Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Eric James Shigongo (17 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kusimama ndani ya Bunge hili. Naishukuru familia yangu, Wajumbe wote na wananchi wote wa Buchosa walionipa nafasi ya kuwa hapa, Chama changu Cha Mapinduzi, Mwenyekiti, Katibu wa Chama chetu cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nachukua nafasi hii kuwashukuru sana viongozi wa nchi yetu waliotangulia ambao kwa uwepo wao, maisha yangu leo ni bora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi yetu leo hapa ni kujadili hotuba mbili za Mheshimiwa Rais. Nami nimepata bahati ya kuzisoma kama walivyozisoma wenzangu wote, nimezisoma na nimezielewa. Katika kuzisoma kuna kitu kimoja kikubwa nilichokigundua kwamba Mheshimiwa Rais anawaamini sana Wabunge wake na anaamini kwamba hakuna kiongozi duniani anayefanikiwa peke yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, Musa alichagua wazee; Yesu Kristo alikuwa na wanafunzi wake 12; na Mtume Muhammad alikuwa na Maswahaba wake. Kwa hiyo, sisi hapa ndani ni Maswahaba wa Mheshimiwa Rais, ametuamini, amekuja kutusomea hotuba hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusoma, nimekumbuka kitabu kimoja nilikisoma kinaitwa Checklist Manifesto. Kwa wale ambao wamekisoma watagundua kwamba hotuba hizi mbili za Mheshimiwa Rais ni Checklist Manifesto mbili; ya kwanza ilikuwa ya 2015 – 2020 ambayo inaonyesha mambo ambayo Mheshimiwa Rais alitaka kuyafanya kwenye kipindi cha miaka mitano. Nikiwauliza kwenye Checklist Manifesto, kazi yako ni ku-list mambo yako, unatiki moja baada ya lingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikikuuliza wewe na Waheshimiwa Wabunge kwamba kwenye miundombinu, Mheshimiwa Rais ametiki au hajatiki?

WABUNGE FULANI: Ametiki! (Makofi)

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikiwauliza kwenye umeme, Mheshimiwa Rais ametiki, hajatiki? Kwenye barabara, ametiki hajatiki? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni mengi yametikika. Sasa tuna Cheklist Manifesto ya pili ya mwaka 2020 – 2025, ni checklist ngumu zaidi ya checklist tuliyomaliza. Ni ngumu kwa sababu nchi yetu iko kwenye uchumi wa kati. Ni checklist ambayo siyo rahisi kama iliyopita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuja kwenu na nazungumza mbele yako na mbele ya Watanzania wote kuwakumbusha kwamba kasi tuliyonayo ni kubwa. Mengi yamefanyika, kazi kubwa imefanyika, nampongeza sana Mheshimiwa Rais wetu, nampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu, nawapongeza Waheshimiwa Wabunge wote, lakini nataka niwakumbushe kwamba kazi tuliyonayo mbele ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu mmoja aliwahi kusema kwamba the smallest of implementation is better than the biggest of intensions. Kama hatutatekeleza hotuba hii, tukabaki na mazungumzo ya hotuba nzuri, hakika hotuba hii ya Mheshimiwa Rais itabaki ni intensions peke yake, hakuna matokeo yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natokea private sector. Kwenye private sector hatuna hotuba nyingi sana, tuna utendaji peke yake. Nazungumza hapa nikiwaomba Waheshimiwa Wabunge, katika Checklist Manifesto ya pili 2025, tufanye kazi, tumuunge mkono Mheshimiwa Rais, tusimvunje moyo Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma katika hotuba yake, ukurasa siukumbuki vizuri, lakini amesema kwamba mazao ya bahari yangeweza kuiingizia nchi yetu shilingi bilioni 320 na kitu hivi kwa mwaka. Tunazozipata ni kidogo mno kwa sababu tulishindwa kudhibiti na kusimamia vizuri, (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia nyuma ya statement hiyo kwa mimi mwanafasihi, nagundua kwamba Mheshimiwa Rais alikuwa na manung’uniko, alikuwa na masikitiko. Nawaomba Waheshimiwa Mawaziri walioko hapa ambao mmepewa jukumu, mmefanya kazi nzuri sana kwenye checklist manifesto ya kwanza. Mmeaminiwa, fanyeni kazi, tumikeni, tengenezeni historia, tuko hapa kujenga historia yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watoto wetu watakapokuja baada ya miaka 20 waseme maisha yao ni bora sana kwa sababu Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuwa kaka yangu Majaliwa. Watoto wetu wasimame waseme maisha yao ni bora kwa sababu sisi tulioko ndani ya ukumbi huu leo tutafanya maamuzi sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kuwaomba ndugu zangu, Watanzania wanatuamini, dunia inatutazama, tutakachokifanya hapa ndani katika kipindi cha 2025 ni kufanya maamuzi ambayo tutatekeleza ndoto ya Mheshimiwa Rais wetu. Viwanda ni ndoto ya Rais wetu lakini hakuna viwanda bila kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikomee hapo. Ahsanteni sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nimshukuru Mungu kwa kupata nafasi ya kusimama tena ndani ya Bunge hili Tukufu kutoa mchango wangu ndani kwa Taifa langu. Naomba tu niishukuru sana familia yangu, wapiga kura wangu kwa kazi kubwa waliyoifanya kunileta hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kutoa matumaini. Najua nasikilizwa hap ana watu hapa ndani, lakini najua nasikilizwa na Watanzania sehemu mbalimbali ya nchi yetu. Naomba tu niseme hivi, nina matumaini makubwa kwa nchi yangu leo kuliko ilivyokuwa jana. My hope for this country is greater today than it was yesterday. Nataka niwaambie Watanzania wanaonisikiliza kwamba tunakokwenda ni kuzuri sana.

Sasa nina bahati ya kuwa hapa ndani leo, tangu nimeingia nasikiliza watu wanaongea, nasikiliza napata muda wa kujifunza. Namshukuru Mungu niko hapa ndani nashiriki, zamani nilikuwa nawaangalia mnaongea nikiwa nje. Najifunza kitu kimoja kikubwa sana. Ukiwa hapa ndani kuna wakati uweke fence kwenye akili yako, ujiwekee fence, useme hiki hakiwezi kuingia kwenye kichwa changu, hiki kinaweza kikaingia maana kuna mtu anaongea kitu halafu najiuliza hivi huyu hajui yanayoendelea? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii inakua, tena inakua kwa kasi! Nani hajui tulipotoka? Nani hajui?

T A A R I F A

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe Taarifa Mheshimiwa Mbunge Eric Shigongo anayeongea kwamba katika Bunge hili sisi tuko kwa niaba ya wananchi tunatoa mawazo yetu na ya wananchi, kwa hiyo pana uhuru wa mawazo yote tunayoongea ni sahihi mahali hapa. Mwisho wa siku tunakuja na kitu kimoja. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shigongo hajamtaja mtu, endelea tu.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa hiyo sijaipokea kwa sababu sijamtaja mtu yeyote. Nataka niwaeleze Watanzania na niwaeleze watu wote walioko hapa ndani kwamba mnapoamua kujenga uchumi kuna transition period. Kuna kipindi cha mpito lazima mpite. Hata ukisoma historia ya China wakati wa Mao Tse Tung kulikuwa na kipindi kigumu sana walikipitia wale watu hatimae wakafika walipo leo. Yawezekana tunapita lakini tumeshaanza kupita kwenye transition hivi sasa mambo yanaenda kuwa safi. Nataka kuwaambia Watanzania wanaonisikiliza kwamba ya kwamba wawe na matumaini, wawe na imani na kiongozi wetu mkuu, wawe na Imani na Bunge hili ya kwamba tunakokwenda ni kuzuri na kazi inafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka nichangie Mpango wa Mwaka mmoja na wa Miaka Mitano. Nasema hivi; nitachangia eneo la digital economy, uchumi wa kidijitali. Eneo la viwanda na nikipata nafasi nitachangia eneo la mitaala yetu ya elimu kwa ajili ya watoto wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijachangia nizungumze mambo matatu tu ya muhimu kwamba we are a blessed country. Tanzania kama Tanzania ni nchi iliyobarikiwa sana. Kuna mtu alisema kwamba Mungu wakati anaumba dunia inawezekana siku ya saba alikuwa yuko Tanzania, maliasili zote aliziacha hapa wakati anakung’uta kung’uta mavazi yake ili arejee alikung’uta kila kitu akaacha hapa. Kaacha gesi, makaa ya mawe, almasi, dhahabu na kadhalika. Wakati anaondoka wanasema akadondosha handkerchief yake pale Arusha kadondosha Tanzanite pale haipo sehemu nyingine duniani. This is a blessed country, tukusanyikeni hapa tuzungumze namna ya kutumia utajiri wetu kupeleka Taifa letu mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nataka kulizungumzia ni uchumi wa kati. Hatujafika kwenye uchumi wa kati accidentally, hatujafika kwa bahati mbaya. Kuna mambo tuliyafanya yametufikisha hapo. Mambo hayo tuliyoyafanya tunayajua, basi tukayafanye mara mbili zaidi tulivyokuwa tukifanya zamani. Tutapanda kutoka uchumi wa kati wa chini kwenda uchumi wa kati wa juu, hili linawezekana. Hilo ni jambo la pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu linahusu kufanya kazi kwa juhudi kubwa. Haukuwepo Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza hapa nikawakumbusha Wabunge juu ya checklist manifesto, kuandaa mpango kama huu uliokuja halafu mnakuwa mna-tick kimoja kimoja mnachokifanya baadaye kwenye siku ya pili au mwaka wa pili mnahama na yale ambayo hamkuyatimiza huko nyuma. Lazima tuwe na checklist manifesto ya namna ya kutekeleza mambo yote tunayoyapanga kwenye mpango huu na tuanze moja baada ya lingine na tupange vipaumbele vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Afrika huwa inateseka na tatizo kubwa sana la kupanga priorities. Sisi tukatae, sisi tuwe watu tunapanga priorities zetu sawasawa, tunaanzia hapa kwa sababu ni muhimu, tunakuja hapa, tunakwenda hapa, tunakwenda pale. Watu tufanye kazi, Rais wetu anafanya kazi sana. Tuna Rais mchapa kazi, Rais visionary, lazima tumuunge mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais huyu hana maneno mengi na hazungumzi sana. Mfano, juzi alikuwa Mwanza akasema huko Dar-Es-Salaam nikija nikute shule imejengwa; imejengwa haijajengwa?

WABUNGE FULANI: Imejengwa.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, huyo ndiye Rais tuliye naye tufananye nae Watanzania wote tufanye kazi kwa nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi napenda kusoma vitabu. Kaka yangu Waziri wa Sheria aliwahi kuniambia msemo mmoja niurudie hapa, akasema ili ufanikiwe lazima uwe na kitu kinaitwa Bibliophilia, yaani usome sana vitabu. Sijasoma sana lakini napenda kusoma sana vitabu. Nimesoma kitabu cha Jack Welch, Jack Welch is a number one general manager in the history of the world. Huyu ndio aliyeitoa General Electric kwenye kufilisika mpaka kuwa number one company in America.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jack Welch alisema ili uongoze watu lazima ufanye mambo mawili. La kwanza uwaongoze kwa compassion, kwa kuwasukuma au uwaongoze kwa persuasion, kwa kuwasihi na kuwabembeleza wafanye kazi. Hapa Tanzania na Afrika Jack Walsh angekuja kufanya kazi hapa angefilisika. Kwa sababu hapa Tanzania ukitaka kuwapeleka watu kwa kuwabembeleza kazi haziendi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina kampuni binafsi; nilijaribu persuasion ikanishinda nikaamua kutumia compassion kwamba anayetaka kusukumwa anasukumwa anafanya kazi anayetaka kubembelezwa anabembelezwa anafanya kazi. Hapa Afrika mambo yote mawili yafanye kazi. Rais wetu anataka kazi. Ukipewa jukumu lifanye kwa nguvu zote ndiyo tunaweza kutoka hapa tulipo kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye digital economy. China wamegundua kwamba, manufacturing imeanza ku-decline, imeanza kushuka, ndiyo maana wakaamua sasa tuwekeze kwenye digital economy, uchumi wa kidigitali, ndio maana wanakimbia kwenye mambo ya 5G tunayaona. Sasa hivi duniani hapa China inaongoza katika mambo ya digital, kwa nini alifanya hivyo? Wanataka ku-cover lile gap ambalo litatokea manufacturing itakapo- fail.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi hakuna ubaya kwa sisi kujikita kwenye kutengeneza viwanda, ni sawa kabisa, lakini hebu tuelekezeni na akili yetu upande wa pili kwenye digital economy. Kwa nini tunaacha nchi jirani hapa zinajivuna kama zenyewe ndiyo Silicon Valley ya East Africa? Tuna vijana wana akili hapa Tanzania sijawahi kuona. Wanagundua vitu vingi, lakini hawana mtaji hawa watoto, wanatoka UDOM hapo; wamejifunza mambo makubwa kabisa ya kuleta solution kwa changamoto tulizonazo lakini hawana capital na hawawezi wakaenda benki leo na idea akapewa mkopo, haiwezekani, benki zetu sio rafiki wa masikini. Sasa kama tunaweza kukopesha fedha kwa kijiji milioni 50, kama tunaweza kupeleka pesa kwenye halmashauri kuna shida gani hawa vijana wetu wakapewa guarantee ndogo tu kwa benki kwamba, you have the best idea, sisi tutaku-sponsor wewe utengeneze application yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni-declare interest, mimi nina run media company. Pale kwetu tuna online radio, tulihangaika sana tulipopata kazi ya kuweka redio kwenye mabasi ya mwendokasi pale Dar-Es-Salaam, tulikosa technology. Tukapata South African partner halafu akajitoa, tukabaki tumekwama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini huwezi ukaamini waliotupa solution hiyo ni vijana wamemaliza UDOM hapa? Vijana wale wametengeneza king’amuzi cha kwao ambacho kinanasa matangazo kutoka ofisini kwetu mpaka kwenye mabasi yote ya mwendokasi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Watanzania let us trust our children, tuwaamini na tuwawezeshe watoto wetu.

