Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Agnes Elias Hokororo (15 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa ni mara ya kwanza nianze kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyetujalia uzima. Pili, nitumie fursa hii kuwashukuru sana akina mama wa Mkoa wa Mtwara ambao wameniwezesha kurudi katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano inayoongozwa na Rais wetu mpendwa, jemedari bingwa, Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa mafanikio makubwa yaliyopatikana katika Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa katika maeneo yote; miundombinu, maji, elimu, afya na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze katika Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa. Mojawapo ya nguzo ya mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa kama ilivyoainishwa kwenye Mpango huo ni ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu.

Naiomba sana Serikali yetu Tukufu, ili kuwajumuisha wananchi wa Kanda ya Kusini, ni muhimu sana Mpango huu wa miaka mitano ukaingiza ujenzi wa reli ya Kusini. Kwa nini naiomba hii? Ujenzi wa reli ya Kusini ulitokana na Mradi wa Mtwara Corridor na mradi huu ulisainiwa na nchi nne; Tanzania, Msumbiji, Malawi na Zambia. Ulisainiwa mwaka 2000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, muasisi wake ni hayati mpendwa wetu Rais Mkapa. Lengo lake lilikuwa kuiwezesha Bandari ya Mtwara. Bandari ya Mtwara imejengwa kwa bilioni 157 lakini juzi swali liliulizwa hapa na Waziri alikiri kwamba Bandari ya Mtwara kwa sasa inafanya kazi chini ya kiwango. Kumbe mradi huu wa Reli ya Kusini ukitekelezwa ina maana Bandari ya Mtwara itafanya kazi ile iliyokusudiwa kwenye huu mradi na miradi ya EPZA ambayo kwa sasa bado haijaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo naiomba sana Serikali, kwenye huu Mpango wa miaka mitano ioneshe waziwazi ni lini mradi wa ujenzi wa reli ya Kusini utaanza na kukamilika ili kuwajumuisha wananchi wa Mikoa ya Ukanda wa Kusini katika ukuaji wa uchumi na maendeleo yao. Vinginevyo tutakuwa tu tunaendelea kushangilia lakini wananchi wa Ukanda wa Kusini kama maeneo haya muhimu katika ukuzaji wa nchi yetu hayatajumuishwa na wao watakuwa wanaendelea kushuhudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natambua kabisa kwamba Serikali imeanza kutekeleza sehemu ya Mradi wa Mtwara Corridor, kama vile ujenzi wa barabara ya kutoka Mtwara mpaka Mbambabay umetekelezwa, lakini pamoja na huo ujenzi wa bandari, pamoja na upanuzi wa uwanja wa ndege, lakini pia pamoja na ujenzi wa Daraja la Umoja lile linalounganisha Tanzania na Msumbiji, lile Daraja la Mtambaswala. Sasa mambo haya yote ambayo Serikali ya Awamu ya Tano na zile zingine imeyatekeleza, hii miradi itaendelea kulala kwa sababu shughuli za kiuchumi zinategemea kwa kiasi kikubwa ujenzi wa mradi wa reli ya Kusini. Naamini Serikali yetu Tukufu itaweza kujumuisha Mradi wa Ujenzi wa Reli ya Kusini ili na sisi tuweze kushiriki kikamilifu katika ile dhana ya uchumi jumuishi, uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nijielekeze katika eneo la kilimo. Kama ambavyo mpango umeainisha kwamba asilimia 65 ya Watanzania wanapata riziki yao kwa kutegemea shughuli za kilimo. Lakini tunaona shughuli za kilimo zinachangia asilimia 27 tu ya GDP na asilimia 24 ya total export.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kinahitajika katika eneo hili; kwa kuwa wananchi wa Mikoa ya Kusini, hasa Mtwara, asilimia 98 ni wakulima, ili tujumuike pia katika ujenzi wa uchumi huu ambao wote tunauhitaji, naomba sana tujikite katika mapinduzi ya kiteknolojia. Wakulima wetu kwa sasa wanatumia jembe la mkono; kwa nini? Trekta ziko bei juu, milioni 45 mpaka milioni 60. Akinamama ambao wanashiriki kwa asilimia 75 kule mashambani na katika shughuli za kilimo hawawezi kununua trekta, mikopo yetu ya vikundi vya halmashauri...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa. Kengele imeshagonga.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiw Rais kwa kazi nzuri katika maboresho ya sekta zote.

Pili, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri kwa kipindi kifupi katika nafasi hiyo; na tatu, kumekuwepo na jitihada ya kuboresha Chuo cha Uvuvi Mikindani, Mtwara ambapo Serikali ilipeleka fedha za kujenga maabara na madarasa, bado samani ili kozi za muda mrefu ziendeshwe. Kwa sasa kuna programu ya atamizi ambayo imekuwa na manufaa sana na wanafuika wamefurahia kujifunza kwa vitendo.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kuharakisha mchakato wa kukamilisha kozi ndefu kwenye Chuo cha FETA Mikindani, Mtwara.

Mheshimiwa Spika, lipo tatizo la kukamilisha mchakato wa muundo wa watumishi wa Vyuo vya FETA ambapo mpaka sasa kwa mfano Meneja wa campus ya Mikindani, Mtwara amekaimu kwa miaka 13 sasa pamoja na vyuo vingine vya Gabimori, Rorya, Kibirizi, Nyegezi Mwanza lakini pia Wakurugenzi wanakaimu na hawajatambuliwa na utumishi jambo ambalo linaondoa ari na ni kinyume na taratibu za utumishi.

Mwisho narudia kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kuanzisha programu ya atamizi ya miezi mitatu kwa wahitimu mafunzo ya uvuvi ili waweze kujifunza kwa vitendo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyopo mezani ya hotuba ya Wizara ya Nishati. Kwanza nianze kutumia fursa hii kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa hakika tumekuwa tukisema kwamba, hakuna kilichosimama na hilo limedhihirika kwa mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere ambao sasa umefikia asilimia 86.89 na kwa kweli tunaimani kubwa kwamba, ule muda uliowekwa wa kukamilika Juni 2024 tunakwenda kuingia kwenye historia nyingine katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaendela kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, wananchi wa Mkoa wa Mtwara habari ya mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia tulishasahau na tukajikatia tamaa, kwa sababu kwenye bajeti ya mwaka jana ni kama hatukuiona hivi, lakini kwenye kitabu cha bajeti ya mwaka huu kwa maneno yaliyoandikwa na hotuba ya Mheshimiwa Waziri, wananchi wa Mtwara kwa sababu shughuli ya gesi asilia ilikuwa imelala kwa miaka hii yote, tunaendelea kuwa na matumaini makubwa sana na Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hakika wananchi wa Mtwara na Watanzania wengine wote kule Mtwara mlitukimbilia sana, watu walijenga hoteli, walifungua shughuli mbalimbali za kibiashara lakini baada ya kuona huu mradi kama umekwama waliondoka, kwa hotuba ya leo tunaamini Watanzania watarudi Mtwara kwa sababu nimeuona mradi upo kwenye kitabu na nitakuja kusema mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake yote kwa nia njema. Lakini kipekee nimpongeze kwa usikivu, unyenyekevu na kuchukua hatua. Kwa nini, nitasema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze katika Mkoa wa Mtwara ninapoitumikia nafasi yangu ya uwakilishi. Tunazo changamoto mbili kubwa, ya kwanza ni upatikanaji wa umeme, kwetu sisi imekuwa ni changamoto kubwa sana. Mkoa wa Mtwara, Mheshimiwa Mbunge aliyekaa sasa hivi anasema kwao kunakatika katika umeme, lakini nitamkaribisha aje Mtwara, alikuja kwenye shughuli moja ya kikazi, Mtwara ndiko mahali ambako umeme kwa siku unaweza kukatika mara 30.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunajua nguvu ya umeme na kwa kukatika huko hakuna shughuli za kiuchumi ambazo zinaendelea vizuri, wajasiriamali wadogo wamekuwa wakilalamika, wanaotunza samaki kwenye friji, wanaofanya shughuli za uchomeleaji, yaani wajasiriamali wote ambao wanatumia umeme wamekuwa wakitoa kilio kikubwa sana. Matokeo yake inasimamisha mtiririko ule wa shughuli za kiuchumi kwa sababu mambo yanasimama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitangulia kusema hapa, Mheshimiwa Waziri ametuambia, na kwenye kitabu chake cha hotuba mimi nampongeza kwa sababu ameweka hoja mahsusi kwa Mkoa wa Mtwara, ametujibu kwamba tutasubiria kwa miezi mitatu (siku 90) lakini kwa hatua za awali tumeona na tumemsoma. Ninaamini pia tutaanza kuona hayo matokeo ya kukatika katika kwa umeme mwishoni mwa mwezi Juni, tuna matumaini, tunamwomba Mwenyezi Mungu atuweke mpaka Desemba ili tuone na tuthibitishe kwa vitendo hayo ambayo ameyasema kwenye hotuba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli ukiacha changamoto nyingine, lakini kwetu sisi nishati ya umeme ni changamoto. Tunaamini Serikali ya Chama cha Mapinduzi ni sikivu na kwa kuwa imedhamiria kutuondolea hii changamoto hata yale madai niliyokuwa nayo ya wananchi ya kuunguziwa friji, TV na vitu vingine, ninayaweka nyuma nisubiri suluhisho ambalo limetolewa na Mheshimiwa Waziri na kwamba ninaamini tutakwenda kufika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya pili ni upatikanaji wa umeme vijijini katika Mikoa ambayo vijiji vyake bado havijafikiwa kwa asilimia 50 kwa Mradi wa REA unaoendelea sasa ni Mkoa wa Mtwara. Tunao Wakandarasi wawili NAMES pamoja na Central, mmoja anaendelea vizuri lakini huyu mwingine anasuasua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina shaka kuwa Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi itafanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa na Kamati ya Nishati zikiwemo pia na changamoto ambazo tunakumbana nazo za Mkandarasi wa Mtwara, hili ninaamini kabisa kwamba Mheshimiwa Waziri unalichukua na umelipa kipaumbele na ndiyo maana umeweka mkakati wa muda mfupi na muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tusiendelee kusubiri vile vijiji 200, 300 ambavyo pengine Mkandarasi anasema anavifanyia kazi tukasubiri mpaka Desemba; tunaamini deadline ni Desemba lakini basi tuanze kuona hayo matokeo, ikishindikana hakuna mtu ambaye yuko juu ya sheria, yaani suluhisho litakuwepo tu. Waitwe watu wengine waje kufanya kazi ambayo mkandarasi ameshindwa ili na sisi kwenye hivi vijiji, mnajua Mtwara tuna ardhi kubwa, tuna msitu mnene, tupate umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua kule kwetu, hasa maeneo ya Newala, ukiona mahali kunawaka taa wanasema kwa Ali Ma-solar, yaani ni kwamba tumezoea kwenda dukani kununua ile panel ndogo na kuweka kwa sababu umeme bado haujafika vijijini. Hizo ndizo changamoto kubwa ambazo tukitatuliwa na Serikali kama ambavyo Mheshimiwa Waziri ametuahidi, tutakwenda kupona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshukuru sana, kwa mara ya kwanza najaribu namna ya kurudisha sauti yangu, ninaishukuru Serikali na ndiyo maana nilimpongeza Mheshimiwa Waziri, nimeona maeneo kadhaa ambayo Mkoa wa Mtwara umetajwa. Kwanza ni huu mradi wa kuzalisha umeme kwa kutumia gesi asilia wa megawati 300 kutoka Mtwara, na wote tunajua. Ndiyo maana Mtwara kwa maana ya gesi ya Madimba iko kwenye chanzo kimoja wapo cha umeme katika nchi hii. Sasa lililonipa faraja ni kwamba Serikali itaanza kulipa fidia kwa wananchi watakaopisha eneo la ujenzi wa kituo na mipaka ya Mkuza kuanzia Mtwara kwenda Somanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba muanze sasa, ukimaliza bajeti hamia kule Mzee, ukaanze kuwaambia wananchi wa Mkoa wa Mtwara namna ambavyo huo utaratibu mzima wa kulipa fidia na kwenye maeneo yote ambayo tunaweza tukanufaika ili kuepusha ile migogoro wanasiasa tutakaporudi kule tuambiwe mbona hakuna kitu. Kwa hiyo, ukitangulia utakuwa umeturahisishia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni mradi wa kuchakata na kusindika gesi asilia (LNG). Hapa niseme kwa dhati ya moyo wangu kwamba, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, amerejesha matumaini ya Wanamtwara kwa asilimia 100. Hii gesi ambayo huko nyuma ilituletea vilio na kutupatia misiba, lakini sasa Mama tunasema ahsante kwa sababu tunajua kurejeshwa kwa huu mradi kwetu utakuwa ni furaha na matumaini ya pekee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo tunajua sasa hata zile Wizara nyingine ile Miji ya satellite ambayo tulikuwa tunaiona itakwenda kutekelezwa, Mheshimiwa Waziri wale watu wa Madimba na maeneo yanayotoka kule nendeni mkaone namna ambavyo mtawatia moyo hata kabla hamjafika hatua ya mbali kwa kuboresha shughuli zao za kijamii, shule, vituo vya afya, zahanati na nyumba zao pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo nilipata nafasi ya kwenda kwenye nchi ambayo inazalisha gesi wanaiita Trinidad and Tobago tuliona. Tunatamani kuona manufaa kama ya nchi hizo ambazo wamekuwa wakizalisha gesi kwenye maeneo yao, mabadiliko yale ya haraka ya kimaendeleo tunayapata na kule kwetu Mtwara kwenye maeneo ambayo gesi inatoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kuna eneo la kwenda kuwaelimisha wananchi na hapa tumeambiwa jitihada mahsusi itawekwa katika Mkoa wa Mtwara. Mheshimiwa Waziri mimi naona kama utakuwa unachelewa, kwamba tusubiri mpaka Julai 01, lakini naomba wakati unapokwenda kufanya hili litakuwa kwetu la heshima sana kwa sababu wananchi wa Mkoa wa Mtwara sasa wataelimishwa namna ambavyo wao watashiriki na kunufaika na huu mradi ili sasa tusiwe wasikilizaji na ndugu watazamaji. Tunataka sisi tushiriki kikamilifu ili tuweze kwenda pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine la mradi ambalo kwenye kitabu cha hotuba nimeona linalotupa faraja ni usambazaji wa gesi asilia ambao unatekelezwa na TPDC ambao sasa umefika asilimia 60 na utakamilika Juni, 2023. Hapa tumeambiwa kwa kuanzia Mkoa wa Mtwara ndiyo umeanza na nyumba 209 zitakuwa zimefikiwa. Tunakusihi sasa ukiweka tu kwenye nyumba hizi 209 lakini tunajua Mtwara ina Wilaya zake Tano za Serikali na za Kichama Sita na huko hatujawahi kuwa na viwanda hata vidogo kwa kutokuwa na umeme wa uhakika, tusipopata hii miradi ya gesi kwenye taasisi za umma kama vile shule, hospitali, vituo vya afya na kwingine kote kunakohitaji, bado kwetu manufaa tutachelewa sana kuyafikia, ninakusihi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, waliosoma zamani kama jirani yangu hapa, kwenye shule zao za sekondari walikuwa wanapika kwa gesi. Hivyo, kwa nini sasa hivi wananchi wakakate marundo ya kuni kule. JKT, Shule za Sekondari, Shule za Msingi, Vituo vya Afya, Magereza na maeneo mengine. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Agnes.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza kwa kuwa nami ni Mjumbe wa Kamati, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza na hoja ambazo pengine watu wamekuwa wakijiuliza, maana ukisikiliza nje ya sisi Wabunge, wapo baadhi ya wananchi katika makundi mbalimbali wanahoji pia kwamba kwa nini Waheshimiwa Wabunge hawa wawili ambao ni mashahidi walitokea mbele ya Kamati ama waliitwa kwenye Kamati yako ya Bunge?

