Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Hassan Zidadu Kungu (6 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Kwanza kabisa nianze na kuipongeza Wizara iliyoko chini ya Mheshimiwa Waziri, kaka yangu Mheshimiwa Ndumbaro pamoja na Naibu Waziri kwa namna wanavyoweza kufanya kazi vizuri; na kwa ushahidi tu wa pekee kwa sababu pia hata tarehe 22 aliweza kutembelea kwenye Jimbo langu hasa kwenye Kata tatu. Kata ya Kalulu, Jakika na Matemanga. Amejionea mwenyewe namna tulivyokuwa na kero kubwa ya tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizo, nianze tu moja kwa moja na kueleza kwenye jimbo langu halafu baadaye nifuate Taifa. Jimbo la Tunduru Kaskazini kwa maana ya Wilaya ya Tunduru, tuna hifadhi za Taifa tatu na pia tuna hifadhi ya misitu ya asilia moja kwa maana ya Mwambesi na vile vile tuna hifadhi za wanyamapori za jamii mbili, yaani Nalika na Chinguli. Vile vile tuna hifadhi za misitu asilia ya vijiji, saba. Kwa hiyo, utaona ni namna gani wilaya hii ilivyozungukwa na hifadhi za wanyamapori. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu, yako maeneo mahususi kwa ajili ya ufugaji, lakini pia yako maeneo mahsusi kwa ajili ya ukulima na sisi wilaya yetu ni mahsusi kwa ajili ya kilimo. Tunalima korosho, mpunga, ufuta mbaazi na kadhalika, lakini kero kubwa ambayo tunaipata kutokana na kilimo ni kutokana na wanyama wakali na waharibifu, yaani tembo. Nikizungumzia athari kubwa ambazo tunazipata kutokana na wanyama hawa waharibifu na wakali, kwa miaka mitano tumepoteza maisha ya watu 24 kutokana na tembo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015/2016 waliuawa watu wawili na tembo; mwaka 2016/2017 waliuawa watu wawili; 2017/2018 waliuawa watu saba na tembo; 2018/2019 waliuawa watu wanne; na 2019/2020 waliuawa watu tisa. Kwa hiyo, utaona takwimu ni namna gani watu hawa wanavyozidi kuongezeka kuuawa. Kwa hiyo, kero hii isipotatuliwa kwa umakini maana yake tunakwenda kupoteza nguvu kazi kubwa kweli kweli. Vile vile wanyama hao hao waharibifu kwa maana ya tembo, wameacha vilema vya kudumu kwa watu 20 kwa miaka mitano tu. Vile vile, ekari zilizoharibiwa na tembo zinazidi 4,679. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii nakueleza uone ni kwa sababu gani tuna kero hii kubwa ya tembo katika wilaya yetu ya Tunduru. Sababu kubwa moja ni wafugaji kwenda kufuga katika maeneo ya hifadhi za wanyamapori. Pili, wakulima kuvamia maeneo ya misitu na pia kwenda kufanya shughuli za kibinadamu kwenye maeneo ya mapito ya wanyama (shoroba).

Vilevile tuna changamoto kubwa sana ambayo inasababisha kutokupunguza tatizo hili kubwa ambalo linatupata sisi kutokana na kwamba tunao Askari wa Wanyamapori ambao wako chini ya Halmashauri. Sasa tunaweza kuona kabisa Halmashauri zetu hazina bajeti kubwa ambayo inaweza kutatua changamoto kubwa ama ika-facilitate kwa asilimia 100 Askari hawa wa Wanyamapori kwenda kutatua hizi changamoto kubwa za watu kuvamiwa na mashamba yao. Hiyo ni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao Askari wasiozidi tisa katika wilaya yenye kata 39 na vijiji 57, lakini askari hawa tisa wanaokwenda field ni saba tu. Kwa hiyo, utagundua tuna vijiji 157 lakini tuna askari saba; na kwa siku kuna kero ambayo wanatoa taarifa vijiji 15 mpaka 20 ambayo vinahitaji msaada wa kwenda kusaidiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawa Askari wa Wanyamapori naona kuna tatizo la kimfumo kwamba Askari wa Wanyamapori wako chini ya Halmashauri; na tunajua kabisa Halmashauri zetu hazina uwezo wa kutosha.

