Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Muharami Shabani Mkenge (14 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. MUHARAMY S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwako kwa kupata nafasi hii. Napenda pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema hadi kufikia siku ya leo. Napenda pia niwashukuru wananchi wenzangu wa Jimbo la Bagamoyo kwa kunipa heshima kubwa ya kuwa hapa leo. Pia napenda niishukuru familia yangu, ndugu zangu na jamaa zangu kwa kuni-support hadi nimefikia hatua hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja katika Mpango. Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango amewasilisha Mpango wake; kwa kweli kabisa ni mpango mmoja ambao ni mzuri sana, kama jina lake lilivyo Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niguse katika suala zima la kilimo. Katika mpango nataka nijikite zaidi katika kilimo cha umwagiliaji. Serikali katika hotuba yake ya Mpango imezungumza kwamba hekta za umwagiliaji ziko 461,378 na ina mpango wa kuongeza hekta hizo hadi kufikia 694,715.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumze; pale kwetu Bagamoyo tuna kilimo cha umwagiliaji katika Bonde la Mto Ruvu. Kilimo hiki kinawasaidia watu wengi sana. Si Mto Ruvu pekee, tuna Mto Wami ambao una nafasi kubwa sana katika kuisaidia nchi katika kilimo hiki cha umwagiliaji, kwa sababu mwaka 1966 mwezi Oktoba kulifanyika study na kampuni moja ya watu wa Sweden ambayo ilikuwa inafanya kazi ya kufanya utafiti wa mradi wa umeme pamoja na bwawa kubwa sana la umwagiliaji katika Mto Wami ambalo lilitakiwa liwe pale Mandera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali, bwawa hili likitumika katika kilimo cha umwagiliaji maeneo mengi sana ya Bagamoyo pamoja na Mkoa wa Pwani, Kibaha, yanaweza yakapata maji mengi sana kupitia mradi huu kwa sababu ni bwawa ambalo limefanyiwa study na makaratasi yake yapo, nafikiri hata Wizara inalitambua hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nirudi katika suala la wavuvi. Bagamoyo kwetu sisi tunashughulika na uvuvi na kwa bahati nzuri Serikali mwaka huu kupitia jemedari wake, Rais Dkt. John Pombe Magufuli, wameamua kununua meli nane za uvuvi. Nina imani katika meli hizo Bagamoyo inaweza ikapatiwa meli moja; sina shaka na hilo kwa sababu Chuo cha Uvuvi Mbegani ambacho kina wataalam wengi sana wanaojua masuala ya uvuvi tuko nacho pale. Niwashauri ndugu zangu, suala hili la uvuvi tukilishikilia linaweza likatuingizia pesa nyingi sana katika nchi yetu. Kwa sababu mwaka 2015/2016 mauzo yalikuwa dola bilioni 379, mwaka 2019/2020, mauzo yanaonesha yalikuwa dola bilioni 506,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri; pale Bagamoyo pana mradi mmoja wa kufuga jongoo bahari. Hawa jongoo bahari bei yake ni kubwa sana duniani. Hata Waheshimiwa Wabunge mki-google katika hizo tablets zenu sea cucumber, world price market ni shilingi ngapi, mtaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Waziri alitembelea pale tulikwenda sehemu ambako wanafugia yale madude. Kilo moja ya jongoo bahari ni Sh.65,000. Sasa tukielekeza katika miradi kama hii Serikali inaweza ikatupatia pesa nyingi sana na kuhakikisha mipango yetu ya maendeleo itakuwa sawa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana, muda umekwisha Mheshimiwa.

MHE. MUHARAMY S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mengi, lakini naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii. Kwanza kabisa napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri, Katibu Mkuu, kwa kazi nzuri wanayoifanya, japo Wizara ina changamoto nyingi sana. Nami naomba tu niwaambie, wanayozungumza Wabunge hapa, hebu yachukueni kwa makini mkayafanyie kazi, msiyaache yakapita ikawa business as usual.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda zaidi kuzungumzia suala la utalii wa ndani. Utalii wa ndani naona umesuasua sana katika Taifa letu. Kila siku Wizara inapiga kelele, inahamasisha, inapiga debe kuhusu utalii wa ndani, lakini bado utalii wa ndani haujawa sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nitoe ushauri. Sasa hivi duniani biashara huwa inamfuata mteja na siyo mteja anayeifuata biashara. Naomba niishauri Wizara, sasa hivi wabadilishe mfumo wa utalii wao wa ndani. Sasa hivi hakuna Watanzania walio wengi wenye uwezo wa kutembelea Ngorongoro, Manyara na Mikumi; na wana hamu ya kuona wanyama katika hizo mbuga na kutembelea mbuga hizo, lakini uwezo wao ni mdogo. Nawashauri kitu kimoja. Kama mnavyofanya Saba Saba katika maonesho, Banda la Maliasili linatembelewa na watu wengi sana kuliko mabanda yote katika maonesho ya Saba Saba. Hii ni kwa sababu gani? Watu wengi wanapenda kuona wanyama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jaribuni sasa hivi kuweka utalii wa mobile. Mtafute viwanja katika miji kama Dar es Salaam na Dodoma, muweke mabanda ambayo wananchi watakwenda kutembelea wanyama na kulipia pesa. Mtaingiza pesa nyingi za kutosha. Mikoa mingi sana haina mbuga za wanyama na hawawajui wanyama hawa wakoje, kwa hiyo, watu wengi sana wanapenda kuona simba, chui na wanyama mbalimbali, lakini wanakosa fursa za kwenda kuwaona. Sasa ifikie wakati mtengeneze hicho kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, pale Dar es Salaam, Coco Beach au pale kwangu Bagamoyo, kuna beach nzuri na maeneo mazuri. Mkiweka zoo pale ya Wanyama, watu waje kutembelea, watu wengi kutoka Zanzibar; Zanzibar inapokea watalii wengi sana, lakini wanaishia kule, hawana pa kwenda. Wakitoka Zanzibar wanaondoka zao kwenda Kenya. Hebu tuwape fursa watalii wengi wanaokwenda Zanzibar waje Bagamoyo. Nawashauri kitu kimoja, mjenge gati pale, mjenge gati ya kupaki speed boat ambapo mtalii anaweza akatoka Zanzibar akaja mpaka Bagamoyo, akatembelea Mbuga ya Wanyama ya Saadani, akatembelea vivutio vilivyo Bagamoyo na halafu akapanda boti akarudi Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itasaidia sana kuamsha uchumi wa utalii, lakini tukitegemea utalii wetu tuone watu wakitembelea mbuga za wanyama, hiyo itachukua muda mrefu sana na hamtatengeneza pesa. Kwa sababu, watu wengi sasa hivi wanapenda kuona Wanyama; vijana wa shule za msingi, vijana wa sekondari, vijana wa vyuo, wote wanapenda kitu hiki. Kwa hiyo, nawaomba sana, mbadilishe mfumo wa utalii wa ndani, mtengeneze zoo katika miji yetu…

