Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Festo Richard Sanga (14 total)

MHE. FESTO R. SANGA Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itarudia zoezi la kuweka alama za mipaka kwa kuwashirikisha wananchi ili kumaliza mgogoro uliopo wa mipaka kati ya Hifadhi ya Kitulo na wananchi wa Vijiji vya Misiwa, Makwalanga, Igofi na Nkondo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mwaka 2016, Serikali ilishaweka alama za mipaka za kati kwenye maeneo ya Hifadhi ya Taifa Kitulo inayopakana na vijiji vya Misiwa, Mwakalanga, Igofi na mwaka 2018 katika Kijiji cha Nkondo.

Mheshimiwa Spika, zoezi hili la uwekaji wa alama lilishirikisha Kamati ya Usalama ya Wilaya ya Makete, Waheshimiwa Madiwani, Serikali za Vijiji, wananchi kwa ngazi ya vijiji, pamoja na wataalam wa ardhi kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Makete. Elimu ilitolewa kwa wananchi kuhusu zoezi la uwekaji alama za mipaka kwenye vijiji hivi kabla ya uwekaji wa alama za mipaka hiyo. Baada ya utoaji wa elimu, wananchi walichagua wawakilishi watano katika kila kijiji ili kujiunga na timu ya watumishi kutoka Hifadhini na wataalam wa ardhi kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Makete, ili kufanya utambuzi wa eneo la mipaka na kuweka mipaka hiyo kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Na.279 la Mwaka 2005 la uanzishwaji wa Hifadhi ya Taifa Kitulo.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa taarifa kwamba maeneo hayo tajwa yalikwishawekewa alama za mipaka na zoezi hilo liliwashirikisha wananchi kikamilifu. Lengo kuu la zoezi hilo lilikuwa ni kuhakikisha kuwa mipaka inaonekana bayana na pia shughuli za kibinadamu hazifanyiki ndani ya eneo la hifadhi.

Mheshimiwa Spika, ni imani yetu kwamba mgogoro wa mipaka kati ya Hifadhi ya Taifa Kitulo na vijiji vilivyotajwa ulishapatiwa suluhu kwa kuzingatia Tangazo la Serikali na tunachokiomba kutoka kwa wananchi ni ushirikiano wao ili kuhakikisha kuwa wanashiriki kikamilifu katika shughuli za uhifadhi.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga Stendi ya Mabasi Makete Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga Mbunge wa Jimbo la Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Makete katika Mwaka wa Fedha 2013/2014 ilitenga eneo lenye ukubwa wa ekari 3.1 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha kisasa cha mabasi.

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2014/ 2015 Halmashauri ilianza ujenzi kwa gharama ya shilingi milioni 40; na katika Mwaka wa Fedha 2022/2023 Halmashauri imepanga kutenga fedha kwenye mapato ya ndani ili kuendelea na ujenzi wa kituo hicho

Mheshimiwa Spika, Serikali inaishauri Halmashauri ya Wilaya ya Makete kufanya tathimini ya ujenzi wa kituo cha mabasi na kuandaa andiko ili kutafuta vyanzo vya fedha kwa ajili ya ujenzi. Ahsante sana.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza:-

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuitangaza Hifadhi ya Taifa ya Kitulo ili ifahamike kwa Watalii wa ndani na nje?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Hifadhi ya Taifa ya Kitulo ilianzishwa kwa GN Na. 279 ya mwaka 2005. Hifadhi hii ina sifa ya kipekee kwa kuwa na jamii mbalimbali za maua na kwa nyakati tofauti Serikali imeendelea kuitangaza hifadhi hii na nyingine ziilizopo hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati iliyopo kwa sasa ni kuendelea kuzitangaza hifadhi zote za Taifa ndani na nje ya nchi ikiwemo Hifadhi ya Taifa ya Kitulo. Miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na kuzitangaza Hifadhi za Taifa kupitia tovuti na mitandao ya Kijamii (Instagram, Facebook na Twitter) pamoja na kuandaa video na filamu mbalimbali na vilevile kuna kuimarisha miundombinu ya barabara ndani ya hifadhi ili kurahisisha kufikika kwa maeneo ya vivutio ndani ya hifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati mwingine ni kuzitangaza hifadhi hizi kupitia chaneli maalum ya “Tanzania Safari Channel”; vile vile kuandaa safari za mafunzo kwa wanahabari, mawakala na wadau mbalimbali wa utalii kwa lengo la kuwapa fursa ya kuvielewa vivutio vya utalii na kuvitangaza ndani na nje ya nchi; kujenga sehemu ya malazi ya bei nafuu kwa ajili ya wageni wa ndani na nje ya nchi; na mkakati mwingine ni kuvutia wawekezaji kujenga kambi za watalii au lodge zenye hadhi za Kimataifa, ambapo maeneo manne ya uwekezaji yamebainishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kuona umuhimu wa maeneo ya uhifadhi, bajeti ya mwaka 2021/2022 pamoja na masuala mengine, imezingatia uimarishaji wa utangazaji wa utalii na kuboresha miundombinu ikiwemo barabara, viwanja vya ndege na maeneo ya malazi ya wageni ili kuvutia watalii kutembelea maeneo hayo kwa urahisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza:-

