Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Michael Constantino Mwakamo (39 total)

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, naitwa Michael Costantino Mwakamo, Mbunge kutoka Kibaha Vijijini. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, najua TASAF ilianza awamu ya kwanza kwa kuwapatia walengwa miradi ya uwekezaji kama majengo mbalimbali zikiwemo kumbi za maonyesho. Katika Jimbo la Kibaha Vijijini, wazee walipewa mradi huu awamu ya kwanza; je, TASAF wana mkakati gani juu ya kuwafanyia ukarabati jengo ambalo walipewa katika awamu ya kwanza ambalo sasa limechakaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutumia nafasi hii kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge, awamu ya kwanza ilijikita zaidi katika ujenzi wa miundombinu na si Kibaha Vijijini tu bali katika halmashauri nyingi sana katika nchi yetu ambazo majengo haya au miradi hii ilifanyika. Sasa baada ya awamu ya kwanza kuisha na kwenda awamu ya pili na sasa tuko awamu ya tatu phase II, ni kwamba majengo haya na miradi hii yote ilikabidhiwa kwa Wakurugenzi wa Halmashauri husika. Na ni wajibu wa Wakurugenzi wa Halmashauri kuhakikisha kwamba wanatunza majengo haya na wasiwaachie tu wale walengwa peke yao; ni wajibu wa Wakurugenzi kuhakikisha sustainability ya miradi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge kuelekea katika halmashauri yake na kuhakikisha tunakwenda kuangalia miradi hiyo na kuwaagiza Wakurugenzi ili kuhakikisha kunakuwa na sustainability.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri juu ya ujenzi wa barabara hiyo, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali imeshafanya upembuzi yakinifu wa kilometa hizo 100 ambazo zinatokea Makofia kuendelea Kisarawe, je, ni lini Serikali italipa fidia wananchi hawa ili kupisha ujenzi huo uendelee kwa sababu ni wa muda mrefu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa barabara hii; na kwenye majibu yake anakiri kwamba ametenga pesa ya kufanyia ukarabati wa muda wakati wakisubiri tukipata pesa, naomba niifahamishe Serikali kwamba kwa sasa barabara hii haijafanyiwa ukarabati huo kwa miaka mingi. Kwa kuwa pesa hizi zimepangwa mwaka huu wa bajeti, je, Serikali haioni sasa ni muda sahihi kutafuta fedha za haraka kuzifanyia ukarabati barabara hizo kwa sasa kwani kipande cha kutoka Mlandizi kwenda Mzenga kina mashimo makubwa utadhani mabwawa ya kuvulia samaki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, kila hatua inayofanyika ndiyo ujenzi wenyewe wa barabara ya lami unavyoendelea. Barabara hii haitaanza kujengwa mpaka kwanza fidia ya wananchi hawa ambao bahati nzuri tayari wameshatathminiwa watakapolipwa.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Mwakamo kwamba wananchi hawa watalipwa fidia pale tu ambapo Serikali itapata fedha. Jitihada kubwa zinafanywa na Serikali kuhakikisha kwamba tunapata fedha ili tuweze kuwalipa hao wananchi ambao tayari wameshaainishwa.

Mheshimiwa Spika, kwa swali lake la pili kwamba barabara hii haijafanyiwa matengenezo; naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kupitia Bunge hili naomba kumuagiza Meneja wa Barabara Mkoa wa Pwani aweze kutembelea barabara hiyo na kuangalia upungufu uliopo aweze kuikarabati kwa sababu fedha imetengwa ili wananchi waendelee kupata huduma ya barabara hii. Ahsante. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa kuwa ahadi ya barabara hizi imetolewa pia kwenye Jimbo la Kibaha Vijijini kwenye Mji wa Mlandizi na tayari kuna barabara ya kilometa moja imeanza kutekelezwa na miezi sita sasa haijalipwa chochote. Je, Serikali haioni ni muda sahihi sasa kumalizia ile fedha ili mkandarasi amalizie ili hata ile kazi ambayo ameshaanza kufanya isiharibike?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa
Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, barabara zote ambazo wakandarasi wako site zitaendelea kulipwa fedha ili ziendelee kukamilika, ikiwemo hii barabara ambayo umeitaja hapa.

Kwa hiyo, haitakwama kwa sababu ninaamini kabisa kwamba, sisi kama Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kupitia TARURA tunapitia zile certificates ambazo wakandarasi wanazileta kwetu na tunazitolea fedha. Kwa hiyo, na hili tumelisikia na nikuhakikishie kwamba, itaisha kwa wakati kama ambavyo iliahidiwa na viongozi wetu wakuu, ahsante.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri yenye mikakati ya Serikali juu ya watumishi wao, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa katika Jimbo la Kibaha na majimbo mengi nchini kuna watumishi ambao wamechelewa kulipwa mafao yao kutokana na waajiri kutokupeleka michango yao kwa wakati. Je, Serikali inawasaidiaje watumishi hao, kwani waajiri wao wamefanya kinyume na utaratibu wa sheria?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kuanzia mwaka 2016 mpaka 2020, kulikuwa na maelekezo mbalimbali ya Serikali juu ya upandishwaji wa vyeo, kuna watumishi ambao wamestaafu wakiwa na barua mkononi lakini wameshindwa kulipwa kutokana na barua zao walizo nazo. Lakini pia kuna watumishi walichelewa kupandishwa vyeo kwa sababu ya waajiri kuwasahau kwenye kuingiza kwenye mfumo.

