Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Nicholaus George Ngassa (15 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia jioni hii kwanza namshukuru Mwenyezi Mungu muumba mbingu na nchi, kwa kupata fursa ya kuwa sehemu ya Bunge la Kumi na Mbili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pili nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi kwa kunipa ridhaa ya kuwa mpeperusha bendera wa Jimbo la Igunga na hatimaye nikaibuka na ushindi na kuwa Mbunge wa Igunga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu, kwa umuhimu mkubwa niwashukuru sana baadhi ya viongozi ambao kwa wakati mmoja mlipita maeneo mbalimbali mkitunadi na mkituombea kura, naamini ushindi wetu umechangiwa na uwepo wenu katika maeneo yetu na hapa nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipowataja majina kwa uchache; kwanza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli, Makamu wa Rais, mama Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu wetu Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, wewe mwenyewe binafsi Mheshimiwa Spika, Job Ndugai, Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi Dkt. Bashiru Ally Kakulwa, Wajumbe wote wa Kamati na Sekretarieti ya Chama Cha Mapinduzi, akiwepo Mbunge mwenzetu Mheshimiwa Humphrey Polepole tunawashukuru kwa kuja kwenye maeneo yetu kutupigia kura. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kwa umuhimu mkubwa niwashukuru wapiga kura wa Jimbo la Igunga ambao walifanya nipate ushindi wa kishindo na hatimaye leo nimeweza kuingia kwenye Bunge hili, ahadi yangu kwao nitawatumikia kwa moyo mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa kuwa nina muda mchache kwanza nijikite katika hotuba ya Mheshimiwa Rais, maeneo ambayo ningependa kuchangia jioni hii ni upande wa huduma za kijamii na miundombinu ya kiuchumi. Kwenye huduma za kijamii, Mheshimiwa tunaanza na suala la elimu, katika upande wa elimu Mheshimiwa amesema tutaendelea kutoa elimu bure ya bila malipo, lakini pia na kuboresha miundombinu ya kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, niwashauri Wizara ya Elimu ambao wanamsaidia Rais na Wizara ya TAMISEMI, waje na mipango madhubuti watakayohakikisha tunapata miundombinu ya uhakika na siyo inapofikia mwezi wa kumi na mbili na mwezi wa kumi na moja tunaanza kusumbuana kuhusu madawati, madarasa na upungufu wa vifaa vya kufundishia mashuleni, naamini kwenye mpango utakaokuja watakuja hatua madhubuti kwa ajili ya kuliona hili.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni kwenye suala la maji, nashukuru sisi Mkoa wa Tabora tumepata Mradi wa Maji wa Ziwa Victoria, changamoto kubwa imebaki kwenye usambazaji na hususani kwenye suala la viwango vya bei, naomba Wizara ya Maji waliangalie hili waje na viwango vipya ambavyo vitaweza kuwasaidia wananchi wengi wa maisha ya chini na hili napenda kutolea mfano kwa mfano kwenye suala la umeme, umeme walikuja na ile programu ya REA wanatoa umeme kwa 27,000 vijijini kwa hiyo na Wizara ya Maji tunawashauri waje na programu itakayowezesha
wananchi wengi kuunganishiwa maji ili waweze kutatua tatizo la ukame kwenye majibo yetu.

Mheshimiwa Spika, jambo la nne ni upande wa afya katika upande wa afya pia kuna changamoto kubwa upatikanaji wa madawa na vifaatiba, lakini pia kuna upungufu wa wahuguzi wa madaktari tunaomba pia Wizara ya Afya na TAMISEMI ambao mnasimamia hutowaji wa hizi huduma na sera muweze kuziangalia pia tuweze kutatua changamoto kubwa hili.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulichangia jioni hii ni suala la kilimo kwenye kilimo sisi ukanda wetu sisi tunalima sana pamba, changamoto ambayo tumekuwa tukikabiliana ni suala la wakulima kuchelewa kulipwa na ninaishukuru mwisho wa mwaka tulipokuwa tunaelekea kwenye uchaguzi kulikuwa kuna madeni, lakini Serikali waliweza kukamilisha hayo.

Namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Bashe, Mbunge na jirani yangu alinisaidia sana ilikuwa ni changamoto sana wakati wa uchaguzi lakini tuliwasiliana naye akatowa maelekezo bodi ya pamba wakatulipa. Tunaomba safari hii msimu wa pamba utakapofika kipindi cha mauzo Wizara ijipange vizuri tuhakikishe wakulima hawatoki na madeni.

Mheshimiwa Spika, lakini changamoto nyingine kwenye kilimo ni suala la stakabadhi ghalani na AMCOS tungeomba pia hili suala hususani wakulima wa choroko linawasumbua sana tunaomba wizara ijipange mapema itakapofika kipindi cha kuuza mkulima anakwenda kuuza kilo mbili kilo tatu kilo tano haitaji kusubiri mwezi moja miezi miwili aweze kupata malipo yake ili itatusaidia sana kuwasaidia wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, mwisho nashukuru sana ahsante sana kwa kupata fursa hii naunga mkono hoja asilimia mia moja nashukuru. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango wa Maendeleo ya Taifa. Wiki iliyopita kwa sisi Wabunge wengi tulioingia Bungeni kwa mara ya kwanza tulitumia nafasi hii pia kushukuru Mungu kwa kuandika historia, lakini pia leo tunaingia katika historia nyingine ya kutoa mawazo kwa ajili ya ujenzi wa Taifa letu kwa sababu tunakwenda kuchangia Mpango wa Maendeleo wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie eneo moja tu, nafasi ya utumishi wa umma katika kufanikisha Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa. Nimeusoma Mpango vizuri kuanzia ukurasa wa 111 mpaka ukurasa wa 120, umeelezea kuhusu maendeleo ya watu na eneo moja kubwa ambalo limekuwa interesting kwangu ni suala la ujuzi. Hotuba ya Waziri na Mpango umeelezea vizuri sana kuhusu ujuzi katika ngazi mbalimbali ambazo namna itakavyotusaidia katika kulisogeza Taifa letu mbele. Hata hivyo, kuna changamoto kubwa sana ambayo Serikali naomba msi-compromise na hili ni suala la utumishi wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna Sheria ya Utumishi wa Umma Na. 8 ya mwaka 2002; tuna Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma za 2003 na Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma za 2009; vyote katika muundo wake na maelezo yake havitoi nafasi katika suala la ujuzi. Sasa huu Mpango tunaoujadili leo Wabunge, wanaoenda kutekeleza, wanaoenda kusimamia na wanaotakiwa kubuni vyanzo vya mapato ni hao hao watumishi wa umma ambao Mpango haujawatambua vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakapolipitisha hili jambo litakwenda na Serikali wasipoliona, matokeo yake baada ya miaka mitano, Waziri ataleta Mpango mwingine utakuja na utakuwa na table inayoandika vikwazo na moja ya kikwazo itakuja ni hili suala. Sasa ushauri wangu ni nini? Sisi kama Taifa linaloendelea tunachukulia mfano wa Malaysia, Malaysia walipofanya mabadiliko yote kwenye kilimo na viwanda walikuja na kitu wanakiita re-energizing civil service; waliamua kuweka nguvu kwenye kubadilisha mfumo wa utumishi wa umma wakaja na mfumo ambao wanaangalia knowledge, skills na ability kwa maana ya kwamba maarifa, uwezo na ubunifu ndiyo vikawa vinampa mtu nafasi ya kufanya maamuzi katika utumishi wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwetu bado tuna mfumo wakwetu tunaita meritocracy na ni mfumo wa kizamani na ndiyo maana mfumo wetu wa utumishi wa umma umejengwa vizuri sana, lakini unafanya kazi kizamani, bado tunatumia model za akina Max Weber za seniority, unapotumia mifumo ya seniority maana yake watu wenye uwezo wenye ubunifu wanakosa nafasi za kufanya maamuzi, michango yao inaishia chini, unakuta maamuzi yanaishia kufanywa na Wakurugenzi, Wakuu wa Idara na Wakuu wa Vitengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naweza kukupa mfano hata huu Mpango tunaoujadili, unaweza kwenda Wizara ya Fedha ukaulizia, ukakuta wanaoufahamu huu Mpango hawafiki watumishi 30, Wizara nzima hawaufahamu. Tuunde mfumo sheria hizi zibadilishwe, kuwe na mfumo wa kubadilisha vikao vya maamuzi vijumuishe na watumishi wa kawaida ambao wengi wanakuwa na uwelewa mpana.

Kwa hiyo tutapokuwa na mawazo ya wachache matokeo yake kwenye utekelezaji tunakwama na ndiyo maana tunatolea mfano suala la ubunifu wa vyanzo vya mapato, kila siku vyanzo vinarudi vilevile, utaishia vichungi vya sigara, utaishia sijui pombe zenye vileo vikali, ukiwaambia watumishi kubuni vyanzo vipya wale wanaobuni miaka yote ni wale wale, ni level ya juu cluster watumishi wa chini hawashirikishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya wazo ambalo ninalo hata kwa watumishi wa umma, inabidi taasisi na idara zote zinazohusika na makusanyo ya maduhuli na mapato waambiwe ili tuwaongezee mishahara na motisha watumishi wenu wabuni vyanzo vipya vya mapato. Tukifanya hivyo tutakusanya trilioni 40 kwa mwaka hili Taifa, lakini sasa hivi mtu anajua ikifika tarehe 23 tarehe ya Baba Jesca imefika nitapata mshahara, hata nisipofanya kazi hamna litakapofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli tumefanikiwa kujenga nidhamu kwenye utumishi wa umma, lakini nidhamu tuliyonayo ni ya watumishi kuingia saa 1.30 anasaini, anasubiri kutoka saa 9.30, hawana ubunifu, wanaishia kuanza kuzunguka maofisini wanauza vocha, wanauza mabuyu kwa sababu kutokana na mfumo huu hauwasaidii. Ofisi zinabebwa na watu wachache na mtu anajua kwamba mimi sasa hivi nimeshaajiriwa ni permanent and pensionable, nisipokifanya leo na mimi labda siku moja nitakuwa Mkurugenzi nitafanya. Tunataka kila mtu atimize wajibu wake. Namna ya kutimiza wajibu wake ni kubadilisha mfumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningeshauri Serikali, Wakuu wa Idara kwa maana ya Wakuu wa Taasisi za Umma Wakurugenzi wapewe mamlaka ya kuweza kuteua na kupendekeza watu kwa Katibu Mkuu wa Utumishi wanaoweza kufanya nao kazi kwenye menejimenti. Menejimenti nyingi hazitoi ushirikiano kwa Wakurugenzi walioteuliwa na Mheshimiwa Rais, unakuta Menejimenti ina watu tisa wanaounga mkono Mkurugenzi aliyeteuliwa na Rais ni wanne au watano anashindwa kufanya kazi na wale watu matokeo yake wanabaki wanamkwamisha, ndiyo ile bureaucracy, unakuta dokezo linahitaji laki mbili, maamuzi yanatumia tisa kuamuliwa, hatuwezi kusogea kama Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tubadilishe huo mfumo Mkurugenzi anapopewa taasisi ya Serikali anapoona kuna watu anashindwa kufanya nao kazi, apendekeze watu kwa Katibu Mkuu wa Utumishi apeleke majina matatu akiletewa moja naye atakuwa hana sababu ya kusema kwa nini nimekwamishwa, lakini atakwamishwa na mwisho wa siku anajua huyu kapewa, baadaye atatumbuliwa atatuacha, ndiyo kauli zinazoendelea kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo jambo lingine ambalo ningependa kupendekeza ni kwenye suala la ubunifu wa vyanzo vya mapato kama nilivyosema. Tunahitaji fedha za kuweza kusaidia huu Mpango; huu Mpango ni wa miaka mitano na Taifa letu tunahitaji lisogee mbele na tuna miradi mikubwa ambayo inahitajika ikamilike tunahitaji fedha. Wapewe nafasi watumishi wabuni vyanzo vipya vya mapato ili kuweza kusaidia Taifa letu kusonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru nami pia kunipatia nafasi ya kuongea na kutoa mchango wangu kwenye bajeti kuu ya Serikali ya mwaka 2021/2022. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niipongeze Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mama yetu Rais Samia Suluhu Hassan kwa consistency nzuri waliyoanza nayo katika ukusanyaji wa mapato, ukijaribu kuangalia taarifa ya Msemaji Mkuu wa Serikali mwezi wa nne tulikusanya trilioni 1.34, mwezi wa tano tumekusanya trilioni 1.3 naamini na mwezi wa sita mtakwenda vizuri, hongereni sana Serikali katika ukusanyaji wa mapato. Ni mwanzo mzuri, Wizara ina vijana wawili mahiri yupo Mheshimiwa Daktari Mwigulu Nchemba yupo na Injinia Masauni ambao kwa nyakati tofauti wameshakuwa mabosi wangu wakati nipo Serikalini nawajua umahiri wao naamini watakwenda vizuri, hongereni sana pia kwa kuaminiwa.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba yangu itakuwa ina pande mbili, upande wa kwanza utakuwa ni wa kitaalam na upande wa pili nitaelezea uhalisia katika yale nitakayoyachangia. Upande wa kitaalam ambao utakuwa ni upande wa nadharia reference nitafanya kwa kutumia sheria mbalimbali na miongozo mbalimbali, sasa naanza na jambo la kwanza ambalo nataka nilichangie jioni hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ni udhibiti na usimamizi wa fedha za serikali, makusanyo ni mazuri tumepanga bajeti ya trilioni 36 kwenda kukusanya na kutumia katika mwaka huu wa fedha, tunayo Sheria ya Fedha Namba 6 ya mwaka 2001 inaitwa Public Finance Act ilipofanyiwa maboresho mwaka 2010 ilizaa baadhi ya taasisi, moja ya taasisi ambazo zilizaliwa inaitwa taasisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Ndani wa Serikali - Internal Auditor General Office ndiyo taasisi ambayo kwenye Halmashauri inaleta watu wanaitwa Internal Auditors au Wakaguzi wa Ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wakaguzi wa Ndani pamoja na majukumu yao mengine yote wana majukumu makubwa matatu ambalo la kwanza ni kuangalia michakato inayoendelea kwenye Taasisi za Serikali tunasema kuangalia zile process. Jukumu la pili ni kuangalia ile assurance udhabiti wa Serikali kwamba tunakokwenda ni uhakika na jukumu la tatu ni kuangalia quality tunasema quality control.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kinachoendelea katika uhalisia katika halmashauri zetu Wakaguzi wa Ndani wamegeuka kuwa Menejimenti za Halmashauri na wenyewe badala ya kuwa wakaguzi. Ukienda kwenye SMT ambayo Mkurugenzi wa Halmashauri au kwenye Taasisi Mjumbe mmojawapo ni Mkaguzi wa Ndani ambaye anatakiwa amkague huyo Mkurugenzi wa Taasisi au Mkurugenzi wa Halmashauri ambaye ni bosi wake, hivi unaweza ukamkagua bosi wako na ukatoa taarifa ya kumkaanga ni jambo gumu sana, matokeo yake ni nini? ndiyo maana tunapokuwa kwenye vikao vya Kamati ya Fedha au Mabaraza ya Halmashauri anapotuhumiwa DT unashangaa Internal Auditor anasimama kumtetea DT, kwa utaratibu huu itakuwa ngumu kwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Wizara hawa watu muwakumbushe majukumu yao, kutumia vyuo mbalimbali mlivyonavyo chini ya Wizara yenu muwajengee uwezo kama ambavyo la wiki iliyopita Mheshimiwa Hasunga alichangia mvitumie hivi vyuo, wakumbushwe majukumu yao, wao ni waangalizi wa Serikali wanawasaidia kuangalia wale ni watchdogs, lakini siyo sehemu ya operations katika Halmashauri zetu.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine kuhusu Wakaguzi wa Ndani, sasa hivi tunasema tuna e-government tunaendesha mfumo wa Serikali kimtandao, unakuta una Mkaguzi wa Ndani mmoja ambaye basically ni accountant namna gani ataenda kukagua hii mifumo ya Halmashauri ya kukusanya fedha ya kieletroniki? Sasa niwaombe Wizara kama mtaomba kibali cha kuajiri tuna halmashauri 185 kuna watu wanaitwa Information System Auditors hiyo Idara ipo pale katika Ofisi ya CAG. Katika Ofisi ya AG pia muiweke muajiri watu ambao wanajua mifumo waende kukaa na kukagua mifumo ili kuwarahisishia wale Accountants katika suala la Ukaguzi wa Mapato ya Serikali na Matumizi ya Serikali, hiyo ni sehemu ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili baada ya sheria kufanyiwa maboresho kuna kitengo kilianzishwa kinaitwa vitengo vya usimamizi vihatarishi (Risk Management Unit), hivi ni vitengo ambavyo vimetengenezwa kwa ajili ya kuangalia viashiria vya viahatarishi Serikalini katika utekelezaji wa mipango yetu kwa kila robo mwaka, naomba pia mviimarishe mwajiri watu au waliopo wapewe mafunzo wajengewe uwezo waweze kuisaidia. Vitengo hivi vinaenda sambamba na vitengo vya Ukaguzi wa Ndani na kila robo mwaka wanaandaa taarifa inapitiwa na Kamati za Uongozi na kuangalia vihatarishi vitakavyokwamisha operations za Taasisi za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ni Halmashauri au Idara zinazojitegemea wanatoa maelekezo na kusema kwamba safari hii tuna Corona tutakwamisha kwa namna moja, mbili, tatu. Safari hii tuna mvua nyingi kwenye ujenzi wa barabara tutakwamishwa na moja, mbili, tatu. Mviangalie hivi vitengo mviimarishe mvijengee uwezo vitaweza kutusaidia sana katika kufikia malengo ya bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunakwenda kitengo cha tatu au taasisi ya tatu ni Ofisi ya CAG, Ofisi ya CAG ipo chini yenu Wizara ya Fedha, sasa unapoongea Ofisi ya CAG ndiyo inaleta watu wanaitwa External Auditors wanapoenda kufanya ukaguzi kwenye taasisi nyingine. Hawa watu wanapofika wanafanya mnasema zile entrance meeting na ukitaka kuondoka unafanya exit meeting, lakini ukifanya uchunguzi kwa kiwango kikubwa wana - collide na Wakuu wa Taasisi katika suala la uandaaji wa hizi hati.

