Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Deodatus Philip Mwanyika (53 total)

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa mradi huu kama alivyosema yeye mwenyewe utachukua miezi 24, miaka miwili na wananchi wa Njombe wakati huo wataendelea kupata tabu na kuteseka hasa wakati wa kiangazi maji yanapopotea kabisa. Je, Serikali itakuwa tayari kutekeleza miradi mingine midogo midogo ambayo baadhi imekwishabuniwa na inafahamika na mingine inaweza kubuniwa, kwa vile Njombe tumezungukwa na mito kila upande?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Serikali ilishatekeleza mradi mdogo katika Mji wa Kibena pale Njombe, kwa kupeleka maji mpaka Hospitali ya Wilaya ya Njombe na kuna tanki kubwa sana wamelijenga pale na tanki hilo lina maji mengi na saa nyingine yanabubujika na kumwagika. Kwa bahati mbaya wananchi wa eneo la Kibena ambao wanaishi maeneo yale bado hawana. Je, Serikali haioni kama itakuwa ni busara na jambo jema badala ya maji yale kuwa yanabubujika na kumwagika sasa wakatoa pesa na kuweka mradi mdogo wa kutawanya maji ili wananchi wa Kibena wapate kuwa na maji ya uhakika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba nijibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwanyika kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala la hofu kwa sababu mradi utaanza mwezi Aprili na yeye anapenda visima ama miradi midogo midogo, nipende tu kumwambia kwamba tayari Wizara inafanya mchakato huo na hili linashughulikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na mradi ambao unapeleka maji kwenye hospitali ya Kibena pale kwa kuhitaji distribution tayari Wizara imetoa maelekezo kwa mameneja walioko pale wanafanyia upembuzi yakinifu ili kuona namna gani kama distribution itawezekana. Naomba kukupa amani Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi huu ambao tunauanza mwezi Aprili, tutaenda kuufanya kwa kasi nzuri na tutaweza kutawanya maji kadri mradi unavyokamilika hatutasubiri mradi ukamilike mpaka mwisho, ukifika hata asilimia 40 wale ambao wanapitiwa na lile eneo ambalo miundombinu imekamilika maji yataweza kutoka. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ambayo inaongelewa ya kwenda Kishapu ni sawasawa kabisa na barabara ya kilometa 60 ndani ya Mji wa Njombe yaani Ntoni na kwenda mpaka Lusitu. Barabara hii tunaambiwa ilishafanyiwa upembuzi yakinifu, imeshafanyiwa usanifu wa kina lakini sio tu hivyo, barabara hii vilevile imekuwa kwenye ahadi za Ilani ya Uchaguzi wa CCM ya mwaka 2015 - 2020 na mwaka 2020 – 2025.

Swali, ni lini sasa Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara hii ambayo ni muhimu sana kiuchumi na inapita katika maeneo ya Njombe Mji, Uwemba, Luponde na Matola? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Njombe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayoisema atakubaliana na mimi kwamba iko sehemu ambayo ndiyo inakwenda mpaka huko Ludewa tayari imeshaanza kufanyiwa kazi na mimi nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge awe na subira, kipindi hiki ni cha bajeti tunatambua umuhimu wa hii barabara na nadhani baada ya bajeti ataamini kwamba Serikali kweli ina mpango wa kuhakikisha kwamba barabara hii ya Njombe – Itoni – Lusitu inajengwa. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii iko kwenye mipango ya Wizara kwa maana ya Serikali kwamba itaendelea kujengwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya swali la msingi lakini niulize swali la kwanza. Kwanza tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa maamuzi aliyoyatoa siku ya Jumatatu ya kuruhusu kuajiriwa kwa walimu 6,000 kwa haraka, tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ni ukweli kwamba walimu 6,000 wanaokwenda kuajiriwa bado wanakwenda kufanya replacement; mahitaji ya walimu katika shule bado ni makubwa sana. Maamuzi ya Serikali ya kutoa elimu bure kwa nia njema yamefanya kuwe na uhaba mkubwa sana wa walimu katika maeneo hasa ya vijijini. Kwa hiyo, pamoja na mipango ambayo imeelezewa lakini bado kuna tatizo kubwa na ninapenda kujua, je, Serikali inaweza bado ikatoa commitment kwamba itaajiri walimu wa kutosha? Kwasababu hii namba iliyotajwa hapa bado haitoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; naelewa kuna vigezo ambavyo vinatumika kwenye ugawaji wa walimu kwenye maeneo mbalimbali. Ni ukweli usiopingika kwamba kwa yale maeneo ambayo ni miji ambayo iko ndani ya halmashauri vigezo ambavyo vinatumika kwa kweli havina uhalisia kwasababu maeneo hayo unakuta yanaangaliwa sana kwasababu yana miji lakini vilevile yana maeneo mengi sana yenye shule nyingi sana ambayo wananchi wamejitoa wakajenga shule ambazo zipo katika maeneo ya vijijini. Wanapoangalia vigezo vya reallocation unakuta kwamba hawaangalii hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali; je, Wizara itakuwa tayari kupitia upya vigezo vya ku-allocate walimu ili maeneo ya halmashauri za miji ambayo yana maeneo makubwa ya zaidi ya kilometa 25 yaweze kupata walimu ili elimu yetu iwe na tija? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri wazi kabisa kwamba alichozungumza Mheshimiwa Mbunge ya uhaba wa walimu nchini pamoja na replacement ya walimu 6,000 ambayo tunakwenda kuifanya hivi karibuni bado upo. Na Serikali imeji-commit hapa katika statement yangu ya awali kwamba tutaendelea kuajiri kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Na mpango huo upo na ni endelevu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge ondoa wasiwasi kwenye hilo kwa sababu Serikali iko makini, na Serikali ya Rais wa Sita, mama Samia Hassan Suluhu, imejipanga kuhakikisha tunaondoa kabisa tatizo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, amezungumzia kuhusu Wizara kama tutakuwa tayari kupitia vigezo vya ugawaji wa walimu upya. Nikubali kabisa hilo tumelipokea, moja, ni kama ushauri, lakini pili, tutaendelea kulizingatia kuhakikisha kabisa ugawanyaji wa walimu wote nchini unafuata usawa na haki katika maeneo yote. Ahsante sana.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Njombe Mjini na sisi tuna Kituo cha Afya ambacho kina uhitaji wa wodi ya kibaba na wazazi na huduma ya upasuaji na Serikali ilishaonesha nia ya kutusaidia.

Swali, je, ni lini sasa shughuli ya ujenzi na ukarabati wa kituo cha afya cha muda mrefu sana Njombe Mjini utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika Jimbo la Njombe Mjini kuna Kituo cha Afya cha Mji Mwema na cha siku nyingi ambacho kina uhitaji mkubwa wa miundombinu ya wodi ya akina baba akina mama lakini na wodi ya watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti ya mwaka huu wa fedha tumetenga fedha kwa ajili ya kwenda pia kuongeza miundombinu katika Vituo vya Afya na nimuhakikishie kwamba Kituo cha Afya cha Mji Mwema katika Jimbo la Njombe Mjini nacho kitapewa kipaumbele.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Moja, baada ya ufuatiliaji wa karibu sana kwenye suala hili imedhihirika wazi kwamba kwa Jimbo la Njombe ni vijiji vinne tu, Mgala, Ngalanga, Mtila na Mbega ndivyo vilivyoingizwa kwenye Mpango ambao Mheshimiwa Naibu Waziri anauongelea. Kuna vijiji takriban 20 ambavyo vimesahaulika, vijiji hivyo ni Hungilo, Uliwa, Utengule, Diani, Makolo, Lugenge, Mpeto n.k. Naomba Serikali itoe kauli kuhusiana na suala hili na iwadhihirishie wananchi wa Njombe kama sasa baada ya maongezi kati yangu, Waziri na REA vijiji vilivyobaki vyote vimeingizwa katika Mpango huo.

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Pamoja na vijiji vingi kuunganishwa na hasa kwenye Jimbo letu la Njombe Mjini bado tuna ukatikaji wa umeme mkubwa sana ambao unaashiria kwamba pamoja na kuunganishwa, tatizo hili litaendelea kuwa kubwa. Tunaomba maelezo ya Wizara kuhusiana na ukatikaji wa umeme katika Mji wa Njombe ambao ni endelevu na hauishi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ni kweli mara ya kwanza vilichukuliwa vijiji vinne lakini baada ya Mheshimiwa Mwanyika kuwasiliana na ofisi na tunamshukuru na kumpongeza kwa ufuatiliaji wake mkubwa, Wizara imeamua iongeze scope ya kazi ya awali na kuongeza vijiji hivyo.