Je, Serikali inawasaidiaje watumishi hao ili waweze kupigiwa hesabu zao kulingana na haki na sheria ilivyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, VIJANA NA AJIRA (MHE. PASCAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Costantino, kwa kufuatilia vizuri sana haki za wananchi wake katika Jimbo la Kibaha Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la kwanza ambalo ameuliza ni utaratibu gani tunaochukua kwa wale waajiri ambao wanachelewesha michango lakini pia wanaosababisha fedha zile zisiweze kulipwa kwa wakati, hasa hizi za pensheni. Tumekwisha kuchukua hatua mbalimbali kwa mameneja wa mikoa wa PSSSF, lakini pia hata kwa NSSF kwenye maeneo ambayo tunagundua kwamba kuna uzembe wa ukusanyaji wa michango. Tumekuwa tukichukua hatua kali kwa wakurugenzi wa PSSSF Mikoa, lakini pia complying officers ambao tumekuwa tukiwaagiza kwa wakati wote watoe taarifa ya wadaiwa sugu kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu waajiri wanapochelewesha michango ni pamoja na kukwepa kodi, kwa sababu kuna PAYE kwenye mshahara wa mfanyakazi, kuna fedha inayopaswa kuinia katika Mfuko wa WCF, kuna fedha inayopaswa kulipwa kama Skills Development Levy, lakini vilevile kuna fedha ambayo ni ya mafao ya mfanyakazi, anapomaliza wakati wake wa kazi itamsaidia kwenye maisha yake. Kwa hiyo tunachukua hatua kali, na sheria inaelekeza na tumekuwa tuna kesi mbalimbali ambazo zinaendeshwa kwenye mahakama mbalimbali hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kuagiza kwamba mameneja wetu wa mikoa na complying officers waweze kufuatilia michango.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili kwa kifupi, ni kwamba swali hili liko Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma, kwa wafanyakazi ambao ni wa Serikali. Nikuombe Mheshimiwa Mbunge, mimi pamoja na wewe tuweze kuiona ofisi ile na tuweze kufuatilia madai hayo ili waweze kupata haki na stahiki zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, ahsante, naitwa Michael Constantine Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini.

Naomba niulize swali la nyongeza; kwa kuwa Kibaha Vijijini kuna scheme ambayo inaendelea kujengwa lakini hijaaza uzalishaji na tatizo kubwa ni mifugo kuingia na kufanya uharibifu.

Je, Serikali itatusaidiaje kuondoa tatizo hilo kuhamisha wafugaji wale kwenda kwenye eneo la ufugaji la NARCO ili wakulima wa eneo lile walime kwa uhakika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hili ni jambo specific na ni jambo linahusu sehemu moja, nitamuomba baada ya hapa tukae tukutane ili tukae na wenzetu wa Wizara ya Mifugo ili tuweze kulijadili na kulitatua kw apamoja. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kwenye majibu ya msingi ya Mheshimiwa Waziri hajaeleza na wala hajaitaja Ranchi ya Ruvu iliyopo pale Vigwaza kama imeshatengwa, sasa kwa kuwa kuna migogoro mingi ya wakulima na wafugaji kwenye Mikoa ya Pwani na maeneo mengine ya jirani kama Wilaya ya Chalinze na Kibaha Vijijini; Je, Serikali haioni huu ni muda sahihi sasa kupanga na Ranchi ile ili kumaliza migogoro ya wakulima na wafugaji kwenye maeneo hayo?

Swali la pili; kwa kuwa Mheshimiwa Waziri anafahamu kwamba migogoro mingi ya wakulima na wafugaji inapelekea watu wengi kupata ulemavu wa kudumu na wengine kufariki na kwa sababu ipo Ranchi hiyo ninayoitaja ya Ruvu ambayo haijafanyiwa; Je, Waziri haoni kwamba ni muda sahihi wa kufika kwenye maeneo ya Mkoa Pwani hasa Wilaya hizo za karibu kuwaelimisha wafugaji wadogo kwenda kuomba na kupata utaratibu wa kukaa kwenye Ranchi hizo kuondoka kwenye Bonde la Ruvu ambalo lina migogoro? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Michael Costantino Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru na kumpongeza sana lakini pili kwanini Ranchi ya Ruvu haikutamkwa katika majibu haya. Ranchi ya Ruvu katika maelekezo ya muda mrefu uliopita ya Serikali haikupangwa kwa ajili ya vitalu vya muda mrefu. Ranchi ya Ruvu na Ranchi ya Kongwa hazikupangwa. Kwa hivyo, baadaye kwa utashi na maelekezo ya viongozi wetu wakuu na tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kutaka kuona tunatatua changamoto ndiyo uamuzi wa kukata vitalu vya muda mfupi ukafanywa kwa hivyo Ranchi ya Ruvu ikapangiwa ikatwe vitalu jumla ya 19 na hivi sasa ninavyozungumza jumla ya Ng’ombe zaidi ya Elfu Tisa katika vitalu hivi vidogo vidogo vilivyopo katika eneo nzima la Ranchi Ruvu vimeshagawiwa kwa wafugaji, hili ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni namna ya kuweza kuwatoa wale wafugaji walioko katika maeneo ya Bonde la Mto Ruvu na labda kuwapa nafasi huku. Serikali jambo hili inalifanyia kazi siyo peke yake katika Mto Ruvu lakini vilevile na mito mingine kama Kilombelo, Ruaha na mingineyo. Maelekezo ya Serikali ni kwamba iko Kamati ya Mawaziri Nane inayofanya tathmini ili tutakapotoka na majawabu, tutatoka na majawabu ya pamoja yatakayokwenda kutatua kabisa tatizo hili la muda mrefu la wafugaji, wakulima na watumiaji wengine wa ardhi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, hali ilivyo kwenye Wilaya ya Newala ni sawasawa na Kibaha Vijijini kwenye shule za Dutumi, Madege na Magindu. Je, Serikali haioni kwamba sasa ni wakati sahihi na kule kulifanyia ukarabati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kumjibu Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza katika jibu la msingi kwamba mwakani tuna madarasa zaidi 12,000 kwa ajili ya ukarabati wa shule za msingi nchini. Kwa hiyo, naamini kwa sababu moja ya utaratibu wetu ni kuhakikisha kwamba tunayafikia majimbo nchini, likiwemo Jimbo la Kibaha Vijijini. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge aondoe wasiwasi kwa sababu tutaweka katika mpango na wananchi wake watapata hiyo faida ya yeye kuwepo ndani Bunge. Ahsanteni sana kwa kunisikiliza. Ahsante sana.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, mkandarasi anayepeleka umeme Kibaha Vijijini kwenye Kijiji cha Kimaramisale, tulikubaliana afike site kwa maelezo yake mwezi wa Sita na mpaka sasa hajafika. Je, ni nini kauli ya Serikali kwa mkandarasi huyu ili akamalizie kazi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Michael, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wakandarasi wote wa REA wako katika maeneo yao ya kazi mbalimbali. Unakuta mkandarasi mmoja katika mkoa mmoja labda ana wilaya nne au tano na tulipunguza kazi. Naomba nieleze kwamba baada ya hapa nitalifuatilia jambo hili kujua kwa nini mkandarasi huyu hajafika na kama amefika maeneo mengine basi ni lini atafika katika eneo la Mheshimiwa Mbunge alilouliza.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Pwani unaongoza kwa zao kubwa la korosho. Je, nini mkakati wa Serikali kufufua Kiwanda cha Korosho TANITA Kibaha?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ambayo pia tunalenga katika kuhakikisha tunaongeza thamani ni kwenye zao la korosho. Viwanda vingi ambavyo vilikuwa havifanyi kazi, mkakati wa kwanza ni kuona vile inavyowezekana kurudisha katika mikono ya Serikali ili tutafutie wawekezaji wengine lakini pia pili, ni kuvutia wawekezaji wapya kuwekeza katika viwanda vipya ambavyo navyo vitaongeza kazi ya kuchakata zao la korosho ili kuziongezea thamani katika Mikoa ya Pwani na Mikoa ya Nyanda za Kusini ambao wanalima zaidi zao la Korosho. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza niikumbushe Serikali kwamba, kuna eneo la Soga kwenye shamba la Mohamed Enterprise tayari kulishakuwa na maelekezo ya ekari 500 kurudi Serikalini. Kwa kuwa, kuna changamoto mbalimbali zinazoendelea kusababisha kutokutekelezwa kwa agizo hilo.

