Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. George Ranwell Mwenisongole (4 total)

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kutokana na mabadiliko ya tabianchi na ikolojia, kilimo cha umwagiliaji hakiwezi kukwepwa katika nchi hii. Miaka michache iliyopita Serikali ilitoa mabilioni ya fedha kununua vifaa vya uchimbaji wa mabwawa, lakini mpaka sasa hivi hakuna bwawa hata moja ambalo limechimbwa na hivyo vifaa vimechakaa na kwa sasa ni kama vile spana mkononi. Sasa nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba mabwawa haya yanachimbwa na kuwekeza fedha zaidi kwenye uchimbaji wa mabwawa ili kukinusuru kilimo chetu na mabadiliko ya tabianchi yanayoikabili nchi hii? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye sekta ya kilimo, miaka yote nchini tumekuwa tukitegemea sana msimu wa mvua ili kuzalisha mazao yetu. Tumegundua kwamba tunayo fursa ya kutumia mabwawa yawe ya asili au ya kuchimba na kuyajaza maji tukatumia kwa kilimo cha kumwagilia. Tumeweka msisitizo kwenye eneo hili, pale ambapo tulichimba mabwawa mengi kwenye maeneo kadhaa lakini pia kuhakikisha kwamba tunakuwa na maeneo ya kumwagilia pale ambako kuna uwezekano mkubwa au kuna mvua nyingi na mabwawa yanajitengeneza. Serikali inaendelea kusimamia jambo hili kwa sababu tumegundua tukiimarisha kwenye umwagiliaji, tunafanikiwa sana.