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta taasisi imepewa hati safi lakini ukifuatilia matumizi yake siyo mazuri, wanaenda wanakaa mezani wanajadiliana kabla hawajafanya exit meeting wanaacha kitu kidogo wanaongezewa pale mlungula wanaondoka ripoti inatoka safi, fanyeni uchunguzi mjiridhishe katika hili wizara. Kwa hiyo, katika upande wa udhimabiti wa fedha za Serikali na Usimamizi wa Fedha itawasaidia sana mkitumia haya maeneo matatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango namba mbili, eneo namba mbili nataka kuchangia Utumishi wa Umma. Wakati nachangia Mpango wa Maendeleo ya Taifa nilisema Utumishi wa Umma ni nyenzo muhimu sana katika kufanikisha mipango hii. Niwapongeze Serikali, niwapongeze Wizara ya Utumishi, TAMISEMI na nyinyi Wizara ya Fedha kwa kuja na motisha mbalimbali mlizotoa kwa watumishi wetu wa umma, hongereni sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine ambayo ninatamani niichangie kuna eneo la kuwajengea uwezo Watumishi wa Umma. Tunayo Sheria ya Utumishi wa Umma Na. 8 ya mwaka 2002, Kanuni za 2013 na Kanuni za Kudumu za 2019 hapa changamoto ipo wapi, wanapoandaa mafunzo kuna mipango ya mafunzo ya muda mrefu na mafunzo ya muda mfupi ni kichaka kingine ambacho Maafisa Utumishi wanakitumia kunyima haki za Watumishi wa Umma. Wakati mwingine mtumishi anahitaji kujisomesha, kujiendeleza na kujijengea uwezo lakini unaambiwa haupo kwenye mpango wa mafunzo, sasa huyu mtu anajisomesha kwa hela yake sasa kwa nini unamzuia? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuangalie tuweke utaratibu kama ambavyo inasema Sera ya Mafunzo ya Utumishi wa Umma ya mwaka 2013 watu hawa wanapohitaji kujiendeleza kwa sababu ni lengo ni kuboresha na kuongeza ufanisi katika kazi, wapewe nafasi ya kwenda kusoma wakirudi waendelee. Kwa sababu Serikali ina fedha ndogo na uwezo wa kusomesha kila mtumishi kadri ya muda wake wa kusoma haiwezi, mtu anapotaka kwenda kujisomesha apewe ruhusa akasome kwa sababu atakaposoma ni faida kwa Serikali yetu, tuepukane na haya matusi wanayotukanwa watalaam wetu kwamba hawana uwezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu amekaa miaka kumi na tano hajawahi hata kupata hata refresher course unadhani atakuwa na uwezo mzuri wa kufikiria? Ndiyo maana hata huko kwenye vyombo vya ulinzi na usalama ukikaa miaka mitatu, minne unapigwa refresher course maana yake ni kwamba kuna vitu vipya hata computer zina software, unasikia tunatoka Window 7 tunaenda Window 8, tunaenda Window 9. Kwa hiyo Serikali hili mliangalie katika kuboresha hili eneo, watumishi wakiongezewa ujuzi litatusaidia sana katika kufikia haya malengo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa kuonesha dira madhubuti katika kuongoza nchi yetu na kuna maeneo manne ambayo mpaka sasa tunasema Mheshimiwa Rais ameupiga mwingi.

Mheshimiwa Spika, eneo la kwanza ni kusimamia ulinzi na usalama wa nchi yetu, eneo la pili ni kusimamia maendeleo na ustawi wa Taifa, eneo la tatu ni kuimarisha utangamano na Jumuiya za Kikanda pamoja na uhusiano wa Kimataifa na eneo la nne ni kulinda tunu za Taifa letu ikiwepo umoja, amani, mshikamano, kulinda Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar, lakini pamoja na Muungano wetu. Hongera sana Mheshimiwa Rais tunakuombea kwa Mwenyezi Mungu akupe afya njema uendelee kutuongoza vyema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, nimesimama kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, pia nimpongeze Mheshimiwa Kassim Majaliwa pamoja na Wasaidizi wake kwa kuendelea kufanya vyema katika kusimamia shughuli za Serikali, pia na kuziratibu shughuli za Serikali pamoja na Bunge.

Mheshimiwa Spika, mimi nitachangia maeneo mawili ya kisera. Eneo la kwanza nitaongelea suala la usimamizi madhubuti wa fedha za umma na eneo la pili nitakalochangia ni suala la uchumi shindani, uchumi jumuishi kwa ajili ya maendeleo ya watu.

Katika mchango wangu moja utajikita kwanza katika kupitia document niliyonayo, Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, hotuba ya Mheshimiwa Rais ya mwezi Aprili mwaka jana 2021 na Sheria ya Fedha za Umma (Public Finance Act, No. 6, ya 2001), lakini pia na Sheria ya Fedha za Umma za Serikali za Mitaa (The Local Government Finance Act) ya mwaka 2019. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu ina mifumo mbalimbali ya udhibiti wa fedha za umma, mimi nitajadili mifumo miwili. Mfumo wa kwanza ni unaosimamiwa na ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani wa Hesabu za Serikali kwa maana ya Internal Auditor General na mfumo wa pili ni ule unaosimamiwa na Ofisi ya Mdhibiti na Msimamizi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa maana ya CAG, chini ya ofisi ya National Audit Office ambayo ni Ofisi ya Ukaguzi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, unapokwenda kwenye Halmashauri zetu kwa sasa tunasema kwenye Majimbo, mama pochi lake limefunguka fedha nyingi zinakwenda. Pamoja na fedha hizi nyingi kwenda tunahitaji mifumo Madhubuti ili tuweze kuzisimamia fedha hizi ili ziweze kutoa matokeo kama ambavyo tunatarajia.

Mheshimiwa Spika, eneo la kwanza ni kuhusu ukaguzi wa ndani kwenye Halmashauri zetu. Unakwenda kwenye Halmashauri kwa mfano Halmashauri ya Wilaya ya Igunga tuna Kata 35 na tuna Vijiji 119, lakini tuna Mkaguzi wa Ndani mmoja tu. Ukisoma Sheria ya fedha ya Serikali za Mitaa na Sheria ya Fedha za Umma inataka hawa watu pamoja na majukumu yao mengine ya ukaguzi, lakini wahakikishe wanafuatilia ile michakato yote ya shughuli zinazofanyika kwenye Halmashauri ambako fedha za umma zinakwenda. Kutokana na uchache wa hawa watu wanajikuta muda mwingi wanaishia kukagua risiti za manunuzi na kukagua vocha za malipo, wanashindwa kuangalia michakato ya fedha zinakokwenda kwa ajili ya kuleta mwandeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndugu zangu, viongozi wangu na chama chetu sasa inabidi tuangalie hili suala tuweze kuongeza rasilimali watu katika hili eneo ili tuweze kusimamia vizuri rasilimali zetu za fedha. Kwa hiyo, katika hili jambo tuwe makini tuhakikishe tunaongeza watu, tuongeze rasilimali watu, tusijikite katika kuwajengea tu uwezo. Unapokuwa na mtu mmoja anasimamia ukaguzi katika Halmashauri moja ambayo ina Vijiji vingi na Sheria hii ya Fedha ya Serikali za Mitaa inasema kabisa huyu mtu anatakiwa kukagua mpaka akaunti za Halmashauri za vijiji, sasa vijiji 119 yuko mtu mmoja katika hali ya kawaida vinaweza kumzidia na asiweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbadala wake ni nini ama alternative? Sheria hii ya Fedha za Umma mwaka 2010 ilifanyiwa maboresho na Bunge likapendekeza kuanzishwe kitengo kinaitwa kitengo cha usimamizi wa vihatarishi Serikalini (Risk Management Unit). Baadhi ya sehemu wameanzisha idara kama Benki Kuu ya Tanzania na baadhi ya maeneo wameanzisha vitengo, lakini bado kuna changamoto kubwa kwenye Halmashauri nyingi wameweka ma-champion tu, ambao utendaji kazi wao pia ni mdogo.

Mheshimiwa Spika, faida ya kuwepo vitengo vya usimamizi wa vihatarishi ni nini? Yule mtu wa ukaguzi anapoendelea kuhangaika na ukaguzi wa vocha zile za malipo, anapohangaika kukagua risiti za manunuzi huyu mtu wa vihatarishi yeye anaangalia zile process na kuhakikisha anatoa assurance kwa hizi taasisi zetu za Serikali, Wizara, Idara za Serikali pamoja na mamlaka mbalimbali. Kwa hiyo, niwaombe Serikali kupitia Wizara ya Fedha na kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu waweze kulisimamia hili ili Idara zetu, Wizara zetu na Taasisi zetu wahakikishe vitengo vya vihatarishi vinaimarishwa katika Taasisi zao ili viweze kutoa assurance ya michakato mbalimbali ya investments na shughuli mbalimbali za Serikali zinazofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo ningependa kulichangia la kisera, linahusu uchumi wa kisasa, shirikishi na shindani. Ilani yetu ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, Ibara ya 18 imeliongelea hili, lakini pia hotuba ya Waziri Mkuu eneo la 14 imelielezea hili. Unapoongelea uchumi shindanishi maana yake lengo letu ni kufungamanisha hizi sekta za uzalishaji na mimi hapa kwa kifupi nitaongelea sekta ya kilimo, lakini pia na sekta ya viwanda.

Mheshimiwa Spika, asilimia zaidi ya 65 mpaka 70 ya Watanzania wako kwenye sekta ya kilimo, sasa kama tunavyoona Serikali imeanza kuweka mikakati mbalimbali ya kuimarisha kilimo tunachokiomba sasa hivi hali ya hewa nchini imekuwa haitabiriki, mvua hazitoshi, pia ukijaribu kuangalia pamoja na kutoa pembejeo maeneo mengi uzalishaji unakuwa mdogo, kwa sababu gani?

Mheshimiwa Spika, hali ya hewa, kuna mabadiliko ya tabianchi, tujikite sana kuwekeza katika kilimo cha umwagiliaji. Niwaombe Wizara ya kilimo, maeneo yenye skimu za umwagiliaji kama kule kwetu Igunga tuna skimu ya Mwanzugi ni kubwa sana, tuna Bonde la Wembele ambalo maji kwa mwaka mzima yanaishia tu yamekaa hayafanyi kazi, waboreshe hizi skimu, wazihuishe ili tuweze kuongeza uzalishaji. Hii itasaidia hata kupatikana kwa malighafi katika viwanda.