Kwa hiyo, nashauri Askari wa Wanyamapori hawa wawe chini ya Wizara kwa sababu tunakumbuka na tunafahamu mwanzo walipokuwa wako chini ya Wizara, maana yake ni kwamba walikuwa wanapata magari ya kutosha, walikuwa wana silaha za kutosha, lakini pia tulikuwa na askari wa kutosha. Kwa sasa, kwa sababu wako chini ya Halmashauri, maana yake bajeti yao ni ndogo. Hakuna Halmashauri inaweza kutenga fedha kwa ajili ya Askari hao wa Wanyamapori. Tuna tatizo kubwa mno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utaona kwa mfano kwenye Wilaya yetu ya Tunduru, kitengo hiki cha Askari wa Wanyamapori wana silaha tisa, lakini silaha hizi ni za kizamani kweli kweli, maana yake zina zaidi ya miaka 40. Kwa hiyo, utakuta mara nyingine wakienda nazo porini zinakataa hata kufanya kazi.

Kwa hiyo, ndiyo maana nashauri hawa Askari wa Wanyamapori wawe chini ya Wizara kwa sababu, Wizara ina Askari ambao wana silaha za kisasa kama vile TAWA na Ngorongoro pamoja na TANAPA. Pia utaona, pamoja na silaha hizi ambazo ni kuukuu, zina zaidi ya miaka 40 bado pia hata risasi zake pia zina bei ghali. Kwa maana ya risasi moja inanunuliwa kwa shilingi 23,000 mpaka shilingi 25,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Askari wale wa TAWA wao wana silaha za kisasa, lakini pia risasi moja inauzwa kwa bei rahisi sana, shilingi 3,000. Kwa hiyo, Askari wa Wanyamapori wakiunganishwa na TAWA tunakwenda kuondoa hili tatizo kubwa ambalo linatukabili kwenye wilaya yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia napenda kushauri, kama wilaya yetu ni mahususi kwa kilimo, naomba sana, hawa wafugaji ambao wanaingia, basi wafuate utaratibu ambao unawekwa na Serikali. Kwa mfano, Halmashauri yetu imetenga vitalu vinavyozidi 200, lakini cha ajabu hawa wafugaji wakiingia na ng’ombe hawaendi kufuga kwenye vile vitalu na badala yake wanakwenda kufuga kwenye hifadhi za wanyamapori. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hili ndiyo tatizo ambalo linasababisha kupata shida kubwa ya tembo kuwasumbua wananchi pamoja na kuwaua kwa sababu, wanapokwenda kufuga kwenye hifadhi zetu wale ng’ombe wanakuwa na harufu za dawa ambazo zinawakinga wao wasishambuliwe na wadudu. Kwa hiyo, ile harufu inawafanya wanyama hawa wakali kutoka nje ya hifadhi na badala yake kwenda kwenye maeneo ya binadamu. Sasa hili ni tatizo kubwa mno. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nashauri, jambo la kwanza, kuwe na sheria ambayo inaweza ikawa kali kwa sababu tunaamini kabisa Watanzania imeshafika stage kwamba tukiwa na sheria laini, sheria nyepesi, hatutekelezi hiyo sheria. Kwa hiyo, mimi ningeomba kuwe na sheria ngumu… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa. Ahsante sana.