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nishukuru kwa kupata nafasi hii kwa jioni hii ya leo kutoa mchango wangu katika Bajeti hii ya Serikali ya mwaka 2021/2022. Kwanza napenda nitoe pongezi za dhati kabisa zinazotoka ndani ya moyo wangu kwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu, jemedari wetu, Amiri Jeshi Mkuu wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Kwa kipindi kifupi ambacho nipo ndani ya Bunge hili, mama huyu kiongozi wetu ametuheshimisha sana Wabunge kwa kutoa pesa, takribani kwa muda mfupi, shilingi bilioni moja na pointi kadhaa katika majimbo yetu. Tunampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, napenda nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba kwa uwasilishaji wa bajeti yake ambayo haijapata kutokea. Miaka yote kabla sijawa Mbunge nilikuwa nasikiliza bajeti, lakini hii bajeti ambayo niko ndani ya Bunge ni bajeti ya aina yake. Nampongeza Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na ninaamini kuwepo katika timu fulani yenye rangi nzuri nzuri kumesababisha na mambo yake yawe mazuri ndani ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nitoe mchango wangu kwanza katika Sekta ya Uvuvi. Serikali mwaka huu katika mipango yake imeamua kujenga Bandari ya Mbegani ya Uvuvi. Naipongeza sana Serikali kwa jambo hili. Bandari hii ya Uvuvi itakapojengwa italeta manufaa makubwa siyo kwa Wanabagamoyo peke yake, ni kwa Watanzania wote kwa sababu Mbegani miaka mingi inafahamika ni Chuo kikubwa sana cha Uvuvi na wanafunzi wengi kwa miaka ya nyuma walikuwa wanasoma pale katika kile Chuo cha Mbegani. Sasa hivi, kile chuo kiko katika hali ngumu kidogo. Katika ujenzi huu wa bandari ya uvuvi ambayo inatakiwa kujengwa, itaifufua sekta ya uvuvi katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naipongeza Serikali kwa kununua meli nne za uvuvi. Hizi meli pamoja na hii bandari vikienda sambamba, basi katika sekta ya uvuvi, Serikali itakusanya mapato mengi ya kutosha. Wenzetu wako mbali katika suala la uvuvi. Kwa mfano, wenzetu Wakenya wana bandari yao pale inaitwa Liwatoni Fishing Port. Ile bandari imejengwa mpya kabisa; na mwaka huu mpaka Juni 2021, wamesema wanaingiza wanafunzi 1,000 pale kwa ajili ya kujifunza masuala ya uvuvi ili ile bandari iweze kufanya kazi kiaina yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo basi, naiomba Serikali katika bandari hii ambayo inatarajia kujenga pale Mbegani, kwanza waanze kutoa mafunzo kwa vijana ambao watakwenda kufanya uvuvi katika hiyo bandari. Halafu bandari itakapokwisha, kazi moja kwa moja inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili nataka kuzungumzia katika sekta ya utalii. Siku moja nilichangia hapa katika mchango wangu kuhusu utalii wa ndani. Utalii wa ndani una pesa nyingi sana, lakini niliwashauri kitu kimoja, sasa hivi ifikie wakati tuanzishe utalii wa kutembea (mobile), kwa sababu Watanzania wengi sana hawana uwezo wa kwenda katika mbuga za wanyama. Tutashawishiwa sisi Wabunge twende Ngorongoro, twende Manyara na Mikumi lakini mtu wangu pale wa Bagamoyo au sehemu nyingine yoyote hawezi kuwa na kipato leo hii cha kwenda kutembea katika mbuga za wanyama za Mikumi, Ngorongoro au Manyara. Hapo itakuwa ni ngumu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naishauri Serikali, kwa sababu mabanda ya maliasili pale Saba Saba yanatembelewa na watu wengi sana katika kuona wanyama, waende kila mkoa wakafungue hizi zoo ndogo ndogo za kutalii watu. Wajenge mabanda, waweke simba, waweke swala, kila mnyama pale, watu wakienda wanalipa viingilio kwenda kuona wanyama. Wanafunzi, watu mbalimbali wakienda huko pesa itapatikana, tena kwa wingi sana, kuliko tukitegemea utalii wa ndani tuwashawishi watu waende Ngorongoro, Manyara na wapi. Watanzania walio wengi uwezo huo hawana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika suala la biashara. Biashara ndiyo inayoleta kodi na kodi ndiyo inatusaidia katika kuendesha nchi yetu. Hata hivyo, kuna changamoto sana katika biashara na hasa katika sheria hizi za TRA, za Utaifishaji. Sheria za Utaifishaji ni changamoto kubwa sana. Hizi sheria naona kwa upande mmoja au mwingine zinatakiwa sasa zifanyiwe mpango zirekebishwe. Kwa sababu leo hii kwa mfano mtu ana gari yake amenunua, amemkabidhi dereva Fuso au lory, amekwenda kubeba mzigo huko, bahati mbaya huo mzigo ni wa magendo. Inafika gari inakamatwa, inapelekwa katika sehemu labda TRA wanaikamata, wanataifisha mzigo, wanataifisha gari, pengine mwenyewe mwenye gari hahusiki. Hii inatia hasara sana kwa watu na watu wengi wanalalamika mno, kwamba kosa kafanya dereva lakini gari linataifishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu hii sheria tuiangalie vizuri kwa kweli, inaumiza sana watu. Pale jimboni kwangu Bagamoyo kuna kijana mmoja ana Fuso zake mbili; madereva walikwenda wakapakia vitenge vya magendo, magari yakakamatwa, yakataifishwa. Kijana wa watu wamemrudisha nyuma. Alikuwa na Fuso mbili ambazo amezitafuta karibu miaka 20, ameanza tena sifuri. Yaani amechanganyika karibu anakuwa chizi. Jamani haya mambo mengine ya sheria tuyaangalie Mheshimiwa Waziri ili wafanyabiashara wetu waweze kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile hizi sheria za kutaifisha tunazozitunga humu ndani, wawekezaji wa nje wakizisikia hawatakuwa na imani ya nchi yetu. Wataona kwamba Tanzania ukienda kuwekeza, kama wenyewe kwa wenyewe wanataifishana, mimi mgeni nikiwekeza mali yangu itakuwa salama? Kwa hiyo, nafikiri kwamba tubadilike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho kabisa nataka kulizungumzia ni la sensa, sensa ni kitu muhimu sana. Kuna kitu ambacho nataka nimshauri Waziri, nchi zilizoendelea nyinginezo sasa hivi sensa yao, pamoja na kwamba, wanapanga kila baada ya miaka fulani wanafanya sensa, lakini wanafanya sensa ya ndani kwa kutumia watu wao. Na sisi Tanzania tuanze kufanya sensa ili tuwe na projection ya kujua maendeleo yetu yanakuaje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu, leo hii tunangojea kila baada ya miaka 10 au mingapi tufanye sensa, tunao watendaji wa vijiji, tunao watendaji wa kata, tuwatume kazi wapite vijijini kuangalia idadi ya watu wanaozaliwa ili Serikali iwe na projection vinginevyo tutakuwa na ule mpango wa zimamoto, hatujui idadi ya watu, watoto wanaoenda sekondari wanaongezeka, tunajenga madarasa ya zimamoto. Lazima tuwe na mipango thabiti katika hii sensa, tuwatumie viongozi wetu wa vitongoji watuletee taarifa wazipeleke katika kata taarifa za watoto waliozaliwa nchini, wa vitongoji wapeleke kwenye kata, watu wa kata nao wapeleke wilayani, watu wa wilayani wapeleke mkoani. Mkoani wapeleke Taifani tupate mtiririko wa idadi ya watu wanaozaliwa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu, tukitegemea taarifa za hospitali tupu, wengine wanajifungulia majumbani hatupati taarifa zao kwa hiyo, inakuwa kidogo kuna ugumu fulani. Niiombe Serikali hili suala la sensa wasingojee mpaka kipindi, walianze mapema kuangalia projection ya nchi inakwendaje katika uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala ambalo la kilimo, nataka kuzungumzia, kilimo cha umwagiliaji. Hiki kilimo cha umwagiliaji tukikifuatilia na tukikitilia mkazo Taifa litatoka kabisa katika maisha tuliyonayo sasa hivi kwa sababu, umwagiliaji ndio wenye tija. Tukitegemea mvua hizi za kunyesha tu za msimu wakulima wetu wengi sana huwa hawazalishi pale ambapo idadi yao au idadi ya mazao wanayohitaji kufikia lengo, lakini kilimo cha umwagiliaji kitatusababishia tufike katika level nzuri kabisa ya uzalishaji katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kutumia nafasi hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia hoja iliyo mbele yet una nitajikita zaidi kwenye upande wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kutumia nafasi hii, kwa niaba ya wananchi wa Bagamoyo, kukupongeza kwa kuchaguliwa kuwa Spika wetu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia napenda kumpongeza Mwenyekiti wetu, Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu, ambaye anatarajiwa kuwa Naibu Spika saa chache zijazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kwanza nizungumze kuhusu suala la mahusiano yetu ya Tanzania na nchi za nje. Napenda kutoa shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kuikuza diplomasia ya Tanzania nje ya mipaka yetu. Mama Samia anafanya kazi kubwa sana. Kwa kipindi kifupi toka ameingia madarakani amefungua milango mingi ya mahusiano ya kimataifa katika nchi yetu; tunampongeza sana kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama unavyotambua katika Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuna vyombo vingi ambavyo vinahusiana na Kamati hii, lakini nizungumze moja kuhusu suala la NIDA. Wananchi wa Tanzania kwa miaka mingi sana walikuwa wakisumbuka katika kupata vitambulisho vyao vya Taifa, lakini leo hii tunakoelekea baada ya Mheshimiwa Rais, mama Samia Suluhu Hassan kuchagua viongozi wapya katika taasisi hii mwelekeo wa upatikanaji wa vitambulisho vya Taifa unaelekea kuwa mzuri katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, siku zilizopita Serikali ilikuwa ikisumbuka sana na suala hili. Mashine zililetwa, mitambo ililetwa lakini kwa bahati mbaya kazi iliyokuwa ikifanyika haikuridhisha Watanzania wengi; idadi kubwa ya watu wamesajiliwa lakini hawajapata vitambulisho vya Taifa. Leo hii Kamati imejiridhisha kwamba kazi inayokwenda kufanyika kwa ajili ya upatikanaji wa vitambulisho vya Taifa ni kazi ambayo itakuwa yenye kutukuka. Tunawapongeza sana viongozi wa NIDA kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea nayo mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo nataka kulizungumzia hapa ni suala la mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki pamoja na Jumuiya ya SADC. Jumuiya hizi zimekuwa na faida kubwa kwetu sisi Watanzania na hasa baada ya Rais wetu, mama Samia Suluhu Hassan, kufanya ziara katika baadhi ya Nchi za Afrika Mashariki na kugundua fursa mbalimbali ambazo tunafaidika nazo hii leo kutokana na uwepo wa jumuiya hii.

Mheshimiwa Spika, katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ni mambo mengi sana ambayo yanafanyika na hasa fursa zilizopo za kibiashara. Ni wajibu wa Serikali sasa hivi kuhakikisha kwamba fursa zilizopo za kibiashara wanaziweka wazi ili wananchi waweze kuzitambua na kuweza kukimbizana nazo ili waweze kuiletea nchi yetu maendeleo.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kuwa Tanzania tuna matajiri wengi, tuna wafanyabiashara wengi, lakini bado mpaka leo hawajapata taarifa rasmi za fursa zilizopo. Kwa hiyo ni jukumu sasa hivi la Wizara zinazohusika pamoja na Serikali kuzitangaza fursa hizi ili wafanyabiashara wetu waweze kuziendea na kuhakikisha kwamba Taifa letu linapata mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Spika, katika mtangamano wa SADC faida nyingi zinapatikana. Niipongeze Bohari yetu Kuu ya Dawa (MSD) kwa kupata tenda ya kuweza ku-supply dawa katika Nchi za SADC. Hii ni hatua kubwa sana ambayo Tanzania imeifikia. Tuna nchi nyingi za SADC lakini Tanzania imeteuliwa MSD kusambaza dawa pamoja na vifaatiba katika nchi hizo; hiyo ni hatua kubwa sana ya kimaendeleo katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa napenda nipongeze Jeshi letu, Jeshi la Wananchi wa Tanzania. Pamoja na kulinda mipaka, Jeshi lina shughuli nyingi ambazo wanazifanya ili kuiletea maendeleo nchi yetu. Ukiachilia mbali ulindaji wa mipaka, Jeshi linashughulika na shughuli mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze kwa kuendesha Kiwanda cha Nyumbu ambacho kinaendesha teknolojia ya kutengeneza magari. Nafikiri kwa siku zijazo Tanzania itakuwa ni nchi moja wapo ambayo itakuwa inashughulika na mambo mengi sana ya kujitegemea na hasa katika uundwaji wa magari.