Mheshimiwa Spika, naweza nikatoa mfano mdogo hapa, hapa nchini sasa hivi tuna uhaba wa mafuta ya kula, kwa sababu mwaka jana kufika mwezi wa Tisa viwanda vingi vya uzalishaji wa mafuta ya kula vilikosa malighafi uzalishaji ni mdogo. Sisi huku tumeweka tozo za kulinda masoko ya ndani ya mafuta ya kula, tunadhibiti yale masoko ya nje, sasa yanapopungua, soko la ndani bidhaa zimekwisha, tunapoanza kutegemea bidhaa na mafuta kutoka nje matokeo yake yanakuja kama sasa hivi tunajikuta bei inaongezeka na kunakuwa na malalamiko ya wananchi kupanda kwa bei ya bidhaa, hususan mafuta ya kupikia au mafuta ya kula. Kwa hiyo, ninaomba tunapoweka hizi kanuni za kulinda masoko ya ndani, tuhakikishe kabisa tunakuwa na uthabiti wa kuhakikisha sekta ambayo inalindwa iwe na uwezo wa kujitosheleza kuzalisha, kama ni kilimo iweze kuzalisha malighafi za kutosha ziweze kwenda katika viwanda ili tuwe na bidhaa muda wote na tusijikute kwamba tunasababisha mlipuko wa bei.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ambalo naweza kulichangia kwa kifupi sana ni katika suala la uchumi shirikishi, lengo letu pia ni kuhakikisha tunaboresha mazingira ya wafanyabiashara. Niwapongeze Halmashauri ya Jiji la Dodoma wameweza kuanzisha soko zuri sana la wamachinga hapa ambalo lipo katikati ya Mji. Hii ndio namna ambayo tunaweza tukasema tunaboresha mazingira ya wafanyabisahara wadogo, huwezi ukatoka unasema unaenda kujenga soko la wamachinga kilometa 10 nje ya mamlaka ya Mji inakuwa ni ngumu. Kwa hiyo, unapoweka mazingira kama haya maana yake unaongeza mzunguko wa fedha, lakini pia ajira kwa wananchi, ajira kwa vijana zinapatikana kwa wingi, nasi kama ilani yetu ambavyo tumeahidi basi tunajikuta kwamba, tumeimarisha na tumeboresha biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa ni suala la urasimu. Tuombe kabisa pia Serikali sera zetu ambazo tunaenda tunapoboresha, hizi sera za kuhakikisha kwamba tunalegeza kuhakikisha kwamba tunalinda masoko ya ndani na kuongeza uzalishaji katika sekta ya uzalishaji tujikute tunapunguza urasimu. Mtu anapohitaji kuwekeza kama ni kiwanda au shughuli nyingine yoyote ya uzalishaji mali asijikute anatumia muda mwingi katika kutafuta vibali na kuzungushwa makoridoni.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Naunga mkono hoja asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kufungua dimba mchana huu wa kuchangia Hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unapoongelea masuala ya Utumishi wa Umma nchini na unapoongelea masuala ya Utawala Bora wasaidizi Namba Moja wa Mheshimiwa Rais ni hizi Ofisi mbili, Ofisi ya Katibu Mkuu Kiongozi na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma. Hawa ndiyo custodian wa mambo yote yanayohusu utawala wa nchi yetu, ndiyo custodian wa mambo yote yanayohusu Utumishi wa Umma, pia ndiyo custodian wa nyaraka zote za Serikali katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mantiki hiyo nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Jenista Mhagama Dada yetu kwa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kuwa Waziri wa hii Wizara. Lakini pia nimpongeze Kaka yetu Deo Ndejembi kwa kuwa Naibu Waziri.

Nimpongeze Mwalimu wangu Daktari Ndumbalo kwa kuendelea kuaminiwa kuwa Katibu Mkuu wa hii Wizara. Pia nimpongeze Xavier Daudi ambaye kwa sasa ni Naibu Katibu Mkuu wa hii Wizara ambae alikuwa ni Mtendaji Mkuu wa Sekretarieti ya Ajira wakati na mimi naingia Serikalini mwaka 2011. Tunawatakia kheri katika kazi zenu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchana huu nitachangia mambo matano ambayo ni mawazo yangu na ushauri na mapendekezo kwa Serikali ambayo naamini yatakuwa na mchango mkubwa katika kuboresha suala la Utumishi wa Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ni mfumo wa kuomba ajira Serikalini. Tuna huu mfumo unaitwa online application portal ambao uko chini ya Sekretarieti ya Ajira. Kwa sasa tunavyo Vyuo Vikuu vingi nchini kwetu lakini pia vinatoa kozi na mafunzo mbalimbali. Mfumo wetu kwa sasa bado unawanyima haki baadhi ya Watanzania katika kuomba maombi ya kazi. Unakuta watu wamesoma kozi hapa nchini au nje ya nchi lakini wanapofika hatua ya kuomba maombi ya kazi unakuta kozi kwenye huu mfumo wetu wa kuomba kazi haupo. Naomba Mheshimiwa Waziri na Wasaidizi wako mkalifanyie hili ili kufungua wigo wa Watanzania wengi kuweza kuomba ajira zinazotolewa na Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine katika mfumo huu ambalo linaonesha udhaifu wake ni wanapoandaa usaili wa waomba ajira. Unakuta wamesema tunahitaji watu wenye kozi zifuatazo, labda wanasema Business Administration, wanasema Economics and other related courses wale watu wanapoomba wakifika kwenye usahili wale watu walio-apply kwa kutumia other related courses siku ya usahili wanatolewa nje wanaambiwa kwamba kozi uliyoomba haihusiani na ajira uliyoomba.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ilitokea sana kwa watu wengi walipoomba kazi za TRA hivi karibuni walipofanya usaili. Mheshimiwa Waziri na Wasaidizi wako tunaomba pia mkalifanyie kazi hili jambo. Mfumo ufunguliwe, baadhi ya selection ziwe hata ikiwezekana mfumo uwe wa kuandika. Sasa hivi dunia ni ya sayansi na teknolojia watu wengi wamehitimu vyuo vikuu, wengine wamehitimu nje ya nchi. Kwa hiyo unapokuwa na mfumo unapokuwa na zile kozi ambazo ni common tu zinazotolewa na vyuo vya nchini, matokeo yake unajikuta watanzania wengi tunawaacha nje katika mfumo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambao ningependa kuchangia mchana huu ni suala la Watendaji Wakuu wa Taasisi, Mamlaka na Wakala kuendelea Kukaimu zaidi ya miezi sita. Mheshimiwa Waziri ukifanya utafiti, ukifanya screening katika Wizara, Idara na Mamlaka za Serikali, utakuwa bado kuna Watendaji Wakuu au Wakuu wa Idara au Wakurugenzi Wakuu bado wanakaimu na Kanuni zetu za kudumu za Utumishi wa Umma Toleo la 2009 zimeweka ukomo wa miezi sita, baada ya pale vetting inakamilika, mapendekezo yanakwenda kwenye mamlaka ya uteuzi kwa kupitia Wizara husika lakini kwa kuwa ninyi ndiyo Wizara kiongozi ni kama kiranja wa Wizara zingine kwa maana ya kwamba mna-deal moja kwa moja na mna-link moja kwa moja na Ofisi Namba Moja ya Ikulu kwa maana Ofisi Kuu ya Nchi. Kwa hiyo, tunawashauri jambo hili la upekuzi lisiwe kisingizio au kichaka cha kuchelewesha watu kuthibitishwa kazini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wanaokaimu zaidi ya miezi sita ni kinyume cha Kanuni za Utumishi wa Umma, ni kinyume cha Sheria ya Utumishi wa Umma wa nchi yetu. Tunaomba hili Mheshimiwa Waziri wewe Dada yetu ni msikivu utalisimamia vizuri na wale wenye sifa waendelee kuthibitishwa na waweze kuwa-full katika nafasi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ambalo ningependa kulichangia mchana huu ni suala la Watumishi wa Umma wanaojisomesha mafunzo ya muda mrefu. Mafunzo ya muda mrefu ni kama vile tunasema mtu amesoma digrii ya Kwanza, aliajiriwa akiwa na diploma ameenda kusoma digrii ya Kwanza amejiendeleza au alikuwa na digrii ya kwanza ameenda kusoma digrii ya pili, wanaporudi kazini kumekuwa na urasimu mkubwa sana katika kuwabadilisha madaraja lakini pia kuwabadilisha kada. Kwa mfano, kama mtu anahitaji kufanyiwa re-categorization unakuta mtu alikuwa ni Katibu Muhtasi ameenda kusoma amepata degree ya Human Resource tuchukulie mfano rasilimaliwatu anatakiwa aje afanyiwe re- categorization awe Human Resource Officer lakini mpaka aje afike hiyo hatua atasugua sana miguu, atapambana sana na mabosi matokeo yake ni urasimu mtupu na inatengeneza mazingira ya rushwa katika Ofisi za Umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba Wizara mlisimamie hili jambo wale wanaostahili mpaka Mtendaji Mkuu au Mamlaka ya Ajira inapotoa kibali cha mtu kwenda kusoma maana yake imeshajiandaa. Sasa unapotoa kibali mtu akirudi kazini unaanza kumfanyia urasimu tunakuwa hatuwatendei haki Watumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la Nne ni suala la mikataba ya huduma kwa mteja. Maboresho katika Civil Service ambayo yalianza miaka ya 1995 wakati huo Katibu Mkuu Kiongozi alikuwa Martin Lumbanga, yalikuja na mapendekezo mengi ikiwepo suala la kuanzisha Client Service Chatter mikataba ya huduma kwa mteja. Sasa lengo hapa ni kuhakikisha mteja kwa maana ya kwamba ama Mtumishi ndani ya Taasisi au mteja anayetoka nje ya Taasisi kupata huduma ya viwango lakini kwa wakati, tunaomba hili Mheshimiwa Waziri mlisimamie.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila Taasisi ihakikishe wana mkataba kwa mteja na ioneshe huduma inayotoa, mteja atatumia siku ngapi kuipata. Kama akiwa anatakiwa kulipa malipo ya awali au amekamilisha maombi, application aambiwe siku 14 kama ni umeme utafungiwa ili kuwe hakuna ujanja ujanja wa kutafuta link na connection. Kama ni suala labda Mfumo wa Jamii au Hifadhi ya Jamii ukikabidhi maombi yako ndani ya miezi mitatu umepata fedha zako. Hii itasaidia sana kutoa malalamiko, itasaidia kutoa usumbufu kwa Waheshimiwa Wabunge katika kuhakikisha wanafuatilia mambo mbalimbali ambayo tu ni mfumo ungewekwa na yangekuwa yamerahisishwa katika kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine la tano na la mwisho ambalo ningependa kulichangia mchana huu ni suala la Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora. Katika historia ya nchi yetu mwaka 1984 Serikali ya kwanza ya Mwalimu Nyerere ilileta Bill of Rights humu Bungeni. Ndiyo ikawa msingi wakuwa na haki za binadamu katika Taifa letu na zikaingizwa katika hii Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Ibara ya 129 na Ibara ya 130 imeeleza majukumu ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, kwa ridhaa yako ningeomba ninukuu mambo mawili ama matatu ambayo ningependa niyachangie kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma Ibara ya 130 Sehemu ya Kwanza, majukumu ya Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora. Jukumu Na. (b) Kufanya shughuli za kupokea malalamiko ya uvunjifu wa haki za binadamu kwa ujumla, kufanya uchunguzi juu ya mambo yanayohusu haki za binadamu na ukiukwaji wa misingi ya utawala bora, kufanya utafiti, kutoa na kueneza nchini elimu kwa umma kuhusu haki za binadamu na utawala bora na ikibidi kufungua mashauri mahakamani ili kuzuia vitendo vya uvunjifu wa haki za binadamu na kurekebisha haki inayotokana na kuvunjwa huko kwa haki za binadamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba nichangie kwa kifupi. Hii Tume yetu ya Haki za Binadamu na Utawala Bora kwa sasa Mheshimiwa Waziri kama vile bado imelala. Tunaomba muende mkawaamshe kidogo hususani kwenye suala la kutoa elimu ya haki za binadamu na utawala bora kwa Watanzania. Mfano mzuri, ninyi chini ya ofisi yenu mnayo TAKUKURU. TAKUKURU wanajitahidi sana kutoa elimu kwa wananchi, wana vipindi kwenye Vyombo vya Habari, wanakwenda mpaka kwenye ma-group ya WhatsApp na hii mkiifanya tume ya haki za binadamu mfanye vizuri ndiyo itakuwa shock absorber mtapunguza hata yale maswali Mheshimiwa Rais yuko sehemu ana ziara unakutana na mabango ya wananchi wanalalamika. Unakuta Mheshimiwa Rais yuko amealikwa kwenye sherehe za siku ya Mahakama au siku ya Sheria Duniani, Mama au Baba anatoka na bango amedhulumiwa haki zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii Tume itasaidia sana kupunguza migogoro, itasaidia kupunguza manung’uniko ya wananchi lakini kiujumla itawasaidia nyinyi Watendaji wa Serikali ndiyo maana composition yake imewekwa watu ambao wana weledi pia hata upatikanaji wao imeshirikisha vyombo vikubwa vya nchi, lengi likiwa ni kuweka watu ambao ni credible wataisaidia Serikali, watamsaidia Mheshimiwa Rais na watawasaidia ninyi katika uendeshaji wa kazi zenu za kila siku na kuzipunguzia taasisi nyingine shughuli kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, waamsheni, waambieni waingie field hawa siyo Criminal Investigation Department hawa ni ombudsmen hawa ni watchdog wa Serikali, watawasaidia na tutasonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Maazimio mawili yaliyopo mbele yetu; azimio la kuenzi kazi za Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Azimio la kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitoe pole kwa Taifa la Tanzania kwa kuondokewa na Rais wetu, nitoe pole kwa familia ya marehemu kwamba tumeondokewa na kiongozi ambaye tulikuwa tunampenda lakini Mwenyezi Mungu amempenda zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wangu nitaongelea mambo kama mawili au matatu kumhusu Mheshimiwa Dkt. Magufuli. Mwaka 1775 -1783, Marekani walikuwa katika vita vya mapinduzi vya kujitelea uhuru. Baada ya kupata uhuru Wamarekani walifanya utafiti kupitia chuo kinaitwa National Institute of Psychology. Katika chuo kile walifanya utafiti ili kujua unapotaka kufanya mabadiliko katika nchi au katika taasisi yaani institutionalization unatakiwa kufanya vitu gani. Marekani walikuja na vitu saba ambavyo walisema lazima waviweke katika vichwa vya watu wao. Jambo la kwanza walilogundua ni kubadilisha attitude na mindset za watu wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo kubwa ambalo Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ametusaidia kama Taifa ni kubadilisha attitude na mindset zetu Watanzania ambapo ilifikia hatua tukawa tunatembea na falsafa kuwa Watanzania siyo masikini na sisi Watanzania siyo maskini na Taifa letu ni tajiri. Jambo hili limeweka msingi mkubwa ambapo imefikia kama taifa tunatumia rasilimali za ndani kuleta maendeleo. Taifa linajiendesha, tunajenga vituo vya afya, tunajenga miundombinu na kila kitu ambacho kinaweka misingi ya maendeleo katika kuhakikisha Taifa letu linasonga mbele. Kwa hiyo, katika hili tutamuenzi Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na hakika tunaendelea kutamba na kutembea kifua mbele kwa ujasiri sisi Watanzania ni matajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni tekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 kwa ufanisi mkubwa sana. Katika hili hakuna ubishi. Unapoongelea Ilani ya Chama cha Mapinduzi kuna kitu kinaitwa Mwelekeo wa Sera za Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwelekeo wa Sera za Chama cha Mapinduzi wa mwaka 2010-2020 ulitaka Serikali ya Chama cha Mapinduzi itakayoingia madarakani 2015 iweke msingi wa kuhakikisha tunafikia uchumi wa kati ifikapo 2025. Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akishirikiana na Makamu wake wa kipindi kile mama Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Majaliwa na Bunge la Kumi na Moja tulifika uchumi wa kati mwaka 2020, miaka mitano kabla. Hili ni jambo la msingi na la kuenziwa na sisi tunawashukuru mliokuwa katika safari ya Bunge la Kumi na Moja. Kwa hiyo, haya ni mambo makubwa na ya msingi ambayo Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyafanya katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ambalo Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Serikali yake ya Awamu ya Tano wamelifanya ni kuhakikisha tunakuwa na mfumo wa malipo Serikalini ya kielektroniki tunasema e-payment. Tulihama kutoka mfumo wa billing system tukaenda electronic payment na tuka-establishi kitu kinaitwa Government Electronic Payment Get Way jambo ambalo leo hii tunatamba na kusema tunajitahidi kukusanya mapato lakini ni kwa sababu ya mfumo imara wa ukusanyaji ambao umehakikisha mapato yanatoka na kwenda katika chungu kimoja. Katika hili tunamshukuru Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Serikali yake ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo kwa upande wa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, nije katika suala la kumpongeza Rais mama Samia Suluhu. Nimesimama hapa kwa niaba wananchi wa Jimbo la Igunga, Mkoa wa Tabora, tunampongeza kwa kuapishwa kuwa Rais wa Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa kuwa alikuwa sehemu ya Serikali ya Awamu ya Tano ya Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, tunaamini gurudumu atalipeleka vizuri, tutakwenda vizuri kama Tanzania na sisi wananchi wa Igunga tupo tayari kumuunga mkono. Walituletea maji ya Ziwa Victoria, tuna tenki kubwa la maji Igunga lenye uwezo wa kubeba maji lita milioni mbili na laki tano kwa wakati mmoja. Tunawashukuru na kuwapongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepata umeme vijiji 30 na sasa tunakwenda kupata umeme vijiji 30 vingine. Jimbo la Igunga tutakuwa na umeme jimbo zima tunawashukuru sana. Pia tumehakikishiwa na tumeendelea kujengewa Chuo cha Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) ambacho kwa mara ya kwanza kiwanja chake kilipatikana mwaka 1995. Serikali ya Mheshimiwa mama Samia Suluhu Hassan na Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli iliyopita wametoa fedha sasa tunajengewa Chuo kikubwa cha Mafunzo ya Ufundi Stadi katika Jimbo la Igunga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kifupi Jimbo la Igunga tunamtakia kheri, tupo naye tutamuunga mkono na tutapigana usiku na mchana kuhakikisha Ilani ya Chama cha Mapinduzi inatekelezwa. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti ya Wizara ya Maji jioni hii. Kwanza nianze kwa kutoa pongezi, nimpongeze kaka yangu Mheshimiwa Juma Aweso kwa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kuendelea na jahazi la kubeba dhamana ya kuhakikisha tunapata maji Watanzania. Nimpongeze dada yangu Mheshimiwa Mhandisi Maryprisca Mahundi naye pia kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kuendelea kumpa msaada Mheshimiwa Waziri. Nimpongeze Ndugu Injinia Anthony Sanga Katibu Mkuu wa Wizara naye kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuwa mtendaji mkuu wa hii Wizara pamoja na Naibu Katibu Mkuu wake dada yetu Kemikimba. Tuwatakie heri, Mwenyezi Mungu awasimamie katika utendaji kazi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na Waheshimiwa Wabunge nadhani mtaungana na mimi moja ya Wizara ambayo inatupa ushirikiano wa karibu sana ni Wizara ya Maji inayoongozwa na Mheshimiwa aweso. Mmekuwa karibu sana, lakini pia mmekuwa watu wenye kutuitikia kwa haraka sana tukiwapigia simu mnapokea, tukiwatumia message mnatujibu na hata tukiwaomba appointment mnatupa nafasi ya kutuona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hiyo pia, niwapongeze wasaidizi wenu wa karibu sana ambao kwa sisi Wabunge wamekuwa wakitupa ushirikiano pale Wizarani nikianza na CPA Joyce Msilu ambaye amekuwa akitupa sana ushirikiano, huyu ni Mkurugenzi wa Usambazaji Maji. Makatibu wako wote wawili Gibson George pamoja na Jafari Athuman na wenyewe wanatupa sana ushirikiano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna wale akinamama secretary pale wasaidizi wako ofisini kwa kweli utawafikishia salamu zetu, siwafahamu majina wapo wawili pale, tukifika mara nyingi wanatupokea vizuri na wanatukirimu. Wakati mwingine hata tukija kama tuna njaa Mheshimiwa baada ya vikao vya saa 07:00 huwa wanatuweka vizuri pale. Hata kama kuna ka-OC kakuongeza Waziri walinde zaidi wale akinamama na Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipowapongeza wasaidizi wako katika ngazi ya mkoa na wilaya nikianza na Mhandisi Lameck Kapufi ambaye ni Meneja wa RUWASA Mkoa wa Tabora, lakini pia Engineer Hussein Nyemba ambaye ni Meneja wa Mamlaka ya Maji Igunga. Mkurugenzi Mtendaji, kijana ambaye anaupiga mwingi sana, lakini pia na Meneja wa RUWASA Mhandisi Marwa Mulaza pamoja na wasaidizi wao wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, waswahili wanasema waswahili wanasema usiposhukuru basi hauna shukrani. Nilitaka kwenda na ule msemo wa Mheshimiwa Waziri, lakini nimeuchapia kidogo, mimi nilikuja na huu kwa maana ya kushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi pale kwetu Igunga tuna mradi mkubwa wa maji ya Ziwa Viktoria ambao Serikali ya Chama Cha Mapinduzi imewekeza bilioni 620. Maji yametoka Mwanza na kufika Igunga takribani kilometa 400, hii ni legacy kubwa sana ya Chama Cha Mapinduzi kwa wananchi wa Jimbo la Igunga, lakini pia na kwa maeneo ya Mkoa wa Tabora ukienda Nzega pamoja na Tabora Mjini na sasa unaelekea maeneo ya Kaliwa, Urambo na Sikonge. Nawashukuru sana Wizara kwa kusimamia huu mradi mkubwa wa kihistoria ambao umetatua changamoto kubwa sana ya maji katika eneo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia niwashukuru kwa kuendelea kutupa support, tuna miradi ya maji mmeendelea kutupatia. Niliingia Jimbo la Igunga takribani huu ni mwaka wa pili, lakini tuna miradi zaidi ya saba ambayo inafanya vizuri sana katika eneo letu. Tumepeleka maji mpaka kule Mwamashimba karibu na Shinyanga, eneo ambalo lilikuwa ni gumu sana kufikiwa na maji. Mheshimiwa Aweso tuliomba fedha ukatupatia kwa maombi maalum na sasa tunakunywa maji ya Ziwa Viktoria tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi pia ya maji mingine ambayo inaendelea na usambazaji, lakini nishukuru zaidi pia kwa mwaka huu wa fedha mmetutengea bilioni moja kwa ajili ya kuunda mfumo wa maji taka katika Wilaya yetu ya Igunga. Hii ni historia nyingine ambayo tutakwenda kuiandika tutakuwa na mfumo wa maji taka katika mji wetu, jambo ambalo katika hali ya kawaida ilikuwa haiwezekani, lakini kwa ushirikiano ambao umetupatia Mheshimiwa Aweso na umetutengea fedha, tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuchangia mambo mawili kama ushauri katika kuhakikisha tunaboresha kazi zetu za usambazaji wa maji. Eneo la kwanza ambalo ningependa kuwashauri jioni hii, sisi ambao tumebobea sana katika masuala ya kiutawala huwa tuna principle moja au kanuni inasema kwamba, unapoongoza eneo dogo mara nyingi tunategemea ufanisi ni mkubwa.

