Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Muharami Shabani Mkenge (6 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. MUHARAMY S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwako kwa kupata nafasi hii. Napenda pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema hadi kufikia siku ya leo. Napenda pia niwashukuru wananchi wenzangu wa Jimbo la Bagamoyo kwa kunipa heshima kubwa ya kuwa hapa leo. Pia napenda niishukuru familia yangu, ndugu zangu na jamaa zangu kwa kuni-support hadi nimefikia hatua hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja katika Mpango. Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango amewasilisha Mpango wake; kwa kweli kabisa ni mpango mmoja ambao ni mzuri sana, kama jina lake lilivyo Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niguse katika suala zima la kilimo. Katika mpango nataka nijikite zaidi katika kilimo cha umwagiliaji. Serikali katika hotuba yake ya Mpango imezungumza kwamba hekta za umwagiliaji ziko 461,378 na ina mpango wa kuongeza hekta hizo hadi kufikia 694,715.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumze; pale kwetu Bagamoyo tuna kilimo cha umwagiliaji katika Bonde la Mto Ruvu. Kilimo hiki kinawasaidia watu wengi sana. Si Mto Ruvu pekee, tuna Mto Wami ambao una nafasi kubwa sana katika kuisaidia nchi katika kilimo hiki cha umwagiliaji, kwa sababu mwaka 1966 mwezi Oktoba kulifanyika study na kampuni moja ya watu wa Sweden ambayo ilikuwa inafanya kazi ya kufanya utafiti wa mradi wa umeme pamoja na bwawa kubwa sana la umwagiliaji katika Mto Wami ambalo lilitakiwa liwe pale Mandera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Serikali, bwawa hili likitumika katika kilimo cha umwagiliaji maeneo mengi sana ya Bagamoyo pamoja na Mkoa wa Pwani, Kibaha, yanaweza yakapata maji mengi sana kupitia mradi huu kwa sababu ni bwawa ambalo limefanyiwa study na makaratasi yake yapo, nafikiri hata Wizara inalitambua hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nirudi katika suala la wavuvi. Bagamoyo kwetu sisi tunashughulika na uvuvi na kwa bahati nzuri Serikali mwaka huu kupitia jemedari wake, Rais Dkt. John Pombe Magufuli, wameamua kununua meli nane za uvuvi. Nina imani katika meli hizo Bagamoyo inaweza ikapatiwa meli moja; sina shaka na hilo kwa sababu Chuo cha Uvuvi Mbegani ambacho kina wataalam wengi sana wanaojua masuala ya uvuvi tuko nacho pale. Niwashauri ndugu zangu, suala hili la uvuvi tukilishikilia linaweza likatuingizia pesa nyingi sana katika nchi yetu. Kwa sababu mwaka 2015/2016 mauzo yalikuwa dola bilioni 379, mwaka 2019/2020, mauzo yanaonesha yalikuwa dola bilioni 506,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishauri; pale Bagamoyo pana mradi mmoja wa kufuga jongoo bahari. Hawa jongoo bahari bei yake ni kubwa sana duniani. Hata Waheshimiwa Wabunge mki-google katika hizo tablets zenu sea cucumber, world price market ni shilingi ngapi, mtaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Waziri alitembelea pale tulikwenda sehemu ambako wanafugia yale madude. Kilo moja ya jongoo bahari ni Sh.65,000. Sasa tukielekeza katika miradi kama hii Serikali inaweza ikatupatia pesa nyingi sana na kuhakikisha mipango yetu ya maendeleo itakuwa sawa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana, muda umekwisha Mheshimiwa.