Mheshimiwa Spika, kimsingi vilikuwa havikuachwa lakini vilikuwa vimebaki kwasababu viko katika eneo linalokaribiana na mji. Kwa hiyo, vilikuwa havikuingia kwenye mradi wa REA lakini tumevichukua tukivi-treat kama peri- urban area. Kwa hiyo, vijiji hivyo 20, nimhakikishie Mheshimiwa Deo Mwanyika kwamba vimeingia na vitafanyiwa kazi katika awamu hii ya kupeleka umeme vijijini.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili, ni kweli. Maeneo ya Njombe yana tatizo kubwa sana la ukatikaji wa umeme. Naomba nitumie muda kidogo tu kukueleza tatizo kubwa tulilokuwa nalo Njombe na hatua taunazozichukua. Njombe inapata umeme kutoka katika kituo chetu cha kupooza umeme cha Makambako na kuna kilometa 60 kutoka pale Makambako mpaka Njombe, Njombe Mji na eneo kubwa la Mkoa. Sasa Njombe tunayo matatizo makubwa matatu.

Mheshimiwa Spika, tatizo kubwa la kwanza ni baraka ambazo Njombe imezipata ya kuwa na miti mingi sana. Ile miti, pamoja na sisi kufyeka ile line ya kupitisha umeme, lakini miti inayokuwa nje ya line yetu ya umeme baadaye inaangukia ndani ya line yetu kwa sababu inakuwa ni mirefu sana. Kwa hiyo, tumeendelea kufyeka na kuhamasisha wananchi basi hata watuongezee line ambayo iko nje zaidi ya line yetu sisi ili tunapofyeka basi miti inayotokea nje ya line
yao isije ikaleta shida kwenye eneo letu.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo linatupa shida sana kwa Mkoa wa Njombe ni radi. Maeneo ya Njombe, kama nilivyowahi kusema hapa, Mkoa wa Kagera lakini pia Mbeya, tunayo matatizo makubwa sana ya radi ambazo zimekuwa zikileta shida kwenye miundombinu yetu ya umeme.

Mheshimiwa Spika, tunachokifanya kwa Mkoa wa Njombe kwa mfano kila tunapofunga transformer tunaifanyia earthing system. Ile earthing system inatakiwa uzamishe chini, lakini unapima udongo kuona resistance value ya udongo ni kiasi gani. Kama iko 0 - 60 inakuwa haina shida, kama iko zaidi ya 60 inabidi kutumia zile njia za kienyeji na za kitaalam za ku--treat udongo ili radi ikienda iweze kumezwa kule, tunatumia mbolea na vitu vingine kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, pengine tukifunga transformer tunachelewa kuiwasha kwa sababu tukipima resistance value ya udongo tunaona bado ina-resist sana radi, kwa hiyo, tunaamua kuiacha kwanza ili ipoe kidogo.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu Waziri.

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie. Naomba niruhusiwe kutoa nondo kama alizozitoa mwenzangu Ndaisaba jana kwa ajili ya uelewa mzuri.

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili tunafunga vifaa vya muhimu sana vinavyoitwa surge arrester and combi unit kuhakikisha kwamba transformer haiharibiki mara kwa mara. Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Deo kwamba tutaendelea kuhakikisha kwamba…

SPIKA: Nakushukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu ambayo Mheshimiwa Naibu Waziri ameyatoa, naomba niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Njombe ni moja katika mikoa mitano bora ambayo imefikia kiwango cha uchumi wa kati kwa watu wake, mkoa huu ni moja kati ya Halmshauri 10 bora kwa makusanyo zinazizidi hata Manispaa zaidi ya 10 katika nchi hii. Mkoa wa Njombe ni mkoa ambao una miradi mikubwa ya kimkakati ikiwemo parachichi pamoja na Liganga.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu; hivi ni kigezo gani kinachotumika maana wasiwasi wetu hata katika viwanja 11 tunaweza tukawa wa mwisho kwa sababu sioni ni vigezo gani, ukienda kwa niliyoyasema Mkoa wa Njombe unatakiwa uwe mkoa wa mwanzo kupata uwanja wa ndege? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tunatambua mchango mkubwa wa kiuchumi kutoka Mkoa wa Njombe kwa ujumla wake pamoja na Njombe Mjini. Lakini vilevile uwezo wa Serikali siyo mkubwa kiasi hicho kujenga viwanja hivi vyote 11 kwa wakati mmoja. Safari ni atua upembuzi yakinifu umefanyika sasa tunajua gharama ya kujenga uwanja wa ndege wa Njombe ni gharama kiasi gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukweli ni kwamba unaangalia, ameuliza vigezo kwa mfano, pale Iringa mjini kuelekea Mkoa wa Iringa karibu kabisa na Makambako na Mkoa wa Njombe, sasa hivi tunazungumza mkandarasi yuko site anaendelea kufanya kazi ya kumaliza runway ili ndege aina zote ziweze kutua eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wakati ambao Serikali inaendelea kupata fedha kutoka mapato ya ndani na washirika wengine wa kimaendeleo, watu wanaotaka kwenda Njombe wanaweza kutumia alternative kutumia uwanja Iringa baada ya kuwa umekamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Serikali yake ni njema tungependa kila Mkoa uwe na uwanja wa ndege na Waheshimiwa Wabunge wakitoka hapa baada ya Bunge kuahirishwa wangependa kutoa katika mikoa yao, lakini kwa kuwa fedha nyingi kiasi hicho tuvumiliane tupeane muda kazi hii itakamilika, ahsante sana.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Njombe tunapitiwa na gridi inayotoka Makambako kwenda Songea, lakini bado tumekuwa na tatizo kubwa sana la ukatikaji wa umeme ambao sisi tunaamini pamoja na maelezo ambayo Waziri ameyatoa siku ya nyuma, tunaamini kutokana na grid stability, ni lini sasa suala la ukatikaji wa umeme usioisha wa Mkoa wa Njombe na Mji ya Njombe utafikia tamati? (Makofi)
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanyika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hasa katika eneo la Njombe pamoja na Ludewa umeme unakatika kwa kiasi kikubwa kwa sababu kuna matengenezo ya kufunga auto recloser ambayo inaimarika ndani ya siku 28. Pia katika maeneo ya Njombe na Ludewa ipo line ambayo tunaongezea, tumetenga shilingi bilioni 270 katika mikoa miwili na bilioni 100 kila mkoa kwa ajili ya shughuli za ukarabati wa mitambo na kuimarisha umeme katika Mkoa wa Makambako, Njombe pamoja na Ludewa. Kwa hiyo niwahakikishie wananchi wa Ludewa pamoja na Njombe kwamba ndani ya muda unaokuja ambao nimeutaja hali ya umeme itaimarika kwa kiasi kikubwa.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Barabara ya Mtila - Lugenge mpaka Usalule ni barabara ya muhimu sana nani barabara inayounga wilaya tatu ikiunga pamoja na Hospitali kubwa ya Mkoa wa Njombe. Je, Serikali haioni kwamba ni muhimu sana hii barabara na yenyewe ikaingizwa katika mpango wa TANROADS kwa sababu mchakato umeshaanza na umekwama mahali Fulani? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanyika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba hoja hii Mheshimiwa Mbunge amefikisha ofisini katika Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Kama alivyosema mwenyewe kwamba mchakato unaendelea, naomba a-speed up process hiyo na sisi tutatoa ushirikiano, itakapokidhi vigezo tutaipokea kama TANROADS, tutaitengeneza na wananchi wake watapata huduma muhimu katika eneo hilo. Ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mkoa wa Njombe mpaka miaka michache iliyopita ulionekana kama ni mkoa mpya. Katika maeneo yaliyosahaulika kwa Mkoa wa Njombe ni Vituo vya Polisi. Je, Serikali ni lini sasa itaanza kukarabati Kituo cha Polisi cha Mkoa wa Njombe ili kiendane na hadhi ya Mkoa wa Njombe? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo ameliuliza, linalozungumzia suala la ukarabati wa Kituo cha Polisi Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba azma yetu ni kuhakikisha kwamba vituo vyote vinajengwa ipo pale pale. Lakini kikubwa nimwambie tu kwamba tutajitahidi pia katika mwaka wa fedha ujao tuhakikishe kwamba kituo hiki nacho tunakijenga kikawa katika hadhi ile ya kuhakikisha kwamba wananchi wanaweza kupata huduma hizi za ulinzi na usalama. Nakushukuru pia.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu yaliyotolewa lakini bado kuna sintofahamu kuhusiana na status ya hiki Kituo. Nitaomba Mheshimiwa Waziri alifuatilie kwa karibu kwa sababu, wananchi wale wenye Bima wanashindwa kupata huduma kwa sababu wanasema officially hakijawa registered kwa hiyo kuna sintofahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, pamoja na Kituo hiki lakini Njombe tuna vituo vingine viwili vya Afya ambavyo havina vifaa ambavyo tumeahidiwa kwa muda mrefu, Kituo cha Makoo pamoja na Kituo cha Kifanya. Mawaziri wametembelea pale lakini tumepewa ahadi na hatuelewi. Sasa je, Serikali inaweza ikatoa kauli kuhusiana na hivyo vituo viwili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Zahanati ya Ihalula imekwisha pandishwa hadhi kuwa Kituo cha Afya na imekwishapewa namba ya usajili kama Kituo cha Afya. Kwa hivyo, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hiyo sintofahamu ilikuwa kwa sababu hatukuwa tumepata namba rasmi ya usajili kuwa kituo cha Afya ili National Health Insurance Fund waanze kuilipa moja kwa moja. Kwa hiyo, sasa limeshafanyika, lakini kama kuna changamoto nyingine zote tutakwenda kuzifuatilia kuhakikisha wananchi wetu wanapata huduma za ngazi ya Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, tumekuwa na ujenzi wa Vituo vingi vya Afya, vikiwemo Kituo cha Afya cha Makoo na Kifanya; na mpango wa Serikali ni kuendelea kutenga fedha za ununuzi wa Vifaa Tiba na Makoo ni moja ya vituo ambavyo Mheshimiwa Waziri wa Nchi alitembelea, aliahidi Vifaa Tiba na utaratibu unaendelea kuhakikisha Vifaa Tiba vinafika pale. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili linafanyiwa kazi. Ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa kumtua mama ndoo kichwani mradi mkubwa ambao utasababisha hili litokee ni mradi wa Miji 26 ambao unafadhiliwa na Serikali ya India. Tunaomba kuuliza Mheshimiwa Waziri.

