Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Venant Daud Protas (24 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais iliyotolewa mwezi Novemba, 2020 na mimi nikiwa kama Mbunge, nimesimama hapa kwenye Bunge hili tukufu kwa mara yangu ya kwanza, nianze kumshukuru kwanza Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema aliyetufikisha hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakishukuru Chama changu cha Mapinduzi ambacho kilinipigania mpaka nimeweza kuingia kwenye chombo hiki muhimu sana. Tatu, nawashukuru familia yangu, walikuwa nami bega kwa bega kupambana katika kuhakikisha mimi nasimama imara kwa maslahi ya Wanaigalula wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo aliitoa ni dira ya maendeleo kwa kipindi cha miaka mitano. Nisiende mbali, kwanza naiunga mkono kwa asilimia mia moja kwa sababu sisi wote wana-CCM tulisimama kote kule tukiinadi Ilani ya Chama cha Mapinduzi na hotuba yake yote imepitia ilani, ndiyo maana akaja na mpangokazi wa miaka mitano, nini Serikali ifanye. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa wasaidizi wake, wameanza kazi vizuri. Tangu ametangaza Baraza la Mawaziri, tumeanza kupishana huko majimboni, wanafanya kazi nzuri sana, tuendelee na mwendo huu huu. Mheshimiwa Rais ameaminika na wananchi wote na Watanzania wote wamemwamini, ndiyo maana wakampa kura zaidi ya asilimia 84, na sisi Wabunge tumeaminiwa na wananchi, wana imani kwa kipindi cha miaka mitano wataona mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichangie sehemu chake, kutokana na muda, sisi tunaotoka majimbo ya vijijini, katika Halmashauri yetu ya Wilaya yetu ya Uyui, changamoto kubwa ni barabara, ndiyo kero ya Waheshimiwa Wabunge wote walioko humu ndani, kila utakapoenda, shida ni barabara. Katika mtandao huu wa barabara, kuna baadhi tukiwaachia TARURA hawawezi kutekeleza kwa kipindi cha miaka mitano. Kuna barabara gharama yake na bajeti inayokuja kwenye Halmashauri ya TARURA, ukiipa kwa kipindi cha miaka mitano ika-deal na barabara moja, haiwezi kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, kuna barabara yenye urefu wa kilometa 89 ya kutoka Miswaki – Roya kwenda Maguliati mpaka Iyumbu, Mkoa wa Singida. Barabara hii ina madaraja 16 madogo madogo na daraja moja kubwa lenye mita 120. Hii barabara kwa takwimu ya mkandarasi ni zaidi ya shilingi bilioni sita. Halmashauri yetu inapokea shilingi bilioni 1.3 kwa mwaka. Kwa hiyo, ukisema uelekeze nguvu kule, haiwezi ikakidhi kwa kipindi cha miaka sita, barabara nyingi zote zitakuwa zimesimama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niungane na Waheshimiwa Wabunge wengine kupiga kelele TARURA iongezewe bajeti ili tuweze kukwamua kero za wananchi wetu, wapate barabara. Kwa sababu na kule kuna wapiga kura, tena wanajitokezaga sana kipindi cha kupiga kura. Naomba sana Serikali itusaidie kwenye hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nirudi kwenye suala lingine. Sisi Wanasiasa na viongozi mbalimbali tumekuwa tukipita kwenye majimbo tukiwahimiza wananchi wetu wachangie baadhi ya maendeleo, lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, muda!

SPIKA: Eeeh! (Kicheko)

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja hotuba ya Mheshimiwa Rais, ahsante sana. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa inayoendelea kufanya kwa kuhakikisha ulinzi na usalama unaendelea kuimarika katika pande zote za nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, polisi wanafanya kazi kubwa sana ila idadi ya polisi ni wachache, naiomba Serikali kuendelea kuajiri askari ili kuendelea kuimarisha ulinzi katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Igalula lina changamoto kubwa ya vituo vya polisi, kwa kutambua hilo wananchi wameanzisha ujenzi wa vituo vya polisi katika Kata za Tura na Goweko; naiomba sana Serikali kutupatia pesa ili tuweze kukamilisha ujenzi wa vituo vya polisi vya Tura na Goweko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na polisi kufanya kazi kubwa sana ila kumekuwepo na kutokulipwa kwa stahiki zao ambazo zipo kwa mujibu wa sheria, kwa mfano pesa ya pango yaani kodi za nyumba kila mwezi. Polisi wamekuwa hawalipwi pesa hizi kwa muda sana, naiomba Serikali itusaidie kuwalipa ili kupunguza rushwa kwa sababu ya maisha magumu ya polisi. Polisi wamekuwa wakidai malimbikizo mengi sana, niiombe Serikali iwalipe polisi ili waweze kuwa na moyo kwa kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na changamoto kubwa sana kwenye upatikanaji wa Vitambulisho vya Taifa, wananchi wanapata changamoto kubwa sana, kwanza ofisi za NIDA ipo moja kila Mkoa, sasa ipo moja tu wananchi kutoka Kata za Mmale, Loya na Tura wanasafiri umbali zaidi ya kilometa 180 - 200 kufuata vitambulisho mkoani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Serikali naomba sana zoezi la vitambulisho warudie tena kuandikisha kwenye kata zetu ili wananchi wengi wapate vitambulisho kuliko usumbufu wanaoupata wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na malalamiko mengi ya OCD wangu wa Wilaya ya Uyui, unyanyasaji wa kituo cha polisi wamekuwa wanawabambikia kesi sana hasa waganga wa kienyeji. Naomba sana Serikali kuchunguza juu ya mwenendo wa OCD Uyui amefikia anakamata watu anawaweka ndani mpaka siku kumi bila hata kuwafikisha mahakamani mpaka Diwani na Mtendaji wa Kata ya Miswaki amewakanata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba msaada wako kufanya uchunguzi wa kina juu ya polisi Uyui.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili nichangie Wizara hii muhimu kwa uchumi wa Taifa letu, Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuipongeza Serikali angalau ilitoa ahadi ya tarehe mosi leo mwezi wa Sita wananchi wetu watapata ahueni ya kupungua kwa bei ya mafuta, sasa Serikali imechukua gape lile, wananchi wameona kidogo imepungua ingawa haijapungua sana, lakini angalau Serikali imeonesha njia na nina imani tunapoenda tutaendelea kupunguza zaidi kupitia Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hapa nitachangia mambo machache sana kwa upole sana ili Mheshimiwa Waziri kwa sababu ni bajeti yake ya kwanza na ametuandikia hapa jarida limetupa vipaumbele na hivi vipaumbele nina imani kavitoa katika Ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi, naamini kama akivisimamia kama alivyoandika mwaka kesho hapa bajeti yake haitokuwa na maswali mengi lakini kama havitakwenda kama alivyoandika basi na yeye kidogo awe amejipanga mwakani atumie nguvu kuipitisha bajeti yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kwa kumpongeza wiki iliyopita alituletea watalaam wetu hapa wa wilaya na mikoa na wakandarasi wote. Tulipita kwenye mabanda kama mlivyokuwa mmeelekeza tuliwakuta mameneja wetu wa wilaya na mikoa na wakandarasi na nikushukuru kwa sababu kwa sisi wengine jimbo letu ni mbali sana na kufika Makao Makuu ya Wilaya, Meneja wangu Grace nilimkuta hapa na nikaongea nae na wakandarasi nikaongea nao, wakanipa ushikiriano mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo ambayo siku ile mlivyotuletea hapa nilijikuta tuna maswali mengi. Wakati tupo site hawajaja hapa tulikuwa tunajua kuna changamoto ya upandaji wa bei ya vifaa vya ujenzi, lakini hapa tena tukaja kukuta mkandarasi mwenyewe na aliyempa ajira yule yaani REA hawaelewani, lakini niliweza kusaidiwa na Mheshimiwa Naibu Waziri ndugu yangu Mheshimiwa Byabato, alimwita mkandarasi na REA wenyewe wakaitwa kuzibaini zile changamoto baina yao za kimkataba, lakini Mheshimiwa Naibu Waziri alitoa maelekezo pale wakakae kikao, alisema jioni wakae kikao, lakini mpaka leo kikao hakijafanyika na mgomo upo palepale, mkandarasi ameshindwa kuelewa kwa sababu REA anampa maelekezo ambayo yapo nje ya mkataba wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe hata ile niliyokuwa nawaambia wananchi tusubiri wanasema wana- bargain bei za vifaa kumbe nilikuwa nawadanganya kumbe ni tatizo la mkandarasi na REA hawajaelewana ndiyo maana kazi imesimama jimboni kwangu. Hata hivyo, nikumbushe mwaka jana 2021 Mheshimiwa Naibu Waziri alifika jimboni kwangu waliahidi Kijiji cha Izumba watawasha umeme baada ya mwezi mmoja, lakini sasa hivi mwaka mmoja na miezi miwili hawajawasha umeme. Nilivyokuja kufuatilia kwa mkandarasi, kuja kumhoji hicho, akaniahidi mpaka kufikia mwishoni mwa mwezi Julai, maeneo ya Songambele, Izumba yatakuwa yamewaka umeme, lakini kwa mgogoro huu kama tusipoutatua mapema mpaka muda huo umeme utakuwa haujawaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri kwa kuwa alituletea wataalam wenyewe, yale maswali yote yaliyoibuka, akae na wataalam wake, wakusanye maoni yote ya Wabunge ambayo tuliyaongea pale wakayafanyie kazi kuliko sasa, walituambia saa kumi watakaa kikao, leo tunaenda siku ya tano au ya sita hawajakaa kikao. Sasa ndiyo Waziri ajue ana watu gani ambao anafanya nao kazi kwa sababu yeye ameingia mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kampuni inaitwa JV POMY walimpa kazi ya kuunganisha umeme, amechukua hela za wananchi wangu, ameondoka LUKU hataki kuwaletea, wakimpigia simu sababu ni nyingi. Niombe kwa sababu zipo LUKU zaidi ya 120, tutoe kauli nini kilicho nyuma ya pazia juu ya mkandarasi huyu je, ni uzembe wake au kuna tatizo gani ambalo limemkumba? Kama kuna tatizo, basi wananchi wapewe taarifa kuliko sasa hela zao zimekaa kule halafu hawajui lini wataunganishiwa umeme. Nimwombe Mheshimiwa Waziri atusaidie hili hii Kampuni ya JV POMY ndio ilitusababishia hata hasara kwa ndugu yangu jirani yangu Mheshimiwa Kakunda, eneo la Makibo umeme umechelewa sana kwa sababu ya uzembe tu na ucheleweshaji mdogomdogo ulionao hii kampuni. Nimwombe Waziri aipitie vizuri, ikiwezekana wampunguzie kazi sehemu nyingine kwanza kumwezesha kumaliza kazi za mwanzo ili kuondoa kelele na lawama kwa Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka nichangie, nilishamlilia Mheshimiwa Waziri na nikamwambia hatujapinga maelekezo ya Serikali kupandisha gharama za umeme, tumemuunga mkono, lakini tunacholia maelekezo ambayo aliyoyaleta walisema vijiji vitaendelea kuwa Sh.27,000 lakini maeneo ya miji itakuwa Sh.320,000 na kwingineko, lakini kwangu kuna vijiji vimeingizwa kwenye Sh.320,000 havina sifa ya kuingizwa huko kikiwemo Kijiji cha Goweko, Kijiji cha Igalula, Kijiji cha Kigwa na Nsololo Tambukareli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atoe kauli moja, wananchi wana hamu ya kuunganishiwa umeme na wao kama wangewaletea wakati ule wangeunganisha mapema, tatizo Serikali yetu ilikuwa inaleta kidogo kidogo, sasa wakati Serikali imefungua kupeleka umeme kwenye vitongoji, leo wanawapandishia bei wanaenda kumuunganishia nani, lakini tunakumbuka bei haikuwa hiyo ilikuwa Sh.170,000 basi wangerudisha hata ile Sh.170,000 kuliko sasa hivi imepanda, ukinunua nguzo moja unalipa mpaka zaidi ya 1,700,000 mpaka 2,000,000, kwa Mtanzania gani na uchumi gani? Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri aweze kutusaidia jambo hilo ili tuweze kulitatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Igalula lina vijiji 46 havina umeme, lakini juzi Mheshimiwa Waziri alitoa takwimu tatizo ambalo saa hivi wanaenda kulitatua kusafirisha umeme kwa umbali mrefu, ninavyoona kuna umeme nautoa Igunga unakuja jimboni kwangu kwenye Kata ya Loya, umeme ule umekuwa na changamoto sana, unakuja mdogo, wananchi hawafanyi kazi, mashine moja ikiwaka mashine zingine zote haziwaki na wananchi hawapati huduma nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe katika utekelezaji wa miradi, tulikuwa tunaomba muweze kujenga Kituo cha Kupozea Umeme hasa katika Kata ya Kigwa, itatusaidia sana kwa sababu vile vijiji 46 kama umeme kweli tukiuchukulia katika Kata ya Kigwa kama walivyo-plan sasa hivi, basi katika vile vijiji vyote kutakuwa kuna tatizo kubwa la umeme kwa sababu umeme unasafiri zaidi ya kilometa 200, kilometa 300 na huko ulipotoka zaidi ya kilometa 800 au 900 sasa unauongozea 200, huku kwenyewe bado unatusumbua unakatikakatika, unapoenda kuuongezea tena 200 zaidi, utaendelea kuwa na matatizo badala ya kwenda kutatua tatizo ndiyo tunaenda kuongeza kelele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri wafanye tathimini waweze kuongeza Vituo vya Kupozea Umeme, pale Kigwa tutampa eneo nadhani tuna maeneo makubwa ili waweze kujenga kituo chao cha kupozea umeme na baadaye twende tukausambaze katika maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine linaloendelea sasa hivi, tumekuwa na plan za muda mfupi, sasa hivi wakandarasi wapo site, tunapitisha nguzo za miti kwenye majaluba, anajua kabisa hili ni jaluba, lakini saa hizi watalaam wa REA wapo, TANESCO wapo, mkandarasi yupo, umeme unapitishwa kwenye jaluba, baadaye masika inakuja nguzo zinakuwa kwenye maji zinaanguka, halafu baadaye wanasema tunaomba fedha za maintenance, kwa nini wasitengeneze mapema nguzo za zege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri waangalie maeneo yote ambayo yana matatizo ya kujaa maji, basi tuanze kugundua mapema wakandarasi wapo kule kama hawayajui hayo maeneo, Viongozi wa Vijiji wapo, Viongozi wa Dini wapo, wawashirikishe watawaambia hapa maji yanajaa wakati gani, hapa maji hayajai. Kama ile route imelazimika ipite palepale, waweke nguzo za zege ili kuweza kusaidia wananchi wetu. Kwa hiyo, kwa mwaka huu yangu ni hayo machache kwa Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kama ushauri, niipongeze Serikali wanaendelea na harakati nzuri za ujenzi wa bomba la mafuta, lakini tulishauri bei ya mafuta inaongezeka hasa Mikoa ya Kagera, Kigoma kule kwa sababu bei ya Dare es Salaam unakuta shilingi 3,100 lakini Kigoma ukienda shilingi 3,600 au shilingi 3,700, lakini wakija kuuliza kwa nini tunatofautiana na Dar es Salaam kitu ambacho kinachosababisha ni kwa sababu kule ni mbali depot zipo Dar es Salaam, tunaongeza cost za transport.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri tulishauri kwenye Kamati, lakini tuendelee kushauri kama sisi wawakilishi wa wananchi, katika Mradi wa Bomba la Mafuta kwa kuwa tumeliunganisha kutoka Uganda mpaka Tanga, palepale tujenge bomba letu lingine tena ambalo litarudisha mafuta mengine ambayo yatasaidia Mikoa hiyo ya Kanda ya Ziwa. Leo meli ikipaki Tanga tuweze kufungua mafuta Tanga tukaweka depot pale Nzega au Bukene, yakaweza kuja magari ya Mwanza yakawa yanachukua pale, magari ya Kigoma yakawa yanachukua pale tutasaidia sana kupunguza bei, lakini vile vile tutasaidia kupunguza mlundikano wa magari kwenda Dar es Salaam. Kwa hiyo, tukiweka vituo vyetu vya Serikali na bomba likawa la Serikali, gharama itakuwa ni cheap ingawa tutaweka tozo kidogo. Kwa sasa hivi kwenda Mwanza ni zaidi ya Sh.150 hadi Sh.170, lakini ukiweka pale kutoka Mwanza kuja Bukene wakachukua mafuta pale watachukua kwa Sh.50 ile nyingine itakuwa cost ambayo tumemsaidia mwananchi...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kauli kwa kusema naunga mkono hoja kwa sababu mabanda yalikuja, majibu mengi niliyapata. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Kamati hizi tatu. Kwanza, nianze kwa kuunga mkono kazi kubwa ambayo imefanywa na Kamati hizi tatu kwa niaba ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa na hoja ndogo yenye masilahi kwa Taifa letu. Nilikuwa nataka niseme jambo moja, kazi ya Bunge ni kuisimamia Serikali, lazima sisi kama wawakilishi wa wananchi tulinde haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nataka nitangulize hivyo kwa sababu gani; nchi hii imekuwa inaibiwa siyo kwa mitutu ya bunduki. Nataka Mheshimiwa Waziri wa Fedha (Mchumi aliyebobea), juzi alisema, namnukuu “Fedha hazipotei, kwa sababu Serikali inalinda mianya ya fedha kupotea”.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwambie kwamba, hatuibiwi kwa kwenda kuvunja nyumba, tunaibiwa kwa kutumia akili, tunaibiwa kwa kuingia mikataba mibovu. Lile suala la kuingia mikataba ndilo limeingiza Taifa letu hasara na tusipokuwa makini tutaendelea kuwa na hasara. Hapa ndio nashindwa kuelewa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu inafanya kazi gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ndiyo maana Mheshimiwa Rais siku moja alisema, sijui hicho cheo cha Mheshimiwa Kabudi (Mzee wa mikataba) kipo? Kwa sababu, tumekuwa na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ambayo inakwenda inakula huku na huku. Kwa sababu gani, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu inatakiwa isaidie Serikali katika kuingia mikataba mbalimbali. Sijawahi kuona Serikali inakwenda kushinda kesi, Serikali inakwenda kutetea mkataba ulioingia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakutolea mfano mwaka 2013/2014 ilikuja hoja hapa ya Tegeta Escrow mnaikumbuka. Mwanasheria Mkuu aliyekuwepo wakati ule alisema zile fedha siyo za Serikali. Wakasema fedha ni za watu binafsi. Kwa kuwa siku hazigandi, hilo jambo limerudi tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme jambo moja ndiyo useme Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na yenyewe inatakiwa iendewe na CAG huko. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliingia mkataba na APTL, tukatengeneza akaunti ya pamoja, tukasema fedha zetu tuziweke mahala fulani, Serikali ikatimiza wajibu wake ikaweka fedha. Wakatokea wajanja wakaenda kuzipakua. Tukaanza kuuliza humu za umma au siyo za umma si za umma? Mwanasheria Mkuu akasema siyo za umma, leo anaumbuka huku zile fedha zilikuwa za Serikali. (Makofi na Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kuna mashtaka yamekwishakuja tunadaiwa zaidi ya dola za kimarekani bilioni 148. Tunatakiwa tulipe dola za kimarekani milioni 148 sawa sawa na bilioni mia tatu na ushee. Sasa, huyu Mwanasheria Mkuu hakuliona hili toka zamani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo hapo nakuja kusema kwamba, kwa nini Ofisi ya Mwanasheria Mkuu haitusaidii? Cha ajabu, yule APTL wakati wanakwenda kutoa hizi fedha wakisema za kwao akasema, likitokea lolote linalohusu Serikali, Serikali haitohusika nitahusika mimi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo inakwenda kudaiwa Serikali na Serikali imekwishajiandaa kuanza kulipa. Mimi ninawambia msilipe, kalipeni hela zenu huko. Mwaka 2018 Mwanasheria Mkuu akapeleka kesi mahakamni kumshtaki huyu IPTL kwa nini ametutelekeza, sijui imekuwaje, mbona tulikuwa wote pamoja, ameingilia wapi? (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama Kuu ikatoa uamuzi wa kwamba, IPTL iilipe Serikali hizo fedha ili likitokea la kutokea iweze kuwalipa wale wanaodai ambao waliikopesha IPTL. Lakini mpaka kufikia tarehe 1 Machi, 2021 ilitakiwa zile fedha ziwe zimwkeishalipwa lakini hadi kufikia Desemba 2022 fedha hizo bado hazijalipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Serikali inaanza kuandaa eti kwa sababu tutakamatiwa ndege, image ya nchi itaharibika. Mimi niwambie hivi, kwa kulinda wezi, wabadhilifu, mlikuja hapa na hoja ya kusema fedha siyo za Serikali kumbe ni za Serikali. Mlikuwa mnajizunguka wenyewe leo mnaumbuka. Mimi niwambie na Kamati imependekeza fedha hiyo isilipwe, watakwenda kuchukua fedha za walipa kodi wa Tanzania kwenda kuhalalisha hela walizokuwa wamezitoa wakati ule kwenda kugawana kwenye viroba na leo hii hatuwajui waliogawana wako wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu ulikubaliana na IPTL fedha ilipwe, nenda ukasimamie hilo jambo. Bunge hili hatutapitisha fedha kwenda kulipwa kwa sababu ya uzembe wa watu. Kwa hiyo, nilikuwa nataka niikumbushe Serikali kwamba, hatuibiwi kwa mitutu ya bunduki kwa sababu hata hao wenyewe wenye mitutu ya bunduki na wenyewe wameshaibiana huko tozo unatozwa polisi wenyewe wameibiana. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hii nchi kila mtu ni mpiga deal. Mlinzi wa amani mpiga deal, ukienda TAKUKURU unakwenda kupumzishwa na hakuna kitu kinachoendelea. Kwa hiyo, haya mambo yaweze kusaidika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni la kusikitisha, Serikali imekwenda kuanzisha vitaasisi vya kufanya biashara halafu hamuwezi kufanya biashara. Leo TANOIL imeleta hasara duniani sijawahi kuona, Serikali ilipeleka bilioni 128 kuusaidia mfuko wa TANOIL ili ifanye biashara ya mafuta. Leo hata bilioni 20 haifiki, hela zote wamekula, tunaanza hapa kuzungushana, tumewafukuza. Umewafukuza wamekwedna wapi? Au ninyi wenyewe mlijitangulizia pasi ili mwende mkafunge? (Makofi/Kicheko)

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Venant, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mwigulu.

