Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Festo Richard Sanga (32 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama kwenye Bunge hili, nipende kumshukuru kwanza Mwenyezi Mungu kwa nafasi niliyoipata. Pia niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Makete kwa kuniamini na kunichagua kuwa Mbunge wao. Kubwa zaidi nimpongeze Mheshimiwa Rais na Wabunge wote wa Chama cha Mapinduzi kwa ushindi mkubwa walioupata, ni kitu ambacho mimi kama Mbunge kwa kweli niseme hongereni sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais naomba kuchangia mambo matatu. Jambo la kwanza naomba kuchangia kwenye sekta ya barabara. Tumeona jitihada za Rais akipambana kuhakikisha kwamba barabara zinajengwa kwenye kila kona ya nchi hii, wilaya na kila mkoa. Kwa kule Makete sisi tumepata barabara kutoka Njombe kuelekea Makete ambayo imekamilika kwa kiwango cha lami. Naomba kuishauri na kuiomba Serikali tuna barabara ya kutoka Makete kuelekea Mbeya, moja kati ya barabara ambazo zimebeba msingi wa uchumi wa Wilaya ya Makete, nawaomba na nawasihi sana wahusika ambao ni Wizara ya Ujenzi waiangalie barabara hii kwa jicho la karibu ili wananchi wa Makete waweze kupata huduma hiyo ya barabara ya lami, kwa sababu uchumi wa Makete unakua lakini unakwamishwa na barabara hiyo ambayo kwa kweli ni barabara muhimu wa Wilaya ya Makete.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, naomba nichangie kwenye sekta ya kilimo. Sisi Makete ni wilaya ya kazi kama ambavyo wananchi wengi wa Tanzania wanafahamu wananchi wa Makete ni watu wa kazi. Kwenye kilimo Mheshimiwa Rais ameonyesha kwenye hotuba kwamba ana lengo la kuboresha kilimo. Changamoto ya kwanza kwa wananchi wa Makete tunalia na lumbesa kwa ajili ya wananchi wetu na wakulima wetu wa Makete. Wakulima wanalima lakini tatizo la lumbesa kwa wananchi wetu ni kubwa. Naishauri Serikali mambo matatu; ushauri wa kwanza kwenye Serikali ni jambo moja, kwanza Wakala wa Vipimo waoneshe kipimo kipi ni rasmi kwa ajili ya kuuzia mazao yetu ya mahindi pamoja na viazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, naomba Wizara husika ya Kilimo waanzishe sales point (vituo vya kuuzia) ili wakulima wetu waweze kuwa controlled kwenye biashara kuondokana na suala la lumbesa. Lumbesa ni kilio, wananchi wangu wa Matamba, Makete na Ujuni wanalia na lumbesa, tunaomba sana ili tuweze kumboresha mkulima huyu lazima tuondoe suala la lumbesa na nawasihi na kuwaomba sana Wizara husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la tatu, naomba kuchangia kwenye suala la mapato. Rais amezungumza mambo mengi sana; hapa tuna mambo ya ujenzi wa barabara, tuna mambo ya umeme, tuna mambo mengi ya kiuchumi ambayo yanahitaji fedha, lakini kuna eneo moja ambalo tumeliacha kwa muda mrefu fedha nyingi zinapotea, nako ni kwenye suala la tozo, kwa maana ya kwamba non tax revenue. Rais amepambana kwa level yake, kwa maana ya kwamba ukiangalia kwenye eneo kama la vitambulisho vya wajasiriamali, mambo ya magawio saa hizi tumeanza kuyapata, naiomba na kuishauri Serikali waanzishe authority kwa maana non tax revenue authority ili iweze kukusanya tozo hizi ambazo zimekuwa zikipotea. Mambo ya fees na mengine yanapotea huko na wafanyabiashara wetu wengi wanahangaika kuona kwamba wanafuatwa fuatwa sana na watu ambao ni wa tozo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba ili tuwasaidie wafanyabiashara, ukifuatilia wafanyabiashara wengi ndani ya nchi yetu ya Tanzania wanaotaka kuanzisha biashara ndogondogo, wanafuatwa na watu wa tozo wengi wengi sana, mtu anaanzisha biashara, hajatulia anaingia mtu wa TBS, anaingia mtu wa NEMC, anaingia mtu wa OSHA, anaingia mtu wa Fire, anaingia mtu wa TFDA, mfanyabiashara huyo ambaye tunatamani awe bilionea kama Rais anavyotaka, atawezaje kama hatuwezi kuanzisha kitu ambacho ni kimoja, tuweza kuweka single point, huyu mtu akilipa kwa pamoja Serikali itafute jinsi gani inaweza ikagawana hayo mapato, siyo kufunga safari kwa kwa mfanyabiashara mmoja watu 20 kwenye Serikali ile ile. Naisihi na naiomba Serikali ianzishe Non Tax Revenue Authority ili tuweze ku-control hizi tozo ndogondogo ambazo zinapotea.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hapo niendelee kumpongeza Rais hata kwa wenzetu tulionao humu ndani ya Bunge, wa upande wa pili, ni kwa sababu Rais aliruhusu demokrasia kwenye nchi hii ndiyo maana na wao wapo. Ninachowasihi ni jambo moja, wawe watulivu, walikotoka wanalaumiwa na hapa wanatulaumu sisi, sasa hawajielewi walipo, wafanyiwe counseling tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa kupewa nafasi ili niweze kuwasilisha mambo machache ya kuishauri Serikali. Vilevile niishukuru Serikali kwa Mpango huu wa Miaka Mitano na hata huu wa Mwaka Mmoja ambao umeletwa mbele yetu kwa ajili ya kuujadili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie mambo matatu. Jambo la kwanza ambalo nataka kulizungumzia ni kwenye sekta ya elimu. Kwenye sekta ya elimu nataka kuzungumzia jambo moja. Rais wetu tuliye naye kwa sasa alikuja na mpango mkakati wa kuhakikisha kwamba, kila shule inakuwa na madawati. Mpango huu ambao Rais alituletea hatujauona nini ambacho Serikali inapanga kwenda kukifanya kuhakikisha kwamba, kila mwaka shule zinakuwa na uhakika wa madawati kuliko kuwa na huu mtindo wa zimamoto. Sijaona mpango wa kuona Serikali na sekta ya viwanda wakijadiliana kwamba, wana uwezo wa kujenga angalau kiwanda kimoja cha kimkakati Mkoa wa Njombe au mkoa wowote ambao unatoa malighafi kama mbao, ili Serikali iweze kupata madawati kwa uhakika kwa ajili ya shule zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukulia mfano mwaka 1985, Mwalimu Nyerere aliamua kujenga kiwanda cha Mgololo kwa ajili ya karatasi, ili shule zetu ziwe na uhakika wa kupata madaftari. Kiwanda hiki kilifanikiwa, lakini kwa sasa kwenye hili suala la madawati hatuoni jitihada zozote ambazo zinafanyika za makusudi za Serikali kuona inajenga kiwanda ambacho kinaweza kikasaidia kupata furniture mbalimbali kwa ajili ya Serikali yetu na kwa ajili ya shule zetu. Sisi watu wa Mkoa wa Njombe tuko tayari ku-offer maeneo kama haya ya viwanda kusaidia Serikali yetu iweze kupata haya mambo ya madawati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nataka nichangie; wewe ni Mbunge wa Kongwa, NARCO ilianzishwa kwa ajili ya kuendesha hifadhi za Taifa, lakini tumeona NARCO ikijikita kwenye kutatua tu migogoro. Miaka inaenda, miaka inarudi hifadhi ya Kongwa pale toka Nyerere alivyoiacha ng’ombe ni walewale inawezekana na idadi imepungua, hakuna ng’ombe wanaoongezeka. NARCO inafanya kazi gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, wewe kwako Kongwa pale, kuna eneo kubwa ambalo hata Watanzania wangetengewa tu sehemu kidogo tu wapewe vile vitalu wafuge, angalau tungeona kwamba, kuna jitihada zinafanyika. Leo ukienda pale Ruvu mradi wa zaidi ya bilioni
5.7 wa machinjio ya kisasa umekufa. NARCO wapo na mambo yanaendelea, wamejikita Misenyi, wamejikita Kagera kwenye kutatua migogoro ya wafugaji tu, lakini NARCO haina mkakati wowote ambao tunauona kwenye Mpango hapa ukurasa wa 89, Kuendeleza Ranch za Taifa. Maeneo yamebaki ni makubwa, hayana msaada wowote kwa Watanzania, ni vema wananchi wangegawiwa, waweze kufuga ili Serikali iweze kukusanya kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni kwenye sekta ya wafanyabiashara. Hivi ninavyozungumza wafanyabiashara Makete, akina mama mafundi cherehani wanaambiwa wawe na mashine ya EFD. Ni masikitiko makubwa kwamba huyu mtu ana kitenge anashona anaambiwa awe na mashine ya EFD. Kodi now is not to collect they are just trying to grab it kitu ambacho siyo kizuri kwa sababu wananchi wetu wana uchumi mdogo, wana tozo nyingi lakini pili ukamuaji wake umekuwa ni wa tofauti. Hata ng’ombe unayemkamua unatafuta jinsi ya kumkamua, unamlisha, unazungumza naye lakini sisi TRA yetu hawafanyi jambo hilo, wanakusanya kodi kwa nguvu. Pia naendelea kusisitiza tozo ni nyingi na zimegeuka kero kwa wafanyabiashara wadogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasihi na naomba TRA watafute mazingira bora na salama. Mbona Rais ametusaidia vitambulisho vya wajasiriamali vimeondoa kero za wafanyabiashara wetu kukamatwa mitaani na mgambo, watafute njia sahihi ya kukusanya kodi. Nashauri wakusanye kodi kwa utaratibu siyo kutuma tax force kama Mheshimiwa Nape alivyosema, wanaenda wanakamata maofisi ya watu na kompyuta za watu, huyo mtu utegemee kesho akusaidie tena kulipa kodi? Ni jambo ambalo linasikitisha, tunaomba TRA wasaidie wafanyabiashara wetu wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kama ambavyo leo tuna vitabu vinavyoonyesha kwamba Wizara ya Kilimo kuna tozo ambazo imeziondoa kwa maana kwamba ni tozo kero, ndivyo tunavyotamani kwamba keshokutwa kwenye Bunge linalofuata au Bunge la mwakani tuje na kitabu kutoka TRA kinachosema hizi tozo ambazo ni za hovyo kwa wafanyabiashara zimepungua kwa sababu wafanyabiashara wetu wanaumizwa. Vijana wadogo ajira mtaani hamna wakitaka kufungua biashara TRA wameingia, watu wa OSHA wameingia, watu wa Bima wameingia, watu wa lift wameingia yaani hadi kukagua lift kukagua ni Sh.400,000 kwa mwaka, lift? Sasa huyu mtu ata-survive vipi na tunatamani tuendelee kukusanya kodi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali hii nchi itajengwa na wenye moyo ambao ni sisi lakini kama mkiendelea kubomoa wafanyabiashara wadogo hatuwezi kukusanya kodi. Mwisho wa siku tunachoomba Wizara husika watuletee takwimu kama idadi ya wafanyabiashara inaongezeka au inapungua kwenye taifa hili. Kwa sababu kila siku wafanyabiashara wanalia kutokana na changamoto za tozo, wapunguze tozo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, mchango mwingine nitaleta kwa maandishi lakini kwa kweli Watanzania wana matumaini makubwa na Mpango huu, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nipende kumshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Mwigulu Nchemba Waziri wa Fedha kwa hotuba yake nzuri ya mpango ambao tunaujadili kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwenye mpango huu naomba nizungumzie jambo moja tu ambalo linahusu sekta ya michezo; na mimi ni mdau wa michezo na nimekuwa kiongozi wa michezo kwenye nchi hii. Kwa leo naomba niitakie kila la heri timu ya Simba Sports Club kwenye mchezo wake pale Misri, na ninaamini kwamba hata wanayanga wenyewe wanaendelea kutuunga mkono kama ambavyo imekuwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye michezo naomba nizungumzie mambo kadha wa kadha. Ninaanza na jambo suala la sheria namba moja kwenye kanuni 17, sheria 17 za mpira wa miguu ambazo zinahusu mambo ya viwanja vya mpira.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanzania tumebahatika sana, takriban kila mkoa tunaviwanja vya mpira wa miguu. Serikali kwa muda mrefu lakini pili sisi kama Chama cha Mapinduzi kwenye ilani yetu kwa muda mrefu tumekuwa tukiweka kwamba tunauwezo na tunafursa ya kuviendeleza viwanja vyetu vya mpira wa miguu. Ukienda ukurasa namba 30, 245 kwenye ilani ya mwaka huu inazungumzia ujenzi wa viwanja kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tulibahatika Mwalimu Nyerere alijenga viwanja maeneo mazuri na viwanja vikubwa ambavyo hadi leo kizazi hiki inavitumia. Hata hivyo sijaona mpango wa moja kwa moja kwa Serikali na Chama cha Mapinduzi ambao ni wamiliki wa viwanja hivi kuendeleza viwanja vya mpira wa miguu. Tumeishia kulalamika kwamba viwanja sio bora, sio vizuri lakini hakuna hatua ya moja kwa moja ambayo Serikali imekuwa ikifanya na kuichukua kwa kuhakikisha kwamba inaviendeleza viwanja hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe na niishauri Serikali. Viwanja vipo maeneo mengi na maeneo potential, viwanja kama Sokoine, CCM Kirumba, Ali Hassan Mwinyi – Tabora, vinahitaji tu fedha ya kuweka hata carpet tu mpira uchezwe kwa sababu majukwaa Nyerere alishatujengea, yako imara na yako vizuri, kinachohitajika ni fedha tu zitengwe kwa ajili ya kuweka hata carpet.

Mheshimiwa naibu Spika, niunganishe moja kwa moja, tunahitaji kuwa mpango wa moja kwa moja. Sisi wote hapa tunafurahia leo, kwamba timu zinacheza vizuri, Timu ya Simba, timu ya taifa zote zinacheza vizuri, lakini ikifungwa tunaanza kulaumu. Hata hivyo kusudi na malengo ya moja kwa moja ya Serikali kuendeleza michezo hatujaiona. Tunazungumzia viwanja hivi lakini hadi sasa hatujaona Serikali ikitoa kodi kwenye vifaa vya michezo. For instance, hizo carpet ambazo tunazizungumzia, ingetenga hata mwaka mmoja kwamba huu ni mwaka wa exemption kwenye vifaa vya michezo kwa ajili ya kutandika carpet kwenye nchi yetu; hata viwanja viwili viwili tu kwa kila mwaka, kwa muda wa miaka mitano tunaviwanja 10 vimetandikwa kapeti mpira wetu unachezwa na watoto wanaweza kupata sehemu ya kuchezea.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali iondoe kodi au iweke tax exemption kwenye vifaa vya michezo; kuanzia jezi lakini pia hizo carpet ambazo tunaweza tukazitandika kwa ajili ya viwanja vyetu hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu pika, jambo linguine, zamani wakati tupo na timu ya taifa tulikuwa na shule nyingi ambazo zinazilisha wachezaji; mathalani shule kama ya Makongo, ambayo ilizalisha wachezaji wengi ambao tulikuwa tunawasifia wakina Kaseja na wachezaji wengine. Tunaomba mpango wa makusudi wa Serikali kujenga shule maalum kwa ajili ya michezo kwenye taifa hili. Shule ambazo either zinaweza zikawa za zonal kwa maana ya kanda kama Dodoma, Mbeya, Mwanza na hata Kusini wajenge shule angalau 10 au tano za michezo tu ambazo zitakuwa zina- feed timu yetu ya taifa na vilabu vyetu vya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu wachezaji wetu ambao tunao hapa hawana uchezaji wa mpira ambao umepitia kwenye darasa, wengi wametokea mitaani, hawana shule maalum kwa ajili ya taifa letu ambazo zinasimamiwa ama na TFF ama na Serikali. Tunahitaji kuwa mpango wa muda mrefu kuhakikisha kwamba michezo ya taifa hili inakuwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe sana Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Waziri wa Fedha, yeye ni mdau wa michezo wa moja kwa moja. Leo hii yeye ni Waziri wa Fedha; aone haja ya moja kwa moja kuinua soka la nchi hii. Amekuwa na club ya Singida United na amewaona jinsi ambavyo ni ngumu kuiendesha; ni kwa sababu timu nyingi hazina fedha. Je? haoni sasa kuna haja ya Serikali, kama nilivyosema, kuondoa kodi kwenye hivyo vifaa? Na isiwe tu kuondoa kodi kwenye hivyo vifaa, lakini pia kampuni, kama betting companies, ambazo zipo ndani ya nchi hii zizonafanya kazi za betting nchi hii haziwezi kujiendesha kama si mpira, maana yake wananufaika moja kwa moja na mpira wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, je? Serikali haioni fursa kwa sasa, kwamba kampuni zote za betting ziwekewe angalau sheria au utaratibu? Kwamba kila kampuni ya betting iwe na uwezo wa ku-finance au kuchangia au ku-sponsor timu yoyote ya ligi kuu? Ziwe za wanawake au timu ya taifa, au timu hizi ambazo tunazo kwa sasa?

Mheshimiwa Naibu Spika, tuione fursa ili betting companies ziweze ku-support kwenye mpira wa Tanzania kwa sababu nazo existence yake, uwepo wake hapa nchini ni kwasababu ya mpira wetu. Kwa hiyo nimuombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Serikali muone haja ya kuweka mazingira salama kwa ajili ya timu zetu kuweza kupata fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuendesha timu za ligi kuu ni kazi ngumu sana, vijana hawa hawana hela, hawana fedha, tunahitaji hatua za makusudi kuwa-support, na kuwaunga mkono.

Mheshimiwa Waziri wa Fedha nikusihi na nikuombe, tax exemption kwenye vifaa vya michezo lakini pili hizi kampuni zingine za betting; lakini si kampuni za betting tu. Tuchukue hata utaratibu ule wa Zambia kipindi cha Kenneth Kaunda kwenye kampuni ya migodi; aliamua kutangaza wazi kama kuna kampuni ipo tayari ku-finance vilabu vya ligi kuu vya nchi yetu; ile KK11 ilikuwa financed na makampuni ya migodi, kwamba tutawaondolea sehemu ya kodi hiyo kodi ipelekwe kwenye michezo; fanyeni hivyo ili msa-port michezo ya nchi yetu hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ambalo nataka nizungumzie, sitazungumza kwa muda mrefu sana; ni jinsi gani ambavyo tunaweza kulinda wawekezaji kwenye michezo yetu? Nataka hapa niweke case study ya Simba Sport Club na hata Young African wanatuunga.

Mheshimiwa Naibu Spika, Simba imepata uwekezaji ambao wanahainga nao na upo kwenye public na Serikali imeingilia kwamba inasimamia ule mchakato uende salama, the same to Young African, wana uwekezaji ambao mchakato wake wameshauanza. Sasa, je wawekezaji wetu wanalindwa? Hawalindwi, intimidation na frustration kwa wawekezaji wetu zimekuwa ni kubwa kwa kiwango ambacho wawekezaji wakati mwingine wanataka hata kukata tamaa. Simba leo ambao tunajivunia, kila mmoja anajikonga kifua kwamba ni Simba kwa sababu inafanya performance ni kwa sababu muwekezaji yule ameweka fedha pale, ameweka fedha lakini kuna watu wanajitokeza wanawa-frustrate kati kati ya mapambano.

Mheshimiwa Naibu Spika, Simba leo ikibeba klabu bingwa Africa, Tanzania itatangazwa all over the world. Si hivyo tu pia tutafungua nafasi kwa mawakala wa wachezaji kuja kufuatilia soka letu la Tanzania. Je, wawekezaji wetu wanalindwa? Serikali ione haja, watu ambao wana- frustrate wawekezaji, kama Mheshimiwa Rais alivyosema, wawekezaji wasibughudhiwe. Yule mwekezaji si mwizi, mchakato upo open kabisa, uko wazi lakini amekuwa frustrated kwa muda mrefu. Akifanya hiki huyu anaingia anasema hivi, akifanya hiki huyu anaingia anasema tunakata bilioni 20. Bilioni 20 hasa hasa kwa Simba Sport Club? Kwa posho ya mwaka huu is over one billion, posho tu. Mwekezaji anaweka over 1.5 billion ruzuku, what is bilioni 20 kwa Simba iliyookolewa hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuombe uwezekano wa Serikali kulinda wawekezaji ambao wanaingiliwa, hasa kipindi kama hiki ambacho Simba inaenda kuchukua ubingwa na kuweka historia kwenye taifa letu. Kwa hiyo lazima tuwalinde.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunalisema hili kimasihara, lakini niseme wazi, Simba inaenda kuandika historia nyingine. Je, hii historia inayoenda kuandikwa inalindwa? Simba inaenda kwenye robo fainali mtu mwingine anajitokeza anatoka billioni 20, billioni 20 za nini? mshahara wa Chama, mshahara wa Bernard Morrison ni zaidi ya billioni 20. Mtu kaamua kuwekeza kwa maslahi na mapenzi ya soka Tanzania, ni vema akapewa heshima na akalindwa. Serikali ione haja ya kuwaita pembeni watu ambao wana-frustrate na ku-intimidate na kuwaambia kwamba huu mchakato haujaisha na si mchakato wa wizi, ni mchakato uko wazi na wanasimba wameridhia kwenye mkutano mkuu wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuombe, Serikali iendelee kulinda. Vilevile na Dar Young African tunawatakia kila la heri, tunajua nanyi mnaenda huko, mnatufata sisi, tunaamini mtafanikiwa. Sasa na ninyi mkiruhusu michakato hii watu kuingilia wawekezaji watakata tamaa, GSM watajitoa pale Yanga kwa sababu watu hamlindi wawekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo lingine ni kuhusu suala la kusaidiwa kwa TFF. TFF ni chombo chetu ambacho tunacho, kinafanya kazi, lakini mzigo wa TFF ni mkubwa. Ninaishukuru Serikali ya Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Kikwete aliamua kuchukua sehemu ya mishahara ya bench la TFF, akasaidia kuibeba TFF, kwa maana ya kulipa makocha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuisaidie TFF, TFFkwa pale walipofikia bajeti yao ni ndogo sana. Timu ya taifa tunatamani ifanya vizuri, kufanya vizuri kwa timu ya taifa ndivyo taifa letu linavyoendelea kutangaza kimichezo na kuendelea kufungua fursa. Serikali inaweza ikachukua jukumu hata la kulipa mishahara tu ya makocha ikasaidia TFF. TFFyetu pale tukiangalia ofisi zao hazina hadhi. Somalia kuna vita lakini wana ofisi nzuri kuliko hata ofisi yetu ya TFF. Ni kitu ambacho kinatia aibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ione haja ya hata kuishauri TFF wajenge majengo yenye hadhi nzuri, lakini si hadhi nzuri tu bali pia muipokee mzigo, mzigo wa TFF ni mkubwa, wamejitahdi kwa level yao. Leo hii tuna timu za wanawake na tuna timu ya taifa zinafanya vizuri na vile vile kuna vilabu ambavyo vinafanya vizuri. Basi Serikali ione sasa, kwamba hawa wenzetu wanapambana kwa level hii lakini kuna majukumu mengine tuwapunguzie, miongoni ni suala la mishahara, wapunguziwe mishahara TFF, Serikali ione haja jinsi kuingilia na kuwasaidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini zaidi ya hapo tuseme tu, Serikali muendelee kuiunga mkono Simba, inaenda kuandika historia ya tofauti kwenye Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara ambayo hata mimi pia ni Wizara ambayo nimehusika kwenye kufanya kazi, kwa maana ya sekta ya michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina mambo mawili ya kuchangia kwenye Wizara hii, jambo la kwanza ni suala la soka, lakini suala la pili ni suala la BASATA.

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza mwekezaji mkubwa aliyeingia kwenye mpira wa miguu, kwa maana ya Azam Media Group kwa kile kitendo alichokifanya ndani ya nchi yetu. Azam Media Group wamewekeza zaidi ya shilingi bilioni 225 kwenye soka la Tanzania na ndio kitu cha kwanza kimefanyika kwenye East Africa, hakuna nchi yoyote ambayo haki ya matangazo imepata shilingi bilioni 225 kwa wakati mmoja ni Tanzania tu imetokea, lakini tu kitendo hiki hakiipi manufaa soka, kitendo hiki kinaipatia Serikali shilingi bilioni 34 kama kodi, kitu ambacho kwa miaka yote hakijawahi tokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kattika kufanya hilo nataka nizungumzie suala la viwanja. Mwekezaji huyu amewekeza fedha zote hizi kwenye soka la Tanzania; ana tv production yenye quality nzuri kama tunaangalia premier league Uingereza, lakini viwanja tulivyonavyo vinatimua vumbi. Inatia hasara sana kwa sababu gani, leo hii tunazungumzia shilingi bilioni 34 ambayo Bakhresa anaenda kuipatia kama kodi nchi hii, bajeti ya Serikali ni shilingi bilioni 54 ya mwaka mzima ya Wizara ya Michezo, lakini bado Serikali haioni haja ya kuhakikisha viwanja hivi vinaenda kuwekwa mikeka ambayo Tanzania nzima tungekuwa tunajivunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nikupe mahesabu machache tu; kiwanja kimoja kuweka mkeka ni shilingi milioni 300; kwenye shilingi milioni 300 maana yake unazungumzia shilingi bilioni tatu ni viwanja 10 na shilingi bilioni sita ni viwanja 20 ambavyo unakuwa umemaliza nchi nzima. Tuiombe Serikali na hapa Mheshimiwa Waziri na nimuombe Mheshimiwa Waziri Mkuu na niiombe Serikali na nimuombe Rais, kama tumeweza kupata shilingi bilioni 34 kwa wakati mmoja tunashindwaje kutenga shilingi bilioni sita tu katika shilingi bilioni 34 tukaweka mkeka nchi nzima na tukawa tumefuta historia ya viwanja katika Taifa hili? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inatia hasira na inasikitisha sana. Utakuja na hoja hapa kwamba hivi viwanja vinamilikiwa na CCM, inawezekanaje baba ambaye ni CCM anashindwa kuongea na mtoto ambaye ni Serikali ili Watanzania waweze kupata nyasi nzuri kwenye Taifa hili? Inawezekanaje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kubaki kwenye michakato, michakato, michakato kuhusu viwanja. CCM kwenye sera yake/kwenye ilani inasema; tutaboresha mazingira ya michezo nchini. Michezo ipi nchini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ukienda pia kwenye Sera ya Michezo ya mwaka 1995 inazungumzia suala la kuboresha viwanja nchini. Serikali inazungumzia kuboresha viwanja, CCM inazungumzia kuboresha viwanja, lakini nenda Jamhuri pale Dodoma angalia, Wabunge tunafanya mazoezi kwenye vumbi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuiombe Serikali na nimuombe Rais, shilingi bilioni 34 atupe bilioni sita tu. Haya mambo ya negotiation kati ya CCM na Serikali yabaki kwao sisi tuone nyasi zinacheza, watoto wa Kitanzania wacheze mpira sehemu nzuri. (Makofi)

Mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri una fursa ya kuandika historia kwenye Taifa hili, una fursa ya kufanya vijana wote wa Tanzania wakusifie, nenda ongea na Rais, ongea na Wizara ya Fedha wakupatie shilingi bilioni sita, weka viwanja…

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Taarifa. Endelea nimekuruhusu.

T A A R I F A

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa Taarifa mzungumzaji katika hoja yake ya viwanja. Yaani hivyo viwanja vya mpira ndio vimegeuzwa pia sasa viwanja vya kila maonesho, viwanja vya bongo flavor kama anavyosema Babu Tale, viwanja vya gospel, yaani kila mtu anayetaka kufanya kitu chake anaenda kwenye hivyo viwanja vya mpira. Na matokeo yake ndio haya ambayo tunaona sasa fedha imewekezwa, lakini wapi tutachezea?

SPIKA: Mheshimiwa Sanga.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, naipokea Taarifa yake kwa sababu ni kweli na amesahau tu kusema pia hata gwaride la majeshi linafanyikia kwenye viwanja hivyo hivyo. Tungekuwa na viwanja ambavyo vina nyasi za bandia, mnazungumza viwanja vyenye nyasi za bandia visingekuwa vinaharibika kama ambavyo vinaharibika hivi. Leo hii ukipanda nyasi kesho kutwa JKT wameingia wanapiga gwaride, nyasi zimekanyagwa zote zimeisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuiombe Serikali angalieni haja, michakato kati ya CCM na Serikali isituumize Watanzania tunaopenda mpira kwenye Taifa hili. Tunaomba shilingi bilioni sita katika shilingi bilioni 34 ambazo mmezipata Serikali mtuwekee viwanja carpet tumalizane na nyie endeleeni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mwalimu Nyerere alijenga viwanja Taifa hili kila kona. Leo wakikwambia utafute uwanja kama wa Jamhuri hapa Dodoma ujenge, utapata sehemu gani ya kujenga uwanja mkubwa kama ule? Nenda Mkwakwani, nenda Sokoine, nenda Ali Hassan Mwinyi pale Tabora, lakini nenda CCM Kirumba wakwambie leo jenga, Nyerere alijenga, sisi Taifa la leo tunashindwa? Watu milioni 55 tunashindwa kuweka nyasi za bandia kwenye Taifa hili? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Nyerere ameweka majengo yote yale tunakaa. Kwa kweli, niombe Mheshimiwa Waziri, nitashika shilingi kama haya mambo hamtayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine nipende kuzungumzia, sitakuwa na mambo mengi; jambo lingine ni suala la BASATA. Ukiangalia BASATA ni Baraza la Sanaa la Taifa, lakini saa hizi imegeuka ni Mahakama ya Sanaa ya Taifa, kitu ambacho mimi niseme kitu kimoja, wasanii wa nchi hii asilimia 90 wamejipambania wao wenyewe hadi pale walipofikia na si kwa jitihada za sekta ya Wizara ya Michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo Diamond ametoka si kwa sababu alipita Chuo cha Bagamoyo, leo Ali Kiba ametoka si kwa sababu alipita Chuo cha Muziki Bagamoyo, ametoka kwa jitihada zake, lakini BASATA wanatengeneza urasimu wa kwamba waanze kuweka kwamba wimbo kabla haujatoka lazima upitie kwao, ukaguliwe ili waangalie ubora wa huo wimbo. Hiki kitu ni mlango, hili ni dirisha la kuwaumiza wasanii; ndio maana nasema ni mahakama, kwa nini?

Mheshimiwa Spika, leo hii kama kuna mtu ana bifu (ugomvi) na Ali Kiba, Ali Kiba akitoa wimbo huyo mtu anazunguka BASATA anawapa hela BASATA wanazuia ule wimbo. Tunatengeneza wizi, katika hili nimheshimu Mheshimiwa Waziri kwa sababu aliingilia kati akajenga heshima kwenye nchi, hali imetulia. Msingefanya vile mnataka kumgombanisha Rais na wasanii wa Tanzania hii kwa uzembe wa BASATA. BASATA kazi zake ilizonazo, kazi ambazo BASATA wanazo ni kusimamia maendeleo ya muziki wala sio kufungia wasanii na wala sio kufungia muziki kwenye Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unapomfungia Diamond, diamond peke yake unapomfungia maana yake umefungia wasanii wengine walioko nyuma yake, maana yake umefungia producer wa muziki, maana yake umefungia bodyguards wake, maana yake umefungia shughuli nyingi asimame asifanye kazi.

Mheshimiwa Spika, sasa tutakuwa tunazalisha wasanii au tunaonesha? Ndio zile sheria ambazo ulisema ni za kikoloni, zimejikita kwenye kudhibiti kuliko ku-facilitate wasanii wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuombe BASATA hawana jukumu lingine la kufanya Taifa hili zaidi kusimamia muziki uwe bora. Diamond amefika pale si kwa ajili ya nguvu ya BASATA, leo hii Ali Kiba amefika pale si kwa ajili ya nguvu ya BASATA, wala Harmonize alipo si kwa ajili ya nguvu ya BASATA. BASATA wasimamie tu maudhui kama wimbo ni mbovu wausimamishe, waurekebishe uendelee kufanya kazi, lakini hili jambo ambalo nyie BASATA mnalifanya hatutawaacha, hatutawaacha salama…

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa, nimekuruhusu Mheshimiwa Saashisha.

T A A R I F A

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante, nataka kumpa msemaji tTaarifa kwamba pamoja na mchango wake mzuri na kule kwetu Hai tuna vipaji vya kutosha, wasanii wa kila aina, lakini mpaka sasa hivi BASATA imeshindwa kutusaidia. Sasa nilikuwa namwambia tu kwenye hoja yake aiombe Serikali, BASATA wawekwe pembeni tutafute chombo ambacho kinaweza kutusaidia, ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Unapokea Taarifa hiyo Mheshimiwa Sanga?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, naipokea kwa sababu gani?

Mheshimiwa Spika, BASATA hawana manpower ya kuchunguza huo muziki ni bora au sio bora. BASATA hawana miundombinu yoyote ya kuchunguza huo muziki ni bora, wanatengeneza dirisha la kuwaonea wasanii wetu katika nchi hii na mimi naungananae kwamba tutafute chombo kingine ambacho kitakuwa na manpower inayojua muziki, imesomea muziki, kitakuwa na watu wataalam wanaojua muziki ili waweze kufanya hiyo kazi.

Mheshimiwa Spika, lakini mambo mengine sina la kuzungumza, zaidi niungane na Mbunge wa Morogoro kwamba, nchi hii bila arena ni ukoloni. Bila arena nchi hii tunakuwa tumebaki sehemu ambayo haina maendeleo. Dare es Salaam tunahitaji arena ya michezo, sports arena, Dar es Salaam ya watu 60,000; watu 50,000. Rais akitaka kuongea na Taifa hili Uwanja wa Taifa, mvua ikinyesha watu wanaanza kukimbia. Tafuteni arena ambayo Rais akitaka kuongea na watu mnaingia mle ndani mvua inyeshe au isinyeshe Rais anazungumza na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pli, leo boxing inakua, mtafanya sehemu gani? Vikumbi vyenyewe vya watu 2,000/ watu 1,000. Tafuteni Tanzania Arena, andikeni hata JPM Arena au Samia Arena halafu mwisho wa siku Watanzania watawakumbuka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante, lakini sitaunga mkono hoja hadi pale ambapo mtatupa majibu kuhusu BASATA na kile ambacho wanakifanya. Ahsante. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi ya kuchangia Mpango wa Maendeleo. Nitajikita kwenye mambo mawili, jambo la kwanza litakuwa sekta ya kilimo, lakini pia nitazungumzia suala la umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naendelea kwenye sekta ya kilimo ambapo hata Mjumbe aliyepita ameishia. Kwanza niipongeze Serikali kwa kazi ambayo inaendelea na kwa mpango ambao imeusoma, lakini nataka kuzungumzia kilimo kwenye mambo ya mabenki, sekta ya mabenki ndani ya Taifa letu, jinsi ambavyo yana wajibu wa kuchangia kwenye kilimo lakini tumekwama hapo kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ndicho kinachoongoza kwenye pato la Taifa kwa asilimia 26.9 kama ambavyo kwenye Mpango inaoneshwa, lakini mabenki ya Taifa hili ambayo tunafanya nayo kazi na yanachangiwa sana na Serikali ni moja kati ya maeneo ambayo yamekuwa yakikwamisha kilimo kwa muda mrefu kutokana na taratibu zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabenki yanapokea mitaji kutoka kwenye Serikali yetu, lakini pia kwa kipindi hiki yamepunguziwa riba ili yaweze kuhudumia wakulima wa Tanzania na Watanzania wote. Lakini nataka nitoe takwimu chache, kwa mfano wa Benki za NMB au CRDB kwenye sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka 2018, Benki ya NMB imekopesha wafanyakazi kwa asilimia 54, lakini kwenye kilimo imekopesha kwa asilimia 4.0 tu. Mwaka 2019, Benki ya NMB imekopesha wafanyakazi asilimia 58, lakini kwenye kilimo imekopesha asilimia 5.0 tu. Benki ya NMB mwaka 2020 kwa wafanyakazi imekopesha asilimia 65, kwenye kilimo imekopesha asilimia 6.0 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya CRDB mwaka 2019 kwa wafanyakazi imekopesha asilimia 45, kwenye kilimo imekopesha asilimia 1.0. Mwaka 2020 kwa wafanyakazi imekopesha asilimia 48, kwenye kilimo wamekopesha asilimia 2.0.