Ni lini mradi huu utaanza na umefikia wapi? (Makofi)
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge lakini kama unavyotambua program ya kumtua mwana mama ndoo kichwani ni programu ya Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan. Serikali inatekeleza miradi mbalimbali ya maji kupitia bajeti ya Serikali lakini kupitia wadau mbalimbali wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Serikali ya India tunatarajia kutekeleza miradi ya Miji 28 zaidi ya dola milioni 500 na mpaka sasa hatua ambayo tumefikia taratibu zote za kimanunuzi kama Wizara ya Maji tumeshazikamilisha. Tunasubiri kibali (no objection) kutoka Exim Bank na hivi karibuni tutapata, katika kuhakikisha tunatekeleza miradi hiyo na wananchi waendelee kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Jimbo la Njombe Mjini tuna vituo viwili vya afya ambavyo vimejengwa kwa nguvu za wananchi na mapato ya ndani. Vituo hivi vimetembelewa na Mawaziri karibu wote wa TAMISEMI. Nipende kuuliza; ni lini sasa vituo hivi ambavyo viko tayari kwa asilimia 100 vitapata vifaa na watumishi ili viweze kuanza kutoa huduma kwa wananchi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mwanyika kwa kuwasemea kwa ufasaha sana wananchi wa Jimbo la Njombe Mjini na kwa kweli hoja hii ameizungumza hapa zaidi ya mara mbili na sisi kama Serikali tumhakikishie tulishachukua hoja hii kwa ajili ya kupeleka vifaatiba kwenye vituo vile viwili vya afya, lakini pia kufanya mpango wa kupata watumishi pale na fedha tayari ziko MSD.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachosubiri ni manunuzi ya vifaatiba hivyo ili viweze kupelekwa kwenye Jimbo la Njombe Mjini. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili linafanyiwa kazi. Ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Naibu Spika, swali kwanza, kwa vile wananchi wachimbaji wa Njombe, kupitia chama chao cha wachimbaji kinaitwa WANANJO, walishafikisha kilio kwa Mheshimiwa Waziri na Waziri akatoa maelekezo kwa Katibu Mkuu kwamba, watafutiwe na watengewe maeneo kama inavyofanyika maeneo mengine katika nchi yetu. Na kwa vile mchakato huo ulishafanyika na RMO alishafikisha hayo mapendekezo ya maeneo wizarani.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali, ni lini sasa wananchi hawa watapewa hayo maeneo ambayo tayari yameshatambuliwa kwamba, ni muhimu kwa uchimbaji wa wachimbaji wadogo wa Njombe?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa, ameongelea kuwasaidia kwa kupitia training mbalimbali pamoja na mikopo. Wananchi, wachimbaji wale, hawana Habari na hiyo training ni kalenda ambayo Wizara wamejipangia. Naomba tupate uhakika na wao wasikie, ni lini mafunzo haya yatafanyika katika Mkoa wa Njombe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali madogo ya nyongeza ya Mheshimiwa Deodatus Mwanyika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa swali lake la kwanza ambapo anataka kujua kwamba, wachimbaji wadogo walioahidiwa maeneo ya kuchimba makaa ya mawe, na ninafahamu ni katika eneo la Ludewa, ni lini watapewa hayo maeneo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumhakikishia kwamba, taasisi yetu husika ambayo ni Tume ya Madini walishakwenda kupima maeneo hayo na mpaka sasa wameshapata kilometa za mraba 10.33 ambazo zinatosha kutoa leseni za wachimbaji wadogo 120. Na wanaendelea kutafuta maeneo ya ziada ili kuwapatia wachimbaji wote wadogo maeneo ya kuchimba kulingana na maombi yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa swali lake la pili, napenda kumhakikishia Mbunge, Ndugu yangu Mwanyika ambaye nampongeza sana kwa jinsi anavyowapambania wachimbaji wake wadogo kule katika jimbo lake ya kwamba, ratiba ilishapangwa. Taasisi yetu husika imeanza kuzunguka katika Kanda ya Ziwa tunavyoongea wanatoa mafunzo mbalimbali. Na mwaka huu wa fedha kabla haujaisha watakuja pia na Mbeya na GST nao wale wanaofanya mambo ya jiolojia watakuja kutoa semina katika mwaka ujao wa fedha ya jinsi ya kuchukua sampuli na jinsi ya kutambua maeneo yenye madini kwa ajili ya kunufaisha wachimbaji wadogo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi. Kijiji cha Uliwa kata ya Uhungilo kijiji ambacho kina shule, kina sekondari, kina zahanati lakini hakina mawasiliano kabisa ya aina yoyote, ni lini sasa Serikali itapeleka mawasiliano katika kijiji hicho cha Uliwa?
WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli maeneo aliyoyataja ni katika orodha tuliyowasilisha hapa Bungeni katika ile miradi 763 ya Tanzania ya kidijitali, maeneo aliyoyataja baadhi yake yamo na nimuahidi kwamba tutakapotangaza miradi hiyo basi ujenzi utaanza mara moja. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo kama Njombe ambayo ni Miji inayokua inauhitaji mkubwa sana wa makazi kwa sasa na maofisi. Ni lini, Shirika la Nyumba litakwenda kuanza mpango wa kujenga nyumba katika maeneo hayo ya Njombe?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, nipende kujibu swali la Mheshimiwa Deo, Mbunge wa Njombe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi National Housing inafanya mabadiliko makubwa sana ambayo yanakwenda kuanzisha ujenzi katika maeneo mengi sana ya nchi na hasa pembezoni mwa miji ambayo kwa kweli ilikuwa imesahaulika. Nikuombe tu Mheshimiwa Mbunge kwenye eneo lako hilo muweze kuandaa maeneo ambayo shirika litakapofika lipate ushirikiano wa kupata maeneo ya kujenga nyumba, ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiacha eneo la Liganga na Mchuchuma, eneo la Njombe kwa ujumla mpaka maeneo ya Mufindi hayajafanyiwa utafiti kabisa. Pamoja na kueleza kwamba, nchi nzima inafanyiwa utafiti ni lini sasa Serikali itaifanya GST ianze utafiti kwenye maeneo ya Njombe ambayo hayajafanyiwa utafiti?
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanyika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli katika Nyanda za Juu Kusini hasa Mikoa ya Ruvuma, Njombe na hususan kule Ludewa, kuna maeneo makubwa sana yenye madini ya chuma na madini ya makaa ya mawe. Wizara inaendelea kuchakata kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Uwekezaji utaratibu mzuri wa kuwapata wawekezaji wakubwa wa kuyachimba madini hayo, lakini pia, tuko katika hatua za mwisho kabisa za kubainisha maeneo ya kuwagawia wachimbaji wadogo ili madini hayo yaweze kuleta tija kwa Taifa letu na raia wake.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Mradi wa Igongwi ambao unahudumia Kata tatu Matola, Luponde na Uwemba tunashukuru Serikali kwa pale tulipofikia, lakini unasuasua sana. Mheshimiwa Waziri anatoa kauli gani kwa wananchi wa Njombe kuhusiana na mradi huo?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, natambua mradi ule ni wa kimkakati ambao utatoa huduma kwa watu wengi sana. Mwezi huu tumekwishapokea zile fedha na moja ya maeneo ambayo tunatakiwa tulipe ni mradi ule. Nataka nimhakikishie mwezi huu tutalipa mradi ule wa maji.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Makambako - Songea tunajua kipande cha Songea mpaka mpaka na Njombe tayari kimeishapata mpango wake. Lakini kutoka mpakani mwa Songea na Njombe mpaka Makambako Serikali ina mkakati gani kuhusiana na kipande hiki cha barabara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha kufanya matengenezo makubwa kwa barabara yote ya Makambako - Njombe hadi Songea. Kwa sasa kama alivyosema mpakani mwa Njombe na Ruvuma tayari tumeishapata fedha na Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kufanya matengenezo makubwa kwa kipande ambacho kimeharibika sana kati ya Makambako - Njombe hadi mpakani mwa Mkoa wa Ruvuma, ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona. Kwa kuwa kuwa barabara kuu ya Makambako – Songea inayopitia katika Mji wa Njombe imezidiwa na inahitaji ukarabati mkubwa: Je, ni lini barabara hii sasa itaanza kukarabatiwa au kujengwa upya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deodatus Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara aliyoitaja ambayo inaanza Makambako, Njombe hadi Songea ni kati ya barabara za zamani sana kujengwa miaka ya 1984. Tayari usanifu ulishakamilika na Serikali inaongea na Word Bank ili tuweze kupata fedha kwa ajili ya kuikarabati barabara hii. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali tayari ipo kwenye mchakato wa kuongea na hizi taasisi za kibenki kwa maana ya kifedha ili tukishafanikiwa basi ukarabati wa barabara hii uanze.
MHE. DEOGRATIUS P. MWANYIKA : Mheshimiwa Naibu spika, nashukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri. Pamoja na uwekezaji anaouongelea wa bilioni 13 changamoto kubwa ya reli ya TAZARA ni kwamba hata ukiwekeza hizo fedha, uendeshaji kibiashara ni tatizo. Sasa Serikali ina mpango gani wa muda mfupi ili reli hii iendeshwe kibiashara iondoe maroli mengi ambayo yako barabarani badala ya kutumia mzigo uende kwa treni?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tuliambiwa hapa na kulikuwa na ushauri wa Kamati ya Bajeti, kwamba mkataba wa uwekezaji wa Reli ya TAZARA ndilo moja ya tatizo kubwa sana linalotufanya tusiweze kuitengeneza reli hii vizuri. Sasa swali, Serikali ina mpango gani na imechukua hatua gani mpaka muda huu kurekebisha mkataba huo au kuu-terminate kabisa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. FREDY A. MWAKIBETE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa ujenzi na uchukuzi napenda kujibu Maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwanyika kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia suala hili la Reli ya TAZARA, pamoja na Wabunge wote wa Nyanda za Juu Kusini wamekuwa kila mara wakifuatilia jambo hili. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Nyanda za Juu Kusini, mpango wa muda mfupi ndio huo ambao tumetenga fedha kiasi cha Shilingi bilioni 13.1 na tutafanya manunuzi ambayo nimejibu kwenye jibu langu la Msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Mkataba, mkataba ama Sheria Namba 4 ya mwaka 1995 ya TAZARA ndiyo ambayo inakwamisha tusiendelee hasa katika uwekekezaji kama nchi. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Rais wa Zambia walipokutana walielekeza Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi tukutane na wenzetu wa Zambia. Mikutano hii imefanyika mwezi uliopita tarehe 14/10/2022 mpaka tarehe 15/11/2022 na mimi kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri nilimwakilisha Lusaka Zambia kwa ajili ya kujadili Sheria hii. Mwishoni mwa Desemba tutakutana tena ili tuihuishe halafu baadae tutaileta kwenye Mabunge yote mawili ya nchi ya zambia pamoja na nchi ya Tanzania ili sasa kila nchi ipate fursa ya kuwekeza upande wake.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwanja wa Njombe Mjini ni uwanja ambao wananchi wanauhitaji mkubwa sana wa usafiri wa anga, na kwenye ahadi ya Chama cha Mapinduzi umesemwa, Waziri Mkuu ameahidi.

