Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Festo Richard Sanga (71 total)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Makete naomba kuuliza kuhusu ujenzi wa barabara ambayo ipo kwenye Ilani ya kutoka Chimala – Matamba – Kitulo kilometa 51, ilikuwa ni ahadi ya Waziri Mkuu mstaafu, kwa muda wa miaka 10 hadi sasa haijatekelezwa. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayoizungumzia Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete ni kati ya barabara ambazo zimetajwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi kuanzia ukurasa wa 72 – 76. Pia katika kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Rais ameeleza kwamba katika kipindi cha utekelezaji wa Ilani hii pamoja na ahadi alizozitoa atahakikisha kwamba anajenga na kukamilisha barabara zote ambazo zinaendelea zenye urefu wa kilometa 2,500 lakini pia ataanza ujenzi na kukamilisha barabara zenye urefu wa kilometa 6,006 na barabara hii ya Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete ni kati ya barabara ambazo zimetajwa ama zimetolewa ahadi na mwenyewe Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, nimpe uhakika kwamba barabara hiyo itajengwa na kukamilika.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Majibu ya Serikali hayajaniridhisha kwa sababu wananchi wetu kwenye zoezi hili la kuweka beacon walishirikishwa kuweka beacon tu, hawakushirikishwa kwenye mipaka itawekwa maeneo gani.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari baada ya Bunge hili tuongozane kwenda Makete tukawape majibu wananchi wetu na kurudia zoezi la kuweka beacon? Kwa sababu zoezi hili limesababisha wananchi wangu wengi saa hizi wako ndani lakini sehemu ya shule zimewekwa beacon…

SPIKA: Mheshimiwa Festo…

MHE. FESTO R. SANGA: Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari twende wote?

SPIKA: Nisikilize kwanza; swali lako halijaeleweka kabisa, kwamba wananchi wako wlaishirikishwa kuweka beacon lakini hawakushirikishwa mahali pa kuweka, sasa…

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, kilichotokea wananchi wamefika wamekuta watu wa kutoka Serikalini wanaweka beacon, hawajaambiwa kwamba ni eneo hili la mpaka au wapi. Kilichotokea nyumba nyingi za wananchi ziko ndani ya hifadhi, kitu ambacho hakikuwepo, siku za nyuma mipaka ilikuwa mbali. Leo hii wananchi wangu wengi wako ndani ni kwa sababu ya hilo jambo. Sasa ninachomuomba Naibu Waziri tuongozane baada ya hili Bunge twende Makete akawape wajibu wananchi wetu turudie zoezi; hicho ndicho ninachomwomba. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara iko tayari kuhudumia wateja wa aina yoyote akiwemo Mheshimiwa Sanga, hivyo naahidi baada ya Bunge lako Tukufu nitaongozana naye nikiwa na wataalam kwenda kuonesha hiyo mipaka ili wananchi watambue mipaka ya hifadhi ni ipi na iendelee kuheshimiwa. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo. Kwa kuwa na sisi watu wa Makete tuna changamoto ya hospitali ya wilaya toka mwaka 1982 kituo cha afya kilivyopandishwa hadhi kuwa hospitali ya wilaya, hadi sasa hatuna hospitali ya wilaya. Je, ni lini Hospitali ya Wilaya ya Makete itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2020/2021, kiasi cha shilingi bilioni 27 kimetengwa kwa ajili ya kujenga hospitali za halmashauri zile ambazo ni chakavu, tutajenga hospitali za halmashauri mpya na Halmashauri ya Makete ni miongoni mwa halmashauri ambazo tutakwenda kutenga fedha na kuhakikisha kwamba ujenzi wa hospitali ya halmashauri unaanza.
MHE. FESTO T. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali dogo la nyongeza. Naomba kuuliza, changamoto ya barabara ya Kilindi – Gairo ni sawasawa kabisa na changamoto ya kutoka Isyonji Mbeya kuelekea Kitulo Makete, barabara ambayo ina urefu wa kilometa 97.6 na kwa muda mrefu imekuwa na changamoto wananchi wetu wa Makete wamekuwa wakipata changamoto.

Naomba kuuliza ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kwa sababu ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa miaka mitano mfululizo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Tuntemeke Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Sanga amekuwa anaifuatilia sana hii barabara ya Isyonje – Kitulo – Makete na ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Sanga, Mbunge wa Makete kwamba barabara hii iko kwenye mpango wa ujenzi wa kiwango cha lami, kwa hiyo, labda tusubiri bajeti itakapopitishwa nadhani tutapata majibu sahihi zaidi. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, swali langu lilikuwa linaendana na haya mahusiano kati ya bodaboda na Trafiki na kule Makete mahusiano ya bodaboda na traffic ni kama Refa ambaye yuko uwanjani ana kadi nyekundu tu, mahusiano yao ni mabaya sana kwa kiwango ambacho Traffic wanatoza faini ya shilingi laki mbili, tofauti na utaratibu wa kawaida. Tumejaribu kufanya vikao vya negotiation kati ya sisi na watu wa Trafiki lakini imeshindikana. Pili, Traffic wanafuata bodaboda wangu mashambani kule Matamba, kule Makete, kitu ambacho ni kunyume na utaratibu. Sasa je, Mheshimiwa Naibu Waziri anatupa kauli gani na maelekezo yapi kwa Trafiki Mkoa wa Njombe hususani Wilaya ya Makete dhidi ya vitendo viovu ambavyo vinafanywa na wao dhidi ya bodaboda wa Makete? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba sasa kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utaratibu wetu kwenye PGO na utaratibu uliowekwa kwenye ile sheria au kanuni ya 168 ambayo imefanyiwa mabadiliko mwaka 2002, umesema ni Shilingi elfu thelathini, sasa kama kutatokezea askari au yoyote ambaye anayehusika na hili akawatoza watu zaidi ya kiwango kilichowekwa maana huyo anafanya kosa kwa mujibu wa taratibu kwa mujibu wa Sheria.

Mheshimiwa Spika, watu kuwafuata huko, unajua mtu anapokuwa mhalifu kwa mujibu wa utaratibu vyombo vinavyohusika kumkamata vina uwezo wa kumfuta popote alipo endapo amefanya makosa, lakini sasa hiyo namna ya kumfuata nayo ina utaratibu wake. Kwa hiyo, niseme tu kwamba, kama kutakuwa kuna askari amechukua zaidi ya hizo, maana huyo anavunja sheria, nadhani Mheshimiwa tushirikiane katika hili kuweza kuwakamata na kama tunawajua tuwalete katika ofisi yetu, tujue namna ya kuwashughulikia kwa mujibu wa taratibu. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali lakini nilikuwa napenda kumuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Makete ya mwaka 2014 na Makete ya sasa ni ya tofauti sana. Kutokana na utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi imejengwa lami ambayo imefika hadi Makete, na kwa hiyo mabasi kutoka Dar es salaam na mikoa mingine tayari yameshaanza kuingia Makete.

Je, Serikali ipo tayari kutupatia fedha kutoka kwenye mpango wa miradi ya kimkakati ili Makete ipate kituo cha mabasi kizuri ambacho kinaendana na uhitaji mkubwa wa sasa ambao tunao?

Mheshimiwa Spika, jambo la pili; nakuomba Mheshimiwa Naibu Waziri baada ya Bunge hili kama utakuwa tayari twende Makete kwa ajili ya kuangalia ukubwa wa uhitaji wa kituo cha mabasi pale ndani ya Wilaya ya Makete. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Festo Richard Sanga kwa kazi kubwa sana anayoifanya ya kuwatetea wananchi wa Jimbo la Makete katika miradi mbalimbali ya kiuchumi pamoja na ya kijamii.

Mheshimiwa Spika, pili, nimhakikishie kwamba Serikali inatambua kwamba baada ya utekelezaji mzuri wa Ilani na barabara ya lami kutoka Njombe kwenda Makete, ambayo pia itatoka Makete kwenda Mbeya Mji wa Makete utafunguka na una kila sababu ya kupata stendi ya kisasa ya mabasi. Ndiyo maana katika katika jibu la msingi, na ninaomba niendelee kusisitiza, kwamba tunawashauri Halmashauri ya Makete, waandae andiko la kimkakati la ujenzi wa stendi ya mabasi ya kisasa ambalo litaonesha business plan yake na uwezo wa kulipa fedha zile ili tuweze kutafuta vyanzo vya fedha, iwe Serikalini au kwa wadau mbalimbali, lakini pia na mapato ya ndani ya Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, tatu; nipo tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge hili. Naomba tukae ili tupange ratiba yetu tufike pale; pamoja na mambo mengine tuangalie ujenzi wa stendi ya kisasa ya mabasi. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Makete, hasa Kata za Ipepo na Ikuo, wana changamoto pia ya kituo cha afya. Kwa Ikuo wana majengo tayari wameshajenga kwa nguvu za wananchi lakini bado Serikali haijamalizia na Ipepo tayari wameshaandaa tofali kwa ajili ya kujenga kituo cha afya. Je, ni lini Serikali itaongeza nguvu kuhakikisha kwamba majengo haya yanakamilika kwa ajili ya wananchi wangu wa Ipepo na Ikuo, hasa ikizingatiwa kwamba wana zaidi ya kilometa 20 kwenda kufuata huduma za afya na tayari wameshaonesha jitihada za kuweka nguvukazi hizo?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba majibu ya Serikali kwa ajili ya wananchi wangu hao.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kuwapongeza wananchi wa Kata za Ipepo na Ikuo katika Jimbo la Makete kwa kuonesha nguvu kubwa ya kuwekeza katika ujenzi wa vituo vya afya na hatua nzuri ambayo wameifikia. Serikali imeendelea kusisitiza wananchi kuchangia nguvu zao kuanza ujenzi wa miradi ya vituo vya afya na zahanati na Serikali kuchangia nguvu za wananchi katika umaliziaji wa vituo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Festo Sanga kwamba katika mwaka ujao wa fedha, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuchangia nguvu za wananchi katika ukamilishaji wa maboma. Nimhakikishie kwamba katika maeneo ambayo tutawapa kipaumbele ni pamoja na Kata hizi za Ipepo na Ikuo ili wananchi waweze kupata nguvu ya Serikali kukamilisha vituo hivyo vya afya.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza: kwenye Hifadhi ya Kitulo kwa sababu ni hifadhi yenye upekee na hifadhi nyingine za Tanzania: Je, Serikali haioni haja kuwavutia zaidi wawekezaji kwa kupunguza gharama za uwekezaji; kwa sababu, gharama zimekuwa ni kubwa? Kwa maana, ukiangalia kuna wana- Makete na Watanzania ambao wako tayari kuwekeza kwenye hifadhi hizi, lakini gharama kwa mfano za environmental assessment tu ni zaidi ya shilingi milioni 50, kitu ambacho kimekuwa kiki-discourage wawekezaji.

Sasa je, Serikali umuhimu wa kupunguza gharama ili wawekezaji wawe wengi kwenye hifadhi zetu na ziweze kutangazwa?