TAARIFA

WAZIRI WA FEDHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mchangiaji. Pamoja na mchango mzuri anaochangia naomba nimpe taarifa kwamba, hizi taarifa tunazojadiliana ni moja ya sehemu ya kazi nzuri zinazofanywa na taasisi zetu ikiwepo TAKUKURU pamoja na CAG. Inawezekana katika utendaji wa kazi na taasisi akawepo mtu mmoja mmoja. Hata hivyo, ningeomba hiki chombo chako ambacho ndiyo mtungaji wa Sheria, kiepuke ku-generalize taasisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu inaheshimika kwa taasisi. Inaweza ikawa na mtu mmoja mmoja akafanya hivyo lakini taasisi zetu ni moja ya nchi ambayo inaheshimika sana. Pia, TAKUKURU ni moja ya taasisi yetu ambayo inaheshimika kama taasisi. Kwa hiyo, nilitaka nikubaliane na michango yake na hisia aliyonayo lakini nimuombe asi-generalize taasisi kama taasisi, bali twende kwenye maeneo moja moja ambalo tunaona mapungufu. Pia, Serikali iko kwa ajili hiyo na huo ndio utawala wa Sheria unavyotaka. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Venant, unapokea hiyo taarifa?

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza amekula dakika zangu tatu, zilindwe. CAG alisema, Jeshi la polisi fedha zilizopotea za tuzo na tozo na hajamtaja mtu mmoja mmoja. Sasa, kama kuna mtu mmoja mmoja mtuletee tuwashughulikie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, CAG yeye alifanya Jeshi la polisi, sasa kumbe mnawafahamu mtu mmoja mmoja. Mtusaidie hilo jambo...

MHE. CHISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa, Taarifa.

TAARIFA

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji makini anayezungumza jambo hili kwa uchungu unaostahili. Jambo la msingi na namna bora ya Bunge hili kujiheshimisha kwa wale waliotuleta hapa, kuhitimisha hoja hizi kubwa tatu, ni kwa Bunge hili kuweka Azimio madhubuti na kuhakikisha kwamba Wizara zote ambazo ufisadi umetokea wa matrilioni ya fedha hizi, Mawaziri wanaohusika, narudia kusema Mawaziri walioshindwa kusimamia taasisi zilizoko chini ya Wizara zao wawajibike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawatowajibika hakuna namna nyingine. Kama hawatowajibika wao, twende na shingo ya yule ambaye tuna mamlaka naye ili boti letu lililotobolewa leo na mafisadi wasiendelee kwenda kushangilia kula hela ya umma huko halafu tunalijadili jina la jambo hili kwa wepesi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima Bunge hili lilinde heshima ya Bunge kwa kuwachukulia Mafisadi hatua na kuwachukulia wale walioshindwa kuwawajibisha. Nataka kumuunga mkono kwa kusema hivyo, acheni masihara. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Venant, unapokea taarifa ya Mheshimiwa Olesendeka?

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea. Kwa kuongezea kuweka msisitizo wa mtoa taarifa, nilikuwa nagusia Taasisi ya TANOIL ambayo imetupotezea zaidi ya bilioni mia moja na kidogo. Yaani hatua, Serikali inasema tumewaweka pembeni. Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na pia ni Waziri wa Nishati, ninakuheshimu sana. Nikuombe, nenda pale TANOIL na Kalandinga, ukamuache mhudumu tu. Wengine wote kamata mwende mkawaweke huko. Aliyehusika akae huko, hajahusika mumtoe kwa utaratibu uliopo. Lakini pale TANOIL kuna uozo mkubwa na sisi huku tumetoa mapendekezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kupitia Bunge lako, tunapigwa ndani na nje, tusipodhibiti sisi wenyewe, hakuna baba ambaye atakuja kutuokoana haya yatakuwa watendaji wa Serikali...

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jenista.



TAARIFA

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza kabisa naomba niendelee kumpongeza mchangiaji kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuendelea kutoa ushauri na kuungana na ripoti ya CAG kupitia kwenye Kamati husika. Lakini naomba tu nikumbushe maneno mengine ambayo mchangiaji amekuwa akiyatumia mara kadhaa leo kwamba, tunapigwa, tunapigwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tunapigwa, naomba tu nikumbushe Bunge lako Tukufu kwamba, yako makosa na baadhi ya watumishi kweli wanatukosea na wanafanya isivyo haki. Lakini bado Serikali yetu ya Awamu ya Sita imeendelea kufanya kazi nzuri katika miradi mingi na maeneo mengi. Kwa hiyo, ninachotaka kutoa taarifa, makosa haya yatachukuliwa na kufanyiwa kazi kwa uzito wake kwa idadi ya makosa yaliyopo. Lakini hayatochukua nafasi ya kazi nzuri sana ambayo imefanywa na Serikali ya Awamu ya Sita katika kuwahudumia wananchi.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Venant, malizia.

MHE, VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inafanya kazi vizuri, hatujakataa. Hao mnaowasema mmoja mmoja kwa nini mnawachelewesha huku mtaani wanaendelea kutusumbua? Wachukulieni hatua mapema. Hapa mnapokuja, hapa CAG mlikwishashindana huko ndiyo maana mmekuja humu Bungeni. Tunachokisema, tumekwishawaita kwenye Kamati wamejitetea na hakuna utetezi zaidi ya kuchukua hatua… (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa, muda wake umekwisha nilimpa dakika moja tu amalizie.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, basi.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, wamenilia dakika zangu lakini yote kwa yote, Bunge hili tusilete ushabiki. Ni lazima tuisaidie nchi, lazima tumsaidie Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Rais amesema tumsaidie. Inaweza kuwa ninyi Mawaziri hamjui huko ni nini kinachoendelea. Sisi tukijua mkayafanyie kazi, msianze kukinga kinga hapa mtakuwa hamtusaidii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia hotuba ya bajeti Ofisi ya Waziri Mkuu, kwanza nianze kabisa kwa kuunga mkono hoja hotuba nzuri ambayo imewasilishwa na Waziri wetu Mkuu ambaye imetupa matumaini kwa kipindi kilichopita utekelezaji wake na kipindi ambacho tunachokwenda cha bajeti cha mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizi tunafahamu Serikali iliyoko inatekeleza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, na Ilani yetu imejipambanua vizuri sana, Ilani ya 2020 – 2025 yenye ukurasa 303 kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu la Igalula Serikali kupitia hotuba ya Waziri Mkuu imewasilisha ni jinsi gani imejali katika sekta ya afya. Na katika hotuba yake imesema kwa kipindi kilichopita wameweza kujenga zahanati zaidi ya elfu moja na mia moja na kidogo. Lakini vilevile wameweza kujenga vituo vya afya zaidi ya mia nne katika nchi nzima ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika Jimbo langu la Igalula, Jimbo lenye wakazi zaidi ya laki tatu waliopiga kura waliojiandikisha mwaka 2020 walikuwa zaidi ya laki moja na kidogo. Lakini Jimbo langu lina zahanati 17 tu ambazo zinatoa huduma kwa wananchi zaidi ya laki tatu, ukigawa uwiano wa zahanati hizo ni zaidi ya kila zahanati inaenda kuhudumia zaidi ya watu 20,000 ambayo kwa kuzingatia Ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi kufikia na kufikisha huduma bora kwa wananchi wetu si sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Jimbo la Igalula ni waungwana sana wamekuwa wakiibua miradi mbalimbali ikiwemo miradi ya zahanati na shule. Na wamekuwa wakijitolea sana kwa kuwa wao ndio wanaona ndio vipaumbele vyao. Nilipochaguliwa na wananchi wa Jimbo la Igalula nimefaya ziara katika vijiji takribani 30 kati ya 58 kuangalia nini mahitaji yao na kila nilipokwenda wanahitaji shule na zahanati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia hotuba ya Waziri wetu Mkuu ambayo amewasilisha katika Bunge hili. Niiombe Serikali, juzi wakati tunachangia mpango wakati wa majumuisho Mhehimiwa Ummy Mwalimu alisema mwaka huu atajielekeza katika kutatua na kuweka vifaa tiba katika vituo vyetu vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hilo ni jambo jema zaidi, lakini niwakumbushe kuna maboma mengi ambayo yameibuliwa na wananchi wanahitaji yamalizike. Tukisema twende tukupeleke kwenye vifaa tiba kwenye kituo cha afya kimoja katika jimbo la Igalula hatuwasaidii wana Igalula. Leo hii aliyekuwa Waziri wa Ofisi ya Rais, nani hii Jafo, alikuja katika Kata ya Igalula, aliwakuta wananchi wamechangia kwa nguvu zao wodi ya mama na mtoto akavutiwa na uwekezaji ule na juhudi zile aliweza kutupatia fedha na sasa tumejenga kituo cha afya kilichopo katika Kata ya Igalula. Niwaambie kituo cha afya kimekamilika tangu mwaka 2019 mpaka leo hakijaanza kazi. Sasa lengo la Serikali ni kuongeza huduma kwa wananchi na si kuua huduma kwa wananchi. (Makofi)