Je, ni lini sasa uwanja huo utaanza ujenzi?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli uwanja wa Njombe unatakiwa ujengwe na tayari upembuzi yakinifu ulishafanyika. Serikali inatafuta fedha ili iweze kufanya usanifu wa kina wa uwanja huu ili uweze kujengwa hasa tukizingatia kwamba nguvu kubwa ya kiuchumi ya Mkoa wa Njombe, kwamba tunahitaji kuwa na uwanja kwa ajili ya ku-attract si tu wafanyabiashara, lakini pia tunajua ndiyo kuna uwekezaji mkubwa wa madini ya makaa ya mawe na chuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuna uhakika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha kufanya usanifu na hatimae kuujenga huo uwanja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maelezo aliyoyatoa Mheshimiwa Naibu Waziri, tumekaa hapa tunaongea lakini huko Halmashauri zetu wanatunga Sheria Ndogondogo ambazo zilizopo nyingi zinakwenda kupunguza attraction ya wawekezaji hasa wa ndani.

Je, ni mkakati gani wa sasa ambao Wazira inao kuhakikisha inaratibu zoezi hili ili liweze kuhakikisha kwamba Wawekezaji hasa wa ndani wanaweza wakafanya kazi bila ya kuwa na Sheria Ndogondogo hasa za tozo?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Napenda kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli moja ya changamoto tulizonazo kwenye utekelezaji wa mradi wa blueprint au MKUMBI ni katika ngazi za Halmashauri. Wizara tumeshaanza kuliona hilo na moja ya utekelezaji tumeanzisha madawati au kitengo mahususi kinachoshughulikia masuala ya viwanda, biashara na uwekezaji katika ngazi ya Halmashauri. Tunaamini kitengo hiki kitasaidia moja, kuhakikisha tunaharakisha utekeklezaji wa yale maboresho ambayo tumeyafanya, lakini pili kuwaelimisha wenzetu wa Halmashauri ili wawe wanatunga Sheria au Kanuni ambazo si kinzani na nia hii ya Serikali ya kuboresha mazingira ya uwekezaji na ufanyaji biashara hapa nchini. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru saba kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa mikoa ambayo inategemea sana uchumi wa misitu; mikoa ya nyanda za juu Kusini na hasa Mkoa wa Njombe, wananchi wamepata umasikini mkubwa sana kutokana na moto ambao unatokea mwaka baada ya mwaka. Serikali ina mpango gani wa kuwa na mkakati wa kusaidia kwa kuleta vifaa vya kisasa kwenye maeneo hayo ambayo yanashambuliwa sana na moto?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli anayoyasema hutokea kwenye mikoa na wilaya nyingi zenye misitu. Kwa kutambua hilo ndiyo maana Mkoa wa Njombe hadi sasa wanayo magari mawili, moja liko Njombe Mjini na lingine liko Makambako. Ni dhamira ya Serikali kadiri uwezo wetu utakavyoongezeka wa kununua magari ya kuzimia moto, Mkoa wa Njombe pia utazingatiwa.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi; zao la chai linahitaji sana umwagiliaji, ni lini Serikali italeta hizo scheme kwenye maeneo ya Igominyi, Tarafa ya Igominyi kwa ajili ya umwagiliaji wa chai?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nimepokea swali la Mheshimiwa Mbunge, tutawaelekeza wenzetu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji kuyapitia maeneo hayo ili kama kuna uwezekano na maeneo hayo yanaruhusu kuweka skimu hizo tuweze kuifanya kazi hiyo kwa uharaka.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona niulize swali dogo la nyongeza. Pamoja na kugawa mbegu bure ambapo tunashukuru, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba wananchi hasa wakulima wadogo wadogo wanapata utaalam hasa kwenye maeneo ya dawa na magonjwa yanayoshambulia zao hili la parachichi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deodatus Mwanyika kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema pale awali katika majibu yangu ya msingi, zao la parachichi ambalo ni dhahabu ya kijani tunalipa kipaumbele kikubwa na tunakuja na mkakati madhubuti wa kuhakikisha tunawasaidia wakulima wetu kuanzia huduma za ugani mpaka upatikanaji wa pembejeo na waweze kuzalisha kwa tija. Nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba ni zao ambalo tunalipa kipaumbele na tutahakikisha kwamba wakulima wetu wanapata elimu ya kutosha na kanuni bora za kilimo ili waweze kulima kwa tija. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya udharura na kwa ruksa yako naomba kwanza niwape pole wananchi wa Njombe kwa ajali kubwa iliyotokea na iliyouwa watu nane siku ya juzi.

