Tanganyika, Majengo ya Ndani na Masuguru ambazo zilienda kubadilisha mabomba kwa sababu, tulikuwa na mabomba ya chuma yaliyooza ambayo yalikuwa hayapitishi kabisa maji na hata yanapopitisha maji mengi yalikuwa yanamwagika njiani, hela hii ilienda kufanya kazi inayostahili.

Mheshimiwa Spika, pia tumepata Milioni 150 kuimarisha miundombinu kutoka NHC kwenda Mdote, Milioni 700 kwa mradi mpya wa Kata ya Kwemkabala ambayo ilikuwa haijawahi kuwa na mradi wowote. Tunatarajia kupokea milioni 370 kwa mradi wa Muheza Estate wakati wowote na tumepokea bilioni moja kwa ajili ya mradi wa majitaka na Mkandarasi yupo kazini. Miongoni mwa mambo anayofanya ni kutujengea sehemu ya kuhifadhia majitaka, pia kutununulia gari la majitaka na miradi mingine midogomidogo kama kuweka matundu nane ya vyoo kwenye Shule ya Sekondari ya Bonde, nane ya vyoo kwenye Shule ya Msingi niliyosoma mimi ya Mdote na matundu Sita kwenye Soko jipya la Michungwani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile wiki iliyopita tu tumepokea milioni 408 kwa ajili ya miundombinu, Mabanda ya Papa kwenda Ngwaru. Milioni 91 Makete kwenda Masuguru, milioni 38 Swafaa kwenda KKKT, milioni 33 Majengo Ndani, maeneo ya Elephant milioni 40.7, Tanganyika Milioni 119, Majengo ya Nje ambapo panahitaji milioni 220 kwa sasa pamepata milioni 70 na ninategemea mtaenda kugonga mlango kwa mzee wa mnara, Engineer Antony Sanga na ataniongezea fedha hizi wakati wowote mradi huu uende kukamilika na hiyo ni kwa Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kwa RUWASA tumepokea fedha PDR Milioni 735.3, Mfuko wa Maji Bilioni Moja na Mradi wa UVIKO Milioni 506 ambao umeenda kutekeleza mradi wa Mizembwe ambao kwa sasa umefikia asilimia 86 na tarehe 20 wananchi wataanza kupata maji. Wiki ijayo tunasaini pia mradi wa Mbomole Sakario ambao unagharimu milioni 664, Mradi wa Kwatango Milioni 591 na DDCA wanatuchimbia visima karibu 20 kwenye Kata za Kilulu, Mtimbilo, Mkuzi, Tingeni, Kwebada, Kwakifua, Kwafungo na Makole ambao wanaanza hivi karibuni. Kwemdimwa wameshakamilika na unatoa maji na Kilongo umefika asilimia 83 na mwezi ujao Vijiji Sita vitaanza kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimetaja yote haya siyo kwa sababu na ninajua nilikuwa na uchache wa muda kwa sababu sitaki kuwekwa kwenye kundi lile analolisema Mheshimiwa Waziri la mioyo isiyo na shukrani ambayo inafifisha yaliyo mema. Mimi nimeyasema haya ili Mheshimiwa Waziri ajue kwamba tunamshukuru, lakini tuna mapendekezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Shilingi Bilioni 6.05 ni fedha nyingi. Ukiniuliza kama zimefika, zimefika. Ukiniuliza kama hali ya upatikanaji wa maji Wilayani Muheza imeimarika, nitakwambia imeimarika kutoka asilimia 50 kipindi cha masika mpaka asilimia 18 wakati wa kiangazi ilipokuwa mwaka 2020 mpaka sasa asilimia 65 kipindi cha masika mpaka asilimia 50 kipindi cha kiangazi kwa hiyo, tumepiga hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ukiniuliza kama nafikiri Bilioni Sita zimefanya kazi niliyokuwa naitarajia kichwani kwangu, nitakujibu hapana. Ningetegemea Bilioni Sita zitengeneze siyo tu kwa kuonekana kidogo tofauti ya ilivyokuwa 2020 na 2022, lakini zifanye upatikanaji wa maji Wilayani Muheza angalao ufike kile kiwango cha Kitaifa cha asilimia 74. Kwa hivyo, naamini Mheshimiwa Waziri atanisikia nikiomba kutoa mapendekezo ya kwamba, fedha hizi zinapopelekwa kwenye Wilaya basi ziangaliwe, zikaguliwe sawasawa ili kuhakikisha kazi zilizopangwa kufanyiwa zinafanyiwa kweli na hatuwi na miradi chefuchefu tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ninalotaka kulisema ni kuhusiana na mradi wa Miji 28. Kusema kweli, sijawahi kuongea na Mheshimiwa Waziri au Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji na nikamaliza maongezi yangu, hata kama yalikuwa yanahusu kitu kingine nisiulizie mradi huu. Mradi huu uliwapa matumaini mengi akinamama wa Wilaya ya Muheza na Miji mingine 27 ambayo inakwenda kufaidikanao na umetumia muda mrefu sana, una miaka Nane sasa haujatekelezeka.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili nililotaka kulisema ni kuhusiana na mradi wa miji 28 kusema kweli sijawahi kuongea na Mheshimiwa Waziri au Katibu Mkuu wa Wizara ya maji na nikamaliza maongezi yangu hata kama yalikuwa yanahusu kitu kingine nisiulizie mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi huu uliwapa matumaini mengi akinamama wa Wilaya ya Muheza na miji mingine 27 ambayo inakwenda kufaidika nayo na umetumia muda mrefu sana una miaka nane sasa haujatekelezeka. Lakini taarifa ambazo nimezipata mpaka mwisho ambazo ni za kutia moyo kusema ukweli naamini kwamba mradi huu sasa unakwenda kutekelezeka na haubaki tena kwenye makaratasi. Nafahamu hili la signing ceremony lipo juu ya viwango vyetu vya mishahara wote siyo sisi kama Wabunge na nyinyi kama Wizara. Lakini Mheshimiwa Rais ratiba yake siyo rafiki sana na ana mambo mengi tunaomba kila nafasi mnayoipata kama ambavyo sisi wengine tulikuwa wasumbufu kwenu mkumbushe Mheshimiwa Rais mmuombe na mumuulizie kuhusiana na mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, najua kama kuna wakati akinamama wa nchi hii wanaamini kwamba matatizo yao ya maji yanakwenda kuisha, ni wakati huu ambapo nchi hii ina Rais mwanamama. Kwa hivyo nitumie fursa hii kuomba tena mkumbushe, mmuombe na mmuulize kwa unyenyekevu mkubwa Mheshimiwa Rais kuhakikisha sherehe hii inafanyika haraka na mradi unakwenda kuanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kauli mbili suala la upatikanaji wa maji halifai tena kuwa suala la kisiasa linafaa kuwa suala la kibinadamu watu wetu wengi wanafikiri mradi huu uko kwenye makaratasi na tunawaletea siasa tu kwenye masuala ya utekelezaji wa mradi huu, kwa sababu umechukua muda mrefu. Naomba kama kuna uwezekano masuala ya upatikanaji wa maji kuanzia sasa yawe ni masuala ya kibinadamu na kama linaweza kutusaidia huko mbele kwenye siasa zetu basi lifanye hivyo. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Spika, najua umeshawasha mic nikushukuru naomba kuwasilisha naunga mkono hoja. (Makofi)