Je, Waziri atakuwa yupo tayari kuambatana nami mara baada ya Bunge kwenda kusaidia kuondoa hizo changamoto zinazosababisha utekelezaji wa agizo hilo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, pale Kata ya Kikongo kuna mwekezaji anaitwa Trans-continental na shamba moja la UFC ambalo lipo mikononi mwa Serikali, kuna wananchi ambao wapo pale muda mrefu, wana miaka mingi, karibu 15 mpaka 20, na wawekezaji hao hawajaendelea.

Je, Serikali inatoa tamko gani kuwaruhusu wawekezaji hao kuendelea na shughuli zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Michael Costantino Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza kuhusiana na suala la Soga kwenye shamba la Mohamed Enterprise naafikiana nawe Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakwenda kutatua kero hizi maana tunaambiwa yanayoendelea huko siyo mazuri sana.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili kuhusiana na jambo la trans- continental kule Kikongo na Waya mifugo, Mheshimiwa Mbunge nataka nikuhakikishie utayari wa Serikali, kwenda kushirikiana nawe kutatua kero hizi. Pili, katika Shamba la Waya, tutashirikiana na Wizara ya Mifugo kuhakikisha kwamba hatua zinazostahiki kufuatwa ili kukabidhiwa shamba hilo kama ambavyo Serikali iliamua nazo pia zinafuatwa. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi hii, lakini nitumie nafasi hii kwanza kuipongeza Serikali, nimepitia taarifa yao ya miradi ya Tanzania ya Kidigitali, nimeona Kata za Gwata, Bokomnemela na Dutumi zimewekwa kwenye orodha ya Kata 763; nawashukuru sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa swali la nyongeza; je, ni lini wakandarasi hawa ambao wameshapatikana watafika kwenye kata hizo na kuanza utekelezaji wa mradi husika? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni kwa kiwango gani huduma ya 3G inawasaidia Watanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tumejibu katika swali la msingi, tender ya upatikanaji wa mawasiliano katika miradi ya World Bank ambayo ilitangazwa tarehe 24 itafunguliwa tarehe 2 Desemba. Na baada ya kufunguliwa, mchakato wa upatikanaji wa vibali na hatimaye kuanza kwa hatua za ujenzi utakapokamilika ujenzi wa mawasiliano katika hizo kata utaanza mara moja.

Mheshimiwa Spika, katika kipande cha pili cha swali la Mheshimiwa Mwakamo, ni kwamba huduma ya 3G itawafikia lini Watanzania?

Mheshimiwa Spika, labda nitoe tu takwimu za harakaharaka; katika teknolojia ya 2G mpaka sasa kwa population coverage mpaka sasa Tanzania tumefikia asilimia 96; lakini kwa 3G tumeshafikia asilimia 72; 4G tumeshafikia asilimia 55. Internet penetration mpaka sasa kwa nchi yetu ni asilimia 50. ahsante sana.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, Mji wa Mlandizi unakua kwa kasi na pale Mlandizi kuna majengo kwenye Kituo cha Polisi yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi. Je, ni lini Serikali itaweka nguvu za Serikali kusaidia nguvu za wananchi kumaliza nyumba zile? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Michael, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tutaomba uongozi wa Polisi wa Mkoa ilipo Wilaya ya Mheshimiwa ili iweze kufanya tathmini kujua kiwango cha fedha zinazohitajika kwa ajili kukamilisha ili tuweze kuingiza kwenye mpango na hatimaye kiweze kumaliziwa. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa jibu la Serikali la mara zote ni kuendelea kutafuta fedha kwa ajili ya utengenezaji wa barabara hizo zilizotajwa lakini kwa kuwa pale ni eneo muhimu na kuna ajali nyingi zinatokea. Je, Serikali haioni kwamba tunaweza kutanua maeneo yale kama ambavyo imetanuliwa barabara ya pale Picha ya Ndege, Kongowe na Chalinze ili kuweza kupunguza msongamano wa eneo lile la Mlandizi?