Mheshimiwa Spika, pia niwapongeze sana Jeshi letu katika suala zima la kilimo na hasa JKT, wanajihusisha sana katika kilimo na hiki kilimo kwa siku zijazo wataisaidia sana nchi yetu katika usalama wa chakula; niwapongeze sana kwa jambo hili.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwanza kabisa napenda nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya kuhakikisha Tanzania inatoka hatua moja kwenda hatua nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili napenda nimpongeze Waziri wa TAMISEMI ndugu yangu Bashungwa kwa kazi kubwa anayoifanya. Mheshimiwa Bashungwa anafanyakazi kubwa kwa kipindi kifupi tu tunaona ni jinsi gani ambavyo anapambana kufuatilia mambo. Ni juzi tu hapa lilitokea tatizo Mwanza kule aka-act mara moja mambo yakaenda vizuri na sasa hivi kuna barua moja inatembea ya mtandaoni taarifa kwenye vyombo vya habari kwamba kuna Mkurugenzi mmoja ambaye hajatii maelekezo amewekwa pembeni kidogo. Wizara inataka namna hiyo hii Wizara Mheshimiwa Waziri ni Wizara ambayo Wabunge wote tunaitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii itakapokuwa haijafanya vizuri basi sisi sote Wabunge tutakuwa hatujafanya vizuri katika Majimbo yetu, kwa hiyo tukupongeze sana na tutakupa moyo pamoja na kukusaidia ili uweze kufanikisha azma yetu tunayoikusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la elimu. Kwanza niishukuru Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kweli katika Jimbo langu la Bagamoyo kwa kipindi kifupi tu tumepatiwa madarasa yasiyopungua Shilingi Bilioni Moja na Milioni Mia Tatu. Hii ni kazi kubwa sana ambayo ameifanya Mheshimiwa Rais na hii imesababisha vile vile katika kipindi kifupi hiki kupata shule mbili za Sekondari mpya kabisa kuna shule ya Sekondari ya Makurunge ambayo ujenzi unaendelea zimepatikana pesa Milioni 600, kuna shule mpya ya Kata ya Nianjema ambayo ujenzi umekamilika na wanafunzi wanaendelea kusoma, kwa hiyo tunazidi kuipongeza sana Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Mama Samia kwa kazi hii kubwa ambayo wanaifanya. Vilevile kuna shule shikizi ambazo tumepatiwa pesa na shule hizi nazo zishaanza kufanyakazi baadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi katika suala la afya, kuna suala la vifaa tiba. Halmashauri zetu nyingi zina vituo vya afya ambavyo vimejengwa mimi niishukuru Serikali, pale kwangu Bagamyoyo Fukayosi Milioni 500 imepatikana na kituo cha afya kinaendelea kuimarika na kitakamilika muda si mrefu. Lakini tatizo kubwa linalotukabili ni vifaa tiba katika vituo vyetu vya afya hakuna zahanati zetu vile vile hazina vifaa tiba, kwa mfano kituo cha afya cha Matimbwa Yombo hakina vifaa tiba kwa hiyo kinashindwa kufanya kazi vile inavyostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo cha afya cha Kerege nacho kina changamoto ya vifaa tiba zahanati ya Buma, Kilomo, Zahanati ya Tungutungu Mapinga, Zahanati ya Mkenge, Zahanati ya Kidomole zote hizi zinakumbwa na changamoto kubwa ya vifaa tiba kwa hiyo naiomba sana Wizara izidishe juhudi kuhakikisha kwamba, katika mwaka huu wa bajeti vifaa tiba vinapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala la TARURA kazi kubwa TARURA wameifanya pesa tulizopata tumefanya mambo makubwa katika Majimbo yetu na mimi kwa upande wangu wa Bagamoyo barabara nyingi sasa hivi ambazo zilikuwa zina matatizo ya kujaa maji na hasa Bagamoyo mjini, maji sasa hivi hayapo kwa sababu barabara zimejengwa kwa kiwango cha mifereji kiasi kwamba maji yanapita na naomba niishauri tu Wizara sasa hivi katika bajeti ijayo basi, tuhakikishe katika barabara zetu tunaimarisha mifereji. Kwa sababu tunapoimarisha mifereji ndiyo barabara nyingi zinadumu lakini tukisema kwamba tunafanya ukarabati wa barabara maji yakijaa yanajaa udongo unaondoka mwakani tunapeleka pesa tena.

Mheshimiwa Spika, kama hizi Bilioni 802 ambazo mmezienga kwa ajili ya TARURA kwa kipindi cha bajeti ijayo mtazifanyia kazi vizuri na mifereji ya barabara itatengenezwa basi itakuwa jambo la kheri na busara kabisa kabisa kwamba barabara zetu nyingi zitapitika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala la maji RUWASA inajitahidi sana katika suala zima la kusambaza maji vijijini. Mimi kwangu pale Bagamoyo katika Kata ya Fukayose nina mradi wa shilingi milioni 300.000 karibuni na 50,000 lita 75,000 zinajengwa ambazo nina imani wananchi wangu wa vitongoji vya Lusako, Umasaini, Engelo, Mkenge na sehemu zinginezo watapata maji ya kutosha katika kipindi kijacho niipongeze sana Wizara kwa kazi kubwa ambayo mnafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala vilevile la barabara kuna barabara ambazo ni muhimu sana zinakwenda katika mashule pamoja na vituo vya afya na zahanati barabara hizi zipewe kipaumbele katika kuimarishwa kwa sababu wanafunzi wanapata taabu sana wakati wa mvua kwa hiyo katika bajeti hii ijayo Serikali ijitahidi sana kuhakikisha kwamba hizi barabara zinapatiwa kipaumbele na zinaimarishwa, naunga mkono hoja ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii ya kuchangia bajeti kuu ya Serikali. Kwanza kabisa napenda nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuhakikisha kwamba Watanzania tunaishi katika maisha mazuri. Ni ukweli usipingika kwamba katika kipindi chake cha uongozi hakuna hata jimbo moja katika nchi hii ya Tanzania ambalo limekosa mradi mkubwa wa maendfeleo kutoka kwa Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi zangu za pili, naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Dkt. Mwigulu Nchemba pamoja na Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu na wafanyakazi wote wa Wizara ya Fedha kwa kazi kubwa wanayoifanya, na hasa hii ya kutuandalia bajeti, ambayo itakuwa mkombozi kwa wananchi wetu wa hali ya chini katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa vipaumbele vyake vya bajeti ya mwaka 2023/2024. Kwanza kabisa nianzie katika miradi mikubwa ya maendeleo; Bwawa la Mwalimu Nyerere. Bwawa hili litakapo kamilika litakuwa mkombozi mkubwa sana kwa wananchi wa Tanzania na hasa kwa kutupatia umeme wa uhakikia na wenye unafuu. Ni matumaini yangu kabisa, litakapokwisha Bwawa hili, la Mwalimu Nyerere, Watanzania wengi watanufaika na kufaidika na umeme wa bei rahisi kama ilivyoelezwa na viongozi wetu hapo nyuma, kwamba Bwawa la Mwalimu Nyerere litakapokwisha basi hali ya umeme nchini itarudi katika ubora wake na wananchi watapata unafuu wa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nimpongeze pia Mheshimiwa Rais kwa Mradi wa SGR. Mradi huu utakapokamilika utaleta maendeleo makubwa sana katika nchi yetu. Pia nipongeze Wizara ya Fedha kwa kuongeza bajeti katika Wizara ya Kilimo hadi kufikia bilioni 170.8. Haya ni maendeleo makubwa sana ambayo tunakwenda kuyapitia katika nchi yetu. Pia nipongeze Wizara kwa kutenga fedha katika vipaumbele vyake kujenga mabwawa 100 kwa ajili ya shughuli za umwagiliaji. Hii itasaidia sana katika sekta ya kilimo na wananchi wa Tanzania watapata manufaa makubwa kupitia mabwawa haya 100 ambayo yanakusudiwa kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi zangu zingine nizitoe kwa Mheshimiwa Rais na Serikali yake kwa ujumla katika kipaumbele cha Mradi wa SEZ Bagamoyo. Mradi huu ni wa miaka mingi. Tangu wananchi walipofanyiwa tathmini yapata miaka kumi na nne. Lakini sasa Serikali ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan inayoongozwa na Chama cha Mapinduzi pamoja na viongozi wake wameamua sasa mradi huu waupe kipaumbele katika bajeti ya mwaka huu. Hii ni kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wananchi wa maeneo ya Zinga Bagamoyo wanafaidika na wananufaika ili miradi ya maendeleo ya viwanda pale iweze kuanza na wananchi pamoja na nchi nzima iweze kufaidika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuzungumzia suala moja, jana wachangiaji wengi sana walizungumza kuhusu suala la kodi ya ngano, na mimi nataka nilizungumzie kidogo suala hili. Kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mwigulu Nchemba pamoja na Mawaziri wenzie wa Afrika Mashariki kwa kazi kubwa ambayo wameifanya. Wameona ni jinsi gani hizi nchi za Afrika Mashariki zinavyotaabika katika suala zima la chakula. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amezungumza kabisa, mwaka 2019 uchumi katika kwa upande wa mfumuko wa bei ilikuwa 3.5 percent lakini mpaka kufika mwaka 2022, mfumuko wa bei umefikia asilimia 8.7 hii ni hatari sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hii inasababishwa na Vita ya Ukraine pamoja na Ugonjwa wa Covid ambao ulitupitia. Sasa basi naomba kitu kimoja, tuiunge mkono bajeti hii na hasa katika suala zima la kupunguza kodi katika chakula. Mimi nikupongeze Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na Mawaziri wenzio wa Afrika Mashariki kwa hatua mliyochukua. Leo hii kwa mfano suala la ngano, wafanyabiashara wa Tanzania, uzalishaji wao wa ngano ni tani milioni moja na laki moja mpaka tani milioni moja na laki mbili. Uzalishaji wetu katika nchi sidhani kama unazidi tani laki moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukisema kwamba unawapandishia kodi ya ushuru wa forodha asilimia 35, Mama Ntilie wetu, wapika chapati, wapika mandazi hivi watakuwa katika hali gani? Kwa sababu mfanyabiashara utakapompandishia kodi lazima na yeye atapandisha bei ya bidhaa, na atakapo pandisha bei ya bidhaa wanaokuja kuathirika ni wananchi wakawaida. Kwa hiyo nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa hatua hii, hakuna jambo baya ambalo limefanyika, jambo ni kunusuru maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina jambo lingine ambalo nilikuwa nataka kulizungumza. Naomba Mheshimiwa Waziri hili kidogo alitilie mkazo. Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake wametoza bidhaa za viwango vya asilimia 20 kwenye mashine za kamari zinazoagizwa nchini. Mimi kwa maoni yangu hizi mashine za kamari ni janga kubwa sana katika Taifa letu. Pamoja na kwamba tunapata mapato kwa kupitia mashine hizi za kamari lakini kipato tunachopata ni kidogo kuliko athari ambayo wanaipata wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii baba ana shilingi 15,000 yake baada ya kwenda kununua unga wa watoto wakale nyumbani anakwenda kucheza kamari, akifika kule fedha zote analiwa, akirudi nyumbani hana chakula cha watoto, fedha yote kaibwaga katika kamari. Halafu Je, tuna control gani ya hawa wanaochezesha kamari kama hizi fedha wanapeleka benki? Asilimia kubwa wakitoa fedha kwenye mashine zao wanapeleka majumbani mwao kuhifadhi, mzunguko wa mabenki unapungua.

