Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Eric James Shigongo (22 total)

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba na mimi niulize swali moja la nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Sengerema ina halmashauri mbili, Halmashauri ya Sengerema na Halmashauri ya Buchosa. Mimi ni Mbunge wa Buchosa, wakati wa kampeni nilimuomba Mheshimiwa Rais Halmashauri ya Buchosa nayo iwe Wilaya. Kwa hiyo, naomba kujua ni lini sasa Buchosa nao watakumbukwa kuwa Wilaya? Halmashauri hii ina mapato makubwa, ni halmashauri inayojitosheleza na inafaa kabisa kuwa wilaya ili huduma ziweze kuwasogelea wananchi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Erick Shigongo, Mbunge wa Buchosa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tunahitaji kusogeza huduma za jamii karibu zaidi na wananchi na kuanzisha maeneo mapya ya utalawa. Ni sehemu ya kusogeza huduma kwa jamii.

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri ya Buchosa ambayo Mheshimiwa Shigongo anaielezea, naomba nimshauri kwamba utaratibu wa kuomba maeneo mapya ya utawala unafahamika na Ofisi ya Rais, TAMISEMI bado haijapata taarifa rasmi kutoka Mkoa wa Mwanza, ukihitaji kuomba Halmashauri ya Buchosa kuwa Wilaya. Kwa hiyo, naomba nimshauri Mheshimiwa Mbunge, wafuate utaratibu huo na Serikali itaona namna gani ya kulifanyia kazi suala hili. (Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa suala hili limekuwa la muda mrefu sana, lina jumla ya miaka kama minne au mitano, wananchi wanaendelea kupata mateso ya kulipa 600 wakati wa kuingia na 600 wakati wa kutoka, wananchi hawa maskini. Mimi binafsi nimeshasumbuka sana suala hili nimezungumza na Mheshimiwa Kakoko, nimezungumza na Mheshimiwa Abood, nimezungumza na Mheshimiwa Waziri Mkuu. Bahati nzuri Mheshimiwa Waziri Mkuu amenijibu na barua ninayo hapa ya kwamba amewaagiza TPA washughulikie suala hili mara moja. Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kutoa tamko hapa kwamba tozo hizo zitapunguzwa mara moja ili wananchi waweze kuondoka kwenye mateso? (Makofi)
WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shigongo, Mbunge wa Buchosa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama ilivyojibiwa katika swali la msingi tozo hizo zinatolewa kwa mujibu wa sheria na zinafuata tariff book ambayo ni ya TPA. kama ambavyo imejibiwa katika jibu la msingi, sasa hivi tunafanya majadiliano ili tuweze kupunguza tozo hizo kulingana na malalamiko ya wananchi ili tuweze kwenda kisheria. Hatuwezi kupunguza sasa hivi kwani ndiyo mambo haya haya ambayo yatazuka tena katika Ripoti ya CAG kwamba tumetoza kinyume na Tariff Book. Kwa hiyo, tunafanya marejeo hayo na tutakapoyakamilisha, tutawasiliana na vijiji vyote kama vilivyotajwa pale katika Visiwa vya Kasalazi, Yozu, Gembela watashirikishwa katika kikao cha wadau ili tuweze kupata tozo muafaka ambazo zitakubalika kwa wananchi wote. Ahsante. (Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Matatizo yanayowapata wananchi wa Igunga ni sawasawa kabisa na matatizo yanayowapata wananchi wa Jimbo la Buchosa hasa katika Visiwa vya Kome na Maisome. Naomba Mheshimiwa Waziri anieleze kwamba ni lini watajenga minara katika maeneo hayo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Eric Shigongo, Mbunge wa Buchosa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo ya Buchosa yameshaingizwa tayari kwenye mpango wa utekelezaji katika zabuni itakayotangazwa ya awamu ya sita ili eneo hilo sasa lipate mawasiliano kwa ajili ya wananchi wa Jimbo la Buchosa. Ahsante.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Sasa ninalo swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tatizo la Buyagu sasa linaelekea kufikia hatma, lakini bado wananchi wa Kata ya Ilunda Wilayani Sengerema wana adha ya namna hiyo ya kuwa na kivuko kidogo: Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka kivuko kikubwa katika eneo hili la Ilunda? (Makofi)