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga hoja mkono.(Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hoja iliyoko mbele yetu. Naomba nijielekeze kwenye eneo dogo tu ama eneo moja la michezo. Kwenye michezo changamoto kubwa tuliyonayo ni uwekezaji na uwezeshwaji hafifu wa makampuni ya taasisi za kiserikali kwenye michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyikiti, nashauri mambo yafuatayo: Moja, Serikali ijaribu kushawishi makampuni na taasisi za kiserikali; kwenye fungu la Corporate Social Responsibility kwa kiasi kikubwa ielekezwe kwenye michezo. Mfano mzuri ni Geita Gold Mine, kwenye CSR yao wamewekeza kwenye upande wa Geita Football Club. Pia Kampuni ya Barrick imeweza kuwekeza kwenye timu ya Biashara United. Kwa hiyo, nashauri Serikali isukume makampuni hayo na taasisi za kiserikali ziweze kuelekeza CSR ziende kwenye michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Serikali itoe incentives kwa makampuni yote yanayowekeza kwenye michezo. Hii inafanywa sana na nchi nyingi zilizopiga hatua. Mfano, Serikali inaweza ikaamua makampuni yote yanayowekeza kwenye michezo, pale wanapokwenda kulipa Corporate Tax, basi lile fungu ambalo wamewekeza kwenye michezo lihesabiwe kwenye Corporate Tax. Hii italeta hamasa kwenye makampuni mengine yote kuweza kuwekeza kwenye mchezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na machache tu. Naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nichangie kwenye hotuba hii ya Nishati. Kwanza kabisa nami niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna anavyoweza kufanya kazi iliyo bora na iliyotukuka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa sababu ametupunguzia maswali mengi na ametufanya tuelewe vitu vingi kwa wakati mmoja. Kile kitendo alichokifanya cha yeye kuwaleta wataalam hapa, pamoja na Mameneja wa Wilaya zote, maana yake ni kwamba pale ametupunguzia muda wa kwenda kuwafikia hawa watu wote, lakini pia naamini wazi kuwa imepunguza maswali mengi na hata vilevile michango haitakuwa mingi sana kutokana na jambo lile alilolifanya. Kwa hiyo, ni pongezi kubwa kwake na natamani hata Wizara nyingine zingefanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja niende kwenye mchango wangu, kwenye Jimbo langu ama Wilaya ya Tunduru. Wilaya ya Tunduru tunapokea msongo wa umeme wa kilovoti 33 kutokea Songea Mjini na umeme ule unasafiri kwa kilomita 260. Kama unasafiri kwa kilomita 260 maana yake ni kwamba huku njiani kote umeme huo unatumika na tunautumia kwa Wilaya mbili, kwa maana ya Wilaya ya Namtumbo na Wilaya ya Tunduru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa inapotokea hitilafu Namtumbo maana yake ni kwamba Namtumbo wanakosa umeme na sisi Tunduru tunakosa umeme pia vilevile. Kwa hiyo, jambo hili limepelekea umeme wa Tunduru kukatikakatika mara nyingi sana na tunapata adha kubwa mno. Ulifikia wakati kwa siku umeme unakatika mara 12 mpaka mara 17. Wakati mwingine unaweza ukakatika siku nzima umeme usipatikane. Wakati mwingine tunalala na giza usiku kucha. Lakini ukiuliza ni kwamba unakuta hitilafu imetokea Namtumbo, kwa hiyo, mpaka wenzetu wa Namtumbo washughulikie hitilafu hiyo ya umeme ndipo na sisi Tunduru tuweze kupata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya adha hiyo kubwa, tarehe 4 Septemba mwaka jana niliweza kuuliza swali la msingi hapa ambalo Wizara kama inaweza kutujengea substation ya kilowati 132 pale Tunduru. Kwa bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Waziri wa Wizara hii aliweza kujibu kwamba watatuletea ama watatujengea mradi huo wa kilowati 132 pale Tunduru na alisema ataingiza kwenye mpango huu ili sasa Tunduru tuweze kupata hiyo substation na tuondokane na tatizo hili la kukatikakatika kwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashangaa nimepitia mpango huu mara mbili, mara tatu, sijaona kabisa hilo jambo kama limeingizwa kwenye huu mpango. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa, anipe commitment ama aseme na wananchi wangu wa Tunduru kule wasikie kama ni kweli huu mradi upo ama haupo, kwa sababu tuliambiwa utaingizwa kwenye huu mradi lakini sijaona kama umeingizwa kwenye huu mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa aniambie ni kweli huu mradi utatekelezwa kwa kipindi hiki? Kama utatekelezwa je, ni lini utaanza huu mradi? Naomba pia utakapotekelezwa huu mradi ama utakapoanza kujengwa huu mradi, niombe sana utakapokuwa unatoka Songea kuja pale Tunduru Mjini, basi zijengwe njia tatu za usambazaji. Njia ya kwanza irudi Hulia, njia ya pili iende Nanyumbu Masasi na njia ya tatu itumike palepale Tunduru Mjini. Hapo Waziri atakuwa ametusaidia sana na tatizo hili litaenda kwisha kabisa na Mheshimiwa Waziri tutampongeza mno na tutamwombea aendelee kudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kutokana na ukubwa wa Wilaya ya Tunduru ilivyo, tunahitaji angalau tupate sub office nne ambazo hizi zinaweza kufanya kazi kwa urahisi, kuwafikia wadau wa umeme kwa urahisi kutokana na eneo lenyewe namna lilivyokuwa kubwa. Kwa hiyo, sub office hizi zipatikane nne ambazo zitakuwa na ikama za kiofisi zilizokamilika. Sub office moja ijengwe Milonde, ya pili iwe Nakapanya sub office na ya tatu iwe Nalasi sub office na ya nne iwe Lukumbule sub office. Kwa kufanya hivyo maana yake ni kwamba tutakwenda kusaidia kwa haraka matatizo haya ya umeme kwisha katika Wilaya ya Tunduru kutokana na kwamba jiografia ya Tunduru ni kubwa mno. Kwa kutumia ofisi moja tu na wana gari moja tu, kukitokea changamoto tatu kwa siku moja maana yake ni kwamba wanawafikia wananchi kwa ugumu mno. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne, nataka nishauri kwamba hizi transfoma zinazojengwa kwenye vijiji lazima tuziangalie kwa umakini ama tuangalie namna ya kufanya, kwa sababu zile transfoma zinazidiwa haraka sana na wateja wa umeme kwa sababu zina KVA 50. Kwa hiyo, kama zina KVA 50 maana yake ni kwamba kama zina wateja wengi inazidiwa kwa haraka na kunatokea tatizo tena la kukatika kwa umeme. Kwa hiyo, nashauri badala ya kufunga transfoma za KV 50 basi zifungwe transfoma za KV 100 na kama siyo hivyo basi kwenye kijiji kimoja zifungwe transfoma mbili, tatu na kuendelea kulingana na ukubwa wa kijiji chenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Na mimi pia niungane na Wabunge wenzangu kuipongeza bajeti hii ya Waziri Mkuu. Nimpongeze Waziri Mkuu pamoja na wataalam wote waliohusika kuiandaa bajeti hii. Lakini pili, nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kutupa miradi mingi kwenye majimbo yetu na sisi Wabunge wote ni mashahidi, tunamshukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, nianze kwa kuchangia upande wa afya. Wilaya ya Tunduru tuna Hospitali ya Wilaya ambayo ni kongwe kweli kweli. Hospitali ile imejengwa mwaka 1905, majengo yake mpaka hivi sasa ni chakavu kweli kweli. Niliwahi kukutana na Waziri wa TAMISEMI, kwa kipindi kile, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, nilipiga picha ile hospitali majengo yake nikamuonyesha ili kutaka kuomba fedha ya ukarabati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Ummy Mwalimu yeye mwenyewe akaridhia akasema kwamba, majengo haya kama tunakarabati ni sawa na kupoteza fedha za Serikali. Kwa hiyo, tukashauriana kwamba nitafute eneo ambalo tunaweza kupata hospitali mpya ya wilaya. Bahati nzuri tumepata hekari 20 ambapo tunaweza kujenga hospitali mpya ya wilaya, pamoja na nyumba za watumishi wa afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na uchakavu wa hospitali ile ya wilaya bado pia ina idadi chache sana ya watumishi. Ikama yake ni asilimia 55 katika 100. Lakini pia, katika hospitali ile tunao pia uhaba wa mtoa huduma wa mionzi, yupo mmoja tu. Sasa anapopata dharura ya kuugua ama akasafiri kwa muda wa wiki nzima maana yake huduma ya X-Ray inakosekana kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunashukuru hotuba hii ya Waziri Mkuu imezungumzia watumishi kwa hiyo, niombe watumishi watakapopatikana basi tuangaliwe sana katika Hospitali ya Wilaya ya Tunduru. Lakini pia, upande huo huo wa afya tukienda kwenye vijiji vyetu kuna zahanati, lakini katika zahanati zile bado watoa huduma wa afya ni wachache mno. Zahanati nyingi