Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. AMINA DAUD HASSAN: Mheshimiwa Naibu Spika, sina budi kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuwa mzima na kuendelea na Bunge lako Tukufu salama.
Nampongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuleta bajeti hii yenye faida kwa Watanzania, vilevile na Rais wa Zanzibar kwa kuwasilisha bajeti yake yenye muono wa uchumi wa bluu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Waziri wa Fedha na Naibu wake na watendaji wake wote kwa kazi nzuri waliyoifanya kukamilisha bajeti hii yenye mashiko, bajeti hii imebeba sekta tofauti tofauti na mimi nichangie sekta ya wafanyakazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua na inathamini mchango wa sekta ya umma na binafsi katika kukuza pato la Taifa kwa kupunguza kodi ya mapato ya ajira kutoka asilimia tisa hadi asilimia nane. Kodi ya wafanyakazi kwa kiwango kimepunguzwa kutoka asilimia 11 mwaka 2015. Serikali imetenga shilingi bilioni 449 kwa ajili ya kuwapandisha vyeo watumishi 926,619. Natoa hongera sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, vyanzo vya kodi, ada na tozo mbalimbali nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kupendekeza na kufanya marekebisho ya vyanzo vya kodi hizi ikiwemo tozo na ada ikiwemo tozo na ada zitokanazo chini ya Sheria ya Ajira na usimamizi wa mapato ya Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Madiwani kwa kuwa awamu ya tano na ya sita imejenga utaratibu na uzoefu wa kukaa pamoja katika sekta zisizo za Muungano, namuomba Waziri wa Fedha akae na Waziri mwenzake wa Zanzibar haya mambo mazuri yanakwenda kukivusha Chama chetu cha Mapinduzi mwaka 2025, tuhakikishe nayo yanakwenda kufanyika na upande wa Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeweka posho kwa Madiwani wa Tanzania Bara basi tuhakikishe na upande wa Zanzibar yanakwenda kufanyika lakini ni ndogo mno, kwa hivyo ni vyema iongezwe ili waweze kufanya kazi kwa weledi zaidi na kudumisha Muungano wetu wa Tanzania.
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja asilimia mia moja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. AMINA DAUDI HASSAN: Mheshimiwa Spika, napenda kumpongeza sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa fedha nyingi katika Wizara ya Maji ili kuhakikisha maji yanapatikana na kumtua mama ndoo kichwani katika kutafuta maji.
Mheshimiwa Spika, pia nimpongeze Waziri wa Maji na Naibu wake kwa kuaminiwa na Rais kwa kazi nzuri wanayoifanya kwa kuendeleza malengo ya Rais wetu kuwa wanahakikisha maji yanapatikana.
Mheshimiwa Spika, mimi nijikite katika suala la uchimbaji wa mabwawa na visima nchini, naishauri Serikali iongeze fedha katika uchimbaji wa mabwawa na visima ili kutatua tatizo la maji katika maeneo ambayo hayana vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Spika, lingine kuna maeneo ambayo maji yanaharibika kwa kuwa hakuna usimamizi katika maeneo ya vyanzo vya maji. Niiombe Serikali isimamie na kulinda maeneo hayo kwa kuweka walinzi ili kulinda maji ambayo ni uhai.
Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.