Mheshimiwa Mwenyekiti, angalia benki za mataifa yanayotuzunguka kwa mfano Cooperative Bank ya Kenya, mwaka 2019 kwenye kilimo wamekopesha asilimia 88. Mwaka 2020 kwenye kilimo wamekopesha asilimia 91…

MWENYEKITI: Hiyo ni Kenya Commercial Bank?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naam?

MWENYEKITI: KCB?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni KCB. Tunakwenda ZANACO Bank, Zambia; mwaka 2019 Benki ya Zambia, ZANACO, wamekopesha asilimia 53 kwenye kilimo. Mwaka 2020 wamekopesha kwa asilimia 65 kwenye kilimo. Sisi Tanzania tunacheza na asilimia 4.0 kwa mabenki yetu yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa tuna swali la kujiuliza, Wizara ya Fedha; ni wapi ambapo tunakwama kwenye kilimo kwenye Taifa hili? Mabenki yanatukwamisha. Wanapokea mitaji ya Serikali, wamepunguziwa riba, lakini wao wameshindwa kupunguza riba kwa wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoka Mkoa wa Njombe. Mkulima akienda kukopa anakopa kwa asilimia 17, 18 hadi 20 riba. Huyu mkulima leo ni nani atakwenda kukopa? Akienda kupeleka collateral hata ya shamba lake wanamkatalia, wanataka kuona collateral ya vitu ambavyo vinaonekana ambavyo ni vikubwa ambavyo wakulima wetu wa Tanzania wengi wanashindwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niishauri Wizara ya Fedha, wapitie mchakato upya kuangalia jinsi gani mabenki yanatukwamisha sisi Watanzania kwenye kilimo. Hizi benki zinatumia mitaji ya Watanzania mingi na BOT imewaondolea riba na wao wana wajibu wa kuondoa riba kwa wakulima wetu ili waweze kupata fedha, waweze kuendeleza kilimo, tofauti na hapo tutaendelea kulia. Wenzetu wa Kenya wametuacha mbali, wanakopesha asilimia 98 kwenye kilimo, lakini sisi tumekwama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umezungumza suala la mbolea hapa, natoka Mkoa wa Njombe, gunia la mahindi Makete gunia la mahindi linaunzwa shilingi 15,000, mkulima ananiuliza Mheshimiwa Mbunge ninatakiwa niuze magunia saba ili kupata mfuko mmoja wa mbolea lakini leo kwenye Mpango hatuoni makusudi yoyote ya Serikali ya kutoa dharula, yakutoa hata ruzuku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu alitusaidia tulipata kwenye mahindi bilioni 50 kwa ajili ya NFRA. Lakini bado tuna msiba hapa kwenye mbolea kwa sababu mwakani kama hatuta waokoa wakulima leo mwakani tutaingia kwenye crisis ya njaa. Kwa sababu wakulima hawawezi tena kulima, mabenki hayawakopeshi, mbolea hakuna, wanalia na mbolea tunaomba ruzuku sana kwenye hii mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba, Serikali itusikilize, itafute fedha iweke kwenye ruzuku kwa wakulima, ili wakulima wetu hawa tuwaokoe mwakani tusiingie kwenye crisis Tanzania na itakuwa ni aibu, Taifa ambalo tuna ardhi ya kila kona lakini leo tunaingia kwenye crisis ya njaa kwa kukosa ruzuku kwenye mbolea hilo lilikuwa ni la kwangu kwenye Sekta ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nije kwenye Sekta ya Nishati, ukienda kwenye Sekta ya Nishati hotuba ya Waziri ukurasa wa 14, anazungumzia usambazaji wa umeme vijijini. Kwanza tushukuru kwamba ni kweli umeme vijijini umeendelea kusambazwa naonesha kwenye ripoti mmetumia zaidi ya Bilioni 88.1 kwenye kusambaza umeme vijijini. Lakini hoja inakuja, umeme huko vijijini umewafikia Watanzania haujafikia, kwa sababu asilimia kubwa umeishia kwenye taasisi, kwenye mashule zahanati lakini ukienda kufuatilia, hapa nimefanya uchunguzi wa haraka, TANESCO, TANESCO sasa hivi hawana bajeti ya kusambaza umeme kwenye makazi ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kama Serikali inanisikiliza, ifanye sensa ya kujua ni Watanzania wangapi wamesuka umeme toka 2019 hadi leo wamekwamba kuunganishiwa umeme kwa sababu TANESCO hawana fedha. Tumewaachia REA wanatupa kilomita moja moja kuelekea kwenye Makanisa, Zahanati, Vituo vya Afya, ukishafika huko makazi ya watu ambao ni wapiga kura wa Taifa hili wengi hawana umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamebaki kuomba nguzo kwa Wabunge, wanaomba nguzo kwa Wabunge, wanaomba angalau hawa watoe fedha maana yake wapo tayari kutoa fedha zao wanunua lakini TANESCO wamekwama hawana fedha za kwenda kusambaza umeme kwa wananchi. Na nimuombe Waziri wa Nishati afanye sensa kila jimbo, kila wilaya…

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nafurahishwa na mchango wa mdogo wangu nataka tu kumuongezea taarifa kwamba, pamoja na kwamba asilimia 78 REA wamesambaza umeme lakini ni asilimia 18 mpaka 20 tu ya Kaya zote zimeunganishiwa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika watumiaji potential milioni 11.4 waliounganishiwa umeme ni milioni 2.8 peke yake. Kwa hiyo, hali ni mbaya pamoja na kwamba tumeufikisha vijijini lakini unaingia kijijini, umeingia Kaya mbili tatu sisi tunadhani umeme umefika lakini ukweli ni kwamba namba za vijiji zinatupotosha sasa twende kwenye namba za Kaya. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sanga, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea hiyo taarifa kwa sababu ndiyo uhalisia uliopo kwenye majimbo ye tuna kwenye mikutano na Wabunge wenzangu wananiunga mkono. Kwamba hapa tu simu ambazo tunazipokea ambazo zinahusisha wananchi wakiomba kuunganishiwa umeme ni nyingi yaani Wabunge ndiyo tumegeuka TANESCO kwa sasa, wakati TANESCO wanawajibu wa kupata fedha kwa ajili ya kusamba umeme kwa Watanzania. Kwa hiyo, tusijidanganye na namba ya kwamba tumefikisha kila Kijiji lakini je mpiga kura wa Tanzania hii, mpiga kura ambaye tunamtegemea 2025 atusaidie amefikishiwa umeme? Unakuta kwamba asilimia 90 wengi hawajapata umeme na wapo tayari kuunganishiwa umeme na wapo tayari kutoa fedha zao mifukoni lakini TANESCO imekwama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naunga mkono Mpango wa Bajeti lakini natoa mapendekezo haya; waangalie mabenki kwenye kilimo, waangalie ruzuku kwenye mbolea, lakini pili TANESCO wasijifiche kwenye kichaka cha umeme kufika kila Kijiji waende wakaangalie uhalisia wafanye sensa kila Mbunge alete hapa ni Kaya ngani ambazo hazijaunganishwa umeme halafu wataona maajabu yaliyopo. Mimi Makete nikianza nina zaidi ya nyumba 2000 zimesukwa lakini umeme toka 2019 hadi leo hazijaungwanishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante ni hayo mawili tu. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Ripoti ya CAG, lakini na ripoti za Kamati hizi. Kwanza nakupongeza sana kwa uamuzi uliochukua kutoa siku zote hizi tuweze kujadili ripoti na haya mambo ya Kamati. Nakupongeza kwa sababu hii inaonesha ni jinsi gani ambavyo umenuia kulisaidia Taifa na kumsaidia Mheshimiwa Rais. Naamini tutakapokuwa tunafunga tutakuwa tumetoka na maazimio makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa sana kwenye kutafuta fedha za Taifa hili, lakini ukiisoma Ripoti ya CAG, narudia lugha moja kwamba, ukiwa huna akili huwezi kupata shida, ila ukiwa na akili timamu hii Ripoti ya CAG unaweza ukachukua maamuzi magumu sana. Ukisoma Ripoti ya CAG anazungumzia mtiririko wa matumizi mabovu ya fedha kwenye Taifa letu kwa muda wa miaka mitatu mfululizo. Kwa mwaka 2018/2019 CAG anasema matumizi mabovu yalikuwa ni bilioni 14. Mwaka 2019/2020, CAG anasema matumizi mabovu yalifika bilioni 380. Mwaka 2020/2021, CAG anasema matumizi mabovu yamefika bilioni 1.14, maana yake kila siku fedha za Serikali zinapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa Joe Biden, Rais wa Marekani alizungumza alisema: “Corruption is a cancer, a cancer that eats away at a citizen’s faith in democracy, diminishes the instinct for innovation and creativity.”

Mheshimiwa Spika, Rais Rodrigo wa Ufilipino anasema: “Where there is no corruption, there will be no poverty.”

Mheshimiwa Spika, sasa hapa nataka kuzungumzia nini? Nataka kuzungumzia shirika moja tu la umma kwa mfano, Wakala wa Huduma za Manunuzi Serikalini (GPSA). CAG anamtaja GPSA kama ni mtu ambaye hadi dakika hii amechukua zaidi ya bilioni 10 na hajaleta magari ndani ya miaka mitatu, ndani ya miaka miwili. Utajiuliza huyu GPSA ni Wakala wa Serikali, nakupa mfano mmoja tu, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa wanamdai GPSA zaidi ya magari 500 na fedha amelipwa kwa muda wa miaka miwili, lakini hajaleta magari hadi leo. Ukimuuliza GPSA anasema kulikuwa na Covid. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa namuuliza GPSA Bandari ya Dar-es-Salaam ni lini ilisimama kutoa huduma wakati wa COVID? Soko la Kariakoo lilisimama wakati wa COVID, lakini GPSA alisimama kutoa huduma wakati wa COVID, Serikali inamdai magari. Achana na hapo, Wizara ya Afya wamempelekea GPSA ombi la kuwanunulia magari ya bilioni 17. GPSA kawaletea quotation ya magari 487 kwamba, kwenye hizo bilioni 17 nitanunua magari 487. Wizara ya Afya wakajiongeza wakasema sisi hatununui kupitia wewe, wameenda UNICEF, wameenda kupata magari 663.

Mheshimiwa Spika, sasa unajiuliza UNICEF sio shirika letu la ndani ambalo tunafanya nalo kazi, ila tuna Wakala ambaye ni GPSA ameweka difference ya magari 100 ndani ya Wizara ya Afya, yeye angenunua angenunua magari 400, lakini UNICEF ameweza kununua magari 663 kwa fedha zilezile bilioni 17. Sasa najiuliza Serikali yetu, wataalam wetu wana lengo gani na wana nia gani na Serikali yetu?

Mheshimiwa Spika, Bodi ya Mikopo inahangaika hawana fedha, GPSA hela anayo na ameshalipwa. Kwa hiyo, nashauri ni vema GPSA ikaangaliwa, ikaundiwa tume, ikachunguzwa. Hakiwezekani kikawa ni chombo cha kunyonya badala ya ku-regulate matumizi ya fedha ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naenda kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, nazungumzia vitu vitatu. Kuna kitu ambacho sijakisoma, hata kwenye Kamati humu sijakiona, kuna kitu kinaitwa bakaa. CAG anazungumzia bakaa kwamba halmashauri zetu nchini zilivuka na bakaa ya bilioni 30. Waheshimiwa Wabunge naomba tuelewane, mimi niko Kamati ya USEMI, halmashauri nyingi nchini zina-underestimate ukusanyaji wa mapato, zikisha- underestimate ukusanyaji wa mapato, ndani ya muda mfupi unashangaa wamevuka lengo la ukusanyaji wa mapato.

Mheshimiwa Spika, leo nazungumza, Halmashauri ya Tunduma anakotoka Mheshimiwa David Silinde, tayari robo hii wameshavuka tayari nusu ya ukusanyaji wa mapato wa bajeti waliyotuomba sisi. Maana yake ni nini? Wataenda zaidi ya asilimia 120 au 150, ile fedha inayobaki ya bakaa Wabunge jiulizeni wanaifanyia nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda halmashauri mbalimbali hapa, ukienda Halmashauri ya Kinondoni walivuka karibu na milioni 500. Ukienda kwa Mheshimiwa Cosato Chumi wamevuka karibu na bilioni moja. Ukienda Halmashauri ya Mwanza wameenda zaidi ya bilioni moja. Hawa wote wanabakiwa na bakaa hizi ambazo ukifuatilia matumizi yake ni matumizi ya chinichini, fedha za Serikali zinapigwa. Naomba sana LAAC wachunguze matumizi ya bakaa kwenye halmashauri zetu kwa sababu kimekuwa ni kichaka cha ku-underestimate ukusanyaji wa mapato, wanavuka lengo, fedha zinazobakia wanazipiga kupitia vikao na mambo ambayo hayamo kwenye bajeti na utunzaji wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine kuna suala la POS. CAG anazungumzia POS anasema halmashauri 46, Mamlaka za Mitaa 46, kwa muda wa siku tatu hadi siku 400, hizi POS zilikuwa zinapotea, nyingine zinaonekana leo, kesho zinapotea kwenye mfumo hazionekani. Serikali imepoteza mapato zaidi ya bilioni 427. Sasa ni lazima tutafute mfumo bora wa jinsi gani ya kukusanya mapato kwenye halmashauri zetu, kwa sababu hizi POS zinatumika ni kichaka pia cha kuiba fedha za Serikali.

Mheshimiwa Spika, kuna jambo lingine, hili la asilimia 10. Asilimia 10 nilizungumza hapa kwa muda wa miaka mitatu yote hadi sasa tuna zaidi ya bilioni 100 za asilimia 10 ziko mitaani, lakini kwenye Taifa hili wenzetu wa Jiji la Dar-es-Salaam walijaribu kutumia DCB Bank kama sehemu ya kusambazia fedha na DCB Bank ilifanya kazi vizuri sana. Walivyogundua kwamba, inafanya vizuri sana kazi wakaiondoa kwa sababu walikuwa hawana sehemu ya upigaji, wameirudisha kwenye mfumo wa kawaida fedha zinapigwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda Burundi, Serikali ya Burundi inajua sana kusimamia hizi fedha. Wameandaa madirisha ya kibenki kwa ajili ya wanawake na vijana ili hizi fedha ziweze kusimamiwa vizuri, lakini kwenye Taifa letu wanakwepa huo mlango kwa sababu unakwepa mianya ya upigaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, CAG anasema mwaka 2020/2021 bilioni 47 hazijarejeshwa, ziko kwenye mifuko ya watu, lakini halmashauri hazijapelekwa zaidi ya bilioni sita, unakuta is a lot of money. Mheshimiwa Rais anatafuta hela ya ruzuku ya mafuta, hela zimefichwa. Mheshimiwa Rais anafuta ruzuku kwa ajili ya mbolea, hela zimepigwa. Tunamsaidiaje Mheshimiwa Rais wetu kama hizi fedha tutaendelea kuruhusu kuendelea kupigwa hivi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna watu walishauri hapa kwamba, watu wengine wapigwe risasi na wengine wanyongwe, lakini nasema kabla hatujalifanya hilo lazima tufanye list of shame. Lazima tutangaze list of shame of this country kwenye institutions za Serikali, kwenye Mawakala wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakupa mfano, kwenye list of shame mojawapo, kuna watu hapa wanaitwa Mamlaka ya Maji Safi ya Dar-es-Salaam. CAG anasema wamekusanya zaidi ya milioni 755 kwa kudanganya sio kusoma mita; wanafika mtu wanamwambia tupe hizo hela, zaidi ya milioni 700, hii lazima iingie kwenye list of shame.

Mheshimiwa Spika, nenda pia kwenye Shirika la Bima ambalo tuna ndege 11, lakini wanakata zaidi ya dola milioni tano wakati Rwanda wana ndege 12 wanakatwa kwa dola milioni mbili. Maana yake ni Shirika letu la Bima nalo ni kichaka cha wizi wa fedha ambazo ni fedha nyingi zinakwenda huko kwenye bima. Achana na hilo tu, Shirika la Bima la Afya limeacha dola laki tatu kwenye akaunti namba 1156119 kwenye benki iliyoko Uingereza kwa zaidi ya miaka mitano, halisemi kama hizo fedha zipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, twende kwenye Shirika la Bandari. Ukienda kwenye shirika hili napo kuna upigaji. Wana zaidi ya vifaa vya bilioni mbili ambavyo vilitakiwa vipigwe mnada kwa miaka mitatu iliyopita, wanapiga chenga, vinaibiwa, vimepotea, vifaa vya bilioni mbili, lakini wana fedha zaidi ya dola laki tatu kwenye Benki ya Deutsche akaunti iliyoko Uholanzi, hawajawahi kuzisema kwa muda wa miaka mingi zipo kule. Mheshimiwa Rais anatafuta fedha hizi kila siku. Rais hawezi kufika kila kona, Watanzania hili ni Taifa letu tunataka tuamini kwamba, hii nchi inajengwa na wenye moyo na inaliwa na wenye meno? Hatuwezi kuamini katika hilo. Hili ni Taifa letu lazima tulipiganie na hawa wataalamu wanatusikia, nawaomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nenda kwenye Bodi ya Mikopo. Bodi hii ilikopa mkopo, ambao Mheshimiwa Mkenda anahangaika nao, walikopa mkopo wa bilioni 54, wame- delay kulipa, saa hizi wanadaiwa bilioni 68. Yaani kutoka bilioni 54 waliyokopa, sasa hivi wanatakiwa walipe bilioni 68, over 100% wanadaiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nenda kwenye Mamlaka ya Elimu. Mamlaka ya Elimu ya Ufundi, Makete Jimboni kwangu, wameingia mkataba wa kujenga na Wakala wa Nyumba za Taifa, jengo la bilioni 1.5 hadi leo; mtu amelipwa, majengo hayajajengwa, ametawanyika hadi saa hizi hayupo, hii ni list of shame kwenye Taifa letu, mnataka list of shame ipi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakuomba tutakavyoondoka kwenye maazimio haya, hawa watu wasione kama sisi tunapiga story, ni muda muafaka wa Bunge lako, wa Kiti chako kuonesha kwamba, tuna msuli wa kupigania Taifa letu, kuonesha kwamba, tuna uwezo wa kuwawajibisha. Kama hatuwezi kuwapiga risasi basi hata kesho tuwaone magerezani. Kama hatuwezi kuwanyonga basi kesho tuwakute magerezani kwa sababu, wote ni Watanzania wenzetu na wananufaika kwa pesa za Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na Mungu akubariki sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza kabisa nimpongeze Waziri wa Elimu, Profesa Ndalichako kwa hotuba yake, lakini pia na Kamati nzima kwa hotuba ambayo wameitoa.

Mheshimiwa Spika, najikita kwenye mambo matatu ya haraka. Jambo langu la kwanza, ukifuatilia kwenye hotuba ya Rais wetu ukurasa namba 28 anazungumzia suala la elimu akiwa anazungumzia kwenye kujikita kuimarisha miundombinu mashuleni, mimi nitazungumzia suala la madawati. Suala la madawati ni bado changamoto kwenye nchi yetu licha ya kwamba TAMISEMI wanakuja na mpango wa mkakati wa dawati za milioni saba kwa mwaka unaofuata, lakini nina mapendekezo kwenye Serikali na hasa Wizara ya Elimu kwamba tunahitaji kuongeza kiwango cha madawati kwa kuwa na mkakati wa pamoja.

Mheshimiwa Spika, naishauri Serikali sisi Makete, Njombe na Iringa ndio wazalishaji wakubwa wa malighafi za mbao. Ubao wa mbao unaouzwa Mwanza shilingi elfu saba elfu nane, Makete unauzwa shilingi elfu mbili ubao ambao unauzwa Dodoma shilingi elfu saba Makete unauzwa shilingi elfu moja. Je, hatuoni kama kuna haja sasa kwa Serikali kujenga kiwanda cha kimakakati na sekta binafsi, ikaingia mkakati binafsi na private sector ikajenga kiwanda katika Mkoa wa Njombe pale Makete au ikageuza VETA ya Makete kuwa sehemu ya uzalishaji wa madawati tu, mwaka mzima, miaka mitatu, miaka mitano wanazalisha madawati tu kwa ajili ya Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, tuna JKT, tuna Magereza lakini tuna vijana wa VETA wengi tu ambao wanamaliza ufundi seremala, tungeweza kuwapa hizo ajira wakatengeneza madawati na tukaanza kusambaza kwenye Taifa hili kwa sababu magari ya jeshi yako mengi ya kuweza kusambaza mashuleni kwetu na changamoto ya madawati ingekuwa imemalizika kwenye Taifa hili.

Mheshimiwa Spika, sisi Makete tuna eneo, tuna mbao, tuna malighafi za katosha, tunaomba Wizara ya Elimu waone kama hii ni haja ya Serikali kuliko kumwachia Waziri Mkuu, ikifika siku ya enrolment mwezi Januari aanze kusema watumishi wa Serikali msiondoke maofisini hadi madawati yapatikane. Sasa twende na mpango mkakati wa kuwa na kiwanda maalum cha kuzalisha madawati na fanicha za nchi hii.

Mheshimiwa Spika, jambo langu la pili…

T A A R I F A

SPIKA: Haya mwenye taarifa nampa ruhusa, Mheshimiwa Tabasamu.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, kusafirisha dawati kutoka Makete mpaka Sengerema au mpaka Bukoka ni gharama kubwa kuliko kusafirisha mbao.

Mheshimiwa Spika, naomba kama mbao zipo aishauri Serikali sisi tuweze kuletewa mbao tutengeneze dawati kutokea kwake sio kubeba dawati kulipeleka Sengerema na sisi tuna vijana wa kufanya kazi.

SPIKA: Unapokea hiyo taarifa, Mheshimiwa Festo Sanga?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimwa spika sijaipokea kwa sababu, sisi tuna uwezo wa kulisafirisha dawati kama dawati tunafanya assembling Sengerema ili tuwe na madawati mengi yanayosafirishwa kwa wakati mmoja kwenye magari ammbayo tunaona yanafaa kama magari ya jeshi. Sasa niseme jambo moja magari ya jeshi yapo na kazi maalum ipo, nchi hii haina vita na wanaomba bajeti za mafuta kila mwaka, tungetumia magari ya jeshi kwa ajili ya kwenda kusafirisha mizigo kama hiyo kuliko kufanya hiki ambacho Mheshimiwa Mbunge anakishauri.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo nataka kushauri ni kwenye sekta ya michezo, Mheshimiwa Ndalichako, mawakala na Wabunge wengi asilimia 90 waliopo humu ndani wanaahadi nyingi mashuleni kwenye suala la kugawa vifaa vya michezo. Tunaomba Wizara ya Elimu, Wizara ya Habari na Wizara ya TAMISEMI waone haja ya kutengeneza agency, wakala wa vifaa vya michezo mashuleni wa Serikali ili waweze kutoa ruzuku au kupunguza kodi, vifaa vya michezo mashuleni viweze kupatikana kwa wingi, kuliko kuendelea kusubiria kila Mbunge hapa aagize vifaa China, aweze kusambaza mashuleni, wakati tuna uwezo wa kutengeneza wakala wa vifaa vya michezo na tukasambaza nchi nzima na vijana wetu wakapata.

Mheshimiwa Spika, ile hoja ya Wizara ya Michezo na Wizara ya Elimu kuona UMITASHUMTA na UMISETA vinakuwa kwenye hii nchi ingekuwa kama tungekuwa na hili jambo. Naomba Wizara iifikirie na hili kwa kweli nimwambie Mheshimiwa Waziri kabisa nitashika shilingi kama watakuwa hawana majibu ya kujibu.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, lilikuwa kwenye taulo za kike. Kwanza I call for the ladies of this country even the girls’ student wa nchi hii. Hili taifa kwa sasa ndio kwa wakati mmoja limeanza kupata viongozi sita wanawake watupu. Naanza wa kwanza mtu wa kwanza ni Raisi wetu mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ni mwanamama; mtu wa pili ni Mheshimiwa Ndalichako Professor Waziri wa Elimu ni mwanamama; mtu wa tatu ni Waziri wa Afya, Mheshimiwa Dorothy Ngwajima ni mwanamama; mtu wa nne ni MheshimiwaJenista Mhagama ni mwanamama; mtu wa tano ni Naibu Spika, Mheshimiwa Tulia ni mwanamama na akina mama wengine wote na Mheshimiwa Ummy Mwalimu Waziri wa TAMISEMI ni mwanamama.

Mheshimiwa Spika, watoto wa na nchi hii watawalilia kama suala la taulo za kike hawataweza kuli-solve, wanategemea halmashauri zitenge bajeti kwa ajili ya taulo za kike, ni jambo ambalo sikubaliani nalo. Nawaomba na nawashauri kwamba Tanzania tuingie ubia na viwanda, tuweze kutengeneza taulo za kike zenye ubora ambao watoto wanaweza wakazitumia, kwa sababu watoto wengi wa kike wanakosa masomo…

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge wanawake kweli mmejaa humu mnategemea Festo Sanga ndio awaongelee hili jambo. Mheshimwa Festo nakuunga mkono malizia hoja yako.

MBUNGE FULANI: Taarifa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, kwa ripoti ya UNESCO inaonyesha kati ya watoto kumi wa kike kwa siku watoto wawili au watatu wanakosa kuingia darasani kwa sababu ya hedhi isiyo salama. Nataka ninukuu wanasema menstruation is not a problem but hygiene is a problem.

MBUGE FULANI: Taarifa.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge wanaume mpigieni makofi Mheshimiwa Festo Sanga (Kicheko)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, naomba wasimalize dakika zangu naomba nizungumze.

SPIKA: Ahsante sana, wananyanyuka wenyewe Bunge nitalishindwa dakika za mwisho, wenyewe wanataka kuja moto, hapa Waheshimiwa mnasaidiwa kazi hapa. (Kicheko)

Kwa hiyo Wabunge wanaume kumbe tuna faida na sisi. Ahsante sana umetubeba Mheshimiwa Festo Sanga.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa. Mimi nitachangia mambo mawili. Jambo la kwanza ni jambo la ATCL na pili litakuwa ni jambo la kilimo na mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais Mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya kwa sababu mpango wa kununua ndege tano tayari kuna malipo ya fedha ameshayafanya na ndege tano zinategemea kuingia nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nizungumzie ATCL kwa maana ni nini inatakiwa tusaidie kwenye mpango na kama ambavyo kamati imeshauri. ATCL ina ndege 11 lakini tuna changamoto kubwa sana katika uendeshaji wa Shirika letu la Ndege la ATCL. Changamoto yetu ya kwanza ni kwenye suala la gharama za tiketi. Gharama zetu za tiketi kwenye Shirika la Ndege zimekuwa ziko juu sana, kiwango ambacho hadi Mbunge anafikiria kusafiri kwa ndege anaona ni bora asafiri kwa gari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaweza kutolea mfano wa gharama ya tiketi ya ndege kutoka Katavi kuelekea Dar es Salaam. Unazungumzai shilingi za Kitanzania 800,000, 600,000, 700,000. Nauli ambayo unaweza ukaitumia kusafiri kuelekea Rwanda na ukaelekea na mataifa mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe kwenye mpango wa Serikali waweze kuisaidia ATCL na kupunguza gharama za uendeshaji, kwa maana ya hizi tiketi. Tunajua ATCL inakodi ndege kutoka TGFA (Tanzania Government Flight Authority), ambapo analipa zaidi ya dola 1,500,000 kila mwezi kwa kukodishiwa ndege. Kwa hiyo ni vyema ATCL ikapewa jukumu la kuendesha hizi ndege in full capacity ili hizi gharama ziweze kushuka chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Mtanzania ukisimama ukamwambia ATCL nauli zake ziko sawa wakati katika nchi hii na Taifa hili tulishaona fastjet a private company, a private entity ilishawahi ku-operate na akarusha airbus kwa 100,000, 90,000, 150,000 lakini leo hii ATCL ambayo ni ndege ya Serikali ni kodi za watanzania ina viwanja nchi hii, inapaki nchi hii bado gharama zake za tiketi ziko juu. Kwa hiyo ninaomba kwenye mpango wa Serikali ione ni namna gani ya kuisaidia ATCL. Kwenye ATCL pia, hii ndege Watanzania wanavyoenda kulala saa tatu usiku na ndege zinaenda kulala kwa sababu hazina viwanja vya kuruka vyenye mataa. Kwa hiyo niombe ATCL isaidiwe kutoka kwenye TAA (Tanzania Aviation Authority) waweke mataa kwenye viwanja vingi ili ndege zi-operate zaidi usiku kuliko ku- operate mchana. Haiwezekani ukaona ndege 11 tukienda kulala na zenyewe zinaenda kulala (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba kwenye Mpango wa Serikali, ni fedha chache, ni fedha kidogo kulisaidia Taifa hili mchana watu wafanye kazi, mtu asiwaze flight. Ni jambo linahuzunisha sana. Ukienda Bukoba Kiwanja cha Ndege usiku hakitui, ukija Dodoma unaambiwa Kiwanja cha Ndega usiku hakitui, ukienda Tabora Kiwanja cha Ndege usiku hakitui. Ni vyema tukaondoka kwenye hili ombwe tuisaidie ATCL. (Makofi).

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili tunaomba ATCL pia wasaidiwe control tower ziongezeke. Moja ya changamoto kubwa ambayo ATCL inaipata, Mfano Bukoba hakuna control tower ya ndege wanatumia ya Mwanza. Ni vyema ATCL, TAA wakaisaidia ATCL iweze kuongeza Tower kuongozewa ndege kwenye maeneo tofautitofauti kama pale Tabora. Kwa hiyo ninakuomba sana shirika hili la ndege ili liwe na msaada kwa nchi yetu, liwe msaada kwa Watanzania na watu waendelee kupanda ndege kama walivyokuwa wanapanda kwenye Fastjet, wajisikie amani kwenye Taifa hili. saidieni hili shirika, geuzeni madeni yaliyoko kuwa mtaji ili shirika lisonge mbele, wasitumie sehemu ya tiketi kuwa ndiyo sehemu ya kutengeneza faida. Oncourse lazima watengeneze faida lakini hatuhitaji muda wote wawe wana-maximize super profit kwa kuwaumiza Watanzania ambao walitegemea kodi zao ziweze kuwasaidia kwa ajili ya Taifa lao, huu ni mchango wangu kwenye suala la ATCL.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo mengine ni kwenye mpango wa mambo ya kilimo. Tunakubaliana kabisa tuna hekta zaidi ya milioni 29 kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji. Naomba nisema, hatujaona mpango mkakati wa Serikali wa kusaidia kuboresha mazingira. Leo hii tunazungumzia mvua hakuna, hali ya hewa imebadilika. Lakini hatuzungumzii upandaji wa miti kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri tunaenda kuzungumzia umwagiliaji, maji mtatoa wapi kama mvua hakuna? Maana yake ni kwamba lazima tupande miti, ni lazima tuhamasishe Watanzania kupanda miti. Otherwise tuseme kwamba tunamsubiri Mheshimiwa Rais aanzishe kampeni ya kupanda miti nchini, wakati Rais anahangaika kutafuta fedha kuna mambo kama Taifa, tuamue tukiwa ndani, Rais ashtukie watu tunafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe mfano mmoja. Tunajenga Bwawa la Mwalimu Nyerere, mimi ni Mbunge wa Makete, Jimbo la Makete ndilo linalo-offer maji kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere. Tunamwaga maji kuelekea Mbarali, yanatoka Mbarali yanaelekea Ruaha, yatoka Ruaha yanaingia Rufiji kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere, lakini hakuna mti hata mmoja mliohamasisha, then mnategemea mkifukuza wananchi kutoka kwenye mita 60 ndiyo itakuwa solution ya kutunza vyanzo vya maji? siyo sahihi. Lazima tuhamasishe upandaji wa miti kwenye Taifa letu. Anzeni kampeni hii mapema, huu ni mpango, tengeni bajeti, na fedha ziko nyingi. Kusafisha Coco beach si usafi wa mazingira tu ni kazi ya Halmashauri ya Kinondoni. Kamam Taifa lazima tuwe na mpango mkakati kwa ajili Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili liende sambamba na timu ya Mawaziri nane walivyoenda Mbarali, wamesema kuanzia leo vijiji 48 vilivyoko karibu na Hifadhi ya Ruaha viondoke. Nataka kuita hii as a Mbarali crisis, kwa nini? leo hii unaenda kuondoa vijiji 48 kwa sababu tu unasema wako karibu na vyanzo vya maji na wananchi hao kupitia Ilani ya CCM tuliwaambia kwamba tutali-solve hilo tatizo kwa kukaa nao mezani tukiwaambia wanambarali kwa sababu nyie mnalilisha Taifa, kwa mwaka jana tu Mbarali imelisha ekari tani 600,000 za mchele…

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunawaambia watu wa Mbarali vijiji 48 waweze kuondoka…

MWENYEKITI: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na nimpe taarifa mzungumzaji kwamba, hata kule KIA - KADCO inataka kufuta kijiji kimoja chenye ekari 15,000 na vijiji vingine viwili kwa madai kwamba wako kwenye eneo la Kiwanja cha Ndege na kiwanja hiki kinadai eneo lake ni kilomita za mraba 110,000. Lakini ukubwa wake ni kilomita za mraba 12…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Pallangyo sasa unachangia naona.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa yake. Mbarali vijiji 48 unaviambia viondoke kwenye hifadhi ya maji. Wananchi wamesema tuko tayari kukaa mita 100 ili maji yaendelee kupita tunajua uhitaji huo. Lakini nizungumze hivi, leo hii tunazungumzia mgao wa umeme kwa sababu ya kupungua maji, leo hii tunazungumzia mgao wa maji kwa sababu ya mabadiliko ya tabianchi. Leo hii na kesho tunaenda kwenye Dinner table ya nchi yetu kwa mgao wa chakula.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mbarali anayelisha tani 600,000 za mchele kwa mwaka unamwambia leo akusanye virago aondoke. Huyu Mbarali ana viwanda visivyopungua 30, huyu Mbarali ana ajira za Watanzania zisizopungua 100,000, huyu Mbarali unayemzungumzia ana makazi ya watu na watoto wako pale, huyu Mbarali amekutwa na GN ya mwaka 2008 wakati wao walikuwepo toka mwaka 1972. Huyu Mbarali unayemzungumzia ni Mtanzania mwenzangu, ana familia na watoto anaosomesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mawaziri nane wanaoenda kuzunguka kwenye kijiji hiki wanatumia ripoti za maeneo yale ndio wanaenda kuamulia. Tunawaomba msitengeneze vidonda mnakokwenda, nendeni mkaponye matatizo ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Mheshimiwa Mwigulu umesaini mikataba 15 Mbarali yenye thamani ya shilingi bilioni 54 ya umwagiliaji, mmesema yakajengwe mabwawa Mbarali, Waziri wako ameenda kufuta hivyo vijiji 48, mpo mnaleta hapa mpango wa kwamba nyie mmesaini mikataba ya umwagiliaji 48…

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati kule mmenda kufuta…

MWENYEKITI: Taarifa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mnaenda kujenga wapi hayo mabwawa?