Mheshimiwa Spika, naomba niliweke wazi hili kwa sababu pengine hawajui kwamba mashauri haya yote mawili yameshughulikiwa chini ya Sheria ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge Sura ya 296. Kwa hiyo, siyo suala tu kwamba labda mhimili huu wa Bunge uliamua tu wenyewe bila kufuata sheria; ni kwamba ni suala la kisheria. Pia niwaambie wale ambao pengine wamepata mashaka kwamba masuala haya yote mawili yameshughulikiwa kwa mujibu wa Kanuni za Bunge. Bunge lako Tukufu linaendesha shughuli zake kwa kufuata Kanuni za Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba nilieleze hili kwa sababu baadhi huko ukisilikiliza wanasema wameonewa, mtu kwa nini ameitwa? Kwa nini hakwenda huku? Kwa nini huku? Pengine wanadhani ni shinikizo la mtu mmoja, lakini kumbe huu ni utaratibu wa kibunge. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mashauri haya yote mawili kama ambavyo Mwenyekiti wa Kamati amewasilisha mbele ya Bunge lako Tukufu, yote yameangukia katika Kanuni ya 85 - Utovu wa Nidhamu Uliokithiri.

Mheshimwia Spika, hapa pia naomba nianze na shauri lile la kwanza la Msheshimiwa Josephat Gwajima. Sote tunatambua kwamba Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imetoa uhuru wa kuabudu, lakini uhuru huo wa kuabudu tunaopewa Watanzania na watu kuanzisha taasisi za kidini hupaswi kuvunja masharti ambayo Katiba hiyo imeweka na sheria nyingine za nchi yetu. Tunajua sote kwamba hakuna uhuru usio na mipaka; yaani haiwezekani mimi leo; na kwa sababu kuanzisha Kanisa au taasisi ya kidini mtu yeyote anaruhusiwa; haiwezekani leo nikatoa maneno ambayo yanavunja sheria nyingine za nchi tu kwa kisingizio cha uhuru wa kuabudu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa maneno ambayo yalisemwa na shahidi hayana shaka. Naomba niungane na Wabunge ambao wametangulia kwamba maneno yale yanaweza kuvunja amani na utulivu wa nchi yetu. Sasa tukiachia hiyo tukasema sasa kila mtu aamke tu, sidhani kama tunaweza tukaendelea kufurahia nchi yetu katika uwanda huu mpana wa utulivu ambao unamwezesha kila Mtanzania kufanya shughuli zake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge King hapo amesema, ukiacha ile mifano ya Kibwetere, tuliona pia kwenye maeneo mbalimbali; nakumbuka kama sikosei kule Kagera kuna mchungaji alitokea Kanisani akasema ameoteshwa aoe mke wa mwingine Kanisani, lakini tuliona Serikali pia ambaye ni Mkuu wa Wilaya alienda akachukua hatua kuhusiana na lile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia yapo maeneo mengine. Kwa hiyo, kwa ufupi tu tuseme kwamba hili pia ambalo limefanywa na Mheshimiwa Gwajima kwa kisingizio kwamba alikuwa anasema yale maneno akiwa anahubiri waumini wake kwenye nchi 142; na kwa kuwa alikiri Tanzania ni miongoni mwa hizo nchi 142; kwa kufanya hivyo kwa kweli sioni kama kuna shaka kwamba alikuwa anajaribu kuizua Serikali kutekeleza wajibu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwasihi Wabunge kuliunga mkono Azimio hili la Bunge ili kuendelea kuulinda utulivu wa nchi yetu, kuilinda amani ya nchi yetu na pia kuleta ustawi wa jamii zetu. Hii chanjo ambayo pengine watu wanahimizwa wasiende kuchanja, tuliambiwa wote ni kwa hiari, lakini pia mashaka yale mengine ambayo yametolewa na mzungumzaji yanaendelea kuwachanganya wananchi. Kwa sababu akisema daktari yeyote atakayebisha amepewa pesa, sasa tunaendelea kuwachanga wananchi. Kwamba hawa hawa Wabunge wanasema hii chanjo isichanjwe kwa sababu hakuna nafasi ambapo Mbunge anapofanya shughuli nyingine nje ya Bunge utasema sasa mimi Agness Hokororo sio Mbunge, nafanya kazi zangu kama mwananchi wa kawaida kwa sababu wote tumekula kiapo kwa mujibu wa Katiba.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana, ahsante Mheshimiwa.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono hoja.
Hoja ya Kuazimia Kuwahamisha Maafisa Ushirika katika Tume ya Maendeleo ya Ushirika na Maafisa Ugani chini ya Wizara ya Kilimo
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza nianze kusema kwamba siungi mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge wenzangu Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ibara ya 145 na ibara ya 146 kwa ruhusa yako sijui nirejee ama muda hautoshi? Muda hautoshi, lakini Serikali za Mitaa imeandikwa kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hatuwezi kurekebisha kwa mtindo huo. Kama kuna udhaifu wa Sheria Na. 6 ya Vyama vya Ushirika ya Mwaka 2013, sehemu ya kuyafanyia marekebisho ni kuileta hiyo Sheria irekebishwe lakini siyo kwa kunyofoa vipande kwa vipande. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maelezo ya mtoa hoja yamejieleza vizuri sana kwamba Mrajisi Msaidizi wa Ushirika wa Mkoa kwa sasa ni sehemu ya TAMISEMI, halikadhalika Maafisa Ushirika waliopo kwenye halmashauri zetu ni TAMISEMI. Tatizo liko wapi? Usimamizi unawezekana, warajisi wasaidizi wa mkoa ni sehemu ya TAMISEMI, wawasimamie vizuri hao Maafisa Ushirika kutoka kwenye halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiniuliza, iko changamoto kubwa ambapo upungufu uko kwenye hiyo Sheria Na. 6 iliyoanzisha vyama vya ushirika ya 2013 iletwe Bungeni, tuifanyie marekebisho ili warajisi waweze kufanya kazi yao vizuri na Maafisa Ushirika na Maafisa Ugani kwenye ngazi za vijiji na kata waweze kufanya kazi zao. Hatuwezi kuacha wazururaji wasimamiwe na Tume ya Ushirika kutoka Makao Makuu, kwenye Tawala za Mikoa hakuna, kwenye Halmashauri Mkurugenzi hawajui, Madiwani hatuwajui, watakuwa wanafanya kazi za nani? Ugatuaji (D by D) lazima iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)

MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Spika, taarifa.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nampongeza Mheshimiwa Waziri, kaka yangu, Mheshimiwa Aweso na nina matumaini makubwa kwamba atafanya vizuri kwa sababu naye hakutoka Oysterbay wala Masaki na anajua taabu na shida za mama zake kule vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sina mashaka pia na Naibu wake, Mheshimiwa Eng. Maryprisca, kwa sababu ni mama. Kwa hiyo, hata Mheshimiwa Rais anapohimiza suala la kumtua mama ndoo, yeye ni mama. Kwa hiyo, wote kwa kweli tuna matumaini na ninyi na tunawaombea kwa Mwenyezi Mungu mwendelee kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru pia kwenye bajeti hii nimeona kuna miradi 84 na hiyo ni usanifu, ukarabati, uchimbaji wa visima katika Mkoa wa Mtwara, lakini naomba nijielekeze kwenye utekelezaji wa bajeti iliyopita 2020/2021. Kama ambavyo imeonekana kwenye hotuba ya bajeti ya Mheshimiwa Waziri, utekelezaji wake ni asilimia 54 tu. Mkoa wa Mtwara kulipangwa shilingi bilioni 21 na zikapatikana ama zilizotumika ni shilingi bilioni sita tu, sawa na asilimia 39. Kwa hiyo, hapa changamoto kubwa ni suala la upatikanaji wa fedha kwa ajili ya utekelezaji, ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe ushauri kwenye hili eneo. Kwa sababu kwa sasa Mfuko wa Maji ambao ndiyo Wabunge wote wanautegemea na kila mmoja hapa kwenye eneo lake ana changamoto ya maji na fedha zile ambazo zinapelekwa ni shilingi 50/= ya mafuta, mimi naamini Waheshimiwa Wabunge kwa sababu tunaona bado kuna kadhia kubwa ya uhitaji wa maji, pengine mfuko huu uongezewe uwezo. Kama kwa bajeti ya mwaka 2020 iliweza kutekelezeka kwa asilimia 54, hatutegemei miujiza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba mwaka huu zimetengwa shilingi bilioni 680 lakini kwa utaratibu huo huo kama fedha haitakwenda yote hatutegemei Mheshimiwa Aweso na wenzake kwamba watafanya miujiza kwa sababu hiyo iko kwenye imani zetu za kidini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto ya uwekezaji mdogo katika ujenzi na uboreshaji wa miundombinu unachangiwa na ukosefu wa fedha. Kwa hiyo, nadhani iko haja ya kuangalia vyanzo vingine ili sasa hili suala la maji litekelezeke kwa kipindi kifupi na Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuongea habari nyingine.

Mheshimiwa Spika, nijielekeze katika Mkoa wa Mtwara. Kama ambavyo nimetangulia kusema, kwamba upatikanaji wa fedha pia ndiyo ilikuwa changamoto, sisi wananchi wa Mkoa wa Mtwara, nikisema hapa habari ya kuokota, dada yangu, Mheshimiwa Tunza amesema, hamtuelewi. Maana yake, kwenye vile vyanzo vitatu vya chini ya ardhi na juu ya ardhi, sisi tunatumia kwa kiasi kikubwa maji yale mvua inaponyesha, iwe ni nyumba ya nyasi yale maji meusi au yale yanayotiririka juu ya ardhi, tunayakinga kwenye mashimo halafu wenye uwezo wanaweka shabu, tusio na uwezo tunayanywa vilevile. Ndiyo maana ya maji ya kuokota kaka yangu, Mheshimiwa Waziri Aweso. Hiyo inatusababisha kutumia pia fedha nyingi kwenye matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana, hii changamoto ya maji ya Mkoa wa Mtwara kwenye Wilaya za Tandahimba, Newala, Mtwara Vijijini, Masasi, Nanyumbu ndiyo mara 200, haitaweza kuondoka kama Serikali haitakuwa na dhamira ya dhati ya kuanza kutekeleza Mradi wa Maji wa Mto Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeona huku kwenye bajeti iko ile shilingi bilioni sita, Mto Ruvuma kupeleka Manispaa ya Mtwara Mikindani na vijiji vya jirani, vijiji 73 vya Jimbo la Nanyamba au Mtwara Vijijini, lakini bado kule Nanyumbu, Newala, Tandahimba, Masasi, Majimbo ya Lulindi na Ndanda kuna adha kubwa. Kila siku mama analazimika kwenda mtoni. Kama mto utakuwa umekauka, basi tufukue kisima tuweze kuchota maji. Hata ukiona hata rangi ya yale maji hutakunywa. Hutaweza, nina uhakika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaishauri Serikali ianze kutekeleza Mradi wa Maji wa Mto Ruvuma. Wenzetu tunasikia; maji ya Ziwa Victoria, maji sijui ya nini, sisi chanzo cha uhakika tulichokuwa nacho ni Mto Ruvuma. Pamoja kwamba kuna mto wa pili ambao haukaushi maji, Mto Lukuledi, lakini bado pia huo utasaidia kwenye maeneo machache. Ili tunufaike wananchi wote wa Mkoa wa Mtwara, ni muhimu sana kuona mradi wa chanzo cha Mto Ruvuma unatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Mtwara una vijiji 809. Kwa sasa vijiji 450 ndiyo vinapata maji na siyo saa zote, yaani 450 ndiyo vinapata maji. Ndiyo hayo sasa ya mdundiko, ama ya kuchota angalau. Vijiji 359 havipati maji. Kwa hiyo, wakati Ilani inasema itakapofika 2025 vijijini ni asilimia 85, sisi hiyo ni ndoto, kwa sababu kwa sasa kwa upande wa vijijini ni asilimia hiyo ambayo tunasema ndiyo ya wataalam, inawezekana 58 au 59, hatuwezi tukafanya maajabu kwenye hii miaka mitano tukafika kwenye hiyo asilimia 85.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana ukiniuliza kipaumbele cha kwanza kwa Mkoa wa Mtwara, ni maji; cha pili, changamoto ni maji; cha tatu changamoto ni maji. Tunaiomba sana Serikali yetu sikivu ya Chama cha Mapinduzi ijielekeze kwenye hilo eneo ili nasi tutuliwe ndoo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwanza kwakunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyopo mezani kwanza nianze kwa kuunga hoja zote tatu mkono.

Mheshimiwa Spika, vilevile nimshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo anaendelea kututumikia Watanzania na tunaridhika na kazi nzuri anayoifanya. Vilevile nitakuwa mchoyo wa fadhira nisipokushukuru na kukupongeza wewe kwa umakini, unaona kabisa kwamba kazi ya kuisimania Serikali kwa siku hizi mbili, tatu ukitoka nje ya Bunge lako hili wananchi wanaifurahia ni kwa sababu unatuelekeza vyema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nichangie kwenye hoja Mahsusi ya Hesabu za Serikali za Mitaa, Mimi ni Mjumbe wa Kamati. Taarifa ya CAG inaonyesha dhahiri kwamba dosari zote za matumizi mabaya ya fedha za Serikali yanatokana na mambo matatu:

(i) Kutokuzingatiwa kwa Sheria ya Fedha za Umma;

(ii) Kutokuzingatiwa kwa Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa; tunaijua wote Sheria Na. 9 Sura ya 283 ya Mwaka 1982 na marekebisho yake;

(iii) Kutokuzingatiwa kwa Sheria ya Manunuzi ya Umma. Hapo ndiyo msingi wa mambo yote ambayo Wabunge wako hapa wamekuwa wakiyachangia katika nyakati tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa najiuliza, hivyo sasa kama Bunge lako linakaa hapa tunatunga Sheria nikawa najiuliza inawezekana kwa sababu siyo Mwanasheria lakini wewe ni mbobevu kwenye hili eneo, hizo Sheria tunazozitunga kwenye Bunge lako Tukufu hili hazitoi adhabu? Sheria zinapaswa kusimamiwa na tunajua asiyetekeleza jambo lolote kwa mujibu wa Sheria husika, kwa maana anayevunja hiyo Sheria anapaswa kuchukuliwa hatua za kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa maeneo ambayo yanaonekana hayaridhishi naomba tu niseme mifano michache. Kwenye taarifa ya CAG imeonekana matumizi ya fedha mbichi, fedha ambazo hazikupelekwa benki kiasi cha Shilingi Billion 17 ambazo hizo ni kwa Mamlaka 147 tu, kwa maana POS zimekusanya lakini hizi fedha zimetumika mbichi. Jambo la kusikitisha siyo kwamba zimetumika kwa shughuli za maendeleo, hazijulikani!

Mheshimiwa Spika, hiyo imethibishwa na baadhi ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa zilizotokea mbele ya Kamati. Eneo lingine ni Matumizi ya Fedha za akaunti ya Amana. Akaunti ya Amana siyo akaunti ya matumizi kwa Halmashauri za Wilaya lakini inaonekana Jumla ya Shilingi Billion 9.74 kwa Halmashauri 81 haya matumizi yake hayakusimamiwa. Inasikitisha, Mkurugenzi mmoja wapo kwenye Kamati alipoulizwa kwa nini ulitumia fedha zilizopo kwenye akaunti ya Amana zaidi ya Million 95? Alijibu kwa jibu ambalo linasikitisha bila kuogopa akasema hizo fedha za Akaunti ya Amana hazina rangi kwani fedha zina rangi? Maana yake nini? Maana yake Maafisa Masuuli hawana uwoga na fedha za umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine limetajwa sana, hivyo wakati Watanzania wengi wanalalamika kwamba hakuna dawa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya. Ukiangaria ripoti ya CAG kwa miaka mitatu mfulilizo jumla yake ni Billion 12.362, dawa ambazo zimekwisha muda wake kwa kipindi cha Miezi Mitatu mpaka miaka 20, madhara yake dawa hizi pia zikiingia kwa watumishi wasio waadilifu Watanzania tutapata madhara. Hata hivyo taarifa ya CAG inasema anaona mapendekezo yake aliyotoa kwa miaka mitatu mfululizo hayajafanyiwa kazi. Je, Bunge napo linapofanya kazi yake ya kuisimamia Serikali bado yasifanyiwe kazi? Hayo ndiyo maswali ya kujiuliza.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika ile Sheria ya Manunuzi malipo ya bidhaa za huduma ambazo hazikupokelewa Billion 8.44 kwa Halmashauri 61. Ununuzi wa bidhaa zenye thamani ya Shilingi Billion 7.93 kwa Halmashauri 42, pamoja na hasara zinazopelekewa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa kutoka kwa baadhi ya Taasisi za Serikali kama vile Mfuko wa Bima ya Afya, MSD, GPSA, TEMESA na zinginezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Tanzania kwenye maeneo mbalimbali kwa sasa wanalitegemea Bunge lako Tukufu. Wabunge wanafanya kazi yao ya kuisimamia Serikali, hivyo ninaungana na mapendekezo yaliyotolewa kwenye Kamati lakini na Wabunge kwamba ni wakati sasa wa kuhakikisha hatua za kisheria zinachukuliwa dhidi ya wale wote wanavunja Sheria. Haiwezekani, kwanini tukae hapa Bunge litunge Sheria, lakini Sheria zinapaswa kusimamiwa, lakini ziwe zinavunjwa halafu hakuna hatua zinazochukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zile Halmashauri chache tu ambazo zilitokea mbele ya Kamati inaonyesha kwamba ukiharibu Halmashauri ‘A’ unahamishiwa Halmashauri ‘B’. Ukiharibu Halmashauri ‘B’ unahamishiwa Halmashauri ‘D’, sasa huo utaratibu huo ndiyo unazozifanya Mamlaka za Serikali za Mitaa kuendelea kutokufanya vizuri, ni kwanini? Kwa sababu hawana woga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa je, tutaendelea kwa utaratibu huu halafu tutasema tunamsaidia Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania? Hapana, inatosha! Kwa sababu, CAG ameonesha mapungufu hayo yote, na sisi tunayatambua hayo maeneo; jukumu letu hapa kwa kamati hizi na kwa taarifa hizi kwa kipindi hiki ni kuisimamia Serikali. Kwa hiyo, mimi nadhani naomba nisisitizwe, kwamba hoja za Wabunge walizosema, kwamba sasa Bunge liazimie katika eneo lolote ambapo sheria ilivunjwa hatua stahiki zichukuliwe. Kwa utaratibu gani, Bunge liielekeze Serikali kwa sababu, lina wajibu wa kuisimamia. Hiyo itatuepusha sisi kurudi hapa kuja kusema kila mwaka tunarejea kwenye hoja zilezile ambazo kimsingi hazionekani kurekebishika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kwa mifano hiyo unaona namna ambavyo Serikali inapata hasara. Sasa kumbe kwenye maeneo hayo yote iwapo usimamizi huo ungekuwa thabiti ina maana tungeweza kuikoa fedha ya Watanzania. Fedha hizi zingeweza kutoa huduma katika maeneo yetu mbalimbali tunayotoka na hivyo Watanzania pia wangeweza kuwa na amani.