zina mtoa huduma wa afya mmoja mmoja. Tunazo zahanati takriban 11 ambazo zina mtoa huduma wa afya mmoja mmoja. Kwa mfano, Zahanati za Kidodoma, Nampungu, Majala, Cheleweni, Kitanda, Twende Mbele, Kajima, Kalulu, Mkowela pamoja na Zahanati ya Machemba. Hizi zote zina watoa huduma wa afya mmoja mmoja. Sasa, wanapopata changamoto ama dharura ya kawaida, ama siku wanakwenda kupokea mshahara mjini basi zahanati zile huwa zinafungwa na watu wanakosa huduma kabisa ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia upande wa elimu, nako kuna walimu wachache kweli kweli. Shule nyingi zina walimu wanne mpaka walimu watatu. Kwa hiyo tunaomba ajira hizi za walimu zikipatikana basi tuangaliwe kwa macho mawili kweli kweli.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia, namshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kutupatia shule za sekondari, na shule zile tayari tumeanza kuzijenga. Lakini kuna jambo ambalo limejitokeza, ama BOQ inaeleza kwamba tujenge kwa kuilaza tofali. Sasa, tunaona, tangu tumeanza mwanzo shule nyingi zinajengwa kwa tofali za inchi sita, na tofali zile zinakuwa zimesimama na majengo yanadumu na yapo mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia, BOQ inaeleza kwamba tulaze tofali kwenye majengo yote. Sasa tukiangalia kwa namna ya wingi wa majengo na idadi ya fedha iliyopo kwa kweli tunaona kana kwamba bado haitoshi, na kwamba tutahitaji fedha iongezeke zaidi. Kwa hiyo, kwa namna ya kujenga tofali kwa kuilaza kwa kweli bila shaka tunaweza kuwalaumu Wakurugenzi, kwa sababu ya kwamba fedha haikidhi majengo ni mengi. Kwa hiyo, niishauri TAMISEMI, kupitia wakandarasi wake ama mainjinia waangalie namna nyingine ya kuweza kutoa BOQ, ambayo inaeleza tujenge tofali la inchi sita kwa kawaida kwa namna tunavyojenga ya kusimama badala ya kulaza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Tunduru tulikuwa na uwanja wa ndege. Uwanja wa ndege ule una miaka zaidi ya 20 sasa haufanyi kazi, na kwa tafsiri sahihi ni kwamba umesimama ama umefungwa kabisa, haupo; na eneo lile lipo katikati ya mji. Kwa hiyo nilikuwa naomba Serikali, ikiwezekana eneo lile litolewe na wagawiwe wananchi ili wafanye shughuli za maendeleo, kama vile ujenzi wa nyumba za makazi; nilikuwa naomba sana hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kuhusu miundombinu ya elimu ya msingi, ambayo kwa kweli ni mibovu sana. Tunaishukuru Serikali kwa fedha ile za UVICO upande wa elimu ya sekondari tuko vizuri. Sasa, nilikuwa naomba tugeukie kwenye upande wa shule za msingi. Miundombinu ya elimu ya shule za msingi imechakaa mno, tena sana. Lakini pia, shule hizo hizo za msingi pamoja na miundombinu hiyo ya elimu hazina vyoo kabisa. Unakuta shule moja ina uhaba wa matundu 22, shule nyingine ina uhaba wa matundu 30. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana kwenye upande huu, basi na sisi tuweze kukaa sawa sawa na hatimaye tuweze kuboresha elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, tunavyo vituo vya afya ambavyo vinafanya kazi vizuri lakini pia, vituo vile, kwa mfano Kituo cha Afya cha Nakapanya jengo la upasuaji limekamilika. Tunayo Ambulance, tunamshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja kwenye kuomba kura tulimuomba na alituahidi kutuletea; na tunamshukuru tumepata Ambulance. Hata hivyo upasuaji haufanyiki kutokana na kwamba tumekosa baadhi ya vifaa vichache ili hospitali ile, tuweze kupata huduma ya upasuaji na hatimaye tumsaidie mama na mtoto. Vilevile katika Kituo cha Afya cha Matemanga majengo yote yamekamilika na vifaa vyote… (Makofi)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa, taarifa, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Nataka nimpe taarifa kaka yangu Hassan Kungu kwamba, ni kweli kabisa kile Kituo cha Afya cha Nakapanya, kutoka Nakapanya mpaka Makao Makuu ya Wilaya ni kilomita 80, ambapo wanawake wengi sasa wamekuwa wakijifungulia njiani. Sasa ni vizuri sasa Serikali ikasaidia kuleta hivyo vifaa kukamilisha kwa haraka sana ili wanawake hao wasiendelee kupata adha hii ambayo wanajifungulia barabarani. Ahsante. (Makofi)