MHE. MUHARAMY S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mengi, lakini naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii. Kwanza kabisa napenda nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri, Katibu Mkuu, kwa kazi nzuri wanayoifanya, japo Wizara ina changamoto nyingi sana. Nami naomba tu niwaambie, wanayozungumza Wabunge hapa, hebu yachukueni kwa makini mkayafanyie kazi, msiyaache yakapita ikawa business as usual.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda zaidi kuzungumzia suala la utalii wa ndani. Utalii wa ndani naona umesuasua sana katika Taifa letu. Kila siku Wizara inapiga kelele, inahamasisha, inapiga debe kuhusu utalii wa ndani, lakini bado utalii wa ndani haujawa sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nitoe ushauri. Sasa hivi duniani biashara huwa inamfuata mteja na siyo mteja anayeifuata biashara. Naomba niishauri Wizara, sasa hivi wabadilishe mfumo wa utalii wao wa ndani. Sasa hivi hakuna Watanzania walio wengi wenye uwezo wa kutembelea Ngorongoro, Manyara na Mikumi; na wana hamu ya kuona wanyama katika hizo mbuga na kutembelea mbuga hizo, lakini uwezo wao ni mdogo. Nawashauri kitu kimoja. Kama mnavyofanya Saba Saba katika maonesho, Banda la Maliasili linatembelewa na watu wengi sana kuliko mabanda yote katika maonesho ya Saba Saba. Hii ni kwa sababu gani? Watu wengi wanapenda kuona wanyama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jaribuni sasa hivi kuweka utalii wa mobile. Mtafute viwanja katika miji kama Dar es Salaam na Dodoma, muweke mabanda ambayo wananchi watakwenda kutembelea wanyama na kulipia pesa. Mtaingiza pesa nyingi za kutosha. Mikoa mingi sana haina mbuga za wanyama na hawawajui wanyama hawa wakoje, kwa hiyo, watu wengi sana wanapenda kuona simba, chui na wanyama mbalimbali, lakini wanakosa fursa za kwenda kuwaona. Sasa ifikie wakati mtengeneze hicho kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, pale Dar es Salaam, Coco Beach au pale kwangu Bagamoyo, kuna beach nzuri na maeneo mazuri. Mkiweka zoo pale ya Wanyama, watu waje kutembelea, watu wengi kutoka Zanzibar; Zanzibar inapokea watalii wengi sana, lakini wanaishia kule, hawana pa kwenda. Wakitoka Zanzibar wanaondoka zao kwenda Kenya. Hebu tuwape fursa watalii wengi wanaokwenda Zanzibar waje Bagamoyo. Nawashauri kitu kimoja, mjenge gati pale, mjenge gati ya kupaki speed boat ambapo mtalii anaweza akatoka Zanzibar akaja mpaka Bagamoyo, akatembelea Mbuga ya Wanyama ya Saadani, akatembelea vivutio vilivyo Bagamoyo na halafu akapanda boti akarudi Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itasaidia sana kuamsha uchumi wa utalii, lakini tukitegemea utalii wetu tuone watu wakitembelea mbuga za wanyama, hiyo itachukua muda mrefu sana na hamtatengeneza pesa. Kwa sababu, watu wengi sasa hivi wanapenda kuona Wanyama; vijana wa shule za msingi, vijana wa sekondari, vijana wa vyuo, wote wanapenda kitu hiki. Kwa hiyo, nawaomba sana, mbadilishe mfumo wa utalii wa ndani, mtengeneze zoo katika miji yetu…

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nishukuru kwa kupata nafasi hii kwa jioni hii ya leo kutoa mchango wangu katika Bajeti hii ya Serikali ya mwaka 2021/2022. Kwanza napenda nitoe pongezi za dhati kabisa zinazotoka ndani ya moyo wangu kwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu, jemedari wetu, Amiri Jeshi Mkuu wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Kwa kipindi kifupi ambacho nipo ndani ya Bunge hili, mama huyu kiongozi wetu ametuheshimisha sana Wabunge kwa kutoa pesa, takribani kwa muda mfupi, shilingi bilioni moja na pointi kadhaa katika majimbo yetu. Tunampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, napenda nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba kwa uwasilishaji wa bajeti yake ambayo haijapata kutokea. Miaka yote kabla sijawa Mbunge nilikuwa nasikiliza bajeti, lakini hii bajeti ambayo niko ndani ya Bunge ni bajeti ya aina yake. Nampongeza Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba na ninaamini kuwepo katika timu fulani yenye rangi nzuri nzuri kumesababisha na mambo yake yawe mazuri ndani ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nitoe mchango wangu kwanza katika Sekta ya Uvuvi. Serikali mwaka huu katika mipango yake imeamua kujenga Bandari ya Mbegani ya Uvuvi. Naipongeza sana Serikali kwa jambo hili. Bandari hii ya Uvuvi