Swali la pili: Hifadhi ya Kitulo inaenda kupitiwa na barabara ya kiwango cha lami inayotoka Isyonje kwenda Kitulo kupitia Makete, lakini bado miundombinu ya ndani ya hifadhi siyo mizuri kwa maana ya barabara: Ni mpango upi wa Serikali kupitia Wizara ya Maliasili kuhakikisha kwamba miundombinu ndani ya Hifadhi ya Kitulo inaimarishwa ili tuweze kuvutia wawekezaji wengi zaidi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Naibu Spika, ahsante. Kwanza naomba nimpongeze Mheshimiwa Sanga kwa kuwa na jitihada nyingi sana za kuhakikisha kwamba hifadhi yetu ya Taifa ya Kitulo inapaishwa vizuri, hasa kiuwekezaji, lakini pia kwenye maeneo ya utalii. Napenda nimweleweshe Mheshimiwa Mbunge kwamba, sisi kama Wizara ya Maliasili na Utalii hatuna gharama yoyote inayohusiana na uwekezaji. Wawekezaji wa aina mbalimbali wa ndani na nje ya nchi wanaalikwa kwenye maeneo yote ya uhifadhi kuja kuwekeza uwekezaji mbalimbali, ikiwemo ujenzi wa hoteli, ma-tent, camps, hostels mpaka na lodge. Sisi tunawaalika wawekezaji wote bila kubagua. Gharama kama gharama ni taratibu za uwekezaji ambazo haziko kwenye Wizara yetu, isipokuwa mwekezaji yeyote anatakiwa kufuata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande wa miundombinu Serikali imejipanga kwa mwaka wa fedha 2021/2022 kuhakikisha kwamba maeneo yote ya uhifadhi yanatengewa fedha ya kutosha kuhakikisha miundombinu yote ndani ya hifadhi inaimarika vizuri ili kwenye upande wa utalii sasa tuweze kuhamasisha utalii na maeneo yale yaweze kupitika kwa urahisi. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali dogo la nyongeza. Changamoto ya barabara ambayo imetoka kutajwa ya Kirando – Katete ni sawasawa na changamoto ya kutoka Wanging’ombe kwenye Jimbo la Naibu Waziri, Mheshimiwa Dkt. Festo Dugange, kutoka Wanging’ombe kuelekea Kipengele, Lupira, Kijombo hadi Lumbira ile barabara ambayo iko chini ya TARURA. Naomba kuuliza, je, ni lini Serikali itajenga barabara hii kwa sababu hadi dakika hii ninavyozungumza wakazi wamekuwa wakilala njiani wakati wanaposafiri kutokana na changamoto ya barabara hiyo? Kwa hiyo, naomba majibu ya swali hili. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika,
ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Festo Sanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anafahamu na bahati nzuri ameainisha katika eneo ambalo Naibu Waziri mwenzangu, Mheshimiwa Dkt. Festo Dugange, jimboni kwake ndiko barabara ilikoanzia, lakini kwa sababu mimi na Mheshimiwa Mbunge pamoja na yeye mwenyewe anafahamu katika bajeti fedha ambazo tumekuwa tukitenga na tunaahidi mbele yako kwamba tutaendelea kutenga fedha kwa kadri zinavyopatikana kuhakikisha hii barabara inapitika wakati wote. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza niipongeza Wizara ya Maji kwa kazi wanayoifanya, lakini naomba kuuliza swali dogo la nyongeza. Kutokana na ongezeko la watu kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Makete, hasa hasa Makete Mjini tuna uhitaji mkubwa wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Mradi wa Maji wa kutoka Kitulo, Isapulano kwenda Iwawa Makete Mjini ili kuongeza upatikanaji wa maji kutokana na kwamba tayari kama halmashauri tulishawasilisha andiko letu la mradi wa bilioni 3.1 kwenye Wizara? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Festo Sanga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli andiko hili tumeshalipokea pale Wizarani na mipango ya kuona namna gani ya utekelezaji itaweza kufanyika tayari pia tunashughulikia. Pia nipende kumpongeza sana Mheshimiwa Festo Sanga amekuwa ni mfualitiaji mzuri wa miradi hii yote, yeye mwenyewe amefuatilia na sasa hivi tumeshampelekea Mradi wa Maji wa Lupila milioni 100, lakini vile vile tumempelekea Mradi wa Maji wa Bulongwa milioni 100. Yote haya ni matunda ya yeye kuwasemea vyema wananchi wake. Hivyo sisi kama Wizara hatutakuwa kikwazo kwa Mheshimiwa Sanga na kwa wote anaowawakilisha, tutahakikisha na mradi huu wa bilioni 3.0 nao tunakuja katika utekelezaji. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kuuliza swali dogo la nyongeza. Nafahamu nchi inatambua kwamba, tarehe 22 kutakuwa na mchezo mkubwa ambao unaweza ukabeba record ya nchi wa Simba Sports Club na Kaiza Chiefs hapa Dar es Salaam. Nataka niulize kwa sababu, mchezo huu unaenda kubeba mafanikio ya timu karibu nne endapo Simba itafuzu, Yanga na timu nyingine. Je, ni mkakati upi wa Serikali wa makusudi kuhakikisha Simba Sports Club tarehe 22 inashinda na mashabiki wanajaa uwanjani?
WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza nikupongeze Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kuchaguliwa na kurudi kwenye Kiti chako, unatosha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya swali la msingi. Sasa napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sanga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tumekuwa tukisema timu inaposhinda na kuiwakilisha nchi yetu inakuwa ni timu ya Taifa. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kuipongeza Simba Sports Club kwa hatua waliyofikia na nitoe wito kwa Watanzania wote kuhakikisha tunaiunga mkono timu ya Simba Sports Club ili match itakayoicheza tarehe 22 waweze kupata ushindi. Ushindi huo utakuwa ni heshima kwa nchi yetu. Kwa hiyo, tunawatakia heri Simba Sports Club na sisi Serikali tuko pamoja nao pamoja na vilabu vyote nchini kwa manufaa ya maendeleo ya michezo nchini. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza naishukuru Serikali kwa majibu mazuri, lakini nilikuwa naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. La kwanza, kwenye shamba hili Serikali imeeleza kwamba inaweza ikatenga shilingi bilioni sita kwa maana ya mwaka 2021/2023.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nauliza: Je, Serikali iko tayari kuingia partnership kwa sababu Benki ya TADB (Tanzania Agriculture Development Bank), iko tayari kutoa hizi fedha na ikafanya iwekezaji kwenye shamba hilo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni maslahi ya wafanyakazi wa shamba lile kwa maana ya vifaa na madeni ya wafanyakazi wale, kwa muda mrefu hawajalipwa: Je, ni lini Serikali itakuwa tayari kuhakikisha maslahi ya wafanyakazi na pia vifaa vya shamba viwe vinanunuliwa?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, juu ya uwekezaji, tuko tayari na milango yetu iko wazi, karibu sana tuweze kujadili jambo hilo. Jambo la kuboresha maslahi ya wafanyakazi na ununuzi wa vifaa ni sehemu ya pesa zilizopangwa kutumika katika bajeti hii. Kwa hiyo, tunalielekea pia.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, kwanza niipongeze Wizara ya Nishati kwa sababu mradi huu wa Bwawa la Rumakali, bwawa linajengwa Wilaya ya Makete, lakini power plant inajengwa Busokelo kwa ndugu yangu Mwakibete.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu dogo la nyongeza lilikuwa Waziri alipokuja Makete mwezi wa kwanza aliahidi kwamba mradi huu utaanza mwezi Machi kwa maana ya demarcation kuweka alama, lakini hadi sasa haujaanza. Je, ni lini Serikali itaanza kuweka alama (demarcation) kwenye mradi huu ili wananchi waendelee na shughuli za kijamii, waachane na hii changamoto waliyonayo sasa wanashindwa kuendelea na shughuli za kijamii kwa sababu, hawajui bwawa mipaka itaishia wapi? Naomba pia kujua kuhusu mambo ya fidia. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mwezi Januari Mheshimiwa Waziri alitembelea mradi ule kuona maandalizi yake yamefikia wapi na sisi kama Serikali tumejipanga kuanzia tarehe Mosi, mwezi Juni, wataalam wa Wizara na TANESCO wataenda katika eneo la mradi kwa ajili ya kuhakiki mipaka na kuweka demarcation na kufanya maandalizi ya kulipa fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, fidia italipwa katika maeneo makubwa matatu. Fidia kwenye eneo ambapo litajengwa bwawa, lakini fidia katika eneo ambalo litaenda kuweka hiyo power house, sehemu ya kuzalisha umeme kwa sababu kutoka kwenye bwawa kushuka mpaka sehemu ya kuzalisha umeme kuna kilometa kama saba. Vile vile fidia italipwa kutoka kwenye njia ya kuzalisha umeme mpaka kwenye kituo chetu cha Iganjo ambapo kuna kilometa kama mia moja hamsini kutoka kwenye lile eneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo maeneo yote hayo kuanzia tarehe Mosi mwezi Juni yataanza kufanyiwa kazi ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini kwa ajili ya kuweza kulipa fidia na mradi uweze kuendelea kama ilivyosemwa kufikia mwezi Oktoba.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, aya ya tatu ya jibu lako, kuna sehemu inasomeka hadi kituo cha kupooza umeme cha Iganjo Mkoani Mbeya. Sasa hiki kituo cha kupooza umeme hii Kata hii inayoitwa Iganjo mlipoweka kituo hiki cha kupooza umeme, Mtaa wa Igodima hauna umeme, sasa mmeweka kituo cha kupooza umeme, lakini mtaa hauna umeme. Huo mtaa utapata lini umeme? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na kama tulivyokuwa tukieleza hapo awali ni nia ya Serikali kuhakikisha kila mwananchi wa nchi hii anapata umeme katika eneo lake. Katika eneo hili sasa ni eneo la kipaumbele kwa sababu siyo vema kumpelekea mtu shughuli ambayo wananufaika nayo wengine. Kwa hiyo, nitoe ahadi ya Serikali kwamba, tutahakikisha hicho kituo kinapowekwa pale basi tunaweza kupata umeme wa kuhudumia yale maeneo yote ya jirani kama ambavyo tumefanya hivi karibuni katika Bwawa la Mtera kwa kuongeza pale transformer ya kuhudumiwa wale wananchi wanaoishi katika maeneo yale kwa haraka kabisa.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. naomba kuuliza swali dogo la nyongeza kwa niaba ya wananchi wa Makete.

Mheshimiwa Naibu Waziri Tarafa ya Ikuo haina huduma kabisa ya Mahakama; na ni umbali wa kilometa karibu 170 kwenda kufuata huduma ya Mahakama kwenye Tarafa ya Matamba:-

Je, ni lini Serikali itajenga Mahakama kwenye Tarafa ya Ikuo kwa sababu kwa muda mrefu tumekuwa tukiomba huduma hiyo na hatujapewa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi na jibu la nyongeza la Mheshimiwa, tutakuweka kwenye kipaumbele kwenye bajeti baada ya hii tunayoijadili leo. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Swali langu lilikuwa, kwanza niwapongeze Makete tumepata Chuo cha VETA ambacho kwa Mkoa mzima wa Njombe kipo Makete tu. Lakini tuna changamoto ya kozi ambazo mnazitoa pale nyingi hazipo kwenye soko kwa mfano; hatuna kozi ya ufundi magari, hatuna kozi ya ufundi umeme majumbani, hatuna kozi ya ambayo inashughulikia masuala ya mabomba kwa maana ya ufundi mabomba.

Je, ni lini Serikali italeta hizo kozi ambazo kwa sasa ziko kwenye soko Tanzania kutokana na hizi ambazo tunatekeleza kwenye Ilani hasa hasa suala la umeme vijijini ambapo wana Makete wengi wangependa wafanye kazi kwenye mazingira hayo lakini kozi hizo hazipo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia naomba nijibu swali la Mheshimiwa Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tuna kozi ambazo ziko standard karibu kwenye maeneo mengi sana na kwa sasa hivi kunaonekana kama kuna uhitaji mkubwa sana kwenye baadhi ya maeneo kwamba tubadilishe kozi kuendana na maeneo yale yalivyo. Mfano, nilikuwa kule Mwanza katika Visiwa vile vya Ukerewe hakuna kozi zinazohusiana na masuala ya uvuvi. Lakini wakasema sasa ni muhimu sana tuweze kuianzisha kozi ile. Nimtoe wasi wasi Mheshimiwa Sanga kwamba jambo hili tunakwenda kulifanyia kazi, tutakwenda kukaa na uongozi wa Mkoa na kuhakikisha kwamba kozi hizi ambazo ni muhimu, lakini vilevile zenye soko kwenye maeneo hayo zinaenda kuanzishwa mara moja. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Changamoto ya vifungashio ambayo ipo kwenye mawese ni sawasawa na changamoto ambayo ipo kwenye zao la viazi kule Makete, Mbeya na sehemu nyingine na Serikali ilituahidi.

Je, ni lini vifungashio rasmi vya viazi vitapatikana kwa wananchi wa Makete, Mkoa wa Njombe, Mbeya na sehemu nyingine ili tuondokane na changamoto ya lumbesa ambayo imekuwa ikisumbua kwa muda mrefu hadi sasa?
NAIBU WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema hiyo timu ambayo tumeiunda tumeshawapa deadline, kama ambavyo pia umesema, ndani ya mwezi mmoja waje na mkakati au mpango ambao utaweza kutatua changamoto hii. Kama nilivyosema, si kwa zao moja tu la viazi au michikichi na mazao mengine yote. Kwa sababu changamoto ya lumbesa iko katika mazao mengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lumbesa ni tatizo pale ambapo inazidi vipimo ambavyo vimekubalika katika zao husika. Kwa mfano katika hali ya kawaida tunasema gunia moja liwe kati ya kilo 95 mpaka 105, kwa hiyo zaidi ya hapo inakuwa ni shida. Sasa inaweza kuwa kifungashio ni kidogo kiasi kwamba ikaonekana kama ni lumbesa lakini kiko ndani ya uzito unaokubalika. Hata hivyo, tunachukua changamoto hizi, kama nilivyosema, Kamati hii itakwenda kuweka sasa mkakati au guidelines maalum kwa ajili ya kupata vifungashio specific kwa mazao maalum likiwemo hili la viazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, changamoto ambayo ipo kwa Mheshimiwa Mpakate kuhusu umeme wa REA pia ipo Makete ambapo mkandarasi aliyemaliza kutekeleza mradi wake yeye anasema amemaliza lakini bado tuna changamoto ya kwamba kuna Vijiji kama Mago, Mbela na Kinyika ambako tuna zaidi ya nyumba 1,000 ambazo wananchi wameshasuka umeme toka 2019 lakini hadi ninavyozungumza muda huu wananchi hao hawajaingiziwa umeme kwa sababu ya kwamba mita na nguzo zimeisha.