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa hii kwa mikono miwili. Lakini pia, kwa kuongezea hapo, akina mama wajawazito huwa wanakwenda Wilaya ya Jirani ya Nanyumbu kwenda kufuata huduma ya upasuaji, na hatimaye Mbunge wa kule huwa ananitania sana kwamba hatuna Vituo vya Afya. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana Serikali tupate hivyo vifaa tukamilishe na tuweze kutoa hiyo huduma. Lakini pia, Kituo cha Afya cha Matemanga majengo yote yamekamilika vifaa vyote vipo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na mimi kwa kunipa nafasi leo kuchangia Mpango huu wa Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwanza na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna anavyoweza kuisimamia Serikali vizuri na maendeleo yanakimbia kweli kweli. Pili nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii ya Madini pamoja na Naibu wake na watendaji wote wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu kwanza kabisa mimi naomba uelekee kwenye eneo moja, ambalo Serikali kwa sasa imeweka zuio ama inaweka zuio la matumizi ya kemikali aina ya mercury ama zebaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaweka zuio la kutumia mercury na badala yake wanataka kuruhusu matumizi ya kemikali aina ya cyanide ndiyo itumike mbdala wa zebaki. Sasa mimi naomba niishauri Serikali kupitia Wizara ya Madini; na niliwahi kuuliza swali hapa namna ya usalama wa watumiaji wa kemikali ile ya cyanide usalama wao utakuwaje, na nilijibiwa na Wizara ya Afya badala ya kujibiwa na Wizara ya Madini. Kwa sababu, matumizi makubwa ya Mercury yanatumiwa na wachimbaji wadogo wadogo si Wizara ya Afya, si na watabibu; watabibu ni asilimia ndogo sana; lakini kwa upande wa wachimbaji wanategemea sana matumizi ya mercury, tena hasa wachimbaji wa dhahabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachomaanisha mimi ni kwamba kemikali aina ya cyanide ni hatari sana kwa matumizi ya binadamu. Kwanza kabisa namna ya upatikanaji wake ni gharama kubwa mno kuipata, kwa sababu ili uweze kuagiza lazima uwe na kibali maalum na kibali kile unalipia fedha nyingi kweli kweli ambapo mchimbaji mdogo hawezi kumudu hiyo gharama ya kulipia hicho kibali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni namna ya kuweza kuitumia ama kui-handle inahitaji utaalam wa kutosha mno. Ndipo najiuliza, je, Serikali imetoa elimu kwa kiasi gani kwa wachimbaji wadogo wadogo ili kuweza kuitumia ile kemikali hatari ili isiweze kuleta madhara? Kwa sababu ukiangalia madhara ya mercury na madhara ya cyanide, mercury ina madhara madogo sana, katika asilimia 100 labda ni asilimia 10 tu lakini cyanide madhara yake ni makubwa mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu cyanide ni hatari; kwa nini nasema hivyo? kama mtu yoyote anaweza kuweka kijiko kimoja cha cyanide kwenye maji ama kwenye mto wa maji ambayo yanatiririka basi maji yale mtu yeyote atakayeweza kuoga, akitoka hapo anakuwa ni mwekundu si mweupe tena, hata kama akiwa mweusi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama bahati mbaya tone moja la maji lenye cyanide binadamu yoyote akaliweka mdomoni basi huyo tunamzika kwa dakika mbili tu, madhara yake ni hatari kweli kweli kuliko mercury. Mercury tumeitumia kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mchimbaji, nafahamu na nimeitumia sana mercury. Mercury tumeitumia kwa muda mrefu sana, kwa miaka mingi, tunaona madhara yake ni machache na ni madogo sana kuliko cyanide. Lakini achilia mbali ya mdhara yanayopatikana ni kwamba sasa upatikanaji wa hiyo cyanide ni mgumu na ni mdogo ukilinganisha; wachimbaji wadogo wadogo wametapakaa Tanzania nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiidhinisha matumizi ya cyanide maana yake watakaokuwa na uwezo wa kuleta ile cyanide na kuitumia ni kampuni kubwa tu. Yaani tunazungumiza Barrick Geita huko na maeneo mengine. Lakini Ukienda kule Tunduru, Ruangwa na maeneo mengine hawana uwezo wa kuagiza cyanide na kuitumia. Lakini hasa zaidi wachimbaji hawa hawana kabisa elimu ya hiyo kemikali ya cyanide.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. HASSAN Z. KUNGU: …Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili nataka kuzungumzia suala la…