itakapojengwa italeta manufaa makubwa siyo kwa Wanabagamoyo peke yake, ni kwa Watanzania wote kwa sababu Mbegani miaka mingi inafahamika ni Chuo kikubwa sana cha Uvuvi na wanafunzi wengi kwa miaka ya nyuma walikuwa wanasoma pale katika kile Chuo cha Mbegani. Sasa hivi, kile chuo kiko katika hali ngumu kidogo. Katika ujenzi huu wa bandari ya uvuvi ambayo inatakiwa kujengwa, itaifufua sekta ya uvuvi katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naipongeza Serikali kwa kununua meli nne za uvuvi. Hizi meli pamoja na hii bandari vikienda sambamba, basi katika sekta ya uvuvi, Serikali itakusanya mapato mengi ya kutosha. Wenzetu wako mbali katika suala la uvuvi. Kwa mfano, wenzetu Wakenya wana bandari yao pale inaitwa Liwatoni Fishing Port. Ile bandari imejengwa mpya kabisa; na mwaka huu mpaka Juni 2021, wamesema wanaingiza wanafunzi 1,000 pale kwa ajili ya kujifunza masuala ya uvuvi ili ile bandari iweze kufanya kazi kiaina yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo basi, naiomba Serikali katika bandari hii ambayo inatarajia kujenga pale Mbegani, kwanza waanze kutoa mafunzo kwa vijana ambao watakwenda kufanya uvuvi katika hiyo bandari. Halafu bandari itakapokwisha, kazi moja kwa moja inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili nataka kuzungumzia katika sekta ya utalii. Siku moja nilichangia hapa katika mchango wangu kuhusu utalii wa ndani. Utalii wa ndani una pesa nyingi sana, lakini niliwashauri kitu kimoja, sasa hivi ifikie wakati tuanzishe utalii wa kutembea (mobile), kwa sababu Watanzania wengi sana hawana uwezo wa kwenda katika mbuga za wanyama. Tutashawishiwa sisi Wabunge twende Ngorongoro, twende Manyara na Mikumi lakini mtu wangu pale wa Bagamoyo au sehemu nyingine yoyote hawezi kuwa na kipato leo hii cha kwenda kutembea katika mbuga za wanyama za Mikumi, Ngorongoro au Manyara. Hapo itakuwa ni ngumu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naishauri Serikali, kwa sababu mabanda ya maliasili pale Saba Saba yanatembelewa na watu wengi sana katika kuona wanyama, waende kila mkoa wakafungue hizi zoo ndogo ndogo za kutalii watu. Wajenge mabanda, waweke simba, waweke swala, kila mnyama pale, watu wakienda wanalipa viingilio kwenda kuona wanyama. Wanafunzi, watu mbalimbali wakienda huko pesa itapatikana, tena kwa wingi sana, kuliko tukitegemea utalii wa ndani tuwashawishi watu waende Ngorongoro, Manyara na wapi. Watanzania walio wengi uwezo huo hawana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika suala la biashara. Biashara ndiyo inayoleta kodi na kodi ndiyo inatusaidia katika kuendesha nchi yetu. Hata hivyo, kuna changamoto sana katika biashara na hasa katika sheria hizi za TRA, za Utaifishaji. Sheria za Utaifishaji ni changamoto kubwa sana. Hizi sheria naona kwa upande mmoja au mwingine zinatakiwa sasa zifanyiwe mpango zirekebishwe. Kwa sababu leo hii kwa mfano mtu ana gari yake amenunua, amemkabidhi dereva Fuso au lory, amekwenda kubeba mzigo huko, bahati mbaya huo mzigo ni wa magendo. Inafika gari inakamatwa, inapelekwa katika sehemu labda TRA wanaikamata, wanataifisha mzigo, wanataifisha gari, pengine mwenyewe mwenye gari hahusiki. Hii inatia hasara sana kwa watu na watu wengi wanalalamika mno, kwamba kosa kafanya dereva lakini gari linataifishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hebu hii sheria tuiangalie vizuri kwa kweli, inaumiza sana watu. Pale jimboni kwangu Bagamoyo kuna kijana mmoja ana Fuso zake mbili; madereva walikwenda wakapakia vitenge vya magendo, magari yakakamatwa, yakataifishwa. Kijana wa watu wamemrudisha nyuma. Alikuwa na Fuso mbili ambazo amezitafuta karibu miaka 20, ameanza tena sifuri. Yaani amechanganyika karibu anakuwa chizi. Jamani haya mambo mengine ya sheria tuyaangalie Mheshimiwa Waziri ili wafanyabiashara wetu waweze kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile hizi sheria za kutaifisha tunazozitunga humu ndani, wawekezaji wa nje wakizisikia hawatakuwa na imani ya nchi yetu. Wataona kwamba Tanzania ukienda kuwekeza, kama wenyewe kwa wenyewe wanataifishana, mimi mgeni nikiwekeza mali yangu itakuwa salama? Kwa hiyo, nafikiri kwamba tubadilike. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la mwisho kabisa nataka kulizungumzia ni la sensa, sensa ni kitu muhimu sana. Kuna kitu ambacho nataka nimshauri Waziri, nchi zilizoendelea nyinginezo sasa hivi sensa yao, pamoja na kwamba, wanapanga kila baada ya miaka fulani wanafanya sensa, lakini wanafanya sensa ya ndani kwa kutumia watu wao. Na sisi Tanzania tuanze kufanya sensa ili tuwe na projection ya kujua maendeleo yetu yanakuaje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu, leo hii tunangojea kila baada ya miaka 10 au mingapi tufanye sensa, tunao watendaji wa vijiji, tunao watendaji wa kata, tuwatume kazi wapite vijijini kuangalia idadi ya watu wanaozaliwa ili Serikali iwe na projection vinginevyo tutakuwa na ule mpango wa zimamoto, hatujui idadi ya watu, watoto wanaoenda sekondari wanaongezeka, tunajenga madarasa ya zimamoto. Lazima tuwe na mipango thabiti katika hii sensa, tuwatumie viongozi wetu wa vitongoji watuletee taarifa wazipeleke katika kata taarifa za watoto waliozaliwa nchini, wa vitongoji wapeleke kwenye kata, watu wa kata nao wapeleke wilayani, watu wa wilayani wapeleke mkoani. Mkoani wapeleke Taifani tupate mtiririko wa idadi ya watu wanaozaliwa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu, tukitegemea taarifa za hospitali tupu, wengine wanajifungulia majumbani hatupati taarifa zao kwa hiyo, inakuwa kidogo kuna ugumu fulani. Niiombe Serikali hili suala la sensa wasingojee mpaka kipindi, walianze mapema kuangalia projection ya nchi inakwendaje katika uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala ambalo la kilimo, nataka kuzungumzia, kilimo cha umwagiliaji. Hiki kilimo cha umwagiliaji tukikifuatilia na tukikitilia mkazo Taifa litatoka kabisa katika maisha tuliyonayo sasa hivi kwa sababu, umwagiliaji ndio wenye tija. Tukitegemea mvua hizi za kunyesha tu za msimu wakulima wetu wengi sana huwa hawazalishi pale ambapo idadi yao au idadi ya mazao wanayohitaji kufikia lengo, lakini kilimo cha umwagiliaji kitatusababishia tufike katika level nzuri kabisa ya uzalishaji katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda kutumia nafasi hii kutoa shukrani zangu za dhati kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia hoja iliyo mbele yet una nitajikita zaidi kwenye upande wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa napenda kutumia nafasi hii, kwa niaba ya wananchi wa Bagamoyo, kukupongeza kwa kuchaguliwa kuwa Spika wetu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia napenda kumpongeza Mwenyekiti wetu, Mheshimiwa Mussa Azzan Zungu, ambaye anatarajiwa kuwa Naibu Spika saa chache zijazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kwanza nizungumze kuhusu suala la mahusiano yetu ya Tanzania na nchi za nje. Napenda kutoa shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kuikuza diplomasia ya Tanzania nje ya mipaka yetu. Mama Samia anafanya kazi kubwa sana. Kwa kipindi kifupi toka ameingia madarakani amefungua milango mingi ya mahusiano ya kimataifa katika nchi yetu; tunampongeza sana kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama unavyotambua katika Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuna vyombo vingi ambavyo vinahusiana na Kamati hii, lakini nizungumze moja kuhusu suala la NIDA. Wananchi wa Tanzania kwa miaka mingi sana walikuwa wakisumbuka katika kupata vitambulisho vyao vya Taifa, lakini leo hii tunakoelekea baada ya Mheshimiwa Rais, mama Samia Suluhu Hassan kuchagua viongozi wapya katika taasisi hii mwelekeo wa upatikanaji wa vitambulisho vya Taifa unaelekea kuwa mzuri katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, siku zilizopita Serikali ilikuwa ikisumbuka sana na suala hili. Mashine zililetwa, mitambo ililetwa lakini kwa bahati mbaya kazi iliyokuwa ikifanyika haikuridhisha Watanzania wengi; idadi kubwa ya watu wamesajiliwa lakini hawajapata vitambulisho vya Taifa. Leo hii Kamati imejiridhisha kwamba kazi inayokwenda kufanyika kwa ajili ya upatikanaji wa vitambulisho vya Taifa ni kazi ambayo itakuwa yenye kutukuka. Tunawapongeza sana viongozi wa NIDA kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea nayo mpaka sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo nataka kulizungumzia hapa ni suala la mtangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki pamoja na Jumuiya ya SADC. Jumuiya hizi zimekuwa na faida kubwa kwetu sisi Watanzania na hasa baada ya Rais wetu, mama Samia Suluhu Hassan, kufanya ziara katika baadhi ya Nchi za Afrika Mashariki na kugundua fursa mbalimbali ambazo tunafaidika nazo hii leo kutokana na uwepo wa jumuiya hii.