Mheshimiwa Spika, lakini ukiangalia haya mapungufu ndiyo yanayowagonganisha wananchi na Serikali. Sasa mtu mmoja anapoamua kufanya hili huyo yeye achukuliwe hatua stahiki ili Serikali iwe salama kwa wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na sasa ukiangalia mapendekezo ya CAG, ambapo kwenye maeneo mengi sana wajumbe wamesema, anashauri, anashauri; lakini kwenye maeneo mengine amebainisha kwamba mapendekezo anayatoa hayafanyiwi kazi. Tujiulize kuna nini? Hivi si kweli kwamba kuna eneo labda wale wanaofanya pengine kuna, mimi sijajua, lakini pengine kama Bunge tutafakari, kuna nini? Kwamba CAG anapotoa pendekezo, anaposhauri halifanyiwi kazi, mtu anahamishwa kutoka Point A kwenda Point B akaendelee kuharibu; kuna nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa wengine wanaweza wakatoa majibu ya haraka tu, hayo hayahitaji chuo kikuu. Mwingine atasema labda kuna kulindana, mwingine atasema labda sijui ni nini, labda ni mtoto wa fulani.

Mheshimiwa Spika, sasa sisi hapa Wabunge ni wawakilishi wa wananchi. Sisi hatuna cha mtoto wa shangazi, hatuna cha mtoto wa mjomba, sheria ifuate mkondo wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaunga mkono hoja nikiamini kwamba hayo yote yatafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, lakini kabla sijamaliza, yale mapungufu yote kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa, kuna Sekretarieti ya Mkoa pale. Mimi ninaomba niwashawishi Wabunge moja ya azimio liwe Serikali ifanye tathmini ya kina nini kazi inafanywa na Sekretarieti za Mikoa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu, wakuu wa section wapo hapo, inakuwaje mpaka mwaka unaisha ndipo kunaonekana madudu mpaka CAG anaenda kufuatilia, wakuu wa section wapo? Wanasubiri Mkuu wa Mkoa aende kwenye ziara? Wanasubiri Waziri aende kwenye ziara? Wana jukumu gani pale? hilo ni suala la kufanyiwa tathmini ya kina. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naamini wote tunatambua kwamba afya ni sehemu muhimu ya kuimarisha mtaji watu hasa katika kuendana na sera yetu ya uchumi wa viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianzie kwenye upatikanaji wa dawa. Kama ambavyo Mheshimiwa Noah amechangia na katika bajeti hii imeonekana ni asilimia 26.6 tu ndio iliyopokelewa kwa bajeti ya mwaka uliopita 2021. Hata hivyo, kinachokwamisha zaidi ukiacha ule utaratibu ambao ni wa ununuzi wa madawa kupitia MSD wa dawa nyingi yaani bulk procurement inaonesha pia kwenye vituo vya kutolea huduma ya afya utaratibu wa manunuzi ndio hasa umekuwa kikwazo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika vituo vya afya ama zahanati ambapo wakati mwingine wanakuwa na fedha, lakini katika utaratibu wa manunuzi inaweza ikachukua miezi miwili mpaka mitatu huku wananchi wanaendelea kuumia. Ikikupendeza katika Bunge lako hili Tukufu inawezekana kufanyike utaratibu wa kubadilisha hata sehemu ndogo ya Sheria ya Manunuzi ili kuwaokoa wananchi wengi wanaosubiria dawa wakati kwenye vituo vya kutolea huduma ya afya hiyo ingewezekana, sio kwa kusubiri huo utaratibu wa miezi miwili mpaka mitatu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze katika Mkoa wa Mtwara. Kama ambavyo taarifa imeonesha katika hotuba ya bajeti kwamba Kamati imebainisha wazi upatikanaji wa fedha katika bajeti iliyopita ndio ilikuwa kwa kiwango si cha kuridhisha, lakini natambua kabisa kwamba kwa bajeti ya mwaka huu 2021/2022, bajeti ya Wizara ya Afya imeongezeka kwa asilimia 31 na ongezeko kubwa limeonekana katika miradi ya maendeleo. Naiomba sana Serikali yetu sikivu ijielekeze pia katika kukamilisha ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mtwara ambayo ni hospitali ya kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hospitali hii ikikamilika itawanufaisha wananchi wa Mkoa wa Mtwara, Mkoa wa Ruvuma, Mkoa wa Lindi, lakini pia hata nchi jirani ya Msumbiji. Kwa sasa katika Mikoa hii ya kusini wananchi wote wanakwenda kufuata matibabu ya ngazi ya rufaa katika Hospitali ya Muhimbili, lakini Serikali ikikamilisha ujenzi wa Hospitali ya Rufaa inayojengwa pale Mtwara Mitengo ina maana hata mzigo ule wa Muhimbili utapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kwamba yale yaliyoelekezwa kwenye Ilani ya Uchaguzi 2020 - 2025 inawezekana ikatekelezwa na iwapo Wizara itahakikisha hili inalitekeleza. Kwa sasa ujenzi wa hospitali hii umefikia asilimia 40, kwa hii miaka mitano naomba sana, kwa yale majengo tisa yaliyoanza ambayo kwa sasa kwa kweli inaonekana lakini haitawezekana kutoa huduma kama haitakamillishwa kama ilivyoelekezwa na Ilani ya chama changu Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Mtwara vituo vya kutolea huduma ya afya vipo 251 na katika hivyo tunazo zahanati 227 sawa na asilimia 22 tu, bado tupo chini na mahitaji ya zahanati yalitakiwa 985, lakini hadi sasa tunao ujenzi wa zahanati 28 ambao wananchi na halmashauri wamejitahidi. Naiomba Serikali ijitahidi kukamilisha haya maboma ili angalau haya 28 yakaongeze ile 227 na wananchi kwenye maeneo mbalimbali waweze kupata huduma ikiwemo kule Lukuledi, ule ujenzi wa zahanati na ikiwezekana iwe kituo cha Afya Chiroro na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara hii. Kwanza niungane na mzungumzaji aliyetangulia, Mheshimiwa Ungele kusisitiza barabara ya Masasi – Nachingwea ambayo ndio pia inakwenda mpaka Liwale.

Mheshimiwa Naibu Spika, mara nyingine huwa hatueleweki, lakini pia nina maswali madogo ambayo ninajiuliza na pengine Mheshimiwa Waziri atakapokuja kutoa ufafanuzi atuambie. Sera ya barabara inasema ni lazima kuunganisha mkoa kwa mkoa, hivyo watuambie wameunganisha kwa kiwango cha lami Mkoa wa Mtwara na Lindi kutoka Liwale – Nachingwea na Masasi Lami imepita hewa gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu wakati mwingine hata tunajichanganya wenyewe, kama Serikali hii hii inasema masuala ya uwezeshaji wananchi kiuchumi, moja ya kigezo ambacho kinapaswa kuzingatiwa ni uimarishaji wa miundombinu ikiwemo barabara. Sasa maeneo ambayo yanatoka mazao ya korosho, huko Nachingwea, huko Liwale ambayo inapaswa sasa kuja kusafirishwa huku Bandari ya Mtwara na kipande cha Masasi – Nachingwea ni kilometa 45 tu. Nimepata bahati ya kusikia ahadi za viongozi, lakini pia kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi tangu mwaka 2010 - 2015 na 2015 – 2020, lakini mpaka sasa barabara hiyo haijaguswa.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Hokororo, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kuchauka.
T A A R I F A

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, Nataka nimpe taarifa mzungumzaji. Barabara ya Nachingwea – Masasi imefanyiwa upembuzi yakinifu mwaka 2014, lakini mpaka leo bado inatafutwa fedha ya kujenga.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Agnes Hokororo.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea na tena imeniwahi, ahsante sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama upembuzi yakinifu ulikamilika tangu 2014 pamoja na kwamba ahadi ilikuwa ni ya miaka 20 sasa. Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie maana kwenye taarifa yake inasema Serikali inatafuta fedha na ikisema Serikali inatafuta fedha, hilo jambo ni kama halipo. Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI amekwenda Nachingwea, kimsingi hata sasa hivi kama ungenipa nafasi niongozane na Naibu Waziri ama yoyote kwenye Serikali. Ukiwa mjamzito kwenye barabara ile ya Masasi – Nachingwea unapata, sijui nisemeje?