Je, ni ipi kauli ya Serikali kwa huyu Mkandarasi wa REA ambaye hajakamilisha kazi yake ipasavyo ndani ya Jimbo la Makete na wananchi wangu wanaendelea kuteseka? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunapompatia mkandarasi kazi, tunampa wigo wa kufanya kazi ambayo tunaita ni wateja wa awali. Na kwa wakandarasi wa REA III Round One wako wakandarasi kama wanne ambao walikuwa hawajakamilisha kazi zao ambao tumewaelekeza ifikapo mwishoni mwa mwezi wa 10 wawe wamekamilisha kazi zote. Hivyo, tunatarajia kuanzia mwezi wa 11 hakutakuwa kuna mkandarasi ambaye alikuwa anafanya kazi tofauti na REA III Round Two ambaye atakuwa bado yupo kazini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baaada ya hapa nitafuatilia na kujua hivyo vijiji vilivyobaki ni vingapi na avikamilishe kwa sababu kwenye REA III Round Two hatutaacha kijiji hata kimoja ambacho hakitapata umeme ifikapo Desemba mwakani. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Changamoto iliyopo Bukene ni sawasawa na changamoto iliyopo Makete katika Kituo cha Afya cha Matamba ambacho kinahudumia zaidi watu 25,000, lakini hakina jengo la mama na mtoto, hakina X-ray. Kwa hiyo, naomba Serikali iniambie ni lini italeta fedha pale Matamba ili wananchi wangu waweze kupata huduma? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Matamba Makete ni kituo ambacho kinategemewa na wananchi wengi zaidi ya 25,000, lakini ni kweli kwamba kina upungufu wa miundombinu ya majengo likiwemo jengo la mama na mtoto.

Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imechukua changamoto hiyo tunatafuta fedha ili twende kujenga majengo hayo mengine kuhakikisha wananchi wa Matamba wanapata huduma za kituo cha afya kilichokamilika. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante Jimbo la Makete linakata 23, kata tatu hatuna shule za Sekondari na katika vipaumbele ambavyo nilivileta kwenye wizara ni Kata ya Mlondwe ndiyo ianze kujengwa shule ya Makete Boys na tuliahidiwa kupewa milioni mia 600, lakini hadi sasa milioni 600 hatujazipata.

Je, ni lini milioni 600 zitafika ili tuanze ujenzi wa Makete boys na baadaye tufuate shule Kigala na baadaye tufuate shule ya sekondari Bulongwa? Naomba majibu ya Serikali.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MITAA NA
SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri Silinde kwa majibu mazuri sana kwa maswali yaliyotangulia nimesimama kuhusu swali lililoulizwa na Mheshimiwa Sanga ni lini shilingi milion 600 zitatoka kwa ajili ya kujenga sekondari katika Kata ambazo hazina sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumekamilisha orodha ya sekondari 214 za kila Jimbo ambazo zitapata shilingi milioni 600, lakini Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amesema atatupa shilingi milioni 470 kilichonikwamisha hatujatoa mkeka Waheshimiwa Wabunge wanabadilisha mara kwa mara. Kwa hiyo, hapa simu yangu imekufa nilikuwa nitoe taarifa na ndiyo maana nimesimama kutoa taarifa kwa Waheshimiwa Wabunge kujiridhisha na kile kipaumbele ulichoweka cha Kata yako nitatuma ujumbe kwenye group la Wabunge kusema umpigie mtu gani, uangalie je, hiyo kata yako iliyowekwa ndiyo kata ya kipaumbele. Lakini Mheshimiwa Dkt. Mwigulu yuko tayari tumekwama sisi kwa sababu Wabunge wanabadilisha badilisha.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ile shule ya Mkoa mmoja na waomba sana Waheshimiwa Wabunge tuliomba mchakato uanze kwenye RCC. Kwa hiyo, tumeandikiwa barua na Makatibu Tawala wa Mikoa, wakisema kwamba shule ile moja. Kwa hiyo, kutakuwa na 214 za kila Jimbo, halafu tutanza na moja ya kila mkoa, naomba sana Wabunge mapendekezo yametoka kwa Makatibu Tawala wa Mikoa. Kwa hiyo, tunaomba sana tumeona kuna watu wanabadilisha toa wilaya hii peleka hii sisi tumezingatia ushauri wa Makatibu Tawala wa Mikoa.

Mheshimiwa Spika, by tarehe 15 Mheshimiwa Sanga mkitupa confirmation, hela Mheshimiwa Dkt. Mwigulu yupo tayari zitakuwa zimeshaenda kwenye halmashauri zenu. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninashukuru kwa kupewa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Naomba kuuliza, barabara ya kutoka Makete kwenda Mbeya takribani kilomita 97 ni barabara ambayo ilipata kibali cha Mheshimiwa Rais katika barabara 16 ambazo tulisomewa kwenye bajeti. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais ameongeza kutoka kilomita 25 kwenda kilomita 36.5 za kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami, lakini hadi dakika hii ninapozungumza ni kwamba bado tumebaki kwenye mchakato wa tendering toka mwezi wa Tisa.

Je, ni lini mchakato wa tenda utakuwa umeisha na barabara hii iweze kuanza kujengwa kwa sababu hili ndilo geti la uchumi kwa Wilaya ya Makete lakini pia kwa Mkoa wa Mbeya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GEOFREY G. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru kwa kuipongeza Serikali na kwamba barabara yake ni kati ya barabara zilizopata vibali. Hata hivyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Sanga Mbunge wa Makete, kwa kuwa barabara ilishapata kibali cha Mheshimiwa Rais kwamba iendelee kujengwa, taratibu za manunuzi haziwezi zikakiukwa. Kwa hiyo, kama kuna changamoto ambayo ipo, labda Mheshimiwa Mbunge baada ya hapa naomba tukutane tuone kuna tatizo gani? Ila ni kweli kwamba ikishapata kibali inatakiwa ujenzi uanze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba baada ya kikao hiki tuone kama kuna changamoto yoyote tofauti na taratibu za kawaida ili kama Wizara tuweze kuzitatua. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kuuliza swali dogo la nyongeza ambalo limejikita kwenye sekta hii hii ya zao la parachichi.

Nilisimama Bungeni hapa nikaomba kuhusu ugawaji wa miche ya parachichi kwa wakulima wetu. Kwa sababu, wakulima wetu wa Mkoa wa Njombe, Mkoa wa Mbeya, Mkoa wa Iringa wamejiwekeza sana kwenye kilimo cha parachichi, tukasema, kama ambavyo Serikali imefanya kugawa miche bure ya michikichi, miche bure ya pamba, miche bure ya korosho ili ku-boost wakulima wa mazao hayo, nikaiomba Serikali kuona ni mkakati upi ufanyike kwenye zao la parachichi ambapo wakulima wengi hawana fedha za kununua miche, lakini ni zao linaloonekana ni dhahabu ambalo sisi tunaita dhahabu ya kijani Mkoa wa Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu, je, Serikali ina mkakati upi wa kuandaa vitalu ili iweze kugawa miche bure kwa wakulima ku-boost zao hili, kutoka kwenye kilimo cha kawaida kwenda kwenye zao la biashara ambalo kwa sasa ni hot kwenye Taifa letu? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu aliyoyatoa ya ufasaha. Nataka nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali imetoa ruzuku katika miche ya kahawa, tumetoa ruzuku katika miche ya korosho. Nataka nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba sasa hivi Serikali inafanya mapping katika mikoa mitano, inayozalisha parachichi na kwa kutumia Taasisi zetu za TARI na TOSCI, tumeanza kutengeneza Regulation na Standardization ili kuondoa tatizo la miche inayouzwa na kila mwananchi barabarani ili tusije tukaua zao la parachichi na hivi karibuni tuta-launch hizo guideline. Tunaanza programu kupitia private sector partnership kama Serikali kuanzia mwaka ujao wa fedha. Tutazalisha miche, tutagawa kwa subsidized rate kwa sababu sasa hivi najua wakulima wananunua kati ya shilingi 5,000 na shilingi 6,000 kwa mche mmoja ambao ni ghali sana. Kwa hiyo, tutaanza kugawa miche ya ruzuku ya parachichi katika mikoa yote inayolima parachichi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili tutakalofanya kama Serikali katika eneo la parachichi ni kwamba, kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri, tutajenga common use facility tatu, moja tutaiweka kati ya Iringa na Njombe nyingine tutaiweka Dar es Salaam na nyingine tutaiweka Mkoa wa Kilimanjaro. Hizi zitatumika, wale wanunuzi wanaotoka nje watanunua parachichi, watafika katika hizo facility, watapata huduma kwa kuzilipia na zitawekwa alama ya kwamba ni product za Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu umwagiliaji. Timu yetu ya Umwagiliaji sasa hivi inafanya mapping katika mikoa hiyo ili tuone ni wapi ambapo tutaweza ku-facilitate kuweza kugawa mipira na nini ambako wananchi wamewekeza. Kwa sababu ni zao ambalo linahitaji uwekezaji wa muda mrefu na linahitaji government intervention, niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge tutafanya strong intervention kwenye parachichi kwa sababu tunaamini tunazo competitive aids zote. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ninaomba kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Lupila kuelekea Kipengere ni barabara ambayo inaunganisha Wilaya za Ludewa, Makete na Wanging’ombe na tumeiombea kibali kwenye RCC cha kupandishwa hadhi ya TANROADS, hadi leo takribani miaka mitatu imepita.

Je, ni lini Wizara itatoa kibali barabara iwe chini ya TANROADS ili iweze kujengwa na kupitika kwa uhakika kwa sababu wananchi wangu wanateseka sana?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zote ambazo zinahudumiwa na TAMISEMI kwa maana ya TARURA zina utaratibu wake. Naomba kama imefanyiwa tathmini inawezekana imeshindwa kukidhi viwango, lakini tunaomba Mheshimiwa Mbunge baada ya hapa tuonane ili tuweze kuona ni kitu gani kinakwamisha barabara hii kama inakidhi viwango isiweze kupandishwa hadhi na kuhudumiwa na TANROADS. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwanza niishukuru Wizara ya Nishati hasa Mheshimiwa Rais, Makete tulikuwa na vijiji 37 havina umeme, lakini mkandarasi amekuja na anaendelea kazi vizuri, lakini changamoto ambayo tuko nayo, swali la kwanza, ni kwa mkandarasi wa REA phase III round one ambaye hadi sasa hajakamilisha kazi ya kusambaza umeme kwenye vijiji baadhi ya Makete. Je, ipi kauli ya Serikali kwa mkandarasi huyo ambaye hadi dakika hii amefelisha zoezi la kusambaza umeme kwenye vijiji kadhaa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Makete tulipewa bwawa la umeme la Lumakalia sisi tunaita bwawa la Luvaninya, hili bwawa kwa muda mrefu limekuwa likitamkwa wananchi wangu hawajajua hadi sasa hivi ni lini linaanza kujengwa. Sasa naomba kauli ya Serikali, ni lini Serikali itaanza kujenga bwawa hili ambalo linaenda kutatua kero ya umeme kule Makete na mikoa ya karibu kama Mbeya?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, nipende kupokea shukrani alizozitoa kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha kwamba umeme unafika katika vijiji vyote na sisi kama Serikali tunaendelea kumsaidia Mheshimiwa Rais kutekeleza majukumu ambayo ametupatia.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba REA III round ya kwanza kuna maeneo hayajakamilika. Zilikuwepo lots 29 na zilizokamilika kabisa ni lots 21, lots nane bado hazijakamilika na eneo la Makete likiwemo. Kauli ya Serikali ni kwamba tumeingia mkataba wa nyongeza ya muda kidogo na wakandarasi na tumekubaliana nao ifikapo Machi mwaka huu, kazi zote zimekamilika.

Mheshimiwa Spika, niseme moja wapo ya sababu kubwa ambayo ilichelewesha miradi hii ni UVIKO ambao ulichelewesha vifaa kupatikana, lakini sababu nyingine kubwa ambayo ilikuwa inatokea ambayo maelekezo ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan tumeyatekeleza na kubadilisha utaratibu REA III round one ilikuwa inaenda kwa utaratibu unaoitwa goods na siyo works, yaani wakandarasi walikuwa wanapewa pesa, wanunua vifaa ,wakishafikisha vifaa ndiyo sasa tunaanza kuwapa utekelezaji wa kazi. Hii imepelekea sasa wakandarasi wengine washindwe kufanya kazi na mikataba yao ikabidi tuivunje ili kupata wengine, kwa hiyo muda ukapotea.

Mheshimiwa Spika, kwenye REA III round II maelekezo tuliyoyapata na tutayatekeleza ni kwamba, mradi unatekelezwa kwenye utaratibu wa works, mkandarasi analipwa kwa kile kiwango cha kazi aliyofanya na tunaamini hiyo itatusaidia kukamilisha kazi zetu zote tulizonazo kwa wakati kwa sababu usipokamilisha kazi inabakia kazi sawa na pesa ambayo haujaifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la pili, ni kweli kwamba kule Makete na maeneo mengine ya Njombe kuna Mradi unaitwa Rumakali ambao Serikali inatarajia kuutekeleza na pale tutapata Megawatts 222. Feasibility ya pale ilifanyika mwaka 1998 na kwa kuwa tumeona uwezo wa kupata fedha wenzetu wa TANESCO wamemweka Consultant mpya wa kufanya update ya ile feasibility study ili tuendane na hali ya sasa. Kwa hiyo, kinachofanyika sasa, mkandarasi wa feasibility study ameanza kazi yake Januari, tunatarajia atamaliza mwezi wa Tano na kuanzia mwezi wa Tano itaanza kufanyika evaluation kwa ajili ya compensate wale watu walioko maeneo yale.