Mheshimiwa Spika, katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ni mambo mengi sana ambayo yanafanyika na hasa fursa zilizopo za kibiashara. Ni wajibu wa Serikali sasa hivi kuhakikisha kwamba fursa zilizopo za kibiashara wanaziweka wazi ili wananchi waweze kuzitambua na kuweza kukimbizana nazo ili waweze kuiletea nchi yetu maendeleo.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli usiopingika kuwa Tanzania tuna matajiri wengi, tuna wafanyabiashara wengi, lakini bado mpaka leo hawajapata taarifa rasmi za fursa zilizopo. Kwa hiyo ni jukumu sasa hivi la Wizara zinazohusika pamoja na Serikali kuzitangaza fursa hizi ili wafanyabiashara wetu waweze kuziendea na kuhakikisha kwamba Taifa letu linapata mafanikio makubwa.

Mheshimiwa Spika, katika mtangamano wa SADC faida nyingi zinapatikana. Niipongeze Bohari yetu Kuu ya Dawa (MSD) kwa kupata tenda ya kuweza ku-supply dawa katika Nchi za SADC. Hii ni hatua kubwa sana ambayo Tanzania imeifikia. Tuna nchi nyingi za SADC lakini Tanzania imeteuliwa MSD kusambaza dawa pamoja na vifaatiba katika nchi hizo; hiyo ni hatua kubwa sana ya kimaendeleo katika Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa napenda nipongeze Jeshi letu, Jeshi la Wananchi wa Tanzania. Pamoja na kulinda mipaka, Jeshi lina shughuli nyingi ambazo wanazifanya ili kuiletea maendeleo nchi yetu. Ukiachilia mbali ulindaji wa mipaka, Jeshi linashughulika na shughuli mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze kwa kuendesha Kiwanda cha Nyumbu ambacho kinaendesha teknolojia ya kutengeneza magari. Nafikiri kwa siku zijazo Tanzania itakuwa ni nchi moja wapo ambayo itakuwa inashughulika na mambo mengi sana ya kujitegemea na hasa katika uundwaji wa magari.

Mheshimiwa Spika, pia niwapongeze sana Jeshi letu katika suala zima la kilimo na hasa JKT, wanajihusisha sana katika kilimo na hiki kilimo kwa siku zijazo wataisaidia sana nchi yetu katika usalama wa chakula; niwapongeze sana kwa jambo hili.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo machache, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwanza kabisa napenda nitoe pongezi zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya kuhakikisha Tanzania inatoka hatua moja kwenda hatua nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili napenda nimpongeze Waziri wa TAMISEMI ndugu yangu Bashungwa kwa kazi kubwa anayoifanya. Mheshimiwa Bashungwa anafanyakazi kubwa kwa kipindi kifupi tu tunaona ni jinsi gani ambavyo anapambana kufuatilia mambo. Ni juzi tu hapa lilitokea tatizo Mwanza kule aka-act mara moja mambo yakaenda vizuri na sasa hivi kuna barua moja inatembea ya mtandaoni taarifa kwenye vyombo vya habari kwamba kuna Mkurugenzi mmoja ambaye hajatii maelekezo amewekwa pembeni kidogo. Wizara inataka namna hiyo hii Wizara Mheshimiwa Waziri ni Wizara ambayo Wabunge wote tunaitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii itakapokuwa haijafanya vizuri basi sisi sote Wabunge tutakuwa hatujafanya vizuri katika Majimbo yetu, kwa hiyo tukupongeze sana na tutakupa moyo pamoja na kukusaidia ili uweze kufanikisha azma yetu tunayoikusudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la elimu. Kwanza niishukuru Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kweli katika Jimbo langu la Bagamoyo kwa kipindi kifupi tu tumepatiwa madarasa yasiyopungua Shilingi Bilioni Moja na Milioni Mia Tatu. Hii ni kazi kubwa sana ambayo ameifanya Mheshimiwa Rais na hii imesababisha vile vile katika kipindi kifupi hiki kupata shule mbili za Sekondari mpya kabisa kuna shule ya Sekondari ya Makurunge ambayo ujenzi