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sanga kuna taarifa.

T A A R I F A

MHE. ASKF. JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa mzungumzaji kwamba kile kitendo cha Mheshimiwa Waziri wa Fedha kusaini mikataba ya kuwasaidia wananchi, halafu mwingine akaja kukifuta ndicho nachoita kukosa mipango ya muda mrefu. (Makofi)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napokea taarifa. Waziri wa Fedha nachokwambia mikataba 15 uliyoisaini yenye thamani ya shilingi bilioni 54 Kamati ya Mawaziri nane imeenda kufuta hilo eneo unalokwenda kujenga hayo mabwawa. Kwa hiyo ujue kwamba Serikali nyie wenyewe hamuelewani sasa sisi wananchi tutaelewanaje sasa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ilani ya Chama cha Mapinduzi iliwaambia wale wananchi kuwa tutawalinda maslahi yenu, tutalinda haki zenu, tutalinda kwa sababu Mto Ruaha umesimama nyie mlikuwepo. Leo hii Kamati ya Mawaziri nane inaenda kufuta. We are going to the dinner table of this country na watu wenye njaa. Wabunge hatuwezi tukakaa hapa tukajadiliana wakati wananchi wetu wako under crisis kule. Wabunge hatuwezi tukajadiliana hapa sisi tumeshiba, wenzetu kule wanafukuzwa wanazalisha tani 600,000 kwa maslahi ya watu binafsi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia, lakini nimpe hongera sana na pongezi nyingi sana Mheshimiwa Rais Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nyingi ambazo anazifanya Makete, lakini
Mheshimiwa Waziri kaka yangu Innocent Bashungwa ni mmoja ya Mawaziri ambao sisi vijana tunajivunia sana kwa jinsi ambavyo anatusikiliza na anatupa nafasi kwenye wakati tofauti tofauti ambapo tunakuwa na matatizo, lakini pia Naibu Mawaziri wake wote wanatupa ushirikiano mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nimpongeze sana Mkuu wangu wa Wilaya Ndugu Juma Sweda anafanya kazi nzuri sana, Mkurugenzi wangu Ndugu William Makufu anafanya kazi nzuri sana kule Makete, lakini na Watendaji wote wa Halmashauri wanatupa ushirikiano mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Serikali hii sisi wana Makete tunaipongeza kwa sababu kuna mambo ambayo yamefanyika kwa muda ambao Halmashauri ya Makete ilikuwepo haya mambo hayakufanyika. Mimi nimeingia nikiwa Mbunge wa Makete tulikuwa na vituo vitatu tu vya afya, ninavyozungumza leo tumejengewa vituo vitatu vingine vya afya vya shilingi bilioni 1.5. Lakini tuna kata ambazo zilikuwa hazina shule Kata ya Bulongwa, Kata ya Mlondwe na Kata ya Kigala, tayari tumeanza mkakati Serikali imetupatia fedha, tunajenga shule ya Mlondwe na bado shule mbili mradi wa zaidi shilingi bilioni 1.8; lakini tuna shughuli nyingi ambazo tunaendelea nazo kwenye ujenzi wa madarasa ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Makete. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niombe Wizara mtukumbuke sana Makete kwenye suala la ukarabati wa shule za msingi. Tuna shule za msingi nyingi ni kongwe kwenye nchi hii hazijakarabatiwa kwa muda mrefu, tuna shule ya Misiwa, tuna shule ya Igorwa, tuna shule ya Asunzi tuna shule nyingi ndani ya Wilaya ya Makete, tunaomba Wizara itukumbuke ili shule hizi ziweze kufanyiwa ukarabati na kujengwa. Lakini tuna vituo vya afya kwa mfano Kituo cha Afya cha Lupila, wananchi wa Makete wanasafiri zaidi ya kilometa 100 kutoka Lupila kwenda Makete Mjini, kwa ajili ya kufuata huduma za afya pale ambapo kwenye kituo cha afya imeshindikana, hawana ambulance hawa wote wanatumia bodaboda kilometa 100, tunaomba mtukumbuke ambulance kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Lupila. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mimi nizungumze mambo mawili makubwa leo. Leo nina jambo kubwa la TARURA; kwanza niwapongeze TARURA kwa kazi ambayo wanaifanya na nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri maana break yake ya kwanza baada ya kuteuliwa breki ya kwanza ilikuwa Makete kwa ajili ya shughuli ya TARURA. Mheshimiwa Waziri uliona hali ya Makete ya barabara sisi Wilaya ya Makete inaitwa Wilaya ya Kazi wananchi wetu ni wachapakazi wakubwa, lakini changamoto kubwa tuliyonayo sisi ni barabara za vijijini hazipitiki, uliona hali halisi. Nawapongeza TARURA kwa yale wanayoendelea nayo, lakini ninaushauri na hii kwa Mheshimiwa Waziri unaweza ukawa ndio game changer wa TARURA ndani ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2019 TAMISEMI mliandika barua kwenda kwenye Halmashauri mkizuia, kuna Halmashauri ambazo tulikuwa tayari kukopa mitambo ya kujenga barabara kwenye Halmashauri zetu. TAMISEMI wakazuia kwamba Halmashauri zisinunue wala zisikope kwa namna ya kwamba mnataka kulinda local constructors (wakandarasi wa ndani) waliopo ndani. Lakini nikuombe Mheshimiwa Waziri kama ambavyo leo Wizara ya Maji wananunua mitambo kwa ajili ya kuchimba mabwawa, ni wajibu sasa na ni wakati sasa TARURA kwa sababu ni department na ni Wakala, ruhusuni wawe na mitambo ya ujenzi wa barabara kwenye Miji na Halmashauri ambazo tuna mazingira magumu kama Makete. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii mwananchi wa kutoka Lupila kwenda Makete kupita Kipengele anasubiri fedha ya maintenance ya barabara kutoka Mkoani hadi ije ikamilike masika imepita, watu wamefariki, mazao yameozea shambani. Lakini tungekuwa na mitambo ya barabara pale Makete kutoka TARURA tungeenda na mitambo yetu, tungemwaga kifusi, tungesafisha barabara. Kwa ununuzi wa fedha za Serikali mitambo hata shilingi bilioni mbili haizidi mngefanya kwa nchi nzima, mngekuwa mmeokoa mambo mengi sana na fedha ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawasihi na ninawaomba tusije tukaja na hoja ya kulinda hawa wakandarasi kwamba wakandarasi wadogo tutawazuia. Mheshimiwa Waziri wajibu wa kwanza wowote wa Serikali ni kuhudumia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la watu wa private sector hilo ni hatua nyingine ninyi nendeni mkajenge barabara hawa nao watapata nafasi zao. Kwa sababu, mmejenga vituo vya afya msingejenga tungetegemea hospitali binafsi tungefika leo hapa? Tunaomba TARURA wawezeshwe… (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa napenda tu kumpa taarifa Mheshimiwa Sanga anaongelea hoja ambayo ni valid sana, ukizingatia barabara hizi ambazo ziko chini ya Halmashauri au TARURA ni takriban asilimia 85 na tunajua kabisa kwamba upande wa maji kule tuna DDCA. Kwa hiyo, ni mbadala sasa hivi kuweza kuhakikisha kwamba wale ambao wanajiweza kununua mitambo wanunue mitambo. Kwa sababu kama DDCA ipo na haizuii contractor hawa ambao ni local kwa nini mzuie kwa upande wa Halmashauri. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sanga taarifa hiyo.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninaipokea taarifa hiyo na ninaomba Mheshimiwa Waziri ataandika historia kwenye Taifa hili, ni mmoja kati ya vijana ambao tunawategemea ni kuruhusu jambo kama hili lifanyike kwenye nchi yetu. Halmashauri zenye uwezo wa kuwa na excavator, kuwa na ma- roller, kuwa na ma-tiper ziruhusiwe. Wataalam watakudanganya tu hapa kukupiga bumbuwazi ili watengeneze chain na watu ambao ni constructors ambazo ni private sector.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninakuomba simamia msimamo huo kama Mheshimiwa Aweso anavyokwenda kuchimba mabwawa, anza kujenga barabara vijijini na tutakuja kukushukuru.

Mheshimiwa NaibU Spika, barabara vijijini ndio sera ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan anasema tuwezeshe barabara vijijini zipitike. Nakuomba sana Mheshimiwa Waziri una nafasi ya kuyafanya haya mambo ndani ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo ninataka kuzungumza ni kwenye asilimia 10 kwenye 10 percent ambazo zilianzishwa na sheria yetu hapa nchini kwa makusudi mazuri sana ya kuona tunasaidia vijana, akina mama na watu wenye ulemavu. Hii sheria ilianzishwa kwa ajili ya kusaidia watu hawa ambao ni vijana wenzetu, lakini 10 percent ambayo tumekuwa tukitenga kwa ajili ya vijana wa Taifa hili, kwa ajili ya akina mama wa Taifa hili imegeuka ni 10 percent ya watu ambao wana uwezo na sio vijana wa Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumza kwa data ukisoma kwenye hotuba ya Waziri kwenye moja kati ya maelekezo toka tuanze kukopesha 10 percent mwaka 2017/2018 hadi 2021 nchi hii tumekopesha zaidi ya shilingi bilioni 300 kwa asilimia 10. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini toka tumeanza kukopesha tuna zaidi ya shilingi bilioni 222 ziko kwenye mikono ya wanyang’anyi na ninataka nikupe mfano Mheshimiwa Waziri; mfano ni Mkoa wa Tabora toka mwaka 2018 hadi 2021 wamekopesha shilingi bilioni 5.7, lakini fedha zilizorudi hadi leo ni shilingi bilioni mbili tu fedha zingine zote ziko mifukoni kwa watu. Ukienda Mkoa wa Pwani mwaka 2018 hadi 2021 wamekopesha shilingi bilioni 11 lakini hadi leo wamerudisha shilingi bilioni nne tu fedha zingine zimepotea. Ukienda Mkoa wa Mwanza wamekopesha shilingi bilioni 8.9, wamefanikiwa kurudisha shilingi bilioni 3.9 tu fedha zingine zote zimepotea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Mkoa wa Dar es Salaam wamekopesha bilioni 52.3 wamefanikiwa kurudisha bilioni 14 tu fedha nyingine zote zimepotea; ukienda Mkoa wa Mbeya anakotoka Spika wa Bunge wamekopesha bilioni 12 toka mwaka 2018 hadi leo wamerudisha bilioni saba tu fedha nyingine zote zimepotea; achana na Simiyu wamekopesha bilioni nne imerudi bilioni moja, achana na Geita wamekopesha bilioni sita zimerudi bilioni tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha hizi zipo kwenye mikono ya wanasiasa, zipo kwenye mikono ya watumishi wa Serikali ambao wanatengeneza vikundi vya vijana, wanawa-lob, wakifika pale wanakopeshwa fedha zinaingia mifukoni mwao, vijana hawafaidiki chochote. Kwa hiyo… (Makofi)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba, anachokiongea ni very valid na kuna muongozo wa 10% ambao uliandaliwa na Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, mpaka tunavyozungumza bado haujapelekwa kwenye Halmashauri kwa ajili yak u-guide na muongozo huo ungekuwa suluhisho kwenye matatizo ambayo anazungumza mzungumzaji anayechangia sasa hivi, ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Sanga, Taarifa, unaipokea?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea. Mheshimiwa Naibu Spika, nini nataka kuzungumza, Mheshimiwa Innocent Bashungwa, Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, anaweza kuzifuatilia fedha hizi zaidi ya bilioni 222 zilizoko mikononi kwa wahuni. Kwa nini nasema ziko kwenye mikono ya wahuni?

Mheshimiwa Naibu Spika, nenda ukafuate Halmsahauri ya Temeke ufuatilie fedha ziko kwa nani…

(Hapa kipaza sauti kilizimwa)

NAIBU SPIKA: Tayari, muda wako umekwisha.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, bado sijamaliza, bado dakika moja. Naomba dakika moja tu.

NAIBU SPIKA: Aah, sekunde tatu, sekunde tatu maliza.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakuomba Mheshimiwa Waziri fedha hizi shilingi bilioni 222 zilikuwa zina uwezo wa kutafutwa na zikaenda kutatua matatizo ya barabara, kuweza kununua mashine za kufyatulia tofali mkawapa vijana, mkaenda mkanunua mitambo mingine ambayo imeandikwa kwenye project ikasaidia vijana. Tafuta bilioni 222 ziko wapi zisaidie nchi yetu kwa sababu ni fedha ambazo ziko kwa viongozi wa taasisi, zipo kwa wanasiasa… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante, umeeleweka, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Jambo la kwanza naomba niunge mkono hoja iliyoko mezani. Naunga mkono hoja kwa sababu ripoti inaonyesha mambo mengi yamefanyika ni mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa na mambo machache sana ya kuzungumza. Jambo la kwanza ni kumpongeza Mheshimiwa Rais. Kwa niaba ya Wananchi wa Makete tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi ambazo anazifanya na hata kwa hatua ambazo anazichukua dhidi ya watu ambao wanaonyesha kabisa wakimvuta shati na kumrudisha nyuma hasa hasa haya mambo ambayo yamekuwa yakijitokeza kwenye taifa letu. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi anayofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwa miradi ambayo anaileta kwenye Jimbo langu la Makete. Sasa hivi tuna mradi wa Barabara ya kutoka Mbeya kuelekea Makete, barabara ya kiwango cha lami na mkandarasi alishasaini tayari barabara ile lakini niombe tu kwamba Serikali hii mikataba ambayo imeshasainiwa Serikali iweze kutoa advance payment kwa wakandarasi ili ziweze kujengwa kwa kasi kwa sababu barabara hii hadi sasa mkandarasi bado anasua sua kutokana na kwamba hajalipwa advance payment ili aweze kuanza kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba Serikali iweze kushughulikia hilo jambo ili barabara ile iweze kujengwa kwa sababu ni barabara ya kiuchumi na ni barabara ya kimkakati na ni barabara ambayo kwa Jimbo la Makete wananchi wangu wanaisubiri kwa hamu sana ili iweze kutekelezeka na shughuli za kiuchumi ziweze kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nataka kuzungumzia nataka kuzungumzia kwenye suala moja linalohusu Kariakoo. Naizungumzia Kariakoo kwa sababu karibia 50% ya wafanyabiashara wa Kariakoo ni Wananchi wa Wilaya ya Makete na ni wananchi ambao wanafanya kazi pale lakini pia Kariakoo ni moja kati ya kitovu cha uchumi cha Taifa letu. Kwa hiyo, nazungumzia Kariakoo kwa mantiki hii hapa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nimeiita hii; how TRA is trying to kill Kariakoo, yaani nimejaribu kuielezea jinsi gani TRA wanajaribu kuimeza na kuiua Kariakoo sehemu ambapo tunategemea kama Taifa tunapata mapato yetu mengi kwenye ukusanyaji wa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nina mambo matatu makubwa ya kuizungumzia Kariakoo; jambo la kwanza, Kariakoo ilikuwa inafanya vizuri sana kwenye soko la vitenge. Katika ukanda wa Afrika Mashariki Kariakoo ilikuwa inaongoza kwenye soko la kitenge lakini leo ninavyozungumza soko la kitenge Kariakoo limekufa. Kwa nini limekufa? Limekufa kwa sababu ilipitishwa Sheria hapa ya Ongezeko ya mita moja ya kitenge kutoka dola 0.4 kwenda 0.8 kwa maana kwamba 100% ya ongezeko kwa minajili ya kwamba tunalinda viwanda vya ndani lakini nikuelezee tu leo hii ukienda Zambia, ukienda Congo, ukienda Malawi ndiko vitenge vinakouzwa zaidi kuliko Dar es Salaam – Kariakoo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wafanyabiashara wa Kariakoo wengi wamepoteza vitenge, wamepoteza mitaji tumeua Soko la Kariakoo. Kwa hiyo, TRA kwa kulinda viwanda vya ndani ambavyo pia havitoshelezi soko wameweza kuizamisha Kariakoo kwenye soko la vitenge leo hii mapato kupitia vitenge hatuwezi kuvipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la tatu, Kariakoo inakufa, kwa nini inakufa? Ukienda leo hii kuna suala la wafanyabiashara wa kigeni. Wafanyabiashara wa kigeni wananunua sana mizigo kwenye Soko la Kariakoo, mizigo yao mingi ni whole sale. Wakinunua TRA wamekaa kuvizia, wanavizia kwa ajili ya kuwakamata, wakiwakamata wanasema mzigo wako ulionekana ni mkubwa risiti ni ndogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali ni vyema wakatafuta utaratibu mwema jinsi ya ku-deal na suala la ukusanyaji wa mapato kwenye Kariakoo. Wafanyabiashara wengi wamepungua wa kigeni wanakimbia, wako ndani, bidhaa zao zimeshikwa wanashindwa tena kurudi kufanya kazi kwenye Soko la Kariakoo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti niiombe TRA na Mheshimiwa Waziri Mkuu anatusikia, ni vyema kuweka kikosi kazi maalum cha kwanza kuangalia jinsi gani wafanyabiashara wanavyoweza kufanya kazi hasa hasa hawa wafanyabiashara wanaotoka nje kuja kununua mizigo kwenye Soko letu la Kariakoo ili Kariakoo iendelee kubaki salama iweze kuendelea kuilisha Taifa letu tubaki kwa na brand kwenye nchi yetu. Tofauti na hapo kuendelea kuvizia wafanyabiashara wa kigeni, wamenunua mizigo uwakamate tunaendelea kuiumiza taifa, tunaendelea kuiumiza Kariakoo ambacho sisi kwetu ni kitovu cha uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili niombe sana Serikali ilichukue katika uzito mpana sana. Hatuyasemi haya kwamba labda tunalengo baya na TRA, tunayasema haya tuna malengo mazuri. Ng’ombe yoyote unayemlisha lazima akutolee maziwa vizuri. Sasa hawa wanakamua tu, wanakamua tu lakini hawatengenezi mazingira mazuri ya kuiona Kariakoo inazidi kuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine juzi TRA wametoa waraka kuhusu consolidation. Utaratibu wa nyuma wote ulikuwa unaonyesha nina bidhaa naenda kununua China kwa mfano. Naungana na mwenzangu labda wawili, watatu tunaagiza mzigo kwenye container moja tunalileta Kariakoo. Watu wa cargo consolidation wanaweza kulishughulikia container na mizigo nikapata. Juzi umetoka waraka wa kwamba wafanyabiashara wote mnaoagiza mizigo China ni lazima mizigo yenu ikifika hapa kila mtu alipie kwa mzigo wake pale bandarini. Kwa maana ya kwamba mizigo ikifika inamwagwa, mfanyabiashara analipia pale mzigo wake ndiyo atoe aende nao kwenye soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu hiki kinaenda kuimaliza Kariakoo kabisa. Ninalisema leo hapa na kesho kutwa yatakuja kutokea. Nimeagiza piece 500 za mzigo, siweze kwenda tena bandarini nikaanze kusema jamani mzigo wangu ni huu hapa naomba nilipie. Tuna manpower gani bandari yetu ya kwamba imwage container mfanyabiashara aanze kuchagua mzigo pale ili aweze kulipia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hizi zote ni bureaucracy za kutengeneza za kuiba, bureaucracy za kupoteza mizigo ya wateja, bureaucracy ya kuhakikisha wafanyabiashara hawakui, bureaucracy ya kuhakikisha Kariakoo inakufa, bureaucracy ya kuhakikisha kwamba watu wanajilimbikizia mali wanatafuta kupitia Soko la Kariakoo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Wizara iangalie hili jambo. Ni jambo ambalo linaenda kuua wafanyabiashara kwa sababu hatuna manpower ya kutosha ya bandari yetu kumwaga mzigo chini ili kila mfanyabiashara aanze kulipia mzigo wake aliouchukua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ruhusuni cargo, hizi cargo hawa Watanzania wenzetu wamefungua cargo ziweze ku- facilitate hilo jambo. Kutengeneza hizi bureaucracy ni kuendelea kulifanya Taifa letu liendelee kudidimia. Kwa hiyo, haya mambo matatu if you don’t take care kwenye haya tunaenda kuizamisha Kariakoo. Kariakoo is our brand, Kariakoo ni chanzo chetu, Kariakoo ni eneo letu, TRA inafanya kazi vizuri ya kukusanya mapato lakini watendaji wao wa chini wanaenda kuizamisha Kariakoo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu lingine ni suala la maadili na malezi. Kama kuna mambo makubwa mawili kwenye nchi yanayotikisa kwa wakati huu ni suala la maadili na mmomonyoko wa malezi ya watoto wetu. Sisi ni Bunge hapa leo tunazungumza mambo mengi sana ya msingi kwa ajili ya Taifa letu lakini nakuhakikishia miaka 30 ijayo, miaka 40 ijayo kama suala la mapenzi ya jinsia moja hatutaipigia kelele, sisi Wabunge hapa miaka 30 ijayo, miaka 50 ijayo, tunaweza kuja kuwa na viongozi ambao wako kwenye sekta hiyo ya mashoga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo…

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mchangiaji wakati anaifikiria miaka 30 ijayo na siye Wabunge tupo, si tukubaliane tu hapa kwamba tukipima mtu akaonekana anafanya mambo yale anyongwe tumalize kabisa? Tutakuwa tumekomesha kuliko haya ya kusubiri miaka 30. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa unaipokea hiyo taarifa?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, anaongea jambo la msingi sana na tuna sheria zetu kwa maana ya kwamba kuna sheria zinazosema ni miaka 30 au kifungo cha maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukijidai kama hapa sisi ni vipofu hatuoni kinachoendelea kwamba kwa sababu ni Mbunge ninauwezo wa kum-protect mtoto wangu akawa anaishi mazingira mazuri anasoma shule nzuri. I am telling you, ubunge wetu ni sisi ni kwa sababu ya wananchi walioko kule mtaani ambapo haya wanayashuhudia yanatokea na sisi tuko kimya. Ni vyema kama nchi tukaanza kuchukua hatua immediately. Huu siyo utamaduni wa Kiafrika hata Biblia inakataa, hata Qurani inakataa. Miaka 30 ijayo nusu ya Bunge inaweza ikawa mashoga wamekaa hatuwezi kuwa na Taifa kama hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunajenga SGR, tunajenga hizo airport, Mheshimiwa Rais ana-invest fedha nyingi kwenye miradi. Tunakuja ku-invest kwa ajili ya kizazi kipi? Leo nina watoto wangu. Watoto wangu nisipowalinda, watakuja kudondokea kwenye huu mtego.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana lazima tuanze ultimatum kama nchi ya kwamba Taifa letu kwenye suala la malezi ya watoto limebadilika. Lazima tuanze mfumo wa tofauti kuhakikisha kwamba tuna-protect kizazi chetu. Tofauti na hapo kwa sababu ya misaada, kwa sababu tunapewa fedha, kwa sababu ya nini tuwe tayari kuachia damu zetu ziingie kwenye Sodoma na Gomora. Hiyo ni kitu ambacho hakiweze kuruhusiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama makanisa hayatasimama, kama Bunge halitasimama, kama misikiti haitasimama kuna siku misikiti na makanisa na Bunge vitaongozwa na watu ambao wako kwenye upande huo. Niombe tuchukue hatua kali dhidi ya watu hawa. Nimshukuru sana Mkuu wa Wilaya mmoja amefuta taasisi mojawapo. Juzi kuna kesi imetokea kule Mtwara mtu amefungwa. Tuanze Wakuu wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa, Wakurugenzi kila mmoja kwa nafasi yake alipo tutakuja kupata viongozi wa Jeshi, niliona ile takwimu imetoka jeshini wamepima waliokwenda jeshini wamekuta wengine wako kwenye upande huo. Tutakuja kupata jambo gani? Lazima tushughulike na jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe kama Mbunge kwa niaba ya Wananchi wa Makete, sisi Wanamakete suala la ushoga tunasema no, suala la mapenzi ya jinsia moja tunasema no, Biblia na Quran havijatutuma huko, msingi wetu ni kuhakikisha kwamba tunazaliana. Na mnajua kwamba vita yote hii ni kwa sababu Afrika tunazidi kuwa wengi, Wazungu wanajaribu ku-impose taasisi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuamini kwamba adui ameonyesha mlango aliopo na sisi tuonyeshe silaha tulizonazo kuukataa ushoga. Msaada wowote wenye element hizo Serikali tunaomba isiwe sehemu kwa sababu hautakuwa na baraka katika Taifa letu. Hatuwezi kuruhusu kizazi chetu kikapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo niende kuunga mkono hoja, niishukuru Serikali kwa ajili ya Jimbo la Makete na miradi ya maendeleo inayokuja. Niseme, tunawakati wa kuilinda Kariakoo lakini pia maadili na malezi kwa watoto wetu lazima tusimamie. Sisi kama Wabunge lazima tuonyeshe upande wetu ni upi nalitetee Taifa letu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwanza kabisa nianze kwa kupongeza hotuba ya Mheshimiwa Waziri hasa kwenye mambo ya ujenzi. Nianze kwa kuchangia kwa kuzingatia mambo mawili kwanza hotuba ya Rais lakini pia Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na pia nikijikita kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Nitajikita zaidi kwenye jimbo langu la Makete kwasababu ndipo ambako tuna changamoto kubwa ya barabara hasa hasa kutokana na kwamba sisi ndio wilaya pekee Nchini tuna miezi minane ambayo mvua inanyesha bila ya kusimama. Kwa hiyo Makete ina uhitaji mkubwa wa barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha kwanza nataka nizungumzie barabara ya kutoka Isyonji – Makete kwa maana ya kupitia Kitulo ambayo ukisoma kwenye ripoti kwa maana ya hotuba ya waziri ipo kwenye ukurasa namba 148 lakini ukisoma kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi iko kwenye ukurusa namba 74. Hii barabara kwanza niseme ni barabara ambayo Mheshimimiwa Rais aliagiza alipofika Makete akawaahidi wananchi kwamba barabara hii itajengwa tena Rais mwenyewe ni huyu huyu Mama Samia Suluhu Hassan akasema barabara hii itajengwa. Na niwaombe Mheshimiwa Waziri, ninajua kwamba ipo katika mkakatati wa kutangazwa barabara hii ili iweze kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini ninaizungumzia barabara ya Makete kutoka Isyonjo kuja Makete kupitia Kituro ni kwa sababu moja barabara hii ndio oxygen ya uchumi wa Wilaya ya Makete. Ni oxygen kwa mantiki ipi ni kwamba barabara hii inapita kwenye mbuga ya Kituro, hifadhi pekee ya tofauti kabisa ndani la Bara la Afrika, hifadhi ya Kituro inategemea barabara hii ya kutoka Isyonji kuja Makete. Lakini pia nazungumzia barabara hii ni kwa sababu, barabara hii ndio inabeba uchumi mzima wa wafanyabiashara wa Makete na kwa zaidi ya miaka 30, 40, 50 ambayo tangu nimezaliwa barabara hii wananchi wangu wanateseka kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili barabara hii ndio inapeleka karibia wagonjwa wote wanaotokea Mkoa wa Mbeya kwenye hospitali bora za Nyanda za Juu Kusini, Hospitali ya Ikonda. Wagonjwa wengi wanatoka Mbeya wanapita pale lakini wengi wanafia njiani kutokana na changamoto ya barabara hii. Barabara hii ni kitovu cha uchumi wa Wilaya ya Makete.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri; kwa uhitaji mkubwa tulionao barabara hii ni vyema tangazo likatoka mapema wananchi wakatangaziwa kwamba barabara hii inaanza kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nizungumzie barabara nyingine, barabara kutoka Chimara, Matamba, Kitulo; kwanza nizungumze jambo moja kwamba Waheshimiwa Mawaziri hasa hasa Wizara ya Ujenzi, ukiangalia Wabunge wengi hapa wana ahadi nyingi za viongozi ni vyema Wizara ya Ujenzi ikawa na benki ya ahadi za vongozi kwa wananchi wetu. Kwa sababu gani? Viongozi wakubwa wa Serikali wanapokuja kuahidi hizi barabara wanafanya wananchi waamini kwamba hizi barabara tayari zinakwenda kujengwa. Barabara ya Chimala, Kitulo, Matamba ambao ni kilometa 51 ni ahadi ya Waziri Mkuu Pinda hadi leo hii haijawahi kujengwa. Sasa wananchi wa Matamba, wananchi wa Makete wanaamini kabisa Waziri Mkuu akisema ndio tayari imeshatekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vyema wizara ikaanda benki ya statistics takwimu za ahadi zote za viongozi zilizotolewa kwenye majimbo mbalimbali ili tukawasaidia, tukawasaidia Wabunge hawa barabara hizo zitengenezwe. Ahadi ya Rais ni utekelezaji; kwa hiyo, ni vyema Wizara ya ujenzi ikaamua kufanya hicho kitu kuandaa takwimu zile ili kwenye bajeti hapa muweze kubeba pia viongozi wetu wa kitaifa wasionekane walivyoviahidi haviweze kutekelezeka. Zaidi ya miaka 10 ninayoizungumzia toka Mheshimiwa Pinda alipokuwa Waziri Mkuu hadi leo barabara ya Chimala, Matamba, Kitulo kilometa 51 tu, hadi leo hii haijajengwa. Kwa hiyo. niwaombe ni vyema mkaingalia barabara ile kwa jicho la ukaribu sana. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kitu kingine nizungumzie barabara ya kimkakati ambayo inatoka Songea inakuja Ludewa, inapita Lupila inakuja Ikonda, inakuja hadi Bulongwa kwa maana kupitia Ruvuma hii ni barabara ambayo inapita kwenye mpaka kati ya Tanzania na Malawi. Ni barabara ya kimkakati niiombe Serikali na hasa hasa nimpongeze Meneja wangu wa Mkoa wa TANROADS Injinia wetu Sharua ni mama ambaye anachapa kazi sana pale Mkoa wa Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana kwasababu gani, changamoto ya mvua yote tunayoizungumzia lakini barabara kama hii haijawahi kuhudumiwa mama yule anapambana na mfuko wa fedha ni mdogo kwa maana ya TANROADS lakini mama yule anapambana usiku na mchana kuhakikisha kwamba barabara hizi zinajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe wizara muiangalie Mkoa wa Njombe kwa jicho la karibu miezi nane mvua zinanyesha mkoa huu barabara huwa zinafungwa takribani miezi mitatu, minne watu hawafanyi shughuli za kiuchumi na wakati sisi ni wazalishaji wakubwa wa mbao, wazalishaji wakubwa wa parachichi, wazalishaji wakubwa wa viazi vya chips ambavyo mnavitumia, mngetukumbuka ili tuweze kutumia mkoa wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili kule Makete kuna mradi mkubwa ambao unakuja wa ujenzi wa bwawa la Lumakalya, ukitoka kwenye lile bwawa kuja kuitafuta Mbeya ambako kutakuwa na power plant ni zaidi ya kilometa 200 lakini hapo hapo kwenye lile bwawa unaweza ukatengeneza barabara fupi ya kilometa angalau 17 tu ambayo toka kipindi hicho Waziri Profesa Mwandosya anaipigania barabara ya kutoka Madiyani - Lufliyo kuelekea Tukuyu ni barabara fupi sana ambayo ingeweza kusaidia hata huu mradi mkubwa wa kimkakati wa umeme ukajengwa ili iweze kusaidia wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe Wizara ya Fedha pamoja na Wizara ya Ujenzi, mtusaidie barabara hizi zijengwe. Kuna sehemu nimesema viongozi wangu, hakuna heshima yoyote ile ya Ubunge, na heshima ya Ubunge wangu yoyote ile haitokani na tai au suti nzuri nilizovaa ni hii miradi kuona inatekelezwa ndio heshima yangu ya Ubunge. Heshima ya Waziri haitokani na kusoma vizuri bajeti ni utekelezaji wa bajeti hizi, watu wengi wanalalamika hapa, kuona kwenye Ilani zimo, kwenye kitabu cha Rais imo, lakini kwenye kitabu pia cha waziri mwenye imo lakini barabara hizi zinaishia kwenye makaratasi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, heshima ya bajeti kama hizi ni kuona zinatekelezwa, fedha zinatoka. Watu wametoa mawazo hapa kujenga miradi mikubwa ya zege ya matrilioni kwa own source tunaiumiza Nchi labda tuache mfumo huo twende kwenye mfumo ambayo hizi fedha za own source ziweze kusaidia kujenga barabara hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Mheshimiwa Waziri, heshima yako itatokana na utekelezaji wa Ilani, heshima yangu na Ubunge wangu 2025 utagemeaje na kwamba barabara ya kutoka Makete kwenda Kitulo hadi kufika Isyonja imetekelezwa ndio heshima ya Ubunge wangu, heshima ya Ubunge wangu sio uzuri wa tai niliyonayo ni kuona kazi inafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sina mambo mengi lakini barabara za Makete naamini zitakumbukwa kwenye wizara hii. Mungu abariki sana. Ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza kabisa niseme naunga mkono hoja, na nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake ambayo ameitoa leo; ni hotuba ya matumaini. Hata uteuzi wake alipokuwa anateuliwa kwenda Wizara ya Afya watumishi walitabasamu sana wakijua wamepata mtu ambaye walifanya naye kazi lakini kipindi chote amekuwa akionesha uwezo alionao wa hali ya juu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha kwanza, niseme wazi, kwa Watanzania wafahamu jambo moja, kwamba Mheshimiwa Rais kwenye Wizara ya Afya amefanya vitu vingi sana ambavyo havikuwepo kwa muda wa miaka mingi sana tangu nchi yetu ilipopata uhuru. Naenda tu kwa takwimu, kwamba, tulikuwa na Mheshimiwa Rais kwa kipindi chake tu kifupi ameongeza MRI sita ambazo hazikuwepo nchini, lakini Mheshimiwa Rais ameongeza CT-Scan 32, ambazo hazikuwepo kabisa nchini. Lakini wakati huo tayari sasa hivi ameshaanza kununua gari za ambulance 727, na tayari gari hizo zimeshaanza kuwasili nchini. Hii yote ni jitihada za Mheshimiwa Rais kwa ajili ya kuhakikisha kwamba sekta ya afya na Wizara ya Afya inaweza kutimiza malengo yake na inaweza kutimiza majukumu yake kama ambavyo Watanzania wamekuwa wakitegemea; ukiachana na ujenzi wa miundombinu kwa maana vituo vya afya na hospitali za mikoa. Mheshimiwa Rais kwa kweli anastahili kila heshima ambayo inatakiwa sisi kama Tanzania tumpe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya jambo kubwa kwenye taifa lolote lile ni suala la afya. Mtaji wa kwanza wa mwanadamu ni afya, si suala la fedha, si suala la nini, ni afya.