Mheshimiwa spika, swali la pili, kama tatizo ni fedha na barabara hii inayozunguzwa, amezungumza barabara ndefu na mimi shida yangu ni pale Mlandizi, hatuwezi kuweka taa za haraka barabarani za kuongozea magari ili kupunguza misongamano iliyopo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Kibaha na sote ni mashahidi ambao wengi tunapita kwenye barabara hii. Kutokana na hoja ya Mheshimiwa Mbunge na jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia ni kweli tulichosema ndio mpango wetu wa Wizara, lakini Wizara baada ya kufuatilia tunajaribu kuangalia uwezekano, tutafanya study tuwe na mpango wa muda mfupi ili kupunguza ajali, lakini pia na msongamano.

Kwa hiyo tutaangalia kama njia sahihi na rahisi itakuwa ni kupanua barabara kwa maana ya njia nne kama sehemu nyingine ama kuweka taa ili kwanza kuokoa ajali, lakini pia kupunguza msongamano ambao sasa umekuwa ni adha kubwa kwenye hiyo barabara. Msongamano huo pia upo hasa katika hizi njia ndogo zinazotoka Bagamoyo kwenda Mzenga ambapo wananchi wengi sana wanachelewa kukatisha ile barabara na kuona magari makubwa tu ndio yanayopita kwa muda mrefu. Kwa hiyo, tumelichukua na Wizara tunachukua kwa umuhimu mkubwa ili kuokoa ajali na pia kupunguza msongamano. Ahsante.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niipongeze Serikali kwa majibu mazuri, lakini niongezee nyongeza moja kwamba hadi leo hii lile eneo ambalo tulilizungumza na liliuliziwa swali, Serikali imetekeleza vizuri na limeziba lile eneo, kwa hiyo tunawapongeza sana. Swali moja dogo la nyongeza; kwa kuwa wakulima wa bonde hilo walikuwa wanazuiwa kuendeleza shughuli zao za kilimo katika maeneo hayo kutokana na Mto Ruvu kupungua kasi yake ya maji na sasa eneo lile limeshazibwa.

Je, Serikali inampango gani sasa wa kuwasaidia wakulima wale waendelee na shughuli zao za umwagiliaji mdogo?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nipende kushukuru kwa kupongeza jitihada kubwa ambayo taasisi ya DAWASA imeweza kufanya na sasa maji hayatapakai tena. Vile vile Serikali ina mipango mbalimbali kuhakikisha suala la maji kuchepuka kutoka kwenye mto tunakwenda kulidhibiti. Hili tutalifanya kwa kutumia Bonde la Maji ya Wami-Ruvu na tayari wameshapata mhandisi mshauri ambaye anafanya usanifu kwa ajili ya kujenga bomba kuu moja ambalo wananchi watapaswa kujiunga katika kikundi kimoja ili waweze kuhudumiwa kwa sehemu moja halafu wao sasa ndio watachepusha kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuipatia Wizara fedha. Tayari tumeshaingiza mitambo ya kuchimba mabwawa na tunatarajia kama Wizara tuweze kuchimba mabwawa madogo madogo ambayo nyakati za mvua tutaweza kuvuna maji, tutayahifadhi pembezoni mwa mto huko ili wananchi waweze kuja kuyatumia kwa ajili ya umwagiliaji na wasiweze kudhuru mto katika shughuli za kuleta chanzo cha maji kwa shughuli za kibinadamu.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, kwenye Jimbo la Kibaha Vijijini kwenye Kata ya Magindu, Ruvu, Gwata na Dutumi kuna wafugaji wa kutosha lakini majosho hakuna: Je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kunipatia sehemu ya majosho aliyoyataja kwamba yapo kwenye bajeti? (Makofi)
WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakamo, Mbunge wa Kibaha kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tutapanga vizuri kwenye majosho ambayo Serikali itatupa fedha kwa mwaka wa fedha ujao ili kuhakikisha kwamba Jimbo la Kibaha pia linapata majosho, yanaweza yasiwe yote lakini angalau maeneo yaliyo muhimu yenye wafugaji wengi, tutaongea pamoja na Mheshimiwa Mbunge ili tuone kwamba maeneo hayo yanapata majosho pia.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa stendi ya Mbezi ni miongoni mwa miradi ya kimkakati inayosimamiwa na TAMISEMI. Je, ni lini mradi wa kimkakati wa Soko la Mlandizi utajengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya tathmini ya maeneo yote ambayo yanahitaji kujengewa stendi za kimkakati ikiwepo Halmashauri ya Kibaha. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tushaelekeza halmashauri walete andiko walishaleta na najua kulikuwa kuna mazungumzo ya eneo wapi tujenge ile stendi. Nikuhakikishie kwamba TAMISEMI tunaendelea na kufanya tathmini ya mapendekezo ya halmashauri ili twende kujenga stendi ile na tutafanya hivyo mapema iwezekanavyo. Ahsante.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru Serikali kwa majibu mazuri ya kuihakikishia Halmashauri au Wilaya ya Kibiti kupata Mahakama ya Wilaya. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa sasa hivi Mahakama hiyo iko kwenye jengo la Mahakama ya Mwanzo ambalo limechakaa. Je, Serikali ina mpango gani kulitumia au kulifanya ukarabati jengo hilo ambalo litabaki kutumika kama Mahakama ya mwanzo?