Mheshimiwa Spika, tunatarajia mwishoni mwa mwaka huu mambo yote yatakuwa yamekamilika, hivyo mwaka ujao pesa ya kujenga mradi itakuwa imepatikana na tunaweza kuanza kutekeleza mradi huo kwa ajili ya kuongeza umeme unaozalishwa kwenye maji katika Gridi ya Taifa.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ninaomba kuuliza swali dogo la nyongeza kwa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tamko ambalo limetolewa na Waziri wa TAMISEMI kuomba kibali cha ajira za watumishi 7,000 walimu. Na kwenye nchi hii tuna walimu wengi wanaojitolea kufanya kazi bila kulipwa. Kule Makete nina watumishi karibia 100 ambao ni walimu wanaojitolea; je, ni upi mpango wa Serikali kuwapa kipaumbele walimu hawa au wafanyakazi hawa ambao wameonesha moyo wa utayari na uzalendo wa kufanya kazi bila malipo na wanakwenda kuomba ajira? Naomba majibu ya Serikali. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Tuntemeke Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Bungeni Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, alishatoa kauli ya kuwaagiza waajiri wote kwa maana ya wakurugenzi wa halmashauri mbalimbali nchini, kuhakikisha wanafikisha majina ya watu wote wanaojitolea katika sekta ya afya na katika sekta ya elimu ili iwekwe katika kanzidata yao katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili waangalie utaratibu bora wa kuweza kuwaingiza katika utumishi wa Umma pale ajira zinapotolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nirudie kauli ile tena ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ya kuwataka wakurugenzi wa halmashauri zote kuhakikisha majina ya wanaojitolea walimu shule za msingi na sekondari, wale wauguzi na katika sekta ya afya kwa ujumla wawasilishe majina hayo Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili utaratibu huo maalum unaoangaliwa uweze kufanyika kwa haraka wakati majina hayo yapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nitoe angalizo; katika kuleta majina hayo watende haki. Walete majina ya wale ambao wamejitolea kwa muda mrefu, wasilete majina ya watu ambao huenda amesikia kauli hii anakwenda kujitolea kesho na anataka jina lake na yeye liweze kuingizwa. Waangaliwe wale waliojitoa kwa muda mrefu na tutashirikiana na wenzetu wa TAMISEMI kuona namna bora ya kuweza kuwaingiza katika utumishi wa Umma. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante hili suala la Hifadhi ya Kitulo liko pia Makete ambako ni wilayani kwangu. Kuna mgogoro mkubwa kati ya wananchi na Hifadhi ya Kitulo kwa sababu uwekaji wa beacon ya mipaka haukushirikisha wananchi kitu ambacho kimesababisha mgogoro mkubwa. Pia tuna hifadhi ya Mpanga Kipengele ambako kuna Vijiji vya Ikovo, Kimani na kwenye Hifadhi ya Kitulo mgogoro mkubwa uko kwenye Vijiji vya Chankondo, Misiwa kule Itelele.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Bunge hili ilituahidi kwamba itakuja Makete kutatua hii kero na haijaja hadi leo. Ile timu ya Mawaziri Nane pia ilisema itafika Makete haijafika hadi leo.

Je, ni lini Serikali itakuja kutatua changamoto hii ya migogoro ili wananchi wangu waweze kupata maeneo kwa kufanya kazi kwa sababu ndiyo waliotumia kuhifadhi hii Hifadhi ya Kitulo hadi Serikali imekuja kuichukua mwaka 2005?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na maelekezo ya Mheshimiwa Rais ambaye aliandaa Kamati ya Mawaziri Nane ambao walikuwa wanapaswa kuzunguka nchi nzima. Zoezi hili tulilianza kipindi cha mwaka uliopita na tulizunguka kwenye baadhi ya maeneo. Nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Sanga kwamba zoezi hili bado ni endelevu tutafika kwenye maeneo yote yenye migogoro na tutatatua.

Mheshimiwa Naibu Spika, yale ambayo yameshapitiwa na kamati hii tutahakikisha kwamba yanarudishwa kwa wananchi. Yale ambayo ni migogoro mipya Mheshimiwa Waziri ameshaunda kamati nyingine ambayo tumeanza kupitia tena upya maeneo ambayo yana migogoro ili kuhakikisha kwamba wananchi na maeneo ya hifadhi yanahifadhiwa vizuri na wakati huo huo wananchi wanaendelea na shughuli zao za kila siku. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kupitia Bunge Mheshimiwa Rais na Bunge tulipitisha kuondoa kodi kwenye nyasi bandia na hii ilikuwa ni kulenga kuboresha viwanja vya michezo kama sera inavyosema, lakini hali ya miundombinu ya viwanja nchini ni mbaya. Hatuoni mpango wowote wa maksudi wa Serikali kuongea ama na taasisi binafsi ambao wanamiliki viwanja au Halmashauri kuhakikisha tunatumia fursa hii ambayo Mheshimiwa Rais ametupa ya kuweka nyasi bandia nchini.

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa makusudi wa kuboresha hali ya viwanja nchini ili Simba na Yanga ziache kulalamika kutokana na viwanja kama uwanja wa Manungu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, sisi tunalishukuru Bunge kwa kutupitishia exemption kwenye nyasi bandia ya VAT na Baraza letu la Michezo la Taifa (BMT) linaratibu zoezi la Halmashauri zetu wanapohitaji hizo nyasi bandia za grade gani wanaweza wakapata, tunaweza tukaratibu, tutakuunganisha, utapata hizo nyasi Mheshimiwa Mbunge kwa sababu viwango tunavyo vya class A, B, C na bei zake. Kwa hiyo, tushirikiane ili pale mnapohitaji muweze kuzipata.

Mheshimiwa Spika, mkakati wa kuboresha viwanja vyetu sasa hivi TFF imeingia mkataba pia na Chama cha Mapinduzi ambacho kina viwanja vikubwa katika mikoa yetu. Viwanja kumi tunaenda kuviboresha kupitia mkataba huu ambao tutakuwa tumemaliza kukubaliana nao. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwenye Bunge la Bajeti lililopita tulipitisha bajeti ya shilingi bilioni 10 kuweka nyasi bandia kwenye viwanja vya michezo nchini; je, Serikali imefikia hatua gani kwenye kuweka nyasi bandia kwenye viwanja vyetu kwa sababu ligi inaendelea na bado viwanja haviridhishi?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi kuweza kujibu swali la Mheshimiwa Festo Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba katika bajeti iliyopita ya Bunge tulipitisha zaidi ya shilingi bilioni 10 kuhakikisha kwamba tunaboresha viwanja vya Arusha, Mwanza, Tanga, Dodoma, Mbeya na viwanja vyetu vikuu vya Mkapa ambavyo sasa vinatumika na vya Uhuru.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara tumeshaanza mchakato kuhakikisha kwamba mwaka huu wa fedha haupiti bila hizi fedha kutumika. Kwa hiyo, Wizara kupitia kitengo chetu cha manunuzi wameshaanza mchakato na tumeendelea kusisitiza kwamba jambo hili la kuboresha viwanja hivi iweze kuanza mapema ili hivi viwanja viweze kutumika. Ahsante.

WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba nilithibitishie Bunge lako tukufu na Watanzania kwa ujumla kwamba viwanja hivi ambavyo Mheshimiwa Sanga amevizungumza havitawekwa tu nyasi bandia na nyasi za kawaida, tutakwenda kuweka viti vya kisasa kabisa. Pia viwanja hivi tunakwenda kuvitengeneza kwa namna ambavyo tunaweza kuvitumia kimataifa na mchakato huu wa ujenzi utaanza mwaka huu. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nyakati tofauti Serikali imekuwa ikisisitiza kutokufungia akaunti wafanyabiashara, lakini tumeendelea kupokea malalamiko wafanyabiashara wanafungiwa akaunti. Hata kama kuna changamoto za kikodi lakini kumekuwa na tatizo hilo.

Je, ni ipi kauli ya Serikali kwa TRA kuacha utaratibu wa kufungia akaunti wafanyabiashara hata kunapotokea changamoto za kikodi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwamba kauli ya Serikali katika jambo hili ni ile kutaka mamlaka ya mapato kufuata sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa na Serikali katika majukumu yao ya kila siku. Suala la kufunga akaunti bila vielelezo hili hakuna. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba kuuliza swali dogo la nyongeza; ni lini Serikali itaanza upembuzi yakinifu wa Barabara kutoka Mfumbi – Matamba – Kitulo (kilometa 51) ili iweze kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu ni ahadi ya Serikali na ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni kama barabara ya uchumi ambako tunajua kunalimwa viazi vingi sana na mazao ya mbao. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ina mpango wa kuanza kuifanyia usanifu barabara hii ili kupata thamani ama gharama ya hiyo barabara na baadaye Serikali itafute fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Swalli langu dogo la nyongeza, barabara ya Makete-Mbeya-Isionji, ni barabara ambayo tayari upembuzi yakinifu, hatua za manunuzi, na hata upekuzi wa kampuni iliyoshinda umeshafanyika. Mheshimiwa Waziri mbele ya Mheshimiwa Rais alituahidi mwezi wa tisa mkandarasi atafika site.

Je, ni lini mkandarasi atasaini mkataba ili aanze kujenga barabara hii ambayo ni uti wa mgongo wa uchumi wa Wilaya ya Makete?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara anayoitaja Mheshimiwa Festo ilitangazwa, lakini ilikosa Mkandarasi kwa sababu ya udogo, Mheshimiwa Rais akaongeza kilomita. Barabara hii ilishatangazwa na tayari mikataba imeshaandaliwa. Tunapoongea sasa hivi iko kwa Mwanasheria Mkuu kwa ajili ya kuifanyia vetting na tunategemea mara itakapotoka mwezi huu, basi mikataba hiyo itasainiwa ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kuuliza swali dogo la nyongeza kwamba Tarafa ya Matamba kuna kituo cha afya cha Matamba kina takribani miaka 30, hakina jengo la Mama na Mtoto na wala hakina jengo la mochwari. Huduma ya mochwari tunaenda kupata kwenye Wilaya ya jirani inaitwa Chimala. Sasa tunaomba ni lini Serikali itatupatia fedha tuweze kujenga jingo la mama na mtoto lakini eneo la kuhifadhia wenzetu kwa maana ya mochwari, kwa sababu ni umbali mrefu tunaenda kuhudumiwa kutoka kwa Jirani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga Mbunge wa Jimbo la Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ameainisha kwamba Tarafa ya Matamba ina kituo cha afya lakini hakina huduma ya mochwari pamoja na mama na mtoto, kwa hiyo alichoomba tu ni kwamba Serikali lini tutapeleka fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwambie tu kwamba tumelipokea hili ombi na tutaliweka katika mipango yetu ya baadaye ili tuhakikishe kwamba hizi huduma mbili ambazo ameziainisha Mheshimiwa Mbunge zinapatikana. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Swali langu pale Makete tuna pori la Mpanga Kipengele ambalo linazunguka vijiji vya Ibaga, Ikovo, Kiimani na Kigala. Pori hili limegeuka ni mwiba kwa wananchi wa Makete kwa sababu mifugo yao imekuwa ikiingia na watu wanakamata lakini bikoni zimewekwa kwenye maeneo ya wananchi; na nililalamika hapa Bungeni na ukaniahidi Mheshimiwa Waziri utakuja.

Je, ni lini Serikali itekwenda kuweka bikoni ili wananchi wangu wawe salama katika eneo hili?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tulikuwa kwenye ziara ya Mawaziri nane ambao wanatatua changamoto hizi za migogoro ya ardhi.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu kwamba nitafika kama sio mimi basi ni Mheshimiwa Waziri kuhakikisha kwamba tunafafanua wapi mipaka ilipo ili wananchi waweze kuielewa na hatimaye tuendelee kushirikiana kulinda maeneo ya hifadhi.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, asanye Mradi wa Matamba Kinyika ni mradi ambao ulikuwa unatekelezwa kwa bilioni nne lakini Mheshimiwa Waziri Aweso amepambana hadi umetekelezwa kwa bilioni mbili, lakini mradi huu una miaka minne na hadi sasa haujakamilika. Wananchi wa Kitongoji cha Itani, Mlondwe, Ngonde na Nungu bado wanahangaika na maji kupitia mradi huu. Je, ni lini Serikali itakamilisha mradi huu ili wananchi wao wapate maji ya uhakika?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipokee shukrani, salamu za pongezi kwa niaba ya Waziri. Mradi huu kama alivyosema kwa jitihada za Mheshimiwa Waziri ameweza kuona kwamba ameupunguza na sasa hivi tutaendelea kuleta fedha ili kuona kwamba tunaenda kuukamilisha hivi punde, kama si ndani ya mwaka huu wa fedha kufika Juni, kabla ya mwaka 2022 kwisha tutahakikisha kwamba tunakuja kufanya kazi kwa sehemu kubwa.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, barabara hizi nyingi za Nyanda za Juu Kusini zimekuwa na changamoto ya mvua ya muda mrefu, na barabara nyingi hazijafikiwa kiwango cha changarawe. Ni upi mkakati wa Serikali? Na ukifuatilia maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuwa anazungumza na watu wa TARURA kwamba maeneo ya Kusini ambayo ni ya uzalishaji barabara hizo zijengwe kwa kiwango cha changarawe kwa wingi.