Mheshmiwa Naibu Spika, swali la pili: Kwa kuwa Wilaya ya Sengerema inayo majimbo mawili; lipo Jimbo la Buchosa na Mheshimiwa anafahamu kwamba watu wa Kome, Nyakalilo, Nyakasasa, Mtama wana matatizo makubwa ya usafiri: Je, Serikali itatimiza ahadi yake ya kupeleka kivuko kikubwa katika maeneo haya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shigongo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza katika eneo la Sengerema – Buchosa wana bahati kwamba tunajenga daraja kubwa pale Kigongo – Busisi na kuna vivuko kadhaa vinafanya kazi katika Ziwa Victoria. Baada ya barabara hiyo na daraja kukamilika, maana yake vivuko vile vitahamishwa kwenda maeneo mengine; na maeneo haya ambayo Mheshimiwa Mbunge anataja ndiyo sehemu mojawapo tunaenda kumaliza changamoto hii ili kuweza kutoa huduma katika eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyozungumza sasa tunajenga kivuko kipya ambacho kitafanyakazi Kata Nyakarilo na Kome kitaenda katika eneo hilo. Vile vile tunafanya ukarabati wa kivuko cha MV. SabaSaba ili kiende kusaidia MV2 Kome kuweka huduma katika eneo hilo. Kwa hiyo, naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali ipo makini sana kupeleka vivuko kwa sababu mbili; moja, ni sehemu ya biashara na pili, ni sehemu ya kutoa huduma. Watupe subira kazi zitakamilika na shida ya usafiri katika eneo hili kwenye visiwa mbalimbali Ziwa Victoria itakuwa imekamilika. Ahsante. (Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwa kuwa yanayomkuta Mheshimiwa Sangu huko Kwela yanafanana kabisa na yanayotokea huko Jimboni Buchosa; na kwa kuwa kilimo sasa kimeshathibitika kwamba ni uti wa mgongo na unategemewa na Taifa letu: -

Je, Mheshimiwa Waziri yupo tayari kutembelea skimu ya Uchiri iliyopo Buchosa ambayo imetelekezwa kwa muda mrefu, akiwa katika utaratibu wa kuifufua iweze kuwasaidia wananchi wa Buchosa na Taifa kwa ujumla? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Eric Shigongo, Mbunge wa Buchosa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, niko tayari kwenda kutembelea Jimbo la Buchosa na niko tayari kwenda kutembelea Jimbo la Sengerema kuangalia mabwawa, ambayo fedha zake zilitolewa na hayajafanya kazi vizuri. Kwa hiyo, tutashirikiana Waheshimiwa Wabunge, tutakwenda pamoja. (Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Nianze kwanza kwa kutoa pongeza nyingi sana kwa Serikali kwa namna ilivyoshughulikia matatizo ya wananchi wa Jimbo la Buchosa. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu kwa juhudi zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo mradi wa Lumea, Nyakariro, Karebezo hadi Nyehunge wa shilingi bilioni 1.6. Mradi huu ni kichefuchefu, ulijengwa chini ya kiwango, mabomba yanapasuka, maji yanamwagika chini na wananchi hawapati maji: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri, ni lini atatembelea mradi huu ili kuweza kuwa na utaratibu wa kufanya maboresho na wananchi waweze kupata maji?

Pili, ni lini Serikali itapeleka watalaam kuchunguza na kugundua watu waliohusika na ubadhirifu kwenye mradi huu ili waweze kuchukuliwa hatua kuepusha kuharibu sifa ya Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Eric Shigongo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la kwenda kutembelea Mheshimiwa Mbunge mantahofu, mara baada ya Mkutano huu tutakwenda kutembelea na kujionea na kuona kwamba kazi zinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la Watalaam kwenda kuchunguza, Mheshimiwa Waziri ameshatengeneza task force ya kufuatilia miradi yote kichefuchefu na kuona kwamba inafanyiwa kazi na inakamilika na huduma ya maji inapatikana bombani na tunamtua ndoo mwanamke kichwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, napenda kusema kwamba, ile task force naamini wamesikia na ninasisitiza maagizo ya Mheshimiwa Waziri mara wasikiapo maagizo haya waweze kwenda mara moja ili kuchunguza na miradi ile iweze kukamilika na lengo la kutoa maji na kumtua mama ndoo kichwani liweze kutimilika. (Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana. Kwa sababu mahitaji ya wananchi wa Mchinga ni kufanya biashara na kuongeza kipato, na kivuko hiki ni muhimu sana kwa ajili ya maendeleo ya uchumi wa jimbo hili. Ningependa kupata tamko rasmi la Serikali kwamba ni lini hasa watarajie kwamba ahadi hii ya Serikali itatekelezwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshi mi wa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali dogo la nyongeza Mheshimiwa Shigongo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu katika swali la msingi, Mheshimiwa Mbunge ametaka kujua ni lini hasa. Nimemueleza hapa kwamba tulishafanya tathmini, na daraja hilo linahitaji shilingi milioni 147, na imetengwa katika bajeti ambayo tutapitisha katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo katika mwaka wa fedha unaokuja daraja hili litajengwa, na hiyo nina uhakika kwa asilimia 100. Ahsante sana.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa changamoto wanayoipata wananchi wa maeneo ya Tanga na Pangani ni sawa sawa na matatizo waliyonayo wananchi wa Buchosa ambao ahadi ya Serikali ilikuwa ni kujenga barabara kutoka Sengerema, Nyehunge mpaka Kahunda, lakini wananchi wale wamesimamisha shughuli zao wakisubiri fidia na ujenzi uanze: -