Swali la pili; Mkoa wa Pwani una Mahakama za Mwanzo 21, kati ya hizo zipo ambazo zimechakaa na nyingine zimebomoka babisa ikiwemo ya Kibaha Vijijini pale Kata ya Ruvu na Kata ya Magindu. Je, Serikali ina mpango gani wa kuzijenga hizi zilizobomoka na kuzifanyia ukarabati zile ambazo zimechakaa.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika,
ninakushukuru, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Michael Mbunge wa Kibaha Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nipende kufahamu endapo tutajenga Mahakama hii ya Kibiti hilo jengo ambalo sasa linatumika kama tutalikarabati. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jengo hilo litaendelea kutumika na Mahakama ya Mwanzo kwa kuwa saa hizi wametuhifadhi Mahakama ya Wilaya, kwa hiyo tutalikarabati.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili anapenda kufahamu katika Mkoa wa Pwani Mahakama ya Mwanzo hizi mbili ambazo amezitaja. Mahakama yetu imeweka mpango kabambe wa kuhakikisha tunakarabati Mahakama zote ambazo zimechakaa, katika Mkoa wake wa Pwani tunakwenda kukarabati Mahakama 19 pamoja na hizi mbili ambazo amezitaja.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali itapeleka wakandarasi kwenye Vijiji vya Bokomnemera, Kimalamisale na Mpiji ambapo wana shida ya mawasiliano?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mwakamo tayari ameshalifikisha jambo hili na tulishaongea na tayari hatua zimeshaanza kuchukuliwa ili kufikisha huduma ya mawasiliano katika eneo hilo.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa gari analolizungumza Mheshimiwa Naibu Waziri ni gari aina ya lori na kituo kile kina shughuli nyingi za kipolisi kwa sababu eneo la Mji wa Mlandizi limejengeka. Je, Serikali haioni iko haja sasa ya kuwapelekea gari dogo litakaloendana sawa na kasi ya kukabiliana na uhalifu katika Mji ule?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili jengo la Kituo cha Polisi Mlandizi linatumika kwa ajili ya OCS pamoja na OCD, sasa kwa kuwa jengo hili ni dogo hawaoni sasa ni muda muafaka wa kutafuta eneo lingine kuzitofautisha ofisi hizi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwakambo Michael, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mosi, tunatambua kwamba lori kwa kweli lina changamoto kwenye ufuatiliaji wa doria hasa kwenye vichochoro na njia kama hizo, lakini kwa shughuli nyingi za kiuchumi zinazoendelea pale Mlandizi wanayo kweli haki ya kupata gari ndogo. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mwakambo pamoja na Wabunge wote kwamba Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Jeshi la Polisi, karibuni itapata magari kwa ajili ya kuwezesha ofisi zote za ma OCD kupata gari ndogo kuwezesha kufanya kazi zao kwa ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu jengo hili, tumeeleza ofisi zitakazoongezeka kama kwenye jibu langu la msingi tulivyosema lakini kutokana na hoja kwamba eneo ni dogo, namwomba Mkurugenzi, kwa maana ya Halmashauri ya Wilaya ya Kibaha, kutafuta eneo, na pale litakapokuwa limepatikana, sisi always tutakuwa tayari kushirikiana na Halmashauri hiyo kuimarisha majengo yanayotakiwa kwenye kituo kile, nashukuru.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa kwenye majibu ya Mheshimiwa Waziri eneo ambalo tayari limeshafanyiwa upembuzi yakinifu liko Mkoa wa Morogoro na Wilaya ya Morogoro Vijijini.

Je, Serikali haiko tayari sasa kuja kufanya upembuzi yakinifu kwenye Jimbo la Kibaha Vijijini kwenye Kata za Ruvu, Dutumi, Kwala, Gwata, Kikongo ili tuweze kuona namna bora ya kuwahudumia wakulima wadogo katika eneo hilo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Tunaposema wakulima kwenye Bonde la Ruvu ni wakulima wadogo, ni wadogo kweli kwa sababu wanatumia umwagiliaji kwa kutimia mashine ndogo na keni za mkono; na kuna katazo la watu kufanya umwagiliaji kwa kutumia Mto Ruvu. Je, Serikali inatoa tamko gani kuwasaidia watu wa Jimbo la Kibaha Vijijini kuendelea na umwagiliaji wa kutumia keni kwa kuwa hawajawa na mabwawa ya kutosha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe 20 Machi, 2023 tuliingia mikataba na washauri waelekezi kwa ajili ya kwenda kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina katika mabonde 22 hapa nchini Tanzania likiwemo Bonde la Mto Ruvu. Nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba katika skimu alizizozitaja zitaingia ndani ya mpango huo wa Serikali ambapo kazi inaanza mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusiana na katazo; kwa mujibu wa sheria inayoongoza matumizi ya maji na sheria za mabonde, imeweka utaratibu wa matumizi ya maji kupitia kibali maalum. Sisi kama Wizara tutakaa na wenzetu wa bonde kuweka utaratibu mzuri ili mwisho wa siku wakulima wetu wale wadogo walime kupitia taratibu zote za kisheria na kutunza mazingira pia. Kubwa zaidi ni kwamba tutaweka miundombinu mikubwa zaidi ili wananchi waachane na changamoto hiyo ya kubeba makopo kwenda kumwagilia.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, kwenye mradi wa SGR kwenye eneo la Kikongo pamoja na Msuwa kuna uhitaji wa kuweka kivuko na TRC waliahidi kuweka ni muda mrefu sasa.

Je, Waziri atakuwa yuko tayari kutoa agizo kwa Mkururgenzi wa TRC kukamilisha mradi huo kabla haujaanza utekelezaji wake?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakamo Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumejadili na Mheshimiwa Mbunge na tayari nilishatoa maelekezo kwa Mtendaji wa TRC ili waweze kuangalia eneo hilo ambalo ni muhimu sana kuwa na kivuko kwa waenda kwa miguu ili waweze kuangalia uwezekano wa kujenga kivuko mahali aliposema Mheshimiwa Mbunge, ahsante.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, Jimbo la Kibaha Vijijini kwenye Kata ya Kwala, tulipokea pesa kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya; je, ni lini Serikali itamalizia fedha zilizobaki kwa ajili ya kukamilisha na kuanza kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali inafanya tathmini ya vituo vya afya vyote vilivyopelekewa pesa na ambavyo havikukamilika. Pale tathmini itakapokamilika, basi tutatenga fedha kwa ajili ya kuweza kumalizia vituo hivi vya afya.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa diplomasia ya kiuchumi inafanya watanzania wengi kwenda nchi mbalimbali duniani kutafuta mazingira ya kiuchumi na ili wasibaguliwe kule na wanataka kufaidika na huduma hiyo…