Unapoimarisha miundombinu ya afya kwenye taifa lolote umepigania maslahi ya taifa kwa kiwango kikubwa sana. Kwa hiyo mimi nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa sababu hata ukisoma takwimu na idadi ya vifo vya mama na mtoto vimepungua kwa kiwango kikubwa sana. Kwa hiyo tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa haya yote ambayo anayafanya; na hata ununuzi wa digital x-ray ameshanunua digital x-ray 199 na hata Wilaya ya Makete tumepata digital x-ray ambayo kitu ambacho sisi Makete hatukuwahi kukitegemea kuwa na digital x-ray tungeweza kupata pale Makete.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili, tumeona emergency ya hizi block, kwa maana EMD tayari hata Makete pia zimeshajengwa. Kwa hiyo, kwa niaba ya wananchi wa Makete, Mheshimiwa Waziri tunawashukuru sana kwa jinsi ambavyo mnafanya kazi, tunashukuru sana kwa maana ya kwamba Wakurugenzi na Wataalamu wa Wizara ya Afya, kwa kweli sisi kama Wabunge na mimi Mbunge wa Makete wanatupa ushirikiano.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo moja ambalo naliomba kwa ajili ya Makete, na wananchi wa Makete wanatusikiliza; ni suala la usambazaji wa dawa na vifaa tiba nchini. Hili ni lazima tuliangalie kwa ukaribu sana. Kwa mfano, mimi nina vituo vya afya takribani vinne vimekamilika, Kituo cha Afya Bulongwa, Kituo cha Afya Kitulo, Kituo cha Afya Mbalache kimeshakamilika, Kituo cha Afya Lukalilo kimeshakamilika, lakini hivi vyote vina changamoto ya kutokuwa na vifaa tiba ili vianze kutoa huduma. Tusingetamani sana vikae muda mrefu kwa sababu vitaanza kuleta taswira ya kwamba majengo yamejengwa lakini huduma haipatikani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naongea na Mkurugenzi wa MSD sasa hivi, na ameniahidi, nimpongeze sana Mkurudenzi wa MSD, anafanya kazi kubwa sana, ametuahidi kwamba atatuletea vifaa tiba pale Makete. Kwa hiyo nikuombe sana Mheshimiwa Waziri kwenye hili jambo muweze kutusaidia. Jambo langu kubwa lingine Mheshimiwa Waziri kuna hili jambo la wanafunzi ambao wanasoma udaktari; na hapo Mheshimiwa Waziri naomba tusikilizane sana. Tuna wanafunzi ambao wanasomea utabibu, mambo ya utabibu; wanasoma kwa muda wa miaka mitano. Wakishasoma kwa miaka mitano mnawapeleka internship, kwa maana wanakuwepo na ile pre-internship exam.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kunakuwa na changamoto kubwa sana. Watoto hawa wengi ni watoto wa masikini. Amesoma kwa muda mika mitano ameenda kufanya field, ametoka kwenye field mnampa mtihani huu. Huu mtihani ambao kwa kweli kwenye syllabus haupo, ila ninyi miliweka kama sehemu ya kuchujia kama sikosei au mlikuwa mna lengo gani? Lakini hawa watoto wamesoma miaka mitano, na ukisoma kwa takwimu za mwaka 2021/2022 kuna madaktari 200 ambao wamemaliza miaka mitano au wamesomeshwa na Maprofesa wetu hapa nchini, lakini baada ya kufanya mtihani wa pili internship exam wamekwama, mmewaondoa kwenye mfumo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa issue ni moja. Miaka mitano daktari amewekeza kenye kusoma lakini mtihani huo ambao si tu wa chuoni ni mtihani kutoka kwenye Baraza la Madaktari mnaita MCT. Ninaomba sana Mheshimiwa Waziri kumbuka hawa ni watoto wa masikini, angalieni utaratibu upya jinsi gani ya kuweza kuwasaidia. Kwa sababu hata rufaa zao ukataji wa rufaa kwa mtu ambaye amefeli hii pre- internship exam, mwanafunzi huyu utaratibu wa ukataji rufaa haupo open. Ninaomba sana Mheshimiwa Waziri, tuna watoto madaktari zaidi ya 200 wamekuwa disqualified licha ya kusoma miaka mitano darasani na wamefundishwa na maprofesa wetu hawa, lakini pili wameenda field na wamefanya vizuri. Huu mtihani ambao hauna syllabus inawezekana ninyi mmeweka ndio mlango wenu wa kufungulia mtu aweze kupita, lakini sasa umekuwa ni kikwazo kikubwa sana kwa madaktari wetu nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati ambao Taifa linahangaika na upatikanaji wa madaktari kwenye vituo vyetu vya afya na hospitali zetu ninaomba Mheshimiwa Waziri uliangalie jinsi gani ya kuliangalia. Ninajua mlichokuwa mnakiangalia. Kwamba kuna sekta binafsi ambayo imekuwa ikipitisha madaktari ambao wako disqualified wanaenda kutusababishia matatizo, lakini tafuteni namna jinsi gani ya kuweza kuwasaidia wanafunzi ambao wamepita Chuo Kikuu cha Muhimbili na Maprofesa ambao tunawaamini waweze wakaende kulisaidia Taifa. Hawa watu 200 ni watu wengi sana, wamesomea miaka mitano, mama ameuza miti ameuza kuni amefanya nini…

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa Taarifa mzungumzaji kwamba, ni muhimu sana tuka-standardize Madaktari ambao wametoka kwenye vyuo na sasa wanaenda kugusa mgonjwa kwa sababu, sasa inakuwa utaalam na huduma watakayoitoa inahusu kifo ama uzima wa mteja. Kwa hivyo, ni suala ambalo kama Taifa hatupaswi ku-compromise nalo kwa hivyo, pamoja na gharama mtu anayeweza kuingia kwenye training, lakini at the end of the day, daktari anaenda kugusa mtu na hujui atagusa nani; atakugusa wewe Mbunge, atagusa mkeo ama mtoto, usalama ni muhimu sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Haya ahsante. Taarifa hiyo Mheshimiwa Sanga.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Namheshimu sana Mheshimiwa Kigwangalla kwa sababu, hii ni field yake na hata mimi mawazo yangu yalikuwa ni hayo kwamba…

NAIBU SPIKA: Sasa mwite basi Dkt. Kigwangalla.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa, Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla. Mawazo yangu nami yanaendana na hayo, kwa sababu huu mtihani ulikuwa una lengo fulani ambalo Waziri analifahamu, lakini umekuja ku- include hata vijana ambao wako qualified na wamesomeshwa na Madaktari wetu. Kwa hiyo, naomba kama ni mchakato uweze kuangaliwa ni jinsi gani ya kuweza kudhibiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika jambo ambalo hatuwezi ku-compromise ni suala la afya na uhai wa mwanadamu. Hili pia nipitie hapohapo, kati ya jambo ambalo Mheshimiwa Waziri anatakiwa aliangalie sana ni maslahi ya Madaktari kwenye Taifa letu. Namwomba sana kati ya watu ambao tunaweza tukawa tunazungumza sasa hivi kwa sababu, tuna afya njema, toka hapa nenda Benjamin Mkapa, Muhimbili, sijui hospitali gani ya Mkoa, Rufaa, Bugando, Madaktari wanafanya kazi katika mazingira magumu kwa 24 hours. Naomba sana Mheshimiwa Waziri aangalie maslahi ya Madaktari kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi hapa tumeshiba tunaona ni jambo rahisi, lakini ukienda kwenye mazingira ambayo wanafanya kazi ni mazingira magumu. Takwimu zinaonesha mwaka huu tu 2022/2023, wagonjwa milioni 35 wamepitia kwenye mikono ya Madaktari wetu. Kwa hiyo, hili ni jambo muhimu sana na siamini kama Serikali inaweza ku- compromise kwenye kuboresha maslahi ya Madaktari wetu kwenye Taifa letu kwa sababu, sisi wote jeuri yetu ni afya. Wabunge, Mawaziri na watu wengine kama wakulima jeuri yao yote ni afya. Kwa hiyo, naomba sana Waziri aangalie suala la maslahi ya Madaktari kwenye Taifa letu wanafanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nenda kwenye vyumba vya watoto njiti na hili pia niweze kusaidia, Hospitali yetu ya Benjamin Mkapa ina changamoto ya mashine ya oxygen kwa ajili ya watoto njiti. Namuomba Mheshimiwa Waziri, hili waweze kulifanyia kazi, mashine za oxygen pale zimepungua na nimeshuhudia kwa macho yangu. Ni vyema sana wakiweza kusaidia Hospitali ya Benjamin Mkapa wakaongezewa mashine kwa ajili ya oxygen kwa ajili ya watoto wetu njiti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii, lakini nasema wazi kabisa Mheshimiwa Waziri anafanya kazi nzuri, Mheshimiwa Mollel anafanya kazi nzuri, lakini the master of all these ni Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ameenda kuifanya Sekta ya Afya ionekane ni moja kati ya sekta muhimu kwenye Taifa letu na ameweza kutusaidia kwenye mambo mengi sana. Mungu ambariki sana Mheshimiwa Waziri, achape kazi, sisi wadogo zake tuko nyuma na Mungu amsaidie sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi; cha kwanza nipende kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri ambayo ameiwasilisha, lakini kubwa ambalo nataka nizungumzie sehemu mbili; nataka kuzungumzia kuhua NARCO, lakini pia nizungumzie kuhusu Bodi ya Maziwa ambayo hiko chini ya Wizara yao.

Mheshimiwa Spika, ukizungumzia kwanza kuhusu Bodi ya Maziwa na mimi kule Makete nina shamba la Kitulo ambalo ni shamba bora na ni shamba zuri ambalo Wizara yenyewe inalisimamia kwa sababu liko chini ya Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Shamba lile juzi wakati nauliza swali hapa walinijibu kwamba Wizara inatenga kununua mitambo mitano ili kuliwezesha lile shamba kuendelea na uzalishaji wa maziwa. Mimi nisema jambo moja Wizara ninawaomba na ninawashauri ukiangalia hapa kwenye matumizi ya fedha ambapo tunazitumia kuagiza maziwa nchini ni zaidi ya shilingi bilioni 30 tunaagizwa kutoka nje kuleta kutoka nje kuleta ndani ya Tanzania, lakini Makete tuna shamba la Kitulo ambalo ng’ombe mmoja tu ana uwezo wa kutoa lita 50 kwa siku; je, Serikali haioni haja ya kuwekeza kwenye shamba lile ambalo kwa muda mrefu limekuwa likizorota, sasa hivi liko katika hatua ambayo kwa kweli haipendezi lakini eneo ni kubwa lipo.

Mheshimiwa Spika, niwaombe Wizara ili kukimbizana na hili jambo la maziwa njooni Makete kwenye shamba la Kitulo muwekeze. Wana Makete wako tayari wawekezaji wako tayari mfanye partnership na watu ili uweze kuwekeza tuwape maziwa ya kutosha, kwa sababu ukisoma kwenye hotuba ya waziri anazungumzia kwamba wanahitaji kuongeza vituo karibu 50 vya ukusanyaji wa maziwa nchini. Mnakusanya maziwa kutoka wapi wakati hamna mpango wa mkakati mzuri wa kuhakikisha mashamba haya ya Serikali ya uzalishaji wa maziwa yanatoa maziwa vizuri na naomba kwamba idadi ya ng’ombe waongezeke pale Kitulo.

Mheshimiwa Spika, lakini miundombinu ya shamba lile iongezeke, lakini pia maslahi ya wafanyakazi pale Kitulo yaboreshwa ili lile shamba liweze kufaidisha Watanzania wetu, lakini Wanamakete wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine ambalo nataka nizungumzie ambalo jana Mheshimiwa Spika jana alizungumzia, suala la NARCO lisiwe tena mjadala Wizara ni lazima iende ijitathmini jinsi ya kuipa majukumu mapya NARCO.

Mheshimiwa Spika, na uzuri ni kwamba mnasehemu ya kuanzia kwenye kikao cha Baraza la Mawaziri nilizungumza Waraka wa Baraza la Mawaziri wa mwaka 2002 Waraka Namba 2 walionyesha kabisa kwamba NARCO kuna mambo ambayo wameshindwa, kuyafanya ni vema Serikali ikaingia sasa mkakati wa kuwapa private sector maeneo yale muweze kuyasimimamia na kuyaendesha.

Lakini pili nikazungumzia kwamba kwenye kikao cha Waziri Mkuu cha tarehe 26 Februari, 2016 pale Kagera na bahati nzuri na mimi nilikuwepo kwenye kikao hicho, Waziri Mkuu aliagiza akasema kubainisha mpango bora wa matumizi ya ardhi ya NARCO ili kama Serikali haina uwezo wa kuendesha tujue ni nani aweze kupewa mashamba hayo. Waziri Mkuu alitoa hapa mna sehemu ya kuanzia na Waziri Mkuu alikuwa ni huyu Kassim Majaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaombe watu wa Wizara ya Mifugo NARCO ibadilishieni majukumu ya kazi ili maeneo yale ambayo Spika mwenyewe ameyazungumzia kwamba yamebaki wazi muda mrefu, Watanzania na vijana wa Kitanzania waweze kupewa na Wizara iweze kuwasimamia mashamba yale yaweze kuendeshwa, kwa sababu ukiangalia Kagera tu ina ranchi karibu nne, NARCO kazi wanayoifanya kule Kagera ni kutatua migogoro, hawajikiti kwenye kutatua suluhisho la hizi ranchi ziwezekufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, leo hii NARCO wanakuja na mpango wa mkakati wa kwamba Mtanzania awekeze kwa mkataba wa mwaka mmoja, hata mimba yenyewe ya huyo ng’ombe ndani ya mwaka mmoja haiwezi ikawa amepata mimba jamani, tusema jambo jema muwe na vitu vyenye tija kama Wizara kusaidia wananchi wetu utawekaje mkataba mwaka mmoja mtu akaweke uwekezaji pale, ongezeni kwenye majukumu kwenye NARCO iweze kufanya kazi ambayo sisi watanzania tutaona ina tija.

Mheshimiwa Spika, niendelee kusisitiza pia kwamba NARCO wenyewe watambue kwamba ule Mradi wa Ruvu na mtupe majibu leo hii hapa, Serikali mradi wa Ruvu wa shilingi bilioni 5.7 kwa nini hadi leo umelala huko kwenye coma, uko ICU, haujawahi endelea zaidi ya miaka kumi.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Festo Sanga.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, naomba muendelee kutupa majibu hayo ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii muhimu, Wizara ya Maliasili na Utalii. Jambo la Kwanza nipende kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi ambayo wanaifanya, lakini pia kwa wasilisho zuri la bajeti yao hapa Bungeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mambo mawili ya kuchangia; unapotaja utalii kwa kipindi cha sasa huwezi kuiacha Makete nyuma kwa sababu Makete ina hifadhi ya Kitulo, hifadhi ya kipekee hifadhi ambayo ukiambiwa utafute Bara zima la Afrika hata duniani ikiwezekana utaikuta Makete tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu umejikita kwenye mambo mawili; cha kwanza ni kuitangaza Hifadhi ya Kitulo. Kuna Wabunge wamezungumza hapa jana kwamba tumejikita kwenye kuzungumzia vyanzo vilevile vya utalii kwa maana Serengeti, Ngorongoro tunavitaja hivyo, lakini Hifadhi ya Kitulo ambayo kwa muda mrefu na ina upekee tumekuwa tukietelekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri wauiangalie sana Hifadhi ya Kitulo. Kwanza afahamu jambo moja kwamba kwa upande wa Nyanda za Juu Kusini kwa maana za highlands, Hifadhi ya Kitulo ndio ina mlima kwa maana iko kwenye ukanda wa juu zaidi kuliko hifadhi yoyote, kwa maana kwamba ina mlima ambao unaitwa Mtorwi Mountain ambao una urefu wa mita 2,961 kutoka usawa wa bahari, hamna sehemu nyingine ukiambiwa utafute nyanda za juu kusini iko ndani ya Kitulo, ndani ya Wilaya ya Makete.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba sana watu wasikimbilie tu kupanda mlima Kilimanjaro, Makete pia tuna hii, waanze kuitangaza, lakini ukiwa kwenye mlima huu unaiona moja kwa moja Malawi, Kyela na Matema. Ni fursa sasa kwa Wizara ya Maliasili kuruhusu hata uwekezaji binafsi kama Serikali imeshindwa tuite uwekezaji binafsi, waweke hata aerial cables, kwa maana zile aerial car cables za kutoka kwenye milima ya Livingstone, ukipita kule Unyangala, ukipita kule Utengule ukipita Kitulo yenyewe, ukielekea kule Busokelo inatakiwa watu wasafiri at least kwa aerial car cables kwenda kufika Matema, Kyela na utalii wetu ukakua, kuliko kuendelea kujikita kubaki kule Serengeti na Ngorongoro na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namsihi Mheshimiwa Waziri, sisi Makete hizi fursa zipo wazitumie wananchi. Sasa kwa nini tunapiga kelele? Ile hifadhi…

T A A R I F A

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kiruswa.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba niliwahi kwenda Taifa la Jamaica nikakuta mtindo wa utalii unaotumia hiyo kamba inaitwa aerial cable inaitwa zipline, unatoka mlima mmoja unakwenda mwingine kwa kuambaa angani na watalii waliokuwa wanakuja ku-experience jinsi ya kusafiri kwenye zipline walikuwa wanazidi milioni 12 kwa mwaka kwa nchi ile na uliwaingizia mapato makubwa sana.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Sanga unapokea taarifa hiyo?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea kwa mikono miwili, lakini naomba ulinde dakika yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kitulo tunaiomba sana waiangalie kwa jicho la pekee, zile aerial cables zinaruhusu kabisa mazingira ya kule na ukipita kule utadhani huko Alaska, kumbe upo Makete jinsi ambako kumepangika. Hiyo ni fursa ya namna nyingine

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nizungumzie jambo lingine kwa haraka kwa sababu dakika ni chache, ni suala la migogoro ndani ya hifadhi ya TANAPA kwa maana ile ya Kitulo na hii Game Reserve ya Mpanga Kipengele.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kitulo imezungukwa na maeneo mengi ambayo wananchi wanaishi. Kuna Vijiji vya Makwaranga, Misiwa, Nkondo, Lugoda, Kinyika na vingi ambavyo vinazunguka hifadhi hii. Hadi leo hadi GN inatoka tuliyoitunza ile hifadhi ni Wanamakete, lakini kilichojitokeza sasa hivi ni changamoto ya mipaka ile mikubwa kwa kiwango ambacho hakijawahi kutokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyozungumza muda huu kwenye Kijiji cha Lugoba kuna mwananchi wangu amefyekewa mazao na watu wa TANAPA, amefungwa ndani, wanasema ameingia kwenye eneo la hifadhi, lakini Mheshimiwa Waziri ukisoma Sheria ya Uhifadhi inakwambia kabisa; ibara ya 16 kifungu cha 5 inasema hivi: “For the purpose of the subsection (4), sitaisoma, the Minister shall ensure that no land falling under the village land is included in the game controlled areas.”

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo lakini Wizara wamechukua kwenye makaburi ya wananchi wetu. Hii hapa Mheshimiwa Waziri ataisoma. Ukienda kule Makete sehemu kwa mfano ya Mpanga Kipengere eneo la makaburi ya wananchi ambao kwa miaka mingi wamekuwa wakiishi, limechukuliwa limeingiwa ndani ya hifadhi. Juzi wananchi wawili wamefariki, wanaenda kuzika wamefukuzwa na watu wa game reserve. Pia angalia ukienda hapa maeneo ya Kinyika wananchi wangu shughuli zao kubwa ni za kulima viazi wanafukuzwa na watu wa TANAPA.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, watu wa TANAPA si wastaarabu, kwamba at least wangekuwa na mahusiano mazuri na wananchi; wanafyeka mazao, wanazuiwa watu kwenda kuzika kwenye maeneo ambayo walikuwepo, lakini nikwambie kitu kingine hadi shule wamechukua, wanasema inasoma ndani ya hifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, you can be a champion to this country, juzi tumefungua kitabu cha sensa, provision inaonyesha Watanzania tunaenda kuwa milioni 64. Mheshimiwa Waziri anaandaa mazingira yapi ya kukaa na watu milioni 100 Tanzania kwenye hifadhi ambazo wanaendelea kuwa nazo.

Je, tukiendelea na hizi sheria ambazo zinadhibiti wananchi kwa kiwango hiki, Watanzania wakiwa milioni 100 watawapeleka wapi. You need to be a champion to this country kuandaa sheria ambazo zitalinda nchi hii ikiwa na watu millioni 100 au 200.

Mheshismiwa Naibu Spika, kama tumeshindwa kujenga barabara zinazoweza kuishi miaka 20, tutashindwaje kuunda sheria inaweza ikawa na Watanzania milioni 200 mwakani; you can be a champion kwa kuunda sheria ambayo inatuhifadhi Watanzania zaidi ya milioni 200 kama ambayo milioni 64 wanakuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru lakini namwomba Mheshimiwa Waziri…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. FESTO R. SANGA: Dkt. Ndumbaro tunaamini katika hili ataandaa sheria ambayo itawa-acommodate watanzania milioni 200.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara hii, jambo la kwanza nipende kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri ambayo anaifanya kuhakikisha masuala kwenye Wizara ya Ardhi inakwenda vizuri, lakini pili nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri na kwa moyo wa dhati kabisa Mheshimiwa Waziri nakushukuru pamoja na Wizara ya Maliasili, tulikuwa na mgogoro uliochukua takribani miaka karibu kumi pale Kata ya Mfumbi, Wilaya ya Makete ulikuwa na changamoto kati ya Mpanga Kipengele na wananchi wa Mfumbi. Tunapozungumza haya ni kabisa wananchi wangu wanawashukuru sana kwa sababu mgogoro ule umeenda kutatuliwa katika ekari milioni 2.3 ambazo Mheshimiwa Rais amezitoa kwa wananchi na sisi Wanamakete tumenufaika kwenye eneo lile, wananchi wale wanawashukuru sana kwa niaba ya wananchi wa Makete tunawashukuru kwa haya yanayoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nipende kumshukuru sana Katibu Mkuu wa Wizara hii Engineer Anthony Sanga kwa kazi kubwa ambayo anaifanya na kwa kweli kwa sababu mimi ni Mjumbe wa Kamati hii tunafahamu Engineer Anthony Sanga saa hivi yuko na jukumu la kuhakikisha kwamba mifumo ya ulipaji wa kodi kwenye Wizara hii yanaenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunampongeza sana Mheshimiwa Katibu Mkuu na tunategemea kwamba suala la kwamba mfumo uko chini, watu wanashindwa kupata hati kwa wakati, litakuwa limeisha kwa sababu kote alikopita Anthony Sanga ameacha rekodi nzuri ya utendaji, kwa hiyo tiunaamini kabisa kwamba atatusaidia kwenye Wizara hii na mimi niamini kabisa kwamba kwa sisi Wanamakete tunajivunia kuwa na mtumishi ambaye anafanya kazi vizuri kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili napenda kumpongeza Mkurugenzi wa National Housing, Ndugu Hamad Abdallah, unajua Watanzania hawafahamu sasa hivi umekuja mfumo mpya wa PPP kwenye ujenzi wa hizi nyumba za National Housing na Mkurugenzi ameshatuonesha kwamba kuna viwanja kadha wa kadha kwenye Taifa letu na vipo kwenye eneo potential kama Kariakoo na maeneo mengine ambapo Watanzania wanaweza kushiriki kujenga nyumba hizi ambazo zinaweza kusaidia kwenye ukuaji wa sekta binafsi, lakini pia kwenye Shirika letu la Nyumba, kwa hiyo nawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo yangu mawili, la kwanza ni tuna migogoro mingine Mheshimiwa Waziri ndani ya Wilaya ya Makete, tuna mgogoro kati ya Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Mbeya kwenye eneo la Mbarali kwa maana Kata ya Mfumbi. Watu wako kutoka Wizarani walifika kwenye eneo husika wakaainisha eneo la mipaka, lakini changamoto iliyopo ni kwamba hamjaweka beacon.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokuweka beacon kumesababisha bado mgogoro uendelee kuwepo na hili ilitupa changamoto kubwa Mheshimiwa Waziri kwenye anuani na makazi, tuna vijiji zile anuani za makazi hazijawekwa kwa sababu ya mgogoro wa mpaka huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba mgogoro kati ya Mbeya na Njombe eneo la Chimala, eneo la Mbarali uweze kukamilishwa kwa kuweka beacon ili wananchi wa Makete wajue mpaka wao ni upi na wananchi wa Mbarali wajue mpaka ni upi ili tuondoe changamoto ya migogoro ambayo sisi Wanamakete tumeanza kuipata ya wafugaji kutoka Mbarali kuingia kwenye Jimbo letu la Makete.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mgogoro mwingine upo kati ya Njombe na Mbeya kwenye eneo la Kikondo ambapo huko nyuma ilikuwa ni kati ya eneo la Hifadhi ya Kitulo na baadae tukawaondoa wananchi likabaki kuwa eneo la Makete, lakini kuna changamoto pale kati ya wananchi wa Makete na wananchi wa Mbeya Vijijini, tunaomba mtusaidie kwa ajili ya kutatua mgogoro huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli mkitusaidia sisi Wanamakete tutashukuru sana ili shughuli zetu za kiuchumi ziweze kwenda vizuri na shughuli zetu za kiuchumi kwa wananchi wetu ziweze kwenda vizuri na niseme wazi kabisa kwamba Mheshimiwa Waziri suala la ardhi ndio suala mtambuka kwenye Taifa letu ambalo linaweza likatatua migogoro mingi sana. Sisi hatukuwepo na migogoro hii ya wafugaji na wakulima, sasa imeanza kujitokeza kutokana na kwamba matumizi bora ya ardhi yamekuwa ni changamoto na hayajafanyika katika Wilaya ya Makete.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu la pili ni kwenye suala la huu mkopo wa bilioni 350; Mheshimiwa Waziri na hii is for the good na ni kwa maslahi mapana ya Taifa letu, Taifa la Tanzania, Mheshimiwa Waziri tusaidie jambo moja tu hizi bilioni 350 Watanzania wanatusikiliza huko nje unapozungumza kwamba kwenye bilioni 350 kwenye uendeshaji tumekwenda kuweka bilioni 2.4, kwenye uratibu tumeweka bilioni 29 na kwenye dharura tumekwenda kuweka bilioni 17.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninavyozungumza hata kwenye vikao vya harusi siku hizi wameacha kuweka kitu kinaitwa contiguous kwa maana ya fedha ya dharura kwa sababu unapoweka fedha ya dharura kwenye eneo lolote lile una-rise doubts kwa sababu unapoweka hela ya dharura wakati kuna uhitaji wa fedha kwenye Tume ya Mipango kuhakikisha maeneo yetu ya ardhi mengi yanapimwa nchini, lakini unafedha ya dharura ya bilioni 17; hii dharura ni dharura ipi ambayo inaweza kwenda kutokea na ikatumia fedha zote hizo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaposhauri Mheshimiwa Waziri tunashauri for good, kwa sababu Watanzania wanatusikiliza na sisi ni Wajumbe wa Kamati, hizi bilioni 17 tungeweza kuwapa Tume ya Mipango wakatusaidia kupima ardhi kwenye maeneo mengi zaidi kuliko haya ambayo mmeyaainisha na Mheshimiwa Waziri wanapozungumzia bilioni 47 kwamba ziko kwenye uratibu, kwenye udharura na kwenye uendeshaji; trilioni 1.3 ya Mheshimiwa Rais tulitumia bilioni tano tu kwenye kuratibu mkopo mzima wa trilioni 1.3 kwenye mkopo wa Covid.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni jambo jema kama mtachukua hatua kuhakikisha kwamba fedha hizi bilioni 17 au bilioni 47 zinaenda kufanya kazi iliyokusudiwa. Mheshimiwa Waziri haileti tija na haina mantiki kwa mwananchi yeyote yule awe ameenda shule au hajaenda shule katika mkoa wa bilioni 350 tunaenda kutumia bilioni kumi tu kupima ardhi ni sahihi? (Makofi)

Ni sahihi Mheshimiwa Waziri? Unaweza ukazungumza kwamba tunakwenda kusimika mitambo, tunaenda kujenga nyumba, si tunataka tuangalie kipaumbele chetu kama nchi ni kipi? Ni kutatua migogoro ya ardhi au ni kujenga nyumba? Kwa sababu nchi hii ina majengo ya halmashauri sehemu zote ambapo tunaweza tukatumia ofisi za halmashauri tukafanyia kazi hii, tukapima ardhi yetu hizo nyumba zikafuata baadaye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuna uhitaji mkubwa wa kutumia hela nyingi kwenye…

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuna haja ya kutumia fedha nyingi sana kwenye kujenga nyumba na hivi vitu vingine ambavyo mmevizungumza tukaacha kupima ardhi yetu.

Mheshimiwa Waziri kipaumbele cha Taifa na cha Mheshimiwa Rais ni kuona migogoro ya ardhi kwenye Taifa letu inaisha na sio kuhakikisha kwamba kila ofisi au kila mkoa au kila wilaya imejenga ofisi ya ardhi. Hiyo sio kipaumbele chetu, kwa sababu gani Mheshimiwa Waziri? Sitaki kuamini kwamba hadi dakika hii Maafisa Ardhi wa Wilaya wanafanya kazi chini ya miti maana yake wanamaeneo yenye ofisi. Kwa hiyo, huu mkopo ungekuwa na tija endapo ungeelekezwa kwa kiwango kikubwa kwenda kupima ardhi. Mheshimiwa Waziri tulikuwa wote pale Arumeru Mashariki… (Makofi)

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

TAARIFA

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sanga pokea taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kingu.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nimpe Mheshimiwa Sanga taarifa kwamba kwa maneno ya msingi anayoyazungumza na kwa uzalendo ninaoujua kwa Mheshimiwa Waziri wetu wa Ardhi, nina imani kabisa kwa uzalendo nimeshafanya naye kazi, ninajua ushauri wa Mheshimiwa Sanga ataupokea Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sanga unapokea taarifa hiyo aliyokupatia Mheshimiwa Kingu?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea kwa moyo mzuri kabisa, kwa nini kwa sababu in their records wanajua kwamba Kamati ya Bajeti iliwashauri kuhusu mradi, Kamati ya Maliasili na Ardhi tunawashauri kuhusu mradi na sisi ni Bunge na sisi ndio Watanzania walioko nje tunasimama kwa niaba yao. (Makofi)

Kwa hiyo, tunachokizungumza hapa hatuzungumzi for bad, tunazungumza kwa jambo jema tu. Ngoja nikupe mfano kwenye Halmashauri ya Arumeru Serikali ilikopesha bilioni 1.6, Halmashauri ya Arumeru inaenda kuzalisha bilioni nane na imeshalipa na deni lote. Maana yake tukipima ardhi kwa kiwango kikubwa tutaingiza fedha nyingi kwa ajili ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Wizara ni Wizara mtambuka, hii Wizara inafanya parallel na Wizara ya Kilimo, hii Wizara inafanya parallel na Wizara ya Maliasili na Utalii. Leo hii Mheshimiwa Rais ameshusha mikopo ya kilimo kuja kwenye single digit kwa maana kwa asilimia tisa. Ukienda NMB, ukienda CRDB mikopo imeshuka, sasa mkulima hawezi kukopesheka kwa sababu ardhi yake haijapimwa. Kwa hiyo, hatuwezi kuwekeza bilioni 350 kwenye eneo ambalo linaenda kwa ajili ya kujenga ofisi, kusafiri, kununua nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ardhi si kwamba haina magari, ina magari, ina ofisi, inavyo vyote. Nimuombe Mheshimiwa Waziri this is for good, this is for your record, utaondoka kwenye Wizara hii, utaandika kitabu chako kama Mzee Mwinyi alivyosema cha kwamba ulifanya jambo kubwa la kupima ardhi kwenye Taifa letu, kutoka kwenye asilimia 23 zilizopimwa kwa sasa ukafika zaidi ya asilimia 50 kwa kutekeleza Ilani ya CCM na kwa kuokoa mauaji yanayoendelea Tanzania kutokana na migogoro ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Waziri tunaamini wewe ni mtu rahim, wewe ni mtu mwema, wewe ni msikivu, wewe ni mtu ambaye hutashupaza lolote kwamba sisi labda tuna nia mbaya kwa ajili ya hili, no this is our money, ni mkopo ambao wananchi wa Makete, mwananchi wa Bulongwa, mwananchi wa Iwawa, mwananchi wa Karagwe, mwananchi wa Mpanda, mwananchi wa wapi atalipa fedha hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunasimama kwa niaba yao ili bilioni 350 zikapime ardhi na sio bilioni 47 ziende kwa ajili ya kusimika mitambo ya ofisi wakati nchi yetu ina ofisi kila kona.

Mheshmiwa Mwenyekiti, ahsante, naamini Mheshimiwa Waziri ametusikiliza, naamini kabisa nimewawakilisha wananchi, mawazo ya wananchi wa Makete na mawazo ya Watanzania kwamba ….

(Hapa kengele ililia kiashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FESTO R. SANGA: Kwa maslahi yao. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Festo.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan. Tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa sababu yeye ndio ameitengenezea njia Wizara ya Maliasili na Utalii ikafanya vizuri sana kwenye suala la ukuaji wa utalii nchini kupitia the royal tour. Kwa maana ya filamu yetu ambayo imetangaza vyanzo vingi ambavyo tunavyo nchini na hifadhi zetu na baadaye tukafanya vizuri na kwa East Africa na ikiwezekana kwa Afrika nzima tukawa tunaongoza kwa idadi kubwa ya watalii ambao wamekuja kutokana na hii filamu ambayo Mheshimiwa Rais ameitengeneza. Kwa hiyo nipongeze sana hilo ambalo Mheshimiwa Rais amelifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha pili niweze kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri kaka yangu Mchengerwa ulikotoka umeacha miguu yako salama sana kwa sababu unafahamu na Wabunge wanafahamu na Watanzania wanafahamu kwamba kati ya Wizara ambazo zilikuwa kidogo tuseme ziko kwenye utulivu ilikuwa ni Wizara ya Michezo lakini ulivyopita wewe umeonesha kwamba Wizara ya michezo inaweza kuwa ni Wizara ambayo Watanzania wote wakajivunia lakini kelele zote zikawa zimeisha lakini pia business as usual ikawa imeondoka kwenye Wizara ya Michezo na hatimaye kila mmoja anakumbuka miguu uliyoikanyaga kwa Wizara ya Michezo. Wewe pamoja na Katibu Mkuu Dkt. Abbas ambaye mnashirikiana kwa ukaribu sana. Hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya kwetu ni matarajio kwamba hata kwenye Wizara hii, Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ambayo kwa kweli kwa historia Mawaziri wengi sana hawajadumu kwa muda mrefu kutokana na changamoto ambazo zipo kwenye Wizara hii lakini tunaamini wewe utakwenda kuwa mwarobaini kwa ajili ya kutusaidia kutatua changamoto hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, la kwanza nitazungumzia ongezeko la wageni. Ongezeko la wageni, tunaona kabisa takwimu zinaonesha kwamba tumetoka kwenye 1,700,000 na baadaye tumefika 3,800,000 kwa maana wageni wameongezeka kwa wingi sana. Mheshimiwa Waziri sasa ninaushauri kwenye jambo hili. Ushauri wangu wa kwanza tengeneza chain, mnyororo wa jinsi gani mgeni ameingia, amehudumiwa, amefika hifadhini, amelala, ametoka kwenye nchi yetu na in your record ujue mtalii huyu je, alirudi au hakurudi? Kwa sababu takwimu zinaonesha pia tuna changamoto ya watalii kutokurudi, sasa je, sababu ni nini? Mheshimiwa Waziri kwa hiyo, ninakuomba kwa sababu unataka kuifanya hii wizara iwe ni ya kiutofauti na watalii waongezeke zaidi naomba usaidie kujua chain. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimejifunza watu wanaokaa muda mrefu na watalii ni pamoja na madereva kwa maana kwenye tour guides wanajua mambo mengi sana ambayo watalii wanayazungumza. Usi-base sana kuzungumza na hawa ambao ni stakeholders wa sekta ya utalii kwa maana ya hawa wakubwa lakini nenda kwa hawa wa chini ambao ni madereva na hata tour guides wale wadogo, wapagazi pia. Jifunze watalii wanazungumnza nini kuhusu utalii wetu ndani ya nchi. Mheshimiwa Waziri kwa hiyo unaweza ukajifunza mambo mengi sana ambayo yanaweza kusaidia sekta yetu ya utalii kukua.