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza, kwa kuwa suala la gharama na hasa zao la Parachichi lina ushindani mkubwa sana kwenye soko, na suala la gharama ni suala la muhimu sana kuzingatiwa kwa maana ya kupunguza gharama hizo.

Je, Serikali itatuhakikishiaje kwamba mamlaka hii inayoenda kuundwa haitaongeza gharama kwa wakulima wadogo kwa kupitia tozo na gharama za uendeshaji?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Je, ni lini sasa hayo mabadiliko yatafanyika kwa kuletwa Muswada hapa ndani. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwajika Mbunge wa Njombe Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba inakuza tasnia hii ya mazao ya mbogomboga na mazao ya bustani na hivyo moja kati ya maeneo makubwa ambayo tutayasimamia ni kuhakikisha kwamba mkulima hapati changamoto kubwa ya tozo nyingi ambazo zitamfanya akate tamaa ya kilimo chake.

Mheshimiwa Spika, nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ya kwamba Serikali katika uanzishwaji wa mamlaka hii itahakikisha kwamba inalinda maslahi ya mkulima na mkulima anufaike na kilimo chake.

Mheshimiwa Spika, pili kuhusu ni lini tutaleta mabadiliko haya ya sheria, mchakato umeshaanza ndani ya Wizara ya kuanza kupitia marekebisho haya ya sheria na pindi itakapokamilika kwa mujibu wa taratibu za Bunge utawasilishwa hapa Bungeni kwa ajili ya majadiliano na kupitishwa.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Jimbo la Njombe limekuwa na vituo vitatu vimekamilika muda mrefu sana; na huu mgao wa equal unatupa wasiwasi kwa vile vituo ambavyo vinangojea magari na vimeahidiwa miaka zaidi minne: Je, Serikali itatusaidia kwenye hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tunahitaji vituo vyetu viwe na magari ya wagonjwa kila kituo kiwe na gari la wagonjwa. Safari ni hatua. Kwa sasa tunaanza na vituo vile vya kimkakati, lakini mara nyingi uzoefu unaonesha vituo vya afya vingine vinaweza vikawa saved na magari ya wagonjwa yaliyo katika Hospitali za Halmashauri au katika vituo vya afya vya jirani. Kwa hiyo, tutaendelea kuangalia umbali wa kituo cha afya kutoka hospitali na pia population ambayo ina- save ili kuhakikisha kwamba tunapeleka magari katika vituo hivyo. Ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Njombe Mjini, Kata ya Lugenge, Kata kubwa watu wengi iko karibu kabisa na Mjini mpaka leo hakuna umeme hata Kijiji kimoja.

Ni lini sasa Serikali itapeleka umeme kwenye Kata hiyo ya Lugenge?
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deodatus Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeingiza vijiji vyote vilivyobakia katika nchi hii katika mradi wa REA awamu ya tatu na mzunguko wa pili ulioanza kutekelezwa mwezi Aprili mwaka jana. Kata hii ipo katika mpango huo na itapata umeme na mradi huo kukamilika kabla ya Desemba 2022.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi fupi kuuliza swali la nyongeza. Mifumo ambayo ni effective ni ile ambayo inatatua matatizo ya wawekezaji kwa muda na kwa haraka.

Mheshimiwa Spika, hii blue print tumeisikia muda mrefu sana. Ni lini hasa itatoka au ni document nyeti? Tunaomba kauli ya Serikali kwenye hilo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema blue print ni mfumo ambao unashughulikia au kurahisisha ufanyaji biashara hapa nchini. Tumeshaanza utekelezaji wake, hoja ya Mheshimiwa Mwanyika ni kwamba tayari kuna kero mbalimbali. Mwanzoni mpaka mwaka 2020 tulikuwa tumeondoa kero 232 lakini sasa tumeshafika 280. Lakini zaidi tumeshaanzisha mifumo ya kielektroniki ambayo inasomana kupunguza kero mbalimbali ambazo zilikuwa zimeainishwa katika matrix ile kwenye blue print.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea kutekeleza hatua kwa hatua. Ninyi ni mashahidi kwamba sasa tumepunguza baadhi ya kero ile ya kupanga foleni kwenda kulipa kwa mfano katika taasisi mbalimbali tunatumia kielektroniki lakini pia moja ya changamoto kubwa ambazo tulikuwa tunazishughulikia ni miundombinu wezeshi ambayo Serikari ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan tunatekeleza barabara na miundombinu mingine ambayo tunaamini hiyo itaongeza ufanisi katika ufanyaji biashara na uwekezaji hapa nchini.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa wananchi wa Njombe walishakamilisha ujenzi wa vituo vya afya viwili kwenye Kata mbili, Kata ya Mamangolo na Kata ya Kifanya; na tumekuwa tukiomba sana hapa. Nini kauli ya Serikali kuhusu kutoa vifaa tiba kwenye hospitali ili mama mtoto aweze kupata huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deodatus Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, baada ya ukamilishaji wa vituo hivyo kinachofuatia ni kutafuta vifaa tiba na ambavyo vipo katika mpango. Kwa hiyo, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tunanunua vifaa tiba kwa ajili ya vituo vya afya ambavyo vimeshakamilika. Vitakapokuwa vimepatikana tutavipeleka pale kwa wananchi, ahsante sana.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Barabara ya Makambo – Songea barabara kubwa ya kiuchumi ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza na Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii tayari imeshapata fedha kutoka World Bank ambapo tutaanzia mbele ya Njombe kuelekea Songea na kipande cha Njombe kuja Makambako Serikali inaendelea kutafuta fedha. Kwa hiyo sasa hivi tuko kwenye maandalizi ya kuanza kuitangaza ili ianze kujengwa kwa maana ya kukarabatiwa upya total rehabilitations, ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali ambayo ni majibu ya kawaida (generic answers). Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, Mkoa wa Njombe na Halmashauri ya Mji wa Njombe ndiyo ina uzalishaji mkubwa sana wa zao la parachichi. Kwa bahati mbaya sana uzalishaji huo ni mkubwa lakini asilimia 90 mpaka 99 ya mazao ya matunda ya parachichi yote yanasafirishwa nje bila kuongezwa thamani kwa maana halisi ya uongezaji wa thamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali langu; Mheshimiwa Waziri anaweza kutoa commitment hapa leo kwamba watachukua suala la Mji wa Njombe na Mkoa wa Njombe kama special case ili waweze kuanzisha maeneo maalum kwa ajili ya uzalishaji na uchakataji wa parachichi tuache kupeleka maparachichi zikiwa ghafi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kama ataitoa commitment hiyo na atakubaliana nami na sioni kwa nini asikubaliane nami. Je, kuonesha umuhimu wa suala hilo, Waziri yuko tayari twende pamoja Njombe baada ya kusoma bajeti yake ili tukaanze majadiliano ya awali ya kuanzisha mchakato huo wa kuanzisha viwanda vya kuchakata parachichi badala ya kusafisha, kupaki na kusafirisha ambayo inatupotezea sisi mapato? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA:
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli moja ya vigezo ambavyo vinatakiwa kwa ajili ya kuanzishwa maeneo ya uwekezaji kwa ajili ya kuzalisha bidhaa kuuza nje (Special Economic Zones) ni uwepo wa malighafi; pili ni uwepo wa ardhi; zaidi ni miundombinu wezeshi kwa ajili ya kuzalisha bidhaa hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe commitment ya Serikali na niwaagize Mamlaka ya EPZA waanze mchakato mara moja wa kuwasiliana na Mkoa wa Njombe, na kutafuta wadau wengine. Kwa sababu katika maeneo haya ya uwekezaji kwa ajili ya mauzo nje tunashirikiana pia na sekta binafsi ili kuhakikisha mkoa huu sasa unakuwa na eneo kwa ajili ya kuzalisha bidhaa au kuzalisha maparachichi ambayo yatauzwa nje ikiwa ni bidhaa zake au maparachichi yenyewe ili kuongeza uchumi wa Mkoa wa Njombe na azma ya kupunguza kuuza malighafi nje, yakiwemo na maparachichi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya commitment hiyo na EPZA wataanza kufuatilia, na mimi nikubaliane naye, nitakwenda Mkoa wa Njombe ili tuweze kuona namna ya kujadiliana na wadau ukiwemo mkoa, kupata ardhi na wadau wengine kwa ajili ya kuwekeza au kuanzisha maeneo huru ya uwekezaji katika Mkoa huo wa Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kituo cha Njombe Mjini ni kituo kongwe katikati ya Mji, kimekuwa na ahadi za muda mrefu: Ni lini sasa kituo hiki kitapanuliwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Njombe Mjini ni kikongwe na ni chakavu, na pia kina miundombinu michache na Serikali imeshafanya tathmini ya uhitaji wa majengo ya ziada na kazi inayoendelea sasa ni kutafuta fedha ili fedha ikipatikana tukaongeze majengo yale na kukiwezesha kile kituo cha afya kufanya kazi inayotarajiwa, ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kunipa nafasi. Mkoa wa Njombe una majanga makubwa sana upande wa misitu, na misitu ndio uchumi. Anaweza kutoa kauli ya Serikali kuhusiana na kutoa kipaumbele kwa mkoa huu muhimu na Mji wa Njombe? (Makofi)
NAIB WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nimuahidi kwamba itaendelea kutoa kipaumbele kama ambavyo sasa hivi ina gari mbili, moja iko Njombe Mjini nyingine liko Makambako.