SPIKA: Mheshimiwa swali lako.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka wa kufanya marekebisho ya sheria hizo ili Watanzania hao waweze kufaidika na uchumi wa dunia? (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu katika majibu yangu ya swali la msingi la Mheshimiwa Agnesta, kwamba Serikali imeona juu ya umuhimu wa waliokuwa watanzania hawa waliochukua uraia wa nchi nyingine kuweza kufaidika na fursa mbalimbali hapa nchini. Lakini siyo tu kwa wao kufaidika, hata kutoa michango yao katika uchumi wa nchi yetu na maendeleo ya nchi hii.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana nimeeleza kwamba katika kuliona hilo tupo katika hatua za kuweza kuruhusu utaratibu wa hadhi maalum kwa raia hawa ambao wataweza kufaidika na mambo mbalimbali na wataweza kuchangia vilevile katika maendeleo ya nchi yetu. Miongoni mwa fursa hizo ni fursa tatu tu ambazo zitahitaji baadae marekebisho ya sheria na wakati huo utakapofika tutazileta, lakini fursa zingine zote hazihitaji mabadiliko ya kisheria na zitaweza kuruhusika kwa pale ambapo utaratibu huu utakapokuwa umekamilika.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa Jimboni Kibaha Vijijini kuna kongani kubwa ya viwanda Kwara na viongozi wa eneo hilo hawana uelewa wa kutosha juu ya miongozo hiyo. Je, Serikali haioni ipo haja sasa ya kufika Jimboni Kibaha kuwapa mwongozo ili waweze kusimamia chanzo hiki cha mapato?

Swali la pili, kwa kuwa maeneo ya Kibaha Vijijini , viwanda vingi vitajengwa na vingine vitatumia Sheria ya EPZ. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kubadilisha sheria ili viwanda hivi vitakavyojengwa kwenye EPZ viweze kuchangia shughuli ya maendeleo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ni kweli Kibaha katika Mkoa wa Pwani ni moja ya maeneo ambayo kuna uwekezaji mkubwa sana wa viwanda hapa nchini. Kwa takwimu tulizonazo kwa Aprili tu takribani miradi saba imewekezwa katika eneo hili ambalo ni muhimu sana kwa wawekezaji wengi.

Mheshimiwa Spika, Wizara na Serikali kama nilivyosema, maeneo yote ya uwekezaji pamoja na eneo la Kwala Industrial Park ambalo linajengwa pale, tunawaelekeza wawekezaji kuhakikisha wanachangia maendeleo na miradi ya kijamii. Pili katika maeneo hayo tumeshaweka kwenye Serikali za Mitaa Idara Maalum ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara ambao kazi yao wao ni kuwaelimisha wawekezaji hawa kwa kushirikiana na TAMISEMI kuhakikisha wanachangia mapato wanayopata kutoka na uwekezaji huo.

Mheshimiwa Spika, pili, kwenye maeneo ya uzalishaji kwa ajili ya mauzo nje EPZ tumeshasema na tunao mpango wa kuweka utaratibu wa uwekezaji, ambao unaelekeza wawekezaji hawa ambao wanafaidika, wananufaika na vivutio maalum ambayo kimsingi ni kodi za Watanzania, kuhakikisha mapato wanaopata au faida wanazopata kutokana na uwekezaji huo waweze kurudisha kwa wananchi kupitia shughuli mbalimbali za kijamii, kama ni elimu, afya, maji au barabara kulingana na mahitaji ya maeneo husika ambayo wanawekeza wawekezaji hao, nakushukuru sana.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Barabara ya Makofia- Mlandizi – Mzenga mpaka Vikumbulu miaka mitatu iliyopita walifanyiwa tathmini ya kilomita 30 na miezi miwili iliyopita wamerudi kubadilisha kurudi kwenye mita 22.5;

Je, ni lini wananchi wale watalipwa fidia pamoja na mabadilko hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, tayari tumekwenda kwa ajili ya kufanya tathmini kwa watu ambao wapo ndani ya mita 22.5. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba maandalizi yanafanyika ndiyo maana tumekwenda sasa hivi ili waweze kulipwa fidia. Ahsante.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Serikali ilishatupa taarifa Wabunge juu ya uwepo wa minara hiyo 758; je, ni lini sasa Wabunge tutapata taarifa rasmi na kuzirudisha kwa wananchi kwamba kazi hiyo inaanza? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, tumeingia mikataba na mikataba ya utekelezaji wa miradi hii ni kuanzia miezi tisa mpaka miezi 20. Kwa sababu muda wa mkataba ndio ambao Serikali tunaosimamia, tunahakikisha kwamba ndani ya muda wa makubaliano watoa huduma wote, kulingana na idadi ya minara ambayo waliipata, miradi hiyo iwe imekamilika ndani ya muda wa mkataba, ahsante sana.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niombe kufanya marekebisho kidogo kwa sababu Bonde la Wami Ruvu sio Bonde la Mto Ruvu haya ni mabonde mawili tofauti lakini pamoja na marekebisho hayo na majibu mazuri ya Serikali juu ya Bonde la Wami Ruvu naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, Serikali haioni sasa ni muda sahihi Wizara ya Maji kushirikiana na Wizara ya Mifugo kwenye Jimbo la Kibaha Vijijini kwenye Kata ya Kwala na Dutumi kujenga mabwawa ili kuzuia mifugo isiende kuharibu kingo za Mto Ruvu?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa kuna kazi nzuri imefanywa na Serikali kwenye Bonde la Wami Ruvu la kuunda vikundi na kutambua namna wanavyoweza kutoa huduma kwa wafugaji.