Mheshimiwa Spika, pia hifadhi za utalii zimekuwa ni zile zile kwa muda mrefu ambazo zinatamkwa. Mheshimiwa Rais kwa sasa amekuwa na mpango wa the hidden Tanzania, ni muda mwafaka sasa na nyie kwenda kuionesha dunia kwamba Tanzania kuna vivutio tofauti na hivi vya Serengeti na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, mojawapo ikiwa ni hifadhini kwetu Kitulo ambapo ni Jimbo la Wilaya ya Makete. Pale Kitulo ni moja kati ya hifadhi ya tofauti kabisa barani Afrika. Utofauti wake ni kwamba ni hifadhi ya maua ni bustani ya Mungu, ambayo Mheshimiwa Waziri nadhani mnaweza mkatumia pia hifadhi hii ikaweza kutusaidia na Mheshimiwa Rais ametupatia barabara ya lami ya kutoka Mbeya kwenda Makete, sasa hivi tunapita katikati ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni muda mwafaka mradi wa re-grow unaweza ukaenda kuisaidia hifadhi ile ikakua na ikawa na manufaa kwa ajili ya wananchi wetu wa Jimbo la Makete lakini na Watanzania wenzetu wote. Mheshimiwa Waziri pia nikuombe kuongeza idadi ya wanayama, mlitupatia pundamilia, mmetupatia wanyama wengine swala. Tunaomba muongeze idadi ya wanyama kwenye hifadhi hii kwa ajili ya kuendelea kukuza hifadhi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kwenye hili jambo pia la kukua kwa maana ya ongezeko la wageni. Nikuombe sana flow imekuwa ni kubwa sana ya wageni kwenye Taifa letu. Jambo ambalo tumepata changamoto ni malazi. Tulienda Karatu na unakumbuka tulivyokuwa kule, tumeona flow ya watalii ni kubwa na vyumba vya malazi vimeisha kabisa. Sasa sekta za kibenki zimelekea sana kwenye sekta ya kilimo na sekta nyingine. Ni muda mwafaka sasa wa kukaka katikati na benki ukazungumza nazo ikiwemo benki ambayo Serikali ina hisa nyingi Azania Benki ikaweza kusaidia na ikaweza kutangaza fursa za watanzania kukopa na kujenga na kuwekeza kwenye sekta ya utalii ili utalii wetu uweze kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nataka kulizungumzia ni jambo la reforms. Mheshimiwa Waziri lazima ufanye reforms. Hili niseme kwa sekta yako ya utalii hatuwezi kuendelea na business as usual kwenye suala la uendeshaji wa Wizara ya Maliasili na Utalii. Watakukasirikia, watakuchukia, watafanya kila kitu lakini ni lazima ufanye reforms. Reforms ya kwanza ni namna jinsi gani tunaweza kuutangaza utalii wetu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ukumbuke kwamba sisi tuko kwenye namba moja Barani Afrika kati ya Taifa lenye vivutio vya asili. Tanzania tunaongoza Barani Afrika, sasa haiwezekani kwenye mataifa madogo kuliko Tanzania yanafanya vizuri kwenye sekta ya utalii tena wana kivutio kimoja tu yawezekana ni Nyani lakini sisi tuna vivutio vingi tumeshindwa kufanya vizuri kwenye utangazaji wa utalii wetu.

Mheshimiwa Spika, sasa niombe kupitia bodi ya utalii Tanzania nina Imani kubwa sana Mkurugenzi wa Bodi ukimsikiliza mawazo yake ni makubwa sana muweze kwenda kutangaza utalii zaidi kuliko hapa ambapo Mheshimiwa Rais ametangaza.

Mheshimiwa Spika, nimeona una mpango wa kutangaza kupitia kwenye timu za mipira kwa maana kwenye michezo mbalimbali. Sasa Mheshimiwa Waziri tusirudi kwenye mkenge ule ule. Wakati ule tulitangaza utalii wetu kupitia Sunderland ikaenda ikazama, ikazama na utalii wetu. Ni muda mwafaka sasa kwenda kutafuta timu ambayo ina consistency nzuri kwenye performance ambazo zitaenda kutufanya tusikike na tufanye vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri kwa sababu nina records nimekuwa ni mdau wa michezo na wewe umekuwa mwanasheria kwenye mpira wetu Tanzania. Unajua kabisa timu inayofanya vizuri na watu wanaongezeka kwenye kui-support na inapofanya vibaya watu wanatoweka. Mnavyoenda kutafuta hizi timu kama mnatafuta ni Manchester, kama ni Real Madrid kama ni PSG ni nini, ninaomba Mheshimiwa Waziri usiingie mkenge wa kutafuta timu ndogo ndogo zikazama na utalii wetu. kwa sababu gani? Mheshimiwa Waziri nimejifunza hilo sana kupitia Sunderland ambavyo jinsi iliweza kutoweka.

Mheshimiwa Spika, pili Mheshimiwa Waziri lazima kwenye kuongeza Watalii tuwe na neno moja la kuitangaza Taifa letu. Tutambulike kwa neno moja leo hii ukienda huyu anasema visit Tanzania, ukitoka hivi anasema Tanzania ni forgettable sijui mwingine anaenda hivi. Lazima tuwe na slogan moja ya kufanya utalii wetu utambulike kwa namna moja kwenye Taifa letu. Kwa hiyo, reforms zingine utaendelea kuzifanya Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala la Ngorongoro. Tumehamisha watanzania wenzetu pale wameelekea kule Handeni kwa maana ya kupisha uotoasili wa Ngorongoro. Mheshimiwa Waziri lile jambo lazima mchakato uende haraka sana. Kumbuka kwamba maadui zetu na marafiki zetu wa karibu hawatutakii mema kuona sisi tunafanya hili jambo. Tulijitanabaisha, tulijionesha kwamba tuna uwezo wa kufanya hilo jambo na tumeweza kwa kiwango kikubwa na nipongeze Mheshimiwa Rais lakini kuendelea ku-delay wale watu unaweza kuona wanaanza kurudi sasa. Wanarudi kwa njia tofauti, tofauti kupitia makongamano kuhamasisha vitu kama hivi. Acha huu mchakato tuumalize kwa haraka andika historia Mheshimiwa Waziri kwamba uikamilishe hii safari kwa haraka ili wananchi wetu wa Ngorongoro wapate eneo salama na mchakato wa Ngorongoro uishe. Majirani wanatumia hawa watu kutugombanisha, majirani wanatumia hawa watu kuhakikisha kwamba utalii haukui, majirani wanatumia hawa watu kuhakikisha kwamba tunakwama. Kwa hiyo, mchakato wa Ngorongoro uweze kukamilika vizuri.

Mheshimiwa Spika, jambo langu lingine ni kwenye suala la migogoro. Kwanza nikupongeze umeshaanza ziara ya kuzunguka kwenye Mikoa tofauti tofauti. Mheshimiwa Waziri tunaomba sana changamoto ya Mawaziri nane ambao walikuwa wanazunguka, lazima tukubali changamoto ilikuwepo. Mara nyingi walikuwa wanafika muda mwingine Mkoani hawafiki kwenye kiini kabisa cha migogoro kule chini.

Mheshimiwa Waziri sasa tumia fursa hiyo, nikuombe sana nenda kwenye maeneo yale kwa sababu migogoro yetu mingi Tanzania ni kwa sababu ya kukosa ushirikishwaji. Ukiwasikiliza wale wananchi ambao walikuwa wanakupongeza juzi kwamba toka waisikie Serikali wewe ndio Waziri wa kwanza umegusa kufika kule Serengeti na ukawasikiliza. Lile jambo sisi kama Wabunge tunajifunza kumbe wananchi wako tayari kupokea maelekezo ya Serikali lakini changamoto ni kwamba Serikali haiwafikii wanafika pale wanawamrisha wananchi, hawawashirikishi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokuwashirikisha wananchi ndio kunasababisha migogoro mikubwa zaidi. Ni vema mkafika pale mkakutana na wazee wa eneo lile, mkakutana na wenyeviti wa vijiji wa eneo lile kwenye maeneo tofauti. Mheshimiwa Waziri na utakapokuja hapa nikuombe utupe umeainisha migogoro mingapi mikubwa nchini ambayo unampango mkakati nayo ya kwenda kuitatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kukuteua kitendo cha kufika kule Serengeti kimetupa majibu ya kwamba sehemu kubwa ya viongozi hawafiki chini kwenye migogoro. Wananchi hawana changamoto kabisa, kwa mfano kule Makete sasa hivi tumeanza tena migogoro na hifadhi ya TANAPA kwa sababu wananchi hawakushirikishwa. Mheshimiwa Waziri kwa hiyo, nikuombe sana, nakupongeza kwa sababu umenisaidia kumaliza migogoro kwenye Mpanga, Kipengele na wananchi wa Makete nawashukuru sana watu wa Maliasili na Utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mgogoro kati ya TANAPA-Kituro na wananchi wangu wa vijiji vya Makwaranga, Isapurano na maeneo ya Igenge maeneo mengine kama Makwaranga, maeneo kama Kigara yanatokana kwa sababu TANAPA wakifika wanachomeka bikoni wanaondoka. Huu sio utaratibu mzuri. Taifa letu halina shida sana, migogoro inatengenezwa na sisi viongozi. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, lakini baada ya kusema hayo niseme jambo moja tu kwamba ninamtakia kila lakheri Mheshimiwa Waziri ulifanya vizuri kwenye Wizara uliyopita ya Michezo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa kengele ya pili imegonga.

MHE.FESTO R. SANGA: Naam.

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana, nimtakie kila lakheri Mheshimiwa Waziri. Wewe ndio Ronaldo wetu, Messi wetu tumekuachia mchezo huu cheza sana. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri lakini cha pili nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa jinsi alivyoweka mguu wake asilimia 100 kwenye suala la michezo Tanzania, nina kila sababu ya kujivunia kama mdau wa michezo nchini kuona kwamba Mheshimiwa Rais ameweka asilimia 100 mguu wake kuona ana-support michezo nchini Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nimpongeze sana Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Michezo na kuna mambo nitakayomshauri hapa, lakini nimpongeze pia ndugu yetu Mapana kwenye BASATA. Naenda haraka kwa sababu dakika ni chache na hii inaonyesha kwamba hii Wizara pia kuna changamoto, huu muda ilitakiwa tuchangie mambo mengi sana kwa ajili ya ku-support Wizara yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dkt. Mapana wakati kuna siku mimi nilisimama hapa nilisema, “BASATA imegeuka kuwa mahakama ya wasanii” lakini Dkt. Mapana ameibadilisha BASATA sasa imekuwa ni sehemu ambayo wasanii wanapata haki zao. Kwa hiyo ninampongeza sana Mtendaji Mkuu wa BASATA kwa kile ambacho anakifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nina hoja zangu. Kabla ya hapo pia niipongeze Yanga kwa yale ambayo wameyapata kule Algeria na ni wamefanya kitu kizuri na kwa sababu ya Yanga pia hata Simba tumeweza kuhudhuria jana kwenye mwaliko wa Mheshimiwa Rais na wanamichezo wengine, kwa hiyo, tunawapongeza. Pia niipongeze timu ambayo pia ni sehemu ya uongozi timu ya Singida Big Stars kwa kuingia kwenye michuano ya Shirikisho, mwakani Big Stars Singida tunaingia kwenye Shirikisho Barani Afrika na tuwahakikishie Watanzania tutafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ya kwanza iko kwenye michezo kwenye viwanja. Mheshimiwa Waziri mwaka jana tulitenga bajeti hapa ya shilingi bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa viwanja. Hakuna sehemu inasomeka kwenye bajeti yenu suala la shilingi bilioni 10 popote pale halisomeki. Sasa mimi niwape tu ushauri kwa bajeti ya shilingi bilioni 35 hii hamuwezi kufanya kitu chochote, lazima mtoke out of the box kwenye kutafuta ni namna gani mtasaidia ujenzi wa viwanja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fanyeni kama Zambia niliwashauri, jambo la kwanza, tunajenga mradi wa SGR, mradi wa SGR Mkandarasi yule ilitakiwa CSR yake tumpe kazi ya kujenga uwanja mmoja, angeweza kuwasaidia na mkaondokana na changamoto hii. Tunajenga Bwawa la Mwalimu Nyerere, CSR ya ujenzi wa Mwalimu Nyerere mngempa kazi ajenge bwawa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zambia walifanya hivyo kwenye coper belt wamejenga viwanja vyao kule kwamba CSR inayotokana na migodi tunajenga viwanja. Sisi kwa shilingi bilioni 35 hapa tutaendelea kupigana chenga, kwa sababu gani Mheshimiwa Waziri? Shilingi bilioni 35 itaenda kujenga nini kwenye viwanja vyetu vya nchi yetu? Nikuombe tokeni nje, tafuteni watu, tafuteni wadau waweze kuwa-support kujenga viwanja. Tafuteni fedha kwenye makampuni haya. Mgodi kama wa Barrick mwaka huu wametoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa mashule, Makete nimepokea karibu shilingi milioni 540. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barrick wapeni task wajenge angalau uwanja mmoja. Nendeni pale GGM, pale Geita Gold wajenge uwanja mmoja. Mimi nawapa mbinu tu za kuweza kupata fedha ili muweze kusaidia kujenga viwanja nchi hii, tofauti na hapo ni danadana tutamaliza miaka mitano kwenye Ilani tutakuwa hatujatekeleza kitu na mpango wa Mheshimiwa Rais ku-support michezo nchini utakuwa haujafikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu lingine ni kwenye suala la reforms. Kuna sheria ambazo zipo ndani ya TFF na taratibu. Moja kati ya jambo ambalo ningetamani TFF na Watanzania ni suala la kwenye makato kwenye mapato ya viwanja kwa wachezaji wetu. Hizi timu zinatumia gharama kubwa sana kwenye uendeshaji. Sasa inapotokea timu imeenda kwenye mechi imecheza, yale makato ya mapato kwa maana ya gate fee ni lazima Serikali ione, lazima TFF waone jinsi gani ya kuzi-support timu zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natolea tu mfano kwenye ule mchezo ambao ulipita mchezo wa Simba Sports Club dhidi ya Yanga ambapo kwenye mchezo wa Simba Sports Club dhidi ya Yanga zilipatikana jumla ya shilingi 410,000,000 lakini Simba wameenda kuambulia shilingi 183,000,000. Angalia mgawanyo pale, kuna VAT, kuna gharama ya tiketi shilingi milioni 22, kuna uwanja shilingi milioni 47, kuna FA (Chama cha Mkoa) shilingi milioni 18, kuna Bodi ya Ligi shilingi milioni 25, kuna TFF shilingi milioni 12. Saidieni hivi vilabu. Mheshimiwa Waziri nikikwambia bajeti ya kuifanya klabu ikae camp. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikikaa camp Simba Sports Club kwenye mchezo wa Yanga they are spending zaidi ya shilingi milioni 100. Sasa leo unaenda kupata zaidi ya shilingi milioni 410 kwenye mchezo wao wanaenda kupata shilingi milioni 138 tu, zaidi ya shilingi milioni 300 zimeenda kwenye mifuko ya watu wengine. Mheshimiwa Waziri mimi nimekuwepo kwenye mpira, ukienda hawa watu ambao wanapatiwa hizi fedha wana udhamini kutoka Azam. Azam anavyotoa udhamini kuna fedha inaenda Bodi ya Ligi. NBC anavyotoa udhamini kuna fedha zinaenda Bodi ya Ligi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa watu wana faini kwa wachezaji kila siku unasikia sijui Morrison kafungiwa analipa shilingi milioni tatu, sijui ukisikia Simba imefanya nini, imelipa shilingi milioni tano, ukisikia sijui Yanga imefanya jambo gani inalipa shilingi milioni 10. Hawa watu they accumulating a lot of money. Hizi fedha zingine waweze kuvisaidia vilabu vyetu vikaendesha kwenye mambo yao ya michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine Mheshimiwa Waziri ambalo nataka kukushauri, kwanza kukupongeza ni jinsi gani ambavyo sekta ya uigizaji Tanzania inafanya vizuri, ninakuomba Mheshimiwa Waziri BASATA, Bodi ya Filamu Tanzania wanafanya jambo zuri sana, hapa nitoe complement yangu kwa huyu mtu anaitwa Leah Mwendamseka (Lamata) amefanya jambo moja kwenye uigizaji, anatengeneza series, amefanya jambo zuri sana sasa Tanzania inaenda kutambulika angalau kwenye uzalishaji wa series umeenda kwenye jambo zuri, anazalisha vizuri. Huyu mtu tumpongeze na tuone hata wadau wengine ambao wanafanya hii kazi ya uzalishaji kwenye Bongo Movie na kwenye uigizaji tuweze jinsi ya kuwa-support. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua hawa waigizaji wakienda sehemu kuigiza, vibali vya kupata vya kuigizia maeneo fulani ya Serikali inakuwa ni ngumu kupata. Tuweze kutengeneza mazingira ambayo inaweza kuwasaidia ili filamu zetu Tanzania ziweze kuzalishwa katika ubora. Kwa hiyo, ninatoa complement kwa Lamata kwa jinsi alivyoifanya Jua Kali na kampuni inavyofanya vizuri na kwenye nyanja za Kimataifa nadhani katika uzalishaji ameenda vizuri sana. Kwa hiyo, nipende kupongeza kwenye hilo na niombe Mheshimiwa Waziri waigizaji nchini waweze kuangaliwa kwa jicho la karibu ili mazingira yao ya kufanya kazi yawe katika ubora, hasa maeneo ya kuigizia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine Mheshimiwa Waziri ni jambo la shule. Mlisema mnajenga shule za michezo nchini na tunaye Leonard Tenga hapa yuko hapo juu, anajua kabisa tulikuwa na Makongo ikazalisha wachezaji wengi ambao wamekuja kulisaidia Taifa letu. Leo hii alipita hapa Waziri Bashungwa huyo hapo nyuma, alituahidi kwamba mnajenga shule, akapita Waziri Mchengerwa akaahidi anajenga shule, unakuja wewe anaahidi mnajenga shule, hamna shule iliyojengwa hata moja, shule za michezo nchini ambazo zinaenda kuzalisha specific kwa ajili ya kuzalisha soka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Makongo ilizalisha wachezaji wengi kwenye Taifa letu. Fanyeni mchakato wa kujenga shule, hata mkianza na mbili za mfano, sisi wadau wa michezo watajisikia amani kuona kwamba mnaenda kulisaidia Taifa letu. Kwa hiyo ni vema….

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kw Amuda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana muda wetu umeisha.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kengele ya pili?

MWENYEKITI: Ee ndiyo, unga mkono hoja muda wako umeisha Mheshimiwa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa niseme naunga mkono hoja lakini nilikuwa na jambo kubwa sana kuhusu mfuko wa maendeleo. Wanakusanya fedha lakini hatujui ni kiasi gani kimekusanywa hadi leo. (Makofi)

MWENYEKITI: Utaleta kwa maandishi.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye hoja iliyoko mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ninaunga hoja mkono asilimia 100 kabisa na kwa upekee kabisa nipende kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Niseme wazi kabisa kwamba Mheshimiwa Rais kazi anayoifanya ni kubwa kwa kiwango ambacho tumetekeleza bajeti kwa Wizara zote kwa zaidi ya asilimia 50. Hii inaonyesha kwamba Wizara ya Fedha pia na Mamlaka ya Mapato Tanzania wanafanya makusanyo vizuri. Tuwapongeze sana; kwa sababu sehemu kubwa ya miradi ya maendeleo inatekelezwa vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nina hoja zangu mbili. Hoja ya kwanza ni kuhusiana na suala la unclaimed financial asset. Nilizungumza wakati ule na niliahidiwa kwamba litakuja kutolewa ufafanuzi mwaka huu; na niko hapa nikisubiria ufafanuzi kuhusu unclaimed financial assets kwenye Taifa letu. Hawajawahi kuzungumza popote ambapo hizi fedha ambazo zimekuwa unclaimed kwenye benki, kwenye mitandao ya simu na hata kwenye maliasili, kwenye vituo vya polisi. Ukisoma kwenye ripoti ya CAG anazungumzia bodaboda zipo kwenye vituo vya polisi zina miaka mitatu, minne zinauzwa hadi kwa shilingi 20,000 kwenye ripoti ya CAG. Kwa hiyo ni vyema Mheshimiwa Waziri wakatoa ufafanuzi fedha hizi zinaenda wapi, ambazo ni mali ya Watanzania na walituahidi kwamba watakwenda kulifanyia kazi kupitia Ofisi ya PST. Kwa hiyo ninaomba majibu Mheshimiwa Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nipende kupongeza, tulishauri kwenye Bunge kuhusu kupunguza msururu wa watendaji wa Serikali kuingia kwenye maduka ya Watanzania na wafanyabiashara wanaonzisha biashara zao. Tulizungumza hapa kwamba mtu anaanzisha biashara lakini kuanzisha kwake biashara ni kama anafanya kitu haramu kwa sababu akiamka asubuhi watu wa fire wameingia, watu wa NEMC wameingia, watu wa OSHA wameingia, watu wa TRA wameingia, watu wa service levy wameingia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukashauri hapa Serikali itafute namna moja ya ku-centralize hii iwe ni moja tu. Mtu alipe tu hiyo Serikalini kwa mwezi kugawana. Na naona kuna mawazo yako kwenye bajeti hii umeyatoa; nikupongeze sana, kwamba kwa hili unakwenda kuilinda sekta binafsi, na kwamba ni nia ya dhati ya Mheshimiwa Rais kuona sekta binafsi nchini inalindwa ili mfanyabiashara apate muda wa kuhudumia zaidi wateja kuliko kuhudumia watumishi wa Serikali; na kwa kweli mnaenda kuandika historia. Ule mfumo, tulisema hata waleti mwanaume kujaa waleti mfukoni vimejaa vitambulisho sio jambo zuri tuwe na kitambulisho kimoja ambacho kinaweza kikasaidia. Kwa hiyo niseme hili unaloenda kulifanya unaenda kufanya jambo la kizalendo kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuzuia kamata kamata. waheshimiwa Wabunge walipiga kelele hapa wakati NEMC wamefungia na maeneo tofauti tofauti. Bado ni mwendelezo wa Mheshimiwa Rais kulea sekta binafsi kwenda kuzuia sasa kamata kamata tu-deal na muhusika ambaye amefanya hujuma yoyote ile ndiye tuhangaike naye. Hii itasaidia hata Kariakoo na maeneo mengine ya masoko na hata sekta ya biashara kukua ili tuli-deal na hawa wahusika ambao sioy kuliko ku-deal na biashara ambayo tunakuwa tunasababisha Serikali inakosa mapato. Kwa hiyo mimi nipongeze kwenye hayo mambo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa jambo langu na agenda yangu ipo kwenye jambo moja; na hili ndio nililotumwa na Makete hili wamenituma watanzania, hili wamenituma wakulima wa ngano kwenye Taifa letu. Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yako ukurasa namba 149 unasema una mpango wa kutoa unafuu wa ushuru wa forodha kwa uratibu wa duty remission kwa kiwango cha asilimia 10 badala ya 35 kwa mwaka mmoja kwenye ngano inayotambulika kwa HS Codes hizo hapo, lengo lake ni kupunguza gharama za maisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa Waziri inawezekana una nia ya dhati kabisa lakini nia yako ya dhati inawezekana inaenda tofauti na mpango wa Mheshimiwa Rais, tofauti na Waziri wa Kilimo, tofauti na kile kinachofanyika field. Mimi ni Mbunge wa Makete, Mheshimiwa Rais ametupa ngano tani 80 kwa ajili ya wananchi wetu na amegawa bure Makate na inawezekana na mikoa mingine kama Arusha ameigawa bure. Lengo la Mheshimiwa Rais ni kumsaidia mkulima na ngano iweze kuoteshwa kwa wingi nchini ili soko la ndani la ngano liweze kufanya vizuri. Unapokuja na mpango huu Mheshimiwa Waziri unataka kutuambia ni kama mnataka kumuhujumu mkulima. Kwa nini? ukisoma ukurasa wa 257 kwenye hansard za Bunge za Waziri wa Kilimo Mheshimiwa Hussein Mohamed Bashe anazungumza naomba Wabunge mnisikilize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bashe anasema hivi; “Mheshimiwa Spika, niongelee hii issue ya ngano na alizeti. Sisi tuna-import ngano tani milioni moja kwa mwaka. Ili tujitosheleze ngano tunahitaji ngano tani 50,000 za mbegu za kwenda kumpa mkulima alime. Tumechukua hatua gani?” Akaendelea; “Mheshimiwa Spika, nataka niseme mbele ya Bunge lako tukufu niseme mbele ya Wabunge na mbele ya Watanzania kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu 2025/2026 tunaendelea kuzalisha ngano. Mwenye mamlaka ya kuwapa cheti cha ku-import ngano ndani ya nchi ni Waziri wa Kilimo. Kama nitakuwa kwenye kiti viwanda vitageuka chuma chakavu, hawataingiza hata kilo moja kama hawajanunua ngano ya Watanzania.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bashe anazidi kuongea, anasema; “Mheshimiwa Spika, Watanzania hawatakufa kwa kukosa ngano, haiwezekani unambembeleza. Mmefanya nao trial tumewapa mbegu wao wenyewe kwenye maabara zao wamesema inafaa halafu wakati wa ku-sign MOU wanasema hatutaki. Over my dead body wata-sign mkataba, wasipo-sign hatutawapa phyto sanitary ya kuingiza ngano, watajua watakachokifanya na viwanda vyao”. Huyu ni Waziri wa Kilimo analizungumza hilo, huyu ndiye aliyesambaza mbegu kwa wakulima, huyu ndiye aliyetuma hasa ikazalishe mbegu, huyu ndiye anakaa na Mheshimiwa Rais kwenye sekta ya kilimo, wanapanga ili ngano izalishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kila mwananchi wa Makete amezalisha ngano leo unakwenda kumwambia huyu mtu aingize ngano kwa ushuru wa kutoka 35 kuja kwenye 10 percent, hii ni sabotage kwa mkulima wetu, hii ni sabotage kwa wana-Makete, hii ni sabotage kwa mwananchi aliyeko Mbulu. Hii ni Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania; mnazungumza jambo moja lakini kwa lugha tofauti. Tukimruhusu mfanyabiashara aingize ngano Mheshimiwa Waziri Bashe anasema hawa watu wamemkataa kwenye MOU manake unataka utuambie amezunguka nyuma, wamekutana na watumishi wako wa Wizara wamemwambia shusha kutoka asilimia 35 percent uje kwenye asilimia 10 percent. Kufanya hivyo ili Waziri wa Kilimo aendelee kubaki katika msisitizo wa kwamba hawa wanabaki na viwanda vyao kumbe wametengeneza lango lingine la kuingiza ngano kwa kupitia kushusha ushuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa Waziri Mwigulu una heshima kubwa kwenye Taifa letu, ninakuomba sana achana na hii biashara. Tumepita kwenye covid tukiwa kwenye asilimia 35, tumepita kwenye mtikisiko wa uchumi tukiwa na asilimia 35, unaendaje saa hizi angalau hali iweze kupoa tunaanza kushusha kwenye asilimia 10? Tunaua viwanda vya ndani. Mimi nitaenda kuwaambia nini wananchi wa Makete, Matamba na Ikuo ambao wameacha mazao yote nimewaambia limeni ngano? Leo hii mnaenda kuwaambia wafanyabiashara washushe ngano waingize kwa asilimia asilimi 10 waache 35.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Mheshimiwa Waziri kwa kushirikiana na Waziri wa Viwanda na Biashara; kweli inawezekana tuna upungufu wa ngano tafuteni utaratibu wa kuweka kibali maalum kwa ajili ya kuingiza huyo mtu lakini si kwa asilimia hii mliyoitaja, tunaenda kuua wakulima wetu. Yaani Mheshimiwa Anthony Mtaka pale Njombe amepambana kweli kuhakikisha ngano inaota. Mimi nimepambana kweli kuona ngano inaota. Mkuu wa Wilaya ya Makete Mheshimiwa Juma Sweda amepambana kweli kuona ngano inaota. Mkurugenzi wangu Ndugu William Makufwe amepambana kweli kuhakikisha ngano inaota. Na hata juzi Tume ya Mipango imekuja tumeanza kupima vijiji 41 na kuwapa hati kwa sababu ya zao la ngano. Leo tunakuja kusomewa hapa mfanyabiashara anaongezewa dirisha la kuingiza ngano nyingi ili ngano ya ndani izame. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba sana Mheshimiwa Waziri, hili ni jambo la muhimu sana kwenye Taifa letu. Waziri wa Viwanda na Biashara, Waziri wa Kilimo kaeni chini tusaidieni. Mheshimiwa Waziri najua una nia njema ninajua una nia njema lakini nia yako njema inaenda kuzamisha watoto wako wa ndani, unaenda kuzamisha familia yako Mheshimiwa Waziri. Nikuombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha nikuombe…

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri anakuomba tu huyo utakuja kumjibu.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikuombe unafanya vizuri sana kwenye Wizara yako, miradi iko kedekede umetupelekea fedha huku hatujawahi kuziona fedha nyingi kwa kiwango hicho…

MHE COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. FESTO R. SANGA: …hili kosa la kuruhusu ngano iingie lisiende kufanyika …

MWENYEKITI: Kuna taarifa Mheshimiwa Festo.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, unanizamisha mimi, unazamisha Wabunge, unazamisha Wabunge ambao kila siku…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Festo kuna taarifa yako, Mheshimiwa Cosato Chumi.

TAARIFA

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba, mojawapo ya hatua ambazo tunatakiwa kuzifanya ni kuhakikisha kwamba tunapunguza kuagiza bidhaa muhimu kutoka nje ili kujijengea uwezo wa ndani. Sasa basi analolisema la kibali ni muhimu, tumefanya hivyo katika sukari matokeo yake tulikuwa tunaagiza tani 300,000 leo hii tunaagiza tani 15,000 na viwanda ndani vimeshamiri na wananchi wetu wanapata ajira. Kwa hiyo anachokitetea siyo kwa wananchi tu wa Njombe, wa Makete, ni wa Tanzania nzima na Taifa kwa ujumla. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Festo, unaipokea hiyo taarifa?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea hii taarifa, kwa sababu tunaenda kulinda viwanda vya ndani, tunaenda kulinda wakulima wetu napokea kabisa. Nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, aachane na hii biashara, huu ni mchezo, wamemzunguka Mheshimiwa Bashe kule kwenye MoU, mbegu wameenda nayo maabara wao wenyewe, wamepima wakasema Waziri hapa tutaingia pamoja kwenye hii. Walivyofika kwenye kusaini mezani wakamgeuka kumbe wameona dirisha nyuma ya Waziri, wamepita huko, wameenda kushusha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri aachane na hii biashara, amsaidie Mheshimiwa Bashe, awasaidie wakulima wa Makete, Njombe, Iramba, Kisasatu na awasaidie wakulima wa kila eneo la Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, hoja yangu ni ngano na nitakufa nayo, kwa sababu hizi ndiyo kura za CCM, hizi ndiyo kura za Mheshimiwa Rais, hizi ndiyo kura za Taifa langu, lazima niwapiganie, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye bajeti hii iliyoko mbele yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza nipende sana kumshukuru Mheshimiwa Rais Mama yetu Samia kwa jinsi ambavyo anachapa kazi. Lakini Zaidi nimshukuru Waziri wa Fedha Mheshimiwa Mwigulu Nchemba kwa bajeti ambayo kwa kweli mimi kama kijana najivunia na kama Mtanzania najivunia kwamba ni bajeti ambayo imeenda kuleta mabadiliko makubwa sana. Shukrani hizi nazitanguliza na quote moja kutoka kwa Rais Mstaafu wa Marekani Barack Obama, anasema; “Change will not come if you wait for someone or other person. We are the ones we have been waiting for, we are the change that we seek.”