Je, Mheshimiwa Waziri anaweza kuwaambia wananchi wa Buchosa ni lini fidia zitalipwa na lini barabara itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Eric Shigongo, Mbunge wa Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara anayoitaja ya Sengerema – Nyehunge hadi Kahunda yenye kilomita zisizopungua 82 ipo kwenye maandalizi. Kama nilivyosema kwa barabara iliyopita, ni kati ya barabara ambazo zinategemea kuanzwa kujengwa kwa kiwango cha lami kuanzia mwaka huu wa fedha. Kabla ya kuanza ujenzi sheria inatuambia tuwalipe kwanza fidia. Kwa hiyo, mara tutakapoanza kutangaza ujenzi huo, basi na wananchi watapatiwa fidia kwanza. Ahsante. (Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali. Nataka niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru sana Serikali kutuletea barabara ya lami, lakini ilishafanyika tathmini lakini wananchi wanasubiri malipo. Kwa sababu mchakato unaendelea, je tathmini italipwa lini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa sababu barabara hii inahusisha Majimbo mawili, Jimbo la Sengerema na Jimbo la Buchosa, je Serikali iko tayari kuchukua ushauri wa wananchi wa Buchosa, kwamba ujenzi wa barabara hii uanzie Buchosa kuelekea
Sengerema badala ya Sengerema kuelekea Buchosa?
(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Eric Shigongo, Mbunge wa Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilimuelewa kuhusu tathmini, nadhani ni fidia, italipwa lini? Kama nilimuelewa ni kwamba fedha ambazo tumetenga, kitu cha kwanza itakuwa ni kulipa fidia ya wananchi ambao watapisha ujenzi huo, halafu barabara itaanza kujengwa. Kwa hiyo, itakuwa ni hatua ya kwanza ya kufanywa kabla ya kuanza ujenzi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ushauri alioutoa, kwa mujibu wa barabara ilivyo ni Sengerema-Nyamazugo- Nyehunge; hili suala ambalo tayari hata zabuni kama zimeshatangazwa, maana yake zinataja kuanzia wapi kwenda wapi. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, pamoja na kwamba majimbo ni hayo mawili lakini barabara itaanzia huku tulikoitaja na kwenda pale inapokwisha kwa sasa. Ahsante sana.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, kwanza nipongeze Serikali ya Awamu ya Sita kwa jitihada ya kujenga madarasa katika Jimbo la Buchosa.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Jimbo la Buchosa lina kata 21 na watu takribani 400,000 lakini ina high school moja tu. Nilishapeleka maombi Wizarani kwa ajili ya kuomba Shule ya Sekondari Kakobe, Bupandwa na Nyakahilo ziweze kupandishwa hadhi kuwa high school.

Je, Mheshimiwa Waziri, anaweza kutamka wananchi wa buchosa wamsikie ni lini shule hizi zitapandishwa madaraja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Eric Shigongo, Mbunge wa Jimbo la Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mpango tulionao Ofisi ya Rais- TAMISEMI, ni kuziongezea, yaani kwa maana kuzipanua, shule mia moja nchini ili kuzipa hadhi za kidato cha tano na sita kutokana na idadi kubwa ya wanafunzi iliyoongezeka. Miongoni mwa shule ambayo ipo ni pamoja katika Jimbo la Buchosha. Kwa hiyo nimuhakikishie tu kwamba kuna fedha ambayo tunaisubiria, ikishafika tu tutatekeleza hilo, ahsante sana.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza swali moja la nyongeza.