WABUNGE FULANI: Unazaa.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, unazaa kabla ya wakati. Ile barabara nikiongea kwa lugha ya kikwetu si dhani kama nitaeleweka, lakini ni kwamba unakuwa unatingishika kuanzia unapoanza mpaka, hapa wiki iliyopita niliuliza swali, wakasema fedha imetengwa lakini tuendelee kusubiria. Jamani! Mkoa wa Mtwara na Mikoa hii ya Kusini niwakumbushe tu, kwamba ilihusika kikamilifu katika kuziletea ukombozi Nchi za Kusini mwa Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa labda Serikali ama Waziri aje kutuambia, hivi ile barabara haitengezwi kwa sababu kuna vikosi vya majeshi kule? Kwa hiyo wananchi wote waendelee kuishi nao kijeshi! Sasa unasemaje uwezeshaji wananchi kiuchumi, miundombinu haijakamilika, ni kwa miaka 20 iko kwenye ahadi, upembuzi umekamilika, nini kikwazo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wote tunajua kwamba Nchi hii ni kubwa na Serikali ina mzigo mkubwa, lakini iko haja ya kuangalia maeneo ambayo kimsingi yameachwa nyuma kwa muda mrefu. Hawa wananchi sehemu ambayo na nilisema hapa uliponipa nafasi ya swali la nyongeza, sehemu ambayo nauli ilipaswa kuwa shilingi 750 wanalipa shilingi 6,000, huu mzigo unakwenda kwa mwananchi wa kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli Waziri atakapokuja hapa bila kutupa maelezo ya kutosha, mimi siwezi kupiga sarakasi kwa sababu najua, lakini tunakwendaje kwenye bajeti hii bila ya kuwa na matumaini kwamba angalau hicho kipande tutatengenezewa. Kwa sababu hii habari ya kutengenezwa kila mwaka ndio kila siku mvua ikija inaosha, mvua ikija inaosha, lini Serikali itaanza kutekeleza kipande cha kilometa 45 kuunganisha Mkoa wa Lindi na Mtwara? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante nakushukuru kwa kunipa nafasi, kwanza awali ya yote niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri inayoendelea kuifanya na hasa kuwaunganisha watanzania wote wa mjini na vijijini kwenye mtandao wa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa sababu imetambua kwamba umeme ni suala la msingi na wala si la luxury na kwa msingi huo inaendeleza ujenzi wa mradi wa umeme ambao unajulikana kwa jina la Mwalimu Nyerere ambao utazalisha megawatts nyingi na kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamesema mradi huo utatusaidia kwa kiasi kikubwa kuondokana na giza.

Mheshimiwa Spika, lakini Serikali pia inaendeleza mradi wa REA kwa sasa ni mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili ambapo na hiyo inafanyika kwa nia njema ya kuwaunganisha wananchi vijijini wao waweze pia kupata umeme. Natambua juhudi zinazofanywa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi, lakini naomba tu nichangie kwa uchache sana katika Mkoa wa Mtwara ambapo ninawawakilisha wanawake wa Mkoa wa Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwamba katika Mkoa wa Mtwara bado tunavyo vijiji 281 ambavyo havina umeme, lakini natambua pia kwamba ipo jitihada Mheshimiwa Waziri anaifanya ya kuwapelekea vijiji hivi 281 umeme wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa pili, lakini ningeomba tu kwamba kwakuwa vijiji hivi ni vingi pengine wakandarasi wawili wasingetosha na ili pia mradi utekelezeke kwa haraka. Pengine wakandarasi wangeongezeka wangekuwa watatu kama ambavyo tuliahidiwa huko nyuma pengine vijiji hivi 281 vingefikiwa kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, niishukuru sana Serikali, huko nyuma kabla ya mwezi wa 3 Mkoa wa Mtwara ulikuwa na tatizo kubwa la kukatikakatika kwa umeme kwenye wilaya zote sita. Lakini Serikali ilituletea mashine mbili za kuchakata umeme, kila mojawapo ilikuwa na uwezo wa kuchakata megawati 4.3. Ninaishukuru sana Serikali kwa sababu, sasa kwenye wilaya nne umeme umekaa vizuri hauna tatizo kubwa la kukatikakatika. Changamoto imebaki katika Wilaya za Masasi na Nanyumbu, huku kuna tatizo kubwa la kukatika kwa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe ushauri kwa Serikali na kwa kuwa natambua ni Serikali sikivu. Kwa upande wa Masasi, ambako kumekuwa na tatizo kubwa la kukatika kwa umeme kwa sababu tu, umeme wake unaunganishwa kutoka Mkoa wa Ruvuma kule Madaba. Unatoka Madaba unapita Songea, unapita Namtumbo, unapita Tunduru, unakuja Mangaka ndio unakuja Masasi. Lakini pia, kuna njia nyingine inayotoka Mahumbika ambayo iko Mkoa wa Lindi. Kwa hiyo, hizo zote mbili haziwapatii wananchi wa Masasi umeme wa uhakika na hivyo wameendelea kuukosa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashauri, ili kuondoa tatizo hili kwa suluhisho la muda mfupi, Serikali ijenge line mpya kutoka Mahumbika kwenda Masasi na hii itaondoa tatizo la umeme ule wa Masasi kutumika njiani kabla haujafika Masasi. Lakini halikadhalika watu wa Nanyumbu waunganishwe pia kwenye gridi hiyo, ikiwezekana sasa hivi waunganishwe watu wa Nanyumbu kwenye gridi ya Mtwara, ambayo imeimarika itasaidia kuondokana na hilo tatizo. Lakini, pale Masasi tunacho kifaa ambacho wataalam wanajua tunakiita AVR Automatic Voltage Regulator tunacho pale Masasi. Lakini wakati mwingine pengine hakitusaidii kwa sababu, tayari ule umeme unapofika unakuwa umeshapungua nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Serikali kifaa hiki AVR, kiwekwe Tunduru na kiwe kifaa kikubwa kisaidie sasa ule umeme wa Tunduru, lakini pamoja na Nanyumbu na Masasi kwa sasa ambao ndio tunatumia uwe ni umeme wa uhakika. Lakini kwa suluhisho la muda mrefu nilikuwa napendekeza pia, kwa sababu Mtwara tunatambua kuna gesi ambayo tayari imeshaanza kutumika. Kwa suluhisho la muda mrefu kwa Wilaya za Masasi na Nanyumbu ni vyema pia, kungejengwa bomba la gesi kutoka Mahumbika kuja Masasi, ambapo pia wanufaika watakuwa Wilaya za Masasi na Wilaya za Nanyumbu na kuendelea kwa sababu bado tutakuwa tunauhitaji huu umeme kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napendekeza hayo kwasababu, tunatambua kwamba kwa sasa, Serikali inafanya jitihada pia ya kutafuta wawekezaji kwa ajili ya kuweka viwanda mbalimbali katika Mkoa wa Mtwara na hasa Masasi pia, kwa ajili ya kuchakata korosho, mabibo na yale mabibo yaliyokauka ambayo tumependekeza kutengenezwe spirit na viwanda vya mafuta ambapo kuna uhaba wa mafuta ya kula. Tunao ufuta na karanga kule, lakini wawekezaji hawa watakwama kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wamechangia kutokana na kukosa umeme wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni imani yangu umeme ukiimarika kwa Serikali kuweka hayo masuluhisho ambayo nimeyapendekeza, hiyo changamoto itakuwa imeondoka. Na hivyo wawekezaji watavutika kuja kuwekeza katika Mkoa wa Mtwara katika wilaya zote kwa sababu ya uhakika na hivyo kutakuwa na shughuli za uzalishaji mali na wananchi wataondokana pia na umasikini ambao kwa namna moja au nyingine, wanashindwa kujikwamua kutokana na mazingira ambayo kimsingi Serikali yetu sikivu inaweza kuyatibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa sasa tatizo la kukatika kwa umeme lililopo, inapelekea wajasiriamali na wananchi kwa ujumla kuunguza vitu vyao na tunajua sote kwamba, hakuna utaratibu mwananchi mmoja mmoja anapofanya shughuli zake kama labda ana mashine, labda saluni, ama mashine ya kusaga, ama fridge wapo wakinamama wanaotengeneza ice cream, waweze kuuza na shughuli zingine zozote zinazohusisha umeme. Vifaa hivyo vimekuwa vikiungua kwa sababu, umeme unakuja na nguvu kubwa pengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wananchi wanaathirika kwa hiyo, wanapata hasara kubwa, lakini hata wale wafanyabiashara wanaouza hivyo vifaa vya umeme. Kwa sababu, kama wanapewa warrant ina maana kila siku wakiuza wanatakiwa warudishe ama wafidie, wakiuza wafidie. Kwa hiyo, kwa kiasi kikubwa hiyo imekuwa ni changamoto kubwa kwa wajasiriamali, lakini na kwa wafanyabiashara wa Mkoa wa Mtwara, ambapo ninaamini kabisa, Serikali yangu ya Chama Cha Mapinduzi, inaweza ikalitibu hili tatizo kwa njia hiyo ya muda mfupi lakini pia kwa njia hiyo ya muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaamini kabisa umeme huu utakapokuwa umeimarika hata zile changamoto za Kituo cha Afya kama Nagaga na vingine kule Newala vitakuwa pia ambapo hawapati umeme wa kutosha, Newala, Nanyamba, Mtwara Vijijini, Jimbo la Ndanda, Lulindi ambako kumekuwa na tatizo la umeme usiokuwa wa uhakika basi hiyo changamoto itaondoka. Katika Wilaya ya Masasi pale mjini tunavyo vijiji 19 lakini pia, tuna mitaa kadhaa ambayo haijaunganishwa kabisa haina umeme. Ni imani… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa...

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyopo mezani. Awali ya yote nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wetu kipenzi Mama Samia Suluhu Hassan, kwa namna anavyoendelea kuchapa kazi na kuhakikisha maendeleo yanapatikana kila uchao, niwaombe tu tuendelee kumuombea sana Mama yetu Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kupongeza kazi nzuri zinazofanywa na ofisi ya Waziri Mkuu kwenye maeneo mbalimbali, naomba nitoe ushauri kwenye Wizara ya Kazi, Vijana na Watu Wenye Ulemavu, hasa kwenye eneo la vijana.

Mheshimiwa Spika, tukiangalia kwa mwaka wa fedha 2021/2022 fedha ya Mfuko wa Vijana iliyokuwa imetengwa ilitolewa yote Shilingi Bilioni Moja, lakini kwa masikitiko makubwa kwamba fedha hizo ambazo kila mwaka Waheshimiwa Wabunge walivyokuwa wanachangia huku tulikuwa tunasikia kwamba walikuwa wanaomba hizo fedha ziongezwe.

Mheshimiwa Spika, kwa bajeti ya 2020/2021 fedha hizo hazikuwa zimepatikana na mwaka huu ambao tunamalizia sasa Shilingi Bilioni Moja iliyokuwa imetengwa yote ilipatikana lakini matumizi yake kwa vijana ni Shilingi Milioni 205.

Mheshimiwa Spika, lazima kujiuliza na ukiuliza unaambiwa kwamba vijana wa Kitanzania waliokuwa wametengewa fedha Shilingi Bilioni Moja hawakukidhi vigezo vya kuweza kuitumia hiyo Shilingi Bilioni Moja. Sasa hivyo jukumu la kuwawezesha hawa vijana wakatumie fedha Shilingi Bilioni Moja iliyokuwa imetengwa na imepatikana ili waweze kujikwamua kiuchumi ilikuwa ni jukumu la nani?