Mheshimiwa Waziri nikuombe sana hili suala mliangalie kwa kina either kama tunahitaji kupata kodi katika hizi mashine za kamari basi tuongeze kodi kubwa sana. Na kama hatupati kodi ya kutosha basi tuziache kwa sababu hazituletei faida, zinaumiza wananchi wetu. Wananchi kwa kweli wamekuwa mateja wamekuwa addicted na hizi kamari, uchumi wao unakuwa mbaya, maisha yao yanakuwa magumu kwa kwa sababu ya kucheza kamari kila siku. Mheshimiwa Waziri mimi naomba sana, kuna vitu vingi vya mapato vya kubuni lakini hiki sio chanzo ambacho ni afya kwa maendeleo ya wanajamii yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala taasisi zinazokopesha. Kuna taasisi ambazo zimezuka mitaani huko zinakopesha watu, hizi taasisi kwa kweli ni janga kwa wananchi wa Tanzania. Kuna taasisi ambazo wananchi wanafikia hatua mpaka wanakimbia majumbani kwao. Leo mwananchi wa kawaida mama wa Bagamoyo ambaye hakusoma unamwambia nitakukopesha kwa asilimia ya 45 riba, hajui maana ya asilimia 45 ni nini, anachukua mkopo baadaye anaambiwa katika laki moja uliyochukua unatakiwa ulipe shilingi 45,000, anashangaa. Yeye anafikiri kaambiwa kwamba alipe shilingi 45,000 ya kuchukua laki moja, sasa hii inaleta changamoto kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi taasisi mmezipa vibali nyingi sana, hazifanyi kazi yenye kutukuka kwa wananchi wetu. Watu wanaacha nyumba zao, wanakimbia kwa sababu ya kukimbia mikopo ambayo inakopeshwa na hizi taasisi. Naomba Wizara ichukue hatua kuhakikisha kwamba kunakuwa na taasisi maalum ambazo zitapewa vibali zenye kukopesha tena kwa masharti ya riba maalum ili wananchi waweze kupata hiyo mikopo na wasiathirike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kazi kubwa anayoifanya, kazi ya kuandaa bajeti sio kazi ya mchezo. Bajeti hii ni bajeti ya mfano wa kuigwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kazi kubwa anayoifanya. Kazi ya kuandaa bajeti sio kazi ya mchezo. Bajeti hii ni bajeti ya mfano wa kuigwa. Bajeti ambayo itakwenda kurejesha uhai wa wananchi wa Tanzania. Nimshauri Mheshimiwa Waziri, maneno yapo mengi, watu wanasema sana, lakini kazi wanayoifanya ni kubwa. Leo hii mmekaa katika hizo nafasi sio kwa nia mbaya ya kuwadhulumu au kuwanyanyasa Watanzania. Lengo na madhumuni yao ni kuwajenga Watanzania. Kwa hiyo, wajitahidi, pale ambapo wataona panafaa, basi wahakikishe kwamba bajeti wameitengeneza vizuri na wananchi wapate faida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hayo machache, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE: MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii. Kwanza kabisa ningependa kuchukua nafasi hii kutoa pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwana Masauni, pamoja na Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu pamoja na timu yote ya Wizara ya Mambo ya Ndani kwa kazi kubwa wanayoifanya. Nawapongeza sana.

Mheshimiwa Spika, mimi kwanza kabisa naomba nizungumzie suala la wahamiaji haramu. Nchi yetu imekumbwa na tatizo kubwa sana la wahamiaji haramu. Mpaka sasa tunavyozungumza kutokana na taarifa ambazo wamezitoa katika hotuba ya Waziri na taarifa ya Kamati, inanesha kuwa kuna wahamiaji haramu wasiopungua 4,025 ndani ya nchi kutoka katika nchi mbalimbali. Wenzetu nchi za jirani hawa wahamiaji haramu wanapokuja katika nchi zao huwa hawakai, wanawaruhusu wanaondoka lakini Tanzania tumejijengea utaratibu kwamba hawa watu wakija tunawapokea, tunawashtaki na tunawaweka katika magereza yetu. Hii inasababisha gharama kubwa sana kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi kama Ethiopia, katika sera yao ya mambo ya nje ni kwamba wanawaruhusu watu wao waende popote kule duniani wanakotaka, hawawakatazi. Kwa hiyo katika nchi nyingi sana wanapita na hawa wahamiaji haramu wa Ethiopia walio wengi hawana dhumuni la kukaa hapa nchini kwetu; nia yao kubwa wao wapite njia. Kwa sababu sisi Tanzania watu wetu wenyewe bado ajira hazijatosha. Kwa hiyo wao hawana nafasi ya kupata ajira katika nchi yetu. Kwa hiyo wanapita njia kuelekea nchi zingine. Kwa hiyo naomba Serikali sasa hivi iangalie ni jinsi ambavyo watawaruhusu hawa watu wapite waende kule wanakotaka badala ya kuwaweka magerezani na kutumia rasilimali zetu za nchi, kwa kuwalisha kwa muda wote ambao wanakuwepo magerezani na kukaa hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwangu pale Bagamoyo mpaka leo hii nina wahamiaji haramu wasiopungua 252 wako pale na wanakula tu siku zinaondoka. Kuna Waethiopia 237, kuna Wasomali 13, kuna Mburundi mmoja na kuna Mkenya mmoja, sasa wote hawa wanakaa wanaitegemea Serikali. Kile tunachokipata kuendesha mambo yetu katika nchi tunaamua kuwahudumia wao. Sasa kwa hiyo niiombe Serikali wafanye haraka iwezekanavyo kuwaondoa hawa watu, wanatutia hasara katika nchi. Kule wenzetu wanapokuwa wanatoka kwao kwa mfano Ethiopia wanawaachia wakifika mpakani wale Maafisa Uhamiaji wakiwa Mashekhe, Mapadri mpaka dua wanawaombea nendeni salama huko mnapokwenda mje kuinufaisha nchi yetu, sisi tunakuja hapa tunawazuia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili nataka kuzungumzia juu ya uzalishaji mali katika Jeshi la Magereza. Jeshi la Magereza linafanya kazi kubwa sana katika uzalishaji mali. Kwa hiyo, niiombe Serikali ili-support sana Jeshi la Magereza na nina imani kabisa kwamba watakapowa-support watu wa Magereza katika suala zima la uzalishaji, Magereza itajitosheleza kwa chakula, Serikali itaondokana na kuhudumia hawa watu. Wao wenyewe wanaweza wakajitosheleza. Wawape vifaa, wawanunulie Matrekta na vifaa vingine vyote. Mashamba wanayo ya kutosha ili waweze kuisaidia nchi katika suala zima la chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala jingine nataka kuzungumza ni suala la vitendea kazi katika Jeshi letu la Polisi. Kumekuwa na lawama kubwa zinazowapata Polisi wetu, Polisi inatokea tukio wanaweza wakachukua dakika 40, hadi dakika 50, lakini gari ileile moja imetoka imeenda katika sehemu nyingineyo. Kwa hiyo magari ni tatizo kubwa sana. Wapatie gari za kutosha ili waweze kuyawahi matukio. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho, suala la hali ya usalama.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa. Ahsante sana.

MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, napenda kushukuru kupata nafasi hii ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwanza kabisa napenda nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaifanya katika kuliongoza Taifa hili la Watanzania.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiofichika, ndani ya kipindi cha miaka miwili ya kiongozi wetu Mama Samia, mambo makubwa sana yamefanyika katika nyanja mbalimbali katika kuendeleza nchi yetu. Mimi binafsi nianzie katika suala la miundombinu.

Mheshimiwa Spika, katika suala la miundombinu Mheshimiwa Rais pamoja na Serikali yake wamejitahidi kwa hatua kubwa sana, nikichukulia kwangu kwa mfano Bagamoyo, ndani ya miaka miwili ya Mama Samia tumepata zaidi ya shilingi bilioni moja katika ujenzi wa barabara zetu, ukiachilia mbali barabara na taa za barabarani sasa hivi zinawaka, kwa hiyo Bagamoyo inawaka na Bagamoyo inang’ara, hizi zote ni juhudi za Mheshimiwa Rais wetu kipenzi Mama Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la nishati. Mheshimiwa Waziri Mkuu katika hotuba yake amezungumzia suala la nishati na amezungumza karibuni sasa hivi asilimia
76.7 ya nishati tuko vizuri lakini bado kuna changamoto nyingi sana katika suala la nishati na hasa katika suala la umeme. Katika suala la umeme bado vijiji vingi pamoja na vitongoji vingi havijapata umeme. Ukienda sehemu mbalimbali bado utakuta nguzo zimewekwa lakini huduma ya umeme bado katika usambazaji wake. Suala la nishati ni muhimu sana katika nchi, wananchi wanapopata umeme ndipo maendeleo yanapopatikana.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo bado tunanishati ya kupikia, nishati ya kupikia bado Tanzania tuna changamoto kubwa sana. Watanzania wengi sana asilimia kubwa wanatumia mkaa, hii inasababisha misitu yetu pamoja na vyanzo vyetu vya maji kuharibiwa kutokana na watu kukata misitu, hii kwa kweli ni changamoto kubwa sana. Hivyo basi, nilikuwa naishauri Serikali katika hili suala la nishati ya kupikia waweke mipango madhubuti kabisa kama walivyofanya ruzuku katika mafuta, watoe ruzuku katika gesi, watoe ruzuku katika vifaa vinavyoshughulika na majiko ya gesi ili Watanzania wengi waweze kupata gesi.