Je, ni upi mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba barabara hizi zinajengwa kwa kiwango cha changarawe, hususan kwenye Mikoa ya Ruvuma, Lindi na Njombe hususani Wilaya ya Makete?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa Serikali ni kwamba moja tunataka kuwahakikishia tunapandisha hadhi barabara za udongo kwenye changarawe na pili, zile za changarawe kuzipeleka katika kiwango cha lami; na tunafungua barabara nyingi mpya. Kwa hiyo sehemu ya miradi mikubwa ambayo tumeielekeza katika Nyanda za Juu Kusini ikiwemo Agri-connect ni ujenzi wa lami ili maeneo hayo yaweze kupitika muda wote na shughuli za kiuchumi ziweze kuendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Serikali ipo kazini na tutaendelea kuongeza fedha ili kuhakikisha hizi barabara ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja zinafanyiwa kazi.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika,ahsante. Kwa mara ya pili ninaomba kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, Tarafa ya Ikuwo haina Mahakama ya Mwanzo, wananchi wanalazimika kusafiri zaidi ya kilimita 100 kwenda kupata huduma za kimahakama kitu ambacho kinawafanya wananchi wakate tamaa wasiendelee kufuatilia haki zao. Ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Mwanzo kwenye Tarafa ya Ikuwo ili wananchi wangu waweze kupata huduma hiyo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nipende kujibu swali la Mheshimiwa Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika hali ya kawaida nimuombe Mheshimiwa Mbunge tuwasiliane baada ya kikao hiki ili niweze kumpa mkakati ambao tumeuweka, kwa sababu katika kipindi hiki tuna miradi Sitini ambayo iko katika hatua mbalimbali na kwa sababu katika kipindi hiki tunayo miradi 60 ambayo ipo katia hatua mbalimbali na kwa sasa, kwa vile sina kumbukumbu sahihi hapa niwasiliane naye ili niweze kumsaidia kujua Mahakama yake inaenda kuanza lini ujenzi. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Zao la parachichi ukienda kwenye soko la nje inaonekana parachichi nyingi zinatoka kwenye nchi ya jirani, lakini uzalishaji mkubwa unafanyika Njombe na Mikoa ya Tanzania. (Makofi)

Ni lini tutatengeneza ownership ya soko hili la parachichi lionekane ni la Tanzania na siyo la nchi jirani ambao wanunuzi wengi wananunua Tanzania na wanafanya packaging kwa jina la nchi ya jirani? (Makofi)
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sanga la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sababu za parachichi zetu kuwa- branded nje ni kwa sababu sisi kama nchi tumekuwa kwa muda mrefu hatuna infrastructure. Kwa hiyo, watu wanakuja kununua raw wanapeleka wanakwenda ku-brand nje.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuanzia mwaka kesho tutatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa common use facility tatu, moja tutaijenga Mkoa wa Iringa ambapo itafanya kazi ya sorting, grading na branding na yeyote anayenunua huko atanunua akifikisha pale ataikuta hiyo huduma inafanyika na itakuwa-branded kama produce of Tanzania.

Mheshimiwa Spika, vilevile, zipo kampuni ambazo sasa hivi zimeshaanza ku-brand parachichi yetu na kui-brand kama produce of Tanzania kama Eat Fresh na Kampuni zingine ambazo zipo katika Nchi yetu. Kwa hiyo, jambo hili lipo na Serikali tunachukua hatua kuanzia mwakani tutakuwa na common use facility tatu moja Dar es Salaam, moja Iringa na moja Kilimanjaro. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, asante uwanja wa ndege Mkoa wa Njombe haupo kabisa kwenye utekelezaji wa bajeti uliopita na hata bajeti iliyopo ya sasa, lakini kwenye ilani umekuwa ukiutaja kama ni moja kati ya viwanja mnaenda kuvitenga.

Wananjombe wanauliza ni upi mkakati wa Serikali kujenga uwanja wa ndege Mkoa wa Njombe kwa sababu uwekezaji wa parachichi na mambo mengine sasa hivi wanauhitaji mkubwa, lakini wananjombe walioko nje wengi matajiri wanahitaji kusafiri kupitia ndege kurudi Njombe ni upi mkakati wa Serikali?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nikweli kwamba uwanja wa Njombe ni muhimu na eneo lipo tayari. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itakapopata fedha na hasa kulingana na umuhimu wa uwanja huo tutaanza kufanya kwanza utwaaji na kulipa fidia lakini pia kuanza usanifu wa kina, lakini hili Mheshimiwa Mbunge itategemea na upatikanaji wa fedha na utekelezaji wa ilani ni wa miaka mitano. Kwa hiyo nikuhakikishie kwamba hata kama kwa sasa hatujaanza kutekeleza lakini utatekelezwa katika miaka hii mitano, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kutokana na majibu ya Serikali, kwa kuwa suala la kutoa elimu kwa wananchi limekuwa likifanyika mara kwa mara, lakini halijawa na tija ya kutibu tatizo la lumbesa. Ni upi mkakati wa Serikali kusimamia Sheria ya Vipimo, Sura 340, kuhakikisha kwamba suala la lumbesa linaisha kabisa nchini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, Serikali haioni ni wakati muafaka kati ya Wizara ya Kilimo na Wizara ya Viwanda na Biashara kuanzisha selling point ili kuwekwe mizani katika maeneo hayo ili kudhibiti suala la lumbesa nchini kwenye mazao ya viazi, vitunguu na mazao mengine ambayo yamekuwa msiba kwa muda mrefu kwa mkulima ambaye amekuwa akinyonywa kwenye Taifa letu?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli moja ya changamoto tuliyonayo ni usimamizi wa kutekeleza hii Sheria na mkakati uliopo ni kupitia wenzetu Serikali za Mitaa kwa maana TAMISEMI, kuhakikisha wanasaidia kwanza maeneo yale ambayo kuna mauzo kuwe na mizani ambayo itatumika kuhakikisha wale wote wanaonunua wanapima au wananunua kwa uzito.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ambalo nalo linaendana na hili ni kwamba, hiyo ndiyo mikakati ya Serikali ambayo tunataka sasa tuhamasishe wananchi kujiunga katika vyama vya msingi au kuimarisha ushirika katika maeneo ya mashambani ili waweze kuwa na uwezo au nguvu ya ku-bargain. Moja, ili wapate bei nzuri na pili, ili sheria hii iweze kutumika ni lazima wawe na maeneo ya kuuzia.

Kwa hiyo, mpango uliopo kupitia Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara vile vile Kilimo na wenzetu wa TAMISEMI ni kuona tunawa-organize sasa wakulima wale wawe na maeneo mahususi ya kuuzia mazao yao ili tuwapatie uwezeshaji wa kuwa na vipimo, kwa maana ya mizani lakini pia wawe na nguvu ya kudai bei stahiki ya mazao yao. Nakushukuru.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, Wilaya ya Makete mlitupatia shilingi bilioni 1.7 za mradi wa maji kutoka Lumage kwenda Madihani na kutoka Usalimwani kwenda Mfumbi, mkandarasi hajafika hadi leo.

Ni ipi kauli ya Serikali dhidi ya mkandarasi huyu ambaye anaigharimu Serikali hadi sasa kwenye suala la maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara tulishatoa tamko kwa wakandarasi wote ambao watataka kuturudisha nyuma watarudi wao. Mheshimiwa Mbunge nafuatilia mkandarasi huyu sababu zilizompelekea kutofika, mimi na wewe naomba tukutane baada ya Bunge hili tuweze kufanyia kazi.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali, barabara ya kutoka Chimara kwa maana ya Mfumbi kuelekea Matamba-Kitulo, kilometa 51. Barabara ambayo inaelekea kwenye hifadhi ya utalii. Ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hii kwa sababu upembuzi yakinifu ulishaanza kufanyika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuifungua barabara hii kwa ajili ya kuunganisha maeneo ya Chimara - Itamba hadi Makete, lakini pia tunajua tutakuwa tunafungua utalii eneo hilo, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza ninaipongeza Wizara, walituma timu kwa ajili ya kutatua mgogoro kwenye Hifadhi ya Kitulo na Mpanga Kipengele. Swali langu; ni lini wananchi hawa wa maeneo ya Ipelele, Ikovo na Mfumbi ambao wanapakana na Hifadhi ya Kitulo pamoja na Pori la Mpanga Kipengele mtawapatia barua, kwa sababu mlionesha nia ya kuwaongeza maeneo, ili waanze kufanya shuguli zao za kichumi kwa kuwa muda mrefu sasa wameendelea kusubiri barua lakini hawajapata maamuzi ya Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Jimbo hili kwamba, Serikali iliunda Kamati ambayo ilienda kufanya tathmini uwandani, na Kamati hii imeshapita maeneo takribani nchi nzima, ikiwemo eneo la Mheshimiwa Sanga. Kwa hiyo, sasa hivi kinachofanyika ni utekelezaji wa uchambuzi uliofanyika uwandani. Wakati wowote naomba nimuahidi Mheshimiwa Mbunge na wananchi wanaozunguka Hifadhi ya Kitulo kwamba kuanzia sasa utekelezaji wake utafanyika na tutawajulisha wananchi maeneo husika, kwamba sasa tathmini imeenda hivi. Tutapita pia kijiji kwa kijiji, hifadhi kwa hifadhi, tunashirikiana kuweka vigingi ili kuondoa hii taharuki ya wananchi kutofahamu mipaka halisi. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, katika Ujenzi wa barabara za TANROAD huwa kunakuwa na package ya taa za barabarani kwenye barabara ambazo zimeanza kujengwa kuanzia mwaka 2019. Barabara kutoka Njombe kuelekea Makete ni barabara ambayo ilikuwa ni package ya nyuma.

Je, ni lini Serikali itaingiza package ya taa ya barabarani kwenye Mji wa Handara na Makete Mjini, angalau na sisi Makete tuanze kuona taa za barabarani kama maeneo mengine. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hiyo aliyoitaja ndiyo kwanza inakamilishwa kwa kiwango cha lami na Meneja wa Mkoa wa Njombe ameshatoa tathmini ya barabara, kwa maana ya gharama ambapo tutaweka taa za barabarani Mji wa Ramadhani, Ikonda na Makete yenyewe. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, barabara ya kutoka Makete kwenda Mbeya ni barabara ya kiuchumi, na katika barabara 16 ambazo Mheshimiwa Rais alisaini zianze kujengwa moja ni barabara kutoka Makete kuelekea Mbeya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mmekuwa mkituambia mko kwenye tendering, tunaomba majibu wananchi wa Makete; ni lini barabara hii itaanza kujengwa ili ifanye ukombozi wa uchumi wa wananchi wa Makete?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Makete – Kikondo kwenda Isyonje ni barabara ambayo ilipata kibali cha kutangazwa na ilitangazwa lakini ilikosa wakandarasi. Barabara hiyo imetangazwa tena na tarehe 22 mwezi uliopita ndiyo ilikuwa mwisho na sasa hivi barabara hii tuko kwenye evaluation ili tujue mkandarasi yupi atapata hiyo kazi.

Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa hivi tuko kwenye taratibu za manunuzi, tunafanya evaluation ya tender, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi, naomba niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Matamba kinahudumia Kata tano za Kinyika, Matamba, Mlondwe, Itundu na Mfumbi. Kituo hiki kina zaidi ya miaka 30 hakijakarabatiwa.