Mheshimiwa Spika, ni jukumu la Serikali kuwajengea uwezo na hivyo vigezo vilivyokuwa vimewekwa na Serikali ni vigumu kiasi gani kiasi kwamba vijana wa Kitanzania hata wale wahitimu wa elimu ya juu na kati hawawezi kuvikidhi? Nilikuwa nadhani Serikali kupitia Wizara husika inayo sababu ya kuhakikisha kwamba hivyo vigezo vinajulikana lakini na kuweka utaratibu rahisi ili hao vijana waweze kutumia ama kupata hizo fedha ambazo kimsingi mwisho wa bajeti zitabaki na sijui kama hiyo itakuwa imekuwa ni lengo la kutengwa kwa hizo fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa najaribu kuangalia kama jumla ya Shilingi Bilioni Sita imetumika katika program ya kukuza ujuzi kwanini isiwiane na Bilioni Moja iliyokuwa imetengwa kwa vijana ili waweze kujikwamua kiuchumi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi nzuri iliyofanyika ya kutoa mafunzo ya ujuzi na stadi za kazi kwa vyuo 72 na mafunzo ya uzoefu wa kazi kwa wahitimu 2,215 nilikuwa najiuliza fedha hizo zisingeweza kutumika kwa mfano kwa vyuo vya maendeleo ya wananchi, vijana ambao wanahitimu kwenye chuo cha Maendeleo ya Wananchi Masasi, Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Newala pale Kiduni, Chuo cha Maendeleo ya Wananchi pale Mtwara – Mtawanya, ili vijana hawa wanapokuwa wamepata huo ujuzi ambazo wamekwenda kujifunza, wakapata mitaji ambayo itawawezesha kujikwamua kiuchumi, kwa hiyo pengine kuna haja ya kuongeza ama kuweka mipango zaidi ya kuwawezesha vijana kutumia hizo fedha Shilingi 795,000,000 ambayo mpaka sasa haijaweza kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia taarifa ya utafiti wa watu wenye uwezo wa kufanya kazi, imeonekana kwamba Milioni 25.9 ya Watanzania ndio wanauwezo wa kufanya kazi na kati ya hao Vijana ni Milioni 14.2. Hata hivyo, inaonesha ukosefu wa ajira kwa vijana ni takribani asilimia 12.2, hasa nikawa najiuliza hivyo kweli kama vijana asilimia hii 12 wenye umri wa miaka 15 mpaka 35 tunaamini wengi wao watakuwa wameshamaliza vyuo vikuu na vyuo vya kati, kwanini hii Bilioni Moja isiishe yote, ikawapatia ajira wakaweza kujiajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Je, Maafisa Vijana tulionao kwenye Serikali za Mitaa kwenye ngazi ya Mikoa na Wilaya wanatimiza wajibu wao kuhakikisha hizo fedha zinatumika na vijana wanaweza kujiajiri?

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nadhani hapo kuna kazi ya kufanya ili tuweze kimsingi kuwawezesha vijana kiuchumi na hatimaye suala la uwezeshaji wananchi kiuchumi liweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili nichangie kwenye eneo langu Mkoa wa Mtwara. Nilikuwa naangalia kwamba tunapoelekea sasa hivi tunaanza kuandaa mashamba yetu ya Korosho, lakini changamoto kubwa pamoja na mambo mengine ni ukosefu ama uhaba wa vifungashio kwenye zao la Korosho hasa magunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba kwa vile tunajua Watanzania wote tunategemea kilimo na wananchi wa Mkoa wa Mtwara tunajitahidi kupambana katika kuhakikisha kwamba hicho kilimo cha Korosho kinatukwamua na umaskini, sasa hii changamoto ya mifuko ambayo kimsingi inaonekana kama haijapata tiba kwamba kila inapofika msimu kila mwaka kunakuwa na changamoto ya magunia. Je, hatuwezi tukapanga kabla, hatuwezi tukafanya maoteo ya kupata hayo magunia ili kuondokana na hivyo changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa na hiyo ingewezekana kama tungeweza kutumia viwanda vya ndani, kama kuna hiyo Mikao ambayo inalimwa zao la kimkakati Mkonge tunashindwaje kupata magunia ya kufungasha korosho na hivyo kupelekea Korosho kurundikwa chini na kukosa ubora kila msimu tunapokuwa tumevuna hizo korosho, ni imani yangu kwa mwaka huu na kwa vile Waziri wa Kilimo anafanyakazi vizuri ni imani yangu kabisa kwamba hiyo changamoto haitatokea tutakapokwenda kwenye msimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niongeze pia na Mnyororo wa thamani tunaposema kwamba korosho lazima ibanguliwe ili bei yake iweze kupanda sasa hata vile viwanda ambavyo tumekuwa tukivilalamika kwamba viboreshwe na vile vilivyokufa vihuishwe, mpaka sasa hivi hatujaona hata kiwanda kimoja ambacho katika Mkoa wa Mtwara kilikuwa kimekufa kimeanza kuboreshwa, sasa huu mnyororo wa thamani hatutaweza kuufanya wala kufikia, kwa hiyo ninaiomba Serikali, naamini Serikali yangu ni sikivu sana.

Mheshimiwa Spika, sasa tunapokwenda katika bajeti ya mwaka huu Mheshimiwa Waziri Mkuu na unajua kabisa namna ambavyo wananchi wa Ruangwa Mkoa wa Lindi na Mtwara hatuna zao lingine zao letu sisi ni korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiimarisha kwenye eneo hili tunauhakika nyumba hizo za nyasi, sijui na nini, wananchi wote watakuwa wanaishi kwenye makazi ya kisasa na tutakuwa pia tuna uwezo wa kuhakikisha kwamba tumejikwamua na tupo kwenye maisha bora na salama.

Mheshimwia Spika, nakushukuru naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja iliyoko mezani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza na kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kauli mbiu yake ya kumtua mama ndoo. Wote tunatambua imeitikiwa sana na inafanya vizuri. Lengo la mama lilikuwa ni kuhakikisha kwamba kila mama anayetafuta maji ayapate ndani ya mita 200 na ndio maana umeona wabunge wengi hapa wanasimama kupongeza. Kwa hiyo tunamshukuru sana Mheshimiwa wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pili nimpongeze Mheshimiwa Waziri Aweso pamoja na timu yake yote bila kumsahau Mheshimiwa Engineer Naibu Waziri pamoja na timu yote kama ambavyo wanafanya kazi. Kimsingi wameonyesha nia thabiti ya kupata majibu ya changamoto ya uhaba na upungufu wa maji safi na salama; kama sehemu yao ya kazi ninawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Waziri. Kuna wakati kule Mtwara uwa hakukaliki kabisa na sauti zilipaswa kwa kiasi kikubwa. Mheshimiwa Katani jana alisema, Mheshimiwa Waziri alikuja na alijionea hali halisi mimi hapa ndani kila ninaposimama ninakuwa nikiuliza maswali ya maji ya kuokota; na nilitamani sana Mheshimiwa Wiziri ama waziri mdogo Naibu Waziri wangekuja kujionea hayo maji ya kuokota.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wenzangu, kwa sisi wananchi wa Mkoa wa Mtwara bado changamoto ya upatikanaji wa huduma ya maji safi na salama ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nikuambie leo, kuna kipindi wakati wa kiangazi sisi wananchi wa Mtwara tunakosa maji hata ya kupikia chakula; na hiyo ilishuhudiwa na viongozi wetu wa Chama cha Mapinduzi Kitaifa, Mheshimiwa Naibu Katibu Mkuu, wali ulipikwa kwa maji ya tikiti sijui kama ninaeleweka vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunavyozungumzia suala la upungufu ama uhaba ama hii changamoto ya maji safi na salama nadhani kwa Mkoa wa Mtwara ndio inaongoza, namba moja. Hata takwimu za upatikanaji wa maji, zile ambazo zimekuwa zikiandaliwa na wataalam kwenye mkutano wa RCC zilikataliwa, na hapo ilikuwa inaonyesha ni asilimia 61. Lakini kiuhalisia, kule vijijini maji hakuna kabisa ndiyo maana tunapopata mvua zinaponyesha yale maji yanayotiririka juu kabisa tunayakusanya tukichota kwenye ndoo tunayaweka ili lile tope likae chini halafu ndipo tunakunywa hayo maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba, kwenye hilo eneo tu, hivi Serikali ilishawahi kufanya coordination kati ya Wizara ya Maji na Wizara ya Afya ikajua kwamba ikitatua hii changamoto ya maji kwa kiasi kikubwa tutapunguza gharama za matibabu kule kwenye Wizara ya Afya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wa Mtwara wamesema; mimi sisemi kwamba Serikali haijafanya kazi, imefanya, na Mheshimiwa Waziri alikuja na tumeona alikwamua miradi chechefu lakini pia yapo maeneo pia kwama vimeshimbwa lakini bado changamoto yetu ni kubwa sana hali ya upatikanaji wa huduma za maji vijijini tunavijiji 800 kati ya hivyo vijiji 800 vijiji visivyo na maji ni 324 unaweza ukajionea hali ilivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suluhisho la kwetu sisi ni maeneo mawili tu kwanza ni chanzo cha Mto Ruvuma ambapo kwenye kitabu cha waziri inasema hiyo ndio maeneo ya miradi ya kimkakati lakini pili ni chanzo chetu cha Makonde ambayo inajazwa kwa chanzo cha Mahuta Mkunya pamoja na Mitema.

Mheshimiwa Mqwenyekiti, sasa, ukienda kwenye chanzo cha Mitema reserve yake kwa mwaka ni mita za ujazo milioni 65 lakini kwa mahitaji ya watu wa Newala Tandahimba na Nanyamba kwa siku ni mita za ujazo elfu 27; ukifanya kwa mwaka ni mita za ujazo milioni 9.9. Ukienda Mtwara peke yake mahitaji ni mita za ujazo 21, na ukifanya kwa mwaka ni milioni 7.7. Total ya mahitaji yetu sisi kwa Nanyamba Mtwara Newala na Tandahimba ni mita za ujazo elfu 17 wakati chanzo cha Mitema uwezo wake kwa mwaka ni mita za ujazo milioni 65; maana yake ni kwamba inatumika kwa asilimia 27 tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri watu huku wamepongeza, na wewe umekuwa ukisema ndio mheo wa mgonjwa ndio utaweza kutoa dawa. Nikuombe sana kaka yangu Aweso, hiki chanzo cha Mitema kitumike chote kiweze kutatua tatizo la maji kwenye hizi wilaya nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mradi hapa tumeona imeandikwa Makonde, lakini Mheshimiwa Waziri hatujui, hivyo scope ya mradi huu wa Makonde ni ipi? inaanzia wapi? Mawanda yake yanaanzia wapi na yanaishia wapi? Fedha zake pia hazionekani, ndiyo tunasubiri fedha za ndani, ni Shilingi ngapi, zitafanya nini, zitawanufaisha wananchi wangapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini, mimi bado naona kama hali ni tete na haitabiliki. Ukienda kwenye Mradi wa Kuboresha Miji 28 imetajwa pale Makonde. Sasa mimi nikawa najiuliza, hivyo beneficially wa Makonde ni akina nani? Haitaji kwenye kitabu. Je ni Newala, Tandahimba, Nanyamba, Mtwara? Sasa hapo ndipo ambapo panaleta kizungumkuti. Ni vema Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atuambie, nani maana Makonde ni chanzo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti ninaomba sana; pamoja na hilo ukarabati wa mabomba ya Mtwara ukafanyiwe kazi kwa sababu yale mabomba bado yana miaka 40 na pengine tutakapokuja mwakani na sisi hatutasema kwa sauti hizi kwa sababu tutakuwa tumenufaika…

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Agnes kwa mchango wako.

MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Awali ya yote nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya katika nchi yetu; na hilo wala halina ubishi kwa sababu hata ukisikiliza kwenye redio za nje, TV za nje Dkt. Samia ni mwamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kwenye hoja hii na nimpongeze kaka yangu Mheshimiwa Bashe na Naibu wake. Kwa sababu ya muda, tunajua wote wanafanya kazi nzuri, lakini tunao wajibu wa kuendelea kumshauri ili aendelee kufanya kazi. Sasa yako maswali ambayo pengine hata nikimuuliza leo Mheshimiwa Waziri pengine atashindwa kunijibu lakini ninaamini atakuja kuyajibu baada ya kuwa amefanya utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo moja wapo ni eneo la uzalishaji. Ukiangalia kwenye hotuba yake anasema ilitarajiwa tuzalishe zao la korosho tani 400,000 lakini hadi Aprili tumezalisha tani 182,270. Sasa sababu aliyoitaja amesema kwamba uzalishaji umepungua ama umekuwa mdogo kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa, inaweza kuwa. Lakini hapa nilikuwa mimi najiuliza, pamoja na wakulima wengine wa korosho; kwa msimu uliopita nadhani umefanikiwa sana; kwamba sulphur ya unga wakulima wa korosho waliipata kwa takribani asilimia 60 ikiwa ni tani 15,000 na dawa ya maji zaidi ya milioni 2.6 sawa na zaidi ya 100%.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapo tulitarajia, na wakulima walionufaika ni takribani 483,000 sasa ukiangalia nguvu uliyoitumia na wakulima waliopata hizo pembejeo tulitarajia uzalishaji uongezeke lakini badala yake uzalishaji umepungua. Kwa hiyo yapo maswali ya msingi; tunadhani nini hasa kilichotokea? Ndiyo maana, kwa vile hatuna majibu ya utafiti, hakuna study zilizofanyika ndiyo maana wakulima wanasema zile sulphur ama zile pembejeo ambazo ulitupatia hazina ubora. Siwezi kuthibitisha kwa sabbau bado study haijafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tunasema hivyo? Kwa sababu dawa zingine ulivyokuwa ukimaliza tu kumwagilia ama kupuliza kwenye ile mikorosho, mikorosho inanyauka na maua yanadondoka. Kwa hizo hoja na ndiyo maana tunaona pengine kuna walakini kwenye dawa ama pembejeo ama viuatilifu vya korosho ambavyo tumetumia mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye hilo eneo pia mimi bado nina swali. Zamani wakati sisi tuko wadogo tulikuwa tunatumwa Kwenda kuokota korosho na reki, tulikuwa hatuokoti moja moja hivi lakini enzi hizo wataalamu hawakuwepo na dawa hazikuwa zinapatikana hivi, hivyo kwa mkulima wa kule Tandahimba wa kule Malokopareni kwetu Masasi ukimpa dawa ukimpa sulphur yeye anaenda kupiga tu kuanzia pale inapotakiwa kwenye kalenda. Je, wataalamu wetu wapo wa kutosha wa kutuambia kwamba huu mkorosho kwa sasa hauumwi? Hivyo binadamu anapotumia dawa kila siku hata kama haumwi kwa vyovyote vile atakufa. Je, mimea mingine ambayo tunazalisha kwenye mazao ya kimkakati inapewa dawa kila siku? Hayo ni maswali ya kujiuliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye eneo la pili, kuhusu bei. Msimu uliopita Mheshimiwa Waziri ni shahidi, wakulima wamelalamika sana. Bei aliyoipata mkulima mkononi, acha ile ambayo pengine ndio iliyokuwa inatolewa kwenye mnada, ile pesa ya mkulima mkononi. Sisi kwenye chama chetu cha MAMCU ni 1,350 mpaka 1,400. Lakini wakati anachangia Mheshimiwa Cecil hapa makato ni 1,100 sasa ukijumlisha hapo utapata bei ya korosho. Bei hii ni duni bei hii ni ya kutupa, bei hii haimlipi mkulima kwa kazi ya korosho ambavyo inavyokuwa kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa ndipo tunapoomba sasa sekta mbalimbali ama Wizara zisomane. Ijumaa tumemaliza Wizara ya Viwanda na Biashara, kama zingekuwa sekta hizi zinasomana pengine kazi yako ingekuwa ni nzuri na ingekuwa ina tija. Kwa sababu sisi kwenye korosho kuna ile korosho ambayo ndio tunalalamika inauzwa ghafi kwa sababu suala la viwanda tumeshasamehe, tumesahahu kwa sababu tunaona huo ni ugonjwa mwingine tunauacha pembeni. Lakini kama tungekuwa tunauza ile korosho halafu tunauza na lile bibo kwa ajili ya kutengeneza mnyororo wa thamani, kwamba zile pombe alizokuwa amezileta Mheshimiwa Condesta hapa tungetengeneza kwa mabibo ina maana zao la korosho kwetu sisi lingekuwa lina tija kubwa, kwa sababu tungeuza ile korosho na yale mabibo yangeweza kutengeneza pombe ndani na hivyo mkulima wa korosho angendela kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nina uhakika hata wabunge wengine wakitoka wakienda Mtwara sasa hivi watajiuliza, hivi hawa Wabunge wa Mtwara miaka nenda rudi wamekuwa wakisema wao zao lao ama dhahabu yao ni korosho, watakuta umasikini uliokuwepo kule ni kwa sababu mnyororo wa thamani huu haujafungamanishwa. Mimi niombe sana, najua Serikali yetu ni Sikivu, wizara zisomane ili na Mheshimiwa Bashe na wewe uvunje, uweke rekodi tuone namna ambavyo wakulima wa korosho tutainuka kupitia Wizara yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo i nilikuwa najiuliza; hivi ni kweli Serikali inaweza kumaliza kangomba? Inaweza? Kwa sababu kangomba kwa msimu uliopita watu wameuza korosho ama wamenunua kwa 2,000 halafu bei ya mnada ni 1,300 sasa mkulima ataenda wapi? Hivi kwa nini asiuze korosho yake kwa kangomba? Kwa sababu kangomba inauzwa 2,000 bei ya mnada mkulima anatoka na 1,300 tena anaisubiria benki mpaka anachakaa, tena juzi juzi tulivyoenda kwenye mwenge tukaambiwa kuna watu sijui wa benki yetu wakulima waliuza korosho mpaka sasa hivi hawajapata hela yao ndiyo maana sasa inakuwa ni changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi moja ya maswali ambayo nitaomba uje utuambie, je, kangomba itaondoka kama bei ya korosho inaendelea kushuka kwa kiasi hiki? Kwa sababu hivi vitu lazima vyote vitakapokuwa vinashughulikiwa ukishughulikia jambo moja kwa uzuri ndivyo utakavyoondoa changamoto kwenye eneo lingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninadhani hilo ni eneo lingine ambalo Wizara hii itakapokuja kujibu hapa ituambie. Mimi sina shaka kwenye utendaji wa Mheshimiwa Waziri, nina uhakika akiyachukulia haya mambo yote kwa umakini inawezekana tukatoka hapo tulipo tukaenda kwenye hatua nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nisisitize suala la uatafiti kuhusiana na visababishi ambavyo kwa namna moja ama nyingine vinapelekea zao la korosho kudondoka ni muhimu likazingatiwa. Nimeona bodi ya korosho imesambaza miche 11,000 kwa mikoa 13, nikajiuliza, sasa ilikuwa inapata 900,000 ama 800,000? Lakini hata nikipiga hesabu kwa wale wakulima 483,000 waliopata viuatilifu, nikafanya hesabu pale, nikasema kwa hiyo kumbe kila mkulima pengine angehitaji mbegu ya korosho au miche, angepata miche 0.022. Kwa hiyo ni kama vitu havioani hivi, yaani jitihada hiyo siioni kwa hiyo ni muhimu sana hayo mambo yote yakafungamanishwa Pamoja ili tuweze kuona tija ya zao la korosho na tuone kazi nzuri itakayokuwa imefanywa na Serikali kupitia Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia hoja iliyopo mezani. Kwanza kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa sababu naamini Watanzania wengi wanajua hili neno la kumtua Mama ndoo kichwani, yeye ndiye Muasisi aliyeasisi alipokuwa Makamu wa Rais. Sasa hivi yeye anaitekeleza akiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania na anatekeleza kwa kasi. Kwa hiyo, nadhani wote tuna kila sababu ya kumpongeza kwa sababu hata tumeona kwenye bajeti hii imeongezeka kwa asilimia saba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Aweso kwa kazi nzuri anayoifanya, Mheshimiwa Naibu wake Engineer Maryprisca Mahundi, Katibu Mkuu Engineer Nadhifa na Naibu wake Watendaji wote lakini bila kusahau Mameneja wa RUWASA hasa Meneja wa RUWASA wa Mkoa wa Mtwara Engineer Primy Damas na mameneja wetu wa wilaya kwa kuwa nafanya kazi Mkoa wote wa Mtwara. Kwa nini nampongeza Mheshimiwa Waziri? Kwa sababu ni kweli kabisa kwamba amekua akijua mihemo ya wagonjwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana wakati nachangia hapa nadhani moja ya Wabunge waliyolia hapa kuhusiana na maji ya kuokota nilikuwa ni mmoja wapo na hasa nilipowapa ile hisroria ya kwamba watu walikuwa wanatumia maji ya tikitiki wakati fulani kwa sababu ya shida ya maji katika Mkoa wa Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niruhusu nimshukuru Mheshimiwa Aweso, kwa sababu waswahili wanasema kushukuru ni kuomba tena. Namshukuru sana Waziri kwa sababu kuna miradi kadhaa ambayo imetekelezwa kwenye Mkoa wetu wa Mtwara. Hivyo nitakwenda kuishukuru hiyo nianze kwanza kwa kuunga mkono mapendekezo yote, ama maoni ya kamati kwa kuwa ni mjumbe wa kamati na yeye amekuwa ni msikivu na timu yake yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye yale maoni kumi naomba nisisitize kwenye mambo mawili; la kwanza, ni Wizara haina namna nimuhimu sana ikatengeneza mpango kabambe wa maji hii tunayosema kwa kilugha chetu cha kimakua National Water Master Plan, hili lazima lipatikane lakini pia Wizara lazima iwe na gridi ya maji na hili linawezekanaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge hapa wamesema; Mheshimiwa Waziri, unganisha vyanzo vikubwa vya maji kwa maana ya Maziwa, Ziwa Victoria, Ziwa Tanganyika, Ziwa Nyasa na mito mikubwa kama Mto Ruvuma na Mto Rufiji na hapo sasa utaona namna ambavyo mambo ama azma ile ya Mheshimiwa Rais ya kumtua mama ndoo kichwani itawezekana. Kwa sababu utakuwa tumeweza kuya–tap hayo maeneo muhimu na unakuwa na gridi ikinyofoka huku unawasha huku, hilo ndiyo jambo ambalo litakutoa na nadhani utaweka historia katika maisha yako ya kuwahudumia watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili kwenye yale mapendekezo kumi ya kamati, nisisitize kwenye kutumia watalamu wa ndani. Tulipokuwa kwenye kamati tumetembelea miradi, tumeona ule wa Babati pale namna ulivyokuwa mzuri na umetekelezwa na watalam wa ndani sina shaka watalamu wa ndani wa wizara yako wanaweza wape nafasi wakatekeleze miradi mingine kule ambako Waheshimiwa Wabunge wanakuomba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niendelee kukushukuru Mheshimiwa Waziri nakushukuru kwa kipindi kirefu sisi mradi wetu wa Makonde tangu enzi hizo ulivyojengwa ulikuwa unaingia kwenye vitabu lakini ulikuwa hautekelezeki. Kwa mara ya kwanza safari hii wewe na Naibu wako na Katibu Mkuu pale mmeweka alama, kwa nini? Kwa sababu mradi ule wa bilioni 84.7 tayari fedha bilioni 12 ikiwa ni malipo ya awali zimeishakwenda na mkandarasi yuko site kazi ya kusafisha maeneo ya kujenga matenki kwenye majimbo manne inaendelea. Newala Mji, Newala Vijijini, Tandahimba na Nanyamba hapa ninaomba tu kama nilivyotangulia kukushukuru na ninakuomba tena kwamba phase one ya mradi huu ni muhimu ikaunganisha maji katika maeneo yote muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye ule mchoro wa maji utakuta kwa mfano pale Nanyamba inapitia kata kumi lakini kata tatu ndiyo zinaonekana zitakwenda hali kadhalika Tandahimba. Kwa hiyo, ni muhimu phase one hii ikaenda maeneo yote ya mradi ili RUWASA waje kuwa na kazi ndogo. Kwa sababu unajua fedha zao pia haziwatoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ya pili kwa sababu umeweka alama na unakusudia kutuwekea alama ili mimi mwakani nisije tena kusema habari ya kuokota maji hapa ni vizuri mradi ukatekelezwa kwa kasi na fedha ikaenda ili tuone matokea ya kazi yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ninalo kushukuru Mheshimiwa Waziri sisi tuna Mamlaka pale MANAWASA Masasi kwa fedha za 2021/2022 tayari umepeleka milioni 434 kati ya 738 nikuombe kwa zile fedha za 2022/2023 milioni 940 peleka kaka wakaweze kusambaza maji mjini Masasi na Nachwingea lakini na vijijini ambako ndiyo tunatoka sisi kule vijiji ambavyo vinazunguka kwenye ule mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu; ambalo namshukuru Mheshimiwa Waziri kweli umejua shida za watu wa Mtwara. Kwa sababu jambo ambalo lilikuwa linaniliza mwaka jana la kutekeleza mradi wa Mto Ruvuma angalau umeonyesha kwa hatua za awali kwenye bajeti hii ipo miradi inayotekelezwa.