MWENYEKITI: Ahsante sana ni kengele ya pili.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekit, ahsante sana. Naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naomba nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu kwa Taifa langu katika bajeti hii ya mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijazungumza mengi, naomba nitoe shukrani nyingi sana kwa Serikali ya Awamu ya Sita; kwa Mheshimiwa Rais kwa mambo ambayo mimi peke yangu, sijui kwa wenzangu; amenitendea kwenye jimbo langu. Katika historia, tangu mwezi Januari mpaka Aprili, nimeshapokea karibu shilingi bilioni tatu za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo, mimi na Wabunge wenzangu tulipata nafasi ya kukutana na Mheshimiwa Rais kabla hajaja Mwanza kwenye kikao kidogo, nikawa nimeomba kupewa kituo cha afya kwenye Kisiwa cha Maisome. Ni jana Waziri wa TAMISEMI, dada yangu Mheshimiwa Ummy, alinipigia simu ya kwamba kituo hicho kitajengwa. Kwa hiyo, natumia nafasi hii kuishukuru sana Serikali hii kwa usikivu na namna ambavyo inafanya kazi kuwatumikia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango nitakaoutoa leo nilikuwa nimetarajia kuutoa wakati wa Wizara ya Afya, lakini bahati mbaya nafasi haikupatikana. Hata hivyo, kwa sababu tuna Wizara ya Fedha na Waziri wa Fedha yuko hapa na ndio mpangaji wa ceiling za kisekta na Wizara zote, ni vizuri nikazungumza suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna uhusiano mkubwa sana (correlation) kati ya afya za watu na maendeleo ya Taifa. Kuna uhusiano mkubwa sana. Wanasema there is a correlation between the wellbeing of the people and socio-economic development. Nchi yoyote ambayo watu wake hawana afya, haiwezi kuwa nchi yenye maendeleo. Nchi yoyote ambayo vijana wake ni wagonjwa, haiwezi kuwa nchi yenye maendeleo. Kwa hiyo, kuna umuhimu wa kuwa na Taifa lenye afya. Watu wenye afya wataleta maendeleo ya nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama huo ni ukweli, nataka nikurejeshe wewe na Wabunge wenzangu kwenye Azimio la Abuja. Mwaka 2001 mwezi Aprili, nchi zote za Afrika ikiwemo Tanzania chini ya OAU, walikutana Abuja na zikakubaliana na wakaazimia ya kwamba fifteen percent ya annual budget itaelekezwa kwenye huduma za afya. Hayo yalikuwa ni makubaliano. Hayati Mzee Mkapa alikuwa pale na wote walikubaliana na nchi zote zikakubaliana kwamba kila tunapopanga bajeti yetu, asilimia 15 lazima iende kwenye afya kwa sababu tunataka kujenga Taifa la watu wenye afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa, miaka 20 baadaye; nina habari ya kusikitisha kuhusu azimio hilo ya kwamba hatujaweza bado kutimiza suala hilo, nafahamu ya kwamba tuna matatizo ya bajeti, uchumi kwenda taratibu, lakini ipo sababu ya Wizara ya Fedha kutazama na kupanga jinsi ya kuiwezesha Wizara ya Afya iweze kutimiza majukumu yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka 20 baadaye, nitakupa mfano wa mwaka 2017 na 2018 tulikuwa asilimia 7 tu, ya bajeti yetu kwa Wizara ya Afya na hiyo ilikuwa chini ya azimio la Abuja ambalo lilitaka asilimia 15. Mwaka 2018/2019 tulishuka na kwenda asilimia 6.7 inaendelea kushuka bajeti ambayo inatakiwa kuhudumia afya ya watu wetu. Mwaka 2021/2022 bajeti tunayoijadili hapa leo tumeshuka mpaka asilimia 2.7 maana yake nini, maana yake ni kwamba tuna bajeti ya trilioni 1 kwa afya, lakini tuna trilioni 36 annual budget hiyo peke yake inaashilia ya kwamba tumeshuka mpaka 2.72 percent hiyo ndiyo allocation yetu kwa afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina wasiwasi kama tunaweza kuwa na Taifa lenye afya kwa bajeti ambayo tumeipanga kwa mwaka huu. Nafahamu kabisa ya kwamba tuna matatizo kama nchi, nafahamu ya kwamba mnahitaji kufunga mkanda kama Taifa. Lakini afya za watu wetu ni kitu cha muhimu sana na kikubwa kabisa ambacho nataka nikizingumzie hata hiyo kidogo ambayo tunaipata, tunai-allocate yote huwa haiendi kwenye wizara. Tunawezaje kuwa na Taifa lenye afya linaloweza kujenga ustawi wa watu wake wakachangia utumishi wake, hatuwezi mpaka tuweze kuhakikisha ya kwamba hata kama hatuendi 15 percent, lakini lazima tuweze kupandisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna kodi hapa, kodi mpya tunampongeza sana Mheshimiwa Waziri, tumekuja na kodi mpya, kodi ya simu, kodi ya majengo, kwenye mafuta tumeweka shilingi 100 na fedha hizi zimeelekezwa kwenye ujenzi wa miundombinu, kwenye elimu, kwenye maji na vilevile kwenye afya, ndiyo maana nazungumza hapa leo ya kwamba ipo sababu kubwa sana ya Mheshimiwa Waziri atakavyopata fedha hizi azielekeze kwenye afya za watu wetu ili bajeti iweze kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikupe mfano, mfano huu ni wabajeti ya Wizara ya Afya mwaka 2019, nitakueleza jinsi ilivyogawanywa, asilimia 41.9 kwa mujibu wa health forum chini ya UNICEF ilielekea Wizara ya Afya na nyingine asilimia 40.7 ilielekea kwenye TAMISEMI ambayo ndiyo watekelezaji wa Sera huo ndiyo ulikuwa mgawanyo, nyingine ikaenda NHIF asilimia 10, nyingine 0.4 ikaenda TACAIDS sasa tuachane na hizo zilizoenda TAMISEMI tuachane na hizo zilioenda NHIF na TACAIDS.

Mheshimiwa Naibu Spika, twende moja kwa moja kwenye iliyokwenda Wizara ya Afya, nionyeshe namna ambavyo fedha hiyo iliweza kutumika na nionyeshe ni kiasi gani kama Taifa hatupo serious kwenye suala la kuzuia magonjwa yasitokee.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunachokifanya ni kama tunatamka hivi ugueni mkishaugua mje tutawatibu, kama Taifa nimeona hatuna capacity ya kuwatibu watu wote wanaougua ipo sababu ya kuyazuia magonjwa kabla hayajatokea. Leo hii wote tunafahamu ya kwamba kansa inatafuna Taifa letu, lakini wangapi wanafahamu ya kwamba kansa inayotusumbua inasababishwa na Aflatoxin sumu kuvu ambayo ipo kwenye mazao. Niishukuru sana Wizara ya Kilimo wanajenga ghala kwenye jimbo langu kwa ajili ya kuhifadhi mazao ili watu wasiweze kuhifadhi mazao vibaya hatimaye kukawa na sumu kuvu ikawasababishia kansa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapo ni suala la elimu tu, ni elimu peke yake ikitolewa hapa nchini watu wataweza kuepuka kansa inayosumbua Taifa. Wizara ya Afya asilimia 41.6 inayokwenda kule 33.5 inalipa mishahara, asilimia 31.8 inakwenda kwenye capacity building mambo ya kuelimisha watu, kuelemisha watumishi wetu wa wizara ya afya ili waweze kufanya kazi vizuri, sina tatizo lolote na capacity building hata kidogo ni sawa, lakini asilimia 31.8 capacity building, asilimia 7.1 inakwenda kwenye tiba, sasa sikiliza hapa, asilimia ngapi inakwenda kwenye preventive medicine, asilimia inayokwenda kwenye preventive medicine ni asilimia 3.7, tunawezaje kuzuia watu wetu wasiugue kwa asilimia 3.7? Hiyo ndiyo hoja yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana nazungumza hapa leo natoa mchango wangu kumkukumbusha Mheshimiwa Waziri na nimeikubali bajeti yake na haya kama hayatafanyiwa kazi hivi sasa, yafanyiwe kazi huko mbele tuongeze bajeti yetu kwenye preventive medicine asilimia 3.7 haitoshi kuzuia watu wetu wasiugue.

Mheshimiwa Naibu Spika, napozungumza hapa leo, tarehe hii ya leo infant mortality rate kwenye Taifa letu, watoto wanaokufa chini ya miaka mitano wanakufa watoto 60 katika kila watoto 1000, katika kila watoto 1000 watoto 60 wanakufa. Navyozungumza leo kwa mambo ambayo yangeweza kuzuiliwa kwa elimu peke yake, leo ninapozungumza hapa, leo siku ya leo, jioni ya leo mortality rate ya kinamama wanaojifungua ni wakina mama 558 katika kila vizazi 100,000, tunawapoteza wakina mama wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wiki mbili zilizopita mama kapoteza maisha akiwa ndani ya Mtumbwi anaenda hospitali mtoto katanguliza mkono, tutawazuiaje wakina mama wasiendelee kufa mpaka tutenge elimu, pesa ya kutosha, wakina mama wetu wasiendelee kuugua, inawezekana. Navyozungumza leo hapa hepatitis B, Homa ya Ini ni asilimia 6 watu wengi wana Homa ya Ini tunaweza kuwazuia kwa kuwachanja watu wetu kuna shida gani kama NHIF wakikubali Chanjo ya Homa ya Ini iingie kwenye Bima ya Afya?

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuwezi kuendelea kupoteza maisha ya watu wetu ni lazima sasa Mheshimiwa Waziri akumbuke suala la muhimu sana kwenye Taifa hili preventive medicine tuzuie watu wetu wasiugue kwa kuongeza bajeti angalau kutii azimio ambalo tulilisaini wenyewe, Azimo la Abuja, Abuja declaration. Nchi yetu inapita kwenye wakati mgumu na ninafahamu nani wajibu wetu kama watanzania kujua tunawezaje kufunga mkanda ninachokiomba, Mheshimiwa Waziri nakusihi rafiki yangu wakumbuke Wizara ya Afya uokoe maisha ya watu ambao hawatakiwi kuugua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kuunga mkono hoja na baada ya hapo nitoe shukrani nyingi sana kwa Serikali ya Awamu ya Sita, Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa mambo ambayo ameyafanya kwa ajili ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa ajili ya miundombinu, niendelee tu kukumbusha kwamba, barabara ya kutoka Sengerema kuelekea Nyehunge - Buchosa bado inahitaji kutiwa angalao lami ili wananchi wa Buchosa nao waweze kuona lami kwa mara ya kwanza katika maisha yao. kwa hiyo, nilitaka tu kukumbusha hilo kabla sijaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukrani hizo nitazungumzia maeneo mawili. Eneo la kwanza kama walivyotangulia wenzangu nitazungumza juu ya kilimo cha nchi yetu na baada ya hapo nitazungumzia suala la uwezeshaji wa wazawa wa nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo cha nchi yetu kama ambavyo tumetangulia kusikia kinaajiri watu asilimia 65. Mchango wa kilimo kwa Taifa letu kama ambavyo tumesikia wote ni asilimia 26.9 ya pato la Taifa. Hii ni dalili kabisa ya kwamba, kilimo chetu kinatoa mchango mkubwa sana kwa Taifa letu. Sasa nimeusoma mpango, nimepitia ndani, sijaona mahali popote ambapo wamezungumza juu ya taasisi zifuatazo: Sijasikia wamezungumza juu ya TANTRADE, sijasikia wamezungumza juu ya TIRDO, sijasikia wamezungumza juu ya TEMDO, CAMARTEC na SIDO.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nazitaja hizi taasisi? Nazitaja kwa sababu ya mfano wa nchi kama Taiwan, ninapozungumzia suala la maendeleo ya kilimo huwa napenda sana kuchukua mfano wa nchi ya Taiwan. Watu wa Taiwan mwaka 1950 walifikia uamuzi ya kwamba baada ya vita ya pili ya dunia walime na wakaamua kulima sana na wakawa wana-export mazao kwa wingi sana kwenda nchi za nje, lakini baadae wakasema haifai kuendelea ku- export mazao ghafi, badala yake ni bora waanze kutengeneza bidhaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, walichokifanya ndiyo hicho ambacho Baba wa Taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliki-copy na kukileta hapa nyumbani ya kwamba, tunalima halafu tunatengeneza bidhaa ndiyo tunazipeleka nje. Alipokuja hapa Mwalimu alikuja kuanza na taasisi ya kwanza ya Board of Internal Trade na baadaye akawa na Board of External Trade ambayo kwa sasa inaitwa TANTRADE ambayo kazi yake ni kutafuta masoko ya bidhaa mbalimbali. Kwa hiyo, tulikuwa tunaanzia sokoni kutafuta kwanza masoko halafu tukishapata masoko tunakuja hapa nyumbani tunawaambia sasa nyie watu wa Tanga mtalima katani, nyie watu wa Kilimanjaro mtalima kahawa, watu wa Mwanza mtalima pamba kwa sababu soko lipo, hilo ndilo lilikuwa likifanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo taasisi za utafiti kama TIRDO ilikuwa inafanya utafiti wa kutengeneza vifaa vya kiwandani, mashine za kiwandani kwa ajili ya kutengeneza bidhaa kutokana na kilimo tulichokuwa tunafanya. TEMDO walikuwa wanafanya pia na wenyewe utafiti na CAMARTEC wanatengeneza mashine za kutumia katika kilimo chetu huko vijijini. Sasa sijaona kiasi cha fedha ambacho kimetengwa kwa ajili ya taasisi hizi. Ndiyo ninataka kumkumbusha Mheshimiwa Waziri ni bora akalizingatia suala hili kwa sababu hatuwezi kunufaika na kilimo chetu kama tutaendelea tu ku-export raw mazao ambayo ni ghafi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, jambo la muhimu sana ni kuhakikisha kwamba, tunatengeneza products na tunazi-export kwenda nje. Nilitaka kukumbusha kuhusiana na suala hilo ni la muhimu sana kwa ajili ya kilimo chetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumzia suala hilo nataka nizungumzie suala moja muhimu sana juu ya National Whisper, yaani mnong’ono wa Taifa. Sisi kama Taifa, kama Tanzania, tunanong’ona nini juu ya wafanyabiashara wetu? Tunanong’ona nini juu ya vijana wa Taifa hili? Tukiwa tumekaa peke yetu sisi wenyewe tunaongea nini juu ya maendeleo ya vijana wetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasikitika tu ya kwamba, vijana wetu wa Tanzania walioko katika nchi hii hatuwapi kipaumbele kikubwa linapokuja suala la maendeleo ya Taifa lao. Nasema hivi kwa sababu, wote tunaona kwa macho na wote tunashuhudia kabisa kwamba, vijana wetu tunawapeleka shule, wanasoma, wanapata elimu, wakitoka shuleni wanakuwa hawana chakufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri ni kuanza kufikiria namna ya kuanzisha mfuko wa ubunifu wa Taifa ambao utakuwa na kiasi cha fedha cha kuwasaidia vijana wetu ili waweze kuwa na ubunifu na mfuko huo uwasaidie kuweza kutengeneza bidhaa mbalimbali ambazo zitaweza kuingia sokoni. Hilo ni jambo muhimu sana kwa ajili ya nchi yetu, hatuwezi kuwa na vijana ambao wamesoma, wana elimu, lakini elimu yao haitumiki kwa ajili ya maendeleo ya Taifa. Kwa hiyo, ninaomba sana na ninaomba nisisitize kwa mara nyingine kwamba ni jambo muhimu sana kuhakikisha ya kwamba, kunakuwa na mnong’ono wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnong’ono wa Taifa namaanisha nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zote za nchi hii, utajiri wote wa nchi hii uko hapo chini kwenye hivyo viti vya hapo mbele vilivyokaa hapo. Utajiri wote wa Taifa hili uko hapo mbele, nikianzia huko kwa Mheshimiwa Mashimba nikaja mpaka huku kwa Mheshimiwa Kipanga, trilioni 33 za nchi hii ziko hapo chini, nani anazipata, ndiyo swali la kujiuliza, nani anazipata? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kunong’ona kama Taifa kwamba, tumeamua kama nchi tenda zote za kuanzia kiasi hiki cha fedha ziende kwa vijana wa Kitanzania? Hatuwezi kuongea kama Taifa ya kwamba, fedha hizi akija mwekezaji yeyote katika nchi hii lazima ashirikiane na Mheshimiwa Tale? Maana yake nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni kwamba, kwa kufanya hivyo fedha hizi zitabaki kwa Watanzania wenyewe zinazunguka hapahapa nyumbani na tutatengeneza mabilionea wengi ambao unawaongelea hapa ndani. Tusipofanya hivyo watakuwa wanakuja hapa watu na begi baada ya miaka mitano ameshakuwa bilionea anaondoka zake sisi tunabaki tunashangaa. Matokeo yake vijana wetu wanajaa chuki ndani ya mioyo yao wanaanza kuchukia Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali yetu ni lazima itengeneze mazingira ya kuwawezesha vijana wa nchi hii kutajirika. The Government must create environment ambayo ina-foster development ya vijana wetu. Kama hatutengenezi mazingira ya vijana wetu kutajirika hakuna kijana wa nchi hii atakuwa bilionea na mabilionea wataendelea walewale kila mwaka, mwaka huu na mwaka ujao. Kama tuna nia ya kutengeneza mabilionea wengi ni lazima tuseme kwa nia moja kwamba, tumenong’ona kama Taifa ndani ya chumba ambacho hatuzungumzi wala hatuandiki gazetini wala mahali popote ya kwamba, tumeamua kama Taifa vijana wetu ni lazima watajirike. Kwa hiyo, ukiwa kama ni mradi, Rais wetu alizungumza juzi akasema nimeleta fedha hizi zisaidie wawekezaji wa ndani. Ile kauli tafsiri yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Buchosa kwenda Sengerema itengenezwe na mzawa. Tukifanya hivyo utajiri huu utazunguka kwa vijana wetu hawahawa ambao tunawatazama leo, mwisho wa siku nakuhakikishia mabilionea wataongezeka. Tusipofanya hivyo tutaendelea kushuhudia watu wanakuja hapa Tanzania baada ya muda mfupi ni mabilionea wanaondoka wanatuacha hapa tunalalamika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati umefika wa kuhakikisha kwamba, vijana wa nchi hii, vijana wa Taifa hili wananufaika na utajiri wa Taifa lao ili mwisho wa siku waweze kuanzisha viwanda wao wenyewe waajiri wenzao hapahapa nyumbani. Jambo hili linawezekana, South Africa walifanya, South Africa walikuja na utaratibu wa Black Empowerment. Black Empowerment ikawawezesha akina Motsepe na Rais wa South Africa wa sasa kuwa mabilionea mpaka leo. Sisi kama Taifa tunashindwa wapi? Tunashindwa nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kama Taifa kuamua kwa nia moja kwamba, tumeamua kutengeneza mabilonea 20 katika nchi hii, tukaenda TIRDO, TIRDO wanayo incubation center ambapo vijana wetu wana products nyingi wamebuni lakini hawana mitaji ya kufanyia biashara. Wakienda kwenye benki za biashara kukopa wanaombwa nyumba na kama kijana hana nyumba hawezi kutengeneza product yoyote ile. Hatuwezi kama Taifa kusema, Mheshimiwa Waziri unanisikia, sehemu ya tozo hii tuchukue pesa kidogo tuanzishe National Innovation Fund ambayo kijana akiwa na idea yake yuko COSTECH au yuko TIRDO awe supported atengeneze bidhaa hatimaye aje aajiri wenzake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya mambo yanawezekana. Nia ya wazee wetu wa mwanzo ilikuwa ni kuona Watanzania wanatajirika. Hatuwezi kuendelea kukaa hapa tunashuhudia wanatajirika watu, wanakuja wanatajirika wanaondoka, hatutakubali. Tukiendelea hivi baada ya muda utaanza kuona kutakuwa na chuki dhidi ya kundi fulani la watu. Tuwasaidie vijana wa nchi hii waweze kufanya vizuri maishani mwao na waweze kufanikiwa kwa sababu, hii ni nchi yao na wana haki ya kutajirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante kwa kunisikiliza. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, naomba kwanza nianze kwa kukushukuru wewe mwenyewe kwa kunipa nafasi ya kuzungumza ndani ya Bunge hili Tukufu. Ninamshukuru sana Mwenyezi Mungu kunipa uhai. Namshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na ninampongeza sana kwa kazi kubwa anayoifanya.