Mheshimiwa Spika, hakuna ubaya wowote kusema kwamba mwezi huu tunatoa ruzuku ya mafuta, mwezi huu tutatoa ruzuku katika gesi ya kupikia na vifaa vya gesi kama majiko pamoja na vifaa vinginevyo ili Watanzania wengi waweze kupata nafuu ya kupika kwa kutumia nishati hii ya gesi ili kuepuka kukata misitu hovyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo napenda sana niipongeze Serikali ya Mama Samia ni suala zima la bandari. Suala la bandari Mheshimiwa Rais amejitahidi sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu jana katika hotuba yake amezungumzia kuna bandari ya nchi kavu ambayo iko maeneo ya Kwala, hii bandari ujenzi wake umefikia asilimia 87 itakapokamilika bandari hii itasaidia sana kukuza uchumi wa nchi. Kuna faida nyingi za bandari ile ikimalizika, hata msongamano wa magari makubwa kutoka Vigwazo kuelekea Dar es Salaam, utapungua kwa kiasi kikubwa sana, kwa hiyo watu wengi watafanya shughuli zao kwa wepesi zaidi.

Mheshimiwa Spika, tuzungumzie sula la Bandari ya Bagamoyo. Nimefarijika sana jana katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kuzungumzia bandari ya Bagamoyo. Kwa kweli sasa imefika wakati hii bandari itakapojengwa uchumi wa Taifa utakua.

Mheshimiwa Spika, kuna changamoto ambazo zinaukabili ujenzi wa bandari ya Bagamoyo. Bandari ya Bagamoyo inajengwa katika Kata ya Zinga sambamba na ujenzi wa bandari, iliunganishwa ujenzi wa bandari fidia zile pamoja na kongani za biashara - EPZA mpaka sasa mwaka wa 13 wananchi wa Kata ya Zinga hawajui nini wafanye kutokana na fidia ambazo hawajalipwa na hivyo wanasikia kuwa ujenzi wa bandari unakuja na wao bado hawajalipwa fidia zao, kwa hiyo ninaiomba Serikali ihakikishe kwamba inafanya juhudi za maksudi kabisa wananchi wa Zinga waweze kupata fidia zao ili kuwe nafuu zaidi katika suala zima la ujenzi huu wa bandari.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la maji, ninaipongeza Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan imefanya kazi kubwa katika miradi ya maji. Mimi kwangu kule Bagamoyo watu wengi karibia asilimia 87 wanapata maji katika Jimbo langu, lakini kuna baadhi ya sehemu zina changamoto kubwa ya maji hasa katika kata mbili, Kata ya Makurunge pamoja na Kata ya Fukayosi, hizi Kata zina changamoto kubwa sana ya maji, inafikia hatua wananchi wanakaa mpaka mwezi mzima maji ya bomba hayatoki, unapowauliza wenzetu wanaoshughulika na masuala ya maji watakwambia kwamba mitambo imekorofisha, umeme mdogo. Kwa hiyo, ninaiomba Serikali ijitahidi kabisa kuhakikisha kwamba suala la upatikanaji wa maji katika hizi Kata na maeneo yote ambayo hayana maji katika nchi hii yanakuwa sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nirudi sasa katika suala la kilimo, ninaipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Mama Samia katika suala zima la kilimo. Ule mpango wa Serikali kuandaa vijana ili waende sasa wakalime ni jambo la msingi sana, lakini naomba kadri siku zinavyokwenda waongeze idadi ya vijana katika suala zima la kilimo. Kwa sababu tumeangalia takwimu ambazo zimechukuliwa mwaka huu, kila Wilaya imepata vijana Wanne. Hivi kweli kila Wilaya ikipata vijana Wanne kutakuwa na maendeleo gani katika suala la kilimo? At least tuongeze wigo sasa kuhakikisha kwamba vijana wengi wanachukuliwa kutoka katika Wilaya zetu kwenda kushiriki katika mafunzo waweze kupata tija katika hayo mafunzo ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache ninashukuru sana, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda nishukuru kwa kupata nafasi hii ya mwanzo kuchangia Wizara hii ya Viwanda na Biashara. Kwanza kabisa, napenda nitoe shukrani zangu kwa Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, pili, napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara pamoja na wasaidizi wake wote kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kuimarisha Wizara hii ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Spika, pia napenda kutoa pongezi zangu kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuleta uwekezaji hapa nchini. Kwa kweli Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa sana, wawekezaji katika nchi hii sasa hivi wanakuja kwa wingi sana, na nina imani kabisa Tanzania itakwenda mbele zaidi kibiashara pamoja na Sekta ya Viwanda.

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumzie suala moja kuhusu ushindani wa kibiashara. Katika suala hili, kidogo bado kuna changamoto, na hasa katika suala la biashara ya mafuta ya kula. Pale kwangu Bagamoyo, pamoja na shughuli nyingine za watu wa Bagamoyo, biashara kubwa sana pale inayofanyika kupitia Bandari yetu ya Bagamoyo ni ni biashara ya mafuta. Wafanyabiashara wengi wa Bagamoyo wanatoa mafuta kutoka Zanzibar, wanayaleta Bagamoyo na hatimaye kwenda kuyauza katika sehemu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, wafanyabiashara hawa wanapata changamoto kubwa sana ya ushindani. Wanalalamika kwamba wenye viwanda, Serikali katika bajeti iliyopita wamewapatia zero percent ya import duty, lakini hii zero percent wafanyabiashara wanatakiwa walete mafuta ghafi (crude oil). Inavyosemekana ni kwamba wafanyabiashara hawa hawaleti mafuta ghafi, wanaleta mafuta yaliyosafishwa ambayo ni refined oil na kwenda kuya-park katika viwanda vyao, na hivyo kwenda kuyauza. Hili linajidhihirisha wazi kwamba mpaka sasa bei ya mafuta pamoja kwamba Serikali imeshusha, wanafanyiwa zero percent, lakini bado bei ya mafuta iko juu, pamoja na kwamba Serikali imewapunguzia kodi hawa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfanyabiashara wa kawaida anachajiwa asilimia 25 ya kodi, lakini mfanyabiashara mkubwa anawekewa zero. Sasa hii kweli tutaleta ushindani wa kibiashara na tunaweza kuwakuza kweli wafanyabiashara wetu katika nchi hii?

Mheshimiwa Spika, leo hii mtu wa Bagamoyo anachukua dumu la mafuta kutoka Zanzibar, likifika Bagamoyo pale linachajiwa shilingi 33,000 kodi, ukijumlisha bei ya manunuzi aliyonunulia kule, na gharama nyinginezo za TBS, mionzi, sijui nini, dumu hili linafikia mpaka shilingi 75,000 au shilingi 78,000 mpaka shilingi 80,000. Hivi huyu mtu anafanya biashara gani?

Mheshimiwa Spika, ile bandari kipindi cha nyuma tulikuwa tunafanya biashara, TRA walikuwa wakipata mapato makubwa sana. Ilifikia wakati tunatengeneza mpaka Shilingi bilioni mbili na zaidi kwa mwezi kwa kupitia Bandari ya Bagamoyo na wafanyabiashara wa Bagamoyo, lakini leo hali ni tofauti. Namwomba Mheshimiwa Waziri, katika ushindani wa biashara azungumze na Wizara ya Fedha, hizi kodi ambazo wanawapunguzia wafanyabiashara wakubwa katika mafuta ya kula, zinawapa changamoto wafanyabiashara wadogo, wanashindwa kuendelea, hawafiki mbali kibiashara.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo nataka kuzungumza ni suala la SEZ (Special Economic Zone) Bagamoyo. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri kipengele cha 195 ameelezea vipaumbele vya bajeti ya mwaka 2023/2024 katika maeneo maalum ya uwekezaji. Nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri hili. Nimeona Bagamoyo katika mipango yako ya vipaumbele umeiweka katika kipaumbele. Nashukuru sana kwa niaba ya wananchi wa Bagamoyo kuwajali katika hili.

Mheshimiwa Spika, vilevile katika malengo ya Wizara kwa mwaka 2023/2024 sehemu ya 196 Mheshimiwa Waziri amezungumzia uendelezaji wa miradi ya Kitaifa ya kielelezo, (National Flagship Projects). Kwa kweli kwa hili wananchi wa Bagamoyo wanampongeza sana Mheshimiwa Waziri na wanamshukuru sana, amewatendea jambo la haki sana.

Mheshimiwa Spika, haitoshi, katika kipengele hicho hicho Mheshimiwa Waziri amezungumzia suala la fidia kwa watu wanaopitiwa na huu mradi wa SEZ. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri, kwa kweli amefanya kazi kubwa sana, wananchi wa Bagamoyo Kata ya Zinga, maeneo ya Mlingotini, Pande na maeneo mengineyo ya Kondo walikuwa wanalalamika sana kuhusu hili jambo, na kwa bahati nzuri Mheshimiwa Waziri ameituma timu kule inayoongozwa na Dkt. Mchome wa Chuo Kikuu cha Ardhi Dar es Salaam, wanafanya kazi nzuri, nami nimezungumza nao, wanaendelea na kazi nzuri kabisa ili kuweza kuliweka jambo hili sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, itakapofikia kipindi, wananchi wa Bagamoyo wamelipwa katika hili jambo kwa kweli watampongeza sana Mheshimiwa Waziri na watamwombea sana kwa Mwenyezi Mungu. Maana ni mwaka wa 13 sasa hivi, wananchi wa Bagamoyo wa sehemu hizo bado hawajapata malipo yao. Kwa bajeti ya mwaka huu, kwa kulizungumzia hili la fidia ya wananchi hawa, kwa kweli sina budi kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri katika jambo hili.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala ushindani wa biashara, naomba Mheshimiwa Waziri wa hii Wizara na Waziri wa Fedha waangalie jinsi gani ya hizi kodi zitashuka ili wafanyabiashara nao wapate kufanya biashara zao na kupata faida. Bagamoyo inaendeshwa na bandari, wafanyabiashara wengi wanaendeshwa na bandari ya ile, mama ntilie wanafanya kazi kupitia ile bandari, wabebaji mizigo wanafanya kazi kupitia ile bandari, lakini suala la mafuta ya kula, itakapokuwa kodi kubwa, wafanyabiashara wa Bagamoyo hawatapata fursa ya kuendesha maisha yao.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kupata nafasi hii leo ya kuchangia Hotuba ya Wizara hii ya Maji. Kwanza kabisa ningependa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uzima wa kuwa hapa siku ya leo na pili ningependa kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya na hasa katika sekta hii ya maji.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais, ana azma kubwa ya kumtua ndoo mama kichwani, katika kuhakikisha kwamba Tanzania inakuwa na miradi mingi ya maji. Lakini Mheshimiwa Rais si kumtua ndoo mama kichwani peke yake hata sisi wababa wanatutua mizigo ya mawazo vichwani kwa sababu wake zetu walikuwa wanatumia muda mwingi sana kwenda kufuatilia maji ambayo shughuli nyingine zenye maendeleo nyumbani zilikuwa zinasinyaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri ndugu yangu Mheshimiwa Jumaa Aweso kwa kazi kubwa anayoifanya. Mheshimiwa Aweso pamoja na Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Viongozi wengine wa wizara hiyo wanaitendea haki wizara yao kwa kuhakikisha kwamba miradi ya maji inafanikiwa katika nchi nchi hii.