Sasa kuna eneo moja ambalo mnaweza mkaliangalia na wasaidizi wako mlifanyie kazi; kwenye wilaya ambazo zina mamlaka mbili za maji kwa mfano Igunga tuna mamlaka ya mjini ambayo ni IGUWASA na mamlaka ya vijijini RUWASA, jitahidini kuwagawia maeneo haya watu ili angalao waweze kusaidiana katika kutatua changamoto ya maji. Tusijikute hizi mamlaka za mjini kati ya maeneo ya Mamlaka ya Mji unakuta kwa mfano Igunga mamlaka yetu hii ya mjini inahudumia kata takribani tatu, lakini mamlaka hii ya vijijini ina kata zaidi ya 34 kwa hiyo, inajikuta mzigo mkubwa unamuendea yule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama unavyoelewa sisi hapa tuna life span, tuna miaka mitano, lakini bajeti yetu inakwenda annually na kila annual moja ina quarter nne. Sasa ukijikuta huyu ana miradi mingi kwa mfano RUWASA, kama mfano Tabora tuna majimbo 12 kama kila jimbo tu likiwa lina miradi minne maana yake ana miradi kama 48. Sasa miradi 48 kwa mwaka mmoja kwa mtu anayetegemewa mkoa mzima utekelezaji wake na ufanisi utakuwa mdogo ndio maana nimekuja na hii hoja ya kusema tuwapunguzie maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukachukulie mfano kwa Igunga ukimpa IGUWASA hata kata 10 yule mwingine akabaki na kata zile 20 ufanisi utakuwa ni mkubwa hata mwaka mmoja unapokuja kufanya tathmini performance unajikuta performance iko vizuri.

Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nikasema nishauri hili mlichukue na ninadhani unaelewa tulifika Wizarani tukaliomba na umesema hivi karibuni utatupatia ile GN ili IGUWASA iweze kuongeza mtandao wao wa kutoa maji, tunashukuru sana kwa kupokea pia ombi letu hilo. Hili unaweza ukaliangalia pia maeneo mengine linaweza likasaidia kujenga ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa pili lilikuwa ni suala la manunuzi, hata mdogo wangu Mheshimiwa Arthur Makanika hapa aliliongelea. Ni suala la ku-centralize, ukifanya centralization katika mfumo wa manunuzi kwa mfano kwa Mkoa wa Tabora tunaposema majimbo 12, ukiwa na miradi minne-minne, anapofanya manunuzi mtu wa mkoani inapofikia hatua mfano inahitajika tu koki, mpaka itoke mkoani waanze zile process maana yake ndio hii unakuta mradi wa bilioni moja imekosekana koki ya milioni mbili hamna mradi unaendelea pale, tutaendelea kuwasumbua sana kama Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ninadhani unakumbuka hata sisi Igunga lilitokea hili. Tulikuwa na mradi mmoja wa Mwalala ulikuwa chini ya RUWASA, ilikufa pump ilihitajika milioni 11 tu, ilitusumbua zaidi yam waka mmoja wananchi wakawa hawapati maji, lakini ulipotoa maelekezo kwa Mkurugenzi Mtendaji wa IGUWASA alienda alipiga kambi pale siku moja, saa 07.00 usiku mzigo umenyanyuka, tumemaliza kwa sababu, mamlaka za mjini wana uwezo wa kununua wao wenyewe palepale wanafanya procurement katika ngazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti kwa hiyo, angalieni Instrument Act ya RUWASA mbadilishe hii item. Mnaweza mka-categorize, kwenye ngazi ya wilaya kuna manunuzi labda ya kwenda mpaka milioni kadhaa, ngazi ya mkoa wanakwenda milioni kadhaa halafu na Taifa mnaenda na miradi mikubwa ya billions of money, sawa Mheshimiwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani hapo tutakwenda vizuri. Itawasaidia kupunguza sana jam ili matatizo madogomadogo haya sijui pump imeungua inahitajika waya milioni moja milioni mbili, ukaanza mchakato wa manunuzi wa kuchukua muda mrefu, tutajikuta tunakaa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niwashukuru sana kwa ushirikiano mkubwa mnaoendelea kutupatia. Sisi tupo kazini kama ambavyo tunasema na mama yetu tunamshukuru sana anatenga fedha nyingi za miradi ya maji na sisi tunashukuru. Aliposema atamtua mama ndoo kichwani, kweli anamtua ndoo kwa vitendo na sisi tunasema sana tunaishukuru Serikali ya Chama Cha Mapinduzi. Naunga mkono bajeti ya 2022/2023, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Bajeti Kuu ya Serikali jioni hii. Kwanza kabla ya kuchangia nilikuwa nataka nitoe pongezi zangu kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa statement ya kusamehe madeni ya wafanyabiashara ya miaka ya nyuma. Jambo hili ni kubwa, limejenga confidence kwa wafanyabiashara, limeleta harmonization na sasa wafanyabiashara wetu wanafanya biashara zao kwa amani. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni suala la elimu bila malipo. Tunamshukuru pia Mheshimiwa Rais kwa kutoa dira na sasa tutakuwa na wanafunzi wanasoma kuanzia Darasa la Kwanza mpaka Kidato cha Sita bure. Kwa sisi ambao tumetoka kwenye jamii za wakulima na wafugaji tunajua thamani ya jambo hili, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni nyongeza ya mishahara kwa Watumishi wa Umma. Mheshimiwa Rais ameongeza mshahara kwa watumishi wa Umma, tunamshukuru pia kwa hili, kwa kuona hii sekta ya muhimu katika uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na jambo la nne ambalo ningependa kutoa pongezi ni suala la udhibiti na usimamizi wa fedha za umma. Tunashukuru sana kwa Serikali kuchukua mawazo mbalimbali ya Bunge toka bajeti ya mwaka 2021 tulipokuwa tukichangia na Mpango wa Maendeleo ya Taifa, tulisema kwamba, Ofisi ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali zijengewe uwezo; na kwa safari hii wameliona, ofisi zote mbili, kwa maana ya Internal Auditor General na Ofisi ya CAG kwa maana ya National Audit Office wamejengewa uwezo na wametengewa fedha za kutosha kwa ajili ya kuimarisha kazi zao. Tunawashukuru na kuwapongeza Serikali kwa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina mambo takribani sita ningependa niyachangie jioni hii, ambapo nitayachangia kwa ufupi ili niweze kuyamaliza. Jambo la kwanza nitachangia ni mfumo wa kodi na ukusanyaji wa mapato nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1977 ilipovunjika Jumuiya ya Afrika Mashariki tulianza mchakato wa kuirejesha mwaka 1999 na mwaka 2000 Jumuiya ya Afrika Mashariki ikawa imeanza. Tuliporudi kwenye Jumuiya ya Afrika Mashariki nchi zilizokuwa tatu zikiunda Jumuiya ya Afrika Mashariki wakati huo, kila moja ilikuja imeboresha mfumo wake wa ukusanyaji kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Uganda walikuja na mamlaka yao ya mapato wanaita Uganda Revenue Authority ambayo waliitengeneza mwaka 1991. Kenya walikuja na mamlaka yao ya mapato wanaita Kenya Revenue Authority, (Mamlaka ya ukusanyaji Mapato ya Kenya) ambayo waliitengeneza mwaka 1995, na sisi Tanzania tukaingia na mamlaka yetu ya ukusanyaji wa mapato ambayo tuliitengeneza mwaka 1995 chini ya utawala wa Mheshimiwa Hayati Benjamin Mkapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifuatilia study mbalimbali na chambuzi mbalimbali, mpaka sasa tunapoongea Mamlaka yetu ya Mapato Tanzania ni moja ya mamlaka za mapato bora sana katika ukanda wa Afrika Mashariki na Kati na nchi za Kusini mwa Jangwa la Sahara. Tuna mfumo mzuri wa uendeshaji, lakini tuna mfumo mzuri wa muundo kwa maana ya institution, lakini tuna changamoto ambayo tukiweza kui-address inaweza ikawa na msaada sana katika ukusanyaji wetu wa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wetu wa mapato, tuna kodi za aina mbili; tuna kodi za moja kwa moja kwa maana ya kusema direct tax. Pia tuna kodi ambazo siyo za moja kwa moja kwa maana ya indirect tax kwa mfano VAT. Changamoto kubwa tuliyonayo ni kwenye kodi za moja kwa moja na hususan hapa tunapokenda kwenye income tax. Nitaongea kidogo, niwaombe Serikali mlichukue mliangalie, hata kama siyo bajeti ya mwaka huu, basi bajeti ya mwakani mnaweza mkaliangalia, kwani litapunguza sana usumbufu kwa wafanyabiashara wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi kodi ambazo ni direct, (za moja kwa moja), kwa mfano tuna corporate tax, tuna withholding tax, tuna income tax, tuna service levy, na kadhalika; ukija katika mfumo wa hizi kodi za moja kwa moja kwa mfano kodi ambazo zinahusisha vibali na leseni, huwa hazina changamoto sana kwa sababu, zenyewe zina tozo ambazo zimepangwa ziko fixed. Kwa hiyo, mtu anajua mimi ninapotaka kuanzisha biashara, leseni yangu ni kiasi fulani. Nataka nisajili kampuni, badaye nitatakiwa kulipa kiasi fulani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto inakuja kwenye hizi biashara ambazo tunahitaji kufanya bargaining, kwa wafanyabiashara wa hizi biashara zetu za kawaida kwenye kodi ya mapato, ndiyo shida kubwa inapoanzia hapo inaleta manung’uniko. Inasababisha mambo makubwa matatu; jambo la kwanza, kunakuwa kuna inconsistency. Unakuta mfanyabiashara mmoja ana kiwango sawa na biashara ya mwingine na mtaji sawa, lakini mapato na kodi wanalipa tofauti. Matokeo yake inaleta malalamiko kwa wafanyabiashara wetu. Kwa hiyo, tunaomba Serikali mlichukue hili mchakate vichwa na wataalamu wenu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu, muweze kuja na mpango mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbele ya safari mje na scientific approach ya kukusanya hizi kodi, tuondokane na huu mfumo wa bargaining na ku-compromise, unasababisha pia rushwa kwa wananchi, matokeo yake tunajikuta kwamba Maafisa wetu wa TRA wengi wana-compromise wanaingia katika mitego ya rushwa. Anakwambia ili nikukadirie kodi kiasi fulani, basi hii hela nyingine nipe mimi, weka pembeni au kampatie mtu fulani. Hii ndiyo msingi wa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo, kama Wizara, kama taasisi mliopewa dhamana ya kusimamia masuala ya kodi nchini chakateni vichwa, tumieni wataalamu wenu, shirikisheni wasomi mbalimbali mje na schedule, au scientific approach itakayotusaidia kama nchi kutoka hapa tulipo tusiendelee kuwa na mfumo wa kodi wa kufanya bargaining na matokeo yake inasababisha rushwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia madhara ya huu mfumo Serikalini yanaleta inefficiency, maana yake ufanisi unakuwa haupo, na ndio maana unakuta tunakadiria kodi, tunasema tutakusanya Shilingi trilioni 31, matokeo yake tunaishia kwenye Shilingi trilioni 27. Hii ni kwa sababu tunajikuta tunaweka viwango ambavyo siyo realistic. Kwa hiyo, katika hilo naiomba Serikali ilichukue na ilifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili la msingi ninalopenda kuchangia ni ushirikiano kati ya Serikali na wafanyabiashara katika dhana ya kujenga uchumi jumuishi. Tunasema tunajenga uchumi jumuishi na uchumi wa watu. Sasa Mheshimiwa Waziri naomba hili tuliangalie, kuna wafanyabiashara wa juu, wa kati na wa chini. Wote katika kipindi hiki ambacho tunafanya transformation, basi tujitahidi kuwagusa kadiri ya changamoto wanazokabiliananazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mimi naweza nikatolea mfano kwangu pale Igunga, kuna wafanyabiashara takribani 209 walinyang’anywa vibanda na Serikali kwa maana ya kupitia Halmashauri. Mheshimiwa Jafo alianza kulifanyia kazi hili, akaja Mheshimiwa Ummy na nimemuona Mheshimiwa Bashungwa. Tunaomba hili Serikali mlichukue mlifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyabiashara ambao ndio chanzo cha kutoa kodi, na pia ni wadau wa maendeleo katika maeneo yetu ambao wanatoa ushirikiano kwa Serikali na kwa chama chetu, wanapokuwa wanasumbuliwa na kunyang’anywa vibanda vyao kabla ya mkataba; mkataba umenyang’anywa na Serikali kabla ya miaka miwili, tunaomba Serikali ilimalize hili, wafanyabiashara wetu warudishiwe vibanda vyao. Mkataba wao utakapoisha, watakaa mezani na Serikali, wataweza kujadiliana. Tunafungua nchi. Katika kufungua nchi, ndiyo namna hii ya kuwasaidia wafanyabiashara hata wa ngazi ya chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu napenda kuchangia jioni hii ni suala la mafao ya wastaafu. Katika nchi mpaka sasa tunafanya vizuri na niwapongeze Serikali mnakwenda vizuri; kumekuwa na changamoto moja katika suala la mafao. Unakuta mstaafu anastaafu kwa Daraja F, lakini mafao analipwa kwa Daraja E. Hii nayo imekuwa ni changamoto kubwa na ninadhani maeneo mengi katika nchi hili limekuwa ni tatizo. Mwingine amestaafu kwa kutumia Daraja G, lakini analipwa Daraja F. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuwaombe Serikali muweke modality nzuri ya kuhakikisha mtu anapofikia hatua amestaafu, kuna zile tunaita declaration; katika zile fomu asaini tamko la mwisho kwamba hiki ndiyo kiwango cha mafao yangu nitakayoyapata, ili tuepushe usumbufu kwa hawa watu wanapostaafu. Kwani hela wanazopewa za pension wanaanza tena kutumia katika nauli za kuja Dodoma au kwenda Dar es Salaam katika kufuatilia mafao yao. Ni usumbufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inapofikia mwisho mtu anastaafu, akiwa anaondoka kwa Afisa Utumishi wake au kwa mwajiri wake anajua mimi nitapokea Shilingi milioni 50, hii mwisho na anaweka saini kwenye tamko, maana yake hatakuwa na usumbufu mwingine wowote. Hawa ma-accounting officers kwa maana ya waajiri, kama mtu bado ana tatizo kuhusu mafao yake asiruhusiwe kusaini ile declaration kwa sababu inakuja kuwa ni usumbufu baadaye. Kwa hiyo, naomba Serikali mlichukue na lenyewe muweze kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne ningependa kuchangia jioni hii ni suala la ruzuku ya pembejeo za kilimo. Naishukuru na kuipongeza Serikali, mmeongeza fedha kwenye kilimo, mmeweka fedha za pembejeo. Hapa Serikali naomba mtusaidie maeneo mawili, jambo la kwanza Serikali tunaomba ruzuku iliyotolewa iwahusishe walengwa, iwafikie walengwa ambao ni wakulima wetu wote ambao wapo katika maeneo mbalimbali ya nchi hii. Kumekuwa na tabia au ukiangalia historia, maeneo mengi ambayo fedha za Serikali huwa zinapigwa, ni ama zimetoka kwenye ruzuku kwa maana ya subsidy au zile stimulus package. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba katika hili Serikali, naamini Wizara ya Kilimo kaka yangu Mheshimiwa Hussein Bashe na kaka yangu Mheshimiwa Mavunde mtalisimamia vizuri, ruzuku hii iweze kuwanufaisha wakulima wetu. Jambo la pili mtakalotusaidia hapa, ruzuku hiyo ifike katika kipindi kinachoendana na misimu ya kilimo. Tunaomba kama ni pembejeo tutakapozipata zikitoka ambazo zimeambatanishwa kwa ruzuku hii, basi zifike katika kipindi kinachohusisha misimu ya kilimo tusije tukapishana na msimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tano ni suala la nishati. Napenda kuchangia kwenye suala la umeme na mradi wa bomba la mafuta la kutoka Uganda kwenda Tanga. Sisi Igunga hili bomba linapota pale. Kuna baadhi ya wananchi walipitiwa, wanatakiwa kulipwa fidia. Walishafanyiwa assessment, wamefungua account, lakini mpaka leo hawajalipwa fidia zao. Naomba wananchi wa Igunga walipwe hii fidia. Wamelipa fidia eneo la Bulyang’ombe tu pale ambapo wanajenga site camp, lakini maeneo ambayo bomba linapita bado hawajalipwa fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna vitongoji ambapo bomba linapita walisema wakati wanatambulisha mradi kwamba watapeleka umeme.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba pia umeme katika hivi vitongoji uweze kupelekwa ili hata watakapoanza shughuli zao za bomba basi umeme uwepo wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ningependa kuchangia jioni hii ni suala la…

MWENYEKITI: Mheshimiwa kengele ilishalia.

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Naam!

MWENYEKITI: Kengele yako ilishalia, nimekuachia umalizie hiyo sentensi.