Mheshimiwa Spika, nimewahi kusema huko nyuma kwamba mwanadamu hupimwa kwa matendo yake, narudia tena kusema leo ya kwamba Tanzania ina Rais smart, Rais intelligent na Rais mwenye uwezo mkubwa sana wa kufanya kazi. Ushahidi wa jambo hili ni kwamba alichukua nchi hii ikiwa inakua kwa asilimia 2.2. Leo ninavyozungumza Tanzania inakua kwa asilimia 4.5, inaelekea Tano. Alichukua nchi hii ikiwa imeanza kupunguziwa misaada ya wahisani kwa sababu ilikuwa imeshatambuliwa kama nchi ya uchumi wa kati, wahisani walikuwa wanaondoa misaada kwa kuona kama vile mtoto sasa amekuwa anaweza kujitegemea. Alichukua nchi ikiwa kwenye ugumu wa uchumi lakini ameweza kudhibiti mfumuko wa bei.

Mheshimiwa Spika, ninavyozungumza hapa leo unaweza kusema kwamba Tanzania ina bei mbaya ya bidhaa. Lakini wacha nikupe record kidogo. Mfumuko wa bei nchini Sudan ni asilimia 285; mfumuko wa bei Nchini Kenya ni asilimia 6.7; mfumuko wa bei Nchini Uganda ni asilimia 7; mfumuko wa bei Tanzania ni asilimia 4.4. Tanzania ni nchi yenye lowest inflation katika nchi za Afrika Mashariki. Naomba tumpongeze sana Rais wetu kwa sababu anatupeleka vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, asubuhi ya leo nilikuwa napiga hesabu ya saa ambazo Mheshimiwa Rais amekwenda nje ya nchi kuitafutia Tanzania riziki. Amesafiri nje ya nchi saa 263, hivi ninavyoongea, Rais wangu yuko China anatafuta riziki kwa ajili ya watu wake. Kwa wanaosafiri kwa ndege wanaelewa maana ya saa 263. Tunastahili kumpongeza sana Rais wetu, mimi binafsi niseme jukumu langu la kwanza litakuwa ni kumlinda na kumtetea Rais wa nchi yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme – na Mungu anisaidie – niseme yale ambayo naamini Mungu ametaka niseme. Nchi yangu inaumwa. Tulipoitwa na Rais Ikulu wakati ule nilisema Tanzania inaumwa widespread Institutional failure; mtakumbuka. Taasisi zimefeli. Nataka niseme leo ya kwamba Tanzania nchi yangu inaumwa magonjwa makubwa mawili; ugonjwa wa kwanza ni anemia ya integrity; ugonjwa wa pili ni anemia ya accountability. Tanzania inaumwa ukosefu wa uadilifu na pili ni ukosefu wa uwajibikaji. Magonjwa haya ndiyo yamesababisha tatizo tulilonalo leo la widespread institutional failure.

Mheshimiwa Spika, tangu nimekuwa Mbunge nikiingia hapa ndani ripoti ya CAG ikija ni watu wameiba. Nilizungumza hapa mara ya mwisho nikasema na iko siku mtakuja kukubaliana na mimi ya kwamba iko sababu kubwa sana ya kuanzisha taasisi ya monitoring and evaluation. Mheshimiwa Engineer Ulenge huwa anazungumzia suala hili sana, na mimi ninataka kusisitiza, watu wanaiba. Sasa siyo kwamba hatuna watu waaminifu, wapo! Lakini katika asilimia kubwa ya watu wetu uadilifu na uwajibikaji umemomonyoka sana.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi katika Taifa hili niseme bila kupindisha maneno, tumefika mahali inaanza kuaminika kwamba mtu asipokuwa mwadilifu ni hero. Tanzania mtu asipokuwa mwadilifu ameanza kutafsirika kama hero. Kwamba alikuwa Mtumishi wa Umma akajenga ghorofa Nane, akanunua mashamba makubwa, sasa ameacha kazi anaonekana alikuwa smart, na watoto wake wanasema Baba yetu alikuwa Kiongozi, alikuwa very smart. Kumbe mwizi! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, yule aliyekuwa mwaminifu sana kwa Taifa lake, akaitumikia Tanzania kwa akili yake yote, kwa uaminifu, akaondoka kazini maskini, wakati mwingine amemwagiwa tindikali kwa sababu alikuwa TRA hataki kupokea rushwa, leo hii anateseka wanasema Baba yetu alikuwa Serikalini lakini alikuwa mjinga. Hatuwezi kuwa na Taifa ambalo wezi wanaonekana heroes. Hatuwezi! (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kwanza nipongeze sana Bunge leo, tangu nimeingia hapa ndani Bunge la safari hii nimefurahi sana. Natamani Bunge hili liendelee kama lilivyo hivi sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakumbuka huko nyuma nilikuwa nawaambia kuna na Bunge la Speed and Standards. Natamani Bunge hili liwe la Quality and Perfection, chini ya uongozi wako ujipatie sifa ya kuwa na Bunge la 12 la Quality na Perfection ambalo tunakuja hapa kusimamia mambo bila hofu wala woga, tumsaidie Rais wetu aweze kuongoza Taifa letu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lazima tutibu tatizo la integrity na uwajibikaji ndiyo maana tuko hapa, ndiyo maana tumeaminiwa na Watanzania wote tuje hapa tutibu tatizo hili. Taasisi za dini BAKWATA, Episcopal Conference na CCT, walim-hire marehemu Prof. Ngowi ili afanye utafiti kuonesha ni kiasi gani cha pesa kinapotea kila mwaka, ripoti hiyo nimeisoma ina kurasa 64.

Mheshimiwa Spika, Tanzania inapoteza karibu Dola Bilioni Moja kila mwaka kwenye mapato yake kwenye mikono na mifuko ya watu wasiokuwa waaminifu. Lazima tuzuie mambo ya namna hii. Sitaki kupita kwenye details za kwamba ripoti ikoje, yameshasemwa yote hapa, kila mtu anasema ni madudu, ni wizi na wizi zaidi.

Mheshimiwa Spika, nami naungana na wote waliozunguma. Nilimsikia Kaka yangu Mheshimiwa Tarimba akiongea jana kwa uchungu, nikamsikia Dada yangu Mheshimiwa Kapinga anaongea kwa uchungu; na wote wameongea kwa uchungu kwamba tunaibiwa. Nasi kazi yetu kama Wabunge ni kuisimamia Serikali yetu tuzuie fedha zisiibiwe ili ziende kwenye huduma za jamii yetu.

Mheshimiwa Spika, wewe ni Mwanasheria unafahamu Katiba yetu imetamka na mimi nitanukuu Katiba ilivyotamka. Katiba imesema: “We, The People of The United Republic of Tanzania, do sovereignly agree that we are going to build a country under the principles of freedom, justice, fraternity and concord.” Tumekubaliana kujenga Taifa ambalo litajengwa chini ya uhuru, haki, udugu na amani.