Tutaendelea kuimarisha utoaji wa gari hizi ili hatimaye kua- address matatizo ya majanga yakijitokeza katika mkoa huo, nashukuru.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kituo cha Polisi katika Mji wa Njombe ni kichakavu sana na cha zamani. Je, ni lini ujenzi wa Kituo kipya cha Polisi utaanza?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara kupitia Jeshi la Polisi itaanza na kazi ya kufanya tathmini ya kiwango cha uchakavu wa majengo ya Kituo cha Polisi ngazi ya Wilaya cha Njombe. Iwapo itathibitika kwamba gharama za ukarabati zitakaribia kulingana na gharama za ujenzi wa kituo kipya, uamuzi utafanyika kwa ajili ya kujenga kituo kipya, lakini kama gharama zitakuwa manageable tutakikarabati kituo hicho ili kiweze kuwa cha kisasa zaidi, nashukuru.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, pamoja na majibu ambayo ni mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, tatizo la kiwanda siyo tu wanahisa, tatizo la kiwanda ni deni la Benki yetu ya Kilimo.

Swali la kwanza, je, Waziri haoni haja sasa ya kuhakikisha kwamba anaratibu majadiliano akishirikisha Wizara ya Mifugo ambayo ndiyo inasimamia sekta hiyo kwa haraka sana? (Makofi)

Swali la pili, anawahakikishiaje Wananjombe na wafugaji wa Njombe kwamba majadiliano hayo sasa yatafanyika kwa haraka katika kipindi hiki cha Bunge au mara tu baada ya kuisha Bunge hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA:
Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kama nilivyosema nia ya Serikali ni kuona kiwanda hiki kinafanya kazi na kwa taarifa tu kwa sababu ya umuhimu wake Wizara wenye dhamana ya kuhakikisha maendeleo ya viwanda nchini yanafanikiwa na kuwa na tija, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutaratibu majadiliano ya wanahisa kwa maana ya NJOLIFA, Njombe Wilaya, Njombe Mji, Roman Catholic ambao nao wanahisa na wengine. Muhimu zaidi kama nilivyosema moja ya sababu iliyopelekea kukwama kiwanda hiki ni mtaji ambao sasa kupitia Benki ya Kilimo (TADB) ilitoa zaidi ya shilingi bilioni 1.6. Sasa tutaandaa kikao, tutawaita kabla ya kuisha Bunge hili ili wanahisa wote na wenzetu wa TADB tuje tukae hapa, tuone namna gani tunakwamua mkwamo wa kiwanda hiki ili kiendelee kuzalisha kwa tija lakini pia kupata manufaa kwa nchi katika sekta ya viwanda.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Mkoa wa Njombe ndio Mkoa ambao hauna chuo kikuu wala chuo cha juu na Mheshimiwa Rais alipotembelea Mkoa wa Njombe tarehe 9 Agosti, 2022 alipokea ombi la wazee wa Njombe kuhusu kujengewa chuo kikuu katika Mkoa wa Njombe na Mji wa Njombe. Je, Serikali itaanza lini mchakato wa kuhakikisha kwamba na sisi tunapata chuo kikuu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni kweli Mheshimiwa Rais alifanya ziara katika Mkoa wa Njombe, tarehe 9 Agosti, 2022 na miongoni mwa ahadi alizozitoa ni ujenzi wa kampasi mojawapo ya chuo kikuu pale Njombe, ingawa katika mgawanyo huu wa miradi ya HEET katika mikoa ambayo haitapata fursa katika awamu hii ya kwanza ni Mkoa wa Njombe. Kwa vile tayari Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, alishatoa hiyo ahadi na sisi kama Serikali ahadi hii ya Mheshimiwa Rais tunaendelea kuifanyia kazi, hivyo, nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mwanyika na wananchi wa Mkoa wa Njombe, tuko njiani kuja Njombe na tutahakikisha kwamba, tunaleta taasisi ya elimu ya juu katika Mkoa wa Njombe.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu aliyoyatoa, naomba kuuliza swali kwamba, Jimbo la Njombe Mjini ambalo ndiyo Halmashauri kubwa kuliko Halmashauri zote katika nchi hii; je, litaangaliwa kwa namna ya kipekee katika hiyo tathmini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, Njombe Mjini na maeneo mengine yote ya nchi yetu ya Tanzania ambayo Waheshimiwa Wabunge mnatokea, yataangaliwa kwa vigezo vile vile ambavyo nimevitaja hapa. Ukubwa au urefu wa barabara katika wilaya husika, kuangalia ukubwa wa eneo husika, kuangalia milima, kuangalia wingi wa mvua, kuangalia shughuli za kiuchumi kama kilimo…

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa ameshakuelewa.

MHE: DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la watumishi linaendana na vifaa tiba. Njombe tuna vituo vya afya viwili vimejegwa kwa nguvu za wananchi na mapato ya ndani. Watumishi wameshapelekwa tunashukuru Serikali, lakini watumishi hao sasa ni kama hawana kazi kwa sababu vifaa tiba havijapelekwa.