Meshimiwa Naibu Spika, wameweka vigezo, kulikuwa kuna zahanati jirani wanasema tuhamishe vifaa tupeleke kwenye kituo cha afya sijajua hayo maelekezo yanatoka huku juu au wenyewe maamuzi yao. Lengo la kuongeza vifaa, vitoa huduma ni lengo la kuwasaidia wananchi, haiwezekani palikuwa na zanahati na tunasema tuna zahanati elfu moja na ushee pamoja na ile zahanati halafu unakwenda kuiua, unasema vile vifaa tuhamishie kwenye vituo vya afya, hata ukiangalia mwongozo wa afya, vifaa vya kwenye zahanati na kituo cha afya ni vitu viwili tofauti.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali kupitia kituo chetu cha afya katika Kata ya Igalula tupate vifaa tiba na ile zahanati iendelee kuwepo na wananchi waendelee kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna maboma ambayo Serikali imeomba tuwasilishe kupitia halmashauri zetu. Niombe yale maboma yote ambayo yapo katika hatua ya umaliziaji na ni nguvu ya wananchi watu wengine, wananchi wengine baadhi ya kata na vijiji wamejenga zaidi ya miaka sita, mingine miaka minne mitano, wakiwa wanapita pale wanaangalia nguvu zao zimepotea basi Serikali kupitia bajeti hii iweze kuweka fedha ya kwenda kumalizia yale maboma ikiwemo maboma ya zahanati na shule, hivi hivi niombe Serikali iweze kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la miundombinu juzi wakati wanachangia hapa Wabunge wenzangu kuna mbunge mmoja alisema yeye katika Mkoa wa Dar es Salaam haitaji kilimo kwasababu hana eneo la kulima. Alisema anahitaji barabara ili aweze wanachi wake waende kutafuta kipato warudi nyumbani wakiwa salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wangu wanahitaji miundombinu ya barabara, barabara zetu za vijijini tofauti na za Dar es Salaam. Barabara zetu za vijijini wanahitaji kiwango cha changarawe ili ziweze kupitika muda wote. Tukija kwenye masuala ya sekta nitachangia zaidi kutokana na muda niseme tu itoshe ninaunga mkono hoja hotuba ya Waziri Mkuu. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia mawasilisho ya Kamati tatu zinazosimamia fedha za umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwapongeza wachangiaji waliotangulia, na nimpongeze Mheshimiwa Spika kwa kuona unyeti wa kujadili fedha za wananchi na fedha za walipa kodi kwa kina ili kuona namna ya kutekeleza ripoti ya CAG, kama jicho letu kama Bunge kikamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Serikali ya Mama yetu ya Mama Samia ambayo imekuwa ikitafuta vyanzo na ikitafuta fedha usiku na mchana. Serikali imekuwa ikisafiri kutafuta wahisani mbalimbali kuja kuwasaidia Watanzania. Lengo la Serikali si kumaliza matatizo yote ya wananchi lakini angalau kupunguza shida zao kama inavyoonekana kule kwenye majimbo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa leo tunajadili ripoti ya kamati tatu, Kamati inayosimamia halmashauri zetu (LAAC), Kamati ya Mitaji ya Umma na Kamati ambayo inasimamia Mashirika ya Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na michango mingi sana ya Wabunge; nikianza kwanza na Kamati ya kwanza inayosimamia halmashauri zetu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumekuwa na tatizo moja, unakuta Waziri Mkuu anakuja kwenye maeneo yetu kukagua miradi, Waziri Mkuu ndiye anayekuja kugundua kuwa top za milango zina ufa; Waziri Mkuu anakuja kwenye miradi ndiye anayegundua kibanda cha 1,200,000 kimejengwa kwa 20,000,000 ilhali Serikali ipo kuanzia ngazi ya kitongoji, Kijiji kuja kwenye kata, wilaya na mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi napata kigugumizi sana. Kama kweli katiba yetu tulivyoitengeneza tungeisimamia vizuri kazi ingekuwa ndogo sana. Haya mambo yanayokuja kugundulika na viongozi wa kitaifa wakija katika maeneo yetu si kama viongozi waliopo kule hawajayasema. Shida yetu iko moja, hata sisi wanasiasa, tuposema au tunaposhauri watu wanaona wanasema wanasiasa acha waongee na hivyo hakuna utekelezaji wake. Kwa hiyo mimi niiombe Serikali kupitia Bunge hili kwa sababu Bunge limeumbwa na wanasiasa na Mheshimiwa Rais ni mwanasiasa. Kwa wale ambao wanaoona siasa haiwezi kufanya kazi au kushauri basi wakatafute kazi nyingine ya kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wametuleta huku kuja kuwatetea, wametuleta huku kuja kuwasemea. Leo tukienda kule zahanati ya pale kijijini mwananchi mwenyewe anakwambia mifuko ya cement ilikuwa inaondoka hapa halafu watu wanasema wanasiasa wanapiga kelele. Kwa hiyo mimi niombe, sisi wanasiasa ni kweli tuna maneno mengi lakini kwenye ubadhilifu lazima tuwe wakali; na ndiyo maana nimempongeza Mheshimiwa Spika kwa kuongeza muda wa kujadili ili Wabunge wote waseme nini kilichopo katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kwenye Bunge la Bajeti nilisema hapa, kwamba tumekuwa na tatizo moja; fedha za Serikali zinapokuja kwenye miradi vitu vinapanda bei lakini chanzo cha kupandisha bei hatukioni. Juzi mmepeleka bilioni 160 kwaajili ya kujenga madarasa 8,000, cement ilikuwa 20,000 kwenye mikao ya mbali lakini baada ya kufika zile fedha siku mbili kabla cement imefika 24,000 mpaka 25,000 katika baadhi ya maeneo. Tatizo ni nini? pochi ya mama imetema. Sasa kama pochi ya mama anahangaika kutafuta fedha halafu na sisi Serikali tunajua hakuna kitu kilichosababisha kupandisha bei na tumekaa kimya, hakuna hata Waziri wa Viwanda na Biashara kwenda kubainisha na kutoa taarifa kama uhaba wa cement. Mimi niiombe Serikali kwenye haya tuwe serious.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikirudi kwenye Kamati ya PAC; tumejadili sana. Ukija kuiangalia ripoti ya CAG imebainisha sana, na sisi kama Bunge tumeiamini taasisi yetu ya CAG Kwenda kutuangalizia. Inapotuletea hapa inatuonesha kabisa kwamba sehemu fulani kuna mianya. Sisi tusipochukua hatua tunaivunja moyo taasisi ambayo sisi tuliiamini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nishauri jambo moja. Si kama hawa watu hatuwahoji. Tumekaa hapa tangu mwezi wa 10, tumeita mashirika mbalimbali na tumewahoji ni aibu sana. Kwa kweli ni aibu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba, kama kanuni haziruhusu hebu tuone haya mashirika yakiitwa kwenye kamati ambayo ni Bunge dogo ambalo limeundwa na Mheshimiwa Spika kwa niaba ya Bunge zima ameyagawa mabunge madogomadogo ili kusimamia shughuli za Bunge. Hebu sasa kama tunaweza kurusha live humu ndani hebu na kwenye kamati tuwe tunarusha live waone wataalamu tuliowapeleka kule. Unakuta kabisa mwanasheria mbobevu, msomi darasa la saba anamuuliza swali la kitoto anashindwa kujibu. Sasa wakipigwa mara tatu mpaka nne kwa mikataba fake ambayo inatuingizia gharama wananchi. Wanalipa kodi kwa shida halafu fedha zinakwenda kupotea kirahisirahisi halafu mtu anajibu kirahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi naliomba Bunge hili kama kanuni hazipo, kamati zote wanapoitwa, hasa hizi zinazosimamia fedha za umma, CAG akionyesha mianya, basi na vyombo vya habari viwe vinaingia ili virushe moja kwa moja ili wananchi waone kama tulihoji na wao wamejichanganya vipi. Hii itaongeza ufanisi mzuri katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, asubuhi hapa Wabunge wengi wamezungumza kuhusu Kampuni ya KADCO. Ukija kuangalia sinema inayochezwa kule na KADCO ni aibu kubwa. Serikali imenunua hisa halafu bado ikajipangisha yenyewe. Imetengeneza mkataba ambako inamiliki asilimia 100 halafu yenyewe tena inaanza tena kujipangisha. Sasa nashindwa kuelewa kama mimi nina nyumba ninamiliki asilimia 100 halafu tena naanza kujilipa kodi, inaingia akilini kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kamati ililiona hilo, tumewaita KADCO wanachokisema pale yaani kama watu vile wanaona tu hili acha goma liende kwa sababu halina mwenyewe. Sasa mimi niwaambie wenyewe ndio sisi kwa niaba ya wananchi. Kama tusiposema, tusipotetea siku ya mwisho tutakuja kuhukumiwa. Jumba hili limepewa heshima kwa niaba ya wananchi milioni 60; na Tabora tumekuwa wa tatu tunaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo milioni 61 wametuamini sisi mia tatu, mia mbili na tisini na kidogo kwenda kuwatetea tunapokuja humu tunaleta maigizo, ngonjera, kuona kama hatuoni kumbe tunaona tutakuja kupata adhabu kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niombe Bunge hili litoe maelekezo. KADCO tumependekeza kwenye kamati kwamba irudi chini ya usimamizi wa viwanja vya ndege. Lirudi kwenye usimamizi wa viwanja vya ndege kwa sababu Serikali ndiyo inamiliki hisa asilimia 100. Kama tunamiliki asilimia 100 na TAA iko chini ya Serikali kwa hiyo huyu akija haina tija tutakuwa tumemwongeza mtoto mwingine hata kama alikuwa wa kambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kuangalia KADCO hii tunayoizungumza yaani iliweka mkataba wake ambao unaisha tarehe 16 yaani ilisema hivi, asitokee mtu yoyote hate yenyewe Serikali isijenge uwanja wa ndege wowote zaidi ya kilometa 240 kila upande kutoka KIA. Hii maana yake ni kwamba Arusha wasijenge uwanja wa ndege na watu wa Manyara wasijenge uwanja wa ndege. Mimi niiombe Serikali kupitia hili irudishe KADCO iwe chini ya usimamizi wa TAA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Ahsante nakushukuru sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia mpango uliowasilishwa na Waziri wa Fedha. Nami niungane na Wabunge wenzangu waliotangulia kuchangia, kwanza kwa kuipongeza Serikali yetu, Serikali ya Rais wetu, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuhangaika huku na kule kuhakikisha Watanzania na sisi kama wawakilishi wa wananchi tunatekeleza yale aliyokuwa amedhamiria kwa kipindi chake cha miaka mitano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tunazungumzia mpango wa Serikali ambao utatusababisha kutengeneza Bajeti Kuu ya mwaka 2023/2024; lakini pia tumekuwa na mpango wa miaka mitano. Waziri wa Fedha alishawasilisha mpango wa miaka mitano, nini Serikali itafanya kwa kipindi cha miaka mitano, kwa hiyo ndiyo maana tunaivunja hii mipango tunaiweka kwa mwaka mmoja mmoja ili iweze kutekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi wamezungumza hapa kuhusu Serikali kuwa na mipango mingi bila utekelezaji, lakini tumekuwa na mipango ya muda mfupi. Tunatengeneza mpango wa miaka mitano, lakini baada ya miaka mitano ule mradi unakuwa hauna tija tena kwa jamii. Ndicho alichokuwa anakisema Mheshimiwa Shabiby. Tulitengeneza mpango wa kutengeneza ICD nje ya Dar es Salaam kilometa 40 ya Kwala pale, lakini sasa hivi ile ICD inaonesha haiwezi kuwa msaada kwa Watanzania ilhali wataalamu wetu walisema itakuwa msaada, na tayari shilingi bilioni 30 imeshakwenda pale. Kwa hiyo tunapokuja kujadili mipango basi iwe yenye tija na inakuwa msaada kwa muda mrefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge walishasema, tunapo-design miradi basi tuwe tunaangalia na muda wa mradi utatekelezwa kwa kipindi cha miaka mingapi. Hauwezi kwenda ku-design mradi wa trilioni za fedha halafu life span yake inaishia miaka 10; hiyo tunakuwa tunakuwa tunamaliza fedha za wananchi na walipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishashauri hapa tukasema na kama Mbunge mmoja alisema hapa kama tungechora vizuri mradi wa Ziwa Victoria, tukatengeneza design ya kuleta maji safi na maji ambayo yatakuja kutumika kwenye kilimo nchi hii leo ingefungua fursa ya kilimo; lakini wataalamu wetu hawakulifikiria hilo wakafikiria kwenda kuwatibu wananchi halafu wakasahau wananchi wanahitaji kula. Na ndiyo maana wanasema kula ni lazima kuoga hiyari, hawakuliangalia hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa kuwa tumeshakosea, tunashauri tena. Tuna mradi wa bomba la mafuta kutoka Uganda kuelekea Tanga, lakini linapotoka Uganda linapita nchini ketu kwa asilimia zaidi ya 70. Nchi yetu itakuwa inanufaika kwa kiasi kikubwa. Tulishauri hapa kwa kuwa, wenzetu wa Uganda wanapitisha bomba hilo la kupeleka mafuta ghafi kwenye Bandari ya Tanga, tukasema kupitia mradi huohuo na fidia hizohizo tutumie tena mradi huo tutengeneze bomba kwa upande mwingine ambalo litarudisha mafuta safi, ili tutakapokuwa tunalilinda kwa gharama zilezile za kulilinda kwa kupeleka mafuta ghafi na ndizo hizohizo gharama tutatumia kurudisha mafuta safi. Ambapo tungejenga matenki makubwa kwa ukanda wa Tabora pale Bukene, tungeweka matenki pale watu wa Mwanza, watu wa Shinyanga, Tabora, Kigoma na Katavi wangeweza kunywa mafuta pale na; malori yote yanayokwenda Dar-es-Salaam leo tusingeyaona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tungeenda kuweka huko kwa wajomba zangu huko Bukoba matenki mengine, yangeweza kulisha ukanda ule wote, yangeweza kutusaidia. Hata hao waganda wangeweza kupitisha mafuta safi kurudisha katika nchi yao, tungeweza kuokoa fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ukienda mji wa Dar es Salaam mpaka wanaweka limit ya malori kuingia mjini kwa sababu bidhaa, kila kitu tumeweka Dar-es-Salaam. Leo ile barabara ya Morogoro – Dar-es-Salaam siku ikija kupata majanga ya kufungwa barabara kwa siku tano na barabara ya Arusha, huku Kanda ya Ziwa kote mawasiliano yanakatika, hususan nishati ya mafuta. Kwa hiyo tulikuwa tunashauri jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo tunashauri hapa; wataalamu wa uchumi wamesema sekta ya kilimo inachangia Pato la Taifa kwa zaidi ya asilimia 30, na Serikali yetu ya Awamu ya Sita imejikita kwenye kuwasaidia wakulima wetu; kwa sababu wanafahamu unaweza kuzunguka popote lakini jioni lazima ukumbuke chakula. Hata kama ukisema uende siku mbili, siku tatu, lakini ya nne lazima ule na chakula chetu lazima tukizalishe nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tumepitisha hapa bajeti ya Serikali zaidi ya bilioni 900 ambayo inakwenda kwenye sekta ya kilimo. Ni katika historia hatujawahi kupitisha bajeti ya namna hii, lakini sasa wataalamu wetu bado wako nyuma. Tunaona kila mwaka maji yanapotea, kila mwaka tunasema mito imejaa wakati wa masika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa naomba Wizara ya Kilimo, hakuna njia bora ambayo tunaweza kuwaokoa Watanzania kama tukiwekeza kwenye kilimo. Leo ukija pale katika Mkoa wa Tabora; huu ni Mkoa ambao uko kimkakati wa kulisha chakula mikoa ya Kanda ya ziwa, Kanda ya kati na Mkoa wa Dar es Salaam, pale chakula kingi kinatoka. Kule tuna mbuga nyingi nzuri ambazo zinatoa mchele mzuri, lakini leo mimi nashangaa hata kwenye Wizara yetu hatuna block farm hata moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Kilimo ielekeze Mkoa wa Tabora kutenga maeneo ambayo yatakwenda kusaidia kutengeneza block farm ambayo tuzalisha chakula ambacho kitalisha mikoa hiyo niliyoitaja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale katika Jimbo langu la Igalula kuna maji mengi ikifika wakati wa masika yanaleta maafa katika Kata ya Loya na Miswati. Yale maji tukiyawekea mtiririko mzuri, tukaweka kilimo cha umwagiliaji, basi hata yale maafa ambayo huwa yanatokea kila mwaka katika Kata za Loya na Miswati hatutayaona. Kwa hiyo, tunaomba Serikali ilete mipango ya muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la tatu. Tumetengeneza SGR, SGR hii ni kwaajili ya kwenda kufungua fursa ya kiuchumi katika nchi yetu, lakini tumeweka lot zaidi ya tano ambazo zinaendelea sasahivi katika ujenzi wa reli. Sasa, kuchelewa kwa miradi hii ambayo tunaweka fedha nyingi basi ndiyo tujue tunasababisha wananchi wetu kuchelewa kupata maendeleo kwa sababu wananchi wamefunga mikanda kusubiria miradi yao iweze kukamilika. Leo tunasema mradi wa SGR kutoka Dar-es-Salaam kuja Morogoro na kutoka Morogoro mpaka Dodoma umechelewa kwa zaidi ya miezi 12 na zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukija kuangalia mradi ambao tumesaini wa kutoka Makutupora kwenda Tabora na Makutupora kwenda Kigoma ambao tunategemea utakamilika 2024 kwa delay hii ambayo tumeiona tunapata mashaka, kwamba kama tusipojipanga vizuri kama Serikali hata hiyo miradi haitakamilika kwa wakati. Mimi niiombe Serikali kwenye hii miradi, ambapo tumeamua kufungua nchi, lazima tuwe serious ili tuweze kufikia malengo. Watanzania wana imani kubwa na Serikali yao, lakini watakuwa na imani kubwa kama hii miradi tukiifikisha na ikianza kuleta tija kwa wananchi wetu. Kwa hiyo lazima tuangalie jambo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine ambalo tunatakiwa tuliangalie, lazima tutengeneze viwanda vyetu vya ndani viweze kufanya kazi. Sasa, hatuwezi kutengeneza viwanda kama hatuna umeme wa kutosha. Leo tunapeleka umeme kila Kijiji, bado hatujaunganisha umeme kila Kijiji, lakini kuna tatizo kubwa la umeme katika nchi yetu kiasi kwamba sijawahi kuona. Vijiji vyenyewe mnasema tupeleke kule, bado hatujapeleka resources nzuri za kutosha ambazo zitakwenda kudhibiti upatikanaji wa umeme wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi jiiombe Serikali kuna umuhimu wa kuhakikisha tunaharakisha bwawa letu la Mwalimu Nyerere ili likamilike haraka ili liweze kwenda kufungua nchi. Leo viwanda vinaendeshwa kwa gharama kubwa kwa sababu ya ukosefu wa umeme, lakini kama tukitengeneza umeme wetu wa uhakika na ukatufikisha katika vijiji vyetu, leo tunapeleka umeme kule angalao bora tungewaacha na solar zao zina uhakika zaidi kuliko umeme huu wa TANESCO ambao tunaupeleka. Dakika 10 umekatika, dakika mbili umerudi, taabu tupu inaendelea huko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niiombe Serikali, pamoja na nia njema ya kupeleka umeme kwa kila Kijiji lazima na sisi tujipange. Kule tunapeleka umeme watu wa Mwamabondo kule ambako hawajawahi kufikiwa na umeme wakiona shoti watafute solution kwa kutumia njia gani? Maana tunaweza kupeleka umeme kule, hakuna wafanyakazi, hakuna vifaa vya kuwawezesha TANESCO kufika kutatua na matatizo kule; tunakuwa tumepeleka matatizo kwa wananchi wetu. Kwa hiyo mimi nilitaka nichangie katika mpango huu ambao tunaenda kuujadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la mwisho ni kuhusu sekta ya ufugaji ambayo inasemekana inachangia baadhi ya pato katika mfuko mkuu wa Serikali. Hata hivyo wafugaji wetu tumewarundikia mrundikano wa tozo nyingi sana. Mimi nimuombe Mheshimiwa Waziri, hebu pitieni hizi tozo. Kila siku, mara chanjo ya mapele, inakuja heleni, heleni yenyewe ambayo tunaiweka unaweza kuitengeneza hata kwa kupitia Wizara yako kwa shilingi 200, lakini mmempa mzabuni anaenda kuwatoza wafugaji shilingi 1,700. Bora hata ingekuwa inaingia kwenye Serikali wananchi wajue wanaisaidia Serikali kuingiza mapato yataenda kuwaletea maendeleo, lakini inakuwa fedha hii inaingia mfukoni mwa watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa hii nafasi. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Igalula nianze kuchangia kwasababu ya ufinyu wa muda, nianze kwa kuchangia suala la barabara, Jimbo la Igalula tumekuwa tukipiga kelele mara kadhaa hapa kulalamikia barabara zetu, nyingi hazipitiki hasa wakati wa masika.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto ya baadhi ya barabara na baadhi ya kata tangu dunia iumbwe, tangu tumepata uhuru hawajawahi kuona caterpillar la kusafisha barabara limepita katika maeneo yao. Kwa mfano katika kata ya Male toka tumeanzisha hii kata, halijawahi kupitiwa na barabara yoyote kwa bahati mbaya kupitia Serikali. Pia, Kata ya Nsololo haijawahi kupitiwa na caterpillar ambalo linasafisha barabara katika kata hiyo. Vile vile kuna barabara za Ipururu – Igalula haijawahi kupitiwa kabisa. Barabara za Kawekapina kuja Igalula hazijawahi kupitiwa. Ziko changamoto kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali kwasababu tuna chombo na taasisi ambayo kimeanzishwa na Serikali TARURA, tuiombe Serikali iongeze fedha kwasababu yawezekana caterpillar haziendi katika maeneo haya kwa sababu ya ufinyu wa bajeti lakini TARURA ikiongezewa fedha na halmashauri yetu ikaletewa fedha kupitia mfuko wa TARURA nina imani katika maeneo haya na wananchi wataona ma- caterpillar yamepita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna changamoto ya daraja, jana Naibu Spika amesema katika Jimbo lake kuna watu watano wamepoteza maisha, roho inamuuna sana. Kila mwaka zaidi ya watu 20 wanapoteza maisha katika Kata ya Loya ili mtu aweze kuja kupata matibabu katika Kijiji cha Loya kutoka Mwamabondo lazima avuke mto. Kila mwaka akinamama wajawazito, watoto wanaoenda shule wanapoteza maisha zaidi ya 20 kila mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, imekuwa likipigiwa kelele Daraja hili la Loya tangu mwaka 2013. Nimejaribu kupitia Hansard za Wabunge waliopita mwaka 2013 mpaka 2015 Mbunge aliongea, 2020 Mbunge alizungumza na baadaye akaamua kuwa maji yamemfika shingoni akaamua kwenda kuwadanganya wananchi akawaambia kuna fedha imetengwa ya kuja kujenga daraja.

Mheshimiwa Spika, mara baada ya kupita kuwa Mbunge nilikuja kufuatilia fedha hizi sijaona fedha yoyote iliyotengwa. Niiombe Serikali, kwa haya madaraja ambayo ni kiungo ya kijiji na yenye huduma kwa wananchi muda wote niiombe Serikali iwekee kipaumbele, tuna hitaji Daraja la Loya lijengwe kwasababu limeanza kupigiwa kelele zaidi ya miaka 10. Niombe Serikali iweze kusaidia katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya TAMISEMI 2021/ 2022 sijaona wametutengea fedha za kuweka vifaatiba katika kituo chetu cha afya. Tumejenga majengo mazuri, Serikali imewekeza fedha nyingi, tunashindwaje kuweka vifaatiba ili wananchi wetu waanze kutumia yale majengo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, majengo yamekaa kila siku tunapeleka wanafunzi wanakwenda kukalia, yanakuwa machafu nyoka wanaingia kwenye majengo. Niiombe Serikali, kwa hivi vituo ambavyo vimekamilika, wapeleke vifaatiba ili wananchi waanze kupata huduma. Vile vile tuna majengo mengi ya zahanati lakini kwenye bajeti hii wametuwekea kila jimbo angalau watapata zahanati mbili. Nina maboma zaidi ya 10 yapo, wananchi wameweka nguvu zao wanahitaji wapate huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwananchi anapochangia hela yake ya kwenda kujenga kitu, ana malengo nacho kwasababu amepata shida kwa muda mrefu. Kwa hiyo, yale majengo naomba Serikali itanue wigo wa kuongeza bajeti ya kujenga haya maboma. Sisi kazi yetu tunanyanyua maboma lakini Serikali mnapokuja na Mpango wa zahanati mbili mbili, kwa hiyo, nitachukua zaidi ya miaka 20 kumaliza maboma yangu. Niiombe Serikali, kwenye bajeti hii watuongezee ili wananchi wanapotoa nguvu zao basi waone matokeo kwa uharaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru, niachie wigo na wenzangu waendelee kwasababu niliomba tu dakika tano na wewe umenipa. Ahsante, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niwe mmoja wa wachangiaji katika mjadala huu wa Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja kwa sababu tangu asubuhi Mheshimiwa Waziri amewasilisha bajeti yake ya Wizara ya Maji na nimepitia alhamdulilahi Jimbo langu la Igalula nimeona vijiji vingi. Namshukuru sana Naibu Waziri na Waziri wake, kweli Jimbo la Igalula tunakwenda kwenye mapinduzi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wiki iliyopita kupitia Bunge lako hili Tukufu katika maswali ya nyongeza niliuliza Mradi wa Maji wa Ziwa Victoria unaotekelezwa kwenye Jimbo langu la Igalula katika Kata za Goweko, Igalula, Nsololo na Kigwa. Nikasema mradi ule utekelezaji wake umesimama na nikaiomba Serikali iweze kunipatia fedha kwa sababu umesimama kutokana na kutokuwa na fedha. Kwa Serikali Sikivu ya Chama cha Mapinduzi niliweza kuletewa shilingi bilioni moja ili mradi ule uanze utekelezaji wake wa kupeleka maji katika Jimbo langu la Igalula.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado tuna changamoto katika mradi huu. Nimshukuru Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Tabora ameweza kuuzungumzia. Mradi wa Ziwa Victoria katika Mkoa wetu wa Tabora Jimbo la Igalula halikuwepo katika mpango. Wakati kampeni tulivyokuwa tunanadi sera alipokuja Hayati Dkt. John Pombe Magufuli tulimuomba Jimbo la Igalula liingizwe katika mpango wa kupelekewa maji ya Ziwa Victoria naye alipokea na akatoa maagizo na ule mradi ukawekwa katika mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi ule ni mkubwa sana, unakwenda takriban vijiji 16 vilivyoko katika maeneo hayo na una vituo 100 lakini tangu tumeubariki mradi ule mpaka saa hizi na malengo ya kukamilika mradi kufikia mwezi Desemba, 2021 sasa hivi tuko mwezi wa tano nikuambie kupitia Bunge hili mradi ule umekamilika kwa asilimia 10. Tumekuwa tukifanya ziara mbalimbali kuuliza kwa nini mpaka saa hizi tunakwenda taratibu na wananchi wana hamu na shauku ya kupata maji kutoka Ziwa Victoria, wanasema tatizo ni fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekwenda kwa Mheshimiwa Waziri mara nyingi sana, mradi ule ni wa kiasi cha shilingi bilioni 11 mmetupelekea shilingi milioni 900 ya kwanza mkatuongezea shilingi bilioni moja na kwenye bajeti hii nimeona mmeweka shilingi bilioni 1.4 kwa maana kwamba huu mradi utakwenda kukamilika baada ya miaka mitatu. Nimwombe Mheshimiwa Waziri hebu aliangalie Jimbo la Igalula kwa sababu tangu tumeumbwa hatujawahi kufungua maji yanayotokana kwenye koki. Kwa hiyo, wananchi wa Jimbo la Igalula, kupitia kata hizo nne watafurahi sana huu mradi ukikamilika kama ulivyopangwa Desemba, 2021. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimboni kwangu nina changamoto kubwa sana ya maji na mlifanya juhudi za makusudi kututolea maji ya Ziwa Victoria kuyaleta Tabora, ni umbali mkubwa sana lakini mlitambua kuwa ardhi na eneo letu la Mkoa wa Tabora upatikanaji wa maji ya kuchimba kwa kutumia visima ni mgumu sana. Nimwombe Mheshimiwa Waziri katika kuibua vyanzo vya upatikanaji wa maji hebu tubuni mbinu mbadala kwa haya maeneo ambayo yamekuwa yana changamoto ya uchimbaji wa visima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimboni kwangu mimi naishukuru Serikali imechimba visima vingi lakini vinafanya kazi kwa miezi miwili, mitatu ni kwa sababu ardhi yetu ina miamba haina maji. Vilevile mmekuwa mnapoteza fedha nyingi, mkandarasi mnampa tenda ya kuchimba visima anawaambia eneo hili lina maji akienda kuchimba anasema maji yalikimbia yakahamia upande mwingine sasa fedha inapotea, haileti tija kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali tubuni vyanzo vingine, kwetu tuna majaluba mengi sana, kuna mikondo mingi ya maji yamekuwa yanaleta mafuriko kwa nini tusiyavune haya maji tukatengeneza mabwawa makubwa. Tukiweka bwawa pale katika Kata yetu ya Kizengi ninyi wenyewe mashahidi wakati wa masika kabla hatujatengeneza barabara ya Chaya - Nyaua ilikuwa kila mwaka barabara inakatika eneo la Kizengi kwa sababu ya maji mengi lakini tungebuni pale yale maji yasiende barabarani yakategwa yangeweza kusaidia hata katika shuhuli za kilimo siyo tu matumizi ya binadamu. Katika eneo letu hasa Mkoa wa Tabora Jimbo la Igalula naomba Wizara ibuni vyanzo vingine vya upatikanaji wa maji maana yapo kwa sababu kila msimu mvua inanyesha na maji yanakuwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mradi katika Kata yangu ya Tura alishawahi kuja Waziri wa wakati huo Mheshimiwa Prof. Mbalawa Machi, 2019. Alivyokwenda kwenye Kata ya Tura alikuta kuna bwawa ambalo liliachwa na mkoloni ambalo linatumiwa na Railway Station akasema hiki ni chanzo kizuri pale pale akatoa shilingi milioni 300 ili wananchi waanze kutumia maji katika Kijiji kile cha Tura. Wakaahidi baada ya miezi mitatu maji yataanza kutumika katika Kijiji cha Tura leo mwezi wa 18 maji wananchi wa Tura wanayasikia kwenye redio tu, hawajawahi kutumia maji yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sisi tumeenda kufanya ziara pale tukimuuliza mkandarasi anakuambia tulipewa shilingi milioni 300 mradi wa shilingi milioni 800, kwa hiyo tunasubiri shilingi milioni 500 zingine ili tuweze kuukamilisha. Sasa tunakuwa tunamlaumu mtaalamu, engineer tunaanza kumpigia kelele lakini ukija kuangalia tatizo lingine huku fedha Serikalini hazijatoka. Niiombe Serikali ule mradi ni mzuri sana, ni bwawa kubwa sana lina maji mengi tukiutengeneza vizuri hata wananchi wangu wa Vijiji vya Kalangasi, Malema, Kizengi, Maguliati na Migongwa wanaweza kupata maji kwa sababu ni chanzo kikubwa ambacho waasisi wetu walituachia. Katika bajeti hii nashukuru vijiji vyangu vingi umeniwekea fedha lakini kwenye hii miradi inayoendelea hasa ya Ziwa Victoria na ule mradi wa Tura, naomba aniongezee fedha ili niweze kukimbia na wananchi waweze kuona matunda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini namshukuru Mheshimiwa Waziri amenipa visima sita katika Kata za Mmale, Mwaokoyesengi, Migongwa, Mbulumbulu na Misole. Kwa hivi visima amasema atanipa shilingi milioni 156 huyu mkandarasi anayekuja wamlipe baada ya kutumia maji ndani ya miezi sita asije akaniachia mashimo halafu akaondoka na fedha zikaondoka. Anapokuja kuchimba visima katika haya maeneo ambayo umeniainishia tuone tija ya wananchi wetu ya upatikanaji wa maji kwa sababu tunajua kabisa upatikanaji wa maji kule ni tatizo asije akachukua hizi fedha kwa sababu wamezileta akadhani ni gombania goli.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Waziri yeye ni mkali asimamie haya, wamekuwa wakichimba wanaacha visima havitoi maji na ushahidi upo. Kila siku mnatenga hela za ukarabati wakati visima havitoi maji na penyewe mpaangalie, haiwezi kuwa kila siku tunakarabati kisima halafu hakitoi maji wawaambie visima vinavyotoa maji viko wapi? Katika Jimbo langu la Igalula labda bomba moja au mawili ndiyo yanayotoa maji lakini kwenye takwimu za Waziri unaweza kukuta zaidi ya mambo 40 lakini hayatoi maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai maana binadamu kila siku lazima atumie maji, akila chakula atatumia maji, ni lazima tuliangalie hii sekta katika kipaumbele chake. Nakuomba Mheshimiwa Waziri mradi wangu wa Ziwa Victoria wananchi wa Igalula, Kata za Kigwa, Goweko, Nsololo na mimi nimekuwa nikikuambia kila mara mzee nisaidie na kweli nisaidie nipelekee maji kwenye vile vituo 100 ambavyo umeviandika kwenye bajeti hii wananchi wanasubiri maji kwa hamu ili akina mama wapumzike kuamka alfajiri na kwenda kutafuta maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo na mimi niunge mkono hoja, ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, Ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi ambayo imewasilisha hotuba yake leo asubuhi. Kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali na Wizara kwa ujumla kwa kujenga Barabara ya Chaya - Nyahua ambayo ilikuwa ni kero kwa wakazi wa Mkoa wa Tabora, lakini nishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kuikamilisha kwa asilimia 100 ambayo ilikuwa katika Jimbo langu la Igalula, wananchi wa Igalula wanashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii imetoa fursa kwa watumia barabara hasa wa Mikoa ya Shinyanga, Simiyu na Mwanza badala ya kupita Igunga sasa wanapitia Jimbo la Igalula. Nitoe wito wanapopita katika Jimbo la Igalula tuna migahawa mizuri sana wakifika Tula pale kuna mama mmoja anaitwa mama Tausi, wakifika wapite pale kuna kuku wa kienyeji, anajua kuwapika vizuri. Vile vile wakipita Kizengi pale kuna mgahawa mmoja unaitwa Tula Mgahawa, basi mambo yanakuwa mazuri. Naibu Spika nawe karibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya shukrani zangu hizo nirudi, mkandarasi amemaliza ujenzi wa barabara, Mheshimiwa Waziri, Katibu Mkuu Wizara ya Uchukuzi nilikwishamwandikia barua ya kumwomba majengo yale ya Kizengi. Naomba wakimaliza na wakakabidhi mradi, basi naomba yale majengo waikabidhi halmashauri yangu ili tuweze kufanyia utaratibu mwingine hasa tuweze kupata kituo cha afya kwa sababu Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi imetuelekeza tutajenga vituo vya afya kwa kila kata. Kwa hiyo, wakinikabidhi yale majengo nitayatumia kwa ujenzi wa kituo cha afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nichangie baadhi ya mambo kidogo, pamoja na mazuri wanayoyafanya Serikali lakini bado tunachangamoto ya upatikanaji wa barabara. Kuna Kamati iliundwa ya Mapitio ya Barabara, sasa hii kamati ilivyoundwa ilikuwa inaenda kuzitambua barabara ambazo zinatekelezwa na TARURA, lakini mpaka leo kamati hii imekwishamaliza kazi, lakini hatujui hizi barabara ni lini zitaingizwa kwenye mfuko wa upatikanaji wa fedha wa barabara.


Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, kwangu kuna barabara ambazo ni uchumi, ni muhimu sana katika maeneo yangu, zinaunganisha wilaya na wilaya, lakini zingine zinaunganisha mkoa na wilaya nyingine ndani ya mkoa mwingine. Kwa mfano, kuna Barabara ya Makibo – Msololo – Goweko - Kamama mpaka Nyahua. Hii barabara ina zaidi ya kilometa 80, tunapoisema barabara hii ni muhimu sana kwa sababu inatoka katika Wilaya ya Sikonge inakuja katika Wilaya ya Uyui. Tukisema itekelezwe na TARURA haiwezekani.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwanzoni tulikuwa tumeweka utaratibu mzuri wa kuainisha hizi barabara, tunazipandisha hadhi TANROAD wanafanya utaratibu mzuri wa kuweza kuzitengeneza, lakini utaratibu ule Wizara waliukataa, wakasema hizi barabara zitekelezwe na TARURA. Leo wilaya yangu inapata bajeti ya TARURA 1.2 bilioni, ukisema utekeleze hii barabara yenye kilometa 80, tutakuwa tunawaonea TARURA. Niombe Serikali ni ile ile, TARURA ni ile ile, niombe Waziri atakapoongeza fedha kwenye Mfuko wa TARURA hata kwa emergency, basi atakuwa ameokoa wananchi wa Kata ya Jimbo la Igalula. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Barabara ya Sikonge inakuja Igalula inatokea Goweko, nayo barabara ni nzuri sana kwa uchumi wa wananchi wa Sikonge na wananchi wa Jimbo la Igalula, Wilaya ya Uyui. Leo Mheshimiwa Kakunda akiwa anataka kwenda kufanya ziara kwenye kata moja inaitwa Makibo, lazima afike Tabora Mjini, baadaye arudi tena huku Makibo, ni kilometa nyingi sana anapoteza rasilimali mafuta, lakini angeweza kupita hii barabara basi angeokoa mafuta na hizo fedha zingine akaelekeza kwenye miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya barabara kila mahali ipo, lakini hizi barabara ambazo tunazozipigia kelele, Waziri anaweza kusema TARURA wanatekeleza kwa bajeti iliyopo kiuhalisia TARURA hawawezi kutekeleza bajeti hii. Nimwombe Waziri kupitia mafungu yake akipeleka TARURA fedha za dharura kule, basi wanaweza kuzifungua barabara hizi na hatimaye zikafunguka na wananchi wakaweza kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nije kwenye suala lingine ambalo ni kuhusu TRC, kwangu wananchi wanategemea sana uchumi kwa kupitia reli ya kati. Hata hivyo, tulikuwa tuna urekebishaji wa miundombinu ya reli ya kati ambayo walimtafuata mkandarasi akawa anatengeneza reli ya kutoka Manyoni kuja Tula, Malongwe ikaelekea Goweko mpaka Tabora Mjini. Sasa cha ajabu ninachokishangaa tulikuwa na miundombinu ya njia tatu katika Station ya Goweko, huyu mkandarasi badala ya kurekebisha reli akaanza kung’oa tena njia zingine, ameua njia zingine, zile reli hatujui amezipeleka wapi, sasa wananchi wa Kata ya Goweko wanauliza alikuwa anakuja kubomoa miundombinu au alikuja kurekebisha miundombinu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tunategemea zile reli kwa kukuza uchumi wa wananchi wetu kwa kukata mabehewa na kupakia mizigo pale, lakini vile vile, train ikiwa inapita pale ikiweka njia mbili upishano wa train na train wananchi wetu wanapata biashara, lakini sasa leo imekuwa njia moja, train inasimama kwa dakika tano, wananchi hawafanyi biashara. Nimwombe Mheshimiwa Waziri tunataka kujua zile reli zimekwenda wapi? Wananchi wanahitaji pale reli ziwe za njia mbili train ipishane, mabehewa yakatwe, ili waweze kupata uchumi na pale sisi tunatengemea sana uchumi wa train. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, station ile pale tunategemea sana katika uchumi na abiria wapo wengi sana, lakini leo cha ajabu tangu shirika limeanza ile station hatuna choo cha abiria, abiria wakija pale wao wameshajisevia kutoka nyumbani wakifika pale hakuna huduma nyingine itakayoendelea. Kwa hiyo, tunaingiza fedha nyingi kupitia station ile, tunashindwa kujenga hata choo cha shilingi mbili na tuna kampeni nzuri ya choo bora, lakini station yetu kupitia Wizara yetu inashindwa kujenga choo. Niiombe Serikali yangu, Wizara yangu wakajenge choo pale gharama yake ni ndogo sana ili wananchi na abiria wanaowasafirisha wapate huduma nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna changamoto nyingine, Serikali imeleta umeme ambao ni Sh.27,000/=, lakini station ile imekuwa giza miaka yote na umeme upo, lakini mpaka leo tunashangaa kwa nini train zikipita usiku wananchi wanapata adha, pale kuna uwizi unaotokea wakati wananchi wanasubiri abiria iweze kuja pale, giza limekuwa kubwa Sh.27,000 mimi Mbunge wao nitalipa wakafanye wiring.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, naam, muda umekwisha, jamani!

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa hii nafasi niwe miongoni mwa watu ambao watachangia Wizara hii ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, kwanza anianze kwa kumpongeza Waziri kwa kazi nzuri yeye na Naibu wake, Katibu Mkuu kwa kweli wanafanya kazi usiku na mchana kuhakikisha wananchi wetu wanapata mwanga ingawa kuna changamoto. Lakini pia niwapongeze viongozi wa REA, DG wa REA naye anafanya kazi nzuri kuhakikisha anasambaza umeme na sisi tunajivunia kuwa na DG huyu kwa sababu umeme kweli umefika katika vijiji mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo bado tuna changamoto nilipochaguliwa na wananchi wa Jimbo la Igalula nilikuja hapa kujua hatma ya vijiji vyangu ambavyo bado havijafikiwa na nishati ya umeme na uzuri Mheshimiwa Waziri alinijibu Bungeni na bado tukafanya naye safari ya kwenda kwa wananchi wangu kuwaambia lini umeme utawafikia wananchi wangu. Hilo nilikushukuru sana Mheshimiwa Waziri, tulifika katika Kijiji cha Izumba, Kata ya Miyenze na ulikuta watu wengi, walikupokea kwa furaha kwa sababu walijua wewe ulikuja na umeme. Lakini matarajio yao hayakuwa kama tulivyokuwa tumetarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka na naomba nikunukuu na siku ile tulikuwa wote wewe Waziri na Naibu wako na Mkurugenzi wa REA naye alikuwepo na Bodi yako yote ya REA ilikuwepo. Uliwaambia wananchi ilikuwa tarehe 16 Machi ukawahakikishia kufikia mwisho wa mwezi wa nne umeme Izumba utakuwa umewaka na ukawahakikishia ukasema leo umekuja na wakandarasi utawaacha pale pale ili waanze kuwasambazia wananchi umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ni mwezi Juni tarehe 2, 2021; wananchi wa Izumba hawajaona nguzo, yule mkandarasi tulivyoondoka na yeye akaondoka, sasa hivi amebaki anakwenda anaondoka. Nikuombe Mheshimiwa Waziri tunamaliza Bunge tarehe 30 ya mwezi Juni, 2021 ninakwenda ziara kule sasa kama nikizomewa ujue umenisababishia wewe ule mzomeo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nikuombe Mheshimiwa Waziri kwa hizi siku chache naomba uniwashie umeme, nikiunganishi kati ya wananchi na Serikali, ninapokwenda kule tena kuwaambia nitaenda kuiambia Serikali wakati Serikali ndiyo niliipeleka kweli Mheshimiwa Waziri utanipa wakati mgumu mwisho wake na mimi nitakuwa upande wa Serikali nikabaki nashangaa kauli ya Serikali haijatimizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Kata za Miyenze, Tura, Miswaki na Lutende wote wanahitaji na wanamatumaini makubwa ya kupatiwa umeme, naomba uwasaidie kwa sababu ulitoa kauli hiyo kwa bashishi kubwa na wao wakakupigia makofi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada za Serikali kutupelekea umeme, mkandarasi amekwenda kwenye baadhi ya vijiji ameenda kuwashirikisha Waheshimiwa Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji wakisema jiandaeni umeme unakuja. Lakini mkandarasi anasema mimi nitaleta umeme, nitasambaza kilometa moja tu kwenye kijiji.

Mheshimiwa Spika, mimi niiombe Serikali pamoja na nia njema ya kupeleka umeme, msitupelekee mgogoro mwingine ambao utazalika ndani ya mgogoro mwingine kwa sababu unapopeleka kilometa moja na mkaweka idadi ya watu labda 20 wataunganishiwa wakati watu ambao wapo tayari kuunganishiwa umeme zaidi ya 20.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali kama yule mkandarasi mnampa mkataba wa kilometa moja muwe mna fedha za ziada anapomaliza kilometa moja TANESCO anaanza kazi ya kuunganishia wateja wengine ambao waliobaki. Leo unaponiambia mji kama wa Kata ya Tura unapeleka nyumba 20 nani umpelekee nani usimpelekee, Mji katika Kata ya Miyenze unapeleka nyumba 20 nani umpelekee na nani usimpelekee; wale wote ni wapiga kura. Niiombe Serikali itusaidie hii scope iongezwe kidogo kutoka kwenye kilometa moja basi angalau kwenye kijiji ifike hata kilometa tatu au nne itakuwa imetusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna changamoto moja ambayo Serikali maana kwamba Wizara na TANESCO wanacheza ngoma mbili tofauti. Leo Serikali inatuambia mwananchi akilipa shilingi 27,000 anaunganishiwa nishati ya umeme. Lakini ukienda kwenye uhalisia sivyo mwananchi analipa shilingi 27,000 unakuta nishati ya umeme iko zaidi ya kilometa moja huyo akilipa shilingi 27,000 kweli kiuhalisia atapata umeme?

Mheshimiwa Spika, ukienda TANESCO anakwambia sina bajeti, siwezi kupeleka umeme kwa sababu inahitaji nguzo zaidi ya kumi, sasa TANESCO hujampa fedha na amepokea fedha ya mteja, unapotoa kauli kama Waziri kusema shilingi 27,000 wananchi wanataka kweli kulipa shilingi 27,000 wapate umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali hebu kuweni na dawati maalum la kutoa elimu. Ile shilingi 27,000 ukomo wake uko wapi, je, kama kuna ziada muda gani wa kusubiri ili ninyi mjipange muweze kufanya hiyo kazi ya kumuunganishia umeme, kuliko sasa hivi imekuwa vurugu match. Leo hii Kata ya Goweko kuna umeme jazilizi ambao umepelekwa kule mradi ambao nilikuomba Mheshimiwa Waziri. Lakini wamepeleka kwa idadi ya nguzo 35 zimekamilika, lakini wananchi bado na wameshalipa shilingi 27,000 wanasema sasa sisi tunafanyaje, wameenda TANESCO wanaambiwa sisi hatuna bajeti. Nikuombe Goweko pale tuongezee nguzo zingine kwa sababu ulisema hii kauli na wenyewe wanaisimamia hata kama ipo nje ya ule mkataba mimi nikuombe sana nisaidie hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nirudi sasa kwenye sekta ya mafuta; kwanza niipongeze Serikali kwa jitihada zake za kuchukua jukumu la kuweka vinasaba, niipongeze sana, mlipoipeleka TBS kule mmefanya uamuzi mzuri na sisi kama Wabunge tulitoa hilo kwa sababu kuiona kampuni inanufaika kushinda Serikali na ndiyo maana tukasema hivi vinasaba tuviweke wenyewe. Nikiri tu ni mdau mzuri wa mafuta katika sekta hii naomba nishauri jambo moja. EWURA wanafanyakazi nzuri sana, lakini wao nao wana changamoto, leo EWURA amekuwa akienda tu sehemu kama kuna makosa, haulizi hata kosa limetokana na nini yeye kazi yake ni kufungia tu kituo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa sijui ndiyo wamesoma professional ya kufunga tu, lakini wao hawajikagui kama wana upungufu, wenyewe wanaona wafanyabiashara ndiyo wana mapungufu. Mimi nitoe ushahidi kidogo juu ya EWURA wanavyofanya leo tunasema vinasaba viwekwe kwenye mafuta, lakini mafuta yaliyowekewa vinasaba na ambavyo havijawekewa vinasaba kwa mteja wa kawaida hajui kitu chochote, hata mwenyewe sijui mafuta yapi yamewekewa vinasaba na yapi hayajawekewa vinasaba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo akija yeye na machine yake ndiyo anaiamini kama Msahafu au Biblia akiweka pale ikikataa anasema hii ina vinasaba kidogo haijafikia kile kiwango. Sasa hicho kidogo nani aliweka? Na ikiwekwa inaoneshaje kama imewekwa kidogo? Nikuombe Mheshimiwa Waziri na hili naomba ulichukulie u-serious hawa jamaa wanasumbua sana wafanyabiashara yaani wamekuwa wao ndiyo miungu watu wakifika pale funga kiri hapa kuwa nimekuta kuna kosa na kama nataka nifanye biashara na kiri haraka haraka nikulipe faini yako tuachane kisalama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini unakuta muda fulani wameonea ukichukua yale yale mafuta ukaenda kupima machine nyingine inaleta kipimo tofauti ya kwao ya kwanza, wamepima na wamekufungia na wamekudhalilisha imesema inamakosa, umeenda kwingine ipo sawa ukirudi huku wanasema aisee kanuni ya fidia hamna wewe endelea kufanya biashara. Badilisheni hizi kanuni la sivyo wajiangalie na wao na siye tutakuja siku moja wakaja wakakutana na magumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hapa watu wamesema vituo vya vijijini vipunguziwe masharti ni kweli, leo mnaruhusu watu kulala na petrol mnashindwa kumruhusu mtu haraka haraka aweke mafuta pale nje pump moja mnaweka mavibali mengi, yaani kibali kukamilisha kupata shell ya mafuta yaani uwe na siyo chini ya shilingi milioni 30. Sasa kwa mwananchi wa kijijini ukimwambia milioni 30 anaipata wapi? Kuna teknolojia zimekuja nyingi kuna kontena linatembea yaani ukiweka kontena…