Mheshimiwa Spika, tukizungumzia haki, haki ya Watanzania kupata huduma za afya, haki ya Watanzania kupata elimu, haki ya Watanzania kupata maji. Hatuwezi kutimiza haki hii kama watu wanaiba kiasi hiki. Ni lazima tuzuie wizi, na tunaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa maslahi ya muda niseme nini kifanyike. Jambo la kwanza, kuna kitabu kimoja aliandika Jack Welch ambaye anaaminika kama the number one General Manager in the world, aliandika kitabu kinaitwa ‘‘Straight from the Gut’’, akasema kuna njia mbili za kuongoza watu, njia ya kwanza ni persuasion (kuwasihi) ili waweze kwenda na wewe au compassion kuwalazimisha waende. Watanzania kwa kuwasihi hawawezekani, tuwalazimishe kuwa waadilifu, walazimishwe kuwa waadilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, moja, tupandikize uadilifu kwenye mioyo ya watoto wetu. Watoto wetu wasione kwamba wezi ndiyo mashujaa wa Taifa letu, ifanyike kwenye mitaala yetu, wazazi nyumbani watimize wajibu wa kuongea na watoto wao ili ionekane ya kwamba uzalendo, uadilifu kiwe kitu cha kwanza kwa kila mtoto wa nchi hii. Hilo likiingia ndani ya mioyo ya watoto wetu nakuhakikishia tutajenga Taifa la watu ambao watalipeleka mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, tukimalizana na watoto, sisi watu wazima tulioshindikana – rafiki yangu, Mheshimiwa Dkt. Ntara, amenipa maneno hapa, yanasema hivi: Waarabu wanao msemo unasema: ‘Yamshillah Jabari illah jadhaa’ ikiwa na maana kwamba punda haendi bila bakora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ingekuwa ni maamuzi yangu Shigongo ningetangaza tuwe na siku ya uchapaji bakora Kitaifa. Fimbo zitoke Mbeya, wachapaji watoke Tarime halafu tukutane Uwanja wa Jamhuri siku ya uchapaji bakora Kitaifa. Unakuja pale na mke wako na watoto wako kama siku ile ulipokuwa unaapishwa, halafu unatajwa, Hamisi Taletale, unakwenda mbele, unachapwa, ili tujenge jamii ya watu wanaoogopa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hatutaki kuwachapa watu wetu, tumepitisha Sheria Tano katika Bunge hili, sheria ya kwanza ni Sheria ya TAKUKURU; Pili, Sheria ya Fedha; Tatu, Sheria ya Manunuzi; Nne, ni Sheria ya Utakatishaji Fedha na Sheria ya Tano ni Sheria ya Uhujumu Uchumu. Bunge hili limepitisha sheria hizo zisimamiwe! Kuwe na law enforcement. Changamoto yetu ni law enforcement. Tunayo sheria nzuri lakini hatuzisimamii. Kuna watu wanaishi uraiani walitakiwa kuwa jela leo kwa sababu ya sheria hizi. Tuzisimamie sheria zetu, mwenye haki ya kuwa jela awe jela, mwenye haki ya kuwa uraiani awe uraiani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wa Jimbo langu la Buchosa pale, nimesoma ripoti hii wametajwa kabisa kwamba wamekula Milioni 94 za bakaa. Halafu mimi naona aibu, hela za amana wamekula bila wasiwasi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie kwa kusema maneno machache tu. Kwanza, lazima sheria zisimamiwe. Mwisho Waheshimiwa Wabunge niwaombe, neno la Mungu linasema kwenye Mathayo 12.25 ya kwamba Taifa lolote linalopingana lililogawanyika, halidumu. Nyumba yoyote inayopingana na iliyogawanyika, hufa. Ninawaomba Waheshimiwa Wabunge kwa umoja wetu tusimame pamoja kwenye suala hili, tupambane kukomesha wezi kwenye Taifa letu, inawezekana. Utakumbukwa mbele tunakokwenda, Watoto wetu na wajukuu zetu watasema Bunge la 12 chini ya Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson Mwansasu lilibadilisha Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mungu wa Mbinguni awabariki sana. Ahsante kwa kunisikiliza. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nasimama hapa jioni hii ya leo kutoa pole kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa msiba mkubwa ambao umelipata Taifa letu. Natoa pole kwako wewe mwenyewe Naibu Spika na Spika wa Bunge letu. Natoa pole kwa Wabunge na Watanzania wote kwa msiba huu uliotupata. Ni msiba mkubwa ambao kwa kweli umetutikisa, lakini nashukuru kwamba tunaendelea vizuri kama Taifa. Ni jambo la kumshukuru Mungu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, siku ya Ijumaa tarehe 26 nilipokea simu kutoka kwa rafiki yangu kutoka Australia. Alinipigia simu kutoka Australia akiniambia kwamba, ameshuhudia bendera katika taifa lile zikipepea nusu mlingoti. Nilifurahi sana moyoni mwangu nilipojua kwamba bendera ile ilikuwa inapepea nusu mlingoti kwa sababu ya rais wangu Hayati John Pombe Magufuli. Ni jambo la kujivunia sana na kwa kweli sio jambo dogo kijana kutoka Chato kufanya bendera za dunia hii zipepee nusu mlingoti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kama raia wa nchi hii ambaye nina kila sababu ya kujivuna kuwa na kiongozi kama Mheshimiwa Magufuli ambaye alijitoa sadaka, alijitoa uhai wake, alijitoa nafsi yake kwa ajili ya Watanzania masikini wa nchi hii. Amefanya mambo mengi ambayo siwezi kuyataja yote, wote mnayafahamu. Ameuthibitishia ulimwengu ya kwamba Tanzania inaweza kuendesha mambo yake bila kumtegemea mzungu. Tanzania inaweza kujenga reli yake yenyewe bila kutegemea mkopo. Tanzania inaweza kujenga bwawa la umeme bila kutegemea msaada wa mtu yeyote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni jambo kubwa. Kwa miaka mingi sana tumeishi tukiamini ya kwamba sisi ni watu masikini, hatuwezi kufanya lolote bila msaada wa mzungu, lakini Mheshimiwa John Pombe Magufuli amezunguka nchi hii akiwaambia Watanzania nchi hii ni tajiri. Nimesimama hapa leo napeleka ujumbe kwa dunia nzima wapate kuelewa ya kwamba, mimi Erick Shigongo sitoki Taifa masikini, ninatoka Taifa tajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ilifika mahali anakuja mzungu hapa mbeba mizigo tu kule, lakini ukimuona unaona kwamba ni msaada. Sisi Watanzania, sisi waafrika, tunao uwezo wa kujiletea mabadiliko wenyewe bila kumtegemea mzungu wala mtu mwingine yeyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu inakwenda kwa kasi. Nchi yetu leo iko kwenye uchumi wa kati. Ni kweli, ziko nchi zilizoingia uchumi wa kati, lakini baadaye zikarudi nyuma kuwa masikini tena. Kama Watanzania tunapaswa kujituma, kuteseka, kutimiza ndoto za Rais wetu, Hayati John Pombe Magufuli, ambaye ametangulia mbele za haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kufikiria kwa dakika moja, wakati Mheshimiwa anatuacha alikuwa anafikiria nini akilini mwake. Najua alikuwa anafikiria angetamani kuona Daraja la Busisi magari yanapita, angetamani kuona treni inapita pale TAZARA, treni inaenda kwa kasi kwenda Morogoro, hayo yote hayakutokea. Mahali fulani naamini ya kwamba, alikuwa ana disappointment kwa sababu ameondoka mapema. Kazi yetu sisi tuliobaki ni kumpa furaha Rais wetu, ni kumpa furaha Hayati Magufuli huko aliko kwa kuyatimiza haya mambo aliyokuwa ameyaanzisha, na inawezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, azimio la pili ni la Mheshimiwa Rais Suluhu Hassan ambaye, kwa kweli nataka nikuhakikishie moyoni mwangu sina hofu hata kidogo wala sina wasiwasi. Matumaini yangu ni makubwa sana leo kwa sababu naamini uwezo wa mwanamke. Wanawake wana uwezo mkubwa sana, wanaume naomba tukubali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanasayansi walifanya utafiti katika Chuo Kikuu cha Havard wakagundua ya kwamba, mwanamke ana-emotional intelligence kubwa kuliko mwanaume, na ndiyo maana anaweza kufanya kazi tano kwa wakati mmoja, mwanaume ukipewa kazi moja unateseka. Kama hiyo ni kweli nina uhakika nchi yangu iko katika mikono salama, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan atalivusha Taifa hili mpaka kwenye uchumi wa juu kabisa badala ya uchumi wa kati. Tumempata na Makamu wa Rais mtaratibu, mnyenyekevu, wote hapa tumetoa kura asilimia 100. Huyu mtu atamsaidia Rais wetu kutumiza ndoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nisiongee mambo mengi. Nataka niwaombe wote pamoja tumuunge mkono Rais wetu kuipeleka nchi yetu mahali inapotakiwa kwenda. Ahsanteni kwa kunisikiliza, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa ninapenda niende moja kwa moja kwenye hoja kwasababu ya muda, lakini naomba tu kwanza kwa kusema kwamba ninatangaza mapema kabisa kabla ya wakati kwamba nitashika shilingi kwenye mshahara wa Waziri wakati utakapofika kwasababu ya suala zima la RPL- Recognition of Prior Learning ambayo Wizara iliifuta na hatimaye inawanyima watu ambao hawakupata nafasi ya kupata elimu ya Sekondari kuweza kupata elimu ya chuo kikuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaielezea baadaye vizuri zaidi wakati wa kushika shilingi utakapofika, naomba nizungumzie suala zima ambalo ninaliona kama changamoto kwenye Taifa langu, changamoto namba moja ninayoiona ni utekelezaji wa mambo tunayozungumza ndani ya Bunge, tangu nimefika hapa nikisikia michango inayotolewa hapa ndani najiuliza tatizo lipo wapi? Hapa ndani kuna michango very constructive watu wanaongea vitu vya maana tatizo kubwa kabisa ni utekelezaji na ninaomba namuomba Mheshimiwa Waziri haya yanayozungumzwa hata kama sio yote akayafanyie kazi ni kufanya kazi peke yake itatutoa tulipo kwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tusijekuwa Taifa la watu tunaozungumza watu tumeacha shughuli zetu kuja hapa tunaongea alafu hayafanyiki, haya yanayosemwa hapa yakifanyika nchi hii inabadilika. Tatizo kubwa kabisa ninaloliona katika nchi hii na ambalo ninaamini ni solution la matatizo ya nchi zote za Afrika ikiwemo Tanzania ni mabadiliko ya mind set ni mabadiliko ya akili za watu namna wanavyotazama mambo, shinda kubwa kabisa tuliyonayo bado hatujabadilika jinsi tunavyotazama mambo na namna tunavyofanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumnukuu Dkt. Gwajima mara ya mwisho alipozungumza aliongea suala la human resource is far better above natural resources. Alisisitiza kwamba kinachohitajika katika nchi yoyote duniani ni watu kuwa na akili. Watu wakiwa na akili wataweza kutafsiri Liganga na Mchuchuma kuwa barabara, watu wakiwa na akili wanaweza kutafsiri utajiri walionao uweze kuwa elimu au huduma za afya, changamoto yetu ndiyo iko hapo tu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, elimu ya vyuo vikuu, shule za msingi inachangia kuweka akili kwenye vichwa vya watu. Kama siyo shule basi ni familia, kama siyo familia basi ni society tunazoishi ndani yake. Tunatia akili kwenye vichwa vya watu wetu ili waweze kutusaidia kutatua changamoto zetu. Ndiyo kazi ya shule, kazi ya vyuo vikuu ni kuweka akili na ufahamu kwenye vichwa vya watu ili waweze kuwa na uwezo wa kutatua changamoto zinazowazunguka.

Mheshimiwa Naibu Spika, tofauti na hapo hatutaweza kuhama mahali tulipo. Ndiyo maana leo nimesimama hapa kusema kwamba naona kuna tatizo kubwa sana kwenye mtaala wa elimu ya Tanzania. Hii ndiyo inasababisha nchi hii isiende mbele kwa kasi. Simaanishi kwamba hakuna kilichokwishafanyika, mambo mengi mazuri yamefanyika na yanaendelea kufanyika lakini mimi naomba mtaala huu ufumuliwe upya na kama ilivyoamuliwa uweze kupangwa upya ili uweze kupeleka Taifa letu mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitatoa mfano na mfano huu ni wangu mimi mwenyewe niliyesimama hapa. Mpaka mwaka 2017 nilikuwa darasa la saba, sikuwahi kusoma sekondari mahali popote kwenye nchi hii. Baadaye nikasema bora nirudi shule nikasome ili niweze kupata elimu ya kuniwezesha kufanya kazi zangu ofisini. Nikaenda TCU nikapeleka vitabu ambavyo nimeviandika nikawaonyesha walipoona vitabu vyangu wakasema unaweza kusoma chuo kikuu, nikapewa mtihani nikaufanya nikafaulu nikaingia degree ya kwanza Tumaini University, one of the best University in the country kutoka darasa la saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma pale miaka mitatu nimemaliza mwaka jana chuo kikuu, nina degree yangu safi, kutoka darasa la saba mpaka university na nimemaliza. Fuatilia pale utaambiwa nimemaliza na GPA 4.8 nikiwa best student katika chuo kile kutoka darasa la saba. Kilichonipeleka chuo kikuu mimi ni RPL lakini Mheshimiwa Waziri kaifuta. Kwa kuifuta anawanyima watu wengi sana fursa ya kupata elimu. Leo hii nimekaa hapa nasema kama RPL hairudishwi shilingi mimi sitaitoa, nataka kusema wazi hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme hapa mambo anayotakiwa kufanya Mheshimiwa Waziri kwa ajili ya elimu ya nchi yetu, naomba Waheshimiwa Wabunge hapo mlipo muandike neno UKUTA kwenye karatasi zenu, nataka kusema nini kifanyike kama solution.

Kwanza, lazima mtaala utakaokuja ufundishe ujasiriamali na uzalendo kwa taifa letu. Watoto wetu wafundishwe uzalendo kwa Taifa na ujasiriamali, itawasaidia sana baadaye hata wakikosa kazi waweze kuajiri wenzao. Mimi nimeajiri watu katika taifa hili na elimu yangu ndogo niliyokuwa nayo nimefanikiwa kuajiri watu ofisini na wanafanya kazi mpaka leo, jambo hilo lazima liwefundishwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, U tumeizungumzia K ni Komputa, lazima watoto wetu wafundishwe komputa tangu wadogo. Haiwezekani Taifa hili hatufundishi watoto wetu elimu ya computer. Kuna shida gani tukifundisha coding kwa watoto wetu ili waweze kuwa na uwezo wa kutengeneza software na application mbalimbali? Taifa letu linaenda kwenye digital economy, dunia imebadilika sasa hivi digital economy ndiyo inayotawala dunia bila kuwapa watoto wetu elimu ya computer watawezaje kushindana? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la tatu ni U, nimesema UKUTA, U inayofuata hapo ni uamuzi either Kiswahili au Kiingereza basi. Hatuwezi kuwafundisha watoto wetu Kiswahili mpaka darasa la saba halafu form one tunaanza Kiingereza, ni uongo. Wabunge wote walioko hapa ndani anyooshe mkono Mbunge yeyote ambaye mtoto wake anasoma Kiswahili, tunawadanganya wananchi wetu. Sisi hapa wote watoto wetu wanasoma international schools na shule ambazo zinatumia Kiingereza kufundisha; wakulima wetu tunawafundisha Kiswahili akifika form one wanafundishwa Kiingereza watoto wana-fail masomo, hatuwezi kuendelea namna hiyo.

Mheshimiwa Spika, jambo la nne ni T ambayo ni tuamue, practical ni lazima iwe 70% na theory iwe 30% ili watoto wetu waweze kuwa-competent. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naona muda haunitoshi lakini naomba niseme kwamba nitawasilisha mchango wangu kwa maandishi, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wa rafiki yangu Mheshimiwa Condester umenichukua kidogo, nikawa nimepoteza kidogo direction.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuishukuru sana Wizara ya Viwanda na Biashara kwa kazi kubwa ambayo amekuwa akiifanya. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Makamu, Katibu Mkuu na ninawashukuru pia Wajumbe wenzangu wa Kamati ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu Tanzania miaka miwili iliyopita tulisherekea tukashangilia kwa pamoja kupanda mpaka uchumi wa kati. GDP ya Taifa ilikua, per capital income ikaongezeka, na hivyo tukasherekea kwamba nchi yetu inakwenda vizuri, lakini ninavyozungumza na wewe hivi sasa, nchi yetu imerudi ilipokuwa. Pato la Taifa (per capital income) la Mtanzania imeshuka mpaka 976. Ina maana tumeporomoka chini kwa sababu yoyote ile; iwe ni sababu ya COVID au ya kitu chochote, lakini ukweli ni kwamba tumeporomoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi yetu kama Wabunge, kama Watanzania ni kuhakikisha tunafanya kazi kwa nguvu tena kurudi tulipokuwa na kwenda mbele zaidi. Hili litawezekana kwa jambo moja kubwa, Agriculture. Kilimo peke yake; kilimo cha nchi yetu ndiyo kitatupeleka tena tulipokuwa na hata kuwa na per capital income ya dola 4,000 au 5,000 tuweze kukua zaidi. Kilimo peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia Kamati ya Viwanda na Biashara leo, sizungumzii Wizara ya Kilimo. Sasa hoja yangu iko wapi? Watanzania wanalima sana, lakini kinachowasumbua ni soko la mazao yao. Watanzania siyo masikini, ila wanakosa soko la mazao yao. Hili lazima nilizungumze kwa utaratibu na nieleweke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo cha nchi hii kinachangia asilimia 27 ya pato la Taifa. Maana yake ni kwamba kama tukiamua kulima kwa nguvu kubwa zaidi, tutaweza kuchangia hata asimilia 50 ya pato la Taifa. Ardhi tunayo, ardhi yetu ni square kilometer 940 arable land. Inayoweza kulimika ni square kilometer 345,000 hivi, lakini nchi kama Malawi inatuzidi kwenye pato la Taifa katika kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka kuzungumza kitu kimoja, Wizara ya Viwanda na Biashara ina Kitengo kinachoshughulika na masoko, na Kitengo hiki ni TANTRADE, wapo hapa wananisikia. Nimeshawahi kukutana nao mpaka ofisini kwangu nimeongea nao, nimewaleza what to do? Tufanye nini kama Taifa ili tuweze kusaidia kilimo chetu? Mheshimiwa Bashe analima sana, lakini hauzi mazao. Kazi ya Bashe ni kulima, na kazi ya kuuza mazao ni ya dada yangu Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji. (Makofi)

Mheshimiwa Menyekiti, sasa TANTRADE hawa ninaowaongelea, nitumie neno hili; linaweza kuwa siyo zuri lakini naomba wanivumilie, wako ICU. TANTRADE wako ICU, hawana pesa za kutafuta masoko, wanawezaje kushindana na Kenya? Wanawezaje kushindana na Malawi? Hawana fedha halafu tunategemea Mheshimiwa Bashe alime, halafu atafute masoko. Watatafutaje masoko hawa? Hawana uwezo, hawana technology.

Mheshimiwa Mweneyekiti, ninachokizungumza na nieleweke, kama tumedhamiria kurudi tulipokuwa kiuchumi, pato la Taifa liongezeke, per capita income iongezeke, ni lazima kuanzia sasa tuamue kuwekeza. Hatuwezi kupeleka wanajeshi wetu vitani bila silaha. Tuna tabia ya kupeleka wapiganaji halafu hatuwapi silaha. Unategemeaje wewe Mheshimiwa Bashe unalima, halafu kesho unataka uongeze pato la Taifa, halafu hutafuti masoko?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtafuta masoko hana fedha anahangaika, kazi yake imebadilika kuwa kuandaa sabasaba kila mwaka; kazi ya TanTrade siyo kuandaa sabasaba, kazi ya TanTrade ni kutafuta masoko yenye mazao ya nchi yetu. (Makofi)

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge Eric Shigongo kwamba amesema tuliingia uchumi wa kati lakini tena tumerudi tulipokuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumtaarifu ni kwamba, kilichotuingiza uchumi wa kati tumekiacha ndiyo maana tumerudi tulipokuwa; hii ni kwa sababu ya kukosa dira ya taifa na maono ya taifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shigongo taarifa hiyo unaipokea?

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu, naweka sawa hiyo.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee au nikae kwanza?

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri ulikuwa unasemaje.