Je, upi ni mkakati wa Serikali wa kuendeleza Shamba la Mifugo la Kitulo?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Shamba la Kitulo ni miongoni mwa mashamba matano ya Serikali ya kuzalisha mifugo na ni shamba pekee linalozalisha ng’ombe aina ya Freisian halisi (pure). Mkakati uliopo ni wa miaka mitatu (2020/2021 – 2022/ 2023) ambao umelenga kuendeleza shamba kwa kuongeza ng’ombe wazazi kutoka 350 hadi 700, kununua madume ya ng’ombe wazazi 20, kuboresha malisho kwa kupanda malisho eneo la hekta 150, kuimarisha huduma ya uhimilishaji kufikia uhimilisha wa ng’ombe 300 kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, katika kutekeleza mkakati huo, Wizara kupitia Bajeti ya Mwaka 2021/2022 imenunua madume matano ya ng’ombe wazazi kutoka shamba la Shafa Farm lililopo mkoani Iringa, kilo 400 za mbegu za malisho kutoka Marekani na kilo 100 kutoka Kenya kwa ajili ya kuongeza uzalishaji wa malisho. Aidha, shughuli nyingine ni uhimilishaji ambapo ng’ombe 135 wamehimilishwa na ununuzi wa tenki la kupoozea maziwa lenye ujazo wa lita 3,000 ambapo utaratibu wa manunuzi unakamilishwa.

Mheshimiwa Spika, Shamba la Kitulo linahitaji uwekezaji wa kiasi cha shilingi bilioni 6.6 ili kufikia kiwango cha juu cha uzalishaji. Aidha, uwekezaji huu utaendelea kufanywa na Serikali kadri ya upatikanaji wa fedha kwa kushirikiana na wadau wengine wa maendeleo.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Kituo cha Afya Ikuwo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuboresha huduma za afya katika Wilaya ya Makete, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Makete shilingi milioni 400 katika mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Ipelele. Ujenzi wa Kituo hicho umekamilika na kinatoa huduma zikiwemo huduma za dharura za upasuaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Makete shilingi milioni 150 kwa ajili ya ukamilishaji wa Zahanati za Usungilo, Nungu na Matenga. Vilevile, Mei 2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Makete shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Kitulo. Aidha, ombi la Kituo cha Afya Ikuwo limepokelewa na linafanyiwa tathimini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaipitia na kuiboresha Sera ya Ujenzi wa Zahanati kila Kijiji na Kituo cha Afya kila Kata ili ujenzi ufanyike kimkakati na kwa tija zaidi badala ya kila Kijiji na kila Kata. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA aliuza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutekeleza Mradi wa REA katika Wilaya ya Makete ili kuhakikisha umeme unafika kila Kijiji?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Makete ina jumla ya vijiji 93 na vijiji 56 vimekwisha fikishiwa umeme. Vijiji 37 ambavyo havikuwa na umeme vinapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA awamu ya III, mzunguko wa pili unaoendelea kutekelezwa na Mkandarasi M/S JV Silo Power Limited na Guangzhou Yidian Equipment Installation Company Limited. Mkandarasi anaendelea na kazi ya usanifu wa kina, upimaji, uandaaji wa michoro na manunuzi ya vifaa.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa kupeleka umeme katika Wilaya ya Makete unahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo kilovoti 33, zenye urefu wa kilomita 222.5; kilomita 37 ya njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4; ufungwaji transfoma 37 za KVA 50; pamoja na kuunganisha wateja wa awali 814. Gharama ya mradi ni Shilingi bilioni 9.95 na utekelezaji unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba, 2022.
MHE. NEEMA W. MGAYA K.ny. MHE. FESTO R. SANGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Bwawa la Umeme la Mto Lumakali Wilayani Makete?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO inaendelea na maandalizi ya utekelezaji wa Mradi wa Rumakali wa kuzalisha megawati 222 ulioko katika Wilaya ya Makete, Mkoani Njombe.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2022/2023 Serikali imetenga shilingi bilioni nane kwa ajili ya maandalizi ya awali ya mradi wa Rumakali. TANESCO imehuisha upembuzi yakinifu pamoja na kukamilisha nyaraka za zabuni za kumpata mkandarasi wa ujenzi. Aidha, uthamini wa mali za wananchi zinazopitiwa na mradi utakamilika mwezi Oktoba, 2022. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kuanza mwaka ujao.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza: -