Je, ni lini Serikali itakarabati kituo hiki ili kiweze kupata majengo mapya ikiwemo mochwari ambapo wananchi wanatumia Wilaya ya Mlale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Festo Sanga Mbunge wa Jimbo la Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Matamba ni cha muda mrefu na ni tegemeo la wananchi kutoka katika kata takribani tano katika Wilaya ya Makete. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imekwishaainisha vituo vya afya vikongwe na chakavu na vyenye upungufu wa miundombinu kwa ajili ya kupeleka fedha kwa awamu kwa ajili ya kukarabati na kuvipanua. Kwa hiyo tutatoa kipaumbele pia katika kituo hiki cha Matamba kwa kadri ya bajeti ambavyo tunakwenda kuipanga; ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya kutoka Jimboni kwako Mheshimiwa Waziri Wanging’ombe kuelekea Lupira, kwa maana Kipengere - Lupila na barabara ya Esaprano. Barabara hizi ni za kiuchumi lakini zimekuwa zikisumbua kwa muda mrefu.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Sanga Mbunge wa Jimbo la Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mbunge jirani yangu amekumbusha suala la msingi na tayari nimhakikishie kwamba kwenye bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI suala hilo ni kipaumbele kujenga barabara kutoka kipengere kuelekea kule Lupila na itatekelezwa, ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naipongeza Serikali kwa kujenga vyuo vya VETA lakini kwenye vyuo hivi vingi vya VETA vilivyopita, masomo yanayotolewa mengi hayana soko kubwa kwenye ajira ya sasa lakini kuna masoma kama ufundi bomba, ufundi umeme wa magari, umeme wa majumbani unakuta kozi nyingi hazipo kwenye vyuo vya VETA mathalani Makete. Ni lini Serikali itaanza kuongeza masomo hayo ambayo yanaajira nyingi kwa vijana wetu ili waweze kupata kusoma?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejibu katika swali nadhani namba 96 la kuhusiana na suala la upitiaji wa mitaala. Tumeanza upitiaji wa mitaala katika elimu yetu ya msingi lakini tunafanya mapitio ya mitaala katika elimu ya sekondari, vyuo vya ualimu, vyuo vikuu pamoja na vyuo vya VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mapitio hayo ya mitaala vile vile katika maeneo haya ya vyuo vya VETA tunakwenda kuongeza idadi ya masomo lakini vile vile kufanya review ya hata hayo masomo yote tunayoyatoa kuhakikisha kwamba tunakwenda kweli kujibu changamoto za wananchi zile ambazo katika maeneo yao ambao wanahitaji.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kwa niaba ya wananchi wa Makete nipende kuishukuru Serikali kwa kuichukua barabara hii ya kutoka Chimala kuelekea Matamba kilomita 20 ambayo ina kona 53 kwenye milima. Barabara hii ni ya kiuchumi na barabara ya kimkakati, kwenda TANROADS ni msaada mkubwa ambao Serikali imeweza kutusaidia.

Je, kwa kipindi hiki ambacho mvua nyingi zinaendelea Matamba na Makete ni upi mpango wa Serikali kutusaidia barabara hii iweze kupitika kwa sababu wananchi wanaitumia sana kwa muda mwingi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuna barabara kutoka Kitulo kuelekea Busokelo kwa Mheshimiwa Naibu Waziri wa Uchukuzi, upi mkakati wa Serikali kuimalizia barabara hii ili iweze kujengwa irahisishe mawasiliano kati ya wananchi wa Makete na wananchi wa Jimbo la Busokelo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Richard Sanga Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Matamba hadi Kitulo ni eneo ambalo kwa kweli Mheshimiwa Mbunge atakubaliana na mimi lina mvua nyingi sana, na TANROADS wako barabarani kuhakikisha kwamba inapitika lakini yako maeneo ambayo tunashindwa kufanya kazi kwa sababu ya mvua nyingi sana ambayo inaendelea kunyesha. Hivi tumewaagiza TANROADS kuhakikisha kwamba muda mwingi wawepo maeneo hayo ili pale ambapo jua linatoka basi waweze kuhakikisha kwamba wananchi wanapata mawasilano na kurekebisha zile barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa swali lake la pili, kuhusu kutengeneza barabara ya Kitulo kwenda Busokelo; hii barabara haikuwepo, ni mpya. Atakubaliana nami kwamba tumeshaanza kuifungua na tumeifungua yote, kinachosubiriwa sasa ni kuikamilisha, kwa maana ya kujenga makalavati na kuweka changarawe ili kuhakikisha kwamba wananchi wa pande hizi mbili wanaweza kuwasiliana, na hasa wananchi wa Busokelo kwenda Hospitali ya Ikonda ambao wanaihitaji sana, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Naomba kuuliza Swali dogo la nyongeza. Wakati ambapo wenzetu wanazungumzia kuboresha Vyuo Vikuu chakavu, Mkoa wa Njombe hauna Chuo Kikuu hata kimoja, mara kwa mara tumekuwa tukiomba na kwa kuwa Wilaya ya Makete tuko tayari kutoa eneo kwa ajili ya ujenzi wa Chuo Kikuu chochote kile ambacho unaweza kuona kinafaa;

Je, ni lini Serikali na ipi ahadi ya Serikali kwa wananchi wa Jimbo la Makete na Mkoa wa Njombe kwamba mtajenga Chuo Kikuu?
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza hakuna Mkoa hapa nchini ambao hauna Tawi la Chuo Kikuu Huria, ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Sanga kwamba Njombe siyo kati ya Mikoa ambayo inayo au itanufaika sasa hivi kwa mradi wa HEET kwa kuwa na kampasi ya Chuo Kikuu kwa jitihada ambayo Serikali imefanya kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais, tumesambaza kampasi katika Mikoa kadhaa. Mipango iko mbioni ya mazungumzo na Mkoa wa Njombe kuhakikisha kwamba tunapeleka kampasi kule. Ningeomba details tuzitoe baada ya kukamilisha mikakati hii, lakini tunatambua umuhimu huo na tunajua kwamba kulikuwa na ahadi ilitolewa pale Njombe kwamba Njombe na yenyewe itapata kampasi ya Chuo Kikuu.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Swali langu, Mkoa wa Njombe na halmashauri mbalimbali nchini ikiwemo Makete wanalipa ushuru wa fire lakini maeneo haya hayana gari za fire. Ni ipi kauli ya Serikali kwa halmashauri zote nchini ambazo haziona gari za fire na wanalipa ushuru wa fire iktu ambacho kwa wnanchi kimekuwa ni kero na wamekuwa wakituuliza maswali mengi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika,ushuru unaolipwa si kwamba ndio unaokwenda kununua gari za zimamoto kwa sababu ni ushuru kidogo sana ukilinganisha na gharama za gari hizi; gharama za gari hizi hutegemea bajeti ya Serikali. Hata hivyo fedha zile zinalipwa kuwezesha Jeshi la Zimamoto na Ukoaji kutoa elimu ya namna ya kujikinga na majanga ya moto na majanga mengine ya kibinadamu kwenye maeneo hayo. Nikuahidi Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote, kwamba kipaumbele cha Serikali kuanzia mwaka ujao ni kupata fedha ili kuweza kuzipatia wilaya zote gari za zimamoto kwa kadri fedha zitapopatikana, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Wakati Kinondoni wanaomba fedha kwa ajili ya kujengewa lami, Wilaya ya Makete na Mkoa wa Njombe tunaomba fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara za changarawe kwenye barabara ya kutoka Kinyika – Kikondo – Nkenja – Ikuwo, barabara ambazo zimeharibika sana kutokana na mvua nyingi zinazoendelea Jimboni Makete.

Je, Serikali itafanya nini itusaidie tupate fedha hizo kwa sababu barabara hizi ni barabara za uzalishaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mwaka wa fedha huu Bunge lako tukufu limeipitishia TARURA bajeti ya zaidi ya bilioni 772 tutaangalia barabara hii ya Kinyika – Kikondo katika Jimbo la Makete kule kama nayo imetengewa fedha kwenye bajeti hii. Kama haijatengewa fedha tutaangalia mwaka wa fedha unaofuata tuweze kutenga fedha kwenye bajeti kutengeneza barabara hii.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante Wilaya ya Makete mmetupatia mradi wa ujenzi wa Bwawa la Umeme la Rumakali mmeishafanya demarcation, mmeifanya tathimini ni takribani miezi mitano toka mmefanya hivyo amjaanza kulipa kwa maana kuwalipa wafanyakazi wale. Muda huu wananchi wa Makete wanawasikiliza ni lini Serikali itawalipa wananchi wanaozunguka bwawa hilo ili waachane na shughuli za kilimo na za kiuchumi zilizoko pale waanze kufanya shughuli zingine? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikweli Serikali ya Awamu ya Sita inayo dhamira ya kujenga Mradi wa Rumakali wa kuzalisha megawati 222 kwa kutumia nguvu ya maji. Kama alivyosema Mheshimiwa Festo tayari tumeishafanya upembuzi yakinifu na tathimini ya site imeishafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachotarajiwa sasa ni mwezi unaofuata wa sita wananchi wataenda kuonyweshwa nani atalipwa shilingi ngapi, ili kwenye mwaka wa fedha unaokuja kuanzia Julai fidia hiyo iweze kufanyika. Kwa hiyo, wananchi wawe na subiri kidogo ndani ya miezi miwili, mitatu fidia yao itaanza kulipwa kwa ajili ya kupisha maeneo ya mradi.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Barabara ya kutoka Igawa kuelekea Mbeya inapita Jimbo la Makete. Ni barabara yenye volume kubwa ya magari na inachangia uchumi wa Tanzania kwa kiwango kikubwa sana. Je, ni ipi commitment ya Serikali ili iweze kujenga barabara hii ambayo pia anaitumia Mheshimiwa Spika na imekuwa ni nyembamba kwa kiwango ambacho inahatarisha sana usalama wa wapitaji wa barabara ile? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Festo Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii aliyoitamka ya Igawa kwenda Makete inapita milimani na ni barabara muhimu sana katika uchumi wa wananchi wa maeneo hayo. Pia amesema kwamba ni barabara ambayo Mheshimiwa Spika anapita. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wote wa maeneo hayo kwamba, hii barabara ni miongoni mwa barabara ambazo ziko kati ya huu Mradi wa EPC + Financing kuanzia Igawa – Mbeya mpaka Tunduma.

Mheshimiwa Spika, barabara nyingine ambazo zinakwenda kusainiwa, kwa ridhaa yako naomba nizitaje hapa ili Waheshimiwa Wabunge wasipate nafasi ya kuwa na mashaka.

(i) Ifakara – Malinyi – Lumecha hadi Songea;

(ii) Igawa - Mbeya – Tunduma;

(iii) Karatu – Haydom – Mbulu – Sibiti hadi Maswa;

(iv) Mafinga – Mgororo;

(v) Masasi – Nachingwea – Liwale;

(vi) Kongwa – Kibaya – Arusha; na

(vii) Handeni – Kiberashi – Chemba - Kwa Mtoro hadi Singida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, barabara hizi zitasainiwa mwezi wa sita, na tumshukuru sana Mheshimiwa Rais, katika historia ya nchi hii tunakwenda kusaini kilometa zaidi ya 2000 na Mheshimiwa Waziri alikwisha tamka akiwa pale Singida.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kuuliza swali la nyongeza. Kupitia Bunge hili tuliahidiwa kwamba, umeme wa Makete watabadilisha line kutoka Mbeya kuja Makete ni line ambayo inasumbua na imechoka kwa muda mrefu na inasababisha umeme Makete kukatika mara kwa mara. Wakatuahidi kwamba, watajenga substation Wanging’ombe ili wananchi wa Makete tuchukue umeme kutoka Njombe. Je, hatua hiyo imefikia wapi ili wananchi wa Makete wanaosikiliza sasa hivi wapate uhakika wa majibu ya Serikali? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya changamoto ambayo tumekuwa nayo ni umeme kusafirishwa umbali mrefu kutoka kwenye chanzo. Tulifanya tathmini kupitia TANESCO na tukabaini makundi matatu, kuna wale ambao wana shida zaidi, kuna wenye shida za kati na kuna wale ambao maisha yanaweza yakaendelea.


Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwenye maeneo yenye shida zaidi tunaishukuru Serikali ya Awamu ya Sita imetupatia pesa bilioni 500 kwa ajili ya kutekeleza Mradi unaitwa Gridi Imara na utajenga vituo vya kupoza umeme 14 katika awamu hii ya kwanza. Sasa nimhakikishie Mheshimiwa Festo kwamba, eneo lake nitaenda kuliangalia limewekwa kwenye category ipi katika yale maeneo matatu yenye matatizo makubwa, matatizo ya kati na matatizo ya juu na nitamfahamisha endapo kitajengwa kituo cha kupoza umeme kipindi hiki au kitajengwa katika awamu inayofuata, lakini kabla ya miaka sita ijayo kwisha tunatarajia kuwa na kituo cha kupooza umeme kwa kila wilaya ili kuondoa matatizo ya umeme kusafirishwa kwa muda mrefu.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, kwa sababu ndani ya kipindi cha muda mfupi cha miaka miwili amejenga vituo zaidi ya vinne vya afya ndani ya Wilaya ya Makete kitu ambacho kwa historia ya Wilaya ya Makete hakikuwepo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa maswali yangu ya nyongeza ni haya swali la kwanza; kuna Kituo cha Afya Kitulo, Kituo cha Afya Bulongwa, Kituo cha Afya Lupalilo na sasa Kituo cha Afya Mbalache hivi vimejengwa, vimekamilika lakini havina vifaa tiba, ipi ni kauli ya Serikali ili vifaa tiba vianze kupelekwa hapa na wananchi wa maeneo yale waweze kuanza kupata huduma kwa ajili ya kuwasaidia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; kuna Kituo cha Afya cha Ipepo au kwa maana ya eneo la Ipepo, wananchi wale wameandaa tofali zaidi ya laki moja, wameandaa mawe kwa ajili ya kuanza kujenga kituo cha afya. Je, ni upi mkakati wa Serikali kuwasaidia wananchi wa Kata ya Ipepo ili waweze kuwa na kituo cha afya kwa sababu wanasafiri umbali wa zaidi ya kilomita 50 hadi 100 kwenda kufuata huduma ya afya kwenye Jimbo langu la Wilaya ya Makete? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la kwanza la Mheshimiwa Sanga la vifaa tiba, Serikali imetenga fedha katika mwaka wa fedha huu ambao tupo wa 2022/2023, shilingi milioni 450 kwa ajili ya kununua vifaa tiba kwa vituo vya afya vilivyopo Wilayani Makete lakini vilevile kuna shilingi milioni 50 kwa ajili ya zahanati zilizokuwepo katika Wilaya ya Makete.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nimtaarifu Mheshimiwa Mbunge na Wanamakete kwa ujumla kwamba kuna shilingi milioni 600 ambayo imetengwa kwenye bajeti ya mwaka 2023/2024, kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwenye vituo hivi vya afya ambavyo Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan imejenga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikienda katika swali lake la pili la lini Serikali itasaidia nguvu za wananchi pale kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Ipepo katika Kata ya Ipepo kule Makete. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba inakuwa na vituo vya afya katika maeneo ya kimkakati na hivi Mheshimiwa Mbunge ameitaja hapa kwamba ipo kilomita 50 kutoka Makao Makuu ya Wilaya, basi nichukue nafasi hii kumwelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Njombe kuhakikisha anafika katika eneo hili la Ipepo na kufanya tathmini na kuona kama kituo hiki cha afya kinastahili kupandishwa hadhi sasa kuwa kituo cha afya kamili na walete taarifa yake Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hiki cha afya.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, licha ya majibu mazuri ya Serikali ya kuitangaza Hifadhi ya Kitulo lakini Serikali ina mradi wa regrow mradi ambao umejikita kwenye kutangaza utalii Kusini mwa Tanzania na hifadhi hii ni hifadhi ya kipekee Barani Afrika na Tanzania, kwa nini mradi regrow haujaenda kwenye Hifadhi ya Kitulo ili uweze kuisaidia hifadhi hii kutangazwa kwa ukubwa zaidi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwenye Hifadhi ya Kitulo kumekuwa na changamoto ya kimahusiano kati ya wananchi na hifadhi kwa maana ya migogoro ya mipaka. Sasa katika jitihada za kutangaza utalii ni upi mkakati wa Serikali kutatua migogoro iliyopo kwenye vijiji vya Misiwa, Ujuni, Nkondo, Makwalanga, Lugoda na Igenge. Vijiji hivi kwa muda mrefu vimekuwa na mgogoro na hifadhi, upi mkakati wa Serikali kutatua mgogoro huu ili mahusiano yaweze kuimarika kati ya hifadhi na Wananchi wa Wilaya ya Makete?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Richard Sanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa miradi ya regrow, mradi wa regrow phase one ulikuwa unawezesha kufanya maboresho katika hifadhi nne ambazo ilikuwa ni Mikumi, Nyerere, Udzungwa na Ruaha, lakini Serikali inatarajia kuingia mkataba tena kwenye REGROW Phase Two ambayo Hifadhi ya Kitulo pia itaingizwa katika mradi huo. Kwa hiyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Kitulo itaingizwa kwenye phase two na maboresho yatafanyika.

Mheshimiwa Spika, kwenye upande wa migogoro tulishapeleka tathmini tayari ilishafanyika na sasa hivi ni utekelezaji tu wakuainisha mipaka mipya. Kwa hiyo, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi sasa naomba nielekeze tu TANAPA waende kuweka vigingi katika maeneo ambayo yameainishwa baada ya tathmini kuwa imefanyika lakini na sisi pia tutaenda kujihakikishia.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, kikao cha Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mameneja wa TARURA, aliagiza Mikoa ya Kusini hususan Njombe, ikiwemo Wilaya ya Makete kuangaliwa kwa jicho la karibu kutokana na kwamba ni wilaya ambazo mvua zinanyesha kwa muda mrefu na Makete bajeti ya TARURA ni ndogo sana. Je, ni lini Serikali itaongeza fedha hizi na kuzingatia maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli yalikuwa ni maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, na sisi Ofisi ya Rais, TAMISEMI kazi yetu ni kutekeleza maelekezo hayo. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tumeshafanya tathmini ya halmashauri zenye mvua nyingi, milima na aina ya udongo ikiwemo Halmashauri ya Makete na bajeti ya barabara katika Halamashauri ya Wilaya ya Makete itaendelea kuongezwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mradi wa maji wa Usalimwani - Mvumbi, Kitulo- Ijuni, Kidepwe - Madihani, Mariwa - Ikete ni miradi ambayo imesimama. Ni lini Serikali itatoa fedha ili miradi hii iweze kukamilika kwa ajili ya wananchi wa Wilaya ya Makete?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, Mbunge machachari kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha tayari zimeanza kutoka wiki hii, tutarajie hata Wakandarasi wanaofanya miradi hiyo aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge watalipwa.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa uzoefu ambao nimeupata kujifunza kwenye halmashauri mbalimbali nchini, kumekuwa na halmashauri nyingi ambazo zinavuka na bakaa kwa maana ya salio.

Je, Serikali haioni ni wakati sahihi kuzielekeza halmashauri zote nchini kutumia mapato ya ndani kuwaongeza Madiwani kwa sababu sehemu kubwa Serikali imechukua mzigo huo na halmashauri nyingi zimekuwa zikivuka na bakaa na salio?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, ni kweli kuna baadhi ya halmashauri zimekuwa zikivuka na fedha katika mwaka wa fedha unapoisha kwenda mwaka mwingine kwa maana ya bakaa na Mheshimiwa Mbunge anapendekeza kwamba salio lile litumike kwa ajili ya kuwalipa nyongeza posho Waheshimiwa Madiwani, lakini niseme zile fedha ambazo zinavuka mwisho wa mwaka wa fedha mara nyingi ni fedha za miradi ambayo inasubiri kutekelezwa. Kwa hiyo, ni fedha ambazo tayari ziko committed, lakini zinakwenda kutekeleza miradi ile katika first quarter ya mwaka wa fedha unaofuata.

Mheshimiwa Spika, jambo la msingi ni kwamba tunajua kuna umuhimu wa kuongeza posho Waheshimiwa Madiwani, Wenyeviti wa Serikali za Mitaa ni jambo ambalo tutaendelea kulifanyia kazi na kadri uwezo wa Serikali utakapoongezeka suala hilo litaendelea kushughulikiwa, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Afya Lupila kwa sababu, majengo yake yamechakaa sana na ni ya muda mrefu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Kituo cha Afya Lupila kimetengewa fedha za World Bank na kitaenda kujengwa katika mwaka huo wa fedha. Vilevile kuna maombi maalum ya Mheshimiwa Mbunge ya Kituo cha Afya Mfumbi ambayo nayo yanafanyiwa kazi, ili kituo cha afya hicho kiweze kujengwa.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa kila Mbunge anayesimama anaomba minara na maeneo mengi hata Mjini mtandao unasumbua. Ni upi mkakati wa Serikali kutumia satellite ili kuondokana na changamoto hii ya mawasiliano ambayo hata maeneo ya Mijini yenye mabonde na miteremko kumekuwa na vurugu sana za kukosekana kwa mawasiliano. Ni upi mkakati wa Serikali wa kutumia satellite ili mawasiliano yapatikane nchi nzima?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mikakati mingi. Serikali iliingia kwenye utatatibu wa Ujenzi wa Mkongo wa Taifa ili tuondokane na matumizi ya microwave ambayo ilikuwa na changamoto kubwa sana, ni ya gharama lakini kulingana na jiografia ya nchi yetu ilivyo ilileta changamoto kubwa. Vilevile, kuna maeneo ambayo tunatumia satellite.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kutoa maelekezo mahsusi ili tuanze mchakato wa kupata satellite yetu kama nchi. Tunaamini kwamba kwa kufanya hivyo tutakuwa tumetatua chanagamoto nyingi sana za mawasiliano ambayo ni mchango mkubwa sana katika uchumi wa sasa. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, mkakati wa Serikali ni kuhakikisha kwamba tunaji–engage na kila teknolojia inayoibukia ili kuhakikisha kwamba kwanza kabisa tuwe na teknolojia rahisi na inayoweza kwenda kutatua matatizo katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu mara nyingine unakuta kuna mnara hapa lakini sehemu ya pili mawasiliano hauwezi ukapata, kunakuwa na dark sports za kutosha. Kwa hiyo, sisi kama Serikali tumejipanga na tunaendelea na uchambuzi wa kina kuangalia ni teknolojia ipi ambayo itakuja kutupa majibu sahihi kwa ajili ya kutatua changamoto ya mawasiliano kwa wananchi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali langu kule Makete hamna Nyumba za Jeshi la Polisi, ukienda Dodoma hapa nyumba za askari polisi hapa hazifai, ukienda Oster Bay Dar es Salaam hazifai ni upi mkakati mahususi wa Serikali wa kujenga nyumba za polisi nchini kama ambavyo JWTZ imefanya kwa ajili ya maaskari wao? Kwa hiyo tunaomba majibu ya Serikali kwa kushirikiana na National Housing.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa swali la mkakati zaidi. Niliwahi kueleza hapa katika moja ya maswali kwamba Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia Jeshi la Polisi inao mpango wa miaka kumi wa ujenzi na ukarabati wa Vituo vya Polisi na Makazi kwa ajili ya Askari. Kwa hiyo, mpango tunao kazi tuliyonayo ni kutafuta fedha kadri tunavyoendelea utekelezaji tunapata fedha kutoka kwenye tozo lakini tutapata fedha kutoka kwenye bajeti ya maendeleo kwa madhumuni ya kujenga vituo na nyumba hizo. Kwa hiyo, maeneo yote yatafikiwa kadri ya upatikanaji wa fedha. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Jambo la kwanza kwa niaba ya wananchi wa Makete tuishukuru Serikali kwa mradi huu ambao ni mradi mkubwa ambao tayari dermacation imeshafinyaka na sisi wananchi wa Makete tupo tayari kupokea. Utayari wa Serikali kwamba Mwezi wa saba itaanza kulipa fidia kwa wananchi wetu kwa mwaka huu. Maswali yangu mawili ya nyongeza ni yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wanaozunguka eneo hili la bwawa wa Vijiji vya Busokelo, Madihani, Bulongwa, Mwakavuta, Itete pamoja na Ruangwa; vijiji hivi vyote sasa hivi shughuli za kiuchumi zimesimama kwa sababu ya dermacation. Sasa tulikua tunaomba kujua;

Je, mko tayari kuturuhusu wananchi waweze kulima yale mazao ambayo yanaweza kuondoka wa mfupi kwa maana ya mahindi, njegere na shughuli zingine ambazo hazichukui muda mrefu, kwa sababu muda huu shughuli zote zimesimama?

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, bwawa hili linahusisha miradi ya ujenzi wa barabara, kwa maana ya kutoka Makete kuelekea Busokelo kwa Mheshimiwa Mwakibete;

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha miundombinu hii inajengwa kwa sababu huu ni mradi mkubwa ambao utapitisha vifaa vingi; Serikali itajenga barabara hizi lini wakati wa utekelezaji wa mradi huo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa niaba ya Serikali na mimi nipokee shukurani na pongezi za Wananchi wa Mkoa wa Njombe kwa ujumla na Mkoa wa Mbeya ambako bwawa linafika hadi Busokelo. Lakini nimuombe Mheshimiwa Sanga aendelee kuwashawishi wananchi watuvumilie kwa sababu tunatarijia kuanza kulipa fidia mwezi unaokuja au labda mwezi unaofuata baada ya hapo. Katika muda mfupi wananchi watapata kile ambacho wanakistahili ili eneo hili waliweze kuliacha kwa ajili ya sasa Serikali kuwa tayari kufanya shughuli zake ambazo ni za uendelezaji wa mradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimuahidi Mheshimiwa Sanga kwamba wananchi hawatachukua muda mrefu watakuwa wamepata fidia yao na wanaweza wakaendelea kujiendeleza kwenye maeneo yao na maeneo yao. Lakini pembeni ya hilo tutaendelea kujadiliana na tuzungumze. Tunayo experience mbaya, kwamba tunapotoa nafasi kama hiyo wananchi sasa wanarudi moja kwa moja hata baada ya kulipwa fidia wanataka waendelee kubaki kwenye maeneo yao. Kwa hiyo, tutajadiliana na viongozi wa Serikali wa maeneo husika na wewe Mheshimiwa Mbunge ili tuone namna bora ya kuwahudumia wananchi katika kipindi hiki ambacho ni cha mpito