SPIKA: Ahante sana.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, huku ndiyo kulikuwa panoge, nakushukuru sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa nafasi hii kuwa miongoni mwa watu ambao watachangia bajeti kuu ya Serikali, iliyowasilishwa na Waziri wa Fedha. Kwanza nianze kuipongeza Serikali, nimpongeze Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri ambayo wameifanya, kwa muda mchache ameleta bajeti yenye matumaini makubwa kwa wananchi, kwa sababu wananchi wetu walikuwa na kero kubwa sana juu ya maendeleo yao sasa hata kodi zetu ambazo tunakwenda kuzilipa zitaleta tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanachi walitaka hatima ya maboma ambayo wanayaanzisha yaweze kukamilika, pia kwenye bajeti hii imejipambanua wazi kabisa kuwa maboma yetu yanakwenda kukamilika na watu wataanza kupata hudama, hongereni sana Serikali. (makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watanzania wanahitaji kulipa kodi, lakini waione kodi yao inafanya kazi. Leo tumeleta mpango wa kufuta baadhi ya kodi na kuongeza baadhi ya kodi, lakini inahitajika elimu iongezeke zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, tunaishukuru Serikali kwa kupunguza tozo au faini ambayo ilikuwa ilikuwa inatozwa kwa watu wa boda boda wanashukuru sana, na tumekuwa tunapokea simu hasa mimi kutoka jimboni wanasema mmetupunguzia faini lakini mmeongeza fedha kwenye mafuta, ukiangalia uhalisia fedha kwenye mafuta haijaongezwa ni utaratibu wa kawaida ambao ulikuwa tangu zamani, na wananchi wanaona mafuta yamepanda zaidi kwa kipindi hiki kifupi, basi wanajua fedha sasa Serikali imepunguza faini imekuongeza kodi kwenye mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali, tunapokuwa tunafanya hivi vitu basi tuongeze na wingo wakutoa elimu. Kwa mfano watu wa mamlaka inayohusika na upandishaji wa bei za mafuta, basi wanapokuja kupandisha au kushusha wanatakiwa watoe taarifa kwa wananchi ili waweze kujua tumeongeza kwa sababu gani au tumepunguza kwa sababu gani, ili tuweze kupunguza haya mengine ambayo wananchi wanashindwa kuelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze kwa kupunguza faini kutoka shilingi 30,000 mapaka shilingi 10,000, mmewasaidia sana boda boda na Mheshimwia Waziri ulisema hapa unahitaji boda boda wasiwe ndio chanzo cha mapato ya Serikali, unahitaji Polisi wafanye kuwaelimisha boda boda ili wesiwe miongoni mwa wavunja Sherika. Nikupongeze sana, maana Polisi walibadilika kuwa mungu watu. Sisi kwetu kule boda boda ndio ambulance ya kupeleka wangojwa, ili mgonjwa aweze kukaa vizuri kwenye pikipiki lazima ubebe na mtu mwengine wa kumshikilia, ukikutana na Polisi anawaza tu yeye kutoza faini, sasa ilibadilika kuwa ni kero kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kwa kuipunguza hii imetusaidia sana. Na mimi niiombe na nimuombe Waziri wa Mambo ya Ndani, Polisi wetu watusaidie sana kuwapa watu elimu. Unajua kuna mazingira mengine hayahitaji hata faini, unaweza kukutana na mtu amevunja taa kwa bahati mbaya wakati huo huo umekutana naye anakwambia gari lako bovu, ukumwambia nimevunja sasa hivi anakwambia hamna lete nikupige faini, wakati ilikuwa ni kitendo cha kuweza tu kumwambia, changamato hii nenda kairekebishe, hilo litatusaidia sana na litatupunguzia malalamiko kwa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwa Madiwani, niipongeze Serikali kwa kulibeba jukumu hili ambalo lilikuwa ni kero kwa madiwani wetu. Madiwani kero kubwa ilikuwa ni kupata ile stahiki yao kwa wakati, ilo sasa Serikali mtakwenda kulifanya kwa utumilifu, kwa uhakika mkubwa kwa sababu Serikali ikipanga jambo lake na likiingizwa kwenye bajeti basi haliwezi kukwama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Madiwani walikuwa hawahitaji kulipwa ile pesa kwa wakati tu, bali walikuwa wanaomba waongezewe posho, kiukweli sisi wenyewe tunajua tukirudi kule majimboni tunakuwa sisi wenyewe ni madiwani, wananchi wote wakiwa na matatizo basi kabla hawajaenda sehemu yoyote basi wanamkimbilia Diwani, wanamkimbilia Mbunge, wanakimbilia sehemu zengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali. Kwa kuwa tulimebeba hili jukumu basi tuone namna gani ya kuwasaidi hawa Madiwani. Na pia tumepata changamoto nyengine, kuna muongozo ulikuja kule kuna Madiwani wamekuwa wakikatwa posho zao, leo tunakwenda kulalamika kumkata Diwani shilingi laki moja na ishirini eti kwa sababu anakaa Makao Makuu ya Halmashauri, hiyo imeleta changamoto sana, majukumu ya Diwani ni yale yale, ni sawa sawa na mbunge anaetoka Kongwa, anaetoka Bahi ukamkata usimlipe per diem, hiyo sasa siyo sawa kwa sababu wale wadiwani wanaposafiri kwenda pale wamebeba dhamana ya wananchi wao kutoka kwenye kata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali, tuwaangalie madiwani wanamajukumu makubwa sana kama tulivyo sisi, tunapokwenda kuwapunguzia posho zao. Kwanza posho ni ndogo, unaenda kupigana nae kwa shilingi laki moja, anafanya kazi kubwa, anapitisha mapato yote ambayo yanatekelezwa katika halmashauri. Kwa hiyo, niombe Serikali itusaidie hili nalo litoe muongozo, kwa sababu wamekuwa wakigombana na wakurugenzi, wakurugenzi wanaosimamia sheria, inakuwa imeleta tabu. Kwa hiyo, niiombe Serikali iweze kutusaidia katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lengine kuhusu tozo za simu. Serikali imekuja na nia njema sana katika kukusanya kodi kwa kupitia simu zetu, niiombe Serikali. tumekuwa tukifanya miamala tunalipa mara mbili mbili, leo ukitaka kutuma milioni moja kwanza wewe unaetuma unakatwa shilingi elfu nne, yaani unatuma kwa mtu akapate hela wanakatwa elfu nne, akifika tena yule mtu kabla hajaitoa anakatwa elfu nane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali kama mnataka kuitoza vizuri hii kodi, wale makampuni tunahitaji waendelee ku-survival katika ufanyaji wa biashara, basi kama inakatwa ile ya kutumia iwe ya Serikali, ile nyingine iwe ndio iwe makato ya kampuni na wale wengine watoa huduma, kwa sababu unakuta milioni kuituma na kuitoa zaidi ya shilingi 12,000. Serikali inaenda kupata haifiki hata elfu tatu, sasa zingine zote zinapotelea hewani hewani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niiombe Serikali. Tumekuja na mpango mzuri lakini kuna sehemu kuna linkage hasa hii mitandao ya simu, imekuwa kero kwa sababu wanaongeza tu yaani makato yamekuwa yanaongewa kiaina aina tu hata haieleweki. Leo wanakwambia kufikia 5599 ikifika tu na kamili ile wanaongeza tena 300 zaidi ya ile kilichokuwa. Kwa hiyo, niiombe Serikali iangalie hili suala, na ndio maana tulikuja hapa kwenye uchangiaji wa sekta ya mawasiliano, tulisema tuimarishe shuirika letu la TTCL, haya yote hayatokuwepo, lile shirika ni la Serikali asilimia mia moja, haya makampuni mengine yapo kibiashara na hii tukiimarisha shirika letu linaweza kutusaidia hata tozo zenyewe za makato yakapungua, watu wakapiga simu vizuri, Serikali ikapata fedha zake vizuri bila ya hata kulalamika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe Serikali, kwa kuwa imekuja na mpango huu mzuri tuangalie na sehemu zinapo-link haya matatizo yanayotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja, nakushkuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia angalau dakika tano nami nitoe mchango wangu katika Mpango huu wa Serikali. Awali ya yote nianze kumshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kupambana kuhakikisha wananchi wetu wanapata huduma nzuri. Fedha hizi zilizoletwa katika historia nilikuwa naona mikopo mingi inakwenda kwenye miradi ya Kitaifa, lakini mkopo huu umekwenda kuwagusa wananchi wa chini zaidi hasa wa vijijini. Tunamshukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi nyingi, tunakwenda kujenga madarasa, shule na mbiundombinu mbalimbali ya afya; lakini tujiandae na mambo mengine ambayo yatajitokeza hususan kwa watumishi wetu. Kwa hiyo, naiomba Serikali katika mpango wao ambao utakuja kwenye bajeti ijayo, iangalie namna gani ya kutusaidia kuongeza watumishi hasa katika Sekta ya Elimu. Madarasa ni mengi, idadi ya wanafunzi ni kubwa lakini idadi ya walimu ni ndogo. Kwa hiyo, naiomba Serikali ije na mpango huo wa kuweza kuongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye kuchangia Mpango. Serikali yetu katika Mpango wake ambao ulikuja mwaka 2020, wa miaka mitano, ilituelekeza itakwenda kujikita kwenye Sekta ya Kilimo, nami wananchi wangu wengi ni wakulima. Mpaka sasa hivi, Serikali imekaa kimya, haijatoa mwongozo wa nini kinakwenda kutokea juu ya ongezeko la bei ya mbolea. Tumekuwa na kigugumizi, hatujapata bei elekezi mbolea ni shilingi ngapi? Tunakwenda kwenye msimu ambapo mvua kwenye baadhi ya mikoa imeshaanza. Leo hii tunapokea simu kutoka kwa wananchi, wanauliza nini kilichotokea? Nasi hatuna majibu.

Naiomba Serikali isimame mbele, itoe mwelekeo na dira kwa wakulima kwa sababu msimu umeshaanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mbalimbali ya kuisaidia Sekta ya Kilimo, naishukuru Wizara ya Kilimo inaendelea kupambana, lakini kuna mpango walikujanao wa kuwakopesha wakulima matrekta. Katika mkoa wangu na Jimbo langu wapo wananchi ambao walikopa. Ile mikopo ilikuwa ni kichefuchefu. Yamekwenda matrekta hayalimi hata nusu eka kwa siku, lakini wamekwenda kukopeshwa, na wale waliowakopesha kupitia Wizara ya Kilimo hawafuatilii changamoto gani wanazozipata kwenye kukusanya madeni. Wamekwenda TAKUKURU, eti TAKUKURU wakakusanye madeni. Sijawaji kuona aliyekopesha ni mwingine, anayekwenda kukusanya ni chombo kingine cha Serikali tena kikubwa kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali, yale matrekta ambayo yalikuja kule, wananchi wameyapaki. Agizeni vyombo vyenu mkachunguze.

MWENYEKITI: Aina gani Mheshimiwa, hayo yanayolipa nusu eka kwa wiki.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, yanaitwa Ursus yametoka NDC. Yale matrekta nusu eka hayalimi. Kwa hiyo, naiomba Serikali, wananchi wangu wameyapaki, hawayatumii tena, wanahitaji wavunje mkataba. Wale jamaa wanapigiwa simu hawapokei. Nendeni mkachukue trekta zenu, mkataba uishe. TAKUKURU hawataki kuwaona huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ili tusaidie wakulima wetu katika maeneo yetu, lazima kama Serikali tuone namna gani ya kuweza kuwasaidia hususan kuwaletea zana bora za kilimo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niwe miongoni mwa watakaochangia katika uwakilishi wa Kamati hizi mbili; ya Miundombinu na Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza mimi nianze kwa kuwapongeza viongozi wote na Kamati zote mbili kwa kufanya kazi kubwa, hasa Wizara yetu ya Nishati na Madini, nina mambo mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza; Serikali Awamu ya Kwanza ilikuja hapa ikatuambia tuna upungufu wa mabwawa hayajajaa maji kwa hiyo tutakuwa na tatizo la umeme. Mwenyezi Mungu akashusha neema mvua zikaanza kunyesha. Wakati mvua zinanyesha wakabadilisha gia hewani wanafanya service ya mitambo siku kumi. Siku kumi zimekwisha lakini tatizo la upatikanaji wa umeme katika maeoneo yetu bado ni changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hayo kwa sababu watu tuliwapelekea umeme wakatoa zile mashine ambazo zilikuwa zinawasaidia kukoboa kwa njia ya mafuta. Unapokata umeme kwa wiki mbili au tatu unasababisha disaster kubwa sana katika maeneo yetu. Kwa hiyo mimi niiombe Serikali, kwenye hili hebu itusaidie. Wabunge wengi wametoa changamoto zao ikiwemo kuangalia namna bora ya kutatua hizi changamoto za ukatikaji wa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ninavyokwambia katika kata zangu zaidi ya sita katika jimbo langu hazina umeme, kila siku umeme unakatika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ulitupa matumaini kuwa kazi inafanyika na tunaiona, lakini ongeza spidi utusaidie hili tatizo la ukatikaji wa umeme lisiwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mmetuletea hapa bei ambazo Mheshimiwa Rais na Waziri naye ameanza kuzishughulikia, na wametuletea mwongozo kule ni vitu gani ambavyo vitasababisha wengine walipe 27,000 na wengine walipe 320,000. Mimi niiombe Serikali; wananchi wanaotumia umeme huu ni watu wa maisha ya chini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapompelekea umeme wa 320,000 wakati hata zile huduma za kuvuta umeme, yaani kununua vifaa vya wiring vya 200,000 vinawashinda, leo kweli tunakwenda kuwasaidia kwa kuwaongezea huduma ya kulipia nishati ya umeme ya 320,000? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhumuni la Serikali kwanza ni kutoa huduma kwa wananchi, siyo kufanya biashara kwa wananchi. Kwenye Kamati kule wametuletea TANESCO imepata faida. Sasa kama imeweza kupata faida kwa nini inashindwa kujiendesha? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe, hebu wakati wanaangalia changamoto ni nini ya kushindwa kujiendesha na waangalie watu gani ambao wanaweza kuwabana. Hatujakataa kwenye miji yetu mpandishe hizo tozo, lakini kwenye vijiji kule hali yetu ni mbaya. Kwa hiyo, mnatukataza watu wasijenge sekondari, mnatukataza watu wasijenge vituo vya afya, mnatukataza tusiwe na masoko wala huduma ambazo ni muhimu sana kwa maisha ya binadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la Serikali ni kukusanya mapato baadhi ya maeneo, lakini kwenye hili hebu wajaribu kuliangalia. Hamuwezi kwenda kutuongezea gharama ya kulipa umeme. Wiring tu zenyewe wananchi zinawashinda. Maeneo mengi tumepeleka umeme kwenye vijiji, nyumba zilizounganishwa hazifiki hata asilimia 50, leo mnakwenda kuongeza gharama. Kwenye hili mimi niiombe Serikali ije na njia nyingine ya kuona namna gani tunaweza kuongeza huduma hii ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapeleka umeme wa REA kwenye vijiji. Tumejipanga na hii taharuki ambayo itakuja kujitokeza? Lazima tuwe na mbinu nyingine. Leo unapeleka kilometa 200 kutoka Makao Makuu ya TANESCO; je, ikitokea hitilafu ya umeme kule kuna mafundi, kuna wataalam? Sasa kuliko kupeleka umeme kule ikatokea shoti mnashindwa kuitafuta shoti imetokea wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo lengo la Serikali ni kupeleka umeme kwa kila kijiji lakini iangalie namna gani ya kusaidia isije ikatokea giza siku moja kwenye hii nchi kwa sababu ya ukosefu wa miundombinu kuwa bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikushukuru sana, niunge mkono hoja za Kamati. Nakushukuru sana kwa nafasi; ahsante.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nami niungane na Wabunge wote kukupongeza kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi kuwa Spika wa Bunge letu, nasi kama Wabunge tupo tayari kukupa ushirikiano wa asilimia mia moja. Ondoa shaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi zote hizi, nirudie maneno yako ambayo nilikunukuu siku umekalia Kiti hicho kwa mara ya kwanza. Ulisema, sisi Wabunge ni daraja kati ya wananchi na Serikali. Tunapokuja humu, tumeleta mawazo ya Watanzania zaidi ya milioni 60 kwenda 70 waliopo nje. Tunayaleta matatizo katika Serikali yetu. Nami niseme, nina imani nawe, ninaamini kwenye daraja hili utakuwa kiungo kizuri cha kuweza kutufikishia maendeleo kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakuna asiyejua kwamba lengo la kuja humu kusema ni kuishauri Serikali na Serikali kupokea mawazo yetu. Leo tunaposema huko nje Watanzania wote wanafahamu tuna changamoto kubwa ya ukatikaji wa umeme, hakuna asiyejua. Kila mahali umeme ni changamoto. Kwa hiyo, tunapokuja humu kuishauri Serikali, basi isitokee mtu akaona kama tunamwonea, hapana. Tunatoa tu maelekezo ayafuate mawazo yetu ili tukatatue tatizo na kuwasaidia wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, nimeanzia hapo kwa sababu gani; leo tumekuja hapa kuchangia ripoti ya kamati mbili za PAC na LAAC. TANESCO wana matatizo makubwa sana, leo tukisema TANESCO kwenye ripoti ya CAG inasema imetengeneza faida mwaka 2019/2020 walitengeneza faida ya bilioni 45, kama waliweza kutengeneza faida kwa nini bado kuna changamoto?

Mheshimiwa Spika, nimnukuu Mheshimiwa Waziri alisema hapa, tuna matatizo mengi. Mchangiaji mmoja hapa amesema ukiangalia assets na madeni ya TANESCO ukiyalinganisha hakuna TANESCO. Kwa hiyo, tumekuja kutoa changamoto zilizoko katika Shirika letu la TANESCO watusikilize na changamoto ni kuipitia hii Ripoti ya CAG itawaonesha nini changamoto inayoikabili TANESCO kuliko kuanza kukimbia. Kama hukunitaka kwa nini unataka nini?

Mheshimiwa Spika, hakuna mtu ambaye anataka cheo cha mwenzake hapa. Kwa hiyo, tunapokuja humu tunaleta mawazo ya wananchi. Tunapokuja humu tunaishauri Serikali iende ikafanyie kazi. Kwa hiyo, nilitaka niseme TANESCO bado changamoto ipo na tusipokwenda vizuri bado tutaendelea kuwa na changamoto.

Mheshimiwa Spika, CAG amebainisha baadhi ya changamoto, lakini sasa ukija kuangalia inawezekana wamepikapika tu hesabu kuonesha wana faida, ili waturidhishe watanzania, lakini hakuna kinachoendelea katika shirika letu ndio maana hata wanaongeza gharama za kuunganisha umeme. Kwa hiyo, Serikali ichukue hatua ikiwemo kusikiliza na kufuatilia nini CAG aliandika.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto za TANESCO, lakini kumekuwa na changamoto kubwa sana. Wote sisi Wabunge kuna miradi inayoendelea ya REA, hii miradi inayoendelea ya REA fedha zinazotumika ni za watanzania wote, tumeongeza fedha kwenye tozo za mafuta kwa lengo la kufikisha huduma za umeme katika vijiji vyetu.

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Venant Daudi, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Sophia Mwakagenda.

T A A R I F A

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, nataka nimpe Taarifa mchangiaji anayechangia sasa kwamba, anatoa mchango mzuri sana unaohusu nishati, lakini hapo najua ni hoja ya kamati, lakini Waziri wa Nishati wala Naibu wake hayupo. Kwa hiyo, wakati unachangia ufahamu hilo, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge nilishawahi kutoa ufafanuzi huko nyuma, nirudie tena; Serikali iko Bungeni. Serikali iko Bungeni na kwa kuwa, Serikali iko Bungeni tusiwe na wasiwasi mawazo yetu tunayoyatoa yote yanapokelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Venant Daudi malizia mchango wako.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, nikushukuru, ninafahamu watapitia hata kumbukumbu za Bunge, watayakuta haya.

Mheshimiwa Spika, kuna kiradi inayoendelea katika maeneo yetu, miradi hii gharama inayotumika au fedha zinazotumika ni za watanzania. Leo, kama kamati, tulikwenda kutembelea miradi mitatu katika mikoa mbalimbali, tuliyoyakuta huko Mungu atusaidie.

Mheshimiwa Spika, tumekwenda kukuta mkataba unasainiwa, labda mradi utatekelezwa kwa bilioni 30, wamefanya tathmini TANESCO, anakuja REA anabadilisha tena anasema mlikosea kufanya tathmini nitatekeleza kwa bilioni 37, inaongezeka bilioni saba zaidi ya asilimia 20. Kama yule wa kwanza alibaini biloni 30 kwa nini huyu anakuja miezi mitatu baadaye bilioni saba zaidi?