Sasa swali langu, Serikali haioni ni busara kuhakikisha kwamba pale ambapo watumishi wamepelekwa, lakini vifaa tiba havijaenda basi wakafanya haraka kupeleka vifaa tiba ili watumishi hao sasa wafanye kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanyika la vifaa tiba, kwanza nichukue nafasi hii kuwapongeza sana wananchi wa Jimbo la Njombe kwa kujenga kwa nguvu zao wenyewe vituo hivi vya afya na vilevile Halmashauri ya Mji kwa kujenga pia kwa kupitia mapato yao ya ndani na hili ndio tunatamani kuliona kila Halmashauri ikitenga fedha kwa ajili ya kujenga miundombinu ya kusaidia wananchi katika sekta ya afya na sekta ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa suala la vifaa tiba ni kipaumbele cha Serikali hii ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha vifaa tiba vya kisasa vinakwenda katika maeneo yote nchini ikiwemo kule Wilayani Njombe na tutakaa na Mheshimiwa Mbunge na kuangalia kwenye bajeti iliyotengwa ni kiasi gani kimetengwa kwa jaili ya vifaa tiba na hiyo fedha iliyokuwepo basi vifaa tiba hivyo viweze kupataikana mara moja.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Skimu za umwagiliaji wa maeneo ya chai kwenye Tarafa ya Igominyi katika Jimbo la Njombe Mjini: Nini kauli ya Serikali kuhusu utekelezaji katika kipindi hichi cha bajeti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA (K.n.y. WAZIRI WA KILIMO): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Skimu ya Igominyi na maeneo mengine kama alivyosema, ni skimu muhimu sana kwa ajili ya kuhakikisha kilimo cha chai kinaendelea kuchangia katika uchumi wa nchi. Ni nia ya Serikali kuona skimu zote ambazo ziko kwenye mpango wake zinatekelezwa. Kwa hiyo, fedha zitaendelea kupelekwa katika maeneo ambayo yamepangwa kulingana na mpango wa fedha katika mwaka wa fedha huu wa 2023/2024, nakushukuru. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Hospitali ya Rufaa Njombe, tunaishukuru Serikali kwanza kwa kuleta vifaa tiba na kuweza kuiboresha, lakini bado wananchi katika Mkoa wa Njombe wana matatizo makubwa sana ya uhitaji wa kusafishwa damu na bado inawabidi wasafiri: Ni lini Serikali italeta mashine ya kusaidia kusafisha damu kwa wagonjwa wa figo katika Hospitari ya Rufaa ya Njombe?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimemsikiliza, kama vile anasema suala la upatikanaji wa damu, lakini nilichomwelewa anamaanisha kusafisha figo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeagiza hospitali zote za mikoa, na vifaa vipo kwa ajili ya kuweka majengo ya kusafisha damu. Kwa sababu hospitali yetu ni mpya, namwomba Mheshimiwa Mbunge tufanye mawasiliano tujue jengo kwa ajili ya kusafisha damu, kwa maana ya kutibu wagonjwa wa figo, lipo kwenye hatua gani ya ujenzi ili vifaa viweze kwenda kwa ajili ya kutatua tatizo hilo.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, pamoja na maelezo aliyoyatoa sasa hivi, kulikuwa na ahadi ya Serikali kwamba majimbo yale ya mjini, ambayo yana mjini na vijijini yatapewa bajeti kubwa zaidi upande wa TARURA. Nini kauli ya Serikali kuhusu kutekeleza azma hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli ilikuwa ni ahadi ya Serikali na niseme ahadi hiyo imeanza kutekelezwa. Kwa maana ya Manispaa na miji ambayo ina hali ya miji lakini pia vijijini, Serikali imeendelea kuongeza bajeti kuwezesha barabara za vijijini zijengwe vizuri, pia na barabara za mijini zijengwe vizuri.

Mheshimiwa Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge likiwepo Jimbo la Njombe Mjini, tutahakikisha tunaendelea kuboresha utaratibu huu, ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, katika Mji wa Njombe tuna Kituo cha Polisi ambacho hakina hadhi ya makao makuu ya mkoa; je, ni lini kituo chenye hadhi ya mkoa kitajengwa katika Halmashauri ya Mji wa Njombe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba mikoa yote ambayo haina vituo vya ngazi ya mkoa, vinajengewa vituo hivyo. Tumeanza kwa awamu katika maeneo mengine na Njombe ni eneo lingine ambalo litapewa kipaumbele katika mwaka ujao wa fedha, kuanza kujenga Kituo cha Polisi ngazi ya mkoa, nashukuru. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza. La kwanza kwa kuwa kuna uhaba mkubwa sana wa ardhi maeneo ya Kata ya Luponde ambako ndiko shamba kubwa hilo lipo na mashamba makubwa ya chai yako kule, na vijana ni wengi sana ambao wanauhitaji wa ardhi;

Je, kwa nini Serikali isifikirie ndani ya eneo hili ikagawa sehemu kuwapa vijana katika mpango wa BBR au BBT?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kituo cha utafiti cha Igeri ambacho ndicho kimekuwa na shamba hili kwa muda mrefu sana kimekuwa dormant kwa miaka mingi sana hakujakuwa na uwekezaji, na vile vile kituo kidogo cha Ichenga ambacho ni cha utafiti eneo hilo hilo na chenyewe cha matunda kimekuwa dormant na hakina fedha na hakifanyi shughuli yoyote wakati tuna zao la parachichi ambalo linahitaji sana utafiti;

Je, Serikali ina mpango gani kutoa fedha za kutosha kwenye vituo hivi vya utafiti?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza kuhusu vijana na ushiriki wa vijana kwenye kilimo. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ya kwamba ni dhamira ya Serikali kuhakikisha vijana wengi zaidi wanashiriki kwenye kilim,o na ndio maana tumekuja na programu ya BBT. Na kwa kuwa kuna changamoto ya ardhi kama alivyosema, mimi nitaandaa safari kwenda jimboni kwake Mheshimiwa Mbunge tukakae na uongozi wa wilaya kwa pamoja tutafute namna bora ya kuweza kuwawezesha vijana hao washiriki kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili la kuhusiana na kituo hiki cha utafiti. Kama nilivyosema katika majibu yangu ya msingi, mwaka wa fedha unaokuja wa 2023/2024 tumetenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunalima eneo lote kwa ajili ya kutayarisha mbegu zile ambazo ni pre-basic seeds na basic seeds ili baadaye tusaidie kwa ajili ya kuzisambaza, hasa kwenye zao la ngano na zao la pareto. Kwa hiyo nimwondoe hofu Mheshimiwa Mbunge ya kwamba hatujakitelekeza, tumeshakitengea fedha, kitaanza kuwa operational kuanzia mwaka wa fedha ujao.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi;

Je, ni nini mkakati wa Serikali kuanzisha miradi ya umwagiliaji kwenye maeneo ya wakulima wadogo wadogo wa chai eneo la Igomini Tarafa ya Igomini Halmashauri ya Njombe?

NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, nataka kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hii ni hoja ambayo Mheshimiwa Mbunge alishaifikisha katika Wizara ya Kilimo na tumemuahidi baada ya Bunge hili la bajeti namwelekeza Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Taifa ya Umwagiliaji ndugu yangu Raymond Mndolwa waongozane na Mheshimiwa Mbunge kwenda kufanya tathmini katika maeneo yaliyotajwa ili tuweze kuwasaidia wakulima wa chai katika eneo hilo.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali. Napenda kusema tunashukuru sana Serikali hata kwa hicho cha kuanza na ukarabati wa barabara kutoka Songea mpaka Lutukila. Hata hivyo ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, barabara hii ni mbaya sana, ni barabara kubwa ya kiuchumi na kuna shughuli nyingi sana sasa hivi. Sasa Serikali, wakati fedha zinatafutwa, hawaoni kwamba kuna umuhimu wa angalau kutenga fedha za kutosha ili maeneo ambayo ni hatarishi kwa magari mengi ya mkaa yaweze kuanza kushughulikiwa kwenye kona kali na miteremko?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Barabara hii ilifanyiwa redesign 2012, wakati huo Njombe haikuwa mkoa. Mji wa Njombe ambapo barabara hiyo inapita umebadilika, unakua kwa kasi, umekuwa na activities nyingi. Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza kutoa maelekezo kwamba sasa wafanye redesign pale katikati ya mji kutoka Kibena mpaka kufika Nundu ili paendane na uhalisia wa Mji wa Njombe ambao unaenda kuwa Manispaa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni utaratibu ambao umezoeleka kwamba katika hizi barabara kubwa, na hasa barabara aliyoitaja ni ya zamani, tumeendelea na tutaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kufanya ukarabati maeneo yale yote ambayo yanakuwa yamechakaa sana ili kuhakikisha kwamba wanaosafiri na wasafirishaji hawapati changamoto. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi huo Mheshimiwa Mbunge, Serikali itaendelea kukarabati yale maeneo yote korofi katika hiyo barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, ni kweli kama alivyosema, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Njombe ni mji unaokua sana kama mji na unapitisha magari mengi makubwa. Sisi kama Wizara tunataka tumhakikishie kwamba tutafanya redesign. Itakuwa ni dual carriageway katika Mji wa Njombe kuanzia Kibena Hospitali hadi Hagafilo na zitakuwa ni njia nne ili kuhakikisha kwamba hakutokei changamoto ya msongamano katika Mji wa Njombe, ahsante. (Makofi)
MHE DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Jimbo la Njombe Mjini pamoja na kwamba linaonekana ni jimbo la mjini, uhalisia ni kwamba lina vijiji vingi sana ambavyo bado havina huduma ya maji kama Uliwa, Ihanga, Mikongo, Liwengi na Mtira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawajaingizwa katika mpango mkubwa wa maji wa P4R. Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba na vijiji hivi vinapata huduma hii ya maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika Mbunge wa Njombe Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yote haya aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge ni kweli. Mheshimiwa Mbunge nikupongeze hili mimi na wewe tumeshalijadili na tayari tumeanza kulifatilia. Maeneo ambayo hayata nufaika na mradi wa P4R ambao tunautekeleza kwa kutimiza vigezo vya masharti ya namna ambavyo unatekelezeka yatafanyiwa huduma kwa kupitia fedha za mfuko wa maji lakini vile vile fedha nyingine ambazo tunazipata kwenye namna nyingine ya upatikanaji wa fedha ndani ya Wizara.