Je, nini mkakati wa Serikali kuondoa changamoto ya Lumbesa kwa wakulima wa zao la viazi nchini?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA aljibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali kupitia Sheria ya Vipimo, Sura 340, mapitio ya mwaka 2002 na marekebisho yake ya mwaka 2018 wa kuondoa changamoto ya lumbesa ni kuendelea kutoa elimu kwa umma juu ya matumizi sahihi ya vipimo. Mazao ya mashambani ikiwemo viazi yatafungashwa kwa uzito usiozidi kilogramu 100 na hatua zitachukuliwa kwa wote watakaobainika kuvunja sheria hiyo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza: -

Je, ni hatua gani ya upembuzi yakinifu wa barabara ya Chimala – Matamba hadi Kitulo imefikiwa na lini ujenzi utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Chimala – Matamba yenye urefu wa kilometa 20.1 ni barabara ya Wilaya ambayo imekasimiwa kwa TANROADS kuanzia mwaka wa fedha 2023/2024. Baada ya kukasimiwa TANROADS, barabara yote kuanzia Chimala – Matamba hadi Kitulo ambayo itakuwa na urefu wa kilometa 41.1 itaingizwa kwenye mpango wa kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami katika mwaka wa fedha wa 2023/2024, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaongeza majengo katika Kituo cha Afya cha Matamba Wilayani Makete?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka 2018 hadi 2022 Serikali ilitenga na kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya vinne vya Ipelele, Kitulo, Bulongwa na Lupalilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi na upanuzi wa vituo vya afya kwenye maeneo ya kimkakati ikiwemo kuongeza majengo ya Kituo cha Afya Matamba katika Halmashauri ya Wilaya ya Makete kadri ya fedha zitakavyopatikana.
MHE. FESTO R. SANGA: Aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuitangaza Hifadhi ya Taifa ya Kitulo?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuitangaza hifadhi ya Taifa Kitulo Kitaifa na Kimataifa kwenye maonyesho na matamasha mbalimbali kama vile Karibu Kusini, Kili-fair, Sabasaba, na Nanenane. Pia, tumeanza kuitangaza kwa njia ya kidigitali, mitandao ya kijamii, majarida na Safari Channel. Lengo ni kuvutia watalii na wawekezaji.

Mheshimiwa Spika, aidha, Wizara imeanza kuboresha miundombinu ndani ya hifadhi ikiwemo ujenzi wa nyumba tatu na tunatarajia kujenga nyumba mbili na kambi moja ya kuweka hema katika mwaka huu wa fedha wa 2023/2024, pamoja na kukarabati miundombinu ya barabara.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza:-

Je, lini wananchi waliopitiwa na ujenzi wa Bwawa la Umeme la Mto Lumakali Makete watalipwa fidia?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa ujenzi wa Bwawa la Mto Lumakali unalenga kuzalisha umeme wa MW 222 kwa kutumia maji ya Mto Lumakali mkoani Njombe na unahusisha pia ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme yenye msongo wa kV 220 yenye urefu wa kilometa 65 kutoka kwenye mitambo hadi Kituo cha Kupoza Umeme cha Iganjo mkoani Mbeya. Gharama za ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme ni takribani shilingi trilioni 1.42 na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ni takribani shilingi bilioni 50.3.

Mheshimiwa Naibu Spika, tathmini ya awali ya mali za wananchi wanaopisha Mradi wa Ujenzi Bwawa la Umeme la Mto Lumakali imekamilika na Serikali imetenga fedha katika mwaka wa fedha 2023/2024 kwa ajili ya kuanza malipo ya fidia kwa wananchi hao. Kwa sasa kazi ya uhakiki inaendelea kwa mwezi Juni, 2023 na baada ya kazi hiyo kukamilika malipo ya fidia kwa wananchi wanaopisha mradi yanatarajiwa kuanza kulipwa kuanzia mwezi Julai, 2023, nashukuru.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Hospitali mpya ya Wilaya ya Makete?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imeitenga shilingi milioni 900 kwa ajili ya kufanya ujenzi na ukarabati wa majengo ya Hospitali hiyo ili iweze kuwa na miundombinu bora yenye hadhi ya Hospitali ya Wilaya, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza: -

Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa mradi wa maji Kata ya Iwawa Makete Mjini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali inaendelea na utekelezaji wa mradi wa maji wa kuhudumia Kata ya Iwawa kwa kutumia chanzo cha Mto Isapulano. Mradi huu unahusisha ujenzi wa chanzo, ulazaji wa bomba kuu umbali wa kilometa 12.5, ulazaji wa mabomba na usambazaji umbali wa kilometa 39 na ujenzi wa matanki matatu yenye ujazo wa lita 450,000. Utekelezaji wa mradi huo unatarajiwa kukamilika katika mwaka wa fedha 2022/2023.