Je, Shughuli hizi ambazo zimefanywa kwenye Bonde la Wami Ruvu Serikali haioni sasa ni muda sahihi kuja kuzifanya kwenye Bonde la Mto Ruvu?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Michael Mwakamo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote Mheshimiwa Mbunge nakupongeza kwa uelewa, hili ni Bonde la Wami Ruvu lakini unahitaji zaidi tujikite kwenye Bonde la Ruvu na huku kote Bodi yetu ya Maji ya Wami Ruvu inafanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na ushirikiano na Wizara ya Kilimo nikutoe hofu sisi ni Serikali tunafanya kazi kwa team work kwa hiyo, tutashirikiana na Wizara ya Kilimo kuhakikisha tunaendelea kujenga maeneo ya kunyweshea mifugo maeneo yale kule yenye wafugaji kwa lengo la kuzuia uharibifu kwenye kingo za huu Mto Ruvu na hili tutalifanya kwa umoja wetu kwa kushirikiana kama Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na Jumuiya za watumia maji upande wa Ruvu. Tutahakikisha viongozi ambao wanasimamia Bonde la Wami Ruvu namna walivyofanya upnde huu wamesikia watafanya. Lengo ni kuhakikisha ushirikishwaji wa pamoja unafanyika kwa pande zote.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini, Bagamoyo, Kibaha Mjini na Kisarawe wamepewa ahadi ya ujenzi wa barabara yao ya lami ya Makofia – Mlandizi – Kisarawe kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi hii inayoendelea.

Je, ni lini itaingia kwenye kusainiwa mikataba kama ilivyofanywa barabara za juzi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii ni muhimu sana kwa maendeleo yetu na hasa inayounganisha barabara ya Bagamoyo na hii barabara ya Morogoro. Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kitu cha kwanza ambacho kitafanyika kwanza ni kulipa fidia kwa wananchi ambao tayari walishaainishwa ili waweze kupisha barabara na tumetenga fedha kwa mwaka ujao kwa ajili ya kuanza hiyo barabara ya Makofia – Mlandizi kwenda Mzenga huko Kisarawe, ahsante. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Mwaka mmoja nyuma Waheshimiwa Wabunge wote tulitakiwa kutoa vipaumbele vya ujenzi wa Vituo vya Afya kwenye majimbo yetu. Mimi Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini ni miongoni na nilipewa Kituo cha Afya cha Kata ya Ruvu, lakini hadi leo hakuna kinachoendelea; je, nini kauli ya Serikali kwenye kuanzisha ujenzi wa kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha wa 2021/2022 Serikali ilijenga vituo vya afya 234 kote nchini, na hii ni commitment kubwa ya Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuhakikisha tunapata vituo vya afya kwenye maeneo yote ya kimkakati hapa nchini ikiwemo kule Kibaha Vijijini alipotaja Mheshimiwa Mwakamo. Tutakaa tuone katika mipango iliyowekwa mwaka 2023/2024 wa fedha, ni kiasi gani kimetengwa kwa ajili ya Kibaha Vijini ili kqenda kujenga kituo cha afya hicho cha kimkakati ambacho amekitaja Mheshimiwa Mwakamo.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa majibu yao. Nitakuwa na swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa majibu yameonesha kanuni zipo na wananchi wanafahamu lakini kule bado kuna changamoto kwenye Jimbo la Kibaha Vijijini, je, Waziri atakuwa yuko tayari baada ya Bunge hili twende tukasaidiane kuwaelekeza kanuni na taratibu za uvunaji wa mazao hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa wazo hili tunatamani sana tuendelee kutoa elimu kwa wananchi ili waweze kufahamu umuhimu wa uhifadhi lakini kuwepo na uvunaji endelevu wa mazao wa misitu. Kwa hiyo natoa ukubali na utayari wa Wizara, tuko tayari kukutana na Wananchi wa Kibaha na maeneo mengine ili kutoa elimu na kuzungumza nao kwa ajili ya kutoa miongozo sahihi, ahsante.
MHE. MICHAEL C. MAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naishukuru Serikali kwa kunipatia majibu kwenye swali hili la msingi, lakini nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa kutokana na uwekezaji mkubwa wa Serikali kwenye maeneo mbalimbali ya nchi hii kujenga Shule za Kata, kunakopelekea watoto wengi kumaliza Kidato cha Nne kwa alama hizo za Daraja la Nne au Sifuri na kwa vyuo hivyo vinavyotajwa na Serikali ni taasisi za Umma ambavyo vimejengwa kwa malengo ya kutoa elimu hizo kwa vijana wetu:-

Je, Serikali haioni sasa ipo haja ya kuwapangia moja kwa moja kwenye vyuo hivyo badala ya wao kuamua wenyewe?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tubebe ushauri wa Mheshimiwa Mbunge, kwa sababu utaratibu huu sasa haupo wa kuwapangia moja kwa moja wale waliopata division four na zero au wale waliofeli darasa la saba. Kwa vile umetoa ushauri huo, acha tuuchukue kama Serikali twende tukaufanyie kazi, tufanye tathmini ya kina kama iwapo jambo hili linawezekana, basi tutaliingiza kwenye mipango yetu kama Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kutokana na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini kwa kuwa Wabunge wote katika swali hili linaonesha ni namna gani wananchi wanakerwa pamoja na kuwa na huo mwongozo.

Je, Serikali haioni ipo haja sasa ya kuwaelekeza Walimu na hizo Bodi wasitumie mwongozo huo kama uchochoro wa kuwapatia wazazi mzigo mzito?(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tumepokea wazo la Mheshimiwa Mbunge na tunatoa maelekezo kuwakumbusha shule zote nchini juu ya utekelezaji wa mwongozo huo. Ahsante sana
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mwaka jana Wabunge wote tulitoa vipaumbele vya vituo vya afya kwenye Kata mbalimbali nchini. Je, ni lini Serikali itatupatia fedha za Kituo cha Afya cha Kata ya Ruvu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mwakamo, amekuwa mchapakazi sana, mwakilishi mzuri wa wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini, tunafahamu kwamba Kata ya Ruvu inahitaji kituo cha afya, kwa sasabu ya idadi ya wananchi waliopo na tayari tumeweka kwenye mpango mkakati kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya katika Kata ya Ruvu kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuwa usafirishaji wa abiria ni jambo la muhimu kwenye nchi yoyote yenye ustaarabu.