Mheshimiwa Mbunge, nikuondoe hofu, kwa maeneo ambayo P4R haitafika haimaanishi hatutaweza kutekeleza miradi. Tutatekeleza miradi na wananchi watapata maji safi na salama ya kutosha na wote wataendelea kunufaika na kutuliwa ndoo kichwani.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Mji wa Njombe kwa sababu ya wingi wa malori unahitaji kuwa na bypass. Je, ni lini Serikali itaanza kufanya bypass kutoka Kibena kwenda mpaka Yakobi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tulishatoa maelezo hapa kwamba tuna mambo mawili tutafanya. Moja, kuanzia hapo Kibena tunategemea kujenga barabara za njia nne kwa ajili ya kupunguza msongamano, lakini pia sasa hivi Meneja wa Mkoa kulingana na ukuaji wa Mji wa Njombe wameanza kufanya study ya kuona wapi barabara ya bypass itapita na hasa tukizingatia kwamba Mji wa Njombe umekua, kwa hiyo wanaangalia maeneo ambayo hawataingia gharama kubwa ya kutoa fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sasa hivi wako wanatembea, baada ya hapo sasa wataweka hiyo ramani kwenye maandishi kwa ajili ya kuiombea fedha kuanza hiyo kazi ya kutengeneza hiyo bypass, ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Njombe, ni miaka 10 toka umeanzishwa na mpaka leo hatuna Kituo cha Polisi kinachoendana na hadhi ya mkoa? Ni lini sasa kituo hicho cha Polisi kitajengwa katika Mji wa Njombe?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanyika, Mbunge kutoka Njombe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyokwishasema, tunatambua mikoa mipya iliyoanza kwenye miaka ya 2012 ukiwemo Mkoa wa Njombe, hauna kituo kikuu cha Polisi kwa maana Ofisi ya RPC. Kwa kweli Mkoa wa Njombe tayari uko kwenye mpango na Mheshimiwa Mbunge anajua. Katika vipaumbele ambavyo mwaka huu tunaendelea navyo, ni ujenzi wa ofisi ya RPC Njombe. Nadhani baada ya Bunge hili tutatembelea maeneo hayo kuona maandalizi na harakati za ujenzi zinavyoendelea Meshimiwa Mwanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Magari yanayotumika kuwapeleka mahabusu na wafungwa mahakamani kwenda na kurudi yana uchakavu mkubwa sana. Ni lini sasa Serikali itafanya utaratibu wa kubadilisha magari hayo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba ni kweli kwamba magari katika maeneo mengi yamechakaa na kama mtakumbuka tumesema mwaka huu kuna bajeti imeongezeka haitaweza kutatua matatizo yote ya uchakavu wa magari ya mahabusu lakini at least tutaanza kununua kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, siku za karibuni kumekuwa na taarifa ambazo zimekuwa zikitapakaa kwenye mitandao pamoja na picha zikionesha kwamba parachichi ya Tanzania haikidhi viwango, jambo ambalo siyo kweli. Nini kauli ya Serikali kuhusiana na suala hili? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwahakikishie Watanzania na niwahakikishie wateja wote wanaonunua parachichi za Tanzania kuwa parachichi za Tanzania zinakidhi vigezo vya kimataifa na ndiyo maana tumekuwa sasa hivi tukifungua masoko mapya na hivi karibuni tumefungua soko la India, na ni Tanzania pekee ambayo imepata import duty exemption ya parachichi yake katika soko la India, hili ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili; tunazo international certification institutions ndani ya nchi yetu. Kwa hiyo, parachichi yetu inapotoka nje ya mipaka inakuwa na certifications za kimataifa zote ambazo zinakubalika katika soko la dunia. Kumekuwa na tatizo la competitors wetu na mimi nataka niwaombe exporters wa Tanzania wahakikishe wanapo-export parachichi ya Tanzania inaondoka na trademark iliyoandika Produce of Tanzania ili kuweza kui-protect image ya parachichi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushindani upo, watu watataka ku-distort image yetu. Niwaombe Watanzania, yeyote anayepata taarifa yenye mashaka kuhusu product ya Tanzania awasiliane na Wizara ya Kilimo na sisi tutakuwa tayari kui-protect bidhaa yetu popote pale.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu aliyoyatoa, nina maswali mawili ya nyongeza.

Ningependa nimwambie Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba kule Njombe tuna Kiwanda cha Maziwa ambacho kimefungwa kwa muda mrefu na kiwanda kile kina wadau mbalimbali ambao wanahusika na kina changamoto nyingi sana.

Swali la kwanza je, Mheshimiwa Waziri anaweza kuniambia Wizara hii ambayo kazi yake ni uratibu; je, anaweza sasa kuchukua hilo jukumu la kufanya uratibu ili wadau mbalimbali wa kiwanda kile waweze kukutana na kutatua hizo changamoto?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Waziri au Naibu Waziri anaweza kutoa commitment hapa sasa kwamba yeye pamoja na hao wadau watakuja Njombe ili kukaa na wakulima ambao wanaumia sana kutokana na kiwanda kile kutokufanyakazi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deodatus Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Deodatus Mwanyika kwa kufuatilia sana kuhusiana na viwanda katika Mkoa wa Njomba na hasa Kiwanda hiki cha Maziwa ambacho muda mwingi anafuatilia.

Mheshimiwa Spika, ni kweli viwanda vingi havifanyikazi kutokana na changamoto mbalimbali na Serikali kama nilivyosema kupitia mpango wa kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara tunapitia mojawapo ni kuhakikisha tunatatua changamoto zinazokabili viwanda hivyo, ikiwemo kiwanda hiki cha maziwa cha Njombe; tutafanya tathmini tuone nini changamoto zilizowasibu mpaka kisiwe kinafanyakazi hivi sasa na hatimaye Serikali tutachukua hatua.

Mheshimiwa Spika, la pili; kwa sababu kweli kiwanda kinahusisha sekta tatu kwa maana ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara lakini tutashirikiana na wenzetu Wizara ya Kilimo, lakini Mifugo na Uvuvi ili tuweze kukitembelea kama nilivyosema kubaini changamoto ambazo zinazikabili kiwanda hiki ambacho kama anavyosema Mheshimiwa Mbunge hakifanyikazi. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi na mimi kuuliza swali dogo la nyongeza.

Katika Jimbo la Njombe Mjini kumekuwa na ahadi ya muda mrefu ya kupanua Kituo cha Afya cha Njombe Mjini kwa sababu hakina wodi za wanaume. Ni lini sasa Serikali itatekeleza ahadi hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deodatus Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Njombe Mjini ni moja ya vituo ambavyo Serikali tayari imeanza kufanya tathmini ya majengo ambayo yatahitajika ili utanuzi uweze kufanyika na kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi hiyo itafanyika na tunatafuta fedha kwa ajili ya kupanua Kituo cha Afya cha Njombe.