Mheshimiwa Spika, mimi nikuombe, dakika moja kwa kumalizia, nikuombe kupitia Bunge lako iundwe kamati maalum ambayo itakwenda kuchunguza miradi ya REA tangu tumeanza na ilete ripoti katika Bunge lako tukufu. Ahsante nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili kuwa mmoja wa wachangiaji katika hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Awali ya yote, nianze kwa kuipongeza Serikali inayoongozwa na Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa inayoendelea kuifanya katika maeneo yetu na katika majimbo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepata fedha nyingi ambazo kila jimbo, kila kata na kila kijiji kuna miradi inayoendelea chini ya Serikali yetu ya Chama Cha Mapinduzi. Katika Jimbo langu la Igalula juzi tu nimepokea fedha za kwenda kujenga Vituo vya Afya vya Tula na Kata ya Loya ambavyo wananchi hawa hawakuwa kabisa kwenye mafikirio ya kupata huduma bora ya afya, kwa hiyo sina budi kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Igalula kufikisha salamu zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakwenda kujadili hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo ameiwasilisha hapa yenye mambo mengi ambayo yatakwenda kusaidia wananchi wetu katika majimbo yetu. Kazi yetu sisi Wabunge ni kuishauri na kuisimamia Serikali pindi inapofanya vizuri lazima tuipongeze lakini pindi ambapo wanaenda ndivyo sivyo lazima tuwape ushauri ili waweze kwenda kwenye mstari. Jukumu la kuleta maendeleo ni la sisi sote wala siyo Serikali peke yake na ndiyo maana kuna miradi ambayo wananchi wao wenyewe wanaanza kwa kujenga na baadaye Serikali inaiunga mkono. Kwa hiyo Serikali ina jukumu la kuwaletea maendeleo lakini na sisi wenyewe kama wananchi tuna jukumu la kusaidiana na Serikali kuleta maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nishauri kwenye mambo machache. Jambo la kwanza tumekuwa na miradi mingi sana ambayo ipo katika maeneo hasa miradi ya maji, tunaiomba Serikali sasa ifike mwisho miradi hii iwe inafika mwisho kuliko kuwa tunaenda vipande vipande na baadaye haileti tija. Kwa mfano, mimi nina mradi wa tangu mwaka 2019 wa kutanua maji ya Ziwa Victoria ambao umeanza kuongelewa toka mwaka 2019 katika Kata za Goweko, Igagula, Nsololo na Kigwa, lakini mpaka leo mradi huu unakwenda taratibu. Kwa hiyo, naiomba Serikali kupitia bajeti hii basi tutenge fedha ambayo tutakwenda kumaliza mradi huu ambao tumekadiria wananchi zaidi ya 150,000 watanufaika na vijiji zaidi ya ishirini watanufaika na upatikanaji wa maji haya. Kwa hiyo, niiombe Serikali twende tukamalize changamoto hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, wote ni mashahidi tulipokea fedha ambazo Mheshimiwa Rais alikwenda kuzitafuta kule na zikaenda kila mkoa, kila jimbo. Fedha hizo zimeenda kutekeleza miradi mbalimbali, lakini kuna baadhi ya maeneo ambayo fedha hiyo ipo lakini bado haijaanza kutelekeza miradi hiyo. Kwa mfano, katika jimbo langu tulipewa bilioni moja na milioni mia tano kwenda kutekeleza barabara tatu katika kata tatu tofauti tofauti; kuna barabara ya kutoka Izumba kupitia Idekamizo mpaka Simbojigulu mkandarasi amesaini mkataba lakini mpaka leo hajaanza kazi. Vilevile kuna barabara zingine wakandarasi wapo site lakini hawafanyi kazi kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa jukumu la kuleta maendeleo ni letu sote ni kuikumbusha Serikali iweze kuongeza speed governor ya kuwasimamia vizuri wakandarasi hawa basi wamalize kazi na makusudio ya Mheshimiwa Rais kuwasaidia wananchi kufungua mitandao ya barabara yaweze kutimia.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo lakini wananchi wa Jimbo la Igalula walinituma; wana changamoto kubwa Serikali ilitoa maelekezo ya upandaji wa uunganishaji wa nishati ya umeme, wakasema zaidi kwamba kutoka shilingi 27,000 mpaka shilingi 320,000; Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuwa wewe ndiye baba wa Wizara zote niiombe kupitia Wizara ya Nishati iweze kuangalia kuna maeneo mengine wameyapandisha kimakosa wananchi sasa wameshindwa hata kuendeleza kupata huduma ambayo Serikali ilikusudia kuwafikishia hasa katika Kata ya Goweko Kijiji cha Goweko wamekipandisha hadhi ya kutoka shilingi 27,000 kwenda shilingi 320,000. Kata ya Kigwa, Kijiji cha Kigwa wamekipandisha hadhi kutoka shilingi 27,000 mpaka shilingi 320,000; vilevile Kata ya Igalula na kwingineko katika Jimbo la Igalula.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali, kama mnaona hii miji imekuwa kwa sababu wananchi wanapenda maendeleo na sisi Serikali kazi yetu ni kuwasaidia wananchi yale maendeleo yao yasiweze kuwaponyoka katika mikono yao, tusiende kuwavuna sana. Niiombe Serikali iweze kuangalia ni namna gani ya kuwasaidia angalau kushusha kufikia hata nusu au robo ya gharama hizo ilimradi wananchi wengi wapate huduma na sababu Serikali kusudio lake si kufanya biashara ni kufikisha huduma kwa wananchi niiombe Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na pongezi hizo sasa nirudi kwenye michango na mijadala ambayo ipo katika nchi yetu kwa sasa. Kila Mbunge humu nadhani kama alifanya mikutano wiki mbili au tatu zilizopita, wamekutana na maswali mengi kwa wananchi wao hasa mfumuko wa upandaji wa bei. Bado Serikali ina haja ya kuliangalia hili suala kwa umakini mfumuko huu wa bei watu wamechukua advantage kwa sababu wamekwisha ona na sisi watu wa Serikali tumeanza kulalamika kuwa kuna hiki kimesababisha mfumuko wa bei, lakini kuna bidhaa ambazo hazihitaji kabisa kupandishwa bei, lakini wananchi au wafanyabiashara wameona wapitie humo humo kwa sababu na sisi kama Serikali tumeanza kulalamika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, leo tuna bidhaa ambazo tunazizalisha humu, zimepanda mara mbili kwa kile ambacho tulichokuwa tunakizania. Kwa hiyo kuna haja kama Serikali kuangalia huu mfumuko wa bei, tusiruhusu sasa wafanyabiashara wakaanza kupitisha mambo yao ambayo yanakwenda kuwaumiza wananchi ninyi wote ni mashahidi wakati tumeingiza fedha za UVIKO ziliingia katika majimbo yetu, miradi mingi ikaenda kutekelezwa kule tulikuwa tuna janga la COVID-19 ilikuwa ikiendelea katika nchi yetu, lakini mfahamu baada ya fedha kupatikana wafanyabiashara walichukua fursa hiyo ya fedha nyingi zimeletwa na Mheshimiwa Rais wakapandisha vifaa vya ujenzi mara mbili tofauti na awali walivyokuwa wanauza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ilipanda cement kutoka shilingi 19,000 mpaka tukaenda shilingi 24,000 mpaka shilingi 26,000 katika baadhi ya maeneo, lakini leo ninavyokuambia cement imeshuka na vita ya Ukraine inaendelea, imeshuka mpaka shilingi 18,500. sasa najiuliza kwa nini wakati ule fedha zilizopatikana walipandisha saizi wameshusha kitu gani kilichosababisha kushusha wakati nchi sasa hivi tunasema tupo kwenye janga kubwa la vita ya wenzetu kule Ukraine na Urusi, lakini bidhaa hii imeshuka. Vilevile Waziri wa Viwanda na Biashara yupo, hakuna majibu ambayo tuliyatoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunaishauri Serikali, iangalie huu mfumuko wa bei umetokana na nini? Mfumuko wa bei ni halali kweli bei kupanda maana sasa hivi bajaji au bodaboda tulikuwa tunaenda kwa sh.1,000 imekuwa Sh.3,000 imepanda kwa asilimia 200. Je, yale mahitaji yamepanda kwa asilimia hizo? Nauli za mabasi sehemu ya Sh.15,000 imekwenda mpaka Sh.25,000 au Sh.30,000, uhalisia wa upandaji wa gharama za uendeshaji na uhalisia wa upandaji ambao wanatozwa wananchi wetu hauendani. Kama Serikali tuone ni namna gani ya kuboresha katika suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo mijadala ambayo inaendelea na nataka nigusie na Serikali itusaidie, tunapoleta humu changamoto tunahitaji tuweze kutengeneza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niwe miongoni mwa wachangiaji katika Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumekuja hapa leo kujadili ripoti tatu mbazo zote zinahusu usimamizi wa fedha za walipa kodi. Sisi kama Bunge anayetusaidia kwenda kwenye ukaguzi kwenye taasisi zetu na mashirika na halmashauri zetu zote nchini ni CAG ambaye kwa mujibu wa Katiba tumempa mamlaka hiyo kama Bunge, lakini na sisi Bunge tuna haki ya kuhoji na kuisimamia Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumesimama hapa kama Wabunge kwa Kanuni mbalimbali za Bunge na sisi hapa tupo kwa niaba ya wananchi wa Tanzania nzima, kwa hiyo tunapoleta maoni yetu hapa si maoni ya sisi kama Wabunge tulipo huku ndani, ni maoni ya wananchi waliotutuma kuja kuwawakilisha. Kwa hiyo, tunaposema ubadhilifu wa fedha zinazotokea katika Serikali, mambo hayaendi sawa katika Serikali, si kama sisi Wabunge ndio tunayasema ni wananchi wanasema mambo hayaendi sawa. kwa hiyo tunaomba tueleweke kwa namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika ripoti zote za CAG kila mwaka tunapokuja hapa, hata hizi ripoti za Kamati za Fedha, hatuwezi kwenda hata siku moja tukasema Serikali hakuna sehemu ambapo tumepoteza au tumepata hasara. Kila siku tunapata hasara na hasara kila siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi katika mchango wangu nataka tuishauri Serikali; tuna miradi mikubwa ambayo Serikali inatafuta fedha, tuna Mradi mkubwa wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambao tunaweka matrilioni ya fedha, tuna mradi mkubwa wa SGR. Kama tusipoweka mipango madhubuti ya usimamizi wa fedha hata hizi fedha tutakuja tutakaguliwa tena tutaambiwa zimepigwa na bado Watanzania wataendelea kuumia. Katika ripoti ya CAG ambayo leo tumekuja kuijadili hapa, kuna changamoto kubwa ya riba ambazo tunalipa kwa wakandarasi; na hii yote inasababishwa na uzembe wa watumishi wetu katika Wizara na taasisi mbali mbali. Sasa wewe unakuta mkandarasi una mcheleweshea malipo mpaka siku 205, halafu tunakwenda kulipa the deference ya riba ya zaidi ya bilioni 11 halafu bado watu tunakuja hapa, mnasema kama hatuwezi tujadili masuala ya uganga wa kienyeji, tukae kimya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi niwaombe Waheshimiwa Wabunge kama tusipojisimamia sisi wenyewe kuna siku hapa mtakuja mtukanwe na bado mtapiga makofi. Kwa hiyo, mimi niwaombe tunapokwenda kuishauri Serikali si kwa nia mbaya ni kuisaidia Serikali iweze kufanya kazi. Sasa waganga wa kienyeji tupo, sasa tunawapa mkeka. Wizara ya Fedha, hizi variations zote ambazo tunazisema; wakandarasi kulipwa kwa kuchelewa, tunakwenda kulipa fedha nyingi, zote zinasababishwa na Wizara ya Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia TAA tu, nilikuwa napitia hapa ripoti ya CAG, kuna mkandarasi ambaye alipewa kutengeneza mitambo na mfumo katika Uwanja wa Julius Kambarage Nyerere. Alicheleweshewa malipo zaidi ya siku 216 tukalipa zaidi ya bilioni 13, tukijadili hapa tena unaambiwa kazi yetu kujadili waganga wa kienyeji. Bilioni 11 imekwenda lakini waliochelewesha ni Watumishi wa Wizara ya Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini palikuwa na ukarabati wa Uwanja wa Ndege wa Mwanza, mkandarasi amecheleweshewa malipo tukalipa bilioni 2.5, Wizara ya Fedha, lakini vile vile palikuwa na ucheleweshaji wa msamaha wa kodi ambapo kontena 223 zilikaa bandarini pale tukalipa tena mkandarasi delay ya kucheleweshewa msamaha wa kodi, zaidi ya bilioni 11. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatujawahi kusema shilingi 10,000 shilingi 100,000 kila siku tunazungumzia mabilioni. Ni lini tutashuka kutoka kwenye bilioni kuja kwenye mamilioni, tuje kwenye maelfu?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tuna miradi mikubwa ambayo tunaenda nayo, Mama yetu anajitahidi kuhakikisha miradi iliyoachwa inaendelea na inakamilika na imaleta tija. Kwa stahili hii miradi, tumekadiria Bwawa la Mwalimu Nyerere liishe kwa trilioni 6.5 ngapi huko litaisha kwa trilioni 8. Kama tusipodhibiti mapema kuzuia waganga wa kienyeji kudhibiti hizi fedha; kama mradi wa SGR tumehakikisha tutumie trilioni kumi na ngapi sasa zitaisha kwa zaidi ya trilioni 40. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niiombe Serikali, tunapokuja humu kuishauri Serikali watusikilize, ndiyo kazi yetu. Wananchi walijipanga mstari kwachagua wabunge kwa niaba yao kwenda kuwasemea. Sasa wanatozwa tozo wanavumilia. Hizo tozo ambazo wanajibana na familia zao leo tena zinakuja kuibiwa huku, eti sisi tuwe tumekaa. Sasa tuna maana gani ya kukaa kama Bunge? Basi ijulikane kuna mihimili miwili, Mahakama na Serikali, kazi iendelee, sie tukalime, Wizara imeongezewa bajeti ya kilimo, tukaongeze mashamba, uzalishaji watu wa mjini waje wapate…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi kunipa nafasi hii ya kuwa mmoja wa mchangiaji katika wizara hii muhimu ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa jitihada zake za makusudi za kwenda kutatua changamoto za maji katika nchi yetu ya Tanzania na majimbo yote ya Tanzania likiwemo Jimbo langu la Igalula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo nimshukuru na nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa jitihada na kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya. Shukrani hizi zienda kwenye Wizara nzima ya Maji, Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu; kiukweli mimi wamekuwa wakinipa ushirikiano mkubwa pindi ninapopata changamoto kwenye miradi yangu ambayo nitaitaja hapo baadaye. Nikiwa nawakimbilia basi wao wananipa ushirikiano na changamoto hizo kuzitatua. Mimi niwashukuru sana, endeleeni kutulea na endeleeni kutusikiliza kwa sababu sisi tumeletwa hapa kwa nia ya kuwatetea wananchi na wananchi tukileta shida zao kwenu na nyie mnazitatua kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani hizo ngazi ya Wizara pia niwashukuru viongozi ambao wao wanawasaidia kutatua changamoto katika mikoa yetu na wilaya. Nimshukuru Meneja wa RUWASA mkoa wetu wa Tabora Ndugu Kapufi, anafanya kazi nzuri sana na ndio maana mkoa wetu umeheshimika kwa kuwa wa kwanza kitaifa kwa kutoa huduma bora ya maji.

Nimshukuru Meneja wetu wa Wilaya Mr. Shibiki, kiukweli anafanya kazi kubwa sana. Kuna kipindi Mheshimiwa Waziri nilikuwa meneja huyu amekosa usafiri lakini kwake usafiri haukuwa kigezo kutokufika site, alikuwa anatuma mpaka bodaboda ili aweze kwenda kutatua na kusikiliza kero ambazo zilikuwa zinawakabili wananchi. Nilikuja kwako na umeshanipa ahadi yakuniletea gari basi ninaami akipata gari changamoto zote za maji katika jimbo langu litakuwa limetatulika kwa asilimia kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninayo mambo machache sana nimempongeza Mheshimiwa Waziri na niendelee kukuomba tena. Tarehe 29 mwaka 2021 niliuliza hapa swali la msingi kuhusu Wizara ya Maji, niliuliza kuhusu Mradi wa Ziwa Victoria ambao unaendelea katika Jimbo la Igalula ambapo utatatua changamoto katika kata nne za Goweko, Igalula, Kigwa na Nsololo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri kupitia majibu yako, na siku hiyo Mheshimiwa Naibu Waziri hakuwepo, ulijibu wewe mwenyewe Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Wizara ya Maji; uliniambia mradi huu utakwenda kukamilika kabla ya mwaka wa fedha 2022 kuisha. Leo tumebakiza siku kama arobaini na tano mwaka wa fedha uishe lakini mradi ule huko katika asilimia thelathini kwenda arobaini, na haujafika zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimuombe Mheshimiwa Waziri; lengo la huduma na limeshaonyesha dhamira kwa sababu mradi huu umeanza; na juzi hapa Mheshimiwa Mkuu wetu wa Mkoa alikuja na viongozi wa chama tukaja ofisini kwako tukafanya kikao na wataalam. Kulikuwa changamoto ya ulipaji baadhi ya certificate. Siku ileile ulitoa maelekezo na certificate zililipwa na yule mkandarasi alileta mabomba yako site.

Mheshimiwa Mwenyekiti, palikuwa na changamoto ya mkandarasi wa kuchimba msingi kwa sababu ya masika. Sasa, masika imekwisha na sasa mmuagize arudi site aendelee na kazi ili kuwafikishia maji wananchi wa Jimbo la Igalula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe jambo lingine Mheshimiwa Waziri. Hii mikataba ambayo wanatuletea kule inakuwa na mkanganyiko mkubwa sana. Unakuta mtekelezaji ni RUWASA kule ngazi ya wilaya lakini anayetumika kununua mabomba ni anatoka Makao Makuu yani Wizarani sasa mnakuwa mtu wa wizara atambui umuhimu wa adha anayoipata kule Meneja wa RUWASA wa wilaya na wa mikoa. Sasa ninyi mna-relax kwa sababu ya ucheleweshaji wa kulipa certificate hasa ususani wa supply ya vifaa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimuombe Mheshimiwa Waziri, kwenye mradi wangu aliniahidi ataenda kuongea na supplier alete mabomba yote lakini jambo lile bado halijafanyika. Nimbuombe atakapopata muda amuite supplier huyo alete, na asianze kutupa vigezo, kwamba akifikisha kilometa haleti vifaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo lingine, Mheshimiwa Waziri tuna mradi ambao wewe ulikuwaga Naibu Waziri wakati huo waziri Professor Mbalawa mlikuja katika Kata ya Tura pale mwaka 2019 mkaahidi kwamba ku- supply katika Mji wa Tura utakamilika baada ya miezi mitatu. Tangu mwaka 2019 mpaka leo ule mradi haujakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini changamoto si mameneja wangu wa Wilaya na Mkoa, changamoto iko katika hatua ya manunuzi ngazi ya Taifa. Niombe Mheshimiwa Mheshimiwa Waziri waendeni wakatatue changamoto hii. Wananchi kila siku nikienda kule wananiuliza ni lini sasa kitendawili naomba ukakitatue ili waweze kupata maji katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la tatu ambalo nilitaka nishauri, na niombe Mheshimiwa Waziri mwaka jana aliniahidi kuwa usanifu wa bwawa la Kizengi umekamilika, lakini kwenye bajeti hii nimefungua vifungu vyote na majedwali yote sijaona amelipangia fedha. Nimuombe Mheshimiwa Waziri, Jimbo la Igalula lina changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa maji. Nishukuru kwenye fedha za UVIKO nilipata milioni 505 ambazo zitawezesha kuchimbwa visima 15; lakini kwa takwimu mpaka sasa hivi vimechimbwa visima sita ambapo katika Vijiji vya Kalangatu, Mwisolo pamoja na Isaga wamechimba wamekosa. Ni vijiji vitatu tu ambako wamechimba maji wamepata ambavyo ni Vijiji vya Kalangale, Mwamabondo na Mwamdalaigo, wamechimba maji wamepata lakini si mengi sana. Kwa hiyo ukiangalia jiografia ya Jimbo la Igalula maji ya visima si muhimu sana. Ili kutatua changamoto hizo ni kuwepo kwa upatikanaji wa maji ya mabwawa. Nimuombe; kwenye Bwawa la Kizenji usanifu umekamilika; sasa anipelekee fedha ili zikatatue asilimia zaidi ya 80 ya upatikanaji wa maji kwa wananchi wa Jimbo la Igalula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru juzi ameniletea wasanifu wengine waliokwenda kufanya usanifu kwa ajili ya kujenga Bwawa katika Kata ya Miswaki. Hata hivyo solution ya Jimbo la Igalula ni kuniletea mabwawa na si visima. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri pamoja na jitihada kubwa unazozifanya za kumsaidia Mheshimiwa Rais za kuweza kwenda kutatua changamoto ya maji miradi iliyoanzishwa awali naomba iende ikakamilike kwenye mwaka huu wa fedha ili, wananchi wetu waone yale maneno wanayosema Mheshimiwa Rais akiwa kwenye majukwaa na mikoa mbalimbali basi yawafikie wananchi wetu wa Jimbo la Igalula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba niunge mkono hoja na niwapongeze wizara iendelee kufanya kazi nzuri. Ahsanteni sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi kuwa mmoja wa wachangiaji katika ofisi ya Waziri Mkuu katika bajeti ya mwaka 2023/2024.