Mheshimiwa Spika, waswahili wanasema mnyonge mnyongeni haki yake mpeni lakini Mheshimiwa Aweso hatonyongwa atapewa haki yake akiwa mzima na bajeti yake leo itapitishwa hapa ili aweze kwenda kutuhudumia watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia napenda niwapongeze wenzangu katika Jimbo la Bagamoyo na hasa viongozi, ma– engineer wanaotoa huduma katika maji ningependa nichukue nafasi hii kumpongeza engineer James Kionaomela ambaye yeye huwa mara nyingi sana anatupatia taarifa au Mbunge wake ananipatia taarifa katika miradi ya maji ambayo inayoendelea katika Jimbo la Bagamoyo. Pia ningependa kumpongeza manager wa DAWASA wa Mapinga ndugu yangu Abrahamu Mwenyemaki ambaye naye pia amekuwa msaada mkubwa kwangu kunipatia taarifa mbalimbali kuhusu masuala ya maji katika Jimbo langu la Bagamoyo.

Mheshimiwa Spika, tarehe 16 Machi, 2023 Mheshimiwa Waziri Mkuu alizindua mradi kubwa kabisa wa uhifadhi wa maji, alizindua tenki la maji la lita milioni tano pale maeneo ya Kibaha. Mradi huo wa maji umesaidia sana au unaendelea kusaidia sana Mikoa ya Dar es salaam na Pwani. Kwa sababu mradi huu utahudumia watu zaidi ya 37,000 katika Miji wa Dar es Salaam na Mji wa Bagamoyo.

Mheshimiwa Spika, ningependa kabisa nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwamba mradi huo wa maji ambao uko pale uliyozinduliwa wa lita milioni tano unasaidia katika kata zangu za Mapinga na hasa katika vitongoji vya Kibosha pamoja na Kimele, na vilevile unasaidia katika Kata ya Kerege katika vitongoji vya Kitanga, pamoja na Nyakahamba kwa kweli juhudi kubwa imefanyika na Serikali katika kuifanya hili zaidi ya dola milioni 86 zimetumika katika mradi huu.

Mheshimiwa Spika, kuna mradi mwingine wa upanuzi wa mradi wa maji wa Kidomole ambao umetumia shilingi milioni 334, zaidi ya milioni 334 mradi huu kwa kwakweli utakuwa mkombozi mkubwa sana kwa wananchi wangu wa kata ya Fukayosi hasa maeneo ya Kidomole katika Vitongoji vya Relini, kitongoji cha Mwanasenga, kitongoji cha Kinyamvuu pamoja na kitongoji cha Vihagata. Huu mradi utakapokamilika wananchi hawa nafikiri wataishukuru sana Serikali kwa kiwango kikubwa sana, kwa sababu miaka mingi sana hawana maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kuna mradi wa shilingi milioni 583 wa kupeleka maji katika Kijiji cha Kitame. Mradi huu wa maji wa milioni 385 unaendeshwa na mkandarasi mmoja anaitwa Amkami Mheshimiwa Waziri. Naomba nikwambie mradi huu ushafikia asilimia 35 lakini mpaka leo mkandarasi bado hajalipwa, ametumia pesa zake mwenyewe kwa uzalendo wake. Kwa hiyo, tunaomba muongeze juhudi katika kuwalipa wakandarasi ili miradi hii ya maji iweze kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna mradi mwingine wa maji ambao unaitwa Mradi wa SE Kitongoji cha Segwa pamoja na Magofi wa milioni 155. Mradi huu unaendelea vizuri na wananchi muda si mrefu wata-enjoy kupata maji.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Makurunge na Kata ya Fukayosi bado tuna changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa maji. Watu wa Fukayosi na Makurunge wanapata maji kutoka katika Mradi wa Wami, lakini sijui mpaka sasa hivi Mheshimiwa Waziri nini kinaendelea? Watu wa Makurunge, watu wa Fukayosi wanakaa mpaka miezi mitatu bila ya kupata maji.

Mheshimiwa Spika juzijuzi hapa watu walinipia simu ilifikia hatua mpaka walimu wakataka kufunga Shule Msingi pale Mkenge kwa sababu wanafunzi hawana maji ya kutumia. Nikamuomba Meneja wa DAWASA wa Chalinze Fumbuka ilibidi atume doza la kupeleka maji pale shuleni wananchi ili waweze kunusurika. Kwa kweli Waheshimiwa Waziri hali ya pale mbaya sana.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri nimeona katika hotuba yako nimeona pesa ambazo umezitenga kwa kipindi cha bajeti ya Mwaka 2023/2024 kuna miradi ambayo nitanufaika nayo. Mradi wa Kifuda Razaba, Mradi wa Wami Fukayosi, Makurunge, Mkenge Fukayosi, Kalimeni yote imeingizwa katika programu ya kupatiwa pesa kwa kipindi hiki kijacho hili miradi hii iweze kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala moja ambalo nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri. Suala la Misamaha ya Kodi kwa Vyombo au Vifaa vya Miradi ya Maji. Mheshimiwa Waziri hakuna kitu kinachokuchelewesha sana katika miradi yako kama jambo hili hebu jaribu kufanya kila njia utakayoiweza. Kaa na mamlaka zinazohusika pale wakandarasi ambapo wameishapata tender kuhakikisha wanapatiwa hii misamaha ya kodi haraka iwezekanavyo ili miradi iweze kuendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu leo hii utakuta mkataba wa mradi unasainiwa lakini bado mradi unaweza ukakaa zaidi ya miezi minne, mitano mpaka sita au mwaka mmoja ukiulizwa mradi huu kwanini hauendelei utaambiwa kwamba bado hatujapata msamaha wa kodi. Kwa hiyo, niombe Wizara yako nikuombe Mheshimiwa Waziri, uwe karibu na viongozi hawa ambao wanatoa hii misamaha ya kodi kwa ajili ya hii miradi ya maji kukufanyia haraka na wepesi zaidi ili…

SPIKA: Mheshimiwa, Kengele imeishagonga.

MHE. MUHARAMI S. MKENGE: …ili uweze kuhakikisha kwamba Miradi hii inafanyika kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache nashukuru sana, Ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kukushukuru kwa kupata nafasi hii. Kwanza kabisa ningependa nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anafanya kwa bajeti hii ya kihistoria ambayo ameipatia Wizara hii ya Kilimo, Pili napenda kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na crew nzima ya Wizara ya Kilimo kwa kazi kubwa wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita katika masuala makubwa matatu. Suala la kwanza ni suala la motisha kwa Maafisa Ugani. Wiki chache zilizopita umefanya jambo kubwa sana kugawa pikipiki 7,000 kwa Maafisa Ugani, haijapata kutokea toka Wizara ya Kilimo imeanza. Hili ni jambo la kutia moja kwa maafisa wetu wa ugani ambao wanafanya kazi kubwa kabisa katika kuinusuru sekta hii ya kilimo nchini. Vilevile nilikusikia ulimuomba Mheshimiwa Rais kwamba pikipiki zile wakizitumia kwa muda wa miaka miwili basi wazichukue ziwe mali yao, hili ni jambo kubwa sana na jambo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakuomba isiishie hapo tu hawa Maafisa Ugani sasa hivi wanatakiwa wapangiwe utaratibu kwa mazao yote ya kimkakati katika Mikoa, wanatakiwa sasa hivi waambiwe kabisa kwa mfano, ile sehemu ambayo wanatakiwa walime alizeti wapewe kiwango au target kwamba tunataka Mkoa fulani mzalishe tani fulani na mtakapozalisha tani fulani za alizeti basi mtapata percent fulani itakuwa mali yenu, ninakuakikishia hao watafanyakazi usiku kucha hawatalala kwa sababu ya kufukuzia hizo percent ambazo utawapatia na mambo yatakuwa mazuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni kuhusu umwangiliaji, nimeona bajeti kubwa sana ya umwangiliaji imeongezeka kutoka Bilioni 46.5 mpaka Bilioni 361.5 haya ni mageuzi makubwa sana. Lakini kuna sehemu ambazo umezisahau katika miradi ya umwagiliaji, kwa mfano pale kwangu Bangamoyo kuna skimu ya umwangiliaji ya Ruvu maarufu kama JICA haimo kabisa katika mpango wako, siyo tu Bangamoyo nimesoma almost hotuba yako yote, Mkoa wote karibu skimu niliopata ni moja tu ambayo iko Rufiji inaitwa Ngongoro ambayo iko katika upembuzi yakinifu, lakini katika skimu za umwangiliaji zilizofanyiwa upembuzi yakinifu hakuna, skimu za umwangiliaji za Mwaka wa Fedha 2022/2023 hakuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama unavyotambua Bangamoyo kuna mradi mkubwa sana, sasa hivi tunawaandaa outgrowers kwa ajili ya kilimo cha miwa ili waweze kulisha shamba la Bagamoyo Sugar lakini hakuna utaratibu wowote na wala hakuna mpango wowote wa kujenga bwawa au kuweka miundombinu ya umwangiliaji kwa ajili ya kunusuru wakulima hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala langu la mwisho ni la uboreshaji wa masoko, tutakuwa tunasema kilimo tunapanga mipango ya kulima kwa bidii zote lakini tusipokuwa na masoko kwa bidhaa zetu tunazolima tutakuwa tunajisumbua. Lazima tuwekeze nguvu zetu sasa hivi kuhakikisha kwamba tunapata masoko kwamba wananchi wanapohamasishwa kulima wanalima lakini baadaye inakuja wamelima kwa nguvu zote, masoko hakuna wanarudi nyuma, mwaka unaofuata hawalimi tena Taifa linakuwa kila siku linapiga mark time tu haliendi, kwa hiyo tuelekeze nguvu zetu katika Maafisa wa Masoko.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata ikiwezekana hawa Maafisa wa Masoko waambieni kabisa mtu atakayetutafutia soko la bidhaa fulani nchi fulani tutampa kamisheni kutokana na mauzo yatakayofanyika ya yale mazao ambayo yataunzwa katika nchi husika. Kwa hiyo hapa kutakuwa na jitihada kubwa sana ambayo inafanyika watajitahidi, vilevile tusisite tuongee na Wizara ya Mambo ya nchi za Nje, tuwatumie diaspora kule watutafutie masoko ya bidhaa zetu kwa sababu tunalima. Tumeona miaka miwili iliyopita anguko la mbazi, mbaazi ilikuwa bei yake kubwa sana, mimi niliwahi kulima mbaazi, niliuza kilo Shilingi 2,300 shamba kipindi cha nyuma, lakini baadaye mbaazi ikashuka ikawa inauzwa mpaka Shilingi 300 kwa kilo na wanunuzi hakuna. Sasa lazima tujipange kuhakikisha kwamba masoko yanafanyiwa kazi na hawa Maafisa Masoko waandaliwe ili waweze kuinusuru Wizara na kulinusuru Taifa ili liweze kufanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kushukuru sana kwa kupata nafasi ya kwanza katika uchangiaji wa leo. Kwanza kabisa napenda nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kupata tuzo ambayo imeiheshimisha nchi yetu kimataifa. (Makofi)