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi niseme jambo moja, kwamba Mheshimiwa Waziri you are the game changer. Wewe ni game changer kwenye siasa ya Serikali yetu kwa sababu gani, bajeti hii inatubeba Wabunge wote katika majimbo yetu huko tunakoenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa muda mrefu tumekuwa tukilisubiria jambo kama hili, kuwa na bajeti ambayo ni inclusive kwa mawazo ya Wabunge, ya Mawaziri na wananchi. Ndiyo maana wakati wote Mheshimiwa Waziri wa Fedha akiwa anasoma bajeti hii hapa alisema nimeagizwa na mama tuzungumze na Waziri wa TAMISEMI, nimeagizwa na mama tuzungumze na Waziri wa Mambo ya Ndani, nimeagizwa na mama niongee na Waziri huyu; maana yake ni kwamba ni bajeti ambayo ni inclusive kuanzia Mawaziri hadi Wabunge. Hili ni jambo ambalo nasema wewe ni game changer. Kwa hiyo mimi nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nasimama kwa mara nyingine tena nikishukuru. Mimi hili ni Bunge langu la kwanza la Bajeti, lakini nilishauri mambo karibia Matano kama siyo manne ndani ya Bunge hili na yote yamependekezwa kwenye bajeti hii na yanaenda kupitishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza nilishauri Serikali iondoe kodi kwenye nyasi bandia, Serikali imepokea na imeenda kulifanyia kazi. Nilishauri kwenye Bunge hili kwamba kwenye michezo ya betting, betting companies zichangie michezo kwenye nchi hii, bajeti imelichukua imeingizwa humu ndani, asilimia tano za betting companies zitakuwa zinapelekwa kwenye michezo. Nilisimama kwenye Bunge hili nikashauri kuwa gharama za bodaboda ni nyingi, mama yetu amesikia kilio cha bodaboda zimeondolewa toka elfu 30 hadi elfu 10.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nikasimama kwenye Bunge hili tena nikashauri viwanja vyote vya mpira kwenye nchi hii viwekwe nyasi bandia. Rais akiwa Mwanza juzi ameagiza Chama cha Mapinduzi kuanzia sasa kiruhusu mchakato wa kuweka nyasi bandia kwenye taifa hili. Kwa niaba ya wanamichezo wa taifa hili nimesimama kushukuru na kusema ahsante sana. Kwa sababu haya ambayo mmeyafanya hamyafanyi kwa maslahi ya Watoto wenu mnafanya kwa maslahi ya Watanzania wote. Wanamichezo walioko huko saa hizi wanasherehekea kuona kwamba sasa mpira wao utaenda kufanyika vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si hivyo tu, masuala ya betting companies sasa yataenda kuchangia michezo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sitatumia dakika nyingi sana nikuombe jambo moja tu katika wakati wako na wakati mwingine hayo umetupokea. Suala lingine nilishauri Serikali iangalie namna ya kuunda ama kampuni au wakala wa kuruhusu vifaa vya michezo vipunguzwe kodi mashuleni; mambo ya jezi na mipira, nilishauri hapa ndani ya Bunge. Na ninakusihi Mheshimiwa Waziri, ninakumbuka una ahadi kule Ruruma Sekondari, ninakumbuka una ahadi kule Kengege Sekondari. Kila Mbunge ameahidi vifaa vya michezo huko kwenye shule mbalimbali. Ukienda kwa Mheshimiwa Tulia, Mbeya Sekondari ameahidi vifaa vya michezo, ukienda kwa Mheshimiwa Waziri wa Ardhi ameahidi vifaa vya michezo kule Iringa. Kila Waziri hapa ameahidi vifaa vya michezo shuleni.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ione tija sasa kuwa na wakala maalum ambako sisi Wabunge tutaenda kununua vifaa vya michezo kwa punguzo ili nchi nzima watoto wetu wasianze kushangaa kuona jezi wakienda kwenye UMITASHUMTA, jezi wakutane nazo tangu wakiwa shuleni. Kwa sababu kwa sasa kila Mbunge anatumia fedha zake nyingi za mfukoni kuagiza vifaa vya michezo China ili aende aka- support michezo jimboni kwake. Tuliomba Serikali ihangaike. Kama tuna wakala wa mbegu kama tuna kampuni za ranchi za taifa kama tuna kampuni za ndege, kwanini tusiwe na wakala wa vifaa vya michezo shuleni ambaye atasimamiwa na Serikali? Na hivyo vifaa vitakuwa vimepunguzwa ruzuku au imeondolewa kodi ili sisi Wabunge iwe ahueni kwetu na watoto wetu waweze kupata vifaa vya michezo vingi na vya kutosheleza na hatimaye michezo ya nchi hii iweze kukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi sina mambo mengi sana, na niwaombe watanzania kwa haya aliyoyasema Mheshimiwa Waziri tuunge mkono bajeti. Hatuwezi kujenga nchi kwa kufurahia tu kodi kupunguzwa, tufurahie kujenga nchi yetu pia kwa kulipa kodi kwa wakati na kodi ambayo inastahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi niwaombe Watanzania kokote waliko yeyote anayekushauri uilalamikie bajeti hii anakupotosha, kwa sababu nchi itajengwa na wenye moyo na wenye moyo ni Watanzania wote. Kwa hiyo mimi niombe tumuunge mkono Mheshimiwa Waziri, tuiunge mkono bajeti ya Serikali na tumuunge mkono Mheshimiwa Rais wetu. Ameonesha njia na ameshirikisha mawazo ya Wabunge walio wengi. Wakati ni wa kwetu sisi Wabunge, tukitoka hapa twende majimbo ili tukai-support bajeti hii asilimia 100.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa lugha za vijana mjini Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mama Samia wameupiga mwingi sana. Kwa sababu gani, leo hii hakuna bodaboda anapiga kelele kuhusu mambo ya bodaboda., hata traffic wenyewe wataacha kusumbua. Shilingi elfu 10 ni reasonable, kwa sababu kama basi lilikuwa linapakia watu 30, lilikuwa inapakia watu 60 analipa 30,000, boda boda anapakia mtu mmoja analipa 30,000, ile imetuonyesha kabisa sisi ni watu wa aina gani. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri you are the really game changer na kwa hili Mungu akubariki sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sina mambo mengi, ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Nishati. Kwanza nipende kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Mama yetu mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri ambayo ameifanya hadi leo mafuta yamepungua bei. Watanzania wafahamu mafuta si kama yamepungua bei, yameshushwa bei na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo tunampongeza sana Mheshimiwa Rais. Pia niwapongeze wataalam wa Wizara na nampongeza Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa smart kwa sababu hata kutuletea REA na TANESCO ndani ya Bunge ni kuonyesha jinsi gani ambavyo anatamani matatizo ya Wabunge yaweze kutatuliwa papo kwa papo, tunampongeza sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo ya kuchangia kwenye vipaumbele vyako 12 ambavyo tunavyo hapa, ninaweza nikaanza na kipaumbele Namba Moja, Namba Mbili na Namba 12 ndivyo nitakavyovizungumzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipengele Namba Mbili, Mheshimiwa Waziri umezungumzia kuhusu kutekeleza miradi ya nishati vijijini pamoja na kuanza utaratibu wa kupeleka umeme katika vitongoji vyote nchini. Mheshimiwa Waziri nizungumze wazi, utekelezaji wa REA kwenye sehemu kubwa ya Majimbo kipindi cha nyuma haukuwa mzuri sana. At least Makandarasi wa sasa japokuwa nao wapo wanaosuasua ila kwa Jimbo la Makete Mkandarasi wa sasa anaunafuu, lakini wale waliopita wana changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunalitekeleza hili, kabla hatujaenda kwenye kuangalia vitongoji, tufanye sensa ni Watanzania wangapi wamesuka nyumba kwenye Taifa hili na hawajaingiziwa umeme hadi sasa. Kwa sababu gani, umeme huu umeishia sehemu kubwa kwenye vituo vya afya na maeneo mengine. Watanzania wengi wamejitoa kwa moyo kusuka umeme toka mwaka 2019, 2018, 2020 lakini hadi sasa hawajaingiziwa umeme. Hao wangepewa special task kuangalia jinsi gani tunaweza tukawasaidia, wakaweza kupata umeme kwenye Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwa ni maswali tukienda Wabunge kwenye mikutano wanauliza, mimi nimesuka Mheshimiwa Mbunge umeme utafika lini? Mimi nimesuka umeme utafika lini? Tunaomba sana mfanye sensa kwa Mameneja wetu wa Mikoa watuambie. Kwa mimi Makete tu nina kijiji cha Mago, na kijiji kama cha kule Matamba na vijiji kama vya Lupalilo, hivi vyote vinawakazi takribani zaidi ya 2,000 hadi 3,000 wamesuka umeme lakini hawajaingiziwa. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri kwenye jambo kama hilo uweze kutusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Makete tunalo Bwawa la Umeme la Mto Lumakalya. Ninyi mnaita Lumakalya lakini sisi ni Mto Luvanyila. Hili Bwawa la Mto Lumakalya ni bwawa ambalo linaenda kuzalisha zaidi ya megawati 222. Lakini pili tuna bwawa la Mto Luhuji, zaidi ya megawati 300, kwa maana kwamba megawati karibu nusu zinazotumika kwenye Taifa hili zinaweza zikaenda kuzalishwa ndani ya Mkoa wa Njombe. Ninakuomba Mheshimiwa Waziri, nimeona kwenye bajeti umenitengea Bilioni Nane, imani yangu ni kwamba hii Bilioni Nane ni kishika uchumba tu kwa sababu mradi una zaidi ya Bilioni 787 thamani yake. Kwa hiyo, ninaamini hii Bilioni Nane ni ya kuanzia tu. Nikuombe, wananchi wetu wamekuwa stranded kwa muda mrefu hawajui mradi unaanza lini. Pili tathmini ya gharama ambazo wananchi wanazunguka bwawa lile la Mto Lumakalya inafanyika lini ili wananchi wetu waweze kupewa fidia na waweze kupata fedha ambazo zitatokana na fidia za maeneo yale. Ninaomba sana huu mradi uweze kuanza, utakuwa umeandika Mheshimiwa January Makamba. Ninakuomba sana sana sana. Hii miradi miwili ikisimama inaweza kutusaidia sana katika kuondoa gap la umeme kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ninalotaka kulizungumzia Mheshimiwa Waziri ni kwenye Mikoa na maeneo kadhaa ambayo Serikali inatumia fedha nyingi kununua umeme na kuwapa umeme na wengine hawatumii umeme. Tunatumia fedha nyingi za Serikali kuhakikisha kwamba wanapata umeme. Kwa mfano, nizungumzie, tuna Mkoa kama wa Kigoma Mheshimiwa Waziri. Mkoa wa Kigoma wanatumia kwa mwezi 1.4 Bilioni kununua mafuta kwa ajili ya kuendeshea Mkoa ule umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba gridi ya Taifa iweze kwenda Kigoma. Wakati Serikali inatumia Bilioni 1.4 kununua mafuta, return yake ni chini ya Milioni 800. Kwa hiyo, tunatengeneza hasara zaidi ya Milioni 700 kila mwezi kwenye Taifa hili kwa ajili ya Mkoa wa Kigoma. Ni lazima uangaliwe kwa jicho la karibu Mkoa wa Kigoma ili tuondokane na hii debt ambayo tunaitengeneza kila siku ya kupoteza Milioni 800. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nenda Mkoa wa Kagera mimi nilikuwa Kagera juzi. Mkoa wa Kagera tunanunua umeme kutoka Uganda, megawati 10 tunanunua kutoka Uganda. Lakini megawati tano zinatumika na kiwanda cha Kagera Sugar. Megawati tano ndiyo zinatumika na Mkoa wa Kagera. Tunatumia zaidi ya Bilioni Moja na Milioni Mia Mbili kwa mwezi kununua umeme kutoka Uganda. Miundombinu ile siyo ya kwetu, ni miundombinu ya kutoka Uganda. Wakati huo huo pale tuna uwezo wa kutoa umeme Nyakanazi na tukapeleka Kagera na watu wa Kagera wakawa wameondokana na tatizo la umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hilo tu, Kiwanda cha Kagera Sugar wanao uwezo wa kuzalisha zaidi ya megawati 25 na waka-supply kwenye Mkoa wa Kagera. Tunaomba sana Mheshimiwa Waziri zungumza na watu wa Kagera Sugar waweze kukusaidia jinsi gani ya kutatua na uzuri mitambo wanayo, wanachokwama ni sheria za nchi zinawazuia kuwauzia umeme watu wa gridi ya Taifa, lakini hapo anao uwezo wa kukupa megawati 20 na ukatatua tatizo la kununua umeme Uganda ambapo tunapoteza over 1.4 billion, 1.2 billion kununua umeme. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Mkoa wa Katavi tunanunua umeme kutoka Zambia. Tunatumia over 1.5 billion kununua umeme kutoka Zambia, lakini watu wa Katavi na Sumbawanga wanao uwezo wa kupata gridi ya Taifa ili tukaondokana na fedha hizi nyingi ambazo tunatumia kununua umeme kutoka nje. Ninakuomba Mheshimiwa January Makamba, imekuwa ni muda mrefu Mikoa hii wanahangaika na umeme, tunaomba utusaidie, Watanzania hawa wapate umeme wa ndani na hizi fedha ambazo tunapeleka kwenye Mataifa mengine tuweze kutatua changamoto za Watanzania ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha Mheshimiwa Waziri, nenda pale kwenye mgodi wa Geita Gold Mining. Geita Gold Mining wanatumia mafuta, hawatumii gridi ya Taifa na sijajua ni mchezo gani unaendelea. Kwa sababu wanapata exemption kwenye mafuta, wanaingiza mafuta hawataki kuingiza gridi ya Taifa kwenye mgodi wao. Ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri…. (Makofi)

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MWENYEKITI: Taarifa.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, aah ananikata upepo huyo…

T A A R I F A

MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza natambua mchango mzuri wa Mheshimiwa Sanga, lakini Geita tayari kuna substation ambayo imekamilika ina megawati 98 ina mwaka mzima na laini ya umeme ilishaingia mpaka mgodini lakini hawajaanza kutumia umeme kwa kisingizio kwamba umeme ule hauko stable. Kwa hiyo, ni muda muafaka Mheshimiwa Waziri kuwasimamia wa-stabilize umeme kuokoa gharama ambazo wanazitumia kwenye mafuta ya diesel.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Festo Sanga unapokea hiyo taarifa?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napokea taarifa yake na ndiko nilikokuwa naelekea, kwamba Mheshimiwa Waziri watu wa Geita Gold Mining ule mgodi unatumia mafuta. Mafuta ambayo wanayatumia ndani ya mwezi wanatumia mafuta ya Bilioni 3.3 ambayo yana exemption ambayo kodi hiyo ingeweza kuingia Tanzania na ingetusaidia Serikali yetu, kwa siku wanatumia zaidi ya megawati tano hadi 10 kwenye mgodi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale tumetengeneza substation. Substation tuliyoitengeneza ipo kwenye Kijiji cha Mpumbwi kama sikosei, Kijiji cha Mpumbwi ni kilomita sita tu kuelekea mgodini, umeme uingie ili hawa Geita Gold walipe fedha hizi. Megawati tano kwa siku ni fedha nyingi, lakini inaonekana kuna mchezo hapo unaendelea wa uchelewashi wa wale kuingiziwa umeme, na Shirika letu la TANESCO linazidi kukosa mapato kutoka kwenye mgodi wa Geita Gold kwa sababu hawataki kutumia, wameona mlango na dirisha kwenye mafuta, kwenye exemption hawataki kuja kuingia kwenye gridi ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ninakuomba Kaka yangu January Makamba, tuna imani na wewe vijana, wana CCM tuna imani na wewe, Bunge lina imani na wewe, unaenda kuwa ni game changer, issue ni moja kwamba una long strategic plan ambazo wengi hawawezi kukuelewa, lakini ninakusihi kwenye haya maeneo ambayo nimeyazungumza, nenda katatue matatizo ya Watanzania. Suala la umeme kwenye Geita Gold lianze kufanya kazi. Hii exemption ya mafuta tupate fedha hii, hii ni fedha Gold Mining hapa kuna kitu wanakicheza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba nishukuru na niunge mkono hoja na nikutakie kila la kheri, ninaamini hii ni moja kati ya bajeti super na Kaka yangu nakutakia kila la kheri. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Wizara ya Michezo. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri inayoonesha mwelekeo mzuri kwenye sekta yetu ya michezo hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa, niweze kuwapongeza Serengeti Girls kwa mafanikio makubwa ambayo wameyapata jana. Nimpongeze sana paka mweusi Bakari Shime pamoja na Edna Lyimo, kocha msaidizi, kwa kazi nzuri ambayo mmeifanya. Kwa sababu ni muda mrefu hizi timu zimeandaliwa lakini leo Mungu ameamua kutupa nafasi ya kwenda kushiriki Kombe la Dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba nichangie kwenye mambo kama matatu hivi, jambo la kwanza ni suala la mfumo wa mchezo nchini kwetu na suala la maendeleo ya viwanja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, jambo la kwanza ambalo ninajisifia kwamba Wizara imepata mwanamichezo hilo ni la kwanza. Wakati mimi nahangaika na Singida United wewe ulikuwa ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Nidhamu, Haki na Hadhi za Wachezaji TFF, changamoto za wachezaji, changamoto za mpira, vyote unavifahamu. Kwa hiyo, ninafurahi kwamba tunakwenda kufanya kazi na mtu ambaye hii ni sehemu yake na ninafurahia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, mpira wetu una safari. Safari ndefu inaanzia kwenye mfumo wa soka letu la Tanzania, nitajikita sana kwenye soka. Mfumo wetu wa mpira wa Tanzania ambao tunaenda nao ni mfumo ambao wakati mwingine ni kama wa zimamoto, kwa sababu tunatamani sana tuwe na matokeo mazuri lakini hatujatengeneza grassroots nzuri za kuzalisha wachezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Taifa hili leo tunaona Serengeti Girls wanakwenda huko, lakini mfumo wetu je, unawaandaa wengine kama hawa? Unakuta hauwaandai. Tunao majirani zetu ambao ni Watanzania wenzetu, Zanzibar. Zanzibar ndiyo watu ambao wana the best model ya mpira Afrika na Afrika Mashariki. Zanzibar wamechukuliwa model yao ya soccer development imekwenda kuwa applied Cameroon, Ghana na nchi nyingi, model ya soccer la Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, kwa nini nazungumzia soccer. Katika Taifa lolote lile duniani lazima nchi ijipambanue nini inataka kwenda nacho. Leo nikiitaja Marekani ninataja basketball, nikiitaja Brazili ninataja samba, soccer, nikizungumzia Afrika Mashariki nikiitaja Kenya ninaitaja riadha. Leo nikiitaja Burudi ninataja makocha. Makocha wa timu zetu za Ligi Kuu karibu zote ni Warundi. Wenzetu waliamua wawekeze kwenye makocha. Nikiizungumzia Rwanda ninazungumzia basketball. Leo hii ndiyo wana-host basketball kwenye Afrika nzima. Sisi Tanzania tunajiangalia wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, tuna kitu cha kufanya kwa ajili ya Taifa letu. Sheria Na. 1 ya FIFA inazungumzia Taifa lolote lazima liwe na viwanja ndipo mpira uchezeke. Taifa letu kwenye suala la viwanja bado umekuwa ni mgogoro. Siku ile niliongea, mwaka jana, nikaomba hapa kwenye bajeti kwamba Mheshimiwa Rais atuondolee kodi kwenye nyasi bandia, akaondoa. Wakati ambao Taifa letu limepata political will ya Rais ni kipindi hiki. (Makofi)

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

NAIBU SPIKA: Taarifa.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Mchangiaji ameongelea viwanja. Hapa Dodoma tuna uwanja wa kawaida sana, Uwanja wa Jamhuri, lakini ninapoongea hapa muda mwingi uwanja unatumika kwa maonesho na kufungiwa. Kwa hiyo, hata viwanja tulivyonavyo havitumiki kwa matumizi stahiki. (Makofi)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na ninapokea mchango wa Dada yangu ni mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, suala la viwanja limekuwa ni changamoto. I ask myself, was it the intention ya Mwalimu Nyerere kujenga viwanja nchi nzima, leo vigeuke magofu, vigeuke sehemu ambazo hazitumiki kwa ajili ya kuchezea, vimegeuka mazizi ya ng’ombe viwanja hivi, was that the intention of Mwalimu Julius Kambarage Nyerere? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Chama changu kina kazi ya kufanya. Nyerere alijenga viwanja kwa ajili ya michezo. Political will aliyonayo Mheshimiwa Samia kwa sasa kwenye michezo hadi akasema Mwanza kwamba nakielekeza Chama changu cha Mapinduzi kiweke nyasi bandia kwenye viwanja hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma kwenye ukurasa wako wa 62, unasema tunatenga bilioni 10. Bilioni 10 unatenga kwa ajili ya ukarabati, hatua ya kwanza, hatua ya pili kwa ajili ya ukarabati, hatua ya tatu kuweka nyasi bandia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, nikuombe Ligi Kuu ya Tanzania haihitaji ukarabati viwanja, inahitaji kuwekwa nyasi bandia. Mwalimu Nyerere alitujengea viwanja akiwa na Watanzania milioni 20 tu, leo tupo milioni 64 tunashindwa kuweka nyasi bandia kwenye Taifa hili? Mheshimiwa Waziri, nikuombe, hizo Bilioni 10 fanya kazi ya kuweka nyasi bandia kwenye viwanja vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2027 tunakwenda ku-host AFCON, tuta-host vipi AFCON kwa nyasi hizi? Kwa sababu hawa watu ambao tunakwenda ku-host AFCON wataenda kuangalia viwanja vyetu miundombinu yake ikoje. Nikwambie mbinu ambayo wametumia Zambia, waliamua CSR kwenye migodi ndiyo itumike kuweka nyasi bandia kwenye viwanja vya Zambia. Tanzania tunayo makampuni mangapi nchi hii yanayochimba madini? Tuna makampuni mangapi nchi hii yanayowinda wanyama wetu? Tuna makampuni mangapi nchi hii wanatengeneza bidhaa zao na wanauza? CSR ingetumika kuweka nyasi bandia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, you’ll be the game changer. Nikuombe Kaka yangu, viwanja, viwanja viwanja. Viwekwe nyasi bandia. Hiyo Bilioni 10 ninajua huna, unakwenda kumuomba Mama. Nitumie nafasi hii kumuomba Mheshimiwa Rais, Bilioni 10, achukue hata – kuna hizi fedha huwa mnarudisha mnaziita gawio – achukue hata gawio la Vodacom au Tigo au kampuni yoyote aweke kwenye viwanja, hapo tutakuwa tumemaliza tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, umezungumza hapa kwamba unakwenda kutengeneza ajira za vijana karibia 72,000 kupitia mtaa kwa mtaa. Hawa vijana utakwenda kuwapeleka wapi hatuna viwanja, hatuna academy. Mimi ninatoka Makete na hata hizi shule 56 za academy unakwenda kujenga, my suggestion is jenga kwa zones. For instance, kuna timu za Taifa zinakwenda kucheza maeneo ya baridi. Sisi tuna maeneo ya baridi ambayo ni Njombe, Makete na Mbeya, ungeweza kwenda kujenga kule shule moja kwa ajili ya kuwekea camp ili wanapokwenda kwenye mechi huko wakatumia hapa nchini. Kuliko hela za kambi, hela nyingi, tunakwenda kutumia nje wakati tungeweza kuja kuweka maeneo haya. Hizi 56 ni nyingi, hata chache tu anza nazo kwa sababu safari ni hatua. Ninakuomba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, wewe ulikuwa TFF, unajua wachezaji wetu walivyo na changamoto ya maslahi, it’s the time now. It’s high time now kwenye Taifa letu, lazima tuweke salary scale, lazima mishahara ya wachezaji wetu wa Ligi Kuu, wachezaji wetu wa Ligi Daraja la Kwanza, wachezaji wetu wa Timu za Taifa wawekewe kiwango cha mishahara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, vijana wetu wanacheza kwa jasho na damu, wanalipwa laki mbili kwenye ligi kuu, wanalipwa laki tatu. Hawa vijana wanapata magonjwa wanalazwa mahospitalini tunaanza kuchangishana, lazima tuweke salary scale ya kwamba mchezaji wa ligi kuu lazima alipwe Milioni Moja minimum. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna fedha nyingi sana kwenye mpira zinapotea, tungewasaidia vijana hawa ambao leo hii hapa kila mtu anawapigia makofi wakiwa wamekaa pale juu, lakini do you know how much they get, wanapata shilingi ngapi? Inawezekana hata laki mbili mfukoni hawana leo. Lazima kama Taifa tufanye mabadiliko ya sera zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, umeweka Mpango Mkakati wa Maendeleo ya Soka 2022 - 2032 miaka kumi hapa, moja ya vitu ambavyo unatakiwa uingize ni maslahi ya wachezaji wetu. Tutamshambulia Ndugu Karia lakini Ndugu Karia is the best president, amefanya kazi vizuri, anafanya kazi vizuri ndiyo maana leo wote tunajivunia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, ninakuomba fanya mabadiliko…

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Sanga, kengele ya pili.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, wewe ni mwanamichezo, tuendelee kum-support ndugu yangu na Kaka yangu, all the best. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupewa nafasi niweze kuchangia kwenye Mpango wa Serikali. Kwanza ninaipongeza Serikali, kwa mapendekezo waliyonayo kwenda kwenye bajeti ijayo ya trilioni 47 na katika hizo shilingi trilioni 47 Serikali imetoka kwenye trilioni 14 za maendeleo kwa sasa imeenda kutenga trilioni 15 kwa ajili ya maendeleo. Kwa hiyo niipongeze Serikali kwamba inaenda kuongeza zaidi ya shilingi trilioni moja kwenye utekelezaji wa miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inaonesha kabisa dhamira ya Mheshimiwa Rais ipo wazi kwenye kuhakikisha kwamba miradi ya maendeleo haisimami kwenye nchi yetu na inaweza kutekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite kwenye suala la financing ya Mpango wenyewe, kwenye Kamati wamezungumzia hata Serikali imezungumzia kwenye financing ya mpango wenyewe. Tuna Mpango mzuri sana lakini ku-finance Mpango wenyewe inatakiwa tufanye nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi najikita kwenye mambo matatu. Nitajikita kwenye kodi, mifumo lakini nitazungumzia suala la utalii kwa maana ya Sekta ya Utalii. Ukisoma kwenye Mpango, Mheshimiwa Waziri anazungumza kwamba moja kati ya changamoto ya Serikali ya ukusanyaji wa mapato ni wigo mdogo wa vyanzo vya mapato. Ukienda kwenye mifumo mingi ya Serikali na ambayo tunategemea ndiyo source ya ukusanyaji wa mapato, kumekuwa na changamoto kubwa ya mifumo kusuasua, lakini pili kumekuwa na changamoto kubwa ya mifumo kutokusomana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu inakusanya mapato lakini mapato yanayokusanywa ni theluthi ndogo tu kuliko mapato mengi zaidi ambayo yangekusanywa kwa ajili ya ku-finance mipango na miradi yetu ya maendeleo. Changamoto hii naweza nikatolea mfano, kwenye mfumo mmoja tu ambao umefungwa kwenye Daraja la Kigamboni, Daraja la Kigamboni wamefunga mfumo wa ukusanyaji wa mapato, kabla ya ukusanyaji wa mapato kupitia mfumo, daraja la Kigamboni lilikuwa linaingiza Shilingi milioni 150, 200 hadi 300, baada ya kuweka mfumo Daraja la Kigamboni la Mwalimu Nyerere pale linaingiza Shilingi bilioni moja na milionii 300 kwa mwezi. Hii inamaanisha nini? Watu wengi wanakwepa mifumo Serikalini kwa sababu inawabana na wizi ambao wanaufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakupa mfano mwingine, hospitali ya Kibaha pale Tumbi. Kabla haijafunga mfumo kwa mwezi walikuwa wanaingiza shilingi milioni 13, 12, baada ya Serikali kwenda kufunga mfumo wanaingiza shilingi milioni 350, 400 kwa mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inatafsiri ya magnitude kubwa iliyopo kati ya wizi na ukwepaji wa kwenye mifumo. Ukienda kwenye Wizara ya Ardhi, hapa tukiondoka tukienda pale TAMISEMI au kwenye Wizara ya Ardhi hapo, mfumo sasa hivi utakuta upo chini. Ukienda kwenye afya hospitalini kuna wagonjwa inawezekana wanatusikiliza sasa hivi wapo kwenye foleni mfumo upo chini. Ukienda TRA mifumo ipo chini, lakini hatujawahi kuona hata siku moja mfumo wa ulipaji mishahara ukiwa chini hata siku moja kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inatupa alarm kwamba siyo kwamba mifumo ina changamoto, changamoto ipo na watu wanaoitumia hiyo mifumo, kwa sababu wanatumia mifumo hiyo kama njia ya wizi. Ndiyo maana CAG anasema wana uwezo wa kuzima POS kwa siku elfu moja na Serikali isifanye kitu! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi mapendekezo yangu kwa Serikali, tuiiombe ione dhamira ya wazi kwanza ya kufanya mifumo isomane, kilio cha Mheshimiwa Rais kwa muda mrefu ilikuwa ni hicho, hasa hasa pale bandarini na maeneo mengine. Pili, kuhakikisha mifumo hii inafanyakazi, kwa sababu tunaweza tukafunga mifumo lakini isifanye kazi. Hilo ni pendekezo langu kwenye suala la mifumo, nikiiomba Serikali, hatuna sababu ya kuruhusu watu waendelee kukutana face to face, kukutana kwa watu face to face kwenye suala la payment kunasababisha majadiliano na rushwa, Serikali inaenda kupoteza fedha nyingi kwa sababu watu wanajadiliana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tukifunga mifumo kwenye maeneo mengi kutatusaidia sana kwenye kusimamia fedha na kukusanya mapato mengi ili Mheshimiwa Mwigulu na Mheshimiwa Waziri wa uwekezaji tuweze…

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Festo Sanga, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kingu.

TAARIFA

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mchangiaji Kaka yangu Festo, Mbunge makini kabisa. Hospitali ya Taifa ya Bugando kabla ya kufungiwa mifumo ilikuwa inakusanya shilingi milioni 800 baada ya kufungiwa mfumo wanakusanya shilingi bilioni 3.5. Mifumo hii imefungwa na kampuni ya vijana wa Kitanzania wazalendo, Mheshimiwa Ummy Waziri wa Afya ni shahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya KCMC kabla ya kufungiwa mifumo ilikuwa inakusanya only shilingi milioni 300, 400 na baada ya kufungiwa mfumo wanakusanya mpaka 1.5 billion. Hospitali ya Amana ya Serikali, haya nayasema Mheshimiwa Waziri wa Afya yupo hapa kama nasema uwongo atasimama kunikanusha. Kabla ya mifumo walikuwa wanakusanya milioni tisa, leo tunazungumza baada ya kufungiwa mifumo tena mifumo imebuniwa na vijana wazalendo wa Kitanzania, wapo hapa lakini bado kigugumizi pia cha kuwatumia vijana hawa ni kikubwa. Kwa hiyo, nakubaliana na Mheshimiwa Festo, kwamba watu wanakataa mifumo kwa sababu ya corruption na wizi wa fedha za Serikali. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Festo Sanga, taarifa hiyo unaipokea?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea taarifa hii kwa sababu ninatambua anachokizungumza ni sawasawa na kile ambacho nilikuwa nakizungumza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii ukienda Morogoro kituo cha mabasi wana zaidi ya miaka mitatu wanahangaika kuvutana kwenye Baraza la Madiwani jinsi ya kufunga mfumo, kwa sababu pale junction ya mabasi mengi lakini watu hawataki, wanataka waendelee kutumia cash, fedha mbichi kuliko kutumia mifumo. Kwa hiyo ni kweli Serikali inachangamoto ya ufungaji wa mifumo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la ulipaji wa kodi. Serikali, kwanza lazima tutambue wafanya biashara nchini ni sekta binafsi, Serikali haifanyi biashara. Kama mtu anafanya sekta binafsi, kuna siku anaweza akaamua aamke aende ofisini au asiamke kwenda ofisini. Kwa hiyo, unapoenda kudai kodi lazima tuwe na lugha ya customer care, lugha nzuri, lugha yenye kumshawishi mtu alipe kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwigulu, kwenye kitabu chake cha bajeti anasema; “Mheshimiwa Spika, katika kutatua kero hizo napendekeza kuanza matumizi ya mfumo wa pamoja wa ukusanyaji wa ada, tozo na adhabu za taasisi, udhibiti, ‘single window payment system na taasisi za udhibiti kuweka utaratibu mzuri wa ukaguzi ambao hautasababisha usumbufu kwa wafanyabiashara bila kuathiri majukumu ya msingi ya taasisi hizo napendekeza hatua hizo zianze kufanyika mwaka 2023/2024”. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sisi ambao Mheshimiwa Mwigulu, tunakufahamu hili limekuwa ni moja kati ya maono yako ya muda mrefu. Leo Mheshimiwa Mwigulu, ukienda kwa mfanyabiashara, watu wa leseni asubuhi wameingia dukani, watu wa OSHA asubuhi wameingia dukani, watu wa fire asubuhi wameingia dukani, watu wa TRA asubuhi wameingia dukani, watu wa service levy asubuhi wameingia dukani! Hatuwezi kuwa na Taifa la walipa kodi wa aina hiyo ambao wanafanya kazi ya kupokea wataalam wa Serikali kila asubuhi kuliko kupokea wateja wanaokuja kununua bidhaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango ya Serikali lazima iwe ni jinsi gani ya kuisaidia sekta binafsi ya wafanyabiashara ifanye biashara katika mazingira mazuri. Kuliko hiki cha kuruhusu asubuhi watu wanaacha kazi maofisini wanapanga foleni kwenye maduka ya watu, kiasi kwamba kuna Watanzania wengi wamekufa mioyo kufungua maduka kwa sababu ya mifumo hii ya ufanyaji biashara. Ndiyo maana mataifa yanayotuzunguka Zambia, wameweka mazingira mazuri, watu wanakimbilia Zambia. Mheshimiwa Waziri wa Fedha, ili upate kodi kwa Watanzania tengeneza kwanza wafanya biashara wawe marafiki wa TRA, fanya reformation kule TRA, reform TRA yote jinsi gani inavyo-operate na wafanya biashara. Tatu, kwa nini leo mfanyabiashara ukienda kununua mzigo anakwambia mimi nakukatia risiti ya shilingi milioni moja, huu mzigo wa Shilingi milioni 10 sitaki kukukatia risiti ya shilingi milioni 10, kwa nini wanakwepa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuende far kwa wataalam wetu kufikiria kwanini wafanya biashara hawopo tayari kukatia risiti ya milioni 10, wapo tayari kudanganya watoe risiti ya milioni moja. Wafanyabiashara lazima wataalam wetu wawaze mbali ili kuweza kukusanya hizo fedha za ku-finance huu mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika zangu zisije zikaisha niende kwenye Sekta ya Utalii. Mheshimiwa Rais, juzi alizungumza kuhusu utalii. Kwanza ni support kwamba utalii wetu unaongezeka, unakua kutokana na jinsi ambavyo Mheshimiwa Rais, aliondoa mguu wake ofisini na akaenda site kwenda kutengeneza The Royal Tour, ambayo leo kila mmoja na Wizara inajinasibu kwamba utalii umekua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu linabaki kwenye sekta hii, utalii kwa asilimia 90 inafanya kazi sekta binafsi. Mtalii akishuka Airport anakutana na dereva, mtalii akienda site kwa maana kwenye hifadhi atakutana na dereva na tour guides. Leo hii wizara inampango gani wa kukutana na drivers, kukutana na tour guides kukutana na hao wote ambao ni mnyororo wa thamani kwenye utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtalii anayetoka nje akija Tanzania ana uwezo wa kutumia masaa arobaini, katika masaa arobaini, masaa thelathini anakuwa kati ya yeye na dereva au na tour guides. Tour guides tumewapa level gani ya ubalozi wa kuelimisha kuhusu utalii? Kumekuwa na changamoto kubwa sana kwenye sekta hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeomba dakika mbili nimalizie. Ukija kwenye suala lingine, Mheshimiwa Rais amezungumza, Serikali inatakiwa iwe na mpango, kuna changamoto ya malazi kwenye sekta yetu ya utalii, malazi imekuwa ni changamoto ya watu kwa kulala. Ukienda Serikali ilishawahi kuwa na lodge na hoteli 23, leo hii nataka nikuambie katika mchakato ambao Serikali inaufanya, hoteli hizo zimekufa, hoteli hizo hazifanyi kazi. Nakupa tu mfano mmoja hapa nazungumza. Mfano katikati ya Jiji la Dar es Salaam, premium area kuna hoteli inaitwa Embassy Hotel, kwa muda wa miaka 14 haieleweki ni ya Serikali, haieleweki ni ya uwekezaji, lakini Taifa letu linachangamoto kubwa ya kutokuwa na hoteli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoteli ya Ngorongoro, kuna hoteli ya Seronera Wildlife, Lobo Wildlife, TRA wanasema hawajui hizi hoteli zinamilikiwa na nani. Mheshimiwa Rais, anazungumza kwamba Taifa letu lina changamoto ya maeneo ya malazi, lakini hoteli hizi ni za Serikali zipo kwenye potential area, kuna haja ya Serikali kuwa na mpango mahsusi kuufanya utalii ukue, kuufanya utalii uonekane. Tunazungukwa na Rwanda na Mataifa mengine yanafanya vizuri, hata juzi tulijiuliza tupo kwenye kufungua michuano ya kimataifa ndani la Taifa letu ambalo tunajinasibu kutangaza utalii lakini tunatangaza visit nchi nyingine wakati sisi tulikuwa na uwezo wa kufanya matukio makubwa kwa ajili ya Taifa hili. Ahsante. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Katiba na Sheria kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli zake kwa Mwaka 2021
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nimpongeze sana Mwenyekiti kwa wasilisho lake zuri, lakini pia niipongeze Serikali kwa maana ya Mawaziri kwa kazi nzuri wanayoifanya, hasa hasa Waziri wa TAMISEMI kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo machache ya kuchangia ambayo yamejikita kwanza kwenye upungufu wa wafanyakazi. Kwanza tuipongeze Serikali kwa kazi kubwa ambayo imeifanya ya kujenga vituo vya afya lakini pia kuongeza ujenzi wa madarasa katika sehemu mbalimbali za nchi hii. Hata hivyo, changamoto kubwa ambayo tumekuwa nayo ambayo tunaipata hadi sasa hivi ni wimbi kubwa la vijana kukosa ajira ambapo mimi kama Mbunge ningependa kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na watu wengi kustaafu, lakini pili kumekuwa na wenzetu ambao wanafariki na kutangulia mbele ya haki. Hawa wote tungetamani nafasi zao ziwe zinajazwa kwa wakati, kwa sababu wanakuwa wako kwenye payroll ya Serikali. Hii ingeweza kusaidia kuendelea kupunguza gaps lililopo la watumishi kwenye nchi yetu ambalo limekuwa ni kubwa. Kuna watu ambao wamemaliza toka miaka 2012, 2013, 2014 hawajaajiriwa hadi wanakuwa wazee, wamekosa ajira. Kwa hiyo, tungeiomba Serikali na ningeishauri Serikali ijitahidi kutoa vibali mapema kwa hizi gaps ambazo zinakuwa zipo za watu ambao wamestaafu na wangine wametangulia mbele ya haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo lingine, ni kwenye suala la fedha za miradi. Kwanza tuipongeze sana Serikali, mama yetu anaupiga mwingi sana. Mama Samia anaupiga mwingi sana kwenye ujenzi wa miradi kwenye nchi hii. Unaweza ukaangalia kwa asilimia 100 kama siyo 90 na kitu halmashauri zote nchini zimepata fedha za maendeleo za bajeti ambazo walikuwa wameomba, ni kitu ambacho hakijawahi kutokea kwa miaka mingi toka tumepata uhuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto ambayo tunaipata, kwenye uwiano wa kugawa fedha hizi. Watu walioko Makete, Kiteto, Nyamagana kule Mwanza, Musoma, Mbinga na watu waliopo maeneo mbalimbali anapewa milioni 20 ajenge darasa, wakati huo huo hiyo milioni 20 anapewa mtu aliyopo Dar es Salaam ajenge darasa. Halafu tunategemea hawa watu wote wawe na darasa sawa la Dar es Salaam na la Makete kule Ipepo, na la Makete kule Matamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto inayokuja kujitokeza, watu waliopo kule mikoa ya mbali kama Kigoma, Makete Wilayani wanahangaika kuhakikisha wana-meet kile kiwango ambacho Serikali imetaka darasa likamilike, lakini si kwa zile fedha ambazo muda mwingine zimetolewa na Serikali, wanakwenda kuingia hadi mifukoni mwao kuhakikisha wanatekeleza lile jambo ambalo Serikali inataka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tungetumia mfumo ambao EWURA wanavyofanya kwenye kugawa mafuta. Bei ya mafuta Dar es Salaam ni tofauti na bei ya mafuta iliyoko Mwanza. Ndivyo ambavyo tunatakiwa tufanye hivyo hata kwenye miradi hii ya Serikali, angalau tungetambua kwamba Zone hii ya Mwanza au Lake Zone au Zone ya Mbeya, ujenzi wa madarasa siyo milioni 20 kwa darasa moja, ni milioni 25. Wangefanya hivi ingeweza kusaidia kwa watumishi na wafanyakazi wetu waliopo kule chini, kwa sababu wana- suffocate, wanapata wakati mgumu, kuhakikisha kwamba wana-meet kile ambacho Serikali inataka, lakini usawa huu ungeondolewa ili kuweza kuwasaidia ndugu zetu ambao wapo huko wanahangaika na kutekeleza miradi ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ningeomba sana watumishi walizingatie, wanateseka sana Watendaji wa Kata, wanabanana sana na Wakurugenzi kuhakikisha kwamba hii miradi inakamilika kwa uwiano wa kugawa fedha kwenye majimbo yote nchini, wangetenga kwa zone ingetusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu la mwisho, ni kwenye suala la Sekretarieti ya Maadili ya Utumishi wa Umma. Hii Sekretarieti imeanzishwa kwa sheria, ibara ya 132 kwenye Katiba yetu, ndiyo ilianzisha hii Sekretarieti ya Maadili ya Umma. Changamoto ambayo tunaipata kwenye hii Sekretarieti ya Maadili ya Umma. Tumekuwa na changamoto ya Viongozi wengi na watumishi wengi wa Serikali kutokuwa na maadili ya umma kama ambavyo tunatoka kwenye sheria, lakini hii Sekretarieti imekuwa kimya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kati ya majukumu yake wanasema, kuna mojawapo wanasema, Sekretarieti ya Maadili ya Umma inasema to conduct investigation into allegations or complex against any public leader. Sasa tumeanza kushangaa kwamba hadi anakwenda Rais anasema hadharani kwamba kiongozi huku amefanya moja, mbili, tatu, nne, tano au hadi watu waweke bango barabarani kwamba kiongozi huyu ana moja, mbili, tatu, nne, tano, lakini hii Sekretarieti ya Maadili ya Umma ilikuwa na kazi hiyo ya kufanya investigation kujua viongozi wapi wanafanya moja, mbili tatu ili achukuliwe hatua za haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kuna vijana ambao wanahangaika mahakamani kwa kesi mbalimbali, lakini kuna mambo yalikuwa wanayafanya hadharani na hii Sekretarieti ilikuwa kimya, lakini leo hao viongozi wanahangaika kwenye hayo mambo.