Mheshimiwa Spika, Serikali huko awali tulinunua mitambo hiyo ambayo Mheshimiwa Mwenisongole amesema imechakaa. Ni kweli, lakini kwa kuwa sasa tunakisimamia kilimo na maendeleo yake, Wizara ya Kilimo hapa hata walipokuja mbele yetu kuja kuomba kuongezewa bajeti, walieleza waliomba fedha ambayo Waheshimiwa Wabunge wameipitisha kwa ajili ya kuongeza mitambo mbalimbali kwa ajili ya kupanua wigo wa kilimo cha umwagiliaji. Lengo mitambo ile isambazwe kwenye kanda zetu na ifanye kazi ya kuchimba mabwawa kwenye maeneo hayo, yatumike kwa kilimo, lakini wakati mwingine pia na wafugaji watatumia kwa kunyweshea mifugo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Serikali ilishatoa fedha kwa ajili ya kununua mitambo hiyo ili kuendelea kuimarisha mitambo iliyopo kwa kununua vipuli ile iliyoharibika, lakini mipya kwa ajili ya kuendelea kuchimba mabwawa yetu. Kwa hiyo eneo hili tutaendelea kulisimamia kwa sababu tumegundua kwamba lina tija na hasa kipindi hiki ambacho tunaambiwa hali ya hewa ina badilikabadilika, kama tutakuwa na mabwawa na maeneo haya ya kumwagilia, tunaweza tukapata kilimo kizuri tu na tukavuna mazao mengi tu kama ambavyo maeneo yote yenye mabwawa yanavyoweza kufanikiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mwenisongole kwamba, eneo hili kwa fedha ambayo tumeitoa, tutanunua mitambo na kama haitoshi tutaona uwezekano wa kuongeza ili iweze kufanya kazi ya kuchimba mabwawa katika maeneo yote kadiri ya uhitaji kwenye maeneo haya. Ahsante sana.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Waziri Mkuu. Maji ni nyenzo muhimu sana katika Maisha ya binadamu na hata katika mahitaji makuu matatu ya binadamu maji ni sehemu mojawapo. Na katika Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi inasema kwamba kufika mwaka 2025 lazima maji yawe yamefika kwa asilimia 95 mijini na asilimia 85 vijijini.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hatukaribii kufikia hayo ingawa Serikali imepeleka fedha nyingi sana vijijini lakini ukiangalia maji yanafika kwenye vituo kuna umbali mkubwa sana kati ya kituo kimoja na kituo kingine. Sasa Serikali kwa nini isishushe bei za kuunganisha maji vijijini kwa wananchi wote nchi nzima iwe kama umeme wa REA ili wananchi maskini wale wafaidike na huduma hii ya maji ambayo wanatembea umbali mrefu nchi nzima kuangalia hivyo? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kuujibu swali la Mheshimiwa Mwenisongole Mbunge wa Mbozi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sera yetu ya maji nchini iko wazi kwamba matumizi ya maji yatakuwa yanafika mpaka vijijini tena kwa wingi na gharama nafuu. Mheshimiwa Mbunge anahitaji kujua gharama za kuvuta maji kwenye maeneo yetu. Sera yetu inaeleza kwamba wananchi watachangia kwakulipia miundombinu ya kuvuta maji kwenda mahali alipo ikiwa na umbali usiozidi mita 60 ni umbali mfupi ambao gharama yake si kubwa. Lakini pale ambapo umbali ni zaidi ya mita 60 gharama hizo zitaingiwa na Serikali. Na ndio kwa sababu Serikali sasa inatoa fedha nyingi kutoka mahali maji yanatoka kwenda kwenye eneo la makazi ya wananchi. Pale ambako mwananchi anahitaji kupeleka maji kwenye nyumba yake basi zile gharama za kutoka kwenye nyumba yake mpaka pale kwenye chanzo kama iko chini ya mita 60 ataendelea kugharamia yeye mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo Waheshimiwa Wabunge na Watanzania mnajua kwamba Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan alipokuwa Makamu wa Rais Serikali ya Awamu ya Tano moja kati ya majukumu ambayo viongozi wetu wakuu, Rais na Makamu wa Rais waligawana, Mheshimiwa Makamu wa Rais ndio alipewa jukumu la kusimamia usambazaji wa maji nchini. Na akauanzishia kampeni ya kumtua ndoo mama kichwani na aliweza kusimamia kupunguza gharama za maji katika upatikanaji wa gharama za maji kwa wananchi na ndio kazi ambayo sasa inafanyika kwamba kiwango unacholipia kwenye maji ni kuchangia tu gharama ambazo kamati ya maji iliyoundwa na wananchi kwenye kijiji husika ndizo zinazotumika pindi miundombinu iliyowekwa inapoharibika ili wananchi wenyewe waweze kukarabati miundombinu hiyo muweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumetumia utaratibu huo ambao ni rahisi kwa kuchangia maji kwa kiwango kidogo pia kuvuta maji kupeleka nyumbani kwako kwa umbali usiozidi mita 60 utaugharamia mwenyewe lakini ikiwa zaidi ya mita 60 Serikali inawajibika kuleta maji mpaka mahali ulipo. Kwa utaratibu huu sasa tunaanza kuona huduma za maji zinasambaa maeneo yote na malengo yetu kila Kijiji kipate huduma za maji kama sio kwa mtandao wa bomba unaofata makazi ya watu basi tutajenga vilura kwenye maeneo ambayo wananchi waweze kupafikia kwa ukaribu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea kuhakiki bei zetu na kwa kuwa Wizara ya Maji inaanza leo kuwasilisha bajeti yake tutapata maelezo mazuri zaidi kwenye eneo hili na Waheshimiwa wabunge mtapata fursa ya kuchangia na Serikali tunaendelea kupokea maoni yenu, ushauri wenu namna mtakavyoboresha utoaji wa huduma za maji nchini, ahsante sana. (Makofi)
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, kuna mifugo, mali nyingi za wananchi zilizokamatwa kwa kuingia hifadhini, na umesema kwamba ipo haja ya kuimarisha mahusiano kati ya wahifadhi na wananchi. Kwa nini usitoe kauli hapa Bungeni kuitaka mifugo yote, mali zote za wananchi zilizokamatwa kwa sababu ziliingia kwenye hifadhi ziachiwe ili kufungua ukurasa mpya tuanze moja? (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa taarifa nimeitoa hapa leo na kutoa maelekezo kwa vyombo vyote vya Serikali kuchukua hatua hizi. Hatua zote za awali, taratibu, sheria na kanuni ambazo zipo ziendelee kufuatwa ili haki iweze kutendeka kwa haraka sana kama ambavyo nimesisitiza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, maelekezo yangu yamebaki, yamekuwa wazi na sahihi. Kwa hiyo, hatua hizo ziharakishwe ili wananchi waweze kutambua haki zao na upande wa Serikali uwajibike kutoa elimu kuanzia sasa na kuendelea. Ahsante.
MHE. GEORGE. R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Sera ya Ushirika ya Vyama vya Msingi ililetwa kwa nia njema ya kumsaidia mkulima wa Kahawa lakini kwa wakulima wa kahawa ya Arabica nchini sera hii imekuwa kama kaburi kwao. Kwa sababu kwenye hivi vyama vya msingi makato ni mengi, wizi na viongozi wengi wa vyama vya ushirika ni wezi na wanawaibia wakulima na imekuwa kama inamdidimiza mkulima.