Pili napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mama yetu Mabula, Naibu wake Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, Katibu Mkuu na iongozi wote wa Wizara, kwa kweli kazi kubwa wanaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi mchango wangu nianzie katika suala la muster plan, sasa hivi nchi inajitahidi sana na hasa Wizara kuhakikisha kwamba master plan zinakaa vyema katika nchi yetu, lakini mimi ningependa tu niwashauri Wizara hii master plan wasiziachie Halmashauri zetu, waibebe moja kwa moja Wizara ndio washughulike nayo, kwa sababu Halmashauri zetu fedha zenyewe ni za kuokoteza na zina mambo mengi kwa hiyo miradi ya master plan katika Halmashauri tukiiachia miradi hii itachelewa sana kufanyika kwa sababu uwezo wetu ni mdogo wa kukusanya fedha katika Halmashauri ili tuweze kumudu gharama za master plan.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Wizara inatakiwa kwamba itoe fedha zote kuhakikisha kwamba master plan zinakuwa katika miliki yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nilikuwa nataka kuzungumzia ni suala la Serikali kuchukua ardhi za watu bila fidia. Imekuwa ni tatizo sugu sasa Serikali kuchukua ardhi pasipo kulipa fidia, mfano mmoja ni kule kwangu Bagamoyo EPZA wamechukua ardhi wa wananchi wa Zinga kwa miaka sasa 13 watu bado hawajalipwa fidia, lakini EPZA ipo chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, lakini katika hili dhambi zote na lawama zote zinawaangukia Wizara ya Ardhi kama vile wao ndio wahusika wakuu, lakini wao kazi yao ni kupima tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niwaomba Wizara ya Ardhi mjaribu sasa hivi kuangalia kwamba mtakapowapimia…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge wa Bagamoyo kwamba mchango wake mzuri sio tu eneo la Bagamoyo, EPZA kwenye kanda zote kumi ambazo wamechukua wameendeleza Kanda tatu tu, na hawajalipa maeneo mengi zaidi ya miaka kumi ikiwepo na Kata ya Guta, Bunda Mjini, ahsante.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Muharami, taarifa?

MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea taarifa, kwakweli hali inahuzunisha na inasikitisha ukienda kwa wakazi wangu wa Mlingotini wakazi wa Zinga, wakazi wa Pande, wakazi wa Kondo, wana malalamiko makubwa sana kuhusu EPZA miaka 13 sasa bado hawajalipwa na unakuta unakwenda kuongea na wazee mtu unamkuta mzee ana umri wa miaka 70 analia anatoa machozi, haki yake hajapewa bado eneo limezuiwa hawezi kuuza, akienda ardhi anaambiwa eneo hili limeshawekwa GN ni mali ya Serikali hauwezi kufanya chochote. Sasa hii kwa kweli mimi naomba sana Serikali iliangalie upya Wizara ya Ardhi msiwapimie EPZA wala TIC, wahakikishe kwamba fedha ipo ubaoni ya kulipa wananchi ndio muwapimie, vinginevyo mtabeba lawala ninyi wakati nyinyi mnafanya kazi yetu kwa uzuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ni suala la migogoro ya ardhi; migogoro ya ardhi bado ni mingi kiasi kwamba inaanza kupungua Wizara inajitahidi sana, nimpongeze sana Waziri aliyepita Mheshimiwa Lukuvi kazi kubwa aliifanya alikuja kwangu tarehe 19 Julai, 2021 kwa kweli tulifanya mikutano kama miwili mikubwa sana na wananchi na aliwatia msukosuko baadhi ya watu kiasi kwamba kidogo mambo sasa hivi yanaanza kutulia, kwa kweli wanajitahidi sana Wizara katika kuhakikisha kutatua migogoro ya ardhi bado ni mingi, halafu wajitahidi kuzielekeza na kuzishawishi Mahakama za Ardhi kuhakikisha kwamba wanafanya kazi zake kwa uharaka zaidi maana yake masuala ya ardhi yanapokuwa mahakamani yanachukua muda mrefu, yanachukua miaka mingi kiasi kwamba haki za watu zinakuwa zinapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ninataka kuzungumzia suala la wananchi wangu la Lazaba Makurunge, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri umekwenda kule, umezungumza na watu wa Batini, lakini Lazaba inatatizo kubwa, wananchi wengi la Lazaba walikuwa wakiishi katika ardhi ya Serikali ambayo mwaka 2016 Mheshimiwa Rais Hayati Magufuli alimkabidhi mwekezaji Bagamoyo Sugar ambaye ni Bakharesa hekta 10,000 ambazo zilikuwa zikiishi watu ndani yake. Baada ya kukabidhi fidia zikafanyika, lakini wananchi wale hadi sasa bado wana tangatanga hawana pa kukaa, wanakaa katika eneo la Serikali bado na hadi sasa hawajielewi wanakwenda wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lile la Lazaba lilikuwa na hekta 28,000 hekta 10,000 amepewa mwekezaji, hekta 6,000 ni mali ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na hekta 12,000 bado zimebaki mali ya Serikali. Kwa hiyo niiombe Wizara iwafikirie wale watu japo kuwapa hekta 1,000 tu waweke makazi kwa sababu hadi sasa yule mwekezaji bado anapata changamoto ya kupata rasilimaliwatu, anaenda kufuata rasilimaliwatu kilometa 25 wakati pale wangepewa makazi watu ambao jirani na mwekezaji watu wangeweza kuishi na wakafanya kazi katika kiwanda ambacho kinajengwa na mashamba ya miwa wakapata riziki zao.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa, muda wako umekwisha. (Makofi)

MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, napenda kushukuru kwa kupata nafasi hii niweze kuchangi machache katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda nimpongeze ndugu yangu Waziri Mchengerwa kwa kazi kubwa anayoifanya, na Naibu Waziri dada yangu Pauline Gekul, Katibu Mkuu, Dkt. Abbas, Naibu Katibu Mkuu, Bwana Saidi Yakubu na timu yote ya Wizara na pia sitamsahau Mkuu wa Chuo changu cha Bagamoyo TaSUBa kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pongezi za pili ziende kwa mama yetu, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa aliyoifanya ya Royal Tour. Jambo la Royal Tour Mheshimiwa Rais amelianzia pale Bagamoyo na jambo lolote likianza Bagamoyo basi mambo yake yatakuwa mazuri kabisa na mnaona kabisa idadi ya utalii imeongezeka sana katika nchi yetu. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nazungumzia suala la Taasisi ya Sanaa na Utamaduni Bagamoyo au Chuo cha Sanaa Bagamoyo. Chuo hiki cha siku nyingi sana lakini kazi kubwa sana chuo hiki imekifanya na viongozi waliyoko pale wanaendelea kudumisha na kuhakikisha kwamba kazi kubwa iliyokuwa inafanyika inaendelea kuwa nzuri. Mwaka 2021 kulikuwa na Tamasha la Sanaa Bagamoyo tarehe 28 mpaka 30 Oktoba, lilifanyika mwaka jana. Tamasha hili kwa kweli lilikusanya watu wengi sana; wa ndani na wa nje ya nchi, makadirio ya Wizara wanasema kama watu 75,000 lakini mimi ninasema zaidi ya 100,000; yalikuwa makadirio madogo sana. Kwa kweli chuo hiki kinafanya kazi kubwa na chuo hiki kinaitangaza nchi yetu, kwa mfano mwaka 2021 Chuo cha Sanaa Bagamayo wamechukua Uni Award ya mwaka 2020/2021 wameingia nusu fainali. Mwaka huo huo 2021 katika Uni Talent katika suala la kuimba wameingia fainali, katika Taifa Cup, katika masuala ya bongo fleva wameshika nafasi ya kwanza, katika Uni Talens ya 2022 katika suala la kuimba wameshika nafasi ya kwanza na vilevile wameiwakilisha nchi katika suala zima la kuhamasisha Royal Tour kule Marekani, wamefanya maonesho kadhaa.