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nashukuru. Naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi ya kuchangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa 2024/2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2000 wakati tunaweka Dira ya Maendeleo ya Taifa kwa maana ya 2000/2025 kama Taifa tuliweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha tunapambana na umaskini na kukuza uchumi. Tulianza na Mkakati wa Kupunguza Umaskini (Poverty Reduction Strategy Paper) tukaja MKUKUTA I, MKUKUTA II na sasa tumeingia katika ungwe ya Mpango ya Maendeleo ambayo kwa sasa tupo Mpango wa Tatu wa 2021 mpaka 2026. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipo hapa na niliposikia na kuchangia Mpango wa 2021 nilijipa kazi ya kufanya utafiti kidogo na kujua vitu gani vinatushika miguu kama Taifa katika kuhakikisha mipango yetu inafanikiwa. Jambo la kwanza, nilipitia Dira ya Maendeleo ya Taifa na kuona malengo makuu matano ambayo yameenda na Dira ya Maendeleo ya Taifa. Lengo la kwanza ilikuwa ni kuboresha hali ya maisjha ya Watanzania; lengo la pili kuwepo mazingira ya amani, usalama na umoja; lengo la tatu kujenga utawala bora; na lengo la nne ilikuwa kuwepo kwa jamii iliyoelimika vema na kujifunza na lengo la tano ilikuwa ni kujenga uchumi imara unaoweza kukabiliana na ushindani kutokana na nchi nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kupitia hayo malengo nilikuja kubaini kuna baadhi ya mambo, nilibaini mambo mengi lakini leo nitachangia mambo kama manne ambayo yamekuwa yakituvuta miguu katika kuhakikisha Taifa letu linakimbia katika kufikia malengo ya Mpango wa Maendeleo Taifa lakini pia katika mipango hii ambayo tumekuwa tukijiwekea na leo tuko Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo nimekuja kuligundua katika utafiti wangu mdogo ambalo linatushika miguu kwa kiwango kikubwa ni urasimu katika sekta ya umma. Serikalini bado kuna urasimu mkubwa sana jambo ambalo limekuwa likitukwamisha sana katika kukimbia. Unaenda kwenye ofisi za Umma jambo linalohitaji kufanyiwa maamuzi ndani ya siku mbili au siku tatu linakaa zaidi ya wiki mbili mezani na inatakiwa watendaji wetu wachukue mfano wa Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Wabunge tutakapopitisha sheria itakapofika kwenye meza ya Mheshimiwa Rais huwa haichukui zaidi ya masaa 24 Mheshimiwa Rais ameshasaini zile sheria. Ninyi kama viongozi wetu mnatupatia taarifa Bungeni lakini bado kwenye utumishi wetu wa umma urasimu umekuwa ni mkubwa vitu vinakaa muda mrefu mezani, hata kwenye suala la uwekezaji, tunawakatisha tamaa wawekezaji kwa sababu ya urasimu ambao unaendelea. Waheshimiwa Mawaziri ambao mmewasilisha leo taarifa zenu tunaomba hili jambo mshirikiane na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma lakini na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa ambapo kuna asilimia 80 ya watendaji wote, urasimu upungue ili tuweze kusonga mbele na tuweze kukimbizana kama Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nilishawahi kutoa pendekezo moja, hakikisheni kwenye kila taasisi na Idara za Serikali wana Client Service Charter, kwa maana ya mkataba wa huduma kwa mteja. Wapeni muda, file likifika mezani ndani ya masaa 48 liwe limetoka ila tukiendelea, mtu anatoka ofisini hakaimishi ofisi anaenda kwenye kazi field anafunga ofisi anatumia siku tatu, nne ofisi imefungwa file limelala. Mwisho wa siku hata wananchi wetu tutaendelea kuwakatisha tamaa. Kwa hiyo, jambo la urasimu tuliangalie sana, linatukwamisha katika maendeleo yetu na kutekeleza Mipango ya Maendeleo ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ni jambo la muhimu sana ni miundombinu ya kiuchumi. Katika suala la miundombinu ya kiuchumi tunasema hii ndio ile mishipa ya damu katika uchumi wa Taifa letu na hapa naongelea suala la umeme, barabara, reli, mawasiliano na huduma za kifedha. Kwenye suala la umeme, tunaomba kabisa Serikali kwenye huu mpango muende mkalisimamie Bwawa la Mwalimu Nyerere likamilike tuanze kuzalisha umeme wa uhakika. Uzalishaji wa sasa kwa kutumia mafuta umekuwa na hasara kubwa sana kwa wawekezaji wa nchi hii, lakini pia katika ukuzaji wa uchumi ni jambo ambalo limekuwa likilitia hasara lakini pia na gharama ya uzalishaji imeongezeka matokeo yake tunawatia hasara wawekezaji wetu, wazalishaji na pia tunaathiri uchumi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwenye suala la barabara kumekuwa na mkazo sana, tumejikuta tumeweka nguvu kubwa sana, tumetengeneza hizi barabara kubwa kwa maana ya trunk roads highways. Tunaomba sasa Serikali muweke mkazo kwenye barabara za ndani feeder roads ambazo ndizo zinalisha maeneo mengi zinatoa uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano, pale kwetu Igunga tuna barabara moja ya Igulubi – Mutu – Igunga – Mwanzugi – Itumba, haya ni maeneo makubwa sana ya uzalishaji, tumekamilisha kufanya usanifu kupitia TARURA na tuliambiwa tutapewa shilingi bilioni 3 na milioni 500 kwa ajili ya kukamilisha hili. Naomba Waziri wa Fedha katika bajeti ijayo jambo hili ututilie mkazo, tupatiwe fedha. Sisi tunalima pamba kwa wingi, asilimia 90 ya pamba inayotoka Mkoa wa Tabora inatoka kwenye Wilaya ya Igunga na ukanda wote wa Igulubi ndio wakulima wakubwa wa pamba. Tunaomba tupatiwe fedha tuweze kurekebisha barabara hii ambayo ni muhimu sana katika uchumi wa Wilaya yetu, Mkoa wetu na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nimekuja kugundua linatushika kamba ni suala la ushiriki wa sekta binafsi. Tumekuwa tukisema kwamba tutashirikisha sekta binafsi katika ujenzi wa uchumi. Hii dhana ya sekta binafsi inaeleweka sana kwa ngazi yenu huku juu ngazi ya Mheshimiwa Rais na ninyi Mawaziri lakini kule chini bado watendaji wenu wa Serikali hawatoi ushirikiano mzuri kwa sekta binafsi. Bado kuna harassment kubwa sana kwa wafanyabiashara wadogo wadogo na wafanyabiashara wa kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo ambalo tunahubiri lakini katika utekelezaji linakwenda tofauti, tunaomba Waheshimiwa Mawaziri hili jambo mkalisimamie vizuri ili angalau sekta binafsi kinachohubiriwa na Mheshimiwa Rais na ndiyo maana mnaona Mheshimiwa Rais anapofanya ziara ukiacha wale watu anaoambatana nao kwa sababu za kiitifaki anaenda na wafanyabiashara, lengo ni kuhakikisha sekta binafsi inakuwa ni engine katika kusaidia Serikali kuendesha uchumi lakini kwa juu limekaa vizuri ukienda huko ngazi za chini kwenye Wilaya zetu, kwenye Mikoa yetu bado hali si nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumzia la nne katika mambo ambayo yanakwamisha sana mafanikio kwenye Mpango wa Maendeleo ya Taifa ni suala la Utumishi wa Umma. Kwenye utumishi wa umma bado kuna changamoto kubwa, jambo mojawapo ambalo ningependa kabisa kama Serikali mlitilie mkazo ni nidhamu ya kazi, bado nidhamu ya kazi siyo nzuri huko kwenu chini katika maeneo mengi ambayo sisi tunaendelea kuyaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta kuna mabishano, Mkuu wa Mkoa anabiashana na Watendaji. Mkuu wa Mkoa anatoa maelekezo anaandikia barua Watendaji kwa mfano TRA au Taasisi nyingine zozote wanambishia maelekezo hawayafanyii kazi. Sasa hii ni discipline ya aina gani katika utumishi wa umma? Tunaomba hili mlifanyie kazi ili angalau mipango yetu inapokwenda kule na kuweza ku-harmonize situation ili tuweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kulisema katika upande wa utumishi wa umma ni motisha, kuhakikisha watumishi tunaendelea kuwapa motisha na motisha siyo lazima iwe fedha kwa upande wa utumishi wa umma, hata mahusiano. Wale Watendaji Wakuu wa Taasisi mhakikishe wanaishi katika mahusiano ambayo ni mazuri na watumishi wao wanaowaongoza ili waweze kuwapa ushirikiano na tuweze kujenga Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache, nashukuru sana kwa kunipa nafas. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuchangia hotuba muhimu ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Kabla ya kuchangia naomba ku-declare interest mimi kabla ya kuwa Mbunge nilikuwa mtumishi wa Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa miaka kumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimefanya kazi na Mheshimiwa Simbachawene, nimefanya kazi na Mheshimiwa Mwigulu na Mheshimiwa Masauni. Kwa hiyo, baadhi ya development ambazo nitazichangia hapa ni jitihada ambazo zimeanza siku nyingi naamini wataendelea kuzifanya vizuri.

Mheshimiwa Spika, sasa nitachangia maeneo matatu kutokana na muda. Eneo la kwanza, nitachangia kuhusu makazi na nyumba za askari; eneo la pili, nitachangia kuhusu Jeshi la Polisi na Jeshi la Zima Moto na Uokoaji; na eneo la tatu, kwa mapana nitachangia kuhusu vitambulisho vya Taifa.

Mheshimiwa Spika, sasa katika upande wa makazi na nyumba za askari, Wabunge wengi wamechangia hiyo concern kuhusu kuboresha nyumba za makazi. Kwa kweli kwa mfano mimi kwenye jimbo langu la Igunga, tuna nyumba zimejengwa mwaka 1993 mimi nilikuwa darasa la kwanza, mpaka leo hazijawahi kufanyiwa maboresho. Kwa hiyo kama Wizara ijaribu kuangalia kuja na package ambayo itasaidia kuanza kuboresha nyumba za askari.

Mheshimiwa Spika, katika hilo nina wazo ambalo naweza kulitoa. Kwa mfano tunaangalia tunapopata fedha ya barabara tunapotoa kwenye mafuta, sasa kuna faini na tozo mbalimbali ambazo zinatoka kwenye taasisi za Wizara ya Mambo ya Ndani, inaweza Wizara ikajenga hoja Serikalini na ikaja hapa ikipitishwa na tukakubaliana, katika tozo na faini mbalimbali angalau kila asilimia kumi basi ikaingizwa kwenye Mfuko Maalum kwa ajili ya kuboresha nyumba za makazi ya askari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, itakapotoka hii fedha itakuwa na Mfuko Maalum halafu itaenda kufanya kazi kwa mfumo wa force account kupitia hata Jeshi la Magereza kwa maana itatusaidia sana kuboresha nyumba za askari na kujenga nyumba mpya.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ni kwenye suala la Jeshi la Zima Moto na Uokoaji, kama alivyosema Waziri wamepanga kununua magari mawili lazima pia wawe na wilaya za kimkakati. Kwa mfano Wilaya yetu ya Igunga, pale bomba la mafuta kutoka Uganda linapita na litakuwa na kituo kikubwa cha koki, sasa wilaya ina ofisi ya zima moto lakini haina gari la zimamoto. Kwa hiyo tunaomba Waziri maeneo kama haya ambayo ni ya kimkakati kwa sababu lile bomba ni kubwa, ni la gharama kubwa, ikitokea eruption ya moto bila kuwepo na gari pale tutatafutana na tutauwa wananchi wengi. Kwa hiyo maeneo kama haya, yawe ya kimkakati kwa Wizara ili waweze kuyapa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, suala lingine katika Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ni suala la motisha kwa wafanyakazi. Wale wafanyakzi wanafanya kazi wakati mwingine katika mazingira magumu ya kuokoa watu kwenye moto, kwenye majanga, kwenye maji. Sasa unashangaa, inabidi Wizara waweke mfumo mzuri pia wa motisha itakayowasaidia hawa watumishi wa jeshi la zimamoto wote kwa ujumla. Tusiwe tunasubiri kwamba mtu amefanya wonderfully deeds, kaokoa mtoto au kafanya nini, ikishaanza kusambaa kwenye ma-group ya WhatsApp ndio anatafutwa awe awarded. Kwa hiyo naomba tubadilishe huo mfumo hili tuweze kuwapa motisha askari wetu.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ambalo napenda kulichangia kwa upana kidogo ni suala la vitambulisho vya Taifa. Kwa kweli wakati design ya National ID inafanyika, NIDA imeanzishwa mwaka 2008, moja ya jambo kubwa ambalo lilikuwa ni lengo lake, ukiacha la kiusalama, ni kuhakikisha inatusaidia kutambua walipa kodi wa nchi hii, taxpayer identification. Kwa kipindi kile walipa kodi walikuwa milioni mbili lakini walikuwa wanatakiwa kuwa milioni 14, sasa kama Wizara ifanye tathmini hili limetusaidia vipi katika kuongeza walipa kodi mpaka sasa hivi.


Mheshimiwa Spika, kuna suala la kuzalisha vitambulisho, lazima itoke kwenye hili suala la namba, twende tukazalishe ili watu wengi waweze kutambulika. Sasa hivi katika moja ya vitu ambavyo inakwenda ni digital economy. Watu wanalipa kwa kutumia kadi, hizi kazi za vitambulisho vya Taifa, hata katika design yake ni kwamba baadaye tunasema tutumie kama e- wallet ambayo maana yake ni kwamba, malipo haya yanayofanyika katika huduma mbalimbali, mtu anaenda na kitambulisho cha Taifa na ile namba yake ya utambulisho, analipa anatoa kadi inachanga malipo yanafanyika. Tukifikia hivyo, Serikali itapata kodi lakini tutakuwa tumebadilisha pia mfumo wa kutembea na pochi kubwa hiizi mifukoni zenye hela nyingi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kumshauri Waziri na Wizara wasaidie, NIDA wakati inafanyiwa design na sasa hivi ilipo, nyaraka nyingi zimekuwa za kipindi kile NIDA bado ina watumishi zaidi ya 100. Sasa hivi NIDA ina-oparate nchi nzima, ina ofisi nchi nzima na ndio maana ugumu unakuja kufanya kazi, mtumishi wa NIDA aliyepo Kongwa akihitaji kununua kalamu, lazima awasilisane na Makao Makuu Dar es Salaam, ni ngumu sana kufanya kazi na kutoa matokeo. (Makofi)


Mheshimiwa Spika, naomba wabadilishe, kwenye majeshi mengine yaliyoko chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani, wanaona namna tunavyo-oparate kupitia Makamanda wa Mikoa, sasa na NIDA tubadilishe ili mamlaka katika wale Maafisa wa NIDA wa Mikoa wawepe nguvu ya kuweza kusimamia maafisa walioko katika maeneo yao. Sio mtumishi anahitaji pini ya kubana fomu ya usajili, anatakiwa aombe Dar es Salaam ndio ipelekwe kule Wilayani. Hilo waliangalie sana.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo ni la muhimu, naomba Mheshimiwa Waziri akalifanyie kazi kulikuwa na mikataba miwili, naomba waiangalie vizuri, ambayo baadaye itawasadia. Kulikuwa na mkataba wa ujenzi wa ofisi za NIDA nchi nzima, walijenga awamu ya kwanza, wanatakiwa kwenda awamu ya pili wakaangalie wamefikia wapi. Mkataba mwingine wa muhimu...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)

Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Mkataba wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika wa Kuzuia na Kupambana na Ugaidi ya Mwaka 2004
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Itifaki ya Mkataba ya Umoja Nchi Huru za Afrika wa Kuzuia na Kupambana na Ugaidi wa Mwaka 2004.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unapoongea neno ugaidi, haraka haraka kichwani linakujia jambo linalohusiana na vifo, ukosefu wa udhibiti na amani, uharibifu wa majengo na miundombinu, kuzalisha vikundi vya uhalifu kwa maana ya insurgency groups; kuzalisha vikundi vya Itikadi kali kwa maana Extremists groups; lakini pia na umaskini katika nchi zetu. Sisi kama Taifa tumeamua kupitisha Itifaki hii ya Kuzuia na Kupambana na Ugaidi. Kwanza niipongeze Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi inayoongozwa na Mheshimiwa Masauni, Naibu wake Mheshimiwa Sagini, lakini pia na Katibu Mkuu Ndugu Christopher Kadio; wameweza kufikisha Itifaki hii kwenye Bunge letu Tukufu na leo tunakwenda kuridhia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi wamechangia faida zitakazotokana na kupitishwa kwa Itifaki hii, nami kama Mbunge pia ningependa kuchangia machache ambayo naamini kama Taifa letu litanufaika kutokana na kupitishwa kwa itifaki hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza na la msingi kama Taifa wajibu wetu ni kuhakikisha ulinzi na usalama. Hiyo ndiyo dhamana kuu ya Taifa lakini pia ndiyo dhamana ambayo tumepewa sisi Chama cha Mapinduzi kupitia Serikali yetu hii ya Awamu ya Sita; kuhakikisha kwamba tuna ulinzi na usalama katika Taifa kwa maana ya political stability. Tutakaporidhia Itifaki hii, basi tutakuwa tunatengeneza mazingira mazuri ya kuhakikisha Taifa letu lipo salama na shughuli zote zinazofanya na wananchi zinaendelea kuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo kama Taifa tutafaidika na Itifaki hii, ni kupata na kujengewa uwezo wa mafunzo na mbinu mpya za kupambana na udhibiti wa ugaidi. Kama ambavyo Itifaki inasema tutashirikiana na mataifa ya wenzetu na Jumuiya za Kikanda, tuna Jumuiya ya Afrika Mashariki, SADC lakini pia Jumuiya mbalimbali za Kikanda ambazo tutashirikiana nao. Pia tutaendelea ku-share experience kwa maana ya uwezo kupitia vyuo vyetu mbalimbali vya mafunzo, sisi kaka Taifa tuna NDC - Nation Defense College ambapo tumekuwa tukiona mataifa mengine yanaleta pale watu, Wakufunzi lakini pia na Maafisa mbalimbali wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama kwa ajili ya ku-share experience. Kwa hiyo, kama Taifa tutajenga uwezo na tutapata mafunzo na mbinu mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu na la muhimu litakalotusaidia ni kuimarisha ushirikiano wa kikanda. Sisi Waafrika katika makuzi na malezi yetu tunaamini akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki, kwa maana ya kwamba tutakaposhirikiana kwenye changamoto mbalimbali za kukabiliana na hivi vikundi kama Boko Haramu, Anti Balaka, Ansar Dine, Al-Qaida, Al-Shabab, hivi vikundi mbalimbali vya kigaidi tutakaposhirikiana na mataifa mbalimbali, basi tutakuwa tunaimarisha ushirikiano wa kikanda, lakini pia inafanya tunakuwa wamoja na matatizo ya majirani zetu na sisi yanakuwa matatizo yetu. Atakapopata jambo Msumbiji, basi Tanzania utakwenda mbele, utakapopata jambo Tanzania, Malawi atakwenda mbele na hivyo hivyo ndivyo tunavyojenga ushirikiano wa Kikanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne na la mshingi ambalo tunaweza kulipata kupitia Itifaki hii ni kuweza kutumia kanzidata ambayo ipo Algeria kama ambapo Waheshimiwa Wabunge wamesema. Katika kupambana na ugaidi nyenzo muhimu kuu ni mbili; kwanza ni taarifa na jambo la pili ni fedha. Sasa kwenye suala la taarifa tutapata access ya data kupitia itifaki hii tutakapoiridhia kama Taifa. Hii itatusaidia sana kuwa na taarifa, lakini pia ugaidi unashamiri sana kwa kupitia pia taarifa na fedha. Kwa hiyo, hivi vitu vinategemeana, lakini kama Taifa kwa kuwa tumepata access ya hii kanzidata maana yake tutakuwa tunapata taarifa mapema lakini pia tunaweza kujiimarisha na kudhibiti ugaidi katika Taifa letu lakini pia katika Jumuiya ya Kikanda zinazotuzunguka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tano na la muhimu, ni kuimarisha kwa uchumi wa nchi, kuongeza uwekezaji na ustawi wa jamii. Katika mataifa ambayo yanakabiliwa sana na wimbi la ugaidi, ni vigumu sana kwa uchumi kuimarika lakini pia na wawekezaji wanakuwa na mashaka ya kuwekeza mitaji yao. Kwa hiyo, kama Taifa tunaishukuru Serikali kwa kuweza kufikia hatua hii katika hili jambo zito na la muhimu, tuendelee kuimarisha usalama wa Taifa letu na kuhakikisha tunavutia uwekezaji na hatimaye kukuza ustawi wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hotuba ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi jioni hii.