Je, Serikali haioni ni muda sahihi sasa wa kuhakikisha wanatengeneza mkakati maalum wa kuzijenga stand kwenye miji inayoendelea ikiwemo Mlandizi ili kuachana na mipango ya mradi wa kimkakati ya Halmashauri isiyotekelezeka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mwakamo kwa ambavyo anawakilisha ipasavyo wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini, lakini Serikali ilishaweka mkakati tayari wa kujenga stand katika maeneo yote ambayo yanahitajika na ndiyo maana tunatekeleza kwa njia ya aina mbili; moja kwa mapato ya ndani ya Halmashauri kwa gharama zile ambazo zinafikika lakini kwa kutumia miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mkakati tayari upo na tunaendelea kuutekeleza, suala ni Halmashauri pia kuhakikisha kwamba wanawasilisha mahitaji hayo Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kutokana na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini kwa kuwa Wabunge wote katika swali hili linaonesha ni namna gani wananchi wanakerwa pamoja na kuwa na huo mwongozo.

Je, Serikali haioni ipo haja sasa ya kuwaelekeza Walimu na hizo Bodi wasitumie mwongozo huo kama uchochoro wa kuwapatia wazazi mzigo mzito?(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumepokea wazo la Mheshimiwa Mbunge na tunatoa maelekezo kuwakumbusha shule zote nchini juu ya utekelezaji wa mwongozo huo. Ahsante sana.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza: Kwa kuwa Muswada huu una muda mrefu takribani miaka 20 sasa na lilikuwa ni tegemeo la wazee wengi kupokea sheria hii: Je, Serikali inaweza ikatueleza vikwazo vilivyosababisha kuichelewesha sheria hii kutungwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa wazee hawa wamelitumikia Taifa hili kwa muda mrefu: Je, Serikali ina mipango gani ya haraka ya kuwahudumia wazee hawa ili waweze kupata huduma zinazostahili kwenye ofisi za Serikali wakati wakiwa wanasubiri sheria hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUMU: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ili Muswada ukamilike na ufikishwe Bungeni kuna taratibu na sheria na miongozo ambayo iliyowekwa na sasa inafanyiwa kazi. Mara baada ya kumalizika Muswada huo, utawasilishwa Bungeni kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inajali sana wazee; na katika Sheria mpya ambayo imetungwa tumeweka kipengele cha ulinzi na usalama kwa wazee. Kwa hiyo, kupitia Bunge lako tukufu naelekeza kwamba taasisi zote za Serikali na binafsi ziweze kuweka utaratibu maalum wa kuwasaidia wazee katika huduma za jamii pale wanapofika sehemu hizo, kwani Serikali inawapenda wazee na wazee ni tunu ya Taifa letu, ahsante. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pale Jimboni Kibaha kwenye Kitongoji cha Disunyala kipo Kituo cha Rasilimali za Kilimo kilichoanza kujengwa tangu mwaka 2007 na mpaka leo hakijakamilika kujengwa. Je, nini mpango wa Serikali kumalizia kituo kile?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge, kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Spika, jambo hili Mheshimiwa Mbunge alishalileta ofisini, tumezungumza na tulimpa ahadi ya kwamba lengo letu ni kuhakikisha kwamba tunakamilisha Vituo vyote vya Rasilimali za Kilimo vipo katika Kata ili mwisho wa siku tuweze kuwafikia wakulima kwa ukaribu. Katika baadhi ya maeneo tumelenga kuvifanya vituo hivi kuwa ni mechanization center ambayo itasaidia wakulima kwenda kukopa au kukodisha vifaa vya kilimo kupitia centers hizo. Kwa hiyo, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba, pale kwake pia tutakamilisha ili mwisho wa siku malengo yaliyokusudiwa yaweze kutimia.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Jimboni Kibaha kwenye Kata ya Kwara na Magindu kuna mabweni mawili-mawili kila shule ya sekondari yaliyojengwa kuanzia mwaka 2018 hadi 2019 ambayo hayajakamilika na mabweni haya yangekamilika yangewasaidia watoto wanaotokea katika Kijiji cha Dutumi na Kijiji cha Lukenge ambao ni umbali wa karibu kilometa kumi kila kimoja.

Je, Serikali ina mpango gani wa kutuongezea fedha ili kukamilisha majengo yale ili watoto wayatumie?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, katika bajeti yetu tumetenga fedha kwa ajili ya kumalizia baadhi ya mabweni ambayo yalijengwa katika EP4R Awamu ya Saba na Awamu ya Nane ambayo yalikuwa katika mwaka 2017/2018 katika bajeti kuu, kuhakikisha tunamalizia ili mabweni yale yaanze kutumika yakiwemo ya jimboni kwake. Ahsante sana.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, Kata ya Magendo, Kibaha Vijijini tumepokea jokofu la kuhifadhia maiti lakini mortuary haijajengwa; je, lini tutapata pesa kwa ajili ujenzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakamo kuwa Serikali ilishatoa maelekezo kwa Halmashauri zetu kote nchini, kwamba Mheshimiwa Rais anapopeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya, lakini anapopeleka fedha kwa ajili ya vifaatiba, kuna baadhi ya miundombinu ambayo iko ndani ya uwezo wa mapato ya ndani ya Halmashauri kama majengo ya mortuary.

Mheshimiwa Spika, natumia fursa hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kumuelekeza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Kibaha, kutenga fedha kwenye mapato ya ndani kujenga jengo la mortuary ambalo ni jengo la gharama ya kawaida kabisa ili wananchi waendelee kupata huduma katika eneo hilo. Ahsante.(Makofi)