Je, Serikali haioni ipo haja sasa ya ku-review hii sera ili kuwaruhusu wanunuzi binafsi nao wapate nafasi kumruhusu mkulima auze kokote anakotaka? Ahsante.
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kujibu swali la Mheshimiwa Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, niungane na Watanzania wote kuipongeza klabu yetu ya Dar young Africans. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hakika Dar Young Africans inaendelea kupeperusha vema bendera ya Tanzania na niwapongeze sana kwa matokeo ya jana. Tunawaombea sana kwa mchezo wa marudio kule Afrika Kusini mshinde kwa magoli mengi. Watanzania tuna hamu ya kuona Tanzania ikiingia kwenye mashindano haya kwenye ngazi ya fainali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia niipongeze Klabu ya Simba kwa hatua waliyofikia, tunaamini wamejifunza na wameona kutoka klabu jirani na hatua waliyofikia. Kwa hiyo, msimu ujao tunaamini vilabu vyetu viwili au zaidi vitafanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nirudi kwenye swali la msingi linalohusu ushirika. Ni kweli kwamba ushirika una malengo mazuri sana kwa wakulima, si tu kwa wakulima bali kwenye vikundi vilivyoamua kukaa pamoja. Ushirika kwa mazao yetu nchini unatazamiwa na unatarajiwa kuwakusanya wakulima, mazao hayo pamoja ili kuwaongezea nguvu ya kupata maelekezo bora ya namna ya kulilima zao lenyewe lakini pia namna ya uhifadhi, elimu ya jumla ya zao hili lakini pia kuwapa nguvu ya pamoja ya kutafuta masoko.

Mheshimiwa Spika, tunakiri kwamba tunazo changamoto kwenye ushirika kutokana na baadhi ya viongozi waliopewa dhamana ya kuongoza ushirika kufanya mambo tofauti na misingi ya ushirika ulivyo. Kwa bahati nzuri siku tatu zilizopita Mheshimiwa Hussein Bashe, Waziri wa Kilimo, alitumia muda mrefu sana kueleza faida na umuhimu wa ushirika na kwamba ushirika hauepukiki katika kuleta maendeleo ya mkulima na mazao haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja kati ya mambo makubwa ambayo yameleta udhaifu kwenye ushirika ni pale viongozi wanapoona kwamba hiyo ni fursa ya kupata kipato kupitia uongozi wao kwenye ushirika. Hiyo ni kasoro na tutaendelea kuisimamia. Tumeshuhudia viongozi wasiokuwa waadilifu kuweka makato mengi sana kwenye ushirika na kupunguza mapato ya mkulima.

Mheshimiwa Spika, tumeyaona hayo kwenye zao la korosho ambako kulikuwa na makato zaidi ya 25 tumeyapunguza na yakabaki matano na inawezekana na ndio yanayoendelea. Kwenye zao la kahawa lenyewe kulikuwa na makato 47 tumeyapuinguza tumefika makato matano mpaka sita yale ya msingi tu na kumwezesha mkulima kupata fedha nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ushirika huu pamoja na changamoto hizo ambazo Serikali tunaendelea kuzifuatilia na kuzitatua imeleta pia mafanikio ya kupanda kwa bei ya mazao kwa mfano zao lenyewe la kahawa. Nitoe mfano wa mkoani Kagera ambako zao hili wakulima wake wengi walikuwa wanaamua kulipeleka nchini Uganda kwa gharama kubwa tu kwa sababu tu ya kero walizoziona. Baada ya Serikali kuingilia kati na kuzitatua changamoto hizi leo wanauza kutoka shilingi 1,200 ya awali tumeenda mpaka shilingi 1,800 mpaka shilingi 2,000 kwa sasa na kupitia usimamizi wa ushirika.

Mheshimiwa Spika, hii ina maana ya kwamba ushirika unaweza kuongeza nguvu ya wakuilima kupata soko zuri badala ya kuruhusu mnunuzi mmoja mmoja kwenda kwa mkulima nyumbani kwake na kumshawishi kununua kwa bei ambayo anaona yeye inafaa, wakati mwingine anauza kwa bei ndogo sana kuliko hata ile iliyokuwa inauzwa. Hata hivyo, tunaendelea kuangalia mifumo mizuri zaidi ya kuuza mazao yetu chini ya ushirika. Ushirika unaweza ukatoa kibali kwa watu waliolima kahawa nyingi kama soko linakuwa lina mwelekeo mzuri tunaweza kuruhusu.

Mheshimiwa Spika, nataka niwaahidi na nimwahidi Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge ambao pia tunalima mazao yale makubwa yenye ushirika, kwamba tunaendelea kufanya mapitio, tunaendelea kusimamia kikamilifu ushirika ili ulete manufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha majibu ya swali hilo.