Nilishawahi kuripoti mradi wa Kalumea - Nyehunge Nyakalilo ni kichefuchefu, Mheshimiwa Waziri aliahidi kutembelea mradi ule ili aweze kutoa fundisho kwa watu wanaochezea fedha za Serikali naomba kuuliza tena.

Je, Mheshimiwa Waziri wako tayari kutembelea mradi wa Lumea ili kwenda kutoa fundisho kwa Wakandarasi wanaotumia vibaya fedha za Serikali?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shingongo Mbunge wa Sengerema, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sengerema mimi mwenye nilifika na tuliweza kufanya kazi nzuri na maeneo yale tuliyopita yanakwenda vizuri kwenye mradi huu anaouongelea Mheshimiwa Mbunge mara baada ya Bunge hili tutawasiliana kuona namna gani ya kuweza kufika pale kwa pamoja.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni kweli Mamba wawili walikutwa wamekufa ziwani, si kwamba walivunwa kama ambavyo Mheshimiwa Waziri amesema, na kwa kuwa akina mama wananchi wa Buchosa bado wanaendelea kuliwa na Mamba mpaka sasa; swali la kwanza;

Je, Waziri anaweza kuchukua hatua kwa watumishi wake ambao nina uhakika kwamba wamemdanganya ili jambo hili lisitokee siku nyingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; wananchi wa Buchose wanahitaji commitment ya Serikali ya kwamba ni lini sasa vizimba hivi vitajengwa ili kuokoa maisha yao wakati wanateka maji? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Eric James Shigongo Mbunge wa Jimbo la Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumshukuru na kumpongeza sana Mheshimiwa Erick Shigongo kwa kuendelea kufatilia eneo hili ambalo kumekuwa na changamoto ya wanyama wakali hususan mamba. Ni kweli alikuja na alimwona Mheshimiwa Waziri, lakini pia tulipeleka askari kule, wamekuwa wakifatilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ikidhibitika kweli kwamba hawa askari wamedanganya kwamba hawakwenda na wale mamba wamekutwa wako pembeni wamekufa, hatua za kinidhamu na za kiutumishi ninamwelekeza Katibu Mkuu azichukue haraka mara moja; kama itathibitika tu kwamba hawa askari wamedanganya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la pili nimwahidi tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii tumekuwa tukijenga vizimba vya mfano kuonyesha namna ambavyo hawa wanyama wanaweza wakadhibitiwa na wananchi wakaendelea na shughuli zao za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwahidi tu kwamba tutapeleka wataalamu wataenda kujenga kizimba cha mfano ambacho kanda ya ziwa pia wataenda kujifunza pale. Lakini kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, ni kwamba kwa kuwa haya maeneo kwa asilimia kubwa yanamilikiwa na Serikali za Mitaa zikiwemo Halmashauri. Tunazielekeza Halmashauri ziweze kutenga fedha kwa ajili ya kujenga vizimba ili kusaidia hawa wananchi waendelee na shughuli za kibinadamu, ahsante.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Jimbo la Buchosa lina idadi ya watu wasiopungua 400,000 na vituo vya afya vinane, lakini lina gari la wagonjwa moja na watu wengi wanaishi visiwani. Je, Serikali iko tayari sasa kutamka kwamba Jimbo la Buchosa litapata magari ya wagonjwa katika miongoni mwa magari haya ya wagonjwa yanayotolewa na moja lipelekwe visiwani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba katika magari 316 ya wagonjwa, Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa pia itapelekewa magari mawili ya wagonjwa, ahsante sana.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona. Mradi wa maji kutoka Kijiji cha Lumea, Kalebezo hadi Nyehunge ulijengwa chini ya kiwango, mabomba yanapasuka na kusababisha maji kukatika. Mheshimiwa Naibu Waziri aliwahi kuahidi kwamba atautembelea mradi huo ili ikiwezekana kuufanyia ukarabati na marekebisho upya.