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye eneo la pili, ni kweli tutagenga miundombinu mbalimbali katika maeneo hayo barabara, madaraja kwa ajili ya kubeba mzigo kuhudumia mradi. Na kwa sababu mradi bado haujaanza, plan yetu ni kuanza kulipa fidia tukamilishe mambo madogo madogo halafu tujenge miundombinu kwa ajili ya kuweze kufikia lile eneo. Kwa hiyo kabla ya mradi kuanza mwaka wa fedha ule mwingine unaokuja barabara na maeneo mengine yanayotakiwa kuwekea miundombinu itawekwa ili ihudumie eneo la mradi lakini pia ihudumie wananchi kwa maendeleo yao ya kila siku.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kuuliza swali kwamba, zamani tulikuwa na vyuo kama Sokoine kinahusika na kilimo, IFM kilikuwa kinahusika na fedha, Mzumbe inahusika na sheria na utawala, ardhi kinahusika na ardhi, lakini siku hizi kumekuwa na kozi mbalimbali zinazoingia ambazo zinatofautiana na asili ya vyuo hivi. Ni upi mkakati wa Serikali kuona vyuo hivi vinabaki kwenye asili yake, ili tuendelee kuzalisha wataalamu bora zaidi? (Makofi)
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Sanga kwamba, kuna wakati vyuo vilipoanzishwa vilikuwa vina-specialize katika maeneo mbalimbali na vingine kwa kweli, vilikuwa ni taasisi ya elimu ya juu, lakini sio vyuo vikuu kwa tafsiri ambayo tulikuwanayo kwa mfano Mzumbe kilikuwa kinatoa Advanced Diploma badala ya kutoa Degree. Baada ya mageuzi ambayo yalitokea hapo kabla vyote vilipewa vibali vya kuwa vyuo vikuu na hivyo walikuwa wanaweza wakaanzisha programs mbalimbali na wakipata kibali walikuwa wanaendelea kwa hiyo, maana yake hata vyuo kama Sokoine vimeongeza baadhi ya programs nje hata ya eneo ambalo mwanzoni walikuwa wamelizingatia.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, hivyo tuna-insist na tutaendelea kufanya jitihada kuhakikisha kwamba, kila chuo kikuu kinajaribu kuwa na eneo ambalo wame-specialize, ili kuwa na competence kubwa zaidi. Kwa hiyo, kama Sokoine tutatarajia kwamba, waongeze nguvu sana kwenye kilimo, kuna chuo kama Nelson Mandela ambacho kime-specialize kwenye sayansi na teknolojia tungependa wa-focus zaidi kwenye sayansi na teknolojia na kadhalika.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali ninaomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, shule hii ya Mjimwema Makambako ni shule ambayo Mheshimiwa Mbunge aliiweka moja kati ya vipaumbele vya shule zake ambazo tulivileta TAMISEMI ili ziweza kujengwa kutokana na eneo hili kuwa na uhitaji mkubwa wa sekondari.

Je, ni lini Serikali itafanyia kazi mapendekezo ya Mheshimiwa Mbunge ili shule iweze kujengwa pale?

Swali la pili, hata Wilaya ya Makete nilileta kipaumbele kwenye Kata ya Kigala ambayo kwa muda mrefu haina Shule ya Sekondari ya Kata. Ni lini Serikali itajenga Sekondari ya Kata kwenye Kata ya Kigala ili wananchi waweze kupata elimu kwa mazingira ya karibu? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza. Kuhusu swali hili la kwanza la Kata ya Mjimwema kupata shule, kama nilivyokwisha sema kwenye majibu yangu ya msingi, Serikali kwa sasa ipo mbioni kupeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya katika Kata ambazo hazina shule kwenye Halmashauri mbalimbali nchini na kila Halmashauri kwenye Halmashauri 184 itapata shule moja. Tumetenga kiasi cha shilingi milioni 570 kwa ajili ya ujenzi wa shule hizo. Awamu ya kwanza ya hizo shule 231 ilienda milioni 470, Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeangalia hali ya mabadiliko ya vifaa, bei na kadhalika na kuweka minimum kuwa ni milioni 570. Sasa ni wajibu wa Halmashauri ya Mji wa Makambako wenyewe kuhakikisha kwamba fedha hii inapofika waweke kipaumbele Shule ya Mjimwema ili iweze kujengwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili la Kata ya Kigala kule Makete vilevile Halmashauri ya Wilaya ya Makete itapokea shilingi minimum milioni 570 kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya katika Halmashauri yao, hivyo basi ni wajibu wao kuhakikisha kwamba wanapeleka fedha katika Kata hii ya Kigala kwa ajili ya ujenzi wa sekondari mpya.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali ya Wilaya ya Makete ni moja kati ya hospitali chakavu sana. Ni hospitali ambayo imetembelewa na Mawaziri tofauti, Mheshimiwa Ummy akiwa TAMISEMI amefika, Mheshimiwa Bashungwa, Mheshimiwa Jafo amefika na Kamati ya Bunge ya TAMISEMI imefika wamejionea hali ya Hospitali ya Wilaya ya Makete.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipi ni kauli ya Serikali mimi kama Mbunge ningeomba msifanye ukarabati mjenge. Je, ipi ni kauli ya Serikali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, tuna vituo vya afya cha Kitulo, tunayo zahanati ya Nungu, Kisungilo na Unyangogo, hizi zahanati zimekamilika hazina vifaatiba. Je, ni lini Serikali itapeleka vifaatiba ili huduma zianze kutolewa kwa sababu wananchi wangu wa Makete, wametoa nguvu kazi yao wamejenga zahanati hizi na vituo vya afya lakini vifaatiba hamna. Ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Sanga kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya kwa wananchi wa Jimbo la Makete, nimhakikishie kwamba Serikali itaendelea kumpa ushirikiano ili kuhakikisha wananchi wa Makete wanapata maendeleo ambayo yanatarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Makete ni kweli ni hospitali chakavu, Mheshimiwa Mbunge ameuliza hapa mara kadhaa Serikali hii sikivu ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ikamuahidi kupeleka fedha na sasa tumetenga mwaka ujao wa fedha milioni 900. Hii ni miongoni mwa hospitali 19 ambazo mwaka ujao wa fedha zitakabarabitiwa au kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli ya Serikali ni kwamba tunafanya tathmini na kuona hospitali zile zenye uchakavu mkubwa beyond repair tunafanya ujenzi mpya, lakini zile ambazo zinaweza kukarabatika, tutakarabati. Kwa hiyo, kauli ya Serikali ni kwamba kufuatia tathmini ambayo tutaifanya katika hospitali ya Makete tutatoa maelekezo rasmi kwamba Shilingi Milioni 900 inakwenda kujenga ama inakwenda kukarabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Vituo vya Afya vya Kitulo, Zahanati ya Nungu na nyingine kuhitaji vifaatiba. Katika mwaka wa fedha ujao, Serikali imetenga milioni 450,000 kwa ajili ya vituo vya afya na zahanati katika Jimbo la Makete ili vituo hivi viweze kupata vifaatiba. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri ni takribani mwaka mmoja umeisha tangu Rais atoe maelekezo kwenye Wizara kufanya marekebisho ya viwanja nchini, lakini hadi sasa hakuna kiwanja kilichofanyiwa marekebisho kupitia Wizara:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ipi kauli ya Serikali kwa sababu hali ya viwanja nchini ni mbaya na bado wanamichezo wanazidi kuweka matumaini kwa Serikali?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sanga, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Wizara tunashirikiana na wadau mbalimbali kurekebisha viwanja. Hivi ninavyoongea, sasa hivi tunakamilisha maridhiano na Chama cha Mapinduzi ambao wanamiliki viwanja nchi nzima kwenye mikoa, vile viwanja vikubwa, na tunategemea tutaanza ukarabati wa viwanja hivi na mwaka huu unaoanza Mheshimiwa Sanga tutaanza na viwanja saba. Tumetenga zaidi ya Shilingi bilioni 10 kwa ajili ya ukarabati wa hivi viwanja. (Makofi)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, kauli ya Mheshimiwa Waziri Mkuu wakati anaongea na Mameneja wa TARURA nchini, alisema kuna mikoa kama Njomba na Mbeya ambayo hali ya barabara ni mbaya lakini ni mikoa ya uzalishaji, TARURA lazima muwape kipaumbele kuwapa fedha; kwa mfano Makete, hali ya barabara ni mbaya.

Ni lini mtaongeza fedha kwa ajili ya mikoa hii ya uzalishaji katika Taifa letu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kuonesha kwamba Serikali inazingatia maeneo yenye uzalishaji mkubwa ndiyo maana utaona katika hizo nyanda ambazo Mheshimiwa Mbunge ameziainisha kuna miradi maalum ikiwemo miradi ya RISE ambayo haiko maeneo mengine, lakini iko katika maeneo ambayo yanazalisha. Tumepeleka huko ili kuongeza fedha nyingi kwa ajili ya uzalishaji katika maeneo hayo. Kwa hiyo, hilo ndiyo jibu sahihi, sio tu fedha za TARURA, ni pamoja na miradi husika. Ahsante sana.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwanza niipongeze Serikali kwa sababu mradi huu unatumia takribani shilingi 3,000,000,000 kwenye utekelezaji wake lakini tayari wameshatoa shilingi 500,000,000. Ni lini Serikali itatoa shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kukamilisha mradi huu kwa ajili ya wananchi wa Kata ya Iwawa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kuna mradi wa Matamba - Kinyika ambao Serikali imetumia zaidi ya shilingi bilioni 2.8 kuujenga, lakini hadi leo hamjaukamilisha takribani miaka saba.

Ni lini Serikali itakabidhi mradi huu kwa wananchi wa Kijiji cha Nungu, Ng’onde, Mbela na Hitani ili waweze kupata huduma ya maji kwa sababu imebaki tu eneo la distribution kwa maana ya usambasaji? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mradi ambao tayari tumeshautolea shilingi milioni 500 na utekelezaji wake unakwenda vizuri ni ule mradi ambao umetumia fedha za mapambano dhidi ya UVIKO-19 na fedha iliyobaki tutaendelea kutoa kuanzia mwezi huu wa Juni, tutaendelea kuongeza fedha. Mheshimiwa Mbunge baada ya hapa tuonane tuliweke sawa hili kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Mradi wa Matamba - Kinyika ni kweli mradi umechukua muda mrefu, lakini ni katika ile miradi ambayo ilikuwa ni chechefu na tayari tunaendelea kuikwamua, hivyo mradi huu pia kwa sasa hivi umeshafikiwa hatua nzuri ni zaidi ya asilimia 80 umeshaweza kutekelezwa, tutakuja kuumalizia hivi punde na watu wa IRUWASA watakabidhi kwa watu wa NKOMBEWASA ili waweze kufanyakazi ndani ya mkoa wao.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Waziri kwenye Kata ya Lupila kuna sekondari na kuna kituo cha afya, umeme REA III Round Two haujaweza kufika kwenye eneo lile. Je, nini kauli ya Serikali kuweza kutuongezea scope ya kufika umeme kwenye eneo la taasisi hizi mbili?
WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni mpango wa Serikali kupeleka umeme na kuweka vipaumbele katika taasisi za umma. Lakini vilevile tunaongea na wenzetu ndani ya Serikali ikiwemo TAMISEMI kwamba pale ambapo kuna ujenzi wa hizi taasisi, basi kupeleka huduma ya umeme iwe sehemu ya gharama ya ujenzi wa hizo taasisi ili kurahisisha kazi ya upelekaji wa umeme.

Mheshimiwa Spika, lakini katika maeneo aliyozungumza Mheshimiwa Sanga ya Kata ya Lupila, naomba nikutane naye kwa mahususi ili tuweze kulifanya jambo hili kwa umahususi wake.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Mwaka 2021 niliomba Mahakama kwenye Tarafa ya Ikuwo, Tarafa ambayo wananchi wake wanatembea zaidi ya kilomita 120 kwenda kufuata huduma Mahakama ya Mwanzo. Niliahidiwa kwamba nitapewa Mahakama, lakini tunaenda mwisho wa mwaka, hadi leo hatujajengewa Mahakama. Ni lini Serikali itajenga Mahakama ya Mwanzo kwenye Tarafa ya Ikuwo ili iweze kuhudumia Kata ya Kigala na Mfumbi ili wananchi wao wasipoteze haki zao za Kimahakama ambazo wamekuwa wakizikosa kwa muda mrefu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kumjibu Mheshimiwa Sanga swali lake la nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ujenzi haujaanza na kama nilivyojibu jana swali la msingi, niliwaeleza juu ya mkakati wa mwaka mpya huu wa fedha ambao tunakwenda kuanza ujenzi wa sehemu kubwa sana wa zile Mahakama za Tarafa. Namwomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira kidogo katika kipindi hiki kinachofuata ambapo bajeti yake imeshaidhinishwa, tunaenda kuanzisha ujenzi ambao utakwenda kutibu kiu ya wananchi wetu hawa. Ahsante.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kutokana na uchakavu wa majengo kwenye shule za msingi kule Makete, Waratibu Kata Elimu leo wamekuja kutoka Makete wako hapa wanataka kujua ni lini Serikali itapeleka fedha za kukarabati Shule ya Msingi Lupalilo, Shule ya Msingi Ikungula, Shule ya Msingi Iwawa na Shule ya Msingi Kijombo? Waratibu wangu wa Elimu Kata wako hapa leo, wanataka waondoke na majibu ya Serikali. Ni lini fedha zitatoka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Naibu Spika, fedha itapelekwa na Serikali katika Shule za Msingi Lupalilo, Ikungula na maeneo mengine ambayo ameyataja Mheshimiwa Sanga hapa kadri ya upatikanaji wa fedha hizo. Kama nilivyomjibu Mheshimiwa Ngassa, kwa hiyo na tathmini inayofanyika hivi sasa na baada ya tathmini hiyo kukamilika, Serikali itatafuta fedha hizo na kuweza kupeleka huko.