Kwa hiyo, nasema Serikali ione umuhimu wa kuhakikisha kwamba Sekretarieti ya Maadili ya Watumishi wa Umma inafanya kazi kwelikweli kumsaidia Mheshimiwa Rais kwa Wakurugenzi na wateuliwa wengine wa Rais ambao wamekuwa wakikiuka maadili na tunawaona wapo kimya na hii Sekretarieti ya Maadili ya Umma ipo kimya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ingefanya kazi vizuri, ingewasaidia hata vijana ambao wanakua wajue kuna chombo ambacho kinafanya kazi kabla ya Mheshimiwa Rais kuchukua hatua. Hiki chombo ambacho kiliundwa na Sheria na ni chombo huru, kina uwezo wa kufanya kazi hadharani na watu tukaona tukajua nchi yetu ukikosea hiki unachukuliwa hatua hii, lakini sasa tumeona kwamba kumekuwa na ukimya huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti baada ya kusema hayo nikushukuru sana na naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja za Kamati zilizopo mezani kwetu. Ninataka kuchangia mambo mawili. Jambo la kwanza ni kuhusu Mradi wa SEQUIP na jambo la pili ni Wizara ya Michezo.

Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru kwa ujenzi wa shule za kata ambao umefanywa na Mheshimiwa Rais, karibu kata zote nchini. Kwa kweli sisi kama Wabunge huko majimboni tumepata kitu kikubwa cha kukisema na wananchi ambao walikuwa hawana matumaini kabisa ya kuwa na shule lakini sasa wana shule kupitia huu Mradi wa SEQUIP, na sehemu kubwa hii miradi ya shule Mheshimiwa Rais ametoa fedha na wananchi wametoa nguvu kazi kidogo sana.

Mheshimiwa Spika, lakini, hoja yangu ni nini ambayo napenda kuishauri Serikali; kwenye hii miradi ya SEQUIP ambayo imelenga kwenye kila kata, ukizingumzia kila kata, si kata zote zinahitaji hiyo shule moja. Kuna kata zingine kwenye miji kwenye majiji zinahitaji zaidi ya shule mbili. Sasa tuone haja ya Serikali kuongeza kwenye kata mbali mbali kwa sababu idadi ya wanafunzi imekuwa ni wengi kwenye kata mbali mbali. Kwa hiyo tungeweza kuongeza idadi ya shule kwenye kata hizo ili iweze kuendana na wingi wa wanafunzi ulipo pale.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, kwa sisi kwenye Kamati yetu tumezungukia tumeona kwamba kumekuwa na variation kubwa sana ya ujenzi wa shule hizi. Ukienda kwenye halmashauri mbali mbali kuna halmashauri ambazo zina upungufu wa zaidi ya milioni 51 ili kukaimisha ujenzi wa shule hii, lakini kuna halmashauri zingine zimefika hadi milioni 150 zinahangaika kutafuta hizo fedha ili zikamilishe ujenzi wa shule hii. Hii inatokana na umbali wa shule zilizopo pamoja na upandaji wa gharama za vifaa kwenye ujenzi wa shule hizi. Sasa Serikali ione concern, shule ambayo ipo Namanyere haiwezi kuwa sawa sawa na shule ambayo iliyoko Dar es Salaam kwenye gharama za ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni vyema Serikali ikaona namna gani ya kuweza kuziunga, kuzi-support au kuziongezea nguvu kuliko kuwaachia Wakurugenzi na halmashauri waendelee kuhangaika na ujenzi wa shule hizi ili ziweze kukamilika. Milioni 470 tu haiwezi kutosha, hata mimi kule Makete bado na changamoto ya fedha nyingi ambazo nazihitaji kwa ajili ya ujenzi wa shule hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine ni kwenye suala la Wizara ya Michezo. Nimesikiliza hoja ya Kamati. Kwenye suala la Wizara ya Michezo, mimi kama Mbunge nina hoja ambazo zinazungumzia kwenye suala la ujenzi wa shule zile za michezo lakini pia kwenye suala la viwanja nchini. Kamati imeshauri kwamba Wizara ione utaratibu wa kufanya partnership na sekta binafsi. Mimi ninauliza, leo tunaenda karibu robo ya tatu ya utekelezaji wa bajeti, lakini hadi dakika hii ninanvyozungumza kwenye ujenzi wa viwanja nchini hakuna chochote ambacho tumeanza kukifanya. Watanzania wana swali kubwa sana huko nje, tumekuwa tukipigia kelele kuhusu ubora wa viwanja vya Taifa letu, na Serikali ilikuja hapa ikatuahidi kwamba kutokana na bajeti ya bilioni 10
kwenye viwanja saba ambavyo tumeitengea itaanza mchakato wa ujenzi wa viwanja.

Mheshimiwa Spika, mimi niiambie Serikali, suala la michezo nchini limekuwa ni suala ambalo linaleta fedha nyingi kwenye Pato letu la Taifa. Kwa mwaka 2020/2021 Serikali imeingiza zaidi ya bilioni tatu kupitia mapato ya magetini kwenye mpira wa miguu. Vilevile, Azam (Bakhresa) amewekeza zaidi ya bilioni 225 kwenye kudhamini ligi kuu, na analipa zaidi ya bilioni 34 VAT. Hivi ninavyozungumza, jitihada za Serikali kupitia kwa Mheshimiwa Waziri wa Wizara husika tunaziona, lakini je wamepata fedha zozote za kuanza mchakato huu? Tuliahidiwa kwamba watajenga shule 56 za michezo nchini lakini hadi ninavyozungumza sasa hivi hakuna hata shule moja iliyoanza kujengwa. Uzuri Waziri wa Fedha mwenyewe ni mdau wa michezo nchini. Je, ni kipi kinaichokwamisha Serikali kutoa fedha ili viwanja wa michezo vianze kuboreshwa?

Mheshimiwa Spika, ninavyozungumza sahizi, Azam ambaye anafanya production ya mpira kwenye Taifa letu, uwekaji wa taa kama uwanja wa Jamhuri Dodoma zile taa zimewekwa kwa dola laki tatu, zaidi ya milioni 700. Serikali inashindwaje kumuunga mkono kwa kuweka angalau uwanja ambao unaweza kuchezeka mpira? Anapambana kuweka mazingira mazuri ya soka kama mwekezaji lakini sisi kama Serikali bado tumekuwa tukimkwamisha kwenye suala la kuboresha miundombinu.

Mheshimiwa Spika, niiombe Wizara ya Fedha, Wizara ya Michezo inafanya kazi nzuri sana, ipatieni fedha idara hii ili iweze kuboresha viwanja nchini. Watanzania wanapenda michezo, Watanzania wanapenda soka, lakini kumekuwa na changamoto ya kuboresha miundombinu. Leo ninavyozungumza tuna zaidi ya viwanja sita ambavyo vimefungiwa na TFF mpira usiendee kuchezwa kwa sababu ya ubovu wa viwanja hivyo.

Mheshimiwa Spika, na hii imekuwa ikisababisha gharama kwenye timu kuhamia kwenda eneo lingine kuwaleta wachezaji, kusafirisha timu kwa sababu ya ubovu wa viwanja vya michezo. Nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Mheshimiwa Waziri wa Fedha kama mdau wa michezo, ona umuhimu wa kuisaidia Wizara ya Michezo ili iweze kuboresha miundombinu ya viwanja vyao. Mlituahidi kwamba tutajenga uwanja Dodoma, na hapa ndiyo Makao Makuu ya nchi na Watanzania wanajua kwamba mlituahidi mtajenga uwanja lakini hadi sahizi Wizara ya Michezo haijaanza kujenga; ukifuatilia hawana fedha ambayo wamepata kutoka Serikalini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pili, hizi shule saba ambazo mlisema angalau mtaanza nazo hakuna shule hata moja ambayo imeanzwa kujengwa. Kwa hiyo, niishauri Wizara ya Fedha, ni vyema mkatoa fedha angalau kuweza kui-support Wizara ya Michezo ili angalau Watanzania waone mwanga kwenye kuboresha viwanja vyetu nchini.

Mheshimiwa Spika, mimi baada ya kusema hayo, sina mambo mengine ya ziada lakini ilikuwa ni hoja yangu ya msingi, kwamba kilio cha viwanja nchini kimekua ni kukubwa na ni vyema Serikali ikachukua hatua ili kuunga mkono juhudi za Mheshimiwa Rais lakini pili kumuunga Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Michezo ambaye amekuwa akifanya kazi nzuri sana katika kuhamasisha michezo nchini.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo ahsante sana. (Makofi)
Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Nianze kwanza kwa kuunga hoja mkono. Hoja hii ni hoja mahususi na nadhani matumaini kubwa ya Watanzania yalikuwa ni jinsi gani Bunge litajadili hili jambo na kwa kweli nimefurahishwa kwamba tumepewa nafasi ya kulijadili jambo hili mahususi kwa ajili ya Taifa letu na ni la dharura.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli hali ya wananchi huko nje ni mbaya sana. Leo ninavyozungumza wananchi wangu wa Makete wananunua mafuta kwa bei ya Sh.3,400 mpaka Sh.3,500 na kwenye vidumu wanakaribia karibu Sh.4,600 na kuendelea. Hali ya wananchi wetu ni mbaya na bahati mbaya sana suala la mafuta lina athari nyingi za kimnyororo kwenye maisha ya wananchi. Suala la mafuta sio kama jambo dogo, ni jambo kubwa ambalo linaathiri kuanzia maisha ya mtu wa chini kabisa hadi mtu wa mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali, hata kama tuko kwenye mazungumzo, kwenye vikao tunavyoendelea navyo, hili jambo ni la dharura lazima tulichukue katika udharura wake. Kwenye hizi kodi na tozo ambazo tunazizungumza, bei ya mafuta duniani hadi yanafika Dar es Salaam ni Sh.1,162 kwa lita, lakini msalaba na mnyororo wa kodi zilizoko na tozo zilizoko kwenye mafuta ni zaidi ya shilingi 1,300, yaani bei ya mafuta duniani ni ndogo kuliko mnyororo wa kodi tulizonazo nadhani za nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi niombe Serikali ione umuhimu wa kuzipunguza hizi tozo ambazo hazina umuhimu kwenye maisha ya Watanzania. Kwa sababu hata tukifanya vipi tukasema bei ya mafuta shilingi 1,000 kwa lita lakini kama huu mnyororo hapa wa hizi tozo TBS, TASAC, EWURA... (Makofi)

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Sanga kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Nollo.

T A A R I F A

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, nataka tu nimpe taarifa mzungumzaji badala ya kutumia mifano ya mbali sana kwa nchi zingine, tofauti tuna Zanzibar hapo Zanzibar lita ni Sh.2,600 na huku iko hivyo. Kwa hiyo, tutumie tu ka-treatment ka Zanzibar hapo ili tuweze ku-rescue situation ambayo ni nchi moja. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Festo Sanga unaipokea taarifa hiyo?

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, naipokea na hili ndio maana nalisisitiza, hizi tozo ambazo zipo kwenye mafuta zingepunguzwa. Nataka tujenge msingi kwa mfano EWURA, wako kwenye maji, wako kwenye umeme, wako na maeneo mengine; EWURA wangeondolewa mle kwa sababu kwa kipindi hiki, kwa udharura huu, hawana haja TASAC wangepunguziwa lakini hizi excise duty kwenye kodi karibu shilingi 400 zingepunguzwa hizi zote ili tuweze ku-rescue hali ya nchi kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, kwa upande mwingine nazungumzia tupate mkopo popote pale kwa ajili ya kuweka ruzuku kwenye mafuta ili yaweze kupungua. Kwa sababu tukiendelea kuacha hali hii na kwa jinsi tunavyofanya projection inawezekana mbele mafuta yakazidi kupanda bei, tutasema nini kwa Watanzania. Ni vyema tukaanza ku-rescue kwa uharaka zaidi hali hii kwa kutafuta fedha mahali pengine tukaweka kwenye mafuta, Watanzania wakarudi kwenye hali ya kawaida, nauli zitashuka, bodaboda sasa hivi huko nje ukiangalia hata bei zimepanda, yaani hali sio nzuri kwa wananchi huko nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuiombe Serikali, hatua zinachukuliwa ikiwemo ya kusaidia kuongeza watu wanaoagiza mafuta nje, lakini kwa wakati huu na Mheshimiwa Rais anaupiga mwingi na tunaamini hili atalipiga mwingi kuhakikisha kwamba tunapata fedha ya kuweka ruzuku kwenye mafuta ili bei ishuke.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na hayo tu kwamba Serikali ichukue hatua hiyo kuhakikisha kwamba tunashusha bei kwenye mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze nichangie kwenye Wizara ya Elimu. La kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri na inayoonesha mwelekeo mpya kwenye Wizara ya Elimu. Nina mambo matatu nataka kuchangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza nataka kuchangia kuhusu Sheria ya Elimu ya Mwaka 1978. Mheshimiwa Waziri katika mambo yako saba ambayo unataka kuyafanyia kazi kwenye Wizara ya Elimu, umeyaorodhesha kwamba mojawapo ni Sheria ya Elimu ya Mwaka 1978. Ninakupongeza na ninaomba tu nikukumbushe jambo moja kwamba, mmesema mmekusanya karibu maoni 100,000 kama siyo 1,000,000; mfumo wetu wa elimu umekuwa ukichezewa sana. Katika mabadiliko ya sheria ambayo mnaenda kuyafanya, mojawapo ni kuhakikisha jinsi gani tunakwenda kuilinda elimu yetu isipate mawazo ya mtu binafsi yakaingizwa kwenye mfumo wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye nchi hii kuna mambo ambayo yametokea takribani matano kama siyo sita ambayo naweza kusema ni ya ovyo au siyo ya ovyo, lakini ni mambo ambayo yanaonesha ni jinsi gani elimu yetu inachezewa. Ukimsikiliza Nelson Mandela kwenye kitabu chake cha Long Way to Freedom anasema: “Education is a most powerful weapon which you can use to change the world.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye nchi yetu Mawaziri kadhaa wamepita na wamekuwa wakifanya maamuzi ya ajabu ajabu sana. Kuna Waziri siku moja aliamka akafuta UMISETA kwenye nchi hii, kwenye michezo; kuna Waziri siku nyingine akaamua kuchanganya Chemistry na Physics kuwa somo moja; kuna Waziri akaja akaondoa Division kwenye nchi hii akaweka GPA. Namshukuru Mheshimiwa Mama Ndalichako alikataa. Aliporudi kuwa Waziri, akairudisha Division. Siyo hayo tu, kuna mambo mengi sana ambayo Mawaziri mnaamua tu, leo hii elimu ya nchi ielekee huku, leo elimu ielekee huku mnavyotaka nyie.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaomba mlete sheria hapa Bungeni tuifanyie marekebisho, tuweke sheria jinsi ya kuilinda elimu yetu isichezewe. Kusiwe tu na kikundi cha mtu mmoja anaamua kubadilisha elimu yetu ifanye inavyotaka. Lazima ipate public opinion kuanzia Wabunge na hata wananchi ili tunapofanya mabadiliko yoyote, yawe ni mabadiliko yenye tija kwa Taifa letu. Siyo Waziri tu anaamka leo kutokana na utashi wa Profesa Mkenda, leo akiamua kufuta Form Three, anafuta. Hapana, lazima tuwe na namna ya kuilinda elimu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo nataka kuchangia ni kwenye utitiri wa kozi kwenye vyuo vyetu. Mheshimiwa Waziri, ubora wa elimu yetu umeendelea kupungua kila siku. Ubora wa elimu yetu unapungua kutokana na kuondoka kwenye mlengo wa vyuo kadha wa kadha ambavyo Mwalimu Nyerere alivianzisha kwa makusudi. Kwa mfano, kuna chuo kama cha SUA (Sokoine University) kilianzishwa kwa ajili ya mambo ya Kilimo, lakini leo wanatoa education, tofauti kabisa na malengo ya chuo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda Chuo cha Ardhi ambacho kilianzishwa kwa malengo ya vijana wetu kusoma kuhusu Ardhi, leo wanaotoa Accountants na Finance. Ukienda kwenye Chuo cha UDOM, wakati tuna MUHAS ambayo inahangaika na masuala ya udaktari wa mifupa na binadamu, leo UDOM wanatoa hiyo kozi pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, vyuo vipo tofauti tofauti ambavyo vimekuja kutuvuruga. Mzumbe kilianzishwa kwa ajili ya Sheria na Utawala, lakini leo nenda kuna kozi za Education na Tourism. Kwa nini wanafanya hivi? Wanafanya hivi ili wafanye enrollment ya wanafunzi wengi wapate fedha, kwa ajili ya kuendeshea vyuo vyao. Hili Taifa haijafikia uwezo huo wa kushindwa kupeleka fedha kwenye vyuo, hadi vyuo vinaenda kuingiza kozi ambazo ni nje ya mlengo wa chuo husika ili wapate fedha kwa sababu ya enrollment ya wanafunzi na pressure ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, hakuna relationship au mahusiano ya karibu kati ya Wizara ya Elimu, Wizara ya Utumishi na TCU. Nataka nikupe mfano Mheshimiwa Waziri; kwenye meza yako leo watu wa ADEM pale Bagamoyo, kile Chuo cha Bagamoyo ni kwa ajli ya Short Courses, leo hii TCU imewapitishia waanze kufundisha ADEM kwenye suala la Uongozi, wanasema Udhibiti wa Elimu, wakati kwenye Utumishi ukienda hakuna ajira inayohusisha Mambo ya Udhibiti wa Elimu. Wale wameanzisha kozi ambayo wao na TCU wameelewana lakini hakuna mawasiliano na Wizara ya Utumishi. Kwa hiyo, tunaenda kuzalisha watu ambao baadaye wanakwenda kukaa kwenye benchi, wanaanza kulalamika kuhusu ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, pitia vyuo vyote; kama SUA tulianzisha kwa ajili ya kilimo, angalia kozi zinazotolewa pale ziwe za Kilimo. Kama DUCE ilianzishwa kwa ajili ya Education, DUCE ina uwezo wa kuzalisha branch nyingine kwa ajili ya Education. Siyo kwenda ku-impose kwenye vyuo vingine. Leo tutashangaa IFM nao wanaanza kutoa Education. Itakuwa ni nchi hii Mheshimiwa Waziri? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunamwomba na kumsihi sana Mheshimiwa Waziri, yeye ni academician, ni msomi, tunategemea sana kwamba ataenda kufanya reformation kwenye mfumo wetu wa elimu. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Mama Ndalichako aliamua kufuta majoho, maana yake mliamua kuidhalilisha elimu yetu, hadi chekechea wakawa wanavaa majoho, na nyie mpo tu. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Mama Ndalichako, leo hii angalau; kwa sababu ilikuwa mtu ukivaa joho lazima ulipambanie. Siyo tu mtu kutoka chekechea anavaa joho; ataona wapi umuhimu wa elimu? Ni kwa sababu nyie Mawaziri mnafanya business as usual, mmetulia, mmekaa, nawaomba mfanye reformation. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii inaenda sawa sawa na mlundikano wa vitabu kwenye mfumo wetu wa elimu. Leo hii Eng. Chiwelesa akiamua kuandika kitabu, anakiingiza kwenye mfumo wetu wa elimu na kinatumika. Hakina ithibati, hakina chochote, na ukienda kila darasa vitabu vipo vingi, havina utaratibu wowote ule, kiasi kwamba tumeanza kuwachanganya Watoto. Huyu definition ya geography ilisomwa hivi; huyu definition ya geography anaijua hivi; huyu definition ya biology anaijua hivi, huyu definition ya biology anaijua hivi. Tumeruhusu mlundikano wa vitabu kwenye mfumo wetu wa elimu, vitabu ambavyo havina ubora havina ithibati ya Serikali kwamba viweze kutumika kwenye mfumo wetu. Ninakutegemea sana kama yangu Mheshimiwa Mkenda, utatusaidia kubadilisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza sheria iletwe hapa ili na wewe usifanye maamuzi unayojisikia kwanza leo unataka uibadilishe elimu yetu unavyotaka. Lete sheria tuweze kubadilisha ili sheria yetu tuweze kuiwekea ukingo, isianze kutumika ovyo ovyo. Tunaomba pia kwenye vyuo; vipitie vyote ujue vinavyofanya ndiyo yale malengo yaliyokusudiwa au ni pressure ya kupata fedha ili waweze kuendesha vyuo vyao? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. Nami niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hili alilolifanya leo. Hiki alichokifanya Mheshimiwa Rais kuweka fedha kwenye mafuta ndicho ambacho Watanzania wengi leo mioyo yao imetibiwa. Nampongeza sana Rais wangu kwa niaba ya wananchi wa Makete, tunampogneza Mheshimiwa Rais kwa niaba ya bodaboda, bajaji na wananchi wote wa Taifa hili kwa kusikiliza kilio cha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye hoja hii ya kumpongeza Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Engineer Chiwelesa kwa kuleta hoja hii, mimi Mbunge wa Jimbo la Makete nina kila sababu za kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, kuna hoja kadha wa kadha ambazo unaweza ukamzungumzia Mheshimiwa Rais kwa yale ambayo ameyafanya mengi.

Mheshimiwa Spika, kwanza ukiangalia kwenye sekta kwa mfano ya utalii, wakati dunia ina-suffocate kutokana na suala la Covid na watalii kupungua, Tanzania tumeweza ku-excel kwa kuongeza idadi ya watalii wengi kutokana na juhudi za Mheshimiwa Rais programu ya Royal Tour.

Mheshimiwa Spika, kwa idadi ya watalii tu, tumetoka kutoka 900,000 tumeenda 1,500,000 kwa kipindi hiki cha mwaka 2021 kuja mwaka huu. Haya yote ni matunda ya Mheshimiwa Rais. Ukienda kwenye suala la makusanyo ya fedha kwenye utalii, tumetoka dola milioni 1,300,000, tumeenda dola 2,500,000 ndani ya muda mfupi sana ambao Mheshimiwa Rais amefanya. Kwa hiyo, mimi kama Wabunge wengine, ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi ambazo amezifanya.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kwenye suala la miradi ya maendeleo, kuna miradi mikubwa ambayo tunaendelea nayo kama SGR, ununuzi wa ndege na ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere. Ni miradi ambayo certificate zina-mature mara kwa mara na zinatakiwa zilipwe. Hata hivyo, at the same time ukienda kwenye Halmashauri, miradi mingi inaendelea na fedha zinashuka kwa kiwango ambacho wakati mwingine ule haijawahi kushuka. Kwa hiyo, Mheshimiwa Rais anafanya kazi ngumu, anafanya kazi nzuri, anastahili sana kupongezwa.

Mheshimiwa Spika, nawaomba Watanzania ambao wanatufuatilia, wafahamu kabisa kwamba Mheshimiwa Rais anachohitaji sasa ni kutiwa moyo tu. Haya mambo anayoyafanya, ukienda kwenye Halmashauri, Wakurugenzi, miradi ilivyokuwa ni mingi, madarasa yanavyojengwa, kwenye Mataifa mengine tunaona wanavyolia. Nenda kwenye suala la inflation rate kwa maana ya mfumuko wa bei, Taifa letu na Mataifa mengine yote yaliyoko kwenye Afrika Mashariki, Tanzania inafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii yote ni kwa sababu Mheshimiwa Rais ameweza ku-maintain uchumi wa Taifa letu kwa kiwango kikubwa sana. Kilo moja leo hapa Tanzania, ndiyo, ni kweli vitu vimepanda bei, lakini la kujiuliza, na sehemu nyingine zipo kama Mataifa ya jirani yanayoendelea huko, sisi tuko chini sana kwenye suala la mfumuko wa bei. Pia bado Mheshimiwa Rais anatoa ruzuku kwenye mafuta, anatoa ruzuku kwenye mbolea, lakini bado wanafunzi wa vyuo vikuu anahangaika aweze kuwaongezea mikopo. Hii yote ni kwamba Mheshimiwa Samia anafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kazi nzuri ambazo anafanya Mheshimiwa Rais ikiwemo pia maridhiano haya ya kisiasa, na hata sasa ukiangalia anaendelea kuunda timu kwa ajili ya kuboresha diplomasia ya uchumi kwenye Wizara ya Mambo ya Nje, ameunda kikosi kazi chini ya Balozi Yahya Simba ili waangalie tathmini ya utendaji kazi wa Wizara ya Mambo ya Nje ili kuendelea kuboresha diplomasia yetu ya uchumi kupitia Wizara ya Mambo ya Nje. Ni jitihada za kweli za Mheshimiwa Rais anaendelea kuhakikisha Taifa letu linazidi kufunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kwa haya anayoyafanya, maridhiano ya vyama vya siasa kwenye Taifa letu na demokrasia, hata vyama vingine viweze kuiga ambacho Mheshimiwa Rais anafanya. Mheshimiwa Rais anatengeneza maridhiano. Hata wao kwenye vyama vyao, tuwaombe wawe na maridhiano kwa sababu Taifa hili tumeamua kusamehe yote yaliyopita, tumeamua kuanza ukurasa upya. Hata wao wawe na ukurasa mpya kwa sababu kama wameridhia kuchukua ruzuku kutoka Serikalini kutokana na idadi ya Wabunge na idadi ya kura, basi waridhie hata kuwasamehe hawa ndugu zetu ambao pia walikuwa na changamoto hizo. Kwa sababu ruzuku hiyo imetokana na wao wanayoichukua. Sasa huwezi ukatambua ruzuku, lakini usiwatambue Wabunge ambao tuko nao humu ndani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tu, hata maridhiano hayo yaendelee kufanyika kwenye maeneo mengine. Jitihada za Mheshimiwa Rais ziguse kila mtu, na wao kwenye vyama vyao viweze kuwagusa.