Je, yuko tayari kutembelea mradi huu ili kujionea yanayoendelea?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Eric Shigongo kuhusiana na mradi huu ambao tayari Mheshimiwa Mbunge tumeongea mara kadhaa alipofika Wizarani, niseme kwamba niko tayari na tutakwenda kuhakikisha maeneo yote ambayo yalipata uharibifu tunayafanyia kazi kwa haraka. (Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona. Shule ya Msingi Bupandwa, Kasisa, Ruhama, Mwabasabi zina uhaba mkubwa sana wa walimu na hivyo kuwafanya walimu kufundisha kwa masaa mengi kuliko kawaida na watoto kushindwa kuelewa: Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuwasiliana na Waziri wa TAMISEMI ili aweze kututafutia walimu wa kutosha watoto wetu waweze kujifunza kwa urahisi na kuelewa?
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shigongo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna maeneo yana uhaba mkubwa wa walimu, mtawanyiko wa walimu siyo sawia kama ambavyo tungependa. Bahati nzuri kuna nyongeza, walimu wataajiriwa hivi karibuni na tunazungumza na wenzetu wa TAMISEMI ili kuhakikisha kwamba walimu wale wanatawanywa maeneo yale ambayo yana uhitaji mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, sasa hivi tuna utaratibu wa kuweza kutumia walimu wa kujitolea kwa ajili ya kuendelea kupunguza uhaba wa walimu na tutaendelea na jitihada hizi ili kuhakikisha kwamba kweli wanafunzi wote popote pale Tanzania wanapata huduma ya kufundishwa kama inavyotakiwa.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mji wa Nyeunge una idadi kubwa sana ya watu na unahudumiwa na mradi wa maji wa Rumea, Karebezo hadi Nyeunge ambao ulijengwa chini ya kiwango; je, Serikali iko tayari kuufanyia kazi mradi huu ili uweze kutoa huduma ya uhakika?

NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Eric Shigongo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala hili la ukarabati wa mradi, Mheshimiwa Mbunge ameshafika ofisini na tumeweza kuongea pamoja na wataalam. Naomba nimhakikishie, tulivyomuahidi mradi huu ni lazima tunakwenda kuutekeleza na tutahakikisha ukarabati uwe na tija na huduma inayotarajiwa ya maji safi na salama bombani iweze kupatikana kwa wakati.
MHE. ERIC J SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kuishukuru sana Serikali kwa kutekeleza jambo hili ambalo kwa muda mrefu nimekuwa nikilipigia kelele, kwamba fedha milioni 500 wakati vifaa havikuwa vimenunuliwa. Sasa ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa ina mahitaji ya watumishi 166 lakini waliopo ni watumishi 39 pekee na hili linafanya vifaa hivi vishindwe kutumika ipasavyo;

Je, Serikali iko tayari kufanya commitment ya lini watumishi hawa watapelekwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kumbukumbu za wananchi wa Buchosa hasa katika Kisiwa cha Kome kwenye Kituo cha Afya cha Nyamisri waliwahi kuahidiwa kupelekewa X–Ray mpya, wakati ule Waziri wa TAMISEMI akiwa dada yangu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu;

Je, Serikali inaikumbuka ahadi hii au imekwishakuisahau; na kama inaikumbuka, iko tayari kuitimiza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, nikijibu swali la kwanza la nyongeza la Mheshimiwa Shigongo la kuhusu ni lini Serikali itapeleka watumishi katika Hospitali ya Wilaya ya Buchosa: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imetangaza ajira za sekta ya afya 8,070 nchini, na hii ni kwenda kujazia maeneo yenye upungufu wa watumushi, ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa. Hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika hawa watakaoajiriwa hivi karibuni nao watapata watumishi hawa katika hospitali ya wilaya.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la X-Ray iliyoahidiwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, katika Kituo cha Afya Nyamisi; tutatekeleza ahadi hii kadiri ya upatikanaji wa fedha. na tutaangalia katika bajeti ya mwaka 2023/2024 kama kituo hiki kimetengewa fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba basi x-ray iwe kipaumbele kupelekwa kwa ajili ya kuhudumia wananchi.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwanza ninaishukuru Serikali kwa kusaini mkataba wa Barabara ya Sengerema kwenda Nyehunge klilomita 54 lakini awali barabara ile ilisomeka Sengerema - Nyehunge na kipande cha Kahunda kilometa 32. Kilometa 32 za Nyehunge - Kahunda zimeondolewa.