Mheshimiwa Spika, ninachotaka kusema Mheshimiwa Waziri hiki chuo kinatakiwa kiangaliwe kwa jicho la tatu, siyo macho mawili; maana yake ni chuo ambacho kinafanya kazi kubwa sana. Nimeona katika bajeti ya mwaka huu 2022/2023 chuo kimetengewa shilingi milioni 550 kwa ajili ya kununua vifaa vya kufundishia na kufundisha, kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu, mabweni, ukumbi, jengo la maji safi, maji taka, kununua vifaa vya uzio, kununua vifaa vya tv, kununua vifaa vya redio na kuweka mtambo wa redio pale. Kwa hiyo hivi vitu naomba Mheshimiwa Waziri, kama mmedhamiria kuvifanya mvifanye kweli kweli kwa sababu hiki chuo kinatembelewa na watu wengi na hiki chuo kimefundisha wageni wengi sana.

Mheshimiwa Spika, miaka iliyopita mpaka wazungu walikuwa wanacheza ngoma pale, wengi kabisa, kabisa, wanakuja wanajifunza. Mimi hiki chuo natamani kukiita Chuo cha Kimataifa cha Sanaa Bagamoyo kwa sababu ni chuo ambacho kinatambulika dunia nzima na kazi kubwa inafanyika na waliopo pale viongozi wangu wanafanya kazi kubwa sana. Naomba Mheshimiwa Waziri hebu jaribu sana kuongeza bajeti hii ya hiki chuo ili kiweze kuwa bora kiweze kushindana kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nataka kuzungumzia, Mheshimiwa Waziri siku moja ulinidodosea na tulizungumzia kuhusu sports arena na ukanihakikishia siku moja ungeweza kufanya mpango tukapata sports arena pale Bagamoyo. Kwa sababu kuna Chuo cha Sanaa pale, kuna utalii Bagamoyo, ni jambo la msingi lile wazo lako kwa sababu sijaliona katika bajeti yetu ya mwaka huu. Naomba liwepo Bagamoyo ipatiwe sports arena kwa sababu ni sehemu ambayo ina utalii wa hali ya juu sana ukichukia na Chuo cha Sanaa cha Bagamoyo pale cha Utamaduni, ukichukua na vivutio vya kitalii basi mkiweka sports arena pale mambo yatakuwa mazuri kabisa.

Mheshimiwa Spika, niipende sana kuipongeza timu yetu au timu zetu za Serengeti, timu za wanawake kwa kazi kubwa wanayoifanya, nizipongeze timu zote za mpira wa miguu Tanzania, niipongeze klabu ya Yanga kwa hatua nzuri ambayo wanaendelea nayo, wanafanya kazi kubwa. Na nawaomba wakaze msuli kwamba baada ya kuchukua kombe mwaka huu lisitoke ndani ya miaka nane mpaka tisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa napenda nitoe shukrani zangu za dhati kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya. Bajeti ya mwaka 2021 Wabunge wengi sana alituvisha nguo katika Majimbo yetu. Miradi mingi ya maendeleo imefanyika na hilo halina ubishi kabisa, kila Mbunge aliyekuwa hapa katika Jimbo lake, basi kuna kikubwa ambacho amekipata kutokana na bajeti ya mwaka uliopita. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, napenda kumpongeza na kumshukuru Waziri wa Fedha kwa kazi kubwa anayoifanya na pia napenda kumpongeza Naibu wake Bwana Hassan Chande, Katibu Mkuu pamoja na viongozi wote wa Wizara, wamejitahidi sana. Bajeti ya mwaka huu ni bajeti ya mfano ambayo inakwenda kuwaweka Watanzania katika hali nzuri ya maisha yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka niuelekeze mchango wangu katika Sekta ya Nishati. Nchi imefunguka, Serikali inataka mapato, lakini mpaka leo bado tuna tatizo kubwa sana katika nchi la Nishati ya umeme. Umeme wetu bado haukidhi vigezo au viwango katika uzalishaji ambao unahitajika katika nchi yetu. Kwa mfano, viwanda vingi sasa hivi vinazalisha lakini unapokatika umeme kunakuwa na tatizo, production ikisimama, mpaka itakapoanza upya ni hasara kubwa ambayo wanaipata wazalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wanalipa umeme bei kubwa sana na matokeo yake wanashindwa kulipa kodi inayopaswa kwa Serikali. Kwa hiyo, naiomba Serikali katika Bajeti ya mwaka huu iangalie sana katika suala zima la nishati ya umeme ili kuboresha viwanda vyetu na hatimaye uzalishaji uweze kufanyika katika kiwango kinachotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ambalo nataka kuipongeza Serikali ni suala la ongezeko la bajeti ya Kilimo. Serikali imefanya jambo kubwa sana, kutoka Shilingi bilioni 294 hadi kufikia Shilingi bilioni 954, siyo padogo! Ongezeko la karibuni Shilingi bilioni 660 ni hatua kubwa mno imepigwa. Naomba Serikali ihakikishe kwamba hii pesa ambayo wametengewa Wizara ya Kilimo, basi yote iende katika Wizara ya Kilimo ili tuweze kuwa na uzalishaji ulio bora wa chakula pamoja na bidhaa nyingine za kilimo ambazo zitakwenda katika viwanda vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kuzungumza ni suala la Bandari zetu. Kumekuwa na changamoto kubwa sana katika Bandari ya Dar es Salaam ambayo kwa sasa hivi imezidiwa. Ukisafiri kama unakwenda Zanzibar utakuta meli zimejazana kule mbele. Kama kilomita chache kutoka Bandarini pale, meli nyingi mno; zaidi ya meli 25 mpaka 30 utaziona zimetia nanga, zinasubiri kwenye kupakua mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la Bandari ya Bagamoyo ambayo kila siku inazungumziwa. Mheshimiwa Waziri katika bajeti yake aliizungumza katika ukurasa wa 47, namnukuu: “Serikali inaendelea na majadiliano na Wawekezaji watakaowekeza katika eneo maalum la uwekezaji la Bagamoyo, hususan katika miradi ya misingi mitatu; Bandari ya Kisasa (Modern Sea Port); sehemu maalum ya kusafirishia na kuhifadhia mizigo (Logistics Park); namba tatu, sehemu ya Mji wa Viwanda (Port Side Industry).

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri umuhimu wa hiyo Bandari unajulikana, kama tunakata Serikali iongeze kipato na ipate pesa, basi ichukue hatua za dharura na za makusudi kabisa kuhakikisha hii Bandari inajengwa haraka. Bandari hii itakapojengwa itaipunguzia mzigo Bandari ya Dar es Salaam na kuiingizia Serikali pesa nyingi za kutosha. Kwani mpaka sasa bado Bandari haifanyi kazi vya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi katika Bandari yangu ya Bagamoyo. Mheshimiwa Waziri, pale kwangu Bagamoyo kuna Bandari. Ile bandari inafanya kazi kwa ufanisi mkubwa sana, lakini nilikuwa naomba sana hapa Bungeni kwamba pale Bagamoyo imefikia wakati sasa Serikali iangalie uwezekano wa kujenga gati la kupaki zile meli (boat) au majahazi yanayokuja kwa ajili ya kushusha mizigo. Bandari hii inaingiza Shilingi bilioni 27 kwa mwaka, Shilingi bilioni mbili kwa mwezi. Hii siyo hela ndogo. Miundombinu ya Bandari ile ya Bagamoyo imechoka, haiko vizuri, sehemu za kupaki meli hakuna. Kwa hiyo, kidogo kunakuwa na changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu tuangalie kwa undani kabisa jinsi gani tunaweza tukairekebisha miundombinu ya Bandari ile ili iweze kuingiza pesa zaidi. Kwa sababu mpaka sasa sehemu kuba sana ya mapato inakwenda katika sehemu tofauti, yaani kuna mianya ya kutorosha mapato. Kuna bandari bubu nyingi, nyingi kule. Hii ni kwa sababu miundombinu ya pale siyo sahihi. Kama kungekuwa na miundombinu sahihi na tukaweka ulinzi katika sehemu za Bagamoyo, nafikiri Bandari hii ingeweza kutuingizia pesa nyingi. Hii Shilingi bilioni 27 kwa mwaka ingekuwa ime-double au ikawa zaidi ya hapo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine ningependa sana niipongeze Serikali kwa kundoa ada katika elimu ya Kidato cha Tano. Kwa kweli Serikali ya Mama Samia naipongeze sana kwa jambo hili, wamefanya kazi kubwa sana na Mwenyezi Mungu atawalipa kwa hili kwa sababu wazazi wengi wamefurahia jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine nataka kuzungumzia kidogo ni suala la utalii na hasa katika upande wa barabara. Pale kwangu Bagamoyo kuna barabara ambayo inaenda Pangani, Tanga, inatokea Makurunge. Ile barabara katika uchumi wa nchi ni muhimu sana, kwa sababu Mbuga ya Wanyama ya Saadan, watalii wote wanapita katika ile barabara. Ile barabara ikinyesha mvua kidogo haipitiki, kwa hiyo, ile Mbuga ya Wanyama ya Saadan ina-cease.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mbuga ya Wanyama ya Saadan ni mbuga ambayo watalii wanaipenda. Kwa sababu ni mbuga ambayo unakaa Baharini unamwangalia twiga, unamwangali mnyama yoyote, ukiwa beach. Kwa hiyo, ni mbuga ambayo ni ya pekee kabisa. Tatizo kubwa ni miundombinu. Kwa hiyo hii barabara ya kutoka Makurunge kwenda Saadan ikianza kutengenezwa itahamasisha utalii, na hii Royal Tour ya Mama Samia, ambayo ameanzisha Rais wetu itakuwa na faida kubwa sana. Kwa hiyo, nawaomba mlizingatie hili, kama tunataka kukusanya mapato, tuangalie sehemu ambazo muhimu zitakazotuingizia mapato haraka zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bagamoyo ina vivutio vingi sana vya utalii. Bagamoyo ni sehemu ambayo ina utalii wa asili, utalii wa bahari. Kwa hiyo, narudi pale pale, itakapotengenezwa gati ya speed boat au gati ya kupaki vyombo vya majini, watalii wengi kutoka Zanzibar watakuja Bagamoyo na hivyo Serikali itaongeza kipato.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)