Mheshimiwa Spika, mimi sina mambo mengi sana, lakini kwa niaba ya wananchi wa Makete, kwa kweli miradi ya maendeleo tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais amefanya kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye hoja hii iliyoko mezani ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara. Nina mambo matatu wakati Mheshimiwa Elibariki Kingu anachangia kuhusu mafanikio ya Mheshimiwa Rais kwenye Uwekezaji wa Sukari na hili waweze kutambua Watanzania ni kwa mara ya kwanza wakati wote wa Ramadhan hatujaona sukari ikihadimika. Hili ni jambo kubwa sana ambalo Mheshimiwa Rais amelisimamia la Mfungo wa Ramadhan umeenda vizuri hakujakuwepo na kelele yeyote kuhusu sukari. Kwa hiyo, ninaunga sana haya maelezo ambayo ameyatoa Mheshimiwa Kingu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo matatu jambo la kwanza ni jambo la lumbesa Mheshimiwa Waziri ni muhanga mkubwa sana wa changamoto ya lumbesa na ninavyozungumza saa hizi Wananchi wa Makete na Mikoa mbali mbali nchini yawezekana wanaweza wakawa na nyota ya nuru na ya matumaini kwamba labda Serikali inaweza ikatoa mwanga kuhusu suala la lumbesa kwenye Taifa letu. Mheshimiwa Waziri mimi nitahitaji kushika shilingi kwa sababu gani? ukikaa na Mheshimiwa Bashe anakwambia suala la lumbesa ni suala la Wizara ya Viwanda na Biashara na unakuta ana asilimia mia moja ni sahihi kwa sababu nyie ndiyo watu wa vipimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Taifa letu la Tanzania ndiyo Taifa pekee ambalo tunapima mtu kwa kumkadiria kwamba gunia likifika kiwango hiki ndiyo limetimia gunia moja. Ukienda Kenya, ukienda East Africa zote nchi hakuna utaratibu wa kupima kwa kumkadiria mtu kwamba kwa kimo hiki ndiyo gunia la vitunguu limetosha pale Singida, kwa kimo hiki gunia la vitunguu limetosha pale Iringa na kwa kimo hiki viazi gunia limetosha. Mheshimiwa Waziri it’s a high time now tuchukue nafasi ya ku–introduce vipimo kwenye upimaji wa mazao yote nchini kwa sababu gani? Suala la lumbesa is a mindset mtu anadhani gunia likiwa limefungwa kile kilemba cha juu ndiyo lumbesa kumbe hicho hicho kilemba ukienda kuweka kwenye mizani yawezekana hakijafika gunia la kilo mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu concept ni hii kilo mia ndiyo sawa sawa na gunia moja hasa wakulima tuwatoe kwenye hili ombwe lakudhani kila kitu ni lumbesa tu–introduce vipimo Mheshimiwa Waziri una nafasi ya kukaa na Tamisemi kuna selling points maeneo tofauti tofauti kwenye Kata zetu, kwenye Vijiji vyetu wekeni mizani wakulima wasiibiwe na mfanyabiashara asiibiwe ili concept ya mind set ya suala la lumbesa iweze kufa kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ninakuomba sana sana sisi Watu wa Makete navyo zungumza saa hizi wakulima kule, wafanyabiashara wanagombana na halmashauri ni lumbesa lumbesa sasa haieleweki yupi anaibiwa? yupi haibiwi? haieleweki kwa sababu gani? Hakuna mizani ya kupima concept yetu ni ile ile mbona sukari mnapima kwenye kilo? Mbona unga mnapima kwenye kilo? Mbona nyama mnapima kwenye kilo? Na hata parachichi nilisema limeanza na mguu mzuri linapimwa kwenye kilo. Ingekuwa parachichi haliuzwi kwenye kilo ingeleta matatizo makubwa kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba sana Wizara kesho mnavyokuja kutusaidia kufunga hoja mtupe majibu suala la lumbesa kwenye taifa letu hili Wananchi wangu wa Matamba, Wananchi wangu wa Makete, Wananchi wangu wa Kinyika waweze kupata suluhisho la suala la changamoto la lumbesa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu la pili kwa Mheshimiwa Waziri wakati nazungumza hapa kuna suala la Kariakoo nimesoma nimepitia Hotuba yako yote swali langu moja tu nataka nijiulize Wafanyabiashara wa Kariakoo anae watetea ni nani kwenye nchi hii? kwa sababu nimepita kwenye Hotuba yako sijaona chochote kinacho zungumzwa Kariakoo is our own Dubai. Kariakoo ndiyo Dubai ya Taifa letu na ndiyo iko chini ya Wizara yako, iko chini ya Wizara ya Fedha, iko chini ya Wizara nyingi tu ni Mpango gani Mkakati wa Serikali yetu kuhakikisha wanazidi kuinusuru Kariakoo? Kwa sababu kiuhalisia Mheshimiwa Waziri Kariakoo inazama hilo ndiyo ukweli ulioko wazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nenda kaangalie floo ya wafanyabiashara wa kigeni Kariakoo imepungua kwa asilimia zaidi thelathini zaidi ya asilimia arobaini kwanini wamepungua? Mheshimiwa Waziri ni vyema mkaenda mkafanya vikao na wafanyabiashara Kariakoo mkakubaliana ni nini kifanyike ili Kariakoo kama Dubai yetu iweze kuinua, ili kama Kariakoo Dubai yetu isizame saa hizi Kariakoo is moving to Uganda Kampala, Kariakoo now is moving to Lusaka, Kariakoo now is moving to Lilongwe biashara sasa watanzania imegeukia kwenda kwenye mataifa ya Jirani. Tumefungua milango kwenye mataifa ya Jirani ndiyo tukafate bidhaa wakati sisi ndiyo tulikuwa tunalisha East Africa nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii bidhaa nyingi tunachukua kutoka kwenye mataifa ya East Africa wapi tumekwama kama Taifa? Kama Mawaziri ninawaomba sana jisikieni uchungu kuona Kariakoo inazama kama kuna changamoto za kikodi kama Mbunge nashauri kaeni na Wizara ya Fedha, kaeni na TRA mjue jinsi gani mnaweza mkainusuru Kariakoo na changamoto za kikodi Kariakoo ikatengama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii unakaa na mfanyabiashara anasema naenda kufata shuka Uganda, naenda kufata mizigo Uganda why Uganda and not Kariakoo there is a problem tunaomba Mheshimiwa Waziri iangalie Karikoo kwa jicho la karibu kwa sababu utasema mbona unaizungumzia Karikoo tu kwanini uzungumzii Arusha? Kwanini uzungumzii Mbeya? Sisi Kariakoo kwa maana Kariakoo ndiyo inalisha Arusha, ndiyo inayo Ilisha Mbeya lile ndiyo shamba kubwa linalolisha Taifa letu ni lazima na ninyi muichukue hii kama Dubai yetu mkaiangalia kwa mtazamo wa karibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyabiashara wamepungua nenda Msimbazi Post, nenda central utakuta wafanyabiashara wa Kikongo, wafanyabiashara wa Nigeria wamekamatwa pale. Kama umekamata risiti ya mzigo iko hovyo deal na yule aliyetoa ile risiti ni nani usi-deal na wafanyabiashara wa kigeni. Ukimwi- intimidate huyu unazuia kesho kurudi, keshokutwa anatafuta njia nyingine ya kwenda. Tunakuomba sana Mheshimiwa Waziri ucheki Kariakoo kwa jicho la karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo langu la mwisho ni kuhusu uwekezaji kwenye Mkoa wa Njombe. Mheshimiwa Waziri ninakuomba sana, suala la Liganga na Mchuchuma, na kwenye hotuba yako hapo ukipitia umezungumzia Liganga na Mchuchuma unasema hivi, matumizi ya chuma nchini yameongezeka kutoka tani 226,000 hadi tani 1,000,000; tangu nimezaliwa inazungumzwa Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna miradi ya SGR, tuna miradi ya Bwawa la Mwalimu Nyerere, na uzuri SGR sio kwamba imekomea hapa, inaendelea. Hii miradi yote inayotumia chuma. Tunaomba Mheshimiwa Waziri Liganga na Mchuchuma ianze kufanya kazi ili tuweze kunusuru Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nilikufuata kwenye meza yako nikakuomba; sisi Makete tuna wheather ambayo inaweza kuzalisha mianzi kwa ajili yakutengeneza toothpick lakini leo hii toothpick zinatoka China. Ninaomba kwa fursa ambayo unayo usi-concentrate sana kwenye coastal zone corridor kwenye uwekezaji. Kuna huku pembezoni mwa nchi kama Makete kuna sehemu nzuri ambazo unaweza ukawekeza na ukalisaidia Taifa letu kwenye maeneo ya kilimo na viwanda mbalimbali. Tunaomba sana utembelee kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo mimi sina mambo mengi sana ni hayo mambo yangu matatu, Mheshimiwa Mungu akubariki na ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Wizara ya Kilimo. Jambo la kwanza napenda kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, moja kati ya Mawaziri ambao ni vijana, tunajivunia lakini na Bunge linajivunia, Mheshimiwa Bashe pamoja na Mheshimiwa Anthony Mavunde kwa sababu wanatupa ushirikiano wa kutosha nyakati zote, hata usiku ukimtafuta anakusaidia. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri anatuongoza vizuri vijana na tuko tayari kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya yanayoendelea kwenye bajeti zote alizozisoma Mheshimiwa Waziri, wakati ule tunagawa vifaa na hii iliyosomwa, inaonesha wazi kwamba kilimo kinaenda kubadilika kwenye Taifa letu. Waziri ana mwono wa mbali kwa kiwango ambacho mimi kama kijana najivunia sana uwepo wa Mheshimiwa kaka Bashe kwenye Wizara ya Kilimo na tunampongeza sana. Kwa niaba ya wananchi wa Makete nimpongeze sana. Uono wake wa mbali ni pamoja na kwenye bajeti yenyewe ambayo alimwomba Mheshimiwa Rais. Kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kufanya change kwenye kilimo kwa kuongeza bajeti hadi bilioni 700.5. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri aliomba zaidi ya trilioni mbili kwenye Wizara ya Kilimo, Mheshimiwa Rais kwa sasa ametuanzia na bilioni 7. Ukienda kwenye bajeti ya Kenya wanacheza na bilioni 900 hadi trilioni moja, kwa hiyo anawafukuzia, yuko nyuma yao kidogo anawasogelea, hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri. Akienda kwenye bajeti za Zambia na Uganda naona bado sisi tunazidi kukimbiza kwa hiki ambacho anaenda kukifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu uko kwenye mambo makubwa mawili. Jambo la kwanza ni suala la mbolea, naungana na Mheshimiwa Waziri kwa asilimia 100. Siku ile alimwambia Mheshimiwa Rais ampe bilioni 150 kwa ajili ya ruzuku kwenye mbolea. Mimi kama Mbunge wa Makete namuunga mkono na kwa niaba ya Wabunge wa Kusini tunamuunga mkono kuhusu ruzuku kwenye mbolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbolea sisi kwetu ni siasa, mbolea kwetu ndio uhai wa wakulima wetu, mbolea kusini ndio kila kitu kwa wananchi wetu. Nimwambie wazi Mheshimiwa Waziri, yeye ndiye amebeba Ilani ya Chama cha Mapinduzi, kwa sababu Chama cha Mapinduzi ni chama cha wakulima na wafanyakazi. Mbolea ni kilio na naiona direction ya Waziri anayoenda kuichukua ya kuomba fedha bilioni 150 kwa ajili ya kwenye ruzuku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amesema jana kwamba ni bora Wizara ya Kilimo isifanye kitu chochote lakini iongeze ruzuku kwa wakulima. Niwaahidi wananchi wa Makete Mheshimiwa Bashe hili tutamwombea kwa Mheshimiwa Rais na namwomba Mheshimiwa Rais bilioni 150 na zaidi hapo aweze kumpatia Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alifika hadi Makete Kijijini kule Kinyika alijionea hali ya wananchi wangu. Changamoto ya parachichi tuliyonayo ni kubwa sana. Parachichi, limeanza na mguu mzuri, parachichi kwa sababu halina lumbesa wanapima kwenye mizani, tunaishukuru Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya kwanza ya parachichi ni kwamba kumekuwa na wakulima holelaholela ambao hawafikiwi na Maafisa Ugani, uzalishaji wa miche holela holela ambao miche mingine ina ubora huu, mingine ina ubora huu. Changamoto tunayoipata tutafika wakati miti imekua hatuna wa uwezo tena wa kurekebisha kwenye miti ya mbolea. Tunaomba wizara iwahi mapema sekta ya parachichi ndani ya Mkoa wa Njombe, Mbeya na maeneo mengine iwekewe mpango mkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ukienda Wakenya wanaingia hadi mashambani kununua parachichi zilizoko kwenye shamba. Sasa ni vyema tukaandaa mazingira, wakulima wetu wawe na muundo mzuri wa jinsi gani biashara ya parachichi itaenda.

Mheshimwa Mwenyekiti, nimemwandikia barua Mheshimiwa Waziri na nimempelekea mezani kwake. Naomba miche milioni 15 kwa ajili ya wananchi wa Makete kwa sababu nina kampeni Makete ya nyumba moja miche 50. Leo naomba tena Waziri atuwekee kitalu cha parachichi Makete, ile miche inayozalishwa pale iendane na hali ya hewa ya Makete na izalishwe katika ubora kupitia Maafisa Ugani. Ninamsihi na namwomba Waziri, miche milioni 15 iko mezani kwake, namwomba wananchi wa Makete wanasubiri kampeni ya nyumba moja miche 50 kwa sababu tunaamini ndiko utajiri uliko na mkakati wa wazi kabisa wa kuwakomboa wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata cold room, Mheshimiwa Waziri amesema anajenga cold room nyanda za juu kusini. Tunaomba hata Makete tuna eneo la karibu na airport ya Mbeya kwa sababu Njombe airport hawajatujengea. Ili tuwahishe mzigo Mbeya kwenye airport yetu ambayo itakuwa inapakia parachichi kwenda kule na kwenye treni, Waziri ajenge cold room Mbeya pale au Makete itusaidie ili wananchi wetu wasipate shida ya kuhangaika kutafuta sehemu ya kuweka cold room.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine sawasawa na hilo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri kuhusu suala la lumbesa. Waziri amehangaika kadri awezavyo, suala la lumbesa na wananchi walimwambia. Lumbesa itatatuliwa tu kwa kuweka mizani na hili ni suala la viwanda na biashara. Watu wa viwanda na biashara kama wako hapa waweke mizani tuondokane na changamoto ya lumbesa. Tuondokane na changamoto ya lumbesa kwa nini?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba dakika moja tu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa, malizia sentensi yako tu.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia sentensi yangu moja. Mheshimiwa Bashe iko hivi, Wakenya wanavyokuja na wakulima wengine wanakuja kununua viazi, wananunua gunia moja lina lumbesa, lakini wakienda kwao wanapima kwa mizani. Kilo mia ni sawasawa na gunia moja. Hapa imeondoka na gunia lina kilo 140. Kwa hiyo kama liliondoka na gunia 300 akifika Kenya anakuwa na gunia 400 mpaka 500. Wakulima wetu huku wananyonywa tunafaidisha wananchi wengine. Serikali iweke mizani ili tuondokane na lumbesa. Wizara ya Viwanda na Biashara tunaomba watusaidie,waweke mizani, lumbesa linawamaliza wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ustawi na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Elimu, Utamaduni na Michezo kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyoko mezani na nitajikita kwenye suala la michezo. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaifanya ya kuhamasisha michezo kwenye Taifa letu. Anafanya kazi kubwa sana ambayo kila mtanzania anaona, na kwa kweli anastahili pongezi nyingi sana kwa ku-support michezo nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mwenyekiti wa Kamati hii ambayo inasimamia mambo ya elimu na michezo kwa uchambuzi wao mzuri ambao umeweka wazi bayana yale yaliyoko na yale ambayo wameyaona kwenye utendaji wa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitaomba nizungumzie suala la michezo; na michezo yote lakini nikijikita zaidi kwenye football. Sisi kama Taifa tumepata nafasi ya kuandaa michuano ya AFCON mwaka 2027 katika zile nchi tatu, kwa maana ya Kenya, Uganda pamoja na Tanzania, lakini niseme wazi hadi dakika hii ninavyozungumza na Watanzania wanaotusikiliza nia ya dhati ya kuhakikisha kwamba Serikali au nchi yetu inafanya vizuri kwenye michezo hiyo hadi dakika hii hatujaiona dhahiri kama ambavyo Kamati imeyasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilichangia hapa kuhusu ujenzi wa viwanja na nitumie nafasi hii kuipongeza Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kwa jinsi ambavyo imejenga uwanja wao imeukarabati, uwanja ambao tumeenda kuushuhudia wakati wa Mapinduzi. Kila Mtanzania aliyeingia pale alitamani anakoenda awe na kiwanja angalau kile. Kiwanja ambacho hakichukui watu wengi lakini kina ubora na kina kidhi mahitaji ya matumizi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii niiombe Serikali, kwamba tujisikie wivu, tujisikie wivu ninarudia tena. Kama Baba wa Taifa Mwalimu Nyerere alijenga viwanja nchi nzima kipindi ambacho teknolojia haipo, kipindi ambacho rasilimali ya watu iko chini, kipindi ambacho fedha hazikuwa nyingi, lakini akajenga viwanja vya Ali Hassan Mwinyi, CCM Kirumba, Sokoine na Mkwakwani; leo Taifa lenye watu milioni 61 tumekuwa tukipiga ajenda kila siku jinsi ya kujenga viwanja kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima Serikali ione dhamira ya dhati jinsi gani ya ku-support michezo hapa nchini. Mojawapo ni hili suala la asilimia tano. Tutamlaumu Ndumbaro, tutamlaumu Mheshimiwa Hamis Mwinjuma Mwana FA, tutalaumu Wizara ya Michezo; lakini Bunge hili lilipitisha five percent ya sport betting ambayo mimi nilichangia wakati ule, iende kwenye kusuport michezo kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii sport betting haipo kama michezo haipo, michezo yenyewe ndiyo inayozalisha fedha hii, kwa hiyo ni wajibu wa Serikali kuendelea kuipatia fedha Wizara; lakini ukisoma kwenye maoni ya Kamati wanasema toka tumepitisha asilimia tano hadi leo hakuna hata shilingi kumi iliyokwenda BMT kwa ajili ya ku-support michezo. Akina Ali Mayai watahangaika tu tutawapigia kelele lakini hawana fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi niiombe Serikali, asilimia tano ni fedhaa ndogo sana; tuombe angalau hata asilimia zaidi ya 60. Ukiwa ni mkakati wa miaka mitatu kuelekea AFCON Serikali iachie fedha za sport betting na zielekezwe kwenye kuwekeza maendeleo ya soka nchini ili Taifa letu tusije tukapata aibu mwaka 2027. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Serikali iwe Sikivu; na bahati nzuri aliyeko kwenye Wizara ya Fedha kwenye kapu la fedhaa ni Mheshimiwa Mwigulu Nchemba ambaye ni mwanamichezo kwenye Taifa letu. Inasikitisha pale ambapo tunaona Waziri wa Fedha hajapeleka hata shilingi moja kwenye michezo. Sport betting wanaripoti kwamba ndani ya mwaka mmoja Bodi ya Michezo ya kubashiri wanatengeneza bilioni 170.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wanatengeneza bilioni 170, bajeti ya Wizara ya Michezo ni bilioni 35 zaidi ya mara sita ya fedha ambayo inazalishwa na sport betting. Kwa kweli Serikali ione haja ya kuwafanya akina Ndumbaro wapate fedha za kuendesha michezo kwenye nchi hii, na kumfanya Ali Mayayi mipango aliyonayo kichwani ya kuifanya TFF na Serikali iweze kufanya kitu kikubwa iweze kutekelezeka. Kwa hiyo niombe sana Serikali iachane na biashara hii ya kukalia hiyo asilimia tano ya sport betting na hivyo iweze kwenda kwa ajili ya ku-support michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kila sababu; ukifuatilia timu za taifa muda mwingine hadi kusafiri zinachangisha fedhaa ili ziweze kusafiri kwenda kwenye michuano. Tusiendelee kuleta mzaha huku kwenye michezo. Kuna sehemu nimezungumza wakati Brazil na Marekani au na Uingereza wanawaza kucheza fainali za Kombe la Dunia sisi Tanzania tunawaza nauli ya kuipeleka Timu ya Taifa kwenye michezo, jambo ambalo kwa kweli kwenye Taifa ni aibu. Ni vyema tukachukua hatua kuhakikisha kwamba hizi fedha zinaenda kwa ajili ya ku-support michezo kwenye Taifa letu ili mwaka 2025 kuwepo na tija kwenye hiki ambacho tunaenda kukifanya na Watanzania waone kwamba kweli Serikali ilikuwa serious na ujenzi wa hiki kinachofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la Uwanja wa Taifa ndani ya mwaka huu 2023/2024; kwa maana Oktoba mwaka jana hadi Juni mwaka huu; Uwanja wa Taifa ni zaidi ya mechi 25 za kimataifa zinachezwa, na the lowest amount ambayo inatolewa ni dola laki mbili tu; the highest amount zinaenda hadi milioni moja, timu kutoka Morocco, timu kutoka Rwanda, kutoka Burundi zinaomba kuchezea Uwanja wa Taifa. Mapato mengi yanakusanywa pale lakini Serikali inayachukua hairudishi tena ku-support Wizara ya Michezo ili iweze ku-run kwa maslahi makubwa ya Taifa letu. Niiombe Serikali uwanja huu uweze kujiendesha lakini pili Wizara ya Michezo iweze kuwezeshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ni kuhusu wachambuzi wa michezo kwenye Taifa letu. Nizungumze wazi; kwanza wachambuzi wasiokuwa na uzalendo, wachambuzi wasiokuwa na nia njema ndio wanweza kuilalamikia Wizara ya Michezo, kwamba wakianzisha Kozi ya Wachambuzi kwenye Taifa letu basi wao watakuwa wamekosa fursa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna-records, Taifa hili mwaka 2012 kuna mchezaji alikuwa anitwa John Bocco aliwahi kujiuzuru Timu ya Taifa kwa sababu ya wachambuzi na Watanzania wasiokuwa na uzalendo wa kuzomea wachezaji wetu. Sasa ni vema wanachoenda kukifanya Wizara ya Michezo lazima tuwe na certified and qualified hawa sport analyst ili watu wajue kwamba ile ni kazi mmalum kama kazi nyingine, kama ambavyo madaktari wako hospitalini wanafanya kazi ya specialist ndivyo ambavyo hii sport analyst iwe na watu ambao wana taaluma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, isingekuwa vyema kuwa na wachambuzi ambao wanaingia kuchambua kwa sababu mtu ana followers wengi Instagram, mtu anaweza kushawishi watu kwa mambo mengine akaenda kuchambua michezo na baadaye kusababisha wachezaji wetu au Taifa letu likaingia kwenye kuwakasirikia wachezaji na kukosa uzalendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hata kipindi hiki cha AFCON kuna wachambuzi wamechambua sana wachezaji wakati Taifa na Serikali inawekeza kuwaita Watanzania walioko nje kuja kulitumikia Taifa lao. Kuna wachambuzi kwenye vyombo vya Habari wamekuwa waki-discourage effort za Serikali wamekuwa wakishambulia wachezaji, ni wachezaji wadogo ambao wanahitaji kuwa moyo wa kulichezea Taifa lao. Sasa wakiona kwamba kuna wachambuzi ambao hawajitambui wanawashambulia kwa kweli inavunja moyo wa Serikali…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Festo Sanga kwa mchango mzuri.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nakushukuru na niseme wazi kwamba Wizara inafanya vizuri; lakini Serikali kuelekea AFCON tujiandae vizuri ili tulifanye Taifa letu liwe na heshima kubwa kwa Watanzania, ahsante. (Makofi)
The Water Resources Management (Amendment) Act, 2022
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye Muswada huu wa Marekebisho ya Sheria ya Matumizi ya Rasilimali Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitajikita kwenye marekebisho ya Kifungu Namba 37 Kipengele Namba 4, kinachozungumzia ulinzi wa maeneo ya uhifadhi wa maji (protected zones).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme naunga mkono kazi nzuri ambayo imefanywa na Kamati pamoja na haya mapendekezo ya Mheshimiwa Waziri. Kuna mwandishi mmoja ameandika, anasema no matter how rich you are or poor you are, you can’t live without water. Kwa hiyo, ninaamini dunia nzima inategemea sana maji ili iweze kuishi. Vilevile, wanasema no water no life, no blue no green. Kwa hiyo tunaamini kabisa maji yanahitajika kwa wingi na yanahitajika kutunzwa zaidi katika Taifa letu na kwenye dunia hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye marekebisho haya namba 37 kwenye kutunza vyanzo vya maji mimi niseme kwamba tuna wajibu wa kutunza maji kama Taifa. Katika marekebisho ya Sheria hii, mapendekezo yangu ilikuwa ni kuangalia maeneo tofauti tofauti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu gani, kwenye marekebisho ya sheria, kwa mfano watu kama wa Makete na maeneo mengine ya milimani, Njombe maeneo kama Ludewa, sheria kama hii kuna maeneo haiwezi kufanya kazi. Hii ni kwa sababu, kwa mfano, Makete ni sehemu ya milima na kuna vijito na mito. Ndani ya mita 30 unakuta kuna makazi na mashamba ya watu. Sasa, sheria hizi zinakuja kuwabana wananchi, kwamba wahame maeneo yale kwa sababu wako ndani ya mita 60 ya maeneo ambako kuna vyanzo vya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, kwa mimi, kama hii sheria ikifanya hivyo Jimbo langu la Makete lote linatakiwa liondoke. Hii ni kwa sababu wananchi wote wanaishi kwenye maeneo ya mito na kwenye vijito. vilevile wanalima kwenye maeneo haya. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ninaomba sana, tunapotunga sheria hizi ni lazima tuangalie na kuzingatia kuwa hizi sheria haziwezi kuwa applied kwenye maeneo yote. Kwa sisi watu wa Makete, kwa mfano maeneo ya Ujuni, hii ni kata yenye vijiji takriban viwili, na hili eneo limezungukwa na maji, na ndiko kwenye wakulima wakubwa wanaobeba uchumi wa Wilaya ya Makete.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye vyanzo vya maji, ndani ya mita 30, 60, sehemu kubwa wamejenga nyumba na ndimo wanamolima. Sasa, watu wa bonde la maji wamekuja pale, na bahati mbaya, nashukuru kwamba wamekupa nafasi ya kuteua watu ambao wana uelewa; wanakuja watu wa bonde la maji wanawaambia wananchi, nyie mnatakiwa muhame na hamtalipwa chochote. Lugha kama hizo zinaumiza wananchi na zinawachonganisha na Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo niombe, kwamba, lazima tuwe na sheria rafiki ambazo zinaendana na wananchi wetu na maeneo husika. Sisi hatukatai kutunza vyanzo vya maji kwa sababu sisi Makete ndio tuna provide maji kwenye bwawa la Mwalimu Nyerere, tunatoa kwenye Kituro, tunatoa Matamba, haya yote yanaenda kwenye bwawa la Mwalimu Nyerere. Na tumefanya hivi kwa miaka yote maji yanaelekea kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni kweli lazima tutunze vyanzo vya maji, lakini sheria lazima iendane na wananchi wetu wanaoishi maeneo yale. Sasa hivi mimi na DC wangu, Mkuu wangu wa Wilaya na Mkurugenzi tunahangaikia namna ya kuweza kutuliza ghasia iliyoko kule kwa wananchi kwa sababu watu wa bonde la maji wamekwenda na lugha iliyowaumiza wananchi wangu. Wananchi wa Kijiji cha Ilolo kule nao wana changamoto hiyo. Kwa hiyo lazima tuwe na sheria ambazo ni rafiki na maeneo husika haziwezi kuwa na applied na maeneo yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nizungumzie, kwa mfano pia marekebisho kwenye kipengele namba 44 (a), hapa inazungumzia kuhusu kosa la matumizi ya maji bila kibali. Waziri ni vyema hata hizi jumuiya za maji zikapewa uwezo wa kuelimisha wananchi. Nakupa mfano mmoja. Nimekwenda sehemu moja inaitwa Matamba, watu wa jumuiya ya maji na wataalamu wa maji, watu wa RUWASA, wanawaambia wananchi kwamba haya maji sheria inasema ni kwa matumizi ya nyumbani. Sasa, mwananchi anatakiwa amwagilie nyanya na bustani zake, lakini anazuia asimwagilie kwa sababu yale maji sheria inasema ni ya matumizi ya nyumbani, akitumia anapigwa faini. Sasa, ni vema tukajikita kuwaelimisha wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika taifa ambalo umwangiliaji bado haujawa katika level kubwa kwenye kilimo wananchi waruhusiwe kutumia maji haya kwaajili ya umwangiliaji. Kama kuna changamoto ya kwamba watatumia maji mengi ni vema Wizara sasa ikajikita kwenye kufunga mita kwa wananchi hawa ili mtu atumie kulingana na kiwango kile ambacho mita itasoma ili aweze kulipia, kuliko mwananchi anatumia kwenye umwangiliaji, anatumia kwenye kufyatua tofali, ambazo zinaleta tija kwenye ukuwaji wa uchumi wa Wilaya yangu ya Makete lakini anaenda kuzuiwa kwamba huwezi kutumia maji haya kwa sababu maji haya siyo kwa ajili ya umwangiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hata hizi faini ambazo mnaweza ku-introduce tunaomba ziwe ni faini rafiki, lakini tusijikite kwenye kuzuia watu kutumia maji tujikite kwenye kuelimisha. Kwa hii sheria namba 44 mtu asiadhibiwe kwa kosa la kutumia maji, mtu aadhibiwe kwa kwamba alipie kile kiwango kilichozidi kwenye matumizi ya maji, siyo aadhibiwe kwanini ametumia maji mengi au kwanini ametumia maji kwa ajili ya umwagiliaji au kwanini ametumia maji kwa ajili ya kufyatua tofali, that is not are mistake, mtu anafanya shughuli zake za kiuchumi ili ajikwamue lakini sisi tunaenda ku- block kwa sheria ambazo siyo rafiki kwa taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri, ni vyema akatusaidia sana sana kujikita kwenye kuelimisha wananchi wetu kuliko kuanza kuzuia wananchi kwamba msitumie maji kwa wingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi sina mambo mengi, yangu yalikuwa ni hayo, mambo mawili; mita 30, hizo mita 60 kutoka kwenye vyanzo vya maji lazima ziwe rafiki, sisi kule Makete his not applied. Mtafanya jimbo langu lote liondoke Makete kwa sababu ya hizi mita 30 kwa sababu mimi niko kwenye maeneo ya milima. Ninaamini kwamba Wizara yetu ni sikivu na inachapa kazi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina jambo lingine na Mungu akubariki sana, ahsante sana. Naunga mkono hoja.
Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote wa Mwaka 2022
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Muswada huu wa Bima kwa Wote.

Jambo la kwanza, niseme tu ninaunga mkono asilimia 100, kwa hili jambo kuja kufanyika wakati huu ambao ni wakati sahihi sana kwetu, tunaona kwa sababu ya yale ambayo nyuma tulikuwa tunaona ni changamoto lakini kwa sasa yamepatiwa ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza nampongeza Mheshimiwa Rais, Mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan. Kwa sababu, kwanza anaenda kuandika historia, kwa kulipitisha hili jambo kipindi ambacho yeye ni Rais akiwa madarakani. Pili, kwenye utekelezaji wa Ilani. Ukisoma kwenye Ibara ya 9 (d) “kutoa huduma kwa wote” na Ibara ya 83 “kuimarisha mfumo wa bima wa afya nchini”. Kwa hiyo, kwetu sisi hili ni goli na ni ushindi kwenye Chama cha Mapinduzi, kwa sababu yale tuliyoandika kwenye Ilani sasa yanatekelezwa na yanaendelea kutekelezwa kwa kiwango cha juu sana. Kwa hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, nampongeza Mheshimiwa Ummy Mwalimu na Wizara na Mheshimiwa DKT. Mollel, kwa jinsi ambavyo wamekuwa wavumilivu licha ya maneno na kauli za hapa kwenda juu lakini amesimama imara kuhakikisha hili jambo hatimaye leo linafika hatua hii ambayo leo hii imefika. Pia, Wizara ya Fedha na wengine wote, baadhi ya Mawaziri kwa hatua hii ya kuleta hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo langu lingine niseme tu kwamba, Watanzania wanaotusikiliza, hili jambo kama Taifa kwanza tumechelewa. Hii ni ajenda ya Kidunia. Dunia nzima wanaenda kwenye Bima ya Afya kwa Wote. Kwa hiyo, kusiwepo na chama au mtu au mpotoshaji yeyote atakayewaambia Watanzania hili tumekosea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huu ndiyo uso wa dunia unavyolitazama hili jambo kwa sasa. Wenzetu majirani zetu Kenya wameshapitisha huu Muswada. Zanzibar wameshapitisha huu Muswada. Tulibaki Tanzania na tulivyobaki tulikuwa na sababu za msingi, kwa sababu tulikuwa na vitu ambavyo watu wamepigia kelele na Serikali imeshachukua hatua. Jambo kubwa ilikuwa ni kufungamanisha bima ya afya na mambo ya vitambulisho na leseni na vitu vingine lakini Serikali imeona haja ya kuondoa hilo jambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu kingine kilikuwa ni funding. Kwa kweli watu tulikuwa na changamoto ya kuangalia funding itatoka wapi lakini niipongeze Wizara ya Fedha, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba na Wizara ya Afya, kwa kuoanisha hivi vyanzo vya mapato ambavyo vinakwenda kutusaidia kwenye utatuzi wa kero ya Bima kwa wote ambapo Watanzania wengi zaidi ya milioni 15 wanaenda kufaidika.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na wasi wasi hata upande wetu wa pili huko, wamezungumza kwamba tumekosea kuweka hivi vyanzo. Hivyo ndiyo vyanzo tulivyonavyo kwa sasa. Lazima tuanze kama Taifa kwenda mbele. Kuna mchangiaji alizungumza kutokea upande wa pili kwamba, tumekosea kufanya hili jambo. Mimi naona tuko sahihi. Hatua ya kwanza tumeianza, hatua ya pili itafuata. Hili ni Taifa letu sisi siyo kisiwa. Lazima tusonge mbele kwenye suala la Bima ya Afya kwa Wote, kwa sababu tofauti na hapo labda wangependekeza vyanzo gani ambavyo ni sahihi kuliko hivi ambavyo tuko navyo sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi naona Serikali yangu iko imara na iko vizuri. Vyanzo hivi ndiyo vyanzo sahihi na ndivyo ambavyo tulikuwa tunavitafuta Watanzaia. Tuwe na uhakika pa kuanzia, haya mambo mengine yatakuja kufuata baadaye.

Mheshimiwa Soika, ombi langu ni moja; suala la Bima kwa Wote siyo suala la Mheshimiwa Ummy Mwalimu. Suala la Bima kwa Wote siyo suala la Wizara ya Afya peke yake. Suala la Bima kwa Wote ni suala la Wizara zaidi ya tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapo unamzungumzia Mheshimiwa Ummy Mwalimu leo lakini kuna TAMISEMI wanaokwenda kuajiri watumishi. Pia, kuna Wizara ya Fedha inayokwenda kukusanya haya mapato, kwa maana ya betting na hivyo vipodozi. Naomba tusilitazame hili suala kama ni la Mheshimiwa Ummy Mwalimu wa Wizara ya Afya peke yake. Mheshimiwa Ummy ameanza, sisi wengine na Wizara zingine wasimuachie mzigo huu Mheshimiwa Ummy Mwalimu peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili hili suala la Bima ya Afya kwa Wote lifanye kazi, lazima ajira ziwepo kwa sababu kuna changamoto. Ukienda Makete kule Uganga, unakuta mtumishi yuko mmoja kwenye kituo cha afya au kwenye zahanati. Tukiwa na huu mchakato wa kutokuwa na watumishi wa kutosha kwenye hivi vituo vya afya na zahanati, hili suala litaendelea kuonekana ni kero kwa wananchi. Kwa hiyo, ni vema Wizara ya TAMISEMI ikalichukua hili jambo, kwa sababu wao wana wajibu wa kuajiri watumishi. Wakaisaidia Wizara ya Afya, wakaisadia Serikali, wakamsaidia Mheshimiwa Rais kuwaajiri watumishi wengi ili waweze kulisaidia Taifa letu na baadaye uonekane umuhimu wa hili jambo ambalo tunalifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu kingine ni suala la elimu. Taifa letu lina changamoto ya kupotosha Umma. Upotoshaji umekuwa ni mkubwa. Sijui changamoto ni kwamba mizani either haija-balance! Kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mollel yeye anasema ana changamoto, watu wenye akili huwa wanateseka sana kwa pale wanapokutana na watu wenye changamoto ya kupotosha potosha mambo. Mheshimiwa Ummy, hili jambo sasa hivi kuna watu watajitokeza kuanza kulipotosha au kuonesha kwamba haliwezekani au kuonekana kama Serikali imeamua kitu tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni vema sasa Serikali ikachukua hatu kwenda huko chini grassroot level kabisa. Mikutano; sisi Wabunge tuna wajibu wa kuelimisha lakini watendaji wa Serikali, Wakurugenzi na Watendaji wa Vijiji na Watendaji wa Kata kuwaelimisha wananchi umuhimu wa hili jambo kama Taifa letu ili tuweze kuvuka. Kwa hiyo, Mheshimiwa Ummy naomba kabisa kwamba, Wizara ina haja ya kuanza sasa kujenga na kutoa elimu kwa nguvu ili wapotoshaji wengine wasipate nafasi ya kudanganya Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kitu kingine ni upatikanaji wa madawa. Hili jambo ni lazima tuliboreshe. Mheshimiwa Ummy tunahitaji sana ili Bima ya Afya kwa wote iweze kufanya vizuri, ni lazima upatikanaji wa madawa uweze pia kuendana na kasi ya hili jambo linavyokwenda. Kumekuwa na changamoto MSD. Muda mwingine halmashauri zinatuma fedha kwa ajili ya kununua dawa, zinachelewa. Sasa, ili na sisi tupate kuzungumza na wananchi vizuri, ni vema dawa zikapatikana kwa wakati lakini zikapatikana kwa wingi ili hili jambo tunapokwenda kulijengea hoja kwa wananchi, liweze kupata baraka na liweze kupata muono wa pamoja na baadaye likawa na faida kubwa.

Mheshimiwa Spika, mwisho ni suala la kwamba, tumeona hapa vyanzo ni vingi kuna betting, kuna vipodozi, soft drinks na hard drinks, tumeziona hapa. Ni Wizara kuwa na account moja kwa ajili ya kusimamia hili jambo la bima ya afya. Hizi fedha zote zikiwa na account moja na ikipendeza, Wizara ya Afya yenyewe kwa sababu mzigo wake siyo mkubwa sana, wakiisimamia itakuwa na tija ili tuweze kufanya suala la kujua maendeleo ya Mfuko wetu wa Bima ya Afya ukoje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi sina mambo mengi lakini naendelea kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa hili aliloliamua, kama Wabunge tunaandika historia kwa wakati mwingine, kwenda kupitisha jambo lenye tija na maslahi kwa Taifa. Hii ni token ya ushindi wa Chama cha Mapinduzi kuelekea 2025. Hakuna mtu atasimama kinyume na hili jambo kwa sababau linakwenda kufanikiwa na kwa sababu pia limekuja katika mlengo mzuri. Kwa hiyo, naipongeza sana Wizara, nampongeza Mheshimiwa Rais lakini nawapongeza Waheshimiwa Wabunge kwa kuendelea kuunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kwa niaba ya wananchi wa Makete na wote ambao wanatusikiliza, tunaunga mkono jitihada hizi za Serikali. Ahsante sana. (Makofi)