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Masauni na Mheshimiwa Sagini kwa kuteuliwa na Mheshimiwa Rais kushika nafasi kuongoza wizara hii. Tunawatakia kheri vijana wenzetu katika kuupiga mwingi na kuhakikisha ndoto ya Mama Samia inafikiwa vizuri katika kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina takribani mambo saba ninataka nichangie mchana huu lakini kwa sababu ya muda nitachangia haraka haraka. Nitayaa-highlight lakini naamini Waziri na wasaidizi wake wizarani watayafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, Jambo la kwanza linahusu madai ya askari wastaafu. Kwa kifupi ninaposema askari nitakuwa namaanisha askari wote waliopo kwenye majeshi yaliopo Wizara ya Mambo ya Ndani, pia itakuwa inahusu makamishna na maafisa wote wanaohusu waliopo chini ya majeshi yalioko Wizara ya Mambo ya Ndani ili nirahisishe kutokana na muda. (Makofi)

Mheshimiwa spika, sasa madai ya askari waliostaafu; hapa naongelea sana sana madai yanayohusu fedha za uhamisho lakini pia kuna madai ya wale waliostaafu fedha za nauli na usafirishaji wa mizigo. Kwa hiyo Waziri na wasaidizi wako nawaomba mkalifanyie kazi hizi Wizarani ili wale askari wote waliostaafu waweze kupatiwa madai haya ili wapunguze manung’uniko huko mtaani kwa kulitumikia Taifa letu kwa muda mrefu. Kwamba, sasa wamestaafu lakini hawajalipwa fedha zao za kusafirisha mizigo na nauli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili; ni madai ya askari wote waliosimamishwa kazi na hatimaye baadaye kutokana na uchunguzi au kufuatana na kutatuliwa kwa changamoto walizokabaliana nazo wanaporudishwa kazini; pia pamoja na madai ya baadhi ya askari ambao bado wapo kazini, ambao walisimamishwa kazi na baadaye kutokana na procedures za kimaadili wakaonenaka hawana shida na kurudishwa kazini. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri naomba pia hili jambo mliangalie. Hii ni kwa sababu tumekuwa tukipata malalamiko huko majimboni ambapo baadhi ya wazee wetu wanatuomba kwamba tusaidieni kupeleka documents; kwamba wanasema mimi nilisimamishwa kazi, na baadaye nikarudishwa, lakini bado malimbikizo yangu ya ile mishahara ambayo nilikuwa nimesimamishwa kazi haijailipwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu; Mheshimiwa Waziri naomba ulifuatilie na wasaidizi wako mlitatue…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Ngassa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Matiko.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nilikuwa nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Ngassa; kwamba katika orodha ya madai anayoorodhesha pia kuna askari wa jeshi la polisi, magereza lakini hata wale wa traffic; unakuta wanaamishwa kituo kimoja kwenda kingine hawalipwi fedha za kuhamishwa tena wanaamishwa tena hawalipwi tena. Kwa hiyo hayo yote Serikali iangalie iweze kuwalipa on time. (Makofi)

SPIKA: Nimeona jina lako hapo unachangia hilo halipo kwenye hoja yako unayochangia. Waheshimiwa Wabunge muda wa kuchangia ni mfupi sana kwa hiyo, unaposimama kumpa mwenzio taarifa angalia ule muda wake pia. Kwa sababu taarifa ikitolewa ukiwa na muda mrefu ni sawa, ukiwa mfupi kidogo inaleta changamoto.

Mheshimiwa Ngassa unaipokea taarifa hiyo.

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naipokea taarifa naomba niendelee kuchangia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nililotaka kuchangia ni suala la madai ya wazabuni na watoa huduma. Mheshimiwa Waziri ukifuatilia kwenye vikosi vyetu mbalimbali, vikosi vya mbwa, vikosi vya farasi huko utaangalia kuna baadhi ya wazabuni walitoa huduma wana madai. Kwa hiyo naomba jambo hili mlifuatilie pia muweze kuwalipa.

Mheshimiwa Spika, jambo la nne, ningependa kulichangia mchana huu ni makazi ya askari polisi, na hivi karibuni pia nilichangia, lakini naendelea kusisitiza kwa sababu nyumba za askari wetu baadhi zimekuwa katika hali isiyo nzuri sana. Tunaomba wizara mlipe kipaumbele mzifanyie maboresho ili askari wetu waweze kuishi maeneo safi na salama kwa ajili ya usalama wa familia zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tano ningeomba kulichangia mchana huu ni kuhusu Jeshi la Zimamoto na Uokoaji. Kwa sasa kuna mradi mkubwa ule wa bomba la mafuta linalotoka Uganda kwenda Tanga, kuna wilaya 24 ambazo tunaomba Jeshi la Zimamoto na Ukoaji wazifanye kuwa wilaya za kimkakati na watupatie gari za zimamoto. Hii ni kwa sababu hili bomba la mafuta linapopita litakuwa ni moja ya risk katika maeneo yetu. Kwa hiyo tutakapokuwa na lile gari hata litakapotokea jambo lolote basi tuwe na uhakika wa kudhibiti janga ambalo litatokea kwa ajili ya wananchi. Kwa hiyo Wizara ya Mambo ya Ndani naomba jambo hili mlizingatie sana; ikiwemo Wilaya ya Igunga ambako bomba la mafuta linapita kwenye takribani kata nne hivi tupate gari moja; na ni kwa sababu kuwa pale sasa hivi pia tuna ofisii ya zimamoto na Jeshi la Uokoaji na tuna afisa pale na wasaidizi wake.

Mheshimiwa Spika, jambo la sita ambalo ningependa kulichangia mchana huu ni suala la Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa. Mheshimiwa Masauni nadhani unakumbuka tulipokuwa wizarani miaka ya nyuma pale tulikuwa tukipambana katika kuinasua taasisi hii, na sasa upo kwenye Wizara. Ninakushauri mambo mawili unayoweza kufanya ili kuisaidia taasisi hii. Jambo la kwanza; Mheshimiwa Waziri ahakikishe bajeti wanayopangiwa na Serikali inakwenda yote ili waweze kuendesha operation zao vizuri. Jambo la pili na la msingi ni kuhakikisha kuwa anasimamia katika kuhakikisha vitambulisho vya Taifa; kwa maana ya zile hard copy, kwamba zinatoka na kuwafikia wananchi. Kwa sababu sasa hivi changamoto kubwa wanayokutana nayo wananchi kule ni wengi kuwa na namba lakini unakuta…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana, kengele imegonga. Uliongea hapo mwishoni ulikuwa umeshazima kisemeo chako umesemaje?

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia Bajeti ya Wizara ya Maji jioni hii. Kwanza nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutekeleza ndoto yake ya vitendo kwa kumtua mama ndoo kichwani kwa kupitia Serikali yake anayoongoza ya Awamu ya Sita, tumpigie makofi kwa wingi Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, niwapongeze Wizara ya Maji, kaka yetu Juma Aweso, lakini pia na Naibu Waziri Mheshimiwa Mahundi, Katibu Mkuu ambaye aliteuliwa hivi karibuni Engineer Kemikimba, Naibu Katibu Mkuu ambaye alikuwa Mtendaji Mkuu wa DAWASA Luhemeja, lakini pia na wasaidizi wao wote wakiwepo Katibu wa Waziri Ndugu Gibson ambaye anaendelea kutupa sana ushirikiano na pia Mkurugenzi wa Mamlaka Maji, CPA Grace Msiru naye anatupa sana ushirikiano.