Kwanza mimi niwaombe Waheshimiwa Mawaziri, mna muda mzuri sana wa kujibu hoja za Wabunge, kwa hiyo tupunguze miongozo. Tumekuja humu kuleta kero na matatizo ya wananchi na ninyi kazi yenu ni kutatua kero na matatizo ya wananchi tunawategemea katika hilo, sasa anaposema Mbunge na nanyi mnanyanyuka mnakuwa mnatuingilia Hansard hazikai sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze kwa mchango wangu nategemea mimi sipati mwongozo mpaka namaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kupongeza Serikali kwa kazi nzuri inayoifanya kwa kuwahakikishia wananchi kuwaletea maendelea. Leo tunapozungumza hapa ukiangalia Serikali zote zilizo pita Serikali ya Awamu ya Sita imevunja rekodi kwa kuleta maendeleo chapu chapu; na sisi viongozi au Wabunge wapya tulioingia mwaka huu tumepata mserereko mkubwa sana, kwa sababu kila kitu tulichokisema kimekwenda. Uiangalia jimbo langu ahadi zote tumemaliza isipokuwa kuna ahadi chache chache tu, na hizo ahadi itabidi niziseme leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kupongeza Serikali, kwanza mimi nishukuru Serikali, tuna mradi mkubwa wa SGR ambapo takriban asilimia 70 au 80 ya Mradi wa Makotopora - Tabora umepita Jimbo la Igalula; hapa ninaombi kidogo kwa Mheshimiwa Waziri Mbalawa. Kuna wananchi ambao reli imewafuata na kuna wanachi ambao wameifuata. Mimi nikuombe, wale wananchi ambao waliifuata reli, wakazi wa kata ya Nsololo na mmoja ambaye ana athirika kwa kubomolewa nyumba yake anataka asilipwe alikuwa mgombea mwenzangu, wa Ubunge wa ACT. Kwa kuwa Mheshimiwa Rais ameweka maridhiano, mimi naomba, kwa sababu wale watu walijenga zaidi ya miaka 20,30 iliyopita basi muwafikirie kuwalipa hata fidia kidogo, basi msiwabomolee na kuwaacha hivyo hivyo. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri Mbalawa katika bajeti hii hao wananchi 20 ambao hawajaingizwa kwenye fidia naomba waingizwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema hapa Mheshimiwa Rais amefanya kazi nzuri na yenye mfano katika vipindi vyote vya marais. Na mimi nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu; anazunguka nchi hii kwenda kuwatia matumaini wananchi kwa kile kinachofanywa na Serikali; na Mheshimiwa Waziri Mkuu inawezekana kuna muda unapiga kazi mpaka watu wanakuhisi hisi mimi nikuhakikishie piga kazi na sisi kama wawakilishi wa wananchi tuko nyuma yako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sisi wawakilishi wa wananchi; ndio hicho nilichosema wananchi mnatakiwa mtujibu hoja, tunapokuja humu tunawaambia Mawaziri kuna changamoto katika majimbo yetu, Waziri anakuahidi tunakwenda jimboni kwa lengo la kwenda kutatua kero na sio kuongeza kero nyingine. Hii lazima tuikemee. Kumekuwa na Waziri tunakwenda nao kwenye majimbo wanakwenda kutuletea matatizo badala ya kutatua matatizo. Wanakwenda kuahidi vitu ambavyo haviwezi kutekelezeka, mnatuachia kero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mimi nina ahadi za tangu Mbunge Mfutakamba Jimbo la Igalula hamjapeleka, akaja Musa Ntimizi hamjapeleka, nimekuja mimi mmenipiga fiksi tena, nimekaribia kumaliza muda wangu hamtapeleka. Mimi niwaombe kama kitu hakiwezekani tusiwalaghai wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema hivi kwa sababu Mheshimiwa Jafo alikwenda mwaka 2019 katika Kata ya Igalula akawaambia wananchi; yaani mimi nikienda tu Dar es Salaam hii wodi yenu nitaimaliza nitaleta shilingi milioni 80, mpaka leo milioni 80 haijaenda; mpaka Jafo amehama Wizara sijui nane sijui ngapi, mpaka leo. Sasa wa kumdai ni nani? Ni akina nani wanao ratibu ahadi za viongozi? Sasa ninyi mnakwenda na msafara mkubwa halafu hamfanyi chochote; sasa mna maana gani ya Kwenda? Mheshimiwa Waziri Mkuu nimekusifia hapa lakini na wewe uliacha deni huko. Kuna shilingi milioni 80 katika Kijiji cha Imalakaseko, ulikwenda na jiwe lako la kumbukumbu liko pale, haijaenda tangu mwaka 2017. Ulikuja na msafara, una Katibu na nani, Dereva, nani mpaka leo haijaenda; sasa walienda kufanya nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunaomba ili tuwape hadhi viongozi wetu wa kitaifa wanapokuja kwenye majimbo yetu msituletee matatizo mengine. Sasa wanakuja kutuambia wewe Mbunge tulikwambia upeleke kero yetu.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. VENANT D. PROTAS: Nani tena huyo?

MWENYEKITI: Mheshimiwa Venance kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Maganga.

T A A R I F A

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa, kwamba mchango wake ni mzuri sana, kweli anaongea vya ukweli kabisa. Ni kweli, unaweza ukapata wageni lakini baadaye wakakuletea matatizo makubwa. Kwa hiyo naomba Serikali ichukue mchango wake maana yapo majimbo mengi viongozi wakiwemo mawaziri wameingia kwenye majimbo yetu na kutuachia ahadi na hazitekelezeki.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Maganga, ahsante. Mheshimiwa Venant taarifa unaipokea?

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa ninaipokea, ndiyo haya matatizo ambayo tunayazungumza. Halafu mbaya zaidi mnampiga fiksi mpaka kiongozi wa Kitaifa. Mheshimiwa Rais alikuja ziara mwaka jana katika Mkoa wetu wa Tabora, alisimama katika Kata ya Kigwa. Mimi mwakilishi wao nikamwambia Mheshimiwa Rais tuna changamoto ya umaliziaji wa maji ya Ziwa Victoria katika kata ya Gowekwe, Igalula na Nsololo na Kigwa akamsimamisha Mheshimiwa Waziri wa Maji. Waziri akaniambia Mheshimiwa Rais hilo limeisha, mwezi wa 12 Maji watayapata hapa; mpaka leo hata dalili hakuna. Sasa wananchi wanachanganyikiwa sasa mpaka Rais anapigwa fiksi sasa sisi ni akina nani, sasa Mwenyekiti…

MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Athuman Almas Maige.

T A A R I F A

MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, hili analoliongelea pacha wangu wa Igalula nami nililiongelea. Marais watatu wana ahadi ya kituo cha afya Uyuwi, Tabora Kaskazini, mpaka leo mwaka wa tano.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Venant, taariifa hiyo unaipokea.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea hiyo taarifa. Kwa hiyo CAG anapokagua fedha kupotea hata hizi ahadi akague. Awakague viongozi ambao wanachimba mashimo kwa wananchi ili sasa tuwe na Serikali ambayo ni yenye matumaini kwa wananchi na si Serikali yenye mashaka kwa wananchi. Kwa hiyo mimi nilitaka nichangie katika hoja hiyo ahadi za viongozi zifuatiliwe.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Venant, ahsante muda wako umeisha.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kengele ya kwanza, au imeisha hiyo?

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umeisha.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya, naunga mkono hoja.(Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na kuwa mmoja katika wa wachangiaji katika Wizara hii ya kilimo. Kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja na pili niipongeze Serikali na nimpongeze Waziri kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya kuwatetea wakulima wa nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajielekeza katika mambo manne, jambo la kwanza pongezi nimeshawapongeza Serikali na Wizara. Jambo la pili nitaelekeza maombi matatu. Jambo la tatu nitajielekeza kwenye ushauri na jambo la nne sintofahamu ambayo inaendelea kwangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza nimwombe Mheshimiwa Waziri, nimeona bajeti ya mwaka jana aliandika skimu za umwagiliaji. Nimshukuru kwangu uliniletea bwawa la bilioni sita Kata ya Goweko, lakini mpaka sasa hivi nimpe taarifa liko asilimia 15 na wanatakiwa kukabidhi mwezi Septemba. Kwa hiyo, nimwombe alisukume hili bwawa liweze kukamilika kwa wakati na upembuzi yakinifu wa mashamba uweze kufanyika, ili sasa kwenye msimu huu tuweze kuanza kuzalisha kupitia Bwawa letu la Goewko. Mwaka jana aliniwekea Skimu ya Umwagiliaji ya Mwamabondo na mwaka huu amenirudishia Mwamabondo Loya. Naomba hii skimu sasa Waziri aitengee fedha iende ikajengwe kwa sababu wananchi wa Loya wananiuliza kila siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nimeona hapa mpango wa kuchimba mabwawa mapya. Wilaya ya Uyui tuna majimbo mawili, uko mpango wa kuchimba bwawa kule Majengo, Tabora Kaskazini. Niombe wataalam wa umwagiliaji waende Kata ya Igalula, kule waonane na Mheshimiwa Diwani Hussein Simba, basi kuna sehemu nzuri ambayo wanaweza kuchimba bwawa na likaleta tija kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa pili, Mheshimiwa Waziri anafahamu wakulima wengi sasa hivi wanategemea mbolea. Palikuwa na changamoto kubwa ya upatikanaji wa mbolea hasa katika vituo vya upatikanaji wa mbolea. Mtu wa kutoka Makoesengi, Mmale, Lutende, Mwamabondo, kwenda kuifuata kilometa 200 mbolea ilikuwa ni adha kubwa sana. Serikali ilitakiwa itoe kauli kwenye hili, lakini kwa kuwa Mheshimiwa Waziri alikuwa na nia thabiti, lakini kuna watu ambao walikuwa wanamkwamisha; niiombe Serikali, mwaka huu achukue fedha zake zote za mbolea ya ruzuku akae nazo, ili sasa a-deal na wale wanao-supply, isiwe kigezo fedha sijui imefanyaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali impe fedha zote za mbolea ya ruzuku Waziri wa Kilimo kwa sababu, mwaka huu wamewacheleweshea wakulima na wamesababisha upatikanaji mdogo wa mazao. Kwa hiyo, niiombe Serikali iweze kusaidia hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, Wizara ya Kilimo itusaidie, watoe maelekezo kwa wanunuzi wanaowanyonya wakulima. Wakulima wananunuliwa na vipimo visivyokuwa sahihi. Sasa Serikali itoe maelekezo vipimo viwe vya aina moja, sana sana twende kwenye kilo ili kuweza kuwasaidia. Sasa kumekuwa kuna ngosha, kuna lumbesa, imekuwa vurugu mechi huko. Mtu anakwenda kununua hapohapo, ukimwambia akuuzie kwa kutumia hichohicho anakataa. Sasa kwa nini wakulima wetu waendelee kuibiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, Mheshimiwa Waziri anafahamu Kata ya Tula, Kijiji cha Kalangazi waliunda mpango wa kuweka block farm. Humu katika mpango wa Waziri sijaiona block farm ya Mkoa mzima, hajatenga sehemu yoyote ya mashamba makubwa. Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Wilaya ya Uyui lilipitisha azimio la kujenga block farm ya ekari zaidi ya elfu 11 na Mheshimiwa Waziri akiwa Naibu Waziri, alikuja pale, akatoa maelekezo ile block farm akaungana na wananchi wa Kalangazi, akaungana na Baraza la Madiwani na akatoa maelekezo ya kwamba, block farm lazima ianze hapa na akaahidi ataniletea tractor. Najua akinipa ahadi lazima nimdai. Naomba tractor lile nilipeleke kule haraka, ili sasa wananchi wakaendelee kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha ajabu na kushangaza na wananchi wanashangaa hapa, ndio maana nasema sintofahamu naiona hapa, sasa kama Waziri anatoa maelekezo, halafu Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa anakwenda tena anasema mimi sasa kutokana na sulphur inayotumika kwenye korosho sio nzuri, sijui nini, naombeni mlime alizeti; yakatoka tena maelekezo mengine ya alizeti. Halafu sasa baadaye tena akaja Mheshimiwa Waziri wa Mazingira tena, akasema kutokana na kutunza mazingira naomba tena tuweke mizinga ya asali, hao wote wateule wa Rais, kauli tatu hata hazieleweki; wa kwanza block farm, wa pili kulima alizeti, wa tatu mazingira weka mizinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niombe, Mheshimiwa Waziri ndiye alikuwa bosi kwa sababu, Mkuu wa Mkoa sidhani kama yuko juu ya Waziri, kama kauli ya Waziri alisema block farm ni korosho na Baraza la Madiwani likasema block farm ni korosho na kijiji kimesema block farm ni korosho, sasa sisi kama wananchi naomba kabla ya Bunge hili hatujalimaliza, Serikali kupitia Wizara ya Kilimo, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Tabora na Ofisi ya Mazingira, Waziri wa Mazingira, wakae watoe direction nini kifanyike kuliko kukaa kimya. Wasipofanya hivyo mpaka tunamaliza Bunge, nikimaliza Bunge nitawaomba wananchi wangu wa Kata ya Tula, Kijiji cha Kalangasi, tukusanyike tarehe nitakayoisema, tutavamia lile shamba, tutafyeka, Waziri atakuta kule na tunaomba atuletee korosho na sisi tutakuwa tayari kupanda korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naiomba sana Serikali, kwenye hili sina mchezo kwa sababu kama tulipanga na Wizara mkakubaliana haiwezekani sasa ikawa kuna danadana, sasa hivi imebaki haieleweki! Mlisema tulime alizeti, wameenda kulima pale heka 80 ikapata gunia tatu! Hiyo ardhi inahitaji korosho, Mzee lete korosho tumalize kazi kwa sababu wananchi wanahitaji korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi nilikuwa na mambo hayo matatu tu, ninakuunga mkono kwa kazi kubwa ambayo unaifanya, Bwawa la Goweko naomba uliwekee msisitizo ili liweze kufanya kazi kwa msimu huu ambao tunaendelea nao. Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami kuwa mmoja ya wachangiaji katika Bajeti hii ya Wizara ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa, hasa ya Mheshimiwa Rais, ya kuhakikisha wananchi wanalindwa saa 24. Nampongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake, kwa kweli wanafanya kazi kubwa na wanajitahidi sana kusikiliza changamoto za wananchi kupitia wawakilishi wao, hasa Wabunge. Hiyo ndiyo sifa ya viongozi ambao sisi kama wenzao tumewatanguliza mbele kwa niaba ya kwenda kuwasikiliza wananchi waliotutuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo machache sana ambayo nataka nichangie. Jambo la kwanza katika Jimbo langu la Igalula, pamoja na ulinzi wa nchi kuwa imara, ambao Mheshimiwa Rais anaendelea kuuimarisha, tuna haja ya kuongeza upatikanaji wa ulinzi zaidi. Katika Jimbo langu la Igalula tuna ujenzi wa vituo vya Polisi ambapo wananchi waligundua kuwa ili waendelee kuwa salama, lazima waanzishe ujenzi wa vituo vya Polisi. Naiomba Serikali, Mheshimiwa Rais amekuwa akisaidia sana ujenzi unapofika katika hatua ya maboma, hata katika zahanati, vituo vya afya na shule, tunaletewa fedha, lakini sasa tuna maboma mengi ya vituo vya Polisi hayaletewi fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba, tuna Mfuko wa Tuzo na Tozo, usiwe tu unahusika kwenye mikoa, basi ushuke na kwenye kata na vijiji ili kwenda kuimarisha vituo vya Polisi katika maeneo yetu. Hii itatusaidia kuondoa mitafaruku ambayo inawakumba wananchi wetu katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata vituo hivyo ambavyo viko katika hatua ya maboma ni Kituo cha Tura na Goweko. Naomba Serikali, Mheshimiwa Waziri nilishakwambia, na nimeshauliza maswali kadhaa hapa mkaniahidi mtatenga fedha za bajeti ili ziweze kwenda kule, lakini kwenye bajeti hii sijaona fedha hizo zimetengwa. Naomba kupitia Bunge hili, unitengee fedha ili vituo vya Polisi viweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto kubwa ya Polisi wetu. Wanafanya kazi kubwa sana. Kazi ya kumlinda binadamu ni kubwa sana. Ninyi wenyewe mnafahamu, binadamu ana mbinu nyingi, lakini Polisi pamoja na uchache wao, wanajitahidi kuwalinda binadamu ili wasifanye madhara katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamekuwa na shida ya mambo mawili; jambo la kwanza, hawalipwi stahiki zao kikamilifu. Leo tunalalamika Polisi wanakula rushwa, lakini rushwa nyingine zinasababishwa na hali duni ya maisha yao. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nakuomba, waimarishieni Polisi mapato, hasa zile posho zao stahiki zilizopo kwa mujibu wa sheria zikiwemo kodi za nyumba, kulipia bili za maji na umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikia leo hii Polisi wakienda kuomba bili za umeme wanaambiwa waende na risiti wakati sasa hivi mtandao umekuwa mkubwa, luku wananunua kwa kutumia simu zao za mikononi, maji wanalipia kwa kutumia simu zao za mkononi. Sasa unapomwomba risiti ni kwenda kuwadidimiza na kuwanyima haki yao ambayo ipo kwa mujibu wa sheria. Kama mlipanga kuwalipa shilingi 50,000 walipeni fedha zao, wao watajua watafanyaje huko. Kama analala kwenye pagale ambalo halina umeme, ni yeye na maisha yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni vitambulisho vya NIDA. Mheshimiwa Waziri hili jambo mimi naomba mfanye assessment ya uhakika, muone kama hili zoezi mnaliweza au tulisimamishe kwa muda ili tujipange upya. Kwa sababu gani nasema hivyo? Tuna changamoto kubwa ya vitambulisho vya Taifa. Leo tumesema kila mwenye laini ya simu lazima asajiliwe kwa kutumia namba ya NIDA, lakini fanya takwimu, simu zipo zaidi ya milioni 50, lakini namba za vitambulisho mmetoa ngapi? Ndiyo maana unakuta namba ya mtu mmoja anasajiliwa mtu mwingine ambalo ni kosa na kinyume cha sheria. Kwa hiyo, mimi namwaomba Mheshimiwa Waziri, hebu angalia hili jambo, kama mnaliweza tuendelee nalo, lakini mwongeze kasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vitambulisho hivi mmeacha kusajili tangu mwaka 2012. Sasa kuna vijana wamefikisha umri wa miaka 18 mpaka leo hamjaweza kusajili upya. Rudisheni zoezi mkasajili upya tena ili sasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Venant, muda wako umeisha. Malizia.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili na mimi niwe mmoja wa wachangiaji katika Bajeti Kuu ya Serikali. Awali ya yote nianze kwa kuipongeza Serikali kwa bajeti hii nzuri pamoja na utekelezaji wa bajeti iliyopita, kwa sababu tunakwenda mwishoni mwa utekelezaji wa bajeti ya 2022/2023. Na Mheshimiwa Waziri nikupongeze, yako mambo yamekwenda Jimboni kwetu ni mazuri mazuri. Hii yote imesababishwa na Mheshimiwa Rais lakini na wewe mshauri wake kwa upande wa fedha, umemshauri vizuri. Sisi tuleteeni fedha kwa sababu wananchi tuliwaahidi maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanza haraka haraka, kwanza mimi nianze kwa kuipongeza Wizara ya Kilimo. Mwaka huu imetusaidia, wakulima wengi waliitikia mwitikio mkubwa katika kujiandisha upatikanaji wa mbolea ya ruzuku na haya yote yalichangia baada ya Mheshimiwa Rais kuweka bilioni 150 kwenye mbolea ya ruzuku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo lakini bado tuna changamoto; changamoto iliyopo kama tumeweza kuweka ruzuku kwenye mbolea sasa Serikali ije na mpango mkakati wa kuweka ruzuku kwenye mbegu hasa za alizeti na mahindi ili sasa ziweze kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu mzalishaji kama umempa mbolea, halafu akaenda kuweka mbegu zisizo bora ni sawasawa na bure. Kwa hiyo, nimshukuru Mheshimiwa Waziri nilipata tani moja, kama kilo 1,000 za alizeti, tayari nimekwenda kuzigawa kule na zimeleta tija sana. Kwa hiyo, mwaka huu aniongezee wakulima watalima sana, anipe tu tani 10 nikalime peke yangu kule Igalula na watu wameitikia kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuipongeza Wizara ya Kilimo kuwa imefanya kazi vizuri, lakini niipongeze Serikali imeendelea kulipa fidia kwa wanaoidai Serikali. Niiombe Wizara ya Fedha, pamoja na changamoto nyingi wanazokabiliana nazo za kifedha, lakini kuna wananchi ambao wamepisha maeneo ili kupisha miradi ya Serikali wakiwemo wananchi wa Kata ya Kizengi ambao wanajengewa mzani pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TANROADS waliwambia wasiendeleze yale mashamba, lakini hadi leo bado hawajawalipa. Ni hela ndogo ambayo haifiki hata milioni 100. Naomba Mheshimiwa Waziri, akitoka hapa akawalipe tu ili waweze kupata fedha zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, waliopitiwa na Mradi wa SGR. Kuna wakazi zaidi ya 30 ambao wamepitiwa na Mradi wa SGR kwa kigezo cha kwamba waliifuata reli (wako ndani ya mita za reli). Sasa, wale wakazi wamekaa pale zaidi ya miaka 30 hadi miaka 40. Nilifika hapa na hoja na nimwombe Waziri, kwa sababu Wizara ya Fedha ndio inayohusika na niliongea na Waziri wa Ujenzi, akaniambia niongee na Waziri wa Fedha. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, niombe kama hawa hawawezi kuwalipa ardhi, basi wawalipe majengo ili waweze kupata fidia kidogo ili wakajenge nyumba kuliko kuwabomolea na wawaache. Vile vile, Serikali ya Mama Dkt. Samia haitaki kuwaonea wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijielekeze kwenye mambo ya kitaifa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kujenga na kuleta maendeleo ni lazima wananchi tulipe kodi na hili Mheshimiwa Waziri amekuwa anasisitiza na Mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia amekuwa akisisitiza sana. Mheshimiwa Waziri, jambo ambalo tunatakiwa tulifanye, la kwanza, Waziri anatakiwa akae na management ya TRA. Customer care ya TRA sio nzuri. Leo wanalazimisha watu wakalipe kodi, lakini wanavunjwa mioyo kwa sababu ya customer care ya TRA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta mwananchi anatoka zaidi ya kilometa 200 pengine zaidi ya kilometa 250, anakwenda pale TRA siku ya kwanza ataambiwa mfumo, siku ya pili ataambiwa anayetoa TIN number ana msiba, siku ya tatu anaambiwa sijui kuna kikao gani. Sasa huyu ametembea kilometa 200 anakula na analala, ndio maana watu wengi hawalipi kodi kwa sababu ya uzembe wa watumishi wa TRA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niiombe Serikali waongeze watumishi wa TRA, lakini wawe na kauli nzuri. Hata kama kuna changamoto ya mifumo waangalie namna ya kuwasiliana na mteja aruhusiwe kwenda halafu mfumo ukikaa vizuri wawasiliane ili aweze kuja kufanya usajili na baadaye awe mlipakodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo linakera, leo ili uweze kukadiriwa, kwanza unakadiriwa hatua ya kwanza na baadaye mnatengeneza hesabu unapeleka. Leo wanatengeneza risiti na wanasema tudai risiti na kweli watu wanadai risiti, lakini risiti zao zinakaa wiki mbili zinafutika. Sasa baadaye akija kuniambia nimeuza mauzo ya bilioni tatu, anasema nilete risiti, risiti zenyewe zimefutika kwa zaidi ya bilioni moja. Baadaye anakuja kumpigia tena kodi mfanyabiashara kwa ile hela ambayo anasema risiti yake haijapelekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Serikali wakae na wataalam, mtu akifanya manunuzi inapoingizwa TIN number kwenye manunuzi yake, basi iwe reflected moja kwa moja TRA, iseme tarehe fulani ulinunua kitu cha milioni 200. Kwa hiyo, hesabu inakuja moja kwa moja ili kama akileta mahesabu, alete yale matumizi ambayo aliyafanya na ambayo hayajapita kwenye TIN number ikiwemo Payee ya mishahara na matumizi mengine ya kawaida ili a-submit pale wamtolee hesabu zao, kuliko sasa hivi unamwambia mfanyabiashara ndani ya mwaka mzima aandae risiti zake ambapo unakuta risiti zimefutika au zimepotea, baadaye TRA hawaelewi wanaanza kumpigia tena kodi ambazo sio rafiki kwa wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, Mheshimiwa Waziri mwaka 2022 alikuja hapa na bajeti nzuri sana na akasema hivi anakwenda kubana matumizi ya Serikali. Nimwambie tu sehemu ambayo anaweza kusaidia Serikali kubana matumizi ni riba za wakandarasi. Hebu waliangalie. Kwa mwaka tunapoteza zaidi ya bilioni 800 kwenda trilioni moja. Sasa hizi fedha ukizi–calculate tunakwenda kuwapunguzia wananchi mzigo. Kwa hiyo, riba za wakandarasi Waziri akizidhibiti vizuri na kupunguza ukiritimba ulioko kwenye Wizara yake na watumishi wake wakawa weledi wa kulipa kwa wakati, nadhani haya mambo hayatokwenda kwa namna hii inavyokwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila siku tunalalamika hapa fedha tumekosa, lakini fedha za riba zinapatikana na wanakwenda kulipa kwa wakati, lakini fedha za kwenda kwenye matumizi ya kawaida na matumizi ya maendeleo kwa nini zinachelewa? Kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri ang’ang’ane hapo hapo, abane matumizi lakini abane riba zisiendelee kupatikana katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo nataka nichangie, takwimu ya sensa ya mwaka 2022 ilionesha Watanzania tuko milioni 62, lakini majengo yako milioni 14. Leo amekuja na bajeti ambayo inakwenda kuongeza tozo kwenye vifaa vya ujenzi hasa cement. Sasa ukiangalia kwa Takwimu kila nyumba moja wanaishi Watanzania wa nne. Leo tunakwendaje kuwasaidia Watanzania kujenga nyumba zao kuwa nyumba bora ambazo sisi wenyewe Serikali tunatoa maelekezo? Kwa hiyo, niombe hii tozo ambayo tunakwenda kuiweka kwenye cement haiendi kuwasaidia wananchi wetu wa kipato cha chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe Serikali iangalie namna bora ya kuongeza hizi tozo katika bidhaa muhimu ikiwemo chakula hebu tuangalie kuweka msamaha. Ndio maana Watanzania hapa kuna wakati huwa wanajiuliza kwa nini makampuni makubwa yanayotoka nje yanasamehewa misamaha mingi ya kodi, lakini sisi wa ndani huku tunabanwa sana?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuwa miongoni wa kuchangia Wizara hii ya Ujenzi muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu. Kwanza nianze kuipongeza Serikali kwa kazi kubwa ya kuendelea kusaidia kufungua fursa hasa za mtandao wa barabara katika maeneo yetu mbalimbali, nimpongeze sana Waziri anafanyakazi kubwa kwa sababu hii Wizara ni kubwa sana, ina vitu vingi sana. Ninawapongeza viongozi wa mashirika hasa TPA na TRC kiukweli mashirika haya ni makubwa sana lakini ma-DG hawa wamekuwa wakifanyakazi kubwa ili kuhakikisha mashirika haya hayatetereki.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimesimama hapa kuipongeza Serikali, ukiangalia katika mtandao wa barabara katika Jimbo langu la Igalula ilikuwa kero kubwa ni barabara ya Chaya – Nyauwa, juzi Mheshimiwa Rais tarehe 17 amekuja kuizindua barabara ile na sasa wananchi wanafurahia matunda hayo, kwa hiyo sitokuwa na barabara nyingine ya kuweza kupata malalamiko bali nilikuwa nataka nimuombe Mheshimiwa Waziri kwa sababu Mkoa wa Tabora unakwenda kufunguka kiuchumi lakini kuna barabara ambayo wakiiangalia kwa bajeti zijazo, barabara ya kutoka pale Mpumbuli ukaenda Izumba, Mwisole ukatokea mpaka Ndala, ukaunganisha na ile barabara ya Puge, Ziba baadaye itokee Nzega barabara hii wakiitengeneza itaokoa zaidi ya kilometa 70, ambapo mtu akipita Manyoni - Itigi, Nzega na yule atakayepita barabara ya Manyoni - Itigi kutokea Puge na Nzega mpaka Mwanza atakuwa ameokoa kilometa 70. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri kwa awamu ijayo naomba mfanye tafiti ili muweze kuiangalia hii barabara kwa sababu tutafungua Mkoa zaidi hasa wananchi wangu wa Kanda ya Ziwa.