unaendelea zimepatikana pesa Milioni 600, kuna shule mpya ya Kata ya Nianjema ambayo ujenzi umekamilika na wanafunzi wanaendelea kusoma, kwa hiyo tunazidi kuipongeza sana Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Mama Samia kwa kazi hii kubwa ambayo wanaifanya. Vilevile kuna shule shikizi ambazo tumepatiwa pesa na shule hizi nazo zishaanza kufanyakazi baadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi katika suala la afya, kuna suala la vifaa tiba. Halmashauri zetu nyingi zina vituo vya afya ambavyo vimejengwa mimi niishukuru Serikali, pale kwangu Bagamyoyo Fukayosi Milioni 500 imepatikana na kituo cha afya kinaendelea kuimarika na kitakamilika muda si mrefu. Lakini tatizo kubwa linalotukabili ni vifaa tiba katika vituo vyetu vya afya hakuna zahanati zetu vile vile hazina vifaa tiba, kwa mfano kituo cha afya cha Matimbwa Yombo hakina vifaa tiba kwa hiyo kinashindwa kufanya kazi vile inavyostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo cha afya cha Kerege nacho kina changamoto ya vifaa tiba zahanati ya Buma, Kilomo, Zahanati ya Tungutungu Mapinga, Zahanati ya Mkenge, Zahanati ya Kidomole zote hizi zinakumbwa na changamoto kubwa ya vifaa tiba kwa hiyo naiomba sana Wizara izidishe juhudi kuhakikisha kwamba, katika mwaka huu wa bajeti vifaa tiba vinapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala la TARURA kazi kubwa TARURA wameifanya pesa tulizopata tumefanya mambo makubwa katika Majimbo yetu na mimi kwa upande wangu wa Bagamoyo barabara nyingi sasa hivi ambazo zilikuwa zina matatizo ya kujaa maji na hasa Bagamoyo mjini, maji sasa hivi hayapo kwa sababu barabara zimejengwa kwa kiwango cha mifereji kiasi kwamba maji yanapita na naomba niishauri tu Wizara sasa hivi katika bajeti ijayo basi, tuhakikishe katika barabara zetu tunaimarisha mifereji. Kwa sababu tunapoimarisha mifereji ndiyo barabara nyingi zinadumu lakini tukisema kwamba tunafanya ukarabati wa barabara maji yakijaa yanajaa udongo unaondoka mwakani tunapeleka pesa tena.

Mheshimiwa Spika, kama hizi Bilioni 802 ambazo mmezienga kwa ajili ya TARURA kwa kipindi cha bajeti ijayo mtazifanyia kazi vizuri na mifereji ya barabara itatengenezwa basi itakuwa jambo la kheri na busara kabisa kabisa kwamba barabara zetu nyingi zitapitika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije katika suala la maji RUWASA inajitahidi sana katika suala zima la kusambaza maji vijijini. Mimi kwangu pale Bagamoyo katika Kata ya Fukayose nina mradi wa shilingi milioni 300.000 karibuni na 50,000 lita 75,000 zinajengwa ambazo nina imani wananchi wangu wa vitongoji vya Lusako, Umasaini, Engelo, Mkenge na sehemu zinginezo watapata maji ya kutosha katika kipindi kijacho niipongeze sana Wizara kwa kazi kubwa ambayo mnafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala vilevile la barabara kuna barabara ambazo ni muhimu sana zinakwenda katika mashule pamoja na vituo vya afya na zahanati barabara hizi zipewe kipaumbele katika kuimarishwa kwa sababu wanafunzi wanapata taabu sana wakati wa mvua kwa hiyo katika bajeti hii ijayo Serikali ijitahidi sana kuhakikisha kwamba hizi barabara zinapatiwa kipaumbele na zinaimarishwa, naunga mkono hoja ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE: MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii. Kwanza kabisa ningependa kuchukua nafasi hii kutoa pongezi zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, Mwana Masauni, pamoja na Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu pamoja na timu yote ya Wizara ya Mambo ya Ndani kwa kazi kubwa wanayoifanya. Nawapongeza sana.