Kiukweli niwapongeza kama Wizara wanatupa ushirikiano mkubwa. Wasituchoke waendelee kutuvumilia, sisi siasa zetu zinabebwa na maji. Kwa hiyo, kwa kiwango kikubwa sana Wizara hii tunaitegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipowapongeza RUWASA Mkoa wa Tabora ambayo iko chini ya Mhandisi Kapufi, lakini pia Mamlaka ya Maja Igunga (IGUWASA) ipo chini ya Mtendaji Mkuu, ambaye tunamwita Murugenzi Mkuu pale Mhandisi Humphrey, lakini pia na Mamlaka ya Maji ya Vijijini Igunga RUWASA iko chini ya Meneja wetu pale anaitwa Mulaza. Wanatupa ushirikiano mkubwa kwa kweli, wanaendelea kutuunga mkono katika utekelezaji wa Ilani yetu kuhakikisha tunapeleka maji vijijini na mijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jioni hii sitakuwa na mambo mengi sana ya kuchangia, lakini nina mambo takribani mawili, moja ni shukrani, lakini pia na mradi mkubwa ambao ningependa kuusemea ambao ningeomba Wizara wausimamie kwa makini kuhakikisha unakamilika. Mwaka jana walitupatia mradi mkubwa sana wa maji kwa kutumia maombi maalum wa kwenda Kijiji fulani kinaitwa Mwamashimba, ni takribani kilometa 45 kutoka Igunga Mjini kule ndio chimbuko langu mimi kama Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa tunakunywa maji kutoka kwenye kitu tunaita malonga, mnachimba maji, mnatumia ng’ombe na binadamu. Tunashukuru tulileta special request Wizara, walitupatia fedha takribani milioni 800, ule mradi umekamilika na sasa tunapata maji. Tunashukuru sana kwa moyo wao wa upendo waliotujalia Wanaigunga. Pia nishukuru Mamlaka ya Mji Mdogo pale Igunga walitupatia fedha takribani bilioni 1.8 kwa ajili ya mradi wa maji taka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wetu wa Igunga unakuwa sana, ni moja ya miji inayokuwa kwa kasi na ni mji wa kijanja, biashara ni kubwa. Kwa hiyo tumepata mradi wa maji safi na maji taka pale, tunawashukuru Wizara kwa kuliona hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la msingi, nimpongeze Waziri, wamekuwa wasikilizaji wazuri wa maoni ya Wabunge. Mwaka jana moja ya eneo ambalo pia nililichangia sana ni suala la kubadilisha utaratibu wa manunuzi kwa Mamlaka ya Vijijini RUWASA. Nimeona hivi karibuni kuna taarifa ya Waziri inatembea, inasema kwamba wameruhusu manunuzi kwenda mpaka ngazi za mkoa kwa Mamlaka ya Maji RUWASA. Hongera sana kwa Wizara kwa hili wametusaidia, kwa sababu tulikuwa tukikwama, tulikuwa tunatoa mifano kwamba inahitajika hata motor ya milioni tatu, milioni nne, lakini idhini mpaka itoke Wizarani. Sasa wameamua kulishusha mpaka ngazi ya mikoa, naamini litaongeza ufanisi na miradi mingi itakwenda kwa wakati. Hongera sana kwa Wizara waendelee kufanya kazi kwa bidii wamsaidie Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi miwili ambayo tunategemea kwa mwaka huu wa fedha pale Igunga. Kwa Mamlaka ya Maji ya Mjini kwa maana IGUWASA kuna mradi mmoja unahitaji milioni 840. Tunafanya upanuzi wa Mradi wa Maji ya Ziwa Victoria kutoka sehemu moja inaitwa Makomero kwenda Mgongolo. Kwa hiyo tunapitisha bajeti ya Waziri na naiunga mkono kwa asilimia 100 ili niweze kupata hizi fedha, tukakamilishe huu mradi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mradi wa pili pale wa kufanya maboresho. Tuna chanzo kimoja cha Bwawa la Bulenya ambapo tumeomba milioni 521. Naamini pia kwa kuwa naenda kuunga mkono hii bajeti kwa asilimia mia moja, basi na zenyewe tutazipata kupitia Mkurugenzi wa Mamlaka za Maji, Ndugu Joyce ili tuweze kukimbizana tuweze kuendelea kumtua mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ambalo ningependa kuchangia jioni hii pale tuna mradi mmoja wa RUWASA ambao ni wa bilioni 20. Kuna kampuni moja inaitwa Help Desk Engineering, naona wapo site na wameshasaini nao mkataba lakini spidi yao sio nzuri sana. Naamini Mheshimiwa Waziri hili watalifanyia kazi, tusirudi kule kwenye ile miradi chechefu ambayo walipambana nayo takribani kwa miaka miwili. Haya makampuni au hawa wakandarasi ndio watamfelisha Waziri ndugu yangu Mheshimiwa Aweso, ajitahidi kuwa makini. Tunapotoa ushauri kwa kuwa anaupokea, mimi ningeshauri kitu kimoja, aweke utaratibu kupitia Kitengo chao cha Monitoring and Evaluation Wizarani. Wanatoa mkataba, mkandarasi akipewa mkataba ndani ya miezi mitatu hajaanza kufanya utekelezaji kwa kiwango wanachoridhika nacho, wavunje mkataba, watoe tenda upya ili tuweze kwenda kwa kasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwalimu Nyeyere aliwahi aliwahi kusema; “we must run while others are walking”, kwa lugha nyepesi ya Kiswahili ni kwamba lazima tukimbie wakati wengine wanatembea. Tunaelekea kwenye uchaguzi wa Serikali za Mitaa, tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu, siasa yetu inabebwa na maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi pia kuchangia Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Kwanza naunga mkono hoja ya Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, lakini pia naunga mkono Taarifa ya Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Spika, duniani kote unapopima uwezo wa taasisi kwa maana ya uthabiti na uimara, basi kuna uhusiano wa moja kwa moja na uimara na uthabiti wa mkuu wa taasisi husika. Kwa mantiki hii nichukue nafasi hii kumpongeza Amir Jeshi Mkuu na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa maboresho mbalimbali ambayo anayafanya kwenye Jeshi letu pamoja na vyombo vya ulinzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kiwango kikubwa ili vyombo vya Ulinzi na Majeshi yaweze kufanya vizuri unahitajika uwekezaji mkubwa sana katika teknolojia, katika rasilimali watu lakini pia na rasilimali fedha. Mheshimiwa Rais amechukua jitihada mbalimbali katika kuhakikisha Majeshi yetu yanafanya kazi vizuri na ndio maana tunaona Taifa letu liko imara na liko salama. Asubuhi nilikuwa namtania kaka yangu Lusinde, namwambia kuna mataifa Wabunge hawatembei mtaani wanazurura tu bila ulinzi au bastola kiunoni, lakini sisi Tanzania tuko imara kwa sababu ya ulinzi na usalama. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri na Wataalam wake wote Wizarani, nampongeza Afande CDF Mkuu wa Majeshi, Majenerali na Makamanda na watumishi wote wa Jeshi pamoja na Wizara. Kazi nzuri wanayoifanya lakini pia na Makamanda wetu walioko maeneo mbalimbali duniani kwa ajili ya kuhakikisha wanaweka usalama mbalimbali kwa maana ya peace keeping mission na peace building mission. Wanajitolea unapoingia katika viwanja vya mapambano maana yake umeweka rehani usalama na uhai wako. Tunawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie baadhi ya maeneo asubuhi hii katika hotuba hii ya Waziri kuhusu Wizara ya Ulinzi. Eneo la kwanza ningependa kuchangia ushiriki wa Jeshi letu kwenye usanifu na usimamizi wa miradi ya kitaifa na miradi ya kimkakati. Tunaamini kabisa Jeshini ni sehemu ya kwanza katika suala la strategy, mikakati na ulinzi. Serikali ningewashauri waongeze wigo wa ushiriki wa Jeshi letu katika usanifu wa miradi hii hususan miradi mikubwa ya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Waziri wa Ulinzi na Waziri wa Nishati hivi karibuni niliwaona wamekaa wakijadiliana kuhusu suala la kuimarisha ulinzi kwenye Mradi wa Bwawa letu la Umeme. Hii ni hatua nzuri wakati mwingine wawe wanashirikishana kwenye miradi mikubwa kama Serikali ya kimkakati. Miradi kama Liganga na Mchuchuma ambayo kwa sasa ndio move ya Taifa letu, wahakikishe wanashirikisha Jeshi letu kuanzia hatua za awali na Jeshi letu limejaliwa wataalam wengi, lina ma-engineer wa kila aina, lakini lina watu wazalendo ambao watafanya kazi kwa maslahi ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ya pili ambayo ningependa kuchangia mchana huu ni suala la Kamandi ya Jeshi la Akiba. Hili ni kama vile limesahaulika kidogo, naomba Wizara na Serikali waongeze nguvu katika kamandi hii. Tumekuwa tukitoa mafunzo kwa askari mgambo, lakini baada ya mafunzo tunajikuta tunawaacha mtaani kwa maana ya notion kwamba ni Jeshi la Akiba. Hawa watu waingizwe kwenye mfumo rasmi wa kiserikali, waweze kuwa-monitor kwa ukaribu, lakini pia waangalie namna ya kuweza kuwasaidia kwa namna yoyote, mbeleni wawe na mipango hata ya kuimarisha bima za afya ili waweze kuwa tayari gado, wakiwa fit, hata inapotokea dharura yoyote watakapowahitaji basi wanaungana na Majeshi yetu katika operation mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Jeshi, Military Act ukijaribu kuangalia hawa watu kunapotokea tafrani, hadhi yao ni sawa na askari wetu ambao wako kazini. Kwa hiyo na wenyewe katika kipindi ambacho ni cha amani na utulivu, basi tujaribu kuangalia namna ambavyo tunaweza tuka wa-accommodate na waka-feel kwamba ni sehemu ya Jeshi letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kuchangia mchana huu ni ujenzi wa anga za ndege za Jeshi ambalo Mheshimiwa Fakharia aliliongelea, niwasisitize tu na kuwaomba Serikali wakamilishe ni anga za kisasa na kubwa ambazo zinaweza zika-accommodate ndege zetu hususan hii ya Dodoma ambapo kwa sasa ni makao makuu, tungependa kuona hivi karibuni imeanza kufanya kazi ili tuweze kuimarisha ulinzi wa Taifa letu na Makao Makuu ya Nchi yetu. Kama tunavyojua tumezindua Ikulu yetu kwa sasa ya Chamwino, basi na Jeshi liwe kamili kamili kabisa kwa lolote ambalo litakuwa tayari kwa ajili ya kukabiliana nalo.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kuchangia ni Mradi wa Nyumbu TATC-Tanzania Automotive Technology Centre ni kituo cha Jeshi kwenye teknolojia, tunaomba Serikali na Wizara waongeze fedha. Kamati tulipita pale tukaona maendeleo yaliyokuwepo mwaka jana na mwaka huu kuna improvement kubwa, tuwatie moyo, waendelee kupambana. Naamini kwamba Jeshini ukiwekeza teknolojia Zaidi, basi tutasonga mbele, utafiti utafanyika kwa kiwango kikubwa, lakini tutabuni mambo makubwa ambayo yatakuwa yanatusaidia katika ulinzi na usalama wa Taifa letu na kupiga hatua mbele katika level ya teknolojia.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho ambalo ningependa kulichangia na kulisisitiza ambalo baadhi ya Waheshimiwa wamelichangia ni kuhusu msamaha wa kodi kwenye vifaa vya Jeshi. Mheshimiwa Waziri ajaribu kukaa na Waziri wa Fedha hili jambo walione ili itakapokuja Sheria ya Fedha tuliangalie kwa mapana. Haiwezekani tukawa na Jeshi ambalo tumeliamini kulinda mipaka ya nchi, tumeweka usalama wetu mikononi mwa Jeshi letu, lakini inapokuja kwenye clearance ya vifaa tunaanza kuwa na kigugumizi. Ni aibu sana, tulifanyie kazi, sisi tumeamua kulisemea Jeshi kwa kuwa linafanya uzalendo wa Taifa letu, linatulinda usiku na mchana na sisi kama Taifa tumebaki imara.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naona watu wa Igunga walikuwa wana-test mitambo lakini imeshindikana. Mambo yanakwenda vizuri. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni hii nami niweze kuchangia Bajeti ya Wizara ya Mambo ya ya Ndani ya Nchi. Kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, kwa kuunda Tume ya Haki Jinai nchini. Ukifuatilia kwa haraka haraka, ukifanya utafiti, hii Tume ya Haki Jinai, asilimia takribani 60 ni wanufaika wa taasisi na vyombo vilivyoko chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa maana ya taasisi zote zilizopo chini ya Wizara, asilimia 30 ya wanufaika ni Wizara ya Katiba na Sheria na asilimia 10 ni taasisi nyingine. Tunamshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kuona, tunaamini tume hii italeta mabadiliko makubwa sana kwenye vyombo vyetu vilivyopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Waziri, kaka yangu Mheshimiwa Engineer Masauni, kwa kazi nzuri ambayo anaendelea kuifanya kwenye hii Wizara pamoja na Naibu wake, kaka yangu, Mheshimiwa Jumanne Sagini. Hongereni, mmeendelea kuaminiwa, mnaendesha vizuri Wizara, mnatoa mwongozo mzuri, nasi kama Wabunge tupo nanyi, tunawaunga mkono na kuhakikisha yale yote ambayo mmepanga yanatimia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitumie nafasi hii kuvipongeza vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vilivyopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi. Nampongeza Inspekta Jenerali wa Jeshi la Polisi, Afande IGP; Kamishna Jenerali wa Uhamiaji; Kamishna Jenerali wa Magereza; Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji; Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa na pia niwapongeze Maafisa wa Bunge, wale ambao wanahudumia Jeshi la Polisi na Magereza ambao wako hapa Bungeni, wanatupa ushirikiano mkubwa katika kuhakikisha mambo yetu yanakwenda vizuri. Nami kwenye bajeti nimeona Gereza langu la Igunga litakamilishwa, kwa kuwa mwaka 2022 nilitoa fedha pale kwa ajili ya cement kama Mbunge, na mwaka huu nashukuru Serikali mmetuunga mkono, mtalikamilisha gereza letu tuwe na gereza la kisasa kwa sababu Wilaya ya Igunga ni ya kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie maeneo matatu, manne, lakini kabla ya kuchangia, niseme naunga mkono hoja Taarifa ya Mheshimiwa Waziri na Taarifa ya Kamati ambayo pia mimi ni Mjumbe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza na Jeshi la Polisi. Waheshimiwa Wabunge wengi wameongelea suala la makazi, sitalisema, mimi napenda kusemea Chuo cha Polisi pale Moshi, kuna miundombinu imechakaa, namwomba Mheshimiwa Waziri alipe kipaumbele katika kuhakikisha anaifanyia maboresho. Ni chuo cha kisasa, kimekuwa cha muda mrefu. Kuna mabweni pale tulijengewa na wahisani kwa kupitia Wachina pale, lakini pia na sisi sasa tuweke jitihda kuhakikisha tunaboresha bwalo letu pale la chakula na yale mabweni kwa ajili ya wanafunzi kwa maana ya maafisa wetu wanapokwenda kozi mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, jambo lingine ambalo napenda kuchangia jioni hii ni sare la Polisi. Tumefika pale tukaona kwa sasa tunazalisha sare zetu wenyewe. Imewapa heshima sana kama Wizara, hongereni. Kwa hilo, ni hatua kubwa. Zamani tulikuwa tunakutana na Askari Polisi, unakuta uniform imechanika, lakini kwa sasa wanazalisha pale kwa ustadi mkubwa, kwa ufanisi. Afande IGP pamoja na wasaidzii wake walituonesha na sisi tumeridhika. Mabadiliko haya sasa yaende pia kwenye majeshi mengine yaliyoko chini ya Wizara hii ili tuweze kuendelea kuzalisha uniform zetu nchini. Uniform zinazalishwa vizuri, zinatoka mpaka na majina na vyeo vya Askari wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuchangia jioni hii ni kuhusu vyombo vya usafiri na doria na patrol. Mheshimiwa Waziri, mama yetu Amiri Jeshi Mkuu, ametenga fedha kwa ajili ya kununua magari. Nasi Jimbo letu la Igunga tunaamini litakuwa miongoni mwa majimbo ambayo yatapewa kipaumbele katika kupata haya magari kwa ajili ya kuimarisha patrol. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru OCD wa Igunga, anatupa ushirikiano mkubwa sana. Mwaka 2022 mimi kama Mbunge niliwachangia matairi, mwaka huu nimeona Serikali inatupatia gari mpya. Basi tunasema Insha’Allah, mama anaupiga mwingi, vijana wanasema apewe maua yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la mwongozo wa ujenzi wa hivi vituo vya polisi vya kwenye kata (police posts); sisi pale tumeanza jitihada pale Jimboni kwetu Igunga, nilipewa fedha kwa ajili ya kuanzisha ujenzi wa Kituo cha Polisi pale sehemu moja inaitwa Mwanzugi eneo ambalo lina uchumi mkubwa sana na mzunguko wa fedha. Naomba na ninyi Serikali basi mtuingilie muongeze nguvu tuweze kukamilisha kile kituo cha Mwanzugi ili tuweze kupata na kuhakikisha raia na mali zao zinakuwa salama. Lakini pia Kata ya Igurubi ambayo ni makao makuu ya tarafa, kule kuna uchimbaji mkubwa wa madini, pia tuna kituo pale cha polisi cha nguvu za wananchi ambacho kimeshafikia hatua ya kupauliwa. Naomba mtuongezee fedha kama Serikali tuweze kukikamilisha mtuletee askari wetu pale waendelee kutusaidia kulinda wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ukweli mnafanya kazi nzuri, tunawapongeza kwa hilo. Lakini pia kuna huu utaratibu wa polisi kata mmesema mnawapatia pikipiki. Ilikuwa ni hoja niliyotaka niijenge hapa, kwamba tuweze kuwasaidia usafiri ili angalau basi wawe huru ili wanapokuwa wanafanya shughuli zao kwenye hizi kata waweze kutembea sehemu moja kwenda nyingine. Mmejitahidi sana polisi kata wanatupa ushirikiano hata sisi tunapokuwa kwenye ziara zetu Waheshimiwa Wabunge tunapata ushirikiano mkubwa Mheshimiwa Waziri tunakushukuru kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la msingi kwenye Jeshi la Polisi ningependa kuchangia pia kamera. Muweke sasa, kama mlivyosema, kwamba mtaweka kamera za usalama barabarani ili zinapotokea ajali au uhalifu mweze ku-track kirahisi. Hili namkumbuka hata Mheshimiwa Kenethy Nola alinisisitiza, akaniambia asubuhi kuwa yeye hatapata nafasi ya kuchangia lakini aliomba niweze kulichangia. Hongereni lakini tunawapa msisitizo miji yetu imekuwa kama Makao Makuu ya Dodoma sasa inahitaji kamera kwa ajili ya usalama barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikimaliza Jeshi la Polisi, naomba niende Jeshi la Uhamiaji. Niongelee suala la Chuo pale cha mafunzo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ngassa muda umeisha, naomba malizia.

MHE.NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa pamoja na yote niliyoongelea ningependa kuchangio la mwisho, upande wa mamlaka ya vitambulisho vya Taifa. Mheshimiwa Waziri naomba nishauri, muwapatie fedha za kutosha ili waweze kukamilisha waweze kununua card ghafi ili wananchi waweze kupatiwa vitambulisho vya Taifa. Lakini pia ukijaribu kufatilia suala la vitambulisho vya Taifa linasaidia utambuzi wa walipa kodi nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nashukuru sana, naunga mkono hoja.