Pia ukuachia hapo kuna mpango wa kuchimba mabwawa, sasa ninakushukuru kwamba kwenye usanifu kwenye miradi ya kuchimba mabwawa yatakayohifadhi maji ya mvua yale 27 kwenye ukurasa wako wa 77 umeonyesha kuna usanifu katika Lukuledi – Masasi, Namasobo – Nanyumbu, Chilunda – Nanyumbu, Mikangaula – Nanyumbu. (Makofi)

Mheshimiwa Mweyekiti, kwa sasa mradi unaoendelea Sengenya – Nanyumbu tunakushukuru sana lakini yatakayojengwa kwa force account Namasobo – Nanyumbu. Nakushukuru kipekee unajua Lukuledi imezungukwa na kata nyingi ambazo hazina maji. Ule Mradi wa Manawasa hautatosheleza kwenye zile kata ambazo inazunguka lakini utafanya usanifu na utajenga umenihakikishia hivyo niseme nini ninakushukuru Mheshimiwa Waziri kwamba kwa bilioni 1.7 na ushehe uko ukienda kutekeleza ile hata Mwenyezi Mungu ataendelea kukubariki kwa sababu umewatibu waliyo wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru pia kwamba kwenye ule utaratibu wakuchimba visima. Visima vilivyochimbwa na bonde kwa mwaka huu uliopita 2022 lakini vile visima vyako vitatu kwenye kila jimbo, kwenye majimbo kumi ya Mkoa wa Mtwara tayari umechimba na bado nane una uhakika utakwenda kumaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa niombe, sasa vile visima ambavyo vimechimbwa tayari ni muhimu sasa wananchi wakayanywa yale maji hasa kwenye maeneo yote nawaombea lakini nimeona kwenye vijiji kadhaa kule Sululu ya leo, Masiku, Chingulungulu umechimba lakini maji hawajaanza kuyanywa maana yake ni kwamba wataenda kule kuyaokota maji sasa na maji haya wanaenda kuyaokota mbali mtoni. Ninajua unajua adha za mama zako na sasa una Naibu mwanamke, nimruhusu kwanza kipindi hiki mwezi ujao ule twende akaone adha ambayo inapatikana katika Mkoa wa Mtwara ili tuweze kwenda sambamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niseme kuna suluhisho la kudumu la upatikanaji wa maji katika Mkoa wetu wa Mtwara na lenyewe si jipya ni suala la kutumia maji ya Mto Ruvuma. Kuna mambo mengi watalamu wanasema maji yanapungua, sijui yanafanyaje? Lakini kama utatengeneza master plan ile inamaana unaweza kuunganisha Ziwa Nyasa na Mto Ruvuma kwa hiyo, wananchi wa Mkoa wa Mtwara, wananchi wa Mkoa wa Ruvuma, wananchi wa Mkoa wa Lindi hii changamoto ya upungufu ama kukosa maji safi na salama tutakuwa tumeondokana nayo. Ukifanya hivyo kwakweli utakuwa si tu kwamba umesikiliza mihemo ya wagonjwa sisi lakini utakuwa umetutibu hata kama ujasomea udaktari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja, ninawatakia kila kheri, chapeni kazi nyingi wote ni vijana na kazi endelee. (Makofi)
THE WRITTEN LAWS (MISCELLANEOUS AMENDMENTS) (NO. 4) ACT, 2021
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba nami nijielekeze katika kuchangia Muswada wa Sheria, Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 4) wa mwaka 2021. Kwanza kabisa, nianze kuipongeza Serikali kwa kuleta Muswada huu ambao kimsingi ndani yake una Sheria 13 na Sheria hizi zina nia ya kuziba mianya inayoweza kuathiri utekelezaji wa Sheria hizo 13 kwa maslahi mapana kwa Taifa.

Mheshimiwa Spika, pili, nampongeza sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na timu yake kwa usikivu wakati wa majadiliano na Kamati lakini kwa ushirikiano mkubwa na ndiyo maana imewezesha Taarifa ya Kamati, kwamba kwenye jedwali la marekebisho kuna mambo mengi ambayo wameyachukua, lakini pia walikuwa tayari kuondoa hata vile vifungu ambavyo vilikuwa havioneshi uhalisia. Kwa hiyo, naomba nimpongeze sana Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na timu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaendelea, naomba pia niunge mkono maoni ya Kamati na niwasihi pia Waheshimiwa Wabunge kuunga mkono maoni ya Kamati kwa nia ile ile njema ya kufanya marekebisho ya Sheria hizi 13 kwa maslahi mapana ya Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, wakati Sheria hizi 13 zinajadiliwa na Kamati, nitoe tu mfano eneo ambalo Kamati imezingatia. Ile Ibara ya 42 ya Muswada inayopendekeza uhiari wa kisheria wa kuanzisha mfumo wa matumizi ya TEHAMA. Kamati iliona kwamba jambo hili likiletwa kwa hiari kwa kuzingatia Sheria ya Utaratibu wa Ajira za Wageni Sura ya 436, litakuwa bado linaturudisha nyuma kama nchi, kama Taifa hasa kwa kuzingatia pia maelekezo ya Mheshimiwa Rais wetu Mpendwa wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan ya kuondoa changamoto zinazoleta urasimu katika masuala ya uwekezaji. Hivyo hivyo ukiangalia katika mapendekezo yale ya Marekebisho ya Sheria ya Ibara ya 42 yalikuwa pia nayo yanaendeleza urasimu. Kwa sababu ukiweka uhiari, ina maana itawalazimu wageni sasa kwenda kwenye ofisi mbalimbali ambapo hiyo pia tunaona itaendeleza urasimu.

Mheshimiwa Spika, kama tunavyojua ina maana itakuwa njoo leo, njoo kesho; kwa maneno mengine full of come tomorrow na hivyo itakuwa inakwambisha pia juhudi za Serikali ya Awamu ya Sita. Sasa hivi tunataka kama Taifa kurahisisha na kufanya mambo haya ya uwekezaji yawe kwa njia ambayo inamwezesha kila anayetamani kufikia kwenye hiyo azma mahali popote anapokuwa; nje ya nchi ama ndani ya nchi na hasa kwa wageni hata wanapokuwa kule nje, wahakikishe wameshatekeleza au wameshajisajili kwa kupitia huo mfumo wa TEHAMA ili kuondoa urasimu kama nilivyotangulia kusema.

Mheshimiwa Spika, nilianza kutangulia pia kumpongeza Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kama ambavyo inaonekana kwenye Ibara ya 58, marekebisho pia pale yalihusu Shirika la Posta kuwa shirika la kipekee la kusafirisha vifurushi kuanzia gramu 500 mpaka kilo 10, jambo ambalo kimsingi lingefunga sasa fursa za vijana, fursa za mawakala, fursa za vyombo mbalimbali vya usafirishaji na ajira kwa kimsingi huo kwa vijana ambao wamekuwa sasa wakitumia nafasi hiyo vizuri.

Mheshimiwa Spika, pia tunatambua sote kwamba Shirika la Posta bado halijajiandaa kikamilifu na hasa kwa kuzingatia pia miundombinu pamoja na upungufu wa watumishi. Kwa sababu pia zipo changamoto ambazo mpaka sasa hivi kwenye Shirika letu hilo la Posta bado hatujaweza kuzifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hapa pia tunaishukuru sana Serikali kwa kuona ukweli ambao Kamati ilijielekeza kwao na hivyo kuamua kuondoa kabisa hilo jambo ambalo kimsingi nimeona ni la msingi kwetu. Kwa hiyo, bado naendelea kuwasihi Waheshimiwa Wabunge kuunga mkono marekebisho ambayo yameletwa na Kamati kwenye Jedwali la Marekebisho ili sote kwa pamoja tuweze kupitisha marekebisho haya mbalimbali ya Sheria ya Muswada (Na.
4) kama ambavyo leo tunajadili.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)