KUHUSU UTARATIBU

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti nataka niweke kumbukumbu sawa; kwamba hatujarudi tulipokuwa; hii naomba isikike vizuri sana. Tulitoka uchumi wa chini, tukaenda uchumi wa kati wa chini, hatujawahi kurudi uchumi wa chini. Nchi yetu bado iko middle income. Tunachokiongelea ni ukuaji peke yake. Yaani hizi terminology za kiuchumi ni vizuri sana kuzisogelea kwa utaratibu. Kuta tofauti sana kati ya level of income ya nchi na growth rate.

Kwa hiyo sasa hivi ambacho kimeathiriwa na COVID pamoja na vitu vingine vyote ni growth rate tu; na yenyewe ni trend zinazobadilika kama mfumuko unavyobadilika. Kwa hiyo kilichobadilika tulishafika asilimia 7 tukashuka mpaka asilimia nne ya ukuaji wa uchumi ile ya annual growth rate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sasa hivi tumeshapanda kutoka hiyo asilimia nne tumeshakwenda asilimia 4.9; na takwimu hizi zinapokamilika za 2021 likely ukichukua quoters ambazo zimekwishajumlishwa, ukijumlisha wastani unakwenda kwenye 5; na 2022 wastani unaotarajiwa ni 5.2…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: …kwa maana hiyo; hata wenzetu wa Benki ya Dunia juzi walisema huenda tukaenda 5.5. Na kwa sasa hivi ambavyo tunategemea kuwekeza pakubwa kwenye bajeti inayokuja kwenye sekta za uzalishaji tunategemea tutakwenda kwenye hiyo saba. Kwa hiyo, hatuongelei level of income tunaongelea growth rate.

MWENYEKITI: Umeeleweka ahsante Mheshimiwa Waziri; Mheshimiwa Shigongo karibu umalizie.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee; na kama siendelei naomba muda wangu uhifadhi kwenye friji.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Shigongo naomba usubiri kuhusu utaratibu. Msiwe mnahata nafasi mimi naangalia sauti yako huku kumbe upo huku. Mheshimiwa kuhusu utaratibu?

KUHUSU UTARATIBU

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu utaratibu ulikuwa unakwenda kwa Mheshimiwa Mwigulu Nchemba. Ulikuwa unatafakari sauti kabla hujaniona; lakini nimesimama kuhusu utaratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwa ni kawaida ambayo inakwenda kinyume na Kanuni zetu. Kwanza tunatakiwa tunapotoa taarifa isizidi dakika mbili; lakini Mheshimiwa Mwigulu Nchemba akisimama anahutubia zaidi ya dakika mbili, kinyume kabisa na taratibu; na hii imeshawahi kutolewa angalizo na Mheshimiwa Spika hapa baada ya kuombewa mwongozo. Tunaomba tu-observe Kanuni zetu, kama Waziri umeshindwa kuvumilia uje kujibu mwishoni basi ukisimama ujihakikishe unaji-confine ndani ya dakika mbili unatoa ule taarifa yako watu wanaendelea siyo unaanza kuhutubia kabla ya muda wenyewe husika.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Easter tumepokea kuhusu huo utaratibu na naamini wenyewe wamesikia na kwa vile imeshatolewa mwongozo basi tunaomba wajirekebishe. Mheshimiwa Shigongo naomba uridhie.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu mimi kama mwanachama wa Chama Cha Mapinduzi, mwaminifu, Mbunge wa Chama cha Mapinduzi siyo vizuri sana kupisha na Waziri wangu wa Fedha. Lakini document hapa inanionesha hivi; qualification of a country to become middle income is per capital income of USD133,000 to USD 445,000; yaani qualification ya nchi yoyote kuwa uchumi wa kati ni pato lake la mtu mmoja per capital kufikia dola 1036 sisi tulifikia Dola 1080; tuka-qualify kuwa uchumi wa Kati. Lakini hivi sasa record zilizopo hapa zinaonesha uchumi wetu sisi sasa hivi pato la mtu mmoja per capital imefikia 976. Ndiyo maana nasema tumerudi kwa sababu per capital income imeshuka.