Mheshimiwa Spika, nianze kuchangia mambo matatu au manne. Kwanza, tuna mradi mkubwa wa SGR ambao asilimia 80 ya mradi wa Makutupora - Tabora unapita katika Jimbo la Igalula, juzi nimeshuhudia Waziri alikuja kufungua ule mradi kuashiria kazi ianze, wananchi wangu wa Jimbo la Igalula kwanza wameupokea mradi kwa kiasi kikubwa na sisi tuko tayari kuwapa ushirikiano ili kuhakikisha ile azma ya Serikali kufungua mtandao wa reli kutoka Dar es Salaam mpaka Kanda ya Ziwa Mwanza na hatimaye Kigoma na nchi jirani unakwenda kutimia.

Mheshimiwa Spika, wananchi wangu wamenituma yafuatayo, kwanza kwa kuwa mradi umekuja tumeshauzindua wataalam wako site wananchi wa Kata ya Tura, Malongo, Goweko, Igalula pamoja na Nsololo wanaomba sana wataalam wawahi kwenda kubainisha maeneo wapi reli itapita. Kwa sababu kumekuwa na uvumi mwingi na wananchi wameshindwa kufanya shughuli za kimaendeleo hawajui wapi wajenge wako sahihi. Kwa hiyo, ninaiomba Serikali twendeni kule tukawape maelekezo wananchi wetu wapi reli itapita na muzuie kama yuko ndani ya zile mita 30 basi wapewe maelekezo mapema kuliko kwenda kuwafanyia fumanizi, lakini kama wako nje ya sheria ile ya reli yaani reli itakuwa imefuata wananchi basi muangalie utaratibu wao wa kuanza kuwaambia wasiendeleze majengo kwa sababu isije baadaye ikatokea mgogoro, kwa hiyo nilikuwa naomba hilo.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine naiomba Wizara kuna wananchi wangu hasa wa Kata ya Goweko na Nsololo wako kwenye zile mita za Serikali ambayo ninyi wenyewe mliziweka hapa ya kuwa mita 30 walijenga tangu miaka 30, 40 iliyopita, wananchi wale walikuwa na kilio kwa sababu kama sheria ilikuwa hivyo sasa hivi wanaoishi pale ni Watoto, wazazi wao asilimia kubwa walishapoteza maisha basi walikuwa wanaomba pale mtakapoenda kuwatoa basi muweze kuwapa kifuta machozi ili sasa wakaendeleze maisha kwa sababu wengi walioko pale ni yatima kuliko kwenda kuwaondoa kwa haraka haraka kwa sababu wao wamerithi wazazi wao ndiyo walijenga pasipo kujua.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ninamshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kuniahidi kunijengea daraja la Loya, kwa sababu ilikuwa ni changamoto kubwa na TARURA kama tungeweza kuwapa huu mzigo tusingeweza kuutatua. Kwa hiyo kwa ujenzi wa daraja la Loya utasaidia sana wananchi wangu kupata huduma na kutokupoteza maisha kila kipindi cha masika.

Mheshimiwa Spika, kuna suala moja ambalo Mheshimiwa Waziri tarehe 17 kuna ugeni wa Rais nililisema na hapa naomba niliseme, Mheshimiwa Waziri ile barabara mlioizindua hiyo tarehe 17 niliomba siku ile matuta hamkunielewa. Mheshimiwa Waziri kumekuwa na vifo vingi sana, watu wanagongwa wanapoteza maisha kwa sababu ya mwendokasi wa magari. Naomba unisaidie kwa haraka, uniwekee matuta hata kwenye zile center za Tula, Kizengi na Kigwa kwa sababu hizi center kubwa watoto wanatoka upande mmoja kwenda upande mwingine wanapoteza sana Maisha.

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa nafasi, ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuwa miongoni mwa wachangiaji katika Bajeti Kuu ya Serikali ya mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kuipongeza Serikali ya Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri bajeti ya mwaka 2021/2022 ambayo Bunge lako Tukufu lilipitisha kwa Jimbo langu la Igalula imekwishafika kwa asilimia 100, hiyo niwapongeze sana Serikali kwa kazi kubwa ambayo mmeifanya, zimebaki chenji tu kidogo za wahisani sasa sijajua zimekwama katika mlengo gani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuipongeza Serikali leo tuko katika Bajeti Kuu ya 2022/2203 ambayo tutakwenda kuitekeleza kuanzia Julai Mosi, mwaka 2022, pamoja na pongezi nzuri lakini mimi nilikuwa kidogo katika Bajeti ya Waziri kuna mambo ambayo nilitaka tuyazungumzie kama wananchi na nchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza kwanza nikupongeze Mheshimiwa Waziri kwa kupunguza tozo ya miamala ya simu ambayo ilikuwa ni changamoto na ilieleta taharuki lakini Mheshimiwa Rais baada ya kusikia kilio cha Watanzania alipunguza hiyo tozo na baadae kwenye bajeti yako hii umeonyesha kuwa utapunguza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunataka tujue kama Watanzania kwa sababu tulipitisha tunaenda kukamilisha mwaka mmoja, tangu tumeanza kuchangia hizi tozo, trip ya kwanza ulikuja ukatuambia tumekusanya mabilioni ya fedha tukaona kwenye TV, lakini baadae tukaona kimya, sasa tunataka tujue haya makusanyo mpaka leo tulikusanya Shilingi ngapi ili tuwapongeze Watanzania ambao walivumilia maumivu na ninyi baadae mmekuja kuwaondolea kwa sababu ya hali ya kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili mimi nikupongeze pamoja na kuendelea kuwaona Watanzania na kuwapunguzia makali, mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri katika bajeti yako umejikita sana kuwapunguzia mzigo Watanzania lakini umeenda zaidi, ukasema baadhi ya milolongo iwezwe kupunguzwa ili wananchi waweze kupata fursa na tunu na maendeleo ya Serikali yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri amesema vizuri wananchi wanasafiri umbali mrefu kwenda kufuata huduma, na hii umeiweka vizuri sana ukasema baadhi ya vitambulisho viweze kutambulika, lakini Mheshimiwa Waziri nikuombe kuna kundi kubwa sana la Machinga na Bodaboda na hapa umeliweka vizuri sana, bodaboda ndio wengi zaidi katika maeneo yetu ya vijijini, sasa mimi nashindwa kuelewa, anayeendesha lori leseni yake ni Shilingi 70,000 anayeendesha Kirikuu 70,000, bodaboda 70,000! mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri, hebu punguza hawa watu wa bodaboda ili wasikimbizane na Polisi iwe tu tozo Shilingi Elfu Ishirini utakuwa umewasaidia sana na wataacha kuwa wanawakimbia Polisi na kwenda kufuata huko leseni, kwa sababu unakuta mafunzo 80,000, leseni 70,000 kabla ajaanza kazi Laki Mbili imeisha sasa unakuwa umemsaidia au umemsababishia hasara kwa sababu hiyo hela ingeweza kuwasaidia wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nijikite kwenye mambo mawili au matatu katika bajeti hii. Kwanza nikupongeze Mheshimiwa Waziri kwa kutambua Sekta ya Kilimo. Nimpongeze Waziri kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya. Mheshimiwa Rais amesema ili kuweza kulikomboa Taifa lazima tujikite kwenye sekta ya kilimo, bajeti tumeiona imeongezeka mara dufu katika sekta ya kilimo, kazi yetu sisi kama Wabunge kwenda kuwahimiza wananchi wetu kuweza kwenda kuitetea sekta hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2021 Mkoa wetu wa Tabora ulizindua kitabu ambacho walikuja Mawaziri wengi, kitabu hicho kilitangaza fursa mbalimbali zilizoko katika Mkoa wetu wa Tabora. Ninakumbuka Mheshimiwa Bashe leo ni Waziri wa Kilimo alikuwepo wakati huo akiwa Naibu Waziri alishiriki katika kongamano hilo la kufungua fursa, kitabu hicho kipo na kumbukumbu ya Serikali ipo. Waliomba Mkoa wa Tabora uweze kutengeneza block farm mbalimbali ili ziweze kusaidia wananchi katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuondoka tuliweza kukaa kama Halmashauri, wakapendekeza eneo la Kalangasi Kata ya Tura Jimbo la Igalula itengenezwe block farm ya korosho. Jambo la kushangaza tulipitia michakato yote ambayo ilikuwa utaratibu na kwa mujibu wa sheria na Baraza la Madiwani liliridhia kuwa Kalangasi sasa tutakwenda kutenga ekari 15,000 itakuwa block farm ambayo tutalima kilimo cha korosho, ajabu imeingia mdudu asiejulikana sasa imeanza kupigwa danadana block farm ile haijulikani kama ipo au haipo, wanataka waweke kilimo cha mizinga ya asali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Bashe unatoka Mkoa wa Tabora hebu naombeni mnitajie ni nani ametajirika kwa asali anayetoka Mkoa wa Tabora? Wananchi wetu wengi matajiri wanatajirika kwa nafaka za chakula, sasa tunakwenda kuweka kilimo cha asali, wananchi wa Kalangasi waliweka block farm ya korosho wameutunza msitu kwa muda mrefu sana. Mheshimiwa Jafo alikuja pale ziara akasema huu msitu muhimu sana. Sasa mimi nashindwa kuelewa, hivi Serikali huwa wanawasiliana?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo anataka block farm, Mheshimiwa wa Mazingira anasema huu msitu utunzwe kwa sababu ya mazingira, sasa mimi niiombe Serikali, wananchi wa Jimbo la Igalula Kata ya Tura, Kijiji cha Kalangasi wako tayari kushirikiana na Serikali kuweka block farm ya korosho, pia wako tayari kushirikiana na Serikali kwa kila hatua ili kuhakikisha mradi huu unaleta tija kupitia Halmashauri yetu na kupitia Taifa na kuingiza pato.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakuomba Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Waziri wa Kilimo yuko hapa kupitia majibu ya Serikali, tunataka tujue tunapoondoka kwenda Majimboni tuondoke na kauli moja, kwa sababu wameshaanza TFS kwenda kupima eti lile eneo liwe la uhifadhi, wakati miaka yote tangu uhuru hawajawahi kwenda kule, wananchi wamehifadhi kwa kutumia gharama zao, leo wanaenda kupima kule nini? Nasi kama Wawakilishi wa Wananchi tunakataa na tunalaani wasisogee tena huko kwenda kupima eneo hilo, nadhani watakuwa wamenielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kufungua uchumi wa Mkoa wa Tabora tumepewa fedha nyingi za kujenga reli ya kisasa (standard gauge) ambayo katika Mkoa wa Tabora asilimia 70 ya reli kutoka Makutupora kwenda Tabora….

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa

T A A R I F A

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka kumpa taarifa mnenaji kwamba mabadiliko ya tabianchi duniani yamekuwa ni mabaya sana na mvua zimekuwa zikipungua mwaka kwa mwaka. Kwa hiyo, kuna umuhimu wa Serikali kuendelea kutunza misitu, kwa hiyo nimeona kusema kwa kutumia neno kusema walaaniwe ni kosa, kwa sababu nchi inateketea na dunia inateketea kwa sababu ya mazingira. Ahsante sana.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Venant.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza hili neno walaaniwe sijalisema yeye ameongeza chumvi misitu Tanzania iko mingi.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa wewe sema tu unaipokea ama huipokei ni vitu viwili tu.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, siipokei taarifa kwa sababu mbalimbali.

NAIBU SPIKA: Endelea na mchango wako.

MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, jambo ninalolisema uhifadhi upo, misitu ipo waende wakahifadhi kule, wananchi hawa walihifadhi kwa miaka yote, sasa hivi wanakuja kufanya nini, kwa hiyo tunataka kilimo cha korosho usinipoteze kwenye mada yangu.