MWENYEKITI: Taarifa kutoka wapi, Mheshimiwa Matiko, taarifa.

TAARIFA

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, nataka nimpe taarifa mzungumzaji ameeleza vyema kwamba cyanide ni gharama kubwa lakini pia ina madhara. Lakini mercury ameeleza ina madhara kidogo kulinganisha na cyanide, lakini kwa sasa hivi inavyosemekana na nilishauliza swali hapa Bungeni bado wachimbaji wadogo wadogo wanaona mercury ni bei ghali zaidi. Pia inasemekana wanatumia mbolea, hizi mbolea ambazo tunatumia kwenye kilimo wanazitumia sasa hivi kusafishia madini. Nataka nimpe taarifa anavyochangia aendelee kuishauri Serikali wafanye tafiti ya kina kama kweli mbolea zinaweza kutumika na tukajua hazina madhara ziweze kutumika kwenye madini pia tuachane na cyanide.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kungu unapokea taarifa.

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa lakini kwa maelezo yafuatayo. Nilipokuwa nasema zebaki kwa maana ya mercury gharama yake ni ndogo yaani mchimbaji anao uwezo wa kununua mercury kwa shilingi 10,000 tena mpaka shilingi 5,000 akaenda kukamatisha dhahabu yake na ina uwezo wa kukamata 0.1 ikashika kulikoni na cyanide. Sasa cyanide kuinunua kibali tu peke yake si chini ya milioni 30 ni kibali tu hapo, hujainunua bado. Sasa najiuliza hawa wachimbaji wadogo wadogo watawezaje kumudu gharama za cyanide? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi nashauri…

MHE. HUSSEIN NASSOR AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa kutoka wapi, Mheshimiwa Hussein Amar.

TAARIFA

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mchangiaji anapozungumzia kwamba madhara ya cyanide pamoja na mercury kwamba mercury haina madhara. Mercury ina madhara makubwa na matumizi ya mercury na cyanide ni vitu viwili tofauti. Cyanide inatumika kwenye makinikia lakini mercury kwenye unga fresh. Lazima aeleze vizuri asilete tishio la kusema kwamba cyanide ni mbaya, cyanide tunaitumia na mimi nimeshaitumia zaidi ya miaka ishirini, nipo kwenye hiyo fani.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kungu unapokea taarifa.