Mheshimia Mwenyekiti, nchi hii imepiga hatua kubwa sana, kazi kubwa sana imefanyika; tulikotoka na hapa tulipo ni pazuri sana; lakini hoja yangu ilikuwa ni kwamba kurudi nyuma kwetu hapa sisi siyo sababu, kazi yetu ni kuwaomba Wabunge na watanzania tufanye kazi kwa juhudi kubwa turudi tulipokuwa. Sasa itawezekanaje hili; hili linawezekana kwa kilimo; na kilimo tuanzie sokoni, kwanza tutafute soko ndipo tuje tuwaambie wakulima walime nini, na hiyo kazi ni Tantrade. Kwahiyo Tamtrade TanTrade wawezeshwe, wapate fedha, watafute masoko halafu wakulima waambiwe walime nini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wangu wa Buchosa wwaliambiwa walime maparachichi, lakini hivi sasa yanawaozea. Sasa watu wanalima miwa inawaozea, TanTrade wapewe fedha, TanTrade wapo ICU, tuwatoe ICU kwa kuwapa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuhakikishia, na kumbukumbu zikae sawasawa; kama tukiwa-impower watafuta masoko wetu; na wananchi wetu wakalima uchumi wanchi hii utakua, pato la taifa litaongezeka na watanzania watakuwa na fedha. Kwa hayo, ninayosema nakuona unagusa kengele bila shaka unataka kunisimamisha; ahsante naomba kuunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nianze na pongezi kwa Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa ambayo wameifanya kwenye Wizara hii. Nina siku mbili tu tangu nimerejea na Mheshimiwa Naibu Waziri kutoka Jimboni kwangu ambapo tumesafiri pamoja kwa mtumbwi mpaka kwenye visiwa ambako amekutana na wavuvi na kusikiliza kero zao; nampa pole sana kwa shida aliyoipata wakati tunapita ziwani kwani alijua asingeweza kurejea mahali hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi kubwa inafanyika katika nchi yetu kwenye suala zima la uvuvi ambalo nitachangia kwalo. Nataka nizungumzie sana suala la uvuvi kwa sababu eneo/Jimbo langu lina visiwa 32 na asilimia 35 ya watu wanaoishi eneo lile wameajiriwa kwenye uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nianze kwanza kwa kusema kwamba kama kweli kama Taifa tuna dhamira ya dhati kabisa ya kukuza uchumi wa nchi yetu, ni lazima sasa tuanze kutumia zawadi ambazo Mungu ametupatia; zawadi mojawapo ni uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu imebarikiwa kuwa na vitu vingi sana, ukienda huko Liganga kuna mlima wa chuma, kando yake kuna mlima wa mawe; vyote hivyo Mungu alitupatia. Ni wakati wetu sasa kuanza kuvitumia vitu hivi, hatukuvinunua, Mungu alitupatia kama zawadi na ile sisi maisha yetu yabadilike ni lazima sasa tuanze kuvitumia, hilo ni jambo la kwanza ambalo nilitaka kuwakumbusha Watanzania wenzangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja kubwa na kama hotuba yangu/mchango wangu huu ungepewa jina ungeitwa contribution of political will kwenye development. Tunazungumza mambo mengi sana mazuri, nakaa hapa ndani nasikia michango mizuri najiuliza what is wrong with us; watu wanajua jinsi ya kutoka mahali tulipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachokikosa kabisa kwenye Taifa letu ni political will, utashi wa kisiasa. Bila utashi wa kisiasa hatutoki mahali tulipo na ndio maana nataka kusema ni lazima sasa tuanze kuwa na utashi wa kisiasa na determination na commitment ya kwamba ni lazima uvuvi ubadilishe maisha ya nchi yetu, ni lazima uvuvi utupandishe kutoka tulipo kwenda hatua ya juu zaidi; bila ya political will hatupigi hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nianze kwa kusema kwamba zawadi tulizopewa na Mungu zipo underutilized, ziwa letu na bahari yetu vipo underutilized; ni wakati wa sisi kuanza kuvitumia hivi vitu kuleta maendeleo ya nchi yetu. Kwa mfano, nataka nikupe data ndogo tu, mchango wa uvuvi kwenye GDP yetu kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri ni 1.7 percent, wakati huo tuna maziwa yote na bado kwenye bahari yetu tuna maili 200 kutoka ufukweni, zote ni za kwetu tunaweza kufanya chochote. Nchi ya Uganda ambayo ina asilimia 45 tu ya Ziwa Victoria na Tanzania ina asilimia 49, GDP yake ni asilimia 12 mchango wa uvuvi. Ukianza kuona hivyo lazima ujue hapa kuna tatizo/kasoro ndio maana nasema kuna mambo ambayo wenzetu wanayafanya sisi hatuyafanyi, tunahitaji political will. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma Sheria ya Uvuvi ya Uganda ya mwaka 2018 na Sheria ya Uvuvi ya Tanzania yam waka 2003 nimegundua kwamba sheria yetu sisi imejielekeza zaidi kwenye ku-control lakini sheria ya wenzetu imejielekeza kwenye ku-facilitate. Hivyo basi, kama sheria yetu inaelekea kwenye ku-control, kila siku tutakuwa tunakamatana na wavuvi wetu, kuwachomea nyavu zao; jambo hili sio sahihi hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tujielekeze kwenye sheria ambayo ita-facilitate wavuvi wetu kuweza kuvua na kujipatia kipato na kuchangia kwenye GDP ya nchi yetu. Kama mambo haya hayawezi kufanyika nataka nikuhakikishie kabisa mchango wa uvuvi utaendelea kuwa mdogo kwa maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, samaki wanachangia asilimia 20 ya protini ya wanyama katika nchi yetu. Kwa Uganda natolea mfano, samaki wanachangia asilimia 50 ya protini ya wanyama. Matumizi ya samaki wa Tanzania kwa mwaka kila Mtanzania anatumia kilo 5.5 tu lakini wenzetu ni kilo 15 mpaka 20. Ni lazima tufike mahali sasa tuamue kwa dhamira moja kabisa ya kuhakikisha kwamba watu wetu wanatumia samaki. Jimboni kwangu samaki imekuwa kitu expensive, watu wa kawaida hawawezi kumudu samaki kwa sababu gharama yake imekuwa kubwa sana. Sasa tufanye nini? Ili uvuvi wetu uchangie kwenye pato la Taifa letu, ili uvuvi wetu uwe na impact kwenye uchumi wetu ni lazima kama nilivyosema tuanze kuhakikisha kwamba kuna political will (dhamira ya kisiasa), tusije hapa kuzungumza tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tunatoa michango mizuri sana, lakini kama hakuna political will hatupigi hatua. Kama Mheshimiwa Waziri hapa hawataachana na hofu na kuanza kutenda, hatupigi hatua hata kidogo. Tutabaki nyuma, tutaendelea ku-lag behind hatuwezi kukuza uchumi wa nchi yetu. Hatuwezi kuendelea namna hii, ni lazima tubadilike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya nchi hii TBS wana kipimo chao cha nyavu na Wizara ina kipimo chake cha nyavu. Lazima hawa watu wawili wakae pamoja na wakubaliane…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa kwa sababu ya ufinyu wa muda, naomba nianze kwa kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuzungumzia moja kwa moja mambo yanayohusu jimbo langu. Nimeshazungumza mara kwa mara na Mheshimiwa Waziri kuhusu tatizo kwenye Visiwa vya Zilagula pamoja na Maisome ambako wananchi wale wanategemea umeme kutoka kwa watu binafsi. Hivi ninavyozungumza wananunua unit moja kwa Sh.2,400. Huyu ni mwananchi wa kawaida, maskini, nimeshazungumza na Mheshimiwa Waziri naomba atakapokuwa anafunga hotuba yake hapa awaeleze wale wanaitwa Jumeme na PowerGen, alishatoa maelekezo wauze umeme kwa Sh.100 lakini baada tu ya Hayati kupumzika wamepandisha bei. Kuna maneno wanayasema kwamba aliyekuwa anatusumbua ameondoka, hawajui kama mama Samia ni moto wa kuotea mbali. Kwa hiyo, mimi nina nia ya kushika shilingi ya Mheshimiwa Waziri kama hatakuwa na maelezo ya kutosheleza kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, naomba nizungumzie maeneo ambayo bado kuna matatizo makubwa sana ya umeme kwenye jimbo langu katika Kijiji cha Itabagumba, Makafunzo, Bupandwa, Nyehunge, Kanyala, bado kuna shida kubwa sana ya umeme. Umeme uko kwenye center tu, ukizama huko ndani kuna nguzo na maeneo mengine hakuna nyaya. REA Mkurugenzi yuko hapa, Mheshimiwa Waziri na Naibu mko hapa mhakikishe sasa umeme unakwenda moja kwa moja mpaka kwenye maeneo ya ndani kabisa ili lawama hizi ziweze kupungua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda niongelee kuhusu suala la nishati, kuna uhusiano mkubwa sana kati ya nishati na maendeleo ya watu. Taasisi moja inaitwa MDI ilifanya utafiti wakasema unapoongeza matumizi ya umeme kwa asilimia moja, unaongeza pato la Taifa kwa asilimia 1.72. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana yangu hapa ni nini? Naomba kwanza nipongeze sana Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuhakikisha kwamba umeme unapatikana kwa asilimia kubwa. Hii imewezesha pato la nchi yetu kukua. Naomba kabisa tuendelee kutafuta nishati kwa gharama yoyote ili nchi yetu iweze kuwa Africa Power House. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili likifanyika, hata kama tunapingwa, mimi nakumbuka wakati tunaanza ujenzi wa Bwawa la Nyerere tulipingwa, walisema kwamba kuna masuala ya mazingira. Namshukuru sana Hayati, namshukuru mama Samia, walisema hata kama kuna issue ya mazingira bwawa litajengwa na bwawa limejengwa. Jana nimesikia wameanza tena Wazungu kusema bomba la mafuta lina issue ya mazingira kwa hiyo hatutapewa mkopo; tusiwasikilize Wazungu, wanajua kwamba tukishakuwa na nishati tutakuwa na nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Baba wa Taifa, Mwalimu J. K. Nyerere alijua kwamba ili tukue kiuchumi tunahitaji nishati. Rais wetu, Hayati, alikuja hapa ametekeleza ndoto ya Baba yetu wa Taifa. Kweli tutakuwa na umeme wa kutosha katika Taifa letu na umeme utakuwa ni wa bei rahisi kuliko wakati mwingine wowote, wawekezaji watakuja na biashara zitaongezeka. Unapoongeza umeme, unaongeza production na GDP ya Taifa lako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri na Waheshimiwa Wabunge tulioko hapa leo, tuna bahati ya kuwa ndani ya Bunge hili, wazee wetu waliotangulia wamefanya maamuzi mazuri sana sisi leo ni Taifa bora na sisi tuliopo hapa ndani tufanye maamuzi bora kwa ajili ya watoto wetu watakaokuja baada ya sisi. Nataka Bunge la Kumi na Mbili likumbukwe kama Bunge lililohakikisha Tanzania inakuwa Africa Power House kwa kuwa na energy ya kutosha ili tuweze kukua na uwezo huo tunao. I don’t care where the source is, as long as ni power, leta power, hata kama ni nuclear power leta nuclear power ili tuweze kuwa na nguvu kama Taifa. Tukiwa na nishati hakuna atakayetutisha, uchumi wetu utakuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa unyenyekevu wake na moyo wa kujituma. Nampongeza sana Naibu wake, TANESCO na REA. Ninachowaomba sasa wakachape kazi zaidi ili Taifa letu liweze kusonga mbele.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, kama hakutakuwa na majibu ya suala la umeme unit moja Sh.2,400 nitashikilia shilingi. Naomba niishie hapo, Mungu ibariki Tanzania, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge la kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kutoa mchango wangu katika kupitisha Azimio hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba ni-declare interest kwamba ni makamu mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda na Biashara na nilikuwepo kwenye mjadala mrefu sana kuhusiana na mkataba huu. Cha kwanza niliposoma mkataba huu mambo mawili yalinikuta la kwanza niliingia hofu, hofu yangu ya kwanza kabisa ilikuwa ni kwamba mkataba huu utaua viwanda vyetu, mkataba huu utaondoa ajira zetu, huo ni upande mmoja, lakini kuna upande mwingine mzuri sana wa mkataba huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ambao ulikuwa ni kwamba Afrika sasa inakwenda kufanya integration, Afrika inaanza kuuziana Afrika kwa Afrika, Afrika inaanza kufanya biashara Afrika kwa Afrika jambo ambalo huko nyuma lilikuwa halifanyiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipofika hapo nikaamua kuchagua upande wa uzuri wa mkataba, nikaamua kabisa kuachana na hofu ambayo ilikuwa imenikamata na hivi sasa nimesimama hapa kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wote kwa ujumla wetu tuweze kuridhia Azimio hili nchi yetu ikaweze kuingia katika mkataba huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa wale waliowahi kusoma kitabu cha Walter Rodney how Europe underdeveloped Africa, alisema Walter Rodney ukitaka kuichezesha Afrika isababishie tu iwe na disintegration yaani tu tuwe hatuna ushirikiano na wakoloni walifanya jambo hili kwa umakini kabisa na wakatugawa wakaweka mipaka ardhini baadaye mipaka hiyo ikaamia kwenye vichwa vyetu. Kwa hiyo, tunatembea hapa Watanzania nikivuka tu pale Namanga kuingia upande wa Kenya hofu inaniingia. Na wakati narudi nyumbani nikivuka Namanga nikiingia upande wa Arusha kiburi kinaanza. Kwa hiyo, kuna mipaka tunayo ndani ya vichwa vyetu hiyo ndiyo itakayotuchelewesha kuweza kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mkataba huu au Azimio hili linakwenda kuondosha barrier zote ambazo zilikuwepo ili sasa Afrika ifanye biashara Afrika kwa Afrika, ukijaribu kuangalia data ambazo zipo Afrika kwa Afrika kwenye Intra business, biashara ya ndani ya Afrika kwa Afrika ni asilimia 17, lakini ukiangalia Asia ni asilimia 69, ukiangalia North America ni asilimia 31. Kwa hiyo, ninachojifunza hapa ni kwamba tunafanya hii biashara sisi kwa sisi kidogo sana hatuwezi kukua mpaka tuweze kuondoa barriers, tuanze ku-trade kati ya Taifa na Taifa. Hapa tunazungumza tuna mahindi si ajabu kuna nchi haina mahindi, inahitaji mahindi lakini unaweza ukashangaa ikaagiza mahindi Brazil badala kuagiza mahindi Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naunga mkono Mkataba huu na ninaomba kabisa Waheshimiwa Wabunge wote turidhie kwa nia moja tuachane na hofu, tukubali kwenda kujifunza tukiwa tunafanya kuna learning unapokuwa unafanya na kuna kujifunza kwanza ndiyo ufanye. Ninawaomba tukubali nchi yetu iingie tukajifunze tukiwa tunatenda, tutarekebisha huko ndani kwa ndani, tutabadilisha mikakati tukiwa tunavyozidi kwenda tuta-change strategies, hatimaye tutaweza kuweza tutaweza kufanya vizuri hatutaweza kupata faidia kwenye mwaka wa kwanza au mwaka wa pili lakini nina uhakika kabisa baada ya muda si mrefu tutafanya vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la muhimu sana ni capacity building ni lazima nchi yetu iwawezeshe wafanyabiashara wetu. Ni lazima wapewe mikopo yenye riba ndogo, ni lazima tutambue ya kwamba Nigeria uchumi wake ni mkubwa sana kuliko uchumi wetu sisi. Ukinipambanisha mimi na Okwonko sasa hivi kuna uwezekano wa ku-fail, lakini kama nimewezeshwa na nchi yangu kama nchi yangu inadhamira ya kweli political will kwamba tunawapeleka hawa watu vitani wakapambane tutahakikisha kwamba wanashinda lazima tutashinda vita hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, South Africa ilifanya hivyo wakapatikana wakina Patrick Motsepe ni wakati wa nchi yetu tutengeneze mabilionea wengine wapya. Tumekuwa na mabilionea wale wale miaka hiyo tangu tukiwa watoto ni wakati sasa tuanze kusikia majina ya Aweso, tuanze kusikia majina ya kina Kigwangalla wakiwa mabilionea tumechoshwa na majina yale yale kila mwaka. Kwa mkataba huu nina uhakika wakiwezeshwa vijana wa kitanzania tutasikia majina mapya, kuna uwezekano kabisa wa kutengeneza wakina MO wengine, kutengeneza wanakina Bakharessa wengine kwa mkataba kama huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niseme kwamba tariff za kodi; tariff za kodi tusipoziangalia vizuri zitatuumiza. Nitatoa mfano mmoja hai nilitembelea kiwanda kimoja cha mapipa pale Mbagala, Mhindi anatengeneza mapipa mazuri tu lakini anashindwa kuuza Kenya, kwa sababu gani anashindwa kuuza kenya Kodi, Wakenya wanapoagiza sheet za chuma pale kwao hawatozwi kodi kwa sababu wananunua kwenye COMESA, wananunua Egypt. kwa sababu wako ndani ya COMESA hawalipi kodi asilimia 10, lakini yeye anapoagiza hapa analipa ten percent na Wakenya wakitengeneza mapipa yao pale kwa sababu ni EAC wanauza soko la Tanzania. Kwa hiyo matokeo yake mapipa yale yanakuwa chini kwa asilimia 10 upande wa bei lakini mapipa ya Mbagala yanakuwa juu, hawezi kuuza Kenya, hawezi kuuza hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kodi zetu tuzitazame vizuri wenzetu tunapotoa tariff ya kodi wanaziangalia hivi Tanzania import duty wameweka shilingi ngapi, wao wanapunguza kidogo ili waweze kushinda kwenye soko/wawe competitive kwenye soko. Ombi langu tariff za kodi tuwe smart kwenye eneo hilo, tuzipitie tuziangalie na tuwe smart kuwashinda wenzetu. Kwa nini mtu anatoka hapa anaenda kununua masharti Kampala anakuja kuyauza Dar es Salaam anapata faida, hapo kuna tatizo kwenye types za kodi kama mnataka bidhaa zetu ziweze kushinda kwenye soko tuziangalie types za kodi na ziweze kupunguzwa kushindana na wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono Azimio. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, kwa sababu ya ufinyu wa muda nianze kwa kukupongeza wewe kwa kupata nafasi ya kuwa Naibu Spika wetu, lakini nichukue nafasi hii poa kumpongeza sana Jirani yangu, dada yangu, Spika, Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson Mwansasu kwa nafasi hii ambayo ameteuliwa kuliongoza Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwanza kwa kumpongeza pia Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa inayoendelea hapa nchini; kwenye miundombinu, afya, kwa kweli mimi binafsi ninaridhika kabisa kwamba kazi inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Ibara ya 8(1) (a) inasema;Lengo kuu la Serikali litakuwa ni ustawi wa wananchi. Hapa inamaana kazi kubwa ya Serikali ni kuhakikisha kwamba wananchi wake wanaustawi katika afya, katika uchumi, katika miundombinu, katika elimu na mambo mengine yote. Ni kazi ya Serikali nadhani nizungumzie suala moja juu ya uwezeshaji wa wazawa kiuchumi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumza hili kwa sababu sisi tulioko hapa ndani tumebahatika kuwa Wabunge, tumebahatika kuwa na Maisha tulioyonayo lakini wako watu wenzetu wengi sana huko nje bado wanaishi Maisha duni na kwenye umasikini mkubwa. Bajeti ya Taifa letu kwa mwaka ni tirioni 34.88 najiuliza swali kila siku, tirioni 34.88 ngapi zimerudi kwa wananchi na ngapi zinaenda nje ya nchi yetu. Nimesimama hapa kuzungumza kwa niaba ya watanzania wazawa na ninaposema wazawa simaanishi rangi namaanisha watu wenye asili ya Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watanzania wanatakiwa wanastahili kunufaika kabisa na fedha hizi tirioni 34.8 inakuwaje fedha hizi sehemu kubwa zinaenda nje ya nchi badala ya kuwasaidia wazawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kwa sababu Bunge lako tukufu mwaka 1994 lilitunga Sheria ya uwezeshaji wazawa kiuchumi na ilisainiwa na Marehemu Rais Benjamini William Mkapa tarehe 19 Januari, 2005 ya kwamba nchi hii itawawezesha wazawa weweze kushikilia vyanzo vya uchumi vya nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa leo ninaposimama hapa bajeti ya miundombinu ya Taifa hili ni tirion 3 nataka nijiulize tirioni 3 hizi za kutengeneza barabara ya miundombinu gapi zinabaki kwa watanzania bajeti hii ya miundombinu peke yake ni trioni 3 ni ngapi zinabaki kwetu sisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wengi wanaendelea masikini mabilionea ni wale wale toka miaka ile na wajibu wa Serikali ni ustawi wa wananchi wake. Napenda kuona wazawa wengi wanafanikiwa kiuchumi katika Taifa hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, haiwezekani na sitaki kutaja nchi yoyote kama alivyozungumza Rafiki yangu Mpina haiwezekani tirioni 3 za barabara fedha inayoenda kwa wazawa ni asilimia 20 peke yake nyingi zinaenda kwa wageni wanaokuja hapa na magegi peke yake baada ya miaka mitano wamekuwa mabilionea na wanatuona sisi wazawa hatuna akili haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama hapa kukuomba wewe na kuomba Bunge hili tukufu kwa sheria hii ya Mwaka 1994 ya kuwawezesha wazawa kiuchumi, wazawa wapewe kipaumbele ni nchi gani duniani ambayo hakuna mnong’ono wa Taifa ni lazima Taifa hili linong’one na kusema ya kwamba biashara ya kiwango hiki itaenda kwa wazawa, barabara ya kilomita hizi zitaenda kwa wazawa, haiwezekani tukawaachia wageni kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayasema hayo siyo kwamba nachukia wageni nchi yangu inahitaji sana mitaji kutoka nje, lakini pamoja na kuhitaji mitaji kutoka nje bado tuwe na uwezo wa kuwa- protect watu wetu na kuwapa watu wetu kipaumbele ya kwamba tumezungumza hapa ndani nataka haya mambo yaende nje ya kwamba tender za aina fulani zitaenda kwa watu wetu hata kama hatuzungumzi, hata kama hatuandiki kwenye magazeti, hatakama hatusemi huko nje tunajua nitakapo tenda mimi na akatenda na huyu kutoka nje nitapewa mimi kwa sababu fedha hizo zitazunguka hapa hapa nchini kwa ajili ya uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili lizingatiwe kwa sababu watanzania wamechoka kuona wageni wanaendelea kutajirika wao wanaendelea kuwa maskini. Ni lazima wao wapewe nafasi ya kutajirika kwenye nchi yao nah ii nchi ni ya kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaandika kwa maandishi mambo yote ninayoyazungumza ahsante kwa kunipa nafasi nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu Subhana Wataallah kunipa nafasi ya kusimama ndani ya Bunge lako Tukufu, nimshukuru sana Jehova kwa upendeleo alionipa kuwa mmoja wa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana wewe kunipa nafasi ya kusimama lakini niwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Buchosa kwa kunituma hapa Bungeni kuwawakilisha, nataka niendelee kuwaahidi ya kwamba nitakuwa mwakilishi bora nitakaye wawakilisha wao hapa Bungeni na sitajiwakilisha mwenyewe hata siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijaenda mbele sana naomba kwanza niunge mkono hoja, lakini niongee mambo matatu au manne hivi kabla sijazungumza hasa jambo nataka kuchangia.

Mheshimiwa Spika, kwanza; nataka nizungumze suala la uwezeshaji wa wazawa kiuchumi, nimezungumza hili suala mara kadhaa nataka nilizungumze tena leo. Kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 8 (1)(b) jukumu kubwa la Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakuwa ni kusimamia ustawi wa watu wake. Mwaka 2004 tukatunga sheria katika Bunge hili ya kuwawezesha wazawa wa nchi hii kushikilia uchumi wa nchi yao baada ya kuona kwamba uchumi ulikuwa mikononi mwa wageni, sheria hiyo ilisainiwa na Rais Mkapa Marehemu mwaka 2005 na ikaunda Baraza la Uwezeshaji wa Wazawa Kiuchumi ambalo lipo mpaka leo.

Mheshimiwa Spika, naomba sana bajeti tunayopitisha mwaka huu ya zaidi ya shilingi trilioni 40 hivi naomba iweze ku-consider sana wazawa wa nchi hii. Wazawa wa nchi hii wamechoka kuona sehemu ya bajeti kubwa kama hiyo inaishia kwenda nje na wao wanabaki na umaskini. Kwa hiyo, naomba hilo lizingatiwe kabla sijaenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili; nchi hii ina vijana wengi sana wabunifu. Nchi hii ina watu wengi sana wenye uwezo mkubwa wa kubuni solutions mbalimbali, lakini wengi wanaenda nazo kaburini kwa sababu ya ukosefu wa uwezo wa kuzalisha bidhaa au kuendelea mbele na ubunifu wao. Naiomba sana bajeti hii izingatie suala zima la kuanzisha National Innovation Fund, Mfuko wa kuwawezesha vijana wabunifu wa nchi hii waweze kwenda mbele na ubunifu wao na kutengeneza bidhaa. Hii ninaongea ni kama mara ya tatu ya nne hapa Bungeni kwa sababu wapo watu wengi sana wana ubunifu upo ndani ya kabati lakini hawana mtaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huko duniani kuna kitu kinaitwa Global Innovation Fund ambayo huwa inatoa fedha nyingi sana kwa mataifa mbalimbali kusaidia wabunifu wao. Ethiopia mwaka jana wamepewa Euro Milioni Sita na hizi zinakuja siyo mkopo zinatolewa kama grant kwa wabunifu wetu wanaotoka vyuo vikuu ambao hawana mtaji na hawakopesheki na benki zetu.

Mheshimiwa Spika, ninawaomba watalaam wetu, PhD ambazo tunazo katika nchi hii ziandike maandiko ili tuweze kupata sehemu ya fedha hizo ziwasaidie watu wetu.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu; nataka kukumbusha kabla sijaenda mbele ni suala zima la kuipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mkataba au makubaliano ambayo iliingia na nchi za Uarabuni kuhusu mafuta. Waliingia makubaliano ya kwamba nchi za Uarabuni zitakuja hapa zitawekeza kwenye mafuta zitaweka matenki makubwa ili mafuta yawe yanawekwa hapa Tanzania igeuke kama Dubai au Gulf ya Afrika Mashariki na Kati. Naomba Serikali yangu itekeleza jambo hili mapema hizi deal na urasimu huu uondolewe ili jambo hili lingekuwa limeshafanyika mapema hakika tusingekuwa pengine tunapata changamoto tunayoipata leo. Kwa hiyo, naomba hilo lifanyike mapema sana.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho na ninaomba niungane na Profesa Kitila Mkumbo ya kwamba ex-ordinary times require ex-ordinary decisions. Nchi yetu inapita kwenye wakati mgumu sana hivi sasa na siyo Tanzania peke yake ni dunia nzima inapita kwenye wakati usiokuwa wa kawaida, ninaiomba Serikali yangu Tukufu ifanye maamuzi magumu kwenye kipindi hiki.