Mheshimiwa Spika, mimi kwanza kabisa naomba nizungumzie suala la wahamiaji haramu. Nchi yetu imekumbwa na tatizo kubwa sana la wahamiaji haramu. Mpaka sasa tunavyozungumza kutokana na taarifa ambazo wamezitoa katika hotuba ya Waziri na taarifa ya Kamati, inanesha kuwa kuna wahamiaji haramu wasiopungua 4,025 ndani ya nchi kutoka katika nchi mbalimbali. Wenzetu nchi za jirani hawa wahamiaji haramu wanapokuja katika nchi zao huwa hawakai, wanawaruhusu wanaondoka lakini Tanzania tumejijengea utaratibu kwamba hawa watu wakija tunawapokea, tunawashtaki na tunawaweka katika magereza yetu. Hii inasababisha gharama kubwa sana kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi kama Ethiopia, katika sera yao ya mambo ya nje ni kwamba wanawaruhusu watu wao waende popote kule duniani wanakotaka, hawawakatazi. Kwa hiyo katika nchi nyingi sana wanapita na hawa wahamiaji haramu wa Ethiopia walio wengi hawana dhumuni la kukaa hapa nchini kwetu; nia yao kubwa wao wapite njia. Kwa sababu sisi Tanzania watu wetu wenyewe bado ajira hazijatosha. Kwa hiyo wao hawana nafasi ya kupata ajira katika nchi yetu. Kwa hiyo wanapita njia kuelekea nchi zingine. Kwa hiyo naomba Serikali sasa hivi iangalie ni jinsi ambavyo watawaruhusu hawa watu wapite waende kule wanakotaka badala ya kuwaweka magerezani na kutumia rasilimali zetu za nchi, kwa kuwalisha kwa muda wote ambao wanakuwepo magerezani na kukaa hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwangu pale Bagamoyo mpaka leo hii nina wahamiaji haramu wasiopungua 252 wako pale na wanakula tu siku zinaondoka. Kuna Waethiopia 237, kuna Wasomali 13, kuna Mburundi mmoja na kuna Mkenya mmoja, sasa wote hawa wanakaa wanaitegemea Serikali. Kile tunachokipata kuendesha mambo yetu katika nchi tunaamua kuwahudumia wao. Sasa kwa hiyo niiombe Serikali wafanye haraka iwezekanavyo kuwaondoa hawa watu, wanatutia hasara katika nchi. Kule wenzetu wanapokuwa wanatoka kwao kwa mfano Ethiopia wanawaachia wakifika mpakani wale Maafisa Uhamiaji wakiwa Mashekhe, Mapadri mpaka dua wanawaombea nendeni salama huko mnapokwenda mje kuinufaisha nchi yetu, sisi tunakuja hapa tunawazuia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili nataka kuzungumzia juu ya uzalishaji mali katika Jeshi la Magereza. Jeshi la Magereza linafanya kazi kubwa sana katika uzalishaji mali. Kwa hiyo, niiombe Serikali ili-support sana Jeshi la Magereza na nina imani kabisa kwamba watakapowa-support watu wa Magereza katika suala zima la uzalishaji, Magereza itajitosheleza kwa chakula, Serikali itaondokana na kuhudumia hawa watu. Wao wenyewe wanaweza wakajitosheleza. Wawape vifaa, wawanunulie Matrekta na vifaa vingine vyote. Mashamba wanayo ya kutosha ili waweze kuisaidia nchi katika suala zima la chakula. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala jingine nataka kuzungumza ni suala la vitendea kazi katika Jeshi letu la Polisi. Kumekuwa na lawama kubwa zinazowapata Polisi wetu, Polisi inatokea tukio wanaweza wakachukua dakika 40, hadi dakika 50, lakini gari ileile moja imetoka imeenda katika sehemu nyingineyo. Kwa hiyo magari ni tatizo kubwa sana. Wapatie gari za kutosha ili waweze kuyawahi matukio. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la mwisho, suala la hali ya usalama.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele imeshagonga Mheshimiwa. Ahsante sana.

MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)