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea hii taarifa lakini nadhani mtoa taarifa hajanielewa vizuri nini namaanisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napozungumzia madhara makubwa kati ya zebaki na cyanide lazima nieleweke. Cyanide kwanza utunzaji wake ni wa hali ya gharama kubwa ukilinganisha na mercury. Mercury hata mimi leo naweza nikawa nayo hapa nikakaa nayo nikaenda nayo popote bila shida yoyote lakini cyanide siwezi hata kuigusa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata wale ambao wanaitumia, wanatumia kwa vifaa maalum, tena kwa uangalizi mkubwa, watu wa usalama lazima wawepo. Sasa, je, yule mchimbaji ambaye hayuko kwenye kampuni atawezaje kutafuta dhahabu yake ya point mbili, tatu na atapataje uwezo wa kuipata hiyo cyanide. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima …

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. MWITA. M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kungu utaendelea kuchangia mpaka leo Spika atakapotoa maelekezo mengine.

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naomba niendelee na mchango wangu. Mimi nimeona matumizi ya cyanide na mimi nimetumia mercury kwa muda mrefu sana. Leo hii unaweza kuweka mercury ndani ya ndoo ya maji ya kuoga kwa bahati mbaya ukaoga na usipate madhara, lakini leo hii ukiweka tone moja tu la cyanide kwenye ndoo ya kuoga hata ukitumbukiza tu mkono usioge mwili mzima mkono huo unakuwa sio mkono wako tena. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini ninachomaanisha? Nachomaanisha ni kwamba kabla ya kuidhinisha matumizi haya cyanide Serikali kwanza iende ikatoe elimu ya kutosha, kwa wachimbaji wadogo wadogo waelewe namna ya kuitumia, waelewe madhara yake, pia waelewe namna ya kujikinga na madhara yatakayotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, madhara ya cyanide ni hatari tena kwa muda mfupi sana. Naomba nihame eneo hilo niende…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nami kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye hutuwezesha kutupa uhai na kusimama kwenye Bunge hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami kwanza kabisa niwapongeze Wenyeviti wote wa Kamati mbili pamoja na Makamu Wenyeviti. Pia nitachangia upande wa elimu kidogo na baadaye nitamalizia upande wa michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kama kuna watu ambao wamefanya miujiza katika nchi hii, basi ni walimu. Kwa sababu tunafahamu kabisa walimu tunao kwa 40% lakini wamefanikisha ufaulu kwa zaidi ya 80%. Sasa nini nakusudia kusema hapa? Ninachokusudia kusema ni kwamba, laiti kama tungekuwa na walimu wa kutosha, tafsiri yake tungekwenda kupata ufaulu kwa zaidi ya 100%. Kwa hiyo, pamoja na changamoto nyingi za kielimu zinazopatikana, jambo la kwanza la kufanyiwa kazi kwa asilimia kubwa au kwa umakini mkubwa ni kuhakikisha idadi ya walimu inaongezeka, inakuwa ile ambayo inastahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, idadi ya walimu inapaswa kwenda sambamba na miundombinu ya elimu. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuweka imara ama kwa kuimarisha miundombinu ya elimu nchini, lakini walimu ni wachache sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakupa mfano, ziko baadhi ya shule unakuta ina madarasa saba lakini walimu ni watatu. Mfano kule Jimboni kwangu mimi kwenye Shule ya Msingi ya Mindu na Shule ya Msingi Nampungu; shule hizi zina madarasa saba saba lakini walimu ni watatu watatu. Sasa nini kinakwenda kutokea pale? Wanafunzi wanaokwenda kusoma, je, watapata elimu bora kama madarasa ni saba walimu ni watatu? Tujaribu kuona. Kwa hiyo, najaribu kuishauri Wizara, itakapotokea ama Mheshimiwa Rais atakapotoa ajira basi naomba tuweke kipaumbele kwenye zile shule ambazo zina uhaba wa walimu ili kuweza kuwasaidia wanafunzi wale wapate elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda kwenye upande wa vyuo, nakipongeza sana ama naipongeza Wizara kwa kuamua Chuo cha Kilimo (SUA) kwa kuweza kusogeza huduma ile ya kilimo ama elimu ya kilimo karibu na wananchi. Kwa upande wangu mimi Tunduru tunalo tawi la Chuo cha Kilimo (SUA) na Chuo kile kilianza muda mrefu sana. Yaani kilianza muda mrefu kabla ya Tawi la Chuo cha SUA Katavi. Mheshimiwa Waziri na Katibu Mkuu kama wananisikiliza, hebu twende tukawasaidie watu wa Tunduru, kwa sababu Halmashauri ya Tunduru ilitenga takribani ekari 300 kwa ajili ya Tawi lile la SUA. Tumeweka majengo ya kutosha karibia asilimia 65, vifaa vipo, majengo yapo, kinachotokea majengo yale yanakwenda kuharibika bila ya kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, hebu afikirie Tawi lile la Chuo cha SUA kikafunguliwe na badala ya kama kilivyo hivi sasa kinafanya kwa siku 14 tu kama practice kwa wanafunzi ambao wanatoka maeneo mengine, tunaomba utuangalie Tunduru Tawi lile la SUA liende likafanye kazi na hatimaye tupate elimu ya kilimo. Kwa maana tunatambua kwamba kila kitu kwa sasa ni elimu. Tunaomba elimu ya kilimo isogezwe Tunduru kwa kwenda kufungua tawi lile la Chuo cha SUA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda upande wa michezo. Michezo zamani ilikuwa ni burudani pekee, lakini kwa sasa michezo ni ajira, michezo ni burudani, michezo ni afya na michezo ni uchumi. Wenzangu wamezungumza sana, tunakwenda 2027 sisi kwa kushirikiana na nchi jirani tutakuwa wenyeji wa AFCON, lakini ili tuweze kuwa wenyeji wa AFCON, tafsiri yake ni lazima tuwe tumekamilisha miundombinu ya michezo kwa maana ya kukamilisha vile viwanja vitatu ambavyo tunapaswa kuvijenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama sikosei tarehe 24 Desemba CAF wanakuja kukagua miundombinu ile ambayo sisi itatufanya kuwa wenyeji, lakini hadi dakika hii bado hatujaanza ujenzi wa viwanja vile vitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini mashaka yangu? Mashaka yangu ni kwamba utafika muda wa CAF kuja kukagua, sisi hatujakamilisha ama hatujafikia hata asilimia 50 ya ujenzi wa viwanja vile. Kitakachokwenda kutokea, tunakwenda kutia aibu kama Taifa kwa sababu tutakwenda kunyang’anywa wenyeji. Wenzetu Morocco waliomba ambao tayari wana viwanja. Sisi tumeomba tunataka kujenga viwanja, lakini mpaka leo jitihada zile za makusudi bado naziona kama ziko nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili, Serikali iliangalie na ichukulie kwa umakini mkubwa sana na ikiwezekana kama zitaanza kazi za ujenzi huo, basi zifanyike usiku na mchana ili kuendana na muda kwa sababu tumebakiza muda mchache sana ili kuweza kuthibitishwa kuwa wenyeji. Sasa naomba tukamilishe angalau hata kwa asilimia 70 au 60 ili tuweze kuwa wenyeji wa michuano hiyo ya AFCON. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na miundombinu hiyo ya michezo, nataka nizungumzie Timu ya Taifa. Timu ya Taifa inapaswa tuiangalie mara mbili. Hatuwezi kuwa wenyeji wa AFCON halafu tukawa na Timu ya Taifa ambayo siyo Madhubuti. Lazima Timu ya Taifa letu iwe madhubuti. Tumeona mfano wenzetu kule Ivory Coast wamefanya vizuri, wamekwenda sawa sawa wamekuwa wenyeji lakini na timu yao imefanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini nataka kuzungumza hapa? Ninachotaka kusema ni kwamba kwenye nchi yetu ni lazima tuingize kitu kinachoitwa uraia pacha. Tunao wachezaji wengi sana wanaocheza nje ya nchi na ni wachezaji wazuri kabisa ambao wangeweza kufanikiwa kuja kwenye Timu yetu ya Taifa, maana yake wangekuja kuiimarisha Timu ya Taifa. Sasa wanashindwa kuja kuiimarisha Timu ya Taifa kwa sababu nchi yetu hairuhusu uraia pacha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, timu nyingi tulizocheza nazo kule, zilizoshiriki AFCON ya hii iliyokwisha…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, muda wako umeisha, malizia.

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie sekunde kama moja au tatu au nne au tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri Cape Verde, yaani katika ile Timu ya Cape Verde waliocheza ambao wametoka nchi angalau kidogo haina upeo mkubwa wa mpira ni wachezaji wawili tu ambao nakumbuka kama alikuwa ni Inonga na Baka, ambao wametokea Tanzania, lakini wengine wote wanacheza Europe na maeneo mengine. Kwa mfano vile Morocco, Tunisia, Algeria, Cameroon, Congo, South Africa, hawa wote wanatumia mfumo wa uraia pacha na timu zao zile zilizoshiriki AFCON…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, muda wako umeisha, nashukuru sana.

MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)