Mheshimiwa Spika, mwaka 1979 baada ya vita ya Uganda nakumbuka Rais wetu Hayati Baba wa Taifa alisema tufunge mkanda kwa miezi 18, watanzania tunatakiwa kufunga mkanda kipindi hiki kwa sababu ni wakati mgumu kabisa na yafanyike maamuzi ambayo yatasaidia wananchi wawe na unafuu wa maisha. Huko vijijini kwa watu wa chini kabisa achana na sisi huku juu, ukienda watu wana malalamiko makubwa sana. Kila kitu kimepanda bei, mafuta ya kupikia, mafuta ya petrol, kila kitu kipo juu na wananchi wanashindwa hata ku-afford Maisha. Kwa hiyo, tufanye maamuzi ambayo yatakuwa na maslahi kwa Taifa.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nizungumzie suala la umaskini wa Taifa hili. Mwaka jana tumesherehekea uhuru wa nchi yetu mwezi wa 12, ni kweli Taifa hili limepiga hatua kubwa sana na mimi nakubali, lakini umaskini bado upo na umaskini unawasumbua sana watu wa nchi hii. Sisi wote hapa tunatoka vijijini na wengi wetu hapa tunatoka katika familia maskini tunaelewa madhara ya umaskini.

Mheshimiwa Spika, Taifa hili umaskini mkubwa unawakabili wakulima wa nchi yetu. Nchi hii wakulima wanapata shida na ndiyo mafukara namba moja, kilimo kimeajiri asilimia 65 ya watu. Naomba nizungumzie suala la kilimo kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Spika, ili nchi hii iondoke kwenye umaskini unaotukabili ni lazima tuwekeze sana kwenye kilimo chetu, hatuwekezi vya kutosha kwenye kilimo. Nchi hii wakulima wanazidi kuwa maskini kila siku, tumeshakuja na mipango mingi sana, siasa ni kilimo, kilimo cha kufa na kupona, kilimo kwanza, mambo mengi tuna-fail wakati umefika tujiulize ni kwa nini tuna-fail. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Taifa hili lina ardhi kubwa sana square kilometer Laki Tisa hivi, na ardhi ambayo inaweza kulimwa ni kama square kilometer za miraba Laki Nne hivi. Lakini nchi ya Malawi ni ndogo, ardhi yao ambayo inaweza ikalimwa ni square kilometer kama 50,000 hivi, lakini wanazalisha soya bean tani 230 kwa mwaka sisi tunazalisha tani 6,000 mpaka 20,000 kwa mwaka na ukubwa wa hekta tunao na mchango wa kilimo kwenye pato la Taifa ni asilimia 26% lakini Malawi ina 42 % what is wrong with us. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka tujiulize kama Taifa nini shida yetu katika kilimo? Naomba uwekezaji kwenye kilimo ufanyike kwa nguvu kubwa sana kuwasaidia wakulima wanchi hii. Mazao ya nchi hii wakulima wetu wanalima lakini mwisho wa siku mazao yanaishia kuharibika, post-harvest loss kwenye Taifa hili ni asilimia 40, tafsiri yake ni kwamba unalima mazao lakini asilimia 40 yanaharibika.

Mheshimiwa Spika, miwa katika Taifa hili tunavuna tani Milioni Nane kwa mwaka, lakini tunatumia tani Milioni Nne peke yake na tani Milioni Nne zinaharibika. Naambiwa na wataalam wa kilimo kwamba tani Milioni Nne zinazoharibika zingeweza kuchakatwa kuwa sukari tusingeagiza sukari, hivyo, forex yetu tungeweza kuiokoa! Kwa nini hatuwekezi kwenye utengenezaji wa mitambo ya kuchakata sukari? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, TEMDO taasisi yetu ya Tanzania Engineering Manufacturing Development Organization wanatengeneza mitambo, wametengeneza mitambo, mimi ni Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda na Biashara wametengeneza mtambo wa kuchakata sukari ambao unaweza kusaidia wakulima wadogo wadogo wakikopeshwa na SIDO, SIDO kuna kitu wanaita NEDF wanakopeshwa wakawa wanatengeneza sukari hii miwa tutaiokoa. Kwa nini hatuwekezi sasa kwenye TEMDO?

Mheshimiwa Spika, kazi ya Mheshimiwa Bashe ni kulima, kazi ya Mheshimiwa Bashe siyo kuuza, kazi ya kuuza ni ya Mheshimiwa Dada yangu Dkt. Ashatu Kijaji, Wizara ya Viwanda na Biashara. Sasa najiuliza tunaweka bajeti kubwa kwenye kilimo lakini kwa nini hatuweki bajeti humu ya kutafuta masoko?

Mheshimiwa Spika, mimi ni Mwenyekiti ninakuambia TANTRADE hawana pesa watatafutaje masoko? Mheshimiwa Bashe atalima atauza wapi? Matokeo yake tutalima lakini mazao yataoza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sana tubadilishe mtazamo wetu kwenye kilimo, ni kilimo peke yake kitaitoa nchi hii hapa ilipo kwenda mbele.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja tena. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kwa kutoa pongezi nyingi sana kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna anavyofanya kazi kubwa sana katika elimu ya Taifa hili. Mheshimiwa Rais alifanya jambo moja kubwa ambalo limemtengenezea heshima kubwa mno. Alichukuwa mkopo kwa ajili ya UVIKO (COVID 19) lakini akatumia fedha mkopo ule wa COVID 19 kujenga madarasa elfu 15 nchi nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, that was the smart decision, katika Afrika hakuna kiongozi yeyote aliyechukuwa uamuzi wa namna ile. Alikuwa na uwezo wa kuamua anunue barakoa au anunue sanitizer lakini akaona jambo la maana sana kwa watu wake ni kujenga madarasa. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Buchosa namshukuru sana Mheshimiwa Rais na tumejenga madarasa 128, hivi ninavyozungumza watoto wanakaa kwenye madarasa mazuri yaliyotengenezwa vizuri. Ahsante sana Mheshimiwa Rais na Waheshimiwa Wabunge naomba tumuunge Rais wetu mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashangaa kwa nini hampigi makofi ya kutosha kwa Mheshimiwa Rais. Nianze na kitu kinachoita form four certificate dilemma, dilemma ya cheti cha form four. Kabla sijakugusa cheti cha form four nisiache kumshukuru kwanza Profesa Mkenda kwa kazi kubwa ambayo ameanza nayo kwenye Wizara ya Elimu, Profesa namwamini sana, nilikuwa na mpango wa kushika shilingi lakini kwa mambo anayoyafanya sitashika shilingi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Naibu Waziri, ndugu yangu Mheshimiwa Kipanga, anazunguka Tanzania nzima kama pier kwenda kila wilaya kuangalia maendeleo ya elimu. Nampongeza sana Naibu Waziri kwa kazi nzuri. Nachukua nafasi hii pia kumpongeza sana Katibu Mkuu wa Wizara hii Profesa Eliamani Sedoyeka. Kwa kweli namfahamu Katibu Mkuu huyu tangu akiwa Chuo Cha Uhasibu Arusha kwa mambo aliyoyafanya pale Arusha. Aliingia Chuo Cha Uhasibu Arusha kikiwa kwenye hati ya kufungwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, chuo hiki kilikuwa na wanafunzi kama sikosei 2,000, amekaa pale si zaidi ya miaka miwili, ameacha kina wanafunzi elfu 10 na kitu na tayari kina majengo ya ghorofa. Kwa hiyo naamini ujio wake kwenye Wizara ya Elimu, hatakubali hata siku moja kuharibu rekodi yake. Kwa hiyo rekodi yake iliyomsababisha akapewa Ukatibu Mkuu aendelee nayo na Watanzania wanufaike kwa kiasi kikubwa sana na umahiri wake. Niwashukuru Manaibu Makatibu Wakuu na pia niwashukuru watumishi wote wa Wizara ya Elimu, tuna kazi kubwa sana kwa ajili ya elimu ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nizungumzie dilemma cheti cha form four. Wengi mnafahamu mimi sikupata nafasi ya kusoma elimu ya sekondari, lakini kwa neema ya Mwenyezi Mungu na kwa kipaji ambacho Mungu alinipa cha uandishi nilitathiminiwa na TCU nikakubaliwa kusoma Chuo Kikuu kwa mfumo uliokuwa unaitwa RPL Recognition of Prior Learning na nikamaliza Chuo Kikuu vizuri kabisa. Nilipotaka kufanya masters Chuo Kikuu cha Dar es Salaam nikakataliwa nikaambiwa huna cheti cha form four na hayo ndio imekuwa vita yangu profesa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshazungumza sana na Mheshimiwa Profesa na dada yangu Mheshimiwa Ndalichako anakumbuka vizuri sana kwa mapambano yangu mimi na yeye humu Bungeni, kwamba haiwezekani mtu nina shahada ya kwanza TCU wamenikubalia, halafu Chuo Kikuu wanakataa nisifanye masters kwa sababu sina cheti cha form four. Hii haiwezekani, wanawanyima watu haki ya elimu, kuna watu wengi nchi hii wamebuni vitu vingi, watu wametengeneza umeme bila elimu ya sekondari, wanajenga nyumba bila elimu ya sekondari, wanataka kusoma Chuo Kikuu wanakataliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Profesa Mkenda, aichukue kazi hii na kazi yangu hii aweze kulikamilisha jambo hili. Namwamini mno Mheshimiwa Profesa na tumeshazungumza mara nyingi sana kuhusu suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, Profesa Ndekidemi anafahamu, kuna mtu mmoja kwenye Taifa hili lazima nimtolee mfano, alikuwa gardener kwenye chuo kimoja cha kilimo, akawa anatengeneza garden nzuri sana na kwa sababu hiyo Wazungu wakaona anafaa kusoma diploma, akapelekwa kusoma diploma, akamaliza best student kwa diploma kutunza gardener.

Mheshimiwa Naibu Spika, alipomaliza hiyo kozi ya gardener, wakasema aaa, umemaliza na distinction, basi distinction yako tunakupeleka kusoma Uingereza, akapelekwa Uingereza kusoma, from a gardener akaenda kufanya degree ya kwanza ya mambo ya kilimo na degree ile akarudi Tanzania baada ya miaka mitatu akarudi na masters, ndani ya miaka mitatu. Alipofika Tanzania, Tanzania yangu, nchi yangu, inayothamini cheti cha form four, alipotaka kufanya masters akaambiwa huwezi kufanya masters huna cheti cha form four.

Mheshimiwa Naibu Spika, huyu mtu yupo ukitaka nikuletee nakuletea na Profesa Ndekidemi yupo pale ni shahidi wangu. Yule mtu ikabidi aache kufundisha aende akasome QT Tanzania, Profesa Mkenda, akaenda kusoma QT miaka miwili, alipopata cheti cha form four ndiyo akafanya PhD na leo ni Profesa, the best professor in the country. Mimi binafsi siko tayari na nimesema sitashika shilingi, namwomba sana Waziri Profesa Mkenda hili jambo ni la kisheria, alete sheria Bungeni tubadilishe ili Watanzania wapate nafasi ya kusoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kengele ya kwanza kulia, sasa nitoe mchango wangu, nina mambo mawili tu. La kwanza medium of instruction, lugha ya kufundishia. Kwa muda mrefu sana nchi yangu imevutana tufundishe kwa Kiswahili, tufundishe kwa Kiingereza, mvutano huu mpaka lini?

Sasa ni wakati wa kufanya maamuzi, mwanangu anasoma darasa la kwanza kwa Kiswahili mpaka darasa la saba kwa Kiswahili. Akianza form one anaanza kwa Kiingereza. Ile transition ya kutoka Kiswahili kwenda kwenye Kiingereza tunapoteza watoto wengi wenye akili form one atakuwa anajifunza Kiingereza. Form two anajifunza Kiingereza form three kaanza kuelewa Kiingereza kidogo, mtihani wa form four umefika anapata division zero.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba sana Mheshimiwa Waziri na nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge kwa umoja wetu tuamueni tunataka tufundishe Kiingereza au Kiswahili.

WABUNGE FULANI: Kiingereza.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, Kiingereza.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hili nisiliseme nimwombe Mheshimiwa Waziri, afanye utafiti aje na majibu ya watu wanataka tufundishe kwa lugha ipi, tuwe na lugha ya kufundishia ili tuwasaidie watoto wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni suala zima la mitaala ya elimu, limezungumzwa. Dunia inakwenda kwenye fourth industrial revolution, mapinduzi ya nne ya viwanda, lazima mitaala yetu ili-reflect kule tunakoelekea hatuwezi kuendelea kuwafundisha watoto wetu kwa mambo ya second industrial revolution kwa mambo ya third industrial revolution, hatuwezi kufanikiwa. Tutakapofika mapinduzi ya nne ya viwanda ambayo kutokana na mambo ya intelijensia ya bandia niseme hivyo, mambo ya five technology, cloud computing, lazima tuwaandae watoto wetu tuanze kuwafundisha kuanzia primary schools, kuna shida gani kumfundisha mwanangu coding akiwa primary school, kuna shida gani? Hatutaki kufanya maamuzi, matokeo yake shule za binafsi watoto wanaandaliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachotokea, huko mbele tunaandaa matabaka ya watu wawili; watoto wenu hapa watakuwa na nafasi kuliko watoto walioko vijijini, hatutaki Tanzania ya aina hiyo. Tunataka Tanzania yenye usawa, kwa hiyo naomba waache maandalizi mtaala huu, tufikirie sana kuwapa watoto wetu elimu ya computer toka Shule ya Msingi. Walimu tunao, hatuna sababu yeyote ile ya kutofanya jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ni suala la maslahi ya Walimu. Ukitaka kufanikiwa kwenye elimu mfurahishe Mwalimu, basi. Walimu lazima wawe na furaha katika nchi yetu, najua wananisikiliza, Walimu wanaouza visheti…

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Shigongo.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mungu kunipa nafasi ya kusimama ndani ya Bunge hili nikiwa mtu wa kwanza kutoa mchango wangu kwa Taifa langu kuhusu idara hii ya afya.

Mheshimiwa Spika, ninamshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na ninampongeza sana kwa niaba ya Watanzania kwa uamuzi wa kuongeza mishahara kwa asilimia 23.3. Nchi nzima imejaa shangwe kwa sababu ya jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naomba nianze kwanza kwa kusema maneno yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, mwaka 2001 nchi za Afrika zilikutana kule Abuja-Nigeria na wakafikia uamuzi wa kwamba bajeti ya Taifa lolote la Afrika Marehemu Mzee Mkapa alikuwa pale ni lazima asilimia 15 ya bajeti ilielekezwe kwenye huduma za afya. Jambo hili halijaweza kutimia 2019 tulikuwa na asilimia Saba, Mwaka 2020 tulikuwa na asilimia 6.7 na ninavyotazama naona kama tunaendelea kushuka. Sasa mimi nilikuwa ninaushauri mmoja kabla sijaanza ni kwamba naomba Serikali yangu ifikirie kuongeza bajeti kwenye afya kwa sababu afya ya Mtanzania ni kitu cha muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la preventive medicine, suala la kuzuia magonjwa yasitokee, tumefanya kazi kubwa sana kama Taifa kutibu watu, tumefanya kazi kubwa sana kuwatibu watu wetu wanapougua lakini hatujawekeza kiasi kikubwa sana kwenye suala la kuzuia magonjwa yasitokee. Katika suala la kuzuia magonjwa yasitokee nitajikita moja kwa moja kwenye chanjo ya homa ya ini na homa ya ini yenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 2014 mimi na wenzangu katika Kampuni ya Global Publisher tuliamua kufanya kampeni nchi nzima kuwaelimisha watu kuhusiana na ugonjwa wa Homa ya Ini. Kilichotufanya tufanye kampeni ile ilikuwa ni data zilizokuwepo za Homa ya Ini zilitushtua, zilitutisha na tukaona kwamba ilikuwa sababu ya mimi na wenzangu kutoa mchango kwa nchi yetu ili kuweza kusaidia watu waweze kupata ufahamu.