Je, Serikali inaweza kutoa commitment ya kwamba kilometa 32 za Nyehunge - Kahunda pamoja na kipande cha Bukokwa – Nyakalilo zitajengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la, Mheshimiwa Mbunge Shigongo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii katika design, ili - design – wa kilometa zote mpaka hizo kilometa 32 kwenda Kahunda. Lakini tumeanza kuzijenga kulingana na upatikanaji wa bajeti na ndiyo maana commitment ya Serikali tayari tumeshasaini kipande hicho cha kilometa kuanzia Sengerema hadi Nyehunge kwa kuanzia na tukitegemea kwamba pengine katika mwaka wa fedha ujao, basi tutakamilisha hizo kilometa zote zilizobaki kwa sababu ndiyo mapango wa Serikali kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, Jimbo la Buchosa lina takriban idadi ya watu wasiopungua 400,000 lakini na kituo cha Polisi katika Mji Mdogo wa Nyehunge ambacho hadhi yake ni ndogo sana. Je, ni lini Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kutembelea kituo hiki ili aweze kukiona na hatimaye kufikia maamuzi ya kujenga kituo kingine?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Eric Shigongo Mbunge wa Buchosha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni bahati njema kwamba nimepanga kufanya ziara katika Mkoa wa Mwanza na Wilaya hii ni sehemu ya Mkoa wa Mwanza. namuahidi Mheshimiwa Mbunge, nitakapofanya ziara eneo hilo nitatembelea eneo ya Nyehunge ili kuona ni nini tushirikiane na Mbunge kufanya kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Polisi kama njia ya kuimarisha usalama wa raia kwenye maeneo hayo. Ahsante sana.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri. Zangu ni shukrani kwa sababu Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo kituo hiki kijengwe baada ya mama mmoja kufia kwenye mtumbwi. Sasa nina swali moja tu la nyongeza.

Je, Serikali iko tayari kuifikiria Kata ya Bukokwa ambayo ina sifa zile zile kama Kisiwa cha Maisome ili iweze kupata kituo cha afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Eric James Shigongo, Mbunge wa Jimbo la Buchoswa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nipokee shukrani zake nyingi sana kwa Serikali ya Awamu ya Sita na Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi kubwa anayoifanya katika Jimbo la Buchosa na nchini kote kwa ujumla, na nimwakikishie tu kwamba kata hii ambayo ameisema ameshakuja kufatilia mara nyingi kuhusiana na uhitaji wa kituo cha afya na tayari tumeanza kufanya tathmini kwa ajili ya kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya, ahsante.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, Jimbo la Buchosa lina takriban idadi ya watu wasiopungua 400,000 lakini na kituo cha Polisi katika Mji Mdogo wa Nyehunge ambacho hadhi yake ni ndogo sana. Je, ni lini Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari kutembelea kituo hiki ili aweze kukiona na hatimaye kufikia maamuzi ya kujenga kituo kingine?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Eric Shigongo Mbunge wa Buchosha, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni bahati njema kwamba nimepanga kufanya ziara katika Mkoa wa Mwanza na Wilaya hii ni sehemu ya Mkoa wa Mwanza. namuahidi Mheshimiwa Mbunge, nitakapofanya ziara eneo hilo nitatembelea eneo ya Nyehunge ili kuona ni nini tushirikiane na Mbunge kufanya kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Polisi kama njia ya kuimarisha usalama wa raia kwenye maeneo hayo. Ahsante sana.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali.

Swali la kwanza, ni kweli kwamba visima hivi vimechimbwa, lakini kwa hivi sasa vimesimama na hakuna fedha ya kuendeleza. Je, Serikali italeta lini fedha ili kukamilisha uchimbaji wa visima hivyo?

Swali la pili, mradi wa maji kutoka Kijiji cha Lumeya, Nyakalilo, Kalebezo, Mizolozolo mpaka Nyehunge haufanyi kazi ipasavyo kwa sababu mambomba yake yanapasuka. Je, Serikali iko tayari pia kuukarabati mradi huu ili uweze kufanya kazi kwa ukamilifu wake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, lini fedha itakwenda kwa ajili ya kuendeleza visima. Tayari Mheshimiwa Waziri ametoa maagizo kwa Mameneja wa Mikoa wote kuhakikisha hivi visima vinaweza kuendelezwa na tija ya uchimbaji visima hivi kunaweza kupatikana kwa maji bombani kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukarabati mradi ambao umekamilika lakini mabomba yanapasuka, hapa kwanza tumshukuru Mheshimiwa Rais, kwa kutupatia fedha na kuhakikisha miradi inakamilika. Unapoona mabomba yanapasuka maana yake maji yamekuwa ni mengi tofauti na ilivyokuwa nyuma. Kwa hiyo, tuko tayari kukarabati ili kuhakikisha maji mengi yaliyopatikana sasa yanawafikia wananchi. (Makofi)