Mheshimiwa Spika, wakati huo 2014 katika akina mama waliofanyiwa uchunguzi wa afya wajawazito asilimia tano ya akina mama wote walikuwa wanakutwa na Homa ya Ini. Damu iliyotolewa kwenye benki ya damu hapo Dar es Salaam na sehemu mbalimbali chupa 100 zilizochukuliwa chupa nne zilikutwa na homa ya ini na uwepo wa homa ya ini katika nchi ulikuwa ni asilimia tano data zile zilitutisha tukaanza kampeni ile, tumefanya kampeni kwa muda tu, wakati ule Waziri wa Afya alikuwa Rais wa Zanzibar sasa hivi Mheshimiwa Hussein Ally Mwinyi, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam alikuwa Mheshimiwa Said Meck Sadiki, Mganga Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam alikuwa Dada yangu Grace Magembe na Meya wa Ilala alikuwa Mdogo wangu Mheshimiwa Jerry Silaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumefanya kampeni ile kwa muda mfupi nikaitwa nikaambiwa Eric kampeni yako ni nzuri lakini tunaomba uiache kwanza inasababisha hofu inaleta taharuki watu wanaogopa, tukakubali kuacha kampeni ile kwa shingo upande. Miaka nane baadaye nikiwa naongea leo naomba nikusomee data za homa ya ini nchini Tanzania. Kwa wajawazito 100 wanaopimwa leo kwenye antenatal clinic zetu asilimia Saba mpaka Nane wanakutwa na homa ya ini, imeongezeka. Benki ya damu wanapotoa damu watu 100 chupa sita zinakutwa na homa ya ini.

Mheshimiwa Spika, rate ya homa ya ini, uwepo wa homa ya ini kwenye Taifa letu sasa hivi ni asilimia mpaka 7.2 katika baadhi ya maeneo. Hii inatisha, hili siyo jambo la kukalia kimya, wala siyo jambo la kuacha kuliongelea.

Mheshimiwa Spika, nimesimama hapa leo kuongea nikiamini ya kwamba tuna uwezo wa kuzuia ugonjwa huu, tuna uwezo wa kuokoa maisha ya watu wetu kwa sababu chanjo ipo na mimi nafahamu Waheshimiwa Wabunge humu ndani mnaonisikiliza wengi mmechanjwa kwa sababu chanjo ililetwa hapa hapa Bungeni, lakini huko nje watu wetu wanashindwa kuimudu hii chanjo, kwa bei ya Serikali ni Shilingi 10,000 kwa chanjo moja mtu anahitaji chanjo tatu na kabla hajachanjwa lazima afanyiwe rapid test kuona kama ameambukizwa au hapana Shilingi Elfu Arobaini, Elfu Arobaini ni nyingi kwa mwananchi wa kawaida. Wananchi wanauliza kama chanjo ya COVID tumechanjwa bure kwa nini chanjo ya homa ya ini tunaombwa pesa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wanakufa, maisha ya watu yanapotea, watu wengi wameambukizwa. Hapa ndani mnaonisikiliza kama haujafiwa, kama humjui mtu aliyekufa basi wewe mwenyewe jipeleleze. Ugonjwa huu unazidi kuenea, kasi ya kuenea ni mara 100 zaidi ya UKIMWI. Tuna sababu ya kuchukua hatua kuokoa maisha ya watu wetu. Tuna kila sababu ya kuchukua hatua kuokoa maisha ya watu wetu, watu wanakufa. Hatuwezi kunyamaza, hatuwezi kujifanya hatuoni, lazima tuchukue hatua tuokoe maisha ya watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuko hapa Bungeni Waheshimiwa Wabunge kwa ajili ya watu waliotuchagua. Tuko hapa Bungeni kama hatuwezi kutetea maisha ya watu wetu waishi hatuna sababu ya kuwa Wabunge. Najiuliza kila siku kwanini hatuchanji? Kuna mtu akaniambia nchi yetu ni maskini na hatuna uwezo. Nikakataa, nikamwambia ukiniambia nchi ni maskini niletee report ya CAG nitakuonesha fedha zinapotelea wapi. Mabilioni ya fedha yanapotea mikononi mwa watu wasiokuwa waaminifu. Tungeokoa fedha zetu kwenye report ya CAG katika nchi hii tungeweza kuwachanja watu wetu wote na chenji ikabaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiachana na hilo, naomba niongee jambo moja la msingi sana na bahati nzuri wataalam wako hapa wananisikiliza. Umuhimu wa kumchanja mtu badala ya kumtibu ni jambo la maana mno. Kansa ya Ini, the Hepatocellular Carcinoma gharama ya kumtibu hapa Tanzania ni Shilingi Milioni 16 mtu mmoja. (Makofi)

SPIKA: Sekunde 30 malizia.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, sasa kama gharama ya kumtibu mtu mmoja hapa Tanzania ni Shilingi Milioni 15 mwenye Kansa ya Ini inayosababishwa na Homa ya Ini. Ni kwanini tusiwachanje watu kuokoa maisha yao? Fedha zipo, tuwachanjeni watu wetu tuweze kuokoa maisha yao. (Makofi)

SPIKA: Haya ahsante sana. Ahsante sana.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
THE WRITTEN LAWS (MISCELLANEOUS AMENDMENTS) (NO. 4) ACT, 2021
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nianze kwa kumshukuru Mungu kunipa nafasi ya kusimama ndani ya Bunge hili kuzungumza suala la marekebisho haya ya sheria.

Mheshimiwa Spika, nitoe shukrani nyingi sana kwa Kamati kwa kutambua jambo ambalo nilizungumza wakati wa bajeti ya Wizara ya Elimu, suala la RPL (Recognition of Prior Learning) nimelikuta na limejadiliwa. Napongeza sana Kamati nzima, Mwenyekiti na Wajumbe wote kwa kutambua jambo hili. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri dada yangu Ndalichako hatimaye kuona kuna umuhimu wa kuanza kuliona jambo la RPL kama ni muhimu kwa maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sina mambo mengi sana ya kusema zaidi ya pongezi hizo. Isipokuwa, ukienda kwenye ukurasa wa 12 pameandikwa amendment of Section 2(31) naomba niisome, inasema “The principal Act is amended in Section 2 by inserting in their appropriate alphabetical order the following new definitions. Recognition of Prior learning means the process of evaluating skills and knowledge acquired outside the classroom for the purpose of recognizing competence against a given set of standards, competence or learning outcome”.

Mheshimiwa Spika, jambo hili nililizungumza wakati ule, wakati wa bajeti na nakumbuka kama nilishikilia shilingi ya Mheshimiwa Waziri. Wako watu katika Taifa hili ambao aidha kwa vipaji au kwa practical experience wameweza kufanya mambo makubwa sana. Nitatoa mfano wa mtu mmoja kule Iringa alifanikiwa kuzalisha umeme na kusambaza kwenye kijiji chake bila elimu formal, bila kupita darasani. Nakumbuka aliitwa Ikulu wakati ule na Hayati na kuzawadiwa.

Mheshimiwa Spika, lakini nitoe mfano wa mtoto mmoja hapa wa kidato cha nne ambaye ametengeneza bulb yake ambayo ameweza kuiamuru kwa maneno ikazima au kuwaka. Hapa ndani ya Bunge lako tukufu wako watu ambao wanaweza kukutajia mpaka mifano, hawana hiyo elimu kubwa lakini wanafanya mambo makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, Mheshimiwa Kibajaji kwa uwezo wake wa ku-present mada hapa Bungeni angeweza kusomea public speaking na akatambuliwa na akasoma na akapata shahada kabisa ya mawasiliano ya Umma bila shida yoyote kwa uwezo tu wa kuzungumza alionao.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Jumanne Kishimba kwa namna alivyofanya toka zero mpaka ku-own companies na elimu yake ya darasa la saba angeweza kabisa kwa utaratibu huu kuruhusiwa kusoma hata business administration.

Mheshimiwa Spika, wewe ni Mgogo unamkumbuka Ukwe Zawose. Ukwe Zawose alikuwa ni kipofu mtaalam wa kupiga ngoma lakini alikwenda Finland akapiga ngoma kwenye chuo kikuu kimoja kwa sababu ya utaalam wake wa kupiga ngoma wakamu-award PHD. Kwa hiyo, ninapoona mambo haya yanaanza kutambuliwa naanza kuona sasa tunaanza kuelekea mahali pazuri kielimu kwenye Taifa langu. Nataka nchi yangu isifunge ilango kwa watu ambao hawakupita kwenye formal education kuweza kupata elimu ya juu. Hiyo ndiyo hoja yangu na hilo ndiyo jambo ambalo nimeliongelea sana kwamba ninapozungumza hapa simaanishi ku-challenge legal framework. Isipokuwa namaanisha kufungua milango kama ulivyofunguliwa kwangu.

Mheshimiwa Spika, ushuhuda wangu sitaki kuurudia tena leo wote mnaufahamu nilishauzungumza Bungeni hapa. Elimu yangu ya darasa la saba kwa kipaji cha kuandika nikapelekwa Chuo Kikuu nikafauli na nikamaliza. Nilipokwenda University of Dar es Salaam ku-apply for masters nikakataliwa kwa sababu sina cheti cha form four. Sasa hii form four hii ndiyo ninayoiongelea leo. Lakini nimeenda Open University nimekuwa accepted, sasa hivi nafanya Masters ya Mass Communication hawajaniuliza cheti cha form four.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa kipengele hiki nilichokisoma kimetambua kwamba wako watu wenye elimu ya vitendo lakini hawama elimu formal…

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nimalizie kidogo tu. Ukienda kwenye sehemu ya 35 hapa mwisho nilikuwa na mapendekezo ambayo baadaye…

SPIKA: 31…

MHE. ERIC J. SHIGONGO: …31 hapo nilikuwa nasoma lakini ukija 35 amendment Section 24 ukienda hapo kuna kipengele M. Ningependekeza, wameandika hivi “prescribing procedures for recognition of prior learning and…” hapo ningeomba tuongeze kipengele ambacho kinamtaka mtu ambaye ametambuliwa na aidha TCU au NACTE akasome popote pale bila kuuliza cheti cha Form Four. Ndiyo hoja yangu. Naomba kuwasilisha.
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana kunipa nafasi ya kutoa mchango wangu mchana huu wa leo. Hoja yangu kubwa itakuwa kwenye suala zima la Transfer Pricing. Jana suala hili limenifanya sikulala vizuri usiku. Nimelala natafakari, nafikiria namna ambavyo nchi yangu inaibiwa fedha nyingi na wajanja wachache.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nilifanya utafiti kidogo, kwanza nilitaka nijielimishe hivi hawa watu wanatuibiaje? Nikaja kugundua kwamba hawa watu wanatuibia kwa namna mbili, kama ambavyo ametangulia kuzungumza Mheshimiwa Yahya ni kwamba kampuni inakuwepo hapa Tanzania labda ni Geita kunakuwa na kampuni nyingine Dubai na kampuni nyingine Mauritius. Kwa mfano kama ni dhahabu inayochimbwa na Shigongo ambayo ni kampuni iko Tanzania anamuuzia aliyeko Dubai, ili kuikosesha Tanzania mapato anauza kwa bei ya chini, badala ya Sh.100/= anauza kwa Sh.10/= ili awaoneshe kwamba aliuza kwa hasara. Anapotaka kununua spare parts zake ananunua kwa kampuni yake nyingine iko Mauritius inamuuzia spare parts kwa bei ya juu ili kusudi aonekane gharama zake za uendeshaji zilikuwa kubwa aoneshe hasara ili Serikali isiweze kupata kodi. Huu ni wizi na wizi wa namna hii hauwezi kuvumiliwa, nchi yetu haiwezi kuendelea kupoteza mapato. Wenzetu wazungu wanaandaa utaratibu huu kwa nia moja tu ya kuziibia nchi za Afrika ziendelee kuwa masikini nao waendelee kujitajirisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Taifa hatuwezi kuruhusu mambo haya yaendelee na nataka nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa sheria ambayo ameileta hapa Bungeni. Ameleta hapa kipengele ambacho kinataka kufanya adjustment kidogo kwenye sheria yetu. Kinasema kwamba tukishamkamata huyu mtu katuibia asilimia 30 yetu kama kodi atulipe, akishatulipa asilimia 30 tumpige asilimia 100 kwenye zote alizokuwa ametuibia. Sasa hatuwezi kuondoa 100 ambayo ni fine kwa lengo tu la kuwaita eti waje kuwekeza nyumbani kwetu, hawa sio wawekezaji hawa ni wezi; hawa ni wezi hatuwataki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kimoja ambacho najua kimempa changamoto Mheshimiwa Waziri ni kwamba wakati anatakiwa kuwabana wawekezaji wakati huohuo anatakiwa aboreshe mazingira wawekezaji waje, kwa hiyo, amejikuta yupo njia panda. Akaja na solution ya kwamba kwa sababu niko njia panda nifanyeje wawekezaji waje ili niweze kupata kodi, uchumi wetu unakua kwa asilimia 4.5 kwa sasa, akajikuta anasema nipunguze angalau tutoke asilimia 100 ya penalty iwe asilimia 75. Mimi nakubaliana na asilimia 75 ambayo Mheshimiwa Waziri ameona inafaa na naomba kabisa kama lengo ni ku-attract investors tuwapige asilimia 75 na wakati uleule tuwapige asilimia 30 ya kodi waliyokuwa wanatuibia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu ni kwamba Kitengo chetu cha International Tax Unit cha TRA hakina uwezo wa kuwakagua wafanyabiashara wote. Hakina uwezo wa kuzikagua hizi multinational zote zilizoko hapa nchini, hakina uwezo, kina wafanyakazi 18 tu mpaka ninavyozungumza hivi sasa. Wafanyakazi 18 hawana uwezo wa kukagua kampuni zote hizi.

Ombi langu mimi kwa Mheshimiwa Waziri ni kwamba waki-strengthen Kitengo hiki kiwe na nguvu, wafanye capacity building ya kutosha watu hawa wawe na uwezo wa kukagua kampuni zote zilizoko hapa nchini ambazo ni multinational ili tuweze kugundua matatizo yote ambayo yanafanyika na wizi wote ambao unatokea. Tukishawakamata hatuna huruma, ni kodi yetu asilimia 30 na asilimia 75 yetu tuwatoze. Watakaotaka kufanya biashara wafanye ambao hawataki kufanya biashara na sisi waondoke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nikukumbushe jambo moja la muhimu sana ya kwamba viwanda vyetu vya alizeti vya kukamua mafuta vikumbukwe. Viwanda vikubwa vinapata zero eighteen percent ya VAT, viwanda vidogovidogo vinapigwa asilimia 18. Naomba Mheshimiwa Waziri awakumbuke wafanyabiashara wadogowadogo wenye viwanda hivi nao pia waweze kupatiwa zero eighteen percent nao waweze kufaidi soko letu la alizeti hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kushukuru sana na baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)